TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA NNE Juzuu 14

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA NNE0%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA NNE Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: Qurani tukufu

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA NNE

Mwandishi: Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya
: HASANI MWALUPA
Kundi:

Matembeleo: 9068
Pakua: 2232


Maelezo zaidi:

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 15 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 9068 / Pakua: 2232
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA NNE

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA NNE Juzuu 14

Mwandishi:
Swahili

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA NNE

IMEANDIKWA NA: SHEIKH MUHAMMAD JAWAD MUGHNIYYA

IMETAFSIRIWA NA: SHEIKH HASAN MWALUPA

IMEHARIRIWA NA: USTADH ABDALLAH MOHAMED

IMEPANGWA KATIKA KOMPYUTA NA: UKHT PILI RAJABU

UTANGULIZI WA MCHAPISHAJI

Kitabu hiki kilichoko mikononi mwako hivi sasa ni juhudi ya miaka mingi sana ya watu waliojitolea kuona kazi hii imefanikiwa bila ya kumsahau Marhum Abu Muhammad wa London.

Kama lilivyo jina la Tafsiri ndivyo ilivyo Tafsiri yenyewe ambayo mwanachuoni huyu mahiri kabisa aliyeifafanua ni mtu aliyebobea katika fani zote ambazo mfasiri (Mfafanuzi) anatakiwa awe nazo.

Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya ameonesha cheche zake katika vitabu vingi alivyoviandika katika maudhui mbali mbalimbali na hivyo kujipatia wasomaji wengi sana.

Msomi huyu, mwenye fikra huru na anayetetea kile anachokiamini, ni mtu mwenye mawazo mapana na kuyaangalia mambo kwa undani sana, kipaumbele chake ni katika maslahi ya umma huu na amejaribu sana kwenda na wakati.

Sifa kubwa pekee ya mwanachuoni huyu ni kuwa yeye hakujihusisha sana na kung'ang'ania madhehebu fulani tu, labda hii yatokana na wadhifa wake wa ukadhi aliokuwa nao katika nchi ya Lebanon ambayo ina madhehebu mengi, ambapo sula la madhehebu ni nyeti nchini humo, hata hivyo yeye aliweza kuamua matatizo ya watu kwenye ofisi yake kulingana na madhehebu yao pale walipomwendea. Hiyo ilimsaidia sana hata kuweza kutoa kitabu kitwacho Al-Fiqh a'laa madhaahabil-khamsah (Fikhi ya madhehebu matano) yaani ya Hanafi, Maaliki, Shafi, Hambali na Shia (ambacho twataraji kitatoka kwa lugha ya kiswahili hivi karibuni Inshaallah).

Jambo lililotupa msukumo wa kukifasiri kitabu hiki kwa lugha ya Kiswahili ni zile faida nyingi atakazozipata msomaji na kujua mambo mengi na ya ajabu yaliyo mapya kwake ambayo si rahisi kuyapata kwa wafasiri wengine.

Msomaji atapata faida katika fani za Sayansi, Siasa, Historia, Mashairi, visa vizuri, na Saikolojia miongoni mwa mengine; ndiyo maana msomaji atashangaa kidogo anapoisoma Tafsiri hii atakapoona mwandishi amewataja na kuwanukuu watu kama kina Mfalme Edward, wanasayansi kama kina Enstein, wasanii kama Charlie Champlin (Mchekeshaji maarufu), na wengineo, hali inayoifanya tafsiri hii kuwa ni ya kipekee kabisa.

Mtindo alioutumia mwandishi ni sahali uliokusudiwa watu wa tabaka mbalimbali, wanavyuoni na watu wa kawaida.

Nia yetu ni kukigawanya kitabu hiki bure lakini tumelazimika kukiuza kwa bei nafuu ili kurudisha gharama za uchapishaji.

Mwisho : Shukrani kubwa iwaendee bila ya kuwataja watu waliojitolea usiku na mchana, jopo la wafasiri, wahariri, wachapaji, waliotupa moyo na kutoa maoni yao na walioisimamia ili kuhakikisha kwamba kitabu kimemfikia msomaji.

MAKOSA YA CHAPA

Sikumbuki kama nimewahi kusoma kitabu kilichotoka kupigwa chapa, cha zamani au cha sasa, bila ya kukuta makosa ya chapa. Nafikiri sitasoma kitabu kisichokuwa hivyo. Nimejaribu sana kuliepuka hilo katika tungo zangu, lakini sikufanikiwa.

Nilikuwa sifikirii kama ninaweza kuona makosa haya katika maandishi ya msahafu mtukufu, kama yale yaliyo katika baadhi ya chapa; kwa mfano neno yabswutu kwa swad, badala ya yabsutu kwa sin, na katika chapa ya Tafsir Arrazi ya Misr ya mwaka 1935, Sura ya (2:146), Imeandikwa La Ya'alamuun, (hawajui) badala ya Ya'alamuun (wanajua). Mfano wa makosa haya hausameheki.

Katika Tafsir Al-Manar, chapa ya Pili, sura (5:212), imeandikwa Fawqahum ila yawmil qiyama badala ya Fawqahum yawamal qiyama. Hatuwezi kusema kosa hili ni kubwa zaidi kuliko lile.

Lakini mkosaji atatuletea udhuru kwa msemo mashuhuri huko kwetu Jabal amil 'Makosa ya chapa.'

Katika Tafsiri Majmau chapa ya Urfan, Sura (46:15), imeandikwa: Hatta idha balagha arbai' na sanah badala ya: Hattaidha balagha ashuddahu arbai ' na sanah"

Kusema hivi sio kama ninajitetea kutokana na makosa ya chapa atakayoyakuta msomaji katika kitabu hiki, ijapokuwa naomba msamaha kama litatokea hili, lakini makusudio yangu hasa ni kumwambia yule atakayefungua macho yake kwenye makosa ya matamko na kuufungia macho uzuri wa maana.

Vilevile ninamwambia yule ambaye siku moja aliniambia: "Vitabu vyako vimejaa makosa ya chapa.” Kama kwamba hakuna kitu chochote katika vitabu hivyo isipokuwa makosa ya chapa tu. Wote hao ninawaambia: Mungu awasamehe na aniongoze mimi na nyinyi.

