16%

10

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TISA

وَتَفَقَّدَ الطَّيْرَ فَقَالَ مَا لِيَ لَا أَرَى الْهُدْهُدَ أَمْ كَانَ مِنَ الْغَائِبِينَ ﴿٢٠﴾

20. Na akawakagua ndege na akasema: Mbona simwoni Hud-hud au amekuwa miongoni mwa walio ghaibu.

لَأُعَذِّبَنَّهُ عَذَابًا شَدِيدًا أَوْ لَأَذْبَحَنَّهُ أَوْ لَيَأْتِيَنِّي بِسُلْطَانٍ مُّبِينٍ ﴿٢١﴾

21. Kwa yakini nitamwadhibu kwa adhabu kali au nitamchinja, au aniletee hoja iliyo wazi.

فَمَكَثَ غَيْرَ بَعِيدٍ فَقَالَ أَحَطتُ بِمَا لَمْ تُحِطْ بِهِ وَجِئْتُكَ مِن سَبَإٍ بِنَبَإٍ يَقِينٍ ﴿٢٢﴾

22. Basi hakukaa sana mara akasema: Nimegundua usiloligundua na nimekujia na habari za yakini kutoka Sabai.

إِنِّي وَجَدتُّ امْرَأَةً تَمْلِكُهُمْ وَأُوتِيَتْ مِن كُلِّ شَيْءٍ وَلَهَا عَرْشٌ عَظِيمٌ ﴿٢٣﴾

23. Hakika nimemkuta mwanamke anayewatawala na amepewa kila kitu na anacho kiti cha enzi kikubwa.

وَجَدتُّهَا وَقَوْمَهَا يَسْجُدُونَ لِلشَّمْسِ مِن دُونِ اللَّـهِ وَزَيَّنَ لَهُمُ الشَّيْطَانُ أَعْمَالَهُمْ فَصَدَّهُمْ عَنِ السَّبِيلِ فَهُمْ لَا يَهْتَدُونَ ﴿٢٤﴾

24. Nimemkuta yeye na watu wake wanalisujudia jua badala ya Mwenyezi Mungu; na shetani amewapambia vitendo vyao na akawazuilia njia. Kwa hivyo hawakuongoka.

أَلَّا يَسْجُدُوا لِلَّـهِ الَّذِي يُخْرِجُ الْخَبْءَ فِي السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ وَيَعْلَمُ مَا تُخْفُونَ وَمَا تُعْلِنُونَ ﴿٢٥﴾

25. Kwamba hawamsujudii Mwenyezi Mungu ambaye huyatoa yaliyofichikana katika mbingu na ardhi na huyajua mnayoyaficha na mnayoyadhihirisha.

اللَّـهُ لَا إِلَـٰهَ إِلَّا هُوَ رَبُّ الْعَرْشِ الْعَظِيمِ ﴿٢٦﴾

26. Mwenyezi Mungu hapana Mola ila Yeye Mola wa arshi tukufu.

MBONA SIMWONI HUD-HUD

Aya 20 – 26

MAANA

Na akawakagua ndege na akasema: Mbona simwoni Hud-hud au amekuwa miongoni mwa walio ghaibu. Kwa yakini nitamwadhibu kwa adhabu kali au nitamchinja, au aniletee hoja iliyo wazi.

Suleiman alikuwa na aina ya ndege wanaofuata amri yake, wakiwa wako huru sio ndani ya tundu. Siku moja alipokuwa anawakaguakagua, kama anavyokagua kamanda jeshi lake, akamkosa Hud-hud, na hakuwa amemruhusu kundoka. Akatishia – mbele ya ndege wengine - kumwadhibu; kama kumtia jela n.k. Au kumuua, ikiwa hatakuwa na hoja wazi ya udhuru wa kutoweka kwake.

Basi hakukaa sana mara akasema: Nimegundua usiloligundua.

