TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TANO Juzuu 15

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TANO0%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TANO Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: Qurani tukufu

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TANO

Mwandishi: Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya
: HASANI MWALUPA
Kundi:

Matembeleo: 14916
Pakua: 2117


Maelezo zaidi:

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 19 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 14916 / Pakua: 2117
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TANO

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TANO Juzuu 15

Mwandishi:
Swahili

15

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TANO

وَاضْرِبْ لَهُم مَّثَلَ الْحَيَاةِ الدُّنْيَا كَمَاءٍ أَنزَلْنَاهُ مِنَ السَّمَاءِ فَاخْتَلَطَ بِهِ نَبَاتُ الْأَرْضِ فَأَصْبَحَ هَشِيمًا تَذْرُوهُ الرِّيَاحُ وَكَانَ اللَّـهُ عَلَىٰ كُلِّ شَيْءٍ مُّقْتَدِرًا ﴿٤٥﴾

45. Na wapigie mfano wa maisha ya dunia ni kama maji tuliyoyateremsha kutoka mbinguni yakachanganyika na mimea ya ardhi ikawa majani makavu yaliyokatikakatika yanayopepeprushwa na upepo, Na Mwenyezi Mungu ana uwezo juu ya kila kitu.

الْمَالُ وَالْبَنُونَ زِينَةُ الْحَيَاةِ الدُّنْيَا وَالْبَاقِيَاتُ الصَّالِحَاتُ خَيْرٌ عِندَ رَبِّكَ ثَوَابًا وَخَيْرٌ أَمَلًا ﴿٤٦﴾

46. Mali na watoto ni pambo la maisha ya dunia. Na vibakiavyo vizuri ndivyo bora mbele ya Mola wako na kwa malipo na tumaini bora.

PAMBO LA MAISHA YA DUNIA

Aya 45 – 46

MAANA

Na wapigie mfano wa maisha ya dunia ni kama maji tuliyoyateremsha kutoka mbinguni yakachanganyika na mimea ya ardhi ikawa majani makavu yaliyokatikakatika yanayopepeprushwa na upepo.

Dunia ni nzuri yenye mandhari ya kijani ya kupendeza, lakini ina ghururi na madhara. Haina kheri katika akiba yake isipokuwa takua; kama alivyosema Imam Ali(a.s) .

Haya ndiyo maana ya Aya; ambapo Mwenyezi Mungu (s.w.t) ameifananisha dunia, katika uzuri wake, na mvua iliyonyesha kwenye ardhi ikairutubisha na ikaota miti ya kila aina, lakini mara inageuka na kuwa kame, majani yakawa makavu yanayopukusika yakirushwa na upepo. Hivi ndivyo yalivyo maisha ya dunia, ni mazuri lakini yameficha ubaya.

Na Mwenyezi Mungu ana uwezo juu ya kila kitu.

Anaweza kuuondoa ulimwengu na kuumaliza kabisa; kama alivyoweza kuumba na kuuleta. Anasema Ibnul Arabi katika kitabu Futahitl-Makkiyya “Mwenyezi Mungu ni muweza wa mambo na ana uwezo wa kuumba” Anakusudia kuwa Mwenyezi Mungu anasifika kuwa ni muweza pale anapotaka kitu kuwa kikawa, ni sawa aseme au asieme na anasifika kuwa ana uweza pale anaposema na kitu kikawa vilevile.

MALI NA WATOTO NI PAMBO LA MAISHA YA DUNIA

Mali na watoto ni pambo la maisha ya dunia.

Pambo la maisha liko aina mbili: La umma na la kibinafsi. La umma ni kama vile kujenga njia za mawasiliano; mfano barabara n.k. Au taasisi; mfano kujenga vyuo vikuu, vituo vya malezi ya watoto viwanda n.k.

Na la kibinafsi ni kama nyumba, gari, mtoto mtiifu aliyefaulu, viwanda, umaarufu katika jamii n.k. Vipambo hivi sio haramu. Vitakuwaje haramu na hali Yeye ndiye aliyesema:

قُلْ مَنْ حَرَّمَ زِينَةَ اللَّـهِ الَّتِي أَخْرَجَ لِعِبَادِهِ وَالطَّيِّبَاتِ مِنَ الرِّزْقِ ﴿٣٢﴾

“Sema: Ni nani aliyeharamisha pambo la Mwenyezi Mungu ambalo amewatolea waja wake, na vilivyo vizuri katika riziki?” Juz. 8 (7:32).

Lakini pambo binafsi halistahili mtu kujitukuza na kujifaharisha nalo. Kwa sababu kipimo cha kutukuzwa pambo ni kwa manufaa ya umma na kubakia vizazi na vizazi. Hili ndilo alilolikusudia Mwenyezi Mungu pale aliposema:

Na vibakiavyo vizuri ndivyo bora mbele ya Mola wako na kwa malipo na tumaini bora.

Kwa sababu mwenye kutekeleza atapata huko Akhera yale aliyoyatumai, mbali ya kupata heshima na kuendelea kutajika katika maisha haya ya dunia.

Kwa ufupi ni kuwa mali ni nyenzo sio lengo. Inapimwa na kukadiriwa kwa natija yake na athari yake. Ikiwa ni kheri itakuwa kheri na ikiwa ni shari basi itakuwa shari. Ikitumika kwa njia ya shari na ufisadi, kama vile mashindano ya silaha, basi itakuwa mali ni shari na ikitumika katika kutekeleza mahitaji, basi mali itkuwa ni kheri.

Na kheri hiyo iko aina mbili: Ikiwa itamletea manufaa mwenye nayo au kumkinga na madhara basi itakuwa ya binafsi na itaisha kwa kuisha. Lakini ikiwa manufaa yake ni kwa umma basi itakuwa ni katika vibakiavyo vizuri.

