Site ya Al-Imaamaini Al-Hassanaini (A.S) ya usambazaji wa utamaduni wa Kiislamu na mafunzo ya Kidini

HISTORIYA YA IMAMU HASSAN (A.S)

0 Voti 00.0 / 5

HISTORIYA YA IMAM HASSAN (A.S)

IMAMU HASSANI BIN ALLY BIN ABI TWALIB AWAPA HABARI WAFUASI WA MUAWIYYAH KUWA MUAWIYYAH ALILAANIWA NA MTUKUFU MTUME SAWW SEHEMU SABA

BAADA YA MAPATANO (SULUHU KATI IMAMU HASSANI AS NA MUAWIYYAH L.A)

Baada ya mapatano haya (Suluhu kati Imamu Hassan a.s na Muawiyyah l.a) kufikiwa, majeshi yalirudi nyumbani. Ufalme wa Muawiyyah l.a ukadumishwa na zaidi ya kuwa na Shamu tu, Muawiyyah alipata Misiri, Iraq, Hijazi (Saudi Arabia ya leo), Yemen, na Iran pia. Baada ya mapatano haya Imamu Hassan a.s alikuwa akisikia maneno ya matusi kutoka vinywani mwa watu wake wale waliokuwa wakimwita, hadi jana yake tu, "Amir wa wenye kuamini" lakini sasa walikuwa wakimwita "Mwenye kuifedhehesha dini". Lakini Mfalme wa uvumilivu Imamu Hassan a.s alinyamaza kimya.

Mara baada ya Muawiyyah kujiona kuwa matatizo yake yamemalizika aliingia Iraq na kupiga kambi mahali paitwapo Nakhilah karibu na mji wa Kufa, na alisema katika hotuba yake ya ijumaa, "Kusudi langu la kupigana katika vita hii si kukuoneni mkiuzingatia uislamu, eti mkisali, mkifunga, mkienda Hijja, au mkifuata mambo mengine ya dini ya kiislam ; kwa sababu mlikuwa mkifanya yote hayo. Hapana nilitaka tu, kuendeleza utawala wangu juu yenu, jambo ambalo nimefaulu kulipata baada ya mapatano haya ingawa ninyi hamkupenda. Na kuhusu masharti ya mapatano, ni nani basi anayeyajali? Ninaweza kuyajali au kutoyajali Kufuatana na mapenzi yangu. "Watu wote walinyamaza kimya, lakini Hakuna aliyeweza kumpinga.

Jambo la haya(aibu) zaidi lilikuwa kwamba, mjini Kufa, mbele ya Maimamu Hassan na Hussein a.s Muawiyyah alimtukana Imamu Aliy as na Imamu Hassan a.s. Imamu Hussein a.s aliposikia hivyo alisimama badala ya kaka yake ili kuzungumza. Lakini Imamu Hassan a.s alimkalisha na akamjibu Muawiyyah kwa kifupi sana lakini kwa maneno makali mno.

Imamu Hassan a.s alimwambia Muawiyyah na wafuasi wake kuwa :. Nakushuhudisheni enyi watu, je mnamjua ambaye mnaye mtukana kuanzia leo ni yule aliyeswali kwa kuelekea kibla zote mbili (Imamu Aliy as alikuwa mtu wa kwanza kusali nyuma ya Mtume wakati Mtume saww alikuwa akielekea Bait ul Muqadas Palestina na baadae kibla kikabadilishwa na Mwenyezi Mungu kuwa waislamu wote waelekee Alkaaba Makkah) wakati huo wewe Muawiyyah ulikuwa Kafiri ukiona kuwa kuswali na kuelekea kibla hizo ni upotofu, ulikuwa ukiabudu Latah, U'zzah na Manatah!

Nakushuhudisheni kwa Mwenyezi Mungu je mwajua kuwa huyu mnaye mtukana na kumlaani alikula kiapo cha utii kwa Mtukufu Mtume saww mara mbili zote, kiapo cha utii kwa ajili ya ushindi wa Makkah na kiapo cha utii kwa Mtukufu Mtume saww kinachitwa bai'atu Ridhiwani. Bai'a moja Wewe Ewe Muawiyyah ulikuwa Kafiri na kwa hii ya pili uliivunja hukutimiza!

Nakushuhudisheni kwa Mwenyezi Mungu je mnamjua mnaye mtukana ndiye mtu wa kwanza kumuamini Mtume saww, na wewe Ewe Muawiyyah na baba yako mlikuwa ni mualafat qulubu (wenye kuengwaengwa ili mumuamini Mtume saww na uislamu) mkificha ukafiri na mkidhihirisha uislamu na mnatamanishwa uislamu kwa kupewa mali!

