TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA SABA Juzuu 17

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA SABA50%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA SABA Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: Qurani tukufu

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
  • Anza
  • Iliyopita
  • 15 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 9441 / Pakua: 4150
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA SABA

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA SABA Juzuu 17

Mwandishi:
Swahili

3

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA SABA

خُلِقَ الْإِنسَانُ مِنْ عَجَلٍ سَأُرِيكُمْ آيَاتِي فَلَا تَسْتَعْجِلُونِ ﴿٣٧﴾

37. Mtu amaeumbwa na haraka. Nitawaonyesha ishara zangu, basi msiniharakishe.

وَيَقُولُونَ مَتَىٰ هَـٰذَا الْوَعْدُ إِن كُنتُمْ صَادِقِينَ ﴿٣٨﴾

38. Na wanasema: Ahadi hii itatokea lini, ikiwa nyinyi mnasema kweli?

لَوْ يَعْلَمُ الَّذِينَ كَفَرُوا حِينَ لَا يَكُفُّونَ عَن وُجُوهِهِمُ النَّارَ وَلَا عَن ظُهُورِهِمْ وَلَا هُمْ يُنصَرُونَ ﴿٣٩﴾

39. Lau wangelijua wale ambao wamekufuru wakati ambao hawatauzuia moto na nyuso zao wala migongo yao na wala hawatanusuriwa.

بَلْ تَأْتِيهِم بَغْتَةً فَتَبْهَتُهُمْ فَلَا يَسْتَطِيعُونَ رَدَّهَا وَلَا هُمْ يُنظَرُونَ ﴿٤٠﴾

40. Bali kitawafikia ghafla, na kitawashtua na wala hawataweza kukirudisha wala hawatapewa muda.

وَلَقَدِ اسْتُهْزِئَ بِرُسُلٍ مِّن قَبْلِكَ فَحَاقَ بِالَّذِينَ سَخِرُوا مِنْهُم مَّا كَانُوا بِهِ يَسْتَهْزِئُونَ ﴿٤١﴾

41. Na hakika walifanyiwa stihzai Mitume kabla yako, kwa hiyo yakawazinga wale waliofanya miongoni mwao yale waliyokuwa wakiyafanyia sthizai.

قُلْ مَن يَكْلَؤُكُم بِاللَّيْلِ وَالنَّهَارِ مِنَ الرَّحْمَـٰنِ بَلْ هُمْ عَن ذِكْرِ رَبِّهِم مُّعْرِضُونَ ﴿٤٢﴾

42. Sema ni nani atakayewalinda usiku na mchana na Mwingi wa rehema? Bali wao wanapuuza kumkumbuka Mola wao.

أَمْ لَهُمْ آلِهَةٌ تَمْنَعُهُم مِّن دُونِنَا لَا يَسْتَطِيعُونَ نَصْرَ أَنفُسِهِمْ وَلَا هُم مِّنَّا يُصْحَبُونَ ﴿٤٣﴾

43. Au wao wana miungu watakaoweza kuwakinga nasi. Hao hawawezi kujinusuru wala hawatahifadhiwa nasi.

بَلْ مَتَّعْنَا هَـٰؤُلَاءِ وَآبَاءَهُمْ حَتَّىٰ طَالَ عَلَيْهِمُ الْعُمُرُ أَفَلَا يَرَوْنَ أَنَّا نَأْتِي الْأَرْضَ نَنقُصُهَا مِنْ أَطْرَافِهَا أَفَهُمُ الْغَالِبُونَ ﴿٤٤﴾

44. Bali tuliwastarehesha hawa na baba zao mpaka umri ukawa mrefu. Je, hawaoni kuwa tunaifikia ardhi tukiipunguza ncha zake; basi je, hao ni wenye kushinda?

MTU AMEUMBWA NA HARAKA

Aya 37 – 44

LUGHA

Kuna tofauti baina ya haraka na upesi upesi (chapuchapu). Haraka ni kufanya jambo kabla ya wakati wake. Upesi upesi ni kulifanya jambo mara tu unapofika wakati wake bila ya ngojangoja. Kulifanya jambo upesi upesi kunasifika. Mwenyezi Mungu anasema:

وَيُسَارِعُونَ فِي الْخَيْرَاتِ وَأُولَـٰئِكَ مِنَ الصَّالِحِينَ ﴿١١٤﴾

“Wanafanya upesiupeesi mambo ya kheri na hao ndio miongoni mwa watu wema.” Juz.4 (3:114)

Kuna kauli masuhuri isemayo: ‘Haraka inatokana na shetani[1]

MAANA

Mtu amaeumbwa na haraka. Nitawaonyesha ishara zangu, basi msini- harakishe.

Mtume(s.a.w.w) aliwahadharisha makafiri na matokeo ya ukafiri na akawahadharisha na adhabu ya Mwenyezi Mungu kama wakiendelea, lakini walizidi kiburi na inadi. Wakafanya masikhara ya kuharakisha adhabu.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) akawaambia, ngojeni mtaona ukweli wa Mtume wangu katika yale aliyowapa kiaga na akawahadharisha kuwa msiaharakie jambo ambalo litakuwa. Mara ngapi anayeharakia jambo likimfikia anatamani, lau lisingekuwa. Wafasiri wamesema, wakifafanua Aya hii, kuwa mtu ana maumbile ya kutaka haraka haraka, na kwamba hiyo iko katika mishipa yake na nyama yake.

Lakini kama ingelikuwa sawa hivyo, basi kusingepatikana utulivu wowote; bali kila mtu angelikuwa na haraka haraka katika kauli zake na vitendo vyake vyote, bila ya kubakia.

Ikiwa utamsifia mtu kwa haraka, kufuru au kukata tamaa n.k. utakuwa unafasiri silika yake katika baadhi ya hali zake, lakini sio kuwa ndio maumbile yake yote. Tumeyafafanua hayo kwa urefu, katika Juz. 12 (11:9) na Juz. 13 (14: 34).

Na wanasema: “Ahadi hii itatokea lini, ikiwa nyinyi mnasema kweli?

Umetangulia mfano wake katika Juz. 8 ( 7:70), Juz. 9 (7:107) na Juz. 12 (11: 32).

Lau wangelijua wale ambao wamekufuru wakati ambao hawatauzuia moto na nyuso zao wala migongo yao na wala hawatanusuriwa.

Makafiri wanaharakia adhabu na wao ni wadhaifu na wako duni kuweza kuizuia au kuweza kuikimbia. Watawezaje, nayo itawagubika kutoka juu yao hadi chini na mbele yao hadi nyuma?

Bali kitawafikia ghafla, na kitawashtua na wala hawataweza kukirudisha wala hawatapewa muda.

Kitakachowafikia ghafla ni Kiyama. Hakuna shaka kuwa kitawajia ghafla bila ya onyo lolote. Hiyo inatokana na kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu:

يَسْأَلُكَ النَّاسُ عَنِ السَّاعَةِ قُلْ إِنَّمَا عِلْمُهَا عِندَ اللَّـهِ ﴿٦٣﴾

“Wanakuuliza kuhusu saa (ya Kiyama). Sema hakika elimu yake iko kwa Mwenyezi Mungu tu.” (33:63).

Ikiwa kitakuja kwa hali hii basi ni lazima kilete mshtuko na mashangao. Kwa hiyo hawataweza kukizuia wala hakitawapa muda wa kupanga mambo yao.

Na hakika walifanyiwa stihzai Mitume kabla yako, kwa hiyo ya kawazinga wale waliofanya miongoni mwao yale waliyokuwa wakiyafanyia sthizai.

Imetangulia Aya hii katika Juz. 7 (6:10).

Sema: ni nani atakayewalinda usiku na mchana na Mwingi wa rehema.

Kadiri mtu atakavyochukua hadhari na kujificha hawezi kujilinda na mambo ya ghafla, isipokuwa kwa msaada wa Mwenyezi Mungu na tawfiki yake. Anawezaje kujilinda mtu na uwezo wa Mungu?

Bali wao wanapuuza kumkumbuka Mola wao.

Waliwafanyia sthizai Mitume wa Mwenyezi Mungu, wakajiaminisha na adhabu ya Mwenyezi Mungu na wakapuuza dhikri ya Mwenyezi Mungu; kwa nini? Kwa sababu wako kwenye starehe, wakiiona kuwa hiyo ni ngome ya kujihifadhi.

Au wao wana miungu watakaoweza kuwakinga nasi, kutokana na adhabu yetu tukitaka kuwaangamiza na kuwang’oa?

Hao hawawezi kujinusuru wala hawatahifadhiwa nasi.

Hao ni hao miungu wao. Kwa maana kwamba washirikina wanataka hifad- hi kwa masanamu, wakati hayo yenyewe hayawezi kujisaidia, hayawezi kujinufaisha na chochote, yatawezaje kumsaidia mwingine?

Katika Tafsirut-tabari imeelezwa kuwa watu wa taawili wametofautiana katika neno yusbihun. Baada ya kunukuu kauli kadhaa, alichagua maana ya kuhifadhiwa. Maana haya ndiyo yanayoafikiana na kauli yake Mwenyezi Mungu katika (23:88).

Bali tuliwastarehesha hawa na baba zao mpaka umri ukawa mrefu.

Mwenyezi Mungu amewapa muda na maisha wakaghurika na muda wakawa wajeuri na wabaya; hawajui kwamba Mwenyezi Mungu anawangoja na anawavuta polepole bila ya kujijua.

Je, hawaoni kuwa tunaifikia ardhi tukiipunguza ncha zake. Basi je, hao ni wenye kushinda?

Imetangulia pamoja na tafsiri yake katika Juz. 13: (13:41).

قُلْ إِنَّمَا أُنذِرُكُم بِالْوَحْيِ وَلَا يَسْمَعُ الصُّمُّ الدُّعَاءَ إِذَا مَا يُنذَرُونَ ﴿٤٥﴾

45. Sema: Hakika mimi ninawaonya kwa wahyi tu. Na viziwi hawasikii mwito wanapoonywa.

وَلَئِن مَّسَّتْهُمْ نَفْحَةٌ مِّنْ عَذَابِ رَبِّكَ لَيَقُولُنَّ يَا وَيْلَنَا إِنَّا كُنَّا ظَالِمِينَ ﴿٤٦﴾

46. Na watakapoguswa na mpulizo mmoja wa adhabu itokayo kwa Mola wako, bila shaka watasema: Ole wetu! Hakika tulikuwa ni wenye kudhulumu.

وَنَضَعُ الْمَوَازِينَ الْقِسْطَ لِيَوْمِ الْقِيَامَةِ فَلَا تُظْلَمُ نَفْسٌ شَيْئًا وَإِن كَانَ مِثْقَالَ حَبَّةٍ مِّنْ خَرْدَلٍ أَتَيْنَا بِهَا وَكَفَىٰ بِنَا حَاسِبِينَ ﴿٤٧﴾

47. Na tutaweka mizani ya uadilifu kwa siku ya Kiyama. Basi nafsi yoyote haitadhulumiwa kitu. Hata ikiwa ni chembe ya khardali tutaileta. Nasi tunatosha kuwa wenye kuhisabu.

وَلَقَدْ آتَيْنَا مُوسَىٰ وَهَارُونَ الْفُرْقَانَ وَضِيَاءً وَذِكْرًا لِّلْمُتَّقِينَ ﴿٤٨﴾

48. Na hakika tulimpa Musa na Harun, upambanuzi, mwangaza na ukumbusho kwa wenye takua.

الَّذِينَ يَخْشَوْنَ رَبَّهُم بِالْغَيْبِ وَهُم مِّنَ السَّاعَةِ مُشْفِقُونَ ﴿٤٩﴾

49. Ambao humwogopa Mola wao faraghani na wanaiogopa saa (ya Kiyama).

وَهَـٰذَا ذِكْرٌ مُّبَارَكٌ أَنزَلْنَاهُ أَفَأَنتُمْ لَهُ مُنكِرُونَ ﴿٥٠﴾

50. Na huu ni ukumbusho uliobarikiwa ulioteremshwa. Basi je, mnaukataa?

NAWAONYA KWA WAHYI

Aya 45 – 50

MAANA

Sema: Hakika mimi ninawaonya kwa wahyi tu. Na viziwi hawasikii mwito wanapoonywa.