وَيَوْمَ نُسَيِّرُ الْجِبَالَ وَتَرَى الْأَرْضَ بَارِزَةً وَحَشَرْنَاهُمْ فَلَمْ نُغَادِرْ مِنْهُمْ أَحَدًا ﴿٤٧﴾

47. Na siku tutakayoipitisha milima na utaiona ardhi iwazi. tutawafufua wala hatuta- muacha yeyote katika wao.

وَعُرِضُوا عَلَىٰ رَبِّكَ صَفًّا لَّقَدْ جِئْتُمُونَا كَمَا خَلَقْنَاكُمْ أَوَّلَ مَرَّةٍ بَلْ زَعَمْتُمْ أَلَّن نَّجْعَلَ لَكُم مَّوْعِدًا ﴿٤٨﴾

48. Na watahudhurishwa mbele ya Mola wako kwa safu. Hakika mmetufikia kama tulivyowaumba mara ya kwanza; bali mlidai kuwa hatutawawekea miadi.

وَوُضِعَ الْكِتَابُ فَتَرَى الْمُجْرِمِينَ مُشْفِقِينَ مِمَّا فِيهِ وَيَقُولُونَ يَا وَيْلَتَنَا مَالِ هَـٰذَا الْكِتَابِ لَا يُغَادِرُ صَغِيرَةً وَلَا كَبِيرَةً إِلَّا أَحْصَاهَا وَوَجَدُوا مَا عَمِلُوا حَاضِرًا وَلَا يَظْلِمُ رَبُّكَ أَحَدًا ﴿٤٩﴾

49. Na kitabu kitawekwa ndipo utawaona waovu wakiogopa kwa sababu ya yale yaliyomo. Na watasema: “Ole wetu! Kina nini kitabu hiki hakiachi dogo wala kubwa ila kinalihesabu? Na watakuta waliyoyafanya yamehudhurishwa, Na Mola wako hadhulumu yoyote.

TUTAWAFUFUA WALA HATUTAMUACHA YEYOTE

Aya 47 -49

MAANA

Na siku tutakayoipitisha milima na utaiona ardhi i wazi.

Ardhi hii tunayoishi leo, Mwenyezi Mungu ameitaja katika Aya nyingi, miongoni mwazo ni hii tuliyo nayo. Hapa Mwenyezi Mungu ameisifu kwa sifa mbili:

Kwanza, kuwa Mwenyezi Mungu ataing’oa milima mahali ilipo na aipeleke kama mawingu, Sifa ya pili, kwamba ardhi yote kuanzia pembe hadi pembe itakuwa wazi bila ya kuweko kizuizi chochote. Hapo ndio itakuwa ufufuo ambao Mungu ameuashiria kwa kusema:

Na tutawafufua wala hatutamuacha yeyote katika wao.

Mwenyezi Mungu atawafufua wote, kuanzia wa kwanza hadi wa mwisho, kwa ajili ya hisabu.

Na watahudhurishwa mbele ya Mola wako kwa safu.

Huko nyuma tumetaja kuwa hisabu na malipo ni kweli isiyokuwa na shaka. Tumelithibitisha hilo kwa dalili mkataa, katika kufasiri Aya zinazoonyesha hivyo; miogoni mwazo ni, Juz; 11 (10:4) kifungu cha ‘Hisabu na malipo ni lazima’.

Aya tuliyo nayo inasema kuwa viumbe watahudhurishwa kwa Mungu kesho wakiwa wamepiga safu. Makusudio ya kuhudhurishwa hapa ni kusimama kwa Mungu kwa ajili ya hisabu.

Ama kuhusu neno safu, wafasiri wametofautiana; wengine wameliacha neno na dhahiri yake, wengine wakaleta sarufi na kulichukulia tamko yale yasiyowezekana. Tuonavyo sisi ni kuwa safu ni fumbo la utaratibu na nidhamu, kwamba viumbe watahudhurishwa kwa mola wao kwa mpangilio madhubuti.

Hakika mmetufikia kama tulivyowaumba mara ya kwanza; bali mlidai kuwa hatutawawekea miadi.

Hivi ndivyo atakavyoanza Mwenyezi Mungu kuwahukumu wale waliokuwa wakipinga ufufuo: Tuliwatoa matumboni mwa mama zetu mkiwa uchi hamna chochote; vilevile leo tumewatoa makaburini mwenu. Hakuna tofauti isipokuwa pale mwanzo mlikuwa hamuulizwi chochote na leo mmetolewa ili muulizwe yale mliyokuwa mkiyafanya, kuyaamini na kuyasema. Miongoni mwayo ni kusema kwenu kuwa ufufuo ni uzushi na vigano. Je, mmeona leo?

Na kitabu kitawekwa ndipo utawaona waovu wakiogopa kwa sababu ya yale yaliyomo.

Hii ndiyo Siku ya Ufufuo mliyokuwa mkiikadhibisha, Kila mmoja atapewa daftari la matendo yake na aambiwe:

اقْرَأْ كِتَابَكَ كَفَىٰ بِنَفْسِكَ الْيَوْمَ عَلَيْكَ حَسِيبًا ﴿١٤﴾

“Soma kitabu chako! Nafsi yako leo inakutosha kukuhisabu” (17:14)

Yaani soma daftari la matendo yako na ujipigie mahisabu wewe mwenyewe. Atasoma huku akitetemeka kwa hofu isiyokuwa na matumini yoyote wala matarajio ya kuokoka. Lau angeliogopa adhabu tangu mwanzo na kajiepusha na njia yake, angelikuwa leo yuko kwenye amani na sala- ma. Lakini alijiaminisha huko na anahofu hapa.

Na watasema: ole wetu! Kina nini kitabu hiki hakiachi dogo wala kubwa ila kinalihesabu?

