25%

2

UTENZI WA IMAM HUSEN

UTENZI WA KISA CHA SAYYIDNA HUSSEIN

544. Nimtazame ambaye, Huseni ampendaye, Nimuangushe rasiye, Na wote wake waladi

545. Na jamii mali yake, Niyatwae niyateke, Dimishiki nipeleke, Ni huo yangu mradi

546. Basi semani upesi, Nijue yenu jinsi, Wote wakenika rasi, Wa khofu nyingi fuadi

547. Jamii wakiolana, Khatimaye wakanena, Aliye bwana ni bwana, Huseni au Yazidi

548. Kwa kula atawalaye, Tutafuata eziye, Hatuna tukataaye, Ali yoyote Sayyidi

549. Kusikiakwe adui, Akaruka kama chui, Kawambia hamjui, Kwamba nyinyi mu abidi

550. Na Yazidi bwana wenu, Aliyemiliki kwenu, Ni haba akili zenu, Ujinga unawazidi

551. Kwamba mmemridhia, Zidi bunu Muawia, Afadhali kutulia, Make mtabaradi

552. Ambaye hakumtaka, Yuwatafuta hilaka, Mimbarini akishuka, Hayo akisha radidi

553. Kitoka msikitini, Akenda kwa Nuamani, Akampa anuwani, Itokayo kwa Yazidi

554. Alipokwisha ijua, Nuamani kamkua, Sisi hatuna uluwa, Wala hatu maSayyidi

555. Ila sisi tu raia, Twawapenda wote pia, Wala hatutakimbia, Kwa amri ya Wadudi

556. Kusikiakwe makali, Abidallahi jahili, Akamnyang'anya mali, Mangi yasiyo idadi

557. Beti asimbakiye, Ila ni yeye rohoye, Sababu asimwambie, Nimpendaye Yazidi

558. Kashukuru Nuamani, Na kuhimidi Manani, Baada sayo yuani, Abidallahi karudi

559. Kenda nyumba ya hukumu, Akawatoa kaumu, Katafuta Mselemu, Katika yote biladi

560. Na Mselemu sikia, Kipindi kilipongia, Ajili kukimbilia, Beti 'l masjidi

561. Akenda akaadhini, Kakaa msikitini, Wote walio mjini, Asimuone wahidi

562. Kasali yeye pekee, Hapo amfuataye, Kataajabu rohoye, Ajabu kubwa shadidi

563. Kwisha kusali yuani, Katoka msikitini, Kamuona ghulimani, Karibu amekaidi

573. Allahumma niauni, Unitie nusurani, Na jeshi ya maluuni, Bi shufaa Muhamadi

564. Mselemu akanena, Nambia ewe kijana, Leo mji nauona, Jamii wote baridi

565. Watu wametaharaki, Gharibi na mashariki, Kusali hawakutaki, Kijana akaradidi

566. Kijana akakalimu, Wailaka Mselemu, Huoni hawa kaumu, Walivyo kujizadidi

567. Jamii wamekuhuni, Hawakutaki mjini, Wala nduguyo Huseni, Hawapendi mshahidi

568. Akamwambia asahi, Mambo ya Abidallahi, Na roho zao kutahi, Na warakawe Yazidi

569. Na wewe wakutafuta, Na pindi wakikukuta, Kitwa chako kitakatwa, Kuuwawa huna budi

570. Ukae ukitambua, Huna budi kuuwawa, Mselemu kamkuwa, Subhana ya Wadudi

571. Akitazama yamini, Asimuone auni, Akiola shimalini, Asione msaadi

572. La haula akasema, Illa billahi Karima, Kamkua Allahumma, Ya Allahu ya Samadi

574. Mara ile kenda zake, Katwaa upanga wake, Ilihamu roho yake, Na matozi yakabidi

575. Silaha kajizaini, Roho haina makini, Akatembea mjini, Makusudi kusharidi

576. Azima ni kukimbia, Hanapo pa kuawia, Mumule katika nyia, Pana nyumba msafidi

577. Na nyumba hiyo yuani, Mwenyewe akitwa Khani, Ali mzee zamani, Wa tangu jadi na jadi

578. Lakini ni Islamu, Yu dini ya Muungamu, Na wote bani Hashimu, Kiwapenda jitihadi

579. Akiwapenda sikia, Dhuria wake Nabia, Na wote 'l Hashimia, Pendo lisilo idadi

580. Kenda kwake Mselemu, Mlangoni akakumu, Kamuuliza khadimu, Yu wapi wako Sayyidi

581. Na kwamba yu humo ndani, Mwambie pana mgeni, Kenda hima ghulumani, Khani akamradidi

