• Anza
  • Iliyopita
  • 5 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 6119 / Pakua: 2208
Kiwango Kiwango Kiwango
MUONGOZO KWA WASOMAJI

MUONGOZO KWA WASOMAJI

Mwandishi:
Swahili

MASOMO YA KI-ISLAMU

MUONGOZO KWA WASOMAJI

KIMEANDIKWA NA: OMAR JUMAA MAYUNGA

KIMETOLEWA WAVUNI NA TIMU YA: AHLUL BAYT DIGITAL ISLAMIC LIBRARY PROJECT

UTANGULIZI

Alhamdulillah, Rehma na Amani zimshukie Mtume wetu na Muombezi wetu Muhammad(s.a.w.w) na Aali zake watukufu waliotakaswa. Ninamshukuru zaidi Mwenyeezi Mungu kwa kuniwafiqisha kuchapisha kitabu: Muongozo wa Wasomao, kama alivyoniwafiqisha kabla ya hiki kuchapisha vitabu: Mut'a ndoa sahihi na Meza ya uchunguzi na vingine vingi, Alhamdulillah, Muongozo wa Wasomao, ni kitabu kilichokusanya maudhui nyingi tofauti kwa muhtasari. Ndani yake tumejaribu kufafanua baadhi ya mambo yaliyoeleweka kimakosa, kwa kuonyesha ushahidi na rejea zake. Nataraji hili litakuwa ni kichocheo cha wasomi (masheikh) kutufunulia yaliyofichikana au kufahamika kimakosa katika tarikh ili waislamu wapate ufahamu vyema Uislamu wao. Ee Mola weta! Tuonyeshe Haki tuifahamu kuwa ni haki uturuzuku kuifuata. Na tuonyeshe batil tuifahamu uwa ni batil uturuzuku kuiepuka.

Omar Jumaa Mayunga 9 Shaaban 1413 1 Februari 1993 Dar Es Salaam

MASOMO YA KI-ISLAMU

MUONGOZO KWA WASOMAJI

MWANZO WA WAHY

Amesema Bukhari na Muslim na wengineo kuwa: Imepokewa kutoka kwa Azzuhry naye amepokea kwa U'rwa bin Zubeir naye amepokea kwa Mwana Aisha (mkewe Mtume) kwamba: Malaika Jibril(a.s) alikuja kwa Mtume(s.a.w.w) naye akiwa katika pango la Hiraa akamwambia: Soma, Mtume akajibu: Mimi sijui kusoma. Mtume anasema: Malaika akanikaba kwa nguvu mpaka nikazidiwa kisha akaniambia: Soma, Mtume akajibu: Mimi sijui kusoma. Kisha ndipo Malaika alipomsisitiza kwa nguvu akisema: "Soma kwa jina la Mola wako, ambaye ameumba. Amemuumba mwanadamu kutokana na damu iliyoganda. Soma na Mola wako ni Mtukufu kuliko wote " Qur'an; 96:1-3.

Baada ya hapo, Mtume(s.a.w.w) alirudi kwa mkewe mwana Khadija(a.s) akiwa amejawa khofu kubwa. Alipoingia ndani alijitupa chini na huku akilalamika: "Nifunikeni, nifunikeni!!" Alipotulia akasema: "Ninaogopa sijui kitanipata nini?!" Khadija akamtuliza: "Sivyo! Wallahi Mwenyeezi Mungu hatakuangamiza abadani, wewe unaunga udugu, unavumilia matatizo, unasaidia wanyonge, unasaidia kuleta haki." Hapo Khadija akamchukua Mtume akampeleka kwa Ibnu ammi yake Waraqa bin Nawfal (alikuwa mnasara, mwandishi wa Injili kwa lugha ya kiibrania). Walipofika kwa Waraqa, Khadija akamwambia: "Ewe Ibnu ammi! Msikilize Muhammad aliyo nayo." Waraqa akamuuliza, "una nini?" Muhammad akamwelezea yote kama aliyoyaona, Waraqa akamwambia: "Huyu ni Malaika ambaye amepata kumteremkia vilevile Nabii Musa(a.s) Ee!" Natamani kama nitakuwa hai wakati watakapokufukuza watu wako! Muhammad(s.a.w.w) akashituka: "Watanifukuza?" Waraqa akajibu: "Ndiyo, hakuna mtu yeyote anayeleta jambo kama hili uliloleta wewe isipokuwa atapigwa vita na watu wake".[1]

