TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA NANE Juzuu 18

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA NANE0%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA NANE Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: Qurani tukufu

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA NANE

Mwandishi: Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya
: HASANI MWALUPA
Kundi:

Matembeleo: 11226
Pakua: 2133


Maelezo zaidi:

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 13 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 11226 / Pakua: 2133
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA NANE

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA NANE Juzuu 18

Mwandishi:
Swahili

7

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA NANE

إِنَّ الَّذِينَ جَاءُوا بِالْإِفْكِ عُصْبَةٌ مِّنكُمْ لَا تَحْسَبُوهُ شَرًّا لَّكُم بَلْ هُوَ خَيْرٌ لَّكُمْ لِكُلِّ امْرِئٍ مِّنْهُم مَّا اكْتَسَبَ مِنَ الْإِثْمِ وَالَّذِي تَوَلَّىٰ كِبْرَهُ مِنْهُمْ لَهُ عَذَابٌ عَظِيمٌ ﴿١١﴾

11. Hakika wale walioleta uzushi ni kundi miongoni mwenu. Msiufikirie ni shari kwenu, bali hiyo ni kheri kwenu. Kila mmoja katika wao atapata aliyoyachuma katika madhambi. Na yule aliyejitwika sehemu yake kubwa miongoni mwao atapata adhabu kubwa.

لَّوْلَا إِذْ سَمِعْتُمُوهُ ظَنَّ الْمُؤْمِنُونَ وَالْمُؤْمِنَاتُ بِأَنفُسِهِمْ خَيْرًا وَقَالُوا هَـٰذَا إِفْكٌ مُّبِينٌ ﴿١٢﴾

12. Mbona mlipousikia, waumini wanaume na waumini wanawake hawakujidhania mema na kusema huu ni uzushi dhahiri?

لَّوْلَا جَاءُوا عَلَيْهِ بِأَرْبَعَةِ شُهَدَاءَ فَإِذْ لَمْ يَأْتُوا بِالشُّهَدَاءِ فَأُولَـٰئِكَ عِندَ اللَّـهِ هُمُ الْكَاذِبُونَ ﴿١٣﴾

13. Mbona hawakuleta mashahidi wane. Na kwa kutoleta mashahidi, basi hao mbele ya Mwenyezi Mungu ni waongo

وَلَوْلَا فَضْلُ اللَّـهِ عَلَيْكُمْ وَرَحْمَتُهُ فِي الدُّنْيَا وَالْآخِرَةِ لَمَسَّكُمْ فِي مَا أَفَضْتُمْ فِيهِ عَذَابٌ عَظِيمٌ ﴿١٤﴾

14. Na lau si fadhila ya Mwenyezi Mungu juu yenu na rehema yake katika dunia na akhera, bila shaka ingeliwapata adhabu kubwa kwa sababu ya yale mliyojiingiza.

إِذْ تَلَقَّوْنَهُ بِأَلْسِنَتِكُمْ وَتَقُولُونَ بِأَفْوَاهِكُم مَّا لَيْسَ لَكُم بِهِ عِلْمٌ وَتَحْسَبُونَهُ هَيِّنًا وَهُوَ عِندَ اللَّـهِ عَظِيمٌ ﴿١٥﴾

15. Mlipoyapokea kwa ndimi zenu na mkasema kwa vinywa vyenu msiyoyajua, na mkifikiri ni dogo kumbe kwa Mwenyezi Mungu ni kubwa.

وَلَوْلَا إِذْ سَمِعْتُمُوهُ قُلْتُم مَّا يَكُونُ لَنَا أَن نَّتَكَلَّمَ بِهَـٰذَا سُبْحَانَكَ هَـٰذَا بُهْتَانٌ عَظِيمٌ ﴿١٦﴾

16. Na mbona mliposikia msiseme: Haitufalii kuzungumza haya; utakatifu ni wako! Huu ni uzushi mkubwa.

يَعِظُكُمُ اللَّـهُ أَن تَعُودُوا لِمِثْلِهِ أَبَدًا إِن كُنتُم مُّؤْمِنِينَ ﴿١٧﴾

17. Mwenyezi Mungu anawaonya msirudie kufanya kama haya kabisa ikiwa nyinyi ni waumini.

وَيُبَيِّنُ اللَّـهُ لَكُمُ الْآيَاتِ وَاللَّـهُ عَلِيمٌ حَكِيمٌ ﴿١٨﴾

18. Na Mwenyezi Mungu anawabainishia Aya na Mwenyezi Mungu ni Mjuzi, Mwenye hekima.

إِنَّ الَّذِينَ يُحِبُّونَ أَن تَشِيعَ الْفَاحِشَةُ فِي الَّذِينَ آمَنُوا لَهُمْ عَذَابٌ أَلِيمٌ فِي الدُّنْيَا وَالْآخِرَةِ وَاللَّـهُ يَعْلَمُ وَأَنتُمْ لَا تَعْلَمُونَ ﴿١٩﴾

19. Hakika wale ambao wanapenda kueneza uchafu kwa waliaomini watapata adhabu chungu duniani na akhera. Na Mwenyezi Mungu anajua na nyinyi hamjui.

وَلَوْلَا فَضْلُ اللَّـهِ عَلَيْكُمْ وَرَحْمَتُهُ وَأَنَّ اللَّـهَ رَءُوفٌ رَّحِيمٌ ﴿٢٠﴾

20. Na lau si fadhila ya Mwenyezi Mungu juu yenu na rehema yake na kwa kuwa Mwenyezi Mungu ni Mpole, Mwenye kurehemu.

WALIOLETA UONGO

Aya 11 – 20

KISA CHA UZUSHI KWA UFUPI

Wameafikiana wafasri na wapokezi wa makundi yote na madhehebu ya kiislamu, isipokuwa waliotoka nje ya kundi, kwamba Aya hizi zilishuka kumuondolea tuhuma ya zina Bibi Aisha.

Sababu ya tuhuma ni kwamba Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w. w ) alikuwa akitaka kusafiri, hupiga kura baina ya wake zake. Yule atakayepa- ta kura huongozana naye.

Mnamo mwaka wa tano wa Hijra, Mtume alipigana vita na Bani Mustalaq. Kura ikamwangukia Aisha, akaongozana naye. Mwenyezi Mungu akampa ushindi Mtume wake na akamuoa binti wa kiongozi wao Harith, baada ya kusilimu huyo binti. Jina lake lilikuwa Barra, Mtume akamgeuza jina na kumwita Juwayriya. Baba yake alisilimu pamoja na watu wengi wa kabila lake.

Mtume akarudi Madina pamoja na msafara wake wa ushindi, akisafiri usiku na mchana. Mpaka ilipofikia usiku wa pili akashuka na jeshi lake kupumzika kidogo.

