TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA SITA Juzuu 16

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA SITA28%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA SITA Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: Qurani tukufu

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
  • Anza
  • Iliyopita
  • 14 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 12157 / Pakua: 4873
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA SITA

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA SITA Juzuu 16

Mwandishi:
Swahili

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA SITA

IMEANDIKWA NA: SHEIKH MUHAMMAD JAWAD MUGHNIYYA

IMETAFSIRIWA NA: SHEIKH HASAN MWALUPA

IMEHARIRIWA NA: USTADH ABDALLAH MOHAMED

IMEPANGWA KATIKA KOMPYUTA NA: UKHT PILI RAJABU

UTANGULIZI WA MCHAPISHAJI

Kitabu hiki kilichoko mikononi mwako hivi sasa ni juhudi ya miaka mingi sana ya watu waliojitolea kuona kazi hii imefanikiwa bila ya kumsahau Marhum Abu Muhammad wa London.

Kama lilivyo jina la Tafsiri ndivyo ilivyo Tafsiri yenyewe ambayo mwanachuoni huyu mahiri kabisa aliyeifafanua ni mtu aliyebobea katika fani zote ambazo mfasiri (Mfafanuzi) anatakiwa awe nazo.

Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya ameonesha cheche zake katika vitabu vingi alivyoviandika katika maudhui mbali mbalimbali na hivyo kujipatia wasomaji wengi sana.

Msomi huyu, mwenye fikra huru na anayetetea kile anachokiamini, ni mtu mwenye mawazo mapana na kuyaangalia mambo kwa undani sana, kipaumbele chake ni katika maslahi ya umma huu na amejaribu sana kwenda na wakati.

Sifa kubwa pekee ya mwanachuoni huyu ni kuwa yeye hakujihusisha sana na kung'ang'ania madhehebu fulani tu, labda hii yatokana na wadhifa wake wa ukadhi aliokuwa nao katika nchi ya Lebanon ambayo ina madhehebu mengi, ambapo sula la madhehebu ni nyeti nchini humo, hata hivyo yeye aliweza kuamua matatizo ya watu kwenye ofisi yake kulingana na madhehebu yao pale walipomwendea. Hiyo ilimsaidia sana hata kuweza kutoa kitabu kitwacho Al-Fiqh a'laa madhaahabil-khamsah (Fikhi ya madhehebu matano) yaani ya Hanafi, Maaliki, Shafi, Hambali na Shia (ambacho twataraji kitatoka kwa lugha ya kiswahili hivi karibuni Inshaallah).

Jambo lililotupa msukumo wa kukifasiri kitabu hiki kwa lugha ya Kiswahili ni zile faida nyingi atakazozipata msomaji na kujua mambo mengi na ya ajabu yaliyo mapya kwake ambayo si rahisi kuyapata kwa wafasiri wengine.

Msomaji atapata faida katika fani za Sayansi, Siasa, Historia, Mashairi, visa vizuri, na Saikolojia miongoni mwa mengine; ndiyo maana msomaji atashangaa kidogo anapoisoma Tafsiri hii atakapoona mwandishi amewataja na kuwanukuu watu kama kina Mfalme Edward, wanasayansi kama kina Enstein, wasanii kama Charlie Champlin (Mchekeshaji maarufu), na wengineo, hali inayoifanya tafsiri hii kuwa ni ya kipekee kabisa.

Mtindo alioutumia mwandishi ni sahali uliokusudiwa watu wa tabaka mbalimbali, wanavyuoni na watu wa kawaida.

Nia yetu ni kukigawanya kitabu hiki bure lakini tumelazimika kukiuza kwa bei nafuu ili kurudisha gharama za uchapishaji.

Mwisho: Shukrani kubwa iwaendee bila ya kuwataja watu waliojitolea usiku na mchana, jopo la wafasiri, wahariri, wachapaji, waliotupa moyo na kutoa maoni yao na walioisimamia ili kuhakikisha kwamba kitabu kimemfikia msomaji.

MAKOSA YA CHAPA

Sikumbuki kama nimewahi kusoma kitabu kilichotoka kupigwa chapa, cha zamani au cha sasa, bila ya kukuta makosa ya chapa, Nafikiri sitasoma kitabu kisichokuwa hivyo. Nimejaribu sana kuliepuka hilo katika tungo zangu, lakini sikufanikiwa.

Nilikuwa sifikirii kama ninaweza kuona makosa haya katika maandishi ya msahafu mtukufu, kama yale yaliyo katika baadhi ya chapa; kwa mfano neno yabswutu kwa swad, badala ya yabsutu kwa sin, na katika chapa ya Tafsir Arrazi ya Misr ya mwaka 1935, Sura ya (2:146), Imeandikwa La Ya'alamuun, (hawajui) badala ya Ya'alamuun (wanajua). Mfano wa makosa haya hausameheki.

Katika Tafsir Al-Manar, chapa ya Pili, sura (5:212), imeandikwa Fawqahum ila yawmil qiyama badala ya Fawqahum yawamal qiyama. Hatuwezi kusema kosa hili ni kubwa zaidi kuliko lile.

Lakini mkosaji atatuletea udhuru kwa msemo mashuhuri huko kwetu Jabal amil 'Makosa ya chapa.'

Katika Tafsiri Majmau chapa ya Urfan, Sura (46:15), imeandikwa: Hatta idha balagha arbai' na sanah badala ya: Hattaidha balagha ashuddahu arbai ' na sanah"

Kusema hivi sio kama ninajitetea kutokana na makosa ya chapa atakayoyakuta msomaji katika kitabu hiki, ijapokuwa naomba msamaha kama litatokea hili, lakini makusudio yangu hasa ni kumwambia yule atakayefungua macho yake kwenye makosa ya matamko na kuufungia macho uzuri wa maana.

Vilevile ninamwambia yule ambaye siku moja aliniambia: "Vitabu vyako vimejaa makosa ya chapa.” Kama kwamba hakuna kitu chochote katika vitabu hivyo isipokuwa makosa ya chapa tu. Wote hao ninawaambia: Mungu awasamehe na aniongoze mimi na nyinyi.

Vyovyote iwavyo, mimi ninaomba msamaha kutokana na makosa ya kifikra na ya chapa. Anasema Amirul Muminiin(a.s) :"Watu wote ni wapungufu wenye kuchanganyikiwa, isipokuwa yule aliyehifadhiwa na Mwenyezi Mungu." Na Mwenyezi Mungu (s.w.t) ndiye mwenye jukumu la kunikubalia yale niliyoyapatia na kunisamehe niliyakosea, kwa jaha ya Mtume na kizazi chake, ziwashukie rehema na amani (Amin).

MUHAMMAD JAWAD MUGHNIYYAH

1

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA SITA

قَالَ أَلَمْ أَقُل لَّكَ إِنَّكَ لَن تَسْتَطِيعَ مَعِيَ صَبْرًا ﴿٧٥﴾

75. Akasema: Sikukuambia kuwa wewe hutaweza kuvumilia kuwa pamoja nami?

قَالَ إِن سَأَلْتُكَ عَن شَيْءٍ بَعْدَهَا فَلَا تُصَاحِبْنِي قَدْ بَلَغْتَ مِن لَّدُنِّي عُذْرًا ﴿٧٦﴾

76. Akasema: Nikikuuliza tena kitu baada ya haya usifuatane nami kwani umekwishapata udhuru kwangu

فَانطَلَقَا حَتَّىٰ إِذَا أَتَيَا أَهْلَ قَرْيَةٍ اسْتَطْعَمَا أَهْلَهَا فَأَبَوْا أَن يُضَيِّفُوهُمَا فَوَجَدَا فِيهَا جِدَارًا يُرِيدُ أَن يَنقَضَّ فَأَقَامَهُ قَالَ لَوْ شِئْتَ لَاتَّخَذْتَ عَلَيْهِ أَجْرًا ﴿٧٧﴾

77. Basi wawili hao wakaondoka, mpaka wakawafikia watu wa mji mmoja, wakawaomba watu wake wawape chakula, nao wakakataa kuwakaribisha. Hapo wakakuta ukuta unataka kuanguka akausimamisha, Akasema (Musa): Ungelitaka ungelichukua ujira kwa haya.

قَالَ هَـٰذَا فِرَاقُ بَيْنِي وَبَيْنِكَ سَأُنَبِّئُكَ بِتَأْوِيلِ مَا لَمْ تَسْتَطِع عَّلَيْهِ صَبْرًا ﴿٧٨﴾

78. Akasema: “Huku ndio kufarikiana baina yangu na wewe. Nitakueleza taawili ya yale uliyokuwa huwezi kuyavumilia.

أَمَّا السَّفِينَةُ فَكَانَتْ لِمَسَاكِينَ يَعْمَلُونَ فِي الْبَحْرِ فَأَرَدتُّ أَنْ أَعِيبَهَا وَكَانَ وَرَاءَهُم مَّلِكٌ يَأْخُذُ كُلَّ سَفِينَةٍ غَصْبًا ﴿٧٩﴾

79. Ama ile jahazi iikuwa ni ya maskini wafanyao kazi baharini. Nilitaka kuitia kasoro, kwani nyuma yao kulikuwa na mfalme anayenyang’anya majahazi yote.

وَأَمَّا الْغُلَامُ فَكَانَ أَبَوَاهُ مُؤْمِنَيْنِ فَخَشِينَا أَن يُرْهِقَهُمَا طُغْيَانًا وَكُفْرًا ﴿٨٠﴾

80. Ama yule kijana wazazi wake walikuwa waumini, tukahofia asiwahangaishe kwa uasi na kufuru.

فَأَرَدْنَا أَن يُبْدِلَهُمَا رَبُّهُمَا خَيْرًا مِّنْهُ زَكَاةً وَأَقْرَبَ رُحْمًا ﴿٨١﴾

81. Basi tulitaka Mola wao awabadilishie aliye bora zaidi kuliko huyo kwa kutakasika na aliye karibu zaidi kwa huruma.

وَأَمَّا الْجِدَارُ فَكَانَ لِغُلَامَيْنِ يَتِيمَيْنِ فِي الْمَدِينَةِ وَكَانَ تَحْتَهُ كَنزٌ لَّهُمَا وَكَانَ أَبُوهُمَا صَالِحًا فَأَرَادَ رَبُّكَ أَن يَبْلُغَا أَشُدَّهُمَا وَيَسْتَخْرِجَا كَنزَهُمَا رَحْمَةً مِّن رَّبِّكَ وَمَا فَعَلْتُهُ عَنْ أَمْرِي ذَٰلِكَ تَأْوِيلُ مَا لَمْ تَسْطِع عَّلَيْهِ صَبْرًا ﴿٨٢﴾

82. Na ama ukuta ulikuwa ni wa vijana wawili mayatima kule mjini, na chini yake ilikuwako hazina yao, na baba yao alikuwa ni mtu mwema. Basi Mola wako alitaka wafikie kukomaa na wajitolee hazina yao. Nirehema itokayo kwa Mola wako. Hayo sikuyatenda kwa amri yangu, Hiyo ndiyo tafsiri ya ambayo hukaweza kuyavu milia.

HUWEZI KUVUMILIA

Aya 75 – 82

MAANA

Juzuu ya 15, imeishia na Aya ya kuuliwa kijana na mshangao wa Musa kwa tendo hilo. Kwenye Aya hii swahibu wa Musa anamkumbusha kuhusu walivyoahidiana:

Akasema: “Sikukuambia kuwa wewe hutaweza kuvumilia kuwa pamoja nami?

Anamkumbusha tena lile sharti na Musa naye anaomba tena msamaha akasema:Nikikuuliza tena kitu baada ya haya usifuatane nami.

Hapo mwanzo yule mtu alimuwekea sharti Musa, hivi sasa Musa anajiwekea mwenyewe sharti kwamba asisuhubiane naye tena kama atamuuliza, na waumini wanalazimiana na masharti yao; sikwambii tena mitume.

Kwani umekwishapata udhuru kwangu; Sababu zote zitakuwa zimekwisha.

Basi wawili hao wakaondoka, mpaka wakawafikia watu wa mji mmoja.

Huu ni ushahidi wa tatu wa kuwa ni wachache wanaovumilia. Ushahidi wa kwanza na wa pili umekwishapita kwenye Juzuu ya 15. Inasemekana mji huo walioufikia ni Antioch. Katika riwaya iliyopokewa kwa Imam Jafar As-Swadiq, inasema kuwa ni Nazarethi[1] .

Wakawaomba watu wake wawape chakula, lakini nao wakakataa kuwakaribisha.

Wafasiri wanasema kuwa Mwenyezi Mungu amesema walikataa kuwakaribisha, badala ya walikataa kuwapa chakula, kwa vile watu wa mji ule walikuwa wabaya sana. Kwani hakuna anayemkataa mgeni ila mtu mbaya, hasa ikiwa mgeni ni wa mbali.

Hapo wakakuta ukuta unataka kuanguka, akausimamisha.

Hapo, ni hapo kwenye mji. Aliyeusimamisha, ni yule mja mwema. Kutaka kuanguka, ni kukurubia kuanguka. Maana ni kuwa Musa na mwenzake walikuta ukuta unakaribia kuanguka, yule mwenzake akautengeneza bila ya malipo yoyote.

Ndipo Musa akastaajabu na akasema: Ungelitaka ungelichukua ujira kwa haya.

Unafanya kazi ya bure tu kwa watu waliokataa hata kutukaribisha tukiwa na shida. Kutoboa jahazi na kuua kijana ni mifano miwili yenye dhahiri ya ubaya na kusimamisha ukuta ni kinyume cha mifano hiyo miwili.

Akasema: Huku ndio kufarikiana baina yangu na wewe. Nitakueleza taawili ya yale uliyokuwa huwezi kuyavumilia.

