TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA SITA Juzuu 16

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA SITA0%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA SITA Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: Qurani tukufu

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA SITA

Mwandishi: Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya
: HASANI MWALUPA
Kundi:

Matembeleo: 10535
Pakua: 2580


Maelezo zaidi:

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 14 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 10535 / Pakua: 2580
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA SITA

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA SITA Juzuu 16

Mwandishi:
Swahili

8

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA SITA

قَالَ قَدْ أُوتِيتَ سُؤْلَكَ يَا مُوسَىٰ ﴿٣٦﴾

36. Akasema: Hakika umepewa maombi yako ewe Musa

وَلَقَدْ مَنَنَّا عَلَيْكَ مَرَّةً أُخْرَىٰ ﴿٣٧﴾

37. Na hakika tulikwisha kuneemesha mara nyingine

إِذْ أَوْحَيْنَا إِلَىٰ أُمِّكَ مَا يُوحَىٰ ﴿٣٨﴾

38. Pale tulipompa wahyi mama yako yale yaliyotolewa wahyi

أَنِ اقْذِفِيهِ فِي التَّابُوتِ فَاقْذِفِيهِ فِي الْيَمِّ فَلْيُلْقِهِ الْيَمُّ بِالسَّاحِلِ يَأْخُذْهُ عَدُوٌّ لِّي وَعَدُوٌّ لَّهُ وَأَلْقَيْتُ عَلَيْكَ مَحَبَّةً مِّنِّي وَلِتُصْنَعَ عَلَىٰ عَيْنِي ﴿٣٩﴾

39. Kwamba mtie katika kisanduku kisha kitupe mtoni na mto utamfikisha ufukweni. Atamchukua adui yangu na adui yake. Na nimekutilia mapenzi kutoka kwangu na ili ulelewe machoni mwangu

إِذْ تَمْشِي أُخْتُكَ فَتَقُولُ هَلْ أَدُلُّكُمْ عَلَىٰ مَن يَكْفُلُهُ فَرَجَعْنَاكَ إِلَىٰ أُمِّكَ كَيْ تَقَرَّ عَيْنُهَا وَلَا تَحْزَنَ وَقَتَلْتَ نَفْسًا فَنَجَّيْنَاكَ مِنَ الْغَمِّ وَفَتَنَّاكَ فُتُونًا فَلَبِثْتَ سِنِينَ فِي أَهْلِ مَدْيَنَ ثُمَّ جِئْتَ عَلَىٰ قَدَرٍ يَا مُوسَىٰ ﴿٤٠﴾

40. Dada yako alipokwenda na akasema: Je, niwajulishe mtu wa kuweza kumlea? Basi tukakurujesha kwa mama yako, ili macho yake yaburudike wala asihuzunike, Na ulimuua mtu nasi tukakuokoa katika dhiki. Na tukakujaribu kwa majaribio. Ukakaa miaka kwa watu Madyana. Kisha ukaja kama ilivyokadiriwa ewe Musa

وَاصْطَنَعْتُكَ لِنَفْسِي ﴿٤١﴾

41. Na nimekuchagua kwa ajili yangu.

UMEPEWA MAOMBI YAKO EWE MUSA

Aya 36 – 41

MAANA

Akasema: Hakika umepewa maombi yako ewe Musa, ya kukunjuliwa kifua, kufanyiwa wepesi kazi, kufunguka ulimi, kuongezewa nguvu kwa nduguyo na kushirikishwa kwenye utume pamoja nawe. Imam Aliy(a.s) anasema: “Kuwa kwenye lile usilolitaraji kuwa unalitarajia zaidi kuliko lile unalolitaraji. Kwani Musa Bin Imran alitoka akitafuta moto, akazungumza na Mwenyezi Mungu akarejea akiwa ni Mtume”

Na hakika tulikwisha kuneemesha mara nyingine.

Neema za Mwenyezi Mungu (s.w.t) kwa Musa zilkuwa nyingi; miongoni mwazo ni hizi zifuatazo:-

Pale tulipompa wahyi mama yako yale yaliyotolewa wahyi. Kwamba mtie katika kisanduku kisha kitupe mtoni na mto utamfikisha ufukweni. Atamchukua adui yangu na adui yake. Na nimekutilia mapenzi kutoka kwangu na ili ulelewe machoni mwangu

Makusudio ya wahyi hapa ni ilham – msukumo wa kufanya jambo. Macho ya Mwenyezi Mungu ni ulinzi wake.

Firauni alikuwa akimchinja kila anayezaliwa wa kiume katika waisrail na akizaliwa wa kike humfanya mjakazi. Mke wa Imran alipomzaa Musa alihofia Firauni, ndipo Mwenyezi Mungu akampa ilhamu ya kumweka kwenye sanduku kisha alitupe kwenye mto Nile, naye akafanya. Mungu akampa uthabiti wa moyo, Mto Nile ukalibebea sanduku hadi ufukweni. Inasemekana kuwa wajakazi wa Asiya, Mke wa Firaun, walitoka kwenda kuoga, wakakuta sanduku, wakalichukua. Mara tu mke wa Firauni alipolifungua na kuona mtoto, Mungu alimtia mahaba katika moyo wake:

وَقَالَتِ امْرَأَتُ فِرْعَوْنَ قُرَّتُ عَيْنٍ لِّي وَلَكَ لَا تَقْتُلُوهُ عَسَىٰ أَن يَنفَعَنَا أَوْ نَتَّخِذَهُ وَلَدًا وَهُمْ لَا يَشْعُرُونَ ﴿٩﴾

“Na mkewe Firauni akasema: Atakuwa kibirudisho cha macho kwangu na kwako. Msimuuwe! Huenda akatufaa au tumpange kuwa mtoto wetu” (28:9).

Kwa hiyo Faruni akambakisha na akalelewa katika kasri yake akilindwa na Mwenyezi Mungu.

Dada yako alipokwenda na akasema: Je, niwajulishe mtu wa kuweza kumlea? Basi tukakurujesha kwa mama yako, ili macho yake yaburudike wala asihuzunike.

Mwenyezi Mungu alitaka Musa arejee kwa mama yake, ili asiwe mbali naye na asiwe na wasiwasi, Mungu akitaka jambo, huliandalia sababu zake, Alizuwiya matiti yote yasiweze kumnyonyesha Musa, kiasi ambacho Firauni alihangaika.

Akaenda dada yake kwenye kasri ya Firauni na kusema mimi nitawafahamisha atakayemnyonyesha. Ndio akaenda na mama yake akakubali matiti yake, Firauni akamkabidhi na akampa ujira wake.

Na ulimuua mtu nasi tukakuokoa katika dhiki.

