TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA SABA Juzuu 17

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA SABA33%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA SABA Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: Qurani tukufu

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
  • Anza
  • Iliyopita
  • 15 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 9442 / Pakua: 4151
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA SABA

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA SABA Juzuu 17

Mwandishi:
Swahili

1

7

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA SABA

Sura Ya Ishirini Na Mbili: Surat Al-Hajj.

Baadhi ya Aya zake zimeshuka Makka na nyingine Madina. Ina Aya 78.

بِسْمِ اللَّهِ الرَّحْمَٰنِ الرَّحِيمِ

Kwa jina la Mwenyezi Mungu Mwingi wa rehema Mwenye kurehemu.

يَا أَيُّهَا النَّاسُ اتَّقُوا رَبَّكُمْ إِنَّ زَلْزَلَةَ السَّاعَةِ شَيْءٌ عَظِيمٌ ﴿١﴾

1. Enyi watu! Mcheni Mola wenu. Hakika tetemeko la saa ni jambo kuu.

يَوْمَ تَرَوْنَهَا تَذْهَلُ كُلُّ مُرْضِعَةٍ عَمَّا أَرْضَعَتْ وَتَضَعُ كُلُّ ذَاتِ حَمْلٍ حَمْلَهَا وَتَرَى النَّاسَ سُكَارَىٰ وَمَا هُم بِسُكَارَىٰ وَلَـٰكِنَّ عَذَابَ اللَّـهِ شَدِيدٌ ﴿٢﴾

2. Siku mtakapoiona, kila mwenye kunyonyesha atamsahau amnyonyeshae na kila mwenye mimba ataiharibu mimba yake. Na utawaona watu wamelewa, na kumbe hawakulewa. Lakini adhabu ya Mwenyezi Mungu ni kali.

وَمِنَ النَّاسِ مَن يُجَادِلُ فِي اللَّـهِ بِغَيْرِ عِلْمٍ وَيَتَّبِعُ كُلَّ شَيْطَانٍ مَّرِيدٍ ﴿٣﴾

3. Na miongoni mwa watu kuna anayejadiliana juu ya Mwenyezi Mungu bila ya elimu na anamfuata kila shetani muasi.

كُتِبَ عَلَيْهِ أَنَّهُ مَن تَوَلَّاهُ فَأَنَّهُ يُضِلُّهُ وَيَهْدِيهِ إِلَىٰ عَذَابِ السَّعِيرِ ﴿٤﴾

4. Ameandikiwa kwamba anayemtawalisha shetani, basi huyo hakika atampoteza na atamwongoza katika adhabu ya moto mkali.

يَا أَيُّهَا النَّاسُ إِن كُنتُمْ فِي رَيْبٍ مِّنَ الْبَعْثِ فَإِنَّا خَلَقْنَاكُم مِّن تُرَابٍ ثُمَّ مِن نُّطْفَةٍ ثُمَّ مِنْ عَلَقَةٍ ثُمَّ مِن مُّضْغَةٍ مُّخَلَّقَةٍ وَغَيْرِ مُخَلَّقَةٍ لِّنُبَيِّنَ لَكُمْ وَنُقِرُّ فِي الْأَرْحَامِ مَا نَشَاءُ إِلَىٰ أَجَلٍ مُّسَمًّى ثُمَّ نُخْرِجُكُمْ طِفْلًا ثُمَّ لِتَبْلُغُوا أَشُدَّكُمْ وَمِنكُم مَّن يُتَوَفَّىٰ وَمِنكُم مَّن يُرَدُّ إِلَىٰ أَرْذَلِ الْعُمُرِ لِكَيْلَا يَعْلَمَ مِن بَعْدِ عِلْمٍ شَيْئًا وَتَرَى الْأَرْضَ هَامِدَةً فَإِذَا أَنزَلْنَا عَلَيْهَا الْمَاءَ اهْتَزَّتْ وَرَبَتْ وَأَنبَتَتْ مِن كُلِّ زَوْجٍ بَهِيجٍ ﴿٥﴾

5. Enyi watu! Ikiwa mna shaka ya kufufuliwa, basi kwa hakika tuliwaumba kutokana na udongo kisha kutokana na tone kisha kutokana na pande la damu kisha kutokana na pande la nyama lenye umbo na lisilokuwa na umbo. Ili tuwabainishie. Na tunaliweka katika matumbo ya kizazi mpaka muda uliowekwa. Kisha tunawatoa hali ya kuwa mtoto mchanga kisha mfikie kukomaa kwenu. Na wapo miongoni mwenu wanaokufa na wapo miongoni mwenu wanorudishwa kwenye umri wa unyonge kabisa hata asijue kitu baada ya kuwa anakijua. Na unaiona ardhi imekufa, lakini tunapoyateremsha maji juu yake, husisimka na kututumka na kumea kila aina ya mimea mizuri.

ذَٰلِكَ بِأَنَّ اللَّـهَ هُوَ الْحَقُّ وَأَنَّهُ يُحْيِي الْمَوْتَىٰ وَأَنَّهُ عَلَىٰ كُلِّ شَيْءٍ قَدِيرٌ ﴿٦﴾

6. Hayo ni kwa sababu hakika Mwenyezi Mungu ni haki na kwamba hakika yeye ndiye Mwenye kuhuisha wafu na kwamba hakika Yeye ni Muweza wa kila kitu.

وَأَنَّ السَّاعَةَ آتِيَةٌ لَّا رَيْبَ فِيهَا وَأَنَّ اللَّـهَ يَبْعَثُ مَن فِي الْقُبُورِ ﴿٧﴾

7. Na kwamba saa itakuja hapana shaka kwa hilo, na kwamba Mwenyezi Mungu atawafufua walio makaburini.

UFUFUO

Aya 1 – 7

MAANA

Katika Aya hizi kuna kutahadharisha kuhusu siku ya Kiyama pamoja na kuashiria vitu na shida za siku hiyo. Vile vile kuwashutumu wale walioghafilika nacho; kisha kutoa dalili ya ufufuo.

Ufafanuzi ni kama ufuatavyo:

1.Enyi watu! Mcheni Mola wenu. Hakika tetemeko la saa ni jambo kuu.

Makusudio ya saa ni siku ya Kiyama. Kimeitwa hivyo kwa sababu kila mtu atakifikia; kama anavyosema Mulla Sadra katika kitabu Al-Asfar.

Maana ya tetemeko la kiyama ni kuharibika ulimwengu ikiwa ni pamoa na ardhi yake na mbingu yake. Hizo zitachanganyika na pia bara na bahari na vizuizi vitaondoka. Miili itatoka makakburini kama picha isiyo na roho.

Siku mtakapoiona, kila mwenye kunyonyesha atamsahau amnyonyeshae na kila mwenye mimba ataiharibu mimba yake. Na utawaona watu wamelewa, na kumbe hawakulewa. Lakini adhabu ya Mwenyezi Mungu ni kali.

Hiki ni kinaya cha vituko vya siku ya Kiyama na shida zake; ambapo hakutakuwa na mnyonyeshaji wala mwenye mimba sku hiyo. Yaani, lau angelikuwako mwenye kunyonyesha basi angelimsau mwanawe na mwenye mimba angelizaa. Na watu wote watagongana huku na huko kama walevi.

MJADALA WAKIJINGA NA UPOTEVU

2.Na miongoni mwa watu wako wanaojadiliana juu ya Mwenyezi Mungu bila ya elimu.

Mtu yeyote atakuwa ni mmoja wapo kati ya wawili: Ama atakuwa hajui au atakuwa ni mjuzi. Huyo mjuzi naye yuko katika hali mbili: Ama atakuwa ni mwenye insafu au atakuwa mpotevu. Mwenye insafu ni yule anayesema yale anayoyajua na kuyanyamazia asiyoyajua. Mwenyezi Mungu ameueleza wadhifa wa asiyejua kwa kusema:

فَاسْأَلُوا أَهْلَ الذِّكْرِ إِن كُنتُمْ لَا تَعْلَمُونَ ﴿٧﴾

“Basi waulizeni wenye kumbukumbu, ikiwa nyinyi hamjui.” (21:7).

Ikiwa atauepuka wadhifa huu, basi atakuwa amehusika na kauli ya Imam Ali(a.s) :“Yu mjinga, anatangatanga gizani bila ya mwongozo.”

Huu ndio ujinga alioukusudia Mwenyezi Mungu kwenye kauli yake hii na pia kauli itakayokuja kwenye Aya ya 8 ya Sura hii: “Na katika watu wapo wanaojadiliana juu ya Mwenyezi Mungu bila ya ilmu wala uongufu wala Kitabu chenye nuru.”

Hajui njia ya kumjua Mwenyezi Mungu, lakini anabishana kuhusu Mungu, huku akisema: lau Mwenyezi Mungu angelikuwako tungelimuona. Kwa mantiki haya, anataka kufasiri mada kwa isiyokuwa mada, kuona kwa macho kile kinachonekana kwa akili tu na kumgusa kwa mkono muumba wa mbingu na ardhi.

Huyu hana tofauti na yule anayetaka kufanya mtihani wa nadhariya ya ‘ushahidi ni wa mwenye kudai na kiapo ni kwa mwenye kukanusha’ kwenye kiwanda. Au kutaka kufanya mtihani wa kuendesha gari kutokana na hisia zake.

Wakati nikiandika maelezo haya nimekumbuka tulipokua Najaf tukisoma, kiasi cha miaka arobaini iliyopita. Siku moja tulipokuwa kwenye darasa tukisiliza mhadhara wa mwalimu, mmoja wa wanafunzi akamkatiza mwalimu na akatoa ushahidi usiokuwa na uhusiano wowote na maudhui kwa umbali wala karibu. Basi mwalimu akaachana naye akawaangalia wanafunzi wengine na akasema:

“Hapo zamani kulikuwa na mtu mmoja mwenye akili punguani, jina lake ni Bau. Siku moja alipita barabarani akaona watu wamekusanyika. Akauliza, kulikoni? Akaambiwa fulani ameanguka kutoka juu ya nyumba, amaevunjikavunjika viungo hatujui kama ataishi na watu wake hawana la kufanya.

Basi Bau akasema: “Mimi nina suluhisho, mfungeni kamba mumkaze sawasawa kisha avutwe mpaka juu ya nyumba kule alikotokea, atapona tu.” Watu walipomcheka, alitoa hoja kwamba mwaka jana fulani alianguka kisimani, wakamfunga kamba na wakamtoa, akasalimika.”

Mantiki haya hasa ndiyo ya yule anayekana kuweko Mungu kwa vile hamuoni. Ulimwengu huu na nidhamu yake anauona, lakini bado anadai kuwa haufahamishi kuwako aliyeutengeneza na kuuwekea nidhamu.

Sisi tunaamini ushahidi na majaribio, lakini tunaamini vilievile kuwa majaribio haya hayawezi kuwa kwenye kila kitu, bali yanakuwa kwenye baadhi ya vitu vya kimaada. Ama vitu vya kiroho na vya kibinadamu vina njia nyingine ya kujua.

Tunasema hivi tukiwa na uhakika kwamba hivi viwili vinakwenda pamoja vikikamilishana na kwamba mtu anahitajia maada. Misimamo kama vile haki na kheri haina budi iwe na athari inayoonekana, vinginevyo ingelikuwa ni matamshi tu yasiyokuwa na maana yoyote.

Lakini hii haimaanishi kuwa ndio njia ya maarifa peke yake; bali inatofautiana kwa kutofautiana vitu. Kwa hiyo ushahidi na majaribio ni sababu ya kujua vitu vya kimaada na akili ni sababu ya kujua vinginevyo visivyokuwa maada.

Tumezungumzia kuhusu maarifa na sababu zake katika Juz. 1(2:3-5)

Kwa ufupi ni kuwa mwenye kusema: Simwamini Mungu mpaka nimuone, amekiri yeye mwenyewe kwamba hataki kumwamini Mwenyezi Mungu, hata kama ataletewa dalili elfu na moja. Maana yake ni kuwa anakubali kuwa yeye ni mjinga mwenye kiburi.

Kwa sababu Mwenyezi Mungu hawezi kuonekana kwa macho na kwamba njia ya kujua haikomei kwenye macho tu. Mwenyezi Mungu anamtaka binadamu afanye utafiti, uchunguzi, mjadala na mdahalo, lakini kielimu na kuchunga haki, sio kiujinga na kiupofu.

Na anamfuata kila shetani muasi.

Kila anayeweza kuvunga na kuficha hakika yake, basi huyo ni shetani. Shetani asi ni yule ambaye vitendo vyake na kauli zake zote zimejaa ufisadi. Shetani huyu akiingia kwenye akili ya mtu tu humuongoza kwenye upotevu na maangamizi. Hii ndio maana ya kauli yake Mwenyezi Mungu:

Ameandikiwa kwamba anayemtawalisha shetani, basi huyo hakika atampoteza na atamwongoza katika adhabu ya moto mkali.

