TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TATU Juzuu 13

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TATU0%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TATU Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: Qurani tukufu

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TATU

Mwandishi: Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya
: HASANI MWALUPA
Kundi:

Matembeleo: 12877
Pakua: 2102


Maelezo zaidi:

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 17 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 12877 / Pakua: 2102
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TATU

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TATU Juzuu 13

Mwandishi:
Swahili

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TATU

IMEANDIKWA NA: SHEIKH MUHAMMAD JAWAD MUGHNIYYA

IMETAFSIRIWA NA: SHEIKH HASAN MWALUPA

IMEHARIRIWA NA: USTADH ABDALLAH MOHAMED

IMEPANGWA KATIKA KOMPYUTA NA: UKHT PILI RAJABU

UTANGULIZI WA MCHAPISHAJI

Kitabu hiki kilichoko mikononi mwako hivi sasa ni juhudi ya miaka mingi sana ya watu waliojitolea kuona kazi hii imefanikiwa bila ya kumsahau Marhum Abu Muhammad wa London.

Kama lilivyo jina la Tafsiri ndivyo ilivyo Tafsiri yenyewe ambayo mwanachuoni huyu mahiri kabisa aliyeifafanua ni mtu aliyebobea katika fani zote ambazo mfasiri (Mfafanuzi) anatakiwa awe nazo.

Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya ameonesha cheche zake katika vitabu vingi alivyoviandika katika maudhui mbali mbalimbali na hivyo kujipatia wasomaji wengi sana.

Msomi huyu, mwenye fikra huru na anayetetea kile anachokiamini, ni mtu mwenye mawazo mapana na kuyaangalia mambo kwa undani sana, kipaumbele chake ni katika maslahi ya umma huu na amejaribu sana kwenda na wakati.

Sifa kubwa pekee ya mwanachuoni huyu ni kuwa yeye hakujihusisha sana na kung'ang'ania madhehebu fulani tu, labda hii yatokana na wadhifa wake wa ukadhi aliokuwa nao katika nchi ya Lebanon ambayo ina madhehebu mengi, ambapo sula la madhehebu ni nyeti nchini humo, hata hivyo yeye aliweza kuamua matatizo ya watu kwenye ofisi yake kulingana na madhehebu yao pale walipomwendea. Hiyo ilimsaidia sana hata kuweza kutoa kitabu kitwacho Al-Fiqh a'laa madhaahabil-khamsah (Fikhi ya madhehebu matano) yaani ya Hanafi, Maaliki, Shafi, Hambali na Shia (ambacho twataraji kitatoka kwa lugha ya kiswahili hivi karibuni Inshaallah).

Jambo lililotupa msukumo wa kukifasiri kitabu hiki kwa lugha ya Kiswahili ni zile faida nyingi atakazozipata msomaji na kujua mambo mengi na ya ajabu yaliyo mapya kwake ambayo si rahisi kuyapata kwa wafasiri wengine.

Msomaji atapata faida katika fani za Sayansi, Siasa, Historia, Mashairi, visa vizuri, na Saikolojia miongoni mwa mengine; ndiyo maana msomaji atashangaa kidogo anapoisoma Tafsiri hii atakapoona mwandishi amewataja na kuwanukuu watu kama kina Mfalme Edward, wanasayansi kama kina Enstein, wasanii kama Charlie Champlin (Mchekeshaji maarufu), na wengineo, hali inayoifanya tafsiri hii kuwa ni ya kipekee kabisa.

Mtindo alioutumia mwandishi ni sahali uliokusudiwa watu wa tabaka mbalimbali, wanavyuoni na watu wa kawaida.

Nia yetu ni kukigawanya kitabu hiki bure lakini tumelazimika kukiuza kwa bei nafuu ili kurudisha gharama za uchapishaji.

Mwisho : Shukrani kubwa iwaendee bila ya kuwataja watu waliojitolea usiku na mchana, jopo la wafasiri, wahariri, wachapaji, waliotupa moyo na kutoa maoni yao na walioisimamia ili kuhakikisha kwamba kitabu kimemfikia msomaji.

MAKOSA YA CHAPA

Sikumbuki kama nimewahi kusoma kitabu kilichotoka kupigwa chapa, cha zamani au cha sasa, bila ya kukuta makosa ya chapa. Nafikiri sitasoma kitabu kisichokuwa hivyo. Nimejaribu sana kuliepuka hilo katika tungo zangu, lakini sikufanikiwa.