Aya hii ni mfano wa kauli yake Mwenyezi Mungu:

وَقُلْ إِنِّي أَنَا النَّذِيرُ الْمُبِينُ ﴿٨٩﴾

“Na, sema: Hakika mimi ni muonyaji niliye dhahiri.” Juz. 14 (15:89).

Mwenyezi Mungu anamwamrisha Mtume wake mtukufu awaambie washirikina kuwa mnakifanyia masikhara Kiyama na vituko vyake na habari hiyo ni wahyi wa Mwenyezi Mungu sio mawazo au njozi. Mimi nawahadharisha kwa amri ya Mwenyezi Mungu sio kwa amri yangu. Lakini mtawezaji kusikia hadhari na maonyo na kwenye masiko yenu kuna uziwi.

Kila asiyeitikia nasaha za Mwenyezi Mungu basi huyo ni kipofu na kizizwi, hata kama ana macho na masikio.

Na watakapoguswa na mpulizo mmoja wa adhabu itokayo kwa Mola wako, bila shaka watasema: “Ole wetu! Hakika tulikuwa ni wenye kudhulumu.

Hapo mwanzo walikuwa wanapoonywa kwa adhabu, wakifanya masikhara na mizaha, lakini itakapowagusa kidogo tu wataanza kulalamika na kunyenyekea huku wakisema: ‘Ole wetu sisi tulikuwa madhalimu.’ Umetangulia mfano wake katika sura hii Aya 14.

MIZANI SIKU YA KIYAMA

Na tutaweka mizani ya uadilifu kwa siku ya Kiyama. Basi nafsi yoyote haitadhulumiwa kitu. Hata ikiwa ni chembe ya khardali tutaileta. Nasi tunatosha kuwa wenye kuhisabu.

Makusudio ya mizani hapa ni hukumu ya Mwenyezi Mungu na sharia yake. Maana ni kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) anapima matendo ya waja kwa amri zake na makatazo yake. Ambaye atafanya matendo yake kulinga na na amri na makatazo yake, basi ni katika ambao mizani zao zitakuwa nzito.

Imam Jafar As-Sadiq(a.s) aliulizwa kuhusu mizani za uadilifu, akasema ni manabii wa Mwenyezi Mungu na mawalii wake; yaani hukumu za Mwenyezi Mungu zinazofikishwa na mitume na mawalii katika waja wake.

Malipo yatakuwa kulingana na misingi hii; hazitapunguzwa thawabu za mwema hata chembe, pengine inawezekana kuzidishwa. Wala haitazidishwa adhabu ya muovu hata chembe, pengine inawezekana kupunguzwa.

Nasi tunatosha kuwa wenye kuhisabu, hatutaziki wala hakitupiti kitu kadiri idadi yake itakavyokuwa.

Mulla Sadra katika Kitabu Al-asfar anasema: “Uwezo wa Mwenyezi Mungu unafichua matendo yote ya waja wake na kipimo cha mema yao, maovu yao na thawabu zake na adhabu yake katika kitambo kidogo, naye ni mwepesi wa kuhisabu”

Kama ataizingatia Aya hii, mwenye kujaribu kuifuatishia Qur’an na sayansi, atasema kianzio cha fikra ya akili ya mashine ni Qur’an. Angalia kifungu cha ‘Qur’an na sayansi’ katika mwanzo wa Juzuu ya kwanza.

Mwenye Al-Asfar amezungumzia kwa urefu kuhusu mizani ya siku ya Kiyama. Kwa kuangalia uwezo wa mtungaji katika falsafa ya itikadi n.k. Tutachukukua baadhi ya ibara zake, kama ifuatavyo, pamoja na nyongeza kidogo kwa ajili ya ufafanuzi:

“Mizani ya Akhera ni ile ambayo hujulikana kwayo usahihi wa elimu, imani ya Mungu, sifa zake, vitendo vyake, malaika wake, mitume wake, vitabu vyake na siku ya mwisho.

Mizani hii ni Qur’an ambayo ameiteremsha mwalimu wa kwanza, ambaye ni Mwenyezi Mungu, kwa mwalimu wa tatu, ambaye ni Mtume, kupita kwa mwalimu wa pili ambaye ni Jibril.

Kwa hukumu ya Qur’an ndio hupimwa elimu ya mtu, akili yake, kauli na vitendo vyake vyote. Vile vile hujulikana mema yake na maovu yake. Ikiwa wema utazidi basi mwenyewe atakuwa ni katika wema na ikiwa uovu utazidi basi atakuwa katika waovu.

Ikiwa mema na maovu yatalingana, basi mwenyewe atangojea mpaka Mungu amuhukumie adhabu au msamaha, lakini upande wa hurumma ndio ulio na nguvu zaidi. Kwa sababu Mwenyezi Mungu ni mwingi wa maghufira Mwenye kurehemu”

Kisha akasema - mweneye Al-asfar – mahali pengine: “Kila kitu kina mizani isipokuwa neno: “Lailaha illa-llah, (Hapana Mola isipokuwa Allah) kwa sababu neno hilo la tawhid halina mkabala na jambo lolote isipokuwa shirk, na shirki haina mizani.”

Akaendelea kusema tena mahali pengine: “Hakika Qur’an ni kama meza yenye aina kwa aina ya vyakula, kuanzia vyakula halisi hadi maganda. Kile halisi ni hekima na dalili na kinahusika na wenye busara. Ama maganda ni ya walio mbumbumbu ambao ni kama wanyama; kama alivyosema Mwenyezi Mungu:

مَّتَاعًا لَّكُمْ وَلِأَنْعَامِكُمْ ﴿٣٢﴾

“Kwa ajili ya manufaa yenu na wanyama wenu.” (80:32).

Kwa haraka haraka mtu anaweza akadhani kuwa ibara ya maganda ni kukikosea adabu Kitabu cha Mwenyezi Mungu na utukufu wake, lakini mwenye Asfar yuko zaidi ya dhana na shakashaka. Mwenye kuyachunguza na kuyataamali maneno yake atajua kuwa makusudio ya maganda ni watu wa hayo maganda, kama wale wanaoganda kwenye dhahiri ya maneno bila ya kuangalia undani wake, hawaoni mbali zaidi ya pua zao, kwa dalili ya yale aliyoyaeleza alipokuwa akifafanua Hadith ya Mtume isemayo: “Qur’an ina dhahiri na batini.”

Hadith hii ameifafanua kwa maneno marefu; miongoni mwa maneno hayo ni haya yafutayo: “Hakika Qur’an ina daraja kama vile watu ambao wako wenye akili na wasiokuwa na akili. Asiye na akili ni kama yule anayechukua mambo kijujuu. Ama roho ya Qur’an na siri yake haigundui isipokuwa mwenye akili na busara. Kwa hiyo mgawanyiko unakuja kutokana na wanavyoifahamu Qur’an sio Qur’an yenyewe.

Na hakika tulimpa Musa na Harun, upambanuzi, mwangaza na ukumbusho kwa wenye takua.

Makusudio ya upambanuzi hapa ni Tawrat, kama alivyoiteremsha Mwenyezi Mungu kwa Musa. Kila Kitabu cha mbinguni ni upambanuzi, kwa sababu kinapambanua uongofu na upotevu, ni mwangaza wa kuondoa giza la ujinga na ukafiri na ukumbusho kwa mwenye kuitafuta takua, kwa sababu kina mkumbusha kuhusu Mwenyezi Mungu na kumbainishia halali na haramu.

Ambao humwogopa Mola wao faraghani na wanaiogopa saa (ya Kiyama).

Haya ndiyo maelezo ya wenye takua, kwamba wao wanamcha Mwenyezi Mungu kwa siri kusiko na watu; sawa na vile wanavyomcha dhahiri. Kwa vile wana imani siku ya Kiyama, hisabu na malipo, huku wakiiogopa siku hiyo na kuifanyia kazi.

Na huu ni ukumbusho uliobarikiwa ulioteremshwa.

Ni ukumbusho kwa mwenye kutaka kukumbuka, ni mawaidha kwa mwenye kuwaidhika na ni kheri kwa mwenye kuamrika na maarisho yake na kukatatiza kwa makatazo yake.

Basi je, mnaukataa?

Na hali hoja na dalili zake ziko wazi.

4

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA SABA

وَلَقَدْ آتَيْنَا إِبْرَاهِيمَ رُشْدَهُ مِن قَبْلُ وَكُنَّا بِهِ عَالِمِينَ ﴿٥١﴾

51. Na hakika tulikwisha mpa Ibrahim uongofu wake zamani na tulikuwa tunamjua.

إِذْ قَالَ لِأَبِيهِ وَقَوْمِهِ مَا هَـٰذِهِ التَّمَاثِيلُ الَّتِي أَنتُمْ لَهَا عَاكِفُونَ ﴿٥٢﴾

52. Alipomwambia baba yake na watu wake: Ni nini haya masanamu mnayoyanga’ng’ania?

قَالُوا وَجَدْنَا آبَاءَنَا لَهَا عَابِدِينَ ﴿٥٣﴾

53. Wakasema: Tumewakuta baba zetu wakiyaabudu.

قَالَ لَقَدْ كُنتُمْ أَنتُمْ وَآبَاؤُكُمْ فِي ضَلَالٍ مُّبِينٍ ﴿٥٤﴾

54. Akasema: Hakika nyinyi na baba zenu mmekuwa kwenye upotofu ulio dhahiri.

قَالُوا أَجِئْتَنَا بِالْحَقِّ أَمْ أَنتَ مِنَ اللَّاعِبِينَ ﴿٥٥﴾

55. Wakasema: Je, umetujia kwa haki au wewe ni katika wafanyao mchezo?

قَالَ بَل رَّبُّكُمْ رَبُّ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ الَّذِي فَطَرَهُنَّ وَأَنَا عَلَىٰ ذَٰلِكُم مِّنَ الشَّاهِدِينَ ﴿٥٦﴾

56. Akasema: Bali Mola wenu ni Mola wa mbingu na ardhi ambaye ndiye aliyeziumba, na mimi ni katika wenye kuyashuhudia hayo.

وَتَاللَّـهِ لَأَكِيدَنَّ أَصْنَامَكُم بَعْدَ أَن تُوَلُّوا مُدْبِرِينَ ﴿٥٧﴾

57. Naapa kwa Mwenyezi Mungu! Nitayafanyia vitimbi masanamu yenu baada ya kunipa mgogo.

فَجَعَلَهُمْ جُذَاذًا إِلَّا كَبِيرًا لَّهُمْ لَعَلَّهُمْ إِلَيْهِ يَرْجِعُونَ ﴿٥٨﴾

58. Basi akayavunja vipande vipande isipokuwa kubwa lao ili wao walirudie.

قَالُوا مَن فَعَلَ هَـٰذَا بِآلِهَتِنَا إِنَّهُ لَمِنَ الظَّالِمِينَ ﴿٥٩﴾

59. Wakasema: Ni nani aliyeyafanyia haya miungu wetu? Hakika huyu ni katika madhalimu.

قَالُوا سَمِعْنَا فَتًى يَذْكُرُهُمْ يُقَالُ لَهُ إِبْرَاهِيمُ ﴿٦٠﴾

60. Wakasema: Tumemsikia kijana mmoja akiwataja. Anaitwa Ibrahim.

IBRAHIM

Aya 51-60

MAANA

Na hakika tulikwisha mpa Ibrahim uongofu wake zamani na tulikuwa tunamjua.

Wametofautiana wafasiri kuhusu maana ya uongofu. Ikasemekana kuwa ni kuongoka kwenye utengenefu wa dini na dunia. Pia ikasemekana kuwa ni utume.

Kauli hii ndiyo yenye nguvu zaidi kwa dalili ya kauli ‘zamani’ maana yake ni kabla ya mitume waliokuja baada ya Ibrahim(a.s) ; kama vile Musa(a.s) , Isa(a.s) na Muhammad(s.a.w.w) . Pia kwa dalili ya kauli yake Mwenyezi Mungu ‘Na tulikuwa tunamjua’ ambayo maana yake ni kauli yake:

اللَّـهُ أَعْلَمُ حَيْثُ يَجْعَلُ رِسَالَتَهُ ﴿١٢٤﴾

“Mwenyezi Mungu diye Mjuzi zaidi wa kujua mahali anapoweka ujumbe wake.” Juz. (6:124).

