TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA NANE Juzuu 18

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA NANE0%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA NANE Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: Qurani tukufu

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA NANE

Mwandishi: Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya
: HASANI MWALUPA
Kundi:

Matembeleo: 11223
Pakua: 2130


Maelezo zaidi:

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 13 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 11223 / Pakua: 2130
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA NANE

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA NANE Juzuu 18

Mwandishi:
Swahili

3

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA NANE

يَا أَيُّهَا الرُّسُلُ كُلُوا مِنَ الطَّيِّبَاتِ وَاعْمَلُوا صَالِحًا إِنِّي بِمَا تَعْمَلُونَ عَلِيمٌ ﴿٥١﴾

51. Enyi Mitume! Kuleni katika vitu vizuri na fanyeni mema. Hakika mimi ni Mjuzi wa mnayoyatenda.

وَإِنَّ هَـٰذِهِ أُمَّتُكُمْ أُمَّةً وَاحِدَةً وَأَنَا رَبُّكُمْ فَاتَّقُونِ ﴿٥٢﴾

52. Na hakika umma wenu huu ni umma mmoja na mimi ni Mola wenu, basi nicheni.

فَتَقَطَّعُوا أَمْرَهُم بَيْنَهُمْ زُبُرًا كُلُّ حِزْبٍ بِمَا لَدَيْهِمْ فَرِحُونَ ﴿٥٣﴾

53. Lakini walikatiana jambo lao kwa vitabu mbali mbali. Kila kundi linafurahia kwa waliyo nayo.

فَذَرْهُمْ فِي غَمْرَتِهِمْ حَتَّىٰ حِينٍ ﴿٥٤﴾

54. Basi waache katika upotevu wao kwa muda.

أَيَحْسَبُونَ أَنَّمَا نُمِدُّهُم بِهِ مِن مَّالٍ وَبَنِينَ ﴿٥٥﴾

Je wanadhani kuwa vile tunavyowapa mali na watoto.

نُسَارِعُ لَهُمْ فِي الْخَيْرَاتِ بَل لَّا يَشْعُرُونَ ﴿٥٦﴾

56. Ndio tunawahimizia kheri? Lakini hawatambui.

MOLA MMOJA NA DINI MOJA

Aya 51 – 56

MAANA

Katika Juz. 2 (2:172) Mwenyezi Mungu (s.w.t) anawaambia waumini: "Kuleni vizuri tulivyowaruzuku na mumshukuru Mwenyezi Mungu." Katika Aya hii anawaambia Mitume: Kuleni katika vitu vizuri na fanyeni mema. Hakika mimi ni Mjuzi wa mnayoyatenda.

Lengo la kauli zote hizo ni kubainisha kuwa dini ya haki ni takua na matendo mema sio kujinyima raha. Kila utakalolifurahia na kuburudika nalo basi hilo ni jema mbele ya Mwenyezi Mungu, ikiwa hakulikataza; sawa na lilivyo jema kwako. Kuna Hadith isemayo:"Hakika Mwenyezi Mungu ni Mzuri na hupenda uzuri."

Na kwamba Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) alikuwa akivaa kila ali- chokimudu katika sufu, pamba (cotton) na vitambaa vinginevyo. Hakuwa akikataa vitu vizuri, lakini hakujikalifisha navyo.

Alikuwa akila haluwa na asali na akizipenda. Akila nyama ya ngamia, kondoo na kuku. Pia alikuwa akila matango na maboga kwa tende mbichi, na akipenda kula tende kwa siagi, mkate kwa nyama na maini ya kuchoma na mkate wa kuchanganywa na mchuzi.

Kwa ujumla Mtume(s.a.w.w) alikuwa akila na kuvaa kile anachokimudu, akikosa huvumilia na kuwa na subira. Na kitu kizuri zaidi ni kula kwa jasho. Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) anasema: "Ni katika uzuri zaidi mtu kula kutokana na chumo lake."

Na hakika umma wenu huu ni umma mmoja na mimi ni Mola wenu, basi nicheni.

Neno umma lina maana nyingi; miongoni mwazo ni hizi:-

1. Kundi la watu: Kama alivyosema Mwenyezi Mungu: "Ingieni motoni pamoja na umma zilizopita." Juz. 8 (7:38).

2. Muda: Mwenyezi Mungu anasema: "Na akakumbuka baada ya muda." Juz. 12 (12:45).

Neno muda limefasiriwa kutokana na neno umma.

3. Mila: Kama ilivyo katika Aya hii tuliyo nayo.

Aya hii inaashiria mila za Mitume wote. Msemo katika neno umma wenu, unaelekezwa kwa watu wote, kwa dalili ya kauli yake Mwenyezi Mungu iliyokuja moja kwa moja 'lakini walikatiana jambo lao ...' ambapo maana ni kwa nini watu wanachukiana na kuwa vikundi mbali mbali, kukawa na kikundi cha Musa, cha Isa na cha Muhammad na hali Mungu wao ni mmoja, dini yao ni moja na lengo lao ni moja? Kuna Hadith isemayo: "Mitume wote ni ndugu, mama zao ni mbali mbali na dini yao ni moja."

Unaweza kuuliza : kwanini sharia za mitume ni tofauti na dini yao ni moja?

Jibu : Kutofautiana sharia hakusababishi kutofautiana dini maadamu msingi ni mmoja; kwa mfano serikali za kikiristo zinatofautiana kikanuni na kisheria, lakini zinakuwa pamoja kiitikadi na kidini.

Lakini walikatiana jambo lao kwa vitabu mbali mbali. Kila kundi linafurahia kwa waliyo nayo.

Hapa wanazungumziwa wafuasi wa Mitume; yaani mitume wako kwenye dini moja, lakini wafuasi wao wako kwenye dini mbali mbali. Kila kundi likafuata Kitabu wanachokiamini na kukikana kingine. Mayahudi waliamini Tawrat baada ya kuipotoa na kuikana Injil na Qur'an. Wanaswara nao waliipotoa Injil na wakiamini pamoja na Tawrt iliyopotolewa na wakaikana Qur'an.