Upotevu na adhabu ya moto hawezi kuepukana nayo yule mwenye kufuata wapotevu na wafisadi, ambao wanayapotoa maneno ya Mwenyezi Mungu, wakihalalisha na kuharamisha kwa hawa zao na matakwa yao.

3.Enyi watu ikiwa mna shaka ya kufufuliwa, basi kwa hakika tuliwaumba kutokana na udongo.

Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kumhadharisha yule anayebishana kuhusu Mwenyezi Mungu bila ya elimu, sasa anataja dalili za ufufuo ambao mjinga anauifikiria kuwa hauwezekani.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) amezileta dalili hizi kwa mifano yenye kuhisiwa, nayo ni kuwa: Hakika Mwenyezi Mungu amemuumba mtu kutokana na mchanga moja kwa moja, au kupitia kitu kingine.

Alimuumba Adam, baba wa watu, moja kwa moja kutokana na mchanga na akatuumba sisi wana wa Adam kupitia kitu kingine. Kila mmoja wenu anakuwa kutokana na manii na damu navyo vinatokana na chakula ambacho kinatokana na mchanga na maji. Kwa hiyo mchanga ndio msingi wa kupatikana mtu, kisha kutokana na tone la manii; kama alivyosema Mwenyezi Mungu:

أَلَمْ يَكُ نُطْفَةً مِّن مَّنِيٍّ يُمْنَىٰ ﴿٣٧﴾

“Je, hakuwa ni tone la manii lililoshushwa?” (75:37).

Kisha kutokana na pande la damu. Tone la manii linageuka kuwa kipande cha damu iliyoganda,kisha kutokana na pande la nyama. Pande la damu nalo linabadilika kuwa pande la nyamalenye umbo na lisilokuwa na umbo. Yaani baadhi yake imetimia umbo na sehemu haijatimia.Ili tuwabainishie uwezo wetu wa kufufua na mengineyo.

Na tunaliweka katika matumbo ya kizazi mpaka muda uliowekwa wa kuzaliwa mtoto.

Kisha tunawatoa hali ya kuwa mtoto mchanga kisha mfikie kukomaa kwenu . Kukomaa ni kukamilika mtu nguvu za kimwili na kiakili.

Na wapo miongoni mwenu wanaokufa kabla ya kukomaa au baada ya kukomaa kabla ya uzee na umri mbaya.

Na wapo miongoni mwenu wanorudishwa kwenye umri wa unyonge kabisa hata asijue kitu baada ya kuwa anakijua.

Ni uzee na ukongwe, udhaifu wa kimwili, kiakili na kumbukumbu. Inapodhoofika akili matamanio yanachukua nafasi na kuzidi kufanya mambo ya kipuuzi.

Mabadiliko haya ya kukua kwa binadamu, kutoka hali duni hadi hali ya juu; kutoka mchanga hadi manii, kisha pande la damu, la nyama, utoto hadi kukomaa, yanafahamisha waziwazi kwamba binadamu ana nguvu na maandalizi yatakayompeleka kwenye ukamilifu na ubora, ikiwa hakutakuwa na vizuizi vya kuzuia kufikia lengo hili.

Na unaiona ardhi imekufa, lakini tunapoyateremsha maji juu yake, husisimka na kututumka na kumea kila aina ya mimea mizuri.

Maji yakishuka kwenye ardhi iliyokufa hutaharaki na kupumua kwa uhai, kisha inatoa aina kwa aina za mimea inayovutia macho na yenye ladha kwa walaji.

Hakuna mwenye shaka kwamba ardhi ni maandalizi ya kuukabili uhai, lakini mpaka kwa idhini ya Mwenyezi Mungu Mtukufu. Kwa sababu kila kitu kinaishia kwenye kauli yake ‘kuwa na kinakuwa’ Baadhi ya masufi wanasema: Makusudio ya ardhi iliyokufa ni ujinga, maji ni elimu na aina mbalimbali za mimea ni sifa za ukamilifu za Mwenyezi Mungu.

Hayo ni kwa sababu hakika Mwenyezi Mungu ni haki na kwamba hakika yeye ndiye Mwenye kuhuisha wafu na kwamba hakika Yeye ni Muweza wa kila kitu na kwamba saa itakuja hapana shaka kwa hilo na kwamba Mwenyezi Mungu atawafufua walio makaburini.

Hayo ni ishara ya mambo yalivyo. Maana ya kuwa Mwenyezi Mungu ni haki ni kwamba hukumu na ufalme ni wake yeye peke yake bila ya kushirikiana na yeyote na kwamba hakuna kupatikana isipokuwa kutokana na yeye.

Hiyo ikiwa na maana kwamba yeye ndiye mwanzishaji na mrudishaji na ufufuo utakuwako tu kama ulivyokuwako uumbaji; bali huo uumbaji ni nyenzo na njia ya kufikia ufufuo ambao ndio lengo la malengo yote.

Kwa sababu mtu anarejea kwa muumba wake kuhisabiwa na kulipwa na pia hapo ndio pa kubakia, lakini kule kuumbwa kwa kwanza kuliisha. Kwisha ni nyenzo ya kubakia.

Hapa ndio tunakuta tafsiri ya kauli yake Mwenyezi Mungu:

وَمَا خَلَقْتُ الْجِنَّ وَالْإِنسَ إِلَّا لِيَعْبُدُونِ ﴿٥٦﴾

“Na sikuumba majini na watu ila waniabudu.” (51:56).

Yametangulia maelezo ya ufufuo katika Aya kadhaa; miongoni mwazo ni: Juz. 1 (2:28-29) kifungu cha ‘Ufufuo,’ Juz. 5 (4:85-87) kifungu cha ‘Njia mabalimbali za kuthibitisha marejeo (ufufuo) na Juz. 13 (13: 5-7) kifungu cha ‘Wanaoamini maada na maisha baada ya mauti.’

وَمِنَ النَّاسِ مَن يُجَادِلُ فِي اللَّـهِ بِغَيْرِ عِلْمٍ وَلَا هُدًى وَلَا كِتَابٍ مُّنِيرٍ ﴿٨﴾

8. Na katika watu wapo wanaojadiliana juu ya Mwenyezi Mungu bila ya ilimu wala uongufu wala Kitabu chenye nuru.

ثَانِيَ عِطْفِهِ لِيُضِلَّ عَن سَبِيلِ اللَّـهِ لَهُ فِي الدُّنْيَا خِزْيٌ وَنُذِيقُهُ يَوْمَ الْقِيَامَةِ عَذَابَ الْحَرِيقِ ﴿٩﴾

9. Anayegeuza shingo yake ili awapoteze watu na njia ya Mwenyezi Mungu. Duniani atapata hizaya na siku ya Kiyama tutamuonjesha adhabu ya kuungua.

ذَٰلِكَ بِمَا قَدَّمَتْ يَدَاكَ وَأَنَّ اللَّـهَ لَيْسَ بِظَلَّامٍ لِّلْعَبِيدِ ﴿١٠﴾

10. Hayo ni kwa sababu ya iliyotanguliza mikono yako na kwamba Mwenyezi Mungu si mwenye kuwadhulumu waja.

وَمِنَ النَّاسِ مَن يَعْبُدُ اللَّـهَ عَلَىٰ حَرْفٍ فَإِنْ أَصَابَهُ خَيْرٌ اطْمَأَنَّ بِهِ وَإِنْ أَصَابَتْهُ فِتْنَةٌ انقَلَبَ عَلَىٰ وَجْهِهِ خَسِرَ الدُّنْيَا وَالْآخِرَةَ ذَٰلِكَ هُوَ الْخُسْرَانُ الْمُبِينُ ﴿١١﴾

11. Na katika watu wapo wanaomwabudu Mwenyezi Mungu ukingoni. Ikimfika kheri hutulia kwayo, na ukimfikia msukosuko hugeuza uso wake. Amepata hasara ya dunia na Akhera; hiyo ndiyo hasara iliyo wazi.

يَدْعُو مِن دُونِ اللَّـهِ مَا لَا يَضُرُّهُ وَمَا لَا يَنفَعُهُ ذَٰلِكَ هُوَ الضَّلَالُ الْبَعِيدُ ﴿١٢﴾

12. Anaomba, badala ya Mwenyezi Mungu, kile kisichomdhuru wala kumnufaisha. Huko ndiko kupotelea mbali.

يَدْعُو لَمَن ضَرُّهُ أَقْرَبُ مِن نَّفْعِهِ لَبِئْسَ الْمَوْلَىٰ وَلَبِئْسَ الْعَشِيرُ ﴿١٣﴾

13. Anamuomba yule ambaye hakika dhara iko karibu zaidi kuliko nafuu yake. Hakika ni mlinzi mbaya na ni rafiki mbaya.

إِنَّ اللَّـهَ يُدْخِلُ الَّذِينَ آمَنُوا وَعَمِلُوا الصَّالِحَاتِ جَنَّاتٍ تَجْرِي مِن تَحْتِهَا الْأَنْهَارُ إِنَّ اللَّـهَ يَفْعَلُ مَا يُرِيدُ ﴿١٤﴾

14. Hakika Mwenyezi Mungu atawaingiza wale walioamini na wakatenda mema katika bustani zipitazo mito chini yake. Hakika Mwenyezi Mungu hufanya ayatakayo.

SABABU YA MAARIFA KATIKA AYA MOJA

Aya 8 – 14

MAANA

Na katika watu wapo wanaojadiliana juu ya Mwenyezi Mungu bila ya ilimu wala uongufu wala Kitabu chenye nuru.

Wewe unaona hii ndiyo haki na ile ni batili, lakini ni lipi lililokujulisha kwamba rai yako ni sahihi na salama? Una dhamana gani ya usahihi huo? Inawezekekana kuwa ile unayoiona ni haki kumbe ni batili na ile unayoiona ni batili kumbe ni haki.

Hakuna njia ya kujua maarifa sahihi isipokuwa kwa kurejea kwenye chimbuko lake na sababu iliyotokana nayo. Ikiwa sababu ni sahihi basi maarifa nayo yatakuwa sahihi; vinginevyo yatakuwa batili. Kwa sababu tawi lina- fuata shina.

Swali linarudi tena : Je, ni ipi hiyo sababu ya maarifa sahihi? Utaitambuaje?

Jamaa katika wanafalsafa wanasema kuwa: sababu ya maarifa sahihi inakuwa kwenye majaribio ya hisia tu. Wengine wakasema ni akili; na hisia ni vyombo tu. Ama Qur’an, katika Aya tunayoifasiri, imetaja sababu tatu za maarifa: Kwanza ni majaribio ya hisiya yaliyotajwa kwa neno ‘ilimu’ Ya pili ni akili iliyoitwa ‘Uongofu’ Ya tatu ni Wahyi iliyokusudiwa kwenye neno ‘Kitabu chenye nuru’.

Majaribo ya hisia yanakuwa ni sababu ya kujua vitu vya kimaada tu. Kwa sababu ndivyo vinavyoweza kuhisiwa na kufanyiwa majaribio. Tena majaribio haya huwa yanahitajia akili, kwa sababu hisia haziwezi kutambua kitu ila kwa msaada wa akili.

Ni akili pekee ndiyo inayoweza kujua na kuthibitisha kuweko Mungu. Ama utume unathibitika kwa akili na kwa miujiza. Ukitaka ibara ya ndani zaidi sema: Utume unathibitika kwa miujiza inayothibitishwa na akili na kuikubali kuwa imetoka mbinguni sio ardhini.

Ama wahyi ni sababu ya kujua kila uliyokuja nayo. Wahyi ndio njia pekee ya kujua mambo ya ghaibu; kama majini, Malaika, Kiyama, namna ya hisabu na na malipo kwenye ufufuo n.k.

Anayegeuza shingo yake ili awapoteze watu na njia ya Mwenyezi Mungu. Duniani atapata hizaya, na siku ya Kiyama tutamuonjesha adhabu ya kuungua.

Kugeuza shingo ni kinaya cha kiburi.

Yeye hajui kitu, anajadili kuhusu Mungu bila ya ujuzi, ana kiburi kinachomuhadaa na ni mpotevu na mpotezaji. Hakuna malipo ya wajinga weneye kiburi isipokuwa kudharaulika na kupuuzwa na watu na adhabu kali kutoka kwa Mwenyezi Mungu.

Hayo ni kwa sababu ya iliyotanguliza mikono yako na kwamba Mwenyezi Mungu si mwenye kuwadhulumu waja. Kwa sababu amewaondolea udhu- ru kwa kuwapa akili, kuwapelekea mitume na akateremsha vitabu.

Na katika watu wapo wanaomwabudu Mwenyezi Mungu ukingoni.

Katika Aya iliyotangulia Mwenyezi Mungu (s.w.t) amemtaja anayemkufuru Mwenyezi Mungu na kumjadili bila ya elimu. Hapa anamtaja yule anayemwabudu Mwenyezi Mungu ukingoni.