Mja mwema alitoa sharti kwa Musa la kutoulizwa, Musa akakubali, lakini pamoja na hayo akauliza, Alipokumbushwa akaomba msamaha, Tena akauliza baada ya msamaha. Alipokumbushwa mara ya pili akajiwekea sharti yeye mwenyewe la kutofuatana naye kama atauliza tena. Lakini bado akauliza, ingawaje alikuwa na hamu sana ya kufuatana naye.

Musa hana lawama yoyote katika yote aliyoyauliza; Kwa sababu nafsi yake inaweza kuvumilia mambo ya kheri na mazuri, lakini yale anayoyaona ni mabaya, hakuweza wala hataweza kuvumilia; hata kama hilo litapelekea kuvunja masharti na maelewano. Ni kipimo gani cha masharti kinachoweza kupimwa kuacha mema na kukataza mabaya.

Imani sahihi haiwezi kuzuiwa na kitu chochote, si msukumo wa nafsi wala mengineyo. Hakuna kitu kigumu zaidi kuliko imani sahihi; na atakayeshindwa na kitu chochote katika hivyo basi hana imani sahihi; hata akiswali, kufunga na kuhiji Nyumba Tukufu ya Mwenyezi Mungu.

Huku ndio kufarikiana baina yangu na wewe , ushike njia yako nami nishike yangu, Hivyo ndivyo alivyomwambia Musa. Lakini kabla ya kutengana, yule mja mwema alimwambia Musa hekima ya yale aliyoyapinga, kama ifuatavyo:

Ama lile jahazi lilikuwa ni la maskini wafanyao kazi baharini. Nilitaka kulitia kasoro, kwani nyuma yao kulikuwa na mfalme anayenyang’anya majahazi yote.

Mwenye akili anavumilia madhara kwa ajili ya kuondoa madhara makubwa; kama anavyosema mshairi: “Nimevumilia nusu shari kihofia shari yote.”

Kuanzia hapa ndio mafaqihi wakaafikiana kuwa dhara kubwa inakingwa na dhara hafifu na yakiingiliana maovu mawili litaangaliwa lile lenye madhara zaidi kwa lile lililo na machache. Kutokana na kawaida hii wametoa hukumu nyingi, kama vile kuruhusiwa kukata kiungo ikiwa kitamletea mtu maangamizi.

Ama yule kijana wazazi wake walikuwa waumini, tukahofia asiwahangaishe kwa uasi na kufuru. Basi tulitaka Mola wao awabadilishie aliye bora zaidi kuliko huyo kwa kutakasika na aliye karibu zaidi kwa huruma.

Imepokewa riwaya kutoka kwa Imam Jafar As-Swadiq(a.s) kuwa huyo kijana aliuawa katika rika la balehe na alikuwa kafiri. Akifanya juhudi kuwaingiza wazazi wake kwenye ukafiri, sawa na wanavyofanya baadhi ya vijana wa kileo.

Tumewahi kuwona maulama wengi wa kidini waliokuwa ni tegemeo kubwa la watu, lakini mara tu walipobalehe vijana wao, wakabomoa yote waliyojenga baba zao kwa muda mrefu.

Kuna kauli mashuhuri ya Imam Ali(a.s) :“Zubeir aliendelea kuwa nasi mpaka alipokuwa na kijana wake Abdullah”

Ahmad Amin wa Misr, katika kitabu Hayati (maisha yangu), anasema: “Hivi sasa mimi na uzee wangu ninakubali kila ambalo nilikuwa nikilikataa na huwa ninaacha misimamo niliyokuwa nayo kwa sababu ya watu na mazungumzo yao na wingi wa watoto.”

• Udogo sikutaka Hawa nafsi yangu

• Zama zikakatika kawa na mvi zangu

• Hawa zikanishika kinyume matakwa yangu

• Laitani ngezalika nao ukubwa wangu

• Udogo wa marika kupinga nafsi yangu

Na ama ukuta ulikuwa ni wa vijana wawili mayatima kule mjini, na chini yake ilikuwako hazina yao, na baba yao alikuwa ni mtu mwema. Basi Mola wako alitaka wafikie kukomaa na wajitolee hazina yao. Ni rehema itokayo kwa Mola wako. Hayo sikuyatenda kwa amri yangu, Hiyo ndiyo tafsiri ya ambayo hukaweza kuyavumilia.”

Kwa ufupi ni kuwa ukuta ulikua wa watoto wawili na chini yake kulikuwa na dafina yao. Mwenyezi Mungu akataka kuilinda mali hiyo isipotee, kwa kubakia ukuta, mpaka wawe wakubwa au wawe na akili, kisha wajitolee mali yao wao wenyewe; na mzazi wao alikuwa mtu mwema “Na wema wa mtu mumini, Mwenyezi Mungu huufanya kwa mtoto wake na mtoto wa mtoto wake.”

Funzo la kisa hiki ni kwamba mtu asijione ni yeye tu na asifanye haraka kujiamulia jambo kwa kuangalia upande mmoja, bali ni lazima aangalie pande zote kwa undani na kulinganisha kisha aangalie ulio bora zaidi; kwani masilahi huwa yanasigana na madhara.

Hakuna jambo lolote la manufaa isipokuwa lina baadhi ya madhara ndani yake; kama ambavyo hakuna jambo lolote ila lina baadhi ya manufaa. Siku zote mazingatio ni kwa lililo na wingi.

وَيَسْأَلُونَكَ عَن ذِي الْقَرْنَيْنِ قُلْ سَأَتْلُو عَلَيْكُم مِّنْهُ ذِكْرًا ﴿٨٣﴾

83. Na wanakuuliza kuhusu Dhul-qarnain, Waambie nitawasimulia baadhi ya habari zake.

إِنَّا مَكَّنَّا لَهُ فِي الْأَرْضِ وَآتَيْنَاهُ مِن كُلِّ شَيْءٍ سَبَبًا ﴿٨٤﴾

84. Hakika sisi tulimmakinisha katika ardhi na tukampa sababu ya kila kitu.

فَأَتْبَعَ سَبَبًا ﴿٨٥﴾

85. Basi akafuata sababu.

حَتَّىٰ إِذَا بَلَغَ مَغْرِبَ الشَّمْسِ وَجَدَهَا تَغْرُبُ فِي عَيْنٍ حَمِئَةٍ وَوَجَدَ عِندَهَا قَوْمًا قُلْنَا يَا ذَا الْقَرْنَيْنِ إِمَّا أَن تُعَذِّبَ وَإِمَّا أَن تَتَّخِذَ فِيهِمْ حُسْنًا ﴿٨٦﴾

86. Hata alipofika machweo ya jua aliona linatua kwenye chemchem yenye matope meusi, Na hapo akawakuta watu, tukasema: Ewe Dhul-qarnain! Ama uwaadhibu au watwae kwa wema.

قَالَ أَمَّا مَن ظَلَمَ فَسَوْفَ نُعَذِّبُهُ ثُمَّ يُرَدُّ إِلَىٰ رَبِّهِ فَيُعَذِّبُهُ عَذَابًا نُّكْرًا ﴿٨٧﴾

87. Akasema: “Ama aliyedhulumu, basi tutamwadhibu adhabu na kisha atarudishwa kwa Mola wake amuadhibu adhabu isiyojulikana.

وَأَمَّا مَنْ آمَنَ وَعَمِلَ صَالِحًا فَلَهُ جَزَاءً الْحُسْنَىٰ وَسَنَقُولُ لَهُ مِنْ أَمْرِنَا يُسْرًا ﴿٨٨﴾

88. Na ama mwenye kuamini na akatenda mema tutamlipa malipo mazuri na tutamwambia lililo jepesi katika amri yetu.

ثُمَّ أَتْبَعَ سَبَبًا ﴿٨٩﴾

89. Kisha akafuata sababu.

حَتَّىٰ إِذَا بَلَغَ مَطْلِعَ الشَّمْسِ وَجَدَهَا تَطْلُعُ عَلَىٰ قَوْمٍ لَّمْ نَجْعَل لَّهُم مِّن دُونِهَا سِتْرًا ﴿٩٠﴾

90. Mpaka alipofika mawiyo ya jua aliona linawachomozea watu tusiowawekea sitara ya kuwakinga nalo.

كَذَٰلِكَ وَقَدْ أَحَطْنَا بِمَا لَدَيْهِ خُبْرًا ﴿٩١﴾

91. Kama hivyo tulizijua vizuri habari zake.

ثُمَّ أَتْبَعَ سَبَبًا ﴿٩٢﴾

92. Kisha akafuata sababu.

DHUL-QARNAIN

Aya 83 – 92

MAANA

Na wanakuuliza kuhusu Dhul- qarnain, Waambie nitawasimulia baadhi ya habari zake.

Wametofautiana kuhusu Dhul-qarnaini huyu kuwa ni nani? Ikasemekana kuwa alikuwa miongoni mwa Malaika, lakini hili ni jambo la kushangaza, Ikasemekana alikuwa Mtume.

Imepokewa kutoka kwa Imam Ali(a.s) kwamba yeye alikuwa ni mja mwema. Hakuna shaka ya wema wake, kwani vitendo vyake na kauli zake, alizozisajili Mwenyezi Mungu (s.w.t) katika kitabu chake, zinatoa ushahidi wa ubora wake na wema wake.

Pia imesemekana kuwa ni Alexandre wa Macedonia (The great Alexandre), mwanafunzi wa Aristotle. Lakini hili nalo ni la kushangaza zaidi, kwa sababu Alexandre alikuwa ni mwabudu masanamu na Dhul-qar-nain alikuwa akimwamini Mwenyezi Mungu na siku ya mwisho. Amenukuu Razi na Abu Hayyani Al-Andalusi (Mhispania), kutoka kwa Abu Rayhan Al-Biruni, kuwa Dhul-qarnaini alikuwa ni mwarabu wa Yemen kutoka kabila la Himayr na jina ake ni Abu Bakr.

Vilevile wametofautiana, kuwa kwa nini aliitwa Dhul-qarnain (mwenye pembe mbii)? Ikasemekana ni kwa kuwa yeye aikuwa ni mtukufu wa wazazi wawili.

Ikasemekana kuwa ni kwa vile alikuwa na misokoto miwili ya nywele. Pia ikasemekana ni kwa vile yeye alimiliki mashariki na magharibi na mengineyo katika kauli za kutofautiana.

Ni ajabu kwa wafasiri kujishughulisha na kuwashughulisha watu kwa jambo lisilokuwa na faida yoyote ya kidunia wala akhera. Tangu lini Qur’an ikajishughulisha na majina na sababu zake? Kama hilo lingekuwa na faida basi Qur’an isingelinyamazia.

Ni kwa ajili hii ndio sisi tukatosheka na dhahiri ya Qur’an na tunasema: watu walimuuliza Mtume mtukufu(s.a.w.w) kuhusu mtu aliyeitwa Dhul-qarnain, Mwenyezi Mungu akamwamrisha awaambie waulizaji kuwa nitawaambia baadhi ya habari zake.

Hakika sisi tulimmakinisha katika ardhi na tumpa sababu ya kila kitu

Makusudio ya kummakinisha hapa ni nguvu na utawala. Na sababu ni nyenzo zinazomfikisha mtu kwenye yale anayoyataka; kama vile elimu, uwezo, afya, mali, watu na zana. Zaidi ya hayo ni tawfiki ya Mungu na msaada wake, Nyenzo zote hizi alikuwa nazo Dhul-qarnain. Kwa hiyo akawa ni mwenye nguvu, Hii ndiyo maana ya kummakinisha katika ardhi. Aya inafahamisha waziwazi kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) analeta vitu kwa sababu zake.

Basi akafuata sababu

Mwenyezi Mungu alimwandalia njia naye akazitumia katika kheri na matendo mema. Miongoni mwazo ni kwenda kwake magharibi ambako amekuashiria Mwenyezi Mungu (s.w.t) katika kauli yake:

Hata alipofika machweo ya jua aliona linatua kwenye chemchem yenye matope meusi.

Makusudio ya machweo ya jua ni miji ya magharibi, Ni wazi kuwa jua haliwezi kuingia kwenye chemchem. Kwa hio makusudio ni chemchem yenye matope meusi ya bahari ambayo yanaonekana na watu kama Jua linatua ndani yake. Bahari hii ni miongoni mwa bahari za miji ya magharibi, lakini ni bahari gani hiyo? Mwenyezi Mungu ndiye mjuzi zaidi wa hilo. Sheikh Maraghi anasema ni bahari ya Atlantic.

Na hapo akawakuta watu, tukasema: Ewe Dhul-qarnain! Ama uwaadhibu au watwae kwa wema.

Makusudio ya hapo ni hapo kwenye chemchem. Dhahiri ya Aya, ikiwa peke yake, inafahamisha kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) alimwachia Dhul-qarnain afanye atakavyo kwa watu wa mji huo, akitaka atawaadhibu na akitaka awafanyie hisani.

Na ilivyo hasa ni kuwa jambo hilo haliafikiani na uadilifu wake Mwenyezi Mungu Mtukufu, kafiri na washirikina, ikiwa watang’ang’ania kufru na shirk, tutapata kuwa watu aliowakuta Dhul-qar-nain huko magharibi walikuwa ni makafiri na kwamba yeye aliwelezea imani wakaikataa.

Unaweza kuuliza : kuwa je, inafaa kuwafanyia wema makafiri?