Tazama tuliyoyaandika kwa anuani ya 'Kila mmoja avutia dini yake' Juz. 1 (2: 111-113).

Basi waache katika upotevu wao kwa muda.

Baada ya Mtume(s.a.w.w) kuwafikishia risala ya Mola wake na akawaondolea nyudhuru zote kwa jinsi alivyowahadharisha, Mwenyezi Mungu alimwamrisha kuachana nao na awaache na upotevu wao.

Hili ni karipio na kiaga kutokana na kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu iliyokuja moja kwa moja Je wanadhani kuwa vile tunavyowapa mali na watoto ndio tunawahimizia kheri? Lakini hawatambui.

Wamedanganyika na watoto na mali wakadhani kuwa watadumu nazo, lakini hakujua kuwa Mungu amewawekea muda maalum, kisha awanyakue kwa mnyakuo wa Mwenye nguvu na ushindi.

إِنَّ الَّذِينَ هُم مِّنْ خَشْيَةِ رَبِّهِم مُّشْفِقُونَ ﴿٥٧﴾

57. Hakika wale ambao humwogopa Mola wao wanamnyenyekea.

وَالَّذِينَ هُم بِآيَاتِ رَبِّهِمْ يُؤْمِنُونَ ﴿٥٨﴾

58. Na wale ambao wanaamini ishara za Mola wao.

وَالَّذِينَ هُم بِرَبِّهِمْ لَا يُشْرِكُونَ ﴿٥٩﴾

59. Na wale ambao hawamshirikishi Mola wao.

وَالَّذِينَ يُؤْتُونَ مَا آتَوا وَّقُلُوبُهُمْ وَجِلَةٌ أَنَّهُمْ إِلَىٰ رَبِّهِمْ رَاجِعُونَ ﴿٦٠﴾

60. Na wale ambao wanatoa walichopewa na hali nyoyo zao zinaogopa kwa kuwa watarejea kwa Mola wao.

أُولَـٰئِكَ يُسَارِعُونَ فِي الْخَيْرَاتِ وَهُمْ لَهَا سَابِقُونَ ﴿٦١﴾

61. Hao ndio wanokimbilia kwenye kheri na ndio watakaotangulia kuzifikia.

وَلَا نُكَلِّفُ نَفْسًا إِلَّا وُسْعَهَا وَلَدَيْنَا كِتَابٌ يَنطِقُ بِالْحَقِّ وَهُمْ لَا يُظْلَمُونَ ﴿٦٢﴾

62. Na hatuikalifishi nafsi ila kwa uwezo wake. Na tuna kitabu kisemacho kweli. Nao hawatadhulumiwa.

TENA SIFA ZA WAUMINI

Aya 57 – 62

MAANA

Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kutaja wale wanaoishi kwenye mghafala wa upotevu, huku wenyewe wakiona kuwa wanaharakishiwa kheri, sasa anawataja waumini, kwamba ni wale wanaosifika na mambo yafuatayo:

1.Hakika wale ambao humwogopa Mola wao wanamnyenyekea.

Unaweza kuuliza kuwa : kunyenyenyekea pia ni kuogopa, sasa itakuwaje wao wawe 'wanaogopa kuogopa'?

Jibu : Makusudio ya kunyenyekea hapa ni kupupia kumtii Mwenyezi Mungu. Makadirio ya maneno ni, wao wanapupia kumtii Mwenyezi Mungu kwa kuhofia adhabu yake.

2.Na wale ambao wanaamini ishara za Mola wao.

Yaani wanaamini dalili za kuweko Mungu na ukuu wake, utume wa Mitume yake na ukweli wa vitabu vyake.

3.Na wale ambao hawamshirikishi Mola wao.

Unaweza kuuliza : Wale ambao wanaziamini ishara zake bila shaka hawawezi kumshirikisha, sasa kuna haja gani ya kurudia maneno? Razi amejibu kuwa makusudio ya shirki hapa ni ile shirki iliyojificha; kama vile ria na kukosa ikhlasi katika matendo. Makusudio ya imani katika Aya iliyotangulia ni kule kuamini tu.

4.Na wale ambao wanatoa walichopewa na hali nyoyo zao zinaogopa kwa kuwa watarejea kwa Mola wao.

Wanatoa katika vile alivyowapa Mwenyezi Mungu na kutekeleza haki yake na haki za watu kwa ukamilifu, lakini pamoja na hayo wanahofia kuwa Mwenyezi Mungu hatawatakabalia.

Hao ndio wanaokimbilia kwenye kheri na ndio watakaotangulia kuzifikia.

Yaani wale ambao wametimiza masharti haya yaliyotajwa ndio wanaoharakia twaa ya Mwenyezi Mungu na wala hawangojingoji. Kwa ajili hiyo basi wao watawatangulia watu kuingia peponi kesho.

Na hatuikalifishi nafsi ila kwa uwezo wake.

Kwa sababu kukalifisha lisilowezekana ni dhulma, na Mwenyezi Mungu ambaye ameikataza dhulma hawezi kuifanya.

Na tuna kitabu kisemacho kweli.

Kinasajili dogo na kubwa na Mwenyezi Mungu atalipa kwacho; ikiwa ni kheri basi ni kheri na ikiwa ni shari basi ni shari.

Nao hawatadhulumiwa kwa kupunguziwa thawabu mwenye kufanya wema wala kuzidishiwa adhabu mwenye kufanya uovu.

