TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA NANE Juzuu 18

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA NANE0%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA NANE Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: Qurani tukufu

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA NANE

Mwandishi: Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya
: HASANI MWALUPA
Kundi:

Matembeleo: 11263
Pakua: 2147


Maelezo zaidi:

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 13 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 11263 / Pakua: 2147
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA NANE

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA NANE Juzuu 18

Mwandishi:
Swahili

9

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA NANE

وَأَنكِحُوا الْأَيَامَىٰ مِنكُمْ وَالصَّالِحِينَ مِنْ عِبَادِكُمْ وَإِمَائِكُمْ إِن يَكُونُوا فُقَرَاءَ يُغْنِهِمُ اللَّـهُ مِن فَضْلِهِ وَاللَّـهُ وَاسِعٌ عَلِيمٌ ﴿٣٢﴾

32. Na waozeni wajane miongoni mwenu na wema katika watumwa wenu na wajakazi wenu. Wakiwa mafukara Mwenyezi Mungu atawa tajirisha katika fadhila zake; na Mwenyezi Mungu ni Mwenye wasaa, Mwenye kujua.

وَلْيَسْتَعْفِفِ الَّذِينَ لَا يَجِدُونَ نِكَاحًا حَتَّىٰ يُغْنِيَهُمُ اللَّـهُ مِن فَضْلِهِ وَالَّذِينَ يَبْتَغُونَ الْكِتَابَ مِمَّا مَلَكَتْ أَيْمَانُكُمْ فَكَاتِبُوهُمْ إِنْ عَلِمْتُمْ فِيهِمْ خَيْرًا وَآتُوهُم مِّن مَّالِ اللَّـهِ الَّذِي آتَاكُمْ وَلَا تُكْرِهُوا فَتَيَاتِكُمْ عَلَى الْبِغَاءِ إِنْ أَرَدْنَ تَحَصُّنًا لِّتَبْتَغُوا عَرَضَ الْحَيَاةِ الدُّنْيَا وَمَن يُكْرِههُّنَّ فَإِنَّ اللَّـهَ مِن بَعْدِ إِكْرَاهِهِنَّ غَفُورٌ رَّحِيمٌ ﴿٣٣﴾

33. Na wajizuilie na machafu wale wasiopata cha kuolea, mpaka Mwenyezi Mungu awatajirishe katika fadhila zake. Na wale ambao wanataka kuandika katika wale ambao imewamiliki mikono yenu ya kuume, basi waandikieni kama mkiona wema kwao. Na wapeni katika mali ya Mwenyezi Mungu aliyowapa. Wala msiwalazimishe vijana wenu wa kike kufanya umalaya kwa ajili ya kutafuta pato la maisha, ikiwa wanataka kujichunga. Na atakaye walazimisha basi Mwenyezi Mungu baada ya kulazimishwa kwao huko ni Mwingi wa maghufira, Mwenye kurehemu.

وَلَقَدْ أَنزَلْنَا إِلَيْكُمْ آيَاتٍ مُّبَيِّنَاتٍ وَمَثَلًا مِّنَ الَّذِينَ خَلَوْا مِن قَبْلِكُمْ وَمَوْعِظَةً لِّلْمُتَّقِينَ ﴿٣٤﴾

34. Na hakika tumewateremshia Aya zinazobainisha na mifano kutokana na waliopita kabla yenu na mawaidha kwa wenye takua.

WAOZENI WAJANE

Aya 32 – 34

MAANA

Na waozeni wajane miongoni mwenu.

Maneno yanaelekezwa kwa Waislamu wote. Wajane ni wale wasiokuwa na wake au wasiokuwa na waume. Amri hii hapa ni ya Sunna sio ya wajibu. Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kuwaamrisha wanaume na wanawake wahifadhi tupu zao na kujizuia na mambo yaliyo haramu na pia kuwakataza wanawake kujipamba na kudhihirisha kipambo mbele ya watu kando.

Sasa anaamrisha kusaidiana kwa kila anayehitajia ndoa baina ya wanaume na wanawake. Kwa sababu ujane ndio chimbuko la uchafu na uovu; kama zina na ulawiti. Na ndoa ni kinga ya hayo. Ndio maana Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w. w ) akasema:"Waovu wenu ni wajane wenu…"

"Ndoa ni katika sunna yangu, atakayejiepusha na sunna yangu basi si katika mimi."

Na wema katika watumwa wenu na wajakazi wenu.