Siku moja Musa alikuwa akipita njiani, akawaona watu wawili wakipigana; mmoja ni wa upande wa Firaun na mmoja ni wa upande wake. Huyu wa upande wake akataka usaidizi kwa Musa, Akampiga ngumi yule mpin- zani, bila ya kukusudia kumuua, lakini akamuua, Musa akahofia kulipiziwa kisasi; Mwenyezi Mungu akamuondolea dhiki hiyo ya kisasi.

Haya yameashiriwa na Aya isemayo:

فَوَجَدَ فِيهَا رَجُلَيْنِ يَقْتَتِلَانِ هَـٰذَا مِن شِيعَتِهِ وَهَـٰذَا مِنْ عَدُوِّهِ فَاسْتَغَاثَهُ الَّذِي مِن شِيعَتِهِ عَلَى الَّذِي مِنْ عَدُوِّهِ فَوَكَزَهُ مُوسَىٰ فَقَضَىٰ عَلَيْهِ ﴿١٥﴾

“Akakuta humo watu wawili wanapigana – mmoja ni katika kundi lake na mwengine ni katika maadui zake, Yule mwenzake akamtaka msaada dhidi ya adui, Musa akampiga ngumi akammaliza.” (28:15).

Na tukakujaribu kwa majaribio.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) humjaribu mja wake kwa furaha na dhiki. Mwenye kushukuru hayo na akavumilia haya, humkurubisha na kumpa thawabu. Na ambaye hazijali neema na akakufuru wakati wa shida, Mwenyezi Mungu humweka mabali na rehema yake. Mwenyezi Mungu (s.w.t) Alimjaribu Musa kwa aina nyingi ya shida na misukosuko, akampata ni mwenye kuvumilia na mwenye kumkumbuka Mungu, ndipo Mwenyezi Mungu akamtukuza kwa utume na kamuinua daraja ya juu.

Ukakaa miaka kwa watu Madyana

Hapo ni baada ya kuchunga wanyama wa Shuayb, kama ilivyoashiria kauli yake Mwenyezi Mungu:

فَإِنْ أَتْمَمْتَ عَشْرًا فَمِنْ عِندِكَ ﴿٢٧﴾

“Kama ukitimiza kumi ni hiyari yako” (28:27)

Na aliitimiza kumi, kama inavyoelezwa katika baadhi ya riwaya.

Kisha ukaja kama ilivyokadiriwa ewe Musa.

Umekuja mahali hapa, kwenye jangwa takatifu la Tuwa; umekuja wakati ule alioukadiria Mwenyezi Mungu kukutuma wewe kwa utume.

Na nimekuchagua kwa ajili yangu.

Yaani nimekuchagua kwa ajili ya wahyi wangu na risala yangu. Kutegemezwa Musa kwa Mwenyezi Mungu ni ukomo wa utukufu na hes- hima; ambapo inaashiria kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) amemjalia ni katika watu wake mahususi.

اذْهَبْ أَنتَ وَأَخُوكَ بِآيَاتِي وَلَا تَنِيَا فِي ذِكْرِي ﴿٤٢﴾

42. Nenda wewe na nduguyo pamoja na ishara zangu, wala msichoke kunikumbuka.

اذْهَبَا إِلَىٰ فِرْعَوْنَ إِنَّهُ طَغَىٰ ﴿٤٣﴾

43. Nendeni kwa Firauni, hakika yeye amepituka mipaka.

فَقُولَا لَهُ قَوْلًا لَّيِّنًا لَّعَلَّهُ يَتَذَكَّرُ أَوْ يَخْشَىٰ ﴿٤٤﴾

44. Mwambieni maneno laini, huenda akazingatia au akaogopa.

قَالَا رَبَّنَا إِنَّنَا نَخَافُ أَن يَفْرُطَ عَلَيْنَا أَوْ أَن يَطْغَىٰ ﴿٤٥﴾

45. Wakasema: ewe Mola wetu! Hakika sisi tunaogopa asije akapindukia mipaka juu yetu au kufanya jeuri.

قَالَ لَا تَخَافَا إِنَّنِي مَعَكُمَا أَسْمَعُ وَأَرَىٰ ﴿٤٦﴾

46. Akasema: msiogope! Hakika mimi niko pamoja nanyi. Nasikia na ninaona.

فَأْتِيَاهُ فَقُولَا إِنَّا رَسُولَا رَبِّكَ فَأَرْسِلْ مَعَنَا بَنِي إِسْرَائِيلَ وَلَا تُعَذِّبْهُمْ قَدْ جِئْنَاكَ بِآيَةٍ مِّن رَّبِّكَ وَالسَّلَامُ عَلَىٰ مَنِ اتَّبَعَ الْهُدَىٰ ﴿٤٧﴾

47. Basi mwendeeni na mumwambie: hakika sisi ni wajumbe wa Mola wako, basi tuachie wana wa israil wala usiwaadhibu. Tumekuletea ishara itokayo kwa Mola wako, Na amani itakuwa juu ya aliyefuata uongofu.

إِنَّا قَدْ أُوحِيَ إِلَيْنَا أَنَّ الْعَذَابَ عَلَىٰ مَن كَذَّبَ وَتَوَلَّىٰ ﴿٤٨﴾

48. Hakika tumepewa wahyi kwamba adhabu itampata anayekadhibisha na akapu- uza.

NENDA WEWE NA NDUGUYO

Aya 42-48

MAANA

Nenda wewe na nduguyo pamoja na ishara zangu, wala msichoke kunikumbuka.

Makusudio ya ishara hapa ni miujiza, amabayo ni fimbo, mkono mweupe na miujiza mingineyo, tuliyoiashiria katika Juz. 15 (17:101). Maana ya msichoke kunikumbuka ni msipuuze risala yangu na kukumbusha amri yangu na makatazo yangu.

Nendeni kwa Firauni, hakika yeye amepituka mipaka.

Nendeni ni kusisitiza ile kauli ya ‘nenda wewe na nduguyo.’ Umetangulia mfano wa Aya hii katika Aya ya 23 ya sura hii tuliyo nayo.

Mwambieni maneno laini, huenda akazingatia au akaogopa.

Kama wenye mashirika ya ukandamizaji watazingatia na kuogopa, basi Firauni angelizingatia na kuogopa.

Aya hii inapangilia mfumo wa kutoa mwito wa dini ya Mwenyezi Mungu. Kwa usahihi zaidi; inapanga mfumo wa kukinaisha haki. Mfano wake ni kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu:

ادْعُ إِلَىٰ سَبِيلِ رَبِّكَ بِالْحِكْمَةِ وَالْمَوْعِظَةِ الْحَسَنَةِ وَجَادِلْهُم بِالَّتِي هِيَ أَحْسَنُ ﴿١٢٥﴾

“Waite kwenye njia ya Mola wako kwa hekima na mawaidha mazuri na ujadiliane nao kwa namna iliyo bora.” Juz. 14(16:125).