Wafasiri wametofautiana katika makusudio ya kabudu ukingoni. Kuna waliosema kuwa ni kumwabudu Mwenyezi Mungu pamoja na shaka katika dini. Wengine wakasema ni kumwabudu kwa ulimi tu sio kwa moyo na kauli nyingine.

Hakuna haja ya kutofautiana huku wakati Mwenyezi Mungu amekwisha mbainisha anayemwabudu ukingoni kwa kusema:

Ikimfika kheri hutulia kwayo na ukimfikia msukosuko hugeuza uso wake.

Makusudio ya kheri hapa ni mambo ya kufurahisha na misukosuko ni madhara. Kutulia ni kuwa na raha na kuendelea na ibada, na kugeuza uso ni kurtadi dini. Maana ni kuwa anayemwabudu Mwenyezi Mungu ukingoni ni yule anayeweka sharti kwa ibada yake, mpaka apate kitu ndio anaabudu vinginevyo humkufuru Mungu, vitabu vyake na mitume yake.

Na yoyote mwenye kumkufuru basi malipo yake ni Jahannam na ni mwisho mbaya.

Amepata hasara ya dunia na Akhera; hiyo ndiyo hasara iliyo wazi.

Amepata hasara ya nyumba mbili: ambapo mwanzo ni balaa na madhara. Pili, atafika kwa Mola wake akiwa anamkufuru. Kuna hasara kubwa zaidi ya ufukara duniani na adhabu akhera.

Ufafanuzi zaidi wa Aya hii ni riwaya inayosema kwamba baadhi ya mabedui walikuwa wakifika kwa Mtume(s.a.w.w) wakihama kutoka ubeduini kwao.

Basi mmoja wao akiwa na mali nyingi huswali na kufunga. Akipatwa na masaibu au akicheleweshewa sadaka basi huritadi. Nimeyashuhudia yanayofanana na haya nilipokuwa nikiishi na baadhi ya wanakijiji.

Baada ya hayo, hakika mumin wa kweli ni yule anayemfanyia ikhlasi Mwenyezi Mungu na kumtegemea katika hali zote; anakuwa na subira wakati wa shida na anashukuru wakati wa raha.

Katika Nahjul balagha kuna maelezo haya: “Haiwi kweli imani ya mja mpaka yawe yaliyo mikononi mwa Mwenyezi Mungu anayategemea zaidi kuliko yaliyo mikononi mwake.”

Anaomba, badala ya Mwenyezi Mungu, kile kisichomdhuru wala kumnufaisha. Huko ndiko kupotelea mbali.

Maana ya Aya hii yametangulia kwenye Aya nyingi, yenyewe pia iko wazi.

Anamuomba yule ambaye hakika dhara iko karibu zaidi kuliko nafuu yake. Hakika ni mlinzi mbaya na ni rafiki mbaya.

Unaweza kuuliza kuwa : katika Aya ya kwanza Mwenyezi Mungu amekanusha kuweko manufaa na madhara kwa yale wanayoyaabudu washirikina, kisha katika Aya hii anathibitisha kuweko manufaa ya mbali na madhara ya karibu. Je, kuna wajihi gani baina ya Aya mbili hizi?

Jibu : makusudio ya chenye kuabudia katika Aya ya kwanza ni mawe; hayanufaishi wala hayadhuru. Na makusudio katika Aya ya pili ni kuwatii viongozi mataghuti na kuwataka usaidizi kwa kukusudia kupata faida na manufaa, na ukubwa wa manufaa ya duniani si chochote kulinganisha na ghadhabu za Mwenyezi Mungu na adhabu yake.

Kwa maneno mengine ni kwamba wao wanamtii kiumbe kwa kumuasi muumba kwa ajili ya manufaa ya dunia, hawajui kwamba adhabu ya Mwenyezi Mungu ni kali na kubwa zaidi.

Hakika Mwenyezi Mungu atawaingiza wale walioamini na wakatenda mema katika bustani zipitazo mito chini yake.

Aya iko wazi na pia imekwishatangulia katika Juz. 1 (2: 25).

Hakika Mwenyezi Mungu hufanya ayatakayo katika kuwapa thawabu wema na kuwaadhibu waovu. Na amekwishapitisha kuwa waliofanya mema atawalipa mema na wabaya atawalipa ubaya kutona na waliyoyafanya.

8

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA SABA

مَن كَانَ يَظُنُّ أَن لَّن يَنصُرَهُ اللَّـهُ فِي الدُّنْيَا وَالْآخِرَةِ فَلْيَمْدُدْ بِسَبَبٍ إِلَى السَّمَاءِ ثُمَّ لْيَقْطَعْ فَلْيَنظُرْ هَلْ يُذْهِبَنَّ كَيْدُهُ مَا يَغِيظُ ﴿١٥﴾

15. Anayedhani kwamba Mwenyezi Mungu hatamnusuru katika dunia na Akhera, basi na afunge kamba mbinguni kisha aikate, aone je, hila yake itaondoa yale yaliyomghadhabisha?

وَكَذَٰلِكَ أَنزَلْنَاهُ آيَاتٍ بَيِّنَاتٍ وَأَنَّ اللَّـهَ يَهْدِي مَن يُرِيدُ ﴿١٦﴾

16. Na namna hiyo tumeiteremsha kuwa ni Aya zilizo wazi na kwamba Mwenyezi Mungu humuongoza anayetaka.

إِنَّ الَّذِينَ آمَنُوا وَالَّذِينَ هَادُوا وَالصَّابِئِينَ وَالنَّصَارَىٰ وَالْمَجُوسَ وَالَّذِينَ أَشْرَكُوا إِنَّ اللَّـهَ يَفْصِلُ بَيْنَهُمْ يَوْمَ الْقِيَامَةِ إِنَّ اللَّـهَ عَلَىٰ كُلِّ شَيْءٍ شَهِيدٌ ﴿١٧﴾

17. Hakika wale ambao wameamini na ambao ni mayahudi na wasabai na wanaswara na wamajusi na wale washirikishao, hakika Mwenyezi Mungu atawapambanua siku ya Kiyama. Hakika Mwenyezi Mungu ni shahidi juu ya kila kitu.

أَلَمْ تَرَ أَنَّ اللَّـهَ يَسْجُدُ لَهُ مَن فِي السَّمَاوَاتِ وَمَن فِي الْأَرْضِ وَالشَّمْسُ وَالْقَمَرُ وَالنُّجُومُ وَالْجِبَالُ وَالشَّجَرُ وَالدَّوَابُّ وَكَثِيرٌ مِّنَ النَّاسِ وَكَثِيرٌ حَقَّ عَلَيْهِ الْعَذَابُ وَمَن يُهِنِ اللَّـهُ فَمَا لَهُ مِن مُّكْرِمٍ إِنَّ اللَّـهَ يَفْعَلُ مَا يَشَاءُ ﴿١٨﴾

18. Je huoni kuwa vinamsujudia Mwenyezi Mungu vilivyo mbinguni na vilivyo ardhini na jua na mwezi na nyota na milima na miti na wanyama na wengi miongoni mwa watu. Na wengi imewastahili adhabu. Na anayetwezwa na Mwenyezi Mungu hana wa kumheshimu. Hakika Mwenyezi Mungu hutenda apendayo.

AJINYONGE

Aya 15 -18

LUGHA

Wengi wamesema kuwa makusudio ya mbingu hapa ni dari ya nyumba, kukata ni kujinyonga na hila yake ni huko kujinyonga kwake. Kwa hiyo maana yatakuwa: Anayedhani kwamba Mwenyezi Mungu hatamnusuru katika dunia na Akhera, basi na afunge kitanzi ajinyonge aone je huko kujinyonga kutamuondolea ghadhabu yake?

MAANA

Anayedhani kwamba Mwenyezi Mungu hatamnusuru katika dunia na Akhera, basi na afunge kamba mbinguni kisha aikate, aone je, hila yake itaondoa yale yaliyomghadhabisha?

Wafasiri wengi wamesema kuwa dhamiri ya ‘hawatamnusuru’ inamrudia Muhammad(s.a.w.w) na maana yawe: Anayedhani katika washirikina kuwa Mwenyezi Mungu hatamnusuru Mtume wake Muhammad(s.a.w.w) , basi na amnyonge aone kama Mwenyezi Mungu hatamnusuru Mtume wake.

Lakini dhahiri ya mfumo wa Aya inaonyesha kuwa dhamiri inamrudia huyo anayedhani, kwa sababu Muhammad(s.a.w.w) hakutajwa katika Aya. Na maana yanakuwa:

Ambaye ameshukiwa na balaa na akachukia kadha ya Mwenyezi Mungu na kadari yake, akakata tamaa kwamba Mwenyezi Mungu atamsaidia duniani na kumpa thawabu akhera kwa sababu ya kuvumilia kwake, atakayekuwa hivyo basi hatakuwa na la kufanya isipokuwa kujinyonga kwa kujifunga kamba kwenye dari ya nyumba yake; kisha aangalie je, hilo ndilo suluhisho?

Mwenye akili anapotokewa na balaa, hufanya juhudi na bidii kuiondoa huku akitaka msaada kwa Mwenyezi Mungu, akifaulu ni sawa, la sivyo humwachia Mwenyezi Mungu mambo yote huku akingoja fursa.

Na namna hiyo tumeiteremsha kuwa ni Aya zilizo wazi na kwamba Mwenyezi Mungu humuongoza anayetaka.

Dhamiri katika iliyoteremshwa inarudia Qur’an. Mwenyezi Mungu (s.w.t) humwongoza anayetaka kuongoka kwa Kitabu chake na humwongoza kwenye wema wa nyumba mbili yule anayetafuta mwongozo kwake na kwa Mtume wake.

Na mwenye kutafuta upotevu na ufisadi ataipata njia yake kwa wafisadi na wapotevu.

Hakika wale ambao wameamini na ambao ni mayahudi na wasabai na wanaswara na wamajusi na wale washirikishao, hakika Mwenyezi Mungu atawapambanua siku ya Kiyama. Hakika Mwenyezi Mungu ni shahidi juu ya kila kitu.

Wasabai wanamwamini Mwenyezi Mungu na siku ya mwisho, lakini wanaamini kuwa baadhi ya nyota zina athari katika kheri na shari, wamajusi wanaabudu moto kwa kusema kuwa kheri inatokana na nuru na shari inatokana na giza na wanaswara ni wakristo.

Mwenyezi Mungu anayajua makundi yote haya sita na atayapambanua kesho siku ya Kiyama na kumlipa kila mmoja kwa vile alivyofanya. Kafiri atamwingiza motoni na mumin atamwingiza Peponi. Umetangulia mfano wa Aya hii katika Juz. 1 (2:117).

Je huoni kuwa vinamsujudia Mwenyezi Mungu vilivyo mbinguni na vilivyo ardhini na jua na mwezi na nyota na milima na miti na wanyama.

Wamesema jamaa katika wafasiri kwamba makusudio ya kusujudi wanyama mimea n.k. Ni kutii amri yake na kwamba yeye anawafanyia vile atakavyo.

Katika Juz. 15 (17:44) tumeeleza kuwa makusudio ya kusujudi vitu visivyo na harakati, miti na mimea ni kule kufahamisha kwake kuweko muumba wake na utukufu wake. Mulla Sadra katika kitabu Al-Asfar anasema: “Vitu vyote vina akili, vinamfahamu Mola wake na kumjua muumba wake, vinasikia maneno yake na kufuata amri yake”

Haya hayako mbali, akili inakubali na dhahiri ya nukuu inalithibitisha. Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema:

وَإِن مِّن شَيْءٍ إِلَّا يُسَبِّحُ بِحَمْدِهِ وَلَـٰكِن لَّا تَفْقَهُونَ تَسْبِيحَهُمْ إِنَّهُ كَانَ حَلِيمًا غَفُورًا ﴿٤٤﴾

“Na hapana kila kitu ila kinamtakasa kwa sifa zake, lakini nyinyi hamfahamu kutakasa kwake.” Juz. 15 (17:44).

Sayansi itagundua hakika hii hivi karibuni au baadaye.

Na wengi miongoni mwa watu wanamwamini na wanamsujudia.Na wengi miongoni mwaoimewastahili adhabu .

Hao ni wale waliomkufuru Mwenyezi Mungu wanaowadharau wale wanaomwamini Mungu. Ilikuwa inafaa kwa mwenye kitabu Al-Asfar, awavue wanaomkana Mungu katika viumbe.

Na anayetwezwa na Mwenyezi Mungu hana wa kumheshimu.

Kabisa! Hakuna wa kumuinua aliyeangushwa na kudhalilishwa na Mwenyezi Mungu, wala hakuna wa kumdhalilisha aliyetukuzwa na kuenziwa na Mwenyezi Mungu, na hakuna utukufu mbele ya Mwenyezi Mungu ila kwa wenye takua.