بَلْ قُلُوبُهُمْ فِي غَمْرَةٍ مِّنْ هَـٰذَا وَلَهُمْ أَعْمَالٌ مِّن دُونِ ذَٰلِكَ هُمْ لَهَا عَامِلُونَ ﴿٦٣﴾

63. Bali nyoyo zao zimo ujingani na haya na wana vitendo vingine wanavyovitenda.

حَتَّىٰ إِذَا أَخَذْنَا مُتْرَفِيهِم بِالْعَذَابِ إِذَا هُمْ يَجْأَرُونَ ﴿٦٤﴾

64. Mpaka tutakapowatia katika adhabu wale waliodekezwa na starehe kati yao, hapo ndipo watakapoyayatika.

لَا تَجْأَرُوا الْيَوْمَ إِنَّكُم مِّنَّا لَا تُنصَرُونَ ﴿٦٥﴾

65. Msiyayatike leo! Hakika nyinyi hamtanusurika nasi.

قَدْ كَانَتْ آيَاتِي تُتْلَىٰ عَلَيْكُمْ فَكُنتُمْ عَلَىٰ أَعْقَابِكُمْ تَنكِصُونَ ﴿٦٦﴾

66. Hakika zilikuwa Aya zangu mkisomewa nanyi mkirudi nyuma juu ya visigino vyenu.

مُسْتَكْبِرِينَ بِهِ سَامِرًا تَهْجُرُونَ ﴿٦٧﴾

67. Na huku mkiifanyia kiburi na mkiizungumza usiku kwa dharau.

أَفَلَمْ يَدَّبَّرُوا الْقَوْلَ أَمْ جَاءَهُم مَّا لَمْ يَأْتِ آبَاءَهُمُ الْأَوَّلِينَ ﴿٦٨﴾

68. Je, hawakuifikiri kauli au yamewafikia yasiyowafikia baba zao wa zamani?

أَمْ لَمْ يَعْرِفُوا رَسُولَهُمْ فَهُمْ لَهُ مُنكِرُونَ ﴿٦٩﴾

69. Au hawakumjua Mtume wao ndio maana wanamkataa?

أَمْ يَقُولُونَ بِهِ جِنَّةٌ بَلْ جَاءَهُم بِالْحَقِّ وَأَكْثَرُهُمْ لِلْحَقِّ كَارِهُونَ ﴿٧٠﴾

70. Au wanasema ana wazimu? Bali amewajia na haki na wengi wao wanaichukia haki.

وَلَوِ اتَّبَعَ الْحَقُّ أَهْوَاءَهُمْ لَفَسَدَتِ السَّمَاوَاتُ وَالْأَرْضُ وَمَن فِيهِنَّ بَلْ أَتَيْنَاهُم بِذِكْرِهِمْ فَهُمْ عَن ذِكْرِهِم مُّعْرِضُونَ ﴿٧١﴾

71. Na lau haki ingelifuata matamanio yao basi zingeliharibika mbingu na ardhi na waliomo ndani yake. Bali tumewaletea utajo wao na wanajitenga mbali na utajo wao.

أَمْ تَسْأَلُهُمْ خَرْجًا فَخَرَاجُ رَبِّكَ خَيْرٌ وَهُوَ خَيْرُ الرَّازِقِينَ ﴿٧٢﴾

72. Au unawaomba ujira? Lakini ujira wa Mola wako ni bora na Yeye ndio mbora wa wanaoruzuku.

NYOYO ZAO ZIMO UJINGANI

Aya 63 – 72

MAANA

Bali nyoyo zao zimo ujingani na haya na wana vitendo vingine.

Wanaelezewa washirikina. Neno 'haya' ni haya aliyoyataja Mwenyezi Mungu (s.w.t) katika Aya zilizotangulia kuhusu sifa za waumini ambazo ni kumwamini Mwenyezi Mungu, kumhofia na kukimbilia kheri.

Maana ni kuwa waashirikina wamo kwenye mghafala na sifa hizi pia wana maovu mengine zaidi ya ushirikina; kwamba wao wanaifanyia maskhara Qur'an na kumzulia Mtume wa Mwenyezi Mungu huku wakisema kuwa yeye ni mchawi mwendawazimu.

Wanavyovitenda.

Unaweza kuuliza : maana ya kutenda si ndio hivyo vitendo, sasa itakuwaje watende vitendo?

Jibu : Makusudio ya vitendo hapa ni vitendo viovu; ni kama Mwenyezi Mungu (s.w.t) amesema wao wanatenda maovu.

Mpaka tutakapowatia katika adhabu wale waliodekezwa na starehe kati yao, hapo ndipo watakapoyayatika.

Hayo ndio mazoweya ya wanaodeka, wanazama kwenye upotevu. Kwa maelezo zaidi tazama Juz. 15 (17:16).

Wao wameghafilika kabisa na mambo ya ghafla yaliyojificha wala hawazingatii mifano ya waliowatangulia, mpaka itakapowafikia siku ya Kiyama na ikafika saa ya hisabu na malipo ndipo watainua sauti zao kwa kulia na kuomboleza, huku wakinyenyeka, wakati ambao hakuna msaada wowote wala maneno yoyote ya kutuliza isipokuwa kauli ya Mwenyezi Mungu, Mwenye nguvu:

Msiyayatike leo! Hakika nyinyi hamtanusurika nasi.

Yaani msitafute msaada wala kunyenyekea, kwani leo ni siku ya hisabu na malipo tu, na wala hataokoka na adhabu yake isipokwa yule aliyefanya matendo kwa ajili ya siku hii.

Hakika zilikuwa Aya zangu mkisomewa nanyi mkirudi nyuma juu ya visigino vyenu.

Mwenyezi Mungu amewahadharisha na siku hii kupitia kwa mitume wake, mara nyingi na kwa mifumo tofauti tofauti, lakini wakakataa isipokuwa kukadhibisha na kufanya inadi. Ndio akawalipa kwa yale waliyoyafanya; wala Mola wako hatamdhulumu yeyote.

Na huku mkiifanyia kiburi na mkiizungumza usiku kwa dharau.

