6%

22

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA TATU

Sura Ya Hamsini Na Tano: Surat Ar-Rahman. Ina Aya 78.

بِسْمِ اللَّهِ الرَّحْمَٰنِ الرَّحِيمِ

Kwa jina la Mwenyezi Mungu Mwingi wa rehema Mwenye kurehemu.

الرَّحْمَـٰنُ ﴿١﴾

1. Mwingi wa Rehema.

عَلَّمَ الْقُرْآنَ ﴿٢﴾

2. Amefundisha Qur’an.

خَلَقَ الْإِنسَانَ ﴿٣﴾

3. Amemuumba mtu,

عَلَّمَهُ الْبَيَانَ ﴿٤﴾

4. Akamfundisha ubainifu.

الشَّمْسُ وَالْقَمَرُ بِحُسْبَانٍ ﴿٥﴾

Jua na mwezi ni kwa hisabu.

وَالنَّجْمُ وَالشَّجَرُ يَسْجُدَانِ ﴿٦﴾

6. Na mimea yenye kutambaa, na miti, inanyenyekea.

وَالسَّمَاءَ رَفَعَهَا وَوَضَعَ الْمِيزَانَ ﴿٧﴾

7. Na mbingu ameziinua, na ameweka mizani,

أَلَّا تَطْغَوْا فِي الْمِيزَانِ ﴿٨﴾

8. Ili msidhulumu katika mizani.

وَأَقِيمُوا الْوَزْنَ بِالْقِسْطِ وَلَا تُخْسِرُوا الْمِيزَانَ ﴿٩﴾

9. Na wekeni mizani kwa haki, wala msipunje katika mizani.

وَالْأَرْضَ وَضَعَهَا لِلْأَنَامِ ﴿١٠﴾

10. Na ardhi ameiweka kwa ajili ya viumbe.

فِيهَا فَاكِهَةٌ وَالنَّخْلُ ذَاتُ الْأَكْمَامِ ﴿١١﴾

11. Humo yamo matunda na mitende yenye mafumba.

وَالْحَبُّ ذُو الْعَصْفِ وَالرَّيْحَانُ ﴿١٢﴾

12. Na nafaka zenye makapi, na mrehani.

فَبِأَيِّ آلَاءِ رَبِّكُمَا تُكَذِّبَانِ ﴿١٣﴾

13. Basi ni ipi katika neema za Mola wenu mnayoikanusha nyinyi wawili?

AMEMUUMBA MTU AKAMFUNDISHA UBAINIFU

Aya 1 – 13

MAANA

Mwingi wa Rehema

Katika sura hii Mwenyezi Mungu (s.w.t) ametaja neema kadhaa kwa waja wake. Ameanza kwa kwa neno Mwingi wa rehma, kwa vile linaashiria neema na fadhila.

Amefundisha Qur’an.

Yaani ameiteremsha. Qur’an inafana na ulimwengu katika njia kadhaa; miongoni mwazo ni hizi zifutazo:

• Qur’an ni katika maneno ya Mwenyezi Mungu Mtukufu na ulimwengu umepatakina kwa neno ‘Kuwa.’

• Kila moja kati ya Qur’an na ulimwengu unafahamisha kwa hisia uwezo na ukuu wa Mwenyezi Mungu. Ulimwengu unaonekana kwa macho na Qur’an inasikiwa kwa masikio. Ndio mmoja wa waumini akasema kuwa Mwenyezi Mungu ana vitabu viwili: kimoja kinasomwa na kusikiwa nacho ni Qur’an na kingine kinaonekana na kuguswa nacho ni ulimwengu.

• Ulimwengu na Qur’an ni katika uweza wa Mwenyezi Mungu pekee yake hakuna anayeweza kuleta mafano wake.

• Qur’an na ulimwengu ni katika neema kubwa aliyoileta Mwenyezi Mungu (s.w.t) kwa mtu. Ananeemeka na heri za ardhi na mbingu na anaongoka kwa Qur’an kueleka kwenye raha na wema wa nyumba mbili.