Alipotangaza kuondoka msafara, Aisha alikwenda haja, aliporudi akapoteza mkufu wake. Akarudi kuutafuta. Aliporudi akakuta msafara wa jeshi umekwishaondoka. Akangoja palepale kuwa pengine wakimkosa kwenye msafara wanaweza kumrudia.

Swafwan bin Mua'ttwal alikuwa nyuma ya msafara, akampitia Aisha na akamjua, kwa sababu ilikuwa ni kabla ya kuteremshwa hukumu ya hijabu. Akampeleka mnyama wake naye akajitenga kidogo, mpaka alipopanda. Akamfikisha kwenye msafara au Madina.

Hapo wazushi wakapata nafasi, wakaanza kueneza uongo na kumtuhumu Aisha kufanya hiyana na Safwan. Wa kwanza aliyeuachia ulimi wake na uongo huu ni raisi wa wanfiki, Abdallah bin Ubayya, akaudakia Hassan bin Thabit, na Misatah na wanafiki wengineo. Ndipo Mwenyezi Mungu akatermsha Aya hizi kumuondolea tuhuma Aisha.

Kwa mansaba huu tunaashiria mambo mawili:

Kwanza : kwamba Shia Imamiya wanaitakidi na kuamini kwamba wake wa mitume wote ni wasafi walio twahara na kwamba Mtume yoyote haweki maji yake ila kwenye tumbo lililo twahara.

Na mke wa Mtume anaweza kukufuru, lakini hawezi kuwa mzinifu. Kwa sababu mtume ni mtukufu zaidi kwa Mola wake, hawezi kumjaalia chini yake muasharati.

Anasema mwanachuoni, Imam Tabrasi (mshia) katika Tafsiri yake Majmau'labayan: "Hakika wake wa mitume ni lazima wawe safi na hali hii, kwa sababu ni aibu.

Mwenyezi Mungu amewatakasa Mitume wake na hilo kwa kuwapa heshima na kawaadhimisha na kuwaepusha na jambo ambalo litasababisha kukataliwa kauli zao na miito yao."

Ibn Abbas anasema: "Hakuzini mke wa Mtume kabisa. Khiyana ya mke wa Nuh ilikuwa ni kumfanya Nabii kuwa mwendawazimu na khiyana ya mke wa Lut ilikuwa ni kuwajulisha wale mahabithi kuhusu wageni wake."

Jambo la pili: Kuna baadhi wamesema kwamba Mtume(s.a.w. w) alimtaka shauri Imam Ali(a.s ) miongoni mwa aliowataka shauri, akamshauri ampe talaka, na kwamba hilo eti ndio lilomfanya Aisha kupigana na Imam katika vita vya Jamal (ngamia). Waliosema kauli hii wameitegemeza kwenye riwaya ambayo hatuijui usahihi wake; mbali ya kuwa Mtume hahitajii ushauri wa yeyote katika maamuzi yake, kwa kuzingatia kuwa yeye ni mjuzi na mbora zaidi ya viumbe wengine wote.

Vipi Mtume anaweza kumtilia shaka mkewe na hali anajua kwamba yeye ni mtukufu zaidi kwa Mwenyezi Mungu kuliko kujaaliwa chini yake kahaba? Lau Mtume angelimtilia shaka Aisha angelikuwa ndiye aliyekusudiwa katika kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Mbona mlipousikia, wau- mini wanaume na waumini wanawake hawakujidhania mema na kusema huu ni uzushi dhahiri?"

Hapana! Muhammad(s.a.w. w ) hakumtilia shaka Aisha. Na mwenye kumnasibishia shaka hii atakuwa ameleta uzushi mkubwa.

Zaidi ya hayo, kuna riwaya nyingine inayosema kwamba Imam Ali(a.s ) alimwambia Mtume wa Mwenyezi Mungu:"Hakika viatu vyako havina najisi je mkeo."

Na kwamba Mtume alifurahi kwa hilo. Ismail Haqiy katika Ruuhl-bayan anasema: "Mtume alimtaka ushauri Ali kuhusu Aisha, akasema kuwa ni msafi na nimeuchukua usafi huo kutokana na tukio lililotutokea siku moja tulipokuwa tunaswali nyuma yako ukiwa na viatu vyako; kisha ukavua kiatu kimoja. Tukasema tuifanye ni sunna hiyo? Ukasema: Hapana Jibril ameniambia kuwa kiatu chako hicho kina najisi.

Basi ikiwa kiatu tu hakiwezi kuwa na najisi, vipi ahli yako? Basi Mtume akafurahi kwa hilo.

Sisi hatutaji riwaya hizi kwa kuwa tunaziamini, isipokuwa ni kuonyesha riwaya zinazopinga ushauri wa talaka.

MAANA

Hakika wale walioleta uzushi ni kundi miongoni mwenu. Msiufikirie ni shari kwenu, bali hiyo ni kheri kwenu.

Wale ambao walimzulia khiyana Aisha ni kundi lililodhihirisha kuwa ni waongo na wazushi; kwamba wao wako kwenye mila ya kiislamu na kumbe hawamo kabisa.

Hilo lilimkera Nabii na maswahaba, ndio Mwenyezi Mungu Mtukufu akawambia msidhanie ni shari na madhara, hapana! Bali kuna manufaa mengi katika hili; ikiwemo kujulikana mumin aliye mwema na yule mnafiki habith ambaye anapenda kueneza uovu kwa wasiokuwa na hatia. Manufaa mengine ni majaribio ambayo yatawazidisha uongofu walioongoka na kuwazidishia wanafiki hasara.

Kila mmoja katika wao atapata aliyoyachuma katika madhambi.

Katika wao hapa ni wale waliozusha uongo. Maana ni kuwa kila mmoja katika hawa ana adhabu kwa kiasi alivyeeneza na kutangaza uongo na uzushi. Kwa kuwa tuhuma ya kutusi iliwathibitikia Hassan Bin Thabit, Mistah na mwanamke mmoja wa kikuraishi, Mtume aliwapa adhabu (hadd) ya viboko thamanini. Lakini Abdallah bin Ubayya alitafuta mbinu za kuhepa na kuponyoka adhabu kutokana na hadhari yake na kuwatosa wenzake. Yeye ndiye aliyekusudiwa katika kauli yake Mwenyezi Mungu:

Na yule aliyejitwika sehemu yake kubwa miongoni mwao atapata adhabu kubwa duniani kwa kumfedhesha kwake na kumdhihirisha vitim- bi vyake kwa watu, kiasi ambacho mmoja wa vigogo wa kabila la Khazraj alikitafuta kichwa. Vilevile kigogo wa kabila la Ausi; kama ambavyo vijana wengi wa kiansari akiwemo mwanawe walimtafuta kumuua. Ama adhabu yake katika akhera ni chungu na kubwa.