Makusudio ya wema hapa ni waumini. Yaani waozeni watumwa wakiwa ni waumini, maudhui haya hayapo, kwa kutokuwepo utumwa.

Wakiwa mafukara Mwenyezi Mungu atawatajirisha katika fadhila zake

Watu wengi hawaangalii maadili ya mchumba, bali wanaangalia cheo chake au mali yake. Ndipo Mwenyezi Mungu akalaumu fikra hii na akasema kuwa yeye ni muweza wa kila kitu. Kuna Hadith isemayo:"Akiwajia ambaye mnairidhia hulka yake na dini yake, basi muozeni; kama hamtafanya itakuwa fitna katika ardhi na uharibifu mkubwa."

Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye wasaa, Mwenye kujua.

Anatoa wasaa kwa anaemuomba na asiyemuomba kwa fadhila zake.

Na wajizuilie na machafu wale wasiopata cha kuolea, mpaka Mwenyezi Mungu awatajirishe.

Unaweza kuuliza : katika Aya iliyotangulia Mwenyezi Mungu amesema kuwa watu waoe tu, wakiwa mafukara atawatajirisha; kisha hapa anasema, tena moja kwa moja baada ya kauli ya kwanza, kuwa mtu asiyepata mahari wala posho asiingie kwenye uovu na kwamba avumilie mpaka Mwenyezi Mungu ampe wasaa, basi kuna wajihi gani baina ya Aya mbili?

Jibu : Hakuna haja ya kuchanganya Aya mbili hizi, kwa sababu kila moja ina makusudio yake. Ya kwanza inawakusudia mawalii, kwamba akija mchumba msimkatae kwa sababu ya ufukara wake. Aya ya pili inamuhusu fukara mwenyewe, kwamba akinyimwa kuoa kwa sababu ya ufukara wake, basi avumilie na afanye bidii mpaka Mungu atakapompa wasaa wa kuweza kuoa.

Na wale ambao wanataka kuandika katika wale amabao imewamiliki mikono yenu ya kuume, basi waandikieni kama mkiona wema kwao.

Ambaye ana mtumwa wa kike au wa kiume anayeweza kuchuma, anaweza kuandikiana naye mkataba kuwa akitoa kiasi fulani cha pesa mara moja au pole pole, awe huru.

Akitekeleza yote basi anakuwa huru au akitoa baadhi atakuwa ana uhuru wa kiasi kile alichotoa, ikiwa hakuna sharti la kutoa chote; vinginevyo hatakuwa na uhuru wowote.

Imesekana kuwa mtumwa hawezi kugawika; ama awe huru kamili au awe mtumwa kamili. Ni Sunna kwa mwenye mtumwa kumwachia kiasi fulani cha mali waliyoelewana. Hayo ndio makusudio ya kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: Na wapeni katika mali ya Mwenyezi Mungu aliyowapa.

Mafaqihi wameweka istilahai ya neno mkataba kwa makubaliano haya, kutokana na Mwenyezi Mungu kutumia neno kitab.

Wala msiwalazimishe vijana wenu wa kike kufanya umalaya kwa ajili ya kutafuta pato la maisha, ikiwa wanataka kujichunga.

Makusudio ya vijana wa kike hapa ni wajakazi, ambao hivi sasa hawako. Watu wa wakati wa ujahiliya walikuwa wakiwalazimisha wajakazi wao kufanya zina kwa kutaka mali, ndio Mwenyezi Mungu (s.w.t) akalikataza hilo.

Unaweza kuuliza kuwa : dhahiri ya kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu 'wakitaka kujichunga,' inaonyesha kuwa kama hawataki kujichunga basi wanaweza kulazimishwa kufanya zina, na hali tunajua kuwa zina ni hara- mu kwa nyanja zake zote?

Jibu : maana ya neno 'ikiwa' yanatofautiana kwa kutofautiana makusudio na maneno yalivyo. Inaweza ikawa kwa maana ya sharti hasa, ilivyo. Kwa mfano kumwambia mtu: Ikiwa utafanya hivi na mimi nitafanya kama utakavyofanya. Hapa utakuwa umeweka sharti kwamba hutafanya mpaka afanye yeye.

Mara nyingine inakuwa bila ya kukusudia sharti; kwa mfano kumwambia sahibu yako: "Ikiwa utaruzukiwa mtoto basi usimnunulie baskeli" hapa haina maana kama hataruzukiwa mtoto basi anaweza kumnunulia baskeli; jambo ambalo litakuwa kama kuchanganyikiwa. Isipokuwa unataka kumweleza maoni yako ya kutotaka watoto wapande baskeli.

