DINI YA KWELI YA MWENYEZI MUNGU

MWANDISHI: DKT. ABU AMINA BILAAL PHILIPS

MFASIRI: MUHAMMAD AL-MAAWY

NI IPI DINI YA KWELI YA MWENYEZI MUNGU?

Kila mtu anazaliwa katika hali isiyokuwa ya uchaguzi wake. Dini ya familia yake au ideolojia ya dola inalazimishwa kwake. Kuanzia mwanzo wa kuwepo kwake katika dunia hii. Wakati anapofika miaka ya ujana, anakuwa tayari ametiwa kasumba kuamini kuwa itikadi za jamii yake ndizo sahihi ambazo kila mtu anafaa kuzifuata. Hata hivyo, pindi baadhi ya watu wanapo baleghe na kuwa na akili timamu na kufunuliwa kwao mifumo ya Imani, wanaanza kuuliza usahihi wa Itikadi zao wenyewe. Mtafutaji ukweli mara nyingi anafikia mahali ambapo anatatizika pale anapotambua kuwa kila dini, dhehebu, ideolojia na falsafa yoyote inadai kuwa ndiyo njia ya pekee iliyo sahihi kwa mwanadamu. Kwa hakika, zote zinawahimiza watu kufanya mambo mema na mazuri. Hivyo, ipi ndiyo iliyo sahihi? Haiwezekani zote kuwa sahihi kwa vile kila moja inadai kwamba zile nyengine hazipo sawa. Kwa hivyo, vipi mtafutaji haki na ukweli ataweza kuchagua njia ya sawa.

Mwenyezi Mungu Ametupatia sote akili na bongo kutuwezesha kufanya uamuzi huu muhimu. Ni uamuzi muhimu sana katika maisha ya mwanadamu. Kwayo kunategemea mustakbali wake. Kwa hiyo, kila mmoja wetu ni lazima achunguze dalili zilizotolewa bila ya jazba wala upendelea na achague ile inayoonekana kuwa sawa mpaka dalili nyengine zitakapopatikana au kujitokeza.

Kama Dini au falsafa nyengine yoyote, Uislamu pia unadai kuwa ndio njia moja na ya pekee katika kumfikia Mwenyezi Mungu. Kwa muono huu haina tofauti na mifumo mingine. Kijitabu hiki kina lengo ya kutoa baadhi ya dalili kwa usahihi wa dai hilo. Hata hivyo, ni lazima kwa wakati wote ifahamike kuwa mtu anaweza tu kuamua njia ya kweli kwa kueka kando mhemuko, jazba na upendeleo ambao mara nyingi zinatupofua katika kuona uhakika wa mambo. Baadaye tu, ndio tutaweza kutumia akili tuliyopewa na Mwenyezi Mungu katika kufanya uamuzi wa kimantiki na wa sawa.

Zipo hoja nyingi ambazo zinaweza kutolewa kuunga mkono dai la Uislamu kuwa ni Dini ya kweli ya Mwenyezi Mungu.

Zifuatazo ni hoja tatu tu za wazi.

Hoja ya kwanza inahusiana na asli yake ya kuwa inatoka kwa Mwenyezi Mungu kwa majina ya Dini na ukamilifu wake katika maana yake.

Ya pili inahusu mafunzo ya kipekee na yasiyokuwa na utata wala mafumbo kwa yale mahusiano baina ya Mwenyezi Mungu, mwanadamu na uumbaji.

Hoja ya tatu inatokana na hakika kuwa Uislamu unaweza kufikiwa kilimwengu na watu wote kwa wakati wote.

Hizi ni sehemu tatu za msingi ambazo mantiki na akili zinaamuru ulazima kwa Dini kutambuliwa kuwa ni Dini ya kweli ya Mwenyezi Mungu. Kurasa zifuatazo zitajaribu kukuuza na kufafanua kwa kina fikra hizi.

JINA LA DINI

Kitu cha kwanza ambacho mtu ni lazima akijue na kukifahamu barabara kuhusu Uislamu ni maana ya neno hili, "Islaam - Uislamu".