Hakika Mwenyezi Mungu hutenda apendayo kuwatukuza wema na kuwatweza wapotevu na wafisadi.

Baada ya hayo. Hakika Mwenyezi Mungu ana desturi katika viumbe vyake haiachi; nayo ni kuwa mwenye kufuata nji ya maangamizi ataangamia, na mwenye kufuata njia ya usalama atasalimika. Njia ya usalama mbele ya Mwenyezi Mungu ni imani ya kweli na matendo mema; na njia ya kufedheheka na kupuuzwa ni unafiki na ufisadi katika ardhi.

هَـٰذَانِ خَصْمَانِ اخْتَصَمُوا فِي رَبِّهِمْ فَالَّذِينَ كَفَرُوا قُطِّعَتْ لَهُمْ ثِيَابٌ مِّن نَّارٍ يُصَبُّ مِن فَوْقِ رُءُوسِهِمُ الْحَمِيمُ ﴿١٩﴾

19. Hawa mahasimu wawili waliohasimiana kwa ajili ya Mola wao. Basi waliokufuru watakatiwa nguo za moto na yatamiminwa juu ya vichwa vyao maji yanayochemka.

يُصْهَرُ بِهِ مَا فِي بُطُونِهِمْ وَالْجُلُودُ ﴿٢٠﴾

20. Kwayo vitayeyushwa vilivyo matumboni mwao na ngozi.

وَلَهُم مَّقَامِعُ مِنْ حَدِيدٍ ﴿٢١﴾

21. Na yatakuwako makomeo ya chuma kwa ajili yao.

كُلَّمَا أَرَادُوا أَن يَخْرُجُوا مِنْهَا مِنْ غَمٍّ أُعِيدُوا فِيهَا وَذُوقُوا عَذَابَ الْحَرِيقِ ﴿٢٢﴾

22. Kila wanapotaka kutoka humo kwa sababu ya uchungu watarudishwa humo humo; na onjeni adhabu ya kuungua.

إِنَّ اللَّـهَ يُدْخِلُ الَّذِينَ آمَنُوا وَعَمِلُوا الصَّالِحَاتِ جَنَّاتٍ تَجْرِي مِن تَحْتِهَا الْأَنْهَارُ يُحَلَّوْنَ فِيهَا مِنْ أَسَاوِرَ مِن ذَهَبٍ وَلُؤْلُؤًا وَلِبَاسُهُمْ فِيهَا حَرِيرٌ ﴿٢٣﴾

23. Hakika Mwenyezi Mungu atawaingiza walioamini na wakatenda mema katika bustani zipitiwazo na mito chini yake. Watapambwa humo kwa vikuku vya dhahabu na lulu na mavazi yao humo ni hariri.

وَهُدُوا إِلَى الطَّيِّبِ مِنَ الْقَوْلِ وَهُدُوا إِلَىٰ صِرَاطِ الْحَمِيدِ ﴿٢٤﴾

24. Na wataongozwa kwenye maneno mazuri na kuongozwa kwenye njia ya mwenye kuhimidiwa.

إِنَّ الَّذِينَ كَفَرُوا وَيَصُدُّونَ عَن سَبِيلِ اللَّـهِ وَالْمَسْجِدِ الْحَرَامِ الَّذِي جَعَلْنَاهُ لِلنَّاسِ سَوَاءً الْعَاكِفُ فِيهِ وَالْبَادِ وَمَن يُرِدْ فِيهِ بِإِلْحَادٍ بِظُلْمٍ نُّذِقْهُ مِنْ عَذَابٍ أَلِيمٍ ﴿٢٥﴾

25. Hakika wale waliokufuru na wakawazuilia njia ya Mwenyezi Mungu na Msikiti mtakatifu ambao tumeufanya kwa ajili ya watu wote sawa sawa, kwa wakaao humo na wageni. Na kila atakayefanya upotofu humo kwa dhulma tutamwonjesha adhabu chungu.

MAHASIMU WAWILI

Aya 19 – 25

MAANA

Hawa mahasimu wawili waliohasimiana kwa ajili ya Mola wao.

Kuna maelezo katika Tafsir At-Tabari kwamba Abu dharr alikuwa akiapa kwa Mwenyezi Mungu kwamba Aya hii imeshuka kwa ajili ya watu sita katika makuraishi; watatu miongoni mwao ni waumini nao ni Hamza bin Abdul-Muttalib, Ali bin Abu Twalib na Ubayda bin Al-Harith.

Na watatu ni katika washirikina nao ni: Utba na Shayba, watoto wa Rabia na Walid bin Utba. Uhasama baina yao ulikuwa katika vita vya Badr walipobariziana; na Mwenyezi Mungu akawapa nusra waumini kuwashinda washirikina.

Jamaa katika wafasiri wamesema kwamba makusudio ya waliohasimiana ni kikundi cha waumini na kikundi cha makafiri ambao ni mayahudi, wanaswara, wasabai, majusi na washirikina. Kwa sababu wote hao wametajwa katika Aya iliyotangulia na kila kundi linasema lina haki kuliko jingine.

Vyovyvote iwavyo ni kwamba uhasama katika dini unatokea baina ya wanaoamini.

Basi waliokufuru watakatiwa nguo za moto na yatamiminwa juu ya vichwa vyao maji yanayochemka. Kwayo vitayeyushwa vilivyo matumboni mwao na ngozi. Na yatakuwako makomeo ya chuma kwa ajili yao. Kila wanapotaka kutoka humo kwa sababu ya uchungu watarudishwa humo humo, na onjeni adhabu ya kuungua.

Baada ya Mwenyezi Mungu kuashiria uhasama wa waumini na makafiri anataja kwamba mwenye kumwamini Mwenyezi Mungu mwisho wake ni Peponi na mwenye kumkufuru mwisho wake ni Jahannam, mwisho mbaya kabisa.

Na kwamba watu wake watavaa kivazi cha moto na watamiminiwa maji ya moto ambayo yatayeyusha mafuta, nyama matumbo na ngozi. Pia nguzo za chuma zitakuwa vichwani mwao kuwazuia kutoka kila wanapojaribu kukimbia. Inawezekena kukimbia hukumu ya Mwenyezi Mungu na matakwa yake? Umepita mfano wake katika Juz. 13 (14: 49 – 50) kifungu cha ‘Jahannam na silaha za maangamizi’

Hakika Mwenyezi Mungu atawaingiza walioamini na wakatenda mema katika bustani zipitiwazo na mito chini yake. Watapambwa humo kwa vikuku vya dhahabu na lulu na mavazi yao humo ni hariri.

Makafiri watakuwa na mavazi ya moto, makomeo ya chuma, maji ya moto na waumini wenye ikhlasi watapata pepo yenye neema, mito yenye kinywaji cha ladha, nguo za hariri na vipambo vya dhahabu na lulu.

Na wataongozwa kwenye maneno mazuri.

Baada ya Mwenyezi Mungu kuashiria kwenye chakula na kinywaji chao, anataja kauli zao ambazo ni nzuri; mfano Alhamdulillah.Na kuongozwa kwenye njia ya mwenye kuhimidiwa. Hiyo ni njia yenye kunyooka waliyoifuata katika maisha ya dunia, ikawapeleka kwenye neema ya Akhera.

Hakika wale waliokufuru na wakawazuilia njia ya Mwenyezi Mungu na Msikiti mtakatifu ambao tumeufanya kwa ajili ya watu wote sawa- sawa, kwa wakaao humo na wageni.

Washirikina wa kikuraishi walikuwa wakiwazuilia watu kuiingia kwenye Uislamu, kuhiji na kufanya umra kwenye nyumba ya Mwenyezi Mungu ambayo ameifanya ni mahali pa kuendewa na watu na mahali pa amani. Umepita mfano wake katika Juz. 1 (2:125).

Na kila atakayefanya upotofu humo kwa dhulma tutamwonjesha adhabu chungu.

Yaani atakayeacha yale aliyoyaamrisha Mwenyezi Mungu na akamfanyia uovu anayeikusudia nyumba ya Mwenyezi Mungu tukufu, basi Mungu atamwadhibu adhabu kubwa.

وَإِذْ بَوَّأْنَا لِإِبْرَاهِيمَ مَكَانَ الْبَيْتِ أَن لَّا تُشْرِكْ بِي شَيْئًا وَطَهِّرْ بَيْتِيَ لِلطَّائِفِينَ وَالْقَائِمِينَ وَالرُّكَّعِ السُّجُودِ ﴿٢٦﴾

26. Na tulipomwekea Ibrahim mahala penye ile nyumba kwamba usinishirikishe na chochote na uitwaharishe nyumba yangu kwa ajili ya wanozunguka na wakaazi na wanaorukui na wanaosujudi.

وَأَذِّن فِي النَّاسِ بِالْحَجِّ يَأْتُوكَ رِجَالًا وَعَلَىٰ كُلِّ ضَامِرٍ يَأْتِينَ مِن كُلِّ فَجٍّ عَمِيقٍ ﴿٢٧﴾

27. Na watangazie watu Hijja; watakujia kwa miguu na juu ya kila mnyama aliyekonda kutoka kila njia ya mbali.

لِّيَشْهَدُوا مَنَافِعَ لَهُمْ وَيَذْكُرُوا اسْمَ اللَّـهِ فِي أَيَّامٍ مَّعْلُومَاتٍ عَلَىٰ مَا رَزَقَهُم مِّن بَهِيمَةِ الْأَنْعَامِ فَكُلُوا مِنْهَا وَأَطْعِمُوا الْبَائِسَ الْفَقِيرَ ﴿٢٨﴾

28. Ili washuhudie manufaa yao na walitaje jina la Mwenyezi Mungu katika siku maalum juu ya wanyama hawa aliowaruzuku.

ثُمَّ لْيَقْضُوا تَفَثَهُمْ وَلْيُوفُوا نُذُورَهُمْ وَلْيَطَّوَّفُوا بِالْبَيْتِ الْعَتِيقِ ﴿٢٩﴾

29. Basi kuleni katika hao na mumlishe mwenye shida aliye fukara, kisha wajisafishe taka zao na watimize nadhiri zao na waizunguke sana nyumba ya kale.

ITWAHARISHE NYUMBA YANGU

Aya 26 -29

MAANA

Na tulipomwekea Ibrahim mahala penye ile nyumba kwamba usin- ishirikishe na chochote na uitwaharishe nyumba yangu kwa ajili ya wanozunguka na wakaazi na wanaorukui na wanaosujudi.

Makusudio ya wakaazi ni wakaazi wa Makka na viunga vyake; na wanorukui wakisujudi ni wanaoswali.

Makuraishi walikuwa wakiabudu masanamu na wakisimamia Al-Kaaba. Baada ya Mwenyezi Mungu kumtuma Muhammad(s.a.w.w) walianza kuwa na uadui naye na kila anayemwamini, tena wakawazuilia waislamu kuizunguka (tawaf) na kuswali hapo; kama ilivyoelezwa kwenye Aya iliyotangulia. Pamoja na hayo Makuraishi walikuwa wakidai kwamba wako kwenye dini ya Ibrahim(a.s) .

Ndio Mwenyezi Mungu akabatilisha madai yao haya, kwamba yeye ndiye mwenye nyumba hiyo na alimpa wahyi kuwa aijenge na aifanye ni mahsusi kwa ibada ya wanaompwekesha Mungu wanaokaa hapo na wanaopita na pia kuwaweka mbali nayo washirikina na mizimu yao.

Haya ndio maana ya kauli yake Mwenyezi Mungu ‘Na uitwaharishe nyumba yangu’ lakini makuraishi waliipindua Aya, wakaijaza masanamu nyumba ya Mwenyezi Mungu, wakaihalalishia washirikina na wafisadi na wakawazulia nayo watu wa tawhid na wema.

Na watangazie watu Hijja; watakujia kwa miguu na juu ya kila mnyama aliyekonda kutoka kila njia ya mbali.

Mwenyezi Mungu alimwamrisha kipenzi chake awaite watu kuhiji kwenye msikiti mtakatifu baada ya kusimamisha misingi yake na kutimia jengo. Akamwahidi kuwa watu watamwitikia na watamjia kwa kila hali; kutembea kwa miguu na kupanda ngamia au farasi waliokonda tena kutoka mbali, sikwambii karibu.

Ili washuhudie manufaa yao.

Hijja ni ibada pekee inayochanganya manufaa ya kidini na ya kidunia. Ama ya kidini ni kumtii Mwenyezi Mungu kwa kutekeleza faradhi ya Hijja, kutubia na kutambua haiba ya Mwenyezi Mungu na utukufu. Ibn Al- Arabi anasema katika Kitabu Futuhatul- Makkiyya:

“Siku moja nilikuwa nikitufu Al-Kaaba nikaiona kama kwamba imenyanyuka kutoka ardhini, wallah, ikaniambia maneno niliyoyasikia: njoo uone nitakavyokufanyia, mara ngapi hadhi yangu unaiweka chini na ya binadamu unaiinua juu?.