Dhamiri katika neno mkiifanyia inarudia Qur'an na kuifanyia kiburi ni kuikadhibisha. Maana yanakuwa wao wameikadhibisha Qur'an na wakafanya hiyo Qur'an na yule aliyeteremshiwa kuwa ni gumzo lao la usiku kwa dharau

Je, hawakuifikiri kauli ambayo ni Qur'an na dalili iliyo nazo juu ya tawhidi na ukweli wa Muhammad(s.a.w.w) . Au yamewafikia yasiyowafikia baba zao wa zamani?

Vipi iwe hivyo na hali Qur'an inasadikisha wale waliotangulia katika mitume na habari ya yaliyowatokea pamoja na watu wao.

Zaidi ya hayo, washirikina wa kiarabu wanamjua Ibrahim, Hud, Swaleh na Shua'yb. Mitume wote hawa watatu ni waarabu. Kwa hiyo basi kuna kioja gani katika utume wa Muhammad?

Au hawakumjua Mtume wao ndio maana wanamkataa?

Au Makuraishi wataleta udhuru kuwa hawamjui Muhammad naye ni miongoni mwao tena walikuwa wakimwita mkweli mwaminifu? Au wanasema ana wazimu? Na hali wanajua kuwa yeye ndiye mwenye akili na mkamilifu wao zaidi? Kwa hiyo hapa kuna mengine sio haya. Kwa muhtasari ni haya yafuatayo:

MWANGA WA JUA NA WANAODEKA NA STAREHE

Bali amewajia na haki na wengi wao wanaichukia haki.

Muhammad alikuja na haki. Hilo peke yake ni kosa kwa wabatilifu. Ni haki gani hiyo aliyokuja nayo Muhammad? Je, ni kutamka shahada mbili tu basi? Ingelikuwa hivyo ingelikuwa wepesi kwa wanompiga vita na viongozi na waanojidekeza na starehe kusema: "Hapana Mola isipokuwa Mwenyezi Mungu na Muhammad ni Mtume wa Mwenyezi Mungu."

Lakini Muhammad hakutosheka na matamshi haya, bali alitaka kuweka ustawi wa jamii kwa misingi ya uadilifu na usawa, usiokuwa na dhalimu wala mdhulumiwa na kila mtu aishi kama sehemu ya mwingine na kiungo cha jamii; astahiki wanayostahiki wengine na wengine nao wastahiki yale anayostahiki yeye, asimwogope yeyote isipokuwa Mwenyezi Mungu mmoja tu peke yake, wala kusiwe na ubora wa kiumbe kwa kiumbe mwingine isipokuwa kwa takua na matendo mema.

Kuanzia hapa ndio ukajitokeza ukali na uadui dhidi ya Mjumbe wa uadilifu na huruma; wakampiga vita kwa kila silaha. Lakini Mtume(s.a.w.w) alikuwa na yakini na jambo lake na kwamba mwisho utakuwa ni wa msin- gi wake na risala yake. Kwa ajili hii alikuwa akiwatazama mahasimu wake, kama anavyotazama mawingu ya kaskazi au kivuli kinachoondoka.

Na lau haki ingelifuata matamanio yao basi zingeliharibika mbingu na ardhi na waliomo ndani yake.

Makusudio ya haki hapa ni Mwenyezi Mungu na matamanio yao ni batili, upotevu, vurugu na ufisadi. Nidhamu ya ulimwengu pamoja na ardhi yake na mbingu yake inasimama kwa misingi ya uadilifu na haki. Kwa hiyo kuharibika ulimwengu hakuna budi ikiwa haki itafuata matamanio yao.

Hapana shaka kwamba lau Mwenyezi Mungu (s.w.t) ataitikia matakwa yao na wanayoyatamani, basi wangelizuia mwanga wa jua kuwafikia wanyonge na wangeliuzia ulimwengu na yaliyomo ndani yake kwa jili yao wenyewe, watoto wao na wakwe zao.

Bali tumewaletea utajo wao nao wanajitenga mbali na utajo wao.

Muhammad(s.a.w.w) aliwaletea waarabu kwa ujumla na hasa makuraishi, utajo wao; yaani utawala wao sifa zao na historia yao, lakini wakamkana bali wakamuwekea vikwazo na kumpiga vita.

Lau si yeye wasingelikuwa chochote cha kutajwa. Mwenyezi Mungu anasema:

وَإِنَّهُ لَذِكْرٌ لَّكَ وَلِقَوْمِكَ ﴿٤٤﴾

"Na hakika hiyo (Qur'an) ni utajo kwako na kwa kaumu yako' (43:44).

Au unawaomba ujira? Lakini ujira wa Mola wako ni bora na Yeye ndio mbora wa wanaoruzuku.

Mtume aliwaletea utukufu wa dunia na akhera, lakini wakaukataa pamoja na kujua kwamba yeye hakuwataka malipo wala shukrani, kwa sababu Mwenyezi Mungu anamtosha kwenye dunia yake na akhera.

4

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA NANE

وَإِنَّكَ لَتَدْعُوهُمْ إِلَىٰ صِرَاطٍ مُّسْتَقِيمٍ ﴿٧٣﴾

73. Na hakika wewe unawaita kwenye njia iliyonyooka.

وَإِنَّ الَّذِينَ لَا يُؤْمِنُونَ بِالْآخِرَةِ عَنِ الصِّرَاطِ لَنَاكِبُونَ ﴿٧٤﴾

74. Na hakika wale ambao hawaiamini akhera wanajitenga na njia hiyo.

وَلَوْ رَحِمْنَاهُمْ وَكَشَفْنَا مَا بِهِم مِّن ضُرٍّ لَّلَجُّوا فِي طُغْيَانِهِمْ يَعْمَهُونَ ﴿٧٥﴾

75. Lau tungeliwarehemu tukawaondolea shida waliyo nayo, bila shaka wangeliendelea na upotevu wao wakimangamanga.

وَلَقَدْ أَخَذْنَاهُم بِالْعَذَابِ فَمَا اسْتَكَانُوا لِرَبِّهِمْ وَمَا يَتَضَرَّعُونَ ﴿٧٦﴾