Utume unatoka kwa Mungu, anamuhusisha nao mwenye kuustahiki, wala haupatikanai kwa bidii ya mtu; kama vile imani na takua. Ndio maana husemwa kuwa mumin, kuwa mcha Mungu, lakini haisemwi kuwa Mtume.

Alipomwambia baba yake na watu wake: Ni nini haya masanamu mnayoyanga’ng’ania?

Swali hili linaelekezwa kwa kila mwenye majukumu ya matendo yake na matumizi yake. Vipi mnavitukuza na kuviabudu visivyodhuru wala kunufaisha; na nyinyi mna akili na utambuzi?

Wakasema: Tumewakuta baba zetu wakiyaabudu.

Mantiki hii anaikimbilia kila mwenye kushindwa na hoja na dalili. Ukimuuliza kwa nini umefanya hivi, atasema: Fulani amefanya.

Hakuna la kuwaambia watu wa aina hii, isipokuwa kauli ya Nabii Ibrahim:

Akasema: Hakika nyinyi na baba zenu mmekuwa kwenye upotofu ulio dhahiri.

Na upotofu hauwezi kubadilika kuwa uongofu hata ukifuatwa na wengi.

Wakasema: Je, umetujia kwa haki au wewe ni katika wafanyao mchezo?

Walijitia mshangao kutokana na kauli ya Ibrahim, kwa vile wanawaona baba zao wametakaswa na makosa; si kwa lolote ila ni kwa kuwa ni baba zao tu.

Mantiki haya hawahusiki nao kaumu ya Ibrahim tu, wala washirikina wengine; bali kila mwenye kuigiza wengine kwa upofu, yuko sawa na waabudu masanamu.

Akasema: Bali Mola wenu ni Mola wa mbingu na ardhi ambaye ndiye aliyeziumba,

Mimi sifanyi mchezo wala sitii shaka. Vipi nifanye mchezo na kutia shakashaka na hali Yeye ndiye muumba wa mbingu na ardhi namimi ni katika wenye kuyashuhudia hayo?

Naapa kwa Mwenyezi Mungu! Nitayafanyia vitimbi masanamu yenu baada ya kunipa mgogo.

Ilivyo ni kwamba masanamu hayawezi kufanyiwa vitimbi, kwa sabau hayana hisia; isipokuwa wanaofanyiwa vitimbi ni waabudu masanamu, kwa hiyo kuyafanyia vitimbi ni majazi, sio hakika; isipokuwa yamefanywa ni nyenzo ya kufanyiwa vitimbi wanaoyaabudu.

Basi akayavunja vipande vipande isipokuwa kubwa lao ili wao walirudie.

Ibrahim aliyavunja masanamu yote na akaliacha lile kubwa lao, ili wale wanaoyaabudu waliulize, kwa nini halikuweza kuwatetea wenzake wadogo nalo lina nguvu? Makusudio yako wazi; nayo ni kuwa washirikina wazingatie kuwa masanamu haya ikiwa hayo yenyewe hayawezi kujitetea, basi ndio hayawezi kumtetea mwengine.

Wakasema: Ni nani aliyeyafanyia haya miungu wetu? Hakika huyu ni katika madhalimu.

Usawa ni kuwa waulize miungu yao imemfanyia nini aliyeyavunja? Lakini haya ndiyo mantiki ya kijinga na kuiga.

Wakasema: Tumemsikia kijana mmoja akiwataja. Anaitwa Ibrahim.

Hii inaashiria kauli ya Ibrahim(a.s) : “Nitayafanyia vitimbi masanamu yenu.”

Baada ya kuandika Juzuu ya sita, nilisoma kwenye mojawapo ya magazeti, kwamba wafukuaji, wamegundua mji wa kwanza wa Ibrahim, Uru. Ikabainika kwamba watu wake walikuwa wakiabudu nyota tatu: ndogo, wastani na kubwa.

Kwa hiyo mpangilio huu uliokuja katika Qur’an kupitia ulimi wa Ibrahim ndio mpangilio wa kimantiki ambao unafuatana na maisha ya wakati huo. Hivi ndivyo elimu inavyoleta dalili kila siku juu ya ukweli wa Muhammad(s.a.w.w) katika kila aliyoyaeleza.

قَالُوا فَأْتُوا بِهِ عَلَىٰ أَعْيُنِ النَّاسِ لَعَلَّهُمْ يَشْهَدُونَ ﴿٦١﴾

61. Wakasema: Mleteni mbele ya macho ya watu, wapate kumshuhudia.

قَالُوا أَأَنتَ فَعَلْتَ هَـٰذَا بِآلِهَتِنَا يَا إِبْرَاهِيمُ ﴿٦٢﴾

62. Wakasema: Je, wewe ndiwe uliyeifanyia haya mingu yetu ewe Ibrahim?

قَالَ بَلْ فَعَلَهُ كَبِيرُهُمْ هَـٰذَا فَاسْأَلُوهُمْ إِن كَانُوا يَنطِقُونَ ﴿٦٣﴾

63. Akasema: Bali ameyafanya hayo mkubwa wao huyu. Basi waulizeni ikiwa wanatamka.

فَرَجَعُوا إِلَىٰ أَنفُسِهِمْ فَقَالُوا إِنَّكُمْ أَنتُمُ الظَّالِمُونَ ﴿٦٤﴾

64. Basi wakajirudi nafsi zao. Wakasema: Hakika nyinyi ndio madhalimu.

ثُمَّ نُكِسُوا عَلَىٰ رُءُوسِهِمْ لَقَدْ عَلِمْتَ مَا هَـٰؤُلَاءِ يَنطِقُونَ ﴿٦٥﴾

65. Kisha wakasimamia vichwa vyao. Wewe unajua kwamba hawa hawasemi.

قَالَ أَفَتَعْبُدُونَ مِن دُونِ اللَّـهِ مَا لَا يَنفَعُكُمْ شَيْئًا وَلَا يَضُرُّكُمْ ﴿٦٦﴾

66. Akasema: Basi nyinyi mnaabudu badala ya Mwenyezi Mungu visivyo wanufaisha kitu wala kuwadhuru?

أُفٍّ لَّكُمْ وَلِمَا تَعْبُدُونَ مِن دُونِ اللَّـهِ أَفَلَا تَعْقِلُونَ ﴿٦٧﴾

67. Kefule yenu na mnavyoviabudu badala ya Mwenyezi Mungu. Basi hamtii akili?

قَالُوا حَرِّقُوهُ وَانصُرُوا آلِهَتَكُمْ إِن كُنتُمْ فَاعِلِينَ ﴿٦٨﴾

68. Wakasema: Mchomeni na muinusuru miungu yenu, ikiwa nyinyi ni watendao jambo.

قُلْنَا يَا نَارُ كُونِي بَرْدًا وَسَلَامًا عَلَىٰ إِبْرَاهِيمَ ﴿٦٩﴾

69. Tukasema: Ewe moto! Kuwa baridi na salama kwa Ibrahim!

وَأَرَادُوا بِهِ كَيْدًا فَجَعَلْنَاهُمُ الْأَخْسَرِينَ ﴿٧٠﴾

70. Na wakamtakia ubaya, lakini tukawafanya wao ndio wenye kupata hasara.

WAKASEMA: MLETENI

Aya 61 – 70

MAANA

Wakasema: Mleteni mbele ya macho ya watu, wapate kumshuhudia.

Walitaka wamsaili na kumhukumu mbele ya watu wamshuhudie; kisha waone adhabu itakayompata.

Wakasema: Je, wewe ndiwe uliyeifanyia haya mingu yetu ewe Ibrahim?

Walimleta na wakaanza kumhoji. Akasema:

Bali ameyafanya hayo mkubwa wao huyu. Basi waulizeni ikiwa wanatamka.

Kutamka ni katika hali ya kukadiria; ikiwa hawa wana hisia basi aliyefanya ni mkubwa wao. Mfano kusema: ikiwa Mwenyezi Mungu ana mtoto, basi mimi ni wa mwanzo wa wenye kumwabudu.

Kwa ujumla ni kwamba makusudio ni kuwanyamazisha kwa hoja, na kwamba masanamu haya, kama yangekuwa ni Mungu yangelikuwa na utambuzi, kusema na kumvunajilia mbali anayetaka kuyafanyia ubaya.

Basi wakajirudi nafsi zao.

Baada ya kusikia aliyoyasema Ibrahim(a.s) waliulizana: Vipi tuabudu mawe na kutarajia kheri na kuhofia shari yake na hayo yenyewe hayawezi kujikinga na madhara.

Wakasema: Hakika nyinyi ndio madhalimu.

Waliishia kukiri kuwa wao wako katika ujinga, lakini mara tu wakarudia kwenye hali yao ya mwanzo.

Kisha wakasimamia vichwa vyao.

Makusudio ya kusimamia vichwa hapa ni kurudi kwenye uovu wao. Neno lililotumika ni nukisu lenye maana ya kuweka kichwa chini miguu juu. Yaani kumpa silaha adui yako akuue nayo, au kumpa hoja mtu kutokana na vitendo vyako au kauli yako; kama walivyofanya kaumu ya Ibrahim, waliposema:

Wewe unajua kwamba hawa hawasemi.

Ikiwa hawasemi, basi vipi mnawaabudu. At-Tabariy anasema: “Kupindua jambo ni kulifanya kichwa chini miguu juu na kupindua hoja ni kuifanya hoja ya hasimu wako ndio hoja yako; kama walivyofanya kaumu ya Ibrahim.”

Akasema: Basi nyinyi mnaabudu badala ya Mwenyezi Mungu visivyo wanufaisha kitu wala kuwadhuru?

Nyinyi mnajua kuwa haya masanamu hayana utambuzi wala matamshi, hayadhuru wala hayanufaishi, basi vipi mnayaabudu?

Kefule yenu na na mnavyoviabudu badala ya Mwenyezi Mungu. Basi hamtii akili?

Utafanya nini na watu wanaong’ang’ania upotevu na wao wanajua kuwa huo ni upotevu. Hakuna cha kuwafanya isipokuwa kuwaaambia: poteleeni mbali, enyi mnaofanana na watu na wala sio watu.

Wakasema: Mchomeni na muinusuru miungu yenu, ikiwa nyinyi ni watendao jambo.

Wanusuruni miungu, lakini miungu yenyewe haiwezi kujinusuru, na bado ni miungu tu! Ni sawa na yule aliyesema: ‘Huyo ni paa hata kama ameruka angani.’ Huko ndiko kuweka kichwa chini miguu juu.

Tukasema: Ewe moto! Kuwa baridi na salama kwa Ibrahim!

Walisema na Mwenyezi Mungu naye akasema. Wala hakuna mwenye kurudisha kauli yake.

Unaweza kuuliza : Kwa kawaida moto unaunguza, vipi uwe baridi.

Jibu : Mwenye kuleta athari wa kwanza kwa kila kilichpo ni Mwenyezi Mungu ambaye umetukuka ukuu wake. Yote hutokana na Yeye, na kwake zinaishia nyenzo zote, ziwe ni sharti, sababu au chochote. Kuunguza kunatokana na moto, moto unatokana na kuni, kuni ni maumbile yaliyotokana na neno lake.

Yeye ndiye aliyeumba moto ambao unaunguza, lakini kwa sharti ya kutouambia ‘kuwa baridi.’ Kwa hiyo kama atauambia hivyo utakuwa kama alivyosema. Kwa maneno mengine ni kuwa kuunguza kwake na kuwa baridi kwake kunafuta matakwa ya Mungu kutokana na kuumba kwake na kuufanya uweko.

Na wakamtakia ubaya, lakini tukawafanya wao ndio wenye kupata hasara.

Waliwasha moto ili umchome Ibrahim, lakini ukawa ni muujiza mkubwa na dalili ya kuthibitisha ukweli wake na utume wake:

وَمَكَرُوا وَمَكَرَ اللَّـهُ وَاللَّـهُ خَيْرُ الْمَاكِرِينَ ﴿٥٤﴾

“Na wakapanga hila; na Mwenyezi Mungu akapanga hila; na Mwenyezi Mungu ndiye mbora wa kupanga hila” Juz. 3 (3:54).

Katika baadhi ya tafsiri za zamani, imeelezwa kuwa Namrud alipoona moto haumuathiri Ibrahim, aliamuru mali zake zichukuliwe na yeye mwenyewe atolewe nchini.