Hapo mwanzo walikuwa wakisema hakuna kitabu wala hisabu.

Na watakuta waliyoyafanya yamehudhurishwa, bila ya kuzidi wala kupungua; Kwanini isiwe hivyona Mola wako hadhulumu yoyote ? Si kwenye thawabu wala adhabu; bali huwa zikaongezwa thawabu kwa mwenye kufanya wema na kusamehewa mwenye kufanya uovu.

وَإِذْ قُلْنَا لِلْمَلَائِكَةِ اسْجُدُوا لِآدَمَ فَسَجَدُوا إِلَّا إِبْلِيسَ كَانَ مِنَ الْجِنِّ فَفَسَقَ عَنْ أَمْرِ رَبِّهِ أَفَتَتَّخِذُونَهُ وَذُرِّيَّتَهُ أَوْلِيَاءَ مِن دُونِي وَهُمْ لَكُمْ عَدُوٌّ بِئْسَ لِلظَّالِمِينَ بَدَلًا ﴿٥٠﴾

50. Na tulipowaambia Malaika: Msujudieni Adam! Walimsujudia isipokuwa Iblis. Alikuwa miongni mwa majini akatoka kwenye amri ya Mola wake. Je, mnamfanya yeye na dhuria zake kuwa mawalii badala yangu, hali wao ni adui zenu? Ni uovu mno badala hii kwa wenye kudhulumu.

مَّا أَشْهَدتُّهُمْ خَلْقَ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ وَلَا خَلْقَ أَنفُسِهِمْ وَمَا كُنتُ مُتَّخِذَ الْمُضِلِّينَ عَضُدًا ﴿٥١﴾

51. Si kuwashuhudisha kuumbwa kwa mbingu na ardhi wala kuumbwa kwa nafsi zao. Wala sikuwafanya wapotezao kuwa ni mkono.

وَيَوْمَ يَقُولُ نَادُوا شُرَكَائِيَ الَّذِينَ زَعَمْتُمْ فَدَعَوْهُمْ فَلَمْ يَسْتَجِيبُوا لَهُمْ وَجَعَلْنَا بَيْنَهُم مَّوْبِقًا ﴿٥٢﴾

52. Na siku atakaposema waiteni hao mliodai kuwa ni washirika wangu, Basi watawaita nao hawatawaitikia. Nasi tutaweka baina yao maangamizi.

وَرَأَى الْمُجْرِمُونَ النَّارَ فَظَنُّوا أَنَّهُم مُّوَاقِعُوهَا وَلَمْ يَجِدُوا عَنْهَا مَصْرِفًا ﴿٥٣﴾

53. Na wahalifu wataona moto na watadhani kuwa wao watauingia wala hawatapata pa kuepukia.

WALISUJUDI ISIPOKUWA IBLISI

Aya 50 – 53

MAANA

Na tulipowaambia Malaika: Msujudieni Adam! Walimsujudia isipokuwa Iblis;

Umetangulia mfano wake katika Juz. 1(2:11), Juz. 8 (7:11) na Juzuu hii ya 15 (17: 61).

Alikuwa miongoni mwa majini akatoka kwenye amri ya Mola wake.

Yaani alitoka kwenye twaa ya mola wake. Mara nyingi tumesema kuwa sisi tunaamini kuweko majini, kwa sababu wahyi unathibitisha hilo na akili haipingi hilo; na kwamba ufafanuzi wake tunamwachia Mjuzi wa ghaibu.

Je, mnamfanya yeye na dhuria zake kuwa mawalii badala yangu?

Qur’an huwa inajifasiri yenyewe na sehemu moja inaitolea ushahidi sehemu nyingine. Katika Aya nyingi imeleta ibara ya kuwa wale wanaoichanganya haki na batili kuwa ni askari wa Iblisi na mawalii wake.

Kwa hiyo hapa inafaa kufasiri kuwa dhuria za Iblisi ni askari wake na wazaidizi wake na kwamba kizazi cha Ibilisi, askari wake na mawalii wake, ni wale wanaoichanganya batili na uongo na kuzulia haki. Sio mbali kwamba ibara ya kuwa hao ni dhuria za Ibilisi, ni kufanana vitendo vyao na vyake.

La kushangaza ni kauli ya asemaye kuwa Ibilisi ana tupu ya kiume katika paja lake la kuume na tupu ya kike katika paja lake la kushoto. Kwa hiyo aniingiza ya kiume kwenye hiyo ya kike na anapata kizazi na dhuria

Hali wao ni adui zenu?

Kila anayekupambapamba na kukudanganya na mambo ya batili au kukusifia mambo usiyokuwa nayo, basi huyo ni adui yako, ujue hilo au usijue.

Ama yule anayezua vigano juu ya Ibilisi na wengineo, basi huyo ni adui wa Mwenyezi Mungu na Mtume wake na pia wa ubinadamu.

Ni uovu mno badala hii kwa wenye kudhulumu.

Madhalimu ni wale wanaobadilsha twaa ya Mwenyezi Mungu kuwa twaa ya shetani; miongoni mwao ni wale wanaowachagua wafisadi kwenye vyeo na kuwafidhilisha kuliko watu wema.

Si kuwashuhudisha kuumbwa kwa mbingu na ardhi wala kuumbwa kwa nafsi zao. Wala sikuwafanya wapotezao kuwa ni mkono.

Ambao hawakushuhudishwa ni ibilisi na dhuria zake. Makusudio ya mkono hapa ni usaidizi. Maana ni kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) akilitaka jambo ni kuliambia kuwa kisha likawa, hamshauri wala hamtaki msaada yeyote, kwa sababu yeye hawahitajii walimwengu.

