TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KWANZA
Kwa jina la Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema, Mwenye kurehemu. Kitabu hiki kilicho mikononi mwako hivi sasa ni juhudi ya miaka mingi sana ya watu waliojitolea kuona kazi hii imefanikiwa bila ya kumsahau Marhum Abu Muhammad wa London. Kama lilivyo jina la Tafsiri ndivyo ilivyo Tafsiri yenyewe ambayo mwanachuoni huyu mahiri kabisa aliyeifafanua ni mtu aliyebobea katika fani zote ambazo mfasiri (Mfafanuzi) anatakiwa awe nazo. Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya ameonesha cheche zake katika vitabu vingi alivyoviandika katika maudhui mbalimbali na hivyo kujipatia wasomaji wengi sana.
Msomi huyu, mwenye fikra huru na anayetetea kile anachokiamini, ni mtu mwenye mawazo mapana na kuyaangalia mambo kwa undani sana, kipaumbele chake ni katika maslahi ya umma huu na amejaribu sana `kwenda na wakati. Sifa kubwa ya pekee ya mwanachuoni huyu ni kuwa yeye hakujihusisha sana na kungangania madhehebu fulani tu, labda hii yatokana na wadhifa wake wa ukadhi aliokuwa nao katika nchi ya Lebanon ambayo ina madhehebu mengi, ambapo suala la madhehebu ni nyeti nchini humo,hata hivyo yeye aliweza kuamua matatizo ya watu kwenye ofisi yake kulingana na madhehebu yao pale walipomwendea, hiyo ilmsaidia sana hata
kuweza kutoa kitabu kiitwacho Al-Fiqh alaa madhaahibil-khamsah (Fikhi ya madhehebu matano) yaani ya Hanafi, Maaliki, Shafi, Hambali na Shia (ambacho twataraji kitatoka hivi karibuni Inshaallah). Jambo lililotupa msukumo wa kukifasiri kitabu hiki kwa lugha ya kiswahili ni zile faida nyingi atakazozipata msomaji na kujua mambo mengi na ya ajabu yaliyo mapya kwake ambayo si rahisi kuyapata kwa wafasiri wengine.
Msomaji atapata faida katika fani za Sayansi, Siasa, Historia, Mashairi, visa vizuri,na Saikolojia miongoni mwa mengine; ndiyo maana msomaji atashangaa kidogo anapoisoma Tafsiri hii atakapoona mwandishi amewataja na kuwanukuu watu kama kina Mfalme Edward, wanasayansi kama kina Enstein, Charlie Champlin (Mchekeshaji maarufu), na wengineo, hali inayoifanya tafsiri hii kuwa ni ya kipekee kabisa. Mtindo alioutumia mwandishi ni sahali uliokusudiwa watu wa tabaka mbalimbali, wanavyuoni na watu wa kawaida.
Ruhusa imetolewa kwa yeyote anaetaka kukichapisha upya kitabu hiki kwa sharti tu kwamba asibadilishe chochote bila ya kutujulisha, na atutumie nakala moja baada ya kukichapisha. Nia yetu ni kukigawanya kitabu hiki bure lakini tumelazimika kukiuza kwa bei nafuu ili kurudisha gharama za uchapishaji. Mwisho, shukrani kubwa iwaendee bila ya kuwataja watu waliojitolea usiku na mchana, jopo la wafasiri, wahariri, wachapaji, waliotupa moyo na kutoa maoni yao na walioisimamia ili kuhakikisha kwamba kitabu kimemfikia msomaji.Mchapishaji.
Kutokana na maombi mengi ya wasomaji wetu wa Kiswahili, ambao ni wa madhehebu mbalimbali za Kiislamu, walioko Afrika Mashariki na Kati, Uarabuni na hata nchi za Ulaya, tumeonelea kukichapisha tena Kitabu hiki ili kupunguza kiu yao kama si kuiondoa kabisa. Tafauti iliyojitokeza katika chapa hii ya pili ni utaratibu mpya uliotumika, ambapo baada ya Aya kufasiriwa, maelezo yake yanapatikana moja kwa moja chini yake bila ya kwenda kwenye ukurasa mwingine, na utaratibu huu ndio utakaotumika katika chapa zote zitakazofuata.