Nilikuwa sifikirii kama ninaweza kuona makosa haya katika maandishi ya msahafu mtukufu, kama yale yaliyo katika baadhi ya chapa; kwa mfano neno yabswutu kwa swad, badala ya yabsutu kwa sin, na katika chapa ya Tafsir Arrazi ya Misr ya mwaka 1935, Sura ya (2:146). Imeandikwa La Ya'alamuun, (hawajui) badala ya Ya'alamuun (wanajua). Mfano wa makosa haya hausameheki.

Katika Tafsir Al-Manar, chapa ya Pili, sura (5:212), imeandikwa Fawqahum ila yawmil qiyama badala ya Fawqahum yawamal qiyama. Hatuwezi kusema kosa hili ni kubwa zaidi kuliko lile.

Lakini mkosaji atatuletea udhuru kwa msemo mashuhuri huko kwetu Jabal amil 'Makosa ya chapa.'

Katika Tafsiri Majmau chapa ya Urfan, Sura (46:15), imeandikwa: Hatta idha balagha arbai' na sanah badala ya: Hattaidha balagha ashuddahu arbai ' na sanah"

Kusema hivi sio kama ninajitetea kutokana na makosa ya chapa atakayoyakuta msomaji katika kitabu hiki, ijapokuwa naomba msamaha kama litatokea hili, lakini makusudio yangu hasa ni kumwambia yule atakayefungua macho yake kwenye makosa ya matamko na kuufungia macho uzuri wa maana.

Vilevile ninamwambia yule ambaye siku moja aliniambia: "Vitabu vyako vimejaa makosa ya chapa.” Kama kwamba hakuna kitu chochote katika vitabu hivyo isipokuwa makosa ya chapa tu. Wote hao ninawaambia: Mungu awasamehe na aniongoze mimi na nyinyi.

Vyovyote iwavyo, mimi ninaomba msamaha kutokana na makosa ya kifikra na ya chapa. Anasema Amirul Muminiin(a.s) :"Watu wote ni wapungufu wenye kuchanganyikiwa, isipokuwa yule aliyehifadhiwa na Mwenyezi Mungu." Na Mwenyezi Mungu (s.w.t) ndiye mwenye jukumu la kunikubalia yale niliyoyapatia na kunisamehe niliyakosea, kwa jaha ya Mtume na kizazi chake, ziwashukie rehema na amani (Amin).

MUHAMMAD JAWAD MUGHNIYYAH

1

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TATU

Mwendelezo Wa Sura Ya Kumi na Mbili: Surat Yusuf

وَمَا أُبَرِّئُ نَفْسِي إِنَّ النَّفْسَ لَأَمَّارَةٌ بِالسُّوءِ إِلَّا مَا رَحِمَ رَبِّي إِنَّ رَبِّي غَفُورٌ رَّحِيمٌ ﴿٥٣﴾

53. Nami sijitakasi nafsi yangu; hakika nafsi ndiyo iamrishayo mno uovu, isipokuwa ile ambayo Mola wangu ameirehemu. Hakika Mola wangu ni Mwingi wa maghufira, Mwenye kurehemu.

NAFSI

Aya 53

Mwanadamu ni mnyama mwenye akili na dini. Yeye kwa unyama wake au kwa nafsi yake anapondokea sana kwenye matamanio na starehe, hajali akili wala dini. Lakini kwa dini yake na akili yake anaizuia nafsi yake na akili yake isipetuke mipaka ya sharia.

Kwa hiyo mwenye kuiachia nafsi yake ifanye vile itakavyo, basi yeye ni mnyama katika sura ya binadamu, bali ni afadhali mnyama, kwa vile binadamu ana majukumu na ataulizwa, lakini mnyama hana majukumu yoyote. Ndio maana Mwenyez Mungu akasema:

إِنْ هُمْ إِلَّا كَالْأَنْعَامِ بَلْ هُمْ أَضَلُّ سَبِيلًا ﴿٤٤﴾

“Hawakuwa wao ila ni kama wanyama, bali wao wamepotea zaidi njia” (25:44).

Ni kweli kwamba wakati mwingine mtu anaweza kuwa dhaifu mbele ya matamanio, lakini muumin mwenye akili anarudi kwenye uongofu wake na kutubia; Mwenyezi Mungu naye humsamehe, kwa sababu ni Mwingi wa Maghufira, Mwenye kurehemu.

Kauli yake Mwenyezi Mungu: “Ispokuwa ile ambayo Mola wangu ameirehemu.” Maana yake ni kuwa nafsi yoyote haiwezi kusalimika na kasoro isipokuwa ile aliyoihifadhi Mwenyezi Mungu kutokan na makosa na madhambi (isma) kama nafsi za mitume na maimamu. Muhimu ni kutong’ang’ania mkosaji na kuachana kabisa na Mola wake. Imam Ali(a.s) anasema:“Dhambi kubwa ni ile ambayo mwenyewe ameipuuza” yaani ameing’ang’ania na wala asiombe msamaha.