Mawaidha mazuri ni kujua mwenye hatia, makosa yake na mpotevu kujua ubaya wake na kujiona kuwa yuko mbali na haki na hali halisi ya mambo:

وَقَالُوا لَوْ كُنَّا نَسْمَعُ أَوْ نَعْقِلُ مَا كُنَّا فِي أَصْحَابِ السَّعِيرِ ﴿١٠﴾

“Na watasema: lau tungelikuwa tunasikia au kuwa na akili, tusingelikuwa katika watu wa motoni” (67:10)

Sharti la kwanza la mawaidha mazuri ni kutotaka lolote anayetoa mwaid- ha, zaidi ya kutengeneza. Kwamba lengo la kwanza na la mwisho liwe ni kuongoza na kurekebisha.

Sharti la pili ni kuwa mawaidha kwa kauli laini. Miongoni mwa aliyoyasema Musa kwa Firauni ni: Je, unapenda kujitakasa? Nami nitakuongoza kwa Mola wako upate kumcha.(79:19).

Wakasema: Ewe Mola wetu! Hakika sisi tunaogopa asije akapindukia mipaka juu yetu au kufanya jeuri.

Ewe Mola wetu unajua ubabe wa Firauni na kwamba hakuna anayeweza kumzuia akiamrisha tuuawe kabla hata hajasikia dalili na hoja tutaka- zomwambia, Je unaweza kutuongeza kitu kitakachohakikisha usalama wetu?

Akasema: msiogope! Hakika mimi niko pamoja nanyi. Nasikia na ninaona.

Mimi ninadhamini usalama wenu, ‘Mwenyezi Mungu ni tosha wa kuhi- fadhi na kunusuru’ Unaweza kuuliza kuwa dhamiri ya wakasema: ni ya wawili, Musa na Harun, na inajulikana kuwa Harun hakuwa na Musa katika majibizano, sasa je, kuna wajihi gani wa hilo?

Baadhi ya wafasiri wamejibu kuwa kauli hii ilikuwa ni ya Musa kwa kusema na ya Harun kwa kihali; Kwa sababu Harun anamfuata Musa. Inawezekana kauli hii inatokana na wote wawili pamoja baada ya kuondoka Musa kwenda Misr na kuungana na nduguye, kabla hawajakwenda kwa Firani. Ni kawaida ya Qur’an kuacha maneno ambayo yatafahamika kutokana na mazingira au na maneno mengine.

Basi mwendeeni na mumwambie: hakika sisi ni wajumbe wa Mola wako, basi tuachie wana wa israil wala usiwaadhibu kwa kuwachukua mateka, kuwadhalilisha, kuwachinja watoto wao wa kiume na kuwatumia watoto wao wa kike. Umetangulia mfano wa Aya hii katika Juz.9 (7:104 –105).

Tumekuletea ishara itokayo kuwa Mola wako, kwa dalili za kutosha na hoja mkataa juu ya ukweli wetu.

Na amani itakuwa juu ya aliyefuata uongofu.

Uingofu ni dini ya Mwenyezi Mungu na amani ni kusalimika na adhabu yake. Yaani mwenye kuingia dini ya Mwenyezi Mungu amesalimika na adhabu ya kuungua.

Hakika tumepewa wahyi kwamba adhabu itampata anayekadhibisha na akapuuza.

Ni makemeo na maonyo kwa Firauni kuwa ataangamia na kubomoka kama atampuuz Musa na Harun kwa kuukana utume wao na kuenedelea kwenye upotevu wake na jeuri yake.

قَالَ فَمَن رَّبُّكُمَا يَا مُوسَىٰ ﴿٤٩﴾

49. Akasema: Basi Mola wenu ni nani ewe Musa?

قَالَ رَبُّنَا الَّذِي أَعْطَىٰ كُلَّ شَيْءٍ خَلْقَهُ ثُمَّ هَدَىٰ ﴿٥٠﴾

50. Akasema: Mola wetu ni yule aliyekipa kila kitu umbo lake kisha akakiongoza

قَالَ فَمَا بَالُ الْقُرُونِ الْأُولَىٰ ﴿٥١﴾

51. Akasema Nini hali ya karne za mwanzo?

قَالَ عِلْمُهَا عِندَ رَبِّي فِي كِتَابٍ لَّا يَضِلُّ رَبِّي وَلَا يَنسَى ﴿٥٢﴾

52. Akasema: Elimu yake iko kwa Mola wangu katika Kitabu, Mola wangu hapotei wala hasahau.

الَّذِي جَعَلَ لَكُمُ الْأَرْضَ مَهْدًا وَسَلَكَ لَكُمْ فِيهَا سُبُلًا وَأَنزَلَ مِنَ السَّمَاءِ مَاءً فَأَخْرَجْنَا بِهِ أَزْوَاجًا مِّن نَّبَاتٍ شَتَّىٰ ﴿٥٣﴾

53. Ambaye amewafanyia ardhi kuwa tandiko, Na akawapitishia humo njia, Na akateremsha kutoka mbinguni maji, Na kwayo tukatoa namna mbali mbali za mimea.

كُلُوا وَارْعَوْا أَنْعَامَكُمْ إِنَّ فِي ذَٰلِكَ لَآيَاتٍ لِّأُولِي النُّهَىٰ ﴿٥٤﴾

54. Kuleni na mchunge wanyama wenu. Hakika katika hayo zipo ishara kwa wenye akili

مِنْهَا خَلَقْنَاكُمْ وَفِيهَا نُعِيدُكُمْ وَمِنْهَا نُخْرِجُكُمْ تَارَةً أُخْرَىٰ ﴿٥٥﴾

55. Kutokana nayo tumewaumba na humo tumewarudisha na kutoka humo tutawatoa mara nyingine.

وَلَقَدْ أَرَيْنَاهُ آيَاتِنَا كُلَّهَا فَكَذَّبَ وَأَبَىٰ ﴿٥٦﴾

56. Hakika tulimwonyesha ishara zetu zote, lakini alikadhibisha na akakataa.

NI YUPI HUYO MOLA WENU?

Aya 49 -56

MAANA

Akasema: Basi Mola wenu ni nani ewe Musa?

Musa na Harun walikwenda kwa Firauni kama walivyoamrishwa na Mwenyezi Mungu, wakamwambia kuwa sisi ni mitume wa Mola wako, tumekujia na hoja na dalili kuthibitisha ukweli wetu. Basi ukiingia kwenye dini ya Mwenyezi Mungu utasalimika na ghadhabu ya Mwenyezi Mungu na adhabu yake; vinginevyo, utakuwa miongoni mwa watakaoangamia.

Hii ilikuwa mara ya kwanza Firauni kusikia neno ‘Mola wako’ kwa sababu yeye hakubali kuwa kuna mola; kama anavyodai kuwa yeye ndiye Mola Mtukufu. Ndio maana akauliza: Ni nani huyo Mola aliyekutuma kwangu?

