TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TATU Juzuu 13

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TATU22%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TATU Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: Qurani tukufu

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
  • Anza
  • Iliyopita
  • 17 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 14811 / Pakua: 3854
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TATU

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TATU Juzuu 13

Mwandishi:
Swahili

1

2

3

4

12

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TATU

وَقَالَ الشَّيْطَانُ لَمَّا قُضِيَ الْأَمْرُ إِنَّ اللَّـهَ وَعَدَكُمْ وَعْدَ الْحَقِّ وَوَعَدتُّكُمْ فَأَخْلَفْتُكُمْ وَمَا كَانَ لِيَ عَلَيْكُم مِّن سُلْطَانٍ إِلَّا أَن دَعَوْتُكُمْ فَاسْتَجَبْتُمْ لِي فَلَا تَلُومُونِي وَلُومُوا أَنفُسَكُم مَّا أَنَا بِمُصْرِخِكُمْ وَمَا أَنتُم بِمُصْرِخِيَّ إِنِّي كَفَرْتُ بِمَا أَشْرَكْتُمُونِ مِن قَبْلُ إِنَّ الظَّالِمِينَ لَهُمْ عَذَابٌ أَلِيمٌ ﴿٢٢﴾

22. Na shetani atasema itakapokatwa hukumu: “Hakika Mwenyezi Mungu aliwaahidi ahadi ya kweli nami nikawaahidi sikuwatimizia. Na sikuwa na mamlaka juu yenu, isipokuwa niliwaita mkaniitikia. Basi msinilaumu mimi, bali jilaumuni wenyewe, Mimi siwezi kuwa mtetezi wenu wala nyinyi hamuwezi kuwa watetezi wangu, Mimi nilikataa tangu zamani kunishirikisha, Hakika madhalimu wana adhabu chungu.

وَأُدْخِلَ الَّذِينَ آمَنُوا وَعَمِلُوا الصَّالِحَاتِ جَنَّاتٍ تَجْرِي مِن تَحْتِهَا الْأَنْهَارُ خَالِدِينَ فِيهَا بِإِذْنِ رَبِّهِمْ تَحِيَّتُهُمْ فِيهَا سَلَامٌ ﴿٢٣﴾

23. Na wale ambao wameamini na wakatenda mema wataingizwa katika Mabustani (Pepo) ambayo hupita mito chini yake.

MIADI YA MWENYEZI MUNGU

Aya 22-23

HOTUBA YA SHETANI

Tumezungumzia kwa ufafanuzi kuhusu fikra ya Iblisi na Shetani, mwan- zoni mwa Juzuu ya kwanza na katika Juz.5 (4:38) na katika Aya nyingine zinazozungumzia shetani tumezungumzia kwa ujumla.

Hapa tunarudia kwa upana zaidi; kwa sababu Aya tuliyo nayo ndiyo iliyowazi zaidi kuonyesha dalili za kuweko shetani na kwamba ni hakika yenye kuthibiti; ingawaje haikueleza vile alivyo. Tutaeleza njia zinazoambatana na Aya hii, kama ifuatavyo:

1- Mwenyezi Mungu (s.w.t) amemtaja shetani, katika Kitabu chake Kitakatifu, kwa ibara mbali mbali. Mara nyingine anasema, Mtukufu, kuwa shetani ni katika aina ya watu na majini; kama pale aliposema:

شَيَاطِينَ الْإِنسِ وَالْجِنِّ يُوحِي بَعْضُهُمْ إِلَىٰ بَعْضٍ زُخْرُفَ الْقَوْلِ غُرُورًا ﴿١١٢﴾

“Mashetani watu na majini Baadhi yao wanawapa wenzao maneno ya kupambapamba kuwahadaa.” Juz.8 (6:112).

Aya hii inaashira kwamba kila kauli ambayo dhahiri yake ni rehema na undani wake ni adhabu, basi hiyo ni kazi ya shetani, hata ikiwa imesemwa na nani.

Mara nyingine anasema Mwenyezi Mungu kuwa shetani ana askari na ana kabila; kama ilivyo katika Aya hizi:

وَجُنُودُ إِبْلِيسَ أَجْمَعُونَ ﴿٩٥﴾

“Na majeshi ya ibilisi yote” (26:95)

يَا بَنِي آدَمَ لَا يَفْتِنَنَّكُمُ الشَّيْطَانُ كَمَا أَخْرَجَ أَبَوَيْكُم مِّنَ الْجَنَّةِ يَنزِعُ عَنْهُمَا لِبَاسَهُمَا لِيُرِيَهُمَا سَوْآتِهِمَا إِنَّهُ يَرَاكُمْ هُوَ وَقَبِيلُهُ مِنْ حَيْثُ لَا تَرَوْنَهُمْ ﴿٢٧﴾

“Enyi wanaadamu! shetani asiwatie katika fitina, kama alivyowatoa wazazi wenu katika Bustani (Pepo) akiwavua nguo zao ili kuwaonyesha tupu zao. Hakika yeye na kabila lake anawaona, na nyinyi hamuwaoni, Juz.8 (7:27).

Aya hizi zinafahamisha kuwa mashetani hawana idadi kwa wingi na kwamba wao hawaonekani kwa macho wala kuguswa kwa mkono.

Mara ya tatu Mwenyezi Mungu anasema mashetani wana marafiki na wasimamizi; kama ilivyo katika Aya hizi:

وَمَن يَكُنِ الشَّيْطَانُ لَهُ قَرِينًا فَسَاءَ قَرِينًا ﴿٣٨﴾

“Na ambaye shetani amekuwa ndiye rafiki yake, basi ana rafiki mbaya, Juz,5 (4:38).

فَقَاتِلُوا أَوْلِيَاءَ الشَّيْطَانِ ﴿٧٦﴾

“Basi piganeni na marafiki wa shetani” Juz.5 (4:76)

Tamko hili peke yake linafahamisha kuwa kupigana jihadi na wapotufu ni lazima na wajib, wajapokuwa ni waislamu. Mara ya nne, Mwenyezi Mungu, ambaye imetukuka hekima yake na maneno yake, anasema:

هَلْ أُنَبِّئُكُمْ عَلَىٰ مَن تَنَزَّلُ الشَّيَاطِينُ ﴿٢٢١﴾ تَنَزَّلُ عَلَىٰ كُلِّ أَفَّاكٍ أَثِيمٍ ﴿٢٢٢﴾

“Je, niwaambie nani wanawashukia Mashetani? Wanamshukia kila mzushi mkubwa mwingi wa dhambi (26: 221-222).

Inafahamisha Aya hii kuwa Mashetani ni wale waongo wazushi.

Ama wadhifa wa shetani na askari wake, kama ulivyoelezwa, ni kupoteza na kudanganya ili kuzuia njia ya haki na kheri, kwa nguvu na kulazimisha; isipokuwa ni kwa wasiwasi, kupambapamba na kudanganya.

Kwa ajili hii, tunasema na tunaendelea kusema kwamba jambo lolote linalompambia mtu kufanya uovu na kumuhimiza shari na ufisadi kwa njia ya hadaa na shauku, basi hilo ni shetani aliyefukuzwa na ibilisi mlaanifu ni sawa iwe ni mtu, mali, jaha, kitabu, gazeti, wasiwasi, mazungumzo ya ndani ya nafsi au kitu chochote kingine kinachoonekana au kisichoonekana.

Hii ndio picha ya shetani iliyoakisi katika akili zetu, tukiwa tunafuatilia na kuzifikiria Aya za Mwenyezi Mungu katika Kitabu chake, tukiziamini pamoja na mitume wa Mwenyezi Mungu.

Mengineyo yasiyokuwa hayo, katika aina na ufafanuzi, tunaiachia elimu ya Mwenyezi Mungu; wala sisi hatukalifiwi nayo au kuulizwa nayo. La wajibu kwetu ni kutohadaika, kutojiingiza katika matamanio na kuacha kuwasikiliza wadanganyifu na wapotevu. Kikitutokea kitu katika hayo, basi tumkumbuke Mwenyezi Mungu kwa ahadi na miadi yake: “Na kama uchochezi wa shetani ukikuchochea, basi jikinge kwa Mwenyezi Mungu; hakika yeye ndiye asikiaye na ajuaye, Hakika wale wanye takua zinapowagusa pepesi za shetani huzinduka, Juz.9 (7:200-201), Rudia huko.

2- Katika nafsi ya binadamu kuna matamanio na silika, navyo ni vitenda- kazi vinavyopelekea kumuasi Mwenyezi Mungu na kuhalifu amri zake, kwa sababu vinakuja kutoka ndani sio nje na kutoka batini sio dhahiri. Kwa hiyo ikiwa ndani mwa mtu hamna nguvu kubwa na ngumu itakayomzuia kupondokea kwa ashetani na kudhibiti ukaidi wake, basi mtu bila shaka atakuwa amepigwa mwereka na matamanio.

3-Na shetani atasema itakapokatwa hukumu.

Kila kitu, isipokuwa Mwenyezi Mungu, kina mwanzo na mwisho. Inawezekana mwanzo wenyewe ukaonekana, kwa dhahiri, ni heri na mwisho ukaonekana, kiuhakika, ni shari na kinyume chake. Kwa ajili hii haifai kukihukumu kitu kwa dhahiri yake na mwanzo wake, maadamu mwisho wake uko kwenye elimu ya ghaibu.

Watu walimfurahia Qarun alipowatokea na kipambo chake na wakasema: Hakika yeye ni mwema na mtu adhimu. Ardhi ilipommeza yeye na nyumba yake, walisema ni mtu mbaya na muovu.

Dunia ni mwanzo na Akhera ni mwisho. Huko zitafunuka pazia na vifuniko; atajulikana kila mtu mwishilio wake, ambapo hakutakuwa na kombokombo wala kufungwafungwa. Hiyo ndiyo maana ya kauli yake Mwenyezi Mungu: ‘Itakapokatwa hukumu’

4-Hakika Mwenyezi Mungu aliwaahidi ahadi ya kweli nami nikaawahidi sikuwatimizia.

Ahadi ya Mwenyezi Mungu ni ufufuo, hisabu na malipo:

فَوَرَبِّكَ لَنَسْأَلَنَّهُمْ أَجْمَعِينَ ﴿٩٢﴾ عَمَّا كَانُوا يَعْمَلُونَ ﴿٩٣﴾

Kwa haki ya Mola wako! Tutawauliza wote yale waliyokuwa wakiyatenda (15:92-93).

Ama ahadi ya shetani ni kupinga ahadi ya Mwenyezi Mungu kuwa haku- na hisabu wala ufuo wala Pepo na moto. “Hakuna kingine ila maisha yetu ya dunia, wala sisi hatutafufuliwa, Jz.7 (7:29).

Haya ndiyo anayoyasema shetani kuwaambia marafiki zake hapa duniani, palipo na kupindisha pindisha mambo na kudanganya, lakini huko Akhera hakuna kitu isipokuwa haki na uadilifu; hata shetani mwenyewe ataji- tokeza wazi na uongo wake, akiri mwenyewe kwa kauli yake kuwa mwanzo alikuwa akiwafundisha watu uongo na uzushi.

5-Na sikuwa na mamlaka juu yenu, isipokuwa niliwaita mkaniitikia.

Kabisa! Shetani anakubali mwenyewe kuwa hana uwezo wala nguvu yoy- ote isipokuwa vitimbi na hadaa. Wala hawamwitikii isipokuwa wale wad- haifu wa akili, nafsi na imani. Kauli yake hiyo shetani ni ile aliyoambiwa na Mwenyezi Mungu:

إِنَّ عِبَادِي لَيْسَ لَكَ عَلَيْهِمْ سُلْطَانٌ إِلَّا مَنِ اتَّبَعَكَ مِنَ الْغَاوِينَ ﴿٤٢﴾

Hakika waja wangu wewe hutakuwa na mamlaka nao, isipokuwa wale wapotofu waliokufuata (15:42).

