Site ya Al-Imaamaini Al-Hassanaini (A.S) ya usambazaji wa utamaduni wa Kiislamu na mafunzo ya Kidini

KIFO CHA MTUME MUHAMMADI (S.A.W.W) SEHEMU YA PILI

1 Voti 03.0 / 5

KIFO CHA MUHAMMAD (s.a.w.w) MTUME WA ALLAH (s.w.t) SEHEMU YA PILI

Jumatatu, Rabi al-Awwal 1, 11 H.A.

Jumatatu, mwezi 1 Rabi al-Awwal ya 11Hijiria ilikuwa ndio siku ya mwisho ya Muhammad ibn Abdullah (s.a.w.w), Mtume wa Allah (s.w.t.) katika dunia hii. Kulikuwa na nyakati ambapo alijisikia nafuu kidogo lakini wakati mwingine, alikuwa dhahiri kwenye maumivu makali. Aisha, mke wake, anasimulia ifuatavyo:

 “Jinsi siku ilivyosogea kuelekea mchana, Fatima Zahra, binti yake Mtume wa Allah (s.a.w.w) alikuja kumuona Mtume. Alimkaribisha na kumwambia akae kandoni mwake. Kisha akamwambia kitu ambacho sikuweza kusikia lakini alianza kulia. Alipoyaona machozi ya binti yake, alimwambia kitu kingine ambacho pia sikuweza kusikia lakini yeye alianza kutabasamu. Yeye alifanana sana na baba yake katika mwenendo, tabia na Sura.”

Muda baada ya kifo cha Mtume (s.a.w.w), Aisha alimuuliza Fatima ni kitu gani ambacho baba yake alimwambia yeye ambacho kwanza kilimfanya alie na kisha kikamfanya atabasamu.

Fatima akasema: “Kwanza baba yangu aliniambia kwamba alikuwa anakaribia kufa. Nilipolisikia hili, nilianza kulia. Kisha akanijulisha kwamba mimi ndio nitakayekuwa wa kwanza kabisa kukutana naye huko mbinguni, nalo pia, ni hivi karibuni tu. Nilipolisikia hili, nilifurahi sana, na nikatabasamu.”

Washington Irving

Mtoto pekee wa Muhammad aliyekuwa amebakia, Fatima, mke wa Ali, alikuja sasa kumuona yeye Muhammad. Aisha alizoea kusema kwamba hajawahi kumuona mtu yoyote anayefanana na Mtume (s.a.w.w) zaidi katika uzuri wa moyo kama huyu binti yake. Alimshuhulikia siku zote kwa upendo wa heshima. Alipokuja kwake, alizoea kusimama, kumfuata, kumshika mkono na kuubusu, na humkalisha kwenye sehemu yake mwenyewe Mtume.

Kukutana kwao katika safari hii kunasimuliwa hivyo na Aisha, katika Hadith zilizohifadhiwa na Abulfida.

 “Karibu mwanangu,” alisema Mtume, na akamfanya akae karibu naye. Kisha akanong’ona kitu fulani katika sikio lake, ambacho kwacho alilia. Katika kutambua huzuni yake, alinong’ona kitu kingine zaidi, na sura yake ikan’gara kwa furaha.

 “Hii ina maana gani?” nilimuuliza Fatima. “Mtume (s.a.w.w) anakuheshimu wewe kwa dalili ya mategemeo ambayo hajayaonyesha juu ya yeyote kati ya wake zake.” “Siwezi kutoa siri ya Mtume wa Allah (s.a.w.w)” alijibu Fatima. Hata hivyo, baada ya kifo chake, alisema kwamba kwanza alimtangazia kifo chake kilichokuwa kinakaribia; lakini alipomwona yeye analia alimtuliza kwa kumhakikishia kwamba angemfuata baada ya muda mfupi na kuwa Malkia wa peponi.” (The Life of Muhammad)

Kuelekea mchana ule Mtume (s.a.w.w) alikuwa na hali ya kutotulia. Aliulowesha uso wake mara kwa mara kwa maji baridi kutoka kwenye gudulia lililokuwa karibu yake. Alipomuona katika maumivu kama hayo, Fatima alilia: “Oh mateso ya baba yangu!” Mtume (s.a.w.w) alijaribu tena kumliwaza, na akasema: “Baada ya siku hii ya leo, baba yako hatakuwepo kwenye mateso tena.” Na akaongeza: “Wakati nikifa, sema, “Sisi wote ni wa Allah na Kwake ndio marejeo yetu.”

Sasa, kupumua kwake kukawa sio kwa kawaida, na alisikika akinong’ona kitu. Ibn Saad anasema katika Tabaqaat yake kwamba Mtume (s.a.w.w) alikuwa akisema: “Ninachokitafuta sasa ni kuwa pamoja na Allah (s.w.t.)” Haya yalikuwa ndio maneno yake ya mwisho.

Muhammad (s.a.w.w) alisikika akiyarudia maneno haya mara tatu, na kisha akanyamaza kimya – daima! Muhammad, Mtume wa Mwisho wa Allah (s.a.w.w) kwenye dunia hii, akafariki.

Aisha anasema: “Niliweka mto chini ya kichwa chake, na nikafunika kichwa chake na shuka. Kisha nikasimama pamoja na wanawake wengine, na wote tukaanza kulia, tukipiga vifua na vichwa vyetu, na kujipiga makofi kwenye nyuso zetu.”

Muhammad (s.a.w.w), Mtume wa Allah (s.w.t.) alifariki siku ya Jumatatu ya kwanza ya Rabi al-Awwal ya mwaka wa kumi na moja Hijiria wakati wa mchana. Alikuwa ameishi kwa miaka 63 iliyopungua siku nane tu.

Wanahistoria wa Ki-Sunni wanasema kwamba Mtume (s.a.w.w) alifariki, sio kwenye tarehe mosi bali mnamo tarehe 12 Rabi al-Awwal. Waislamu wa Shia wanasema kwamba alifariki, sio kwenye mwezi mosi ya Rabi al-Awwal bali siku moja mapema zaidi, yaani mwezi 28 Safar.

Makubaliano ya wanahistoria wa kisasa wa Magharibi, ni kwamba, Mtume (s.a.aw.w) alifariki mnamo tarehe 8 Juni, 632. Tarehe nane ya Juni, kwa bahati, pia ndio siku ya kuzaliwa kwake.

Toa maoni yako

Maoni ya watumiaji

Hakuna maoni
*
*

Site ya Al-Imaamaini Al-Hassanaini (A.S) ya usambazaji wa utamaduni wa Kiislamu na mafunzo ya Kidini