Kwa hiyo Mwenyezi Mungu (s.w.t) amemneemesha mtu kwa jua, mwezi, ardhi, mvua, upepo, mimea, miti, wanyama na mengineyo yasiyokuwa na mwisho.

Amemuumba mtu. Akamfundisha ubainifu.

Makusudio ya ubainifu ni kila linalofahamisha makusudio ya kutamka, hati kuchora au ishara. Hata hivyo kusema, ndio kiungo muhimu zaidi cha ubainifu na chombo chake ni ulimi ambao ndio kiungo kitiifu zaidi kwa mtu, chenye harakati nyingi zaidi na chepesi. Hakijui kuchoka wala kutaabika. Sifa hizi hazipatikani katika viungo vingine.

Ubainifu, hasa maneno, ni katika neema kuu zaidi. Kwayo mtu anaeleza makusudio yake, kufahamu makusudio ya wengine, kujibizana nao kwa upendo, kutekeleza haja zake na za wengine.

Ubainifu unabainisha kufuru na imani, inajikita ilimu, fasihi na fani mbalimbali na kujulikana dini. Baadhi ya ulama wanasema: Kila matumizi ya ilimu yanaelezea ubainifu. Hakuna kitu chochote ila kinatumia ilimu.

Jua na mwezi ni kwa hisabu.

Yaani vinakwenda kwa nidhamu kamili na kanuni thabiti. Kwa nidhamu hii ndio yanahifadhika maisha katika ardhi, ikatofautiana misimu na zikajulikana nyakati.

Na mimea yenye kutambaa, na miti, inanyenyekea.

Neno ‘mimea yenye kutambaa’ tumelifasiri kutokana na neno la kiarabu annajm kama walivyosema hivyo wafasiri wengi. Kwa sababu Mwenyezi Mungu (s.w.t) amelitaja pamoja na mti kwa mkabala wa jua na mwezi.

Maana ya kusujudi ni kuwa yote hiyo inafahamisha kuweko Mwenyezi Mungu na ukuu wake kutokana na usanii wa hali ya juu kabisa. Tazama kifungu cha maneno:

وَإِن مِّن شَيْءٍ إِلَّا يُسَبِّحُ بِحَمْدِهِ ﴿٤٤﴾

Na pana kila kitu ila kinamtakasa kwa sifa zake.’ katika Juz. 15 (17:44)

Na mbingu ameziinua, na ameweka mizani.

Makusudio ya mbingu hapa ni kila kilichomo ndani yake miongoni mwa sayari. Na mizani ni kila hakika ya vitu na vipimo vyake vinavyojulikana; viwe vya kimaada kama vile makopo, mita na mizani au vya kimaana kama vile wahyi na misingi ya kiakili na maumbile.

Vile vile makusudio ni kuwa ulimwengu huu wa maajabu umepangika vizuri. Kwa sababu Mwenyezi Mungu (s.w.t) ameziweka sayari kwenye sehemu zake zinapotakikana; kiasi ambacho lau kama sayari itasogea kidogo tu zaidi ya sehemu yake ilipopangiwa, basi nidhamu ya uliwengu ingelivurugika na kubadilika kila kitu.

Pia hakuna jamii inayoweza kuwa sawa isipokuwa kwa kufuata mizani ya maadili.

Ili msidhulumu katika mizani. Na wekeni mizani kwa haki, wala msipunje katika mizani.

Dhulma ni kupora na kunyang’anya, kupunja ni kutotekeleza haki kwa anayestahiki na kuweka mizani kwa haki ni kutojipunja wala kuwapunja wengine. Ni muhali kupatikana utulivu katika jamii itakayopuuza haki na uadilifu.