Ibrahim akasema: Mkichukua mali zangu basi nirudishieni umri wangu nilioumaliza kwenye nchi yenu. Wakaenda mahakamani, hakimu akatoa hukumu ya kunyang’anyawa mali Ibrahim na Namrud amrudishie umri wake. Hapo akasalimu amri na akamwacha Ibrahim na mali zake. Hekaya hii hatukuinukuu kwa kuamini kuwa ni kwali hivyo; isipokuwa inaonyesha kuwa kila mtu ana haki ya umri wake alioumaliza kwa sharti ya kuwa ameutumia kwenye halali.

وَنَجَّيْنَاهُ وَلُوطًا إِلَى الْأَرْضِ الَّتِي بَارَكْنَا فِيهَا لِلْعَالَمِينَ ﴿٧١﴾

71. Na tukamwokoa yeye na Lut tukawapeleka kwenye ardhi tuliyoibariki, kwa ajili ya walimwengu wote.

وَوَهَبْنَا لَهُ إِسْحَاقَ وَيَعْقُوبَ نَافِلَةً وَكُلًّا جَعَلْنَا صَالِحِينَ ﴿٧٢﴾

72. Naye tukampa Is-haq na Yakub kuwa ni zawadi. Na wote tukawajaalia wawe watu wema.

وَجَعَلْنَاهُمْ أَئِمَّةً يَهْدُونَ بِأَمْرِنَا وَأَوْحَيْنَا إِلَيْهِمْ فِعْلَ الْخَيْرَاتِ وَإِقَامَ الصَّلَاةِ وَإِيتَاءَ الزَّكَاةِ وَكَانُوا لَنَا عَابِدِينَ ﴿٧٣﴾

73. Na tukawafanya maimamu wakiongoza kwa amri yetu. Na tukawapa wahyi watende kheri na wasimamishe Swala na watoe Zaka na walikuwa wanatuabudu sisi.

وَلُوطًا آتَيْنَاهُ حُكْمًا وَعِلْمًا وَنَجَّيْنَاهُ مِنَ الْقَرْيَةِ الَّتِي كَانَت تَّعْمَلُ الْخَبَائِثَ إِنَّهُمْ كَانُوا قَوْمَ سَوْءٍ فَاسِقِينَ ﴿٧٤﴾

74. Na Lut tukampa hukumu na elimu na tukamwokoa na ule mji uliokuwa ukifanya maovu. Hakika hao walikuwa wabaya, mafasiki.

وَأَدْخَلْنَاهُ فِي رَحْمَتِنَا إِنَّهُ مِنَ الصَّالِحِينَ ﴿٧٥﴾

75. Na tukamwingiza katika rehema zetu. Hakika yeye ni miongoni mwa walio wema.

وَنُوحًا إِذْ نَادَىٰ مِن قَبْلُ فَاسْتَجَبْنَا لَهُ فَنَجَّيْنَاهُ وَأَهْلَهُ مِنَ الْكَرْبِ الْعَظِيمِ ﴿٧٦﴾

76. Na Nuh alipoita zamani, nasi tukamwitikia na tukamwokoa yeye na watu wake kutokana na shida kubwa.

وَنَصَرْنَاهُ مِنَ الْقَوْمِ الَّذِينَ كَذَّبُوا بِآيَاتِنَا إِنَّهُمْ كَانُوا قَوْمَ سَوْءٍ فَأَغْرَقْنَاهُمْ أَجْمَعِينَ ﴿٧٧﴾

77. Na tukamnusuru na watu waliozikadhibisha Ishara zetu. Hakika hao walikuwa watu wabaya. Basi tukawagharikisha wote.

TUKAMWOKOA YEYE NA LUT

Aya 71 – 77

MAANA

Na tukamwokoa yeye na Lut tukawapeleka kwenye ardhi tuliyoibariki, kwa ajili ya walimwengu wote.

Makusudio ya aliyeokolewa hapa ni Ibrahim(a.s ) . Lut ni mtoto wa kaka yake. Katika Tafsiri imelezwa kuwa Ibrahim aliondoka akaelekea nchi ya Sham, ambayo ndani ilikuwako Palestina.

Vyovyote iwavyo ni kwamba makusudio ni kumfananisha Muhammad(s.a.w.w) na kaumu yake pamoja na Ibrahim(a.s) na kaumu yake.

Kaumu zote mbili ziliabudu masanamu, zikakataa mwito wa nabii wao na kujaribu kumuua. Manabii wote wawili Mungu aliwaokoa na kuwatengenezea njia ya hijra na kuwaneemesha kwa hijra hiyo.

Naye tukampa Is-haq na Yakub kuwa ni zawadi.

Is-haq ni mtoto wa Ibrahim wa kumzaa, na Yakub ni mjukuu naye ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu.

Na wote tukawajaalia wawe watu wema.

Ibrahim, Is-haq , wote walikuwa wema.

Na tukawafanya maimamu wakiongoza kwa amri yetu. Na tukawapa wahyi watende kheri na wasimamishe Swala na watoe Zaka na walikuwa wanatuabudu sisi.

Maimamu ndio viongozi wa dini ambao amewateua Mwenyezi Mungu, kuwaongoza waja. Sifa yao kuu ni kwamba wao wanaongoza watu kama alivyoamrisha Mungu, si kama wanavyoamrisha wake zao, watoto wao au wakwe zao; wanahimiza kufanya kheri sio chuki za utaifa; na kumfanyia ikhlasi Mwenyezi Mungu peke yake sio mwenginewe.

Na Lut tukampa hukumu na elimu na tukamwokoa na ule mji uliokuwa ukifanya maovu. Hakika hao walikuwa wabaya, mafasiki. Na tukamwingiza katika rehema zetu. Hakika yeye ni miongoni mwa walio wema.

Tazama tafsiri yake katika Juz. 8 (7: 80) na Juz 12 (11:77).

Na Nuh alipoita zamani, nasi tukamwitikia na tukamwokoa yeye na watu wake kutokana na shida kubwa. Na tukamnusuru na watu waliozikadhibisha Ishara zetu. Hakika hao walikuwa watu wabaya. Basi tukawagharikisha wote.

Kisa cha Nuh kimetangulia katika Juz. 12 (11:25).

3

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA SABA

﴿جَعَلَ اللَّـهُ الْكَعْبَةَ الْبَيْتَ الْحَرَامَ قِيَامًا لِّلنَّاسِ وَالشَّهْرَ الْحَرَامَ وَالْهَدْيَ وَالْقَلَائِدَ ذَٰلِكَ لِتَعْلَمُوا أَنَّ اللَّـهَ يَعْلَمُ مَا فِي السَّمَاوَاتِ وَمَا فِي الْأَرْضِ وَأَنَّ اللَّـهَ بِكُلِّ شَيْءٍ عَلِيمٌ﴾

97.Mwenyezi Mungu amefanya Al-Kaaba nyumba tukufu, kuwa ni kisimamo cha watu na miezi mitukufu na wanyama wa kuchinja na vigwe; hayo ni kwa sababu mjue kuwa Mwenyezi Mungu anayajua yaliyomo mbinguni na yaliyomo ardhini na kwamba Mwenyezi Mungu ni Mjuzi wa kila kitu.

﴿اعْلَمُوا أَنَّ اللَّـهَ شَدِيدُ الْعِقَابِ وَأَنَّ اللَّـهَ غَفُورٌ رَّحِيمٌ﴾

98. Jueni kwamba Mwenyezi Mungu ni mkali wa kuadhibu na kwamba Mwenyezi Mungu ni mwingi wa maghufira, Mwingi wa kurehemu.

﴿مَّا عَلَى الرَّسُولِ إِلَّا الْبَلَاغُ وَاللَّـهُ يَعْلَمُ مَا تُبْدُونَ وَمَا تَكْتُمُونَ﴾

99.Haimlazimu Mtume ila kufikisha tu, na Mwenyezi Mungu anajua mnayo yadhihirisha na mnayoyaficha.

NYUMBA TAKATIFU

Aya 97-99

MAANA

Mwenyezi Mungu ameifanya Al-Kaaba, nyumba takatifu, kuwa ni kisimamo cha watu na miezi mitakatifu na wanyama wa kuchinja na vigwe.

Kisimamo cha watu; yaani mahali pa ibada na ibada za Hijja. Miezi mitakatifu ni ile minne Rajab, Dhul-qa'da, Dhul-Hijja na Muharram[5] Mwenyezi Mungu (s.w.t) ameharamisha kupigana huko na katika miezi hiyo; ispokuwa kutetea nafsi au mali. Anasema:

﴿وَلَا تُقَاتِلُوهُمْ عِندَ الْمَسْجِدِ الْحَرَامِ حَتَّىٰ يُقَاتِلُوكُمْ فِيهِ﴾

"Wala msipigane nao karibu na Msikiti Mtakatifu mpaka wakupigeni huko" (2:191) Na akasema tena:

﴿الشَّهْرُ الْحَرَامُ بِالشَّهْرِ الْحَرَامِ وَالْحُرُمَاتُ قِصَاصٌ فَمَنِ اعْتَدَىٰ عَلَيْكُمْ فَاعْتَدُوا عَلَيْهِ بِمِثْلِ مَا اعْتَدَىٰ عَلَيْكُمْ ﴾

"Mwezi mtakatifu kwa mwezi mtakatifu; na vitu vitakatifu vina kisasi. Basi wanaowachokoza, pia nanyi wachokozeni kwa kadiri walivyowachokoza" (2:194)

Mnyama wa kuchinja, ni wale wanaochinjwa Makka. Na kigwe ni ukambaa anaofungwa nao mnyama wa kuchinja kuwa ni alama ya kufahamisha kuwa ni wa Al-Kaaba ili asitaradhiwe na yeyote. Kwa hiyo kuunganisha vigwe kwa wanyama ni kuunganisha maalum katika ujumla.

Makusudio ya kutaja chinjo pamoja na Nyumba takatifu na miezi mitakatifu ni kwamba mnyama wa kuchinja inapasa awe salama yeye na anayemchunga, kwa sababu yeye anakusudia Haram tukufu.

Bali ni kwamba Mwenyezi Mungu (s.w.t) amewapa amani ndege na wanyama walio katika haramu yake; isipokuwa mwewe, kipanga, kunguru, panya, nge, mbwa anayeuma watu na kila tunayemuona anaudhi.

Hayo ni kwa sababu mjue kuwa Mwenyezi Mungu anayajua yaliomo mbinguni na yaliyomo ardhini na kwamba Mwenyezi Mungu ni mjuzi wa kila kitu.

Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kubainisha miko ya Al-Kaaba, miezi mitukufu na wanyama wa kuchinja, anaashiria kwamba hekima ya sharia hii ni kuwa watu wajue kwamba Mwenyezi Mungu anajua ufafanuzi wa mambo katika ardhi na katika mbingu; na ambayo yana masilahi kwa watu katika dini yao na dunia yao.

Kuna masilahi gani makubwa zaidi ya usalama wa maisha ya mtu na mali yake ijapokuwa ni kwa kipindi fulani. Tumeyaona mataifa makubwa yanayotwangana, wakati huu, yakiafikiana kuwa baadhi ya miji iwe ni maeneo maalumu ya amani, haijuzu kwa taifa linalopigana kuishirikisha katika vita wala kuweka vituo vya kijeshi katika ardhi hiyo au kupita wanajeshi wake.

Jueni kwamba Mwenyezi Mungu ni mkali wa kuadhibu na kwamba Mwenyezi Mungu ni mwingi wa maghufira, Mwenye kurehemu.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) amekutanisha adhabu na rehema na maghufira ili mja awe anahofia adhabu yake na kutaraji rehema yake. Kwa sababu mja, akiwa na hofu atajiepusha na maasi na akiwa na matarajio atajitahidi katika twaa.

Razi anasema: "Mwenyezi Mungu (s.w.t) ametaja kuwa yeye ni mkali wa kuadhibu, kisha akafuatishia kwa wasifu wa rehema na maghufira. Na huu ni uzinduzi juu ya undani kuwa kupatikana kiumbe ni kwa ajili ya rehema. Na kwa dhahiri ni kuwa mwisho hauwi ila kwa rehema" Hiyo ni kweli kabisa.

Haimlazimu Mtume ila kufikisha tu.