وَقَالَ الْمَلِكُ ائْتُونِي بِهِ أَسْتَخْلِصْهُ لِنَفْسِي فَلَمَّا كَلَّمَهُ قَالَ إِنَّكَ الْيَوْمَ لَدَيْنَا مَكِينٌ أَمِينٌ ﴿٥٤﴾

54. Akasema mfalme: Mleteni awe wangu mwenyewe. Basi alipozungumza naye alisema: Hakika wewe leo kwetu ni mwenye heshima, mwenye kuaminika.

قَالَ اجْعَلْنِي عَلَىٰ خَزَائِنِ الْأَرْضِ إِنِّي حَفِيظٌ عَلِيمٌ ﴿٥٥﴾

55. Akasema (Yusuf): Nifanye mweka hazina wa nchi, hakika mimi ni mlinzi, mjuzi.

وَكَذَٰلِكَ مَكَّنَّا لِيُوسُفَ فِي الْأَرْضِ يَتَبَوَّأُ مِنْهَا حَيْثُ يَشَاءُ نُصِيبُ بِرَحْمَتِنَا مَن نَّشَاءُ وَلَا نُضِيعُ أَجْرَ الْمُحْسِنِينَ ﴿٥٦﴾

56. Na hivyo ndivyo tulivyompa cheo Yusuf katika nchi akae humo popote apendapo. Tunamfikishia rehema zetu tumtakaye, wala hatupotezi ujira wa wafanyao mema.

وَلَأَجْرُ الْآخِرَةِ خَيْرٌ لِّلَّذِينَ آمَنُوا وَكَانُوا يَتَّقُونَ ﴿٥٧﴾

57. Na ujira wa akhera ni bora kwa wale walioamini na wakawa wanamcha (Mungu).

YUSUF NI MUHESHIMIWA MISR

Aya 54-57

MAANA

Akasema mfalme: “Mleteni awe wangu mwenyewe.” Basi alipozungumza naye alisema: “Hakika wewe leo kwetu ni mwenye heshima, mwenye kuaminika.”

Baada ya mke wa waziri na wale wanawake wengine kukiri na watu wote kujua kuwa Yusuf hana hatia, Yusuf alikubali kutoka gerezani na mfalme alipokutana naye na kumsikiza, alimpenda na akamtaka awe kiongozi katika serikali yake aweze kumsaidia kuendesha serikali, akamwambia: “Wewe ni mwenye heshima na mtu mwenye kuaminiwa kwenye kila kitu katika serikali.“

Mfalme hakuyasema haya ila baada ya kuwa na uhakika wa uwezo wake, ujuzi wake na hekima yake. Inasemekana umri wa Yusuf wakati huo ulikuwa ni miaka 30. Katika Majmaul bayan imeelezwa kuwa Yusuf alimsalimia mfalme kwa lugha ya kiarabu.

Mfalme alipomuuliza umeipata wapi lugha hii, alisema ni lugha ya ami yangu Ismail. Katika tafsir Al-manar imeelezwa kwamba mfalme aliyekuweko wakati wa Yusuf alikuwa ni katika wafalme wa kiarabu walio maarufu kwa jina la Hyksos.

Tabari anasema alikuwa akiitwa Walid bin Rayyan.

Akasema (Yusuf): “Nifanye mweka hazina wa nchi, hakika mimi ni mlinzi, mjuzi.”

Baada ya mfalme kumwachia Yusuf afanye atakavyo na achague cheo, basi alichagua cheo cha wizara ya hazina na uchumi.

Alichagua cheo baada ya kuhiyarishwa na wala hakuanza yeye, isije ikaonekana kuwa anataka cheo. Hata kama tukisema ameanza yeye, basi itakuwa sio kwa maslahi yake bali ni kwa maslahi ya umma na kulinda haki za wanyonge; hasa kwenye mwaka wa kahati na njaa.

Yusuf alijua kuwa nchi inakabiliwa na janga; ikiwa mweka hazina si mjuzi na asiyekuwa mlinzi imara, basi watu hawatapata haki yao; hasa mafukara na maskini.

Zaidi ya hayo ni kuwa wizara hiyo ni nyeti sana; ikishikwa na watu wasio na ujuzi na uamnifu, umma utaangamia tu; hata ikiwa sio wakati wa shida. Lakini ikiwa mikononi mwa wajuzi na walio na uaminifu, umma utaongoka kidunia na kiakhera.