Madda hii (mwanzo wa Wahy) waandishi wameieleza kwa njia nyingi tofauti zenye kugongana. Hapa tutajaribu kuzitaja chache tu:

A . Khadija na Abubakr walimpeleka Muhammad(s.a.w.w) kwa Waraqa bin Nawfal baada ya kuelezwa Waraqa kuwa Muhammad amepata matatizo, Waraqa akamuuliza Muhammad ana nini? Muhammad(s.a.w.w) akamwambia: "Ninasikia ninaitwa nyuma yangu, ewe Muhammad ewe Muhammad, nikisikia hivyo mimi hukimbia ovyo." Waraqa akamkataza asiwe anakimbia bali akaze roho ili ayasikie anayoambiwa..." Muhammad alishika maelekezo hayo, mara aliposikia akiitwa: Ewe Muhammad! Sema, Bismillahir Rahmanir Rahim, Alhamdulillahi rabbil a'lamina.... mpaka mwisho wa suratul Fatiha. Akaambiwa: Sema: "Laa ilaha illallahu" Muhammad(s.a.w.w) baada ya hapo alikwenda kwa Waraqa bin Nawfal, akamjulisha hali hiyo. Waraqa akambashiria habari njema yakuwa: "Hali kama hiyo alipewa pia Nabii Isa bin Maryam".[2]

B . Khadija alipompeleka Muhammad(s.a.w.w) kwa Waraqa na akamweleza yaliyomtokea. Waraqa alisema: "Huyu ni Nabii wa Umma huu, mwambie atulize moyo."[3]

C . Khadija alimwambia Muhammad(s.a.w.w) atakapokufikia huyo anayekusomesha, unambie, Mtume(s.a.w.w) alipofikiwa na hali hiyo akamjulisha mkewe. Khadija akampakata katika mapaja yake, kisha akavua shungi yake, mara Mtume(s.a.w.w) akaona yule aliyemjia anaondoka haraka. Mtume akamjulisha mkewe hilo, Khadija akasema, "Huyo ni Malaika, na wala siyo shetani, basi kaza roho na furahi".[4]

D . Waraqa bin Nawfal alimwambia Khadija: "Muulize Muhammad(s.a.w.w) nani anaemjia! Ikiwa ni Malaika Mikaeli basi amemletea amani. Na ikiwa ni Malaika Jibril basi amemletea vita na mateka. Khadija Alipomuuliza Mtume(s.a.w.w) akajibu: "Ni Jibril". Khadija akapiga uso wake.[5]

E . Khadija alipewa kipande cha karatasi na mganga mmoja ili ampe Muhammad(s.a.w.w) kama hali hii (iliyomfikia Muhammad) inasababishwa na ugonjwa wa kichaa, basi atapona... Khadija aliporudi kwa mumewe akamkuta anasoma Qur'an, Khadija akamchukua akaenda naye kwa yule mganga, walipofika kwa mganga, akafunua mgongo wa Mtume akaona muhuri wa Utume uko kati ya mabega mawili![6]

F . Muhammad(s.a.w.w) alipofikiwa na hali hiyo (ya kujiwa na Malaika) alikuwa akipanda katika kilele cha mlima mrefu na akitaka kujitupa chini (ili afe).[7]

G . Muhammad(s.a.w.w) alirudi kwa mkewe (kutoka katika pango) akiwa nafuraha kubwa akamwambia mkewe: "Nataka kukueleza habari njema, mimi nimeona katika ndoto kuwa Jibril amenijulisha kwamba ametumwa na Mola wangu aje kwangu... Khadija akamwambia: "Furahi, wallahi Mwenyeezi Mungu hatakufanyia lolote ila lililokuwa la kheri... kisha Khadija akaenda kwa mganga wa kinasara, kuuliza uwezekano wa kumuona Jibril. Mganga alishangaa sana kusikia jina la Jibril katika nchi hiyo, kisha akasema kuwa: "Huyo ni Mjumbe wa Mwenyeezi Mungu..."[8]

MJADALA WA RIWAYA ZA WAHY

Kwa kweli tukitaka kuijadili mada hii kwa undani zaidi, itatulazimu tutumie muda mrefu katika kuchambua kifungu kimoja baada ya kingine. Na hilo litahitaji kuchukua nafasi ya kitabu kizima ili kujaribu kutatua utata huo. Lakini, kama wasemavyo wataalamu: "Maa Laa yudraku kulluhu laa yutraku kulluhu" yaani, "Yasiyowe za kupatikana yote, hayaachwi yote". Kwa hiyo nasi hatutaacha kutaja japo kidogo:

1. Kutokana na sanad ya Hadithi, ambapo mategemeo yake yamepokelewa katika sahihi mbili (Bukhari na Muslim) na zingine, ambazo zinaonyesha kama: Imepokewa kutoka kwa Az Zuhry kutoka kwa U'rwa bin Zubeir kutoka kwa Mwana Aisha. Sasa: hapa tutaangalia mambo ya fuatayo:

A . Az Zuhry na U'rwa hawa walikuwa wapinzani wa Imam Ali(a.s) na wakimtukana.[9]

Na Mtume(s.a.w.w) amesema juu ya Imam Ali(a.s) kuwa: "Yeyote mwenye kumtukana Ali basi amenitukana mimi na mwenye kunitukana mimi amemtukana Mwenyezi Mungu".[10]

Kwa hiyo, mtu mwenye kumtukana Mtume(s.a.w.w) hawezi kuwa mwema hata kidogo, licha ya kupokea mafunzo ya dini kutoka kwake.

A . Amma kuhusu Mwana Aisha (mkewe Mtume) ambae katika mwaka wa thelathini na sita Hijra, alitoka nyumbani mwake Madina kwenda Basra ili kumpiga Ali bin Abi Talib(a.s) na akafanya hivyo. Kitendo cha mke wa Mtume cha kutoka nyumbani mwake kwenda nje, ni jambo lililokatazwa na Mwenyeezi Mungu: "Na kaeni majumbani mwenu " Quran,33:33.

Mwana Aisha ameipuuza hukumu hii! Aidha, kitendo cha kumpiga Imam Ali(a.s) ni jambo linalomuweka mtu mahala pabaya. Imepokewa kutoka kwa A'diyyi bin Thabiti kutoka kwa Zuhry amesema: "Amesema Imam Ali kuwa: "Ninaapa kwa ambaye ameumba mbegu na akaumba upepo, hiyo ni ahadi ya Mtume kwangu mimi kuwa: Hanipendi mimi isipokuwa mu'umin na hanibughudhi (hanichukii) mimi isipokuwa mnafiki".[11]

Mwana Aisha ameipuuza hukumu hii! Nanikweli Mwana Aisha hampendi kabisa Imam Ali(a.s) . Hilo linathibitishwa na hali halisi, kwanza, amepigana na Imam Ali(a.s) na kupiga hakuanzi kabla ya kuchukia. Na alipopata habari Mwana Aisha kuwa Imam Ali ameuliwa, alisujudu kumshukuru Mwenyeezi Mungu![12]

Mwenyeezi Mungu anasema: "Haiwi kwa mwanamume aliyeamini, Mwenyeezi Mungu na Mtume wake wanapohukumu jambo wawe na hiari katika shauri lao. Na mwenye kumuasi Mwenyeezi Mungu na Mtume wake, hakika amepotea upotovu ulio wazi " Quran, 33:36.

1. Riwaya za tukio hilo zinagongana kama unavyoziona - kama utarejea kuzisoma utaliona hilo. Lakini, kwanini Jibril amkamate Mtume kisha amkamuekamue mpaka akaribie kuzimia!? Kwanini Mtume akubali kusoma baada ya kukamuliwa kwa nguvu mara ya tatu? Kwanini asikubali tu kusoma mara ya kwanza kabla ya mateso haya? Na, vipi Mtume arudi kwa mkewe akiwa na khofu kubwa kiasi hiki! Je! Muhammad(s.a.w.w) hakuwa na uwezo wa kumpiga kofi malaika huyo?! Kama alivyofanya hivyo Nabii Musa(a.s) alipoijiwa na Malaika I'zrail ili achukue roho yake, Musa alimpiga kofi moja tu mpaka jicho likang'oka![13]

Haiwezekani kuwa Mtume Muhammad(s.a.w.w) alikuwa mwoga hivyo, na Nabii Musa tu peke yake awe shujaa wa kuwang'oa macho malaika!.