Hatakiwi jingine zaidi ya hilo, ambapo hapana udhuru baada ya kufikisha kwa anayepuuza na kupetuka mpaka. Ama hisabu na adhabu hiyo ni juu ya Mwenyezi Mungu pekee Yake. Mwenyezi Mungu anasema:

"Hakika ni juu yako kufikisha tu, na ni juu yetu hisabu." (13:40)

Mwenyezi Mungu anayajua mnayoyadhihirisha katika kauli na vitendo na mnayoyaficha. Haya ni makemeo kwa anayeinyamazia haki, na hasa yule anayeifanyia biashara kwa kujipanua na jina la dini na la nchi.

﴿قُل لَّا يَسْتَوِي الْخَبِيثُ وَالطَّيِّبُ وَلَوْ أَعْجَبَكَ كَثْرَةُ الْخَبِيثِ فَاتَّقُوا اللَّـهَ يَا أُولِي الْأَلْبَابِ لَعَلَّكُمْ تُفْلِحُونَ﴾

100.Sema: Hawi sawa habithi na mwema, hata ukikupendeza wingi wa habith, Basi mcheni Mwenyezi Mungu enyi wenye akili ili mpate kufaulu.

WINGI WA MWOVU

Aya 100

MAANA

Aya hii inarudufu Aya ile isemayo:

﴿لَا يَسْتَوِي أَصْحَابُ النَّارِ وَأَصْحَابُ الْجَنَّةِ أَصْحَابُ الْجَنَّةِ هُمُ الْفَائِزُونَ﴾

"Hawawi sawa watu wa Motoni na watu wa Peponi, watu wa Peponi ndio wenye kufuzu" (59:20)

Wingi wa habithi ni anayoyamiliki miongoni mwa jaha na mali. Mwenye akili hawezi kumweka sawa habithi, na mwema hata kama ana mali nyingi na jaha kubwa. Kwa sababu jaha na mali hazimfanyi mwovu kuwa mwema; wala ufakiri na udhaifu haumfanyi mwema kuwa mwovu.

Mtu habith katika kipimo cha dini ni yule anayeasi hukumu za Mwenyezi Mungu katika kitabu chake na Sunna za Mtume wake. Na katika desturi ya watu ni yule wanayemhofia kwa shari yake na wasiyemwamini kwa jambo lolote na kutomsadiki katika kauli au vitendo vyake. Kimsingi ni kwamba mwenye sifa hizi, ni mbaya pia mbele ya Mwenyezi Mungu. Mtume wa Mwenyezi Mungu anasema:"Utukufu zaidi wa imani ni kuaminiwa na watu." Ama mtu mwema ni yule aliye kinyume cha mtu habithi katika sifa zake zote.

JE RIZIKI NI BAHATI AU MAJAALIWA?

Unaweza kuuliza : Ikiwa habithi anachukiwa na Mwenyezi Mungu na mwema anaridhiwa na Mwenyezi Mungu, kwa nini basi habithi anafaulu katika maisha haya na kuneemeshwa kwa jaha na utajiri, na mwema anaanguka na wala hapati matakwa yake?

Jibu : Maisha yana desturi na kanuni zinazokwenda nayo, na hazigeuki kwa hali yoyote ile. Kwa sababu hisia na uoni unakataa mkorogano katika ulimwengu. Desturi na kanuni hizi ni katika matengenezo ya Mwenyezi Mungu Mtukufu: Kwa sababu yeye ni muumbaji wa asili na vilivyomo katika asili.

Kimsingi ni kuwa desturi ya kawaida ya tabia inakataa kuwa mali, afya na ilimu, vishuke tu kutoka mbinguni. Isipokuwa vitu hivi na mfano wake vinakuja kwa njia zake na sababu zake za kimaumbile. Elimu inatokana na kujifundisha, afya inatokana na lishe na kinga, na mali inatokana na kazi. Kwa hiyo mwenye kujifunza hujua, mwenye kujiepusha na visababishi vya maradhi husalimika, mwenye kujinyonga atakufa tu; awe mwema au mwovu, mumin au kafiri.

Kwa hiyo wema au imani hauoteshi ngano wala hauponeshi ugonjwa wala haumfanyi asiyejua kuwa mjuzi, Yote haya na mfano wake yanakwenda kwa desturi ya tabia na desturi ya tabia inakwenda kwa matakwa ya Mwenyezi Mungu, hilo halina shaka.

Kwa sababu yeye ndiye aliyejaalia kujifundisha ndio sababu ya elimu na kujikinga ndio sababu ya afya na kupanda kuwa ndio sababu ya kuvuna. Yeye ni Muumba wa kila kitu na kwake yeye ni mwishilio wa kila jambo.

Ndiyo! kuchuma mali kuna njia nyingi, na milango mingi, nyingine Mwenyezi Mungu amezihalalisha na nyingine akaziharamisha. Mwenyezi Mungu (s.w.t) amehalalisha biashara, kilimo na viwanda; na akaharamisha riba, utapeli, rushwa, kupora na ulanguzi.

Mwenye kuchuma mali kwa njia ya halali hunasibishwa chumo lake kwake, kwa sababu yeye amejitahidi na kufanya bidii kuitafuta, na vilevile hunasabishwa kwa Mwenyezi Mungu. Kwa sababu yeye ndiye aliyepitisha sababu hizi na kuzihalalisha kwa kila azitakaye, awe mwema au mwovu.

Ama mwenye kuchuma mali kwa njia za haramu; kama vile riba na unyang'anyi; chumo lake litanasibishwa kwake na kwa hali aliyoitumia, wala halinasibishwi kwa Mwenyezi Mungu, kwa sababu yeye Mwenyezi Mungu Mtukufu ameharamisha njia hizi kwa mwema na mwovu.

Utasema : Haya yote ni kweli, lakini hayajibu swali wala hayatatui mushkeli. Tumewahi kumuona mwema na mwovu wote wakifuata njia za sharia za riziki, na kuzitafuta riziki kwa njia zile alizozihalalisha Mwenyezi Mungu na kuziharamisha, lakini pamoja na hayo, riziki inakuwa zaidi kwa mwovu aliye habith na kuwa dhiki kwa mwema, pengine huyu mwema ametoa juhudi maradufu ya yule mwovu, bali mara nyingine riziki humjia mwovu bila ya kutazamia wala maandalizi au juhudi, na inazuilika kumwendea mwema anapoitazamia na kuifanyia maandalizi na juhudi?

Jibu : Baadhi ya watu wanakimbilia kulifasiri hilo kwa kusema ni sadfa au bahati. Hakuna kinachofahamika kutokana na maelezo hayo zaidi ya kushindwa kwao kutoa tafsiri sahihi. Vinginevyo wasingelikimbilia kwenye maelezo ya kubahatisha tu.

Kwa hiyo sisi tunapinga Sadfa na bahati na tunaamini kwa imani ya mkato kwamba kuna chaguo la juu linajiingiza kwa sababu tusizozijua. kwa vile elimu katika masuala hayo na mfano wake, bado ni changa. Na kushindwa kwa elimu hakumaanishi kuwa kitu hakiko. Imani yetu hii inatiliwa mkazo na kauli zake Mwenyezi Mungu zifuatazo:

﴿وَاللَّـهُ فَضَّلَ بَعْضَكُمْ عَلَىٰ بَعْضٍ فِي الرِّزْقِ﴾

"Na Mwenyezi Mungu amewafadhilisha baadhi yenu kuliko wengine katika riziki" (16:71)

﴿اللَّـهُ يَبْسُطُ الرِّزْقَ لِمَن يَشَاءُ وَيَقْدِرُ﴾

"Mwenyezi Mungu hukunjua riziki kwa amtakaye na huidhikisha (13:26) Ay a hii imekuja kwa herufi zake katika 17:30, 28:82, 29:62, 30:37, 34: 36, 34: 39, 39:52, 42:12.

Kwa hiyo basi aliyesema au anayesema: Mwenyezi Mungu amemtajirisha fulani kwa kuwa yeye ni mwema basi atakuwa anazungumza mantiki ya Firaun na kupima kwa kipimo cha Shetani. Hekima yake Mwenyezi Mungu Mtukufu imetaka kumlipa mwema malipo mazuri na kumwadhibu mwovu katika akhera inayobakia sio katika hii dunia inayokwisha. Hii ni Nyumba ya matendo na ile ni Nyumba ya Hisabu. Zaidi ya haya ni kuwa wingi wa mali wa mwovu huenda ukawa ni balaa kwake na sababu ya kuadhibiwa kwake. Mwenyezi Mungu anasema:

﴿ذَرْهُمْ يَأْكُلُوا وَيَتَمَتَّعُوا وَيُلْهِهِمُ الْأَمَلُ فَسَوْفَ يَعْلَمُونَ﴾

"Waache wale na wafurahi na iwazuge tamaa, watakuja jua." (15:3)

﴿يَتَمَتَّعُونَ وَيَأْكُلُونَ كَمَا تَأْكُلُ الْأَنْعَامُ وَالنَّارُ مَثْوًى لَّهُمْ﴾

"Hujistarehesha na hula kama walivyo wanyama, na moto ndio makazi yao." (47:12)

Kwa ufupi ni kwamba riziki inategemea mambo mawili. Kuhangaika na matakwa ya Mwenyezi Mungu. Asiyehangaika ataishi omba omba; na mwenye kuhangaika Mwenyezi Mungu humruzuku kutokana na bidii yake, akitaka humpa nyingi na akitaka humpa chache.

Uhakika huu umo katika maumbile ya binadamu na anaufanya bila ya kujitambua. Mfanya biashara humwomba Mwenyezi Mungu (s.w.t) amruzuku kupata soko zuri la bidhaa zake na watu wazikubali. Mkulima anamwomba Mungu aiteremshie mimea yake mvua; wala hamuombi kumwoteshea mimea bila ya mvua.

Mimi hapa namwomba Mwenyezi Mungu ampe tawfiq mwanangu katika masomo yake na kufaulu mtihani; wala si mwombi akipe mawazo chuo kikuu kimpatie shahada bila ya kusoma na kufanya mtihani. Iko methali isemayo: Mgaagaa na upwa hali wali mkavu.

Pengine inawezekana mahangaiko yasiambulie kitu, lakini pamoja na hayo inatakikana kupanga mipango na kuongeza juhudi. Kwa sababu kuongeza juhudi, kutumia mipango, na kuvumilia tabu ni sababu ya matakwa ya kufaulu kutoka kwake Mwenyezi Mungu Mtukufu.

﴿يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا لَا تَسْأَلُوا عَنْ أَشْيَاءَ إِن تُبْدَ لَكُمْ تَسُؤْكُمْ وَإِن تَسْأَلُوا عَنْهَا حِينَ يُنَزَّلُ الْقُرْآنُ تُبْدَ لَكُمْ عَفَا اللَّـهُ عَنْهَا وَاللَّـهُ غَفُورٌ حَلِيمٌ﴾

101.Enyi Mlioamini! Msiulize mambo ambayo mkidhihirishiwa yatawachukiza. Na mnapoyauliza inapoteremshwa Qur'an mtabainishiwa. Mwenyezi Mungu ameyasamehe hayo. Na Mwenyezi Mungu ni mwingi wa maghufira Mpole.

﴿قَدْ سَأَلَهَا قَوْمٌ مِّن قَبْلِكُمْ ثُمَّ أَصْبَحُوا بِهَا كَافِرِينَ﴾

102.Waliyauliza watu waliokuwa kabla yenu kisha wakawa makafiri kwayo.

MSIULIZEULIZE MAMBO

Aya 101-102

MAANA

Enyi Mlioamini! Msiulize mambo ambayo mkidhihirishiwa yatawachukiza.

Kauli yake Mwenyezi Mungu 'Msiulize' inaishiria kuwa baadhi ya Masahaba walikuwa waking'ang'ania kuuliza mambo yasiyokuwa na dharura yoyote kuyajua na huenda jibu lake likawaudhi waulizaji. Kuna riwaya isemayo kuwa mtu mmoja alimuuliza Mtume(s.a.w.w) : "Ni nani baba yangu?" Mtume akamwambia, "baba yako ni Fulani" Mwingine akauliza "Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu! Baba yangu yuko wapi? Mtume akajibu: "Yuko motoni," ndipo ikashuka Aya hiyo.

