Site ya Al-Imaamaini Al-Hassanaini (A.S) ya usambazaji wa utamaduni wa Kiislamu na mafunzo ya Kidini

BIBI FATIMA (A.S) KIIGIZO CHEMA KWA WANAWAKE 9

0 Voti 00.0 / 5

BIBI FATIMA (A.S) KIIGIZO CHEMA KWA WANAWAKE

Sehemu ya Tisa

MADHARA YA KUCHANGANYIKA WANAUME NA WANAWAKE

Mchanganyiko unaokusudiwa hapa ni ule wa kukaa pamoja wanaume na wanawake wakawa wanatazamana ana kwa ana bila kuwepo kizuizi baina yao kitakacho tenganisha pande mbili hizi.

Kutokana na maumbile ya wanaadamu yalivyo, sheria ya KiIslamu haikubaliani na kitendo hiki cha kuchanganyika wanawake na wanaume, na hapana shaka kwamba Mwenyezi Mungu anachukizwa na jambo hili. Kwa nini basi jambo hili liwe baya?

1. Ni kuvunja moja katika sheria za Kiislamu (Hijabu) na ni kukaribisha maovu katika jamii.

2. Jambo hili huandaa na kurahisisha njia za kupatikana mahusiano ya kijinsiya baina ya pande mbili hizi kinyume na utaratibu uliowekwa kisheria.

3. Jambo hili huwa ndiyo chanzo na sababu ya kuharibu familia na kuzitenganisha na ni kivutio kikubwa cha maovu ndani ya jamii.

4. Jambo hili linasababisha misiba na majonzi, pia linaleta uharibifu mkubwa kati ya pande mbili husika.

Kwa hiyo mchanganyiko kati ya wanaume na wanawake ni kirusi chenye maradhi hatari yanayotishia usalama na mwenendo wa familia, kiasi kwamba tunaweza kuyafananisha na maradhi ya kansa ambayo mgonjwa huwa hapati nafuu isipokuwa kwa kuikata shemu iliyopatwa na ugonjwa huo na kukiondoa kiini cha ugonjwa. Katika nchi au jamii zilizoruhusu mchanganyiko huu, hapana shaka kwamba zimechangia sehemu kubwa ya ongezeko la maovu na kufikia idadi inayotisha hasa katika mashule na vyuo vikuu ambako wasichana na wavulana wanachangaywa pamoja utadhani ni viumbe wenye jinsi ya moja. Matokeo ya mchanganyiko huu ni kugeuka kwa mashule haya na vyuo hivi kuwa vituo vya mafunzo ya uhuni na mambo machafu ambapo lengo lake lilikuwa ni kupafanya kuwa mahali pa kujifunza elimu. Yote haya yanakuja kwa sababu ya kukosekana kwa sitara au kizuwizi cha kuzitenganisha jinsiya hizi mbili.

Katika ripoti moja iliyotolewa na Jaji mmoja wa Kimarekani anasema: "Asilimia 45% ya wasichana wanaosoma katika shule za mchanganyiko hupoteza bikra zao kabla ya kutoka shuleni, na asilimia hii huzidi kadri wasichana wanavyoendelea katika masomo ya juu." Huko Uingereza wasichana wamekuwa wakiandaliwa kutembea na vidonge vya kuzuwiya mimba, na kwamba asilimia 80% ya wasichana hutembea na vidonge hivyo katika mikoba yao. Hii ni dalili ya wazi inayotuonesha kwamba, wasichana hao huwa wako tayari wakati wowote ule kutenda kitendo kichafu kwa kuwa kinga wanayo. Wasichana hawa wanayafanya haya kukwepa matokeo mazito yanayoweza kuwakuta ndani ya uchafu huo wanaoutenda[1]. Lakini je hivi kweli ni sahihi kumuacha msichana akawa katika mazingira kama haya ndani ya jamii hasa ya Kiislamu?

Baada ya maelezo haya bila shaka ina dhihiri wazi hekima kubwa iliyomo katika Uislamu katika kupiga marufuku michanganyiko baina ya wanaume na wanawake. Hapana shaka kabisa kwamba, Uislamu lengo lake ni kutaka kuiepusha jamii kutokana na hatari tulizozitaja hapo kabla. Ndiyo maana umeharamisha mchanganyiko kati ya wanaume na wanawake katika sehemu zote, kama vile mashuleni, vyuoni, katika sehemu za sherehe, na kwa ujumla popote katika jamii mchanganyiko kati ya wanaume na wanawake hauruhusiwi.

Yote haya makusudio ni kuihifadhi jamii kutokana na maovu yanayozaliwa na michanganyiko. Na ama hali ya mikusanyiko ya wanaume na wanawake tunayoiona katika msimu wa Hija na katika maeneo matakatifu na pia ndani ya kumbi za Huseiniyyah, mikusanyiko kama hiyo haikuharamishwa hasa kwa kuwa wanawake wanaohudhuria ndani ya maeneo hayo huwa wako katika hali ya kujisitri kama sheria inavyowataka wajisitri.

 

 


[1]. Kitabu Qadhaya Az ziwaj wal Usrah.

Toa maoni yako

Maoni ya watumiaji

Hakuna maoni
*
*

Site ya Al-Imaamaini Al-Hassanaini (A.S) ya usambazaji wa utamaduni wa Kiislamu na mafunzo ya Kidini