Neno hili ni la Kiarabu "Islaam" ambalo linamaanisha kunyenyekea, kutii au kujisalimisha kwa hiari yake mtu kwa Mwenyezi Mungu wa kweli tu anayeitwa kwa Kiarabu "Allah". Yule anayetii na kunyenyekea kwa Mwenyezi Mungu kwa kupenda kwake anaitwa kwa Kiarabu "Muslim - Muislamu".

Dini ya Kiislau haijaitwa kwa jina la mtu au kaumu wala halikuamuliwa na kizazi cha baadae, kama ilivyo kwa Ukristo ambao uliitwa kwa jina la Yesu Kristo, Ubudha baada ya mwanzilishi wake Gautama Buddha, Ukomfushiasi baada ya Confucius, Umaksi baada ya Karl Marx, Uyahudi kutokana na kabila la Yuda na Ubaniyani kutokana na Mabaniyani (Wahindi).

Uislamu (kunyenyekea kwa kufuata matakwa ya Allah) ni Dini aliyopewa Adam, mwanadamu wa kwanza na Nabii wa mwanzo wa Mwenyezi Mungu na ilikuwa ni Dini ya Manabii na Mitume wote waliotumwa na Allah (Subhaanahu wa Ta'ala) kwa wanadamu. Mbali na hayo jina lake (Uislamu) lilichaguliwa na Mwenyezi Mungu Mwenyewe na kutajwa kwa uwazi katika Kitabu cha mwisho kilichoteremshwa kwa watu. katika Wahyi huo wa mwisho, unaoitwa kwa Kiarabu Qur'aan (Qur'ani), Allah (Subhaanahu wa Ta'ala) Amesema yafuatayo:

الْيَوْمَ أَكْمَلْتُ لَكُمْ دِينَكُمْ وَأَتْمَمْتُ عَلَيْكُمْ نِعْمَتِي وَرَضِيتُ لَكُمُ الْإِسْلَامَ دِينًا ﴿٣﴾

"Leo nimekukamiliishieni Dini yenu, na nimekutimizieni neema yangu, na nimekupendeleeni UISLAMU uwe ndiyo Dini" (5: 3).

وَمَن يَبْتَغِ غَيْرَ الْإِسْلَامِ دِينًا فَلَن يُقْبَلَ مِنْهُ وَهُوَ فِي الْآخِرَةِ مِنَ الْخَاسِرِينَ ﴿٨٥﴾

"Na anayetafuta dini isiyokuwa Uislamu haitakubaliwa kwake. Naye Akhera atakuwa katika wenye kukhasiri" (3: 85).

Kwa hiyo, Uislamu haudai kuwa ni Dini mpya iliyoletwa na Nabii Muhammad (Swalla Llaahu 'alayhi wa sallam) huko Arabuni katika karne ya saba, bali kuwa ni udhihirisho mpya katika mfumo wa mwisho wa Dini ya kweli ya Mwenyezi Mungu Mweza na Mwenye nguvu, Allah (Subhaanahu wa Ta'ala), kama ilivyoteremshwa mwanzo kwa Adam ('Alayhis Salaam) na baadae kwa Manabii waliomfuata. Kwa sehemu hii tunaweza kueleza kwa muhtasari kuhusu Dini nyengine mbili zinazodai kuwa ni njia za kweli. Hakuna kifungu chochote katika Biblia kinachoonyesha kuwa mwenyezi Mungu Aliwafunulia kaumu ya Nabii Musa ('Alayhis Salaam) au vizazi vyao kuwa Dini yao inaitwa Uyahudi, na pia kwa wafuasi wa Kristo kuwa Dini yao inaitwa Ukristo. Kwa maneno mengine, majina "Uyahudi" na "Ukristo" hayatoki kwa Mwenyezi Mungu au kukubaliwa naye. Haikuwa ila baada ya muda mrefu wa kuondoka kwake ndipo jina Ukristo likapatiwa Dini ya Yesu.