Nakushuhudisheni kwa Mwenyezi Mungu hamumjui huyu Ally mnaye mtukana na kumlaani ndiye aliyekuwa ameshika bendera ya Mtume saww siku ya Badr, na bendera ya mushirikina na makafiri ilibebwa ni Muawiyyah na baba yake Abu Sufiyan, kisha mkapambana naye siku Uhudi, siku ya Khandaki Ally akiwa mshika bendera ya Mtume saww na wewe Ewe Muawiyyah umeshika Bandera ya ushirikina na ukafiri na sehemu zote hizo Mwenyezi Mungu alikuwa akimpa ushindi Mtume saww kupitia kwa Ally a.s na kudhihirikiwa na dalili (hoja) zake akiunusuru wito wa Mtume saww, akizikubali hadithi zake saww, na Mtukufu Mtume saww katika sehemu zote hizo alikuwa akiwa radhi naye, na wewe na baba yako Mtume saww akiwakasirikia!

Nakushuhudisha kwa Mwenyezi Mungu ewe Muawiyyah unakumbuka siku moja alikuja baba yako juu ya ngamia mwekundu, wewe ukimswaga na kaka yako Utbah akimuongoza, kisha Mtume saww alipowaona akasema :. Ewe Mwenyezi Mungu Mlaani aliye panda na muongozaji na mswagaji!

Je umesahau mashairi uliomwandikia baba yako ukimkataza kusilimu alipotaka kusilimu :.

Ewe Swakhar usisilimu hata siku moja utatufedhehesha.

Baada ya yale yaliyotokea kule Badr yalitufanya tukagawanyike.

Mjomba, ami yangu, ami wa mama yangu alikuwa ni mtu wa tatu kuuawa (ni Ally).

Handhwala mtu wa Kheir alikuwa akituongoza sisi tukikubali.

Kufa ni ahueni zaidi kuliko neno la kiu adui (mtu kusema Laila haila llah Muhammad Rasulallah huyo ni adui wa Muawiyyah na Abu Sufiyan ):

Wallahi kile ulichoficha katika jambo lako ni kubwa na baya kuliko hili ulionyeshalo.

Nakushuhudisheni enyi kundi je mwajua kuwa Ally ndiye mtu wa kwanza aliye iharamishia nafsi yake matamanio katika maswahaba wote wa Mtume saww Mwenyezi Mungu akateremsha aya ya kwamba asifanye hivyo:

يا الذين آمنوا لا تحرموا طيبات ما أحل الله لكم.

ENYI mlioamini msiharamishe vitu vizuri alivyohslalisha Mwenyezi Mungu kwa ajili yenu.

Hakika Mtukufu Mtume saww aliwatuma maswahaba wakubwa kwenda kwa Bani Quraydhwa kuwalingani kwa mawaidha mazuri na kutumia busara, wao wakaingia katika ngome zao wakashambuliwa wakakimbia.

Kisha Mtukufu Mtume saww akamtuma Ally a.s amebeba bendera akawapelekekea hukumu za Mwenyezi Mungu na hukumu za Mtume wa Mwenyezi Mungu  na wakazipokea, ni hivi hivi hata kule Khaibarah walishindwa na kukimbia Ally a.s akaenda na kuleta ushindi mkubwa!

Imamu Hassan a.s akasema: Ewe Muawiyyah unadhani hujui kuwa mimi najua Dua'a mbaya aliyokuombea Mtukufu Mtume saww pale alipotaka kuwaandikia barua Bani Huzaimah, kisha Mtume saww akamtuma Ibn Abbas aje akuite, akakukuta unakula, kisha akamtuma tena akakukuta unakula, na mara ya tatu uliposema bado unakula, Mtukufu Mtume saww akasema :. Ewe Mwenyezi Mungu usilishibishe tumbo la Muawiyyah, tukawa na wasiwasi kuwa unaweza kula hadi ufe.

Na nyinyi wafuasi wa Muawiyyah nakushuhudisheni kwa Mwenyezi Mungu, je, hamjui kuwa Mtume saww alimlaani Abu Sufiyan sehemu saba hamuwezi kupinga.

Sehemu ya kwanza ni siku alipokutana na Mtukufu Mtume saww nje ya Makkah, Mtume saww akielekea Twaifu kwenda kuwalingania dini Thaqifa, Abu Sufiyan akamtokea Mtume saww akamtukana, akamtolea shutuma mbaya, akamwambia kuwa ni muongo, mpumbavu na akataka kumpiga Mtume saww. Basi Mwenyezi Mungu na Mtume wake saww wakamlaani na wakamuondoa.

