7
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TISA
كَذَّبَتْ ثَمُودُ الْمُرْسَلِينَ ﴿١٤١﴾
141. Thamud waliwakadhibisha mitume.
إِذْ قَالَ لَهُمْ أَخُوهُمْ صَالِحٌ أَلَا تَتَّقُونَ ﴿١٤٢﴾
142. Alipowaambia ndugu yao Swaleh: Je, hamna takua?
إِنِّي لَكُمْ رَسُولٌ أَمِينٌ ﴿١٤٣﴾
143. Hakika mimi kwenu ni Mtume mwaminifu.
فَاتَّقُوا اللَّـهَ وَأَطِيعُونِ ﴿١٤٤﴾
144. Basi mcheni Mwenyezi Mungu na mnitii.
وَمَا أَسْأَلُكُمْ عَلَيْهِ مِنْ أَجْرٍ إِنْ أَجْرِيَ إِلَّا عَلَىٰ رَبِّ الْعَالَمِينَ ﴿١٤٥﴾
145. Na siwataki ujira juu yake, kwani ujira wangu hauko ila kwa Mola wa walimwengu wote.
أَتُتْرَكُونَ فِي مَا هَاهُنَا آمِنِينَ ﴿١٤٦﴾
146. Je, mtaachwa salama katika haya yaliyopo hapa?
فِي جَنَّاتٍ وَعُيُونٍ ﴿١٤٧﴾
147. Katika mabustani na chem- chem?
وَزُرُوعٍ وَنَخْلٍ طَلْعُهَا هَضِيمٌ ﴿١٤٨﴾
148. Na mimea na mitende yenye makole yalioiva?
وَتَنْحِتُونَ مِنَ الْجِبَالِ بُيُوتًا فَارِهِينَ ﴿١٤٩﴾
149. Na mnachonga majumba mlimani kwa ustadi
فَاتَّقُوا اللَّـهَ وَأَطِيعُونِ ﴿١٥٠﴾
150. Basi mcheni Mwenyezi Mungu na mnitii.
وَلَا تُطِيعُوا أَمْرَ الْمُسْرِفِينَ ﴿١٥١﴾
151. Wala msitii amri za waliopituka mipaka.
الَّذِينَ يُفْسِدُونَ فِي الْأَرْضِ وَلَا يُصْلِحُونَ ﴿١٥٢﴾
152. Ambao wanafanya ufisadi katika ardhi wala hawaiten- genezi.
قَالُوا إِنَّمَا أَنتَ مِنَ الْمُسَحَّرِينَ ﴿١٥٣﴾
153. Wakasema: Hakika wewe ni miongoni mwa waliorogwa tu.
مَا أَنتَ إِلَّا بَشَرٌ مِّثْلُنَا فَأْتِ بِآيَةٍ إِن كُنتَ مِنَ الصَّادِقِينَ ﴿١٥٤﴾