582. Mzee Khani kajibu, Na'pite hima gharibu, Akapita Muarabu, Mlango kaukaidi

583. Wakenda wakaonana, Khabari wakauzana, Mselemu akanena, Kama yaliyombidi

584. Khabari akamweleza, Tokea mwanzo wa kwanza, Na jamii miujiza, Hata ya bunu Ziadi

585. Na hivi sasa rijali, Wa kati kunidalili, Wapate kunikutuli, Kwetu Maka nisirudi

586. Kisha sayo kutamka, Khani akaghadhabika, Kwa hayo yalofanyika, Ghadhabu kubwa shadidi

587. Kanena mzee Khani, Na kwamba yali zamani, Sasa ningejizaini, Henda hawa na jihadi

588. Kama banii Hashimu, Huwaje kuwalaumu, Ukataka wadhulumu, Huo ndio wa hasidi

589. Lakini sasa pulika, Hapa umesitirika, Kwa amri ya Rabuka, Watakwisha usitadi

590. Na huyo akutakaye, Rafiki yake ni miye, Labuda asisikiye, Kwamba siwezi jasadi

591. Lakini asikiapo, Hana budi kuja papo, Na pindi hapa ajapo, Kumuua huna budi

592. Ajapo akiwasili, Taja kuweka mahali, Na upangao mkali, Ungoje akikaidi

593. Taja muwekea kiti, Hata akisha keleti, Umuonyeshe mauti, Ahimari na suwedi

594. Akisha kusema hayo, Mselemu kamba ndiyo, Akafurahika moyo, Kwa Khani aloradidi

595. Abidallahi hakika, Siku mbili zikifika, Roho akatia shaka, Khani hajamshahidi

596. Kauliza barazani, Yu wapi mzee Khani?, Kambiwa yuko nyumbani, Ana maradhi shadidi

597. Mara kondoka kitini, Kusudi kwenda kwa Khani, Akipata mlangoni, Kamba wenye nyumba hodi

598. Kisikia sautiye, Wakajua kwamba ndiye, Tena Khani amwambie, Mselemu jizadidi

599. Shika sefu na turusi, Ukae pia nafasi, Hata akisha jilisi, Sikawe kumhusudi,

600. Mselemu kajifita, Paziani akapita, Na sefu kaitafuta, Isiyo shaka na budi

601. Akiweka na siriri, Akitengeza vizuri, Tena kapewa amri, Kupita bun Ziadi

602. Basi akapita ndani, Akaonana na Khani, Mselemu faraghani, Seifi kaikalidi

603. Tena kampa maungo, Khani akamba Muungu, Leo atakata shingo, Ipukane na jasadi

604. Kakaa muda mzima, Khani akaona kimya, Kafazaika mtima, Mbona kimya kinazidi?

605. Basi akatoa fumbo, Kama aimbae wimbo, Akamba mambo si mambo, Si ya jadi na jududi

606. Hino ndiyo kazi yenu, Mliyozoea kwenu, Si kazi yao sununu, Katika zote abadi

607. Kutuka akamuonya, Ni kazi yenu mwafanya, Wala sikukudanganya, Niliyokupa ahadi

608. Nakwambia mara zote, Simama ukiokote, Na lijirilo tu sote, Kwa amri ya Wadudi

609. Khani akisha yasoza, Fumbo la kumuhimiza, Mselemu kanyamaza, Hata saa ikabidi

610. Kasema mara ya pili, Mselemu katwawili, Abidallahi kakuli, Naona mwataradidi

611. Unani mzee Khani, Kwondoa taji kitwani, Ukabanja kitandani, Khatima ukalirudi?

612. Mara wavua kilemba, Na mara nyimbo ukimba, Unani katika nyumba, Jambo lililokuzidi?

613. Mzee Khani kakuli, Ni jua liwapo kali, Hunipungua akili, Na ndwele ikashitadi

614. Ndipo hivi hafanyiza, Fiili na miujiza, Ni ndwele imenikaza, Na akili msharidi

615. Abidallahi kasema, Kwa kheri narudi nyuma, Nijile kukutazama, Khani akenda muwadi

616. Aliporudi nyumbani, Kasema mzee Khani, Mselemu jinsi gani, Usitimize ahadi?

617. Mselemu akakuli, Sefu yali masiluli, Hataka kumkutuli, Hazuiwa yangu yadi

618. Hitaka mwandika sefu, Nimpasue nusufu, Nikasikia khatifu, Na mnada ukanadi

619. Mnada ukatongoa, Usende ukamuua, Na muili hazuiwa, Kujondoa sijimudi