Kwa muhtasari ni kuwa Aya hii, pamoja na ufupi wake, ni kuwa imeashiria yale yanayotimiza na yanayoweka nidhamu ya ulimwengu na jamii. La kwanza ni nidhamu ya ulimwengu aliyoitimiza Mwenyezi Mungu (s.w.t) kwa ukamilifu. Ya pili ni nidhamu ya sharia aliyoiwajibisha Mwenyezi Mungu (s.w.t) kwa waja wake, waichunge na waitekeleze kwa mujibu wake.

Na ardhi ameiweka kwa ajili ya viumbe kuwa ni tandiko na kutafutia maisha.Humo yamo matunda mengi na vyakula vinginevyo na vinywajina mitende yenye mafumba yanayopasuka na kutoa matunda yanapofikia kuiva.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) amehusisha kutaja mti wa mtende kutokana na umuhimu wake kwa waarabu wakati huo[8] .

Na nafaka zenye makapi.

Nafaka ni kwa ajili ya chakula cha binadamu na makapi ni kwa ajili ya wanyama.

Na mrehani kwa ajili ya manukato na kujipamba.

Mrehani ni ule mti maarufu unaoitwa hivyo, lakini imesemekena kuwa makusudio yake hapa ni kila mmea wenye harufu nzuri.

Chakula, matunda na maua yote hayo ni katika heri za ardhi na baraka zake alizowaneemesha Mwenyezi Mungu waja wake, lakini wao wanaishi kwa kuziharibu na ufisadi.

Basi ni ipi katika neema za Mola wenu mnayoikanusha nyinyi wawili?

Wawili hapa anaambiwa jinni na mtu kwa dalili ya kauli yake Mwenyezi Mungu: ‘Kwa ajili ya viumbe,’ inayochanganya aina mbili hizi za viumbe, na pia kauli itakayokuja badae. “Tutawakusudia enyi wazito wawili.”

Maana ni kuwa, je anaweza kukana yeyote, katika majini na watu, neema alizozitaja Mwenyezi Mungu (s.w.t)? Vipi anaweza kuzikataa na yeye yumo ndani yake?

خَلَقَ الْإِنسَانَ مِن صَلْصَالٍ كَالْفَخَّارِ ﴿١٤﴾

Amemuumba mtu kwa udongo mkavu kama uliookwa.