Jibu : Inafaa ikiwa hawakutupiga vita kwenye dini yetu wala hawakututoa majumbani mwetu. Mwenyezi Mungu anasema:

لَّا يَنْهَاكُمُ اللَّـهُ عَنِ الَّذِينَ لَمْ يُقَاتِلُوكُمْ فِي الدِّينِ وَلَمْ يُخْرِجُوكُم مِّن دِيَارِكُمْ أَن تَبَرُّوهُمْ وَتُقْسِطُوا إِلَيْهِمْ إِنَّ اللَّـهَ يُحِبُّ الْمُقْسِطِينَ ﴿٨﴾

“Mwenyezi Mungu hawakatazi kuwafanyia wema na uadilifu wale ambao hawakupigana nanyi kwa ajili ya dini wala hawakuwafukuza katika miji yenu; Hakika Mwenyezi Mungu anawapenda wafanya uadilifu.” (60:8).

Akasema (Dhul-qarnain): Ama aliyedhulumu, basi tutamwadhibu adhabu na kisha atarudishwa kwa Mola wake amuadhibu adhabu isiyojulikana. Na ama mwenye kuamnini na akatenda mema tutamli- pa malipo mazuri na tutamwambia lililo jepesi katika amri yetu.

Hii ndio desturi ya hukumu Dhul-qarnain na utawala wake. Kwa ufupi ni kuwa, upanga ni kwa mwenye kuasi na wema ni kwa mtiifu. Hakika mali, elimu, na utawala ni neema kubwa anayowapa mtihani Mwenyezi Mungu kwayo waja wake.

Basi neema hiyo huwazidisha washari ukafiri na kupitua mipaka, lakini watu wazuri huifanya neema hiyo kuwa ni nyenzo ya kumtii Mwenyezi Mungu na kumridhisha, kama alivyofanya Dhul-qar- nain.

Kisha akafuata sababu, Yaani akafuata njia, Dhul-qarnain alirejea kutoka magharibi na akaelekea mashariki ambako Mwenyezi Mungu (s.w.t) amekuashria kwa kauli yake:

Mpaka alipofika mawiyo ya jua aliona linawachomozea watu tusiowawekea sitara ya kuwakinga nalo.

Makusudio ya mawiyo ya jua hapa ni upande wa mashariki, na sitara ni jengo na mfano wake, kama hema, vibanda na mapango. Maana ni kuwa Dhul-qarnain alipowasili miji ya mashariki aliwakuta watu wanaishi kwenye nchi iliyo wazi ikifikiwa na jua, wakiishi maisha ya kiporini, kama wanyama.

Baadhi ya wafasiri wamesema kuwa nchi hiyo ilikuwa ufuoni mwa Afrika mashariki, Mwenyezi Mungu (s.w.t) hakutaja alichofanya Dhul-qarnain huko; kuwa je alimfanyia wema mwenye kuamini na aka- tenda mema na kumwadhibu mwenye kunga’ang’ania ukafiri na inadi au aliwaacha kama walivyo? Mwenyezi Mungu ni mjuzi zaidi.

Kama hivyo tulizijua vizuri habari zake.

Yaani hii ndiyo habari ya Dhul-qarnain, tunaijua yote.

2

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA SITA

حَتَّىٰ إِذَا بَلَغَ بَيْنَ السَّدَّيْنِ وَجَدَ مِن دُونِهِمَا قَوْمًا لَّا يَكَادُونَ يَفْقَهُونَ قَوْلًا ﴿٩٣﴾

93. Hata alipofikia baina ya milima miwili, alikuta nyuma yake watu ambao takriban hawakuwa wakifahamu kauli.

قَالُوا يَا ذَا الْقَرْنَيْنِ إِنَّ يَأْجُوجَ وَمَأْجُوجَ مُفْسِدُونَ فِي الْأَرْضِ فَهَلْ نَجْعَلُ لَكَ خَرْجًا عَلَىٰ أَن تَجْعَلَ بَيْنَنَا وَبَيْنَهُمْ سَدًّا ﴿٩٤﴾

94. Wakasema: Ewe Dhul-qar-nain! Hakika Juju na Majuju wanafanya ufisadi katika nchi. Basi je, tukulipe ujira ili utujengee baina yetu na wao ngome?

قَالَ مَا مَكَّنِّي فِيهِ رَبِّي خَيْرٌ فَأَعِينُونِي بِقُوَّةٍ أَجْعَلْ بَيْنَكُمْ وَبَيْنَهُمْ رَدْمًا ﴿٩٥﴾

95. Akasema: Yale Mola wangu aliyoniwezesha ni bora. Lakini nisaidieni kwa nguvu nijenge kizuizi baina yenu na wao.

آتُونِي زُبَرَ الْحَدِيدِ حَتَّىٰ إِذَا سَاوَىٰ بَيْنَ الصَّدَفَيْنِ قَالَ انفُخُوا حَتَّىٰ إِذَا جَعَلَهُ نَارًا قَالَ آتُونِي أُفْرِغْ عَلَيْهِ قِطْرًا ﴿٩٦﴾

96. Nileteeni vipande vya chuma, Hata alipojaza baina ya nafasi iliyo kati ya milima miwili, akasema: Vuvieni. Hata alipokifanya moto akasema: Nileteeni shaba iliyoyeyuka niimwagie.

فَمَا اسْطَاعُوا أَن يَظْهَرُوهُ وَمَا اسْتَطَاعُوا لَهُ نَقْبًا ﴿٩٧﴾

97. Hawakuweza kuukwea wala hawakuweza kuutoboa.

قَالَ هَـٰذَا رَحْمَةٌ مِّن رَّبِّي فَإِذَا جَاءَ وَعْدُ رَبِّي جَعَلَهُ دَكَّاءَ وَكَانَ وَعْدُ رَبِّي حَقًّا ﴿٩٨﴾

98. Akasema: Hii ni rehema itokayo kwa Mola wangu, Itakapofika ahadi ya Mola wangu atauvunja vunja. Na ahadi ya Mola wangu ni ya kweli.

وَتَرَكْنَا بَعْضَهُمْ يَوْمَئِذٍ يَمُوجُ فِي بَعْضٍ وَنُفِخَ فِي الصُّورِ فَجَمَعْنَاهُمْ جَمْعًا ﴿٩٩﴾

99. Na siku hiyo tutawaacha wakisongana. Na parapanda itapuziwa na wote watakusanywa pamoja.

وَعَرَضْنَا جَهَنَّمَ يَوْمَئِذٍ لِّلْكَافِرِينَ عَرْضًا ﴿١٠٠﴾

100. Na siku hiyo tutawaonyesha wazi makafiri Jahannam waione.

JUJU NA MAJUJU

Aya 93 – 100

MAANA

Kisha akafuata sababu.

Dhul-qarnaini alirejea mji wa tatu ulioko katika Bahari nyeusi, unaokaliwa na Slaves[2] -kama ilivyosemekana - ambao Mwenyezi Mungu ameuashiria kwa kauli yake:

Hata alipofikia baina ya milima miwili, alikuta nyuma yake watu ambao takriban hawakuwa wakifahamu kauli.

Watu aliowakuta huko walikuwa hawafahamu lugha yake wala hakufaamu lugha yao, lakini walielewana kwa ishara au kwa mkalimani; kama anavyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu:

Wakasema: “Ewe Dhul-qar-nain! Hakika Juju na Majuju wanafanya ufisadi katika nchi. Basi je, tukulipe ujira ili utujengee baina yetu na wao ngome?

Sheikh Maraghi anasema katika Tafsir yake: “Juju ni wa Tatars, na Majuju ni wa Mongoli. Asili yao wanatokana na baba mmoja anayeitwa Turk. Miji yao inaanzia Tibet na China hadi kwenye Bahri iliyoganda. Miongoni mwao ni Changez Khan na Halako.

Kisha akanukuu Maraghi Jarida la Al-Muqtatif la mwaka 1888, kwamba jengo la ukuta wa Dhul-qarnain liko nyuma ya Amou–Daria sehemu za Balkh. Jina lake hivi sasa ni mlango wa chuma na liko karibu na mji wa Tirmidh.

Mtaalamu mmoja wa kijerumani Cyllid Burger, amelitaja katika safari zake zilizokuwa mwanzoni mwa karne ya 15. Vilevile amelitaja mwana historia wa Kihispania Clavijo katika safari zake za mwaka 1402 A.D.

Vyovyote iwavyo ni kwamba watu walimtaka Dhul-qarnain awajengee ngome itakayowakinga na Juju na Majuju waliokuwa wakiishambulia nchi yao, wakiwapa adhabu mbaya ya kuwaua, kuwateka na kupora. Wakajiwekea sharti la kumlipa katika mali zao ikiwa atawajenega ngome.

Akasema: Yale Mola wangu aliyoniwezesha na akanipa utawala na malini bora kuliko yale aliyowapa Mwenyezi Mungu. Nyinyi wenyewe mna haja kubwa ya mali yenu, basi itumieni kwenye masilahi yenu.

Lakini nisaidieni kwa nguvu nijenge kizuizi baina yenu na wao.

Makusudio ya nguvu hapa ni wafanyikazi na vifaa vya ujenzi.

Nileteeni vipande vya chuma. Hata alipojaza baina ya nafasi iliyo kati ya milima miwili.

Yaani alipoletewa vyuma alivipanga mpaka vikajaza nafasi iliyo baina ya milima miwili, kisha wakamletea kuni akawasha moto akaweka mifuoakasema: Vuvieni. Hata alipokifanya (chuma)moto akasema: Nileteeni shaba iliyoyeyuka niimwagie.

Wakamletea, akamwagia kwenye vyuma vilivyo moto, vikashikana, ukawa mlima wa chuma.

Hawakuweza kuukwea hao Juju na Majuju, kutokana na urefu na kutelezawala hawakuweza kuutoboa kutokana na ugumu wake na maki yake.

Akasema: Hii ni rehema itokayo kwa Mola wangu.

Aliyesema ni Dhul-qarnain, akimshukuru Mola wake (s.w.t) kwa rehema na neema hii aliyoitimiza mikononi mwake, Hivi ndivyo anavyokuwa mumin mwenye ikhlasi. Anamnyenyekea Mwenyezi Mungu na kushukuru kila zinapokuwa neema za Mwenyezi Mungu kupitia kwake.

Kujengwa kwa ngome hii ni usadikisho wa mfano kuwa katika historia ya binadamu kulikuwa na kusaidiana baina ya mataifa makubwa na yale madogo yanayoendelea; baina ya taifa lililo na nyenzo za maendeleo na lile lisilokuwa nazo.

Nguvu za Amerika zinafanana sana na nguvu za Dhul-qarnaini, kwa vile haziwezi kukabiliwa na yoyote, lakini kuna tofauti kubwa ya matokeo na natija. Wakati nguvu zote za Dhul-qarnain zilkuwa ni utawala wa kheri ya ubinadamu na ufanisi wake, lakini nguvu za Amerika ni za kuhami uovu wa uzayuni na kutawala nyenzo zote, masoko yote kwa masilahi ya ukoloni na kuwadumaza watu kwa kila namna.

Ushahidi wa hayo hauna idadi. Kuanzia kuusaidia uzayuni dhidi ya waarabu na ubaguzi wa rangi ndani ya Amerika hadi Rhodesia,[3] mapinduzi ya kijeshi katika nchi za kiafrika[4] na kuwapiga vita wapigania ukombozi huko Kongo na kila mahali, Ama huko Vietnam ndio haisemeki. Wamekusanya majeshi na kutumia kila walicho nacho, lakini ukakamavu wa wananchi wa Vietnam umetoa somo kwa Amerika, ambalo hawatalisahau maisha.

Kwa hiyo kila ushindi wanaoupata Amerika wajue huo ni wa muda tu, utaondoka kwa upinzani wa wananchi ambao unazidi siku baada ya siku.

Itakapofika ahadi ya Mola wangu atauvunja vunja.

Yaani huo mlima atauvunja vunja, Maana ni kuwa utakapokurubia wakati wa kutokea Juju na Mjuju nyuma ya ukuta, Mwenyezi Mungu ataleta sababu za kuvunjika kwake.

Na ahadi ya Mola wangu ni kweli haina shaka.

Shekh Maraghi anasema: “Ahadi ya Mwenyezi Mungu Mtukufu ilifika kwa kutoka Changez Khan wakafanya ufisadi katika ardhi”.

Katika Tafsir Ar-Razi imeelezwa kuwa maana ya ahadi hapa ni siku ya Kiyama. Katika Tafsir At-Twabariy imeelezwa ni baada ya kuuliwa Dajjal.

Ama sisi tunapondokea kwenye kauli ya Maraghi, kwa sababu iko karibu na kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu:

Na siku hiyo tutawaacha wakisongana wao kwa wao.

Kwani tunafahamu kuwa Juju na Majuju wataenea katika ardhi baada ya kuharibika ngome na wataharibu maisha ya watu. Mwenyezi Mungu anasema:

حَتَّىٰ إِذَا فُتِحَتْ يَأْجُوجُ وَمَأْجُوجُ وَهُم مِّن كُلِّ حَدَبٍ يَنسِلُونَ ﴿٩٦﴾

“Mpaka watakapofunguliwa Juju na Majuju wakawa wanateremka kutoka kila mlima.” (21:96).

Zaidi ya hayo ni kwamba lau ingelikuwa makusudio ya ahadi yake ni Kiyama au baada ya kufa Dajjal, ingelikuwa ngome bado ipo; na kama ipo basi ingelionekana, hasa kwa kuzingatia kuwa elimu imefanya dunia hivi sasa, pamoja na wakazi wake, ni kama familia moja inayoishi kwenye nyumba moja.

Na parapanda itapuziwa na wote watakusanywa pamoja.

Hii ndiyo siku ya mwisho kwa wale wa mwanzo na wa mwisho. Katika Tafsir Attwabariy imeelezwa kuwa Mtume(s.a.w.w) aliulizwa kuhusu Parapanda, akasema ni pembe itakayopuziwa.