6-Basi msinilaumu mimi, bali jilaumuni wenyewe.

Ikiwa ni ole wake yule aliyekufurishwa na Namrudi, itakuwaje kwa yule aliyekufurishwa na Iblisi? Ikiwa watu wanajilinda na shetani itakuwaje yule anyemtaka huyo shetani amlinde.

Huu ndio mwisho wa yule anayeidharau haki na watu wema kusaidia ufisadi na wafisadi na mwenye kufuata mlio. Tumewaona wengi katika mashetani watu wakiwahadaa walio wadhaifu, wanawaghuri kwa kueneza vurugu. Hata yakiwapata yale waliyoyafanya wenyewe, mashetani wao huwaambia yale yale atakayowaambia Ibilisi wafuasi wake siku ya hisabu na malipo.

7-Mimi siwezi kuwa mtetezi wenu wala nyinyi hamuwezi kuwa watetezi wangu

Yaani shetani kesho atawaambia wafuasi wake: mimi siwatoshelezi na kitu chochte, wala nyinyi pia hamnitoshelezi. Mimi na nyinyi hatuna mawasiliano yoyote.

Mimi nilikataa tangu zamani kunishirikisha.

Ibilisi anawaambia wale wale waliotikia mwito wake: mlinitii katika yale niliyowalingalia, mkanifanya ni mshirika wa Mwenyezi Mungu katika wajibu wa twaa, na mimi ninajiepusha na shirki na yale mliyoyashirikisha; hata kama mtanifanya ni mshirika wa Mwenyezi Mungu.

Hakika madhalimu wana adhabu chungu.

Hii ni jumla nyingine inayoanza, si katika maneno ya Ibilisi, ikiwa na maana ya kutoa miadi. Inawezekana kuwa ni mwishilio wa hotuba ya Ibilisi.

Ajabu ni yaliyoelezwa na baadhi ya wafasiri kwamba Ibilisi atatoa hotuba yake hii kwa watu wa motoni kwenye mimbari atakyowekewa huko! Kama ni hivyo basi, itabidi awekewe spika kubwa, kwa sababu wasikilizaji, ambao ni jeshi lake, ni wengi kuliko idadi ya mchanga.

Na wale ambao wameamini na wakatenda mema wataingizwa katika Mabustani (Pepo) ambayo hupita mito chini yake.

Baada ya Mwenyezi Mungu kutaja wapotevu na adhabu yao, sasa anataja waongofu wenye msimamo na malipo yao; kama iilvyo kawaida ya Qur’an. Umepita mfano wake katika Juz. 11 (10:9).

أَلَمْ تَرَ كَيْفَ ضَرَبَ اللَّـهُ مَثَلًا كَلِمَةً طَيِّبَةً كَشَجَرَةٍ طَيِّبَةٍ أَصْلُهَا ثَابِتٌ وَفَرْعُهَا فِي السَّمَاءِ ﴿٢٤﴾

24. Je, hukuona jinsi Mwenyezi Mungu alivyopiga mfano wa neno zuri; kama mti mzuri, mizizi yake ni imara na matawi yake yako mbinguni.

تُؤْتِي أُكُلَهَا كُلَّ حِينٍ بِإِذْنِ رَبِّهَا وَيَضْرِبُ اللَّـهُ الْأَمْثَالَ لِلنَّاسِ لَعَلَّهُمْ يَتَذَكَّرُونَ ﴿٢٥﴾

25. Hutoa matunda yake kila wakati kwa idhini ya Mola wake. Na Mwenyezi Mungu huwapigia watu mifano ili wapate kukumbuka.

وَمَثَلُ كَلِمَةٍ خَبِيثَةٍ كَشَجَرَةٍ خَبِيثَةٍ اجْتُثَّتْ مِن فَوْقِ الْأَرْضِ مَا لَهَا مِن قَرَارٍ ﴿٢٦﴾

26. Na mfano wa neno ovu ni kama mti muovu uliong’olewa juu ya ardhi, hauna uimara.

يُثَبِّتُ اللَّـهُ الَّذِينَ آمَنُوا بِالْقَوْلِ الثَّابِتِ فِي الْحَيَاةِ الدُّنْيَا وَفِي الْآخِرَةِ وَيُضِلُّ اللَّـهُ الظَّالِمِينَ وَيَفْعَلُ اللَّـهُ مَا يَشَاءُ ﴿٢٧﴾

27. Mwenyezi Mungu huwaimarisha wale walioamini kwa kauli thabiti katika maisha ya dunia na katika Akhera, na anawapoteza madhalimu; na Mwenyezi Mungu hufanya apendavyo.

NENO JEMA NA NENO OVU

AYA 24-27

MAANA

Je, hukuona jinsi Mwenyezi Mungu alivyopiga mfano wa neno zuri, kama mti mzuri.

Imesemekana kuwa maana ya neno zuri hapa ni tamko la Tawhidi: La ilaa-ha illa llah ‘Hapana Mola isipokuwa Mwenyezi Mungu. Hapana mwenye shaka kuwa Tawhid ndio msingi wa haki na chimbuko lake.

Ni kutokana na Tawhid na ikhlasi ya Mwenyezi Mungu peke yake ndio tunaweza kulifasiri neno zuri kwa kila neno linalowanufaisha watu na kuwapatia kheri na utengeneo kwa namna moja au nyingine; ni sawa liwe ni neno la dini au sharia, elimu au falsafa na hata fasihi na fani. Mtu yeyote ambaye watu watanufaika na kauli yake au kitendo chake atakuwa, kwa upande huu, anakutana na misingi ya Uislamu na dini, kwa namana yoyote atakavyokuwa.

Kauli na neno bora zaidi ni neno la mapinduzi na kelele za hasira mbele ya mtawala jeuri na wale wanaomsaidia, miongoni mwa vibaraka na wanoji- weka nyuma. Kwa sababu wao ndio asili ya ugonjwa na chimbuko la balaa.

Amesema Imam Ali(a.s) :“Haikuwa kazi yoyote nzuri na jihadi katika njia ya Mwenyezi Mungu katika kuamrisha mema na kukataza mabaya ila ni kama upumuo katika lindi la bahari na kwamba kuamrisha mema na kukataza maovu hakukurubiwi na ajali wala hakupungukiwi na riziki na bora yake kabisa ni tamko la usawa mbele ya kiongozi jeuri.”

Kwa sababu kiongozi huyo ndio chimbuko la kila uovu; Kwa hiyo mwenye kumkabili na akampinga atakuwa ameupiga vita uovu wote.

Kuna Hadith kadha za Mtume Mtukufu(s.a.w.w) zenye maana ya kauli hii ya Imam Ali, Kila kitokacho kwa Ali Amirul-muminin ni miali ya jua la Muhammad bwana wa viumbe wote.

Hakuna kitu kinachofahamisha kuwa makusudio ya neno zuri ni neno lenye faida na manufaa kuliko kufananishwa kwake na mti mzuri ambaomizizi yake ni imara haungolewi na kimbungana matawi yake yako mbinguni uko mbali na mabalaa ya dunia na uchafu wake.

Hutoa matunda yake kila wakati kwa idhini ya Mola wake sio kuwa mara nyingine unakuwa mkarimu na mara nyingine unakuwa bakhili; kama mfanya biashara wa nipe nikupe, Huu unatoa tu wakati wote.

Na Mwenyezi Mungu huwapigia watu mifano ili wapate kukumbuka.

Hufananisha maana ya ndani kwa maana ya dhahiri ili watu wafahamu njia ya uongofu wapate kuifuata na njia ya uongofu wapate kuiepuka.

Na mfano wa neno ovu ni kama mti muovu.

Kila neno linalodhuru watu wala lisiwanufaishe; hilo ni lenye kulaaniwa; ni sawa liwe linatokana na Mwislamu au asiyekuwa Mwislamu; awe wa hali ya juu au mlalahoi. Bali kunyamazia batili kunahisabika ni katika madhambi makubwa. Kuna hadithi inayosema: “Mwenye kunyamazia haki ni shetani bubu.”

Ghandi alimwandikia Taghore “Hakika wewe ni mshairi adhimu lakini unacheza na nyumba inaungua nyimbo nzuri nzuri hazimshibishi mwenye njaa wala kumponyesha mgonjwa”

Ulion’golewa juu ya ardhi, hauna uimara.

Huu ni mfano sahii kabisa wa batili na watu wake wanojifanya wakubwa na wajinga wakidhaniwa kuwa wao ni watu wazito kumbe ni kama mti tu uliosimama bila ya mizizi, mara moja unaweza ukalala chini unapopigwa na upepo.

Mwenyezi Mungu huwaimarisha wale walioamini kwa kauli thabiti katika maisha ya dunia na katika Akhera.

Makusudio ya wale walioamini sio waliosema tumemwamini Mungu na siku ya mwisho tu, kisha wasiisimamishe haki na kuipinga batili; isipokuwa makusudio ya wale walioamini ni wale aliowakusudia Mwenyezi Mungu katika kauli yake: “Hakika waumini ni wale tu walio mwamini Mwenyezi Mungu na siku ya mwisho; kisha wasiwe na sahaka na wakapigania njia ya Mwenyezi Mungu kwa mali zao na nafsi zao” (49:15)

Lakini wakidai tu kumwamini Mwenyezi Mungu kisha wasiizuie dhulma na ufisadi kwa ushujaa, basi hao ni wenye shaka sio waumini.

Maana ya kuwaimarisha kwa kauli thabiti katika maisha ya dunia ni kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) amewapa habari katika Kitabu chake kupitia Mtume wake kuwa wao wako katika ulinzi wa Mwenyezi Mungu na kwamba Yeye ndiye mlezi wao na msimamizi wao, mwenye kuwahifadhi na kuwanusuru; kama alivyo washujaisha na kuwasifu kwa ukweli na ikhlasi na mengineyo katika fadhila. Ama kuwaimarisha katika maisha ya akhera kwa kauli thabiti ni kauli YakeMwenyezi Mungu:

يَا عِبَادِ لَا خَوْفٌ عَلَيْكُمُ الْيَوْمَ وَلَا أَنتُمْ تَحْزَنُونَ ﴿٦٨﴾

Enyi waja wangu! Hamna hofu leo wala nyinyi si wenye kuhuzunika” (43:68).

Na anawapoteza madhalimu kwa kufuru yao na utwaghuti wao.

Mara nyingi Qur’an hutumia neno dhulma kwa maana ya kufuru na shirki, lakini makusudio ya dhulma hapa ni kuidhulumu mtu nafsi yake kwa kufuru na kumdhulumu mwingine kwa uadui na uzushi; kama ambavyo makusudio ya upotevu hapa ni adhabu; sawa na kauli yake Mwenyezi Mungu:

كَذَٰلِكَ يُضِلُّ اللَّـهُ مَنْ هُوَ مُسْرِفٌ مُّرْتَابٌ ﴿٣٤﴾

Hivyo ndivyo humpoteza Mwenyezi Mungu yule aliyepita kiasi mwenye shaka (40:34).

Na Mwenyezi Mungu hufanya apendavyo katika kumpa thawabu mtiifu na kumwadhibu mfisadi, wala hakuna mwenye kuzuia matakwa yake.

Nikiwa kwenye tafsiri ya Aya hii, nimesoma makala katika gazeti la Al-Ahram la Misr la tarehe 2, February 1969, yenye kichwa cha maneno: “Je ubinadamu utashuhudia kummalizika vita vya Atomic na kuanza vita vya sumu?” Miongoni mwa yaliyomo katika makala hiyo ni: “Imejitokeza silaha mpya hatari zaidi na yenye nguvu kulio silaha za nyuklia.