Haukupita muda wa kutishia Suleiman ila alikuja Hud-hud na akasema: Nimegundua kitu muhimu usichokijua pamoja na upana wa elimu yakona nimekujia na habari za yakini kutoka Sabai.

Hakika nimemkuta mwanamke anayewatawala na amepewa kila kitu na anacho kiti cha enzi kikubwa.

Makusudio ya Sabai (Sheba) ni watu wanaonasibika na Sabai bin Yashjab bin Ya’rub bin Qahtan. Mwanamke (Malkia wa Sheba) alikuwa ni Bilqis bint Sharahil, aliyekuwa mfalme na kurithiwa na binti yake huyo, aliyekuwa akimiliki utajiri na starehe zote.

Alikuwa akikaa kwenye kiti cha hali ya juu na cha thamani, kikiwa kimepambwa na nyoyo za maskini na kupakwa jasho lao na damu zao. Ajabu ni kauli ya baadhi ya wafasiri waliosema kuwa kilikuwa kimeezekwa na kwamba upana wake ulikuwa ni futi 80 za mraba na kimo chake pia ni futi 80.

Nimemkuta yeye na watu wake wanalisujudia jua badala ya Mwenyezi Mungu; na shetani amewapambia vitendo vyao na akawazuilia njia. Kwa hivyo hawakuongoka.

Unaweza kuuliza : Ndege, wanyama na wadudu kwa maumbile yao wanajua chakula chao, kinywaji chao, kinachowadhuru na kinachowanufaisha. Wanajua hivyo na vinginevyo kwa sababu ndio nyenzo za kuishi kwao, kuhifadhi maisha yao na kuendela kuwepo.

Lakini kumtambua mume na mke katika binadamu, kujua kuwa kabila hili ni la wasabai na lile ni la Thamud, kujua hawa wanamuamini Mwenyezi Mungu na wale ni makafiri, haya yote hayalingani na maisha yao kwa umbali wala karibu.

Basi Hud-hud aliwezaje kujua jina la kabila, mwanamke anayewatawala na kwamba wao wanaabudu jua? Sisi wanadamu tu, hatuwezi kutambua baina ya mume na mke katika aina nyingi za ndege, wadudu na wanyama?

Jibu : Aya imethibitisha sifa hizi kwa Hud-hud wa Suleiman tu, jambo ambalo halilazimishi kuthibiti katika ndege wote au kwa Hud-hud wote; kama ambavyo kujua kiingereza kwa mtu fulani hakulazimishi kujua kiingereza kwa watu wote. Ama maarifa ya Hud-hud wa Suleiman kwa aliyoyatolea habari, sisi hatuna tafsiri yake isipokuwa matakwa ya Mwenyezi Mungu.

Kwamba hawamsujudii Mwenyezi Mungu ambaye huyatoa yaliyofichikana katika mbingu na ardhi na huyajua mnayoyaficha na mnayoyadhihirisha.

Makusudio ya yaliyofichikana hapa ni kheri za ulimwengu. Mwenyezi Mungu (s.w.t) huzitoa kwa waja wake kwa sababu zake za kimaumbile; kama mimea inayotoka ardhini kwa sababu ya mvua, kuzaana kwa sababu ya kupandishwa au kwa nyenzo nyingine za kielimu anazozitoa Mwenyezi Mungu kupitia mikononi mwa wataalamu na vifaa vyao.

Sababu na nyenzo zote hizi, Mwenyezi Mungu (s.w.t) ameziletea ibara ya mkono wa Mungu pale aliposema:

أَوَلَمْ يَرَوْا أَنَّا خَلَقْنَا لَهُم مِّمَّا عَمِلَتْ أَيْدِينَا أَنْعَامًا فَهُمْ لَهَا مَالِكُونَ ﴿٧١﴾

“Je, hawaoni kwamba tumewaumbia kutokana na iliyofanya mikono yetu wanyama wa mifugo, na wao wakawa wenye kuwamiliki?” (36:71).