Vyovyote iwavyo, mimi ninaomba msamaha kutokana na makosa ya kifikra na ya chapa. Anasema Amirul Muminiin(a.s) :"Watu wote ni wapungufu wenye kuchanganyikiwa, isipokuwa yule aliyehifadhiwa na Mwenyezi Mungu." Na Mwenyezi Mungu (s.w.t) ndiye mwenye jukumu la kunikubalia yale niliyoyapatia na kunisamehe niliyakosea, kwa jaha ya Mtume na kizazi chake, ziwashukie rehema na amani (Amin).

MUHAMMAD JAWAD MUGHNIYYAH

1

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA NNE

Surah Ya Kumi na Tano: Surat Al-Hijri. Ina Aya 99, immeshuka Makka.

بِسْمِ اللَّهِ الرَّحْمَٰنِ الرَّحِيمِ

Kwa jina la Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema, Mwenye kurehemu.

الر تِلْكَ آيَاتُ الْكِتَابِ وَقُرْآنٍ مُّبِينٍ ﴿١﴾

1. Alif Laam Raa. Hiyo ni Aya za Kitabu na Qur’an inayobainisha.

رُّبَمَا يَوَدُّ الَّذِينَ كَفَرُوا لَوْ كَانُوا مُسْلِمِينَ ﴿٢﴾

2. Huenda waliokufuru wakatamani wangekuwa Waislamu.

ذَرْهُمْ يَأْكُلُوا وَيَتَمَتَّعُوا وَيُلْهِهِمُ الْأَمَلُ فَسَوْفَ يَعْلَمُونَ ﴿٣﴾

3. Waache wale (chakula), na wastarehe na iwazuge tamaa; watakuja jua.

وَمَا أَهْلَكْنَا مِن قَرْيَةٍ إِلَّا وَلَهَا كِتَابٌ مَّعْلُومٌ ﴿٤﴾

4. Na hatukuangamiza mji wowote ule ila una muda maalum.

مَّا تَسْبِقُ مِنْ أُمَّةٍ أَجَلَهَا وَمَا يَسْتَأْخِرُونَ ﴿٥﴾

5. Hauwezi umma wowote kuitangulia ajali yake wala kuchelewa.

HIYO NI AYA ZA KITABU

Aya 1-5

MAANA

Alif laam Raa.

Umetangulia mfano wake na maelezo yake katika Juz. 1, mwanzo wa Sura ya Baqara.

Hiyo ni Aya za Kitabu na Qur’an inayobainisha.

Hiyo, ni ishara ya hiyo Sura yenyewe tunayoifasiri. Makusudio ni kueleza kuwa hiyo ni miongoni mwa Aya za Kitabu cha Mwenyezi Mungu na ni Qur’an inayopambanua baina ya haki na batili.

Huenda waliokufuru wakatamani wangekuwa Waislamu.

Neno ‘Huenda’ hapa lina maana ya maana ya wingi; yaani kila mmoja kati ya wenye makosa, kesho atafunukiwa na pazia na atatamani lau angelikuwa hapa duniani ni miongoni mwa wenye takua ambao wameisalimisha haki na wakaitumia. Angalia kifungu cha maneno ‘Hakika dini mbele ya Mwenyezi Mungu ni Uislamu’ katika Juz. 3. (3:19).

Waache wale (chakula), na wastarehe na iwazuge tamaa; watakuja jua.

Waliathirika na starehe za duniani, Mwenyezi Mungu akawahadharisha na yatakayowapata kesho miongoni mwa adhabu kali.

Na hatukuangamiza mji wowote ule ila una Kitabu maalum.

Kana kwamba muulizaji ameuliza: Kwa nini Mwenyezi Mungu haharakishi adhabu ya wale waliomuasi Yeye na mitume yake? Ndio akajibu Mwenyezi Mungu (s.w.t) kuwa kila adhabu ina muda wake na kwamba Yeye, ambaye imetukuka hekima yake, hakuangamiza umma wowote hapo nyuma ila baada ya kufikia muda wake. Mjinga ni yule anayedanganyika na muda.

Hauwezi umma wowote kuitangulia ajali yake wala kuchelewa.

Angalia kifungu cha ‘Ajali haina kinga’ Juz; 4. (3:145).

وَقَالُوا يَا أَيُّهَا الَّذِي نُزِّلَ عَلَيْهِ الذِّكْرُ إِنَّكَ لَمَجْنُونٌ ﴿٦﴾

6. Na walisema: “Ewe uliyeteremshiwa ukumbusho! Wewe ni mwendawazimu.

لَّوْ مَا تَأْتِينَا بِالْمَلَائِكَةِ إِن كُنتَ مِنَ الصَّادِقِينَ ﴿٧﴾

7. Mbona hutuletei Malaika ikiwa wewe ni miongoni mwa wasemao kweli?.

مَا نُنَزِّلُ الْمَلَائِكَةَ إِلَّا بِالْحَقِّ وَمَا كَانُوا إِذًا مُّنظَرِينَ ﴿٨﴾

8. Hatuteremshi Malaika ila kwa haki na hapo hawatapewa muda.

إِنَّا نَحْنُ نَزَّلْنَا الذِّكْرَ وَإِنَّا لَهُ لَحَافِظُونَ ﴿٩﴾

9. Hakika sisi tumeuteremsha ukumbusho huu na hakika sisi ndio tuulindao.

وَلَقَدْ أَرْسَلْنَا مِن قَبْلِكَ فِي شِيَعِ الْأَوَّلِينَ ﴿١٠﴾

10. Na hakika tulikwishawatuma Mitume kabla yako katika mataifa ya mwanzo.

وَمَا يَأْتِيهِم مِّن رَّسُولٍ إِلَّا كَانُوا بِهِ يَسْتَهْزِئُونَ ﴿١١﴾

11. Na hakuwajia Mtume ila walikuwa wakimfanyia stihzai.

كَذَٰلِكَ نَسْلُكُهُ فِي قُلُوبِ الْمُجْرِمِينَ ﴿١٢﴾

12. Hivyo ndivyo tunavyouingiza katika nyoyo za wakosefu.

لَا يُؤْمِنُونَ بِهِ وَقَدْ خَلَتْ سُنَّةُ الْأَوَّلِينَ ﴿١٣﴾

13. Hawauamini na hali umewapitia mfano wa wa kwanza.

وَلَوْ فَتَحْنَا عَلَيْهِم بَابًا مِّنَ السَّمَاءِ فَظَلُّوا فِيهِ يَعْرُجُونَ ﴿١٤﴾