Silaha hiyo ni ya sumu na kwamba athari yake ni mtu anapoigusa chembe tu, basi viungo vyake vinanywea, macho yanamtoka na kufa papo hapo. Na kwamba Amerika na Uingereza tayari ina viwanda vya kutengeneza silaha hizi na kuzihifadhi mpaka pale zitakapohitajika. Wakati mataifa yakitafuta muafaka wa kummaliza silaha za nyuklia, huku mataifa mawili haya yanatafuta silaha hatari zaidi, kama badili ya mabomu ya Atomic na Haidrojeni.”

Je, imani inaweza kuwa pamoja na nia na maazimio ya kutumia silaha hizi? Je swala za wale wanaowaunga mkono wenye nia hizo na maazimio hayo zitawafaa mbele ya Mwenyezi Mungu?

أَلَمْ تَرَ إِلَى الَّذِينَ بَدَّلُوا نِعْمَتَ اللَّـهِ كُفْرًا وَأَحَلُّوا قَوْمَهُمْ دَارَ الْبَوَارِ ﴿٢٨﴾

28. Je, hukuwaona wale waliobadilisha neema ya Mwenyezi Mungu kwa kufuru? Na wakawafikisha watu wao kwenye nyumba ya maangamivu?

جَهَنَّمَ يَصْلَوْنَهَا وَبِئْسَ الْقَرَارُ ﴿٢٩﴾

29. Nayo ni Jahannam watakayoiingia, Ni mahala pabaya pa kukaa.

وَجَعَلُوا لِلَّـهِ أَندَادًا لِّيُضِلُّوا عَن سَبِيلِهِ قُلْ تَمَتَّعُوا فَإِنَّ مَصِيرَكُمْ إِلَى النَّارِ ﴿٣٠﴾

30. Na walimfanyia Mwenyezi Mungu washirika ili wapoteze katika njia yake, Sema: Stareheni! Kwani hakika marejeo yenu ni motoni.

قُل لِّعِبَادِيَ الَّذِينَ آمَنُوا يُقِيمُوا الصَّلَاةَ وَيُنفِقُوا مِمَّا رَزَقْنَاهُمْ سِرًّا وَعَلَانِيَةً مِّن قَبْلِ أَن يَأْتِيَ يَوْمٌ لَّا بَيْعٌ فِيهِ وَلَا خِلَالٌ ﴿٣١﴾

31. Waambie waja wangu walioamini wasimamishe Swala na watoe katika tulivyowaruzuku kwa siri na kwa dhahiri, kabla ya kuwajia siku isiyokuwa na biashara wala urafiki.

WALIBADILISHA NEEMA YA MUNGU KWA KUFURU

Aya 28 -31

MAANA

Je, hukuwaona wale waliboadilisha neema ya Mwenyezi Mungu kwa kufuru? Na wakawafikisha watu wao kwenye nyumba ya maangamivu? Nayo ni Jahnnam watakayoiingia ni mahala pabaya pa kukaa.

Dhamiri ya wakawafikisha inawarudia viongozi wa kufuru na upotevu. Makusudio ya neema ya Mwenyezi Mungu ni imani na uwongofu. Maana ni kuwa, je, hustajabu ewe Muhammad au ewe msikilizaji na msomaji, hali ya viongozi wa kufuru na upotevu ambao wamehiyari upotevu kuliko uon- gofu na moto kuliko neema, wakiingia humo wao na wafuasi wao, wakawa ndio kuni zake.

Mfano wa Aya hii ni kama kauli yake Mwenyezi Mungu:

أُولَـٰئِكَ الَّذِينَ اشْتَرَوُا الضَّلَالَةَ بِالْهُدَىٰ فَمَا رَبِحَت تِّجَارَتُهُمْ وَمَا كَانُوا مُهْتَدِينَ ﴿١٦﴾

“Hao ndio walionunua upotofu kwa uongofu, lakini biashara yao haikupa- ta faida wala hawakuwa ni wenye kuongoka.” Juz.1 (2:16)

Tabariy amenukuu, katika kufasiri Aya hii, kwamba Umar bin Al-Khatab alisema: “Wale ambao wamebadilisha neema ya Mwenyezi Mungu kwa kufuru ni koo mbili ovu katika maqurayshi: Bani Mughira na Bani Umayya. Ama Bani Mughira mliwatosha siku ya Badr na Bani Umayya watajifurahisha muda mchache tu.”

Na walimfanyia Mwenyezi Mungu washirika ili wapoteze katika njia yake.

Walimfanyia Mwenyezi Mungu washirika, wakiwapenda kama kumpenda Mungu na kuwaabudu kama kumwabudu Mungu.

Ilivyo hasa ni kuwa wao walifanya hivyo kwa kukusudia kuongoka si kwa kukusudia kupoteza njia. Kwa hiyo neno kwa ‘ili’ hapa halina maana ya kuwa ndio lengo bali ni matokeo. Maana yanakuwa kwamba washirikina waliabudu masanamu kwa kukusudia kuongoka nayo na kujikurubisha kwa Mwenyezi Mungu, lakini natija ikawa ni kupotea, kuangamia na kuwa mbali na rehema ya Mwenyezi Mungu. Neno ‘ili’ hapa liko sawa na mfano wa kusema: Amekuja mwenyewe ili afe.

Sema: Stareheni! Kwani hakika marejeo yenu ni motoni.

Mwenyezi Mungu alimwamrisha mtume wake kuwahadharisha washirikina na mwisho mbaya na kuwaambia kuwa starehe za dunia ni chache hata kama zinawapendeza na Akhera ni ya mwenye takua. Lakini lugha ya haki inafaa kitu kwa wale ambao hawatingishwi na lolote zaidi ya faida na chumo?

Waambie waja wangu walioamini wasimamishe Swala ambayo mwenye kuiswali inamkumbusha Mungu na kumhadharisha na adhabu na mateso na kumkataza dhambi na makosa

Na watoe katika tulivyowaruzuku kwa siri na kwa dhahiri.

Zaka ni ndugu yake swala. Swala inamkumbusha Mungu na zaka inamkurubisha kwa Mwenyezi Mungu. Umepita mafano wake katika Juz 3 (2:74).

Kabla ya kuwajia siku isiyokuwa na biashara wala urafiki.

Biashara hapa ni fumbo la fidia. Maana ni kuwa mwenye kutoa mali yake katika njia ya Mwenyezi Mungu atanufaika nayo huko akhera na mwenye kuifanyia ubakhili atakuwa na hasara na adhabu wala haitamfaa siku hiyo ambapo hakutakuwa na fidia wala urafiki, Umepita mfano wake katika Juzuu hii tuliyo nayo (13:18).

13

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TATU

اللَّـهُ الَّذِي خَلَقَ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضَ وَأَنزَلَ مِنَ السَّمَاءِ مَاءً فَأَخْرَجَ بِهِ مِنَ الثَّمَرَاتِ رِزْقًا لَّكُمْ وَسَخَّرَ لَكُمُ الْفُلْكَ لِتَجْرِيَ فِي الْبَحْرِ بِأَمْرِهِ وَسَخَّرَ لَكُمُ الْأَنْهَارَ ﴿٣٢﴾

32. Mwenyezi Mungu ndiye ambaye ameziumba mbingu na ardhi na akateremsha maji kutoka mbinguni. Na kwayo akatoa matunda kuwa riziki kwa ajili yenu. Na akafanya yawatumikie majahazi yanayopita baharini kwa amri yake, na akaifanya mito iwatumikie.

وَسَخَّرَ لَكُمُ الشَّمْسَ وَالْقَمَرَ دَائِبَيْنِ وَسَخَّرَ لَكُمُ اللَّيْلَ وَالنَّهَارَ ﴿٣٣﴾

33. Na akalifanya liwatumikie Jua na Mwezi daima. Na akaufanya usiku na mchana uwatumikie.

وَآتَاكُم مِّن كُلِّ مَا سَأَلْتُمُوهُ وَإِن تَعُدُّوا نِعْمَتَ اللَّـهِ لَا تُحْصُوهَا إِنَّ الْإِنسَانَ لَظَلُومٌ كَفَّارٌ ﴿٣٤﴾

34. Na akawapa kila mlichomuomba, Na mkihisabu neema za Mwenyezi Mungu hamuwezi kuzidhibiti. Hakika mtu ni dhalimu mkubwa mwingi wa kukufuru.

NA AKATEREMSHA MAJI KUTOKA MBINGUNI

Aya 32 -34

MAANA

Aya zote hizi tatu umepita mfano wake kama ifuatavyo:

Kuumbwa mbingu na ardhi: Juz. 7 (6:73).

Kutermshwa maji kutoka mbinguni: Juz. 1 (2:22) na Juz. hii tuliyo nayo (13:18).

Kupita majahazi: Juz. 2 (2:164).

Kunufaika na Jua na Mwezi: Juz. hii (13:2). Usiku na mchana Juz. 11(10: 67).

Mwenyezi Mungu ameweka idadi ya neema nyingi kwa waja wake katika Juz. hii na Juz. 8 (6:143144) na nyinginezo nyingi zilizokwisha tangulia pamoja na tafsiri yake na ufafanuzi wake. Mwenyezi Mungu amerudia hapa au kuzidokeza kwa mnasaba wa kubadilisha neema kwa kufuru.

Kwa ufupi Aya hizi tatu zinamaanisha kuwa neema za Mwenyezi Mungu hazihisabiki; kama vile kuumbwa mbingu na ardhi, kuteremshwa maji kuenda majahazi faida za jua, mwezi, usiku na mchana. Vile vile kuwafadhili watu kwa waliyoomba na wasiyoomba, lakini pamoja na neema zote hizo wengi wanamkufuru na kuzikufuru neema zake huku wakiabudu yasiyowanufaisha wala kuwadhuru.

JE MTU ANA MAUMBILE YA HATIA?

Kwa mnasaba wa kauli yake Mwenyezi Mungu:Hakika mtu ni dhalimu mkubwa mwingi wa kukufuru, tunadokeza kwamba wataalamu wa saikolojia wametofautiana kuhusu binadamu, kuwa je, ana maumbile ya kufanya hatia, kwamba yeye amezaliwa kumfanyia uadui ambaye hajamfanyia uadui na kukufuru neema za aliyemfanyia wema (hana shukrani)

Mnamo mwaka 1832 watalamu 528 walikutana huko Amerika wakilijadili suala hili, Wengi wakaonelea kuwa hakuna dalili kuwa mwanadamu anaweza kuepuka kufanya makosa, lakini kundi jingine likapinga.

Sisi tunaamini kuwa binadamu hakuzaliwa kuwa ni mwenye kufanya makosa; vinginevyo angelikuwa hana taklifa yoyote na kuhisabiwa kwake na kuadhibiwa ingelikuwa ni dhulma na uonevu. Vile vile dini na sharia ingelkiuwa ni upuzi na mchezo; kama vile unyoya kwenye mavumo ya upepo. Isipokuwa anakuwa ni mwenye hatia kwa sababu nyingine za nje; kama vile njaa inayofanya awe mwizi, hadaa zinazomfanya awe na hiyana na kuwa kibaraka n.k.

Hapa ndio unapata tofauti baina ya watu katika nafsi zao, Wengine wanakuwa dhaifu mbele ya hadaa na kushindwa na matamnio; kama vile mwenye chakula lakini bado anataka ziada tena kwa hali yoyote; au mwenye mke anayemtosheleza, lakini anazini; au anayeificha haki kwa kupupia cheo au manufaa yoyote katika starehe za dunia. Hakuna mwenye shaka kwamba huyu amefanya dhambi kwa kutaka kwake sio kwa maumbile yake. Hayo ndiyo aliyoyakusudia Mwenyezi Mungu aliposema:

Hakika mtu ni dhalimu mkubwa mwingi wa kukufuru.