Baada ya hayo yote, tunapenda kujulisha kuwa tuliyoyaeleza au kuyanukuu kutoka kwa wengine kuhusiana na Juju na Majuju, ni kwa njia ya kuleta karibu ufahamisho sio uhakika hasa.

Kwa vile hatukupata rejea za kutegemewa; Kwa sababu hiyo basi tutuatosheka na dhahiri ya Qur’an Tukufu na kuwaachia ufafanuzi wenzetu wengine.

الَّذِينَ كَانَتْ أَعْيُنُهُمْ فِي غِطَاءٍ عَن ذِكْرِي وَكَانُوا لَا يَسْتَطِيعُونَ سَمْعًا ﴿١٠١﴾

101. Wale ambao macho yao yalikuwa kwenye pazia ya kunitaja, Na wakawa hawawezi kusikia.

أَفَحَسِبَ الَّذِينَ كَفَرُوا أَن يَتَّخِذُوا عِبَادِي مِن دُونِي أَوْلِيَاءَ إِنَّا أَعْتَدْنَا جَهَنَّمَ لِلْكَافِرِينَ نُزُلًا ﴿١٠٢﴾

102. Je, wanadhani waliokufuru kuwafanya waja wangu ndio walinzi badala yangu? Hakika sisi tumeiandaa Jahannamu iwe ni mashukio ya makafiri.

قُلْ هَلْ نُنَبِّئُكُم بِالْأَخْسَرِينَ أَعْمَالًا ﴿١٠٣﴾

103. Sema: je, tuwaambie wale wenye hasara mno ya vitendo?

الَّذِينَ ضَلَّ سَعْيُهُمْ فِي الْحَيَاةِ الدُّنْيَا وَهُمْ يَحْسَبُونَ أَنَّهُمْ يُحْسِنُونَ صُنْعًا ﴿١٠٤﴾

104. Ambao juhudi yao katika maisha ya dunia imepotea bure, nao wanadhani kuwa wanafanya kazi nzuri?

أُولَـٰئِكَ الَّذِينَ كَفَرُوا بِآيَاتِ رَبِّهِمْ وَلِقَائِهِ فَحَبِطَتْ أَعْمَالُهُمْ فَلَا نُقِيمُ لَهُمْ يَوْمَ الْقِيَامَةِ وَزْنًا ﴿١٠٥﴾

105. Hao ndio ambao wamezikanusha ishara za Mwenyezi Mungu na kukutana naye; Kwa hiyo vitendo vyao vimepomoka; nawala siku ya Kiyama hatutawapa uzito wowote.

ذَٰلِكَ جَزَاؤُهُمْ جَهَنَّمُ بِمَا كَفَرُوا وَاتَّخَذُوا آيَاتِي وَرُسُلِي هُزُوًا ﴿١٠٦﴾

106. Hiyo Jahanamu ndiyo malipo yao kwa walivyokufuru na wakazifanyia kejeli ishara zangu na Mitume wangu.

JAHANNAMU NA WALIOHASIRIKA

Aya 101 – 106

MAANA

Na siku hiyo tutawaonyesha wazi Jahannam makafiri waione.

Wenye makosa, kesho, watashuhudia kwa macho yao Jahannam kabla ya kuingizwa humo, ili wachomeke kwa aina mbili za moto: Moto wa hofu na moto wa kuungua.

Wale ambao macho yao yalikuwa kwenye pazia ya kunitaja.

Kutajwa huwa kunasikiwa na masikio. Kwa hiyo hapa maana ya pazia ya macho ni mfundo wa makafiri kwa Mtume na waumini, na kwamba wao walikuwa hawawezi kumwangalia Mtume(s.a.w.w) wala waumini.

Na wakawa hawawezi kusikia utajo wa Mungu kutoka kwa Mtume wake Mtukufu.

Kwa maneno mengine ni kuwa wakosefu hawawezi kusikiza haki wala kuwatazama watu wa haki. Haya ndiyo tunayoyashuhudia kwa macho, ikiwa ni matokeo ya mzozo baina ya haki na batili na kheri na shari.

Je wanadhani waliokufuru kuwafanya waja wangu ndio walinzi badala yangu?

Makusudio ya waja wangu hapa ni viumbe ambao washirikina wali- wafanya ndio walinzi wao badala ya Mwenyezi Mungu. Hapa kuna maneno yanayokadiriwa kuwa: Je, wana dhani hawa kuwa tumeghafilika nao?Hapana! Hakika sisi tumeiandaa Jahannamu iwe ni mashukio ya makafiri.

Mashukio ni mahali anapoandaliwa mgeni, vile vile linatumika neno hilo kwa maana ya nyumba. Maana ni kuwa tumewaandalia Jahannam kuwa ndio tosha yao. Hii ni sawa na kumwambia yule unayemdharau: unadhani mimi sikuwezi wewe nawe ni kama hiki kiatu?

THAMANI YA MTU

Sema je, tuwaambie wale wenye hasara mno ya vitendo? Ambao juhudi yao katika maisha ya dunia imepotea bure, nao wanadhani kuwa wanafanya kazi nzuri?

Ufupi wa maana ni kuwa mwenye hasara zaidi katika watu na mwenye kuhangaika bure, ni yule mjinga sana anayeuona ujinga wake kuwa ni elimu, shari yake kuwa ni kheri na uovu wake kuwa ni wema.

Hapana mwenye shaka kuwa huyo ni mwenye hasara duniani, kwa vile yeye anaishi asivyokuwa. Vile vile huko akhera, kwa vile atakutana na Mola wake akiwa na ujinga, ghururi na matendo maovu. Aya inaashiria kuwa thamani ya mtu haiwezi kupimwa kwa kuiona yeye mwenyewe; Kwa sababu mgomvi hawezi kujihukumu. Wala pia haiwezi kupimwa kwa mtazamo wa watu.

Ispokuwa mtu hupimwa kwa kipimo cha Qur’an na misingi yake na kushikamana na mafunzo yake na hukumu zake. Hupimwa kwa ukweli na uadilifu, kuinusuru haki na watu wake na kujitolea kwa hali na mali. Qur’an imejaa aina nyingi za mafunzo haya; kama vile kauli zake Mwenyezi Mungu Mtukufu zifuatazo: “...Na kuweni pamoja na wa kweli” Juz; 11 (9:119)

قَوَّامِينَ بِالْقِسْطِ ﴿١٣٥﴾

“....Kuweni Imara kwa uadilifu” Juz;. 5 (4:135)

كُونُوا أَنصَارَ اللَّـهِ ﴿١٤﴾

“...Kuweni wasaidizi wa Mwenyezi Mungu (61:14)

كُونُوا رَبَّانِيِّينَ ﴿٧٩﴾

“...Kuweni watumishi wa Mwenyezi Mungu”Juz.3 (3:79)

وَجَاهِدُوا بِأَمْوَالِكُمْ وَأَنفُسِكُمْ فِي سَبِيلِ اللَّـهِ ذَٰلِكُمْ خَيْرٌ لَّكُمْ إِن كُنتُمْ تَعْلَمُونَ ﴿٤١﴾

“...Na mpiganie jihadi katika njia ya Mwenyezi Mungu kwa mali zenu na nafsi zenu Juz.10 (9:41)

إِنَّ أَكْرَمَكُمْ عِندَ اللَّـهِ أَتْقَاكُمْ ﴿١٣﴾

“Hakika mtukufu wenu zaidi, kwa Mwenyezi Mungu, ni yule mwenye takua zaidi katika nyinyi” (49:13)

Unaweza kuuliza : Mkosaji anaweza kujiona kuwa amepatia na kwamba amefanya vizuri. Je atakuwa ni miongoni mwa waliohasirika; pamoja na kujua kuwa hakuna mwenye isma (kuhifadhiwa na madhambi) isipokuwa yule mwenye isma?

Jibu : Wenye kukosea wako aina mbili: Wa kwanza ni yule mwenye kukosea baada ya kutafiti na kuhakikisha; sawa na wanavyofanya wale wanaojitahidi, kiasi ambacho natija inayopatikana inaweza kuwa sawa na ya mtaalmu.

Hapana mwenye shaka kuwa mkoseaji huyu hawezi kuwa ni katika wale ambao juhudi zao zimepotea bure, au kuwa ni aibu ukoseaji wake; bali huyu analipwa thawabu kutokana na juhudi yake; kama ilivyoelezwa katika Hadith. Lakini kwa sharti awe na nia ya kujikosoa, yatakapofichuka makosa.

Aina ya pili, ni kukosea kulikotokana na kujiamini kwa juujuu, kulikotokana na mawazo, bila ya kufanya utafiti, kwa vile hajui misingi ya utafiti na elimu, Au anaweza kuwa anaijua, lakini asiitumie au aitumie nusunusu, aitumie kabla ya kuikamilisha. Huyu ndiye aliye miongoni mwa wale waliopata hasara katika kazi zao, hilo halina shaka. Kwa sababu Mwenyezi Mungu ameamrisha kuwa na mazingatio na uthabiti na akakataza pupa na kusema bila ya ujuzi.

Baada ya hayo somo tunalolipata kutokana na Aya hii, ni kuwa tusijidanganye, tukajipa sifa tusizo nazo wala kujidanganya kwa maneno.

Vile vile ni wajibu tujihisabu nafsi zetu zinapokuwa na ghururi na kujitukuza, kabla hajatuhisabu Mwenyezi Mungu na watu. Pia rai zetu na kauli zetu tusizione kuwa ndio sawa mia kwa mia. Makosa yanatokea kwa yeyote.

Hao ndio ambao wamezikanusha ishara za Mwenyezi Mungu na kukutana naye.

Mfumo wa maneno unafahamisha kuwa makusudio ya wale waliokanusha ishara za Mola wao na kukutana naye ndio wale ambao juhudi yao katika maisha ya dunia imepotea bure; ni sawa wawe wameamini ufufuo au wameukanusha. Linalozingatiwa ni imani na matendo kwa pamoja; sio imani peke yake.

Kwa hiyo vitendo vyao vimepomoka na wala siku ya kiyama hatutawapa uzito wowote.

Yaani hatutawathamini, kwa sababu hakuna heshima mbele ya Mwenyezi Mungu isipokuwa kwa yule mwenye takua.

Hiyo Jahanamu ndiyo malipo yao kwa walivyokufuru na wakazifanyia kejeli ishara zangu na Mitume wangu.

Walimkufuru Mwenyezi Mungu na wakaifanyia masikhara haki na watu wake. Moto ndio mwisho na ukomo wa ufisadi na upotevu.

إِنَّ الَّذِينَ آمَنُوا وَعَمِلُوا الصَّالِحَاتِ كَانَتْ لَهُمْ جَنَّاتُ الْفِرْدَوْسِ نُزُلًا ﴿١٠٧﴾

107. Hakika wale ambao wameamini wakatenda mema, mashukio yao yatakuwa kwenye Pepo za Firdausi.

خَالِدِينَ فِيهَا لَا يَبْغُونَ عَنْهَا حِوَلًا ﴿١٠٨﴾

108. watadumu humo; hawatataka kuondoka.

قُل لَّوْ كَانَ الْبَحْرُ مِدَادًا لِّكَلِمَاتِ رَبِّي لَنَفِدَ الْبَحْرُ قَبْلَ أَن تَنفَدَ كَلِمَاتُ رَبِّي وَلَوْ جِئْنَا بِمِثْلِهِ مَدَدًا ﴿١٠٩﴾

109. Sema: Lau bahari ingelikuwa ndio wino kwa maneno ya Mola wangu, basi bahari ingemalizika kabla ya kumalizika maneno ya Mola wangu, hata tungeleta mfano wake kuongezea.

قُلْ إِنَّمَا أَنَا بَشَرٌ مِّثْلُكُمْ يُوحَىٰ إِلَيَّ أَنَّمَا إِلَـٰهُكُمْ إِلَـٰهٌ وَاحِدٌ فَمَن كَانَ يَرْجُو لِقَاءَ رَبِّهِ فَلْيَعْمَلْ عَمَلًا صَالِحًا وَلَا يُشْرِكْ بِعِبَادَةِ رَبِّهِ أَحَدًا ﴿١١٠﴾

110. Sema: hakika mimi ni binadamu kama nyinyi tu, nimeletewa wahyi kwamba Mungu wenu ni Mungu mmoja. Mwenye kutarajia kukutana na Mola wake, basi na atende matendo mema, wala asimshirikishe yeyote katika ibada ya Mola wake.

WALIOAMNI NA WAKATENDA MEMA

Aya 108 – 110

MAANA

Hakika wale ambao wameamini wakatenda mema, mashukio yao yatakuwa kwenye Pepo za Firdausi.

Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kuwahidi makafiri moto, sasa anatoa ahadi ya Pepo kwa waumini. Firdausi ni katika Pepo ya daraja ya juu. Mtume Mtukufu(s.a.w.w) amesema: “Mkimuomba Mwenyezi Mungu muombeni Firdausi.”

Watadumu humo; hawatataka kuondoka.

Yaani Mwenyezi Mungu (s.w.t) atawalipa wema yale ambayo hawatataka mengine, tosha kabisa! Yanatosheleza yote wanayoyataka. Aya inaashiria kuwa hakuna tamaa huko Akhera; vinginevyo ingelikuwa hakuna kutosheka. Kwani mwenye tamaa hatosheki.

Sema: Lau bahari ingelikuwa ndio wino kwa maneno ya Mola wangu, basi bahari ingemalizika kabla ya kumalizika maneno ya Mola wangu, hata tungeleta mfano wake kuongezea.

Bahari ni jina la jinsi, linaenea kwenye bahari zote. Makusudio ya kabla ya kumalizika maneno, ni kuwa hayamaliziki na mfano wake ni mfano wa bahari. Maana ni kuwa lau tuchukulie kuwa bahari zote ni wino wa kuandika maneno ya Mwenyezi Mungu zisingetosha na maneno ya Mwenyezi Mungu yangelibakia bila ya kikomo.