وَخَلَقَ الْجَانَّ مِن مَّارِجٍ مِّن نَّارٍ ﴿١٥﴾

15. Na akawaumba majini kwa ulimi wa moto.

فَبِأَيِّ آلَاءِ رَبِّكُمَا تُكَذِّبَانِ ﴿١٦﴾

16. Basi ni ipi katika neema za Mola wenu mnayoikanusha nyinyi wawili?

رَبُّ الْمَشْرِقَيْنِ وَرَبُّ الْمَغْرِبَيْنِ ﴿١٧﴾

17. Mola wa mashariki mbili na wa magharibi mbili.

فَبِأَيِّ آلَاءِ رَبِّكُمَا تُكَذِّبَانِ ﴿١٨﴾

18. Basi ni ipi katika neema ya Mola wenu mnayoikanusha nyinyi wawili?

مَرَجَ الْبَحْرَيْنِ يَلْتَقِيَانِ ﴿١٩﴾

19. Anaziendesha bahari mbili zikutane;

بَيْنَهُمَا بَرْزَخٌ لَّا يَبْغِيَانِ ﴿٢٠﴾

20. Baina yao kipo kizuizi, haziingiliani.

فَبِأَيِّ آلَاءِ رَبِّكُمَا تُكَذِّبَانِ ﴿٢١﴾

21. Basi ni ipi katika neema ya Mola wenu mnayoikanusha nyinyi wawili?

يَخْرُجُ مِنْهُمَا اللُّؤْلُؤُ وَالْمَرْجَانُ ﴿٢٢﴾

22. Katika hizo bahari mbili zinatoka lulu na marijani.

فَبِأَيِّ آلَاءِ رَبِّكُمَا تُكَذِّبَانِ ﴿٢٣﴾

23. Basi ni ipi katika neema ya Mola wenu mnayoikanusha nyinyi wawili?

وَلَهُ الْجَوَارِ الْمُنشَآتُ فِي الْبَحْرِ كَالْأَعْلَامِ ﴿٢٤﴾

24. Na ni vyake Yeye hivi viendavyo baharini vilivyoundwa kama vilima.

فَبِأَيِّ آلَاءِ رَبِّكُمَا تُكَذِّبَانِ ﴿٢٥﴾

25. Basi ni ipi katika neema ya Mola wenu mnayoikanusha nyinyi wawili?

كُلُّ مَنْ عَلَيْهَا فَانٍ ﴿٢٦﴾

26. Kila kilicho juu yake kitatoweka.

وَيَبْقَىٰ وَجْهُ رَبِّكَ ذُو الْجَلَالِ وَالْإِكْرَامِ ﴿٢٧﴾

28. Na itabakia dhati ya Mola wako Mwenye utukufu na ukarimu.

فَبِأَيِّ آلَاءِ رَبِّكُمَا تُكَذِّبَانِ ﴿٢٨﴾

28. Basi ni ipi katika neema ya Mola wenu mnayoikanusha nyinyi wawili?

يَسْأَلُهُ مَن فِي السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ كُلَّ يَوْمٍ هُوَ فِي شَأْنٍ ﴿٢٩﴾

29. Vinamwomba Yeye vilivyo katika mbingu na ardhi. Kila siku Yeye yumo katika mambo.

فَبِأَيِّ آلَاءِ رَبِّكُمَا تُكَذِّبَانِ ﴿٣٠﴾

30. Basi ni ipi katika neema ya Mola wenu mnayoikanusha nyinyi wawili?

KILA SIKU YUMO KATIKA MAMBO

Aya 14 – 30

MAANA

Amemuumba mtu kwa udongo mkavu kama uliookwa.

Makusudio ya mtu ni Adam baba wa watu.

Katika Juz. 14 (15: 26 – 31) Tumechanganya Aya nne; ambazo ni:

وَلَقَدْ خَلَقْنَا الْإِنسَانَ مِن صَلْصَالٍ مِّنْ حَمَإٍ مَّسْنُونٍ ﴿٢٦﴾

“Na hakika tulimuumba mtu kutokana na udongo mkavu kwa matope meusi yenye kufinyangwa.” Juz. 14 (15:26).

وَهُوَ الَّذِي خَلَقَ مِنَ الْمَاءِ بَشَرًا ﴿٥٤﴾

“Yeye ndiye aliyemuumba mtu kutokana na maji” Juz. 19 (25:54).

كَمَثَلِ آدَمَ خَلَقَهُ مِن تُرَابٍ ثُمَّ قَالَ لَهُ كُن فَيَكُونُ ﴿٥٩﴾

“Ni kama mfano wa Adam; alimuumba kutokana na udongo, kisha akamwambia kuwa akawa.” Juz.3 (3:59)

هُوَ الَّذِي خَلَقَكُم مِّن طِينٍ ﴿٢﴾

“Yeye ndiye aliyewaumba kwa udongo.” Juz. 7 (6:2)

Huko tulithibitisha kuwa hakuna njia ya kujua asili ya mtu isipokuwa kwa wahyi utokao kwa aliyemuumba mtu. Na katika Juz. 8 (7:11) tumedokeza majibu ya nadharia ya Darwin.

Na akawaumba majini kwa ulimi wa moto.

Mara nyingi tumesema kuwa tunaamini kuweko majini kwa vile wahyi umeyathibitisha na akili haikani. Katika kufasiri kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: “Na majini tumewaumba kwa moto wenye joto kali.”

Juz. 14 (15:27), tulisema kuwa wataalamu wamegundua aina ya vidudu ambavyo haviishi isipokuwa katika hewa ya sumu na aina nyingine haiwezi kupata uhai isipokuwa kwenye visima vya mafuta na vitu vinavyowaka.