Vilevile tumejaribu sana kusahihisha baadhi ya makosa ambayo kibinadamu yalikuwa yamefanywa katika toleo la kwanza. Hatuna budi kuwashukuru wote waliotumia wakati na akili zao katika kufanikisha lengo hili adhimu, bila ya kuwasahau wafadhili na wasimamizi wetu.Mwenyezi Mungu awalipe kheri nyingi. Vilevile tunawashukuru sana wasomaji wetu amabao waliotukosoa, hivyo kuchangia, kwa kiasi kikubwa, kuisahisha chapa hii.Na tunawaomba waendelee kufanya hivyo. Mchapishaji
Sifa njema zote zinamstahiki Mwenyezi Mungu Mola wa viumbe. Baada ya hayo: Mimi nimetunga mfululizo wa vitabu vidogo vidogo katika itikadi na misingi yake. Nimevitunga kulingana na mfumo na mantiki ya kizazi cha kisasa, ambacho hakiamini kitu ila kile kinachokitaka na chenye kuafikiana na malezi yake na maendeleo yake.
Alhamdulillah Mwenyezi Mungu amejaalia tawfiki na kufaulu kwa mfululizo huo na umerudiwa kuchapishwa mara nyingi. Kimsingi ni kuwa kila kazi inayoafikiana na hekima na lengo inayolikusudia, Mwen-yezi Mungu huipa ufanisi na tawfiki. Hakika tawfiki inatokana na Mwenyezi Mungu, hakuna shaka, lakini Mwenyezi Mungu amekataa kupitisha mambo isipokuwa kwa njia yake na desturi yake.
Kuandika juu ya karatasi tu, sio sharti la kufaulu katika kitu chochote; isipokuwa kufaulu ni kumridhisha na kumpendeza msomaji kile atakachokisoma. Msomaji naye hawezi kuridhia kitabu chochote, isipokuwa kiwe kwa ajili yake na sio kwa ajili ya mwandishi.Na huko kuridhia kunampa nguvu mwandishi kuendelea. Hapo ndipo msomaji na mwandishi wanapoathiriana. Kwa vyovyote ilivyo, kuenea kwa mfululizo huo wa vitabu vidogo vidogo kumenipa nguvu ya kutunga vitabu vikubwa na vipana; kama vile: Maalimu Falsafatil Islamiya, Alfiqhu Ala Madhahibil Khamsa, Fadhail Imam Ali n.k.
Mwenyezi Mungu naye akavifanyia vitabu hivi kama alivyofanyia vile vingine. Nikapata msukumo wa kutunga Fiqhul Imam Jaffar Assadiq katika juzuu sita kubwa; nacho kikawa kama vingine vilivyotangulia. Kwa hiyo vikanipa msukumo wa kutunga kitabu kikubwa na kitukufu, Tafsir ya Qur`an ambayo nimeiita Tafsir Al -Kashif.
Kwa uwezo wake Mwenyezi Mungu na nguvu Zake, vile vile kwa tawfiki Yake na fadhila Zake, imetimia juzuu hii ninayow-aletea. Ndani yake mna Sura mbili kamili za Al-Fatiha na Al-Baqara. Sijui kama uhai utaniruhusu nione natija ya lile nililojitolea mhanga, au kwamba kudra itafanya kinyume? Na kama ikitimia Tafsir Al-Kashif je, itakuwa na mafanikio, kama ilivyokuwa kwa tungo nilizozitunga, ya kutoa matunda? Je, itazaa kitabu kingine baada yake kama ilivyokuwa kwa Fiqh?
Hayo ni maswali ambayo hapana ajuaye jawabu lake isipokuwa Mwenye tamko la kwanza na Mwenye uwezo wa juu.
﴿وَمَا تَدْرِي نَفْسٌ مَّاذَا تَكْسِبُ غَدًا وَمَا تَدْرِي نَفْسٌ بِأَيِّ أَرْضٍ تَمُوتُ﴾
Na nafsi yoyote haijui itachuma nini kesho, wala nafsi yoyote haijui itafia ardhi gani" (31:34)
Hata hivyo kuamini kwangu ukweli huu hakunizuii kuendelea na juhudi zangu. Kwa sababu, vile vile ninaamini kwamba azma yangu ya kujitahidi ina athari kubwa katika kuhakikisha yale ninayoyataka. Imani hii inanipa msukumo wa kutoa juhudi zangu zaidi, kwa kuogopa kupoteza fursa.