Aya nyingine yenye maana hii ni kauli yake Mwenyezi Mungu: “Na lau miti yote iliyomo ardhini ikawa ni kalamu na bahari (ikawa wino) na ikaongezewa bahari nyingine saba, maneno ya Mwenyezi Mungu yasingelimalizika.” (31:27).

Makusudio ya maneno ya Mwenyezi Mungu hapa sio matamshi yanayotokana na herufi wala si amri ya kitendo inayotokana na ibara ya ‘kuwa na kikawa,’ kwa sababu amri hii haiingii kwenye mahisabu: “Na amri haikuwa ila ni moja tu, kama kupepesa jicho.” (54:51).

Isipokuwa makusudio ya maneno yake hapa, ni kuweza kuvileta vitu vyote, wakati wowote atakao; ni sawa iwe ni kwa kuviambia kuwa na vikawa au aviambie muda ujao, wa karibu au mbali. Uwezo huu hauna kikomo wala mwisho, lakini bahari, miti na mifano yake ina kikomo; na kila chenye kikomo kinakwisha.

Kwa maneno mengine ni kuwa kila kitu kilichopo kitakwisha na kukoma, isipokuwa uwezo wa Mwenyezi Mungu wa kukifanya hicho kitu utabakia.

Tutaifafanua zaidi fikra hii kwa mfano huu: Mtu akiwa na maarifa ya kilimo, maarifa yake haya atakuwa nayo tu wakati wote atakaokuwa hai, lakini kile atakochokilima kitaisha. Uweza wa Mwenyezi Mungu (s.w.t) hauishi kwa vile hauna kikomo ni wa milele, lakini viumbe vyake vimepatikana na kila chenye kupatikana kina mwisho.

Sema: Hakika mimi ni binadamu kama nyinyi tu, sina tofauti na nyinyi isipokuwanimeletewa wahyi kwamba Mungu wenu ni Mungu mmoja.

Ibn Abbas anasema: “Mwenyezi Mungu, kwa Aya hii, amemfundisha Mtume wake unyenyekevu, akamwamrisha aseme yeye mwenyewe kuwa ni binadamu kama wengine, isipokuwa Mwenyezi Mungu amemtukuza kwa wahyi.”

Nasi tunaongezea kauli ya Ibn Abbas: Na ili waislamu wasimfanye Muhammad(s.a.w.w) kama wanaswara (wakristo) walivyomfanya Isa(a.s) .

Mwenye kutarajia kukutana na Mola wake, kwa hisabu, thawabu na adhabu,basi na atende matendo mema, wala asimshirikishe yeyote katika ibada ya Mola wake.

Kila mwenye kufanya amali kwa ajili ya mwengine atakuwa amemshirikisha Mwenyezi Mungu kwenye ibada; ni sawa aseme waungu ni wengi au asiseme.

Tofauti ni kuwa kauli ni shirki ya waziwazi na riya ni shirki ya kificho. Kuna Hadith inayosema:

“Mwenye kuswali kwa riya amefanya shirki na mwenye kufunga kwa riya amefanya shirk”

Fananisha mengine kwenye swala na saumu.

MWISHO WA SURA YA KUMI NA NANE

3

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA SITA

Sura ya Kumi na Tisa: Surat Maryam. Imeshuka Makka ina Aya 98.

بِسْمِ اللَّهِ الرَّحْمَٰنِ الرَّحِيمِ

Kwa jina la Mwenyezi Mungu Mwingi wa rehema Mwenye Kurehemu.

كهيعص ﴿١﴾

1. Kaaf Haa Yaa A’yn Swaad.

ذِكْرُ رَحْمَتِ رَبِّكَ عَبْدَهُ زَكَرِيَّا ﴿٢﴾

2. Huu ni ukumbusho wa rehema ya Mola wako kwa mja wake Zakariya.

إِذْ نَادَىٰ رَبَّهُ نِدَاءً خَفِيًّا ﴿٣﴾

3. Alipomuomba Mola wake kwa siri.

قَالَ رَبِّ إِنِّي وَهَنَ الْعَظْمُ مِنِّي وَاشْتَعَلَ الرَّأْسُ شَيْبًا وَلَمْ أَكُن بِدُعَائِكَ رَبِّ شَقِيًّا ﴿٤﴾

4. Akasema: Mola wangu! Mfupa wangu umedhoofika, na kichwa kiname remeta kwa mvi. Mola wangu! Sikuwa mwenye bahati mbaya kwa kukuomba wewe.

وَإِنِّي خِفْتُ الْمَوَالِيَ مِن وَرَائِي وَكَانَتِ امْرَأَتِي عَاقِرًا فَهَبْ لِي مِن لَّدُنكَ وَلِيًّا ﴿٥﴾

5. Na Mimi nahofia jamaa zangu baada yangu na mke wangu ni tasa, Basi nipe mrithi kutoka kwako.

يَرِثُنِي وَيَرِثُ مِنْ آلِ يَعْقُوبَ وَاجْعَلْهُ رَبِّ رَضِيًّا ﴿٦﴾

6. Atakayenirithi mimi na arithi ukoo wa Ya’qub, Ewe Mola wangu mjaaliye mwenye kuridhisha.

ZAKARIYA

Aya 1-6

MAANA

Kaaf Haa Yaa A’yn Swaad.

Umetangulia mfano wake pamoja na tafsiri katika Juz. 1, mwanzo wa Sura Baqara

Huu ni ukumbusho wa rehema ya Mola wako kwa mja wake Zakariya.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) anamsimulia Mtume wake mtukufu, katika Aya hizi, jinsi alivyompa rehema Zakariya na akamneemesha kwa mtoto wake Yahya. Zakariya anatokana na kizazi cha Suleiman bin Daud. Alimuoa khalat (mama mdogo) wa Maryam. Naye alikuwa ni mlezi wa Maryam, Yametangulia maelezo ya hayo katika Juz; 3 (3:38), Inasemekana kuwa Zakriya alikuwa seremala.

Alipomuomba Mola wake kwa siri Alimuomba Mola wake akiwa peke yake na akasema: Mola wangu! Mfupa wangu umedhoofika, na kichwa kinameremeta kwa mvi. Mola wangu! Sikuwa mwenye bahati mbaya kwa kukuomba wewe.

Zakariya alizeeka bila ya kuwa na mtoto, kwa hiyo akamnyenyekea Mola wake, akimshtakia udhaifu wake na uzee wake. Miongoni mwa aliyoyasema ni: “Mola wangu usiniache peke yangu na Wewe ndiye mbora wa wanaorithi” (21:89). Ninakuomba ewe Mola wangu, nikiwa na matarajio ya rehema yako bila ya kukata tamaa. Vipi nikate tamaa na hali hujawahi kuyaangusha matarajio yangu kwako.

Na mimi nahofia jamaa zangu baada yangu na mke wangu ni tasa. Basi nipe mrithi kutoka kwako atakayenirithi mimi na arithi ukoo wa Ya’qub, Ewe Mola wangu mjaaliye mwenye kuridhisha.

Neno la kiarabu ‘mawalii’ lililofasiriwa jamaa, lina maana ya ndugu wa upande wa baba. Kwa hiyo Zakariya akiwa mzee na mkewe akiwa tasa, alihofia kurithiwa na binamu zake ambao ni wana wa Israil. Inasemekena walikuwa ni waovu.

Na hilo si mbali kwa Waisrail, kuwa wakirithi watawafanyia uovu watu na kuwafanyia ufisadi kwenye dini yao na dunia yao. Pamoja na uzee wake Zakariya na utasa wa mke wake, bado alikuwa na mategemeo makubwa kwa muumba wake, ndio maana akamuomba amtimizie haja yake.

يَا زَكَرِيَّا إِنَّا نُبَشِّرُكَ بِغُلَامٍ اسْمُهُ يَحْيَىٰ لَمْ نَجْعَل لَّهُ مِن قَبْلُ سَمِيًّا ﴿٧﴾

7. Ewe Zakariya! Hakika sisi tunakubashiria mwana, jina lake ni Yahya, hatujapata kumpa jina hilo yeyote kabla yake.

قَالَ رَبِّ أَنَّىٰ يَكُونُ لِي غُلَامٌ وَكَانَتِ امْرَأَتِي عَاقِرًا وَقَدْ بَلَغْتُ مِنَ الْكِبَرِ عِتِيًّا ﴿٨﴾

8. Akasema: Ewe Mola wangu! Vipi nitakuwa na mwana na hali mke wangu ni tasa, na mimi nimekwishafikia ukongwe katika uzee?

قَالَ كَذَٰلِكَ قَالَ رَبُّكَ هُوَ عَلَيَّ هَيِّنٌ وَقَدْ خَلَقْتُكَ مِن قَبْلُ وَلَمْ تَكُ شَيْئًا ﴿٩﴾

9. Akasema, ndio hivyo hivyo Mola wako amesema, haya kwangu ni mepesi. Na hakika nilikuumba wewe zamani na hukuwa kitu.

قَالَ رَبِّ اجْعَل لِّي آيَةً قَالَ آيَتُكَ أَلَّا تُكَلِّمَ النَّاسَ ثَلَاثَ لَيَالٍ سَوِيًّا ﴿١٠﴾

10. Akasema: Mola wangu nijaalie ishara. Akasema, ishara yako ni kuwa hutasema na watu kwa masiku matatu, na hali ni mzima.

فَخَرَجَ عَلَىٰ قَوْمِهِ مِنَ الْمِحْرَابِ فَأَوْحَىٰ إِلَيْهِمْ أَن سَبِّحُوا بُكْرَةً وَعَشِيًّا ﴿١١﴾

11. Akawatokea watu wake kutoka mihirabuni, akawaashiria kuwa mumsabihi asubuhi na jioni.

BISHARA YA YAHYA

Aya 7 – 11

MAANA

Ewe Zakariya! Hakika sisi tunakubashiria mwana, jina lake ni Yahya, hatujapata kumpa jina hilo yeyote kabla yake.

Mwenyezi Mungu aliitikia dua ya Zakariya na akampa habari njema ya kuzaliwa mtoto wa kiume, na kwamba Mwenyezi Mungu amemuita Yahya akiwa bado yuko kwenye uti wa mgongo wa baba yake. Na hakuna aliyewahi kuitwa jina hilo kabla yake. Inasemekana Yahya ndiye Yohana amabye ni maarufu kwa wakiristo kwa jina la Yohana mbatizaji).

Akasema: “Ewe Mola wangu! Vipi nitakuwa na mwana na hali mke wangu ni tasa, na mimi nimekwishafikia ukongwe katika uzee?

Kusema hivi sio kuona kuwa haiwezekani, bali ni kuadhimisha na kushukuru neema za Mwenyezi Mungu na uweza wake ambao umekiuka desturi na mazoweya. Yeye ni mzee na mkewe ni tasa tena ni mzee, lakini pamoja na yote hayo Mwenyezi Mungu amemneemesha kupata mtoto.

Akasema: ndio hivyo hivyo Mola wako amesema, haya kwangu ni mepesi. Na hakika nilikuumba wewe zamani na hukuwa kitu.

Anayesema kauli zote mbili ni mmoja, naye ni Mwenyezi Mungu. yaani Mwenyezi Mungu anamwambia Zakariya kuwa Mola wako amesema. Desturi hii wanaitumia watungaji wengi wa kiislamu.

Mtu anaweza kusema: “Amesema Muhammad yeye ni Bin Malik” akijikusudia yeye Mwenyewe. Mfano mwingine ni wa Tabariy akijizungumzia yeye mwenyewe: “Amesema Abu Jafar Muhammad bin Jarir At-Tabariy”

Aliposema Mwenyezi Mungu haya kwangu ni mepesi, ni kuwa kwa Mungu hakuna kitu chochote kilicho kigumu. Vitu vyote kwake ni sawa tu; hahitajii isipokuwa neno ‘Kuwa’

Akasema: Mola wangu nijaalie ishara. Akasema, ishara yako ni kuwa hutasema na watu kwa masiku matatu, na hali ni mzima. Akawatokea watu wake kutoka mihirabuni, akawaashiria kuwa mumsabihi asub- uhi na jioni.

Makusudio ya kuwaashiria ni kuwaashiria kwa mkono wake au kwa maandishi, kwa sababu yeye amezuiliwa kuzungumza, Umetangulia ufafanuzi wake katika Juz; 3 (3:41).

يَا يَحْيَىٰ خُذِ الْكِتَابَ بِقُوَّةٍ وَآتَيْنَاهُ الْحُكْمَ صَبِيًّا ﴿١٢﴾

12. Ewe Yahya! Kishike kitabu kwa nguvu, Na tulimpa hukumu angali mtoto.

وَحَنَانًا مِّن لَّدُنَّا وَزَكَاةً وَكَانَ تَقِيًّا ﴿١٣﴾

13. Na tukampa huruma itokayo kwetu na utakaso na alikuwa ni mwenye takua.

وَبَرًّا بِوَالِدَيْهِ وَلَمْ يَكُن جَبَّارًا عَصِيًّا ﴿١٤﴾

14. Na mwema kwa wazazi wake wala hakuwa jeuri muasi.

وَسَلَامٌ عَلَيْهِ يَوْمَ وُلِدَ وَيَوْمَ يَمُوتُ وَيَوْمَ يُبْعَثُ حَيًّا ﴿١٥﴾

15. Na amani iwe juu yake, siku alipozaliwa na siku atakapokufa na siku atakapofufuliwa.

YAHYA

AYA 12 – 15

MAANA

Ewe Yahya!

Kauli hii inaelezea moja kwa moja kuwa Yahya amekwishazaliwa, amekuwa na akili ya kufahamu na kutia maanani na ana uwezo wa kutumia Tawrat ambayo ndiyo aliyoikusudia Mwenyezi Mungu aliposema:

Kishike kitabu kwa nguvu.