Mbona mlipousikia, waumini wanaume na waumini wanawake hawakujidhania mema na kusema huu ni uzushi dhahiri?

Mlipousikia, ni huo uzushi. Makusudio ya kujidhania ni kuwadhania wenzao wengine, kwa sababu binadamu wamejengwa kwa mshikamano mmoja; hasa waumini. Kwani imani ni ahadi na kulindana. Kuna Hadith isemayo: "Waumini ni kama nafsi moja" na Qur'an nayo inasema: "Hakika waumini wote ni ndugu" (49:10).

Matumizi haya kwenye Qur'an ni mengi; kama vile: "Wala msijiue." Juz.5 (4:29) pia katika Aya 61 ya Sura hii tuliyo nayo: 'Mjitolee salaam.'

Aya inaashiria kwamba mumin wa kweli, haijuzu kwake kunyamaza kama akisikia maneno ya uzushi na ya ubatilifu. Ama kauli mashuhuri inayosema: 'Ikiwa maneno ni fedha basi kunyamaza ni dhahabu' inakusudia kusema bila ya elimu na maneno ya upuzi na ubatilifu, kama uongo, kusengenya na fitina.

Unaweza kuuliza : Kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu:"Na kusema huu ni uzushi." inafahamisha kuwa ni wajibu kuukadhibisha na kuukana uovu na zina kwa kiasi cha kuisikia tu, bila ya kuthibitisha; jambo ambalo haliafikiani na misingi ya kiakili na kiislamu inayosema: 'Mwenye kukana kwa ulimi ni sawa na mwenye kuthibitisha, kila mmoja wao anahitaji dalili mkataa?'

Jibu : Ndio ni kweli; hakuna shaka kabisa na msingi huu na kwamba unaenea katika kila kitu, lakini makusudio ya kukana hapa sio kuikana hiyo zina yenyewe na kuijua kwake Mwenyezi Mungu, hapana! Bali makusudio hapa ni kukana hukumu yake na matokeo yake, kama kutekeleza adhabu. Kwa hiyo inatakikana izingatiwe kama vile haikutendeka mpaka ithibitike kisharia.

Ndio maana ikawa mwenye kutuhumu anatandikwa viboko thamanini, ikiwa hakuthibitisha. Kwa maneno mengine ni kuwa kukosekana dalili ya kisharia kwenye zina ni dalili ya kukosekana hukumu na matokeo. Ushahidi mkubwa katika hilo ni kauli yake Mwenyezi Mungu:

Mbona hawakuleta mashahidi wane. Na kwa kutoleta mashahidi basi hao mbele ya Mwenyezi Mungu ni waongo; yaani ni wongo katika hukumu ya Mwenyezi Mungu duniani. Ama elimu yake Mwenyezi Mungu Mtukufu ambayo inafungamana na uhakika wa mambo itabakia akhera.

Na lau si fadhila ya Mwenyezi Mungu juu yenu na rehema yake katika dunia na akhera, bila shaka ingeliwapata adhabu kubwa kwa sababu ya yale mliyojiingiza.

Mliyojiingiza ni yale ya uzushi. Rehema ya Mwenyezi Mungu kwa muasi duniani ni kule kumsitiri na kumpa muda ili aweze kutubia. Na katika akhera ni kusamehewa akitubia na kurejea.

Kisha akabainisha Mwenyezi Mungu (s.w.t) sababu ya kustahiki kwake adhabu kubwa duniani na akhera, kwa kusema:

Mlipoyapokea kwa ndimi zenu na mkasema kwa vinywa vyenu msiyoyajua, na mkifikiri ni dogo kumbe kwa Mwenyezi Mungu ni kubwa.

Mnayazungusha maneno ya uzushi kwenye ndimi zenu na wengine wanayachukua bila ya dalili, huku mkidhani kuwa jambo hilo ni dogo, lakini mbele ya Mwenyezi Mungu ni kubwa na lenye dhambi.

Miongoni mwa kauli za Imam Ali(a.s ) ni"Ulimi ni mnyma mkali ukiachiwa unauma"

Na mbona mliposikia msiseme: Haitufalii kuzungumza haya kabisa, sikwambii kuyatilia shaka tena. Bali inatakikana kuuepusha ulimi na kuizungumza zina hata kama itathibitika kisharia isipokuwa katika hali ya kukemea na kukataza. Wale wanojiburudisha kwa kuizungumzia zina na uovu ni wale wapumbavu na waovu zaidi katika watu.

Utakatifu ni wako! Huu ni uzushi mkubwa.

Ni kitu gani kikubwa zaidi kuliko kuwazulia wasiokuwa na hatia? Mumin wa kweli ni yule anayemtetea ndugu yake wala hamtuhumu kwa uovu na shari.

Mwenyezi Mungu anawaonya msirudie kufanya kama haya kabisa ikiwa nyinyi ni waumini.

Anawaonya na anawakataza. Kama haya ni haya ya uzushi. Haijuzu kufanya upuzi na kusikiliza. Kuufunga utiifu na imani ni ishara kuwa mumin akikatazwa na Mwenyezi Mungu kitu au akiamrishwa basi anafuata na kutii

Na Mwenyezi Mungu anawabainishia Aya na Mwenyezi Mungu ni Mjuzi, Mwenye hekima.

Anawafafanulia halali na haramu katika Kitabu chake na katika ulimi wa Mtume wake, anamjua kila mmoja aliye muasi na aliye mtiifu na kuamil- iana naye kwa ujuzi wake, uadilifu wake na hekima yake.

Hakika wale ambao wanapenda kueneza uchafu kwa waliaomini watapata adhabu chungu duniani na akhera.

Uchafu ni mazugumzo machafu. Hakuna tofauti baina ya mwenye kutenda uchafu na mwenye kuutangaza. Kila mmoja ataadhibiwa ikithibitika kuwa amefanya au ametuhumu na akhera atakuwa na adhabu ya kuungua. Kila mwenye kasoro anapenda awe na wanaofanana naye. Kwa sababu mwenye kasoro huwa hawezi kuona ukamilifu kwa mwenzake.

Na Mwenyezi Mungu anajua na nyinyi hamjui.

Mumin hasemi wala hafanyi bila ya kujua, bali anayarudisha asiyoyajua kwa anayejua.

Na lau si fadhila ya Mwenyezi Mungu juu yenu na rehema yake, ingeliwapata adhabu kubwa.