76. Na hakika tuliwatia katika adhabu, lakini hawakuelekea kwa Mola wao wala hawakunyenyekea.

حَتَّىٰ إِذَا فَتَحْنَا عَلَيْهِم بَابًا ذَا عَذَابٍ شَدِيدٍ إِذَا هُمْ فِيهِ مُبْلِسُونَ ﴿٧٧﴾

77. Mpaka tulipowafungulia mlango wa adhabu kali, hapo ndipo wakawa ni wenye kukata tamaa.

وَهُوَ الَّذِي أَنشَأَ لَكُمُ السَّمْعَ وَالْأَبْصَارَ وَالْأَفْئِدَةَ قَلِيلًا مَّا تَشْكُرُونَ ﴿٧٨﴾

78. Yeye ndiye aliyewaumbia kusikia na kuona na nyoyo. Ni kuchache mno kushukuru kwenu.

وَهُوَ الَّذِي ذَرَأَكُمْ فِي الْأَرْضِ وَإِلَيْهِ تُحْشَرُونَ ﴿٧٩﴾

79. Yeye ndiye aliyewaumba katika ardhi na kwake mtakusanywa.

وَهُوَ الَّذِي يُحْيِي وَيُمِيتُ وَلَهُ اخْتِلَافُ اللَّيْلِ وَالنَّهَارِ أَفَلَا تَعْقِلُونَ ﴿٨٠﴾

80. Yeye ndiye anayehuisha na kufisha na Yeye ndiye mwenye mabadiliko ya usiku na mchana. Basi je, hamfahamu?

UNAWAITA K W ENYE NJIA ILIYONYOOKA

Aya 73 – 80

MAANA

Na hakika wewe unawaita kwenye njia iliyonyooka. Na hakika wale ambao hawaiamini akhera wanajitenga na njia hiyo.

Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kuelezea upotevu wa washirikina na kwamba wao hawana udhuru wowote wa kumkanusha kwao Muhammad(s.a.w.w) , sasa anamwambia Mtume wake Mtukufu kwamba yeye anazo hoja za kutosha kuwa yeye ni mkweli katika mwito wake na kwamba washirikina ambao wamemkanusha yeye na siku ya mwisho wameiacha haki na wakapotea njia ya kheri na uongofu. Nao, katika hilo, wanajidhu- ru wenyewe na hawatakudhuru wewe na chochote.

Lau tungeliwarehemu tukawaondolea shida waliyo nayo, bila shaka wangeliendelea na upotevu wao wakimangamanga.

Baada ya Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) kuhamia Madina kutoka Makka aliwapa dhiki makuraishi kwa kutuma vikosi kuwazuilia njia, mara nyingine alikuwa akiviongoza mwenyewe, na akaamrisha kuwakatia uhu- siano. Basi wakaingia kwenye dhiki, lakini bado waliendelea na upotevu wao na kufuru yao. Lau kama Mwenyezi Mungu (s.w.t) angeliwaondolea shida waliyo nayo, wasingelizingatia kuachana na upotevu wao.

Na hakika tuliwatia katika adhabu, lakini hawakuelekea kwa Mola wao wala hawakunyenyekea.

Ukiwahadharisha wanapinga, ukiwatia adabu hawazingatii na ukiwaondolea wanakuwa jeuri. Watakuwa hivi mpaka siku watakapofufuliwa, watakpoondolewa pazia washuhudie malipo ya mghafala wao na jeuri yao. Hapo watakata tamaa ya kuokoka na kujutia yaliyopita.

Mpaka tulipowafungulia mlango wa adhabu kali, hapo ndipo wakawa wenye kukata tamaa na hali Mwenyezi Mungu (s.w.t) alikwishawahadharisha na adhabu hii kali na kuwapa kiaga, lakini wakapuuza nafsi zao wakazipeleka kwenye maangamizi.

Yeye ndiye aliyewaumbia kusikia na kuona na nyoyo za kufahamu, ili mnufaike kwa mtakyoyasikia na kuyaona muweze kujua ya kheri na masilahi.

Neema za Mwenyezi Mungu kwa mtu hazina idadi, kubwa yake ni akili kisha usikizi na uoni. Ametangulia kutaja usikizi kwa sababu mtoto anayezaliwa huanza kusikia tangu kuzaliwa kwake, wala haoni mpaka siku ya nne; kama wanavyosema. Ama kuchelewa akili hilo liko wazi.

Ni kuchache mno kushukuru kwenu; yaani kutii kwenu.

Yeye ndiye aliyewaumba katika ardhi na kwake mtakusanywa.

Alituuumba katika ardhi hii kisha atatufufua kwake baada ya mauti. Yeye ndiye anayehuisha na kufisha na Yeye ndiye mwenye mabadiliko ya usiku na mchana. Basi je, hamfahamu? Hakika huu ni utengenezaji wa Mwenye uweza aliye Mjuzi. Tazama Juz. 1 (2:28 -29) na Juz. 3: (3:26-27).