2. Kwamba, Mtume(s.a.w.w) aliingiwa khofu kubwa, Khadija na Waraqa walimtuliza mpaka akatulia. Sasa, tuangalie hali hii kama ifuatavyo:

A . Inawezekana kwa Mwenyeezi Mungu, kumpeleka Mtume ambaye hajui Utume wake yeye mwenyewe! Ila kwa Kuthibitishiwa na mwanamke na mnasara? Vipi jambo nyeti hili agundue mwanamke kuwa huo ni Utume na wala si kichaa (kama alivyodhani Muhammad) pia mnasara ajue yaqini kuwa huo ni Utume?! Hili linatupa kufikiri kuwa hawa (mwanamke na mnasara) ni wajuzi na watukufu zaidi kuliko Muhammad(s.a.w.w) .

B . Mwenyeezi Mungu anasema: "Na wakasema waliokufuru: mbona haikuteremshwa kwake Qur'an yote mara moja? Ndivyo ilivyo, ili tukuimarishe kwayo moyo wako na tumeipanga kwa mpango ." 25:32. "Waambie (Muhammad) roho takatifu ameiteremsha kutoka kwa Mola wako kwa haki, ili kuwaimarisha wale walio amini, na kuwa muongozo na habari njema kwa waliosilimu ." 16:102.

katika aya hizi timachunguza ibara isemayo: "Ilu Tukuimarishe Kwayo Moyo Wako ". Kwa hiyo, moyo wa Muhammad uliimarishwa na Mwenyeezi Mungu sikiliza Mwenyeezi Mungu analifafanua hili: "Waambie (Muhammad) hakika mimi ninayo dalili ya wazi itokayo kwa Mola wangu " 6: 57.

"Waambie (Muhammad) Hii ndiyo njia yangu, ninaita kwa ujuzi hasa, mimi na wanaonifuata ." 12:108.

Katika Aya hizi tunaangalia maneno: "Mimi Ninayo Dalili Ya Wazi Itokayo Kwa Mola Wangu" "Ninaita Kwa Ujuzi Hasa" kwahiyo, Mtume Muhammad(s.a.w.w) anajua kuwa anayo dalili (ushahidi) ulio wazi, na kwa ajili hiyo, anawaita watu kwa ujuzi kamili. Hii si sawa na kusema: Muhammad(s.a.w.w) uliimarishwa moyo wake na mnasara (Waraqa bin Nawfal).

MUHARRAM SI MWANZO WA MWAKA

Baada ya kujua mwaka wa Kiislaam unaanza tarehe gani ya mwezi gani, kisha umeingia utata juu ya jambo hili kuwa:

Muharram ndiyo mwanzo wa mwaka wa Kiislaamu kwa maana ya Hijra! Ndiyo maana unaona kila uingiapo Muharram baadhi ya Waislam hufanya hafla kubwa kuadhimisha, wakidhani kuwa umeingia mwaka mpya! Ukisoma tarikh utaona kuwa:

A . Imam Ali(a.s) alisema mwaka mpya uanze ile siku aliyofukuzwa Mtume(s.a.w.w) Makka akaenda Madina.

B . Imam Ali aliwaandikia watu wa Najran akasema.... "Na aliandika Ubeidullah bin Abi Rafii tarehe kumi mfungo tisa mwaka wa thalathini na saba kutoka Mtume (s.a.w.w) aingie Madina ".[14]

C . Imam Malik bin Anas anasema: Mwanzo wa mwaka wa Kiislaamu ni mfungo sita, kwa sababu ni mwezi ambao Mtume(s.a.w.w) amehama (kutoka Makka kwenda Madina).[15]

D . Assakhawy amepokea kwa Al'Asmai kuwa wao walikuwa wakiandika mfungo sita, ni mwezi aliohamia Madina Mtume(s.a.w.w) .[16]

E . Amesema Assahib bin U'bbad kuwa: Mtume(s.a.w.w) aliingia Madina tarehe kumi na mbili mfungo sita, na tarehe ikaanzia hapo. Kisha baadae jambo hili liligeuzwa likarudishwa mwezi wa Muharram".[17]

KUONEKANA KWA MWENYEEZI MUNGU

Suala la kuonekana Mwenyeezi Mungu, Waislaamu wamegawanyika makundi mawili, kuna wanaosema kuwa: Mwenyeezi Mungu anonekana hapa duniani na huko akhera. Na kuna wanaosema kuwa: Mwenyeezi Mungu haonekani hapa duniani wala huko akhera. Kila kundi lina hoja zake. Wasemao ataonekana wanategemea hoja mbili: Dalilul a'qly, Dalilun naqly.A. Dalilul a'qly - Kwa kupitia mantiq akili inaona kuwa: kwa kuwa chochote chenye kuwapo lazima uwiano wa kuonekana uwepo.