Na kwa kuwa Mwenyezi Mungu ni Mpole Mwenye kurehemu waja wake akiwatakia kheri hata kama wanajitakia shari.

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا لَا تَتَّبِعُوا خُطُوَاتِ الشَّيْطَانِ وَمَن يَتَّبِعْ خُطُوَاتِ الشَّيْطَانِ فَإِنَّهُ يَأْمُرُ بِالْفَحْشَاءِ وَالْمُنكَرِ وَلَوْلَا فَضْلُ اللَّـهِ عَلَيْكُمْ وَرَحْمَتُهُ مَا زَكَىٰ مِنكُم مِّنْ أَحَدٍ أَبَدًا وَلَـٰكِنَّ اللَّـهَ يُزَكِّي مَن يَشَاءُ وَاللَّـهُ سَمِيعٌ عَلِيمٌ ﴿٢١﴾

21. Enyi ambao mmeamini! Msifuate nyao za shetani. Na atakayefuata nyayo za shetani, basi yeye huamrisha machafu na maovu. Na lau si fadhila ya Mwenyezi Mungu juu yenu na rehema yake, asingelitakasika miongoni mwenu yoyote kabisa. Lakini humtakasa amtakaye na Mwenyezi Mungu ni Msikizi, Mjuzi.

وَلَا يَأْتَلِ أُولُو الْفَضْلِ مِنكُمْ وَالسَّعَةِ أَن يُؤْتُوا أُولِي الْقُرْبَىٰ وَالْمَسَاكِينَ وَالْمُهَاجِرِينَ فِي سَبِيلِ اللَّـهِ وَلْيَعْفُوا وَلْيَصْفَحُوا أَلَا تُحِبُّونَ أَن يَغْفِرَ اللَّـهُ لَكُمْ وَاللَّـهُ غَفُورٌ رَّحِيمٌ ﴿٢٢﴾

22. Na wale katika nyinyi wenye wasaa wasiape kutowapa walio jamaa na maskini na waliohama katika njia ya Mwenyezi Mungu. Na wasamehe na wachilie mbali. Je, nyinyi hampendi Mwenyezi Mungu awasamehe? Na Mwenyezi Mungu ni Mwingi wa maghufira, Mwenye kurehemu.

إِنَّ الَّذِينَ يَرْمُونَ الْمُحْصَنَاتِ الْغَافِلَاتِ الْمُؤْمِنَاتِ لُعِنُوا فِي الدُّنْيَا وَالْآخِرَةِ وَلَهُمْ عَذَابٌ عَظِيمٌ ﴿٢٣﴾

23. Hakika wanaowasingizia wanawake wanaoheshimika, walioghafilika walio waumini, wamelaaniwa duniani na akhera na watapata adhabu kubwa.

يَوْمَ تَشْهَدُ عَلَيْهِمْ أَلْسِنَتُهُمْ وَأَيْدِيهِمْ وَأَرْجُلُهُم بِمَا كَانُوا يَعْمَلُونَ ﴿٢٤﴾

24. Siku ambayo zitawashuhudia ndimi zao na mikono yao na miguu yao kwa waliyokuwa wakiyatenda.

يَوْمَئِذٍ يُوَفِّيهِمُ اللَّـهُ دِينَهُمُ الْحَقَّ وَيَعْلَمُونَ أَنَّ اللَّـهَ هُوَ الْحَقُّ الْمُبِينُ ﴿٢٥﴾

25. Siku hiyo atawatekelezea sawa malipo yao ya haki na watajua kwamba hakika Mwenyezi Mungu ndiye haki iliyo wazi.

MSIFUATE NYAYO ZA SHETANI

Aya 21 -25

MAANA

E nyi am b a o mmeamini! Msifuate nyao za shetani kwa kutangaza uovu kwa wale ambao wameamini, wala kwa jambo linalotia wasiwasi na kuwavutia kwake.

Na atakayefuata nyayo za shetani, basi yeye huamrisha machafu na maovu.

Anayewezwa na shetani nafsini mwake, humuongoza kwenye mabaya na machafu.

Na lau si fadhila ya Mwenyezi Mungu juu yenu na rehema yake, asingelitakasika miongoni mwenu yoyote kabisa.

Mwenyezi Mungu ametufahamisha njia ya kheri na njia ya shari, akatukataza hili na akatuamrisha lile, akatupa uwezo wa kutenda na kuacha na akaufungua mlango wa toba kwa mwenye kuasi. Hii ndiyo fadhila yake. Ama utakaso wake huwa hampi isipokuwa mwenye kusikia na akatii.

Lakini humtakasa amtakaye na Mwenyezi Mungu ni Msikizi ,Mjuzi na mwenye hekima pia. Hawatakasi isipokuwa wenye amali na nyoyo safi.

Na wale katika nyinyi wenye wasaa wasiape kutowapa walio jamaa na maskini na waliohama katika njia ya Mwenyezi Mungu.

Imepokewa kuwa Aya hii ilishuka kwa ajili ya Abu Bakri alipoapa kutomsaidia Mistah Bin Athatha baada ya kushiriki pamoja na aliyeshiriki kueneza uvumi wa uovu kumhusu Ummul-mu'min (Mama wa waumin). Sifa hizi tatu zote anazo Mistah: Ni mtoto wa mama mdogo wa Abu bakr, ni maskini asiyekuwa na mali naye ni katika wahajiri na waliopigana Badri.

Na wasamehe na waachilie mbali. Je, nyinyi hampendi Mwenyezi Mungu awasamehe? Na Mwenyezi Mungu ni Mwingi wa maghufira Mwenye kurehemu.

Hii ni ahadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu (s.w.t), kumsamehe na kumre- hemu atakayemsamehe aliyemfanyia ubaya. Imam Zaynul'abidin(a.s ) alikuwa akimsamehe anayemfanyia ubaya, kisha anamwambia Mwenyezi Mungu: Ewe Mola wetu! Hakika wewe umeamrisha tumsamehe atakayetudhulumu, nasi tumesamehe, kama ulivyoamrisha, basi tusamehe; kwani hakika wewe ndiwe mbora zaidi wa hilo kuliko sisi.

Hakika wanaowasingizia wanawake wanaoheshimika, walioghafilika walio waumini, wamelaaniwa duniani na akhera na watapata adhabu kubwa.

Katika Aya ya 4 ya Sura hii Mwenyezi Mungu (s.w.t) alibainisha kwamba mwenye kumtuhumu mwanamke kwa zina na asilete mashahidi wane basi adhabu yake duniani ni kuchapwa viboko thamanini vyovyote vile atakavyokuwa na hakutaja adhabu yake akhera.