14. Na lau tungeliwafungulia mlango wa mbingu wakawa wanapanda.

لَقَالُوا إِنَّمَا سُكِّرَتْ أَبْصَارُنَا بَلْ نَحْنُ قَوْمٌ مَّسْحُورُونَ ﴿١٥﴾

15. Basi wangelisema: Macho yetu yamelevywa; bali sisi ni watu waliorogwa.

وَلَقَدْ جَعَلْنَا فِي السَّمَاءِ بُرُوجًا وَزَيَّنَّاهَا لِلنَّاظِرِينَ ﴿١٦﴾

16. Hakika tumeweka katika mbingu buruji na tumezipamba kwa wenye kuangalia.

وَحَفِظْنَاهَا مِن كُلِّ شَيْطَانٍ رَّجِيمٍ ﴿١٧﴾

17. Na tukazilinda na kila shetani afukuzwaye.

إِلَّا مَنِ اسْتَرَقَ السَّمْعَ فَأَتْبَعَهُ شِهَابٌ مُّبِينٌ ﴿١٨﴾

18. Isipokuwa asikilizaye kwa kuiba, naye hufuatwa na kijinga kinachoonekana.

WEWE NI MWENDAWAZIMU

Aya 6-18

MAANA

Na walisema: Ewe uliyeteremshiwa ukumbusho! Wewe ni mwendawazimu.

Waliosema ni maquraysh wakimwambia Muhammad aliyeteremshiwa Qur’an, kwa kumdharau. Kwa vile katika mantiki yao na vipimo vyao ni kwamba yeye ni mkichaa kwa kuwa anawaambia mambo yasiyowaingia; hata kama ni rehema kwa walimwengu na muujiza ulioshinda kwa elimu yake na mafunzo yake.

Mantiki haya hayahusiki na waabudu masanamu pekee yao wala wazandiki au walahidi; isipokuwa yanamkusanya kila anyeifanya dhati yake na manufaa yake ndio kipimo cha haki na mizani ya uadilifu, hata kama atasema: Lailaha illallah Muhammadur-rasulullah (Hapana mola isipokuwa Mwenyezi Mungu na Muhammad ni Mtume wa Mwenyezi Mungu).

Kabisa! Hakuna tofauti baina ya Mwislamu huyu wa masilahi, ambaye amekubali utume wa Muhammad na mshirikina ambaye anapinga utume wa Muhammad; isipokuwa Mwislamu huyu amemwamini Muhammad kinadharia na akamakana kimatendo; na mshirikina amemkana kikauli na kimatendo. Kwa hiyo natija kwa upande wa kimatendo ni moja tu.

Mbona hutuletei Malaika ikiwa wewe ni miongoni mwa wasemao kweli?

Hii ni kauli ya washirikina kwa Mtume(s.a.w.w) . Walitoa sharti la kuamini kwao kuwa Malaika wateremshwe kutoka mbinguni na washuhudie utume wa Muhammad, ndio akawajibu kwa kusema:

Hatuteremshi Malaika ila kwa haki na hapo hawatapewa muda.

Ufupisho wa jibu ni kuwa Mwenyezi Mungu huwateremsha Malaika kwa ajili ya kufikisha ujumbe na hawateremshi kwa waongo wenye inadi, isipokuwa kwa adhabu na maangamizi; kama alivyofanya kwa umma zilizopita. Lau kama Mwenyezi Mungu angeliwajibu washirikina kwa kuwateremshia Malaika, wangeliangamia wote. Umetangulia mfano wa Aya hii kwa swali na jawabu katika Juz. 7 (6:8).

Hakika sisi tumeuteremsha ukumbusho huu na hakika sisi ndio tuulindao.

Makusudio ya ukumbusho ni Qur’an. Imesemekana kuwa dhamir katika neno kulinda inamrudia Mtume kwamba yeye ndiye alindwaye kukingwa na maadui zake, lakini hilo ni kinyume na dhahiri ya Aya. Kwa hiyo inarudia kwenye ukumbusho ambao ni Qur’an, kama tulivyofasiri.

Unaweza kuuliza kuwa : Mwenyezi Mungu anailinda na nini? Ikiwa ni kuilinda na kupotolewa, kama walivyosema wafasiri wengi, basi juzi juzi[1] tu Israil ilichapisha maelfu ya nakala za Qur’an na wakaipotosha Aya hii: Na mwenye kutaka dini isiyokuwa Uislam haitakubaliwa kwake, Juz. 3 (3:85), ambayo kwenye Qur’an ya Israil inasomeka hivi: Na mwenye kutaka dini isiyokuwa Uislam itakubaliwa kwake.

Na kama ukisema kuwa makusudio ni kuwa hakuna yeyote atakayeitia ila, itakuwa ni kinyume na hali halisi ilivyo. Sasa ni kulindwa vipi?

Razi na Tabrasi wameleta majibu mengi yasiyokinaisha. Tuonavyo sisi ni kuwa makusudio ya kulindwa Qur’an ni kuwa kila liliomo ndani yake ni haki inayothibiti kila wakati, isiyowezwa kupingwa wala kutiwa ila kwa hoja; bali kila akili na elimu zinaavyozidi kupanuka, hujitokeza dalili mpya za ukweli wa Qur’an na utukufu wake.

Maana haya ya kulindwa Qur’an tunayapata katika kauli yake Mwenyezi Mungu:

لَّا يَأْتِيهِ الْبَاطِلُ مِن بَيْنِ يَدَيْهِ وَلَا مِنْ خَلْفِهِ تَنزِيلٌ مِّنْ حَكِيمٍ حَمِيدٍ ﴿٤٢﴾

“Hautakifikia upotofu mbele yake wala nyuma yake, kimeteremshwa na Mwenye hekima, Msifiwa” (41:42).

Na hakika tulikwisha watuma Mitume kabla yako katika mataifa ya mwanzo, Na hakuwajia Mtume ila walikuwa wakimfanyia istihzai.

Maneno haya anaambiwa Muhammad, Mataifa ya mwanzo ni umma uliokwishapita. Maana ni kuwa hali ya washirikina - kukukadhibisha wewe na kukuita kuwa ni mwendawazimu - ni kama hali ya washirikina wa zamani. Hakuwajia Mtume ila walimkadhibisha. Pamoja na hivyo walikuwa na subira na kuvumilia upumbavu wao. Lengo ni kumtuliza Mtume mtukufu(s.a.w.w) . Umepita mfano wake katika Juz. 7 (6:34).

Hivyo ndivyo tunavyouingiza katika nyoyo za wakosefu hawauamini na hali umewapitia mfano wa wa kwanza.