Nasi tunasema kwa uhakika: hakuna yeyote anayefanya sa’yi au tawaf katika nyumba ya Mwenyezi Mungu kwa ikhlas ila atahisi aina ya kitu kama hiki.

Na walitaje jina la Mwenyezi Mungu katika siku maalum juu ya wanyama howa aliowaruzuku, ambao ni ngamia ng’ombe na mbuzi na kondoo.

Kumtaja Mwenyezi Mungu kwenye wanyama ni kinaya cha kuchinja, kwa sababu kusoma Bismillah ni wajibu katika kuchinja. Makusudio ya siku maalum ni siku za kuchinja katika Hijja, kama inavyofahamisha Aya.

Mafakihi wametofautiana katika idadi ya siku hizo: Shia wamesema ni nne, mwanzo wake ni siku ya Idul-adh’ha na mwisho wake ni tarehe kumi na tatu ya Dhul-hijja. Mafakihi wa madhehbu mengine wamesema ni tatu kwa kuishia tarehe kumi na mbili. Ufafanuzi uko katika kitabu chetu Alfiqh ala madhahibil-khamsa [5] .

Razi anasema kuwa maulama wengi wanatofautisha baina ya siku maalum na siku za kuhisabiwa zilizotajwa katika Juz. 2 (2:203) na wanaona kuwa siku maalum ni siku kumi za mwezi wa Dhul-hijja na za kuhisabiwa ni siku za kuchinja.

Basi kuleni katika hao na mumlishe mwenye shida aliye fukara.

Wameafikiana mafakihi kuhusu wajibu wa kumlisha fukara mnyama wa Hijja na wakatofautina katika wajibu wa mwenyewe kula. Sisi tuko pamoja na wale wanaosema kuwa si wajibu kwa mwenyewe kula. Ni vile atavyoona, akipenda atakula na akipenda ataitoa sadaka yote. Ama kauli yake Mwenyezi Mungu:‘Kuleni katika hao’ ni kwa ajili ya kuondoa fikra ya uharamu wa kula; ambapo wakati wa jahiliya walikuwa hawali wanyama hao wawachinjao wakidai kuwa ni haramu kwao. Ndipo Mwenyezi Mungu akawazindua kosa lao hilo.

Kisha wajisafishe taka zao.

Haijuzu kwa aliye kwenye Hijja akiwa kwenye ihram (Vazi maalum la Hijja) kunyoa, kukata kucha au kujipaka manukato; bali mafakihi au wengi wao wamesema kuwa hata kuua vidudu vya mwilini, kama vile chawa pia ni haramu. Zikiisha zile siku za Ihram basi inakuwa ni halali kwake yale yaliyokuwa ni haramu, basi hapo atanyoa, kukata kucha n.k. Ndipo kwa hili ameshiria Mwenyezi Mungu aliposema:

Kisha wajisafishe taka zao.

Na watimize nadhiri zao, ikiwa wameweka nadhiri siku za Hijja au kabla. Kwa sababu watu wengi huweka nadhiri ya kutoa sadaka ikiwa Mwenyezi Mungu atawaruzuku Hijja.

Na waizunguke sana nyumba ya kale. Kwa sababu ndio nyumba ya kwanza kuwekewa watu kwa ajili ya ibada.

Mwenyezi Mungu ameleta tamko la ‘sana’ kwa sababu ni Sunna kufanya tawaf mara nyingi; kama ambavyo pia ni Sunna kuswali sana. Kuna Hadithi mashuhuri kutoka kwa Mtume wa rehema, aliposema: “Kuizunguka Al-Kaaba ni Swala.’

5

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA SABA

وَدَاوُودَ وَسُلَيْمَانَ إِذْ يَحْكُمَانِ فِي الْحَرْثِ إِذْ نَفَشَتْ فِيهِ غَنَمُ الْقَوْمِ وَكُنَّا لِحُكْمِهِمْ شَاهِدِينَ ﴿٧٨﴾

78. Na Daud na Suleiman walipohukumu juu ya shamba, walipolisha humo mbuzi wa watu usiku. Na sisi tulikuwa wenye kushuhudia hukumu yao.

فَفَهَّمْنَاهَا سُلَيْمَانَ وَكُلًّا آتَيْنَا حُكْمًا وَعِلْمًا وَسَخَّرْنَا مَعَ دَاوُودَ الْجِبَالَ يُسَبِّحْنَ وَالطَّيْرَ وَكُنَّا فَاعِلِينَ ﴿٧٩﴾

79. Tukamfahamisha Suleiman na kila mmoja wao tukampa hukumu na elimu. Na tuliifanya milima na ndege kuwa pamoja na Daud imnyenyekee na imsabihi (Mwenyezi Mungu). Na sisi tulikuwa ni wenye kuifanya.

وَعَلَّمْنَاهُ صَنْعَةَ لَبُوسٍ لَّكُمْ لِتُحْصِنَكُم مِّن بَأْسِكُمْ فَهَلْ أَنتُمْ شَاكِرُونَ ﴿٨٠﴾

80. Na tukamfundisha kutengeneza mavazi ya vita ili kuwakinga katika mapigano yenu. Je, mtakuwa wenye kushukuru?

وَلِسُلَيْمَانَ الرِّيحَ عَاصِفَةً تَجْرِي بِأَمْرِهِ إِلَى الْأَرْضِ الَّتِي بَارَكْنَا فِيهَا وَكُنَّا بِكُلِّ شَيْءٍ عَالِمِينَ ﴿٨١﴾

81. Na upepo mkali kwa ajili ya Suleiman, wendao kwa amri yake, katika ardhi tuliyoibariki. Na sisi ndio tunaojua kila kitu.

وَمِنَ الشَّيَاطِينِ مَن يَغُوصُونَ لَهُ وَيَعْمَلُونَ عَمَلًا دُونَ ذَٰلِكَ وَكُنَّا لَهُمْ حَافِظِينَ ﴿٨٢﴾

82. Na katika mashetani kuna wanompigia mbizi na kufanya kazi nyinginezo; Nasi tulikuwa walinzi wao.

DAUD NA SULEIMAN

Aya 78 – 82

MAANA

Na Daud na Suleiman walipohukumu juu ya shamba, walipolisha humo mbuzi wa watu usiku. Na sisi tulikuwa wenye kushuhudia hukumu yao.

Kuna riwaya iliyo mashuhuri midomoni mwa wapokezi, kwamba watu wawili walikwenda kuamuliwa kwa Daud. Mmoja alikuwa na mimea na wa pili alikuwa na mifugo ya mbuzi na kondoo. Mwenye shamba akasema wanyama wa huyu bwana wamelisha kwenye mimea yangu usiku. Baada ya kumthibitikia hilo, Daud alitoa hukumu kuwa wanyama wawe wa mwenye shamba.

Suleiman alipojua hivyo akasema, ni vizuri mwenye shamba awachukue wanyama, anufaike nao lakini wasiwe wake kabisa, na mwenye wanyama achukue ardhi aishghulikie mpaka iwe kama ilivyokuwa kabla ya kuliwa. Kisha bada ya hapo kila mmoja achukue mali yake. Daud akapendezewa na hukumu ya mwanawe na akaitumia.

Dhahiri ya Aya inaafikiana na riwaya hii. Imethibiti kutoka kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) kwamba yeye amesema: “Linaloafikiana na Qur’an lichukueni na linalokhalifiana nalo liacheni.”

Unaweza kuuliza : Kila mmoja kati ya Daud na Suleiman ni Nabii na Nabii ni maasumu; hasa katika hukumu ya sharia na hukumu ya sawa, sasa je kuna wajihi gani wa kupingana hukumu mbili hizi?

Baadhi wamejibu kuwa kauli ya Daud ilikuwa ni upatanishi sio hukumu. Lakini ijulikane kuwa upatanishi unakuwa kwa baadhi ya mali sio yote na Daud hakumbakishia mfugaji hata mnyama mmoja.

Wengine wakasema kuwa kila mmoja kati ya manabii wawili hao alihukumu kwa ijitihadi yake. Kauli hii vile vile ina kasoro; kwamba Nabii anatumia ijitihadi kama ulama wengine na inajulikana kuwa rai ya ijtihadi inakuwa kwa kukosekana nukuu (Nass) na ilivyo ni kuwa kauli ya Nabii ni nukuu ya haki; na kwamba ijitihadi ina uwezekano wa kupatia na kukosea, jambo ambalo haliswihi kwa maasumu.

Jamaa wamesema kuwa hukumu ilikuwa kama alivyopitisha Daud; kisha ikabadilishwa (naskh), na kauli ya Suleiman[2]

Kauli hii ina nguvu zaidi kwa dalili ya kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu:

Tukamfahamisha Suleiman na kila mmoja wao tukampa hukumu na elimu.

Hapo Mwenyezi Mungu anashudia kuwa kila mmoja ni mjuzi wa hukumu. Kwa hiyo basi kauli yake Mwenyezi Mungu ‘Tukamfahamisha Suleiman’ ni kwamba yeye alimpelekea wahyi wa kubadilisha hukumu ya baba yake. Mafaqihi wametofautiana kuwa je mwenye mifugo atalipa kilichoharibiwa na wanyama wake?

Maliki na Shafi wamesema kuwa atalipa kilichoharibiwa usiku sio mchana. Abu Hanifa akasema halipi kwa hali yoyote; iwe usiku au mchana.

Jamaa katika mafaqihi wa kishia wamesema kama alivyosema Maliki na Shafi na wahakiki katika wao wakasema kuwa litakaloangaliwa ni hali ya uzembe wa mfugaji au la; sio hali ya kuwa usiku au mchana. Ikiwa mfugaji atazembea au kufanya makusudi, basi atalipa. Na ikiwa atajichunga na asipuuze, ikatokea bahati mbaya basi hatalipa.

Na tuliifanya milima na ndege kuwa pamoja na Daud imnyenyekee na imsabihi (Mwenyezi Mungu). Na sisi tulikuwa ni wenye kuifanya.

Imekuwa mashuhuri kuwa Daud alikuwa na sauti nyororo. Majaribio yamethibitisha kuwa wanyama wengi wanaburudika na aina fulani ya nyimbo na muziki [3] 2. Niliwahi kusoma kwenye gazeti kwamba nyoka aliwahi kutoka kwenye tundu yake ili astarehe na nyimbo za Ummu Kulthum, katika moja ya hafla yake. Nyimbo ilipokwisha akarudi sehemu yake.

Ama tasbibih ya mlima ni kwa njia ya majazi na kusifia zaidi tu; kama kusema: Amelichekesha na kuliliza jiwe. Au inawezekana ni kiuhakika hasa. Kwa sababu yule aliyeweza kuufanya moto kuwa baridi na salama kwa Ibrahim, ndiye anaweza pia kulifanya jabali litoe tasbih pamoja na Daud.

Angalia Aya 69 ya Sura hii tuliyo nayo.

Na tukamfundisha kutengeneza mavazi ya vita ili kuwakinga katika mapigano yenu. Je, mtakuwa wenye kushukuru?

Makusudio ya mavazi ya vita hapa ni deraya. Aya inaonyesha kuwa Daud ndiye mtu wa kwanza kutengeneza deraya.

Kuna riwaya inayoelezea kwamba sababu ya hilo ni kuwa Daud alikuwa ni mfalme wa Israil na alikuwa ana desturi ya kupita mitaani kujulia hali za watu, bila ya yeye kujulikana. Siku moja akakutana na mtu akamuuliza kuhusu sera za mfalme Daud.

Yule mtu akasema: Ana sera nzuri sana, kama asingekuwa anakula kwenye hazina ya serikali. Daud akaapa kuwa kuanzia siku hiyo hatakula kitu isipokuwa kilichotokana na mikono yake na jasho lake.

Alipojua Mwenyezi Mungu ikhlasi yake na ukweli wa nia yake, alimalainishia chuma na kumfundisha kutengeneza deraya.

Iwe sahihi riwaya hii au la, ni kwamba inaashria wajibu wa kufanya bidii kubwa kuchunga masilahi ya watu na mali zao. Kuna Hadith mutawatir kwamba Mtume wa Mwenyezi Mungu, Muhammad(s.a.w.w) , alifariki akiwa ameweka rahani deraya yake kwa sababu ya kukopa kiasi fulani cha shayir, huku zikiwa mali za Bara arabu zote ziko mikononi mwake.

Na upepo mkali kwa ajili ya Suleiman, wendao kwa amri yake, kati- ka ardhi tuliyoibariki. Na sisi ndio tunaojua kila kitu.

Dhahiri ya Aya hii inafahamisha kuwa upepo ulikuwa ukimchukua Suleiman kwa amri ya Mwenyezi Mungu. Wala hakuna haja ya kuleta taawili, maadamu akili inakubaliana na dhahiri hiyo.