Maana ni kuwa katika viumbe hai kuna vinavyotokana na maji na vinavyotokana na moto. Vile vile kuna vilivyo katika ulimwengu wa kuonekana na vilivyo kwenye ulimwengu wa ghaibu.

Basi ni ipi katika neema za Mola wenu mnayoikanusha nyinyi wawili?

Ni kwa kuumbwa mtu kutokana na udongo au kuumbwa jini kutokana na ulimi wa moto?

Maana ya ulimi wa moto ni moto bila ya moshi. Nahofia wale wanaolazimisha wahyi uafikiane na sayansi wasiseme kuwa ulimi wa moto ni ishara ya kugunduliwa petroli na sipiriti!

Kukaririka kauli yake Mwenyezi Mungu: “Basi ni ipi katika neema za Mola wenu mnayoikanusha nyinyi wawili,” ni kwa kukaririka sababu ambazo ni neema zenye kuulizwa; sawa na unavyoweza kumwambia uliyemsaidia mambo tofauti: Nimekuokoa na adui yako aliyekuweza na nikakupa pesa, sasa ni lipi kati ya haya mawili unalolikataa? Tena nikakusomeshea watoto wako na nikakujengea nyumba, ni lipi kati ya haya mawili unalolikataa?

Kwa hiyo basi hakuna kukaririka wala msisitizo wa kitu kimoja; isipokuwa ni vitu mabalimbali.

Mola wa mashariki mbili na wa magharibi mbili.

Makusudio ya mashariki mbili na magharibi mbili ni mashariki ya jua na mwezi na magahribi ya jua na mwezi. Maana haya ndiyo yanayokuja haraka akilini na si mengineyo.

Hakuna mwenye shaka kwamba uhai mwingi unahitajia kuangaziwa na kuchwewa na jua na mwezi; bali wamesema kuwa maisha hayayezi kuwa ardhini bila ya hivyo.

Basi ni ipi katika neema ya Mola wenu mnayoikanusha nyinyi wawili?

Je, neema ya kuangaziwa au ya kuchwewa.

Anaziendesha bahari mbili zikutane; baina yao kipo kizuizi, haziingiliani.

Neno Bahari tumelifasiri kutokana na neno la kiarabu bahr lenye maana ya maji mengi, yawe tamu au chumvi. Makusudio ya bahari mbili hapa ni maji ya bahari na ya mito.

Makusudio ya kizuizi hapa ni uweza wa Mwenyezi Mungu unaofanya zisichanganyike zikageuzana. Tazama tafsiri ya kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu:

وَهُوَ الَّذِي مَرَجَ الْبَحْرَيْنِ هَـٰذَا عَذْبٌ فُرَاتٌ وَهَـٰذَا مِلْحٌ أُجَاجٌ وَجَعَلَ بَيْنَهُمَا بَرْزَخًا وَحِجْرًا مَّحْجُورًا ﴿٥٣﴾

“Naye ndiye aliyezichanganya bahari mbili, hii ni tamu mno na hii ni chumvi sana, na akaweka kinga kati yake na kizuizi kizuiacho.” Juz. 19 (25:53).

Bahari zina manufaa mengi na faida kwa viumbe wa Mwenyezi Mungu na waja wake.

Basi ni ipi katika neema ya Mola wenu mnayoikanusha nyinyi wawili?

Ni neema ya bahari au mito au nyingineyo?

Katika hizo bahari mbili zinatoka lulu na marijani.

Wafasiri wengi wametatizika kufasiri Aya hii. Hilo ni kwa kuwa wao walikata kauli kuwa lulu haipatikanai isipokuwa kwenye maji chumvi tu, na Mwenyezi Mungu anasema kuwa inatoka kwenye maji chumvi na maji tamu. Wakatafuta visingizio vya kuleta taawili.

Lakini Razi amesema: “Inawezekana vipi kuamua kuwa lulu inatoka baharini tu, ikiwa waliotembea wameshindwa hata kuyajua yaliyoko nchi kavu wataweza kujua yaliyoko majini?

