TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TANO Juzuu 15

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TANO22%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TANO Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: Qurani tukufu

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
  • Anza
  • Iliyopita
  • 19 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 16827 / Pakua: 3980
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TANO

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TANO Juzuu 15

Mwandishi:
Swahili

1

7

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TANO

وَقُل لِّعِبَادِي يَقُولُوا الَّتِي هِيَ أَحْسَنُ إِنَّ الشَّيْطَانَ يَنزَغُ بَيْنَهُمْ إِنَّ الشَّيْطَانَ كَانَ لِلْإِنسَانِ عَدُوًّا مُّبِينًا ﴿٥٣﴾

53. Waambie waja wangu waseme maneno mazuri. Kwani shetani huchochea baina yao. Hakika shetani ni adui aliye dhahiri kwa mtu.

رَّبُّكُمْ أَعْلَمُ بِكُمْ إِن يَشَأْ يَرْحَمْكُمْ أَوْ إِن يَشَأْ يُعَذِّبْكُمْ وَمَا أَرْسَلْنَاكَ عَلَيْهِمْ وَكِيلًا ﴿٥٤﴾

54. Mola wenu anawajua vilivyo, akipenda atawarehemu na akipenda atawaadhibu. Na hatukukutuma ili uwe mlinzi juu yao.

وَرَبُّكَ أَعْلَمُ بِمَن فِي السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ وَلَقَدْ فَضَّلْنَا بَعْضَ النَّبِيِّينَ عَلَىٰ بَعْضٍ وَآتَيْنَا دَاوُودَ زَبُورًا ﴿٥٥﴾

55. Na Mola wako anawajua vilivyo waliomo mbinguni na waliomo ardhini. Na hakika tumewafadhilisha baadhi ya manabii kuliko wengine; na Daud tulimpa Zaburi.

قُلِ ادْعُوا الَّذِينَ زَعَمْتُم مِّن دُونِهِ فَلَا يَمْلِكُونَ كَشْفَ الضُّرِّ عَنكُمْ وَلَا تَحْوِيلًا ﴿٥٦﴾

56. Sema: Waombeni hao mnaodai badala Yake; hawawezi kuwaondolea madhara wala kuyabadilisha.

أُولَـٰئِكَ الَّذِينَ يَدْعُونَ يَبْتَغُونَ إِلَىٰ رَبِّهِمُ الْوَسِيلَةَ أَيُّهُمْ أَقْرَبُ وَيَرْجُونَ رَحْمَتَهُ وَيَخَافُونَ عَذَابَهُ إِنَّ عَذَابَ رَبِّكَ كَانَ مَحْذُورًا ﴿٥٧﴾

57. Hao wanawaomba, wao wenyewe wanatafuta njia ya kujikurubisha kwa Mola wao, hata walio karibu miongoni mwao, na wanataraji rehema zake na wanaihofu adhabu yake. Hakika adhabu ya Mola wako ni ya kuhofiwa.

WAAMBIE WAJA WANGU WASEME MANENO MAZURI

Aya 53 – 57

MAANA

Waambie waja wangu waseme maneno mazuri.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) alimwamrisha Mtume wake mtukufu awaamrishe waumini au watu wote waseme maneno mazuri, watamke haki na uadilifu kwa thamani yoyote itakayokuwa, Angali Juz; 13 (14: 24–26).

Kwani shetani huchochea baina yao.

Shetani hutafuta makosa ya ulimi ili ayafanye ni kuni za moto wa uadui na chuki baina ya watu. Makosa ya ulimi hayawi tu kwa kutukana bali pia kwa kusifu pasipokuwa mahali pake na kwenye matamshi ya ufuska na uovu.

Hakika shetani ni adui aliye dhahiri kwa mtu.

Uadui huu aliubainisha wazi pale aliposema:

قَالَ فَبِمَا أَغْوَيْتَنِي لَأَقْعُدَنَّ لَهُمْ صِرَاطَكَ الْمُسْتَقِيمَ ﴿١٦﴾ ثُمَّ لَآتِيَنَّهُم مِّن بَيْنِ أَيْدِيهِمْ وَمِنْ خَلْفِهِمْ وَعَنْ أَيْمَانِهِمْ وَعَن شَمَائِلِهِمْ ﴿١٧﴾

“Kwa kuwa umenipoteza, basi hakika nitawakalia katika njia yako iliyonyooka; kisha hakika nitawaendea kwa mbele yao na nyuma yao na kuumeni kwao na kushotoni kwao” Juz; 8 (7:16-17).

Mola wenu anawajua vilivyo, akipenda atawarehemu na akipenda atawaadhibu.

Mwenyezi Mungu ni Mjuzi, Mwadilifu na Mwenye hekima. Anajua hali za waja wake, yale yaliyo na masilahi nao na yale yenye ufisadi na anawachukulia kwa uadilifu wake na hekima yake.

Atamrehemu anayestahiki rehema naye ni yule anayefuata amri na mtiifu; Na atamwadhibu anayestahiki adhabu; naye ni yule muasi jeuri. Hiyo ni baada ya kuwawekea hoja kwa kuwafikishia yaliyo halali na yaliyo haramu kupitia kwa Mtume mtukufu.

Na hatukukutuma ili uwe mlinzi juu yao , bali ni mfikishaji:

فَإِنَّمَا عَلَيْكَ الْبَلَاغُ وَعَلَيْنَا الْحِسَابُ ﴿٤٠﴾

“Basi ni juu yako kufikisha na juu yetu hisabu,” Juz.13: (13:40).

Na Mola wako anawajua vilivyo waliomo mbinguni na waliomo ardhini. Na hakika tumewafadhilisha baadhi ya manabii kuliko wengine; na Daud tulimpa Zaburi.

Mwenyezi Mungu anawajua watu wa mbinguni na wa ardhini na anajua uwezo wa kila mmoja wao. Kwa misingi hiyo ndio huwachagua wajumbe kwenda kwa mitume wake; kama vile Jibril(a.s) . Na hupeleka mitume wabashiri na waonyaji kwa watu.

Kama alivyowafadhilisha baadhi ya Malaika kuliko wengine; vilevile Mitume, baadhi amaewafadhilisha kuliko wengine.

Unaweza kuuliza kuwa : Uislamu unasimama kwenye misingi ya usawa ;sasa kuna maana gani ya ubora huu kwa baadhi kuliko wengine? Kisha ubora huu utapatikana vipi kwa Malika na Mitume na hali tunajua kuwa wote ni waja wa Mwenyezi Mungu wenye kutukuzwa, hawamtangulii kwa jambo lolote na wanafanya kulingana na amri yake?

Jibu : Ndio ni kweli kuwa hakuna tofauti kwa msingi wa utiifu, isma, na utawala kama ulivyo; isipokuwa kwa upande wa sifa; kama vile dhahabu tunajua kuwa yote ina thamani, lakini kuna baadhi inathamani zaidi kuliko nyingine. Vile vile vitu vingine vizuri vinatofautiana kulingana na uzuri wake na daraja yake, sio katika kuwa kwake na hakika yake. Ndio maana ikasemwa: ‘Nuru juu ya nuru’ au ‘kheri juu ya kheri’

Swali la pili : imekuwaje Mwenyezi Mungu kumtaja Daud peke yake kuwa amempa Zaburi na tunajua kuwa Musa alimpa Tawrat, Isa Injil na Muhammad akampa Qur’an?

Amemtaja peke yake kuwarudi washirikina waliosema: vipi Muhammad atakuwa ni mtume na yeye ni yatima fukara. Njia ya kuwarudi ni kuwa Yeye Mwenyezi Mungu (s.w.t) anaujalia ujumbe wake kwa yule anayestahiki - awe yatima aliyefukara, kama Muhammad au tajiri, kama Daud. Katika vitabu vingi vya sera na tarikh, hutajwa Mfalme Daud.

Sema: Waombeni hao mnaodai badala Yake, hawawezi kuwaondolea madhara wala kuyabadilisha.

Wafasiri wengi wamesema kuwa Aya hii na inayofuatia zilishuka kwa ajili ya wale wanaoabudu malaika, Isa na Uzayr. Na kwamba wanokusudiwa hapa sio waabudu masanamu, kwa sababu Mwenyezi Mungu amewataja hao waabudiwa kwa kusema: ‘wao wenyewe wanatafuta njia ya kujikuru- bisha kwa Mola wao,’ na kutafuta nji hakuelekeani na masanamu.

Kwa hiyo maana ni kuwa ewe Muhammad! Waambie wale wanaoabudu Malaika, Isa na Uzayr: yakiwapata madhara, kama ufukara na maradhi, basi waaombeni wale manowaabudu wawaondolee, kisha muangalie, je wanaweza kuwakinga au kuwabadilishia? Hakuna mwenye shaka ya kushindwa kwao, kwa vile wao wenyewe hawawezi kujikinga itakuwaje kwa mwengine?

Hao wanawaomba, wao wenyewe wanatafuta njia ya kujikurubisha kwa Mola wao.

Yaani hao ambao mnawaabudu enyi washirikina wanatafuta kujikuruku- bisha kwa Mwenyezi Mungu kwa twaa, hawajitii kiburi kwa waja wengine, wanamtakasa na kumsujudia Mungu, sasa vipi nyinyi mnawaabudu.

Hata walio karibu miongoni mwao, na wanataraji rehema zake na wanaihofu adhabu yake.

Yaani kila mmoja kati ya Malaika, Isa na Uzayr anajitahidi, kumwabudu Mwenyezi Mungu na kumfanyia ikhlasi ili awe karibu na msamaha wake na rehema zake na awe mbali na machukivu yake.

Hiyo ni kwa vile Hakika adhabu ya Mola wako ni ya kuhofiwa.

Wanaihofia manabii na mawalii, je, wengine? Kila mwenye akili ni lazima ahofie mwisho na kuuandalia maandalizi, kwa hali yoyote atakavyokuwa na cheo na daraja; hasa ikiwa mwenye kuchukua hisabau anajua siri na yaliyofichikana.

وَإِن مِّن قَرْيَةٍ إِلَّا نَحْنُ مُهْلِكُوهَا قَبْلَ يَوْمِ الْقِيَامَةِ أَوْ مُعَذِّبُوهَا عَذَابًا شَدِيدًا كَانَ ذَٰلِكَ فِي الْكِتَابِ مَسْطُورًا ﴿٥٨﴾

58. Hapana mji wowote ila Sisi tutauangamiza kabla ya Siku ya Kiyama au kuupa adhabu kali, Haya yamekwishaandikwa kwenye Kitabu.

وَمَا مَنَعَنَا أَن نُّرْسِلَ بِالْآيَاتِ إِلَّا أَن كَذَّبَ بِهَا الْأَوَّلُونَ وَآتَيْنَا ثَمُودَ النَّاقَةَ مُبْصِرَةً فَظَلَمُوا بِهَا وَمَا نُرْسِلُ بِالْآيَاتِ إِلَّا تَخْوِيفًا ﴿٥٩﴾

59. Na hapana kinachotuzuia kupeleka miujiza ila ni kuwa watu wa zamani waliikanusha. Na wathamudi tuliwapa ngamia jike kuwa ni dalili inayoonekana, lakini wakamdhulumu. Nasi hatupeleki ishara ila kwa ajili ya kuhadharisha.

وَإِذْ قُلْنَا لَكَ إِنَّ رَبَّكَ أَحَاطَ بِالنَّاسِ وَمَا جَعَلْنَا الرُّؤْيَا الَّتِي أَرَيْنَاكَ إِلَّا فِتْنَةً لِّلنَّاسِ وَالشَّجَرَةَ الْمَلْعُونَةَ فِي الْقُرْآنِ وَنُخَوِّفُهُمْ فَمَا يَزِيدُهُمْ إِلَّا طُغْيَانًا كَبِيرًا ﴿٦٠﴾

60. Na tulipokwambia: hakika Mola wako amekwishawazunguka hao watu. Na hatukuifanya ndoto tuliyokuonyesha ila ni fitna (majaribu) kwa watu na mti uliolaaniwa katika Qur’an. Na tunawahadharisha, lakini haiwazidishii ila uasi mkubwa.

MJI WOWOTE

Aya 58 – 60

MAANA

Mahdiy Anayengojewa

Hapana mji wowote ila Sisi tutauangamiza kabla ya siku ya Kiyama au kuupa adhabu kali, Haya yamekwishaandikwa kwenye Kitabu.

Dhahir ya Aya inafahamisha kuwa watu wote watatoweka kabla ya siku ya kiyama, ambapo itafika siku kwenye ardhi kutakuwa hakuna yoyote kabisa; na kwamba jambo hili limekwishaandikwa katika kadha na kadari ambayo haiepukiki. Kuna jamii itatoweka kwa mauti ya kawaida na nyingine kwa adhabu kali, lakini Mwenyezi Mungu hakubainisha wasifa wa hawa wala wale.