Wengi wamenukuu kuwa Yusuf aliposhikilia hazina, na watu kuona uamnifu wake na kumpa kila mtu haki yake, waliamini utume wake; hata mfalme pia alishahadia kuwa hapana Mola isipokuwa Mwenyezi Mungu na kwamba Yusuf ni mjumbe wa Mwenyezi Mungu.

Ismail Haqqiy, anasema katik Rawhul bayan:

“Amesema Mujahid: Mfalme alisilimu kupitia kwa Yusuf, pamoja na watu wengi.” Mwenye Tafsir al-bayan, aliongezea juu ya kauli hii ya Mujahid kwa kusema: Ikiwa hisani na ukarimu wa Yusuf ni sababu ya imani, basi unaonaje yule aliyemsaidia mtume(s.a.w.w) na akamkinga na kumhami muda wa uhai wake. Ambaye ni ami yake, Abu Twalib? Kwa hiyo ukweli hasa, yeye ni katika wale ambao Mwenyezi Mungu amewahuyisha kwa imani, kama ilivyotangulia kuelezwa.”

Yametangulia maelezo ya kusilimu Abu Twalib katika Juz. 11 (9:113).

Hakika mimi ni mlinzi, mjuzi.

Nitailinda mali isipotee bure na kufanyiwa israf, na ninajua wale wanaostahiki kupewa na kila kitu nitakiweka mahali pake panapostahiki.

Imepokewa kutoka kwa Imam Jafar As-Sadiq, amesema: “Inajuzu kwa mtu kujisifu ikibidi kufanya hivyo, kwani Yusuf alisema: “Nifanye mweka haz- ina wa nchi; hakika mimi ni mlinzi, mjuzi.”

Katika baadhi ya Tafsiri imeelezwa kuwa Yusuf hakuwahi kumnyenyekea Mfalme kwa kumwambia: uishi ewe mfalme! Mimi ni mtumwa wako mnyenyekevu; kama wafanyavyo leo wale wanaojipendekeza kwa wakubwa; isipokuwa alitaka yale ambayo anaamini kuwa anayamudu; kama maandalizi ya kukabiliana na majanga na kulinda nchi kutokana na uharibifu. Laiti wale wanaojipendekeza kwa wakubwa wangelisoma Qur’an wakajua kuwa heshima haiji kwa kujipendekeza

Razi anasema: Yamepokewa masimulizi kuwa Mfalme alimwambia Yusuf: “Napenda kukushirikisha kwenye kila kitu isipokuwa katika watu wangu wa nyumbani na kula na mimi.” Yusuf akamwambia: “Siwezi kula pamoja nawe na mimi ni Yusuf bin Ya’qub bin Is-haq bin Ibrahim kipenzi cha Mungu!”

Na hivyo ndivyo tulivyompa cheo Yusuf katika nchi akae humo popote apendapo. Tunamfikishia rehema zetu tumtakaye, wala hatupotezi ujira wa wafanyao mema.

Yusuf alivumilia kutupwa kisimani, kuuzwa utumwani, kutumikia nyumba ya waziri, kutuhumiwa na kufungwa gerezani. Aliyavumilia yote hayo na mengine kwa kumtegemea Mwenyezi Mungu na kutosheka naye. Je, natija yake ilikuwa ni nini? Alitoka gerezani kishujaa akiwa ni mshindi wa vita vya uvumilivu; ni mtu huru na akawa mmoja wa viongozi wa nchi. Hivi ndivyo wanavyolipwa wavumilivu ujira wao katika dunia.

Na ujira wa akhera ni bora kwa wale walioamini na wakawa ni wenye kumcha (Mungu).

Malipo ya akhera ni Pepo ambayo “Haikatiki neema yake, haondoki mkazi wake, hazeeki anayedumu, wala kukata tamaaa anayekaa humo” kama alivyosema Imam Ali.

Sasa iko wapi neema hii na ile ambayo mfalme anazeeka kwa taabu na maumivu. Baadhi ya mapokezi yanasema kuwa mke wa mheshimiwa alimjia Yusuf siku za kahati akitafuta chakula, mumewe akiwa amekufa na yeye dunia imemwinamia, yakawa yamempata yaliyompata.

Yusuf alipomuona alimwambia imekuwaje kuwa katika hali hii, naye akasema:

Ametakataka na maovu ambaye anawafanya wafalme kuwa watumwa kwa kwa sababu ya kumwasi na anayewafanya watumwa kuwa wafalme kwa sababu ya kumtii.