Maana ya kukishika kwa nguvu ni kukitumia kwa bidii na ikhlasi. Kisha akamsifu Yahya kwa sifa zifuatazo:

Na tulimpa hukumu angali mtoto na tukampa huruma itokayo kwetu na utakaso na alikuwa ni mwenye takua na mwema kwa wazazi wake wala hakuwa jeuri muasi.

Makusudio ya kupewa hukumu udogoni ni kujua dini mapema udogoni. Hii ni neema Mwenyezi Mungu aliyomhusisha nayo Yahya; kama alivyomhusisha kwa kuzaliwa na wazazi wazee. Mwenyezi Mungu humhusisha kwa rehema yake amtakaye. Baadhi ya riwaya zinasema kuwa siku moja watoto walimwambia Yahya: “Twendeni tukacheze.” Yahya akasema: “Hatukuumbwa kwa ajili ya kucheza, twendeni tukaswali.”

Makusudio ya upole ni upole kwa waja. Utakaso ni utwahara na utakatifu. Takua ni kumtii Mwenyezi Mungu. Kuwatendea wema wazazi wawili ni kinyume cha kuwaudhi.

Kauli yake Mwenyezi Mungu:Wala hakuwa ni jeuri muasi ni kuunganisha kwa kufafanua. Kwa sababu Mwenye utakaso na takua hawezi kuwa jeuri muasi.

Na amani iwe juu yake, siku alipozaliwa na siku atakapokufa na siku atakapofufuliwa

Hili ni fumbo la kuwa Yahya ni Mwenye kuridhiwa mbele ya Mwenyezi Mungu duniani na Akhera. Ilivyo ni kuwa kumridhia kwake Yahya (a.s.) ni matokeo ya sifa alizomsifu nazo Mwenyezi Mungu.

Unaweza kuuliza : Kwanini Mwenyezi Mungu amemuhusisha Yahya na sifa hizi tele akiwa bado angali mdogo?

Jibu : Hakika Mwenyezi Mungu ana mambo yake kwa viumbe vyake. Anaweza akampa fadhila mdogo na akamnyima mkubwa. Na kila kutoa kwake na kuzuia kwake kuna hekima ambayo akili inaweza kujua na isiweze kujua. Lakini akili huwa inajaribu; kama ifuatavyo:

Sio mbali kuwa makusudio ya kusifika Yahya na sifa hizi katika rika hilo ni kutoa hoja kwa Wana wa Israil, watakapohitilafiana naye na wasikilize nasaha zake na mwito wake, Alimuumba Isa bila ya baba, “ili tumfanye kuwa ni ishara kwa watu na rehema itokayo kwetu” Itakuja Aya hii sehemu inayofuatia hii.

Pamoja na hoja hii ya kunyamazisha, lakini bado walimuasi Yahya na wakamfanyia uadui; mwisho wakamuua yeye na baba yake, si kwa lolote isipokuwa ni kwa kuwakataza mabaya. Hili si ajabu kwa yule aliyesema kuwa mikono ya Mwenyezi Mungu imefunga au Mungu ni fukara na sisi ni matajiri. Rudia Juz. 6 (5:64).

Katika kitabu Qasasul-anbiya (Visa vya mitume) imeelezwa kuwa Herod mfalme wa Palestina, wakati huo, alimpenda Herodias, binti wa kaka yake, kutokana na uzuri wake, na akataka kumuoa. Yahya alipopinga hilo

Herodias alichukia na akatoa sharti kwa ami yake kuwa mahari yake yawe kichwa cha Yahya. Kwa hiyo Mfalme akamchinja Yahya na akampelekea mpenzi wake zawadi hiyo ya kichwa.

Kuna riwaya mashuhuri iliyopokewa kutoka kwa Ali bin Husein bin Ali(a.s) kwamba baba yake, alipokuwa akielekea Iraq, alikuwa akimkumbuka sana Yahya na akisema: “Ni katika utwevu wa dunia kwa Mwenyezi Mungu, kwamba kichwa cha Yahya bin Zakariya kitolewe zawadi kwa kahaba miongoni mwa makahaba wa ki bani Israil.”

وَاذْكُرْ فِي الْكِتَابِ مَرْيَمَ إِذِ انتَبَذَتْ مِنْ أَهْلِهَا مَكَانًا شَرْقِيًّا ﴿١٦﴾

16. Na mtaje Maryam katika Kitabu, alipojitenga na watu wake mahali upande wa mashariki.

فَاتَّخَذَتْ مِن دُونِهِمْ حِجَابًا فَأَرْسَلْنَا إِلَيْهَا رُوحَنَا فَتَمَثَّلَ لَهَا بَشَرًا سَوِيًّا ﴿١٧﴾

17. Na akaweka pazia kujikinganao, Tukampelekea roho wetu, Akajifananisha kwake sawa na mtu.

قَالَتْ إِنِّي أَعُوذُ بِالرَّحْمَـٰنِ مِنكَ إِن كُنتَ تَقِيًّا ﴿١٨﴾

18. Akasema: Hakika mimi najilinda kwa Mwingi wa rehema aniepushe nawe, ukiwa ni mwenye takua.

قَالَ إِنَّمَا أَنَا رَسُولُ رَبِّكِ لِأَهَبَ لَكِ غُلَامًا زَكِيًّا ﴿١٩﴾

19. Akasema: Mimi ni mjumbe wa Mola wako ili nikupe mwana mtakatifu.

قَالَتْ أَنَّىٰ يَكُونُ لِي غُلَامٌ وَلَمْ يَمْسَسْنِي بَشَرٌ وَلَمْ أَكُ بَغِيًّا ﴿٢٠﴾

20. Akasema: Nitakuwaje na mwana hali hajanigusa mtu yoyote wala mimi si malaya.”

قَالَ كَذَٰلِكِ قَالَ رَبُّكِ هُوَ عَلَيَّ هَيِّنٌ وَلِنَجْعَلَهُ آيَةً لِّلنَّاسِ وَرَحْمَةً مِّنَّا وَكَانَ أَمْرًا مَّقْضِيًّا ﴿٢١﴾

21. Akasema; Ndivyo hivyo hivyo, Mola wako amesema, haya kwangu ni mepesi! Na ili tumfanye kuwa ni ishara kwa watu na rehema itokayo kwa kwetu. Nahilo ni jambo lililokwishapitishwa.

MARYAM

Aya 16-21

MAANA

Na mtaje Maryam katika Kitabu, alipojitenga na watu wake mahali upande wa mashariki, Na akaweka pazia kujikinga nao.

Dhahiri ya Aya inafahamisha kuwa Maryamu alijitenga na watu na akawa peke yake upande wa mashariki na kaweka sitara baina yake na wao, kiasi ambacho hawamuoni wala yeye hawaoni wao.

Kwa nini Maryamu alijitenga? Je, ni kwa kuwa aliona mambo yanayomchukiza au ni kwa kujitenga kwa ajili ya kufanya ibada au ni kwa ajili ya jambo jengine? Je, makusudio ya mahali upande wa mashariki ni kunakotokea jua au ni mashariki ya Baytul-maqdis au ni upande wa mashariki wa nyumba ya watu wake. Pia je, ni aina gani ya pazia aliyoweka, ni ukuta au kibanda?

Hakuna kitu, katika Aya, kinachoashiria majibu ya maswali haya; Kwa sababu hayahusiani na itikadi wala maisha. Sio mbali kuwa Mwenyezi Mungu alimpa ilhamu ya kujitenga huko ili apewe habari na Jibril kuhusu kuzaliwa Isa(a.s) akiwa kando na watu.

Tukampelekea roho wetu, akajifananisha kwake sawa na mtu

Makusudio ya roho wetu, ni Jibril. Alijifananisha na mtu kamili. Imeelezwa katika baadhi ya Tafsiri kwamba alikuja na umbo la mtu ili asimwogopeshe. Tafsiri nyingine inasema kuwa aliogopa na akafadhaika, kwa mshtukizo huu.

Mgeni ajitome ndani bila ya hodi na yeye yuko peke yake! Jambo la kushangaza, Kauli hii, ya pili, ina nguvu na usahihi zaidi ya ile nyingine, kwa dalili ya kuwa yeye alifazaika na akasema:

Hakika mimi najilinda kwa Mwingi wa rehema aniepushe nawe, ukiwa ni Mwenye takua.”

Yaani nataka hifadhi kwa Mwenyezi Mungu na shari yako ikiwa wewe unamwamini Yeye na hisabu yake na adhabu yake. Alimuhofisha na Mwenyezi Mungu, kwa sababu hakuwa na nyenzo nyingine yoyote ya kumzuia hapo alipo, isipokuwa hiyo. Vinginevyo yeye ana hifadhi ya Mwenyezi Mungu akiwa anamtegemea Yeye; ni sawa huyo anayemuhofisha ni mwenye takua au muovu.

Akasema: Mimi ni mjumbe wa Mola wako ili nikupe mwana mtakatifu.” Akasema: Nitakuwaje na mwana hali hajanigusa mtu yoyote wala mimi si malaya?

Unanipa habari ya mtoto, vipi na kutoka wapi? Sina mume wala sijafanya uasharati.

Akasema: Ndivyo hivyo hivyo Mola wako amesema, haya kwangu ni mepesi! Na ili tumfanye kuwa ni ishara kwa watu na rehema itokayo kwetu. Na hilo ni jambao lililokwishapitishwa.

Roho mwaminifu alimwambia kuwa sababu za kuzaa, kwa Mungu, sio kuonana na mtu tu. Kama ambavyo Mwenyezi Mungu anafanya vitu kwa sababu zake zilizozoeleka, vile vile anafanya vitu kwa neno ‘kuwa’ sawa na alivyofanya ulimwengu bila ya kitu chochote na Adamu bila ya baba wala mama.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) alitaka azaliwe mtoto kuonyesha dalili wazi ya ukuu wa muumba na utume wa atakayezaliwa, awe ni rehema kwa ubi- nadamu na hoja ya kunyamazisha wana wa Issrail ambao walijaribu kumuua. Tumeyaeleza hayo kwa ufafanuzi zaidi katika Juz. 3 (3: 45)

فَحَمَلَتْهُ فَانتَبَذَتْ بِهِ مَكَانًا قَصِيًّا ﴿٢٢﴾

22. Basi akachukua mimba yake akaondoka nayo mahali mbali.

فَأَجَاءَهَا الْمَخَاضُ إِلَىٰ جِذْعِ النَّخْلَةِ قَالَتْ يَا لَيْتَنِي مِتُّ قَبْلَ هَـٰذَا وَكُنتُ نَسْيًا مَّنسِيًّا ﴿٢٣﴾

23. Uchungu ukampeleka kwenye shina la mtende; akasema: Laiti ningelikufa kabla ya haya nikawa mwenye kusahaulika kabisa.

فَنَادَاهَا مِن تَحْتِهَا أَلَّا تَحْزَنِي قَدْ جَعَلَ رَبُّكِ تَحْتَكِ سَرِيًّا ﴿٢٤﴾

24. Pakanadiwa kutoka chini yake kwamba usihuzunike; hakika Mola wako amejaalia chini yako kijito cha maji.

وَهُزِّي إِلَيْكِ بِجِذْعِ النَّخْلَةِ تُسَاقِطْ عَلَيْكِ رُطَبًا جَنِيًّا ﴿٢٥﴾

25. Na litikise kwako shina la mtende utakuangushia tende freshi zilizo mbivu.

فَكُلِي وَاشْرَبِي وَقَرِّي عَيْنًا فَإِمَّا تَرَيِنَّ مِنَ الْبَشَرِ أَحَدًا فَقُولِي إِنِّي نَذَرْتُ لِلرَّحْمَـٰنِ صَوْمًا فَلَنْ أُكَلِّمَ الْيَوْمَ إِنسِيًّا ﴿٢٦﴾

26. Basi kula na kunywa na uburudishe jicho. Na pindi ukimuona mtu yeyote basi sema hakika mimi nimeweka nadhiri kwa Mwingi wa rehema ya kufunga. Kwa hiyo leo sitasema na mtu.

MIMBA YA ISA

Aya 22 – 26

MAANA

Basi akachukua mimba yake akaondoka nayo mahali mbali

Inasemekana kuwa Jibril alimpulizia kwenye gauni lake, ikawa ndiyo sababu ya kushika mimba; Rejea ya kauli hii ni dhahiri ya Aya hii:

وَالَّتِي أَحْصَنَتْ فَرْجَهَا فَنَفَخْنَا فِيهَا مِن رُّوحِنَا ﴿٩١﴾

“Na (mwanamke) aliyelinda tupu yake na tukampulizia katika roho yetu” (21:91)

وَمَرْيَمَ ابْنَتَ عِمْرَانَ الَّتِي أَحْصَنَتْ فَرْجَهَا فَنَفَخْنَا فِيهِ مِن رُّوحِنَا ﴿١٢﴾

“Na Maryam Binti Imrani aliyelinda tupu yake na tukampulizia humo kutoka roho yetu,” (66:12).

Mara kwa mara tumeishiria kuwa Qur’an inajifasiri yenyewe; yaani Aya zinafasiri Aya nyingine. Kwa sababu chimbuko lake ni moja. Tukiangalia msingi huu tutafahamu, kwa ujumla wake wote kuwa makusudio ya kupulizia ni kuumba na kutengenezwa mimba, na makusudio ya Roho ni Isa mwenyewe; kama inavyofahamisha Aya hii: “Masih Isa bin Maryam ni Mtume wa Mwenyezi Mungu na neno lake tu alilompelekea Maryam, na ni roho iliyotoka kwake.” Juz.6 (4:171)

Maana ya ‘neno lake’ ni neno ‘kuwa,’ambalo anaumbia nalo vitu. Na maana ya ‘alilompelekea Maryam’ ni kuwa Maryam au tumbo lake ndio mahali pa kuumbwa; Kwa ufafanuzi zaidi angalia huko. Kwa vyovyote ilivyo ni kwamba Maryam alipojihisi ana mimba alijitenga kando na watu wake kwa kuona haya.