Na sehemu ya pili alipolaaniwa Abu Sufiyan ni katika msafara wa ngamia, pale msafara huo ulipoonekana kwa Mtukufu Mtume saww walipokuwa wakitoka Shamu, Abu Sufiyan akawafukuza hadi pwani waislamu wakawa wameshindwa basi Mtume saww akamuombea Abu Sufiyan laana juu yake, na tukio hili ndilo lililosababisha vita vya Badr.

Sehemu ya tatu aliyolaaniwa Abu Sufiyan ni siku ya Uhudi pale aliposimama chini ya mlima na Mtukufu Mtume saww akiwa juu ya mlima, huku Abu Sufiyan akiita kwa sauti ya juu :. Hubali aheshimiwe! Akarudi rudia mara nyingi. Basi Mtukufu Mtume saww akamlaani mara kumi siku hiyo na waislamu wote wakamlaani.

Sehemu ya nne: Ni siku Abu Sufiyan na Muawiyyah walipokuja na makundi ya wapiganaji wa makabila na mayahudi katika vita vya Khandaki. Basi Mtume wa Mwenyezi Mungu akamlaani na akamuapiza.

Sehemu ya Tano: Ni siku Abu Sufiyan alipokuja na makurayshi wakamzuia Mtume saww kuingia msikiti Mtukufu wa Makkah, na hiyo ni siku ya Hudaybiyah, basi Mtume saww alimlaani Aba Sufiyani akawalaani Viongozi wao wote na wafuasi wao Mtukufu Mtume saww akasema :. Wamelaaniwa wote hakuna katika wao atakaye amini. Mtume akaulizwa :. Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu je, hakutarajiwi yeyote katika wao anaweza kusilimu vipi unawalaani hivyo? Mtukufu Mtume saww akasema :. Laana hii haitawafika yeyote katika wafuasi, ama Viongozi hawatafaulu katika wao hata mmoja na Viongozi walikuwa ni Abu Sufiyan na wewe Muawiyyah na wengine.

Sehemu ya Sita: Ni siku ya ngamia mwekundu.

Na sehemu ya saba :. Ni siku walipomsimamisha Mtume kule A 'qabah wakimtishia mnyama wa Mtume saww ili amuangushe na wamuuwe. Na walikuwa watu kumi na mbili miongoni mwao ni Abu Sufiyan,  Umar na wewe Muawiyyah.

 

Mtukufu Mtume saww alisema :. Kuna wanafiki kumi na mbili (katika maswahaba wangu) wa nane katika wao hawataingia peponi hadi ngamia aweze kuingia katika tundu la sindano..

Haya ndiyo majibu aliyopewa Muawiyyah ni Imamu Hassan a.s alipoanza kuvunja mkataba wa Makubaliano na kuanza kushutumu na kuwatukana hadharani.

Hata hivyo Muawiya  alikataa kuyafuata masharti yote ya mapatano. Ingawa Imamu alikuwa akiishi hali ya kujitenga (peke yake) na kwa maisha ya usalama hakuachwa atulie. Watu wa ukoo wa Banu Umayyah walianza kumfanyia Propaganda dhidi yake.

Basi ubaya wao wa mara kwa mara, matusi na masingizio yalipofikia kiwango ambacho kiasi chake kinaweza kuonekana kutokana na maneno aliyoyasema Imamu Hussein a.s akimwambia Marwan, wanafiki walipokuwa wakilia katika maziko ya Imamu Hassan a.s, "Leo mnalia ni nyinyi mliompa (Imamu Hassan a.s) mishituko hii ambayo ni sisi tu tunaoweza kuitambua." Kisha Marwan akasema: "ndio, hiyo ni kweli kabisa. Lakini hayo yote nimemtendea yule mtu aliyekuwa na uvumilivu mkubwa kuliko mlima huu."

Rejea: Muruuju dhahab chenye Tarekhul Kamil Jz 6.

Tadhkiratul Khawas.

Nasaihu Kafia. Tarekhul Abil Fidaa Jz 1.

Tarekhul Ibn Asaakir Jz 4.

Al Iqdul Farid Jz 2 na Jz 3 na vingine vingi vya Tarekh.

Rejea sahihi Bukhari.

Fuatana nami sehemu ya saba historia ya Maasumu Hassan bin Aliy a.s.

Toa maoni yako

Maoni ya watumiaji

Hakuna maoni
*
*

Site ya Al-Imaamaini Al-Hassanaini (A.S) ya usambazaji wa utamaduni wa Kiislamu na mafunzo ya Kidini