154. Wewe si chochote ila ni mtu kama sisi. Basi lete ishara ukiwa wewe ni miongoni mwa wasemao kweli.
قَالَ هَـٰذِهِ نَاقَةٌ لَّهَا شِرْبٌ وَلَكُمْ شِرْبُ يَوْمٍ مَّعْلُومٍ ﴿١٥٥﴾
155. Akasema: Huyu ngamia jike; awe na zamu yake ya kunywa na nyinyi muwe na zamu yenu ya kunywa katika siku maalum.
وَلَا تَمَسُّوهَا بِسُوءٍ فَيَأْخُذَكُمْ عَذَابُ يَوْمٍ عَظِيمٍ ﴿١٥٦﴾
156. Wala msimguse kwa ubaya isije ikawashika adhabu ya siku kubwa.
فَعَقَرُوهَا فَأَصْبَحُوا نَادِمِينَ ﴿١٥٧﴾
157. Lakini wakamuua wakawa wenye kujuta.
فَأَخَذَهُمُ الْعَذَابُ إِنَّ فِي ذَٰلِكَ لَآيَةً وَمَا كَانَ أَكْثَرُهُم مُّؤْمِنِينَ ﴿١٥٨﴾
158. Basi ikawashika adhabu. Hakika bila shaka katika hayo ipo ishara, lakini wengi wao si wenye kuamini.
وَإِنَّ رَبَّكَ لَهُوَ الْعَزِيزُ الرَّحِيمُ ﴿١٥٩﴾
159. Na hakika Mola wako ndiye Mwenye nguvu, Mwenye kurehemu.
Aya 141 – 159
Kisa cha Swaleh kimetangulia katika Juz. 8 (7: 73 – 79) na Juz. 12 (11: 61 -68).
Thamud waliwakadhibisha mitume. Alipowaambia ndugu yao Swaleh: Je, hamna takua? Hakika mimi kwenu ni Mtume mwaminifu. Basi mcheni Mwenyezi Mungu na mnitii. Na siwataki ujira juu yake, kwani ujira wangu hauko ila kwa Mola wa walimwengu wote.
Zimetangulia Aya hizi kwa herufi zake katika sura hii Aya 105 – 110, na pia katika sehemu iliyopita bila ya mabadiliko yoyote isipokuwa jina tu la Thamud na Swaleh. Tumesema huko kuwa siri ya hilo ni kuwa risala ya mitume wote ni moja.
Je, mtaacha salama katika haya yaliyopo hapa katika mabustani na chemchem na mimea na mitende yenye makole yalioiva? Na mna chonga majumba mlimani kwa ustadi
Kabila la Thamud lilizama katika anasa na strehe – matunda, mito, makasri, wanyama n.k. Wakiwa wameghafilika na kila kitu isipokuwa matamanio yao na ladha zao. Ndipo ndugu yao Swaleh akawaonya na mwisho mbaya na akawaambia, Je, mmemsahau Mwenyezi Mungu na yeye hajawasahau? Je, mmejiaminisha na matukio ya ghafla?
Basi mcheni Mwenyezi Mungu na nitiini wala msitii amri za waliopituka mipaka ambao wanafanya ufisadi katika ardhi wala hawaitengenezi.
Makusudio ya waliopituka mipaka, walio wafisadi, ni viongozi ambao ndio chimbuko la balaa zote; isipokuwa wachache sana. Hakuna dini wala misimamo, katika ufahamu wao, isipokuwa masilahi yao na masilahi ya jamaa zao.
Wafisadi hawa, katika kaumu ya Swaleh, walikuwa tisa; kama ilivyoelezwa katika Aya nyingine: kwenye juzuu hii. “Na walikuwako mjini watu tisa wakifanya ufisadi katika ardhi wala hawafanyi la masilahi” (25:48).
Wakasema: Hakika wewe ni miongoni mwa waliorogwa tu.
Umerogwa na mchawi mpaka umekuwa hujui unalolisema. Hivi ndivyo wasemavyo vijana wengi wa kileo wanapoambiwa swalini na fungeni.
Wewe si chochote ila ni mtu kama sisi, unakula chakula na kutembea sokoni, sasa vipi unateremshiwa wahyi zaidi yetu sisi?
Basi lete ishara ukiwa wewe ni miongoni mwa wasemao kweli.
Walisema haya wakiwa wameazimia kuendelea na ukafiri wao na inadi yao, hata kama wataletewa dalili elfu na moja; vinginevyo maombi yao yangelikuwa ya haki na ya sawa.
Akasema: Huyu ngamia jike; awe na zamu yake ya kunywa na nyinyi muwe na zamu yenu ya kunywa katika siku maalum. Wala msimguse kwa ubaya isije ikawashika adhabu ya siku kubwa.
Walimuomba awaletee muujiza unaofahamisha utume wake, akawaletea ngamia kwa njia isiyo ya kawaida na akawawekea sharti la maji kwa zamu; siku moja yao na siku moja ya ngamia na kwamba wasimdhuru isije ikawafikia adhabu,
lakini wakamuua wakawa wenye kujuta, Basi ikawashika adhabu.