بَلْ قَالُوا مِثْلَ مَا قَالَ الْأَوَّلُونَ ﴿٨١﴾

81. Bali walisema kama walivyosema wa mwanzo.

قَالُوا أَإِذَا مِتْنَا وَكُنَّا تُرَابًا وَعِظَامًا أَإِنَّا لَمَبْعُوثُونَ ﴿٨٢﴾

82. Je, tukishakufa tukawa mchanga na mifupa ndio tutafufuliwa?

لَقَدْ وُعِدْنَا نَحْنُ وَآبَاؤُنَا هَـٰذَا مِن قَبْلُ إِنْ هَـٰذَا إِلَّا أَسَاطِيرُ الْأَوَّلِينَ ﴿٨٣﴾

83. Tuliahidiwa haya sisi na baba zetu zamani. Hayakuwa haya ila ni vigano vya wa kale.

قُل لِّمَنِ الْأَرْضُ وَمَن فِيهَا إِن كُنتُمْ تَعْلَمُونَ ﴿٨٤﴾

84. Sema, ni ya nani ardhi na vilivyomo ndani yake, kama nyinyi mnajua?

سَيَقُولُونَ لِلَّـهِ قُلْ أَفَلَا تَذَكَّرُونَ ﴿٨٥﴾

85. Watasema, ni vya Mwenyzi Mungu. Basi je, hamkumbuki?

قُلْ مَن رَّبُّ السَّمَاوَاتِ السَّبْعِ وَرَبُّ الْعَرْشِ الْعَظِيمِ ﴿٨٦﴾

86. Sema, ni nani Mola wa mbingu saba na Mola wa arshi tukufu?

سَيَقُولُونَ لِلَّـهِ قُلْ أَفَلَا تَتَّقُونَ ﴿٨٧﴾

87. Watasema, ni vya Mwenyezi Mungu. Sema, basi je, hamuogopi?

قُلْ مَن بِيَدِهِ مَلَكُوتُ كُلِّ شَيْءٍ وَهُوَ يُجِيرُ وَلَا يُجَارُ عَلَيْهِ إِن كُنتُمْ تَعْلَمُونَ ﴿٨٨﴾

88. Sema, ni nani mkononi mwake umo ufalme wa kila kitu? Na yeye ni mlinzi wala hapalindwi kwake, kama mnajua.

سَيَقُولُونَ لِلَّـهِ قُلْ فَأَنَّىٰ تُسْحَرُونَ ﴿٨٩﴾

89. Watasema, ni wa Mwenyezi Mungu. Sema, basi vipi mnadanganyika?

بَلْ أَتَيْنَاهُم بِالْحَقِّ وَإِنَّهُمْ لَكَاذِبُونَ ﴿٩٠﴾

90. Bali tumewaletea haki. Na kwa hakika wao ni waongo.

WALISEMA KAMA WALIVYOSEMA WA MWANZO

Aya 81 – 90

MAANA

Bali walisema kama walivyosema wa mwanzo.

Waliosema ni washirikina waliokuwa zama za Mtume(s.a.w. w ) . Walikanusha ufufuo, wakatoa sababu mbili:

Kwanza : ni kustaajabu walikokuleta kwa ibara hii:

Je, tukishakufa tukawa mchanga na mifupa ndio tutafufuliwa?

Pili : kwamba wao hawajamuona aliyekufa kisha akarudi kuwa hai. Maana haya yamekusudiwa katika kauli yao:

Tuliahidiwa haya sisi na baba zetu zamani. Hayakuwa haya ila ni vigano vya wa kale.

Yaani tumeyasikia kabla yako ewe Muhammad, pia tuliyasikia kwa wazee wetu, lakini hakujatokea athari yoyote. Ni nani aliyekufa kisha akarudi kutoa habari?

Lau wangelitaamali uumbaji wa kwanza wasingelipinga uumbaji wa pili. Umetangulia mfano wake katika Juz. 13 (13:5) na Juz. 15 (17:49).

Mwenyezi Mungu (s.w.t) amewajadili wapinzani hawa, kwa mfumo wa kielimu wenye hekima, katika Aya tatu zifuatazo:-

1.Sema, ni ya nani ardhi na vilivyomo ndani yake, kama nyinyi mnajua?

Alimwamrisha Mtume wake kuwakabili na swali hili. Kwa sababu wao wanakiri na kukubali kwamba Mwenyezi Mungu ndiye muumba wa ulimwengu, kwa dalili ya kauli yake Mwenyezi Mungu:

Watasema, ni vya Mwenyezi Mungu.

Yaani ardhi na vilivyomo ndani yake ni vya Mwenyezi Mungu; wala hakuna maana ya kuwa ni vyake ila ni kwakuwa ameviumba na kuvianzisha. Ikiwa Mwenyezi Mungu ni muweza wa kuumba ardhi basi vilevile Yeye anaweza kufufua wafu.

Basi je, hamkumbuki na kufikiria hakika hii ambayo ni aliyeweza kuanzisha mara ya kwanza pia anaweza kurudisha mara ya pili? Kila anayeweza kitu, asiyekuwa Mwenyezi Mungu, anashindwa na vingine, anajua vichache na hajui vingi. Lakini Yeye Mwenyezi Mungu ni Muweza na Mjuzi wa kila kitu.

2.Sema, ni nani Mola wa mbingu saba na Mola wa arshi tukufu? Watasema, ni vya Mwenyezi Mungu.

Arshi ni kinaya cha ufalme wake Mwenyezi Mungu Mtukufu na utawala wake. Ambaye mbingu na ardhi ni yake basi ni wepesi kwake kumrudisha aliyekufa humo.

Sema, basi je, hamuogopi ghadhabu za Mwenyezi Mungu na adhabu yake?

Tumezungumzia kuhusu mbingu saba katika Aya 17 ya sura hii

3.Sema, ni nani mkononi mwake umo ufalme wa kila kitu?

Makusudio ya ufalme wa kila kitu ni kuwa kila kitu kinamnyenyekea na kumhitajia Yeye Mwenyezi Mungu Mtukufu na kwamba hahitajii chochote.

Na yeye ni mlinzi wala hapalindwi kwake, kama mnajua.

Yeye ni rehema kwa mwenye kutaka rehema na ni uokovu kwa anayetaka kuokoka; wala hapana mwenye kuweza kumrehemu au kumuokoa yule ambaye anastahiki ghadhabu na adhabu yake.

Watasema: ni wa Mwenyezi Mungu.

Ufalme wa mbingu na ardhi ni wake.

Sema: basi vipi mnadanganyika?

Maadamu mnakubali hayo, basi vipi mnaukana ufufuo na kuhadika na haki?

Bali tumewaletea haki.