Akasema: Mola wetu ni yule aliyekipa kila kitu umbo lake kisha akakiongoza

Musa alimjibu Firauni swali lake, kuwa Mola wetu ni yule aliyeumba viumbe akavipa sura na akazifanya nzuri sura zake bila ya kuwa na msaidizi kwenye hilo. Ndiye ambaye amekifanya kila kiumbe kibakie na hali yake. Amesema Imam Aliy(a.s) : “Je, hamuangalii kile kidogo jinsi Mungu alivyokiumba na akapingilia vizuri umbile lake, akakiumbia usikizi na uoni na akakifanyia mifupa na nyama.

Ni kama kwamba Musa anamwambia Firauni: Hakika Mola ni yule aliyeumba vitu kutokana na kutokuwa na chochote. Sasa wewe ni wapi na wapi na huyu? Ni kama ilivyomtokea Ibrahim na Namrud:

قَالَ إِبْرَاهِيمُ فَإِنَّ اللَّـهَ يَأْتِي بِالشَّمْسِ مِنَ الْمَشْرِقِ فَأْتِ بِهَا مِنَ الْمَغْرِبِ فَبُهِتَ الَّذِي كَفَرَ ﴿٢٥٨﴾

“Ibrahim akasema: Hakika Mwenyezi Mungu hulichomoza jua mashariki, basi wewe lichomoze magharibi, Akafedheheka yule aliyekufuru” Juz; 3 (2:258)

Akasema – Firauni – Nini hali ya karne za mwanzo?

Karne za mwanzo anakusudia watu wa Nuh, A’d, Thamud na wengineo ambao walikuwa wakiabudu masanamu badala ya Mwenyezi Mungu. Firauni alitaka, kwa jawabu hili, kumrudi Musa, kwamba lau kungelikuwa na Mungu kwa sifa amabazo umezitaja, basi wangelimwabudu watu waliopita, na tunajua kuwa wao walikuwa wakiabudu masanamu.

Jawabu hili linajipinga lenyewe; Kwa sababu kutoa dalili ya kutokuweko Mungu kwa ibada ya masanamu, ni sawa na poponundu, na upofu wake, kupinga kuweko jua.

Akasema: Elimu yake iko kwa Mola wangu katika Kitabu; Mola wangu hapotei wala hasahau.

Musa alimjibu Firauni kuwa mimi sina ujuzi wa ghaibu mpaka nikupe habari za uma zilizopita. Mwenyezi Mungu peke yake ndiye mwenye ujuzi wa kila kitu na ujuzi wake daima hauingiliwi na mabadiliko wala kugeuka:

يَوْمَ يَبْعَثُهُمُ اللَّـهُ جَمِيعًا فَيُنَبِّئُهُم بِمَا عَمِلُوا أَحْصَاهُ اللَّـهُ وَنَسُوهُ وَاللَّـهُ عَلَىٰ كُلِّ شَيْءٍ شَهِيدٌ ﴿٦﴾

“Siku atakapowafufua Mwenyezi Mungu awaambie yale waliyokuwa wakaiyatenda, Mwenyezi Mungu ameyadhibiti na wao wameyasahau, Na Mwenyezi Mungu ni mwenye kushuhudia kila kitu” (58:6).

Unaweza kuuliza kuwa : Musa alikuwa na uhakika kuwa waabudu masanamu walikuwa katika upotevu, kwanini hakumwambia Firauni kuwa walikuwa kwenye upotevu na badala yake akamwambia Mwenyezi Mungu ndiye ajuye hali yao?

Jibu : Lau angelisema kuwa watu wa karne za kwanza walikuwa wapotevu, Firauni angelimtaka dalili ya kuwakinaisha waliopo au awe na hoja ambayo wasingeweza kuipinga na wakati huo Musa hakuwa nayo. Ndio maana akamjibu Firauni yale ambayo asingeyatakia dalili.

Ambaye amewafanyia ardhi kuwa tandiko.

Umekwishatangulia ufafanuzi wa kutandikwa ardhi na kufanywa kwake tandiko katika Juz.13 (13:3)

Na akawapitishia humo njia ya kufuatia matumizi yenu, Na akateremsha kutoka mbinguni maji; Na kwayo tukatoa namna mbali mbali za mimea

Umetangulia mfano wake katika Juz. 7 (6:99).

Kuleni na mchunge wanyama wenu. Hakika katika hayo zipo ishara kwa wenye akili

Makusudio ya ishara ni dalili za kuweko Mwenyezi Mungu Mtukufu. Wenye akili ni wale wenye busara. Mwenyezi Mungu amewahusisha kuwataja hapa kwa sababu wao wanaipata haki wakiwa wamejiepusha na hawa na matamanio.

Kuna Hadith ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (s.a.w.), kwamba yeye amesema: “Hakika wabora wenu ni wale wenye akili. Wakasema: Ninani hao wenye akili ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu? Akasema ni wale wenye khulka njema, walio makini, wenye kuwapatiliza mafukara, mayatima na majirani, wanawalisha chakula na wanadhihirisha maamkuzi kwa watu”

Kutokana nayo tumewaumba na humo tumewarudisha na kutoka humo tutawatoa mara nyingine.

Mtu ni mtoto wa ardhi kwa mwili wake. Ndiyo mada ya kuumbwa kwake na humo mnatoka chakula chake na kinywaji chake na juu yake anakwenda na kurudi. Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) anasema:“Ardhi ni mama yenu na ni mlezi wenu.”

Ni mama yetu kwa vile tumetokana nayo na ni mlezi wetu kwa vile inatulisha, kama anavyonyonyesha mama mtoto wake. Kisha tutarudi ardhini baada ya kufa, tuwe mchanga kama ilivyokuwa mwanzo, tena tuwe hai mara ya pili kwa ajili ya hisabu na malipo.

Hakika tulimwonyesha ishara zetu zote, lakini alikadhibisha na akakataa.

Aliyeonyeshwa ni Firauni. Makusudio ya ishara ni miujiza aliyoidhihirisha Mwenyezi Mungu mikononi mwa Musa na ikafahamisha waziwazi juu ya ukweli wa utume wake. Lakini itafaa wapi miujiza na maonyo yakigongana na masilahi na manufaa?

9

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA SITA

قَالَ أَجِئْتَنَا لِتُخْرِجَنَا مِنْ أَرْضِنَا بِسِحْرِكَ يَا مُوسَىٰ ﴿٥٧﴾

57. Akasema: Ewe Musa! Hivi umetujia kututoa katika nchi yetu kwa uchawi wako?

فَلَنَأْتِيَنَّكَ بِسِحْرٍ مِّثْلِهِ فَاجْعَلْ بَيْنَنَا وَبَيْنَكَ مَوْعِدًا لَّا نُخْلِفُهُ نَحْنُ وَلَا أَنتَ مَكَانًا سُوًى ﴿٥٨﴾

58. Basi hakika tutakuletea uchawi kama huo. Basi weka miadi baina yetu na wewe ambayo hatutaivunja sisi wala wewe, mahali patakapokuwa sawa.