Hiyo ndiyo dhahir ya Aya, lakini wafasiri wamesema kuwa jamii njema itatoweka kwa mauti ya kawaida na jamii ya ufisadi itatoweka kwa adhabu kali. Lakini haya hayaafikianai na kauli yao katika kufasiri Aya za mwanzo za sura Hajj:

يَا أَيُّهَا النَّاسُ اتَّقُوا رَبَّكُمْ إِنَّ زَلْزَلَةَ السَّاعَةِ شَيْءٌ عَظِيمٌ ﴿١﴾ يَوْمَ تَرَوْنَهَا تَذْهَلُ كُلُّ مُرْضِعَةٍ عَمَّا أَرْضَعَتْ وَتَضَعُ كُلُّ ذَاتِ حَمْلٍ حَمْلَهَا وَتَرَى النَّاسَ سُكَارَىٰ وَمَا هُم بِسُكَارَىٰ وَلَـٰكِنَّ عَذَابَ اللَّـهِ شَدِيدٌ ﴿٢﴾

“Enyi watu! Mcheni Mola wenu, Hakika tetemeko la Saa (ya Kiyama) ni jambo kuu. Siku mtakapoiona, kila mwenye kunyonyesha atamsahau amnyonyeshae na kila mwenye mimba ataharibu mimba yake na utawaona watu wamelewa kumbe hawakulewa. Lakini adhabu ya Mwenyezi Mungu ni kali,” (22:1-2).

Tuonavyo sisi mji alioukusudia katika kauli yake hii ni mji ambao watu wake ni madhalimu; yaani jamii yenye ufisadi tu; na kwamba Yeye ataiangamiza jamii hii au ataiadhibu kabla ya Siku ya Kiyama, wala hawatabakia ispokua watu wema tu, wote wakiwa wanaishi kwenye twaa ya Mwenyezi Mungu wakiwa na amani ya nafsi zao na vitu vyao vyote.

Kuna Hadith nyingi zinazozungumzia suala hilo; miongoni mwazo ni hizi:-

Hadith iliyoko kwenye Sunan Abi Daud As-sasjsataniy, kikiwa ni mojawapo ya Sahih sita kwa masunni, Juzuu ya pili chapa ya mwaka 1952, uk. 422:

“Amesema Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) : Lau haitabaki isipokuwa siku moja ya dunia, basi Mwenyezi Mungu atairefusha siku hiyo mpaka amlete mtu kutokana na watu wa nyumba yangu (Ahli bayti), Jina lake linafanana na jina langu na jina la baba yake ndio jina la baba yangu, ataijaza ardhi usawa na uadilifu; kama ilivyojazwa dhulma baada kujazwa usawa na uadilifu.”

Hadith iliyoko katika Sunan Ibn Maja, Pia nayo ni miongoni mwa sahih sita, juzuu ya pili chapa ya mwaka 1952, Hadith namba: 4083: Amesema: “Mtume wa Mwenyezi Mungu: “Atakuwa katika umma wangu Mahdi, utaneemeka uma wangu neema ambayo haujaneemeka mfano wake.”

Mapinduzi na kujitoa mhanga kwa kujilipua (intifada), kila mahali kwa ajili ya kujikomboa na dhulma, ufisadi, ujinga na umasikini, yana fahamisha waziwazi kuwa hilo litakuwa tu karibuni au baadaye.

Na hapana kinachotuzuia kupeleka miujiza ila ni kuwa watu wa zamani waliikanusha. Na wathamudi tuliwapa ngamia jike kuwa ni dalili inayoonekana, lakini wakamdhulumu.

Washirikina walipendekeza kwa Mtume awaletee muujiza wanaoutaka wao. Miongoni mwa waliyoyasema ni: Tuchimbulie chemchem kutoka ardhini, tuletee Mungu na Malaika, tuletee kitabu kutoka mbinguni tukisome na mengineyo.

Ndio Mwenyezi Mungu akawajibu katika Aya hii, kwamba yeye amekwishapitisha katika kadha na kadari yake, kuwang’owa kwa adhabu kila kaumu iliyokadhibisha miujiza iliyokuja kwa maombi yao.

Wathamudi walimwomba Mtume wao awapatie ngamia wa muujiza. Alipowajia na sifa zile walizozitaka, walimkanusha na wakamchinja. Ukawanyakua ukelele wakawa ni wenye kuangamia; Yametangulia maelezo ya ngamia katika Juz; 8 (7:73 –79).

Imekwishapitisha kadari yake kutowang’oa Makuraishi, kutokana na mapendekezo waliyoyapendekeza kwa Mtume. Kwa sababu watapatikana watu watakaotubia na kuamini, watazaliwa wengine wapigania jihadi kwa Mwenyezi Mungu. zaidi ya hayo kadari ya Mwenyezi Mungu imepitisha kuwa uma wa Muhammad na sharia yake ubakie mpaka siku ya ufufuo. Kwa sababu hii na nyinginezo, Mwenyezi Mungu (s.w.t) hakuitikia maombi ya makuraishi.

Nasi hatupeleki ishara ila kwa ajili ya kuhadharisha.

Hakuna ishara yoyote inayodhihiri mikononi mwa Mtume ila ina malengo; yakiwemo: mawaidha, makaripio na kuhadharisha adhabu isiyokuwa na kinga wala kafara; sasa vipi wao wanaharakia kutoa maombi ya adhabu?

Na tulipokwambia: hakika Mola wako amekwishawazunguka hao watu.

Imeelezwa hapo juu kuwa makuraishi walimtaka Mtume awalete muujiza na kwamba Mwenyezi Mungu (s.w.t) alimpa wahyi Mtume wake kuwa lau atawaitikia maombi yao na wakaasi, wataangamia.

Lakini jawabu hili halikuwakinaisha washirikina na wakamwambia kuwa lau ungelikuwa ni Mtume ungelituletea yale tunayotaka, ndipo Mwenyezi Mungu akamwambia mtume wake kuwa wewe endelea tu, wala usiwajali wale wanaofanya inadi na kiburi. Sisi tunawajua zaidi watu na wanayoy- afanya na tumewadhibiti.

Katika maana ya Aya hii ni ile isemayo:

وَاللَّـهُ يَعْصِمُكَ مِنَ النَّاسِ ﴿٦٧﴾

“Na Mwenyezi Mungu atakulinda na watu,” Juz. 6 (5:67).

Na hatukuifanya ndoto tuliyokuonyesha ila ni fitna (majaribu) kwa watu.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) anasema kuwa alimuonyesha Mtume wake ndoto usingizini na kwamba ndoto yenyewe ni fitna, lakini hakubainisha ilikuwa ya aina gani wala makusudio ya hiyo fitna au majaribu.

Ndio maana wafasiri wakatofautiana katika maana yake, Akataja Razi kati- ka Tafsiri al-kabir, Abu Hayan Al-andalusi katika Al-bahrul-muhit, Muhammad bin Ahmad Al-kalabiy, katika Attas-hil na wengineo, wametaja kauli kadhaa katika tafsiri ya ndoto na fitna.

Miongoni mwazo ni mtume(s.a.w.w) aliota kuwa yeye ataingia Makka pamoja na swahaba, lakini alipotaka kuingia makuraishi walimzuia katika mwaka wa Hudaybiya.

Akaingiwa na shaka mwenye shaka miongoni mwa waislamu kuhusu ndoto ya Mtume, akamwambia: “Si umesema kuwa tutaingia Makka kwa amani?” Akasema: “Ndio, kwani nimesema tutaingia mwaka huu?” Akasema: “Hapana” Mtume(s.a.w.w) akasema: “Inshallah tutaingia” wakaingia mwaka uliofuatia.

Miongoni mwa kauli nyingine zinazotokana na tafsiri ni kuwa Mtume(s.a.w.w) aliona kwenye ndoto bani Umayya wakiiparamia mimbari yake kama anavyoparamia nyani, akahuzunika na akawa hana raha, na hakuonekana akicheka.

Kikundi miongoni mwa swahaba wako kwenye tafsiri hii; miongoni mwao ni Said bin Al-musabbib na Ibn Abbas; kama ilivyo katika Tafsiru-rrazi. Pia Sahal bin Sa’d; kama ilivyo katika Tafsir Al-bahr al-muhit.

Katika Sahih Al-bukhari Juzuu ya tisa Kitabu Al-fitan, imeelezwa kuwa Mtume(s.a.w.w) alisema: “Kuangamia kwa umma wangu kutakua mikononi mwa wafidhuli wa kikuraishi,” Riwaya hii inatia nguvu tafsiri ya ndoto kuhusu Bani Umayya.

Kwa hiyo makusudio yaNa mti uliolaaniwa katika Qur’an ni Bani Umayya. Katika Tafsiru-rrazi imeelezwa kuwa kuna kundi la wafasiri wanasema: “Mti uliolaaniwa katika Qur’an ni mayahudi.” Matukio ya Historia ya kale na ya sasa yamethibitisha kuwa mayahudi ndio mzizi wa fitina.

Na tunawahadharisha, lakini haiwazidishii ila uasi mkubwa.

Mwenyezi Mungu amewahadharisha wanafiki kwa mifumo mbalimbali, lakini haikufaa kitu; bali hizo hadhari ziliwazidishia upotevu, kwa sababu wao hawataharaki isipokuwa kwa wahyi wa masilahi na manufaa. Ama hoja, maadili na misimamo, kwao ni maneno na njozi tu.

8

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TANO

وَإِذْ قُلْنَا لِلْمَلَائِكَةِ اسْجُدُوا لِآدَمَ فَسَجَدُوا إِلَّا إِبْلِيسَ قَالَ أَأَسْجُدُ لِمَنْ خَلَقْتَ طِينًا ﴿٦١﴾

61. Na tulipowaambia Malaika: Msujudieni Adam, wakamsujudia wote isipokuwa Iblis, alisema: Je, nimsujudie uliyemuumba kwa udongo?

قَالَ أَرَأَيْتَكَ هَـٰذَا الَّذِي كَرَّمْتَ عَلَيَّ لَئِنْ أَخَّرْتَنِ إِلَىٰ يَوْمِ الْقِيَامَةِ لَأَحْتَنِكَنَّ ذُرِّيَّتَهُ إِلَّا قَلِيلًا ﴿٦٢﴾

62. Akasema: Unaona! Huyu ndiye uliyemtukuza zaidi kuliko mimi? Kama utaniahirisha mpaka Siku ya Kiyama, bila shaka nitakiburuza kizazi chake isipokuwa wachache tu.

قَالَ اذْهَبْ فَمَن تَبِعَكَ مِنْهُمْ فَإِنَّ جَهَنَّمَ جَزَاؤُكُمْ جَزَاءً مَّوْفُورًا ﴿٦٣﴾

63. Akasema: Ondoka! Atakayekufuata katika wao, basi Jahannam itakuwa ndio malipo yenu, malipo yenye kutimia.

وَاسْتَفْزِزْ مَنِ اسْتَطَعْتَ مِنْهُم بِصَوْتِكَ وَأَجْلِبْ عَلَيْهِم بِخَيْلِكَ وَرَجِلِكَ وَشَارِكْهُمْ فِي الْأَمْوَالِ وَالْأَوْلَادِ وَعِدْهُمْ وَمَا يَعِدُهُمُ الشَّيْطَانُ إِلَّا غُرُورًا ﴿٦٤﴾

64. Na uwachochee uwawezao katika wao kwa sauti yako na wakusanyie jeshi lako la wapandao farasi na wendao kwa miguu na shirikiana nao katika mali na watoto na uwaahidi. Na shetani hawapi ahadi ila ya udanganyifu.

إِنَّ عِبَادِي لَيْسَ لَكَ عَلَيْهِمْ سُلْطَانٌ وَكَفَىٰ بِرَبِّكَ وَكِيلًا ﴿٦٥﴾

65. Hakika waja wangu hutakuwa na mamlaka nao, na Mola wako anatosha kuwa ni wa kutegemewa.

WAKASUJUDU

Aya 61-65

MAANA

Na tulipowaambia Malaika: Msujudieni Adam, wakamsujudia wote isipokuwa Iblis, alisema: Je, nimsujudie uliyemuumba kwa udongo?

Umepita mfano wake katika Juz. 1 (2:35) na Juz, 8 (7:11).

KUMTANGULIZA ALIYEZIDI JUU YA ALIYEZIDIWA

Akasema: Unaona! Huyu ndiye uliyemtukuza zaidi kuliko mimi?