Na wakati alipoumba vitu hakumuhudhurisha yeyote katika wao, hata kama ni mwenye takua zaidi ya wote; sikwambii tena akiwa ni mpotezaji; kama vile Ibiisi na askari wake. Madamu mambo yako hivyo, imekuwaje kuasiwa muumbaji na kutiiwa yule ambaye hawezi kujisaidia hata yeye mwenyewe au kujikinga na madhara?

Na siku atakaposema waiteni hao mliodai kuwa ni washirika wangu, Basi watawaita nao hawatawaitikia. Nasi tutaweka baina yao maangamizi.

Maana ni kuwa Mwenyezi Mungu kesho atawaambia wale waliokuwa wakimfanyia washirika katika twaa yake: wako wapi wale ambao mliwatii na mkadai kuwa wao watawapa manufaa siku hii ya lo ngumu? Hebu waiteni tuone kama watawaitikia. Hapana! Wenyewe wana shughuli inayowashughulisha; wako katika adhabu ya moto, Kauli yake Mwenyezi Mungu kuwa watawaita na wasiwasikie ni fumbo la kukata kwao tamaa kwa matarajio waliyokuwa wakiyatarajia.

Na wahalifu wataona moto na watadhani kuwa wao watauingia wala hawatapata pa kuepukia.

Makusudio ya kudhani hapa ni kujua na kuwa na yakini. Pia kuepukia ni kuepuka na moto. Kukimbia kesho ni sawa na kujaribu kuyakimbia mauti leo hapa duniani.

وَلَقَدْ صَرَّفْنَا فِي هَـٰذَا الْقُرْآنِ لِلنَّاسِ مِن كُلِّ مَثَلٍ وَكَانَ الْإِنسَانُ أَكْثَرَ شَيْءٍ جَدَلًا ﴿٥٤﴾

54. Na hakika tumewaeleza watu katika hii Qur’an kila aina ya mifano. Lakini mtu amezidi kila kitu kwa ubishi.

وَمَا مَنَعَ النَّاسَ أَن يُؤْمِنُوا إِذْ جَاءَهُمُ الْهُدَىٰ وَيَسْتَغْفِرُوا رَبَّهُمْ إِلَّا أَن تَأْتِيَهُمْ سُنَّةُ الْأَوَّلِينَ أَوْ يَأْتِيَهُمُ الْعَذَابُ قُبُلًا ﴿٥٥﴾

55. Na hapana kilichowazuia watu kuamini ulipowajia uongofu na kuomba maghu- fira kwa Mola wao; isipokuwa yawafikie ya wale wa zamani au iwajie adhabu waziwazi.

وَمَا نُرْسِلُ الْمُرْسَلِينَ إِلَّا مُبَشِّرِينَ وَمُنذِرِينَ وَيُجَادِلُ الَّذِينَ كَفَرُوا بِالْبَاطِلِ لِيُدْحِضُوا بِهِ الْحَقَّ وَاتَّخَذُوا آيَاتِي وَمَا أُنذِرُوا هُزُوًا ﴿٥٦﴾

56. Na hatuwatumi Mitume ila wawe wabashiri na waonyaji. Na waliokufuru wanabishana kwa batili, ili waivunje haki kwayo, na wanazifanya ishara zangu na yale waliyoonywa, kuwa ni mzaha.

MTU NI MBISHI SANA

Aya 54 – 56

MAANA

Na hakika tumewaeleza watu katika hii Qur’an kila aina ya mifano, Lakini mtu amezidi kila kitu kwa ubishi.

Makusudio ya mtu hapa sio kila mtu bali ni watu wengi zaidi, kutokana na kauli yake Mwenyezi Mungu kwenye Aya kadhaa: “Watu wengi hawana akili” “watu wengi hawajui” watu wengi hawaamini” n.k. Qur’an ni kitabu cha Mwenyezi Mungu kwa waja wake, kinachowaongoza kwa dalili zake na mawaidha yake na kuhimiza kushikamana na hukumu zake na mafundisho yake.

Mwenyezi Mungu amefafanua mawaidha na dalilil hizi kwa mifumo mbalimbali na akazipigia mifano mbalimbali; ikiwemo ile ya watu wawili waliotajwa katika Aya ya 32 ya Sura hii na kufananisha maisha na maji katika Aya ya 54. lakini watu hawatii akilini na wanabishana katika mambo yaliyo wazi, wakijaribu kubatishilisha haki kwa mambo ya uongo na ya kupambamba.

Na hapana kilichowazuia watu kuamini ulipowajia uongofu na kuomba maghufira kwa Mola wao; isipokuwa yawafikie ya wale wa zamani au iwajie adhabu waziwazi.

Makusudio ya uongofu ni Qur’an na ubanifu wake ulio wazi. kuomba maghufira ni kutubia na yaliyowafikia wa zamani ni maangamivu; kama yaliyowafikia kaumu ya Nuh, Lut, A’d na Thamud.

Maana ni kuwa washirikina hawajaribu kuamni au kufikiria kuamni mpaka wapatikane na moja wapo ya mambo mawili: Kwanza ni kushukiwa na adhabu ya kuwafyeka; kama ilivyowashukia waliokuwa kabla yao; ndipo wataamni; ambapo imani, wakati huo, haifai kitu; kama Firauni ambaye aliamini alipoona maangamizi na kufa maji kunafika. Jambo la pili ni kuiona adhabu ana kwa ana.

Kwa maneno mengine ni kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) alipobainisha, katika aya zilizotangulia, kuwa Yeye ameleta dalii zilizo waziwazi na watu wengi wakakataa isipokuwa ubishi, sasa anasema kuwa dalili hizi hazifai kitu kwa watu wasioamini isipokuwa wakati wa kukata roho au wanapotishika na adhabu wanapoiona kwa macho yao au wanapoamini kuwa itawafikia tu.

Na hatuwatumi Mitume ila wawe wabashiri na waonyaji.