Dhamir ya tunavyouingiza na hawauamini inarudia kwenye ukumbusho (Qur’an). Maana ni kuwa Qur’an haiingii katika nyoyo za wakosefu kiukweli na kiimani; isipokuwa inaingia kidharau na kikejeli.

Kauli yake Mwenyezi Mungu ‘hawauamini’ ni tafsiri ya ‘tunavyouingiza.’ Maana ya ‘umepita mfano wa wa kwanza ni kuwa wakadhibishaji wa sasa ni kama wakadhibishaji wa zamani. Nyoyo zao zinaingia batili badala ya imani na upotevu badala ya uongofu.

Kusema kuwa Mungu anawaingiza ni kunasibisha kitu kwa sababu yake ya mbali moja kwa moja, Yamekwishapita maelezo ya hayo mara kadhaa.

Na lau tungeliwafungulia mlango wa mbingu wakawa wanapanda, basi wangelisema: “Macho yetu yamelevywa; bali sisi ni watu waliorogwa.”

Katika Aya ilyotangulia, wapinzani walimtaka Muhammad(s.a.w.w) kuwateremshia Malaika, Mwenyezi Mungu akwajibu kwamba Malaika hushuka na adhabu ya mangamizi kwa wapinzani na wakadhibishaji.

Kisha katika Aya hii akafuatishia jibu hilo kwa kusema kuwa lau atawafungulia milango ya mbinguni, kisha wapande kwa mili yao na wawaone Malaika na maajabu mengi, wangelisema: hakika Muhammad ameturoga na ametuonyesha njozi kuwa hali halisi na halisi kuwa njozi. Umetangulia mfano wake katika Juz. 7 (6:7).

Hakika tumeweka katika mbingu buruji na tumezipamba kwa wenye kuangalia.

Baadhi ya wafasiri wamesema kuwa makusudio ya buruji ni nyota. Wengine wakasema ni vituo vya sayari ya Jua na Mwezi.

Vyovyote iwavyo, lengo la Aya sio kutufundisha elimu ya falaki ili tujue hiyo buruji hasa ni nini; isipokuwa lengo la kwanza kabisa ni kuzingatia na kutilia manani (tadabbur) uwezo wa Mwenyezi Mungu na hekima yake katika kuumba mbingu na ardhi na kwamba undani, nidhamu na uzuri aliouumba ni dalili wazi ya kuweko Mwenyezi Mungu na umoja wake, kuliko kuteremsha Malaika na kuliko miujiza yote wanayoitaka

Na tukazilinda na kila shetani afukuzwaye; isipokuwa asikilizaye kwa kuiba, naye hufuatwa na kijinga kinachoonekana.

Watu wa wakati wa jahilia walikuwa wakiamini kuwa kila kuhani ana shetani wake apandae mbinguni na kusikiliza mazungumzo ya Malaika kuhusu watu wa ardhini, kisha anashuka ardhini kwa kuhani wake kumpa habari. Aya mbili hizi zinapinga na kukana ngano hizi na kwamba mashetani hawawezi kabisa kupanda mbinguni. Na kusema kwake kijinga kinachoonekana ni fumbo la kuwa shetani hawezi kabisa hata kukurubia kuwasikilza Malaika; kama walivodai watu wa zama za jahiliya.

وَالْأَرْضَ مَدَدْنَاهَا وَأَلْقَيْنَا فِيهَا رَوَاسِيَ وَأَنبَتْنَا فِيهَا مِن كُلِّ شَيْءٍ مَّوْزُونٍ ﴿١٩﴾

19. Na ardhi tumeitandaza na tumeweka humo milima na tumeotesha kila kitu kwa wizani.

وَجَعَلْنَا لَكُمْ فِيهَا مَعَايِشَ وَمَن لَّسْتُمْ لَهُ بِرَازِقِينَ ﴿٢٠﴾

20. Na tumejaalia humo maisha, Na ya ambao nyinyi sio wenye kuwaruzuku.

وَإِن مِّن شَيْءٍ إِلَّا عِندَنَا خَزَائِنُهُ وَمَا نُنَزِّلُهُ إِلَّا بِقَدَرٍ مَّعْلُومٍ ﴿٢١﴾

21. Na hakuna chochote ila hazina yake iko kwetu na wala hatukiteremshi isipokuwa kwa kipimo maalum.

وَأَرْسَلْنَا الرِّيَاحَ لَوَاقِحَ فَأَنزَلْنَا مِنَ السَّمَاءِ مَاءً فَأَسْقَيْنَاكُمُوهُ وَمَا أَنتُمْ لَهُ بِخَازِنِينَ ﴿٢٢﴾

22. Na tukazipeleka pepo za kupandishia na tukateremsha kutoka mbinguni maji tukawanywesha hayo wala nyinyi sio mnaoyaweka akiba.

وَإِنَّا لَنَحْنُ نُحْيِي وَنُمِيتُ وَنَحْنُ الْوَارِثُونَ ﴿٢٣﴾

Na hakika sisi ndio tunaohuyisha na tunaofisha, Na sisi ndio warithi.

وَلَقَدْ عَلِمْنَا الْمُسْتَقْدِمِينَ مِنكُمْ وَلَقَدْ عَلِمْنَا الْمُسْتَأْخِرِينَ ﴿٢٤﴾

24. Na hakika tunawajua watanguliao katika nyinyi na hakika tunawajua wachelewao.

وَإِنَّ رَبَّكَ هُوَ يَحْشُرُهُمْ إِنَّهُ حَكِيمٌ عَلِيمٌ ﴿٢٥﴾

25. Na hakika Mola wako ndiye atakayewakusanya. Hakika Yeye ni Mwenye hekima, Mjuzi.

NA ARDHI TUMEITANDAZA

Aya 19 -25

MAANA

Na ardhi tumeitandaza na tumeweka humo milima na tumeotesha kila kitu kwa wizani.

Umetangulia ufafanuzi wake katika Juz. 13 (13:3).

Kauli yake Mwenyezi Mungu: ‘Kila kitu kwa wizani’ ina maana moja na kauli yake:

وَكُلُّ شَيْءٍ عِندَهُ بِمِقْدَارٍ ﴿٨﴾

“Na kila kitu kwake, ni kwa kipimo” Juz.13 (13:8),

Pia kauli yake:

وَخَلَقَ كُلَّ شَيْءٍ فَقَدَّرَهُ تَقْدِيرًا ﴿٢﴾

“Na akaumba kila kitu na akakikadiria kipimo” (25:2).

