TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA NANE Juzuu 18

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA NANE0%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA NANE Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: Qurani tukufu

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA NANE

Mwandishi: Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya
: HASANI MWALUPA
Kundi:

Matembeleo: 11264
Pakua: 2147


Maelezo zaidi:

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 13 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 11264 / Pakua: 2147
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA NANE

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA NANE Juzuu 18

Mwandishi:
Swahili

5

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA NANE

فَإِذَا نُفِخَ فِي الصُّورِ فَلَا أَنسَابَ بَيْنَهُمْ يَوْمَئِذٍ وَلَا يَتَسَاءَلُونَ ﴿١٠١﴾

101. Basi itakapopuziwa para-panda, hapo hakutakuwa na nasaba baina yao siku hiyo, wala hawataulizana.

فَمَن ثَقُلَتْ مَوَازِينُهُ فَأُولَـٰئِكَ هُمُ الْمُفْلِحُونَ ﴿١٠٢﴾

102. Basi ambao mizani zao zitakua nzito hao ndio wenye kufanikiwa.

وَمَنْ خَفَّتْ مَوَازِينُهُ فَأُولَـٰئِكَ الَّذِينَ خَسِرُوا أَنفُسَهُمْ فِي جَهَنَّمَ خَالِدُونَ ﴿١٠٣﴾

103. Na wale ambao mizani zao zitakuwa nyepesi, hao ndio waliozitia hasara nafsi zao na watadumu katika Jahannam.

تَلْفَحُ وُجُوهَهُمُ النَّارُ وَهُمْ فِيهَا كَالِحُونَ ﴿١٠٤﴾

104. Moto utababua nyuso zao nao humo watakuwa wenye kukunjana.

أَلَمْ تَكُنْ آيَاتِي تُتْلَىٰ عَلَيْكُمْ فَكُنتُم بِهَا تُكَذِّبُونَ ﴿١٠٥﴾

105. Je, hazikuwa Aya zangu mkisomewa na nyinyi mkizikadhibisha?

قَالُوا رَبَّنَا غَلَبَتْ عَلَيْنَا شِقْوَتُنَا وَكُنَّا قَوْمًا ضَالِّينَ ﴿١٠٦﴾

106. Watasema: Mola wetu! Tulizidiwa na uovu wetu na tukawa watu tuliopotea.

رَبَّنَا أَخْرِجْنَا مِنْهَا فَإِنْ عُدْنَا فَإِنَّا ظَالِمُونَ ﴿١٠٧﴾

107. Mola wetu! Tutoe humu motoni. Na tutakaporudia, basi kweli sisi ni wenye kudhulumu.

قَالَ اخْسَئُوا فِيهَا وَلَا تُكَلِّمُونِ ﴿١٠٨﴾

108. Atasema: Tokomeeni humo, wala msinisemeshe.

فَاتَّخَذْتُمُوهُمْ سِخْرِيًّا حَتَّىٰ أَنسَوْكُمْ ذِكْرِي وَكُنتُم مِّنْهُمْ تَضْحَكُونَ ﴿١١٠﴾

110. Hakika lilikuwapo kundi katika waja wangu likisema: Mola wetu tusamehe na uturehemu, na wewe ndiwe mbora wa wanaorehemu.

إِنِّي جَزَيْتُهُمُ الْيَوْمَ بِمَا صَبَرُوا أَنَّهُمْ هُمُ الْفَائِزُونَ ﴿١١١﴾

111. Lakini ninyi mliwafanyia maskhara mpaka wakawasahahulisha kunitaja na mlikuwa mkiwacheka.

قَالَ كَمْ لَبِثْتُمْ فِي الْأَرْضِ عَدَدَ سِنِينَ ﴿١١٢﴾

112. Hakika mimi leo nimewalipa kwa vile walivyosubiri. Hakika hao ndio wenye kufuzu.

HAKUNA UJAMAA BAINA YAO SIKU HIYO

Aya 101 – 111

MAANA

Basi itakapopuziwa parapanda, hapo hakutakuwa na nasaba baina yao siku hiyo, wala hawataulizana.

Kupuziwa parapanda ni kinaya cha kufufuliwa walio katika makaburi. Kutokuweko nasabu maana yake ni kutokuwako kuhurumiana baina ya jamaa na ndugu: "Siku mtakapoiona, kila mwenye kunyonyesha atamsahau amnyonyeshae." Juz. 17 (22: 2).

Siku hiyo hakutakuwa na kitu chochote isipokuwa imani na matendo mema: "Na kila mmoja kati yao atamfikia siku ya Kiyama peke yake. Hakika wale ambao wameamini na wakatenda mema Mwingi wa rehema atawajaalia mapenzi." Juz.16 (19:95-96).