Iblisi anahoji kwa majisifu na ufedhuli akimwambia, aliyemtukufu na kutukuka, kuwa ni nani huyo ambaye umemfadhilisha kuliko mimi? Na ni kitu gani kimemfanya awe na heshima hiyo na ukamilifu? Naona ni kinyume na hivyo:

قَالَ أَنَا خَيْرٌ مِّنْهُ خَلَقْتَنِي مِن نَّارٍ وَخَلَقْتَهُ مِن طِينٍ ﴿١٢﴾

“Akasema: Mimi ni bora kuliko yeye, umeniumba kwa moto naye umemuumba kwa udongo.” Juz; 8 (7:12).

Habithi huyu alijitia ubora kwa kutetea mantiki yake, kuwa yeye ni bora na mkamilifu; Kwa hiyo yeye hafai kumsujudia aliyemzidi.

Ibilisi amekosea katika mantiki yake haya; Kwa sabau yeye si bora kabisa kuliko Adam, bali ni kinyume. Kwahiyo Mwenyezi Mungu hakumtanguliza aliyezidiwa juu ya aliyezidi; kama alivyodai Ibilisi. Ni akili gani inayoruhusu kuwa Mwenyezi Mungu amkurubishe aliye baidi na ambaidishe aliye karibu? Lakini hakika hii imefichika kwa Ashaira[8] na Mu’tazila, waliposema kuwa inafaa kutangulizwa aliyezidiwa juu ya aliyemzidi. Tazama kitabu Al-mawqif Juzuu ya nane Uk. 373.

Wanasema Ashaira; Akili inakubali kuwa Mwenyezi Mungu atamwadhibu mtiifu na kumpa thawabu muasi, kwa sababu, kwa Mwenyezi Mungu hakuna uovu wala hana wajibu wowote. Tazama kitabu hicho hicho Uk. 195. Shia Imamiya wanasema akili haikubali kuwa Mwenyezi Mungu amwadhibu aliyefanya wema, lakini inakubali kuwa anaweza kuwasamehe waovu; sawa na mwenye haki yake, anaweza akasamehe yote au baadhi.

Wakaendelea kusema kuwa haikubaliki kiakili kutangulizwa aliyezidiwa juu ya aliyemzidi kwa sababu ni daraja ya juu na ya chini kulingana na utaratibu wa kimaumbile. Kumfanya aliyejuu kuwa yuko chini na aliye chini kuwa yuko juu ni kinyume na mantiki ya kiakili na kimaumbile.

Kama utaniahirisha mpaka siku ya kiyama, bila shaka nitakiburuza kizazi chake isipokuwa wachache tu.

Ibilisi anatishia kuchukua kisasi kwa kizazi cha Adamu; si kwa jambo lolote ila ni kwa sababu Mwenyezi Mungu amemtukuza Adamu. Anachukua kisasi kwa kuwaburuza kwenye maasi, kama vile anavyokokotwa mnyama; isipokuwa wachache tu ambao ni wale wenye ikhlasi.

Kisha Ibilisi anataka apewe muda katika maisha yake ili apoteze watu na afanye ufisadi; Mwenyezi Mungu akamkubalia maombi yake,akasema: ondoka! Atakayekufuata katika wao, basi Jahannam itakuwa ndio malipo yenu, malipo yenye kutimia.

Ibilisi alipotishia kuwapoteza wanadamu, Mwenyezi Mungu naye akamkemea yeye na wale atakaowapoteza na kumwambia: fanya utakavyo, atakufuata kwenye upotevu yule atakayetaka, kwani mimi si mlazimishi yeyote kwenye twaa na maasi. Wote ninawapa uwezo, akili na utashi na ninawabainishia njia ya kheri na njia ya shari. Ninakataza hili na kuamuru lile. Mwenye kufuata na akatii, basi pepo ni makazi yake na mwenye kuwa jeuri na akaasi basi jahannam ndio makazi ya waasi; watal- ipwa humo malipo wanayostahiki kwa ukamilifu bila ya upungufu.

Na uwachochee uwawezao katika wao kwa sauti yako na wakusanyie jeshi lako la wapandao farasi na wendao kwa miguu.

Hakuna jeshi la hakika hasa la iblisi lililo na farasi au bila ya farasi; isipokuwa ni fumbo la wafisadi, yaani watu wanaofuata hawaa, wahaini na vibaraka.

Amesema Imam Ali katika Nahjul-balagha: “Tahadharini asije aka-chochea -shetani- kwa mwito wake na kuwakusanya kwenye jeshi lake la wapanda farasi na wanaokwenda kwa miguu.” Sheikh Muhammad Abduh naye akaongezea kwa kusema: ”Anawachochea mfanye lile alitakalo, mkichelewa atawakusanyia jeshi lake la wapanda farasi na waendao kwa miguu, yaani wasaidizi wake.”

Umepita mfano wake katika Juz; 8 (7:18). Huko tumejibu maswali matatu: kuwa je, alizungumza moja kwa moja na Mwenyezi Mungu au kwa kupitia kitu kingine? Je, upotevu unatokana na Mwenyezi Mungu au na Ibilisi? Kwanini Mwenyezi Mungu akampa muda Ibilisi ili apoteze watu? Rudia huko.

Na shirikiana nao katika mali na watoto.

Kushirkiana katika mali ni fumbo la kila mali iliyopatikana kwa njia isiyokuwa ya haki; kama vile uporaji, riba, utapeli, hiyana na kuwa kibaraka. Au kuitumia isivyostahiki; kama vile kufanya israfu, kuitumia kwenye pombe, kamari na kwenye mambo ya kujionyesha. Ama kushirikiana katika watoto ni fumbo la zina, kuua watoto kwa kuhofia ufukara na aibu na kuwalea malezi ya ufisadi.

Na uwaahidi na shetani hawapi ahadi ila ya udanganyifu.

Ahadi ya udanganyifu ni kuivisha batili nguo ya haki na makosa kuyavika nguo ya usawa; kwa mfano shetani kumtia wasiwasi anayeamini Mwenyezi Mungu na siku ya mwisho, kuwa usihofie kumuasi Mwenyezi Mungu, kwani Mwenyezi Mungu ni karimu Mwingi wa maghufira, na wewe bado una umri, utatubia kesho na kuomba maghufira.

Kuna baadhi ya mapokezi yanayosema kuwa Ibilisi alimtia wasiwasi mfanya ibada mmoja katika waisrail, afanye dhambi kisha atubie ili ibada yake iwe na nguvu.

Hakika waja wangu hutakuwa na mamlaka nao, na Mola wako anatosha kuwa ni wa kutegemewa.

Umepita mfano wake katika Juz. 14 (15: 42).

رَّبُّكُمُ الَّذِي يُزْجِي لَكُمُ الْفُلْكَ فِي الْبَحْرِ لِتَبْتَغُوا مِن فَضْلِهِ إِنَّهُ كَانَ بِكُمْ رَحِيمًا ﴿٦٦﴾

66. Mola wenu ndiye anayewaendeshea majahazi, ili mtafute katika fadhila zake. Hakika Yeye ni Mwenye kuwarehemu.

وَإِذَا مَسَّكُمُ الضُّرُّ فِي الْبَحْرِ ضَلَّ مَن تَدْعُونَ إِلَّا إِيَّاهُ فَلَمَّا نَجَّاكُمْ إِلَى الْبَرِّ أَعْرَضْتُمْ وَكَانَ الْإِنسَانُ كَفُورًا ﴿٦٧﴾

67. Na inapowagusa dhara katika bahari, hao mnaowaomba wanapotea, isipokuwa Yeye tu, Anapowaokoa mkafika nchi kavu mnageuka. Na Mtu amekuwa mwingi wa kukanusha.

أَفَأَمِنتُمْ أَن يَخْسِفَ بِكُمْ جَانِبَ الْبَرِّ أَوْ يُرْسِلَ عَلَيْكُمْ حَاصِبًا ثُمَّ لَا تَجِدُوا لَكُمْ وَكِيلًا ﴿٦٨﴾

68. Je, mmeaminisha kuwa hataweza kuwadidimiza upande wa nchi kavu au kuwaletea tufani la kokoto, kisha msipate wa kutegemea?

أَمْ أَمِنتُمْ أَن يُعِيدَكُمْ فِيهِ تَارَةً أُخْرَىٰ فَيُرْسِلَ عَلَيْكُمْ قَاصِفًا مِّنَ الرِّيحِ فَيُغْرِقَكُم بِمَا كَفَرْتُمْ ثُمَّ لَا تَجِدُوا لَكُمْ عَلَيْنَا بِهِ تَبِيعًا ﴿٦٩﴾

69. Au mmeaminisha kuwa hatawarudisha humo mara nyingine awapelekee kimbunga cha upepo awazamishe kwa mlivyokufuru, kisha msipate wa kutufuatilia.

ANAWAENDESHEA MAJAHAZI

Aya 66-69

MAANA

Mola wenu ndiye anayewaendeshea majahazi, ili mtafute katika fad- hila zake. Hakika Yeye ni Mwenye kuwarehemu.

Jahazi inatembea kwenye uso wa bahari kwa sababu za kimaumbile, hilo halina shaka, lakini sababu hizi zote zinaishia kwake Mwenyezi Mungu Mtukufu. Kwa sababu yeye ni muumba wa ulimwengu na vilivyomo ndani yake.

Ni kwa sababu hii ndio ikafaa kutegemeza kuendesha kwake Yeye Mwenyezi Mungu Mtukufu. Hekima ya hilo ni kuwa mtu daima awe katika fikra ya kuwa Mwenyezi Mungu ndiye mtendaji mkuu wa vilivyomo ulimwenguni na wala sio maumbile. Ama lengo la jahazi ni kurahisisha mawasiliano.

Na inapowagusa dhara katika bahari, hao mnaowaomba wanapotea, isipokuwa Yeye tu, Anapowaokoa mkafika nchi kavu mnageuka, Na mtu amekuwa mwingi wa kukanusha.

Umepita mfano wake katika Juz. 11 (10:22).

Je, mmeaminisha kuwa hataweza kuwadidimiza upande wa nchi kavu au kuwaletea tufani la kokoto, kisha msipate wa kutegemea?

Watu wote wako mikononi mwa Mungu, popote pale walipo, hata wakiwa kwenye ngome zilizo na nguvu. Wakiwa baharini anaweza kuwangamiza kwa kufa maji, wakiwa nchi kavu anaweza kuwadidimiza ardhini au kunyweshewa na mvua ya mawe na wakiwa kwenye ngome imara anivunjilia mbali. Hawezi kujiaminisha ila mjinga.

Au mmeaminisha kuwa hatawarudisha humo mara nyingine awapelekee kimbunga cha upepo awazamishe kwa mlivyokufuru, kisha msipate wa kutufuatilia.

Humo ni baharini. Maana ni kuwa hakuna njia nyingine ya kuangamia isipokuwa baharini, basi Mwenyezi Mungu ana uwezo wa kuwarudisha humo, awazamishe kwa kimbunga na asipatikane wa kumfuatilia Mungu kwa aliyowafanyia.

Ufupi wa Aya hizo ni kuwa mjinga humhofia Mwenyezi Mungu anapokuwa na shida, lakini shida ikimuondokea anamgeuka; pamoja na kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) ni muweza wa kunufaisha na kudhuru. Ama mumin mwenye akili anapata mawaidha kwa shida na raha, anahofia haya na kutaraji msaada kwa yale.

وَلَقَدْ كَرَّمْنَا بَنِي آدَمَ وَحَمَلْنَاهُمْ فِي الْبَرِّ وَالْبَحْرِ وَرَزَقْنَاهُم مِّنَ الطَّيِّبَاتِ وَفَضَّلْنَاهُمْ عَلَىٰ كَثِيرٍ مِّمَّنْ خَلَقْنَا تَفْضِيلًا ﴿٧٠﴾

70. Hakika tumewatukuza wanaadamu na tumewabeba nchi kavu na baharini na tumewaruzuku vitu vizuri na tumewafadhilisha kwa fadhila kubwa kuliko wengi miongoni mwa tuliowaumba.

يَوْمَ نَدْعُو كُلَّ أُنَاسٍ بِإِمَامِهِمْ فَمَنْ أُوتِيَ كِتَابَهُ بِيَمِينِهِ فَأُولَـٰئِكَ يَقْرَءُونَ كِتَابَهُمْ وَلَا يُظْلَمُونَ فَتِيلًا ﴿٧١﴾

71. Siku tutakapowaita watu kwa Imam wao. Basi atakayepewa kitabu chake kwa mkono wake wa kuume, basi hao watasoma kitabu chao wala hawatadhulumiwa hata chembe.