قَالَ مَوْعِدُكُمْ يَوْمُ الزِّينَةِ وَأَن يُحْشَرَ النَّاسُ ضُحًى ﴿٥٩﴾

59. Akasema: Miadi yenu ni siku ya sikukuu na watu wakusanywe kabla ya adhuhuri

فَتَوَلَّىٰ فِرْعَوْنُ فَجَمَعَ كَيْدَهُ ثُمَّ أَتَىٰ ﴿٦٠﴾

60. Basi Firauni akarudi na akatengeneza hila yake, kisha akaja.

قَالَ لَهُم مُّوسَىٰ وَيْلَكُمْ لَا تَفْتَرُوا عَلَى اللَّـهِ كَذِبًا فَيُسْحِتَكُم بِعَذَابٍ وَقَدْ خَابَ مَنِ افْتَرَىٰ ﴿٦١﴾

61. Musa akawaambia: Ole wenu! Msimzulie Mwenyezi Mungu uwongo, asije akawafutilia mbali kwa adhabu, hakika ameshindwa mwenye kuzua.

فَتَنَازَعُوا أَمْرَهُم بَيْنَهُمْ وَأَسَرُّوا النَّجْوَىٰ ﴿٦٢﴾

62. Basi wakazozana kwa shauri yao wenyewe kwa wenyewe na wakanon’gona kwa siri.

قَالُوا إِنْ هَـٰذَانِ لَسَاحِرَانِ يُرِيدَانِ أَن يُخْرِجَاكُم مِّنْ أَرْضِكُم بِسِحْرِهِمَا وَيَذْهَبَا بِطَرِيقَتِكُمُ الْمُثْلَىٰ ﴿٦٣﴾

63. Wakasema: Hakika hawa wawili ni wachawi, wanataka kuwatoa katika nchi yenu kwa uchawi wao na waondoe njia yenu iliyo bora.

فَأَجْمِعُوا كَيْدَكُمْ ثُمَّ ائْتُوا صَفًّا وَقَدْ أَفْلَحَ الْيَوْمَ مَنِ اسْتَعْلَىٰ ﴿٦٤﴾

64. Kwa hiyo kusanyeni hila zenu zote, kisha mfike kwa kujipanga safu, na kwa hakika leo atafuzu atakayeshinda.

FIRAUNI ANAWAKUSANYA WACHAWI

Aya 57 – 64

MAANA

Akasema: Ewe Musa! Hivi umetujia kututoa katika nchi yetu kwa uchawi wako?

Firauni aligongwa na hoja asizoweza kuzijibu alipokabiliana na Musa. Vipi ataweza kuzijibu nazo ni katika ishara za Mwenyezi Mungu? Firauni alikuwa akijua wazi kuwa Musa na Harun si wachawi na kwamba uchawi hauwezi kumtoa mtu nchini mwake na kwenye ufalme wake.

Kama wachawi wangelikuwa na uwezo huu basi wangelikuwa ndio watawala kila wakati na kila mahali. Lakini Firauni aliposhindwa kujibu mapigo, alikimbila hila, ujanja ujanja, uwongo na uzushi; sawa wanavyofanya leo wakoloni na vibaraka wao, wanapowaita wakombozi kuwa ni waharibifu na wenye nia safi kuwa ni wafanya fujo.

Basi hakika tutakuletea uchawi kama huo. Weka miadi baina yetu na wewe ambayo hatutaivunja sisi wala wewe, mahali patakapokuwa sawa.

Firauni alimtaka Musa apange siku ya mapambano baina yake na wachawi, yawe mahali palipo wazi kila mtu aweze kuona mapambano hayo na kuyafuatilia.

Akasema: Miadi yenu ni siku ya sikukuu na watu wakusanywe kabla ya adhuhuri.

Musa alichagua siku ya sikukuu ndio iwe mapambano baina yake na wachawi, ambapo watu hawatakuwa na kazi waweze kukusanyika na akachaguwa wakati baina ya asubuhi na mchana, kwa vile ndio wakati mzuri wa kukusanyika watu; huku akiwa anataka kuidhihirisha haki na kuivunja batili.

Basi Firauni akarudi na akatengeneza hila yake, kisha akaja.

Aya hii pamoja na ufupi wake ina ubainifu mkubwana na inachukua maana nyingi. ‘Akarudi, akatengeneza, akaja’ Neno akarudi, linaelezea kuondoka Firauni kwenda kwa wasaidizi wake na kushauriana kupanga mipango.

Neno akatengeneza linaelezea kutuma wajumbe katika pembe zote za nchi kutafuta wachawi na kuwaleta. Mshauri wake alimshauri afanye hivyo; kama inavyoashiria Aya katika Juz. 9 (7:112). Na neno akaja, linaelezea kuja kwake na majigambo yake kwenye uwanja wa mapambano.

Musa akawaambia: Ole wenu! Msimzulie Mwenyezi Mungu uwongo, asije akawafutilia mbali kwa adhabu, hakika ameshindwa mwenye kuzua.

Musa alitanguliza nasaha na onyo kwa wachawi kabla ya kuanza kazi yoyote ya uchawi na akawahadharisha na kuondolewa mbali na adhabu kama wataendele kuwadanganya watu na kuwavunga; kisha akawafahamisha kuwa kadiri Firauni alivyo na nguvu ya utawala, lakini ni mdhaifu sana wa kuweza kuwadhuru au kuwanufaisha.

Basi wakazozana kwa shauri yao wenyewe kwa wenyewe na wakanon’gona kwa siri.

Waliozozana ni wachawi. Aya hii inaashiria kuwa baadhi ya wachawi waliathirika na maneno ya Musa au angalau waliingia shaka. Katika Tafsir Aya hii inaashiria kwamba baadhi ya wachawi waliathirika na maneno ya Musa(a.s) , Au angalau yalitia shaka katika nafsi zao. Katika Attabariy imeelezwa kuwa wachawi walisema kutokana na tahadhari ya Musa kuwa maneno haya siyo ya mchawi.

Ni kweli kwamba maneno yakitoka kwenye moyo wa mwenye ikhlasi huchukua mkondo kuelekea kwenye moyo wa mwenye ikhlasi. Waliathirika baadhi ya wachawi kwa mawaidha ya Musa, wakaanza kupingana wenyewe, Kama kawaida yalipita majadiliano kuwa je, waendelee au wasiendelee.

Majadiliano haya yalipita kwa siri asisikie Musa wala Firauni. Lakini mwisho walioshinda ni wale waliong’ang’ania kuendelea na upinzani, kwa dalili ya alivyowasimulia Mwenyezi Mungu:

Wakasema: Hakika hawa wawili ni wachawi, wanataka kuwatoa katika nchi yenu kwa uchawi wao na waondoe njia yenu iliyo bora. Kwa hiyo kusanyeni hila zenu zote, kisha mfike kwa kujipanga safu, na kwa hakika leo atafuzu atakayeshinda.