Huu ndio umuhimu wa Mtume kumpa habari njema ya neema yule mwenye kutii na kumuonya na adhabu yule mwenye kuasi, Maana haya yamekaririka mara nyingi. Tazama Juz. 6 (4:165).

Na waliokufuru wanabishana kwa batili, ili waivunje haki kwayo na wanazifanya ishara zangu na yale waliyoonywa, kuwa ni mzaha.

Ameziweka wazi ishara na akazithibitisha kwa ubainifu na dalili, lakini waliokufuru wakabishana na wakajaribu kuzibatilisha kwa uongo na mizaha. Makusudio ya kuzifanyia mizaha ishara za Mwenyezi Mungu hapa sio mizaha ya kusema tu; bali ni kuwa kila mweye kuijua hukumu, miogoni mwa hukumu za Mwenyezi Mungu, na asiitumie, basi yeye ni katika walioifanya Qur’an na dini ya Mwenyezi Mungu kuwa ni mchezo.

Imam Ali(a.s) anasema:“Mwenye kuisoma Qur’an, kisha akafa akaingia motoni – kwa kutoitumia Qur’an – basi huyo ni katika waliozifanyia mzaha ishara za Mwenyezi Mungu.

وَمَنْ أَظْلَمُ مِمَّن ذُكِّرَ بِآيَاتِ رَبِّهِ فَأَعْرَضَ عَنْهَا وَنَسِيَ مَا قَدَّمَتْ يَدَاهُ إِنَّا جَعَلْنَا عَلَىٰ قُلُوبِهِمْ أَكِنَّةً أَن يَفْقَهُوهُ وَفِي آذَانِهِمْ وَقْرًا وَإِن تَدْعُهُمْ إِلَى الْهُدَىٰ فَلَن يَهْتَدُوا إِذًا أَبَدًا ﴿٥٧﴾

57. Na ni nani dhalimu zaidi kuliko yule anayekumbushwa ishara za Mola wake na akazipuuza na akasahau yaliyotangulizwa na mikono yake? Hakika tumeweka vifuniko juu ya nyoyo zao wasije wakaifahamu, na tumeweka kwenye masikio yao uziwi, Na ukiwaita kwenye uongofu hawataongoka kabisa.

وَرَبُّكَ الْغَفُورُ ذُو الرَّحْمَةِ لَوْ يُؤَاخِذُهُم بِمَا كَسَبُوا لَعَجَّلَ لَهُمُ الْعَذَابَ بَل لَّهُم مَّوْعِدٌ لَّن يَجِدُوا مِن دُونِهِ مَوْئِلًا ﴿٥٨﴾

58. Na Mola wako ni mwenye maghufira na mwenye rehema, lau angeliwachukulia kwa walioyachuma, bila shaka angeliwafanyia haraka kuwaadhibu, Lakini wana miadi ambayo hawatapata kimbilio la kuepukana nayo.

وَتِلْكَ الْقُرَىٰ أَهْلَكْنَاهُمْ لَمَّا ظَلَمُوا وَجَعَلْنَا لِمَهْلِكِهِم مَّوْعِدًا ﴿٥٩﴾

59. Na miji hiyo tuliwaangamiza walipodhulumu na tukawawekea miadi ya maangamizo yao.

ALIYEKUMBUSHWA ISHARA ZA MOLA WAKE AKAZIKATAA

Aya 57 – 59

MAANA

Na ni nani dhalimu zaidi kuliko yule anayekumbushwa ishara za Mola wake na akazipuuza na akasahau yaliyotangulizwa na mikono yake?

Mwenyezi Mungu (s.w.t) ameziweka wazi dalili za kuweko kwake na wajibu wa kumtii Yeye kwa mifumo mbali mbali; kisha akapiga mifano mingi ya hayo. Akamwamrisha mtu kufanya kheri na kutubia dhambi zake zilizopita, akamkataza shari na akamuhadharisha kukhalifu amri na makatazo na kuendelea na dhambi. Lakini mtu ameyapuuza yote hayo na akaitia nafsi yake kwenye maangamivu.

Hakika tumeweka vifuniko juu ya nyoyo zao wasije wakaifahamu na tumeweka kwenye masikio yao uziwi.

Umetangula mfano wake pamoja na tafsiri katika Juz. 7 (6:25) na Juz. hii ya 15 (17: 46).

Na ukiwaita kwenye uongofu hawataongoka kabisa.

Wataongoka vipi na hali kwenye nyoyo zao kuna vifuniko na kwenye masikio yao kuna uziwi. Kila asiyenufaika na mawaidha mazuri, basi huyo ni sawa na kipofu wa moyo na macho na ni kiziwi.

Na Mola wako ni mwenye maghufira na mwenye rehema, lau angeliwachukulia kwa walioyachuma, bila shaka angeliwafanyia haraka kuwaadhibu.

Umetangula mfano wake pamoja na tafsiri katika Juz. 14 (16:61).

Lakini wana miadi ambayo hawatapata kimbilio la kuepukana nayo.

Mausudio ya miadi hapa ni wakati wa kufika mbele ya Mwenyezi Mungu, Ni miadi isiyovunjwa wala kukimbiwa.

Imam Ali (a.s) anasema kumwambia Mola wake:“Wewe ni wa milele huna muda na wewe ni mwishilio usioepukwa na wewe ni ahadi isiyokimbiwa. Uko mikononi mwako utosi wa kila mnyama na kwako ni marejeo ya kila nafsi.”

Na miji hiyo tuliwaangamiza walipodhulumu na tukawawekea miadi ya maangamizo yao.

Makusudio ya miji hapa ni ya kina A’d,Thamud na wengineo katika umma zilizopita. Maana ni kuwa Mwenyezi Mungu alijaalia wakati maalum wa kuaangamia madhalimu, ukifika hawatachelewa hata saa moja wala hawatatangulizwa.