Yaani anachunga kiwango, aina, sura na lengo la kupatikana kitu hicho. Kama ingelikuwa ni sadfa basi kusingelikuwa na mpangilio huu.

Na tumejaalia humo maisha.

Yaani humo ardhini, Maana ya maisha ni zile sababu za maisha; kama vile kilimo, biashara na viwanda. Lakini maisha ya unyonyaji na uporaji hivyo ni viwanda vya shetani, sivyo alivyovijaalia Mwenyezi Mungu.

Na ya ambao nyinyi sio wenye kuwaruzuku.

Kila kiumbe hai ardhini sisi hatukiruzuku wala hatukalifiwi na riziki yake, hilo liko wazi; isipokuwa lengo la ishara hii ni kuwa sisi tujue kuwa viumbe vyote hai vinaishi kwa riziki ya Mwenyezi Mungu, hakuna aliye hai anayeweza kumruzuku aliye hai; hata watoto tuwaleao na wanyama tuwafugao, riziki zao zote zinaatoka kwa Mungu, si kwa mwengine.

Na hakuna chochote ila hazina yake iko kwetu na wala hatukiteremshi isipokuwa kwa kipimo maalum.

Razi anasema: “Wameafikiana wafasiri kuwa makusudio ya chochote ni mvua, kwa vile hiyo ndiyo sababu ya riziki na maisha.” Lakini ukweli ni kuwa makusudio ya chochote ni mvua na mengineo. Kwa sababu neno chochote linaenea kwenye kila kitu; kama kusema sikumuona yeyote. Makusudo ya kuteremsha ni kutoa. Kiwango maalum ni sababu ya riziki. Maana ni kuwa heri yote iko kwa Mungu, Yeye ndiye anayewapa wenye kujitahidi, sio wavivu na wazembe. Mwenyezi Mungu ansema:

هُوَ الَّذِي جَعَلَ لَكُمُ الْأَرْضَ ذَلُولًا فَامْشُوا فِي مَنَاكِبِهَا وَكُلُوا مِن رِّزْقِهِ ﴿١٥﴾

Yeye ndiye aliyewafanyia ardhi iwe laini basi nendeni katika pande zake na kuleni katika riziki zake (67:15).

Kwa maelezo zaidi angalia kifungu ‘Je riziki ni bahati au majaaliwa?’ Juz.7 (5:100).

Na tukazipeleka pepo za kupandishia na tukateremsha kutoka mbinguni maji tukawanywesha hayo wala nyinyi sio mnaoyaweka akiba.

Pepo zimesifiwa kuwa za kupandishia mbegu kwa vile zinaabeba mawingu ya mvua na kufanya miti iwe inamea kutokana na mvua. Kwenye hali hii Mwenyezi Mungu ameishria mahali pengine kwa kusema: “Na yeye ndiye azipelekaye pepo kuwa ni bishara kabla ya kufika rehema yake. Hata zinapobeba mawingu mazito tunayasukuma kwa ajili ya mji uliokufa, Juz. 8 (7:57).

Vilevile zimesifiwa kuwa ni za kupandishia kwa vile zinahamisha mbegu za maua ya kiume na kuzipeleka kwenye maua ya kike ili yaweze kutoa mazao na matunda.

Makusdio ya kusema: ‘wala nyinyi sio mnaoyaweka akiba’, sio kuwa maji yote yako kwenye tangi kubwa lililoko kwa Mwenyezi Mungu, hapana; isipokuwa makusudio ni kuwa Mwenyezi Mungu anayateremsha maji kwa sababu zake za kimaumbile, kuayahifadhi ardhini na kuyatoa kidogo kidogo, kupitia mito, kulingana na mahitaji.

Na hakika sisi ndio tunaohuyisha na tunaofisha, Na sisi ndio warithi.

Sisi ndio warithi ni fumbo la kuwa kila aliyeko ataondoka, hatabaki yoyote isipokuwa dhati ya Mola mwenye utukufu na kutukuka.

Na hakika tunawajua watanguliao katika nyinyi na hakika tunawajua wachelewao.

Razi na Tabrasi wametaja njia sita katika maana ya watanguliao na wachelewao. Usahihi ni kuwa makusudio ni kwamba hakifichiki kitu chochote mbele ya Mwenyezi Mungu katika hali ya waliotangulia na watakaokuja nyuma.

Na hakika Mola wako ndiye atakayewakusanya, Hakika Yeye ni Mwenye hekima, Mjuzi.

Atawakusanya wote siku ya hisabu na malipo na ni Mwenye hekima katika kuwakusanya kwao huko, ambapo mtenda mema atapata thawabu za mema yake na mtenda maovu atapata adhabu ya movu yake. Vilievile Yeye anamjua aliyefanya mema na aliyefanya maovu.

2

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA NNE

وَلَقَدْ خَلَقْنَا الْإِنسَانَ مِن صَلْصَالٍ مِّنْ حَمَإٍ مَّسْنُونٍ ﴿٢٦﴾

26. Na hakika tulimuumba mtu kutokana udongo mkavu kwa matope meusi yenye kufinyangwa.

وَالْجَانَّ خَلَقْنَاهُ مِن قَبْلُ مِن نَّارِ السَّمُومِ ﴿٢٧﴾

27. Na majini tumewaumba kwa moto wenye joto kali.

وَإِذْ قَالَ رَبُّكَ لِلْمَلَائِكَةِ إِنِّي خَالِقٌ بَشَرًا مِّن صَلْصَالٍ مِّنْ حَمَإٍ مَّسْنُونٍ ﴿٢٨﴾

28. Na Mola wako alipowaambia Malaika: “Hakika mimi nitamuumba mtu kutokana na udongo mkavu kwa matope meusi yenye kufinyangwa.

فَإِذَا سَوَّيْتُهُ وَنَفَخْتُ فِيهِ مِن رُّوحِي فَقَعُوا لَهُ سَاجِدِينَ ﴿٢٩﴾

29. Basi nitakapomkamilisha na nikampulizia roho yangu, basi muangukieni kumsujudia.

فَسَجَدَ الْمَلَائِكَةُ كُلُّهُمْ أَجْمَعُونَ ﴿٣٠﴾

30. Wakasujudu Malaika wote pamoja.

إِلَّا إِبْلِيسَ أَبَىٰ أَن يَكُونَ مَعَ السَّاجِدِينَ ﴿٣١﴾

31. Isipokuwa Ibilisi alikataa kuwa pamoja na waliosujudi.

MTU KUTOKANA NA UDONGO

Aya 26 – 31

MAANA

Na hakika tulimuumba mtu kutokana na udongo mkavu kwa matope meusi yenye kufinyangwa.