Katika Aya hii tuliyo nayo, anabainisha malipo yake huko akhera, ambayo ni adhabu kubwa, ikiwa aliyetuhumiwa ni ni msafi mwenye kujiheshimu na hayo aliyotuhumiwa. Ndio makusudio ya wenye kughafilika; yaani wenye kughafilika na zina, hawaifanyi wala hawaifikirii.

Siku ambayo zitawashuhudia ndimi zao na mikono yao na miguu yao kwa waliyokuwa wakiyatenda.

Duniani inahitajika ushahidi ikiwa mwanamke anadai kuwa ametuhumiwa na mdaiwa akikataa. Akishindwa kuthibitisha basi madai yake yatakataliwa. Lakini huko akhera hakuhitajiki ushahidi, kwa sababu mtendaji hana njia ya kukana. Lau tukikadiria kuwa atakana au kujaribu kukana, basi viungo vyake vitamshuhudia. Kila kiungo kitashuhudia kile kilichofanya. Ulimi wake utashuhudia ulichozungumza, mkono na ulichokishika na mguu na ulichokiendea n.k.

Siku hiyo atawatekelezea sawa malipo yao ya haki na watajua kwam- ba hakika Mwenyezi Mungu ndiye haki iliyo wazi.

Yaani Mwenyezi Mungu (s.w.t) atawahisabu kesho na kuwalipa malipo ya haki na ya uadilifu. Hapo ndio watajua kwamba ufufo, hisabu na malipo walioahidiwa ni kweli, hakuna kuyakimbia.

8

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA NANE

الْخَبِيثَاتُ لِلْخَبِيثِينَ وَالْخَبِيثُونَ لِلْخَبِيثَاتِ وَالطَّيِّبَاتُ لِلطَّيِّبِينَ وَالطَّيِّبُونَ لِلطَّيِّبَاتِ أُولَـٰئِكَ مُبَرَّءُونَ مِمَّا يَقُولُونَ لَهُم مَّغْفِرَةٌ وَرِزْقٌ كَرِيمٌ ﴿٢٦﴾

27. Mambo ya uhabithi ni ya mahabithi na mahabithi ni wa mambo ya uhabithi. Na mema ni ya walio wema na walio wema ni wa mema. Hao wameepushwa na wanayoyasema; wao watapata msamaha na riziki ya ukarimu.

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا لَا تَدْخُلُوا بُيُوتًا غَيْرَ بُيُوتِكُمْ حَتَّىٰ تَسْتَأْنِسُوا وَتُسَلِّمُوا عَلَىٰ أَهْلِهَا ذَٰلِكُمْ خَيْرٌ لَّكُمْ لَعَلَّكُمْ تَذَكَّرُونَ ﴿٢٧﴾

27. Enyi ambao mmeamini! Msiingie nyumba zisizo nyumba zenu mpaka muombe ruhusa na muwatolee salaam wenyewe. Hayo ni bora kwenu ili mpate kukumbuka.

فَإِن لَّمْ تَجِدُوا فِيهَا أَحَدًا فَلَا تَدْخُلُوهَا حَتَّىٰ يُؤْذَنَ لَكُمْ وَإِن قِيلَ لَكُمُ ارْجِعُوا فَارْجِعُوا هُوَ أَزْكَىٰ لَكُمْ وَاللَّـهُ بِمَا تَعْمَلُونَ عَلِيمٌ ﴿٢٨﴾

28. Na msipomkuta yoyote humo basi msiingie mpaka mruhusiwe. Na mkiambiwa rudini, basi rudini. Hivyo ni usafi zaidi kwenu na Mwenyezi Mungu anajua mnayoyatenda.

لَّيْسَ عَلَيْكُمْ جُنَاحٌ أَن تَدْخُلُوا بُيُوتًا غَيْرَ مَسْكُونَةٍ فِيهَا مَتَاعٌ لَّكُمْ وَاللَّـهُ يَعْلَمُ مَا تُبْدُونَ وَمَا تَكْتُمُونَ ﴿٢٩﴾

29. Si vibaya kwenu kuingia nyumba zisizokaliwa amabazo ndani yake mna bidhaa zenu. Na Mwenyezi Mungu anajua mnayoyadhirisha na mnayoyaficha.

MAMBO YA UHABITHI NI YA MAHABITHI

Aya 26 – 29

MAANA

Mambo ya uhabithi ni ya mahabithi na mahabithi ni wa mambo ya uhabithi. Na mema ni ya walio wema na walio wema ni wa mema.

Neno uhabithi limefasiriwa kutoka na neno la kiarabu Khabith lenye maana ya uovu na ubaya katika kila jambo, ikiwemo ubaya katika itikadi, nia, sifa, kauli na vitendo vya aina mbali mbali, wala hauhusiki na zina.

Na neno wema limefasiriwa kutokana na neno Twayyib lenye maana ya uzuri katika kila jambo.

Qur'an imelitumia neno uhabithi katika ubaya wa ardhi, mali, maneno na vyakula vilivyoharamu na kila anayestahiki machukivu na ghadhabu ya Mwenyezi Mungu katika majini na watu.

Jamaa katika wafasiri wamesema kuwa makusudio ya neno Khabithat ni wanawake mahabithi na Khabithun ni wanaume mahabith. Vilevile katika wema. Kauli hii haiafikiani na hali halisi ilivyo.

Tumewaona wanawake mahabithi wakiolewa na wanume wema na wanawake wema wakiolewa na wanume mahabithi. Bali hata haiafikiani na Qur'an; Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema:

"Mwenyezi Mungu amewapigia mfano waliokufuru - mke wa Nuh na mke wa Lut walikuwa chini ya waja wetu wema wawili miongoni mwa waja wetu, lakini wakakhini … Na Mwenyezi Mungu amewapigia mfano walioaminimke wa Firauni, aliposema: Mola wangu nijengee kwako nyumba Peponi na uniokoe na Firauni na vitendo vyake" (66:11). Inajulikana kwamba Nuh na Lut walikuwa Manabii, maasumu na Firauni ndiye yule aliyesema: "Mimi ndiye Mola wenu mkuu."

Tuonavyo sisi ni kuwa neno Khabithat lina maana ya mambo ya uhabithi, na neno khabithun lina maana ya walio mahabithi wote wanaume na wanawake. Limekuja kwa dhamiri ya kiume kwa kuchanganya wote. Vile vile Twayyibat na Twayyibun.

Kwa hiyo maana yatakuwa, kauli na vitendo vya uhabithi vinatokana na yule aliye habithi katika wanaume na wanawake. Na kauli na vitendo vyema vinatokana na yule aliye mwema; kama alivyosema mshairi: "Kila kilicho ndani ya chombo kitaiva."