Je, Dini ya Yesu kwa uhakika ilikuwa tofauti kabisa na jina lake?[1]

Dini yale iliakisiwa na kuonekana kwa mafundisho yake, ambayo aliwahimiza kwayo wafuasi wake kuyakubali kama misingi ya uongofu katika mahusiano yao na Mwenyezi Mungu. Katika Uislamu, Yesu ni Mtume aliyetumwa na Allah (Subhaanahu wa Ta'ala), na jina lake kwa Kiarbu ni 'Isa ('Alayhis Salaam). Kama Mitume kabla yake, aliwalingania watu wake kwa ridhaa na hiari yao kujisalimisha kwa maelekezo ya Mwenyezi Mungu (Uislamu unasimamia hilo). Kwa mfano, katika Agano Jipya inaelezwa kuwa Yesu aliwafunza wafuasi wake kumuomba Mwenyezi Mungu kama ifuatavyo:

"Baba! Jina lako litukuzwe; ufalme wako ufike" (Luka 11: 2).

Na pia: "Baba yetu uliye mbinguni: Jina lako litukuzwe. Ufalme wako ufike. Utakalo lifanyike duniani kama mbinguni" (Mathayo 6: 9 - 10)

Fikra hii ilihimizwa sana na Yesu kwa kauli zake nyingi zilizorikodiwa katika Anaajiil (Gospels). Kwa mfano: alifundisha kuwa wale wanaonyenyekea watarithi Pepo.

Yesu aliashiria kuwa yeye pia ananyenyekea na kutii maagizo ya Mwenyezi Mungu.

"Si kila aniambiaye , 'Bwana, Bwana', ataingia katika ufalme wa mbinguni; ila ni yule tu anayetimiza matakwa ya Baba yangu aliye mbinguni" (Mathayo 7: 21).

"Mimi siwezi kufanya kitu kwa uwezo wangu mwenyewe. Mimi nina hukumu kama ninavyosikia kutoka kwa Baba, nayo hukumu yangu ni ya haki. Nia yangu si kufanya nipendavyo mwenyewe, bali apendavyo yule aliyenituma" (Luka 5: 30).

Zipo ripoti nyingi katika Anaajiil (wingi wa Injili) zinazoonyesha kuwa Yesu aliwawekea wazi kabisa wafuasi wake kuwa yeye hakuwa Mwenyezi Mungu mmoja wa kweli. Kwa mfano, alipokuwa akizungumza kuhusu Siku ya Mwisho (Kiyama), alisema:

"Lakini juu ya siku au saa hiyo hakuna mtu ajuaye itakuja lini; wala Malaika wa mbinguni, wala mwana; Baba peke yake ndiye ajuaye" (Marko 13: 32).

Hivyo, Yesu kama Mitume wengine kabla yake na yule aliyekuja baada yake, walifundisha Dini ya Uislamu: Kunyenyekea na kutii kwa amri ya Mwenyezi Mungu mmoja tu wa kweli.

MWENYEZI MUNGU NA UUMBAJI

Kwa vile ujumla wa unyenyekevu kwa hiari ya mtu kwa Mwenyezi Mungu unawakilisha kiini cha 'Ibadah, ujumbe wa msingi wa Dini ya Mwenyei Mungu, Uislamu, ni kumuabudu Mwenyezi Mungu peke Yake. pia inahitajia kuepuka 'Ibadah iliyoelekezwa kwa mtu yeyote yule, pahala popote pale au kitu mbali na Mwenyezi Mungu. Kwa vile vitu vyote mbali na Mwenyezi Mungu, Muumbaji wa kila kitu (na vitu vyote), kuwa ndiyo kiini cha Uislamu, kumuepusha mwanadamu awe mbali na kuabudu viumbe kwa kumlingania na kumuita katika kumuabudu Muumbaji wake peke Yake. ni peke Yake ndiye Anayestahiki kuabudiwa na mwanadamu, kwa sababu ni kwa ridhaa Yake ndio maombi yanakubaliwa na kujibiwa. Kwa hiyo, ikiwa mtu atauomba mti na maombi yake yakajibiwa, si mti uliokubali na kujibu maombi yake, bali ni Mwenyezi Mungu ndiye aliyekubali kw ahali hiyo iliyoombwa kutukia.