Umetangulia mfano wake katika Juz. 8 (7: 77 – 78).
Hakika bila shaka katika hayo ipo ishara, lakini wengi wao si wenye kuamini. Na hakika Mola wako ndiye Mwenye nguvu, Mwenye kurehemu.
كَذَّبَتْ قَوْمُ لُوطٍ الْمُرْسَلِينَ ﴿١٦٠﴾
160. Kaumu ya Lut waliwakadhibisha mitume.
إِذْ قَالَ لَهُمْ أَخُوهُمْ لُوطٌ أَلَا تَتَّقُونَ ﴿١٦١﴾
161. Alipowaambia ndugu yao Lut: Je, hamna takua?
إِنِّي لَكُمْ رَسُولٌ أَمِينٌ ﴿١٦٢﴾
162. Hakika mimi kwenu ni Mtume mwaminifu.
فَاتَّقُوا اللَّـهَ وَأَطِيعُونِ ﴿١٦٣﴾
Basi mcheni Mwenyezi Mungu na mnitii.
وَمَا أَسْأَلُكُمْ عَلَيْهِ مِنْ أَجْرٍ إِنْ أَجْرِيَ إِلَّا عَلَىٰ رَبِّ الْعَالَمِينَ ﴿١٦٤﴾
164. Na siwataki ujira juu yake, kwani ujira wangu hauko ila kwa Mola wa walimwengu wote.
أَتَأْتُونَ الذُّكْرَانَ مِنَ الْعَالَمِينَ ﴿١٦٥﴾
165. Je, katika viumbe wote mnawaendea wanaume?
وَتَذَرُونَ مَا خَلَقَ لَكُمْ رَبُّكُم مِّنْ أَزْوَاجِكُم بَلْ أَنتُمْ قَوْمٌ عَادُونَ ﴿١٦٦﴾
166. Na mnaacha alichowaumbia Mwenyezi Mungu katika wake zenu? Bali nyinyi ni watu mnaoruka mipaka.
قَالُوا لَئِن لَّمْ تَنتَهِ يَا لُوطُ لَتَكُونَنَّ مِنَ الْمُخْرَجِينَ ﴿١٦٧﴾
167. Wakasema: Kama hutakoma ewe Lut bila shaka utakuwa miongoni mwa wanaotolewa.
قَالَ إِنِّي لِعَمَلِكُم مِّنَ الْقَالِينَ ﴿١٦٨﴾
168. Akasema: Hakika mimi ni katika wanaokichukia hiki kitendo chenu.
رَبِّ نَجِّنِي وَأَهْلِي مِمَّا يَعْمَلُونَ ﴿١٦٩﴾
Mola wangu! Niokoe na ahli zangu kwa wayatendao.
فَنَجَّيْنَاهُ وَأَهْلَهُ أَجْمَعِينَ ﴿١٧٠﴾
Basi tukamuokoa na ahli zake wote.
إِلَّا عَجُوزًا فِي الْغَابِرِينَ ﴿١٧١﴾
171. Isipokuwa kikongwe katika waliokaa nyuma.
ثُمَّ دَمَّرْنَا الْآخَرِينَ ﴿١٧٢﴾
Kisha tukwaangamiza wale wengine.
وَأَمْطَرْنَا عَلَيْهِم مَّطَرًا فَسَاءَ مَطَرُ الْمُنذَرِينَ ﴿١٧٣﴾
173. Na tukawanyesheza mvua, basi ni uovu mno wa mvua ya waliyoonywa.
إِنَّ فِي ذَٰلِكَ لَآيَةً وَمَا كَانَ أَكْثَرُهُم مُّؤْمِنِينَ ﴿١٧٤﴾
174. Hakika bila shaka katika hayo ipo ishara, lakini wengi wao si wenye kuamini.
وَإِنَّ رَبَّكَ لَهُوَ الْعَزِيزُ الرَّحِيمُ ﴿١٧٥﴾
175. Na hakika Mola wako ndiye Mwenye nguvu, Mwenye kurehemu.
Aya 160-175
Kisa cha Lut kimetangulia katika Juz. 8 (7:80 –84) na Juz. 12 (11:82– 87).