Maneno yote haya ni ya wachawi na hawa wawili wanawakusudia Musa na Harun. Makusudio ya njia iliyo bora ni dini, kwa dalili ya Aya nyingine isemayo:

“Na Firauni akaema: Niacheni nimuuwe Musa naye amwite Mola wake, mimi nahofia asije kuwabadilishia dini yenu” (40:26).

Maana ni kuwa baadhi ya wachawi walisema kuwa Musa na Haruna ni mahodari katika fani ya uchawi kwa hiyo wanataka watushinde ili waimalize dini yetu wabakie wao ndio mabwana katika miji na wawatawale watu wawe watumwa wao.

Kwa hiyo basi hatuna budi tuwe na mshikamano dhidi yao na tutoe juhudi zetu zote ili tuwashinde, tuwe na cheo siku hii ya leo inayoshuhudiwa.

قَالُوا يَا مُوسَىٰ إِمَّا أَن تُلْقِيَ وَإِمَّا أَن نَّكُونَ أَوَّلَ مَنْ أَلْقَىٰ ﴿٦٥﴾

65. Wakasema: Ewe Musa! Je, utatupa wewe au tutakuwa sisi wa kwanza kutupa?

قَالَ بَلْ أَلْقُوا فَإِذَا حِبَالُهُمْ وَعِصِيُّهُمْ يُخَيَّلُ إِلَيْهِ مِن سِحْرِهِمْ أَنَّهَا تَسْعَىٰ ﴿٦٦﴾

66. Akasema; bali tupeni nyinyi! Mara kamba zao na fimbo zao zikaonekana, kwa uchawi, kuwa zinakwenda mbio.

فَأَوْجَسَ فِي نَفْسِهِ خِيفَةً مُّوسَىٰ ﴿٦٧﴾

67. Basi Musa akaingia hofu katika nafsi yake.

قُلْنَا لَا تَخَفْ إِنَّكَ أَنتَ الْأَعْلَىٰ ﴿٦٨﴾

68. Tukasema; usihofu hakika wewe ndiye utakayeshinda.

وَأَلْقِ مَا فِي يَمِينِكَ تَلْقَفْ مَا صَنَعُوا إِنَّمَا صَنَعُوا كَيْدُ سَاحِرٍ وَلَا يُفْلِحُ السَّاحِرُ حَيْثُ أَتَىٰ ﴿٦٩﴾

69. Na kitupe kilicho kuumeni kwako, kitavimeza walivyovitengeneza, hakika walivyovitengeneza ni hila za mchawi tu, na mchawi hafanikiwi popote aendapo.

فَأُلْقِيَ السَّحَرَةُ سُجَّدًا قَالُوا آمَنَّا بِرَبِّ هَارُونَ وَمُوسَىٰ ﴿٧٠﴾

70. Basi wachawi wakaangushwa kusujudi. Wakasema:tumemwamini Mola wa Haruna na Musa!

قَالَ آمَنتُمْ لَهُ قَبْلَ أَنْ آذَنَ لَكُمْ إِنَّهُ لَكَبِيرُكُمُ الَّذِي عَلَّمَكُمُ السِّحْرَ فَلَأُقَطِّعَنَّ أَيْدِيَكُمْ وَأَرْجُلَكُم مِّنْ خِلَافٍ وَلَأُصَلِّبَنَّكُمْ فِي جُذُوعِ النَّخْلِ وَلَتَعْلَمُنَّ أَيُّنَا أَشَدُّ عَذَابًا وَأَبْقَىٰ ﴿٧١﴾

71. Akasema: Mumemwamini kabla sijawapa ruhusa! Hakika huyo ni mkubwa wenu aliyewafundisha uchawi. Nitawakata mikono yenu na miguu yenu kwa kubadilisha, kisha nitawasu- lubu kwenye vigogo vya mitende. Na hapo kwa yakini mtajua ni nani katika sisi ni mkali wa adhabu na kuiendeleza?

قَالُوا لَن نُّؤْثِرَكَ عَلَىٰ مَا جَاءَنَا مِنَ الْبَيِّنَاتِ وَالَّذِي فَطَرَنَا فَاقْضِ مَا أَنتَ قَاضٍ إِنَّمَا تَقْضِي هَـٰذِهِ الْحَيَاةَ الدُّنْيَا ﴿٧٢﴾

72. Wakasema: Hatutaathirika nawe katika ishara waziwazi zilizotujia na yule aliyetuumba. Basi hukumu utakavyohukumu; kwani wewe unahukumu maisha haya ya duniani tu

إِنَّا آمَنَّا بِرَبِّنَا لِيَغْفِرَ لَنَا خَطَايَانَا وَمَا أَكْرَهْتَنَا عَلَيْهِ مِنَ السِّحْرِ وَاللَّـهُ خَيْرٌ وَأَبْقَىٰ ﴿٧٣﴾

73. Hakika sisi tumemwamini Mola wetu ili atusamehe makosa yetu na uchawi uliotulazimisha kuufanya na Mwenyezi Mungu ndiye Mbora na mwenye kudumu zaidi.

إِنَّهُ مَن يَأْتِ رَبَّهُ مُجْرِمًا فَإِنَّ لَهُ جَهَنَّمَ لَا يَمُوتُ فِيهَا وَلَا يَحْيَىٰ ﴿٧٤﴾

74. Hakika atakayemjia Mola wake naye ni mhalifu, basi kwa hakika yake ni Jahannamu, Hafi humo wala haishi.

وَمَن يَأْتِهِ مُؤْمِنًا قَدْ عَمِلَ الصَّالِحَاتِ فَأُولَـٰئِكَ لَهُمُ الدَّرَجَاتُ الْعُلَىٰ ﴿٧٥﴾

75. Na atakayemjia naye ni mumin aliyetenda mema basi hao ndio wenye daraja za juu

جَنَّاتُ عَدْنٍ تَجْرِي مِن تَحْتِهَا الْأَنْهَارُ خَالِدِينَ فِيهَا وَذَٰلِكَ جَزَاءُ مَن تَزَكَّىٰ ﴿٧٦﴾

76. Bustani za milele zipitazo mito chini yake, watadumu humo milele na hayo ni malipo ya mwenye kujitakasa.

BAINA YA MUSA NA WACHAWI

Aya 65 – 76

MAANA

Wakasema: Ewe Musa! Je, utatupa wewe au tutakuwa sisi wa kwanza kutupa? Akasema; bali tupeni nyinyi! Mara kamba zao na fimbo zao zikaonekana, kwa uchawi, kuwa zinakwenda mbio.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 9 (7:113).

Basi Musa akaingia hofu katika nafsi yake.