Aya iliyo wazi zaidi ya hii ni ile isemayo: “Na Suleiman tukamtiishia upepo mwendo wake asubuhi ni mwezi mmoja na mwendo wake jioni yake ni mwezi mmoja.” (34:12) Yaani asubuhi unakwenda mwendo wa mwezi mmoja kwa kusafiri na ngamia na jioni vile vile.

Makusudio ya ardhi iliyobarikiwa ni ile iliyotajwa kwenye Aya ya 71 ya Sura hii.

Unaweza kuuliza : Hapa Mwenyezi Mungu (s.w.t.) amesema upepo mkali na mahali pengine anasema: pole pole: “Na tukamtiishia upepo uendao polepole kwa amri yake.” (38:36). Je, kuna wajihi gani wa Aya zote mbili?

Jibu : Huwa mara unakwenda kwa kasi na mara nyingine polepole kulin- gana na amri yake; sawa na gari au ndege.

Na katika mashetani kuna wanompigia mbizi baharini na kumtolea lulu na marijani.

Makusudio ya mashetani hapa ni majini

Na kufanya kazi nyinginezo ; kama kujenga mihirabu na picha:

يَعْمَلُونَ لَهُ مَا يَشَاءُ مِن مَّحَارِيبَ وَتَمَاثِيلَ وَجِفَانٍ كَالْجَوَابِ وَقُدُورٍ رَّاسِيَاتٍ ﴿١٣﴾

“Wakimfanyia alipendalo, kama mihrabu na picha na masinia makubwa, kama hodhi na masufuria makubwa yasiyoondolewa mahali pake.” (34:13).

Nasi tulikuwa walinzi wao, kwamba wasitoroke na kufanya ukorofi. Hatuna la kuongeza zaidi ya ulivyothibisha wahyi kuwepo majini na kwamba wao walimtumikia Suleiman na akili hailikatai hilo. Kwa hiyo basi hakuna haja yoyote ya kuleta taawili na kuyazungusha maneno. Imam Ali(a.s) amesema:“Lau kama mtu angeliweza la kumfanya adumu ulimwenguni au kuhepa mauti, basi angelikuwa Suleiman ambaye alitiishiwa ufalme, majini watu, utume na heshima kuu.”

وَأَيُّوبَ إِذْ نَادَىٰ رَبَّهُ أَنِّي مَسَّنِيَ الضُّرُّ وَأَنتَ أَرْحَمُ الرَّاحِمِينَ ﴿٨٣﴾

83. Na Ayyub aliopomlingania Mola wake: Hakika mimi imenigusa dhara, nawe ndiye unayerehemu zaidi kuliko wanaorehemu.

فَاسْتَجَبْنَا لَهُ فَكَشَفْنَا مَا بِهِ مِن ضُرٍّ وَآتَيْنَاهُ أَهْلَهُ وَمِثْلَهُم مَّعَهُمْ رَحْمَةً مِّنْ عِندِنَا وَذِكْرَىٰ لِلْعَابِدِينَ ﴿٨٤﴾

84. Basi tukamkubalia na tukamuondolea dhara na tukampa watu wake na mfano wao pamoja nao kuwa ni rehema itokayo kwetu na ukumbusho kwa wafanyao ibada.

وَإِسْمَاعِيلَ وَإِدْرِيسَ وَذَا الْكِفْلِ كُلٌّ مِّنَ الصَّابِرِينَ ﴿٨٥﴾

85. Na Isamil na Idris na Dhulkifl, wote walikuwa miongoni mwa wanaosubiri.

وَأَدْخَلْنَاهُمْ فِي رَحْمَتِنَا إِنَّهُم مِّنَ الصَّالِحِينَ ﴿٨٦﴾

86. Na tukawaingiza katika rehema yetu. Hakika wao ni katika watu wema.

وَذَا النُّونِ إِذ ذَّهَبَ مُغَاضِبًا فَظَنَّ أَن لَّن نَّقْدِرَ عَلَيْهِ فَنَادَىٰ فِي الظُّلُمَاتِ أَن لَّا إِلَـٰهَ إِلَّا أَنتَ سُبْحَانَكَ إِنِّي كُنتُ مِنَ الظَّالِمِينَ ﴿٨٧﴾

87. Na Dhun-Nun alipoondoka hali ameghadhabika na akadhani kuwa hatutamdhikisha. Basi aliita katika giza kwamba: Hapana Mola isipokuwa wewe, umetakasika. Hakika mimi nilikuwa miongoni mwa madhalimu.

فَاسْتَجَبْنَا لَهُ وَنَجَّيْنَاهُ مِنَ الْغَمِّ وَكَذَٰلِكَ نُنجِي الْمُؤْمِنِينَ ﴿٨٨﴾

88. Basi tukamkubalia na tukamwokoa kutokana na ghamu. Kama hivyo tunawaokoa wenye kuamini.

وَزَكَرِيَّا إِذْ نَادَىٰ رَبَّهُ رَبِّ لَا تَذَرْنِي فَرْدًا وَأَنتَ خَيْرُ الْوَارِثِينَ ﴿٨٩﴾

89. Na Zakaria alipomwita Mola wake: Ewe Mola wangu! Usiniwache peke yangu na wewe ndiye mbora wa wanaorithi.

فَاسْتَجَبْنَا لَهُ وَوَهَبْنَا لَهُ يَحْيَىٰ وَأَصْلَحْنَا لَهُ زَوْجَهُ إِنَّهُمْ كَانُوا يُسَارِعُونَ فِي الْخَيْرَاتِ وَيَدْعُونَنَا رَغَبًا وَرَهَبًا وَكَانُوا لَنَا خَاشِعِينَ ﴿٩٠﴾

90. Basi tukamwitikia na tukampa Yahya na tukamponyeshea mkewe. Hakika wao walikuwa wepesi kufanya kheri na wakituomba kwa hofu na walikuwa wakitunyenyekea.

وَالَّتِي أَحْصَنَتْ فَرْجَهَا فَنَفَخْنَا فِيهَا مِن رُّوحِنَا وَجَعَلْنَاهَا وَابْنَهَا آيَةً لِّلْعَالَمِينَ ﴿٩١﴾

91. Na mwanamke aliyelinda tupu yake na tukampulizia katika roho yetu na tukamfanya yeye na mwanawe kuwa ni ishara kwa walimwengu.

NA AYYUB ALIOPOMLINGANIA MOLA WAKE

Aya 83 – 91

MAANA

Na Ayyub aliopomlingania Mola wake: Hakika mimi imenigusa dhara, nawe ndiye unayerehemu zaidi kuliko wanaorehemu. Basi tukamkubalia na tukamuondolea dhara.

Makusudio ya dhara ni madhara ya nafsi, kama vile maradhi, kutokana na neno la kiarabu dhurr.

Likisomwa dharr ndio linakuwa na maana ya madhara ya kila kitu. Wafasiri na wapokezi wengi wamepokea riwaya nyingi zinazomuhusu Ayyub. Tunalolifahamu sisi, kutokana na Aya zinazomzungumzia kwa uwazi na kwa ishara hapa na pia katika Sura Swad (38), ni kwamba Ayyub alikuwa na afya yake nzuri akiwa hana matatizo yoyote. Kisha mabalaa yakaanza kumwandama kila upande, akawa ni wa kupigiwa mifano.

Masaibu yalimpata yeye mwenyewe binafsi; akavumilia uvumilivu wa kiungwana; na akabakia na yakini yake na kumtegemea kwake Mwenyezi Mungu. Huzuni wala machungu hayakumfanya aache kumtii Mwenyezi Mungu. Lakini muda ulivyomzidi na machungu nayo yakazidi, alimshtakia

Mwenyezi Mungu mambo yake kwa maneno mawili tu: “Imenigusa dhara, nawe ndiye unayerehemu zaidi kuliko wanaorehemu,” na wala hakulalamika kwa kusema balaa gani hii iliyoniandama.

Ndipo Mwenyezi Mungu akamwitikia maombi yake na akamuondolea mabalaa na kumrudisha katika hali nzuri zaidi ya alivyokuwa.

Na tukampa watu wake na mfano wao pamoja nao kuwa ni rehema itokayo kwetu na ukumbusho kwa wafanyao ibada.

Mwenyezi Mungu alimruzuku watoto na wajukuu zaidi ya wale aliowakosa, ikiwa ni rehema na malipo ya uvumilivu wake; na pia kukumbusha kwamba mwenye kuwa na subra na uvumilivu kama wa Ayyub, basi mwisho wake utakuwa kama wa Ayyub. Mwenyezi Mungu amehusisha kuwataja wenye kuabudu kwa kuashiria kuwa Mwenyezi Mungu yuko pamoja na mwenye subra aliye na ikhlasi kwa kauli yake na vitendo vyake.

Huu ndio ujumla wa maelezo ya Aya zinazofungamana na Ayyub; bila ya kuingilia ufafanuzi walioutaja wapokezi na wasimulizi. Kwani huo hauam- batani na itikadi wala uhai kwa mbali wala karibu. Miongoni mwa njia za Qur’an ni kukitaja kisa kwa yale yaliyo na mazingatio yenye kunufaisha na mawaidha ya kukanya.

Na Isamil Na Idris Na Dhulkifl, wote walikuwa miongoni mwa wanao- subiri. Na tukawaingiza katika rehema yetu. Hakika wao ni katika watu wema.

Ismail alifanya subra ya kukubali kuchinjwa na akawa na uvumilivu wa kukaa katika nchi isiyokuwa na mimea wala kinywewa. Idris tumemueleza katika Juz. 16 (19:56).

Ama Dhulkifl wengi wamesema alikuwa Mtume; na baadhi wakasema alikuwa ni mja mwema tu na sio Mtume. Sisi tunaamini kwamba yeye ni miongoni mwa waliokuwa na subira na waja wema, kwa kufuata Qur’an ilivyosema, na wala hatutaulizwa zaidi ya hayo.

Na Dhun-Nun alipoondoka hali ameghadhabika na akadhani kuwa hatutamdhikisha. Basi aliita katika giza kwamba: Hapana Mola isipokuwa wewe, umetakasika. Hakika mimi nilikuwa miongoni mwa madhalimu.

Dhun-Nun ni Yunus. Maana ya neno ‘Nun” ni samaki. Mwenyezi Mungu anasema:

فَاصْبِرْ لِحُكْمِ رَبِّكَ وَلَا تَكُن كَصَاحِبِ الْحُوتِ ﴿٤٨﴾

“Na vumilia hukumu ya Mola wako wala usiwe kama sahibu wa samaki” (68:48).

Hali ameghadhibika ni kuwaghadhibikia watu wake. Neno kudhikishwa limefasiriwa kutokana na neno Naqdira alyh; kama lilivyotumika mahali pengine:

وَمَن قُدِرَ عَلَيْهِ رِزْقُهُ ﴿٧﴾

“Na yule ambaye imekuwa dhiki riziki yake” (65:7).

Makusudio ya katika giza hapa ni ndani ya tumbo la samaki.

Maana kwa ujumla ni: kumbuka ewe Muhammad habari ya Yunus alipowalingania watu wake, lakini hawakumwitikia mwito wake, akawaondokea kwa kuwakasirikia, akadhani kuwa hatutamdhikisha kwa kumzuia n.k. Alipomezwa na samaki akataka uokovu kutoka kwetu,basi tukamkubalia na tukamwokoa kutokana na ghamu. Kama hivyo tunawaokoa wenye kuamini.

Makusudio ya ghamu hapa ni tumbo la samaki; na kuokoka, ni kutolewa humo hadi kwenye nchi kavu. Umetangulia mfano wake katika Juz. 11 (10:98).

Na Zakaria alipomwita Mola wake: Ewe Mola wangu! Usiniwache peke yangu na wewe ndiye mbora wa wanaorithi. Basi tukamwitikia na tukampa Yahya na tukamponyeshea mkewe.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 3 ( 3: 38) na Juz. 16 (19:7).

Hakika wao walikuwa wepesi kufanya kheri na wakituomba kwa hofu na walikuwa wakitunyenyekea.

Wao ni Zakariya, mkewe na Yahya au wale Mitume waliotangulia kutajwa. Wote walifanya kheri kwa kutaka thawabu za Mwenyezi Mungu na kuhofia adhabu yake na walikuwa wakimfuata Mwenyezi Mungu katika kila jambo.

Na mwanamke aliyelinda tupu yake na tukampulizia katika roho yetu na tukamfanya yeye na mwanawe kuwa ni ishara kwa walimwengu.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 3 (3: 45) na Juz. 16 (19: 16).

6

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA SABA

إِنَّ هَـٰذِهِ أُمَّتُكُمْ أُمَّةً وَاحِدَةً وَأَنَا رَبُّكُمْ فَاعْبُدُونِ ﴿٩٢﴾

92. Hakika umma wenu huu ni umma mmoja, na mimi ni Mola wenu kwa hivyo niabuduni.

وَتَقَطَّعُوا أَمْرَهُم بَيْنَهُمْ كُلٌّ إِلَيْنَا رَاجِعُونَ ﴿٩٣﴾

Na wakalivunja jambo lao baina yao. Wote watarejea kwetu.