وَجَاءَ إِخْوَةُ يُوسُفَ فَدَخَلُوا عَلَيْهِ فَعَرَفَهُمْ وَهُمْ لَهُ مُنكِرُونَ ﴿٥٨﴾

58. Wakaja ndugu zake Yusuf wakaingia kwake. Yeye akawajua na wao hawakumjua.

وَلَمَّا جَهَّزَهُم بِجَهَازِهِمْ قَالَ ائْتُونِي بِأَخٍ لَّكُم مِّنْ أَبِيكُمْ أَلَا تَرَوْنَ أَنِّي أُوفِي الْكَيْلَ وَأَنَا خَيْرُ الْمُنزِلِينَ ﴿٥٩﴾

59. Alipowatengenezea mahitaji yao aliwaambia: “Nileteeni ndugu yenu kwa baba. Je hamuoni kuwa mimi ninatimiza kipimo na kwamba mimi ni mbora wa wakaribishao?

فَإِن لَّمْ تَأْتُونِي بِهِ فَلَا كَيْلَ لَكُمْ عِندِي وَلَا تَقْرَبُونِ ﴿٦٠﴾

60. Msiponiletea basi hampati kipimo chochote kwangu wala msinikurubie.

قَالُوا سَنُرَاوِدُ عَنْهُ أَبَاهُ وَإِنَّا لَفَاعِلُونَ ﴿٦١﴾

61. Wakasema: “Tutamrairai baba yake, na hakika sisi tutafanya.”

وَقَالَ لِفِتْيَانِهِ اجْعَلُوا بِضَاعَتَهُمْ فِي رِحَالِهِمْ لَعَلَّهُمْ يَعْرِفُونَهَا إِذَا انقَلَبُوا إِلَىٰ أَهْلِهِمْ لَعَلَّهُمْ يَرْجِعُونَ ﴿٦٢﴾

62. Akawaambia watumishi wake: “Tieni bidhaa zao katika mizigo yao ili wazione watakaporudi kwa watu wao ili wapate kurejea.”

WAKAJA NDUGUZE YUSUF

Aya 58-62

MAANA

Wakaja ndugu zake Yusuf wakaingia kwake, Yeye akawajua na wao hawakumjua.

Kahati ilienea mpaka miji ya jirani, ikiwemo Palestina na Kanani aishipo Nabii wa Mungu, Ya’qub. Ikawa imeenea habari kwamba waziri wa Misr amejiandaa vizuri kuikabili njaa na kwamba yeye anagawanya chakula kwa uadilifu bila ya kumbagua yeyote.

Nyumbani kwa Ya’qub kukawa na shida, kama iliyoko katika majumba mengine, Hivyo akawaamrisha wanawe waende Misr kuhemera chakula.

Basi wakaondoka kuelekea Misr wakiwa ni watu kumi. Walipofika huko waliingia makao ya waziri wakamkuta Yusuf, kwa sababu alikuwa akisimamia kazi yeye mwenyewe, Yusuf akawatambua, lakini wao hawakumatambua.

Alipowatengenezea mahitaji yao

Baada ya kuwaandalia mahitaji yao yote pamoja na yale ya safari,aliwaambia: “Nileteeni ndugu yenu kwa baba.”

Wafasiri wanasema kuwa Yusuf aliwakirimu sana ndugu zake mpaka wakawa hawana wasiwasi naye; wakazungumza naye kuhusu maisha yao na ya baba yao na kwamba wao wana ndugu yao mdogo wa baba mmoja, Ndipo Yusuf akawaambia basi nileteeni huyo ndugu yenu mdogo.

Katika Aya hakuna linalofahamisha kuwa walizungumza naye, lakini kuhusu kuwakirimu kunafahamishwa na kauli:

Je hamuoni kuwa mimi ninatimiza kipimo na kwamba mimi ni mbora wa wakaribishao? Msiponiletea basi hampati kipimo chochote kwangu wala msinikurubie

Maana yako wazi, Kwa mnasaba wa Aya hii, wamekongamana mafakihi kwamba inafaa kwa muuzaji na mnunuzi kuweka sharti lolote apendalo katika biashara, maadam haliharamishi halali wala kuahalalisha haramu. Na sharti la Yusuf ni katika aina hii.

Wakasema: Tutamrairai baba yake; na hakika sisi tutafanya.

Wao walikuwa wanajua kuwa baba yao si rahisi kumtoa, ndio maana wakasema kuwa watamrairai; yaani watajitahidi na kumbembeleza baba yao; pamoja na ugumu wa jambo lenyewe.

Akawaambia watumishi wake: “Tieni bidhaa zao katika mizigo yao.

Yusuf aliwaamrisha watumishi wake warudishe vile vitu walivyonunulia chakula kwenye mizigo yao, bila ya wao kutambua.

Ili wazione watakaporudi kwa watu wao wapate kurejea tena kwa kuwa na tamaa ya ukarimu wa Yusuf. Sio mbali kuwa lengo la Yusuf ni kumtuliza baba yake ili asione uzito kumwachia ndugu yake aje kwake.