Kuna Hadith isemayo kuwa Mwenyezi Mungu siku ya Kiyama atasema: "Leo ninaziondoa nasaba zenu na ninaweka nasaba yangu, wako wapi wenye takua?

Neno nasaba limetokana na kunasibiana. Neno udugu linafasiriwa kutoka neno la kiarabu Qaraba, lenye maana ya ukaribu. Hakuna ukaribu na Mungu isipokuwa kwa takua. Tazama Juz. 4 (3:199 - 200) kifungu cha 'Takua' Vile vile Juz. 11 (10:5-10) Kifungu 'Wako wapi wacha Mungu.'

Basi ambao mizani zao zitakua nzito hao ndio wenye kufanikiwa. Na wale ambao mizani zao zitakuwa nyepesi, hao ndio waliozitia hasara nafsi zao na watadumu katika Jahannam.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 8 (7:8) kifungu 'Mizani ya matendo.' Vilevile tumeizungumzia mara ya pili mizani hii katika Juz. 17 (21:47) kifungu 'mizani siku ya Kiyama.'

Moto utababua nyuso zao nao humo watakuwa wenye kukunjana.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) ameleta ibara ya uso kwa niaba ya mwili wote, kwa sababu uso ndio kiungo kizuri zaidi.

Imepokewa Hadith kutoka kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu kwamba yeye amesema: "Moto utababua nyuso zao, ni mbabuo utakaoenea hadi kwenye visigino vyao.

Je, hazikuwa Aya zangu mkisomewa na nyinyi mkizikadhibisha?

Huku ni kusutwa, kwa kukadhibisha kwao hoja za Mwenyezi Mungu na ubainifu wake.

Watasema: Mola wetu! Tulizidiwa na uovu wetu na tukawa watu tuliopotea.

Wanakiri dhambi zao baada ya kukatikiwa na kufungwa mlango wa toba! Umetangulia mfano wake katika Juz. Juz. 8 (7:5) na Juz. 17 (21:14).

Mola wetu! Tutoe humu motoni. Na tutakaporudia, basi kweli sisi ni wenye kudhulumu.

Watayasema haya baada ya kudhihiri hukumu na baada ya kuwathibitikia uhakika. Hapo mwanzo walikuwa wamezama katika uasi wao. Ndio maana Mwenyezi Mungu atasema:

Tokomeeni humo, wala msinisemeshe.

Ni maneno yakukemewa mbwa hayo ambayo yamedhihirisha ghadhabu za Mwenyezi Mungu.

Hakika lilikuwapo kundi katika waja wangu likisema: Mola wetu tusamehe na uturehemu, na wewe ndiwe mbora wa wanaorehemu. Lakini ninyi mliwafanyia maskhara mpaka wakawasahahulisha kunitaja na mlikuwa mkiwacheka.

Baada ya kuwasuta wakosefu na kuwakemea, hapa anawabainishia kwamba wao walikuwa wakiwafanyia kejeli na kuwacheka waja wema wa Mwenyezi Mungu ambao wanataka maghufira na rehema kutoka kwa Mola wao, kiasi ambacho kejeli ziliwafanya wamsahau Mungu.

Hakika mimi leo nimewalipa kwa vile walivyosubiri. Hakika hao ndio wenye kufuzu.

Waumini walivumilia maudhi ya wakosefu, ndio Mwenyezi Mungu akawaneemesha hawa na akawaadhibu hao.

فَالْيَوْمَ الَّذِينَ آمَنُوا مِنَ الْكُفَّارِ يَضْحَكُونَ ﴿٣٤﴾

"Basi hivi leo wale ambao wameamini wanawacheka makafiri." (83:34).

قَالَ كَمْ لَبِثْتُمْ فِي الْأَرْضِ عَدَدَ سِنِينَ ﴿١١٢﴾

112. Atasema: Mlikaa muda gani katika ardhi kwa idadi ya miaka?

قَالُوا لَبِثْنَا يَوْمًا أَوْ بَعْضَ يَوْمٍ فَاسْأَلِ الْعَادِّينَ ﴿١١٣﴾

Watasema: Tumekaa siku moja au sehemu ya siku, basi waulize wanaoweka hisabu.