16

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TANO

وَإِذْ قَالَ مُوسَىٰ لِفَتَاهُ لَا أَبْرَحُ حَتَّىٰ أَبْلُغَ مَجْمَعَ الْبَحْرَيْنِ أَوْ أَمْضِيَ حُقُبًا ﴿٦٠﴾

60. Na pale Musa alipomwambia kijana wake: Sitaacha kuendelea mpaka nifike makutano ya bahari mbili au nitaendelea kwa muda mrefu.

فَلَمَّا بَلَغَا مَجْمَعَ بَيْنِهِمَا نَسِيَا حُوتَهُمَا فَاتَّخَذَ سَبِيلَهُ فِي الْبَحْرِ سَرَبًا ﴿٦١﴾

61. Basi wawili hao walipofika makutano ya bahari mbili, walimsahau samaki wao, naye akashika njia yake kuponyokea baharini.

فَلَمَّا جَاوَزَا قَالَ لِفَتَاهُ آتِنَا غَدَاءَنَا لَقَدْ لَقِينَا مِن سَفَرِنَا هَـٰذَا نَصَبًا ﴿٦٢﴾

62. Waliopokwishapita alimwambia kijana wake: Tupe chakula chetu cha mchana. Kwa hakika tumepata machovu sana kwa hii safari yetu.

قَالَ أَرَأَيْتَ إِذْ أَوَيْنَا إِلَى الصَّخْرَةِ فَإِنِّي نَسِيتُ الْحُوتَ وَمَا أَنسَانِيهُ إِلَّا الشَّيْطَانُ أَنْ أَذْكُرَهُ وَاتَّخَذَ سَبِيلَهُ فِي الْبَحْرِ عَجَبًا ﴿٦٣﴾

63. Akasema: Waona! Pale tulipopumzika penye jabali basi mimi nilimsahau samaki, na hapana aliyenisahaulisha nisimkumbuke ila shetani tu. Naye akashika njia yake baharini kwa ajabu

قَالَ ذَٰلِكَ مَا كُنَّا نَبْغِ فَارْتَدَّا عَلَىٰ آثَارِهِمَا قَصَصًا ﴿٦٤﴾

64. Akasema: Hayo ndiyo tuliyokuwa tunayataka. Basi wakarudi kwa kufuata nyayo zao.

MUSA NA MAKUTANO YA BAHARI MBILI

Aya 60 – 64

LUGHA

Kijana wake, anaweza kuwa mwenzake au mtumishi wae, Makutano ya bahari mbili ni mahali zinapokutana bahari mbili na kuwa moja. Inasemekana hapo palikuwa ni makutano ya bahari nyeupe na bahari nyekundu. Kama ningekuwa mtalamu wa jografia, ningelichanganya kauli zote kisha nikachagua iliyo sahihi zaidi.

MAANA

Na pale Musa alipomwambia kijana wake: Sitacha kuendelea mpaka nifike makutano ya bahari mbili au nitaendelea kwa muda mrefu, Basi wawili hao walipofika makutano ya bahari mbili, walimsahau samaki wao, naye akashika njia yake kuponyokea baharini.

Wametofautiana kuhusu Musa, mhusika mkuu wa kisa hiki; kuwa je, ni Musa bin Imran au ni mwenginewe. Amenukuu Razi kutoka kwa Mayahudi kwamba ni Musa bin Misha bin Yusuf bin Ya’qub. Huyo ni wa mbele kuliko Musa bin Imran. Wafasiri wengi wamesema kuwa ni yule mashuhuri, Musa bin Imran, Hiyo ndiyo kauli iliyo dhahiri.

Kuhusu kijana wake, kauli iliyo maarufu ni Yoshua bin Nun, mtoto wa dada yake Musa bin Imran, mwanaafunzi wake wa karibu na khalifa wake kwa wana wa Israil. Ama yule aliyeambiwa na Musa kuwa nikufuate, kauli maarufu ni Khidhr. Lakini Mwenyezi Mungu amelinyamazia jina la kijana na la aliyemfuata. Kwa hiyo sisi tutajumlisha kwa kusema huyu ni kijana wake na yule ni swahibu wake.

Imesemekana kuwa Khidhr sio jina lake hasa bali ni msimbo. Jina lake hasa ni Fabiliya bin Malkan, Wametofautiana kuhusu kuwa je, yeye alikuwa Mtume au walii? Pia imesemekana kuwa yeye ni katika waliope- wa umri mrefu na kwamba yuko hai hadi siku ya ufufuo.

Ama sisi tunalazimika kunyamaza kuhusu utume wake na uhai wake, kwa vile hakuna dalili ya kukata shaka kutoka katika Qur’an wala Hadithi inayohusiana na mojawapo ya hayo mawili. Wala hayo hayahusiki na itikadi yetu au maisha yetu. Wengine wamesema kuwa ni Malaika. Hiyo ni kauli ya mbali sana.

Kuna riwaya inayosema kuwa mtu mmoja alimuuliza Musa: “Ni nani mwenye elimu zaidi?” Musa akasema ni mimi.

Ndipo Mwenyezi Mungu (s.w.t) akataka kumfundisha kuwa juu ya kila mjuzi kuna mjuzi zidi; Kwa hiyo akampa wahyi kwamba katika makutano ya bahari mbili kuna mtu anajua ambayo huyajui, Musa akasema nitaku- tana naye vipi? Mungu akasema, chukua samaki asiyekuwa na uhai na utakapomkosa samaki huyo, basi hapo ndio kuna huyo mjuzi.