B . Dalilun naqly: Mwenyeezi Mungu anasema:

i.Na alipofika Musa kwenye miadi yetu, na akazungumza na Mola wake akasema: "Mola wangu! Nionyeshe ili nikuone." Akasema "Huwezi kuniona, lakini tazama jabali, kama litakaa mahala pake ndipo utaweza kuniona " Quran: 7:143.

ii. "Nyuso siku hiyo zitang'aa zikitazama kwa Mola wao " 75: 22-23

MAJIBU YETU

Kwanza, ni muhimu kuangalia maana ya tamko la "ARRU-UYA" yaani "KUONA". Taqriban tamko hili linatumika katika nyanja zifuatazo,

(a) Kuona kwa mboni za macho.

(b) Kuona kwa dhana.

(c) Kuona kwa yaqin.

Sasa: Inaposemwa: Mwenyeezi Mungu anaonekana, ni kwa kupitia kigezo gani kati ya vigezo vilivyotajwa hapo juu au chochote kingine. Ikiwa kuwepo kwa kitu ni sharti ya kuonekana, ni nani basi aliyethibitisha mpaka sasa kuwa ameiona Roho, Akili, Nguvu, Sauti, na kadhalika?! Kuhusu aya zilizosomwa kuthibitisha kuwa Mwenyeezi Mungu anaonekana, majibu yake ni kama ifuatavyo:

A . Nabii Musa(a.s) alikuwa akijua vyema kuwa Mwenyeezi Mungu haonekani duniani wala huko akhera. Wala hilo ombi lake hakukusudia kuomba jambo lisilo wezekana, isipokuwa Nabii Musa hapa ametumia uslub (njia) ya kukomesha madai ya watu wake ambao waling'ang'ania kumtaka awaonyeshe Mwenyeezi Mungu waziwazi kama tunavyo soma katika Qur'an: "Ewe Musa, hatutakuamini mpaka tumuone Mwenyeezi Mungu waziwazi ". 2:55

Kwahiyo, Nabii Musa(a.s) alitaka kumaliza ubishi wao, akatumia ibara kati yake na Mola wake ili afute kabisa matumaini ya ombi la watu wake. Qarina ya nukta hii ni pale aliposema Mwenyeezi Mungu kuwa: "Hakika walimuomba Musa makubwa kuliko hayo, na wakasema: Utuonyeshe Mungu wazi wazi ." 4:153

B . Iliposemwa: "Fasawfa Taraani " yaani "Utaniona" ibara hii imetanguliwa na tamko la: " LAN TARAANI " yaani, " HUTANIONA ABADANI " silabi ya " LAN " imekuja katika " NAFYU TAABID " " HUTANIONA ABADAN " matumaini ya kumuona Mwenyeezi Mungu hayako aslan, kwa mujibu wa maweko ya silabi na matumizi yake yaliyokuja katika Aya hii. c. Iliposemwa: " ILA RABBIHA NADHIRA ". yaani,Zikingoja Malipo Kwa Mola Wao " na wala siZikitazama Kwa Mola Wao , hiyo ni tasfiri ya kimakosa kama tutakavyoonyesha. Ku'unganishwa silabi ya "ILA" na silabi ya "Nadhar " hapa kunafidisha maana yaa "Kungojea " Tutaonyesha mfano hapa kuthibitisha hilo kama ifuatavyo: katika kitabu: Lisanul A'rab juzu ya saba ukurasa 72 imeandikwa hivi:- "Innamaa Nandhuru Ila Llahi Thumma Ilayka " akafafanua hapo hapo: "Innamaa Atawaqqau Fadhlallahi Thumma Fadhlak " Maana ya msitari wa kwanza "Kwa hakika tunangojea fadhila za Mwenyeezi Mungu, kisha fadhila zako" katika msitari wa pili, alikusudia kufafanua ibara isemayo: "Nandhuru Ila Llahi " akasema; "Atawaqqau Fadhla Llahi " yaani, "Ninangojea Fadhila za Mwenyeezi Mungu". Hivi ndivyo yalivyo matumizi ya silabi ya "ILA" inapokutana na silabi ya "NADHAR" mara nyingi.