قَالَ إِن لَّبِثْتُمْ إِلَّا قَلِيلًا لَّوْ أَنَّكُمْ كُنتُمْ تَعْلَمُونَ ﴿١١٤﴾

114. Atasema: Hamkukaa ila kidogo, laiti mngelikuwa mnajua.

أَفَحَسِبْتُمْ أَنَّمَا خَلَقْنَاكُمْ عَبَثًا وَأَنَّكُمْ إِلَيْنَا لَا تُرْجَعُونَ ﴿١١٥﴾

115. Je, mnadhani kuwa tuliwaumba bure na kwamba nyinyi kwetu hamtarudishwa?

فَتَعَالَى اللَّـهُ الْمَلِكُ الْحَقُّ لَا إِلَـٰهَ إِلَّا هُوَ رَبُّ الْعَرْشِ الْكَرِيمِ ﴿١١٦﴾

116. Ametukuka Mwenyezi Mungu, Mfalme wa haki. Hapana mungu ila Yeye, Mola wa Arshi tukufu.

وَمَن يَدْعُ مَعَ اللَّـهِ إِلَـٰهًا آخَرَ لَا بُرْهَانَ لَهُ بِهِ فَإِنَّمَا حِسَابُهُ عِندَ رَبِّهِ إِنَّهُ لَا يُفْلِحُ الْكَافِرُونَ ﴿١١٧﴾

117. Na anayemuomba - pamoja na Mwenyezi Mungu - mungu mwingine, hana dalili ya hilo. Basi hakika hisabu yake iko kwa Mola wake. Kwa hakika makafiri hawafanikiwi.

وَقُل رَّبِّ اغْفِرْ وَارْحَمْ وَأَنتَ خَيْرُ الرَّاحِمِينَ ﴿١١٨﴾

118. Na sema: Mola wangu! Ghufiria na rehemu nawe ni Mbora wa wanaorehemu.

MLIKAA MUDA GANI KATIKA ARDHI

Aya 112 – 118

MAANA

Atasema: Mlikaa muda gani katika ardhi kwa idadi ya miaka?

Atakayesema ni Mwenyezi Mungu au malaika atakayeamriwa kuuliza kesho, wanaombiwa ni wale waliokana ufufuo na muda wanoulizwa ni ule walioumaliza katika kufuru duniani. Lengo la swali hili ni kuwasuta na kuwatahayariza kutokana na kuipinga kwao siku hiyo na kuwakejeli wale waliokuwa wakiwaonya na vituko vya siku hiyo na adhabu yake.

Watasema: tumekaa siku moja au sehemu ya siku, basi waulize wanaoweka hisabu.

Wapi sisi na swali hili? Tuliyonayo yanatutosha. Ikiwa hakuna budi na kujibu basi tumekaa masaa tu. Wanaojua zaidi ni wale waliokuwa wakiudhibiti umri wetu na matendo yetu ambao hawaachi dogo wala kubwa, lakini sisi hatuna tujualo. Umetangulia mfano wake katika Juz. 16 (20:103).

Atasema: Hamkukaa ila kidogo, laiti mngelikuwa mnajua.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) anawaambia mmekaa miaka, sio siku moja kama mnavyosema, lakini miaka ni michache kwa vile inaisha, na kila chenye kuisha ni kichache hata kama kitakaa muda mrefu. Laiti mngelijua hakika hii mlipokuwa duniani, mkaiamini siku hii na mkajiandaa nayo, basi leo mngelikuwa kwenye amani na salama, lakini mlikufuru, ikawathibitia adhabu.

Je, mnadhani kuwa tuliwaumba bure na kwamba nyinyi kwetu hamtarudishwa?

Kwa dhahiri maneno yanaelekezwa kwa wale wanaokana ufufuo, lakini kwa uhalisi yanaelekezwa kwa kila muasi na mfisadi; ni sawa awe amepinga ufufuo tangu mwanzo au aliuamini na asiufanyie kazi.

Bure ni kisicho na faida wala hekima ya kuwako kwake. Mwenyezi Mungu (s.w.t) ameepukana na kufanya mambo bure.

Lau mtu asingefufuliwa baada ya mauti, akajulikana mwema na muovu na kulipwa kila mmoja anavyostahiki, ingelikuwa kuumbwa mtu ni bure tu kusiko na faida yoyote.

Ametukuka Mwenyezi Mungu, Mfalme wa haki.

Mfalme ina maana ya muweza mwenye nguvu. Na haki inaondoa batili na bure. Ikiwa haki ndio iliomuumba mtu, itakuwaje kumbwa kwake kuwe bure? Au vipi imuwache bure bila ya taklifa yoyote na hisabu au bila ya swali na jawabu la wema au uovu alioufanya?

Hapana mungu ila Yeye, Mola wa Arshi tukufu.

Yeye ni mmoja katika ufalme wa ulimwengu bila ya mshirika katika kuumba kwake, kupangilia kwake, elimu yake na hekima yake. Basi kuumbwa mtu na asiyekuwa mtu burebure na ufisadi utatoka wapi?