Mwenyezi Mungu hapana Mola ila Yeye Mola wa arshi tukufu, ambaye haufananishwi ufalme wake wala ukuu wake na wa yeyote.

قَالَ سَنَنظُرُ أَصَدَقْتَ أَمْ كُنتَ مِنَ الْكَاذِبِينَ ﴿٢٧﴾

27.Akasema: Tutatazama, umesema kweli au uko katika waongo.

اذْهَب بِّكِتَابِي هَـٰذَا فَأَلْقِهْ إِلَيْهِمْ ثُمَّ تَوَلَّ عَنْهُمْ فَانظُرْ مَاذَا يَرْجِعُونَ ﴿٢٨﴾

28. Nenda na barua yangu hii na uwafikishie, kisha waache na utazame watarejesha nini.”

قَالَتْ يَا أَيُّهَا الْمَلَأُ إِنِّي أُلْقِيَ إِلَيَّ كِتَابٌ كَرِيمٌ ﴿٢٩﴾

29. Akasema: Enyi waheshimiwa! Hakika imeletwa kwangu barua tukufu.

إِنَّهُ مِن سُلَيْمَانَ وَإِنَّهُ بِسْمِ اللَّـهِ الرَّحْمَـٰنِ الرَّحِيمِ ﴿٣٠﴾

Imetoka kwa Suleiman, nayo ni: Kwa jina la Mwenyezi Mungu, Mwingi wa rehema, Mwenye kurehemu.

أَلَّا تَعْلُوا عَلَيَّ وَأْتُونِي مُسْلِمِينَ ﴿٣١﴾

31. Kwamba msinifanyie jeuri na fikeni kwangu mkiwa waislamu.

قَالَتْ يَا أَيُّهَا الْمَلَأُ أَفْتُونِي فِي أَمْرِي مَا كُنتُ قَاطِعَةً أَمْرًا حَتَّىٰ تَشْهَدُونِ ﴿٣٢﴾

Akasema: Enyi waheshimiwa! Nipeni ushauri katika jambo langu hili, kwani mimi sikati shauri lolote mpaka muhudhurie.

قَالُوا نَحْنُ أُولُو قُوَّةٍ وَأُولُو بَأْسٍ شَدِيدٍ وَالْأَمْرُ إِلَيْكِ فَانظُرِي مَاذَا تَأْمُرِينَ ﴿٣٣﴾

33. Wakasema: Sisi ni wenye nguvu na wakali wa vita, na amri iko kwako, basi tazama nini unaamrisha.

قَالَتْ إِنَّ الْمُلُوكَ إِذَا دَخَلُوا قَرْيَةً أَفْسَدُوهَا وَجَعَلُوا أَعِزَّةَ أَهْلِهَا أَذِلَّةً وَكَذَٰلِكَ يَفْعَلُونَ ﴿٣٤﴾

34. Akasema: Hakika wafalme wanapouingia mji wanauharibu na wanawafanya wale watukufu wake kuwa wanyonge, na hivyo ndivyo watendavyo.

وَإِنِّي مُرْسِلَةٌ إِلَيْهِم بِهَدِيَّةٍ فَنَاظِرَةٌ بِمَ يَرْجِعُ الْمُرْسَلُونَ ﴿٣٥﴾

35. Na mimi ninawapelekea zawadi ningoje watakayorudi nayo wajumbe.

NENDA NA BARUA YANGU HII

Aya 27 – 35

MAANA

Akasema: Tutatazama, umesema kweli au uko katika waongo.

Hud-hud alimpa habari Suleiman kuhusu watu wa Sabai, akamwambia tutachunguza maneno yako tuone kama yana ukweli.

Nenda na barua yangu hii na uwafikishie, kisha waache na utazame watarejesha nini.