Riwaya nyingine inasema kuwa Mtume alisema: "Mwenyezi Mungu amewafaradhishia kuhiji, basi hijini." Wakauliza: "Kila mwaka ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu?" Mtume akanyamaza. Wakarudia kuuliza, akasema La; lau ningelisema naam, ingelikuwa wajib." Ndipo ikashuku Aya hii. Riwaya hii ndiyo yenye nguvu kuliko ile ya kwanza.

Na mnapoyauliza inapoteremshwa Qur'an mtabainishiwa.

Yaani msijikalifishe kuuliza mambo ila baada ya kuteremshwa Qur'an. Mtakapoanza kuuliza Mtume(s.a.w.w) atawadhirishia mliyokuwa mkiyauliza.

Kwa hali hii, inatubainikia kuwa riwaya ya Hija ndiyo yenye nguvu katika sababu ya kushuka Aya, kuliko riwaya ya kuuliza mababa na wahenga wa Masahaba. Kwa sababu Qur'an inaanza kuleta itikadi na sharia na wala sio kuanzia kwa mababa na mababu wa Masahaba. Katika Hadith imeelezwa:"Hakika Mwenyezi Mungu ameweka mipaka msiikiuke; amewafaradhishia faradhi msizipoteze; ameharamishia vitu msivifanye; na ameacha vitu vingine si kwa kusahau, lakini ni kwa kuwahurumia, basi vikubalini wala msivifanyie utafiti".

Mwenyezi Mungu amesamehe hayo

Yaani maswali yenu yaliyotangulia, kwa hiyo msiyarudie. Imesemekana kuwa maana yake ni amezuia kutaja vitu mlivyoviulizia, basi nanyi jizuieni wala msijikalifu kuviulizia. Tafsir zote mbili zina uwezekano hazikataliwi na dhahiri ya tamko.

Na Mwenyezi Mungu ni mwingi wa maghufira, Mpole.

Humsamehe mkosaji akikosea tena.

Waliyauliza watu waliokuwa kabla yenu kisha wakawa makafiri kwayo.

Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kuwakataza kuuliza mambo wasiyokuwa na haja nayo, anawapigia mfano wa watu waliokuwa kabla yao, waliuliza wakang'ang'ania kuuliza. Walipobainishiwa na Mwenyezi Mungu walichukia wakaasi na wakastahiki adhabu. Lau wangeliacha kuuliza ingelikuwa bora kwao.

Wafasiri wamerefusha maneno katika kubainisha makusudio ya watu waliouliza, kisha wakawa makafiri kwa sababu ya kuuliza, lakini Aya haikubainisha. Pamoja na hivyo, tunaweza kusema kuwa watu waliouliza wakawa makafiri kwa sababu ya kuuliza ni wana wa Israil, kwa sababu ya kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu akiwasimulia:

﴿فَقَدْ سَأَلُوا مُوسَىٰ أَكْبَرَ مِن ذَٰلِكَ فَقَالُوا أَرِنَا اللَّـهَ جَهْرَةً ﴾

"Hakika walimtaka Musa makubwa kuliko hayo, Walisema: Tuonyeshe Mwenyezi Mungu waziwazi" (4:153)

﴿مَا جَعَلَ اللَّـهُ مِن بَحِيرَةٍ وَلَا سَائِبَةٍ وَلَا وَصِيلَةٍ وَلَا حَامٍ وَلَـٰكِنَّ الَّذِينَ كَفَرُوا يَفْتَرُونَ عَلَى اللَّـهِ الْكَذِبَ وَأَكْثَرُهُمْ لَا يَعْقِلُونَ﴾

103.Mwenyezi Mungu hakujaalia Bahira wala Saiba wala Waswila wala Hami; Lakini waliokufuru wanamzulia Mwenyezi Mungu uwongo na wengi wao hawafahamu.

﴿وَإِذَا قِيلَ لَهُمْ تَعَالَوْا إِلَىٰ مَا أَنزَلَ اللَّـهُ وَإِلَى الرَّسُولِ قَالُوا حَسْبُنَا مَا وَجَدْنَا عَلَيْهِ آبَاءَنَا أَوَلَوْ كَانَ آبَاؤُهُمْ لَا يَعْلَمُونَ شَيْئًا وَلَا يَهْتَدُونَ﴾

104.Wakiambiwa njooni katika yale aliyoyateremsha Mwenyezi Mungu na kwa Mtume, husema: Yanatutosha yale tuliyowakuta nayo babu zetu. Je hata kama baba zao walikuwa hawajui kitu wala hawakuongoka?

﴿يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا عَلَيْكُمْ أَنفُسَكُمْ لَا يَضُرُّكُم مَّن ضَلَّ إِذَا اهْتَدَيْتُمْ إِلَى اللَّـهِ مَرْجِعُكُمْ جَمِيعًا فَيُنَبِّئُكُم بِمَا كُنتُمْ تَعْمَلُونَ﴾

105.Enyi mlioamini! Jiangalie nafsi zenu. Hawawadhuru waliopotea ikiwa mmeongoka. Marejeo yenu nyote ni kwa Mwenyezi Mungu. Atawaambia yale mliyokuwa mkiyatenda.

HAKUNA BAHIRAWALA SAIBA

Aya 103-105

MAANA

Mwenyezi Mungu hakujaalia Bahira wala Saiba wala Waswila wala Hami.

Bahira, ni ngamia aliyetobolewa masikio, watu wa wakati wa Jahilia walikuwa wakifanya hivyo, ikiwa ngamia atazaa mimba kumi ; na inasemekana ni mimba tano. Wanamwacha bila ya kutumiwa na mtu yoyote. Saiba ni ngamia waliyemwekea nadhiri kwa waungu, na wana mwacha akijilisha mwenyewe popote bila ya kufungwa wala kuwa na mchungaji sawa na Bahira.

Wasila ni mbuzi anayezaa mtoto wa kiume na wa kike pamoja. Desturi yao ilikuwa kama akizaa mume wanamfanya ni wa waungu na akizaa mke ni wao. Iwapo atazaa mume na mke pamoja, hawamchinji mume wakisema kuwa ameunganishwa na dada yake. Hami ni dume aliyezalisha mimba kumi, wanamwacha hazuiliwi na maji wala malisho, wakisema ameuhami mgongo wake.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) anabainisha kwamba yote hayo hayamo katika dini, na kwamba dume, jike na mbuzi, vyovyote wanavyofanyiwa, wanabakia na uhalali wake kama walivyokuwa mwanzo na wala hawaharamishwi na porojo hizo.

Lakini waliokufuru wanamzulia Mwenyezi Mungu uwongo na wengi wao hawafahamu.

Watu wa kijahilia walikuwa wakikubali kuweko kwa muumba kwa dalili kwamba wao wamenasibishia uharamu wa Hami, Saiba, Bahira na Waswila, lakini pamoja na hayo Mwenyezi Mungu amewanasibishia ukafiri.

Kwa sababu wao wamemnasibishia uharamu kwa uwongo na uzushi. Kwa hiyo, basi kila anayemnasibishia Mwenyezi Mungu na yasiyokuwa na dalili ya Kitab wala Hadith ya Mtume wake basi huyo ni kafir kwa sharti ya kutegemea kumnasibishia Mungu, huku akijua kutokuwepo dalili.

Hii, kwa lugha ya watu wa sharia, huitwa Bid'a (uzushi). Kuna Hadithi isemayo: "Kila bid'a ni upotevu na kila upotevu ni motoni".

Ilivyo ni kuwa kufaradhia huko kuko mbali na hali halisi ilivyo, Ni nani anayemnasibishia hukumu Mwenyezi Mungu huku akijua kuwa hakuna dalili. Pengine anaweza akadhani ni dalili, lakini kumbe sio dalili.

Wakiambiwa njooni katika yale aliyoyateremsha Mwenyezi Mungu na kwa Mtume, husema: "Yanatutosha yale tuliyowakuta nayo babu zetu. Je hata kama babu zao walikuwa hawajui kitu wala hawakuongoka?

Razi anasema: "Maana yanajulikana, nayo ni jibu la kuwapinga watu wa Taqlid (kufuata)". Tumezungumzia kuhusu Taqlid katika Juz.2 (2:170)

Enyi mlioamini! Jiangalieni nafsi zenu, Hawawadhuru waliopotea ikiwa mmeongoka, Marejeo yenu nyote ni kwa Mwenyezi Mungu.

Razi ametaja njia nane za kufasiri Aya hii. Mmoja wa wafasiri wapya ameandika kurasa 33. Lililowafanya wawili hawa na wengineo kurefusha mambo hivi ni kuwa kuamrisha mema ni wajibu na dhahiri ya Aya inafahamisha kutokuwa wajib na kwamba ni juu ya mtu kujishughulikia mwenyewe. Ama wengine wana majukumu yao juu ya nafsi zao wala si wajibu kwa yoyote kuiongoza au kuikanya nafsi ya mwingine.

Ilivyo tafsir ya Aya hii ni kwamba, ni juu ya mtu kuamrisha mema. Kuamrisha kwake kukinufaisha basi hayo ndiyo yanayotakikana. Vinginevyo basi atakuwa ametekeleza lile aliloamrishwa wala hautamdhuru upotevu wa aliyepotea.

Mwenye jukumu baada ya kuamrisha ni yule aliyepotea na wala sio mwamrishaji. Tafsir hii imetilia mkazo wajibu wa kuamrisha mema na sio kupinga.

3

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA SABA

﴿جَعَلَ اللَّـهُ الْكَعْبَةَ الْبَيْتَ الْحَرَامَ قِيَامًا لِّلنَّاسِ وَالشَّهْرَ الْحَرَامَ وَالْهَدْيَ وَالْقَلَائِدَ ذَٰلِكَ لِتَعْلَمُوا أَنَّ اللَّـهَ يَعْلَمُ مَا فِي السَّمَاوَاتِ وَمَا فِي الْأَرْضِ وَأَنَّ اللَّـهَ بِكُلِّ شَيْءٍ عَلِيمٌ﴾

97.Mwenyezi Mungu amefanya Al-Kaaba nyumba tukufu, kuwa ni kisimamo cha watu na miezi mitukufu na wanyama wa kuchinja na vigwe; hayo ni kwa sababu mjue kuwa Mwenyezi Mungu anayajua yaliyomo mbinguni na yaliyomo ardhini na kwamba Mwenyezi Mungu ni Mjuzi wa kila kitu.

﴿اعْلَمُوا أَنَّ اللَّـهَ شَدِيدُ الْعِقَابِ وَأَنَّ اللَّـهَ غَفُورٌ رَّحِيمٌ﴾

98. Jueni kwamba Mwenyezi Mungu ni mkali wa kuadhibu na kwamba Mwenyezi Mungu ni mwingi wa maghufira, Mwingi wa kurehemu.

﴿مَّا عَلَى الرَّسُولِ إِلَّا الْبَلَاغُ وَاللَّـهُ يَعْلَمُ مَا تُبْدُونَ وَمَا تَكْتُمُونَ﴾

99.Haimlazimu Mtume ila kufikisha tu, na Mwenyezi Mungu anajua mnayo yadhihirisha na mnayoyaficha.

NYUMBA TAKATIFU

Aya 97-99

MAANA

Mwenyezi Mungu ameifanya Al-Kaaba, nyumba takatifu, kuwa ni kisimamo cha watu na miezi mitakatifu na wanyama wa kuchinja na vigwe.

Kisimamo cha watu; yaani mahali pa ibada na ibada za Hijja. Miezi mitakatifu ni ile minne Rajab, Dhul-qa'da, Dhul-Hijja na Muharram[5] Mwenyezi Mungu (s.w.t) ameharamisha kupigana huko na katika miezi hiyo; ispokuwa kutetea nafsi au mali. Anasema:

﴿وَلَا تُقَاتِلُوهُمْ عِندَ الْمَسْجِدِ الْحَرَامِ حَتَّىٰ يُقَاتِلُوكُمْ فِيهِ﴾

"Wala msipigane nao karibu na Msikiti Mtakatifu mpaka wakupigeni huko" (2:191) Na akasema tena:

﴿الشَّهْرُ الْحَرَامُ بِالشَّهْرِ الْحَرَامِ وَالْحُرُمَاتُ قِصَاصٌ فَمَنِ اعْتَدَىٰ عَلَيْكُمْ فَاعْتَدُوا عَلَيْهِ بِمِثْلِ مَا اعْتَدَىٰ عَلَيْكُمْ ﴾

"Mwezi mtakatifu kwa mwezi mtakatifu; na vitu vitakatifu vina kisasi. Basi wanaowachokoza, pia nanyi wachokozeni kwa kadiri walivyowachokoza" (2:194)

Mnyama wa kuchinja, ni wale wanaochinjwa Makka. Na kigwe ni ukambaa anaofungwa nao mnyama wa kuchinja kuwa ni alama ya kufahamisha kuwa ni wa Al-Kaaba ili asitaradhiwe na yeyote. Kwa hiyo kuunganisha vigwe kwa wanyama ni kuunganisha maalum katika ujumla.