Watu wamezungumza mengi sana kuhusu asili ya mtu. Darwin amesema kuwa asili ya mtu ni nyani. Tumefafanua kuhusu dhana ya Darwin na asili ya mtu katika Juz. 8. (7: 11). Hapa tunayarudia maudhui hayo kwa mfumo mwingine:

Maarifa ya kujua mambo yanakuwa tu katika hali zifuatazo:- Majaribio, kushuhudia, akili na wahyi. Ni wazi kwamba, kutokana na utafiti, tunaweza kumjua mtu alivyo. Ama kujua alipatikana vipi na alikuwa katika hali gani, swali hili haliwezi kujibiwa na majaribio.

Tukija kwenye kushuhudia, hakuna mtu aliyeshuhudia uumbwaji wa mtu, wala hakuna kitu, katika vinavyofukuliwa, kinachofahamisha asili ya mtu, Hilo tumelifafanua katika Juz. 8: (7:11–18). Ama tukiuliza akili kuhusu asili ya mtu, ni sawa na kuiuliza hiyo akili, ni nani baba yake fulani, je alikuwa ni mrefu au mfupi? Kwa hiyo basi hakuna kilichobakia katika kuja asili ya kuumbwa mtu isipokuwa ni kwa wahyi tu.

Mwenye kufuatilia Aya za Qur’an yenye hekima, atakuta baadhi ya Aya zinaasema:

وَهُوَ الَّذِي خَلَقَ مِنَ الْمَاءِ بَشَرًا ﴿٥٤﴾

Yeye ndiye aliyemuumba binadamu kutokana na maji (25:54).

Nyingine inasema:

كَمَثَلِ آدَمَ خَلَقَهُ مِن تُرَابٍ ثُمَّ قَالَ لَهُ كُن فَيَكُونُ ﴿٥٩﴾

“...ni kama mfano wa Adam; alimuumba kutokana na udongo, kisha akamwambia kuwa akawa.” Juz.3 (3:59)

Pia kuna ile isemayo: “Yeye ndiye aliyewaumba kwa udongo.” Juz, 7 (6:2) udongo uliokusudiwa hapa, kutokanana neno la kiarabu twin ni udongo mbichi – machanganyiko wa mchanga na maji.

Aya tuliyo nayo inasema kuwa mtu ameumbwa kutokana na udongo mkavu kwa tope nyeusi zinazoweza kufinyangwa, bila shaka hapo itakuwa ni mchanganyiko wa udongo na maji.

Kwa hiyo basi asili ya mtu ni maji na mchanga alioumbia Mwenyezi Mungu baba wa watu.

Na majini tumewaumba kwa moto wenye joto kali.

Jamaa wamekanusha kuweko majini, Baadhi ya waumini wamefasri majini waliotajwa katika Qur’an kuwa ni viini (microbe) visivyoonekana kwa macho. Wamechukulia neno Jinn kilugha, lenye maana ya kitu kililichofichikana na macho.

Wengine wakasema kuwa majini wapo, Wakatunga vitabu kuhusu idadi yao, miji yao, desturi zao, nembo zao na hata viongozi wao. Pia wakaelezea uwezekano wa jini kumuoa mtu au mtu kumuoa jini.

Sisi tunaamini kuweko majini, si kwa jingine isipokuwa tu wahyi umethibitisha hilo na inakubalika kiakili, Hatumwamini yeyote anayedai kuwa ana mawasiliano au kumuona jini. Hatukubali masimulizi yoyote yanayohusiana nao isipokuwa kwa kutamkwa wazi na wahyi.

Aya hii tuliyonayo imeweka wazi kuwa jini ameumbwa kutokana na moto na pia ile isemayo:

وَخَلَقَ الْجَانَّ مِن مَّارِجٍ مِّن نَّارٍ ﴿١٥﴾

Na akawaumba majini kwa ulimi wa moto (55:15).

Kwa hiyo sisi tunaamini kuwa asili ya majini ni moto. Lakini ni aina gani ya moto na je, umbile lenyewe lilikuwaje, Mwenyezi Mungu ndiye ajuaye zaidi.

Katika baadhi ya niliyoyasoma ni kuwa wataalamu wamegundua aina ya vidudu ambavyo haviwezi kupata uhai isipokuwa kwenye hewa ya sumu na vingine uhai wake uko kwenye visima vya mafuta na kwenye mwako.

Kwa hiyo kuna uwezekano kuwa kwenye sayari ya Jua kuna viumbe hai vinavyoafikiana na joto la Jua; kama samaki anavyoishi kwenye maji na kipepeo anavyopata rangi ya waridi na kobe kuwa na rangi ya jangwani.

Na Mola wako alipowaambia Malaika: Hakika mimi nitamuumba mtu kutokana udongo mkavu kwa matope meusi yenye kufinyangwa.

Mwenyezi Mungu aliwaambia hivi Malaika, lakini Malaika nao wakamawambia Mungu:

Je utaweka humo watakaofanya ufisadi humo na kumwaga damu? Juz,1 (2:30).

Tumeeleza huko kuhusu Malaika kujibizana na Mungu na kwamba aliwa- pa nafasi ya maswali na majibizano yaliyofanana na kupinga; kisha akawafahamisha uhakika kwa njia ya upole. Pengine anaweza kupata funzo yule anayejiona ni zaidi ya wote.

Basi nitakapomkamilisha na nikampulizia roho yangu.

Yaani nitakapompa uhai, Angalia Juz, 6 (4: 171 – 173), huko tumefafanua zaidi kuhusu neno roho

Basi muangukieni kumsujudia, Wakasujudu Malaika wote pamoja isipokuwa Ibilisi alikataa kuwa pamoja na waliosujudu.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 1 (2:34).