فَمَن يَعْمَلْ مِنَ الصَّالِحَاتِ وَهُوَ مُؤْمِنٌ فَلَا كُفْرَانَ لِسَعْيِهِ وَإِنَّا لَهُ كَاتِبُونَ ﴿٩٤﴾

94. Na atendaye mema naye ni mumin, basi haitakataliwa bidii yake na hakika sisi tutamwandikia.

وَحَرَامٌ عَلَىٰ قَرْيَةٍ أَهْلَكْنَاهَا أَنَّهُمْ لَا يَرْجِعُونَ ﴿٩٥﴾

95. Na ni haramu kwa mji tuliouangamiza kwamba wao hawatarejea.

حَتَّىٰ إِذَا فُتِحَتْ يَأْجُوجُ وَمَأْجُوجُ وَهُم مِّن كُلِّ حَدَبٍ يَنسِلُونَ ﴿٩٦﴾

96. Mpaka watakapofunguliwa Juju na Majuju, wakawa wanateremka kutoka kila mlima.

وَاقْتَرَبَ الْوَعْدُ الْحَقُّ فَإِذَا هِيَ شَاخِصَةٌ أَبْصَارُ الَّذِينَ كَفَرُوا يَا وَيْلَنَا قَدْ كُنَّا فِي غَفْلَةٍ مِّنْ هَـٰذَا بَلْ كُنَّا ظَالِمِينَ ﴿٩٧﴾

97. Na miadi ya haki itakaribia, ndipo yatakapokodoka macho ya wale waliokufuru. Ole wetu! Hakika tulikuwa tumeghafilika na haya, bali tulikuwa ni wenye kudhulumu.

إِنَّكُمْ وَمَا تَعْبُدُونَ مِن دُونِ اللَّـهِ حَصَبُ جَهَنَّمَ أَنتُمْ لَهَا وَارِدُونَ ﴿٩٨﴾

98. Hakika nyinyi na hayo mnayoyaabudu badala ya Mwenyezi Mungu ni kuni za Jahannam, mtaifikia.

لَوْ كَانَ هَـٰؤُلَاءِ آلِهَةً مَّا وَرَدُوهَا وَكُلٌّ فِيهَا خَالِدُونَ ﴿٩٩﴾

99. Lau haya yangelikuwa ni miungu yasingeliingia na wote watadumu humo.

لَهُمْ فِيهَا زَفِيرٌ وَهُمْ فِيهَا لَا يَسْمَعُونَ ﴿١٠٠﴾

100. Lao humo ni kupiga mayowe na wala hawatasikika.

UMMA MMOJA

Aya 92 – 100:

MAANA

Hakika umma wenu huu ni umma mmoja, na mimi ni Mola wenu kwa hiyo niabuduni.

LUGHA

Maana ya neno umma ni watu wenye lugha moja na historia moja. Kisha neno hili likawa linatumika zaidi kwa maana ya dini na mila. Maana haya ndiyo yaliyokusudiwa hapa.

Umma wenu huu ni itikadi ya mitume ambayo ni tawhid pamoja na kufuata amri za Mwenyezi Mungu kwa kauli na vitendo. Msemo ‘wenu’ unaelekezwa kwa watu wote.

Maana ni kuwa enyi watu wote! Shikeni dini ya Tawhidi waliyokuwa nayo Mitume na mumwabudu Mungu mmoja aliye peke na mumfanyie ikhlasi katika kauli na vitendo.

Na wakalivunja jambo lao baina yao.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) aliwaamrisha wote wawe kwenye itikadi ya tawhidi, lakini wakagawanyika wakawa makundi ya wakana Mungu na washirikina. Hata wale wafuasi wa Mitume nao wanatukanana na kujitenga na wengine; bali hata wafuasi wa Mtume mmoja nao ni hivyo hivyo.

Wote watarejea kwetu.

Haya ni makemeo na hadhari kwa wale wanaofarikiana wakawa vikundi.

Na atendaye mema naye ni mumin, basi haitakataliwa bidii yake na hakika sisi tutamwandikia.

Imani pamoja na matendo mema ni njia ya Peponi na imani bila ya matendo haifai chochote. Hiyo ni kutokana na kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu:

لَا يَنفَعُ نَفْسًا إِيمَانُهَا لَمْ تَكُنْ آمَنَتْ مِن قَبْلُ أَوْ كَسَبَتْ فِي إِيمَانِهَا خَيْرًا ﴿١٥٨﴾

“Basi mtu haitamfaa imani yake ambaye hakuamini zamani, au hakuchuma kheri kwa imani yake.” Juz. 8 (6:158).

Ama matendo mema bila ya imani, humnufaisha mtendaji kwa namna moja au nyingine na huenda ikamfaa huko Akhera kwa kupunguziwa adhabu. Tumeyafafanua hayo katika Juz. 4 (3:158) kwenye kifungu ‘kafiri na amali njema’ Pia Umepita mfano wake katika Juz. 14 (16: 97)

Na ni haramu kwa mji tuliouangamiza kwamba wao hawatarejea.

Aya hii ni jawabu la swali la kukadiria, kwamba je, washirikina katika watu wa kijiji kilichoangamizwa na Mwenyezi Mungu kwa kufuru yao, watarudishwa tena kuwa hai na kuadhibiwa huko Akhera, kama walivyoadhibiwa duniani?

Ndio akajibu Mwenyezi Mungu (s.w.t) kuwa watu wote, kesho watarejea kwa Mwenyezi Mungu; hata wale walioangamizwa duniani kwa dhambi zao na ni muhali kukosa kurejea kwa Mwenyezi Mungu baada ya mauti; bali hakuna budi lazima watafufuliwa.

Swali la pili : je inafaa kuadhibiwa akhera baada ya kuadhibiwa duniani? Huko si ni kuadhibu mara mbili kwa kosa moja?

Jibu : Hapana! Kuadhibiwa kwao duniani kulikuwa ni kwa ajili ya kuwakadhibisha kwao Mitume waliowajia na miujuza; kama zinavyofahamisha Aya hizi zifuatazo na nyinginginezo mfano wake:

وَقَوْمَ نُوحٍ لَّمَّا كَذَّبُوا الرُّسُلَ أَغْرَقْنَاهُمْ ﴿٣٧﴾

“Na kaumu ya Nuh walipowakadhibisha Mitume tuliwagharikisha” (25:37)

كَذَّبَتْ قَبْلَهُمْ قَوْمُ نُوحٍ وَأَصْحَابُ الرَّسِّ وَثَمُودُ ﴿١٢﴾ وَعَادٌ وَفِرْعَوْنُ وَإِخْوَانُ لُوطٍ ﴿١٣﴾ وَأَصْحَابُ الْأَيْكَةِ وَقَوْمُ تُبَّعٍ كُلٌّ كَذَّبَ الرُّسُلَ فَحَقَّ وَعِيدِ ﴿١٤﴾

“Kabla yao walikadhibisha kamu ya Nuh na watu wa Rassi na Thamud na A’d na Firauni na ndugu wa Lut na watu wa vichakani na kaumu ya Tubbai, wote waliwakadhibisha Mitume, kwa hiyo kiaga kikathibitika juu yao.” (50: 12-14).

Ama adhabu ya Akhera ni ya ukafiri wenyewe na madhambi mengineyo; kama dhulma n.k.

Kwa hiyo adhabu zinakuwa nyingi kutokana na dhambi kuwa aina nyingi, sio kwa dhambi moja.

Mpaka watakapofunguliwa Juju na Majuju, wakawa wanateremka kutoka kila mlima.

Katika Juz. 16 (18: 94) tuliwanukuu baadhi ya wafasiri wakisema kuwa Juju ni wa Tatars na Majuju ni Wamongoli. Vile vile tumesema huko kuwa ukuta wa Juju na Majuju hauko tena. Kwa hiyo basi makusudio ya kufunguliwa Juju na Majuju ni kuenea kwao katika mabara.

Vyovyote iwavyo sisi hatujawahi kusoma ya kutegemewa kuhusu Juju na Majuju, si katika tafsiri wala mahali penginepo. Kwa hiyo tutasimama kwenye dhahiri ya nukuu ya Qur’an tu na ufafanuzi tutawachia wengine.

Na miadi ya haki itakaribia, ndipo yatakapokodoka macho ya wale waliokufuru.

Makusudio ya miadi ya haki hapa ni Kiyama, hapo akili za waliokufuru zitapotea na macho yatatoka kutokana na vituko vya siku hiyo. Umetangulia mfano wake katika Juz. 13 (14: 42).

Ole wetu! Hakika tulikuwa tumeghafilika na haya, bali tulikuwa wenye kudhulumu.

Yaani watasema hivyo. Umetangulia mfano wake katika Juz. 8 (7:5) na katika juzuu na Sura hii tuliyo nayo Aya 14 na 46.

Hakika nyinyi na hayo mnayoyaabudu badala ya Mwenyezi Mungu ni kuni za Jahannam, mtaifikia.

Hapa wanaambiwa washirikina wa Makka. Makusudio ya mnayoyaabudu ni masanamu yao. Maana ni kuwa, enyi washirikina! Nyinyi na masanamu yenu mtakutana kwenye Jahannamu kesho. Kuna Hadithi isemayo: “Mtu yuko pamoja na anayempenda.”

Unaweza kuuliza : Kuna faida gani ya kutiwa masanamu kwenye Jahannamu na ni mawe yasiyokuwa na utambuzi wala hisiya?

Wafasiri wamejibu kuwa lengo ni kuwazidishia masikitiko wale wanaoyaabudu, kila watakapoyaona karibu nao. Lakini jawabu hili ni kiasi cha kuchukulia uzuri na hisia tu. Lilio bora ni kuicha Aya nyingine ijibu:

فَاتَّقُوا النَّارَ الَّتِي وَقُودُهَا النَّاسُ وَالْحِجَارَةُ ﴿٢٤﴾

“Basi uogopeni moto ambao kuni zake ni watu na mawe, uliowekewa makafiri.” Juz. 1 (2:24).

Kuna riwaya isemayo kuwa Ibn Az-Zab’ariy – mmoja wa washirkina wa kikuraishi na mshairi wao – aliingilia Aya hii kama mayahudi wanamwabudu Uzayr na wanaswara (wakristo) wanamwabudu Masihi na hawa wawili ni watu wa Peponi, kama anavyosema Muhammad, sasa vipi aseme kila kinachoabudiwa ni kuni?

Mtume akamjibu: Ni ujinga ulioje wako wewe kutojua lugha ya watu wako. Kwani huoni herufi ma (ambayo) ni ya visivyo na akili?

Zaidi ya hayo maneno yanawahusu washirikina wa kikurashi, kama tulivyotangulia kusema nao wanaabudu masanamu.

Lau haya yangelikuwa ni miungu yasingeliingia na wote watadumu humo.

Haya ni ishara ya masanamu. Maana ya Aya yako wazi, kwamba lau masanamu yangelikuwa miungu yasingeliiingia motoni. Ni kama kusema: Lau ungelikuwa mwaminifu usingelifanya khiyana, lakini umefanya khiyana kwahiyo wewe si mwaminifu. Mfano huu katika mantiki unaitwa kutoa dalili kwa kipimo cha kuvua (istithnaiyy).

Lao humo ni kupiga mayowe na wala hawatasikika.

Hapa anaambiwa kila mkosaji, awe mwislamu au kafiri. Humo ni humo ndani ya Jahannam. Maana ni kuwa kila mkosaji atakuwa katika Jahannam akilalama kwa machungu; hatasikia neno la upole wala huruma, bali atakayemuona atamtahayariza na kumsema:

وَقِيلَ لِلظَّالِمِينَ ذُوقُوا مَا كُنتُمْ تَكْسِبُونَ ﴿٢٤﴾

“Na wenye kudhulumu wataambiwa onjeni yale mliyokuwa mkiyachuma.” (39:24).