Uchungu ukampeleka kwenye shina la mtende; akasema: Laiti ningelikufa kabla ya haya nikawa mwenye kusahaulika kabisa.

Haya ni maneno anayoyasema mtu yeyote anapozongwa na matatizo makubwa, anatamka kupunguza msongo wa moyo na huzuni yake.

Pakanadiwa kutoka chini yake kwamba usihuzunike; hakika Mola wako amejaalia chini yako kijito cha maji.

Yanayokuja akilini mwanzo, kutokana na mfumo wa maneno, ni kuwa aliyenadi ni Isa(a.s) na wala sio Jibril, kama wanavyodai wafasiri wengi. Kunadi huku ni miongoni mwa miujiza ya Isa; sawa na kuzaliwa na kufufua kwake wafu.

Isa aliendelea kumwambia mama yake:

Na litikise kwako shina la mtende utakuangushia tende freshi zilizo mbivu.

Inasemekana huo haukuwa msimu wa tende. Kwa hiyo kupatikana tende ilikuwa ni muujiza. Hili haliko mbali, kwa sababu kila kitu hapa ni muujiza tu na tamko lenyewe pia linafahamisha hivyo.

Basi kula tende na kunywa kutoka kwenye kijito na uburudishe jicho.

Yaani poa moyo kwa kupata mtoto mwenye kubarikiwa.

Na pindi ukimuona mtu yeyote na akakuuliza kuhusu mtoto,basi sema kwa ishara kuwahakika mimi nimeweka nadhiri kwa Mwingi wa rehema ya kufunga kwa kunyamaza, Hiyo ndiyo iliyokuwa Swaumu ya waisrail wakati huo.

Kwa hiyo leo sitasema na mtu.

Hapana haja ya ufafanuzi hapa, isipokuwa kufasiri matamshi, kwa sababu akili haina nafasi katika maudhui haya maadamu dhahiri ya maneno haigongani na hukumu ya kiakili katika maudhui haya; Tazama Juz; 3 (3:45–51) kifungu cha ‘Lisilowezekana kiakili na kidesturi.

4

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA SITA

فَأَتَتْ بِهِ قَوْمَهَا تَحْمِلُهُ قَالُوا يَا مَرْيَمُ لَقَدْ جِئْتِ شَيْئًا فَرِيًّا ﴿٢٧﴾

27. Akaenda naye kwa jamaa zake amembeba. Wakasema: Ewe Maryamu! Hakika umeleta kitu cha ajabu.

يَا أُخْتَ هَارُونَ مَا كَانَ أَبُوكِ امْرَأَ سَوْءٍ وَمَا كَانَتْ أُمُّكِ بَغِيًّا ﴿٢٨﴾

28. Ewe dada wa Harun! Baba yako hakuwa mtu muovu wala mama yako hakuwa kahaba.

فَأَشَارَتْ إِلَيْهِ قَالُوا كَيْفَ نُكَلِّمُ مَن كَانَ فِي الْمَهْدِ صَبِيًّا ﴿٢٩﴾

29. Ndipo Akashiria kwake, Wakasema: Tutamsemezaje aliye bado mdogo susuni?

قَالَ إِنِّي عَبْدُ اللَّـهِ آتَانِيَ الْكِتَابَ وَجَعَلَنِي نَبِيًّا ﴿٣٠﴾

30. Akasema: Hakika mimi ni mja wa Mwenyezi Mungu amenipa Kitabu na amenifanya nabii.

وَجَعَلَنِي مُبَارَكًا أَيْنَ مَا كُنتُ وَأَوْصَانِي بِالصَّلَاةِ وَالزَّكَاةِ مَا دُمْتُ حَيًّا ﴿٣١﴾

31. Na amenijaalia ni mwenye popote pale niwapo. Na ameniusia Swala na Zaka muda wa kuwa niko hai.

وَبَرًّا بِوَالِدَتِي وَلَمْ يَجْعَلْنِي جَبَّارًا شَقِيًّا ﴿٣٢﴾

32. Na kumtendea mema mama yangu, Wala hakunifanya niwe jeuri muovu.

وَالسَّلَامُ عَلَيَّ يَوْمَ وُلِدتُّ وَيَوْمَ أَمُوتُ وَيَوْمَ أُبْعَثُ حَيًّا ﴿٣٣﴾

33. Na amani iwe juu yangu, siku niliyozaliwa na siku nitakayokufa na siku nitakay- ofufuliwa.

ذَٰلِكَ عِيسَى ابْنُ مَرْيَمَ قَوْلَ الْحَقِّ الَّذِي فِيهِ يَمْتَرُونَ ﴿٣٤﴾

34. Huyo ndiye Isa Mwana wa Maryam, kauli ya haki ambayo wanaifanyia shaka.

مَا كَانَ لِلَّـهِ أَن يَتَّخِذَ مِن وَلَدٍ سُبْحَانَهُ إِذَا قَضَىٰ أَمْرًا فَإِنَّمَا يَقُولُ لَهُ كُن فَيَكُونُ ﴿٣٥﴾

35. Haiwi kwa Mwenyezi Mungu Kuwa na mwana, Yeye ametakasika! Anapolipitisha jambo basi huliambia tu: Kuwa! Likawa.

UMELETA KITU CHA AJABU

Aya 27 – 35

MAANA

Akaenda naye kwa jamaa zake amembeba.

Baada ya Maryam kuzaa, alimbeba mwanawe kwenda naye kwa watu wake, akiwa na utulivu bila ya kuwa na wasiwasi; kwani mimba ambayo ilikuwa ni sababu ya kutuhumiwa kwake, sasa ndiyo yenye ushahidi wa kweli wa usafi wake.

Wakasema: Ewe Maryamu! Hakika umeleta kitu cha ajabu kwa kudai kupata mimba bila ya kuguswa na mtu, huo ni uzushi.

Ewe dada wa Harun ! Huyu ni nduguye Musa, na yeye Maryam ni katika kizazi chao. Makusudio ya kumtaja ni kuwa asili yake ni watu wema na kwamba shina likiwa zuri matawi pia yanatakiwa yawe mazuri, sasa imekuwaje kutokewa na yaliyomtokea ambayo hakuna mfano aliyetokewa na hayo?

Baba yako hakuwa mtu muovu wala mama yako hakuwa kahaba.

Unafanana na nani wewe kwa kitendo chako hiki? Hawezi kufanya hivi ila binti wa muovu au wa mama muovu.

Ndipo akaishiria kwake

Yaani kwa mtoto aweze kushuhudia usafi wake naye ni mkweli zaidi ya wanaoshuhudia, kwa sababu anatamka kwa lugha ya Mwenyezi Mungu.

Wakasema kwa mshangao; Tutamsemezaje aliye bado mdogo susuni?

Lakini yule aliye susuni alianza kuwasemesha kabla wao hawajaanza na akasema:

Hakika mimi ni mja wa Mwenyezi Mungu amenipa Kitabu na amenifanya ni nabii.

Yaani atanifanya ni nabii baadaye, kwa sababu kitoto kichanga hakiwezi kuongoza watu na kuwa ni hoja kwao. Ikiwa yeye mwenyewe hana majukumu kwa kauli yake wala vitendo vyake. Atawezaje kuwa na majukumu ya kufikisha risala ya Mwenyezi Mungu kwa waja wa Mwenyezi Mungu?

Huko nyuma tumesema kuwa alitumwa kuwa Mtume akiwa na miaka 30; na kwamba alizungumza utotoni ili kumsafisha mama yake na tuhuma ya zina na uchafu; si kwa kuwa alikuwa ni nabii aliyetumwa, Angalia kifungu ‘Isa na utume wa utoto’ katika Juz.7 (5:109 –111).

Na amenijaalia ni mwenye kubarikiwa popote pale niwapo.

Kila anayewanufaisha watu kwa namna moja au nyingine basi ni mweye kubarikiwa na kila mwenye kumdhuru mtu mmoja - sikwambii watu wengi- basi huyo ni muovu na mfisadi.

Na ameniusia Swala na Zaka muda wakuwa niko hai na kumtendea mema mama yangu.

Yeye mwenyewe anakiri utumishi na utiifu kwa Mungu na kukana kuwa ni Mungu, mwana wa Mungu au mshirika wake; kama wanavyodai wanaswara (wakristo).

Wala hakunifanya niwe jeuri muovu; kama wanavyodai mayahudi. Bali ni mja mwema na Mtume; kama wanvyoitakidi waislamu.

Na amani iwe juu yangu, siku niliyozaliwa na siku nitakayokufa na siku nitakayofufuliwa.

Umepita punde mfano wake katika Aya 15 ya sura hii.

Huyo ndiye Isa mwana wa Maryam, kauli ya haki ambayo wanaifanyia shaka.

Hili ndilo neno la kweli, la kielimu na la kiadilifu, kuhusu Bwana Masih.

Sio mjeuri kama wanavyosema mayahudi; wala si Mungu, mwanawe au mshirika wake; kama wasemavyo wanaswara. Yeye ni Nabii anayefikisha risala ya Mola wake na ni mja miongoni mwa waja wake, anaswali na kutoa Zaka. Vile vile yeye ni mwenye kubarikia anayewanufaisha watu. Pia ni mnyenyekevu anayemfanyia wema mama yake.

Haiwi kwa Mwenyezi Mungu kuwa na mwana, Yeye ametakasika! Anapolipitisha jambo basi huliambia tu: Kuwa! Likawa

Lau Mwenyezi Mungu angelikuwa na watoto wangelijifichia kheri zote na baraka na kuzizuia wengine wasizipate. Pia wangeharibu yale aliyoten- geneza vizuri baba na ulimwengu wangeliujaza shari na upotevu; sawa na wanavyofanya baadhi ya watoto wa viongozi siku hizi. Umepita mfano wake katika Juz. 3 (3:59) na katika Juz.15 (18: 111).

وَإِنَّ اللَّـهَ رَبِّي وَرَبُّكُمْ فَاعْبُدُوهُ هَـٰذَا صِرَاطٌ مُّسْتَقِيمٌ ﴿٣٦﴾

36. Na Hakika Mwenyezi Mungu ni Mola wangu na Mola Wenu, Basi muabuduni, Hii ndio njia iliyonyooka.

فَاخْتَلَفَ الْأَحْزَابُ مِن بَيْنِهِمْ فَوَيْلٌ لِّلَّذِينَ كَفَرُوا مِن مَّشْهَدِ يَوْمٍ عَظِيمٍ ﴿٣٧﴾

37. Lakini Makundi yakahitilafiana baina yao, Basi ole wao waliokufuru kuhudhuria siku iliyo kuu.

أَسْمِعْ بِهِمْ وَأَبْصِرْ يَوْمَ يَأْتُونَنَا لَـٰكِنِ الظَّالِمُونَ الْيَوْمَ فِي ضَلَالٍ مُّبِينٍ ﴿٣٨﴾

38. Watasikia na wataona vizuri vilioje siku watakayotufikia! Lakini madhalimu leo wako katika upotofu uliodhahiri.

وَأَنذِرْهُمْ يَوْمَ الْحَسْرَةِ إِذْ قُضِيَ الْأَمْرُ وَهُمْ فِي غَفْلَةٍ وَهُمْ لَا يُؤْمِنُونَ ﴿٣٩﴾

39. Na waonye siku ya majuto itakapopitishwa amri nao wamo katika ghafla wala hawaamini.

إِنَّا نَحْنُ نَرِثُ الْأَرْضَ وَمَنْ عَلَيْهَا وَإِلَيْنَا يُرْجَعُونَ ﴿٤٠﴾

40. Hakika sisi tutairithi ardhi na walio juu yake na kwetu sisi wata rejeshwa.

NJIA ILIYONYOOKA

Aya 36 – 40

MAANA

Na hakika Mwenyezi Mungu ni Mola wangu na Mola wenu, basi muabuduni, Hii ndio njia iliyonyooka.

Aya hii inaungana na kauli ya Isa (hakika mimi ni mja wa Mwenyezi Mungu...) anawaamuru, kwenye kauli hii, wamwabudu Mungu mmoja wala wasimshirikishe na kitu chochote na kwamaba dini ya tawhid (kumpwekesha Mungu) ndio njia iliyo sawa; mwenye kuifuata ataokoka na mwenye kuiacha atapotea.

Lakini makundi yakahitilafiana baina yao.

Makundi hayo ni kaumu ya Isa. Kuna kundi lililosema kuwa Isa ni Mungu alishuka ardhini kisha akapanda mbinguni, kundi la pili likasema kuwa ni mwana wa Mungu na kundi la tatu likasema ni mja wa Mwenyezi Mungu. Tofauti ilikuwepo hapo zamani, lakini hivi sasa makundi yote yameafikiana kuwa Isa ni Mungu.

Basi ole wao waliokufuru kuhudhuria siku iliyo kuu

Makusudio ya waliokufuru hapa ni kundi la kwanza na la pili. Aya hii ni ibara nyingine ya kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu:

ذَٰلِكَ ظَنُّ الَّذِينَ كَفَرُوا فَوَيْلٌ لِّلَّذِينَ كَفَرُوا مِنَ النَّارِ ﴿٢٧﴾

“Hiyo ni dhana ya waliokufuru ole wao waliokufuru na moto.”(38:27).

Watasikia na wataona vizuri vilioje siku watakayotufikia!