Na anayemuomba - pamoja na Mwenyezi Mungu - mungu mwingine, hana dalili ya hilo.

Ataitoa wapi dalili ya ushirika na kila kitu kinafahamisha kuwa Mungu ni mmoja. Inatosha kuwa ni dalili ya umoja wake nidhamu ya ulimwengu huu ambayo haina kombo wala kuharibika, hakuna anayeweza kupinga hakika hii isipokuwa yule anayepinga misingi ya dhahiri na akakataa dalili zote. Mfano wa mtu huyu ni ni kupuuzwa wala hajadiliwi.

Basi hakika hisabu yake iko kwa Mola wake, naye ndiye atakayemlipa anayostahiki. Kwa hakika makafiri hawafanikiwi, kwa sababu wameiacha njia.

Kama alivyoifungua Mwenyezi Mungu (s.w.t) sura hii kwa kusema: "Hakika wamefaulu waumini." basi anaiishilizia hivyo hivyo.

Na sema: Mola wangu! Ghufiria na rehemu nawe ni Mbora wa wanaorehemu.

Yeye peke yake ndiye anayeombwa kutukunjulia kwa rehema zake na maghufira yake, wala asikate matarajio yetu ya kuneemeshwa na neema zake na ukarimu wake, kwa jaha ya Mtume na kizazi chake, rehema za Mwenyezi Mungu zimshukie yeye na kila mwenye kufuata mwenendo wake.

Mwisho Wa Sura Ya Ishirini Na Tatu

6

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA NANE

Sura Ya Ishirini Na Nne: Surat Nuru.

Razi amesema yote imeshuka Madina, na Tabrasi akasema bila ya kutofautiana. Ina Aya 64

بِسْمِ اللَّهِ الرَّحْمَٰنِ الرَّحِيمِ

Kwa jina la Mwenyezi Mungu Mwingi wa rehema Mwenye kurehemu

سُورَةٌ أَنزَلْنَاهَا وَفَرَضْنَاهَا وَأَنزَلْنَا فِيهَا آيَاتٍ بَيِّنَاتٍ لَّعَلَّكُمْ تَذَكَّرُونَ ﴿١﴾

1. Ni Sura tuliyoiteremsha na tukailazimisha na tukateremsha ndani yake Aya zilizo wazi, ili mkumbuke.

الزَّانِيَةُ وَالزَّانِي فَاجْلِدُوا كُلَّ وَاحِدٍ مِّنْهُمَا مِائَةَ جَلْدَةٍ وَلَا تَأْخُذْكُم بِهِمَا رَأْفَةٌ فِي دِينِ اللَّـهِ إِن كُنتُمْ تُؤْمِنُونَ بِاللَّـهِ وَالْيَوْمِ الْآخِرِ وَلْيَشْهَدْ عَذَابَهُمَا طَائِفَةٌ مِّنَ الْمُؤْمِنِينَ ﴿٢﴾

2. Mzinifu mwanamke na mzinifu mwanamume mtandikeni kila mmoja wao viboko mia. Wala isiwashike huruma kwa ajili yao katika dini ya Mwenyezi Mungu, ikiwa nyinyi mnamuamini Mwenyezi Mungu na siku ya mwisho. Na lishuhudie adhabu yao kundi la waumini.

الزَّانِي لَا يَنكِحُ إِلَّا زَانِيَةً أَوْ مُشْرِكَةً وَالزَّانِيَةُ لَا يَنكِحُهَا إِلَّا زَانٍ أَوْ مُشْرِكٌ وَحُرِّمَ ذَٰلِكَ عَلَى الْمُؤْمِنِينَ ﴿٣﴾

3. Mwanamume mzinifu hamwoi ila mwanamke mzinifu au mwanamke mshirikina. Na mwanamke mzinifu haolewi ila na mwanamume mzinifu au mwanamume mshirikina. Na hayo yameharamishwa kwa waumini.

وَالَّذِينَ يَرْمُونَ الْمُحْصَنَاتِ ثُمَّ لَمْ يَأْتُوا بِأَرْبَعَةِ شُهَدَاءَ فَاجْلِدُوهُمْ ثَمَانِينَ جَلْدَةً وَلَا تَقْبَلُوا لَهُمْ شَهَادَةً أَبَدًا وَأُولَـٰئِكَ هُمُ الْفَاسِقُونَ ﴿٤﴾

4. Na wale ambao wanawasingizia wanawake wanaoheshimika kisha wasilete mashahidi wane, basi watandikeni viboko thamanini. Na msiwakubalie ushahidi wao tena. Na hao ndio mafasiki.