HADITHI ZISEMAZO KUWA ATAONEKANA

Anasimulia Abu Huraira katika Hadithi aliyoipokea kuwa: (siku ya kiyama) "Mwenyeezi Mungu atawaijia (watu) akiwa na sura tofauti na ile wanayomjua, awaambie: Mimi ndiyo Mola wenu. (Watu) watajibu: Mwenyeezi Mungu atuepushe nawe, sisi tutabaki hapa hapa mpaka Mola wetu (tunayemjua) atufikie, na akija sisi tutamjua. Mara Mwenyeezi Mungu atawafikia kwa sura yake ile wanayomjua atasema: Mimi ni Mola wenu. Nao watajibu: (kweli) wewe ndiye Mola wetu, na watamfuata".[18]

Abu Huraira anaendelea kusimulia: "Watu walimuuliza Mtume(s.a.w.w) 'Ewe Mjumbe wa Mwenyeezi Mungu! Hivi tutamuona Mola wetu siku ya kiyama?' Mtume(s.a.w.w) akajibu: 'Hivi mnapata pingamizi gani kwa kutazama mwezi wa siku kumi na tatu?' Wakajibu: 'Hatupati pingamizi yoyote.' Mtume(s.a.w.w) akauliza tena: 'Mnapata kizuizi gani kutazama jua ambalo halina mawingu?' Wakajibu: 'Hakuna kuzuizi chochote.' Mtume(s.a.w.w) akawaambia: 'Basi ndivyo matakavyomuona". Suhaybu anasimulia kuwa: Amesema Mtume kuwa: "Watu wa peponi watakapoingia Peponi, Mwenyeezi Mungu atawauliza: 'Mnataka niwaongeze kitu gani?' Watasema: 'Oh, umekwisha ng'arisha nyuso zetu, umetuingiza peponi na umetuepusha mbali na moto.' (Hapo) Pazia litaondolewa, eeh, hawajapewa kitu kilicho bora zaidi kuliko kumuona Mola wao. Kisha Mtume(s.a.w.w) akasoma aya: "Wale waliofanya wema watapata wema na zaid ". 10:26

Iliposemwa: (katika Aya iliyotangulia), "Waziyadah " maana yake: Kumuona Mwenyeezi Mungu"[19]

MAJIBU YETU

Tamko la "Azziyadah " katika sura ya kumi aya ya ishirini na sita ni: MUB'HAM halionyeshi chochote kuhusu kuona. Kwa hiyo, huwezi kwa tamko hilo kuthibitisha kuwa Mwenyeezi Mungu anaonekana. Bali lililothibiti waziwazi ni hivi asemavyo Mwenyeezi Mungu kuwa, "Maono hayamfikii bali yeye anayafikia "Maono", 6:103. Kwahiyo, zile hadithi zisemazo kuwa Mwenyeezi Mungu anaonekana ni batili kwa sababu zinapinga Aya. Mwenyeezi Mungu anakataa kuwa: "Maono hayamfikii" na maono ni zaidi kuliko macho!!

QUR'AN IMEUMBWA

Ndugu zetu masunni wanaamini kuwa: Qur'an ni ya tangu na tangu (Qadim) Mashia Ithan Ashar wanaamini kuwa: Qur'an imeumbwa. Kwahiyo, hapa tutachunguza kama ifuatavyo:

Katika matumizi ya lugha ya kiarabu, tamko la "JAA'L". Linapotegemezwa kwa Mwenyeezi Mungu huwa kwa maana ya "KHALQ" yaani, "Kuumba ". Na hapa tutataja baadhi ya mifano hiyo:

A . "Wajaa'la min'ha zawjaha " yaani, "Na ameumba mkewe ".

B . "Huwalladhi jaa'la lakumul layla " yaani, "Yeye ndiye aliyewaumbia usiku ".10:6

C . "Inna jaa'lna maa'l ardhi ziinatan laha " yaani, "Kwa hakika tumeviumba vyote vilivyoko juu ya ardhi viwe mapambo yake ". 18:7

D . "Jaa'la laum min anfusikum az'wajan " yaani, "Amewaambieni wake katika jinsi yenu ". 42:11.