Basi Musa akamchukua samaki na akongozana na kijana wake. Akaenda mpaka Musa akachoka, akapumzika na akapata lepe la usingizi. Wakati akiwa amelala yule samaki akapata uhai na akaingia baharini. Hii ni katika miujiza ya Mwenyezi Mungu kwa Musa.

Ikiwa riwaya hii imetegema hali halisi au imetolewa kwenye maelezo ya Aya, lakini inatoa mwanga wa Aya za kisa hiki.

Walipokwishapita alimwambia kijana wake: Tupe chakula chetu cha machana. Kwa hakika tumepata machovu sana kwa hii safari yetu.

Baada ya Musa na kijana wake kupumzika kidogo kwenye makutano ya bahari mbili, walianza upya safari yao. Mpaka wakachoka na kuhisi njaa. Musa akataka chakula kutoka kwa kijana wake. Yule kijana alishuhudia miujiza ya samaki kupata uhai na kuingia baharini, lakini akasahau kumwambia Musa. Musa alipomtaka chakula ndio akakumbuka na akasema:

Waona! Pale tulipopumzika penye jabali basi mimi nilimsahau samaki, na hapana aliyenisahaulisha nisimkumbuke ila shetani tu. Naye akashika njia yake baharini kwa ajabu.

Musa aliposikia maneno hayo akaona dalili za kupata yale aliyoyataka na akasema: Hayo ndiyo tuliyokuwa tunayataka. Basi wakarudi kwa kufuata nyayo zao. Yaani Musa na kijana wake wakarudi nyuma pale alipoingia baharini kwa kufuata ile njia yao ya kwanza.

فَوَجَدَا عَبْدًا مِّنْ عِبَادِنَا آتَيْنَاهُ رَحْمَةً مِّنْ عِندِنَا وَعَلَّمْنَاهُ مِن لَّدُنَّا عِلْمًا ﴿٦٥﴾

65. Basi wakamkuta mja miongoni mwa waja wetu tuliyempa rehema kutoka kwetu na tukamfunza elimu kutoka kwetu.

قَالَ لَهُ مُوسَىٰ هَلْ أَتَّبِعُكَ عَلَىٰ أَن تُعَلِّمَنِ مِمَّا عُلِّمْتَ رُشْدًا ﴿٦٦﴾

66. Musa akamwambia: Je, nikufuate ili unifunze katika ule uongofu uliofunzwa?

قَالَ إِنَّكَ لَن تَسْتَطِيعَ مَعِيَ صَبْرًا ﴿٦٧﴾

67. Akasema: Hakika wewe hutaweza kuvumilia kuwa pamoja nami.

وَكَيْفَ تَصْبِرُ عَلَىٰ مَا لَمْ تُحِطْ بِهِ خُبْرًا ﴿٦٨﴾

68. Na utawezaje kuvumilia yale usiyokuwa na habari nayo?

قَالَ سَتَجِدُنِي إِن شَاءَ اللَّـهُ صَابِرًا وَلَا أَعْصِي لَكَ أَمْرًا ﴿٦٩﴾

69. Akasema: Inshallah utaniona ni mvumilivu wala sitoasi amri yako.

قَالَ فَإِنِ اتَّبَعْتَنِي فَلَا تَسْأَلْنِي عَن شَيْءٍ حَتَّىٰ أُحْدِثَ لَكَ مِنْهُ ذِكْرًا ﴿٧٠﴾

70. Akasema: Basi ukinifuata, usiniulize kitu mpaka nianze kukutajia.

MUSA ANAKUTANA NA SWAHIBU YAKE

Aya 65 – 70

MAANA

Basi wakamkuta mja miongoni mwa waja wetu tuliyempa rehema kutoka kwetu na tukamfunza elimu kutoka kwetu. Musa akamwambia: Je, nikufuate ili unifunze katika ule uongofu uliofun- zwa?

Makusudio ya ‘elimu kutoka kwetu’ ni baadhi ya elimu. Na makusudio ya elimu ni elimu ya ghaibu; yaani tulimpa kitu katika elimu ya ghaibu, akiishiria hilo kwa kuitoboa safina, na kumuua kijana. Masufi wanategemea Aya hii kusahihisha madhehebu yao wanaposema elimu ya kupewa; yaani kuwa na elimu bila ya kusoma.

Maana ni kuwa Musa na kijana wake waliporudi mpaka mahali walipop- umzika mwanzo, walimkuta mtu mingoni mwa waja wema wa Mwenyezi Mungu, aliyepewa rehema na Mwenyezi Mungu na akamneemesha elimu ya kutosha yenye kunufaisha, Musa akamwamkia, naye akamrudishia salam. Musa akamuambia wewe ndiye niliyekuwa nakutaka je, utaniruhusu niandamane nawe na unifundishe uongofu uliofunzwa ninufaike nao?

Wanodai kuwa mtu huyo alikuwa Mtume, wanatoa dalii kwa kauli hii ya Mwenyezi Mungu: ‘tuliyempa rehema kutoka kwetu’ kwa sababu rehema ni utume.

Lakini wamesahau kuwa rehema inaenea kwenye mambo mengine zaidi ya utume; na kupatikana inayoenea zaidi haifahamishi kupatikana mahsusi. Ukisema nimekula tunda, haifahamishi kuwa lazima uwe umekula zabibu, inawezekana ni aina nyingine ya tunda.

Akasema: Hakika wewe hutaweza kuvumilia kuwa pamoja nami. Na utawezaje kuvumilia yale usiyokuwa na habari nayo?

Yule mtu mwema alimwambia Musa kuwa lau utafuatana nami utaonamaajabu yatakayokufanya ushindwe kunyamaza, kwa sababu, kwa dhahiri yake yataonekana kuwa ni mambo mabaya na undani wake utakuwa huujui, nawe utakuwa huwezi kuyanyamazia mambo yanayonekana kuwa ni mabaya.