وَمَن كَانَ فِي هَـٰذِهِ أَعْمَىٰ فَهُوَ فِي الْآخِرَةِ أَعْمَىٰ وَأَضَلُّ سَبِيلًا ﴿٧٢﴾

72. Na aliyekuwa kipofu katika hii, basi Akhera atakuwa kipofu na aliyepotea zaidi njia.

WANAADAMU TUMEWATUKUZA

Aya 70-72

MAANA

Kwanini Mwenyezi Mungu amewatukuza wanaadamu? Kabla ya kujibu swali hili, kwanza tubainishe maana ya matamshi ya Aya.

Hakika tumewatukuza wanaadamu.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) amemtukuza binadamu kwa kumpa uwezo na ujuzi uliomfanya awe ni muheshimiwa mwenye kutukuzwa. Tutataja baad- hi ya ujuzi huu na uweza baada ya kumaliza kufasiri matamshi ya Aya.

Na tumewabeba nchi kavu na baharini.

Kubebwa huku ni baadhi ya mambo aliyomtukuzwa nayo binadamu. Ni wazi kwamba kurahisishiwa mawasiliano ni katika mambo ya kuendeleza maisha watu.

Na tumewaruzuku vitu vizuri.

Kila linalomletea mtu manufaa kwa namna moja au nyingine, basi hilo ni zuri, lenye kheri na jema; liwe la kimaada au la kimaana.

Na tumewafadhilisha kwa fadhila kubwa kuliko wengi miongoni mwa tuliowaumba.

Wafasiri wengi wamesema kuwa makusudio ya wengi katika Aya ni wote. Kwa hiyo wakawaingiza Malaika, Suala hili limechukua kurasa ndefu za tafsiri; pamoja na kujua kuwa halina athari yoyote ya kiutendaji, isipokuwa kurefusha maneno.

Ilivyo hasa ni kuwa Aya iko mbali tena mbali sana na kufadhilisha baina ya binadamu na malaika. Na kwamba neno wengi linabaki kwenye dhahiri yake; kwani hakuna dharura ya kuleta taawili; bali elimu inawajibisha kubakia na dhahiri yake.

Kwani ugunduzi wa elimu umebatilisha nad- hariya isemayo kuwa ardhi ndio kituo kikuu cha ulimwengu na binaadamu ndiye bwana mkubwa wa ulimwengu wote.

Ugunduzi huu umehakikisha upotevu wa binadamu kulingana na ukubwa wa ulimwengu. Ugunduzi unathibitishwa na kukubaliwa na Qur’an, pale iliposema:

لَخَلْقُ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ أَكْبَرُ مِنْ خَلْقِ النَّاسِ وَلَـٰكِنَّ أَكْثَرَ النَّاسِ لَا يَعْلَمُونَ ﴿٥٧﴾

“Umbo la mbingu na ardhi ni kubwa kuliko umbo la watu, lakini watu wengi hawajui (40:57)

Yaani hii sayari ya ardhi ambayo anaishi binadamu ni mojwapo tu ya mamilioni ya sayari ambazo sayansi hazijui idadi yake, pamoja na kuwa imegundua mambo ambayo hayana ukomo. Zaidi ya hayo ni kwamba wataalamu wengi wanasema kuwa kuna sayari zinazokaliwa na viumbe vyenye akili pengine zaidi kuliko binadamu.

Ni kweli kuwa binadamu ni bwana mkubwa aliyetukuzwa, hilo halina shaka, lakini yeye si bwana wa viumbe vyote, bali ni mmoja tu kati ya mabwana. Hakuna jambo linalofahamisha hilo zaidi kuliko ujinga wa binadamu kwenye vitu vingi na kushindwa kwake kuvitumia, Bali hajui vitu vingi vilivyomo ardhini; sikwambii vilivyo katika sayari nyingine. Kimsingi ni kwamba sharti la kwanza la ubwana ni uwezo wa kutumia vitu.

Baada ya kufafanua matamshi ya Aya, sasa tunadokeza mambo ambayo Mwenyezi Mungu amemtukuza nayo binadamu:

1. Mwenyezi Mungu (s.w.t) amemuumba mtu akalifanya zuri umbo lake na sura yake. Mwenyezi Mungu anasema:

وَصَوَّرَكُمْ فَأَحْسَنَ صُوَرَكُمْ ﴿٦٤﴾

“Na akawatia sura na akazifanya nzuri sura zenu.” (40:64).

لَقَدْ خَلَقْنَا الْإِنسَانَ فِي أَحْسَنِ تَقْوِيمٍ ﴿٤﴾

“Hakika tumemuumba mtu katika hali nzuri sana,” (95:4).

2. Akili. Lau si hiyo, binadamu asingekuwa chochote, bali lau si akili muumba asingejulikana. Kwayo tunajua utukufu wa Mwenyezi Mungu na ukubwa wa ulimwengu na ukubwa wa akili yenyewe vilevile.

Mmoja wa wenye akili anasema: “Ikiwa ulimwenguni kuna nyota zinazomeremeta, basi ndani ya akili kuna nyota inayomeremeta na kuangaza. Ikiwa vitu vinavyotuzunguka vimepangiliwa kwa ufundi, basi akili ni kuu zaidi. Ikiwa wataalamu wa falaki wanaona kuwa mpangilio wa ndani wa ulimwengu na ukuu wake ni dalili ya ukuu wa Muumbaji, basi kuweko mtu ni dalili kubwa zaidi ya ukuu wa Mwenyezi Mungu. Ikiwa kuangalia mbin- guni kunamfanya mtu ahisi upotevu wake, basi kujifikiria mtu kunamfanya ahisi ubingwa na ukuu wa aliyemuumba na kuumba ulimwengu wote.”

Ulimwengu ni mkuu na akili ni kuu. Kitu pekee cha kujua ukuu wa Mwenyezi Mungu, ulimwengu na mtu ni akili, Lakini usisahau kuwa sio mtu tu, peke yake ndiye aliyepewa akili.

3. Mtu ana sifa na siri nyingi: elimu na ujinga, dini na kufuru, mapenzi na chuki, upole na hasira, ujasiri na hofu, ukarimu na ubakhili, unyenyekevu na kiburi, uaminfu na hiyana, uthabiti na kuwa kigeugeu na mengineyo mengi yasiyokuwa na idadi. Sijui kama ametia chumvi aliyesema: “Binadamu sio kitu kimoja isipokuwa ni mamilioni ya vitu vilivyo na akili na vilivyo na wazimu, vilivyoendelea na visivyo na maendeleo.”

4. Binadamu huwa anatafuta kuishi kwenye maisha, hata kama tayari yuko katika maisha bora, atatafuta bora zaidi. Kuna Hadith isemayo: “Lau mtu angelikuwa na mlima wa dhahabu na mwingine wa fedha, basi atatamani wa tatu.” Ikiwa binadamu yuko hivyo, basi inafaa kwake pia kuwa na hamu kubwa ya kufikia kwenye utukufu zaidi.

5. Mtu ana sharia na misimamo, ambayo ni lazima aifuate na kuitumia. Ataulizwa na kuhisabiwa; na atakuwa mtukufu au mpuuzi.

6. Mtu anaathirika kwa waliopita na yeye anawathiri wajao, wakati huo huo akiathiriana na alio nao; wanamuathiri naye anawaathiri. Ndio maana akawa ana historia, turathi na athari, ambapo viumbe vingi havina.

7. Mtu ana maisha mengine, amabyo ni uwanja wa hukumu na malipo, kutokana aliyoyafanya katika maisha yake ya kwanza, na mengineyo katika neema alizoziashiria Mwenyezi Mungu kwa kauli yake:

وَإِن تَعُدُّوا نِعْمَتَ اللَّـهِ لَا تُحْصُوهَا ﴿٣٤﴾

“Na mkihisabu neema za Mwenyezi Mungu hamwezi kuzidhibiti,” Juz;13 (14:34).

Siku tutakapowaita watu kwa Imam wao. Basi atakayepewa kitabu chake kwa mkono wake wa kulia , basi hao watasoma kitabu chao.

Imam ni yule anayefuatwa na kufutwa amri zake, Anaweza kuwa mtu, wahyi, akili au hawaa. Kuna Hadith isemayo: “Watu wataitwa Siku ya Kiyama kwa Imam wa zama zao, kitabu cha Mola wao na sunna ya nabiiwao.”

Makusudio ya kitabu katika Aya ni kitabu cha matendo ya mtu, watu wa kuume ni watu watiifu walio wema na watu wa kushoto ni waasi walio waovu.

Maana ni kuwa mnadi atanadi siku ya Kiyama: Wako wapi wafuasi wa Mitume na wa viongozi wema? Wako wapi waliotumia akili na dini? Watakuja na watachukua kitabu cha mambo wema na thawabu zake kwa mikono yao ya kuume, wakiwa na furaha.

Vilevile atanadi mnadi: wako wapi wafuasi wa madhalimu na wasaidizi wao? Wako wapi wahaini na wafisadi? Watakuja na watachukua kitabu cha maovu na adhabu yake kwa mikono yao ya kushoto wakiwa madhalili waliohizika.

Wala hawatadhulumiwa hata chembe.

Yaani Mwenyezi Mungu atamlipa kila mtu kulingana na matendo yake, hapunguzi thawabu za mwenye kufanya wema wala hazidishi adhabu ya mwenye kufanya uovu.

Na aliyekuwa kipofu katika hii, basi Akhera atakuwa kipofu na aliyepotea zaidi njia.

Katika hii, ni dunia na kipofu mbele ya Mwenyezi Mungu ni yule aliyezama kwenye ujinga. Wasifu wa fasaha zaidi katika hilo ni aliyoyasema Imam Ali(a.s) :

“Amepotelewa na makusudio, mwenye uchu wa maneno ya bid’a, mwenye kulingania upotevu. Yeye ni fitna ya mwenye kufitinika na ni mpotevu wa uongofu uliokuwa kabla yake, mpotezaji wa aliyemfuata katika uhai wake na baada ya kufa kwake”.

Kwa ufupi wa maana ya Aya hii ni kwamba ambaye amali yake imekuwa mbaya katika maisha haya, basi mwisho wake huko Akhera utakuwa mbaya. Vile vile Aya hii inafahamisha wazi kuwa thawabu au adhabu kati- ka Akhera inafungamana moja kwa moja na matendo katika maisha ya dunia.

Ndio maana ikasemwa: ‘Dunia ni shamba la Akhera.” Inatosha kuwa ni dalili kauli yake Mtume: “Watu watafufuliwa na niya zao.” Angalia Juz. 4 (3: 142).

5

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TANO

وَآتِ ذَا الْقُرْبَىٰ حَقَّهُ وَالْمِسْكِينَ وَابْنَ السَّبِيلِ وَلَا تُبَذِّرْ تَبْذِيرًا ﴿٢٦﴾

26. Na mpe jamaa wa karibu haki yake na maskini na mwana njia, wala usifanye ubadhirifu.

إِنَّ الْمُبَذِّرِينَ كَانُوا إِخْوَانَ الشَّيَاطِينِ وَكَانَ الشَّيْطَانُ لِرَبِّهِ كَفُورًا ﴿٢٧﴾

27. Hakika wabadhirifu wamekuwa ni ndugu wa mashetani, na shetani ni mwenye kumkufuru Mola wake.

وَإِمَّا تُعْرِضَنَّ عَنْهُمُ ابْتِغَاءَ رَحْمَةٍ مِّن رَّبِّكَ تَرْجُوهَا فَقُل لَّهُمْ قَوْلًا مَّيْسُورًا ﴿٢٨﴾

28. Na ikiwa unajipurukusha nao kwa kutaraji rehema ya Mola wako, basi sema nao maneno laini.

وَلَا تَجْعَلْ يَدَكَ مَغْلُولَةً إِلَىٰ عُنُقِكَ وَلَا تَبْسُطْهَا كُلَّ الْبَسْطِ فَتَقْعُدَ مَلُومًا مَّحْسُورًا ﴿٢٩﴾

29. Wala usiufanye mkono wako umefungwa shingoni mwako, wala usiunyooshe wote kabisa, utabaki mwenye kulaumiwa, mwenye kuishiwa.

إِنَّ رَبَّكَ يَبْسُطُ الرِّزْقَ لِمَن يَشَاءُ وَيَقْدِرُ إِنَّهُ كَانَ بِعِبَادِهِ خَبِيرًا بَصِيرًا ﴿٣٠﴾

30. Hakika Mola wako humkunjulia riziki amtakaye na humpimia amtakaye. Hakika Yeye kwa waja wake ni mwenye habari, aonaye.