Wafasiri wengi wamesema kuwa Musa alihofia nafsi yake, kama ilivyo kawaida ya maumbile, lakini ilivyo hasa hakuhofia nafsi yake. Vipi iwe hivyo naye anajua kuwa wachawi ni wazushi na kwamba Mwenyezi Mungu alimwambia yeye na nduguye kuwa mimi niko pamoja nanyi! Ispokuwa alihofiwa mambo yasivurugike na watu wakachanganyikiwa wakadanganyika na uchawi.

Tukasema; usihofu hakika wewe ndiye utakayeshinda.

Usihofu kuwa watu watachanganyikiwa, hapana! Macho na akili zitafunukiwa kuwa wewe uko katika haki na wao ni wabatilifu; hata wachawi wenyewe watakiri kuwa wewe ni mkweli mwaminifu na kwamba wao ni wazushi, wenye vitimbi na hadaa; na Firauni ndiye aliyewalazimisha.

Na kitupe kilicho kuumeni kwako, kitavimeza walivyovitengeneza, hakika walivyovitengeneza ni hila za mchawi tu, na mchawi hafanikiwi popote aendapo, Basi wachawi wakaangushwa kusujudi. Wakasema: tumemwamini Mola wa Haruna na Musa! Akasema: mumemwamini kabla sijawapa ruhusa! Hakika huyo ni mkubwa wenu aliyewafundisha uchawi. Nitawakata mikono yenu na miguu yenu kwa kubadilisha, kisha nitawasulubu kwenye vigogo vya mitende. Na hapo kwa yakini mtajua ni nani katika sisi ni mkali wa adhabu na kuiendeleza?

Umetangulia mfano wake katika Juz. 9 (7:117)

Wakasema: Hatutaathirika nawe katika ishara waziwazi zilizotujia na yule aliyetuumba.

Firauni alitaka wachawi wamwache Mwenyezi Mungu wamfuate yeye baada ya kufunukiwa na upotevu wake. Wakasema ni kitu gani basi kinaweza kutuathiri! Je, ni hiyo dunia yako, ambayo hata wewe mwenyewe utaiacha, au ni vitisho vyako na adhabu yako, na hali adhabu ya Mwenyezi Mungu ni kubwa na kali?

Basi hukumu utakavyohukumu : Sisi hatuogopi vitisho vyako na mateso yako maadamu tuna yakini na Mola wetu;kwani wewe unahukumu maisha haya ya duniani tu, yawe tamu au chungu. Na sisi si watoto wa dunia isipokuwa ni wa Akhera, ambayo itabaki na wala wewe huna mamlaka huko hata ya kujitetea wewe mwenyewe.

Hivi ndivyo anavyokuwa kila mwenye ikhlasi, haogopi upanga wa wachinjaji kwa ajili ya dini yake na misimamo yake. Ni muhali kabisa kuishi dini au misimamo yoyote ikiwa hakuna watu wa aina hii.

Hakika sisi tumemwamini Mola wetu ili atusamehe makosa yetu na uchawi uliotulazimisha kuufanya na Mwenyezi Mungu ndiye Mbora na mwenye kudumu zaidi kuliko wewe Firauni.

Mapambano yalikuwa yanaonyesha kuwa ni baina Musa na wachawi, lakini kiuhakika hasa yalikuwa ni baina ya chama cha Mwenyezi Mungu na cha shetani.

Katika raundi ya kwanza tu walishuhudia watazamaji, akiwe- mo Firauni na wachawi, kuwa chama cha Mwenyezi Mungu ndio mshindi. Wachawi wakatangaza kuwa wao wamehakikisha haya kwa ujuzi usio na shaka. Na kwamba wao walikuwa kwenye upotevu kwa kumpinga Musa; na Firauni ndiye aliyewaelekeza hayo na kuwalazimisha, Wakamwomba msamaha Mwenyezi Mungu.

Kuomba msamaha kwa wachawi ni dalili wazi kuwa mchawi hana nguvu yoyote; isipokuwa ni kuvungavunga na upotevu; kama alivyosema Mwenyezi Mungu: ‘zikaonekana, kwa uchawi, kuwa zinakwenda mbio.’

Hakika atakayemjia Mola wake naye ni mhalifu, basi kwa hakika, yake ni Jahannamu. Hafi humo wala haishi.

Hili ni fumbo la kudumu na adhabu. Mfano wake ni Aya isemayo: “Hawatamalizwa wakafa wala hawatapunguziwa adhabu yake. (35:36).

Neno mhalifu linatumika kwa kila mwenye kufanya ufisadi na uovu katika kauli au vitendo; awe kafiri au asiwe kafiri. Dalili ya kuwa makusudio ya mhalifu yanaenea ni kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu:

Na atakayemjia naye ni mumin aliyetenda mema basi hao ndio wenye daraja za juu ambapo amekutanisha imani na matendo mema. Maana yake ni kuwa imani bila ya matendo haimnufaishi mwenye nayo.

Kwa maneno mengine ni kuwa waumini ni wale walio wema katika makusudio yao na matendo yao. Ama wale wanaohangaika katika ardhi kufanya ufisadi wao wako katika kundi la wahalifu; hata kama wataijaza ardhi kwa tahlili na takbir.

Bustani za milele zipitazo mito chini yake, watadumu humo milele na hayo ni malipo ya mwenye kujitakasa

Bustani (Pepo) na daraja za juu mbele ya Mwenyezi Mungu ni za wale waliozitakasa nafsi zao kwa mapenzi na ikhlasi kwa watu wote na kuzitwaharisha na kila aina ya khiyana tamaa na karaha. Kuna mamia ya Aya zenye maana hii kwa uwazi na kwa ishara.

وَلَقَدْ أَوْحَيْنَا إِلَىٰ مُوسَىٰ أَنْ أَسْرِ بِعِبَادِي فَاضْرِبْ لَهُمْ طَرِيقًا فِي الْبَحْرِ يَبَسًا لَّا تَخَافُ دَرَكًا وَلَا تَخْشَىٰ ﴿٧٧﴾

77. Na tulimpa wahyi Musa: Toka usiku na waja wangu na uwapigie njia kavu baharini, usikhofu kukamatwa wala usiogope.

فَأَتْبَعَهُمْ فِرْعَوْنُ بِجُنُودِهِ فَغَشِيَهُم مِّنَ الْيَمِّ مَا غَشِيَهُمْ ﴿٧٨﴾

78. Firauni akawafuata pamoja na majeshi yake, Basi kiliwafudikiza baharini kilichowafudikiza.

وَأَضَلَّ فِرْعَوْنُ قَوْمَهُ وَمَا هَدَىٰ ﴿٧٩﴾

79. Na Firauni aliwapoteza watu wake na hakuwaongoza.

يَا بَنِي إِسْرَائِيلَ قَدْ أَنجَيْنَاكُم مِّنْ عَدُوِّكُمْ وَوَاعَدْنَاكُمْ جَانِبَ الطُّورِ الْأَيْمَنَ وَنَزَّلْنَا عَلَيْكُمُ الْمَنَّ وَالسَّلْوَىٰ ﴿٨٠﴾

80. Enyi wana wa israil! Hakika tuliwaokoa na adui yenu! Na tukawaahidi upande wa kuume wa mlima. Na tukawateremshia Manna na Salwa

كُلُوا مِن طَيِّبَاتِ مَا رَزَقْنَاكُمْ وَلَا تَطْغَوْا فِيهِ فَيَحِلَّ عَلَيْكُمْ غَضَبِي وَمَن يَحْلِلْ عَلَيْهِ غَضَبِي فَقَدْ هَوَىٰ ﴿٨١﴾

81. Kuleni katika vizuri tulivyowaruzuku, wala msipituke mipaka katika hayo isije ikawashukia ghadahabu yangu, Na inayemshukia ghadahabu yangu basi huyo amepotea.