Makafiri watakapoiona adhabu siku ya Kiyama watasema:

رَبَّنَا أَبْصَرْنَا وَسَمِعْنَا فَارْجِعْنَا نَعْمَلْ صَالِحًا إِنَّا مُوقِنُونَ ﴿١٢﴾

“Mola wetu! Tumeshaona na tumeshasikia, Turejeshe tukatende mema, kwani hakika sisi tumekwishakuwa na yakini”(32:12).

Walipokuwa wakilinganiwa kwenye haki walikuwa wakisema:

قُلُوبُنَا فِي أَكِنَّةٍ مِّمَّا تَدْعُونَا إِلَيْهِ وَفِي آذَانِنَا وَقْرٌ ﴿٥﴾

“Nyoyo zetu zimo katika vifuniko kwa hayo unayotuitia na masikio yetu yana uziwi” (41:5)

Lakini madhalimu leo wako katika upotofu ulio dhahiri.

Makusudio ya leo hapa, ni siku ya Kiyama; na upotofu ni adhabu, kwa vile siku hiyo hakutakuwa na njia ya uongofu wala upotofu; bali ni hisabu na malipo, hakuna zaidi ya hivyo.

Na waonye siku ya majuto itakapopitishwa amri nao wamo katika ghafla wala hawaamini

Anaaambiwa Mtume(s.a.w.w) awaonye, Siku ya majuto ni Kiyama. Imeitwa hivyo kwa sababu nafsi yenye hatia siku hiyo itasema:

يَا حَسْرَتَىٰ عَلَىٰ مَا فَرَّطتُ فِي جَنبِ اللَّـهِ وَإِن كُنتُ لَمِنَ السَّاخِرِينَ ﴿٥٦﴾

“Ee majuto yangu kwa yale niliyoyapoteza upande wa Mwenyezi Mungu na hakika nilikuwa miongoni mwa wanofanya maskhara.”(39:56).

Amri itapitishwa siku hiyo ambapo hakutakuwa na kubatilika wala kurejea. Wao hivi sasa wameghafilika, kwani wanaweza kujirudi kufuru yao na upotevu wao, wamuombe Mwenyezi Mungu msamaha, lakini wao hawafanyi, na wameendelea na uasi wao.

Kauli yake Mwenyezi Mungu:wala hawaamini, ni kuwa wao hawaisadiki kauli yetu, kwamba wao watafufuliwa, bali wanapeta vichwa vyao huku wakifanya maskhara.

Hakika sisi tutairithi ardhi na walio juu yake na kwetu sisi watarejeshwa.

Ardhi na vilivyomo ni vya Mwenyezi Mungu, hakuna yeyote mwenye kumiliki kitu. Binadamu ni mpita njia tu. Na kila kilicho mikononi mwa mtu ni cha kuazimwa tu, ana majukumu na kuwajibika nacho ili ahisabiwe kwacho.

Kwa ufupi Aya hii inarudufu neno: “Hakika sisi ni wa Mwenyezi Mungu, na Kwake Yeye tutarejea.” Juz. 2 (2:156). Makusudio yake ni kumhadharisha muasi, kumkemea na kupunguza huzuni ya Mtume(s.a.w.w) na uchungu wake kwa kupingwa mwito wake.

وَاذْكُرْ فِي الْكِتَابِ إِبْرَاهِيمَ إِنَّهُ كَانَ صِدِّيقًا نَّبِيًّا ﴿٤١﴾

41. Na mtaje Ibrahi mkatika Kitabu hakika yeye alikuwa mkweli sana, Nabii.

إِذْ قَالَ لِأَبِيهِ يَا أَبَتِ لِمَ تَعْبُدُ مَا لَا يَسْمَعُ وَلَا يُبْصِرُ وَلَا يُغْنِي عَنكَ شَيْئًا ﴿٤٢﴾

42. Alipomwambia baba yake: Ewe baba yangu! Kwa nini Unaabudu visivyosikia na visivyoona na visivyokufaa na chochote.

يَا أَبَتِ إِنِّي قَدْ جَاءَنِي مِنَ الْعِلْمِ مَا لَمْ يَأْتِكَ فَاتَّبِعْنِي أَهْدِكَ صِرَاطًا سَوِيًّا ﴿٤٣﴾

43. Ewe baba yangu! Hakika imenifikia elimu isyokufikia wewe, Basi nifuate mimi nitakuongoza njia iliyo sawa.

يَا أَبَتِ لَا تَعْبُدِ الشَّيْطَانَ إِنَّ الشَّيْطَانَ كَانَ لِلرَّحْمَـٰنِ عَصِيًّا ﴿٤٤﴾

44. Ewe baba yangu! Usiabudu Shetani. Hakika shetani ni Mwenye kumuasi Mwingi wa rehema.

يَا أَبَتِ إِنِّي أَخَافُ أَن يَمَسَّكَ عَذَابٌ مِّنَ الرَّحْمَـٰنِ فَتَكُونَ لِلشَّيْطَانِ وَلِيًّا ﴿٤٥﴾

45. Ewe baba yangu! Mimi nakuhofia isikupate adhabu ya Mwingi wa rehema ukawa ni walii washetani.

قَالَ أَرَاغِبٌ أَنتَ عَنْ آلِهَتِي يَا إِبْرَاهِيمُ لَئِن لَّمْ تَنتَهِ لَأَرْجُمَنَّكَ وَاهْجُرْنِي مَلِيًّا ﴿٤٦﴾

46. Akasema: Unaichukia miungu yangu ewe Ibrahim! Kama hutakoma, Basi lazima nitakupiga mawe na niondokelee mbali kwa muda.

قَالَ سَلَامٌ عَلَيْكَ سَأَسْتَغْفِرُ لَكَ رَبِّي إِنَّهُ كَانَ بِي حَفِيًّا ﴿٤٧﴾

47. Akasema Ibrahim: Amani iwe juu yako (salamun alayka)! Nitakuombea msamaha kwa Mola wangu Hakika yeye ananihurumia sana.

وَأَعْتَزِلُكُمْ وَمَا تَدْعُونَ مِن دُونِ اللَّـهِ وَأَدْعُو رَبِّي عَسَىٰ أَلَّا أَكُونَ بِدُعَاءِ رَبِّي شَقِيًّا ﴿٤٨﴾

48. Nami na ajitenga nanyi na hayo mnayoyaabudu badala ya Mwenyez Mungu na ninamuomba Mola wangu asaa nisiwe na bahati mbaya.

فَلَمَّا اعْتَزَلَهُمْ وَمَا يَعْبُدُونَ مِن دُونِ اللَّـهِ وَهَبْنَا لَهُ إِسْحَاقَ وَيَعْقُوبَ وَكُلًّا جَعَلْنَا نَبِيًّا ﴿٤٩﴾

49. Alipojitenga nao na yale wanayoyaabudu badala ya Mwenyezi Mungu, tulimpa Is-haq na Ya’qub na kila mmoja tukamfanya nabii.

وَوَهَبْنَا لَهُم مِّن رَّحْمَتِنَا وَجَعَلْنَا لَهُمْ لِسَانَ صِدْقٍ عَلِيًّا ﴿٥٠﴾

50. Na tukawapa katika rehema zetu na tukawajaalia kuwa na sifa za kweli tukufu.

IBRAHIM

Aya 41-50

MAANA

Na mtaje Ibrahim katika Kitabu hakika yeye alikuwa mkweli sana, Nabii.

Makusudio ya Kitabu hapa ni Qur’an. Ukweli ni sifa bora na ya ukamilifu zaidi. Tunalolifahamu kutokana na wasifu wa utume baada ya ukweli, ni kuwa yeye kwa maumbile yake ni mkweli hata kama si mtume.

Katika Juz; 7: (6:74) tumetaja tofauti za maulama katika makusudio ya baba wa Ibrahim, aliyetajwa katika Qur’an, kuwa je, ni baba yake wa hakika au ni baba wa kimajazi au ni ndugu wa baba? Tukasema huko, kuwa hakuna faida ya mzozo huu na kwamba lililo wajib kwa mwislamu ni kuamini utume wa Ibrahim(a.s) . Ama kuitakidi uislamu wa baba yake hilo halihusiani na dini; hasa kwa kuwa dhahiri ya Qur’an inafahamisha ukafiri wake.

Kwa vyovyote iwavyo, ni kuwa Ibrahim alimpa mwito baba yake, awe wa kimajazi au wa kihakika, wa uislamu na akamwambia katika yale aliyomwambia:

Ewe baba yangu! Kwa nini unaabudu visivyosikia na visivyoona na visivyokufaa na chochote?

Baba yake alikuwa akiabudu masanamu, kwa hiyo akamuhoji kwa manti- ki ya kiakili na kimaumbile. Mawe yaliyonyamaza, hayadhuru wala kunufaisha, unayaabudu na kuyasujudia? Iko wapi akili yako na fahamu yako?

Ewe baba yangu! Hakika imenifikia elimu isiyokufikia wewe, Basi nifuate mimi nitakuongoza njia iliyo sawa.

Kila anayekataa ibada ya masanamu anakuwa na ufahamu na akili zaidi kuliko wanayoyaabudu; sikwambii tena mitume wanaopata elimu kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Ikiwa kutojua kunakuwa ni udhuru kwa yule asiyejua, lakini masanamu hayo yenyewe hayawezi kuacha udhuru kwa anayeyaabudu.

Ewe baba yangu! Usiabudu shetani. Hakika shetani ni Mwenye kumuasi Mwingi wa rehema.

Makusudio ya kumwabudu shetani ni kumtii, kwa sababu Mwenye kukitii kitu atakuwa amekiabudu; Kwa hiyo basi kila anayemuasi Mwenyezi Mungu atakuwa amemuabudu shetani.

Ewe baba yangu! Mimi nakuhofia isikupate adhabu ya Mwingi wa rehema ukawa ni walii wa shetani.

Walii wa shetani inaweza kuwa kwa maana ya kutawaliwa na shetani au kwa maana ya kuwa mtawala wa shetani katika kuabudu masanamu; sawa na kusema: watu wanajilinda na shetani na shetani anajilinda na watu. Katika makadirio yote, ni kuwa lengo ni kuhofisha na kuhadharisha kumtii shetani na kumfuata.

Akasema: Unaichukia miungu yangu ewe Ibrahim! kama hutakoma, basi lazima nitakupiga mawe na niondokelee mbali kwa muda.

Tulipokuwa tukisoma huko Najaf, siku moja tukiwa tumemzunguka mwal- imu wetu akifafanua maswala muhimu ya elimu ya misingi ya fiqh (Usuulul-fiqh) baada ya kuhakikisha kwamba wanafunzi wake wote wamefahamu, alihitimisha darasa, lakini ghafla mmoja wa wanafunzi akamuuliza swali ambalo lilikuwa mbali kabisa na maudhui ya darasa. Basi mwalimu akaachana naye akawaangalia wanafunzi wengine na akasema:

“Hapo zamani palikuwa na mwanafunzi mmoja aliyejifundisha masuala ya Swaumu kwa mwalimu kwa muda wa zaidi ya mwezi. Baada ya kumaliza darasa yake mwalimu akadhania kuwa mwanafunzi wake ameelewa kila kitu kinachohusiana na Swaumu, lakini mwanafunzi akamwambia umeeleza sana na ukafafanua masuala ya Swaumu, lakini hatukufahamu kuwa Swaumu inakuwa usiku au mchana?!”

Haya hasa ndiyo yaliyompata Ibrahim pamoja na baba yake. Baada ya kumpa dalili zote na kumbembeleza kwa kumwambia ‘ewe baba yangu’ mara nne, lakini alimjibu kwa kumwambia kuwa kweli umeazimia kutowaabudu miungu pamoja nami? Ikiwa ni kweli umeazimia hivi, basi mimi sina jengine ila nikurujumu na kukuua au uniondokelee mbali nisikuone machoni mwangu.

Akasema Ibrahim: Amani iwe juu yako (salamun alayka)! Nitakuombea msamaha kwa Mola wangu, Hakika yeye ananihurumia sana”

Yaani Mwenyezi Mungu anamwitikia maombi yake, Umetangulia mfano wake katika Juz:11 (9:114).

Nami najitenga nanyi na hayo mnayoyaabudu badala ya Mwenyezi Mungu na ninamuomba Mola wangu asaa nisiwe na bahati mbaya.

Ibrahim aliwabughudhi watu wake kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, na akawaondokea kwa ajili ya Mwenyezi Mungu. Mwenyezi Mungu akambadilisha familia bora kuliko wao, pale alipompa Is-haq na baada yake Ya’qub bin Is-haq na akawatukuza kwa utume.

Hayo ndio makusudio ya kauli yake Mwenyezi Mungu:

Alipojitenga nao na yale wanayoyaabudu badala ya Mwenyezi Mungu, tulimpa Is-haq na baada ya Is-haq ni Ya’qub na kila mmoja tukamfanya Nabii.

Hakuna aliyeacha kitu katika mambo ya dunia kwa kutengeneza dini yake ila humbadilishia bora zaidi yake.

Na tukawapa katika rehema zetu

Mwenyezi Mungu hakubainisha aina ya alichowapa, kwa sababu neno rehema zetu linaashiria hilo. Inatosha kuwa ni zawadi radhi za Mwenyezi Mungu na neema zake.

Na tukawajaalia kuwa na sifa za kweli tukufu.

Makusudio ya sifa za kweli ni sifa wanazozikariri watu kizazi baada ya kizazi kusifia Ibrahim, Is-haq, Ismail na Ya’qub.

Aya hizi zinatia mkazo kwamba mwenye kumfanyia ikhlasi Mungu naye Mungu humsafisha na anakuwa pamoja naye popote alipo; sawa na alivyomfanyia Ibrahim(a.s) .


3

4

5

6

7