Maana haya ndiyo yaliyokusudiwa hapa 'ikiwa' limekuja kubainisha hali halisi; kwamba ikiwa wajakazi wanataka kujichunga basi nyinyi itakuwa ni zaidi mjichunge.

Kama tukiliweka neno 'ikiwa' kwa maana ya sharti, itakuwa maana yake ni: walazimisheni wajakazi wenu ikiwa wanataka zina. Na inavyojulikana ni kuwa hakuna kulazimisha ikiwa mtu anataka.

MATAMSHI NA UELEWA

Kwa maneno mengine ni kuwa neno 'ikiwa' au 'iwapo' au 'kama' na mengineyo mfano wake, huwa linafahamisha vitu viwili kwa wakati mmoja: Maana yake kimatamshi na maana yake kiufahamu na kiuelewa ambayo hayakutamkwa lakini yanafahamika kwa ishara. Kwa istlahi ya watu wa elimu ya usul, wanaita mantuq na mafhum

Mantuq ni kwa mfano kumwambia sahibu yako; ikiwa utanikirimu na mimi nitakukirimu. Kwa hiyo kimatamshi hapa imeeleweka kuwa kumkirimu kwako kutategema yeye ikiwa atakukirimu.

Ama kiufahamu, katika mfano huu ni kuwa, ikiwa hukunikirimu basi nami sikukukirimu. Maana haya hayakutajwa, lakini yamefahamika kutokana na jumla ya kwanza.

Aya tuliyo nayo iko katika aina ya kwanza tu, ya kimatamshi; haiwezi kuingia kwenye aina ya pili.

Yaani kutofaa kutolazimisha zina pamoja na kutaka kujisitiri. Hapo ufahamu hauingii, kwa sababu tukileta ufahamu maana itakuwa ni: kujuzu kulazimisha pamoja na kuitaka hiyo zina. Hapo kutakuwa na mgongano, wa kuwalazimisha na wenyewe wanataka, jambo haliwezekani kwa wakati mmoja. Itakuwaje mtu alazimishwe na wakati huo huo mwenyewe anataka. Pia ni muhali kutoka kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu, kulazimisha uovu kwa namna yoyote ile.

Na atakayewalazimisha basi Mwenyezi Mungu baada ya kulazimishwa kwao huko ni Mwingi wa maghufira, Mwenye kurehemu.

Wale waliolazimishwa kufanya zina. Kwa sababu kosa ni la yule aliyelazimisha, sio aliyelazimishwa. Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w. w ) amesema:"Umma wangu umeondolewa yale waliyolazishwa…" Mwenye kumlazimisha mwingine kufanya makosa, Mwenyezi Mungu atamghufiria akitubia na kurejea.

Na hakika tumekuteremshia Aya zinazobainisha na mifano kutokana na waliopita kabla yenu na mawaidha kwa wenye takua.

Makusudio ya Aya ni hukumu za Qur'an na mafundisho yake nazo ziko wazi. Mifano ni habari za waliopita na visa vyao. Mawaidha kwa wenye takua ni uongofu kwa mwenye kutaka kuongoka.

Maana ni kuwa Mwenyezi Mungu Mtukufu ameteremsha Qur'an kubainisha na kuweka wazi hukumu tunazozihitajia, habari za waliopita, uongofu kwa mwenye kuutaka, na nguvu kwa mwenye kumtawalisha Mungu.

اللَّـهُ نُورُ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ مَثَلُ نُورِهِ كَمِشْكَاةٍ فِيهَا مِصْبَاحٌ الْمِصْبَاحُ فِي زُجَاجَةٍ الزُّجَاجَةُ كَأَنَّهَا كَوْكَبٌ دُرِّيٌّ يُوقَدُ مِن شَجَرَةٍ مُّبَارَكَةٍ زَيْتُونَةٍ لَّا شَرْقِيَّةٍ وَلَا غَرْبِيَّةٍ يَكَادُ زَيْتُهَا يُضِيءُ وَلَوْ لَمْ تَمْسَسْهُ نَارٌ نُّورٌ عَلَىٰ نُورٍ يَهْدِي اللَّـهُ لِنُورِهِ مَن يَشَاءُ وَيَضْرِبُ اللَّـهُ الْأَمْثَالَ لِلنَّاسِ وَاللَّـهُ بِكُلِّ شَيْءٍ عَلِيمٌ ﴿٣٥﴾