إِلَّا الَّذِينَ تَابُوا مِن بَعْدِ ذَٰلِكَ وَأَصْلَحُوا فَإِنَّ اللَّـهَ غَفُورٌ رَّحِيمٌ ﴿٥﴾

5. Isipokuwa wale waliotubia baada ya hayo na wakatengenea; kwani hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye kughufiria, Mwenye kurehemu.

HUKUMU YA MZINIFU NA MWENYE KUTUSI

Aya 1 – 5

MAANA

Ni Sura tuliyoiteremsha na tukailazimisha na tukateremsha ndani yake Aya zilizo wazi.

Mwenyezi Mungu alimtereshia Mtume wake mtukufu sura hii, ndani yake mkiwa na mafunzo aliyowajibisha kuyatumia kila mukallaf. Kwa sababu yanalenga kujenga jamii ya binadamu kwa ukamilifu kwa manufaa yake na maendeleo yake.

Mafunzo haya yako waziwazi yasiyohitajia ubishi wala mjadala katika malengo yake ya kumlinda mtu na ufisadi na upotevu. Kwa ajili hii au nyingine ndio ikaitwa Sura ya nuru. Na Qur'an yote ni uongofu na nuru.

Ili mkumbuke.

Mwenyezi Mungu ameteremsha Sura hii iliyo wazi wazi ili mjue na muitumie.

Mzinifu mwanamke na mzinifu mwanamume mtandikeni kila mmoja wao viboko mia.

Maneno yanaelekezwa kwa yule atakayetekeleza adhabu (hadd), ambaye ni Imam au naibu wake mwenye ujuzi na mwadilifu.

Dhahiri ya Aya inaonyesha kuwa mwenye kuzini atapigwa vibogo awe muhsan au asiyekuwa muhsan. Kwa sababu herufi lam ya jinsiya ikiingia katika nomino pekee, inafahamisha kuenea aina zote.

Muhsan ni yule aliye baleghe na akili timamu akiwa na mke anayemtosheleza wakati wowote akitaka kumjamii. Ikiwa atajamii akiwa ni mtoto au mwenda wazimu, au akiwa ni mseja au ana mke, lakini yuko mbali naye au yuko karibu naye lakini ana maradhi ya kushindwa kumjamii, basi huyo siye muhsan. Vile vile mwanamke.

Imam Abu Jafar Swadiq(a.s ) aliulizwa kuhusu muhsan,akasema: ambaye ana tupu anayoweza kuiendea basi huyo ni muhsan.

Hivi ndivyo ilivyofahamisha dhahiri ya Aya, kwamba mzinifu muhasn na asiyekuwa muhsan watandikwe viboko mia. Lakini imethibiti kwa Hadith mutawatir na kongamano la madhehbu zote za kiislamu kwamba hukumu ya muhsan ni kupigwa mpaka kufa. Kwa hiyo hukumu ya viboko ni ya asiyekuwa muhsan.

Bali imekuja Hadith katika Sahih Bukhari kwamba Umar bin Al-khattwab alisema: "Hakika Mwenyezi Mungu alimtuma Muhammad kwa haki na akamteremshia Kitabu kwa haki, katika aliyoyateremsha ni Aya ya kurujumu (kupiga mawe) tukaisoma na tukaitia akilini na tukaihifadhi."

Rejea Bukhari Juz. 8 Uk. 209 chapa ya kiarabu ya mwaka 1377 A.H. Na Muslim Juz. 2, sehemu ya kwanza Uk. 107 chapa ya kiarabu ya mwaka 1348 A.H. Katika riwaya nyingine ya Bukhari Juz. 9 Uk. 86, Umar alisema: "Lau si kuwa watu watasema Umar amezidisha katika Kitabu cha Mwenyezi Mungu, ningeliiandika kwa mkono wangu Aya ya kurujumu."

Unaweza kuuliza : Mwenyezi Mungu mahali pengine anasema: " Juz. 4 (15:4). Katika Aya hii Mwenyezi Mungu amewajibisha mzinifu mwanamke afungiwe nyumbani wala asitoke mpaka afe au Mwenyezi Mungu amjaalie njia nyingine; kisha katika Aya tuliyo nayo Mwenyezi Mungu amewajibisha viboko. Sasa kuna njia gani ya kuchanganya Aya mbili hizi?

Jibu : Kwenye Juz.4 tulisema kwamba makusudio ya kauli yake Mwenyezi Mungu au 'awajaalie njia' ni kwamba yeye Mwenyezi Mungu Mtukufu hakujaalia adhabu ya kufungiwa nyumbani ni ya daima, bali ni kwa muda fulani, kisha alete hukumu ya kudumu. Ndivyo ilivyokuwa, ambapo iliondolewa adhabu ya kufungwa nyumbani na mahali pake pakachukuliwa na adhabu ya viboko au kurujumiwa.