وَإِنِّي لَغَفَّارٌ لِّمَن تَابَ وَآمَنَ وَعَمِلَ صَالِحًا ثُمَّ اهْتَدَىٰ ﴿٨٢﴾

82. Hakika mimi ni mwingi wa maghufira kwa anayetubia na akaamini na akatenda mema tena akaongoka.

WAPIGIE NJIA

Aya 77 – 82

MAANA

Na tulimpa wahyi Musa: Toka usiku na waja wangu na uwapigie njia kavu baharini, usikhofu kukamatwa wala usiogope.

Firauni aling’ang’ania inadi yake na akataa kila kitu isipokuwa kiburi na ujabari na kumpa sifa Musa kuwa ametoka nje na ni mchawi. Akapata wa kumuunga mkono katika hilo:

وَقَالَ الْمَلَأُ مِن قَوْمِ فِرْعَوْنَ أَتَذَرُ مُوسَىٰ وَقَوْمَهُ لِيُفْسِدُوا فِي الْأَرْضِ ﴿١٢٧﴾

“Na wakasema wakuu wa kaumu ya Fir’aun: Je, utamwacha Musa na watu wake walete uharibifu katika nchi.” Juz. 9 (7:127)

Firauni alishikilia kutaka kumuua Musa, ndipo Mwenyezi Mungu akampa wahyi atoke Misr usiku pamoja na wana waisrail na apige bahari kwa fimbo yake ipasuke itokee njia waifuate waisrail hadi upande mwengine wasalimike na maangamizi na Firauni na shari yake:

فَأَوْحَيْنَا إِلَىٰ مُوسَىٰ أَنِ اضْرِب بِّعَصَاكَ الْبَحْرَ فَانفَلَقَ فَكَانَ كُلُّ فِرْقٍ كَالطَّوْدِ الْعَظِيمِ ﴿٦٣﴾ وَأَزْلَفْنَا ثَمَّ الْآخَرِينَ ﴿٦٤﴾ وَأَنجَيْنَا مُوسَىٰ وَمَن مَّعَهُ أَجْمَعِينَ ﴿٦٥﴾ ثُمَّ أَغْرَقْنَا الْآخَرِينَ ﴿٦٦﴾

“Tulimletea wahyi Musa tukamwambia piga bahari kwa fimbo yako, Basi ikatengana, na kila seemu ikawa kama mlima mkubwa, Na tukawajongeza hapo wale wengine, Na tukamwokoa Musa na waliokuwa pamoja naye, Kisha tukawazamisha hao wengine” (26: 63 – 66).

Firauni akawafuata pamoja na majeshi yake; Basi kiliwafudikiza baharini kilichowafudikiza.

Kusema kiliwafudikiza kilichowafudikiza ni kulikuza jambo. Hapo kuna maneno mengi ya kukadiriwa; kama ilivyo kawaida ya Qur’an. Kwa sababu mfumo wa maneno unafahamisha hivyo.

Kukadirwa kwake ni: Musa alitoka na watu wake usiku. Alipofika baharini akapiga kwa fimbo yake na bahari ikapasuka kukawa na njia isiyokuwa na maji, wakaifuata waisrail. Firauni na jeshi lake wakawaandama. Walipofika waisrail upande wa pili na mjeshiya Firauni kuingia yote, bahari ilirudi wakafamaji wote na waisraili wakasalimika wote.

Na Firauni aliwapoteza watu wake na hakuwaongoza.

Aliwapoteza na haki na akawapoteza baharini vilevile. Hapo mwanzo alikuwa akiwaambia:

وَمَا أَهْدِيكُمْ إِلَّا سَبِيلَ الرَّشَادِ ﴿٢٩﴾

“Wala siwaongozi ila kwenye njia ya uongofu” (40:29)

Enyi wana wa israil! Hakika tuliwaokoa na adui yenu!

Firauni aliyekuwa akiwapa adhabu mbaya ya kuwachinja watoto wenu wa kiume na kuwaacha wanawake.

Na tukawaahidi upande wa kuume wa mlima.

Anaishiria Mwenyezi Mungu (s.w.t) ahadi aliyomwahidi Musa baada ya kufa maji Firauni, Ahadi yenyewe ni kwenda Musa upande wa mlimani, ateremshiwe Tawrat, amabayo ndani yake mna ubainifu wa sharia na hukumu.

Na tukawateremshia Manna na Salwa: Kuleni katika vizuri tulivyowaruzuku

Umetangulia mfano wake, kwa herufi zake, katika Juz. 1 (2:57)

Wala msipituke mipaka katika hayo isije ikawashukia ghadahabu yangu. Na inayemshukia ghadahabu yangu basi huyo amepotea.

Katika hayo ni hayo tuliyowaruzuku. Kupetuka mpaka katika hayo, ni kuchukua au kutoa kwa njia isiyokuwa yake ya kisharia.

Maana ni kuwa mwenye kuchuma mali kwa njia isiyokuwa ya halali au kuitumia kwa njia isiyokuwa ya halali, basi malipo yake mbele ya Mwenyezi Mungu ni maangamizi na adhabu ya kuunguza; sawa na Firauni na wengineo katika waasi walio mataghuti.

Hakika mimi ni mwingi wa maghufira kwa anayetubia na akaamini na akatenda mema tena akaongoka.

Mwenyezi Mungu husamehe madhambi kwa masharti mane:

1. Kwanza: kutubia nako ni kujuta kwa maasi yaliyokuwa pamoja na kuomba msamaha.

2. Pili: kuiamini haki, popote itakapokuwa na itakavyokuwa; ni sawa iafikiane na malengo yake au yahalifiane.

3. Tatu: kuitumia haki. Kwani imani bila ya matendo ni kama matamshi bila ya maana.

4. Nne: ni kuongoka. Makusudio yake ni kuendelea kuifuata haki mpaka kufa. Na hapa ndio tunapata jibu la mwenye kuuliza kuwa, kuna haja gani ya kuunganisha mwenye kuongoka na mwenye kuamini na akatenda mema.