620. Ndipo saya yakajiri, Na zohali na usiri, Na Khani akadhukuri, Kheri ni yake Wadudi

621. Baada sayo asahi, Kondoka Abidallahi, Akili katanabahi, Kuzichawanya nakidi

622. Roho yake kaazimu, Azitoe darahimu, Atafute Mselemu, Kwa akili na juhudi

623. Kamwamkua rijali, Jina lake Muakali, Ubazazi na khitali, Apita wote junudi

624. Dinari kazihesabu, Alufu tatu dhahabu, Na maneno kamjibu, Shime yakhe jitahidi

625. Mtafute Mselemu, Kwa akili na fahamu, Ukampe darahimu, Ukisha mpa urudi

626. Ujue nyumba aliyo, Kwa rai na akiliyo, Muakali kamba ndiyo, Inshallah tajitahidi

627. Akondoka Muakali, Akayatukua mali, Akenda akadalili, Katokea masijidi

628. Akaona msikiti, Kaingia akaketi, Ilipofika salati, Akaja mtu wahidi

629. Jina kitwa Mselemu, Bun Ghaushi fahamu, Kaja kampa salamu, Na heshima kamzidi

630. Kamwambia ndugu yangu, Takupa faragha yangu, Maana humu si mwangu, Mimi natoka baidi

631. Mimi ni mtu wa Maka, Huseni kanipeleka, Nitukuzie waraka, Na mali yaso idadi

632. Nijile na darahimu, Kuja mpa Mselemu, Na alipo sifahamu, Nimekwisha usitadi

633. Na kuuliza siwezi, Mji unavyo makonzi, Na mimi ni mwanagenzi, Sijui mtu wahidi

634. Na wewe kukubaini, Ni kwamba natumaini, Yakhi fanyiza hisani, Na haiba nisirudi

635. Twende ukanipeleke, Hampe amana yake, Hima upesi nitoke, Humu siwezi rajidi

636. Kanionyeshe upesi, Hapo alipojilisi, Roho ina wasiwasi, Mselemu karadidi

637. Kanena bunu Ghausha, Takwenenda kuonyesha, Lakini niaminisha, Kwa mithaki na ahadi

638. Muakali kabaini, Nakuapia yamini, Nami ni msikitini, Ni katika masijidi

639. Kisha apa sura mia, Mara iyo kamwambia, Nyumba alokimbilia, Ya banii 'l Asadi

640. Mselemu yu nyumbani, Huko kwa mzee Khani, Muakali kibaini, Kenda hima na juhudi

641. Alipofika nyumbani, Kabisha kangia ndani, Akamwambia yakini, Nijile nina zawadi

642. Kamtaka Mselemu, Kwa wema na tabasamu, Akampa darahimu, Akisha kamradidi

643. Akamwambia Huseni, Ametoka yu ndiani, Atakuja kuawini, Kama yaliyo kubidi

644. Amenipa diinari, Utakako ushitiri, Kula kipasacho shari, Chombo kilicho jadidi

645. Nami hivi nenda zangu, Nina khofu roho yangu, Nakuhongea mwenzangu, Nawe kujificha zidi

646. Kaamini Mselemu, Kapokea darahimu, Akampa na salamu, Nisalimia Sayyidi

647. Muakali akatoka, Kwa upesi na haraka, Barazani akifika, Kwake ibnu Ziadi

648. Muakali akanena, Kamwambia wake bwana, Umekwisha patikana, Uliotaka mradi

649. Khani bin Ghuruata, Ndiye aliyemfita, Hivi tukimtafuta, Anaye zote abadi

650. Kwambiwa kwake juhali, Kawamkua rijali, Majina yao nakuli, Wa kwanza ni Muhamadi

651. Wa pili etwa asema, Na Omari kawatuma, Akamba nendani hima, Khani mukamkaidi

652. Wakenda na furisani, Wakenda mtwaa Khani, Akifika barazani, Salamu akaradidi

653. Jamii wakanyamaza, Kwa hali ya kutukiza, Abidallahi kauza, Kwani Khani kutaadi?

654. Wamficha Mselemu, Nasi ni wetu khasimu, Wewe u mwenda wazimu, Akili umesharidi

655. Naye Khani atongoe, Mwenda wazimu u wewe, Utakae umuuwe, Bin ami Muhamadi

656. U wewe mwenda wazimu, Utakaye Mselemu, Nikupe umdhulumu, Upate kumhusudi

657. Mara akaghadhibika, Abidallahi karuka, Bakora akaishika, Kitaka kumjalidi