Kaumu ya Lut waliwakadhibisha mitume. Alipowaambia ndugu yao Lut: Je, hamna takua?
Ni ndugu yao katika kuwa pamoja na makazi; si katika dini wala nasabu. Kwa kuwa yeye alikuja hapo na ami yake, Ibrahim(a.s) kutoka Babel (Babylon) kupitia Misr hadi Palestina. Lut alikaa katika bonde la Jordan na Ibrahim akakaa katika nyanda za juu kaskazini. Hapo ilikuwa ni karne kumi na tisa kabla ya kuzaliwa Nabii Isa (19 B.C.)
Imetangulia kwa herufi zake, katika Aya 67 na 68 ya sura hii na pia sehemu iliyopita.
“Hakika mimi kwenu ni Mtume mwaminifu. Basi mcheni Mwenyezi Mungu na mnitii. Na siwataki ujira juu yake, kwani ujira wangu hauko ila kwa Mola wa walimwengu wote.
Lut alianza kama alivyoanza Nuh, Hud na Swaleh(a.s ) . Kwa sababu risala ya wote ni moja. Soma katika sura hii Aya zinazomzungumzia kila mmoja katika wao.
Je, katika viumbe wote mnawaendea wanaume?
Mnafanya kitendo hiki cha fedheha kwa wanaume katika wanadamu?
Na mnaacha alichowaumbia Mwenyezi Mungu katika wake zenu?
Kwa hiyo mnahalifu hukumu ya maumbile na kanuni, tabia na lengo la kumbwa mume na mke.
Tendo lenu halikubaliwi hata na wanyama na wadudu. Lakini bunge la Uingereza limeruhusu ulawiti. Hiyo ni dalili kuwa Uingereza ni duni zaidi kuliko wanyama katika hulka yake na thamani yake. Sio mbali kuwa hii ni natija ya historia yake ndefu ya ukoloni unaochukiwa. Kwa sababu utaghuti na uadui una mwisho mbaya.
Bali nyinyi ni watu mnaoruka mipaka.
Mmepituka mipaka yote kwa hawa, usafihi, uasi na ujeuri wenu.
Wakasema: Kama hutakoma ewe Lut bila shaka utakuwa miongoni mwa wanaotolewa.
Umetangulia mfano wake katika Aya 116 ya Sura hii.
Akasema: Hakika mimi ni katika wanaokichukia hiki kitendo chenu.
Katika maana yake ni; Aya 216 ya sura hii! “Na ikiwa watakuasi basi sema mimi ninajitenga mbali na hayo mnayo yatenda.”
Mola wangu! Niokoe na ahli zangu kwa wayatendao. Basi tukamuokoa na ahli zake wote. Isipokuwa kikongwe katika waliokaa nyuma. Kisha tukwaangamiza wale wengine. Na tukawanyesheza mvua, basi ni uovu mno wa mvua ya waliyoonywa.
Umetangulia mfano wake katika Juz. 8 (7:83 – 84) na Juz. 14 (15:59 – 60).
Hakika bila shaka katika hayo ipo ishara, lakini wengi wao si wenye kuamini. Na hakika Mola wako ndiye Mwenye nguvu, Mwenye kurehemu.
Imetangulia kwa herufi zake, katika Aya 67 na 68 ya Sura hii na pia sehemu iliyopita.