E . "Inna jaa'lnahu Qur'anan a'rabiyyan " yaani,hakika tumeifanya (tumeiumba) Qur'an (kwa lugha ya) Kiarabu ". 43:3

f. "Khaaliqu kulli shay'in " yaani, "Muumba wa kila kitu ". 6:102

Sasa, Qur'an ama iwe ni kitu au isiwe ni kitu. Kama itakuwa sikitu, basi yanini kujadili jambo ambalo halipo! Na endapo itasemwa kuwa Qur'an ni kitu, jee! Ni kwa hoja gani Qur'an itatolewa katika umuun ya ibara hii: "Muumba wa kila kitu"? Na hapana shaka yoyote, Qur'an ni kitu, kwa hiyo: kwakuwa vitu vyote vimeumbwa (kama isemavyo Qur'an) Qur'an nayo pia imeumbwa.

TAQIYYA

Maana ya Taqiyya, kama alivyo tafsiri Sahaba Abdullah ibn Abbas ni "Kusema kwa ulimi na hali moyo unatulia kwa imani". Kwa hiyo, Taqiyya ni kuficha imani ndani ya moyo, na kutamka kwa ulimi yaliyo kinyume na ya moyoni.[20]

Kwakupata ufafanuzi katika somo hili, tumsikilize Imam Bukhari anasema: "Imepokewa kutoka kwa Abu Dardai anasema: 'Hakika sisi wallahi tunawakenulia jamaa ili hali nyoyo zetu zinawalaani."[21]

Abu Dardai anatufahamisha hapa yakuwa: Wao wanapojumuika na baadhi ya watu wasioafikiana nao katika jambo fulani, huchanganyika nao kwa bashashi kubwa kwa kicheko na kukenua mena kama kwamba wanakubaliana na yao. Kumbe ndani ya mioyo yao wanawalaani! Hii ndiyo Taqiyya tunayo izungumza hapa, na ndiyo Taqiyya aliyoisema Mwenyeezi Mungu: "Waumini wasiwafanye makafiri kuwa viongozi badala ya waumini. Na atakaefanya hivyo, basi hatakuwa na chochote kwa Mwenyeezi Mungu, isipokuwa kwa kujilinda nao sana " 3:28.

Iliposemwa: "Na atakaefanya hivyo" maana yake: "Atakaewafanya makafiri kuwa viongozi wake" Mwenyeezi Mungu anamwambia: "Hatakuwa na chochote kwa Mwenyeezi Mungu". Kwa mantiq hii, Mwislamu yeyote anayeongozwa na kafiri, hana chochote kwa Mwenyeezi Mungu. Mpaka hapa hukumu hii itawagusa Waislamu wengi sana! Lakini Alhamdulillah hali haiko hivyo, kwa sababu ibara katika Aya inaendelea kusema: "Isipokuwa kwa kujilinda nao sanasana".

Taqiyya imemuopoa Mwislamu katika hukumu aliyohukumiwa laiti isinge kuwapo Taqiyya. Kwa ajili hii, sahaba Ammar bin Yasir alipoadhibiwa na makafiri, akauliwa mama yake, Sumayya, mbele ya macho yake baada ya kuteswa sana. Hilo halikutosha, akachukuliwa baba yake Yasir akawekwa mbele ya macho yake, akateswa sana hatimae akauliwa, kisha ndipo walipomgeukia naye Ammar, akapigwa na kuteswa, Ammari ndipo alipotamka neno la kufru.

Alipofika kwa Mtume(s.a.w.w) Ammar aliliya sana na kusema: "Ewe Mjumbe wa Mwenyeezi Mungu, nitauweka wapi uso wangu ili hali mimi nimesema neno chafu (la kufru) baada ya kuteswa sana, na kuniulia mbele ya macho yangu wazazi wangu wawili baba na mama! Kabla Mtume(s.a.w.w) hajasema lolote Mwenyeezi Mungu akateremsha Aya: "Anayemkataa Mwenyeezi Mungu baada ya imani yake (ataadhibiwa adhabu kali) isipokuwa yule aliyelazimishwa hali moyo wake unatulia kwa imani " 16:106.

Mtume(s.a.w.w) akamsomea Aya hii Ammar bin Yasir, kisha akamwambia: "Basi, kama watarudia (kukutesa) rudia (nawewekuwapa maneno ya kufru).[22]

Hii ndiyo Taqiyya wanayoelekezwa waumini, kama ambavyo Taqiyya inamfikisha Mwislamu katika ngazi ya Uumini. Mwenyeezi Mungu anasema: "Na akasema mtu muumini aliyekuwa mmoja wa watu wa Firauni anayeficha imani yake, jee! Mtamuua mtu kwa sababu anasema Mola wangu ni Mwenyeezi Mungu ? 40:28.