Ni wazi kuwa kupondokea haramu hakuifanyi kuwa ni halali, madamu iko nafasi ya kuweza kufanya subira na kushinda mapondokeo haya. Tumetangulia kueleza yanayoambatana na utafiti huu katika kufasiri Juz. 12 (11:9).

وَإِذْ قَالَ إِبْرَاهِيمُ رَبِّ اجْعَلْ هَـٰذَا الْبَلَدَ آمِنًا وَاجْنُبْنِي وَبَنِيَّ أَن نَّعْبُدَ الْأَصْنَامَ ﴿٣٥﴾

35. Na Ibrahim aliposema: Ewe Mola wangu! Ujaalie mji huu uwe wa amani na uniepushe mimi na wanangu na kuabudu masanamu.

رَبِّ إِنَّهُنَّ أَضْلَلْنَ كَثِيرًا مِّنَ النَّاسِ فَمَن تَبِعَنِي فَإِنَّهُ مِنِّي وَمَنْ عَصَانِي فَإِنَّكَ غَفُورٌ رَّحِيمٌ ﴿٣٦﴾

36. Ewe Mola wangu! Hakika hayo yamewapoteza watu wengi, Basi atakayenifuata, hakika huyo ni katika mimi na atakayeniasi basi hakika wewe ni Mwingi wa maghufira, Mwenye kurehemu.

رَّبَّنَا إِنِّي أَسْكَنتُ مِن ذُرِّيَّتِي بِوَادٍ غَيْرِ ذِي زَرْعٍ عِندَ بَيْتِكَ الْمُحَرَّمِ رَبَّنَا لِيُقِيمُوا الصَّلَاةَ فَاجْعَلْ أَفْئِدَةً مِّنَ النَّاسِ تَهْوِي إِلَيْهِمْ وَارْزُقْهُم مِّنَ الثَّمَرَاتِ لَعَلَّهُمْ يَشْكُرُونَ ﴿٣٧﴾

37. Ewe Mola wetu! Hakika mimi nimeweka baadhi ya dhuria zangu katika bonde lisilokuwa na mmea, kwenye nyumba yako takatifu, ewe Mola wetu, ili wasimamishe Swala. Basi zijaalie nyoyo za watu zielekee kwao na uwaruzuku matunda ili wapate kukushukuru.

رَبَّنَا إِنَّكَ تَعْلَمُ مَا نُخْفِي وَمَا نُعْلِنُ وَمَا يَخْفَىٰ عَلَى اللَّـهِ مِن شَيْءٍ فِي الْأَرْضِ وَلَا فِي السَّمَاءِ ﴿٣٨﴾

38. Ewe Mola wetu! Hakika wewe unajua tunayoyaficha na tunayoyafichua, na hapana kitu kinachofichikana mbele ya Mwenyezi Mungu katika ardhi wala mbingu.

الْحَمْدُ لِلَّـهِ الَّذِي وَهَبَ لِي عَلَى الْكِبَرِ إِسْمَاعِيلَ وَإِسْحَاقَ إِنَّ رَبِّي لَسَمِيعُ الدُّعَاءِ ﴿٣٩﴾

39. Sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu aliyenipa juu ya uzee wangu Ismail na Is-haq. Hakika Mola wangu ni mwenye kusikia sana dua.

رَبِّ اجْعَلْنِي مُقِيمَ الصَّلَاةِ وَمِن ذُرِّيَّتِي رَبَّنَا وَتَقَبَّلْ دُعَاءِ ﴿٤٠﴾

40. Ewe Mola wangu! Nijaalie niwe mwenye kuisimamisha Swala na katika dhuria zangu pia. Ewe Mola wetu! Na utakabalie dua yangu.

رَبَّنَا اغْفِرْ لِي وَلِوَالِدَيَّ وَلِلْمُؤْمِنِينَ يَوْمَ يَقُومُ الْحِسَابُ ﴿٤١﴾

41. Ewe Mola wetu! Nighufirie mimi na wazazi wangu wawili na waumini siku ya kusimama hisabu.

EWE MOLA WANGU UJAALIE MJI HUU UWE WA AMANI

AYA 35-41

Na Ibrahim aliposema: Ewe Mola wangu! Ujaalie mji huu uwe wa amani.

Ibrahim na Ismail ndio waliojenga Al-ka’ba Makka. Angalia Juz. 1 (2:127).

Ibrahim na Ismail walimwomba Mola wao awajalie watu wawe na amani, na akawaitikia dua yao. Walikuwa na wanaendelea kuwa maadui wanakutana bila ya kuhofiana. Katika hili Mwenyezi Mungu ameashiria kwa kusema:

أَوَلَمْ يَرَوْا أَنَّا جَعَلْنَا حَرَمًا آمِنًا وَيُتَخَطَّفُ النَّاسُ مِنْ حَوْلِهِمْ ﴿٦٧﴾

“Je hawaoni kuwa tumeifanya nchi takatifu iwe ya amani na hali watu wengine wananyakuliwa kwa majirani zao? ” (29:67)

Na uniepushe mimi na wanangu na kuabudu masanamu.

Ni muhali kabisa kwa Ibrahim kuabudu masnamu. Itakuwaje ayaabudu naye aliyavunja kwa mikono yake na akawaambia:

أُفٍّ لَّكُمْ وَلِمَا تَعْبُدُونَ مِن دُونِ اللَّـهِ أَفَلَا تَعْقِلُونَ ﴿٦٧﴾ قَالُوا حَرِّقُوهُ وَانصُرُوا آلِهَتَكُمْ إِن كُنتُمْ فَاعِلِينَ ﴿٦٨﴾

Je, mnaabudu badala ya Mwenyezi Mungu yasiyofaa chochote wala kuwadhuru, Kefle yenu! Na mnavyoviabudu badala ya Mwenyezi Mungu, Je, hamtii akili? (21:67-68).

lakini mitume wa Mwenyezi Mungu na manabii wake – pamoja na isma yao – wanaogopa maasi, Hofu hii ndiyo daraja ya juu ya utiifu. Anayejiona ni mtakatifu basi amemfungulia shetani madirisha.

MITUME NA KUITIKIWA DUA

Unaweza kuuliza : kuwa Ibrahim alimuomba Mola wake kuwa watoto wake wawe waumini, asimshirikishe Mwenyezi Mungu hata mmoja wao; na inajulikana kuwa wengi katika kizazi chake walimshirikisha Mwenyezi Mungu, wakaabudu masanamu, wakiwemo maquraish ambao wao ni katika kizazi chake?

Razi amenukuu majibu matano kutoka kwa wafasiri, lakini bado swali liko palepale linataka jawabu.

Tuonavyo sisi ni kuwa dua ni maombi na matarajio; ni sawa iwe inatoka kwa Nabii au mwinginewe. Inaweza kuwa hekima yake Mwenyezi Mungu inataka kuyakubali maombi na wakati mwingine kuyakataa. Wala hiyo haimaanishi kuwa aliyekataliwa maombi hana uzito wowote mbele ya Mungu kuweza kudhuru cheo cha utume na isma yake.

Hapana! Kwani kukataliwa maombi hakummaanishi hasira za mwenye kuombwa kwa muombaji; bali inawezekana kuwa ni mapenzi zaidi kwake na kuchunga masilahi yake. Nuhu(a.s) alimtaka Mwenyezi Mungu kumuokoa mtoto wake kutokana na kuangamia, Mola wake akamjibu kwa kusema: “Basi usiniombe usilo na ujuzi nalo” Juz.12 (11:46).

Kwa maneno mengine ni kuwa dua ya Nabii Ibrahim haina tafsiri nyingine zaidi ya hamu yake na mapenzi. Hakuna mwenye shaka kwamba manabii wana hamu na wanapendelea watu wote waamini na waongoke kwenye haki. Pamoja na hayo Mwenyezi Mungu alimwambia Bwana wa mitume aliyeadhimu:

إِنَّكَ لَا تَهْدِي مَنْ أَحْبَبْتَ وَلَـٰكِنَّ اللَّـهَ يَهْدِي مَن يَشَاءُ ﴿٥٦﴾

Hakika wewe huwezi kumwongoza umpendae, lakini Mwenyezi Mungu humuongoza amtakaye (28:56)

Lau yangehakikia kila wanayoyataka mitume basi asingelipatikana hata kafiri mmoja duniani na mitume wasingelisumbuka; hasa yule bwana wao na wa mwisho wao ambaye alisema: “Hakuudhiwa mtume kama nilivyoudhiwa mimi”

Ewe Mola wangu! Hakika hayo yamewapoteza watu wengi.

Makusudio ya hayo ni ya masanamu. Maana ni kuwa wengi katika watu wamepotea kwa sababu ya ibada ya masanamu; sawa na kusema: mali imempoteza fulani; yaani amepotea kwa sababu yake.

Basi atakayenifuata, katika kizazi changu,hakika huyo ni katika mimi kinasabu na kidini.Na atakayeniasi basi hakika wewe ni Mwingi wa maghufira, Mwenye kurehemu.

Atakayemuasi Ibrahim(a.s) basi yuko mbali naye sana hata kama ndiye aliyekaribu zaidi kiudugu kuliko watu wengine; Kwa sababu atakayemuasi atakuwa amemuasi Mwenyezi Mungu.

Lakini, pamoja na hayo, Ibrahim ni mpole mno mwenye kurudi kwa Mwenyezi Mungu; kama alivyomsifu yule aliyemchagua kuwa kipenzi na akamtakasa. Ndio maana hakuwatakia adhabu waasi katika kizazi chake, bali alimwachia Mwenyezi Mungu mambo yao kwa masamaha wake na maghufira yake.

Ilivyo ni kuwa akili haizuwii kusamehewa washirikina, kwa sababu adhabu ya washirikina ni haki ya Mwenyezi Mungu. Akitaka atwaadhibu na akitaka atawasamehe. Ama kauli yake Mwenyezi Mungu: “Hakika Mwenyezi Mungu hasamei kufanyiwa mshirika, lakini husamehe yasiyokuwa hayo” Juz.5 (4:48), ni dalili ya kiusikilizaji si dalili ya kiakili, Angalia tafsiri yetu huko, tumefafanua zaidi.

Ewe Mola wetu! Hakika mimi nimeweka baadhi ya dhuria zangu katika bonde lisilokuwa na mmea, kwenye nyumba yako takatifu, ewe Mola wetu, ili wasimamishe Swala.

Aliyasema haya Ibrahim(a.s) pale alipomwacha Ismail na mama yake Makka, pakiwa ni bonde kavu, halina chochote, si maji wala mmea; isipokuwa nyumba tu inayosimamishwa swala ndani yake na kukaririwa talbiya. Ni kwa lengo hili Ibrahim aliiweka baadhi ya famila yake mahali hapa pa kame. Lakini binadamu haishi kwa swala peke yake, bali hana budi apate mkate vile vile, ndipo Ibrahim akasema:

Basi zijaalie nyoyo za watu zielekee kwao na uwaruzuku matunda ili wapate kukushukuru.

Ikiwa kwenye nyumba ya Mwenyezi Mungu hakuna mmea wala kiwele, basi watu waelekee huko kwa ibada au biashara wakiwa na mkate na matunda, ili familia ya Ibrahim nayo ipate kula na kuweza kuswali na kushukuru.

Musa(a.s) alisema: “Mola wangu! Hakika mimi ni muhitaji wa heri utakyoiteremsha” (28:24). Imam Ali(a.s) anasema:“Wallahi hakumuomba isipokuwa mkate atakokula” Alisema mshairi aliye faqih: Fadhila ni za mkate lau si huo kamwe hata siku hakuna aabaduo.