Baadhi ya ulama wanasema kuwa hatuwezi kukimbilia kufutwa hukumu mpaka kupatikane nukuu ya kufuta hukumu hiyo au iwe haiwezekani kutumia nukuu mbili. Inavyochukuliwa ni kuwa sharia haikuleta nukuu ya kufuta hukumu hiyo na kwamba kuzichanganya nukuu mbili ni jambo lisilo na uzito, basi inafaa kuzitumia Aya zote mbili, kwamba mzinifu apigwe viboko na pia afungiwe nyumbani vile vile.

Sisi tunaweza kukubaliana na anayesema hivi ikiwa atatukinaisha kuwa makusudio ya 'njia' ni kitu kingine kisichokuwa hukumu ya kudumu ambayo ndiyo inayofahamika mwanzo. Ama kufasiri njia kwa maana ya ndoa, kama alivyosema mwenye fikra hii, hiyo iko mbali na ufahamu.

Wala isiwashike huruma kwa ajili yao katika dini ya Mwenyezi Mungu.

Msicheleweshe hukumu ya mzinifu mwanamume na mzinifu mwanamke, bali mutekeleze wala isiwazuie huruma. Kwa sababu hakuna kuhurumiana katika dini ya Mwenyezi Mungu. Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w. w ) amesema:"Lau Fatima ataiba nitamkata mkono wake." Katika Nahjul-bal- agha, imeelezwa: "Mwenyezi Mungu amefaradhisha kisasi kuhifadhi damu na ameweka adhabu kuheshimu miko."

Ikiwa nyinyi mnamuamini Mwenyezi Mungu na siku ya mwisho.

Huu ni msisitizo na himizo la kutekeleza adhabu na kwamba kuipuuza ni kudharau dini.

Na lishuhudie adhabu yao kundi la waumini.

Lengo la hilo ni kuenea tukio la adhabu kwa watu ili wapate kuonyeka na wakome. Imesemekana kuwa uchache wa kuitwa kundi ni watu watatu, wengine wakasema hata mmoja pia, kwa dalili ya kauli yake Mwenyezi Mungu: "Na ikiwa makundi mawili katika waumini.." (49:9).

Tumezungumzia kwa ufafanuzi kuhusu maelezo ya zina, masharti yake, mafungu yake, njia za kuithibitisha, adhabu na utekelezaji wake, toba yamzinifu na mengineyo waliyoyaeleza mafaqihi, katika kitabu Fiqhul-Imam Ja'farus swadiq(a.s) Juz. 6.

Mwanamume mzinifu hamwoi ila mwanamke mzinifu au mwanamke mshirikina. Na mwanamke mzinifu haolewi ila na mwanamume mzinifu au mwanamume mshirikina.

Imesemkana kuwa Aya hii ni miongoni mwa zenye kutatiza. Kwa sababu dhahiri yake inaonyesha kuwa mwanamume mzinifu haoi ila mzinifu au mshirikina. Vile vile mwanamke; pamoja na kwamba mzinifu huwa anamuoa mwanamke msafi aliye mtukufu.

Vile vile mwanamke mzinifu huwa anaolewa na mwanamume msafi aliye mtukufu. Sasa imekuwaje dhahiri ya Aya ikawa kinyume na hali halisi ya mambo?

Tuonavyo sisi Aya hii iko wazi kabisa. Kwa sababu yenyewe sio kuwa inaleta habari ya hali halisi ya mambo ilivyo, wala sio hukumu ya sharia ya kumlazimisha mzinifu aoe mzinifu mwenzake au mshirikina; kama walivyodai wafasiri wengi. Hapana sivyo kabisa! Kwa sababu Mwislamu haruhusiwi kumuoa mshirikina hata kama imethibiti zina juu yake. Vile vile mwanamke Mwislamu haruhusiwi kuolewa na mshirikina hata kama amezini.

Kwa hiyo hayo siyo makusudio yake; isipokuwa maana yake - bila ya kuangalia sababu iliyoshukia - ni kuwa zina ni jambo ovu na la fedheha kabisa, haifanyi ila malaya muovu.

Akitaka kuzini mtu basi atapata aliye mfano wake katika uovu. Malaya ni wa malaya. Kwa ufupi ni kuwa maana ya Aya yanafanana na kusema: Hakuna anayekubaliana na kosa lako ila mkosa kama wewe ambaye hana dini wala dhamiri. Sasa ni wapi na wapi haya na kuleta hukumu ya sharia?