فَلَمَّا رَجَعُوا إِلَىٰ أَبِيهِمْ قَالُوا يَا أَبَانَا مُنِعَ مِنَّا الْكَيْلُ فَأَرْسِلْ مَعَنَا أَخَانَا نَكْتَلْ وَإِنَّا لَهُ لَحَافِظُونَ ﴿٦٣﴾

63. Basi waliporudi kwa baba yao, walisema: “Ewe baba yetu! Tumenyimwa chakula, basi mtume ndugu yetu pamoja nasi ili tupate kupimiwa na kwa hakika sisi tutamlinda.

قَالَ هَلْ آمَنُكُمْ عَلَيْهِ إِلَّا كَمَا أَمِنتُكُمْ عَلَىٰ أَخِيهِ مِن قَبْلُ فَاللَّـهُ خَيْرٌ حَافِظًا وَهُوَ أَرْحَمُ الرَّاحِمِينَ ﴿٦٤﴾

64. Akasema: Je nikuaminini kwa huyu kama nilivyokuaminini kwa nduguye zamani? Basi Mwenyezi Mungu ndiye mbora wa kulinda, na ndiye anayerehemu zaidi kuliko wanaorehemu.

وَلَمَّا فَتَحُوا مَتَاعَهُمْ وَجَدُوا بِضَاعَتَهُمْ رُدَّتْ إِلَيْهِمْ قَالُوا يَا أَبَانَا مَا نَبْغِي هَـٰذِهِ بِضَاعَتُنَا رُدَّتْ إِلَيْنَا وَنَمِيرُ أَهْلَنَا وَنَحْفَظُ أَخَانَا وَنَزْدَادُ كَيْلَ بَعِيرٍ ذَٰلِكَ كَيْلٌ يَسِيرٌ ﴿٦٥﴾

65. Wailpofungua mizigo yao wakakuta bidhaa zao wamerudishiwa. (Wakasema): Ewe baba yetu! Tutake nini zaidi? Hizi bidhaa zetu tumerudishiwa. Na tutaleta chakula kwa ajili ya watu wetu na tutamlinda ndugu yetu na tutapata ziada ya kipimo cha ngamia mmoja. Hicho ni kipimo kidogo.

قَالَ لَنْ أُرْسِلَهُ مَعَكُمْ حَتَّىٰ تُؤْتُونِ مَوْثِقًا مِّنَ اللَّـهِ لَتَأْتُنَّنِي بِهِ إِلَّا أَن يُحَاطَ بِكُمْ فَلَمَّا آتَوْهُ مَوْثِقَهُمْ قَالَ اللَّـهُ عَلَىٰ مَا نَقُولُ وَكِيلٌ ﴿٦٦﴾

66. Akasema: Sitampeleka nanyi mpaka mnipe ahadi kwa Mwenyezi Mungu kwamba mtamleta kwangu ila ikiwa mmezungukwa. Basi walipompa ahadi yao, alisema: Mwenyezi Mungu ndiye mtegemewa kwa tuyasemayo.

MTUME NDUGU YETU PAMOJA NASI

Aya 63-66

MAANA

Basi waliporudi kwa baba yao, walisema: Ewe baba yetu! Tumenyimwa chakula.

Wakiashiria kauli ya Yusuf Msiponiletea basi hampati kipimo chochote kwangu, Kisha wakamwambia baba yao:

Basi mtume ndugu yetu pamoja nasi ili tupate kupimiwa na kwa hakika sisi tutamlinda.

Walitoa ahadi ya kumlinda na kumhifadhi ili baba yao asiwanyime.

Je nikuaminini kwa huyu kama nilivyokuaminini kwa nduguye zamani? Mlivyomfanyia?

Kisha akaelekea kwa Mwenyezi Mungu na akasema:

Basi Mwenyezi Mungu ndiye mbora wa kulinda na ndiye anayerehemu zaidi kuliko wanaorehemu.

Mimi namtegemea Mwenyezi Mungu katika uhifadhi na ulinzi wa mwanagu sio hifadhi yenu. Na yeye Mwenyezi Mungu ndiye mwenye kuhurumia unyonge wangu na uzee wangu. Inasemekana kuwa jina la huyo mtoto wake mdogo lilikuwa ni Bin-yamin (Benjamin).

Wailpofungua mizigo yao wakakuta bidhaa zao wamerudishiwa.

Wakamkimbilia baba yao wakiwa na furaha na wakasema:

Ewe baba yetu! Tutake nini zaidi?

Yaani tutatoa sababu gani kwake kama hatukwenda na ndugu yetu na ametukirimu namna hii kama uonavyo ameturudishia mali yetu.