كَذَّبَ أَصْحَابُ الْأَيْكَةِ الْمُرْسَلِينَ ﴿١٧٦﴾
176. Watu wa mwituni waliwakadhibisha mitume.
إِذْ قَالَ لَهُمْ شُعَيْبٌ أَلَا تَتَّقُونَ ﴿١٧٧﴾
177. Alipowaambia Shua’yb: Je, hamna takua?
إِنِّي لَكُمْ رَسُولٌ أَمِينٌ ﴿١٧٨﴾
178. Hakika mimi kwenu ni Mtume mwaminifu.
فَاتَّقُوا اللَّـهَ وَأَطِيعُونِ ﴿١٧٩﴾
179. Basi mcheni Mwenyezi Mungu na mnitii.
وَمَا أَسْأَلُكُمْ عَلَيْهِ مِنْ أَجْرٍ إِنْ أَجْرِيَ إِلَّا عَلَىٰ رَبِّ الْعَالَمِينَ ﴿١٨٠﴾
180. Na siwataki ujira juu yake, kwani ujira wangu hauko ila kwa Mola wa walimwengu wote.
أَوْفُوا الْكَيْلَ وَلَا تَكُونُوا مِنَ الْمُخْسِرِينَ ﴿١٨١﴾
181. Timizeni kipimo sawasawa wala msiwe miongoni mwa wanaopunja.
وَزِنُوا بِالْقِسْطَاسِ الْمُسْتَقِيمِ ﴿١٨٢﴾
182. Na pimeni kwa mizani iliyo sawa.
وَلَا تَبْخَسُوا النَّاسَ أَشْيَاءَهُمْ وَلَا تَعْثَوْا فِي الْأَرْضِ مُفْسِدِينَ ﴿١٨٣﴾
183. Wala msiwapunguzie watu vitu vyao, Wala msifanye ufisadi katika nchi mkafanya vurugu.
وَاتَّقُوا الَّذِي خَلَقَكُمْ وَالْجِبِلَّةَ الْأَوَّلِينَ ﴿١٨٤﴾
184. Na mcheni aliyewaumba nyinyi na vizazi vilivyotangulia.
قَالُوا إِنَّمَا أَنتَ مِنَ الْمُسَحَّرِينَ ﴿١٨٥﴾
185. Wakasema: Hakika wewe ni miongoni mwa waliorogwa tu.
وَمَا أَنتَ إِلَّا بَشَرٌ مِّثْلُنَا وَإِن نَّظُنُّكَ لَمِنَ الْكَاذِبِينَ ﴿١٨٦﴾
186. Na wewe si chochote ila ni mtu kama sisi, na kwa hakika tunakuona ni katika waongo.
فَأَسْقِطْ عَلَيْنَا كِسَفًا مِّنَ السَّمَاءِ إِن كُنتَ مِنَ الصَّادِقِينَ ﴿١٨٧﴾
187. Basi tuangushie kipande cha mbingu, ikiwa wewe ni miongoni mwa wasemao kweli.
قَالَ رَبِّي أَعْلَمُ بِمَا تَعْمَلُونَ ﴿١٨٨﴾
188. Akasema: Mola wangu anajua zaidi mnayoyatenda.
فَكَذَّبُوهُ فَأَخَذَهُمْ عَذَابُ يَوْمِ الظُّلَّةِ إِنَّهُ كَانَ عَذَابَ يَوْمٍ عَظِيمٍ ﴿١٨٩﴾
189. Basi wakamkadhibisha, ikawashika adhabu ya siku ya kivuli. Hakika hiyo ilikuwa adhabu ya siku kubwa.
إِنَّ فِي ذَٰلِكَ لَآيَةً وَمَا كَانَ أَكْثَرُهُم مُّؤْمِنِينَ ﴿١٩٠﴾
190. Hakika bila shaka katika hayo ipo ishara, lakini wengi wao si wenye kuamini.
وَإِنَّ رَبَّكَ لَهُوَ الْعَزِيزُ الرَّحِيمُ ﴿١٩١﴾
191. Na hakika Mola wako ndiye Mwenye nguvu, Mwenye kurehemu.
Aya 176 – 191
Kisa cha Shua’yb kimetangulia katika Juz. 8 (7: 85) na Juz. 12 (11:84 – 95).