Akasema Musainshallah utaniona ni mvumilivu wala sitoasi amri yako.

Musa alijitoa kwa kusema inshaalah, kuhofia asije akashindwa kujizuia; kama ilivyotokea.

Akasema: Basi ukinifuata, usiniulize kitu mpaka nianze kukutajia.

Yule mtu mwema alimpa sharti Musa kuwa asimuulize kitu kwa yale atakayoyafanya, kwa hali yoyote itakayokuwa. Musa alikubali lile sharti, kwa sababu aliondoka naye; kama unavyoonyesha ufafanuzi ufuatao:

فَانطَلَقَا حَتَّىٰ إِذَا رَكِبَا فِي السَّفِينَةِ خَرَقَهَا قَالَ أَخَرَقْتَهَا لِتُغْرِقَ أَهْلَهَا لَقَدْ جِئْتَ شَيْئًا إِمْرًا ﴿٧١﴾

71. Basi wawili hao wakaondoka, mpaka walipopanda jahazi akailtoboa, Akasema: Unalitoboa ili uwazamishe watu wake? Hakika umefanya jambo baya.

قَالَ أَلَمْ أَقُلْ إِنَّكَ لَن تَسْتَطِيعَ مَعِيَ صَبْرًا ﴿٧٢﴾

72. Akasema: Sikukuambia kuwa wewe hutaweza kuvumilia kuwa pamoja nami?

قَالَ لَا تُؤَاخِذْنِي بِمَا نَسِيتُ وَلَا تُرْهِقْنِي مِنْ أَمْرِي عُسْرًا ﴿٧٣﴾

73. Akasema: Usinichukulie kwa niliyosahau, wala usinipe uzito kwa jambo langu.

فَانطَلَقَا حَتَّىٰ إِذَا لَقِيَا غُلَامًا فَقَتَلَهُ قَالَ أَقَتَلْتَ نَفْسًا زَكِيَّةً بِغَيْرِ نَفْسٍ لَّقَدْ جِئْتَ شَيْئًا نُّكْرًا ﴿٧٤﴾

74. Basi wawili hao wakaondoka, mpaka wakamkuta kijana; akamuua. Akasema: Umemuua mtu asiye na kosa na hakuua! Hakikia umefanya jambo baya kabisa!

WAKAONDOKA

Aya 71 – 74

KUJIZUIA NA YANAYOTATIZA

Aya hizi zinafahamisha kuwa kuna mambo amabayo dhahiri ni rehema na undani wake ni adhabu na mengine ni kinyume. Na kwamba hukumu kwenye mambo ya namna hiyo ni kungoja kuyaamulia mpaka upatikane uhakika.

Imepokewa Hadithi mutawwatir, Kutoka kwa Mtume mtukufu(s.a.w.w) kuwa yeye amasema: “Halali iko wazi na haramu iko wazi na baina ya halali na haramu kuna mambo yenye kutatiza.”

Watu wengi hawajui ni halali au ni haramu. Mwenye kuyaaacha kwa kuilinda dini yake na heshima yake, atakuwa amesalimika, Na mwenye kuijingiza kwenye kitu chochote katika hivyo, basi atakuwa anakurubia kuingia katika haramu” Hadithi nyingine inasema: “Kujizuia na yenye kutatiza ni bora kuliko kujiingiza kwenye maangamizi.”

Kuna mapokezi yanayosema kwamba Luqman, mwenye hekima, aliingia kwa Daud akamkuta anatengeneza deraya, naye alikuwa hajapata kuiona. Akataka kumuuliza, lakini akaona bora angoje, Daud alipomaliza kuitengeza, aliivaa huku akisema: nguo nzuri sana hii ya vita. Akafahamu Luqman kuwa ile nguo ni ya vita. Akasema: “Kunyamaza ni hekima.”

Ni wachache sana wanoweza kuvumilia hivyo. Yule mtu mwema ameleta mambo matatu ya ushahidi wa hakika hii, kama ifuatavyo:

1.Basi wawili hao wakaondoka, mpaka walipopanda jahazi akalitoboa.

Musa alikwenda na yule mwenzake kwenye ufuo wa bahari, Walipokuta jahazi, wakamwomba mwenyewe awachukue, akakubali.

Walipofika katikati ya bahari, yule mja mwema alilitoboa, kiasi ambacho wangeweza kuzama na kufa maji. Musa akashtuka na jambo hili baya naakasema: Unalitoboa ili uwazamishe watu wake? Hakika umefanya jambo baya kabisa, Musa akachukua nguo yake akaziba ile tundu; kama wanavyodai wafasiri.

Akasema: Sikukuambia kuwa wewe hutaweza kuvumilia kuwa pamoja nami?

Hapo anamkumbusha lile sharti la kutomuuliza kitu, Musa akaomba msamaha na akasema:Usinichukulie kwa niliyosahau. Kwa sababu kusahau hakuna nenowala usinipe uzito kwa jambo langu. Yaani usinid- hikishe kwa kusuhubiana na wewe.

2.Basi wawili hao wakaondoka, mpaka wakamkuta kijana; akamuua.

Moyo wa Musa ukafazaika kutokana na mauaji,akasema: Umemuua mtu asiye na kosa na hakuua! Hakikia umefanya jambo baya. Huyu maskini amefanya nini? Unamuua bure tu. Huu ni ubaya wa wazi.

SHARTI YA KUCHAPA

Sharti ya kuchapa au kusambaza ni kutaja rejeo hili. haki zote zimehifadhiwa na Taasisi ya Al-Hasanain Taasisi ya Imamu Husein(a.s)

Site ya Al-Imaamaini Al-Hassanaini(a.s) ya usambazaji wa utamaduni wa Kiislamu na mafunzo ya Kidini.

MWISHO WA WA JUZUU YA KUMI NA TANO