Ile kuwa wazamiaji hawakutoa lulu isipokuwa baharini, hakulazimishi kuwa haiwezi kupatikana kwingine. Dhahiri ya maneno ya Mwenyezi Mungu ndiyo inayofaa kuzingatiwa kuliko maneno ya watu.”

Sisi tunaunga mkono mantiki hii ya sawa, na inaungwa mkono na Sheikh Maraghi katika tafsiri yake aliposema: “Imethibitika katika ugunduzi wa sasa kwamba, kama inavyotolea lulu kutoka katika maji chumvi, vilevile inaweza kutolewa katika maji tamu. Pia marijani; ingawaje sana sana huwa zinatoka kwenye maji chumvi.”

Basi ni ipi katika neema ya Mola wenu mnayoikanusha nyinyi wawili?

Je ni neema hii ndio manyoikadhibisha?

Shia Imamiya wameambiwa kuwa wao wanaitakidi kuwa makusudio ya bahari mbili ni Ali na Fatima, kizuizi ni Muhammad(s.a.w. w ) na lulu na marijani ni Hasan na Husein.

Mimi kwa wasifu wangu kuwa ni mshia ninakana kabisa madai haya wanayobandikizwa shia na kwamba wao wanaharamisha tafsiri ya undani. Ikiwa atapatikana mwenye rai hiyo basi itakuwa ni rai yake binafsi.

Hii pia inapatikana kwa sunni; kama ilivyoelezwa katika tafsiri zao; ikiwemo Adduril manthur ya Suyut wa madhehebu ya Shafiy, anasema: “Ametoa Ibn Mardawayh kutoka kwa Ibn Abbas, kwamba bahari mbili ni Ali na Fatima, kizuizi ni Nabii na lulu na marijani ni Hasan na Husein. Vile vile ameyatoa haya kutoka kwa Anas bin Malik.”

Ya kushangaza zaidi kuliko haya ni yale aliyoyanukuu Ismail Haqqi, kati- ka tafsiri yake Ruhul-bayan, kutoka kwa baadhi ya ulama kuwa nusu ya wanane aliowaashiria Mwenyezi Mungu katika kauli yake:

وَيَحْمِلُ عَرْشَ رَبِّكَ فَوْقَهُمْ يَوْمَئِذٍ ثَمَانِيَةٌ ﴿١٧﴾

“Na wanane juu ya hawa watachukua Arshi ya Mola wako,” (69:17),

Kuwa ni Abu Hanifa, Shafiy, Malik na Hambali!

Na ni vyake Yeye hivi viendavyo baharini vilivyoundwa kama vilima.

Maana ni kuwa vyombo vya majini vinatembea kwa manufaa ya watu.

Umetangulia mfano wake katika Aya kadhaa ikiwemo Juz. 21 (31:31).

Basi ni ipi katika neema ya Mola wenu mnayoikanusha nyinyi wawili?

Je, ni kule kuumbwa kwenu na kuumbwa mali ghafi ya vyombo vya majini au ni kwa kutembea majini n.k.?

Kila kilicho juu yake kitatoweka. Na itabakia dhati ya Mola wako Mwenye utukufu na ukarimu.

Yeye ambaye imetukuka heshima yake, yuko hai kwa dhati yake; kama ambavyo amepatikana kwa dhati yake, na kila mwenye kupatikana kwa dhati hawezi kutoweka wala kubadilika. Yeye Mwenyezi Mungu (s.w.t) ndio chimbuko la uhai na anayeutoa.

Basi ni ipi katika neema ya Mola wenu mnayoikanusha nyinyi wawili?

Je, ni utukufu wake au ukarimu wake na yasiyokuwa hayo?