Hizi bidhaa zetu tumerudishiwa.

Inasemekana mali yenyewe ilikuwa ni viatu na ngozi.

Baadhi ya wafasiri wa kisasa wanasema kuwa walikuta mali yao tu, sio chakula na kwamba Yusuf alifanya hivyo ili walazimike kurudi na ndugu yao. Lakini hayo ni makosa kwa sababu yanapingana na dhahiri ya Qur’an amabayo ni: “Je hamuoni kuwa mimi ninatimiza kipimo na kwamba mimi ni mbora wa wakaribishao?”

Zaidi ya hayo kuwanyima ndugu chakula wakati wanakihitajia ni roho mbaya na ngumu sana, jambo ambalo liko mbali sana na Yusuf. Ama kauli yao “Tumenyimwa chakula” ni kunyimwa mara ya pili watakaporudi.

Na tutaleta chakula kwa ajili ya watu wetu na tutamlinda ndugu yetu na kila jambo baya.

Na tutapata ziada ya kipimo cha ngamia mmoja.

Kwa sabbu Yusuf alikuwa akimpa kila mtu kipimo cha ngamia mmoja tu, ili watu wote wapate chakula. Kwa hiyo wakienda na ndugu yao watazidisha mzigo wao.

Hicho ni kipimo kidogo.

Yaani ziada itapatikana kwa kuweko ndugu yetu; vinginevyo, hatupati. Yaqub akaona haja ya chakula imezidi na kile walichokuja nacho

kinakaribia kwisha. Hivyo akakubali kwa sababu ya haja si kwa sababu ya shinikizo la wanawe, kuongezea kumwamini waziri kutokana na sifa nzuri alizozisikia na jinsi alivyowafanyia wanawe.

Akasema: Sitampeleka nanyi mpaka mnipe ahadi kwa Mwenyezi Mungu kwamba mtamleta kwangu ila ikiwa mmezungukwa.

Aliwaruhusu kuondoka na Bin-yamin kwa sharti la kutoa ahadi madhubuti kuwa watamrudisha salama isipokuwa wakitokewa na sababu zisizoweza kuzuilika.

Basi walipompa ahadi yao alisema: Mwenyezi Mungu ndiye mtegemewa kwa tuyasemayo.

Yaani walipompa ahadi aliyoitaka, kwamba watamfidia kwa roho zao, alisema Mungu peke yake ndiye shahidi wa haya tuyasemayo. Mkitekeleza, Mungu atawalipa mema na mkihalifu atawalipa adhabu kubwa.

وَقَالَ يَا بَنِيَّ لَا تَدْخُلُوا مِن بَابٍ وَاحِدٍ وَادْخُلُوا مِنْ أَبْوَابٍ مُّتَفَرِّقَةٍ وَمَا أُغْنِي عَنكُم مِّنَ اللَّـهِ مِن شَيْءٍ إِنِ الْحُكْمُ إِلَّا لِلَّـهِ عَلَيْهِ تَوَكَّلْتُ وَعَلَيْهِ فَلْيَتَوَكَّلِ الْمُتَوَكِّلُونَ ﴿٦٧﴾

67. Akasema: “Enyi wanangu! Msiingie mlango mmoja, bali ingieni kwa milango mbalimbali. Wala mimi siwafai na chochote mbele ya Mwenyezi Mungu; hukumu haiko ila kwa Mwnyezi Mungu tu, juu yake yeye ninategemea na juu yake yeye wategemee wanaotegemea.”

وَلَمَّا دَخَلُوا مِنْ حَيْثُ أَمَرَهُمْ أَبُوهُم مَّا كَانَ يُغْنِي عَنْهُم مِّنَ اللَّـهِ مِن شَيْءٍ إِلَّا حَاجَةً فِي نَفْسِ يَعْقُوبَ قَضَاهَا وَإِنَّهُ لَذُو عِلْمٍ لِّمَا عَلَّمْنَاهُ وَلَـٰكِنَّ أَكْثَرَ النَّاسِ لَا يَعْلَمُونَ ﴿٦٨﴾

68. Walipoingia kama alivyowaamrisha baba yao, haikuwafaa kitu kwa Mwenyezi Mungu; isipokuwa ni haja tu iliyo katika nafsi ya Ya’qub aliitimiza. Na hakika yeye ana elimu kwa tulivyomfundisha, lakini watu wengi hawajui.

MSIINGIE MLANGO MMOJA

Aya 67-68

MAANA

Akasema: Enyi wanangu! Msiingie mlango mmoja, bali ingieni kwa milango mbalimbali.