658. Khani alipomshufu, Akaikabili sefu, Kamwegema asikhofu, Kama umeme na radi

659. Dharuba kamsukuma, Akazikata kwa nyuma, Kofia mbili za chuma, Na dirii za hadidi

660. Abidallahi kanguka, Kwa kiwewe kumshika, Roho ikafazaika, Akawambia junudi

661. Kawambia tasihili, Mshikeni mumdhili, Asijesha wakutuli, Khani akaiadidi

662. Akaishika hasama, Jeshini akajitoma, Mithili wimbi la joma, Livumalo na baridi

663. Kawangusha iyo hini, Khamsa wa ishirini, Bi tarafati aini, Kaumu wakamzidi

664. Wakampiga asira, Akafungwa kwa kambara, Na kumpiga bakora, Na dharuba za hadidi

665. Kashahadia Karimu, Kafa ali Islamu, Fi'l janati naimu, Akenda akarajidi,

666. Khabari zilipofika, Nyumani kwake hakika, Mselemu akatoka, Na jitimai shadidi

667. Katoka na jitimai, Hana hila wala rai, Ali katika sarai, Kaona nyumba baidi

668. Nyumba hiyo nitamke, Kamwona mwanamke, Kamuuza hali yake, Yote akamradidi

669. Kasikia nisiwani, Akamba pita nyumbani, Kwani adui mjini, Wa kati kukuadidi

670. Akapita Mselemu, Harume kamuheshimu, Ali na wake ghulamu, Yeye mmoja waladi

671. Kumuonakwe mamaye, Ana fazaa rohoye, Akamuuza haliye, Mama umetasawidi

672. Ni kungia ukatoka, Kitu gani umeweka, Mamaye akatamka, Sikia ewe waladi

673. Nyumbani mna ghulamu, Jina lake Mselemu, Min bani Hashimu, Bin amu Muhamadi

674. Na mimi nimemsiri, Ahadi ni kusafiri, Kijana akadhukuri, Mama kumficha zidi

675. Mara ile akatoka, Barazani akafika, Watu wamekutanika, Kamwita bun Ziadi

676. Yule kijana kasema, Mselemu yu kwa mama, Wapeleke watu hima, Mimi nimemshahidi

677. Kwa mama ndiko aliko, Na mimi natoka huko, Adui keta kacheko, Na kufurahi shadidi

678. Mara ile kasimama, Akawataka kauma, Akamba nendani hima, Na amiri Muhamadi

679. Bun Shiati amiri, Akampa asikari, Khamsamia jifiri, Walio kama asadi

680. Kamwambia tangulia, Mselemu niletea, Basi akashika ndia, Kandamana na junudi

681. Mselemu pakhubiri, Kasikia hawafiri, Na kishindo cha bairi, Kajua ndio hasidi

682. Kamwambia nisiwani, Kanipe maji kuzini, Nisali rakaateni, Nipate omba Wadudi

683 Kasali rakaateni, Akamuomba Manani, Baada sayo yuani, Kamrakibu jawadi

684. Akampanda farasi, Na upanga na turusi, Akamuomba Kudusi, Kawakabili junudi

685. Mbele yao kasimama, Kawauza akasema, Ajili semani hima, Nijue wenu mradi

686. Lililowaleta nini, Msikawe nambiani, Na ambalo mwatamani, Mutafutalo kusudi

687. Mara walipomshufu, Wakamwegema kwa sefu, Wapate kumtilifu, Afungwe kama abidi

688. Kajitia katikati, Akawonesa mauti, Watu khamsamiati, Watu kumi wakarudi

689. Kawapiga kama huwa, Kukata na kuangua, Kama radi ilotia, Shajaria 'l jadidi

690. Akawatawanya damu, Ikenenda milizamu, Wakarejea kaumu, Hata kwa bun Ziadi

691. Wakenda wakimwambia, Kama yaliyo jiria, Sote hatukubakia, Tumebadia suudi

692. Kusikiakwe yuani, Kawatoa shujaani, Idadiye alufeni, Wasioweza taadi

693. Akawambia nendeni, Mselemu mleteni, Msishindwe ni mgeni, Aliyetoka baidi

694. Endani mkamtwae, Upesi muniletee, Tupate hiyo rasiye, Apelekewe Yazidi

695. Wakenenda asikari, Kama rihi na matari, Na kula mtu tayari, Kwa silaha za hadidi

696. Walipomkaribia, Mselemu kawangia, Jeshini kajipakia, Na farasiwe najidi

697. Akamrusha kimatu, Akaja ndani ya watu, Isipate saa tatu, Wote akawasafidi