Huyu bwana alionyesha ukafiri, akasihi pamoja najamaa yake Firauni, lakini kwa ndani alikuwa muumini kweli kweli, akatumia Taqiyya ili Firauni asimjue. Mpenzi msomaji! Bila shaka umeona nafazi ya Taqiyya iliyo nayo katika Uislamu, umefahamu kuwa Taqiyya ni kiungo muhimu sana kati ya Islam na Mwislamu. Umesoma Aya zilizozungumza kuhusu Taqiyya umemuona Sahaba Ammar bin Yasir alivyowakejeli makafir kwa kutamka neno Ia kufru, kisha Mtume(s.a.w.w) akaongeza kusema: "Kama Watarudia Nawe Rudia ".

TAHRIFUL QUR'AN

Takriban, kuna aina tano za Tahrif, nazo ni kama ifuatavyo:

1. Kupungua, au kuzidi, harfu au haraka, wakatihuo huo Qur'an isipotee kitu chochote. Tahrif aina hii, inapatikana katika Qur'an, hili linashuhudiwa kama ifuatavyo:

A . Katika Surat Hud Aya 78 inasomwa: "HUNNA AT'HAARU LAKUM" katika silabi ya RAA kumetiwa dhamma, na katika qiraa kingine, inasomwa: "HUNNA AT'HARA" kwa nasbu.[23]

B . Katika Surat Sabai Aya 19 inasomwa: "RABBANAA BAAI'D BAYNA ASFARINA" na katika qiraa kingine, inasomwa:- "RABBANAA BAA'DA" kwa madhi.[24]

C . Katika Suratul Baqara Aya 259 inasomwa: "KAYFA NUNSHIZUHA" na katika qiraa kingine, inasomwa: "KAYFA NUNSHIRUHA" kwa silabi ya RAA badala ya ZAA.

D . Katika Suratul Waqia'h Aya 29 inasomwa:"WATWAL'H'IN MANDHUD" na katika qiraa kingine inasomwa: "WATWAL'I'N MANDHUD" kwa A'YN badala ya H'AA.

E . Katika Surat Saad Aya 23 inasomwa: "LAHU TIS'U'N WATIS'U'NA NAA'JAH" na katika qiraa kingine inasomwa: "LAHU TAS'U'N WATAS'U'NA".

2. Kupungua, au kuzidi neno moja au zaidi. Pamoja na kuwa nafsi ya Qur'an itabaki salama bila ya kupungua au kuzidi kitu. Katika zama za masahaba hali hii imetokea, ambapo Uthman bin Affan aliiunguza moto misahafu mingi. Na akatoa agizo kwa wawakilishi wake wote popote walipokuwa, waichome moto misahafu yote isipokuwa ile aliyoikusanya yeye.[25]

Kuzidi au kupungua katika Aya au sura. Pamoja na kuwepo ukamilifu wa Qur'an, na wakaafikiiana Waislamu wote kuwa: Mtume(s.a.w.w) aliisoma. Hali hii ipo, na mfano halisi ni kama ifuatavyo: "BISMILLAHIR RAHMANIR RAHIM" Waislamu wote wanakubaliana kuwa, Mtume(s.a.w.w) alikuwa akiisoma kabla ya kila sura isipokuwa Suratut Tawba. Kwa ndugu zetu Masunni imetokea hitilafu kati yao kuwa: "Bismillahi" si katika Qur'an, wengine wakasema: Ni katika Qur'an.[26]

Ama Shia Ithna Ashar, wao wanakubaliana kuwa "Bismillahi" ni sehemu ya kila sura isipokuwa Suratut Tawba.

3. Kuzidi baadhi ya Aya au sura yasiyokuwa Maneno ya Mwenyeezi Mungu. Tahrif aina hii haikubaliwi na Waislamu wote.

4. Kupungua, yaani, Msahafu huu uliopo mikononi mwa Waislamu haukukusanya Qur'an yote iliyoteremshwa na Mwenyeezi Mungu, na kwamba Qur'an nyingine imepotea, Tahrif ama hii ipo, wako wanaothibitisha hilo, na wengine wanakataa kuwa haiko.