Baada ya kusisitiza ahadi yao kwa baba yao, aliwaruhusu kuondoka na ndugu yao mdogo na akawapa wasia huu. Inaonekana kuwa huo mji ulikuwa na milango mingi ya kuingilia, Baadhi ya tafsiri zinasema ilikuwa milango mine.

Wametofautiana wafasiri kuhusu lengo la Ya’qub kwenye wasia huu, Hakuna maelezo ya kutegemewa, Pengine inawezekana kuwa kama wataingia pamoja nao ni genge la watu 11, watu wanaweza kuanza kujiuliza uliza.

Au pengine ni kwa lengo la kuujua mji na kuchunguza habari za Yusuf. Kwa vyovyote iwavyo, sisi hatukalifiwi kutafiti lengo la wasia huo, maadamu Aya haikulidokeza.

Katika tafsir Bahrul Muhit, imeelezwa kuwa Ya’qub aliwatuma wanawe wamplekee salaam waziri kwamba baba yetu anakuombea rehema na anakushukuru ulivyotufanyia. Yusuf aliposikia ujumbe huu alilia. Hayo hayako mbali na maudhui haya.

Wala mimi siwafai na chochote mbele ya Mwenyezi Mungu. Hukumu haiko ila kwa Mwnyezi Mungu tu.

Katika kufasiri Juz.12 (12:40) kifungu ‘Hakuna hukumu sipokuwa ya Mwenyezi Mungu’ tulibainisha kwamba hukumu yake Mwenyezi Mungu inaweza kuwa ni halali na haramu, inayoitwa hukumu ya sharia.

Vile vile inaweza kuwa ni kadha yake na kadari ambayo haiepukiki. Mfumo wa Aya unafahamisha kuwa hayo ndio makusudio yake hapa. Na maana yake ni kuwa mimi ninawapa nasaha na kuwatakia mema, lakini yote hayo hayawezi kuzuia kadari na hukumu ya Mwenyezi Mungu.

Lengo lake katika hilo ni kuwabainishia wanawe kwamba mtu asitegemee vitendo peke yake wala imani peke yake; bali afanye vitendo na kujitahidi huku akimtegemea Mwenyezi Mungu na kuitakidi kuwa yeye ndiye msaidizi wake. Ndio maana akasema:

Juu yake Yeye ninategemea na juu yake Yeye wategemee wanaotegemea.

Yaani mimi ninamwamini Mwenyezi Mungu na ninamtegemea Yeye na kila anayemwamini mwenyezi Mungu anatakikana kuwa hivyo.

Walipoingia kama alivyowaamrisha baba yao, haikuwafaa kitu kwa Mwenyezi Mungu.

Yaani watoto wa Ya’qub waliingia mjini Misr kwa kupitia milango mbalimbali, kwa kufuata amri ya mzazi wao, lakini hilo halikuwafaa kitu wala kuzuia balaa, kama alivyotangulia kusema baba yao: “Wala mimi siwafai na chochote mbele ya Mwenyezi Mungu” amabapo walituhumiwa wizi na kuchukuliwa Bin-yamin wakarudi kwa baba wakiwa hoi; kama itakavyoelezwa.

Ispokuwa ni haja tu iliyo katika nafsi ya Ya’qub aliitimiza.

Wamatofautiana wafasiri kuhusu haja ya Ya’qub iliyotimizwa na Mwenyezi Mungu. Kuna aliyesema kuwa ni kuwa watoto wa Ya’qub wasipatwe na jicho watakapoingia Misr. Mwingine akasema kuwa ni waziri asiwapate na jambo baya.

Tuanavyo sisi, kulingana na hali ilivyo, na kulingana na Aya inayoonyesha kuhangaika kwa Ya’qub juu ya Yusuf na nduguye, ni kwamba haja ya kwanza na ya mwisho ya Ya’qub, katika maisha haya, ni usalama wa Yusuf na nduguye na kuwa pamoja nao ni kitulizo cha moyo wake. Na mwenyezi Mungu alimtimizia aliyoyataka kwa uzuri.

Na hakika yeye ana elimu kwa tulivyomfundisha.

Yeye ni mtume na kila mtume anafundishwa na kupata elimu kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Na miongoni mwa mafunzo hayo kwa Ya’qub ni uvumilivu wake wa misukosuko na kumtegemea kwake Mwenyezi Mungu na kuacha kukata tamaa na rehema ya mwenyezi Mungu. Na miongoni mwa elimu yake ni kuwa mambo yote ya waja yako kwa Mwenyezi Mungu.

Lakini watu wengi hawajui kwamba hukumu ni ya Mwenyezi Mungu na kwamba mipango yote ya waja bila ya msaada wa Mwenyezi Mungu haina manufaa yoyote.