Hapana! Hawakudanganyika na haki wala hawakutatizika na batili, baada ya kuwasimamia hoja na dalili zilizo wazi. Na kwa hakika wao ni waongo. Hawakuhadaika isipokuwa wamejitia kuhadaika na kudhihirisha uongo na uzushi. Wao hawakutosheka na ufufuo kwa hoja kwamba dalili zake zimejificha.

Unaweza kuuliza : Imejulikana vipi kwamba wao walikana ufufuo wakiwa na imani nao, na kuna Aya nyingi zimeonyesha mshangao wao na kutojua kwao kukisia uumbaji wa kwanza na ufufuo?

Jibu : Ndio ni kweli, lakini kila ambaye amepatiwa hoja za kutosha zilizo wazi na akaendelea kukataa, ni sawa na yule anayekataa makusudi.

مَا اتَّخَذَ اللَّـهُ مِن وَلَدٍ وَمَا كَانَ مَعَهُ مِنْ إِلَـٰهٍ إِذًا لَّذَهَبَ كُلُّ إِلَـٰهٍ بِمَا خَلَقَ وَلَعَلَا بَعْضُهُمْ عَلَىٰ بَعْضٍ سُبْحَانَ اللَّـهِ عَمَّا يَصِفُونَ ﴿٩١﴾

91. Mwenyezi Mungu hakujifanyia mwana, wala hanaye mungu mwingine. Ingelikuwa hivyo basi kila Mungu angelichukua alivyoviumba. Na baadhi yao wangeliwashinda wengine. Ametakata Mwenyezi Mungu na wanavyomsifu.

عَالِمِ الْغَيْبِ وَالشَّهَادَةِ فَتَعَالَىٰ عَمَّا يُشْرِكُونَ ﴿٩٢﴾

92. Mjuzi wa ghaibu na dhahiri. Ametukuka juu ya hayo wanayomshirikisha nayo.

قُل رَّبِّ إِمَّا تُرِيَنِّي مَا يُوعَدُونَ ﴿٩٣﴾

93. Sema, Mola wangu! Ukinionyesha waliyoahidiwa.

رَبِّ فَلَا تَجْعَلْنِي فِي الْقَوْمِ الظَّالِمِينَ ﴿٩٤﴾

94. Mola wangu usinijaalie katika watu madhalimu.

وَإِنَّا عَلَىٰ أَن نُّرِيَكَ مَا نَعِدُهُمْ لَقَادِرُونَ ﴿٩٥﴾

95. Na hakika sisi ni wenye kuweza kukuonyesha tuliyowaahidi

ادْفَعْ بِالَّتِي هِيَ أَحْسَنُ السَّيِّئَةَ نَحْنُ أَعْلَمُ بِمَا يَصِفُونَ ﴿٩٦﴾

96. Kinga maovu kwa yaliyo mema zaidi. Sisi tunayajua wanayoyasifia.

وَقُل رَّبِّ أَعُوذُ بِكَ مِنْ هَمَزَاتِ الشَّيَاطِينِ ﴿٩٧﴾

97. Na sema, Mola wangu! Najikinga kwako na wasiwasi wa shetani.

وَأَعُوذُ بِكَ رَبِّ أَن يَحْضُرُونِ ﴿٩٨﴾

98. Na ninajilinda kwako wasinikaribie.

حَتَّىٰ إِذَا جَاءَ أَحَدَهُمُ الْمَوْتُ قَالَ رَبِّ ارْجِعُونِ ﴿٩٩﴾

99. Mpaka yanapomfikia mmoja wao mauti, husema: Mola wangu nirudishe.

لَعَلِّي أَعْمَلُ صَالِحًا فِيمَا تَرَكْتُ كَلَّا إِنَّهَا كَلِمَةٌ هُوَ قَائِلُهَا وَمِن وَرَائِهِم بَرْزَخٌ إِلَىٰ يَوْمِ يُبْعَثُونَ ﴿١٠٠﴾

100. Ili nitende mema badala ya yale niliyoyaacha. Wapi! Hii ni kauli aisemayo yeye tu. Na nyuma yao kuna kizuizi mpaka siku watakapofufuliwa.

MJUZI WA GHAIBU NA YALIYO WAZI

Aya 91 -100

MAANA

Mwenyezi Mungu hakujifanyia mwana.

Hana mshirika wala mtoto. Lau angelikuwa na mtoto angelifanana naye. Na Mwenyezi Mungu (s.w.t) hana mfano na chochote.

Wala hanaye mungu mwingine. Ingelikuwa hivyo basi kila Mungu angelichukua alivyoviumba.

Lau ulimwengu ungelikuwa na waumbaji wawili, basi kila mmoja angelihusika na sehemu fulani ya ulimwengu; angelikuwa na mipaka yake nidhamu yake na mambo yake yasiyoafikiana na sehemu nyingine. Kwa kuwa nidhamu ya ulimwengu ni moja na mambo yake ni mamoja, basi muumba wake ni mmoja.

Na baadhi yao wangeliwashinda wengine.

Vile vile lau waumbaji wangelikuwa wengi, hilo lingesababisha kila mmoja kuwa mshindi juu ya mwingine kwa wakati mmoja. Kwa sababu sifa ya Mungu ni kuwa juu ya kila kitu. Yaani kama waungu wangelikuwa wengi basi kungelikuwa na mashindano; kama inavyokuwa kwa watawala. Na huo ndio ufisadi hasa.

Ametakata Mwenyezi Mungu na wanavyomsifu kuwa ana mwana au washirika. Umetangulia ufafanuzi wake katika Juz. 5 (4:50).

Mjuzi wa ghaibu na dhahiri.

Makusudio ya ghaibu ni yale ambayo viumbe hawawezi kuyajua. Na ya dhahiri ni yale ambayo viumbe wanaweza kuyajua. Kwa hakika ilivyo hasa ni kuwa ugawanyo huu unafaa kwa viumbe, sio kwa muumba. Kwa sababu kwake yeye vitu vyote ni sawa kiujuzi na kiuwezo.