Hao wameepushwa na wanayoyasema; wao watapata msamaha na riziki ya ukarimu.

Hao ni ishara ya walio wema; wanosema ni wale mahabithi. Mwenyezi Mungu (s.w.t) atawaneemaesha na maghufira na pepo hao walioepushwa.

Enyi ambao mmeamini! Msiingie nyumba zisizo nyumba zenu mpaka muombe ruhusa na muwatolee salaam wenyewe. Hayo ni bora kwenu ili mpate kukumbuka.

Mpaka muombe ruhusa ni amri ya kubisha hodi kabla ya kuingia; sawa na kauli yake Mwenyezi Mungu katika Aya 59 ya Sura hii tuliyo nayo: "Na watoto wanapofikia kubaleghe basi nawatake ruhusa."

Kila anayetaka kuingia nyumba ya mwingine ni lazima aombe idhini kwa mwenyewe kwanza. Kwa sababu kuingia ni kutumia mali ya mwenyewe, ambayo haiwezi kuwa halali ila kwa ruhusa yake. Kuanzia hapa ndio mafaqihi wakasema kuwa kuomba ruhusa ni wajibu na salaam ni Sunna. Inatosha kuwa ni kuomba ruhusa kwa jambo lolote lile; kama vile kugonga mlango, kusema hodi! Au wenyewe humo! Baada ya kupewa idhii ndio aiingie atoe salaam!

Na msipomkuta yoyote humo basi msiingie mpaka mruhusiwe.

Unaweza kuuliza : hapa, ikiwa nyumbani hakuna mtu, ni nani atakayetoa ruhusa?

Sheikh Maraghi amejibu kuwa makusudio ni ikiwa hakuna anayeweza kutoa ruhusa; kama mtoto mdogo au mtumishi. Jawabu lilo na nguvu ni ikiwa nyumba haina mtu, basi hairuhusiwi kuingia mpaka amuone mwenyewe kwanza na ampe idhini; kwa mfano kumwambia nenda nyumbani kwangu ukaniletee kitu fulani au tangulia nyumbani kwangu nami naja.

Na mkiambiwa rudini, basi rudini. Hivyo ni usafi zaidi kwenu.

Wala msing'ang'anie kutaka kuingia na msiwe na chuki nyoyoni kwa mwenye nyumba mchukue uzuri tu na kusema ana udhuru wa kisharia. Angalia kifungu cha 'Kuchukulia usahihi' katika Juz.1 (2:83).

Na Mwenyezi Mungu anajua mnayoyatenda.

Hii ni hadhari na kiaga kwa yule anayemshtumu na kumsema ambaye hakumpa idhini ya kuingia nyumbani kwake.

Si vibaya kwenu kuingia nyumba zisizokaliwa ambazo ndani yake mna bidhaa zenu.

Makusudio ya nyumba hizi ni zile sehemu za watu wengi, kama vile mahoteli na maduka.

Kwa hiyo ambaye ana bidhaa zake hotelini au dukani, basi anaweza kuingia na kuchukua bidhaa zake bila ya kmuomba ruhusa mwenyewe, kwa sababu amekwisha fungua mlango kwa wote. Pia hakuna siri kwa mwenye hoteli kwa hilo.

Na Mwenyezi Mungu anajua mnayoyadhirisha na mnayoyaficha.

Hii inaashiria kuwa si halali kwa mtu kuingia nyumba ya mwingine kwa kusudia kufanya khiyana na kuwadhuru wenyewe, na kwamba mwenye kukusudia hivyo, basi Mwenyezi Mungu anajua malengo yake na atamwadhibu nayo.

قُل لِّلْمُؤْمِنِينَ يَغُضُّوا مِنْ أَبْصَارِهِمْ وَيَحْفَظُوا فُرُوجَهُمْ ذَٰلِكَ أَزْكَىٰ لَهُمْ إِنَّ اللَّـهَ خَبِيرٌ بِمَا يَصْنَعُونَ ﴿٣٠﴾

30. Na waambie waumini wanaume wainamishe katika macho yao na wazilinde tupu zao. Hilo ni usafi zaidi kwao. Hakika Mwenyezi Mungu ana habari za wanayoyafanya.

وَقُل لِّلْمُؤْمِنَاتِ يَغْضُضْنَ مِنْ أَبْصَارِهِنَّ وَيَحْفَظْنَ فُرُوجَهُنَّ وَلَا يُبْدِينَ زِينَتَهُنَّ إِلَّا مَا ظَهَرَ مِنْهَا وَلْيَضْرِبْنَ بِخُمُرِهِنَّ عَلَىٰ جُيُوبِهِنَّ وَلَا يُبْدِينَ زِينَتَهُنَّ إِلَّا لِبُعُولَتِهِنَّ أَوْ آبَائِهِنَّ أَوْ آبَاءِ بُعُولَتِهِنَّ أَوْ أَبْنَائِهِنَّ أَوْ أَبْنَاءِ بُعُولَتِهِنَّ أَوْ إِخْوَانِهِنَّ أَوْ بَنِي إِخْوَانِهِنَّ أَوْ بَنِي أَخَوَاتِهِنَّ أَوْ نِسَائِهِنَّ أَوْ مَا مَلَكَتْ أَيْمَانُهُنَّ أَوِ التَّابِعِينَ غَيْرِ أُولِي الْإِرْبَةِ مِنَ الرِّجَالِ أَوِ الطِّفْلِ الَّذِينَ لَمْ يَظْهَرُوا عَلَىٰ عَوْرَاتِ النِّسَاءِ وَلَا يَضْرِبْنَ بِأَرْجُلِهِنَّ لِيُعْلَمَ مَا يُخْفِينَ مِن زِينَتِهِنَّ وَتُوبُوا إِلَى اللَّـهِ جَمِيعًا أَيُّهَ الْمُؤْمِنُونَ لَعَلَّكُمْ تُفْلِحُونَ ﴿٣١﴾

31. Na waambie waumini wanawake wainamishe katika macho yao na wazilinde tupu zao, wala wasionyeshe uzuri wao, isipokuwa unaodhihirika. Na waangushe shungi zao juu ya vifua vyao, wala wasidhihirishe uzuri wao ila kwa waume zao, au baba zao, au baba wa waume zao, au watoto wao, au watoto wa waume zao, au ndugu zao, au watoto wa kaka zao, au watoto wa dada zao, au iliyowamiliki mikono yao ya kuume, au wafuasi wanaume wasio na matamanio, au watoto wadogo ambao hawajajua uchi wa wanawake. Wala wasipige miguu yao ili yajulikane mapambo waliyoyaficha. Na tubieni kwa Mwenyezi Mungu nyote enyi waumini ili mpate kufanikiwa.