Suleiman aliwaandikia barua watu wa Sabai akiwaita kwenye twaa yake na akampatia Hud-hud akamwamabia ifikishe hii kwa njia yoyote, kisha ujitenge nao sehmu ambayo utaweza kujua au kusikia wanasema nini na wanaafikiana nini, kisha urudi uniletee habari.

Akasema: Enyi waheshimiwa! Hakika imeletwa kwangu barua tukufu, imetoka kwa Suleiman, nayo ni: Kwa jina la Mwenyezi Mungu, Mwingi wa rehema, Mwenye kurehemu, kwamba msinifanyie jeuri na fikeni kwangu mkiwa waislamu.

Hud-hud alichukua barua na akaitupa mahali kwenye kasri ya malkia kwa namna ambayo inaweza kuonekana bila ya kujulikana aliyeileta, kama linavyojulisha neno ’imeletwa.’ Kisha Hud-hud akajiweka kando kuchunguza harakati za watu na mazungumzo yao; sawa na mwandishi wa habari.

Malkia alipoiona na akajua kilichoandikwa, aliwakusanya mawaziri na washauri, akawaonyesha na akaisifu kwa utukufu, kwa sababu mwenye barua hiyo ni mwenye cheo kikubwa cha heshima.

Bismillah ilikuwa ni sehemu ya barua hiyo ambayo aliifupisha kwa kutoa mwito wa utiifu bila ya utangulizi wala kuzidisha maneno. Hii ndio desturi ya mitume katika barua zao kwenda kwa wafalme. Mtume(s.a.w.w) alikuwa akifupiliza barua zake kwa wafalme kwa kusema: “Silimu utasalimika” baada ya bismillah na Alhamdu.

Akasema: Enyi waheshimiwa! Nipeni ushauri katika jambo langu hili, kwani mimi sikati shauri lolote mpaka muhudhurie.

Nipeni ushauri, maana mimi sipitishi jambo mpaka nipate rai yenu. Hii inaashiria kuwa demokrasia ya serikali ina mizizi yake katika historia ya mbali; kisha ikakua hadi ilivyo hivi sasa.

Wakasema: Sisi ni wenye nguvu na wakali wa vita, na amri iko kwako, basi tazama nini unaamrisha.

Walisema hivi kwa njia ya kujishasha, kutangaza nguvu zao na kumwachia majukumu yote malkia hata kama uamuzi wake utakuwa na mwisho mbaya.

Akasema: Hakika wafalme wanapouingia mji wanauharibu na wanawafanya wale watukufu wake kuwa wanyonge, na hivyo ndivyo watendavyo.

Mfasiri mmoja wa kisasa akifafanua Aya hii anasema: “Inajulikana kuwa ni tabia ya kimaumbile ya wafalme wanapoingia mji wanaeneza ufisadi na wanawaangusha viongozi na kuwafanya ni watu wa chini. Haya ndio mazowea yao wanayoyafanya.”

Ukweli ni kuwa ufisadi unaenea ardhini kwa kiasi cha nguvu za mfisadi, na unazidi kadiri nguvu zao zinavyozidi, wawe wafalme au si wafalme. Aya imewahusu kuwataja wafalme kwa sababu wao wanakuwa na nguvu zaidi kuliko wengine.

Uhakika wa mhalifu unajificha kwenye unyonge wake, na unajitokeza anapokuwa na guvu. Kwa hiyo ni makosa kuuweka uhakika wa mtu anapokuwa mnyonge.

Kuna badhi ya watu tunaowajua ambao walikuwa ni mashuhuri kwa takua wakati walipokuwa hohehahe, lakini mara tu walipopata madaraka wakaandamwa na tuhuma ambazo hazifutiki hata siku zikipita. Tunamuomba Mwenyezi Mungu atupe hidaya sisi na wao.