Ewe Mola wetu! Hakika wewe unajua tunayoyaficha na tunayoyafichua, na hapana kitu kinachofichikana mbele ya Mwenyezi Mungu katika ardhi wala mbingu.

Baada ya Ibrahim kuuomba watu wafike nyumbani kwake wakiwachukulia familia yake mkate na matunda ili wapate nguvu na uchangamfu wa kuabudu, baada ya haya alisema maombi yangu haya si lolote ila ni unyenyekevu na kukiri kuwa wewe ni Muumba Mwenye kuruzuku. Ama haja yetu na masilahi yetu wewe unayajua zaidi kuliko sisi; tuwe tumekuomba au hatukuomba.

Kwa hiyo kauli ya Ibrahim ‘tunayofichua’ maana yake ni tunayoyaomba na maana ya ‘tunayoyaficha’ ni yale tusiyoyaomba.

Sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu aliyenipa juu ya uzee wangu Ismail na Is-haq. Hakika Mola wangu ni mwenye kusikia sana dua.

Shukrani hii kutoka kwa Ibrahim imechanganya maombi ya msaada wa Mwenyezi Mungu kwa wanawe, Ismaili na Is-haq. Kwa vile Ibrahim amekwishakuwa mzee na muda wake umekurubia, ndipo akawakilisha mambo ya familia yake kwa Mwenyezi Mungu; wala hakuwabainishia kitu au kuwalimbikizia mali watoto wake ili wastarehe na kuwanyima wengine.

Ewe Mola wangu! Nijaalie niwe mwenye kuisimamisha Swala na kati- ka dhuria zangu pia. Ewe Mola wetu! Na utakabalie dua yangu.

Swala ya Ibrahim sio aina ya hii swala tunayoiswali sisi; bali ni katika aina ya swala amabyo Mwenyezi Mungu ameiainisha kwa kusema:

إِنَّ الصَّلَاةَ تَنْهَىٰ عَنِ الْفَحْشَاءِ وَالْمُنكَرِ ﴿٤٥﴾

Hakika Swala huzuia mambo machafu na maovu (29:45).

Ndio hapa mafakihi wakaigawanya swala katika mafungu mawili: Swala ya kutekeleza wajibu tu, lakini mtekelezaji halipwi kitu; na Swala ya kutekeleza wajibu na mtekelezaji analipwa. Hiyo ni ile ambayo inaleta ikhlasi katika matendo na ukweli katika kuamiliana na watu.

Ewe Mola wetu! Nighufirie mimi na wazazi wangu wawili na waumini siku ya kusimama hisabu.

Tumetangulia kueleza katika Juz, 7 (6:74) tofauti baina ya Sunni na Shia kuhusu imani ya baba wa Ibrahim Al-khalil(a.s) . Miongoni mwa tuliyoyasema ni kuwa mzozo huu na mfano wake ni tasa, na kwamba linalotakikana kwa Mwislamu ni kuitakidi isma ya mitume, Ama kuamini kuwa mababa zao walikuwa waumini si itikadi ya uislamu kabisa.

Lau mtu atasema mimi ninamwamini Mungu na umoja wake, mitume na isma yao na siku ya mwisho na hisabu, lakini sithibitishi wala si kanushi imani ya mababa wa Mitume, Atakayesema hivi, tutamwambia kuwa wewe ni Mwislamu, unastahiki wanyostahiki waislamu nawe unawajibu wa kuwafanyia wanayostahiki waislamu wenzako.

8

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TATU

كَذَٰلِكَ أَرْسَلْنَاكَ فِي أُمَّةٍ قَدْ خَلَتْ مِن قَبْلِهَا أُمَمٌ لِّتَتْلُوَ عَلَيْهِمُ الَّذِي أَوْحَيْنَا إِلَيْكَ وَهُمْ يَكْفُرُونَ بِالرَّحْمَـٰنِ قُلْ هُوَ رَبِّي لَا إِلَـٰهَ إِلَّا هُوَ عَلَيْهِ تَوَكَّلْتُ وَإِلَيْهِ مَتَابِ ﴿٣٠﴾

30. Ndio kama hivi tumekutuma kwa umma ambao zimekwishapita kabla yao umma nyingine, ili uwasomee tunayokupa wahyi na wao wamemkufuru Mwingi wa rehema. Sema, Yeye ni Mola wangu hakuna Mola mwengine isipokuwa yeye. Juu yake nimetegemea na kwake Yeye ndio marejeo yangu.

وَلَوْ أَنَّ قُرْآنًا سُيِّرَتْ بِهِ الْجِبَالُ أَوْ قُطِّعَتْ بِهِ الْأَرْضُ أَوْ كُلِّمَ بِهِ الْمَوْتَىٰ بَل لِّلَّـهِ الْأَمْرُ جَمِيعًا أَفَلَمْ يَيْأَسِ الَّذِينَ آمَنُوا أَن لَّوْ يَشَاءُ اللَّـهُ لَهَدَى النَّاسَ جَمِيعًا وَلَا يَزَالُ الَّذِينَ كَفَرُوا تُصِيبُهُم بِمَا صَنَعُوا قَارِعَةٌ أَوْ تَحُلُّ قَرِيبًا مِّن دَارِهِمْ حَتَّىٰ يَأْتِيَ وَعْدُ اللَّـهِ إِنَّ اللَّـهَ لَا يُخْلِفُ الْمِيعَادَ ﴿٣١﴾

31. Na lau kwamba Qura’n ndiyo inayoendeshewa milima au kupasuliwa ardhi au kusemeshewa wafu (wasingeliamini). Bali amri zote ni za Mwenyezi Mungu. Je, hawajajua wale ambao wameamini kwamba lau Mwenyezi Mungu angelipenda bila shaka angeliwaongoa watu wote,Wala wale ambao wamekufuru hawaachi kusibiwa na balaa kwa waliyoyatenda au ikawateremkia karibu na nyumbani kwao mpaka iwafikie ahadi ya Mwenyezi Mungu, Hakika Mwenyezi Mungu havunji miadi.

TUMEKUTUMA KATIKA UMMA

Aya 30-31

MAANA

Ndio kama hivi tumekutuma kwa umma ambao zimekwishapita kabla yao umma nyingine, ili uwasomee tunayokupa wahyi na wao wamemkufuru Mwingi wa rehema.

Maneno yanelekezwa kwa Muhammad(s.a.w.w) . Mwenyezi Mungu amepeleka mitume kabla yao kwenye umma zilizopita kwa lengo hilo hilo, sasa basi kuna kioja gani? Wao si watu wa kwanza kupelekewa mtume na yeye si mtume wa kwanza kuwasomea watu wahyi wa Mwenyezi Mungu.

Sema: Yeye ni Mola wangu hakuna Mola mwengine isipokuwa yeye. Juu yake nimetegemea na kwake yeye ndio marejeo yangu.

Hii ndio imani ya Muhammad(s.a.w.w) na huu ndio mwito wake, Anamwamini Mwenyezi Mungu peke yake na anamwelekea Yeye kwenye mamabo yake wala haoni mwenye uwezo mwingine zaidi yake, Anawalingania watu kwenye imani hii, Ni mwito ambao unajifahamisha wenyewe.

FIKRA YA MATAGHUTI

Na lau kwamba Qur’an ndiyo inayoendeshewa milima au kupasuliwa ardhi au kusemeshewa wafu (wasingeliamini) Bali amri zote ni za Mwenyezi Mungu.

Umepita mafano wa Aya hii mwanzo wa Juz. 8, na tumefafanua huko kwa anuani ya ‘Aina ya watu.’ Pia utakuja mfano wake katika Juz. 15. (17:90).

Tukiunganisha tuliyoyatanguliza ni kwamba Aya hii inaleta picha ya njia wanayoifikiria mataghuti ambao maisha yao yanasimama kwa kuwany- onya wanyonge na kuwafanya watumwa wao. Si maumbile wala akili, hisia, yanayoshuhudiwa, miujiza au chochote kile kitakachoweza kubadilisha ukaidi wa mataghuti na ulafi wao. Dawa pekee ni kuwaondoa na kuondoa misingi yao ya uporaji na unyang’anyi. Pamoja na yote hayo Muhammad anawataka wamkubali yeye na Qura’n.

Lakini wapi? Ni mpaka majabali yaendeshwe na Qur’an? Au mpaka wasemeshwe wafu? Kisha ndio iweje! Watapata faida gani katika hayo? Au kumuona Mungu ana kwa ana kutaongeza faida kwenye mali zao?

Hii ndio fikra yao na hii ndiyo lugha wanayoifahamu na kuisikiliza; wala hawasikilizi lugha nyingine isiyokuwa hiyo – lugha ya uchumi na faida ya paundi na dola. Lakini haki, uadilifu, mantiki na akili ni mazungumzo ya kipumbavu, yanayosadikiwa na watoto na wajinga.

Je, baada ya hayo, mtu anaweza kuuliza kwanini mataghuti hawakumwamini Muhammad pamoja na wito wake wa uadilifu na wema?

Mwito huu unaotaka kung’oa mizizi ya dhulma na ufisadi wanauona ni kosa kubwa. Hii ndio fikra pekee wanyoifikiria wale wanaoishi kwa uny- onyaji na unyang’anyi. Alikuwa nayo fikra hii Abu Jahl na Abu Sufyan wakati wa Muhammad(s.a.w.w) , katika zama zetu wamekuwa nayo Hitler na Musolini na leo hii fikra hii iko kwenye dola za kiukandamizaji zikion- gozwa na Marekani.

Dalili wazi ya hilo ni Marekani. Leo inaushinikiza Umoja wa Mataifa, kwa nguvu zake zote, ijitie hamnazo kwa sula lolote la usawa na uadilifu, ikishindwa inajitokeza waziwazi kupiga vita kila taifa litakalotaka haki na uadilifu na kuisaida dhulma na utaghuti popote ulipo; ni sawa uje kwa njia ya Israil au Ureno au hata kwa serkali ya kibaguzi ya Rhodesia[3] na Afrika kusini au kwengineko.

Siri ya yote hayo ni kuifagilia Marekani, kama kiongozi wa ukoloni. Lakini mwisho wa ubabe huu utakuwa kama wa Hitler, Dalili zimejionyesha wazi katika Vietnam. Ama masononeko yanayosababishwa na siyasa ya ukoloni yameena mashariki na magharibi, na masononeko haya hayatapita bure bila ya kuacha athari.

Mwanzo nilikuwa nikistaajbu kutokana na baadhi ya watu jinsi wanavyowadharau watu wema wenye ikhlasi na wasiwaheshimu, tena wanawaona ni kama watu wa kawaida; hata kama wakifanya maajabu gani na wakajitolea mhanga kuithibitisha haki!

Niliendelea kushangaa hivyo mpaka nilipofikia kufasiri Aya hii tuliyo nayo nikagundua kuwa fikra hii haiko kwa mataghuti na wafisadi tu; isipokuwa watu wengi wameondoa akilini ubora na msimamo na kuupima kwa chumo na faida tu; sawa na wale waliompiga vita Muhammad na waliosimama upande wa Israil katika Umoja wa mataifa na Baraza la usalama; isipokuwa tofauti yao hawa ni kuwa waliifuata njia ya ufisadi na utaghuti, lakini waliposhindwa basi wakabakia kwenye upinzani.

Je, hawajajua wale ambao wameamini kwamba lau Mwenyezi Mungu angelipenda bila shaka angeliwaongoa watu wote.

Neno hawajajua limefasiriwa kutoka neno Yay’as, Tabari anasema: “wametofautiana wafasiri kuhusu neno ‘yay’as’ … Usawa hasa ni kubainikiwa na wamenukuu tafsiri hii wengi akiwemo Imam Ali(a.s) . Na sisi ni miongoni mwa wale wanaoamini kuwa watu wa nyumba ndio wanojua zaidi kilichomo humo nyumbani.”