HIJABU NA KUINAMISHA MACHO

Aya 30 – 31

MAANA

Aya mbili hizi ni miongoni mwa Aya za hukmu, na zimeeleza wajibu wa kuinamisha jicho kwa wanawake na wanaume, kuhifadhi tupu na zina na hijabu. Ufafanuzi ni huu ufuatao:

1.Na waambie waumini wanaume wainamishe katika macho yao.

Mwenyezi Mungu amewaamrisha wanaume wazuie macho yao, lakini hakubainisha wayazuie macho yao kwenye nini. Ameyanyamazia hayo kwa kutaka yafahamike kutokana na mfumo wa maneno. Kwani lilio dhahiri ni kuharamishwa kuwaangalia watu kando.

Wameafikiana mafaqihi wengi kwamba haijuzu kwa mwanamume kuangalia kitu katika mwili wa mtu kando mwanamke, isipokuwa uso wake na viganja kwa sharti ya kuangalia bila ya kujiburudisha na kutohofia kuingia katika haramu. Hii ni kwa mwanamke Mwislamu ambaye dini yake inamkataza kujiweka wazi. Ama yule ambaye dini yake haimkatazi kujiweka wazi, wametofautiana mafaqihi katika kujuzu kuwangalia bila ya kujiburudisha. Wengine wakasema inajuzu kuangalia nywele za wanawake waislamu mabedui wasiokatazika.

2.Na wazilinde tupu zao na zina.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) ameingiza neno 'katika' kwenye macho, lakini hakuingiza kwenye tupu. Kwa sabu ni wajibu kusitiri tupu wakati wote isipokuwa katika faragha ya mume na mke, lakini kuangalia si haramu katika hali zote isipokuwa katika baadhi ya hali.

Hilo ni usafi zaidi kwao. Hakika Mwenyezi Mungu ana habari za wanayoyafanya.

Hilo ni hilo la kuinamisha macho na walio haramu kuwaangalia, jambo ambalo ni twahara zaidi kwa nafsi na karibu zaidi kwa takua na linaweka mbali dhambi.

3.Na waambie waumini wanawake wainamishe katika macho yao na wazilinde tupu zao.

Mafaqihi wa kishia wamesema kuwa ni haramu kwa mwanamke kumtazama mwanamume aliye mtu kando, vile ilivyo haramu kwa mwanamume juu ya mwanamke. Kwa hiyo haijuzu kwa mwanamke kuangalia nywele za mwanamume n.k. Lakini wengine wamesema kuwa inajuzu kwa mwanamke kumwangalia mwanamume sehemu zote isipokuwa sehemu iliyo baina ya kitovu na magoti. Ufafanuzi uko kwenye kitabu chetu cha Fiqh ala madhahibul-khamsa (Fiqh katika madhebu tano) sehemu ya yaliyo wajibu kuangalia na yaliyo haramu.

4.Wala wasionyeshe uzuri wao, isipokuwa unaodhihirika.

Makusudio ya uzuri hapa ni sehemu zao. Kwa sababu si haramu kuangalia uzuri. Makusudio ya unaodhihirika ni sehemu za uso na viganja viwili tu. Mafaqihi wametoa dalili kwa Aya hii, juu ya wajibu wa hijabu na kwamba mwili wote wa mwanamke ni uchi isipokuwa uso na viganja viwili vya mikono.

Imam Ja'far Swadiq(a.s ) . Aliulizwa kuhusu mikono miwilli kuwa je, ni katika uzuri aliouzungumzia Mwenyezi Mungu? Akasema: ndio na sehemu yoyote isiyokuwa uso na viganja viwili ni katika uzuri ulioharamishwa. Katika kitabu Ahkamul-Ayat cha Aljasas, mmoja wa maimamu wa kihanfi anasema:"Makusudio ya unaodhihiri ni uso na viganja viwili" .

Katika Tafsir ya Razi ambaye ni wa madhehebu ya Shafi anasema: "Wameafikiana kuwa uso na viganja viwili si sehemu ya tupu."

Na waangushe shungi zao juu ya vifua vyao.

Neno vifua, limefasiriwa kutokana na neno juyub lenye maana ya uwazi wa magauni. Yaani ni wajibu kwa wanawake kuangusha mitandio yao kwa mbele ili isitiri, shingo na vifua.

Wanawake wa wakati wa jahilia, walikuwa wakifunika vichwa vyao kisha wanangusha shungi zao kwa nyuma, shingo zao na vifua vyao vinakuwa wazi. Wakaendela kuwa hivyo hata wakati wa Uislamu, mpaka iliposhuka Aya hii wakawa wanaangusha kwa mbele na kusitiri shingo na vifua.

KUJIWEKA WAZI AU KUJIUZA?

Uislamu umeruhusu mwanamke afunue uso wake na viganja vyake; kwa sababu kuna dharura ya kimaisha. Sehemu nyinginezo zisizokuwa hizo, zimezingatiwa kuwa ni uchi, kwa sababu ni hatari. Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w. w ) amesema:"Mwenye kuchunga kondoo wake kandokando ya ugo nafsi yake inamvuta kuchunga ndani yake."

Hivi ndivyo ilivyo hasa. Popote uendapo utajionea maajabu. Mwanamke alianza kufunua kichwa chake baada ya kwenda saloni, akendela kufunua kifua na mabega hadi kufikia minisketi na mavazi mengine ya maajabu yanaonyesha umbile zima la mwanamke; huku akijitembeza barabarani kama kwamba ni nyama inayouzwa sokoni. Siri ya hilo ni kwamba wanawake wengi hawaendi mbali zaidi ya kujionyesha na kuonyesha urembo wao tu.

Maajabu zaidi niliyoyasoma kuhusu mambo haya ni kwamba huko mjini Humburg, Ujerumani ya magharibi, kuna barabara ya kutisha ambayo pambizoni mwake mna sehemu zilizo na wanawake wakiwa uchi, katika hali isiyokuwa ya kawaida ambayo haingiliki akilini. Kila ambalo unaliona kuwa haliwezi kufanyika basi hapo linafanyika kiuhakika. Huu ndio upeo wa uhuru.

Nimesoma makala hii nikiwa natetema, na kufikiria kwamba barabara hii iliyo uchi, kama sio hivi karibuni basi baadae itafika kwenye miji yetu; sawa na ilivyofika minisketi na mengineyo; maadamu tunaigiza magharibi. Mungu apishe mbali na yatakayokuja kesho.