Kwa hiyo inatubainikia kuwa sifa ya ufisadi haihusiki kwa wafalme tu wala si tabia yao ya kimaumbile, vinginevyo ingelikuwa ni muhali kupatikana uadilifu na utengeneo kwao. Isipokuwa hiyo ni tabia ya wahalifu wenye nguvu; ni sawa iwe nguvu ya mali, cheo, akili au utawala na, kidini au kidunia. Wala hakuna wa kumzuia mkosefu mwenye nguvu isipokuwa dini tu.

Imam Ali(a.s) anasema: Mwenye uzowefu wa maisha na uelewa wa mambo anaweza akaona ujanja wa kukwepa amri ya Mwenyeezi Mungu akaachana nao; lakini asiyejilinda (na dini) anaitumia fursa hiyo (Nahjul balagha khutba 41).

Na mimi ninawapelekea zawadi ningoje watakayorudi nayo wajumbe.

Mawaziri na washauri walimwachia malkia amri ya vita au usalama. Kabla ya kuamua chochote aliona kwanza ampelekee Suleiman zawadi ya thamani kubwa, kisha aangalie, je, ataikubali au ataikataa. Akiikubali basi atakuwa anatafuta dunia sio dini. Kwa hiyo ataweza kumtengeneza kwa mali na kama ataikataa na kung’ang’ania kuwa tumwendee tukiwa wanyenyekevu, basi atakua ni katika wenye misingi ya risala na misimamo ya itikadi yao wakijitolea muhanga kwa kila hali. Watu wa namna hiyo haifai kuwapiga vita.

فَلَمَّا جَاءَ سُلَيْمَانَ قَالَ أَتُمِدُّونَنِ بِمَالٍ فَمَا آتَانِيَ اللَّـهُ خَيْرٌ مِّمَّا آتَاكُم بَلْ أَنتُم بِهَدِيَّتِكُمْ تَفْرَحُونَ ﴿٣٦﴾

36. Alipokuja kwa Suleiman, alisema: Hivi nyinyi mnanisaidia kwa mali? Aliyonipa Mwenyezi Mungu ni bora zaidi kuliko aliyowapa nyinyi, lakini nyinyi mnaifurahia zawadi yenu.

ارْجِعْ إِلَيْهِمْ فَلَنَأْتِيَنَّهُم بِجُنُودٍ لَّا قِبَلَ لَهُم بِهَا وَلَنُخْرِجَنَّهُم مِّنْهَا أَذِلَّةً وَهُمْ صَاغِرُونَ ﴿٣٧﴾

37. Rejea kwao! Kwa yakini tutawajia na majeshi wasiyoweza kuyakabili na hakika tutawatoa humo na hali wao wamekuwa madhalili na wanyonge.

قَالَ يَا أَيُّهَا الْمَلَأُ أَيُّكُمْ يَأْتِينِي بِعَرْشِهَا قَبْلَ أَن يَأْتُونِي مُسْلِمِينَ ﴿٣٨﴾

38. Akasema: Enyi wakuu wa baraza! Ni nani kati yenu atakayeniletea kiti chake cha enzi kabla hawajanijia nao wamekwisha salimu amri.

قَالَ عِفْرِيتٌ مِّنَ الْجِنِّ أَنَا آتِيكَ بِهِ قَبْلَ أَن تَقُومَ مِن مَّقَامِكَ وَإِنِّي عَلَيْهِ لَقَوِيٌّ أَمِينٌ ﴿٣٩﴾

39. Akasema afriti katika majini: Mimi nitakuletea kabla hujainuka mahala pako. Na mimi hakika nina nguvu, mwaminifu.

قَالَ الَّذِي عِندَهُ عِلْمٌ مِّنَ الْكِتَابِ أَنَا آتِيكَ بِهِ قَبْلَ أَن يَرْتَدَّ إِلَيْكَ طَرْفُكَ فَلَمَّا رَآهُ مُسْتَقِرًّا عِندَهُ قَالَ هَـٰذَا مِن فَضْلِ رَبِّي لِيَبْلُوَنِي أَأَشْكُرُ أَمْ أَكْفُرُ وَمَن شَكَرَ فَإِنَّمَا يَشْكُرُ لِنَفْسِهِ وَمَن كَفَرَ فَإِنَّ رَبِّي غَنِيٌّ كَرِيمٌ ﴿٤٠﴾