698. Akaishika hasamu, Mwana wa bani Hashimu, Akawatawanya damu, Nchi yote ikabidi

699. Akinga simba dharia, Damu ikenda milia, Na watu wakangamia, Wangi wasio idadi

700. Yamini kajipeleka, Wanguka kama mataka, Hata akizungumka, Kupigana akazidi

701. Kawatia mautini, Wote watu alufeni, Wakabaki thelathini, Wasihimili hadidi

702. Wakenda kwa bwana wao, Wakampa hali yao, Wakamba siku ya leo, Adui katuhusudi

703. Tulipowasili kando, Katungia kama nondo, Akitutenda kitendo, Hatuwezi kuradidi

704. Katungia kwa upanga, Jeshi yote kaizinga, Pasi muweza kukinga, Wala mkaa baidi

705. Bwana fanyiza shauri, Adui katuhasiri, Kwambiya siyo khabari, Kawakusanya junudi

706. Kawakusanya sufufu, Ambao ni mausufu, Ithnashara alufu, Akaja kawaradidi

707. Akawambia kaumu, Endani kwa Mselemu, Na mrudipo haramu, Mauti yatawabidi

708. Ambapo mwarejeea, Msipo kuniletea, Tawataka vitwa pia, Hayo nimewaahidi

709. Basi ikenenda jeshi, Kama dharuba ya tushi, Na kutaharaki nchi, Kwa hafiri za jawadi

710. Wakamfika alipo, Wakenda muona yupo, Mselemu iwenepo, Ghadhabu akashitadi

711. Upanga kauzungusha, Farasi akamwegesha, Ukinga mwamba kuusha, Na wingu kubwa na radi

712. Muili ukanafiri, Kwa ghadhabu kukithiri, Kiruka kama namiri, Ghadhabu kinga asadi

713. Dharuba akizitoa, Kama umeme na kuwa, Na kipovu kumuawa, Likachemka zubadi

714. Alikikabili mbele, Kusibakie kisele, Akileneza fumole, Watu hamadi hamadi

715. Muili ukamvimba, Kimatu akinga simba, Mara moja kawaramba, Watu mia wakarudi

716. Barazani wakifika, Mtangani wakanguka, Maneno wakitamka, Sikia bun Ziadi

717. Leo tuwene harubu, Iliyo kubwa ajabu, Vita vyake Muarabu, Ataitwaa biladi

718. 'l Kofu itatwaliwa, Ukae ukitambua, Na wewe utauwawa, Ni huyo mtu wahidi

719. Harubu apiganavyo, Hatuwene kama hivyo, Jamii vita twandavyo, Hatuwenepo abadi

720. Muarifu mwenye nchi, Atudirikiye jeshi, Ila sisi hatutoshi, Kupata huo mradi

721. Fisa khati Dimishiki, Watuletee khaliki, Na Basara na Iraki, Na wakutane junudi

722. Na ufanyapo dhihaka, Usipeleke waraka, Tambua unamtoka, Ulua wake Yazidi

723. Kwambiwa hayo asahi, Keta wino na lauhi, Kandika Abidallahi, Sikia ewe Sayyidi

724. Akaikutubu khati, Ya Yazidi mwenye nti, Tu katika harubati, Na vita vimetuzidi

725. Vita vyake Mselemu, Vyapita jabali gumu, Turidikie kaumu, Hima wapate tufidi

726. Wote watu maarufu, Katika nti ya Kofu, Jamii wametilifu, Watambuao hadidi

727. Mselemu atashinda, Na nti ataivunda, Atakalo atatenda, Ni hayo nakuradidi

728. Ulipokwenda waraka, Kwa Yazidi ukafika, Maneno akipulika, Uso ukamsawidi

729. Kanena akitukana, Watu wa Kofu naona, Hawawezi kupigana, Tokea jadi na jadi

730. Huwaje mtu mmoja, Akajirisha vioja, Tena wakatoa hoja, Kwamba avunja biladi

731. Tapeleka farisani, Kama simba ghadhibani, Mselemu na Huseni, Wakawatoe taadi

732. Kawakusanya sufufu, Watu sitini alufu, Ambao ni mausufu, Wasio shaka na budi

733. Kawambia enendani, Mkifika washikeni, Mselemu na Huseni, Upesi hima murudi

734. Basi jeshi ikatoka, Wakapanda wakishuka, Siku haba zikafika, 'l Kofu wakaibidi

735. 'l Kofu wakiwasili, Jamii wote rijali, Wakafurahi kwa kweli, Kwa kuwasili junudi