Kwa mnasaba huu tunadokeza kwamba, ikiwa mwanamke anapenda sana kuonyesha urembo wake na uzuri wake na kutengeneza shepu yake kwa kila njia, basi kuna wanaume wengi wanaopenda kuonyesha umashuhuri wao, hata kama ni kwa njia ya uongo na kudanganya. Ikiwa mwanamke anamfanyia chuki anayeshindana naye kwa uzuri na urembo, basi wanaume wanaopenda kujionyesha wana hasadi zaidi hasa kwa yule ambaye jina lake linatajwa.

Mnamo mwaka 1957, mwandishi mmoja wa Kimisri, alitoa makala ambayo ndani yake aliibeza fat-wa ya masheikh wa Al-azhar kuharamisha mwanamke kuvaa nguo ya kuogelea. Miongoni mwa aliyoyasema ni: Uislamu uko mbali na fatwa hii.

Mimi nilitoa makala kupinga maelezo yake haya, na nikathibitisha kuwa masheikh wa Al-Azhar wametamka neno la Uislamu na Qur'an, na nikatoa ushahidi wa Aya:'Wala wasidhihirishe uzuri wao.'

Baada ya kupita siku, ikasadifu mimi na mwenzangu mmoja kumtembelea sheikh mmoja. Tulipotulia yule sheikh akanikabili na kusema: "Vipi wewe unahalalisha kuvaa nguo ya kuogelea na kuwarudi masheikh wa Al-azhar ambao wametoa fatwa ya kuharamisha?

Nikamwambia: Hapana ni kinyume na hivyo. Mimi nimewaunga mkono masheikh na nikaiponda rai ya mwenye kuwarudi.

Akasema: "Hapana! Mimi ninalo gazeti lilo na makala hiyo, ngoja nikuonyeshe."

Nikamwambia ailete.

Basi akaenda haraka na akaja na gazeti mkononi mwake, akaanza kulisoma kwa hamasa kubwa.

Nikamwambia: Je, umeona nini?

Akapigwa na butwaa, gazeti likamponyoka mikononi. Alhamdulillah, hapo pia alikuwako rafiki wa sheikh na sheikh mmoja miongoni mwa jamaa zake. Hao wawili bado wako hai hivi sasa tukiwa katika wakati wa kusi mwaka 1969.

Siwezi kupata tafsiri ya sheikh huyu ambaye alijiumbua mwenyewe isipokuwa Mungu amsamehe. Yeye alitaka anitie aibu na kuniumbua, akawa anatafuta taa na utambi, kama wasemavyo watu wa Amol, ili aanze kueneza na kutangaza.

Na pale aliposoma jina langu kwenye gazeti chuki yake iliyojificha ililipuka na kupenda kwake umashuhuri kukampofusha, weupe akauona ni weusi na haki kuwa ni batili. Sio siri kwamba chuki ni sawa na mapenzi, inapofusha na kufanya uziwi. "Wana nyonyo, lakini hawafahamu kwazo, na wana macho, lakini hawaoni kwayo, na wanayo masikio, lakini hawasikii kwayo. Hao ni kama wanyama bali wao ni wapotevu zaidi. Hao ndio walioghafilika." Juz. 9 (7:179).

Sikutaja kisa hiki kwa kulalamika au kushtakia, hapana! Uzoefu umenifundisha kutowajali waongo, lakini kalamu yangu imenizidia na haikunipa hiyari. Hivi ndivyo nilivyo mimi na kalamu yangu.

Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kuwakataza wanawake Waislamu kutofunua sehemu zao isipokuwa uso na viganja, sasa anabainisha wale ambao inafaa kuwadhihirishia ambao ni aina kumi na mbili:

1.Wala wasidhihirishe uzuri wao ila kwa waume zao . Kila mmoja kati ya mume na mke anaweza kumwangalia mwenzake popote atakapo.

2.Au baba zao . Hapa wanaingia mababu wa upande wa baba na mama.

3.Au baba wa waume zao . Wanaingia mababa wa waume na mababu zao wa upande wa baba na mama

4.Au watoto wao. Mtoto wa mtoto, mwanamume au mwanamke, pia ni mtoto.

5.Au watoto wa waume zao na kuendelea chini.

6.Au ndugu zao wa baba mmoja tu au mama mmoja tu au wote.

7.Au watoto wa kaka zao na kuendelea chini.

8.Au watoto wa dada zao vilevile kuendelea chini.

9.Au wanawake wao . Ieleweke kuwa ni haramu kuwa uchi kabisa mwanamke mbele ya mwanamke mwenzake hata kama ni mama yake au binti yake, kama ambavyo ni haramu kwake yeye pia kuwaangalia uchi. Ni halali kuangaliana sehemu zisizokuwa hizo, ikiwa ni Mwislamu. Ama mwanamke asiyekuwa Mwislamu haifai kuwa wazi mbele yake. Hivi ndivyo ilivyofahamisha Aya. Linalokhalifu hilo liachwe. Baadhi ya mapokezi yanasema kuwa wanawake wasiokuwa waislamu wakijifunua mbele ya wanawake wasiokuwa waislamu wanaenda kuwasifia waume zao.

10.Au iliyowamiliki mikono yao ya kuume, katika wajakazi tu . Ama mtumwa wa kiume haijuzu kumwangalia isipokuwa uso na viganja viwili; hata kama ni hasi. Kauli na riwaya zinazokhalifu hayo basi zinaachwa. Kwa vyovyote, ni kuwa maudhui haya hayapo siku hizi, ambapo hakuna utumwa.

11.Au wafuasi wanaume wasio na matamanio. Hao ni wale wanaochanganyika na familia na kuwa nao mara nyingi, waki- wa hawana matamanio ya wanawake, kwa sababu za kimwili; kama uzee na uhanithi au za kuathirika kisaikolojia.

12.Au watoto wadogo ambao hawajajua uchi wa wanawake . Yaani watoto wadogo ambao hawawezi kupambanua baina ya uchi na kiungo kingine.

Wala wasipige miguu yao ili yajulikane mapambo waliyoyaficha.

Wanawake walikuwa wakivaa vikuku miguuni, mpaka sasa desturi hii inaendelea katika miji mingi ya waarabu. Baadhi walikuwa wakipiga miguu yao chini ili vigongane vikuku vyao kuwavutia wanaume au wajue kuwa wamevaaa vikuku. Ndipo Mwenyezi Mungu akawakataza hilo. Hapo inaashiria kwamba haifai kwa mwanamke kufanya jambo lolote litakalomvutia mwanamume.

Na tubieni kwa Mwenyezi Mungu nyote enyi waumini, ili mpate kufanikiwa.

Acheni yale aliyowakataza Mwenyezi Mungu, na ambaye atateleza kufanya makosa basi afanye haraka kutubia.