قَالَ يَا إِبْلِيسُ مَا لَكَ أَلَّا تَكُونَ مَعَ السَّاجِدِينَ ﴿٣٢﴾

32. Akasema (Mwenyezi Mungu): Ewe Iblisi! Una nini hata hukuwa pamoja na waliosujudu?

قَالَ لَمْ أَكُن لِّأَسْجُدَ لِبَشَرٍ خَلَقْتَهُ مِن صَلْصَالٍ مِّنْ حَمَإٍ مَّسْنُونٍ ﴿٣٣﴾

33. Akasema (Iblis): “Haiwi mimi kumsujudia uliyemuumba kutokana na udongo mkavu kwa matope meusi yenye kufinyangwa.”

قَالَ فَاخْرُجْ مِنْهَا فَإِنَّكَ رَجِيمٌ ﴿٣٤﴾

34. Akasema (Mwenyezi Mungu): Basi toka humo, kwani hakika wewe ni mwenye kufukuzwa.

وَإِنَّ عَلَيْكَ اللَّعْنَةَ إِلَىٰ يَوْمِ الدِّينِ ﴿٣٥﴾

35. Na hakika itakuwa juu yako laana mpaka siku ya malipo.

قَالَ رَبِّ فَأَنظِرْنِي إِلَىٰ يَوْمِ يُبْعَثُونَ ﴿٣٦﴾

36. Akasema (Iblisi): “Mola wangu! Nipe muda mpaka siku watakapofufuliwa.

قَالَ فَإِنَّكَ مِنَ الْمُنظَرِينَ ﴿٣٧﴾

37. (Mwenyezi Mungu) akasema: Basi hakika wewe ni katika waliopewa muda.

إِلَىٰ يَوْمِ الْوَقْتِ الْمَعْلُومِ ﴿٣٨﴾

38. Mpaka siku ya wakati maalum.

قَالَ رَبِّ بِمَا أَغْوَيْتَنِي لَأُزَيِّنَنَّ لَهُمْ فِي الْأَرْضِ وَلَأُغْوِيَنَّهُمْ أَجْمَعِينَ ﴿٣٩﴾

39. Akasema (Iblisi): Kwa ulivyonipoteza, basi nitahakikisha ninawazaini hapa ardhini na nitawapoteza wote.

إِلَّا عِبَادَكَ مِنْهُمُ الْمُخْلَصِينَ ﴿٤٠﴾

40. Isipokuwa waja wako waliosafishwa.

قَالَ هَـٰذَا صِرَاطٌ عَلَيَّ مُسْتَقِيمٌ ﴿٤١﴾

41. Akasema (Mwenyezi Mungu): Hii ni njia juu yangu mimi iliyonyooka.

إِنَّ عِبَادِي لَيْسَ لَكَ عَلَيْهِمْ سُلْطَانٌ إِلَّا مَنِ اتَّبَعَكَ مِنَ الْغَاوِينَ ﴿٤٢﴾

42. Hakika waja wangu hutakuwa na mamlaka nao, isipokuwa wale wapotofu waliokufuata.

وَإِنَّ جَهَنَّمَ لَمَوْعِدُهُمْ أَجْمَعِينَ ﴿٤٣﴾

43. Na hakika Jahannam ndipo mahali pao walipoahidiwa wote.

لَهَا سَبْعَةُ أَبْوَابٍ لِّكُلِّ بَابٍ مِّنْهُمْ جُزْءٌ مَّقْسُومٌ ﴿٤٤﴾

44. Ina milango saba, kila mlango una sehemu waliyotengewa.

MUNGU ANAULIZA NA IBLISI ANAJIBU

Aya 32 – 44

MAANA

Mwenyezi Mungu (s.w.t) aliwaamuru Malaika kumsujudia Adam kwa sijda ya kimaamkuzi sio ya kiibada, Wakatii wote, lakini Ibilisi akaasi. Maulamaa wamehitilafiana kuhusu jinsia ya Iblisi, kuwa je, alikuwa Malaika kisha akafukuzwa au alikuwa shetani tangu mwanzo?

Mzozo huu ni tasa. Maadam Ibilisi kwa hali yoyote ni mwenye kulaumiwa na mwenye kufurushwa. Alpojizuia kusujudu Mola Mtukufu alimuuliza:

Akasema (Mwenyezi Mungu): Ewe Iblisi! Una nini hata hukuwa pamoja na waliosujudu?

Je, wewe una cheo zaidi au ni mtukufu sana kuliko waliomsujudia Adam?

Akasema (Iblis): Haiwi mimi kumsujudia uliyemuumba kutokana na udongo mkavu kwa matope meusi yenye kufinyangwa.

Iblisi aliasi na kufanya jeuri, sio kwa kitu kingine isipokuwa ni ubaguzi wa rangi tu. Na kila mwenye kufanya ubaguzi kwa sababu ya asili yake na jinsia yake, basi ni mwenye kulaaniwa, kufukuzwa na kulaumiwa; sawa na Iblisi.

Akasema (Mwenyezi Mungu): Basi toka humo, kwani hakika wewe ni mwenye kufukuzwa na hakika itakuwa juu yako laana mpaka siku ya malipo.

Humo, ni humo mwenye daraja ya juu. Maana ni kuwa Mwenyezi Mungu alimfukuza Iblisi kutoka kwenye rehema yake hadi kwenye adhabu yake na akamfanya ni maluuni kwa ndimi zote mpaka siku ya Kiyama, ikiwa ni malipo ya kiburi chake na kuacha kwake kumtii Mwenyezi Mungu.

Akasema (Iblisi): “Mola wangu! Nipe muda mpaka siku watakapofufuliwa.

Alitaka muda huu kwa haja yake aliyoikusudia, tutakayoifafanua mbele(Mwenyezi Mungu) akasema: Basi hakika wewe ni katika waliopewa muda mpaka siku ya wakati maalum.

Hiyo ni siku ya kupuliziwa parapanda ambayo inafahamishwa na Aya isemayo:

وَنُفِخَ فِي الصُّورِ فَصَعِقَ مَن فِي السَّمَاوَاتِ وَمَن فِي الْأَرْضِ ﴿٦٨﴾

“Na itakapopuziwa parapanda wazimie waliomo mbinguni na waliomo ardhini” (39:68)

Akasema (Iblisi): Kwa ulivyonipoteza,

Yaani kwa sababu ya kunitia mtihani wa amri ya kumsujudia Adam ambayo imeniingiza katika upotevu na uasi,basi nitahakikisha ninawazaini hapa ardhini na nitawapoteza wote, isipokuwa waja wako waliosafishwa.

Iblisi alichukua ahadi ya kuchukua kisasi cha maafa yake kwa kiumbe hiki kilichokuwa ni sababu ya kufukuzwa kwake kutoka rehema ya Mola wake hadi kwenye laana yake.

Akasema (Mwenyezi Mungu): Hii ni njia juu yangu mimi iliyonyooka.