وَلَا تَقْتُلُوا أَوْلَادَكُمْ خَشْيَةَ إِمْلَاقٍ نَّحْنُ نَرْزُقُهُمْ وَإِيَّاكُمْ إِنَّ قَتْلَهُمْ كَانَ خِطْئًا كَبِيرًا ﴿٣١﴾

31. Wala msiwaue watoto wenu kwa kuogopa kuishiwa, sisi tutawaruzuku nyinyi na wao Hakika kuwaua ni hatia kubwa.

وَلَا تَقْرَبُوا الزِّنَىٰ إِنَّهُ كَانَ فَاحِشَةً وَسَاءَ سَبِيلًا ﴿٣٢﴾

32. Wala msiikurubie zinaa; Hakika hiyo ni uchafu na njia mbaya.

وَلَا تَقْتُلُوا النَّفْسَ الَّتِي حَرَّمَ اللَّـهُ إِلَّا بِالْحَقِّ وَمَن قُتِلَ مَظْلُومًا فَقَدْ جَعَلْنَا لِوَلِيِّهِ سُلْطَانًا فَلَا يُسْرِف فِّي الْقَتْلِ إِنَّهُ كَانَ مَنصُورًا ﴿٣٣﴾

33. Wala msiiue nafsi ambayo Mwenyezi Mungu ameharamisha (kuiua), ila kwa haki. Na aliyeuliwa kwa kudhulumiwa, basi tumempa madaraka walii wake, lakini asipetuke mpaka katika kuua, kwani hakika yeye anasaidiwa.

وَلَا تَقْرَبُوا مَالَ الْيَتِيمِ إِلَّا بِالَّتِي هِيَ أَحْسَنُ حَتَّىٰ يَبْلُغَ أَشُدَّهُ وَأَوْفُوا بِالْعَهْدِ إِنَّ الْعَهْدَ كَانَ مَسْئُولًا ﴿٣٤﴾

34. Wala msiikurubie mali ya yatima isipokuwa kwa njia bora zaidi, mpaka afikie kukomaa kwake; Na tekelezeni ahadi. Hakika ahadi itasailiwa.

وَأَوْفُوا الْكَيْلَ إِذَا كِلْتُمْ وَزِنُوا بِالْقِسْطَاسِ الْمُسْتَقِيمِ ذَٰلِكَ خَيْرٌ وَأَحْسَنُ تَأْوِيلًا ﴿٣٥﴾

35. Na timizeni kipimo mnapopima, na pimeni kwa mizani zilizo sawa. Hayo ni kheri kweni na hatima njema.

وَلَا تَقْفُ مَا لَيْسَ لَكَ بِهِ عِلْمٌ إِنَّ السَّمْعَ وَالْبَصَرَ وَالْفُؤَادَ كُلُّ أُولَـٰئِكَ كَانَ عَنْهُ مَسْئُولًا ﴿٣٦﴾

36. Wala usifuatilie ambalo huna ujuzi nalo. Hakika masikio na macho na moyo, hivyo vyote vitasailiwa.

وَلَا تَمْشِ فِي الْأَرْضِ مَرَحًا إِنَّكَ لَن تَخْرِقَ الْأَرْضَ وَلَن تَبْلُغَ الْجِبَالَ طُولًا ﴿٣٧﴾

37. Wala usitembee katika Ardhi kwa maringo. Hakika wewe huwezi kuipasua ardhi wala kufikia urefu wa milima.

كُلُّ ذَٰلِكَ كَانَ سَيِّئُهُ عِندَ رَبِّكَ مَكْرُوهًا ﴿٣٨﴾

38. Hayo yote ubaya wake ni wenye kuchukiza mbele ya Mola wako.

ذَٰلِكَ مِمَّا أَوْحَىٰ إِلَيْكَ رَبُّكَ مِنَ الْحِكْمَةِ وَلَا تَجْعَلْ مَعَ اللَّـهِ إِلَـٰهًا آخَرَ فَتُلْقَىٰ فِي جَهَنَّمَ مَلُومًا مَّدْحُورًا ﴿٣٩﴾

39. Hayo ni katika hekima alizokupa wahyi Mola wako. Usimfanye mungu mwingine pamoja na Mwenyezi Mungu, usije ukalaumiwa, uliyetupwa.

WASIA 10

Aya 26 – 39

MAANA

1.Na mpe jamaa wa karibu haki yake na maskini na mwana njia wala usifanye ubadhirifu.

Amenukuu Tabrasi katika Majmaul-bayan kutoka kwa Assadiy, ambaye ni miongoni mwa wafasiri wakubwa, kwamba makusudio ya jamaa wa karibu ni jamaa wa Mtume(s.a.w.w) .

Abu Hayan Al-andalusi amenukuu kutoka kwa Imam Ali bin Husein(a.s) kwamba yeye amesema: “Hao ni jamaa wa Mtume(s.a.w.w) , Mwenyezi Mungu ameamrisha kuwapa haki yao kutoka katika hazina.

Amesema Abu Bakar Al-mua’firi Al-maliki katika Ahkamul-qur’an: “Anaingia katika jamaa wa karibu jamaa wa Mtume kuingia kwa kutangulia na kwa njia ya aula tu. Lakini hakika Aya ni ya ndugu wa mtu walio karibu zaidi. Ama jamaa wa karibu wa Mtume Mwenyezi Mungu amebainisha kuwahusu wao na akaeleza kwamba kuwapenda ndio ujira wa Mtume kwa yale aliyotuongoza.”

Imesemekana kuwa makusudio ya jamaa wa karibu ni yule ambaye ana haki ya kumtunza na kurithi, masikini ni muhitajia na mwananjia ni msafiri aliyekatikiwa njiani asiyekuwa na uwezo wa gharama za kurudi kwao. Hawa wawili wana haki ya zaka; kama alivyosema Mwenyezi Mungu:

إِنَّمَا الصَّدَقَاتُ لِلْفُقَرَاءِ وَالْمَسَاكِينِ وَالْعَامِلِينَ عَلَيْهَا وَالْمُؤَلَّفَةِ قُلُوبُهُمْ وَفِي الرِّقَابِ وَالْغَارِمِينَ وَفِي سَبِيلِ اللَّـهِ وَابْنِ السَّبِيلِ فَرِيضَةً مِّنَ اللَّـهِ وَاللَّـهُ عَلِيمٌ حَكِيمٌ ﴿٦٠﴾

“Hakika sadaka ni ya (hawa) tu: Mafukara na masikini na wanaozitumikia na wanaotiwa nguvu nyoyo zao na kuwakomboa watumwa na wenye madeni na katika njia ya Mwenyezi Mungu na mwana njia.” Juz.10 (9:60).

Hakika wabadhirifu wamekuwa ni ndugu wa mashetani, na shetani ni mwenye kumkufuru Mola wake.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) ameleta ibara ya wabadhirifu kuwa ni ndugu wa shetani, kwa sababu ubadhirifu ni jambo linalochukiwa na Mwenyezi Mungu na kila linalochukiwa na Mwenyezi Mungu linapendeza kwa shetani.

Hakuna anayetofautiana na wenzake kuwa maana ya ubadhirifu ni kutoa mali kwenye njia isiyokuwa yake na kuiweka mahali pasipokuwa pake, iwe kwa uchache au kwa wingi. Kwa ibara ya watu wa mantiki ni kwamba ubadhirifu ni katika aina si katika idadi.

Unaweza kuuliza kuwa : kauli ya isiyokuwa njia yake na pasipokuwa mahali pake inafanana na maneno yenye kutatiza ambayo yanahitaji ufafanuzi na maelezo; basi ni ipi hiyo njia yake na mahali pake?

Jibu : kila mwenye kutumia mali yake katika mambo yanayomletea madhara au yasiyokuwa na manufaa yoyote, basi huyo ni mwenye israfu, mbadhirifu na safihi, kikawaida na kisharia; isipokuwa mali anayoitoa kwa ajili ya kuvuta sigara. Tumedokeza kuhusu matumizi mabaya na kuzuiliwa kutumia matumizi ya kimali kwa mwenye kufanya hivyo, katika Juz. 4 (4:5).

WAKO WAPI WAADILIFU?

Swali la pili linaweza kuja hivi: Mtu ametumia mali yake kwa kunywa pombe, kula nyama ya nguruwe na mengineyo katika yaliyoharamishwa ambayo yanamletea manufaa ya sasa na madhara ya muda ujao. Mtu huyu watu wengi hawamuoni kuwa ni mbadhirifu wala safihi; sasa je, sharia ya kiislamu inawajibisha kuzuiliwa matumizi ya kimali, kwa vile yeye ni safihi mwenye kufanya israfu?

Jibu : Mtu mwenye akili anayo ruhusa ya kutumia mali yake bila ya kuiingiliwa; awe mumin au kafiri, fasiki au mwadilifu. Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema: “Mkiwaona wana uwekevu, basi wapeni mali zao” Juz. 4 (4:6) na wala hakusema mkiwaona wana uwekevu wa dini au uadilifu. Imepokewa Hadith Mutawatur kutoka kwa Mtume(s.a.w.w) kwamba yeye amesema: “Watu wamesalitiwa na mali zao,” na wala hakusema waumini au waadilifu.

Kwa hiyo sharti pekee la kusihi matumizi haya ni uwekevu katika mali si katika dini. Lau ingelikuwa uadilifu na uongofu ni sharti la kusihi matumizi ya mtu katika mali yake, basi nidhamu ingeliharibika na maisha yangesimama, kwa sababu watu wa duniani wako kama tunavyowajua, tutawatoa wapi watu wa dini na waadilifu?

Hanafi, Malik na Hambali wako katika rai yetu hii. Ama Shafii, wamesema kuwa uongofu ndio unaofaa katika dini na mali, kama ilivyoelezwa katika kitab Al-mughni cha Ibn Abi quddama.

Na ikiwa unajipurukusha nao kwa kutaraji rehema ya Moa wako, basi sema nao maneno laini.

Wakusema nao hapa ni jamaa wa karibu, masikini na msafiri aliyeishiwa njiani. Maana ni kuwa, akikuuliza kitu katika mali na wala usipate cha kumpa na ukamuomba Mwenyezi Mungu amtosheleze yeye na akutosheleze wewe kutokana na fadhila yake na rehema yake, basi sema naye kwa kauli laini kwa kumpa maneno mazuri yatakyompa matumaini na matarajio katika moyo wake. Kuna Hadith isemayo: “ Ikiwa hamna wasaa wa kuwapa watu mali zenu basi mnao wasaa wa kuwapa maadili yenu” Mshairi naye anasema: Kutamka kuwe kwema ikiwa hali si njema.

UISLAMU NA NADHARIA YA MAADILI

2.Wala usiufanye mkono wako umefungwa shingoni mwako, wala usiunyooshe wote kabisa, utabaki mwenye kulaumiwa, mwenye kuishiwa.

Kipimo na uwiano ndio msingi wa kila kitu katika Uislam kiitikadi, kisharia na kimaadili; sio ki ulahidi na kiidadi ya waungu. Na si kwa kuondoa milki ya mtu wala kuweka milki ya utaghuti na wala sio udikteta wa kikundi cha watu au wa mtu mmoja wala si utawala wa kila anayetaka, sio utawa wala sio kuzama kwenye matamanio. Kila kitu kinakuwa na uhalali na uharamu:

وَكُلُّ شَيْءٍ عِندَهُ بِمِقْدَارٍ ﴿٨﴾

“Na kila kitu kwake, ni kwa kipimo” Juz; 13 (13:8).

Kusema kwake ni kwa kipimo ni kuwa na nidhamu inayoafikiana na hekima na masilahi, hakuna kupetuka mpaka wala kupetusha mipaka; wala hivi hivi au kombokombo. Kila kitu kina mpaka wake mbele ya Mwenyezi Mungu ambayo ni wajibu kwa kila mtu asimame kwenye mipaka hiyo bila ya kuikeuka. Kwa mfano mipaka ya hukumu na utawala ni uadilifu; mipaka ya kumiliki ni kutomdhuru mtu au watu; mipaka ya matumizi ni kutofanya uchoyo wala kufanya ubadhirifu na matendo mengineyo.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) ameuletea ibara uchoyo kwa kufunga mkono shingoni, kwa sababu mchoyo anazuia mkono wake kutoa. Na kauli yake: ‘wala usiunyooshe wote kabisa’ anakusudia mkono ambao hauzuii kitu. Mwisho wa wote hawa wawili ni mmoja – kuishiwa na lawama.