Vyovyote iwavyo ni kuwa makusudio ya wale ambao wameamini ni maswahaba wa Mtume(s.a.w.w) pale walipotamaani kuwa washirikina wamuamini Mwenyezi Mungu na Mtume wake. Ndipo Mwenyezi Mungu aliyetukuka akwaambia, mpaka lini mtakuwa na tamaa ya kuamini washirikina?

Je, hajajua na kubainikiwa kuwa wao kivyovyote hawataamini hata kama wafu watazungumza nao au majabali yatembee. Achaneni nao na utaghuti wao! Lau Mwenyezi Mungu angelitaka kuwaingiza kwenye imani angelifanya, lakini hekima yake Mtukufu imepitisha kumwachia mtu na hiyari yake ili kuweza kumpa uhuru na ubinadamu wake.

Lau angelimnyang’anya uhuru huu na hiyari, basi asingelikuwa ni chochote, na wala asingelistahiki kusifiwa au kushutumiwa wala thawabu au adhabu, Angalia tafsir yetu Juz. 12 (11: 118).

Wala wale ambao wamekufuru hawaachi kusibiwa na balaa kwa waliyoyatenda au ikawateremkia karibu na nyumbani kwao mpaka iwafikie ahadi ya Mwenyezi Mungu.

Makusudio ya wale ambao wamekufuru ni wale waliomkadhibisha Muhammad(s.a.w.w) . Maana ni kuwa Yeye Mwenyezi Mungu Mtukufu hawachi duniani hawa waliokadhibisha bila ya kuwatia adabu; bali anawateremshia balaa kila baada ya muda.

Hayo ni kwa sababu ya msimamo wao kwa Muhammad(s.a.w.w) . Au anawateremshia balaa karibu yao iwatie hofu na fazaa nyoyoni mwao. Analifuatilia hilo Mwenyezi Mungu mpaka itimie ahadi yake ya ushindi kwa Mtume wake.

Hakika Mwenyezi Mungu havunji miadi.

Vipi avunje miadi naye ndie mkweli zaidi wa ahadi. Maswahaba na kila mumin ana imani kuwa Mwenyezi Mungu atatekeleza ahadi na atalinusuru jeshi lake tu.

وَلَقَدِ اسْتُهْزِئَ بِرُسُلٍ مِّن قَبْلِكَ فَأَمْلَيْتُ لِلَّذِينَ كَفَرُوا ثُمَّ أَخَذْتُهُمْ فَكَيْفَ كَانَ عِقَابِ ﴿٣٢﴾

32. Na hakika walifanyiwa stihizai Mitume waliokuwa kabla yako, lakini nikawapa muda wale ambao wamekufuru, kisha nikawashika! Basi ilikuwaje adhabu!

أَفَمَنْ هُوَ قَائِمٌ عَلَىٰ كُلِّ نَفْسٍ بِمَا كَسَبَتْ وَجَعَلُوا لِلَّـهِ شُرَكَاءَ قُلْ سَمُّوهُمْ أَمْ تُنَبِّئُونَهُ بِمَا لَا يَعْلَمُ فِي الْأَرْضِ أَم بِظَاهِرٍ مِّنَ الْقَوْلِ بَلْ زُيِّنَ لِلَّذِينَ كَفَرُوا مَكْرُهُمْ وَصُدُّوا عَنِ السَّبِيلِ وَمَن يُضْلِلِ اللَّـهُ فَمَا لَهُ مِنْ هَادٍ ﴿٣٣﴾

33. Je anayesimamia kila nafsi kwa yale iliyoyachuma na wamemfanyia Mwenyezi Mungu washirika! Sema watajeni, Au ndio mnampa habari ya yale asiyoyajua katika ardhi? Au ni maneno matupu? Bali wale ambao wamekufuru wamepambiwa vitimbi vyao na wamezuiliwa njia. Na anayepotezwa na Mwenyezi Mungu hana wa kumuongoza.

لَّهُمْ عَذَابٌ فِي الْحَيَاةِ الدُّنْيَا وَلَعَذَابُ الْآخِرَةِ أَشَقُّ وَمَا لَهُم مِّنَ اللَّـهِ مِن وَاقٍ ﴿٣٤﴾

34. Wanayo adhabu katika maisha ya dunia. Na hakika adhabu ya Akhera ina mashaka zaidi. Na wala hawana wa kuwalinda na Mwenyezi Mungu.

MITUME WALIFANYIWA STIHZAI

Aya 32-34

MAANA

Na hakika walifanyiwa stihizai Mitume waliokuwa kabla yako, lakini nikawapa muda wale ambao wamekufuru, kisha nikawashika! Basi ilikuwaje adhabu!

Mwenyezi Mungu (s.w.t) anamwambia Mtume wake, vumilia na uendele na mwito wako na achana nao wale wanokukejeli na jiweke mbali na maoni yao kwako, Walikwishafanya waliokuwa kabla yako, nikawaacha kisha nikawaadhibu adhabu isiyowezekana. Huu kwa hakika ndio mwisho wa wakadhibishaji.

Mwenyezi Mungu hakumtuma mtume ila anampa mambo mawili: Ujuzi wa dalili za kilimwengu na za kiakili juu ya kuweko Muumba na umoja wake, Na muujiza unaojitokeza mikononi mwake utakaojulisha utume wake. Jambo hilo la kwanza ni kwa ajili ya kuwakinahisha watu na Tawhidi (umoja wa Mungu) na la pili ni kwa jili ya kuwakinaisha watu kuwa yeye ni mtume wa Mwenyezi Mungu.

Wale wasioamini isipokuwa manufaa yao na chumo lao tu walikuwa wakiwakejeli Mitume na kuwafanyia maskhara pamoja na dalili zao na miujiza yao. Mwenyezi Mungu naye huwapa muda ili warudi kwenye uongofu na awaonye kwa kuwapa muda, kama alivyowaonya kwa hoja.

Je anayesimamia kila nafsi kwa yale iliyoyachuma.

Anaichunga nafsi na kuilinda na kudhibiti kila kitu, kisha kuilipa thawabu ikifanya mema na adhabu ikifanya uovu. Mwenye sifa zote hizi anafanywa kuwa wenzake ni mawe?Na wawemfanyia Mwenyezi Mungu washirika! Mwenyezi Mungu anasema:

أَفَمَن يَخْلُقُ كَمَن لَّا يَخْلُقُ أَفَلَا تَذَكَّرُونَ ﴿١٧﴾

Ati anayeumba ni kama asiyeumba? Basi hivi hamkumbuki? (16:17).

Sema watajeni.

Yaani enyi washirikina tajeni angalau sifa moja tu inayostahiki kuabudiwa masanamu yenu, Hii ni dharau na dhihaka, sawa na mwoga kusema: Mimi ni shujaa, kisha aambiwe: tutajie ushahidi mmoja wa ushujaa wako.

Au ndio mnampa habari ya yale asiyoyajua katika ardhi?

Mwenyezi Mungu anasema hana mshirika na nyinyi manasema ana washirika wengi. Maana yake ni kuwa wao wanajua zaidi na Mwenyezi Mungu hajui.

Ametakaka Mwenyezi Mungu na hayo kabisa; kama wase- mavyo watu wa mantiki: kikipatikana chenye kulazimiwa ndio umepatikana ulazima na kikikosekana chenye kulazimiwa ndio umekosekana ulazima – likipatikana jua ndio umeptikana mchana na likikosekana jua ndio umekosekana mchana na ukikosekana mchana ndio hakuna jua.

Kwa hiyo ikiwa kuna mshrika, kwa vyovyote Mwenyezi Mungu atamjua. Kwa kuwa Mwenyezi Mungu hamjui mshirika huyo basi hayupo; vinginevyo Mungu atakuwa halijui hilo, jambo ambalo haliwezekani.

Mwenyezi Mungu amehusisha kutaja ardhi pamoja nakuwa Yeye hana mshirika ardhini na mbinguni, kwa vile mazungumzo yanahusiana na masanamu yaliyoko ardhini.

Au ni maneno matupu.

Hilo ni tamko la kufahamisha maana ya kupatikana. Maneno yoyote yasiyofahamisha kitu halisi basi ni maneno matupu. Na neno washirika hapa ni majina yasiyokuwa na wenyewe:

إِنْ هِيَ إِلَّا أَسْمَاءٌ سَمَّيْتُمُوهَا أَنتُمْ وَآبَاؤُكُم مَّا أَنزَلَ اللَّـهُ بِهَا مِن سُلْطَانٍ ﴿٢٣﴾

“Hayo hayakuwa ila ni majina mliyoyaita nyinyi na baba zenu ambayo Mwenyezi Mungu hakuyateremshia dalili yoyote” (53:23).

Umepita mfano wa Aya hii katika Juz. 8 (7:710) na katika Juz, 12 (12:40).

Bali wale ambao wamekufuru wamepambiwa vitimbi vyao.

Maana ya vitimbi ni hadaa. Washirikina walihadaliwa na masanamu, wakayadhania ni washirika wa Mwenyezi Mungu katika viumbe vyake na wakajipambia wenyewe hadaa hii.

Na wamezuiliwa njia kwa kuchukulia lisilojulikana.

Yaani lile walilojipambia limewazuilia wao na haki na imani ya Mwenyezi Mungu na umoja wake.

Na anayepotezwa na Mwenyezi Mungu hana wa kumuongoza. Tazama Juz. 5 (4:88).

Wanayo adhabu katika maisha ya dunia kwa kupata hizaya na utwevu.

Na hakika adhabu ya Akhera ina mashaka zaidi, kwa sababu kila kitu duniani kusikiwa kwake ni kukubwa kuliko kuonekana kwake na kila kitu katika Akhera kuonekana kwake ni kukubwa kuliko kusikiwa kwake; kama asemavyo Imam Ali(a.s) .

Na wala hawana wa kuwalinda na Mwenyezi Mungu na adhabu yake.

9

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TATU

مَّثَلُ الْجَنَّةِ الَّتِي وُعِدَ الْمُتَّقُونَ تَجْرِي مِن تَحْتِهَا الْأَنْهَارُ أُكُلُهَا دَائِمٌ وَظِلُّهَا تِلْكَ عُقْبَى الَّذِينَ اتَّقَوا وَّعُقْبَى الْكَافِرِينَ النَّارُ ﴿٣٥﴾

35. Mfano wa Bustani (Pepo) waliyoahidiwa wenye takua inapita mito chini yake, matunda yake ni ya daima na pia kivuli chake. Hiyo ndio mwisho wa wale wenye takua. Na mwisho wa makafiri ni moto.

وَالَّذِينَ آتَيْنَاهُمُ الْكِتَابَ يَفْرَحُونَ بِمَا أُنزِلَ إِلَيْكَ وَمِنَ الْأَحْزَابِ مَن يُنكِرُ بَعْضَهُ قُلْ إِنَّمَا أُمِرْتُ أَنْ أَعْبُدَ اللَّـهَ وَلَا أُشْرِكَ بِهِ إِلَيْهِ أَدْعُو وَإِلَيْهِ مَآبِ ﴿٣٦﴾

36. Na wale ambao tumewapa Kitabu wanafurahia uliyoteremshiwa, Na katika makundi mengine wapo wanayoyakataa baadhi yake. Sema: Nimeamrishwa nimwabudu Mwenyezi Mungu wala nisimshirikishe. Ninalingania kwake Yeye, na marejeo ni kwake.