Makusudio ya kutaja chinjo pamoja na Nyumba takatifu na miezi mitakatifu ni kwamba mnyama wa kuchinja inapasa awe salama yeye na anayemchunga, kwa sababu yeye anakusudia Haram tukufu.

Bali ni kwamba Mwenyezi Mungu (s.w.t) amewapa amani ndege na wanyama walio katika haramu yake; isipokuwa mwewe, kipanga, kunguru, panya, nge, mbwa anayeuma watu na kila tunayemuona anaudhi.

Hayo ni kwa sababu mjue kuwa Mwenyezi Mungu anayajua yaliomo mbinguni na yaliyomo ardhini na kwamba Mwenyezi Mungu ni mjuzi wa kila kitu.

Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kubainisha miko ya Al-Kaaba, miezi mitukufu na wanyama wa kuchinja, anaashiria kwamba hekima ya sharia hii ni kuwa watu wajue kwamba Mwenyezi Mungu anajua ufafanuzi wa mambo katika ardhi na katika mbingu; na ambayo yana masilahi kwa watu katika dini yao na dunia yao.

Kuna masilahi gani makubwa zaidi ya usalama wa maisha ya mtu na mali yake ijapokuwa ni kwa kipindi fulani. Tumeyaona mataifa makubwa yanayotwangana, wakati huu, yakiafikiana kuwa baadhi ya miji iwe ni maeneo maalumu ya amani, haijuzu kwa taifa linalopigana kuishirikisha katika vita wala kuweka vituo vya kijeshi katika ardhi hiyo au kupita wanajeshi wake.

Jueni kwamba Mwenyezi Mungu ni mkali wa kuadhibu na kwamba Mwenyezi Mungu ni mwingi wa maghufira, Mwenye kurehemu.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) amekutanisha adhabu na rehema na maghufira ili mja awe anahofia adhabu yake na kutaraji rehema yake. Kwa sababu mja, akiwa na hofu atajiepusha na maasi na akiwa na matarajio atajitahidi katika twaa.

Razi anasema: "Mwenyezi Mungu (s.w.t) ametaja kuwa yeye ni mkali wa kuadhibu, kisha akafuatishia kwa wasifu wa rehema na maghufira. Na huu ni uzinduzi juu ya undani kuwa kupatikana kiumbe ni kwa ajili ya rehema. Na kwa dhahiri ni kuwa mwisho hauwi ila kwa rehema" Hiyo ni kweli kabisa.

Haimlazimu Mtume ila kufikisha tu.

Hatakiwi jingine zaidi ya hilo, ambapo hapana udhuru baada ya kufikisha kwa anayepuuza na kupetuka mpaka. Ama hisabu na adhabu hiyo ni juu ya Mwenyezi Mungu pekee Yake. Mwenyezi Mungu anasema:

"Hakika ni juu yako kufikisha tu, na ni juu yetu hisabu." (13:40)

Mwenyezi Mungu anayajua mnayoyadhihirisha katika kauli na vitendo na mnayoyaficha. Haya ni makemeo kwa anayeinyamazia haki, na hasa yule anayeifanyia biashara kwa kujipanua na jina la dini na la nchi.

﴿قُل لَّا يَسْتَوِي الْخَبِيثُ وَالطَّيِّبُ وَلَوْ أَعْجَبَكَ كَثْرَةُ الْخَبِيثِ فَاتَّقُوا اللَّـهَ يَا أُولِي الْأَلْبَابِ لَعَلَّكُمْ تُفْلِحُونَ﴾

100.Sema: Hawi sawa habithi na mwema, hata ukikupendeza wingi wa habith, Basi mcheni Mwenyezi Mungu enyi wenye akili ili mpate kufaulu.

WINGI WA MWOVU

Aya 100

MAANA

Aya hii inarudufu Aya ile isemayo:

﴿لَا يَسْتَوِي أَصْحَابُ النَّارِ وَأَصْحَابُ الْجَنَّةِ أَصْحَابُ الْجَنَّةِ هُمُ الْفَائِزُونَ﴾

"Hawawi sawa watu wa Motoni na watu wa Peponi, watu wa Peponi ndio wenye kufuzu" (59:20)

Wingi wa habithi ni anayoyamiliki miongoni mwa jaha na mali. Mwenye akili hawezi kumweka sawa habithi, na mwema hata kama ana mali nyingi na jaha kubwa. Kwa sababu jaha na mali hazimfanyi mwovu kuwa mwema; wala ufakiri na udhaifu haumfanyi mwema kuwa mwovu.

Mtu habith katika kipimo cha dini ni yule anayeasi hukumu za Mwenyezi Mungu katika kitabu chake na Sunna za Mtume wake. Na katika desturi ya watu ni yule wanayemhofia kwa shari yake na wasiyemwamini kwa jambo lolote na kutomsadiki katika kauli au vitendo vyake. Kimsingi ni kwamba mwenye sifa hizi, ni mbaya pia mbele ya Mwenyezi Mungu. Mtume wa Mwenyezi Mungu anasema:"Utukufu zaidi wa imani ni kuaminiwa na watu." Ama mtu mwema ni yule aliye kinyume cha mtu habithi katika sifa zake zote.

JE RIZIKI NI BAHATI AU MAJAALIWA?

Unaweza kuuliza : Ikiwa habithi anachukiwa na Mwenyezi Mungu na mwema anaridhiwa na Mwenyezi Mungu, kwa nini basi habithi anafaulu katika maisha haya na kuneemeshwa kwa jaha na utajiri, na mwema anaanguka na wala hapati matakwa yake?

Jibu : Maisha yana desturi na kanuni zinazokwenda nayo, na hazigeuki kwa hali yoyote ile. Kwa sababu hisia na uoni unakataa mkorogano katika ulimwengu. Desturi na kanuni hizi ni katika matengenezo ya Mwenyezi Mungu Mtukufu: Kwa sababu yeye ni muumbaji wa asili na vilivyomo katika asili.

Kimsingi ni kuwa desturi ya kawaida ya tabia inakataa kuwa mali, afya na ilimu, vishuke tu kutoka mbinguni. Isipokuwa vitu hivi na mfano wake vinakuja kwa njia zake na sababu zake za kimaumbile. Elimu inatokana na kujifundisha, afya inatokana na lishe na kinga, na mali inatokana na kazi. Kwa hiyo mwenye kujifunza hujua, mwenye kujiepusha na visababishi vya maradhi husalimika, mwenye kujinyonga atakufa tu; awe mwema au mwovu, mumin au kafiri.

Kwa hiyo wema au imani hauoteshi ngano wala hauponeshi ugonjwa wala haumfanyi asiyejua kuwa mjuzi, Yote haya na mfano wake yanakwenda kwa desturi ya tabia na desturi ya tabia inakwenda kwa matakwa ya Mwenyezi Mungu, hilo halina shaka.

Kwa sababu yeye ndiye aliyejaalia kujifundisha ndio sababu ya elimu na kujikinga ndio sababu ya afya na kupanda kuwa ndio sababu ya kuvuna. Yeye ni Muumba wa kila kitu na kwake yeye ni mwishilio wa kila jambo.

Ndiyo! kuchuma mali kuna njia nyingi, na milango mingi, nyingine Mwenyezi Mungu amezihalalisha na nyingine akaziharamisha. Mwenyezi Mungu (s.w.t) amehalalisha biashara, kilimo na viwanda; na akaharamisha riba, utapeli, rushwa, kupora na ulanguzi.

Mwenye kuchuma mali kwa njia ya halali hunasibishwa chumo lake kwake, kwa sababu yeye amejitahidi na kufanya bidii kuitafuta, na vilevile hunasabishwa kwa Mwenyezi Mungu. Kwa sababu yeye ndiye aliyepitisha sababu hizi na kuzihalalisha kwa kila azitakaye, awe mwema au mwovu.

Ama mwenye kuchuma mali kwa njia za haramu; kama vile riba na unyang'anyi; chumo lake litanasibishwa kwake na kwa hali aliyoitumia, wala halinasibishwi kwa Mwenyezi Mungu, kwa sababu yeye Mwenyezi Mungu Mtukufu ameharamisha njia hizi kwa mwema na mwovu.

Utasema : Haya yote ni kweli, lakini hayajibu swali wala hayatatui mushkeli. Tumewahi kumuona mwema na mwovu wote wakifuata njia za sharia za riziki, na kuzitafuta riziki kwa njia zile alizozihalalisha Mwenyezi Mungu na kuziharamisha, lakini pamoja na hayo, riziki inakuwa zaidi kwa mwovu aliye habith na kuwa dhiki kwa mwema, pengine huyu mwema ametoa juhudi maradufu ya yule mwovu, bali mara nyingine riziki humjia mwovu bila ya kutazamia wala maandalizi au juhudi, na inazuilika kumwendea mwema anapoitazamia na kuifanyia maandalizi na juhudi?

Jibu : Baadhi ya watu wanakimbilia kulifasiri hilo kwa kusema ni sadfa au bahati. Hakuna kinachofahamika kutokana na maelezo hayo zaidi ya kushindwa kwao kutoa tafsiri sahihi. Vinginevyo wasingelikimbilia kwenye maelezo ya kubahatisha tu.

Kwa hiyo sisi tunapinga Sadfa na bahati na tunaamini kwa imani ya mkato kwamba kuna chaguo la juu linajiingiza kwa sababu tusizozijua. kwa vile elimu katika masuala hayo na mfano wake, bado ni changa. Na kushindwa kwa elimu hakumaanishi kuwa kitu hakiko. Imani yetu hii inatiliwa mkazo na kauli zake Mwenyezi Mungu zifuatazo:

﴿وَاللَّـهُ فَضَّلَ بَعْضَكُمْ عَلَىٰ بَعْضٍ فِي الرِّزْقِ﴾

"Na Mwenyezi Mungu amewafadhilisha baadhi yenu kuliko wengine katika riziki" (16:71)

﴿اللَّـهُ يَبْسُطُ الرِّزْقَ لِمَن يَشَاءُ وَيَقْدِرُ﴾

"Mwenyezi Mungu hukunjua riziki kwa amtakaye na huidhikisha (13:26) Ay a hii imekuja kwa herufi zake katika 17:30, 28:82, 29:62, 30:37, 34: 36, 34: 39, 39:52, 42:12.

Kwa hiyo basi aliyesema au anayesema: Mwenyezi Mungu amemtajirisha fulani kwa kuwa yeye ni mwema basi atakuwa anazungumza mantiki ya Firaun na kupima kwa kipimo cha Shetani. Hekima yake Mwenyezi Mungu Mtukufu imetaka kumlipa mwema malipo mazuri na kumwadhibu mwovu katika akhera inayobakia sio katika hii dunia inayokwisha. Hii ni Nyumba ya matendo na ile ni Nyumba ya Hisabu. Zaidi ya haya ni kuwa wingi wa mali wa mwovu huenda ukawa ni balaa kwake na sababu ya kuadhibiwa kwake. Mwenyezi Mungu anasema:

﴿ذَرْهُمْ يَأْكُلُوا وَيَتَمَتَّعُوا وَيُلْهِهِمُ الْأَمَلُ فَسَوْفَ يَعْلَمُونَ﴾

"Waache wale na wafurahi na iwazuge tamaa, watakuja jua." (15:3)

﴿يَتَمَتَّعُونَ وَيَأْكُلُونَ كَمَا تَأْكُلُ الْأَنْعَامُ وَالنَّارُ مَثْوًى لَّهُمْ﴾

"Hujistarehesha na hula kama walivyo wanyama, na moto ndio makazi yao." (47:12)

Kwa ufupi ni kwamba riziki inategemea mambo mawili. Kuhangaika na matakwa ya Mwenyezi Mungu. Asiyehangaika ataishi omba omba; na mwenye kuhangaika Mwenyezi Mungu humruzuku kutokana na bidii yake, akitaka humpa nyingi na akitaka humpa chache.