Mwenye israfu atauma mkono wa kuishiwa, kujuta na kulaumiwa mbele ya Mwenyezi Mungu, watu na yeye mwenyewe, pale atakapokuwa mikono mitupu; wakati ambapo bakhili analaumiwa na kila mtu, na kuishiwa kwake kesho ni zaidi kuliko mbadhirifu. Jambo bora zaidi ni wastani.

Unaweza kuuliza : Je, hii ina maana Uislamu unakubaliana na nadharia ya Socrates inayosema: Kila ubora ni kati ya mabaya mawili. Kwa hiyo ushujaa ni wastani baina ya kujitutumua na woga, ukarimu ni baina ya israfu na uchoyo, unyenyekvu ni baina ya kutahayari na kukosa haya nk?

Jibu : Hapana! Kwani Uislam unapanga ubora na kuweka sharia ya hukumu kwa misingi ya masilahi ya mtu mmoja mmoja hadi watu wengi. Kila jambo ambalo linaendeleza maisha basi ni wajibu wa lazima kwa kiongozi na wajibu wa kutosheana (kifaya) kwa raia.

Na kila lenye manufaa kwa upande fulani basi ni bora; bali ni ibada ya wajibu kwa kila mwenye uweza au suna kulingana na kiwango cha manufaa. Mwenyezi Mungu anasema:

وَأَمَّا مَا يَنفَعُ النَّاسَ فَيَمْكُثُ فِي الْأَرْضِ ﴿١٧﴾

“Ama kinachowafaa watu hukaa kwenye ardhi” Juz; 13 (13:17).

Mtume(s.a.w.w) amesema: “Bora ya watu ni yule wanayenufaika naye.” Dalili wazi zaidi ya hakika hii ni kauli yake Mwenyezi Mungu: “Ambao wanamfuata Nabii asiyesoma wala kuandika ambaye wanamkuta ameandikwa kwao katika Tawrat na Injili ambaye anawaamrisha mema na anawakataza maovu, na anawahalalishia vizuri na kuwaharamishia vibaya, na kuwaondolea mizigo yao na minyororo iliyokuwa juu yao.” Juz.9 (7:157).

Msingi huu wa Qur’an – masilahi - unaweza kulingana na nadharia ya wastani kwenye vitu vyenye wastani; kama vile ukarimu kuwa baina ya uchoyo na israfu. Lakini unatofautiana katika vitu visivyo na wastani; kama vile uaminifu ni dhidi ya hiyana, wala hakuna jingine la kuleta wastani kuwa ni baina ya uaminifu na hiyana; Tumezungumzia kuhusu maadili katika Juz. 6 (5:79).

Hakika Mola wako humkunjulia riziki amtakaye na humpimia amtakaye. Hakika Yeye kwa waja wake ni mwenye habari aonaye.

Makusudio ya kumpimia ni kuifanya finyu. Kila kitu kiko mikononi mwake, riziki na zisizokuwa riziki. Kwa sababu Yeye ni mmliki wa milki zote, lakini hekima yake imetaka na kupitisha kutomruzuku yeyote isipokuwa kwa sababu za kiulimwengu ambazo ameziumba na kuziwekea njia za kuchuma mali n.k. Angalia Juz. 6(5: 66) na Juz; 13 (13: 26).

3.Wala msiwaue watoto wenu kwa kuogopa kuishiwa, sisi tutawaruzuku nyinyi na wao pia. Hakika kuwaua ni hatia kubwa.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 8 (6: 151).

4.Wala msiikurubie zinaa. Hakika hiyo ni uchafu na njia mbaya.

Imekuwa ni uchafu kwa vile mwishilio wake ni kuvurugika na kuchanganyika nasaba. Inatosha zina kuwa ni uovu kwa vile ni katika sifa mbaya za kushutumiwa.

5.Wala msiiue nafsi ambayo Mwenyezi Mungu ameharamisha (kuiua), ila kwa haki.

Umetangulia mfano wake katika katika Juz. 8 (6: 151).

Na aliyeuliwa kwa kudhulumiwa, basi tumempa madaraka walii wake, lakini asipetuke mpaka katika kuua, kwani hakika yeye anasaidiwa.

Kila aliyeuawa bila ya kufanya kosa linalowajibisha kuuliwa basi ameuawa kwa dhulma. Walii wa aliyeuawa ni ndugu zake kwa upande wa baba. Ikiwa hawako basi ni hakimu wa sharia. Kupetuka mpaka katika kuua ni kuua wawili kwa mmoja; kama walivyokuwa wakifanya wakati wa jahilia.

Maana ni kuwa ndugu wa aliyeuawa kwa dhulma wana haki ya kuua aliyeua au kuchukua fidiya; kama ilivyoelezwa katika Hadith tukufu: “Mwenye kuua basi watu wa aliyeuawa wana hiyari mbili: wakipenda wataua na wakipenda watachukua fidiya.”

Kwa vile ndugu wa aliyeuawa wana haki hiyo, basi ni wajibu wa hakimu na kila mwislamu kusaidia kutimizwa haki hii; Yametangulia maelezo kuhusu haya katika Juz. 2 (2:178).

6.Wala msiikurubie mali ya yatima isipokuwa kwa njia bora zaidi, mpaka afikie kukomaa kwake.

Imekwishapita Aya kama hii kwa herufi zake katika Juz. 8 (6: 152).

7.Na tekelezi ahadi; Hakika ahadi itasailiwa.

Kila aliloliamrisha Mwenyezi Mungu na kulikataza ni wajibu kutekelezwa; ikiwa ni pamoja na mapatano ya bei, ajira n.k. Kwa maelezo zaidi angalia Juz. 6 (5:1).

Na timizeni kipimo mnapopima na pimeni kwa mizani zilizo sawa. Hayo ni kheri kwenu na hatima njema.

Kukamilisha kipimo ni wajibu wa kisharia na kidesturi; wala hauhusiki na dini kuliko dini nyingine au desturi kuliko desturi nyingine. Mwenyezi Mungu (s.w.t) amehimiza kukamilisha kipimo kwa mifumo mbalimbali; kama vile: pimeni kwa mizani zilizo sawa, timizeni kipimo na mizani, wala msipunguze na wala msipetuke mipaka. Siri ya hilo ni kwamba ustawi wa jamii hauwezi kuwa bila ya usawa wa vipimo.

KUSEMA BILA YA UJUZI

9.Wala usifuatilie ambalo huna ujuzi nalo. Hakika masikio na macho na moyo, hivyo vyote vitasailiwa.

Neno kufuatilia limefasiriwa kutokana na neno la kiarabu Qafwa lenye maana ya kufatilia athari ya jambo. Miongoni mwa majina ya Mtume(s.a.w.w) ni Almuqfi (mfuatiliaji) kwa vile yeye ni mtume wa mwisho.

Kusema jambo bila ya ujuzi ni vibaya hata kwa yule asiyemwamini Mungu na siku ya mwisho. Mwenyezi Mungu ametaja masikio, macho na moyo akikusudia mwenye vitu hivyo vitatu.

Na kwamba Yeye Mwenyezi Mungu ataviuliza na kuviadhibu ikiwa vitawekewa vitu visivyovijua; kama vile lau mtu atasema nimesikia naye hakusikia, nimeona naye hakuona au ni ninaitakidi na kuazimia naye hana itikadi wala maazimio yoyote.

Hakuna tofauti baina ya anayekusudia uongo na anayekurupuka kusema jambo bila ya kulithibitisha. Kwani kusema kwa dhana na shubha ni kusema bila ya ujuzi. Mwenyezi Mungu (s.w.t) anasema:

إِنَّ الظَّنَّ لَا يُغْنِي مِنَ الْحَقِّ شَيْئًا ﴿٣٦﴾

“Hakika dhana haifai kitu mbele yake haki” Juz; 11 (10:36)

إِن يَتَّبِعُونَ إِلَّا الظَّنَّ ﴿١١٦﴾

“Hawafuati ila dhana na hawakuwa ila wenye kuzua tu.” Juz; 8 (6: 116)

Mwenyezi Mungu amelinganisha dhana na kuzua.

Kutokana na Aya hii yanajitokeza mambo yafuatayo:

(i) Kubatilika na uharamu wa Taqlid (kufuata) kwa yule mwenye uwezo wa kuchambua hukumu kutoka kwenye rejea zake. Kwa sababu ameacha elimu yake na akaumia elimu ya mwingine. Hii ni rai ya Shia Imamia. Zaydiya, Muu’tazila, Ibin Hazm, Sheikh Muhammad Abduh, Sheikh Shaltut na wengineo. Tumezungumza kwa ufafanuzi kuhusu taqlid katika Juz. 8 (2:259).

(ii) Uharamu wa kutoa hukumu kwa kutumia qiyas (kukisia) na istihsan (kuchukulia kuwa ni vizuri).

Qiyas ni kulinganisha jambo ambalo halikutajwa katika hukumu na jigine lililotajwa kutokana na kuwa na sababu moja.

Kwa mfano sharia kusema kuwa nyanya wa upande wa mama anarithi na ikanyamazia nyanya wa upande wa baba. Tukasema kuwa huyu pia atarithi kwa kukisia kuwa yeye pia ni nyanya.

Istihsan ilivyosimuliwa kutokana na Abu Hanifa ni kutoa hukumu kwa atavyoonelea mujtahidi kuwa ni vizuri bila ya kuweko dalili yoyote isipokuwa anavyoonelea yeye tu.

Rejea Kitabu Allami’ fi usulilfiqh cha Abu Is-haq, Ibrahim bin Ali bin Yusuf Fayruz Abadiy, uk; 65 chapa ya 1939. Mwenya kitabu hicho ametoa mfano wa mwenye kusema:

‘Nikifanya jambo fulani basi mimi ni Myahudi’ akifanya jambo hilo itabidi atoe kafara kwa kuchukulia kuwa ni kama aliyeapa kwa kusema: ‘Wallahi nikifanya jambo fulani basi mimi ni Myahudi.’

Kila mwenye kujasiri kutoa fatwa na kubainisha halali na haramu na yeye si kufu wa kufanya hivyo, basi atakuwa amesema uongo na kumzulia Mwenyezi Mungu na Mtume wake na atakuwa ni katika wale waliokusudiwa na ile Aya isemayo:

تَاللَّـهِ لَتُسْأَلُنَّ عَمَّا كُنتُمْ تَفْتَرُونَ ﴿٥٦﴾

“Wallahi! Hakika mtaulizwa hayo mliyokuwa mkiyazua” Juz; 14 (16:56)

Na kauli ya Mtume Mtukufu(s.a.w.w) : “Mwenye kunisemea uongo kwa makusudi basi na ajichagulie makazi yake motoni” Kumsemea uongo Mwenyezi Mungu na Mtume ni kutoa riwaya kutokana nao au kunasibisha halali na haramu kwao.

Siku hizi mamufti wazushi wamekuwa wengi walioifanya dini kuwa ni njia ya kutafutia riziki na pazia ya kuwa wahaini na vibaraka. Wengine wameanzisha vyama vya kutumikia uzayuni na ukoloni, lakini vina majina ya kiislamu na waislamu ili kuwahadaa na kuwapoteza watu.

Sheikh mmoja aliniuliza kuhusu wake wa Habil na Qabil kuwa je, hao ni katika hurilaini wa peponi au sio? Nikamjibu kuwa masuala haya yanaju- likana kwa kunakili sio kwa kiakili, na nukuu yake haitumiwi isipokuwa ikiwa ni ya Qur’an au Hadith mutawatir wala hakuna nukuu yoyote ya hilo. Kwa hiyo inatupasa tunyamaze yale aliyoyanyamazia Mwenyezi Mungu.

Akasema: Itakuwaje? Je, tuseme tumeshindwa tutakapoulizwa? Nikamwambia: Je, tunatakikana tujue kila kitu kwa vile sisi tuna vilemba vya ushekhe?

Wala usitembee katika Ardhi kwa maringo. Hakika wewe huwezi kuipasua ardhi wala kufikia urefu wa milima.

Mjinga anaweza kuwa na kiburi na kujifanya mkubwa anapomiliki ghururi za dunia; kama vile jaha na mali. Lakini likimtokea jambo la ghafla katika mambo yaliyojificha, basi anakuwa mnyonge na kudangana hana la kufanya. Mwenye akili ni yule anayejijua, akafikiri na kuzingatia.

Kauli yake Mwenyezi Mungu‘Wala usitembee katika Ardhi kwa maringo’ ni kukataza kiburi na kuamrisha kunyenyekea. Kauli yake:‘Hakika wewe huwezi kuipasua ardhi wala kufikia urefu wa milima’ ni fumbo la kushindwa mtu na kwamba yeye ni mdhaifu wa kufikia anayoyataka; kama alivyo mdhaifu wa mwili wake kuweza kufikilia jabali kwa urefu na kuweza kuipasua ardhi kwa wayo wake.