Kwa hivyo basi, nitaendelea kuandika na kuwa na ndoto ya kutimia na kufaulu mpaka kufa.Yeye peke yake ndiye ambaye atasimamisha nishati yangu.Nami nitaendelea kutoa juhudi zangu muda wote ule ambao mauti yatakuwa yako mbali nami.
Natamani sana yanijie mauti huku nikiwa ninaandika kulingania kwenye haki na uadilifu. Bali mapendeleo yangu ni kuingia peponi ili niweze kusoma na kuandika, nikiwa sina mawazo mengine yoyote ya kunishughulishi, nitakuwa sina mawazo ya kushughulikia familia na kadhalika.
Mara nyingi sana hunijia swali hili: Kama nikiingia peponi nitakuwa mvivu? Je, itawezekana nisome na niandike? Halafu hujijibu: Ndio, huko kuna yanayofuvi rahiwa na macho na yanayopendwa na nyoyo; hata kama moyo unapenda kusoma na kuandika. Kisha linanijia swali jingine: Nimwandikie nani na watu wote wa peponi ni wakamilifu?
Samahani kwa kuiachia kalamu iandike hayo; au kwa usahihi zaidi, kuiacha dhati yangu kujieleza. Kwa kweli mimi ni mtu wa kawaida tu, ambaye ni vigumu kumtenganisha na dhati yake na ambaye inakuwa vigumu kujizuia kuyaelezea yaliyo katika pango la moyo wake, wakati inapopatikana fursa ya kujieleza.
Kizazi cha kisasa Kila kitu kina sababu ya kutokea kwake, ni sawa kiwe ni cha kimaumbile, kama vile tufani na tetemeko; au cha kijamii, kama vile ujinga na ufukara; au kiwe ni katika mambo ya moyoni, kama vile imani na kufuru. Hakuna kitu chochote kinachotokea kwa sadfa bila ya sababu yoyote, au bila ya mipangilio yoyote. Nitayafafanua maelezo haya kwa swali na jibu lifuatalo:
Kwa nini kizazi cha sasa hakijishughulishi na misimamo ya kidini kama kilivyokuwa kizazi kilichopita? Vijana wengi wa kileo wameachana na ibada na mazingira ya kidini; bali imekuwa uzito sana kwao kusikiliza mawaidha na nasaha za kidini; hata msimamo mzuri wa kiutu - kama udugu, usawa, amani, kusaidiana, ukweli na uadilifu - haumo katika nyoyo zao kabisa.
Inapotokea kuuzungumzia basi wanauzungumzia katika ndimi zao tu, sio katika nyoyo zao; ila ikiwa kuna manufaa ya kibinafsi.
Jibu ni kuwa, mataifa ya Kiislamu ya Kiarabu na yasiyokuwa ya Kiarabu yalikuwa hayategemei misingi yoyote wala misimamo yoyote ila ile iliyotokana na Kitabu cha Mwenyezi Mungu (s.w.t.) na Sunna ya Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) , sio iliyotokana na ujamaa au ubepari, wala demokrasia au ubaguzi. Hakuna kitu chochote walichotegemea isipokuwa wahyi wa Mwenyezi Mungu.
Humo ndimo mlimochukuliwa misingi ya itikadi, adabu, tabia na njia za taaluma. Vile vile kanuni na hukumu zinazotumiwa katika mahakama na mambo mengine ya kibinafsi na ya kijamii, yalitoka humo. Kwa hiyo, ndio maana yakawa mafundi-sho ya dini yako wazi katika bongo za watu wengi; wakawa wanayajua yanayotakiwa na sharia na yanayokatazwa. Yule aliyekuwa akiishi maisha ya dini alikuwa ndio tegemeo la wote na ndio mahali pa amana zao. Na,yule mbaye hana dini hakuaminiwa au kutegemewa katika jambo lolote.Yaani misimamo ya kijamii ilikuwa ni misimamo ya kidini.