40. Akasema mwenye elimu ya Kitabu: Mimi nitakuletea kabla ya kupepesa jicho lako. Basi alipokiona kimewekwa mbele yake, alisema: Haya ni katika fadhila za Mola wangu, ili anijaribu, nitashukuru au nitakufuru. Na mwenye kushukuru kwa hakika anashukuru kwa manufaa ya nafsi yake na mwenye kukufuru kwa hakika Mola wangu ni Mkwasi, Mkarimu.

KITI CHA ENZI CHA BILQIS

Aya 36 – 40

MAANA

Alipokuja mjumbe kwa Suleiman, alisema: Hivi nyinyi mnanisaidia kwa mali? Aliyonipa Mwenyezi Mungu ni bora zaidi kuliko aliyowapa nyinyi, lakini nyinyi mnaifurahia zawadi yenu.

Ujumbe wa malkia ulifika kwa Suleiman ukiwa na zawadi ya thamani kubwa. Alipoiona alimwambia yule aliyekuja nayo kuwa mimi ninawaita kwa Mwenyezi Mungu na nyinyi mnanipa mali nami nina mali nyingi kama uonavyo; bali Mwenyezi Mungu amenineemesha kwa makubwa zaidi kuliko mali, ambayo ni: utume, elimu na kuutumia upepo majini na ndege. Hivi mnanikisia kuwa ni katika waabudu mali?

Kisa hiki kinatukumbusha makuraishi, wakati walipomtaka mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) aachane na jambo lake hili, wakamwambia:“Ukiwa, kwa jambo hili, unataka mali basi sisi tutakukusanyia mali mpaka uwe ni tajiri zaidi kuliko sisi, na kama unataka ufalme tutakupa.

Waliposhindwa naye wakakimbilia kwa ami yake Abu Talib ili amkinaishe mwana wa nduguye akubali mali, vinginevyo atapigwa vita. Mtume(s.a.w. w ) akasema maneno yake mashuhuru:“Wallah! Ewe Ami yangu! Lau wataliweka jua kuumeni kwangu na mwezi kushotoni kwangu kwamba niliache jambo hili sitaliacha mpaka alidhihirishe Mwenyezi Mungu au niangamie.”

Rejea kwao! Kwa yakini tutawajia na majeshi wasiyoweza kuyakabili na hakika tutawatoa humo na hali wao wamekuwa madhalili na wanyonge.

Maneno haya anaambiwa kiongozi wa msafara uliokuja na zawadi. Maana yake ni rejea wewe na wenzako na hiyo mliyokuja nayo. Wambie watu wako kuwa mimi nitakuja na jeshi langu la watu majini na ndege ambalo hamtaliweza si nyinyi wala wengene.

Hud-hud alikuwa amemwambia walivyosema: ‘Hakika wafalme wanapouingia mji wanauharibu na wanawafanya wale watukufu wake kuwa wanyonge.’ Kwa hiyo Suleiman akasisitiza kauli ya malkia kwa kusema: ‘Tutawatoa humo na hali wao wamekuwa madhalili na wanyonge.’

Akasema: Enyi wakuu wa baraza! Ni nani kati yenu atakayeniletea kiti chake cha enzi kabla hawajanijia nao wamekwishasalimu amri.

Msafara uliporeja kutoka kwa Suleiman na wakampa habari Malkia kwa waliyoyaona na kuyasikia, aliona hapana budi isipokuwa kusikiliza na kutii. Akaelekea kwa Suleiman pamoja na wapambe wake. Akakiacha kiti cha enzi kikilindwa na askari.