Ametukuka juu ya hayo wanayomshirikisha nayo, kutokana na kutowatambua hao washirika. Ikiwa kitu hakitambui muumba maana yake ni kuwa hakiko.

Sema, Mola wangu! Ukinionyesha waliyoahidiwa, Mola wangu usinijaalie katika watu madhalimu.

Mwenyezi Mungu alimwamrisha Mtume wake aombe dua ya kuokoka na ghadhabu na adhabu yake itakayowapata wenye hatia na madhalimu, pamoja na kujua kuwa Mtume(s.a.w. w ) yuko katika amani na salama. Lakini lengo la dua hii ni kuhadharisha watu wa shirk na madhalimu. Mara nyingi waongozaji wanatumia mfumo huu kuonyesha kupingana na yule aliyeghadhibikiwa na Mwenyezi Mungu.

Na hakika sisi ni wenye kuweza kukuonyesha tuliyowaahidi.

Mtume(s.a.w. w ) aliwaonya makuraishi kwa adhabu kama watamkadhibisha na kupinga utume wake, wakacheka na wakafanya masikhara; ndio Mwenyezi Mungu akamwambia Mtume wake Mtukufu kuwa usihuzunike! Sisi tunaweza kukuonyesha maangamizi, lakini tunaahirisha kwa hekima na maslahi yako na ya Uislamu.

Pengine hekima hiyo ni kuwa Mwenyezi Mungu anajua kuwa baadhi yao au baadhi ya watoto wao watamwamini Mwenyezi Mungu na Mtume wake, wawe ni nguvu ya kuusaidia Uislamu na waislamu; kama ilivyotokea hivyo hasa.

KUKINGA MAOVU KWA MEMA ZAIDI

Kinga maovu kwa yaliyo mema zaidi. Sisi tunayajua wanyoyasifia.

Ni nini kukinga kwa kutenda yaliyo mema zaidi? Je, ni kuvumilia maudhi na kumnyamazia anayekuudhi, kama wasemavyo wafasiri wengi?

Kinga inatofautiana kulingana na hali. Inaweza ikawa kutumia nguvu dhidi ya adui ndio kukinga kwa yaliyo mema zaidi. Hapo ni ikiwa aliyechokozwa ana uwezo na ikawa kumnyamazia mchokozi kunamtia mori wa kufanya uovu na uadui. Imam Ali(a.s) anasema: "Kutekeleza ahadi kwa wasio na ahadi ni kuvunja ahadi na kuvunja ahadi kwa wasio na ahadi ni kutekeleza ahadi"

Na inawezekana kuwa kumnyamzia mchokozi ni kinga ya kufanya mema zaidi, ikiwa huko kumnyamazia kutamfanya ajute na atubie au ikiwa aliyechokozwa hana nguvu za kutosha kumzuia mchokozi. Kwani hapo itakuwa ni kujiingiza katika mambo ambayo hayana mwisho mzuri.

Kwa ajili hii Mtume alivumilia maudhi akiwa Makka kwa kutokuwa na uwezo, lakini aliwatia adabu wachokozi baada ya kuhamia Madina na kupata nguvu.

Na sema, Mola wangu! Najikinga kwako na wasiwasi wa shetani, na ninajilinda kwako wasinikaribie.

Ni wazi kuwa shetani hana uwezo wowote kwa Mitume, kwa dalili ya kauli yake Mwenyezi Mungu: "Hakika waja wangu huna mamlaka nao isipokuwa wale wapotofu waliokufuata." Juz. 14 (15:42).

Unaweza kuuliza : Ikiwa shetani hana uwezo wowote kwa Mitume, basi kwa nini Mwenyezi Mungu amemwamrisha Mtume wake kujikinga nao?

Jibu : Kujikinga na kitu hakumaanishi kutowezekana kutokea kwake. Kwani maasumu wanajikinga na ghadhabu na adhabu ya Mwenyezi Mungu zaidi kuliko wengine, pamoja na kuwa wao wako katika amani na salama. Kwa maneno mengine ni kuwa kumkimbilia Mwenyezi Mungu ni dua, na dua inafaa kuwa ni kinga ya uovu na balaa hata kama haiko. Huko nyuma tumeashiria kwamba wacha Mungu mara nyingi wanaonyesha uovu katika dua zao kwa unyenyekevu.

Mpaka yanapomfikia mmoja wao mauti, husema: Mola wangu nirud- ishe ili nitende mema badala ya yale niliyoyaacha.

Wakati alipokuwa na fursa ya kufanya matendo mema aliipoteza na kuipuuza. Baada ya kumfikia mauti ndio anataka kurudia uhai ili afanye amali njema. Hivi ndivyo alivyo kila mzembe, anaipoteza nafasi anapokuwa nayo na inapomtoka huanza kuijutia.

Wapi! Hii ni kauli aisemayo yeye tu.

Hakuna kurejea kabisa! Hata kama mzembe huyu atakubaliwa kurudi mara ya pili atarudia uasi wake. Ama kusema kwake 'ili nitende mema' ni maneno matupu tu yasiyokuwa na maana wala utekelezaji. Hilo amelifafanua Mwenyezi Mungu aliposema: "Na kama wangelirudishwa bila shaka wangeliyarudia yale waliyokatazwa na hakika wao ni waongo" Juz.7 (6:28).

Na nyuma yao kuna kizuizi mpaka siku watakapofufuliwa.

Nyuma yao ni kinaya cha kila upande. Maana ni kuwa wao wametaka kurejea duniani na baina yao na maisha ya dunia kuna kizuizi kitaka-chobaki mpaka siku ya kiyama. Hapo ndio kitaondoka kizuizi, lakini itakuwa ni wakati wa viumbe kusimama mbele ya Mola wao kwa ajili ya hisabu na malipo.