Yeyote anayetoka katika msimamo huo,anakuwa ametoka katika usalama.Kisha siku zikapita, yakatokea mapinduzi kutoka nchi za Kimagharibi, wakavamia miji ya Kiislamu.Kwanza kabisa walielekea kwenye sharia ya Qur`an, wakaiondoa katika mahakama. Badala yake wakaleta kanuni za Kifaransa na za Kiingereza.Wakaondoa mafunzo ya kidini katika taaluma. Wakaanzisha majumba ya ufuska; kama vile mabaa, vilabu vya usiku pamoja na kila kitu ambacho waliona kingeweza kuondoa itikadi na maadili.
Kwa hiyo athari za Qur`an na Sunna za Mtume zikafichika katika maisha ya kijamii. Hata lugha ya Kiarabu pia ilipatwa na kile kilichopatwa na dini. Ndio kikawa kizazi hiki hakijishughulishi na dini wala maadili mema. Hiyo ni natija ya ufisadi waliokulia na kulelewa nao. Na kama kawaida, hali hiyo ilienea. Kwa hiyo ni makosa kukitenga kizazi na jamii yake na malezi yake. Hawakukosea wale waliosema: Panapofuka moshi hapakosi moto
Dawa Unaweza kuniuliza: Umeelezea ugonjwa, sasa dawa yake ni nini? Kwa kweli jibu la swali hili si la kujibiwa na msomi mmoja tu; hapana budi zikutane akili kubwa zenye ikhlas. Kwa sababu, tabia na ada zikiingia katika kizazi na zikabaki kwa muda mrefu, huwa zimemea. kazi rahisi kuzing`oa. Kwa vile zinafanya kazi katika nafsi, kama zinavyofanya kazi athari za kisayansi.
Kuzibadilisha kunahitaji juhudi na jihadi ndefu, zenye mashaka; kama juhudi aliyoifanya Mtume(s.a.w.w) katika kubadilisha ada za kijahiliya na itikadi zao. Kuna Hadith zinazoonyesha hayo; kama ile inayosema: "Uislamu ulianza katika hali ya ugeni na utarudi katika hali ya ugeni, kama ulivyoanza." Kwa hivyo, hauwezi kuepukana na ugeni wake na kutulia katika kurudi kwake, isipokuwa kwa kiongozi kama Mtume Muhammad(s.a.w.w) na Masahaba kama Wahajiri na Ansari Mwenyezi Mungu hashindwi kufanya Qur`an, sharia yake na maadili yake kuwa ndiyo inayotawala leo. Lakini ni juu yetu kufanya juhudi kadiri ya uwezo wetu, wala tusingoje muujiza wa mbinguni.
Na kazi ambayo tunaiweza kuifanya, nionavyo mimi,ni:
Kwanza : tuitilie mkazo dini katika mashule, hasa Qur`an, kuisoma, kuihifadhi na kuifasiri.Kwani hiyo ndiyo msingi. Kama wasimamizi wakikataa kufundisha dini katika mashule na watakataa tu,basi ni juu yetu kuanzisha Shule za kibinafsi kwa ajili ya lengo hilo tu. Tuanzishe Shule hizi kutokana na mamillioni yanayotolewa sabili kwa wanavyuoni wakubwa na wengine Wala sijui kama kuna kazi nyingine bora zaidi ya kutumia pesa hizo kuliko kufufua na kuyaeneza mafundisho ya dini.
Pili : kila mmoja katika watu wa dini atekeleza wajibu wake kwa ikhlasi, baada ya kujiandaa kuwa kiongozi mwenye mwamko, anayejua namna ya kuwakinaisha vijana, kuwa dini ndio chimbuko la msimamo ulio sawa, ambalo litawapa maisha mema zaidi.
Tatu : kuufafanua uhakika wa dini, kuufanya mwepesi kufahamika na kuutangaza kwa vitabu, hotuba, makala na matoleo kadhaa. Tumthibitishie mjinga na mwenye shaka kuwa Uislamu kwa sharia na maadili yake, unatosheleza kabisa mahitaji ya mwanadamu ya kiroho na ya kimaada; na unaweza kutatua matatizo yake; na kwamba una lengo la kumfanya afaulu katika dunia yake na akhera yake.
Msomaji atapata dalili ya hayo katika tafsiri hii ambayo inaunganisha dini na maisha, na ambayo imeshughulikia zaidi upande wa ubinadamu kuliko kushughulikia ufasaha wa maneno.