Suleiman alipojua kufika Bilqis alipendelea kumuonyesha miujiza ya kufahamisha utume wake na ukuu wake; na kwamba muujiza huo uwe ni kukichukua kiti chake ambacho ndicho kinachoonyesha enzi yake na umalkia wake. Ndipo akauliza wale waliokuwapo mbele yake, ni nani atakayeniletea?

Akasema afriti katika majini: Mimi nitakuletea kabla hujainuka mahala pako. Na mimi hakika nina nguvu, mwaminifu.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) alimtiishia Suleiman upepo ukienda kwa amri yake. Bila shaka huu ni mujiza. Akamtiisha ndege wakifuata amri yake.

Nao pia ni muujiza. Vile vile Mwenyezi Mungu alimuhusisha na baadhi ya askari binadamu na majini, wakifanya maajabu kulingana na wakati wo. Walikuwa wakiandamana na jeshi la Suleiman, wakisaidiana kumshinda adui; kama wafanyavyo wataalamu wa kiufundi hivi sasa.

Hilo linaashiriwa na matakwa ya Suleiman kwao kuwaletea kiti cha enzi cha Bilqis katika muda mchache na hali anajua kuwa kiko masafa ya mbali sana. Mmoja wa majini akamwambia nitakuletea kikiwa salama, kama kilivyo ukiwa wewe umekaa hapa.

Lakini akasema mwenye elimu ya Kitabu: Mimi nitakuletea kabla ya kupepesa jicho lako.

Ikawa ushindi ni wa huyu ambapo, kwa uweza wa elimu alio nao, aliweza kukileta kiti wakati uliotakiwa.

Haya ndiyo yaliyofahamishwa na dhahiri ya Aya. Ama maswali ya kuwa ni nani huyo aliyekuwa na elimu ya kitabu? Je, alikuwa ni Malaika, Khidhr au mja mwema katika binadamu aliyeitwa Asif bin Barkhiya Na kwamba je yeye alikuwa akijua jina kuu la Mwenyezi Mungu au ni elimu gani hiyo aliyoitumia?

Maswali yote haya na mengineyo mengi, jibu lake liko kwa Mola wangu. Kwa sababu Aya haikuweka wazi hilo, wala hakuna Hadith sahih iliyothibiti.

Uwezekano wa karibu, tunaoweza kusema ni kuwa yeye hakuwa katika majini, kwa sababu alimzidi jini Afrit, kama ilivyoweka wazi Aya, kwamba yeye alikileta kiti kabla ya kupepesa jicho. Miujiza inayodhihiri kwa mitume, pia inadhihiri kwa wale ambao wamechaguliwa na mitume kwa idhini ya Mwenyezi Mungu.

La muhimu kujua, katika tukio hili, ni kwamba Bilqis aliyekuwa na madaraka makubwa na neema, alimnyenyekea Suleiman.

Basi alipokiona kimewekwa mbele yake, alisema: Haya ni katika fadhila za Mola wangu, ili anijaribu, nitashukuru au nitakufuru.

Makusudio ya kukufuru hapa ni kukufuru neema, sio kumkufuru Mwenyezi Mungu. Suleiman hawezi kuzikufuru neema za Mola wake, kwa sababu yeye ni maasum. Alisema haya kama utangulizi wa kusema:

Na mwenye kushukuru kwa hakika anashukuru kwa manufaa ya nafsi yake na mwenye kukufuru kwa hakika Mola wangu ni Mkwasi, Mkarimu.

Katika maana ya Aya hii ni ile isemayo:

إِنْ أَحْسَنتُمْ أَحْسَنتُمْ لِأَنفُسِكُمْ وَإِنْ أَسَأْتُمْ فَلَهَا ﴿٧﴾

“Mkifanya uzuri mnajifanyia wenyewe na mkifanya ubaya mnajifanyia wenyewe.” Juz. 15 (17:7).