Hayo yote ubaya wake ni wenye kuchukiza mbele ya Mola wako.

Hayo ni kuishiria yaliyotangulia kutajwa katika yale aliyoyaamrisha Mwenyezi Mungu na kuyakataza. Makusudio ya ubaya wake ni yale aliyoyakataza hasa. Maana ni kuwa vitu vyote hivi ambavyo amevikataza Mwenyezi Mungu anavichukia, na mwenye kuvifanya ni mwenye kughadhibikiwa na Mwenyezi Mungu na mwenye kustahili adhabu.

Hayo ni katika hekima alizokupa wahyi Mola wako.

Hayo ni ishara ya maamrisho na makatazo yaliyotanglia kutajwa. Hekima ni kukiweka kitu mahali pake; Hakuna mwenye shaka kwamba hukumu zake zote Mwenyezi Mungu ziko mahali pake. Na kwamba mwenye kuichukua atakuwa ameichukua kwa haki, heri na uadilifu.

Usimfanye mungu mwingine pamoja na Mwenyezi Mungu, usije ukalaumiwa uliyetupwa.

Imetangulia Aya hii pamoja na tafsiri yake katika Sura hii Aya 22. Mwenyezi Mungu ameanzia na kukataza shirki na akamalizia nako, kwa sababu tawhid ndio kianzio na lengo la Uislamu, dini ya Mwenyezi Mungu iliyo ya haki. Kwa kuwa hukumu zote zinatoka kwake, basi hakuna halali ila aliyoiamrisha wala haramu ila aliyoiharamisha.

6

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TANO

أَفَأَصْفَاكُمْ رَبُّكُم بِالْبَنِينَ وَاتَّخَذَ مِنَ الْمَلَائِكَةِ إِنَاثًا إِنَّكُمْ لَتَقُولُونَ قَوْلًا عَظِيمًا ﴿٤٠﴾

40. Je, mola wenu amewachagulia waototo wa kiume na yeye akajichukulia watoto wa kike katika Malaika? Hakika nyinyi mnasema kauli kubwa.

وَلَقَدْ صَرَّفْنَا فِي هَـٰذَا الْقُرْآنِ لِيَذَّكَّرُوا وَمَا يَزِيدُهُمْ إِلَّا نُفُورًا ﴿٤١﴾

41. Hakika tumekwishabainisha katika Qur’an ili wapate kukumbuka, lakini haiwazidishii isipokuwa kuwa mbali.

قُل لَّوْ كَانَ مَعَهُ آلِهَةٌ كَمَا يَقُولُونَ إِذًا لَّابْتَغَوْا إِلَىٰ ذِي الْعَرْشِ سَبِيلًا ﴿٤٢﴾

42. Sema lau kama wangelikuwa pamoja naye miungu mingine, kama wasemavyo, basi wangelitafuta njia ya kumfikia Mwenye Arshi.

سُبْحَانَهُ وَتَعَالَىٰ عَمَّا يَقُولُونَ عُلُوًّا كَبِيرًا ﴿٤٣﴾

43. Ametakasika na ametukuka juu kabisa na hayo wanayoyasema.

تُسَبِّحُ لَهُ السَّمَاوَاتُ السَّبْعُ وَالْأَرْضُ وَمَن فِيهِنَّ وَإِن مِّن شَيْءٍ إِلَّا يُسَبِّحُ بِحَمْدِهِ وَلَـٰكِن لَّا تَفْقَهُونَ تَسْبِيحَهُمْ إِنَّهُ كَانَ حَلِيمًا غَفُورًا ﴿٤٤﴾

44. Zinamtakasa zote mbingu saba na ardhi na vilivyomo ndani yake. Na hapana kila kitu ila kinamtakasa kwa sifa zake, lakini nyinyi hamfahamu kutakasa kwake. Hakika Yeye ni Mpole Mwenye maghufira.

JE, MOLA WENU AMEWACHAGULIA WAVULANA?

Aya 40 – 44

MAANA

Je, mola wenu amewachagulia waototo wa kiume na yeye akajichukulia watoto wa kike katika Malaika?

Qur’an inazingatiwa kuwa ni hoja isiyokuwa na ubishi, katika yote iliyoyasema na kuyasajili; Aya hii inaelezea vile washirikina walivyokuwa wakiitakidi kwamba Mwenyezi Mungu ana mabinti katika aina ya malaika. Vile vile walikuwa wakiitakidi kwamba mtoto wa kiume ni bora kuliko wa kike; kama alivyosema Mwenyezi Mungu: “Na mmoja wao akibashiriwa msichana uso wake unasawijika naye amejaa chuki.” Juz; 14 (16:58).

Kwa hiyo basi wao walijinasibishia ubora na uduni wakamnasibishia Mungu. Ndipo Mwenyezi Mungu (s.w.t) akawatahayariza na ujinga huu, akawaambia:

Hakika nyinyi mnasema kauli kubwa , kwa sababu Yeye Mwenyezi Mungu hana mshirika wala aliyeshabihiana naye. Lau angelikuwa na mtoto angelikuwa huyo mtoto wake atamrithi na kushabihiana naye, lau angelikuwa na mzazi angelikuwa mzazi wake ni mshirika wake kwenye utukufu na enzi, bali huyo mzazi angelikuwa ni mtukufu zaidi yake, kwa sababu yeye ndiyo sababu ya kupatikana kwake.

Pengine mantiki ya wajahili ni kwamba siri iliyowafanya wamnasibishie Mungu mabinti na wao watoto wa kiume, ni kuwa Mwenyezi Mungu hahofii ufukara kwa sababu ya kuwa na watoto wengi wala aibu ya kuwa na mabinti.

Hakika tumekwishabainisha katika Qur’an ili wapate kukumbuka, lakini haiwazidishii isipokuwa kuwa mbali.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) ameweka dalili na hoja za kupatikana kwake na umoja wake na akazifafanua kwa kupiga mifano na mifumo mbalimbali ili wafahamu na waelewe, lakini wao wameng’ang’ania njozi na kuiga. Wakazidi inadi na kuwa mbali.

Razi anasema: “Hakika Mwenyezi Mungu amekithirisha kutaja dalili katika Qur’an; kwa sababu Yeye Mwenyezi Mungu Mtukufu alitaka washirikina wazifahamu na kuziamini; Hii inafahamisha kwamba Yeye, aliyetukuka, anafanya vitendo vyake kwa hekima na inafahamisha kuwa Yeye Mwenyezi Mungu Mtukufu alitaka imani kwa kila mmoja ni sawa aamini au asiamini.”

Kauli hii ya Razi inapingana na aliyoyaelezea mara kwa mara kwamba vitendo vya Mwenyezi Mungu havina sababu ya malengo, na kwamba Yeye ndiye aliyetaka kafiri awe kafiri; kama ilivyo kwa madhehebu ya Ashaira. Lakini Mwenyezi Mungu anataka kuinusuru haki na kuidhihirisha hata kwenye ulimi wa yule anayeipinga bila ya kujitambua.

Sema lau kama wangelikuwa pamoja naye miungu mingine, kama wasemavyo, basi wangelitafuta njia ya kumfikia Mwenye Arshi.

Watu wa tafsiri wametaja maana mbili za Aya hizi:

Kwanza: Ikisemwa kuwa kuna miungu wengine pamoja na Mwenyezi Mungu basi msiwahesabu hao waungu kuwa ni nyota, binadadamu, mawe au vitu vingine. Kwa sababu hivi vyote vimeumbwa na Mwenyezi Mungu, vinamwabudu na kujikurubisha kwake.

Basi mambo yakiwa hivi ni juu yenu enyi washirikiakina kumwabudu Mwenyezi Mungu; kama ambavyo vile manvyoviabudu vinamwabudu Yeye tu.

Maana au tafsiri ya pili ambayo ina nguvu zaidi ni: Lau kungelikuwa na waungu wengine, basi wangelipingana na Mwenyezi Mungu na wangelitafuta nji ya kufikia kwenye madaraka. Hakuna mwenye shaka kwamba kupingana na kuzozana viongozi kunaleta vurugu na ghasia; kama alivyosema Mwenyezi Mungu:

لَوْ كَانَ فِيهِمَا آلِهَةٌ إِلَّا اللَّـهُ لَفَسَدَتَا فَسُبْحَانَ اللَّـهِ رَبِّ الْعَرْشِ عَمَّا يَصِفُونَ ﴿٢٢﴾

“Lau wangelikuwemo humo miungu wengine isipokuwa Mwenyezi Mungu, bila shaka hizo mbingu na ardhi zingelifisidika,” (21:22).

Tumefafanua hayo katika kufasiri, Juz; 5 (5:48).

Ametakasika na ametukuka juu kabisa na hayo wanayoyasema.

Amejivua Mwenyezi Mungu (s.w.t) na kauli ya madhalimu na washiriki- na kwamba Yeye ana washirika na watoto.

KILA KITU KINAMTAKASA (KINAMSABBIH)

Zinamtakasa zote mbingu saba na ardhi na vilivyomo ndani yake. Na hapana kila kitu ila kinamtakasa kwa sifa zake.

Ndio! Kila kitu kinamtaksa na kumsifu Mwenyezi Mungu Mtukufu, hilo halina shaka. Tasbih au utakasho wa kitu unatofautiana na kitu kingine kulingana na kilivyo hicho kitu.

Mwenye akili anamtakasa na kumsifu Mwenyezi Mungu kwa ulimi wake, vitu vingine vinamtakasa kwa lugha ya hali. Kwa maneno mengine vinamtakasa na kumsifu kwa jinsi vilivyopatikana umbile lake na mpangilio wake, kuwa yuko mpangiliaji mzuri aliyevifanya viwe hivyo vilivyo; sawa na unavyojulisha mchoro mzuri kuwa mchoraji ni hodari aliye bingwa.

Lugha ya hali ina nguvu na ni fasaha zaidi kuliko lugha ya maneno. Kwa sababu ya maneno inahitajia dalili, lakini ya hali hiyo yenyewe ni dalili inayopeleka kwenye elimu na yakini; Yamekwisha tangulia maelezo ya hayo katika kufasiri Juz; 13 (13:15).

Lakini nyinyi hamfahamu kutakasa kwake; Hakika Yeye ni Mpole Mwenye maghufira.

Hawawezi kufahamu walahidi na washirikina tasbihi zao, kwa sababu ya kujiweka mbali kwao na utukufu wa Mwenyezi Mungu katika kuumba kwake au kwa sababu ya kuzembea kuchunguza na kutambua siri na maajabu ya ulimwengu.

Anasema Ibn Arabi katika kitabu Alfutuhatil-makkiyya Juz; 4: “Mwenyezi Mungu ana ishara aina kwa aina: Kuna zile zinazotambulika kwa kutumia akili, zinazotambulika kwa usikizi na zile zinazotambulika kwa kuona. Kwa hiyo ni juu ya kila mtu kutumia vyombo hivi kuweza kujua ishara za Mwenyezi Mungu ambazo amezitaja katika kitabu chake. Akishajua na kuamini kwazo na akatenda kwa mujibu wake basi atakuwa ni miongoni mwa watu wa Qur’an na watu mahususi wa Mwenyezi Mungu.”

Kisha akaendelea kusema Ibn Arabi: “Chukua kupatikana kote kuwa ni Kitabu kinachotamka haki” Hii ni kama kauli ya mmoja wa wataalamu wa elimu ya Mwenyezi Mungu: “Hakika Mwenyezi Mungu ana vitabu viwili: kimoja kinatamka kwa lugha ya makala, hicho ni Qur’an na kingine kinatamka kwa lugha ya hali nacho ni ulimwengu.”

وَإِذَا قَرَأْتَ الْقُرْآنَ جَعَلْنَا بَيْنَكَ وَبَيْنَ الَّذِينَ لَا يُؤْمِنُونَ بِالْآخِرَةِ حِجَابًا مَّسْتُورًا ﴿٤٥﴾

45. Na unaposoma Qur’an tunaweka baina yako na ya wale wasioamini Akhera pazia linalowafunika.

وَجَعَلْنَا عَلَىٰ قُلُوبِهِمْ أَكِنَّةً أَن يَفْقَهُوهُ وَفِي آذَانِهِمْ وَقْرًا وَإِذَا ذَكَرْتَ رَبَّكَ فِي الْقُرْآنِ وَحْدَهُ وَلَّوْا عَلَىٰ أَدْبَارِهِمْ نُفُورًا ﴿٤٦﴾

46. Na tunaweka vifuniko juu ya nyoyo zao wasije wakaifahamu na tunaweka kwenye masikio yao uziwi, Na unapomtaja Mola wako peke yake katika Qur’an, basi wao hugeuka nyuma wakaenda zao.