Mfasiri Tafsiri, kilugha, ina maana ya kubainisha. Na, katika istilahi ina maana ya elimu inayotafiti maana ya maneno ya Qur`an na yanavyohusika. Ili mfasiri awe na ubainifu katika ambayo yanamstahiki Mwenyezi Mungu, hana budi kuwa na maandalizi yafuatayo:-
Elimu za kiarabu kwa nyanja zake zote, elimu ya Fiqh na Misingi (usul) yake, Hadith na elimu ya Tawhid. Na miongoni mwa maandalizi hayo, kama wanavyoona wengine, ni elimu ya Tajwid na elimu ya kisomo cha Qur`an.
Kuna kitu kingine anachokihitajia mfasiri ambacho ni muhimu na kikubwa kuliko chochote katika walivyovitaja wafasiri katika utangulizi wa tafsiri zao. Kwa sababu, ndio msingi wa kwanza wa kufahamu maneno yake Mwenyezi Mungu (s.w.t.); Wala sijamwona yeyote aliiyekielezea.
Kitu chenyewe ni kuwa, maana ya Qur`an hawezi kuyafahamu na hatayafahamu kwa uhakika wake na kujua ukubwa wake, isipokuwa yule mwenye kuyahisi ndani ya moyo na akili yake. Pia imani yake ichanganyike na maana ya Quan pamoja na damu yake na nyama yake. Hiyo ndiyo siri iliyo katika kauli ya Amirul Muminin, Ali(a.s.) :"Hiyo ni Qur`an iliyonyamaza na mimi ni Qur`an inayotamka."
Vile vile imenijia yakini wakati nikiendelea na tafsiri kwamba mfasiri yeyote asiyeleta fikra mpya, ijapokuwa moja tu, katika tafsiri yake yote, basi atakuwa hana akili ya mwamko, isipokuwa ana akili ya kusoma tu. Anamchorea mwingine yale anayoyasoma, kama inavyoonekana picha ya kitu katika kioo vile ilivyo kwa rangi na umbo.
Hiyo ni kwa sababu maana ya Quran yako ndani sana kiasi ambacho yeyote hawezi kuyafikia kwa vyovyote vile atakavyokuwa na elimu na fahamu; isipokuwa atagundua yale ambayo maarifa yake yanayamudu. Atakaposimama mfasiri aliyetangulia pale alipofikia, kisha akaja mwingine akafuata nyayo zake bila ya kuzidisha chochote ijapokuwa hatua moja tu, basi atakuwa ni kama kipofu kamili anayetegemea fimbo tu; anapoikosa anabakia pale alipo.
Nimepata rai nyingi na itikadi za hapa na pale wakati nilipokuwa nafasiri.Kwa kweli tafsiri imesahihisha fikra zangu nyingi za zamani. Nimekuwa na yakini kwamba hapana imani bila ya takua pepo haipati isipokuwa mwenye kujitahidi na akajitoa mhanga katika njia ya haki na kwamba hakuna msingi wowote katika misingi ya Kiislamu au tawi lolote katika matawi ya Kiislamu - katika kumwamini Mwenyezi Mungu au hukumu ndogo katika sharia - isipokuwa inafungamana na maisha.
Vile vile nimeyakinisha kuwa wengi wa wale ambao hawaujui Uislamu na makusudio yake ni wale wanaojinaki na Uislamu; na mengi ambayo atayakuta msomaji wakati wa kupekuwa kurasa za Tafsir hii, nimeyahusisha hayo katika vifungu mbali kwa vielelezo vyake.
Kwa kweli sijui kama kuna kazi ngumu na nzito kama kufasiri maneno ya Mwenyezi Mungu.Sio kazi rahisi kueleza matakwa yake Mwenyezi Mungu. Lakini jambo la kutia moyo, nikuwa mfasiri hufasiri maana ya Qur`an na makusudio yake kulingana na alivyofahamu yeye, sio kulingana na ilivyo hasa; sawa na mujtahid wa Fiqh ambaye hulipwa thawabu akifutu sawa na husamehewa akikosea, bali hupata thawabu, hata akikosea, kwa sababu ya juhudi yake na kutokuwa mvivu.