Kauli yake Mwenyezi Mungu 'Au mshirkina' ni kuashiria kwamba zina iko kwenye daraja ya ushirikina. Mwenyezi Mugu amelinganisha sawa hukumu ya shirk, kuua na kuzini, pale aliposema: "Na wale wasiomwomba mungu mwengine pamoja na Mwenyezi Mungu, wala hawaui nafsi aliyoiharamisha Mwenyezi Mungu ila kwa haki, wala hawazini na mwenye kufanya hivyo atapata madhambi' (25:68). Mtume(s.a.w .w ) aliulizwa kuhusu madhambi makubwa, akataja haya matatu.

Na hayo yameharamishwa kwa waumini. Hayo ni hayo ya Kuzini. Na wale ambao wanawasingizia wanawake wanaoheshimika, kisha wasilete mashahidi wane, basi watandikeni viboko thamanini.

Makusudio ya kusingizia hapa ni kusingizia zina. Neno la kiarabu, lililofasiriwa 'ambao,' lina dhamiri ya wanaume, lakini wanakusudiwa wote. Makusudio ya wanaoheshimika hapa ni wale wanawake wasafi wanaojichunga na zina; ni sawa wawe wameolewa au la. Ulama wamelinganisha hukumu ya mwanamume sawa na mwanamke. Kwa maneno mengine ni kuwa hukumu ya kutandika viboko inamuhusu mwanamume na mwanamke.

Msingiziaji mwanamume au mwanamke atatandikwa ikiwa hakuleta mashahidi wane walioshuhudia uingiaji wa tupu na utokaji wake, kama kinavyoingia kijiti cha wanja kwenye kichupa chake. Lengo la mkazo huu na mashahidi wengi ni kulinda familia zisitawanyike kwa kusingiziana.

Na msiwakubalie ushahidi wao tena. Na hao ndio mafasiki. Isipokuwa wale waliotubia baada ya hayo na wakatengenea; kwani hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye kughufiria, Mwenye kurehemu.

Wanaelzewa wale wenye kuisingizia. Maana ni kuwa mwenye kumsingizia mwenye kujichunga na asithibishe kwa ushahidi, basi huyo ni fasiki, ushahidi wake haukubaliwi kabisa kwenye jambo lolote, ila baada ya kutubia na kufanya mambo mema. Akishatubia na akawa na sera nzuri, basi ushahidi wake utakubaliwa; ni sawa awe ametubia baada ya adhabu au kabla.

Abu Hanifa anasema: "Ushahidi wake haukubaliki kabisa hata akitubia, kwa sababu kukataliwa kwake ni miongoni mwa adhabu na kutiwa adabu..." Lakini huku ni kutatizika.

Kwa sababu kauli yake Mwnyezi Mungu, 'Hakika Mwenyezi Mungu ni mwenye kughufiria Mwenye kurehemu,' iliyokuja moja kwa moja inaashiria kukubaliwa kwake hata kama ametubia baada ya adhabu. Inayofafanua zaidi Aya hii ni kauli ya Mtume(s.a.w. w ) :"Mwenye kutubia dhambi ni kama asiye na dhambi."

وَالَّذِينَ يَرْمُونَ أَزْوَاجَهُمْ وَلَمْ يَكُن لَّهُمْ شُهَدَاءُ إِلَّا أَنفُسُهُمْ فَشَهَادَةُ أَحَدِهِمْ أَرْبَعُ شَهَادَاتٍ بِاللَّـهِ إِنَّهُ لَمِنَ الصَّادِقِينَ ﴿٦﴾

6. Na wale wanaowasingizia wake zao na hawana mashahidi ila nafsi zao, basi ushahidi wa mmoja wao utakuwa kushuhudia mara nne kwa kiapo cha Mwenyezi Mungu ya kwamba hakika yeye ni katika wasema kweli.

وَالْخَامِسَةُ أَنَّ لَعْنَتَ اللَّـهِ عَلَيْهِ إِن كَانَ مِنَ الْكَاذِبِينَ ﴿٧﴾

7. Na mara ya tano kwamba laana ya Mwenyezi Mungu iwe juu yake ikiwa ni miongoni mwa waongo.

وَيَدْرَأُ عَنْهَا الْعَذَابَ أَن تَشْهَدَ أَرْبَعَ شَهَادَاتٍ بِاللَّـهِ إِنَّهُ لَمِنَ الْكَاذِبِينَ ﴿٨﴾

8. Na mke itamwondokea adhabu kwa kutoa shahada mara nne kwa kiapo cha Mwenyezi Mungu, kwamba huyo mume ni miongoni mwa waongo.