وَكَذَٰلِكَ أَنزَلْنَاهُ حُكْمًا عَرَبِيًّا وَلَئِنِ اتَّبَعْتَ أَهْوَاءَهُم بَعْدَ مَا جَاءَكَ مِنَ الْعِلْمِ مَا لَكَ مِنَ اللَّـهِ مِن وَلِيٍّ وَلَا وَاقٍ ﴿٣٧﴾

Na ndio kama hivyo tumeiteremsha Qur’an kuwa ni hukumu kwa Kiarabu. Na kama ukifuata hawaa zao baada ya kukujia ilimu hii, hutakuwa na msimamizi wala mlinzi mbele ya Mwenyezi Mungu.

وَلَقَدْ أَرْسَلْنَا رُسُلًا مِّن قَبْلِكَ وَجَعَلْنَا لَهُمْ أَزْوَاجًا وَذُرِّيَّةً وَمَا كَانَ لِرَسُولٍ أَن يَأْتِيَ بِآيَةٍ إِلَّا بِإِذْنِ اللَّـهِ لِكُلِّ أَجَلٍ كِتَابٌ ﴿٣٨﴾

38. Na hakika tulikwishawatumma mitume kabla yako na tukawajalia wawe na wake na kizazi. Na haiwi kwa Mtume kuleta muujiza isipokuwa kwa idhini ya Mwenyezi Mungu, Kila muda una kitabu.

MFANO WA BUSTANI

Aya 35-38

MAANA

Mfano wa Bustani (Pepo) waliyoahidiwa wenye takua inapita mito chini yake, matunda yake ni ya daima na pia kivuli chake.

Mwenyezi Mungu alipomaliza kutaja malipo ya makafiri, sasa anataja malipo za wenye takua, kama kawaida yake ya kutaja kitu na kinyume chake. Malipo ya wenye takua ni Bustani (Pepo) pamoja na nema yake ya kudumu – mito, matunda na vivuli.

Hiyo ndio mwisho wa wale wenye takua.

Hiyo ni ishara ya Pepo. Wenye kumcha Mungu ni wale wanoilinda haki na watu wake na kupambana na batili na watu wake. Kuna Hadith isemayo: “Hakika imani iko juu ya Uislamu na kumcha Mungu kuko juu ya Imani na yakini iko juu ya kumcha Mungu” Makusudio ya yakini ni kuwa na imani na Mwenyezi Mungu na kumtegemea Yeye.

Na mwisho wa makafiri ni moto.

Makusudio ya makafiri hapa sio tu wale wanaomkana Mwenyezi Mungu au kumshirikisha; isipokuwa makusudio ni kila anayeipinga haki, huku akiwa anajua. Zimeleza Hadith nyingi kuwa unafiki ni ukafiri n ria ni shirk. Mwenyezi Mungu amewasifu na ukafiri madhalimu, aliposema:

فَأَبَى الظَّالِمُونَ إِلَّا كُفُورًا ﴿٩٩﴾

“Lakini madhalimu hawataki ila ukafiri” (17:99);

kama ambavyo amewasifu makafiri na washirikiana kwa dhulma katika Aya kadhaa.

SHIA IMAMIYA NA SWAHABA

Wamezowea baadhi ya wanaolipwa walio wajinga kuleta fitna na ghasia baina ya Waislamu ili kuuchafua umoja wao na kuwagombanisha. Wamezoya sana hilo kwa njia ya kutia doa na kuleta uzushi kwa Shia kwa kuwazulia kuwatukana maswahaba; kumfanya Mungu Ali, kuwa Qur’an imepotolewa, jambo ambalo linaitingisha Arsh, na mengineyo miongoni mwa uwongo na uzushi.

Nimeandika makala ndefu katika kuwajibu vibaraka na wafanya propaganda hizi. Kisha nikayaweka kwenye vitabu: Ma’shia al-imamiyya, Ashia wal-hakimun, Al-ithnaashariya wa Ahlulbayt, na Ashia wat tashayyu’ ambacho ni kikubwa kuliko vyote.

Lengo langu la kwanza la makala na tungo hizi ni kuuweka wazi uhakika kwa yule anayetaka kuujua na kuubatilisha uongo na uzushi uliosemwa na unaosemwa juu ya taifa hili.

Hapa nimedokeza niliyoyaandika na kuyatunga kuhusiana na maudhui haya kwa mnasaba wa Aya hii tuliyo nayo, kama ifuatavyo:

Na wale ambao tumewapa Kitabu wanafurahia uliyotermshiwa.

Amesema Abu Hayan Al-andalusi, Zamakhshari, Sheikh Al-maraghi, Al-baydhawi na wengineo katika maulama wa kisunni kuwa makusudio ya wale ambao wamepewa Kitabu ni Myahudi na Manaswara wale waliomwamini Muhammad(s.a.w.w) .

Na akasema Tabrasiy, katika Tafsir Majmau’lbayan, ninamnukuu: “Mwenyezi Mungu (s.w.t) anawakusudia maswahaba wa mtume(s.a.w.w) ambao walimwamini na kumsadikisha, wakapewa Qur’an na kuifurahia kushuka kwake” Tabrasiy ni miongoni mwa maulama wakubwa wa kishia (alikufa mwaka 548 AH).

Kwa hiyo basi wanchuoni wengi wa kisunni wamefasiri Aya hii kuwa ni waliosilimu katika Mayahudi na manaswara; na wa kishia wamefasiri kuwa ni Mswahaba wa Mtume mtukufu(s.a.w.w) . Ikiwa wao wanawatukana maswahaba angelielekea Sheikh wao Tabrasiy, katika kufasiri Aya hii kwenye njia ya maswahaba, Hapa unatubainikia uzushi uliowekwa kwenye kundi hili.

Aban bin Taghlab ni mmoja katika wanafunzi wakubwa wa Imam Jafar As- Sadiq(a.s) , kiasi ambacho Imam alikuwa akiwaamuru Shia kuchukua dini kutoka kwake. Siku moja aliulizwa na mtu mmoja anayeitwa Abul-bilad kuhusu Shia, akamwambia: ni wale ambao wakitofautiana watu kuhusu riwaya iliyopokewa kutoka kwa Mtume(s.a.w.w) basi huchukua riwaya ya Ali aliyoipokea kutoka kwa Mtume na wanapotofautiana watu katika riwaya ya Ali huchukua kauli ya Jafar As-Sadiq aliyoipokea kutoka kwa Ali.

Kwa hiyo basi, kwa Shia, kadhia ni mategemezi ya riwaya kutoka kwa Muhammad(s.a.w.w) sio kadhia ya kutukana na kushutumu maswahaba wa Muhammad. Siri ya mategemezi yao Shia kwa Ahlu bayt (watu wa nyum- ba ya Mtume) ni Hadith kadhaa zilizothibiti, zinazohimiza hilo. Miongoni mwazo ni ile allyoipokea Muslim katika Sahihi yake kutoka kwa Mtume, kwenye mlango wa Fadhail Ali bin Abi Twalib (Ubora wa Ali bin Abi Twalib), kwamba mtume amesema:

Mimi ni mtu, mjumbe wa Mwenyezi Mungu anakurubia kunijia nimwitikie; nami ninacha kwenu vizito viwili, cha kwanza ni Kitabu cha Mwenyezi Mungu ndani yake mna uongofu na nuru, basi kichukueni Kitabu cha Mwenyezi Mungu na shikamaneni nacho.

Akahimiza kuhusu Kitabu cha Mwenyezi Mungu na kukipen- dekeza, kisha akasema: Na Ahl bayt yangu (watu wa nyumba yangu) ninawakumbusha kwa Mwenyezi Mungu kuhusu Ahl bayt wangu, Alilikariri hilo mara tatu.

Na katika makundi mengine wapo wanayoyakataa baadhi yake.

Makusudio ya makundi mengine ni watu wa mila na dini nyingine; kama vile mayahudi, manaswara na wengineo wanaoyakataa yale yanayokhalifiana na mapenzi yao na wakayakubali yanayoafikiana na mapenzi yao katika Qur’an.

Ilivyo ni kuwa kupinga kwao hawa na kukubali kwao ni sawa tu, kwa sababu kukubali ni kwa kuafikiana na hawaa zao sio kwa sababu ya Qur’an.

Sema: Nimeamrishwa nimwabudu Mwenyezi Mungu wala nisimshirikishe. Ninalingania kwake Yeye, na marejeo ni kwake.

Huu ndio Uislamu: Hakuna Mola mwingine isipokuwa Mwenyezi Mungu ni wake ufalme na mwito wa kuabudiwa ni kwake Yeye tu, na mwisho marejeo ni kwake yeye.

Na ndio kama hivyo tumeiteremsha Qur’an kuwa ni hukumu kwa Kiarabu.

Makusudio ya hukumu ni Qur’an, kwa sababu ndio hukumu ya Mwenyezi Mungu, isiyokuwa hiyo ni hukumu ya kijahili; kama alivyosema Mwenyezi Mungu:

أَفَحُكْمَ الْجَاهِلِيَّةِ يَبْغُونَ وَمَنْ أَحْسَنُ مِنَ اللَّـهِ حُكْمًا لِّقَوْمٍ يُوقِنُونَ ﴿٥٠﴾

“Je wanataka hukumu za Kijahiliya, Na ni nani aliye mwema zaidi kwa hukumu kuliko Mwenyezi Mungu, kwa watu wenye yakini” Juz, 6 (5:50)

Kama ambavyo Mwenyezi Mungu, alimtuma kila mtume kwa lugha ya watu wake, vilevile alimtuma Muhammad. Mwenyezi Mungu anasema:

وَمَا أَرْسَلْنَا مِن رَّسُولٍ إِلَّا بِلِسَانِ قَوْمِهِ لِيُبَيِّنَ لَهُمْ ﴿٤﴾

“Na hatukumtuma Mtume ila kwa ulimi wa watu wake ili apate kuwabainishia (14:4)

Tumefafanua sababu za kushuka Qur’an kwa kiarabu, pamoja na kuwa Muhammad ametumwa kwa watu wote, katika Juz. 12 (12:2).

Na kama ukifuata hawaa zao baada ya kukujia ilimu hii, hutakuwa na msimamizi wala mlinzi mbele ya Mwenyezi Mungu.

Wanaokusudiwa katika neno hawaa zao ni watu wa mila nyingine isiyokuwa Uislamu. Mwenyezi Mungu anajua kuwa Nabii hafuati wala hatafuata hawaa na matamanio yao. Lengo la ukatazo huu ni uthabiti na kuendelea kuilingania haki, wala asiogope lawama ya mwenye kulaumu. Tumeelza mara kwa mara kuwa amri ikitoka kwa mkubwa hakiangaliwi cheo cha mdogo vyovyote kilivyo

Na hakika tulikwishawatuma mitume kabla yako na tukawajalia wawe na wake na kizazi.

Asiye na haki akishindwa huanza kuzungusha maneno na kupima mambo kwa mawazo na njozi zake. Na hivyo hasa ndivyo ilivyokuwa kwa washirikina na Muhammad(s.a.w.w) . Aliwaletea hoja na dalili, wali- poshindwa kuzijibu wakanza kusema: itakuwaje ni nabii naye ana mke na watoto.

Mantiki hii inafanana kabisa na mantiki ya wanaoamini utawa. Mwenyezi Mungu amewajibu kwa kuwambia kuwa Muhammad ni kama Nuh, Ibrahim, Ismail na wengineo katika mitume ambao wana wake na watoto, sasa kuna ajabu gani katika hilo?

Kuna hadith iliyopokewa kutoka kwa mtume, amesema: Ama mimi ninafunga, ninafungua, ninalala, ninaamka, ninakula nyama na ninaoa. Mwenye kujiepusha na desturi yangu basi yeye si katika mimi.

Na haiwi kwa Mtume kuleta muujiza isipokuwa kwa idhini ya Mwenyezi Mungu.