نَّحْنُ أَعْلَمُ بِمَا يَسْتَمِعُونَ بِهِ إِذْ يَسْتَمِعُونَ إِلَيْكَ وَإِذْ هُمْ نَجْوَىٰ إِذْ يَقُولُ الظَّالِمُونَ إِن تَتَّبِعُونَ إِلَّا رَجُلًا مَّسْحُورًا ﴿٤٧﴾

47. Sisi tunajua vyema kabisa sababu wanayosikilizia wanapokusikiliza, na wanaponon’gona, wanaposema hao madhalimu: nyinyi hamfuati isipokuwa mtu aliyerogwa.

انظُرْ كَيْفَ ضَرَبُوا لَكَ الْأَمْثَالَ فَضَلُّوا فَلَا يَسْتَطِيعُونَ سَبِيلًا ﴿٤٨﴾

48. Tazama vipi wanavyokupigia mfano, Basi wamepotea, kwa hiyo hawawezi kuipata njia.

UNAPOSOMA QUR’AN

Aya 45 – 48

MAANA

Na unaposoma Qur’an tunaweka baina yako na ya wale wasioamini Akhera pazia linalowafunika.

Kuna kauli nyingi katika kufasir Aya hii; Yenye nguvu zaidi ni ile isemayo kuwa jamaa katika washirikina walikuwa – Muhammad anaposoma Qur’an – wanajaribu kumzuia kwa kumuudhi, ndipo Mwenyezi Mungu (s.w.t) akamwambia endelea kusoma Qur’an na kutoa mwito wa Mwenyezi Mungu wala usichoke.

Na tunaweka vifuniko juu ya nyoyo zao wasije wakaifahamu na tunaweka kwenye masikio yao uziwi.

Hili ni fumbo la inadi ya washirikina. Ama kunasibisha vifuniko na uziwi kwa Mwenyezi Mungu (s.w.t), tumekuzungumzia kwa ufafanuzi katika kufasiri Juz; 7 (6:25). Hiyo ni mfano wa Aya hii kinukuu na kimaana.

Na unapomtaja Mola wako peke yake katika Qur’an, basi wao hugeuka nyuma wakaenda zao.

Walikuwa washirikina, inaposomwa Qur’an, wanapomsikia Mtume wa Mwenyezi Mungu akisema: Lailaha illallah (hapana Mungu isipokuwa Mwenyezi Mungu) basi wanaachana naye na kwenda zao huku wakisema:

أَجَعَلَ الْآلِهَةَ إِلَـٰهًا وَاحِدًا إِنَّ هَـٰذَا لَشَيْءٌ عُجَابٌ ﴿٥﴾ وَانطَلَقَ الْمَلَأُ مِنْهُمْ أَنِ امْشُوا وَاصْبِرُوا عَلَىٰ آلِهَتِكُمْ ﴿٦﴾

“Amewafanya miungu wote kuwa ni Mungu mmoja tu? Hakika hili ni jambo la ajabu. Na wakaondoka wakubwa wao wakiwaambia: Nenedeni zenu na dumuni na miungu yenu.” (38: 5-6).

Sio siri kuwa upinzani huu ni kwa vile tu tamko la tawhid linakusanya msingi wa kusema: “Hakika aliye mtukufu zaidi kati yenu ni yule mwenye takua zaidi” (49: 13). Sio utabaka na ubaguzi.

Sisi tunajua vyema kabisa sababu wanayosikilizia wanapokusikiliza, na wanaponon’gona, wanaposema hao madhalimu: Nyinyi hamfuati isipokuwa mtu aliyerogwa.

Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kusema: ‘na tunaweka kwenye masikio yao uziwi’ sasa anasema: Sisi tunajua vizuri kwamba wewe wakati unaposoma Qur’an washirikina hawakusikilizi kwa moyo safi, bali wanakusikiliza kwa kwa roho ya chuki, inadi na kiburi, kisha wanaambiana na pia kuwaambia wengine, kuwa Muhammad ni mchawi ameingiwa na jini linalozungumza hekima na ufasaha huu kwenye ulimi wake; itakuwaje azungumze hivi naye hajui kusoma wala kuandika, tena hana hazina ya dhahabu au fedha wala hana shamba la mitende na mizabibu.

Hii ndio fikra yao ya kitabaka, kwamba mwenye mali tu ndio anayeweza kuwa na cheo kitukufu kiwe cha dini au cha kawaida: “Na walisema: kwa nini hii Qur’an haikuteremshwa kwa mtu mkubwa katika miji miwili hii” (43:31) Ama akili, ukweli na uaminfu kwao hauna maana.

Tazama vipi wanavyokupigia mfano.

Walizidi mno kwa Muhammad(s.a.w.w) kwa vile kuwa ni Mtume wa Mwenyezi Mungu na kutamka maneno ya Mwenyezi Mungu; mara wakamwita mwendawazimu, mara mchawi, mara kuhani na mara nyingine wakamwita mshairi.

Muhammad ambaye ametumwa kukamilisha tabia njema, amekuwa mchawi na mwendawazimu? Kwa nini amekuwa hivyo? Kwa vile yeye anatamka haki na kuitolea mwito na wala hakukubaliana na matamanio ya wabatilifu na wafisadi. Zaidi ya hayo hana farasi wala mali.

Kwa ufupi ni kwamba watu wa matamanio na matakwa, hisia zao ziko upande mmoja tu, matamanio na masilahi yao binafsi. Hawasikii wala hawaoni isipokuwa kwayo tu; kiasi cha kuhalalisha yote kwenye hawa zao na matamanio. Kwa hali hii ndio tunapata tafsiri ya kauli yake Mwenyezi Mungu: “Mwenyezi Mungu amepiga muhuri juu ya nyoyo zao na juu ya masikio yao; na juu ya macho yao pana kifuniko” Juz, 1 (2:7) na tafsiri ya kila Aya iliyo na maana haya katika maneno ya Mtukufu Aliyetukuka.

Basi wamepotea, kwa hiyo hawawezi kuipata njia, ya kuwakadhibisha wenye haki, isipokuwa uzushi, upotevu, ulaghaii, uadui, njama na rushwa.

وَقَالُوا أَإِذَا كُنَّا عِظَامًا وَرُفَاتًا أَإِنَّا لَمَبْعُوثُونَ خَلْقًا جَدِيدًا ﴿٤٩﴾

49. Na wakasema: je, tutakapokuwa mifupa na mapande yaliyosagika, je tutafufuliwa kuwa viumbe wapya?

قُلْ كُونُوا حِجَارَةً أَوْ حَدِيدًا ﴿٥٠﴾

50. Sema: kuweni hata mawe au chuma.

أَوْ خَلْقًا مِّمَّا يَكْبُرُ فِي صُدُورِكُمْ فَسَيَقُولُونَ مَن يُعِيدُنَا قُلِ الَّذِي فَطَرَكُمْ أَوَّلَ مَرَّةٍ فَسَيُنْغِضُونَ إِلَيْكَ رُءُوسَهُمْ وَيَقُولُونَ مَتَىٰ هُوَ قُلْ عَسَىٰ أَن يَكُونَ قَرِيبًا ﴿٥١﴾

51. Au umbo lolote mnaloliona kubwa katika vifua vyenu, Watasema: Ni nani atakayeturudisha tena? Sema: Ni huyo aliyewaumba mara ya kwanza. Watakutikisia vichwa vyao Na watasema: lini hayo? Sema: asaa yakawa karibu.

يَوْمَ يَدْعُوكُمْ فَتَسْتَجِيبُونَ بِحَمْدِهِ وَتَظُنُّونَ إِن لَّبِثْتُمْ إِلَّا قَلِيلًا ﴿٥٢﴾

52. Siku atakayowaita nanyi mkamwitikia kwa kumsifu. Na mkadhani kuwa hamkukaa ila muda mchache tu.

TUTAKAPOKUWA MIFUPA NA MAPANDE YALIYOSAGIKA

Aya 49 – 52

MAANA

Na wakasema: je, tutakapokuwa mifupa na mapande yaliyosagika, je tutafufuliwa kuwa viumbe wapya?

Hii ndio hoja ya mwenye kutilia shaka ufufuo, tangu zamani hadi sasa, kuwa itakuwaje mtu arudi kuwa hai baada ya kuwa vumbi linalotifuka?

Jibu : Yule aliyeweza kuumba kitu na kukifanya kiwepo baada ya kuwa hakipo, basi ni wazi kuwa anaweza kukikusanya baada ya kutawanyika. Mwenyezi Mungu (s.w.t) ameitaja shaka hii na jawabu lake kwenye Aya kadhaa; miongoni mwazo ni ile iliyo katika sura Yasin:

وَضَرَبَ لَنَا مَثَلًا وَنَسِيَ خَلْقَهُ قَالَ مَن يُحْيِي الْعِظَامَ وَهِيَ رَمِيمٌ ﴿٧٨﴾ قُلْ يُحْيِيهَا الَّذِي أَنشَأَهَا أَوَّلَ مَرَّةٍ وَهُوَ بِكُلِّ خَلْقٍ عَلِيمٌ ﴿٧٩﴾

“Akasema: ni nani huyo atakayeihuisha mifupa nayo imekwisha mung’unyika? Sema: atahiuisha huyohuyo aliyeiumba mara ya kwanza na Yeye ni mjuzi wa kila kuumba” (36: 78 – 79).

Tumelifafanua suala hili katika Juz; 13 (13:5).

Sema: kuweni hata mawe na chuma au umbo lolote mnaloliona kubwa katika vifua vyenu.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) anawaambia wale wanaokanusha ufufuo kuwa hata kama mtakuwa mawe au chuma au kitu kikubwa zaidi ya hivyo tutawaumba tu kuwa watu hai.

Anayeweza kuumba kutokana na chuma au jiwe au kitu kigumu zaidi ya hivyo, basi ni muweza zaidi wa kumrudishia uhai yule aliyempa uhai mwanzo. Kwa sababu kuvikusanya vitu baada ya kutawanyika ni rahisi zaidi kuliko kuvianzisha upya.

Kwa ufupi ni kuwa kumfufua mtu baada ya kufa ni wepesi zaidi kuliko kukifanya chuma kuwa mtu, Anayeweza hivi basi hashindwi kufanya vile.

Watasema: Ni nani atakayeturudisha tena kwenye uhaai baada ya kuwa mavumbi yanayopeperuka. Jibu la swali hili ni:

Sema: Ni huyo aliyewaumba mara ya kwanza.

Mwenye kurudisha ndiye yule aliyeanza; Kuanza na kurudisha ni kumoja tu; bali kurudisha ni wepesi zaidi, kwa sababu ni kurudisha ilivyokuwa. Tunasema hivi, kama mfano tu, tukijua kuwa Mwenyezi Mungu anaumba vichache na vingi na pia vidogo na vikubwa kwa neno.

كُن فَيَكُونُ ﴿٨٢﴾

“Kuwa! Na kikawa” (36:82).

Watakutikisia vichwa vyao kwa stihzai na kukadhibishaNa watasema: lini hayo? Makusudio ya swali hili ni kuona kuwa haiwezekani.

Sema: asaa yakawa karibu. Makusudio ya karibu hapa ni kuhakikika na kutokea, kwani ‘Kila lijalo liko karibu.’

Siku atakyowaita nanyi mkamwitikia kwa kumsifu.

Makusudio ya Siku ni siku ya Ufufuo, kuitwa ni kupuziwa parapanda, kuitikia ni fumbo la kutoka kwao makaburini na kumsifu ni kutii na kufuata:

وَنُفِخَ فِي الصُّورِ فَإِذَا هُم مِّنَ الْأَجْدَاثِ إِلَىٰ رَبِّهِمْ يَنسِلُونَ ﴿٥١﴾

“Na itapulizwa parapanda mara watatoka makaburini wakikimbilia kwa Mola wao” (36:51).

Na mkadhani kuwa hamkukaa ila muda mchache tu.

Watu watakapotoka makaburini watadhani kuwa wao hawakukaa duniani isipokuwa siku moja au sehemu ya siku:

قَالَ كَمْ لَبِثْتُمْ فِي الْأَرْضِ عَدَدَ سِنِينَ ﴿١١٢﴾ قَالُوا لَبِثْنَا يَوْمًا أَوْ بَعْضَ يَوْمٍ فَاسْأَلِ الْعَادِّينَ ﴿١١٣﴾

“Atasema: mlikaa muda gani katika ardhi kwa hisabu ya miaka? Watasema tulikaa siku moja au sehemu ya siku,” (23:112- 113).


4

5

6

7

8

9