Watu wa mwituni waliwakadhibisha mitume. Alipowaambia Shua’yb: Je, hamna takua?
Wafasiri wamesema kuwa watu wa mwituni ni watu waliokuwa karibu na Madyan kwenye miti mingi.
Alipowaambia Shua’yb: Je, hamna takua?
Mwenyezi Mungu (s.w.t) hakusema ndugu yao Shua’yb, kama alivyosema ndugu yao Hud, Swaleh na Lut, kwa sababu Shua’yb si mtu wa hapo kinasabu wala hana uhusiano wowote na watu wa mwituni, isipokuwa ujirani. Mwenyezi Mungu alimtuma kwao; kama alivyomtuma kwa watu wake wa Madyan.
Hakika mimi kwenu ni Mtume mwaminifu. Basi mcheni Mwenyezi Mungu na mnitii. Na siwataki ujira juu yake, kwani ujira wangu hauko ila kwa Mola wa walimwengu wote.
Aya hizi zimetanguliwa kwa herufi zake kupitia mdomoni mwa Nuh, Hud, Swaleh na Lut. Hayo ni maneno ya kila Nabii.
Timizeni kipimo sawasawa wala msiwe miongoni mwa wanaopunja. Na pimeni kwa mizani iliyo sawa. Wala msiwapunguzie watu vitu vyao, Wala msifanye ufisadi katika nchi mkafanya vurugu.
Umetangulia mfano wake katika Juz. 8 (7: 85) na Juz. 12 (11:84)
Na mcheni aliyewaumba nyinyi na vizazi vilivyotangulia.
Yaani mhofie adhabu ya Mwenyezi Mungu aliyewaumba nyinyi na wale waliotangulia.
Wakasema: Hakika wewe ni miongoni mwa waliorogwa tu.
Imetangulia kwa herufi zake katika Aya 153 ya sura hii.
Wewe si chochote ila ni mtu kama sisi, na kwa hakika tunakuona ni katika waongo.
Yaani wewe unakusudia uwongo katika madai yako ya utume, kwa dalili ya kuwa wewe ni mtu unayekula chakula na kutembea sokoni. Lau wahyi ungeliwashukia watu basi watu wote wangelikuwa Mitume.
Ibn Hisham katika kitabu Al-Mughni, katika kuelezea watu wasiofaliwa na maneno yoyote, anasema: “Mtu mmoja alimwambia mwengine: ‘Baba yako amemfanyaje punda wako?’ Akasema: ‘Amemuuzo’ akiwa na maana amemuuza. Yule muulizaji akasema kwa mshangao: kwa nini umeweka o kwenye herufi ya mwisho? yule akajibu: si wewe umeweka o kwenye herufi ya mwisho!” Mtu wa namna hii utamwambiaje?
Basi tuangushie kipande cha mbingu, ikiwa wewe ni miongoni mwa wasemao kweli.
Aliwahadharisha na adhabu wakamdharau na wakasema iko wapi hiyo adhabu unayotutisha nayo, basi teremsha kipande cha mbingu kiwe ni adhabu, ukiwa ni mkweli wa madai yako.
Akasema: Mola wangu anajua zaidi mnayoyatenda na amri ni yake peke yake, akitaka ataileta haraka au ataicheleweshwa. Basi wakamkadhibisha, ikawashika adhabu ya siku ya kivuli. Hakika hiyo ilikuwa adhabu ya siku kubwa.
Mwenyezi Mungu (s.w.t) hakubainisha kivuli hicho. Wafasiri wanasema ni mawingu waliyoyafanya kivuli kutokana na joto lililowapata, kisha yakawanyeshea mvua ya moto iliyowaunguza wote.
Hakika bila shaka katika hayo ipo ishara, lakini wengi wao si wenye kuamini. Na hakika Mola wako ndiye Mwenye nguvu, Mwenye kurehemu.
Imetangulia kwa herufi zake, katika Aya 67 na 68 ya Sura hii na pia sehemu iliyopita.