وَالْخَامِسَةَ أَنَّ غَضَبَ اللَّـهِ عَلَيْهَا إِن كَانَ مِنَ الصَّادِقِينَ ﴿٩﴾

9. Na mara ya tano kwamba ghadhabu ya Mwenyezi Mungu iwe juu yake, kama mume ni miongoni mwa wasemao kweli.

وَلَوْلَا فَضْلُ اللَّـهِ عَلَيْكُمْ وَرَحْمَتُهُ وَأَنَّ اللَّـهَ تَوَّابٌ حَكِيمٌ ﴿١٠﴾

10. Na lau kuwa si fadhila za Mwenyezi Mungu juu yenu na rehema yake, na kwamba Mwenyezi Mungu ni Mwenye kutakabali toba, Mwenye hekima.

KUAPIZANA MUME NA MKE

Aya 6-10

MAANA

Katika vitabu vya Fiqh kuna mlango unaoitwa Lian, ambao chimbuko lake ni Aya hizi. Inafanana na kuapizana baina ya mume anayemtuhumu mkewe na zina bila ya kuwa na ushahidi wa madai yake, na mke kuikana tuhuma ya zina yeye mwenyewe. Lengo la kulaniana huku ni kuondoka adhabu ya kutuhumu au kumkana mtoto. Liani haiwi ila katika hali mbili:

Kwanza : Mtu kumtuhumu na zina mkewe wa kisharia aliyemuoa kwa ndoa ya daima. Ni lazima mke awe si kiziwi wala bubu, mume adai kushuhudia na asiwe na ubainifu wa kisharia juu ya hiyo zina, zikikosekana sharti hizi basi haijuzu kulaniana.

Pili : Kumkana mume mtoto wa kitanda chake, ikiwa mimba haikupungua miezi sita au kuzidi mwaka. Vinginevyo anaweza kumkana mtoto bila ya kulaniana.

Basi ikiwa mume atamtuhumu mkewe na zina au kumkana mtoto,anatakikana apate adhabu (had) ya kutukana, ila akileta ushahidi au kulaniana.

Sura ya kulaniana ni kusema mbele ya hakimu wa sharia: Ninashuduia kuwa mimi ni mkweli kwa ninayoyasema kuhusu mke wangu fulani. Atasema hivyo mara nne; kisha atasema mara ya tano baada ya kuonywa na hakimu wa sharia: Laana ya Mwenyezi Mungu iwe juu yangu ikiwa ni muongo.

Mke naye atashuhudia mara nne kwamba huyo mume ni muongo kwa aliyomtuhumu nayo. Mara ya tano atasema ghadhabu za Mwenyezi Mungu zimshukie ikiwa huyo mume ni mkweli.

Ni lazima wote wawili wawe wamekaa wakati wa kulaniana. Kukishatimia kulaniana kwa masharti yake, matokeo yatakuwa ni mambo yafuatayo:-

1. Ndoa itavunjika.

2. Uharamu wa milele baina ya mume na mke (hawawezi kurudiana tena).

3. Adhabu ya kutuhumu itaondoka kwa mume.

4. Mtoto hatakuwa wa mume. Hawatarithiana wala halazimiki kumtunza. Lakini atakuwa ni wa mama kisharia.

Tukijua kulaniana baina ya mume na mke, itakuwa tumejua makusudio ya Aya hizi. Kwa hiyo basi tutafupiliza kufasiri kwa kutaja matamko yanayoashiriwa na mfumo wa maneno.

Na wale wanaowasingizia wake zao kwa zina na hawana mashahidi ila nafsi zao kutokana na madai yao, basi ushahidi wa mmoja wao utakuwa kushuhudia mara nne kwa kiapo cha Mwenyezi Mungu ya kwamba hakika yeye ni katika wasema kweli.

Atayasema hayo mbele ya hakimu wa sharia.

Na mara ya tano kwamba laana ya Mwenyezi Mungu iwe juu yake ikiwa ni miongoni mwa waongo.

Yaani ikiwa ni muongo katika madai yake. Na mke itamwondokea adhabu kwa kutoa shahada mara nne kwa kiapo cha Mwenyezi Mungu, kwamba huyo mume ni miongoni mwa waongo. Mke naye atatoa ushahidi wake mbele ya hakimu wa sharia kama alivyofanya mume.

Na mara ya tano kwamba ghadhabu ya Mwenyezi Mungu iwe juu yake, kama mume ni miongoni mwa wasemao kweli katika haya madai yake kwangu. Na lau kuwa si fadhila za Mwenyezi Mungu juu yenu na rehema yake mngeliangamia. Na kwamba Mwenyezi Mungu ni Mwenye kutakabali, toba Mwenye hekima.

Hii ni kuashria hekima ya sharia ya kuapizana, kwamba lengo ni kusitiri na kuondoa adhabu kwa mume na kutoa nafasi kwa mke kujitetea na tuhumu za mume.