Haya vilevile ni majibu kwa washirikina ambao walimpendekezea mtume miujiza ile waitakayo. Njia ya majibu ni kuwa Yeye Mwenyezi Mungu swt) amemsheheneza mtume wake kwa dalili zinazotosheleza kujulisha juu ya utume wake, kwa yule mwenye kuzingatia na kuitafuta haki kwa njia ya haki. Ama kuitikia mapenzi ya mwenye inadi na kiburi hakukubaliwi na akili wala desturi. Anaachiwa Mwenyezi Mungu na hekima yake.

Kila muda una kitabu.

Yaani kila kitu kina muda wake, kiwe ni muujiza, adhabu, au chochote kile, Na muda umeandikwa hautangulizwi wala kucheleweshwa nao umefichwa, haujui isipokuwa Mwenyezi Mungu

يَمْحُو اللَّـهُ مَا يَشَاءُ وَيُثْبِتُ وَعِندَهُ أُمُّ الْكِتَابِ ﴿٣٩﴾

39. Mwenyezi Mungu hufuta na huthibitisha ayatakayo na kwake kuna mama wa Kitab.

وَإِن مَّا نُرِيَنَّكَ بَعْضَ الَّذِي نَعِدُهُمْ أَوْ نَتَوَفَّيَنَّكَ فَإِنَّمَا عَلَيْكَ الْبَلَاغُ وَعَلَيْنَا الْحِسَابُ ﴿٤٠﴾

40. Na ikiwa tutakuonyesha baadhi ya tuliyowaahidi au tukakufisha, basi ni juu yako kufikisha na juu yetu ni hisabu.

أَوَلَمْ يَرَوْا أَنَّا نَأْتِي الْأَرْضَ نَنقُصُهَا مِنْ أَطْرَافِهَا وَاللَّـهُ يَحْكُمُ لَا مُعَقِّبَ لِحُكْمِهِ وَهُوَ سَرِيعُ الْحِسَابِ ﴿٤١﴾

41. Je hawakuona kwamba tunaifikia ardhi tukiipunguza janibu zake. Na Mwenyezi Mungu huhukumu, hapana wa kupinga hukumu yake; na Yeye ni mwepesi wa kuhisabu.

قَدْ مَكَرَ الَّذِينَ مِن قَبْلِهِمْ فَلِلَّـهِ الْمَكْرُ جَمِيعًا يَعْلَمُ مَا تَكْسِبُ كُلُّ نَفْسٍ وَسَيَعْلَمُ الْكُفَّارُ لِمَنْ عُقْبَى الدَّارِ ﴿٤٢﴾

42. Na wamekwisha fanya vitimbi waliokuwa kabla yao na Mwenyezi Mungu ndiye mwenye vitimbi vyote, Anajua inayoyachumma kila nafsi. Na makafiri watajua ni ya nani nyumba ya mwisho.

وَيَقُولُ الَّذِينَ كَفَرُوا لَسْتَ مُرْسَلًا قُلْ كَفَىٰ بِاللَّـهِ شَهِيدًا بَيْنِي وَبَيْنَكُمْ وَمَنْ عِندَهُ عِلْمُ الْكِتَابِ ﴿٤٣﴾

43. Na wale ambao wamekufuru wanasema wewe hukutumwa. Sema: Mwenyezi Mungu anatosha kuwa shahidi baina yangu na nyinyi na yule mwenye elimu ya Kitabu.

MWENYEZI MUNGU HUFUTA NA HUTHIBITISHA AYATAKAYO

Aya 39-43

MAANA

Mwenyezi Mungu hufuta na huthibitisha ayatakayo na kwake kuna mama wa Kitab.

Mama wa kitabu ni fumbo la ujuzi wake Mwenyezi Mungu wa yaliyokuwa na yatakayokuwa.

Lau ingekuwa inafaa kufasiri matamshi kwa muonjo na kupendeza, basi tungelifasiri kitabu ni ulimwengu na mama ni siri zake; kwa sababu Mwenyezi Mungu ana vitabu viwili: kimoja kinatamka kwa lugha ya hali nacho ni ulimwengu na kingine kinatamka kwa lugha ya maneno nacho ni Qur’an.

Ama kufuta na kuthibitisha, Tabrasi amenukuu katika maana yake kauli nane, iliyokaribu zaidi na maana ni kuwa makusudio ya kufuta ni kufuta sharia za zamani au kufuta baadhi ya hukumu zake; kama vile kufuta hukumu ya kuelekea Baytil-maqds. Ama kuthibitisha, makusudio yake ni kuthibitisha hukumu mpaka siku ya Kiyama.

Kwa hiyo maana ni kuwa Yeye Mwenyezi Mungu (s.w.t) anafuta au kuthibitisha sharia zote au baadhi, vile masilahi na hekima yake inavyotaka. Na Yeye ambaye umetukuka utufu wake anajua yaliyo na maslahi kwa waja na yaliyo na uharibifu. Kwa hiyo anawamrisha hili na kuwakataza lile, daima au kwa muda, kulingana na vile elimu yake inavyojua muda wa madhara na manufaa, Tumezungumzia kuhusu kufuta hukumu katika Juz.1 (2:106).

Na ikiwa tutakuonyesha baadhi ya tuliyowaahidi au tukakufisha, basi ni juu yako kufikisha na juu yetu ni hisabu.

Aya hii ianungana na Aya 31 ya Sura hii. Njia ya kuungana ni dhahiri: Kule amemwambia mtume wake kuwa Yeye kwa vyovyote atamteremshia adhabu yule anayemkadhibisha; hapa anasema kama tutakuonyesha adhabu yao au tutakufisha kabla ya hiyo adhabu, basi umuhimu wako wa kwanza na wa mwisho ni kufikisha tu, mengine tuachie sisi.

Je hawakuona kwamba tunaifikia ardhi tukiipunguza janibu zake.

Ardhi ni tufe, lisilokuwa na ncha, lakini ni pana linaloweza kukaliwa na mamilioni ya aina mbali mbali ya viumbe, Nayo hubadilika daima. Binadamu anaweza kuona au kusikia kuwa ardhi hii ni nzuri kukaliwa na watu itakuwa na maendeleo na ardhi ile haifai ni njangwa. Mara ile iliyoonekana inafaa inakuwa haifai na ile iliyokuwa jangwa isiyofaa inakuwa bustani yenye mito.

Watu wa ardhi pia ni hivyo hivyo, maendeleo yanakuwa hai na mengine yanakufa; ufalme unasimama na mwingine unaanguka, Hivi ndivyo ilivyo dunia ‘kigeugeu’ Hakuna ubaya wala neema inayoweza kudumu hapa ardhini.

Imam Ali (a.s) anasema:“Tahadharini na dunia ina ghururi na inahadaa, inatoa na kuzuia, inavika na kuvua. Haidumu raha yake wala tabu yake haiishi.” Kauli yake Mwenyezi Mungu: Tukiipunguza janibu zake, inaashiria maana hii na kwamba mwenye akili anapata funzo kwa mageuko haya:

أَفَلَمْ يَسِيرُوا فِي الْأَرْضِ فَيَنظُرُوا كَيْفَ كَانَ عَاقِبَةُ الَّذِينَ مِن قَبْلِهِمْ ﴿١٠٩﴾

“Je, hawatembei katika ardhi wakaona ulikuwaje mwisho wa wale waliokuwa kabla yao? (12:109).

Na Mwenyezi Mungu huhukumu, hapana wa kupinga hukumu yake.

Na amekwisha hukumu kuwaangamiza wenye makosa na amekwishaipitisha hukumu hiyo.

Na wamekwisha fanya vitimbi waliokuwa kabla yao na Mwenyezi Mungu ndiye mwenye vitimbi vyote.

Makusudio ya vitimbi vya Mwenyezi Mungu ni kupangua vitimbi, Angalia Juz.3 (3:53).

Anajua inayoyachuma kila nafsi; Kwa sababu yeye ni mwenye wasaa aliye mjuzi.

Na makafiri watajua ni ya nani nyumba ya mwisho. Siku ile watakaporudi kwa Mola wao na kusema leo ni siku nzito.

Na wale ambao wamekufuru wanasema wewe hukutumwa.

Waliukana utume wa Muhammad pamoja na dalili zote, kwa vile huo ni vita dhidi ya dhulma na utaghuti na jambo lolote linalozuia uhuru wa mtu, amani yake na wema wake

RAHA YA DHAMIRI NA MAWAZO

Sema: Mwenyezi Mungu anatosha kuwa shahidi baina yangu na nyinyi na yule mwenye elimu ya Kitabu.

Katika Aya hii Mwenyezi Mungu anamwamrisha mtume wake awaambie: ikiwa mnakanusha utume wangu, basi Mwenyezi Mungu anshuhudia kuwa mimi ni mtume kutoka kwake, vile vile wenye kuchunga haki katika maulama wa Tawrat na Injil wanashuhudia hilo.

Haya ndio maana ya dhahiri na ndio makusudio yake na ndiyo waliyoeleza wafasiri na sisi tuko pamoja nao, lakini zaidi ya hiyo tunagusia maana kubwa zaidi inayofungamana na kila mwenye kuiamini haki akaitumia na akapingwa na wenye kufanya ufisadi katika ardhi na yakampata yaliyowapata.

Muhtasari wa maana haya makubwa na matukufu ambayo yanaashiriwa na Aya ni kuwa kila ambaye dhamiri yake inalionea raha jambo na kushuhudi- wa na mawazo yaliyo salama, basi Mwenyezi Mungu, Malaika wake na wenye kuchunga haki pia wanalishuhudia kuwa ni haki, awe ni Mtume au sio Mtume.

Unaweza kuuliza : Ni wakati gani mtu anakuwa na raha ya dhamiri na kushuhudiwa na mawazo salama?

Jibu : Hakika binadamu hawezi kuwa ni katika mwenye dhamiri hai na mawazo salama ila ikiwa anaamini msimamo wa kibinadamu; kama vile uadilifu, uhuru, ukweli, uaminifu na mengineyo ambayo heri yake inawarudia wote. Pale tu, mtu atakapoamini msimamo huu na ukaoana na vitendo vyake, basi atakuwa amestarehe dhamiri, na kushudiwa na mawazo yake.

Na wakati wowote, vitendo vyake na imani yake vitakapotengana, atakuwa ameitia utumwani dhamiri yake na itamsuta yeye mwenyewe.

Watu wa dhamiri na mawazo hawatilii umuhimu isipokuwa misimamo yao mbele ya dhamiri zao na mbele ya watu wema mfano wao ambao wanashirikiana nao kwa kuonyesha mfano na msimamo wa kibinadamu.

Lakini msimamo wao unakuwa hauna thamani mbele ya asiyekuwa na dhamiri ambaye haoni isipokuwa nafsi yake na masilahi yake tu.

Mimi nina yakini kwamba watu wema zaidi ni wale wenye misimsmo ya haki ambao hawajui starehe yoyote isipokuwa ile inayotuliza dhamiri zao.

Unaweza kuuliza : kuwa watu wengi wanaona raha wanapo pata yale wanayoyataka, ingawaje wao hawamini misingi wala misimamo yoyote; je, hiyo si inamaana wema na raha ni kupata mtu atakacho na ubaya ni kukosa atakacho?

Jibu :kwanza : mazungumzo yetu tangu mwanzo ni juu ya watu wenye dhamiri, na hawa unaowasema hawana dhamiri yoyote.

Pili : watu wengi wanaojionyesha kuwa wanapinga misimamo, huwa kiundani, wanaikubali ndani ya nafsi yao; lakini uovu ulipowashinda walijaribu kuficha kwa kukana yale wanayoyaamini, huku wakijidanganya kwa kusema:

Lau kungelikuwa na msimamo wowote tungelilazimiana nao; sawa na mwenye makosa kukana makosa yake, huku anajua kuwa yeye ni mwenye hatia.

MWISHO WA SURA YA KUMI NA TATU


7

8

9