إِنَّ الَّذِينَ سَبَقَتْ لَهُم مِّنَّا الْحُسْنَىٰ أُولَـٰئِكَ عَنْهَا مُبْعَدُونَ ﴿١٠١﴾

101. Hakika wale ambao umewatangulia wema kutoka kwetu, hao watatenganishwa na hayo.

لَا يَسْمَعُونَ حَسِيسَهَا وَهُمْ فِي مَا اشْتَهَتْ أَنفُسُهُمْ خَالِدُونَ ﴿١٠٢﴾

102. Hawatasikia mvumo wake. Nao watudumu katika yale ambayo nafsi zao zinayatamani.

لَا يَحْزُنُهُمُ الْفَزَعُ الْأَكْبَرُ وَتَتَلَقَّاهُمُ الْمَلَائِكَةُ هَـٰذَا يَوْمُكُمُ الَّذِي كُنتُمْ تُوعَدُونَ ﴿١٠٣﴾

103. Hiyo fazaa kubwa haitawahuzunisha. Na Malaika watawapokea: Hii ndiyo siku yenu mliyokuwa mkiahidiwa.

يَوْمَ نَطْوِي السَّمَاءَ كَطَيِّ السِّجِلِّ لِلْكُتُبِ كَمَا بَدَأْنَا أَوَّلَ خَلْقٍ نُّعِيدُهُ وَعْدًا عَلَيْنَا إِنَّا كُنَّا فَاعِلِينَ ﴿١٠٤﴾

104. Siku tutakapozikunja mbingu mkunjo wa karatasi za vitabu. Kama tulivyoanza umbo la mwanzo tutalirudisha tena. Ni ahadi iliyo juu yetu. Hakika sisi ni wenye kufanya.

وَلَقَدْ كَتَبْنَا فِي الزَّبُورِ مِن بَعْدِ الذِّكْرِ أَنَّ الْأَرْضَ يَرِثُهَا عِبَادِيَ الصَّالِحُونَ ﴿١٠٥﴾

105. Na hakika tulikwishaandika katika Zaburi baada ya ukumbusho kuwa Ardhi watairithi waja wangu walio wema.

إِنَّ فِي هَـٰذَا لَبَلَاغًا لِّقَوْمٍ عَابِدِينَ ﴿١٠٦﴾

106. Hakika katika haya kuna ujumbe kwa wafanyao ibada.

وَمَا أَرْسَلْنَاكَ إِلَّا رَحْمَةً لِّلْعَالَمِينَ ﴿١٠٧﴾

107. Na hatukukutuma ila uwe ni rehema kwa walimwengu.

ARDHI WATARITHI WAJA WANGU WALIO WEMA

Aya 101 – 107

MAANA

Hakika wale ambao umewatangulia wema kutoka kwetu, hao watatenganishwa na hayo.

Mwenyezi Mungu aliwaahidi wenye takua kuamiliana nao kwa wema. Miongoni mwa wema huo ni kuokoka na moto.

Hawatasikia mvumo wake.

Hii ni kusisitiza watakavyokuwa mbali nao.

Nao watudumu katika yale ambayo nafsi zao zinayatamani.

Watasalimika na adhabu ya Mwenyezi Mungu wakineemeshwa kwenye Pepo yake.

Hiyo fazaa kubwa haitawahuzunisha, sikwambii ndogo tena.

Kwani fazaa zina daraja, kuanzia machungu ya kukata roho, upweke wa kaburini, kisha kutoka makaburini kwa ajili ya hisabu hadi kuingia Jahannam.

Na Malaika watawapokea: Hii ndiyo siku yenu mliyokuwa mkiahidiwa.

Malaika watawapokea kwa takrima na kuwaambia kuwa Mwenyezi Mungu amewakusanya kwenye siku hii aliyowaahidi kwa ufalme wa daima na neema isiyokatika. Aya hizi tatu zinafupilizwa na neno:

هَلْ جَزَاءُ الْإِحْسَانِ إِلَّا الْإِحْسَانُ ﴿٦٠﴾

“Je, malipo ya hisani si ni hisani tu.” (55:60)

Au neno:

لِّلَّذِينَ أَحْسَنُوا الْحُسْنَىٰ وَزِيَادَةٌ ﴿٢٦﴾

“Kwa wafanyao wema ni wema.” Juz.11 (10:26).

Siku tutakapozikunja mbingu mkunjo wa karatasi za vitabu.

Makusudio ya vitabu hapa ni maandishi ya matamko yanayoayaandikwa kwenye karatasi. Maana ni kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) atazikunja sayari, siku ya Kiyama, pamoja na ukubwa na wingi wake; kama inavyokunjwa karatasi yenye maandishi; kiasi ambacho kila sayari itafanana na herufi au neno lilo kwenye karatasi.

Kama tulivyoanza umbo la mwanzo tutalirudisha tena. Ni ahadi iliyo juu yetu. Hakika sisi ni wenye kufanya.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) amefananisha ufufuo na kuumba kwa kwanza; kwamba, kama kulivyowezekana kwa kwanza, basi kwa pili pia kuunawezekana. Si muhali kwa Mwenyezi Mungu kutekeleza ahadi yake.

Hilo halimshindi Mwenyezi Mungu; kwani mwenye kuumba ulimwengu basi hawezi kushindwa kuurudisha tena baada ya kuharibika na kutawanyika:

وَهُوَ الَّذِي يَبْدَأُ الْخَلْقَ ثُمَّ يُعِيدُهُ وَهُوَ أَهْوَنُ عَلَيْهِ ﴿٢٧﴾

“Na Yeye ndiye anayeanzisha uumbaji, kisha ataurudisha. Na hilo ni jepesi zaidi kwake” (30:27).

TENA MAHDI ANAYENGOJEWA

Na hakika tulikwishaandika katika Zaburi baada ya ukumbusho kuwa Ardhi watairithi waja wangu walio wema.

Zaburi ni kitabu cha Daud na ukumbusho ni vitabu vya mbinguni vilivyotangulia; kama vile vitabu vya Ibrahim na Musa. Maana yake ni kuwa utawala wa dunia, ingawaje hivi sasa uko mikononi mwa mataghuti waovu, lakini Mwenyezi Mungu atauhamisha uende kwa walio wema. Hilo halina budi. Hapo amani na uadilifu utaenea ardhini na watu wote wataneemeka na kheri za Ardhi na baraka zake.

Kuna Hadithi nyingi zenye maana ya Aya hii; miongoni mwazo ni ile aliy- oipokea Abu Daud katika Kitabu cha Sunan, ambacho ni mojawapo ya Sahihi sita: “Amesema Mtume wa Mwenyezi Mungu:

Lau haitabakia katika dunia isipokuwa siku moja tu, basi Mwenyezi Mungu angeliirefusha siku hiyo mpaka amtume mtu kutoka katika watu wa nyumba yangu (Ahlu bayt) jina lake linafanana na jina langu, na jina la baba yake ni kama la baba yangu, ataijaza ardhi uadilifu baada ya kujazwa dhulma na jeuri” [4] .

Kanuni ya maisha hailikatai hilo, bali inalithibitisha na kulisisitiza. Ikiwa nguvu hivi sasa ziko mikononi mwa unyama wenye kudhuru wa umoja wa mataifa, baraza la usalama n.k. basi hakuna litakalozuia, siku moja kugeuka nguvu hiyo kutoka mikononi mwa madhalimu waovu hadi kwa watu wa haki na uadilifu; bali maumbile yanapenda kujikomboa na dhulma.

Pia kuna misingi isemayo: “Kila kilicho katika ardhi kina harakati, kama ilivyo na harakati ardhi na kwamba kudumu hali ni muhali.” Yote hayo yanapelekea kuwa hatimaye nguvu zitakuwa mikononi mwa wema wanao- faa.

Hakika katika haya kuna ujumbe kwa wafanyao ibada.

Haya ni haya ya kuwa ardhi itarithiwa na waja wema; hata kama ni baada ya muda. Makusudio ya wafanyao ibada hapa ni wale wanaopata mawaidha kwa kuzingatia na kunufaika na maonyo.

Na hatukukutuma ila uwe ni rehema kwa walimwengu.

Maneno yanaelekezwa kwa Muhammad(s.a.w.w) . Risala yake ni rehema kwa wa mwanzo na wa mwisho. Huko nyuma tumeeleza mara nyingi kuhusu misingi ya risala hiyo na mafunzo yake.

Inatosha, kuthibitisha hilo, kauli za mwenye risala hiyo; kama vile: “Hakumwamini Mwenyezi Mungu yule ambaye watu hawamwamini. Likikuhuzunisha ovu na likakufurahisha jema, basi wewe ni mumin.”

Ni kwa hisia hizi ndio uadilifu utasimama, amani kuenea na maisha kuwa bora. Tumezungumzia kwa ufafanuzi kuhusu hilo katika Juz. 7 (6:92).

قُلْ إِنَّمَا يُوحَىٰ إِلَيَّ أَنَّمَا إِلَـٰهُكُمْ إِلَـٰهٌ وَاحِدٌ فَهَلْ أَنتُم مُّسْلِمُونَ ﴿١٠٨﴾

108. Sema: Hakika umeletwa wahyi kwangu ya kwamba hakika Mungu wenu ni Mungu mmoja tu. Je nyinyi mmesilimu?

فَإِن تَوَلَّوْا فَقُلْ آذَنتُكُمْ عَلَىٰ سَوَاءٍ وَإِنْ أَدْرِي أَقَرِيبٌ أَم بَعِيدٌ مَّا تُوعَدُونَ ﴿١٠٩﴾

109. Kama wakikataa, basi sema: Nimewatangazia sawasawa. Wala sijui yako karibu au mbali hayo mliyoahidiwa.

إِنَّهُ يَعْلَمُ الْجَهْرَ مِنَ الْقَوْلِ وَيَعْلَمُ مَا تَكْتُمُونَ ﴿١١٠﴾

110. Hakika Yeye anajua kauli ya dhahiri na anajua mnayoyaficha.

وَإِنْ أَدْرِي لَعَلَّهُ فِتْنَةٌ لَّكُمْ وَمَتَاعٌ إِلَىٰ حِينٍ ﴿١١١﴾

111. Wala sijui pengine huu ni mtihani tu kwenu na starehe mpaka muda kidogo.

قَالَ رَبِّ احْكُم بِالْحَقِّ وَرَبُّنَا الرَّحْمَـٰنُ الْمُسْتَعَانُ عَلَىٰ مَا تَصِفُونَ ﴿١١٢﴾

Akasema: Mola wangu! Hukumu kwa haki. Na Mola wetu ni Mwingi wa rehema aombwaye msaada juu ya mnayoyasifia.

HAKIKA MUNGU WENU NI MMOJA TU

Aya 108 – 112

MAANA

Sema: Hakika umeletwa wahyi kwangu ya kwamba hakika Mungu wenu ni Mungu mmoja tu. Je nyinyi mmesilimu?

Mwenyezi Mungu alimwarisha Mtume wake awaambie washirikina kuwa Mwenyezi Mungu ameniletea wahyi kwamba Yeye ni mmoja tu hana mshirika katika kuumba kwake na wala katika ujuzi wake.

Ulimwengu huu na maajabu yake na kanuni zake unashuhudia kwa uwazi juu ya umoja, uweza na ukuu wake Mwenyezi Mungu Mtukufu.

Basi kwa nini hamuamini na kufuata amri yake? Kwanini mnadanganyika kuacha kumwabudu Yeye na kwenda kuabudu mawe yasiyodhuru wala kunufaisha?

Kama wakikataa, basi sema: Nimewatangazia sawasawa.

Baada ya kuwalazimu hoja ya kufikisha na maonyo, Mwenyezi Mungu alimwamrisha Mtume wake mtukufu awaambie kuwa nimekishatekeleza wajibu wangu na nikafikisha risala ya Mola wangu. Kwa hiyo haukubaki udhuru wowote kwenu.

Wala sijui yako karibu au mbali hayo mliyoahidiwa.

Mimi nina yakini na adhabu yenu, kwa sababu Mwenyezi Mungu ameiahadi na kuwahadhirisha nayo, na ahadi yake Mwenyezi Mungu ni ya kweli na adhabu yake pia ni kali zaidi, lakini sijui itakuwa lini. Ni sawa iwe karibu au mbali, lakini ina wakati wake. Ngojeni nami niko pamoja nanyi katika wenye kungojea.

Hakika Yeye anajua kauli ya dhahiri na anajua mnayoyaficha.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 16 (20:7).

Wala sijui pengine huu ni mtihani tu kwenu na starehe mpaka muda kidogo.

Sijui kuna hekima gani ya kupewa kwenu muda na kucheleweshewa adhabu. Je Mwenyezi Mungu (s.w.t.) ametaka kumdhirisha kila mmoja hakika yake, aweze kutubia mwema na aendelee mouvu au ametaka mustarehe siku zilizobakia kwenye umri wenu? Mwenyezi Mungu ndiye ajuaye.

Akasema (Muhammad): Mola wangu! Hukumu kwa haki.

Yaani idhihirishe haki na uwanusuru watu wake kwa wale wanaoipinga.

Na Mola wetu ni Mwingi wa rehema aombwaye msaada juu ya mnayoyasema kuwa masanamu yenu ni miungu na madai yenu kwangu kuwa ni mzushi.

Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu! Wewe ni mtukufu kwa kila anayekuzulia. Wema ni wa yule anayekufuata, akachukua athari yako na akamwambia mzushi, kama vile ulivyosema wewe:

Na Mola wetu ni Mwingi wa rehema aombwaye msaada juu ya mnayoyasifia.

MWISHO WA SURA YA ISHIRINI NA MMOJA


4

5

6