Site ya Al-Imaamaini Al-Hassanaini (A.S) ya usambazaji wa utamaduni wa Kiislamu na mafunzo ya Kidini

KANUNI ZA NDOA NA MAADILI YA FAMILIA 6

0 Voti 00.0 / 5

KANUNI ZA NDOA NA MAADILI YA FAMILIA

WAJIBU WA MWANAMUME.

Sehemu ya sita

MSIMAMIZI WA WA FAMILIA

MWANAUME UWE NA TABIA NJEMA. 2

Tudhani ya kwamba umepatwa na tukio lisilofurahisha. Tukio hili ama ni Matukio ya kila siku yaliyoambatana na hali ambayo hatuna uwezo wa kuingilia au hatuwezi kusaidia. Au inawezekana tukio hili ni lile ambalo sisi tunaweza kufanya uamuzi wetu.

Ni dhahiri kwamba katika mfano wa kwanza, hasira yetu haingesaidia kwa njia yoyote. Tutakuwa tunakosea kukasirika au kuhamaki. Lazima tukumbuke kwamba sisi hatukusababisha kutokea kwa tukio hilo na hata tujaribu kulikaribisha kwa uso wenye furaha.

Lakini kama tatizo letu ni la mfano wa pili, basi  tunaweza kutafuta ufumbuzi unaofaa.

Kama hatukukata tamaa tunapokabiliwa na shida na kujaribu kujizuia, kwa kutumia busara, tunaweza kuyashinda matatizo yetu. Kwa njia hii hatuta kimbilia hasira ambayo inaweza kuwa tatizo juu ya tatizo.

Tunao uwezo wa kushinda matatizo yote kwa kutumia uvumilivu na hekima. Hivi si jambo la kusikitisha kwamba tunashindwa kudhibiti mambo yanayotokana na Matukio yasiyoepukika maisha?

Zaidi ya haya kwa nini umlaumu mke na watoto wako kwa mabalaa yako,? Mke wako anatekeleza mgawo wa wajibu wake. Anatakiwa kutunza nyumba na watoto. Anatakiwa kufua, kupika, kunyoosha kwa pasi kufanya usafi na kadhalika. Unatakiwa kumtia moyo mke wako kama vile unavyomtendea.

Watoto wako pia wanafanya kazi yao. Wao pia wanamgojea baba yao wajifurahishe. Wafundishe mambo yaliyo Sahihi na uwape hamasa wajifunze zaidi. Je, ni haki kwamba unakutana na familia yako ukiwa na uso wa kikatili na chuki?

Wanatarajia wewe kuwatimizia matakwa ambayo ni haki yao. Wanatazamia wema kutoka kwako na wanataka uzungumze nao kwa upole na uoneshe furaha.

Watachukia sana kama ukidharau hisia zao na kama utageuza nyumba kuwa mahali pa giza ambamo hakuna furaha hata kidogo.

Unajua watateseka kiasi gani kutokana na tabia yako isiyopendeza na ya kikatili? Hata kama haitachukulia familia yako kwa uzito unaostahili angalau ujihurumie wewe mwenyewe. Uwe na uhakika kwamba unaweza kuharibu afya yako kwa kuendeleza ukatili.

 

Unawezaje kuendelea kufanya kazi na unawezaje kufuzu kupata mafanikio? Kwa nini uigeuze nyumba yako iwe Jahannamu? Hivi si vizuri zaidi kwamba wewe uwe na furaha kila mara na uyakubali matatizo yako kwa busara na si hasira?

Hungetaka kuamini kwamba hasira haiwezekani kutatua matatizo yako, isipokuwa hasa zaidi matatizo yataongezeka? Hungekubali kwamba unapokuwa nyumbani unatakiwa kupumzika na kurudisha nguvu zako ili uweze kupata ufumbuzi unaofaa kwa matatizo yako akili yako ikiwa imetulia?

 Kutana na familia yako ukiwa na uso wenye tabasamu; taniana na watu wa familia yako kwa namna nzuri na jaribu kutengeneza mazingira ya furaha nyumbani kwako. Ule na kunywa pamoja nao na upumzike.

Kwa njia hii wewe na familia yako mtafurahia maisha na mtashinda matatizo yenu kwa urahisi. Ndiyo sababu dini Tukufu ya Uislamu inaona tabia njema kuwa Sehemu ya dini na ishara ya kiwango cha juu sana cha imani.

Mtukufu Mtume saww alisema: "Mtu mwenye tabia njema amekamilika zaidi katika imani yake. Mtu mwema zaidi miongoni mwenu ni yule anayeitendea mema familia yake."

Mtukufu Mtume saww pia alisema: "Hakuna tendo jema zaidi kuliko tabia njema."

Imamu Ja'afar Sadiq as alisema:  "Kuwatendea wema watu na kuwa na tabia inayostahili unapokuwa nao hufanya miji kuwa na watu wengi zaidi na umri wa raia huongezeka."

Imamu Ja'afar Sadiq as pia alisema: "mtu muovu hubaki kwenye mateso na uchungu.

Luquman mwenye hekima alisema: "Mtu mwenye busara lazima afanye mambo kama mtoto mdogo wakati anapokuwa na familia yake,na kuendelea kuwa na tabia ya kiwanamume anapokuwa nje ya nyumba yake.

Mtukufu Mtume saww alisema: "Hakuna furaha iliyo nzuri zaidi kuliko tabia njema."

Mtukufu Mtume saww pia alisema: "Tabia njema ni nusu ya dini ya Uislamu."

Imesimuliwa kwamba alipokufa Sa'd bin Muadh Mmojawapo wa sahaba mashuhuri wa Mtukufu Mtume saww, Mtume saww alishiriki kwenye maziko yake bila kuvaa viatu, kama vile alipoteza Mmojawapo wa watu wa familia yake.

Mtukufu Mtume saww aliweka maiti ya sahaba huyo kaburini kwa mikono yake iliyotakasika halafu akaufunika. Mama yake Sa'd ambaye alikuwa anaangalia heshima ya Mtukufu Mtume saww kwa mwanae alimwambia Sa'd: Ewe Sa'd! Furahia pepo" Mtume saww alimwambia:

Ewe mama Sa'd, usiseme hivyo, kwa sababu Sa'd sasa hivi amepata mateso kwa njia ya kugandamizwa kaburini na kadhalika. Baadaye Mtume saww alipoulizwa kuhusu sababu ya mateso ya Sa'd, Mtume saww alijibu; "ilikuwa ni kwa sababu alikuwa anaitendea mabaya familia yake."

Fuatana nami Sehemu ya saba saba kanuni za ndoa na maadili ya familia.

Toa maoni yako

Maoni ya watumiaji

Hakuna maoni
*
*

Site ya Al-Imaamaini Al-Hassanaini (A.S) ya usambazaji wa utamaduni wa Kiislamu na mafunzo ya Kidini