MWENYEZI MUNGU NA MTU NA IBN AL-ARABIY

Muhyiddin Ibn Al-arabiy, katika Futuhatul-Makkiyya kuhusiana na kauli yake Mwenyezi Mungu: ‘Mwenye utukufu na ukarimu,’ ana maneno haya yafutayo:

“Hakika Mwenyezi Mungu ameunganisha ukarimu baada ya utukufu, kwa sababu mtu akisikia wasifa wa Mwenyezi wa utukufu bila ya ukarimu, basi atakata tamaa ya kufika kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu, kwa vile hajioni kuwa ana nafasi yoyote mbele ya Mtukufu.

“Ndio akaondoa Mwenyezi Mungu dhana hii, kwa mtu, kwa kuuunganisha ukarimu kwenye utukufu, kwa sababu maana ya sifa mbili hizi ni kuwa Mwenyezi Mungu hata kama ni mtukufu, lakini Yeye anamkirimu mtu na kumwangalia kwa jicho la huruma kwa kumfadhili na kumkirimu.

“Mtu akijua nafasi yake hii kwa Mwenyezi Mungu, basi anahisi ukarimu wake na kutambua kuwa lau asingelikuwa ni mkarimu asingejishughulisha na usaidizi huu. Hapo anazidi kumtukuza Mwenyezi Mungu kwa sababu naye anajikuta ni mtukufu mbele ya Mwenyezi Mungu.”

Tunaunganisha kauli ya Ibn Al-arabi, kwamba mwenye kukana kuweko Mwenyezi Mungu atakuwa ameiangusha nafsi na mazingatio yote na kuikana dhati yake na utukufu wake bila ya kutaka. Kwa sababu atakuwa amemkosea yule aliyemfanya aweko na kumtukuza, na atastahiki adhabu:

وَمَن جَاءَ بِالسَّيِّئَةِ فَلَا يُجْزَى الَّذِينَ عَمِلُوا السَّيِّئَاتِ إِلَّا مَا كَانُوا يَعْمَلُونَ ﴿٨٤﴾

“Na Mwenye kutenda uovu hawalipwi wanaotendao uovu ila yale waliyokuwa wakiyatenda.” Juz. 20 (28:84).

Vinamwomba Yeye vilivyo katika mbingu na ardhi.

Makusudio ya kuomba hapa ni mahitajio. Maana ni kuwa viumbe vyote vinamuhitajia Mwenyezi Mungu katika kubakia kwake na katika hali zote; kama vinavyomuhitajia katika asili ya kuweko kwake, na kwamaba Yeye anavisaidia kuweko, lau anaviacha kwa muda wa kupepesa jicho tu, kusingelikuwa na kitu.

Kila siku Yeye yumo katika mambo.

Makusudio ya siku hapa ni wakati bila ya kuwa na mpaka. Maana ni kuwa hakuna chochote kinachokuwa ila kinagura kutoka hali moja hadi nyingine wakati wote. Ndio maana ikasemwa: “Ni muhali kudumu hali.” Na vyenye kuweko vinamuhitajia Mwenyezi Mungu katika hali zote. Mwenye nguvu anamhitajia Yeye katika kubakia nguvu zake, na mdhaifu pia anamhitajia kuondoa udhaifu wake.

Hiyo haimaanishi kuwa mtu aache kuhangakia na kufanya kazi kwa kumwachia Mwenyezi Mungu, hapana! Mwenyezi Mungu (s.w.t.) ameamrisha na akahimiza kuhangaika; ndiye aliyesema:

وَأَن لَّيْسَ لِلْإِنسَانِ إِلَّا مَا سَعَىٰ ﴿٣٩﴾

“Na ya kwamba hatapata mtu ila aliyoyahangaikia.” (53:39).

Maana yake hasa ni kuwa mtu afanye matendo kwa kuamini kuwa nyuma yake kuna nguvu iliyojificha ikimsaidia kufanya kazi na kumwandalia njia ya kufaulu.

Basi ni ipi katika neema ya Mola wenu mnayoikanusha nyinyi wawili?

Je, ni huko kuwasaidia kila wakati au ni neema nyinginezo?