736. Wakelezana khabari, Za awali na akheri, Na kama yaliyojiri, Wasibakie wahid

737. Hata kukipambazuka, Basi jeshi ikatoka, Kusudi kwenda mshika, Bun amu Muhamadi

738. Alipokwisha waona, Mselemu kakazana, Meno akajitafuna, Mfano kama asadi

739. Kuionakwe shabuka, Mshipa ukamwinuka, Na tauka na tauka, Na kukazana jasadi

740. Jasadi ikahariki, Akinuka na uruki, Wote wakataharuki, Wasiweze mjalidi

741. Kizinga kama umeme, Kushotoni na kulume, Wali papo wasimeme, Na khofu kubwa shadidi

742. Akaipiga siahi, Ikavuma kama rihi, Zikawapuna silahi, Zilizo katika yadi

743. Akamzinga rikabu, Alisimika dhanubu, Na jamii ya ghadhabu, Siku hiyo akazidi

744. Uso ukaghadhibika, Mato yakahamirika, Na kipovu kumtoka, Yeye na wake jawadi

745. Akajitia jeshini, Akawachenga laini, Ali akenda usoni, Na kinyume akarudi

746. Akanenda kwa shimali, Akawachenga rijali, Kija upande wa pili, Ikiwa hivyo abadi

747. Mselemu kiwangua, Kama matone ya mvua, Pasi muweza jinua, Wala enuaye yadi

748. Na ambaye akabili, Mara huwa mbali mbali, Kushotoni na kuvuli, Wote wakatabaadi

749. Wakatamani kimbia, Hapana pa kuawia, Hali ya kuwazuia, Pasiwe muweza rudi

750. Mselemu akawesha, Kuwaua kiwangusha, Wote akawababusha, Wakawa kama rimadi

751. Siku hiyo maarufu, Arubaini alufu, Aliyo kuwatilifu, Wasazao wakarudi

752. Jamii wakakubali, Kuvushwa nchi ni kweli, Wala hataki wa pili, Kutunyang'anya biladi

753. Mashauri wakanena, Na tutoeni vijana, Twende nao mbali sana, Tukawafiche baidi

754. Hana budi Mselemu, Ataimiliki Rumu, Awaue na kaumu, Ashike ndia arudi

755. Wakawatoa kabili, Wana na wao wavyele, Na walio na uwele, Vipofu na makaidi

756. Wakawatoa viwete, Na wenye madonda wote, Mmoja wasimuate, Ila walio jadidi

757. Wakenenda ughaibu, Hata ipite harubu, Baada sayo najibu, Wakakutana junudi

758. Wakakutana kaumu, Thamaanini timamu, Alufu zilizotimu, Isipungue wahidi

759. Basi shauri waseme, Twendeni tukamwegeme, Mmoja asisimame, Ataghumiwa jawadi

760. Farasi akighumiwa, Mara moja atajiwa, Basi sapo wakaawa, Wote wakajizadidi

761. Hata walipomfika, Jeshini kajichomeka, Kupita zote shabuka, Wote wakamsharidi

762. Kawachawanya khumra, Ikenea zote bara, Na mafisi waking'ara, Kwa hali ya kufaidi