Hii ni ishara ya kujichunga wale wenye ikhlasi kutokana na shetani na upotevu wake.

Juu yangu mimi, yaani ni yenye kuthibiti kwake Mwenyezi Mungu Mtukufu; mfano kauli yake Mwenyezi Mungu: “Mola wenu amejilazimisha rehema, Juz, 7 (6:54).

Maana ni kuwa Mwenyezi Mungu amejilazimishia kwamba ikhlasi ndiyo njia ya kunyooka. Mwenye kuifuata ataokoka na mwenye kukengeuka nayo ameangamia.

Hakika waja wangu hutakuwa na mamlaka nao, isipokuwa wale wapotofu waliokufuata.

Wale wanaoabudu pesa wakiuza dini na nchi kwa kila atakayetoa pesa. Ama wale wema wenye ikhlasi, hawawezi hata kusogelewa na Iblisi, sikwambii kuwa na mamlaka nao. Umetangulia mfano wa Aya hii katika Juz, 8 (7:11- 18).

Na hakika Jahannam ndipo mahali pao walipoahidiwa wote.

Huko kwenye shimo la Jahannam watakutana wote, Iblisi na wafuasi wake. Kila mmoja atamlaani mwenzake na kumkana; mfuaswa atamkana mfuasi, Kwa maelezo zaidi angalia kifungu cha ‘Hotuba ya shetani’ katika Juz. 13 (14:22)

Ina milango saba, kila mlango una sehemu waliyotengewa.

Imesemekana kuwa makusudio ya milango ni milango hasa kwa maana ya tamko lenyewe. Wengine wakasema makusudio ni tabaka na kwamba baadhi ya moto uko juu ya baadhi ya mwingine; na kuwa kila tabaka ina jina lake inalolihusu; kama vile Jahnnam, Jahim, Ladhaa, Saqar, Hutama n.k.

Vyovyote yatakavyokuwa makusudio, hali halisi inajulikana; kwamba maovu yana daraja; kuna yaliyo makubwa ya hatari, yaliyo madogo yasiyo na hatari na yale ya katikati, Kila ovu lina adhabu yake inayolistahili bila ya kuzidi, Tumefafanua katika Juz, 13 (46 – 52), Kifungu cha ‘Jahannam na silaha za maangamizi.

إِنَّ الْمُتَّقِينَ فِي جَنَّاتٍ وَعُيُونٍ ﴿٤٥﴾

45. Hakika wenye takua watakuwa katika Bustani (Pepo) na chemchemi.

ادْخُلُوهَا بِسَلَامٍ آمِنِينَ ﴿٤٦﴾

46. (Wataambiwa): Ingieni kwa salama mkiwa na amani.

وَنَزَعْنَا مَا فِي صُدُورِهِم مِّنْ غِلٍّ إِخْوَانًا عَلَىٰ سُرُرٍ مُّتَقَابِلِينَ ﴿٤٧﴾

47. Na tutaondoa chuki iliyokuwamo vifuani mwao wawe ndugu, juu ya viti wakielekeana.

لَا يَمَسُّهُمْ فِيهَا نَصَبٌ وَمَا هُم مِّنْهَا بِمُخْرَجِينَ ﴿٤٨﴾

48. Humo hayatawagusa machovu wala hawatatolewa humo.

نَبِّئْ عِبَادِي أَنِّي أَنَا الْغَفُورُ الرَّحِيمُ ﴿٤٩﴾

49. Watanabahishe waja wangu ya kwamba mimi ndiye Mwenye kughufiria, mwenye kurehemu.

وَأَنَّ عَذَابِي هُوَ الْعَذَابُ الْأَلِيمُ ﴿٥٠﴾

50. Na kwamba adhabu yangu ndiyo adhabu iliyo chungu.

WENYE TAKUA PEPONI

Aya 45 – 50

MAANA

Bada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kutaja adhabu ya wakosefu na wale waliopotea, na kwamba wao watafufuliwa kesho huku nyuso zao zikiwa zimegubikwa na moto tena wakiwa na nguo za moto, amefuatishia kwa kutaja malipo ya wenye takua, wacha Mungu. Kwamba wao watalipwa raha starehe amani na usafi wa kila aina, kwa ufafanuzi ufuatao:

1.Hakika wenye takua watakuwa katika Bustani (Pepo) na chemchemi.

Maisha ni mazuri katika kila kitu, kuanzia vyakula hadi vinywaji na mandhari hadi Hurulaini.

وَفِيهَا مَا تَشْتَهِيهِ الْأَنفُسُ وَتَلَذُّ الْأَعْيُنُ ﴿٧١﴾

Kuna vinavyopendwa na nafsi na kufurahiwa na macho (43:71).

2.(Wataambiwa): Ingieni kwa salama mkiwa na amani.

Maisha mazuri ya amani yasiyokuwa na hofu wala huzuni

Na tutaondoa chuki iliyokuwamo vifuani mwao wawe ndugu, juu ya viti wakielekeana.

Hata starehe pia ni safi, hakuna chuki zinazochemka nyoyoni; kama ilivyo kwa watu wa motoni, alipowasifu Mwenyezi Mungu kwa kauli yake: “Kila utakapoingia umma utalaani ndugu zake. Juz.8 (7:38).

3.Humo hayatawagusa machovu wala hawatatolewa humo.

Hakuna ufukara, maradhi, hofu wala chuki, Pia hakuna tabu wala kuchoka, Sifa zote hizi ni za kudumu, haziondoki wala kupungua.

Watanabahishe waja wangu ya kwamba mimi ndiye Mwenye kughufiria, mwenye kurehemu, na kwamba adhabu yangu ndiyo adhabu iliyo chungu.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) amekutanisha, katika Aya mbili hizi, bishara na hadhari, ili muasi asikate tamaa na rehema ya Mwenyezi Mungu na maghufira yake, bali arejee na atubie kwake Mwenyezi Mungu Mtukufu na ili awe na hadhari mtiifu kutokana na makosa na ufisadi, na awe mnyenyekevu; wala asijitie majivuno na ghururi. Razi anasema: “Mwenyezi Mungu alipotaja maghufira na rehema alilisisitiza sana kwa matamshi matatu: ‘Hakika mimi, mimi na kuingiza alif na lam katika neno la kiarabu al-ghafur (mwenye kughufiria). Lakini alipotaja adhabu hakusema hakika mimi wala mimi; bali amesema: hakika adhabu yangu.