Mmoja anaweza kusema: "Hiyo ni dhahiri". Hata hivyo, kwa wenye kuabudu mti, si hivyo kabisa. Hivyo hivyo, maombi kwa Yesu, Buddha, Krishna au mtakatifu Christopher, au mtakatifu Jude au hata Muhammad (Swalla Llaahu 'alayhi wa sallam), hayajibiwi na wao, lakini na Mwenyezi Mungu.

Yesu hakuwambia wafuasi wake kumuabudu yeye, lakini aliwaamuru wamuabudu Mwenyezi Mungu, kama inavyosema Qur'ani:

وَإِذْ قَالَ اللَّـهُ يَا عِيسَى ابْنَ مَرْيَمَ أَأَنتَ قُلْتَ لِلنَّاسِ اتَّخِذُونِي وَأُمِّيَ إِلَـٰهَيْنِ مِن دُونِ اللَّـهِ قَالَ سُبْحَانَكَ مَا يَكُونُ لِي أَنْ أَقُولَ مَا لَيْسَ لِي بِحَقٍّ إِن كُنتُ قُلْتُهُ فَقَدْ عَلِمْتَهُ تَعْلَمُ مَا فِي نَفْسِي وَلَا أَعْلَمُ مَا فِي نَفْسِكَ إِنَّكَ أَنتَ عَلَّامُ الْغُيُوبِ ﴿١١٦﴾

"Na pale Allah Atakaposema: Ewe 'Iisaa bin Maryam! Ati wewe uliwaambia watu: Nifanyeni mimi na mama yangu kuwa ni miungu badala ya Allah? (Na 'Iisaa) atasema: Subhanaka, Wewe umetakasika! Hainifalii mimi kusema ambayo si haki yangu. Ikiwa nilisema basi bila ya shaka umekwisha yajua. Wewe unayajua yaliyo ndani ya nafsi yangu, lakini mimi siyajui yaliyo katika nafsi Yako. Hakika Wewe ndiye Mjuzi mkubwa wa yaliyofichikana" (5: 116).

Wala Yesu hakuiabudu nafsi yake pale alipoabudu, lakini alimuabudu Mwenyezi Mungu mmoja tu. Yesu alinukuliwa katika Anaajiil kuwa alisema: "Imeandikwa:

'Utamwabudu Bwana Mungu wako, na kumtumikia yeye peke yake'" (Luka 4: 8).

Kanuni ya msingi inapatikana katika Surah ya ufunguzi ya Qur'ani, inayojulikana kama Suratul Faatihah Ayah ya 5:

"Wewe tu tunakuabudu, na Wewe tu tunakuomba msaada".

Mahali pengine, katika Kitabu na Wahyi wa mwisho, Qur'ani, Mwenyezi Mungu Anasema:

"Na Mola wenu Mlezi anasema: Niombeni Nitakuitikieni" (40: 60).

Ni vyema kutilia mkazo kuwa ujumbe wa msingi wa Uislamu (yaani, kumuabudu Mwenyezi Mungu peke Yake) pia unatangaza kuwa Mwenyezi Mungu na uumbaji Wake (au viumbe Vyake) ni tofauti kabisa. Mwenyezi Mungu hako sawa na viumbe Vyake wala sehemu yao, wala viumbe Vyake haviko sawa na Yeye wala si sehemu Yake.

Hii inaweza kuonekana ni dhahiri kabisa, lakini mwanadamu kuabudu viumbe vyengine, badala ya Muumba ni kwa kiasi na kiwango kikubwa imeegemea ujinga, au kupuuza, kwa fikra na wazo hili. Ni itikadi na imani kuwa kiini cha Mwenyezi Mungu ni kuwa yupo kila mahala katika viumbe Vyake na uumbaji Wake au Uungu Wake kwa dhati Yake ipo au ilikuwepo katika baadhi ya sehemu ya viumbe na uumbaji Wake, ambayo imethibitisha na kutetea masala ya kuabudu viumbe vya Mwenyezi Mungu na kuita jambo hilo kuwa ni kumuabudu Mwenyezi Mungu. hata hivyo, ujumbe ya Uislamu, kama ilivyoletwa na Manabii wa Mwenyezi Mungu, ni kumuabudu Mwenyezi Mungu tu na kujiepusha kuabudu viumbe Vyake ama moja kwa moja au kwa njia nyengine yoyote. Katika Qur'ani Mwenyezi Mungu Anaeleza kwa uwazi kabisa:

وَلَقَدْ بَعَثْنَا فِي كُلِّ أُمَّةٍ رَّسُولًا أَنِ اعْبُدُوا اللَّـهَ وَاجْتَنِبُوا الطَّاغُوتَ ﴿٣٦﴾

"Na kwa hakika kwa kila ummah Tuliutumia Mtume kwamba: Muabuduni Allah, na muepukeni Shetani (na miungu wasio wa kweli)" (16: 36).

Pale wenye kuabudu masanamu wanapoulizwa, ni kwa nini wanayasujudia hayo masanamu yaliyotengenezwa na wanadamu, sikuzote na kila wakati wanajibu kuwa kwa uhakika wao hawaabudu hiyo taswira ya mawe, lakini Mwenyezi Mungu ambaye yupo ndani yake. wanadai ya kwamba hilo sanamu la jiwe ni alama tu ya kutazamia kwa kiini cha Mwenyezi Mungu na sio Mwenyezi Mungu Mwenyewe. Yeyote aliyekubali dhana ya kuwa Mwenyezi Mungu yuko kwa njia yoyote ile ndani ya viumbe Vyake atalazimika kukubali hoja hii ya kuabudu masanamu. Kwa maana, mtu anayefahamu ujumbe wa msingi wa Uislamu na athari yake hatakubali kamwe kumshirikisha Mwenyezi Mungu kwa kuabudu masanamu kwa jinsi yoyote itakavyoelezwa kimantiki. Wale waliodai uungu kwao wao wenyewe katika historia waliegemeza itikadi yao potofu na ya kimakosa kuwa Mwenyezi Mungu yuko ndani ya mwanadamu. Kuchukua hatua moja mbele, walidai kuwa Mwenyezi Mungu yuko ndani yao sana kuliko kwa wengine wetu, hivyo wanaadamu wengine ni lazima wanyenyekee na kuwatii na kuwaabudu wao kama mungu mwenyewe kwa dhati Yake au kama Mwenyezi Mungu aliyejikoleza ndani yao. Hivyo hivyo, wale waliotetea uungu wa wengine baada ya kufa kwao walipata eneo lenye rutuba miongoni mwa wale wenye kukubali itikadi ya uwongo ya kuwepo Mwenyezi Mungu ndani ya binadamu.

Inatakiwa iwe wazi kabisa sasa kuwa yule mwenye kuelewa msingi wa ujumbu wa Uislamu na athari yake hawezi kukubali kuabudu kiumbe kingine kwa hali yoyote ile. Kiini cha Dini ya Mwenyezi Mungu ni mwito wa dhahiri wa kumuabudu Muumbaji na kukataa kuabudu viumbe kwa mfumo wowote ule. Hii ndio maana ya wito wa Uislamu: "Laa ilaaha Illaa Llah"

(Hapana Mola wa kuabudiwa ila Allah).

Tangazo hili la kweli katika ibara hii na kuukubali Unabii moja kwa moja unamleta mtu kuwa Muislamu, na Imani ya uhakika na kweli inamdhaminia mtu Pepo. Kwa hiyo, Mtume wa mwisho wa Uislamu (Swalla Llaahu 'alayhi wa sallam) amenukuliwa akisema:"Yeyote anayesema: 'Hapana Mola wa kuabudiwa ila Allah, na akafa akishikilia (Imani hiyo) ataingia peponi".

Itikadi kwa tangazo hili la Imani inahitaji kuwa mtu anyenyekee na kutii kwa hiari amri za Mwenyezi Mungu kwa njia iliyofunzwa na Manabii wa Mwenyezi Mungu. Pia inahitaji kwa mtu kuwa Muumini kuacha kabisa kuabudu miungu ya uwongo.