763. Akawatenda kitendo, Kuwachawanya uvundo, Kiwopoa kama nondo, Amezaye 'lkurudi

764. Farasiwe apitapo, Hapabaki aliyepo, Kama wingu na upepo, Na dharuba na baridi

765. Akiwangamiza watu, Idadiye wanakwetu, Alufu kumi na tatu, Waliokufa junudi

766. Wote waliobakia, Jamii wakakimbia, Mselemu kawendea, Na sefuye ya hadidi

767. Kiwapiga kwa hasamu, Akawachanganya damu, Wakawa kama ghanamu, Walio katika nadi

768. Kapiga kiwangamiza, Kuno akiwafukuza, Wote wakijelemeza, Masaharati na wadi

769. Wakenda mtashatiti, Kwa kuyakhofu mauti, Wakaikimbia nti, Wote ahali biladi

770. Mselemu akazinga, Akampita kipanga, Mji wote akatanga, Asimuone wahidi

771. Akaizuia Kofu, Thuluthani na nusufu, Na majumba maarufu, Yakawa katika yadi

772. Nusu ya mji baadhi, Yote kaitakabidhi, Pasiwe mtaaradhi, Wala mwenye kutaadi

773. Katamalaki majumba, Mazuri yaliyopambwa, Mwana wa simba na simba, Ni kazi yao abadi

774. Na jamii ya rijali, Kukionakwe kitali, Wakakutanika mbali, Wasiiweze biladi

775. Jamii wakakimbia, Mji wakamuatia, Walipokwisha tulia, Shauri wakafanidi

776. Shauri wakelekeza, Jawabu la kufanyiza, 'lKofu tukakweleza, tukamwondoa hasidi

777. Pana mmoja kanena, Hapana shauri tena, Mji unasha tupona, Na kufa hatuna budi

778. Hawa ni asili yao, Kuwana ni kazi yao, Na ushujaa wa kwao, Jadi zao na jududi

779. Ndio simba wa Mungu, Wanywesa watu matungu, Na katika ulimwengu, Hako aliyewazidi

780. Na roho yangu hiwaza, Yule hatutamuweza, Shauri la kufanyiza, Hapana ila wahidi

781. Na tutimbeni handaki, Ajapo akisabiki, Tufanye kutaharuki, Kinyumenyume turudi

782. Atangia handakini, Tumtie mikononi, Jamii wakayakini, Shauri linalobidi

783. Wakaichimba rijali, Yali usiku laili, Na shimo likenda mbali, Tena wakalisafidi

784. Juu wakalifinika, Farasi akija ruka, Hana budi kuanguka, Kumshika hana budi

785. Kulipokucha sikiza, Wakaitaka baraza, Mselemu katokeza, Mtamboni akanadi

786. Alipokuwatokea, Jamii wakakimbia, Mbele akiwandamia, Na sefuye ya hadidi

787. Kupata punde usoni, Farasi kanguka tini, Akangia handakini, Akaumia jawadi

788. Farasi akavundika, Na Mselemu kanguka, Wakaja wakamshika, Jamii wote junudi

789. Wakakutana asahi, Wakazipiga siahi, Na roho zilifurahi, Furaha kubwa shadidi