Uhakika huu umo katika maumbile ya binadamu na anaufanya bila ya kujitambua. Mfanya biashara humwomba Mwenyezi Mungu (s.w.t) amruzuku kupata soko zuri la bidhaa zake na watu wazikubali. Mkulima anamwomba Mungu aiteremshie mimea yake mvua; wala hamuombi kumwoteshea mimea bila ya mvua.

Mimi hapa namwomba Mwenyezi Mungu ampe tawfiq mwanangu katika masomo yake na kufaulu mtihani; wala si mwombi akipe mawazo chuo kikuu kimpatie shahada bila ya kusoma na kufanya mtihani. Iko methali isemayo: Mgaagaa na upwa hali wali mkavu.

Pengine inawezekana mahangaiko yasiambulie kitu, lakini pamoja na hayo inatakikana kupanga mipango na kuongeza juhudi. Kwa sababu kuongeza juhudi, kutumia mipango, na kuvumilia tabu ni sababu ya matakwa ya kufaulu kutoka kwake Mwenyezi Mungu Mtukufu.

﴿يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا لَا تَسْأَلُوا عَنْ أَشْيَاءَ إِن تُبْدَ لَكُمْ تَسُؤْكُمْ وَإِن تَسْأَلُوا عَنْهَا حِينَ يُنَزَّلُ الْقُرْآنُ تُبْدَ لَكُمْ عَفَا اللَّـهُ عَنْهَا وَاللَّـهُ غَفُورٌ حَلِيمٌ﴾

101.Enyi Mlioamini! Msiulize mambo ambayo mkidhihirishiwa yatawachukiza. Na mnapoyauliza inapoteremshwa Qur'an mtabainishiwa. Mwenyezi Mungu ameyasamehe hayo. Na Mwenyezi Mungu ni mwingi wa maghufira Mpole.

﴿قَدْ سَأَلَهَا قَوْمٌ مِّن قَبْلِكُمْ ثُمَّ أَصْبَحُوا بِهَا كَافِرِينَ﴾

102.Waliyauliza watu waliokuwa kabla yenu kisha wakawa makafiri kwayo.

MSIULIZEULIZE MAMBO

Aya 101-102

MAANA

Enyi Mlioamini! Msiulize mambo ambayo mkidhihirishiwa yatawachukiza.

Kauli yake Mwenyezi Mungu 'Msiulize' inaishiria kuwa baadhi ya Masahaba walikuwa waking'ang'ania kuuliza mambo yasiyokuwa na dharura yoyote kuyajua na huenda jibu lake likawaudhi waulizaji. Kuna riwaya isemayo kuwa mtu mmoja alimuuliza Mtume(s.a.w.w) : "Ni nani baba yangu?" Mtume akamwambia, "baba yako ni Fulani" Mwingine akauliza "Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu! Baba yangu yuko wapi? Mtume akajibu: "Yuko motoni," ndipo ikashuka Aya hiyo.

Riwaya nyingine inasema kuwa Mtume alisema: "Mwenyezi Mungu amewafaradhishia kuhiji, basi hijini." Wakauliza: "Kila mwaka ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu?" Mtume akanyamaza. Wakarudia kuuliza, akasema La; lau ningelisema naam, ingelikuwa wajib." Ndipo ikashuku Aya hii. Riwaya hii ndiyo yenye nguvu kuliko ile ya kwanza.

Na mnapoyauliza inapoteremshwa Qur'an mtabainishiwa.

Yaani msijikalifishe kuuliza mambo ila baada ya kuteremshwa Qur'an. Mtakapoanza kuuliza Mtume(s.a.w.w) atawadhirishia mliyokuwa mkiyauliza.

Kwa hali hii, inatubainikia kuwa riwaya ya Hija ndiyo yenye nguvu katika sababu ya kushuka Aya, kuliko riwaya ya kuuliza mababa na wahenga wa Masahaba. Kwa sababu Qur'an inaanza kuleta itikadi na sharia na wala sio kuanzia kwa mababa na mababu wa Masahaba. Katika Hadith imeelezwa:"Hakika Mwenyezi Mungu ameweka mipaka msiikiuke; amewafaradhishia faradhi msizipoteze; ameharamishia vitu msivifanye; na ameacha vitu vingine si kwa kusahau, lakini ni kwa kuwahurumia, basi vikubalini wala msivifanyie utafiti".

Mwenyezi Mungu amesamehe hayo

Yaani maswali yenu yaliyotangulia, kwa hiyo msiyarudie. Imesemekana kuwa maana yake ni amezuia kutaja vitu mlivyoviulizia, basi nanyi jizuieni wala msijikalifu kuviulizia. Tafsir zote mbili zina uwezekano hazikataliwi na dhahiri ya tamko.

Na Mwenyezi Mungu ni mwingi wa maghufira, Mpole.

Humsamehe mkosaji akikosea tena.

Waliyauliza watu waliokuwa kabla yenu kisha wakawa makafiri kwayo.

Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kuwakataza kuuliza mambo wasiyokuwa na haja nayo, anawapigia mfano wa watu waliokuwa kabla yao, waliuliza wakang'ang'ania kuuliza. Walipobainishiwa na Mwenyezi Mungu walichukia wakaasi na wakastahiki adhabu. Lau wangeliacha kuuliza ingelikuwa bora kwao.

Wafasiri wamerefusha maneno katika kubainisha makusudio ya watu waliouliza, kisha wakawa makafiri kwa sababu ya kuuliza, lakini Aya haikubainisha. Pamoja na hivyo, tunaweza kusema kuwa watu waliouliza wakawa makafiri kwa sababu ya kuuliza ni wana wa Israil, kwa sababu ya kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu akiwasimulia:

﴿فَقَدْ سَأَلُوا مُوسَىٰ أَكْبَرَ مِن ذَٰلِكَ فَقَالُوا أَرِنَا اللَّـهَ جَهْرَةً ﴾

"Hakika walimtaka Musa makubwa kuliko hayo, Walisema: Tuonyeshe Mwenyezi Mungu waziwazi" (4:153)

﴿مَا جَعَلَ اللَّـهُ مِن بَحِيرَةٍ وَلَا سَائِبَةٍ وَلَا وَصِيلَةٍ وَلَا حَامٍ وَلَـٰكِنَّ الَّذِينَ كَفَرُوا يَفْتَرُونَ عَلَى اللَّـهِ الْكَذِبَ وَأَكْثَرُهُمْ لَا يَعْقِلُونَ﴾

103.Mwenyezi Mungu hakujaalia Bahira wala Saiba wala Waswila wala Hami; Lakini waliokufuru wanamzulia Mwenyezi Mungu uwongo na wengi wao hawafahamu.

﴿وَإِذَا قِيلَ لَهُمْ تَعَالَوْا إِلَىٰ مَا أَنزَلَ اللَّـهُ وَإِلَى الرَّسُولِ قَالُوا حَسْبُنَا مَا وَجَدْنَا عَلَيْهِ آبَاءَنَا أَوَلَوْ كَانَ آبَاؤُهُمْ لَا يَعْلَمُونَ شَيْئًا وَلَا يَهْتَدُونَ﴾

104.Wakiambiwa njooni katika yale aliyoyateremsha Mwenyezi Mungu na kwa Mtume, husema: Yanatutosha yale tuliyowakuta nayo babu zetu. Je hata kama baba zao walikuwa hawajui kitu wala hawakuongoka?

﴿يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا عَلَيْكُمْ أَنفُسَكُمْ لَا يَضُرُّكُم مَّن ضَلَّ إِذَا اهْتَدَيْتُمْ إِلَى اللَّـهِ مَرْجِعُكُمْ جَمِيعًا فَيُنَبِّئُكُم بِمَا كُنتُمْ تَعْمَلُونَ﴾

105.Enyi mlioamini! Jiangalie nafsi zenu. Hawawadhuru waliopotea ikiwa mmeongoka. Marejeo yenu nyote ni kwa Mwenyezi Mungu. Atawaambia yale mliyokuwa mkiyatenda.

HAKUNA BAHIRAWALA SAIBA

Aya 103-105

MAANA

Mwenyezi Mungu hakujaalia Bahira wala Saiba wala Waswila wala Hami.

Bahira, ni ngamia aliyetobolewa masikio, watu wa wakati wa Jahilia walikuwa wakifanya hivyo, ikiwa ngamia atazaa mimba kumi ; na inasemekana ni mimba tano. Wanamwacha bila ya kutumiwa na mtu yoyote. Saiba ni ngamia waliyemwekea nadhiri kwa waungu, na wana mwacha akijilisha mwenyewe popote bila ya kufungwa wala kuwa na mchungaji sawa na Bahira.

Wasila ni mbuzi anayezaa mtoto wa kiume na wa kike pamoja. Desturi yao ilikuwa kama akizaa mume wanamfanya ni wa waungu na akizaa mke ni wao. Iwapo atazaa mume na mke pamoja, hawamchinji mume wakisema kuwa ameunganishwa na dada yake. Hami ni dume aliyezalisha mimba kumi, wanamwacha hazuiliwi na maji wala malisho, wakisema ameuhami mgongo wake.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) anabainisha kwamba yote hayo hayamo katika dini, na kwamba dume, jike na mbuzi, vyovyote wanavyofanyiwa, wanabakia na uhalali wake kama walivyokuwa mwanzo na wala hawaharamishwi na porojo hizo.

Lakini waliokufuru wanamzulia Mwenyezi Mungu uwongo na wengi wao hawafahamu.

Watu wa kijahilia walikuwa wakikubali kuweko kwa muumba kwa dalili kwamba wao wamenasibishia uharamu wa Hami, Saiba, Bahira na Waswila, lakini pamoja na hayo Mwenyezi Mungu amewanasibishia ukafiri.

Kwa sababu wao wamemnasibishia uharamu kwa uwongo na uzushi. Kwa hiyo, basi kila anayemnasibishia Mwenyezi Mungu na yasiyokuwa na dalili ya Kitab wala Hadith ya Mtume wake basi huyo ni kafir kwa sharti ya kutegemea kumnasibishia Mungu, huku akijua kutokuwepo dalili.

Hii, kwa lugha ya watu wa sharia, huitwa Bid'a (uzushi). Kuna Hadithi isemayo: "Kila bid'a ni upotevu na kila upotevu ni motoni".

Ilivyo ni kuwa kufaradhia huko kuko mbali na hali halisi ilivyo, Ni nani anayemnasibishia hukumu Mwenyezi Mungu huku akijua kuwa hakuna dalili. Pengine anaweza akadhani ni dalili, lakini kumbe sio dalili.

Wakiambiwa njooni katika yale aliyoyateremsha Mwenyezi Mungu na kwa Mtume, husema: "Yanatutosha yale tuliyowakuta nayo babu zetu. Je hata kama babu zao walikuwa hawajui kitu wala hawakuongoka?

Razi anasema: "Maana yanajulikana, nayo ni jibu la kuwapinga watu wa Taqlid (kufuata)". Tumezungumzia kuhusu Taqlid katika Juz.2 (2:170)

Enyi mlioamini! Jiangalieni nafsi zenu, Hawawadhuru waliopotea ikiwa mmeongoka, Marejeo yenu nyote ni kwa Mwenyezi Mungu.

Razi ametaja njia nane za kufasiri Aya hii. Mmoja wa wafasiri wapya ameandika kurasa 33. Lililowafanya wawili hawa na wengineo kurefusha mambo hivi ni kuwa kuamrisha mema ni wajibu na dhahiri ya Aya inafahamisha kutokuwa wajib na kwamba ni juu ya mtu kujishughulikia mwenyewe. Ama wengine wana majukumu yao juu ya nafsi zao wala si wajibu kwa yoyote kuiongoza au kuikanya nafsi ya mwingine.

Ilivyo tafsir ya Aya hii ni kwamba, ni juu ya mtu kuamrisha mema. Kuamrisha kwake kukinufaisha basi hayo ndiyo yanayotakikana. Vinginevyo basi atakuwa ametekeleza lile aliloamrishwa wala hautamdhuru upotevu wa aliyepotea.

Mwenye jukumu baada ya kuamrisha ni yule aliyepotea na wala sio mwamrishaji. Tafsir hii imetilia mkazo wajibu wa kuamrisha mema na sio kupinga.


4

5

6