35. Mwenyezi Mungu ni nuru ya mbingu na ardhi. Mfano wa nuru yake ni kama shubaka ndani yake mna taa. Taa hiyo imo katika tungi. Tungi hilo ni kama nyota inayomeremeta, inayowashwa kwa mafuta yanayotokana na mti uliobarikiwa, mzaituni. Si wa mashariki wala magharibi. Yanakurubia mafuta yake kung'aa ingawa hayajaguswa na moto - Nuru juu ya nuru. Mwenyezi Mungu humuongoza kwenye nuru yake amtakaye. Na Mwenyezi Mungu huwapigia watu mifano; na Mwenyezi Mungu ni mwenye kujua kila kitu.

فِي بُيُوتٍ أَذِنَ اللَّـهُ أَن تُرْفَعَ وَيُذْكَرَ فِيهَا اسْمُهُ يُسَبِّحُ لَهُ فِيهَا بِالْغُدُوِّ وَالْآصَالِ ﴿٣٦﴾

36. Katika nyumba ambazo Mwenyezi Mungu ameruhusu ziinuliwe na kutajwa humo jina lake, wanamtakasa humo asubuhi na jioni.

رِجَالٌ لَّا تُلْهِيهِمْ تِجَارَةٌ وَلَا بَيْعٌ عَن ذِكْرِ اللَّـهِ وَإِقَامِ الصَّلَاةِ وَإِيتَاءِ الزَّكَاةِ يَخَافُونَ يَوْمًا تَتَقَلَّبُ فِيهِ الْقُلُوبُ وَالْأَبْصَارُ ﴿٣٧﴾

37. Watu ambao biashara wala kuuza hakuwashughulishi na kumdhukuru Mwenyezi Mungu, na kuisimamisha Swala na kutoa Zaka. Wanaihofu siku ambayo nyoyo na macho yatageuka.

لِيَجْزِيَهُمُ اللَّـهُ أَحْسَنَ مَا عَمِلُوا وَيَزِيدَهُم مِّن فَضْلِهِ وَاللَّـهُ يَرْزُقُ مَن يَشَاءُ بِغَيْرِ حِسَابٍ ﴿٣٨﴾

38. Ili Mwenyezi Mungu awalipe mazuri ya yale waliyoyatenda, na awazidishie katika fadhila zake. Na Mwenyezi Mungu humruzuku amtakaye bila ya hisabu.

MWENYEZI MUNGU NI NURU YA MBINGU NA ARDHI

Aya 35 – 38

MAANA

Mwenyezi Mungu (s.w.t) kwenye Kitabu chake kitukufu, mara nyingi ameashiria kwenye ukuu wa ulimwengu na vilivyomo ndani yake. Lengo la kumfahamisha mtu ukuu wa ulimwengu ni kumfahamisha ukuu wa huyo aliyeufanya huo ulimwengu na awe na yakini ya Mola wake na Muumba wake. Mwenyezi Mungu (s.w.t) ametaja katika baadhi ya Aya kwamba kuumba ulimwengu ni kukubwa zaidi kuliko kuumba mtu.

Hilo Mwenyezi Mungu (s.w.t) amelitaja katika Aya kadhaa; kama:

أَأَنتُمْ أَشَدُّ خَلْقًا أَمِ السَّمَاءُ بَنَاهَا ﴿٢٧﴾

"Je, nyinyi ni wenye umbo gumu zaidi au mbingu alizozijenga?" (79:27)

لَخَلْقُ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ أَكْبَرُ مِنْ خَلْقِ النَّاسِ وَلَـٰكِنَّ أَكْثَرَ النَّاسِ لَا يَعْلَمُونَ ﴿٥٧﴾

"Bila shaka kuumba mbingu na ardhi ni kukubwa zaidi kuliko kuumba watu, lakini watu wengi hawajui" (40:57).

Mbingu na ardhi kwa mpangilio wake, nidhamu yake na utaratibu wake ni dalili kubwa na iliyo wazi zaidi ya ukuu wa muumba katika uweza wake, ujuzi wake na hekima yake.

Kwa kuwa kuumba ulimwengu ni dalili wazi zaidi ya kuweko Mwenyezi Mungu na kwa kuwa nuru ndiyo iliyo wazi zaidi ya uwazi wote, ndio Mwenyezi Mungu (s.w.t) akasema:

Mwenyezi Mungu ni nuru ya mbingu na ardhi.

Makusudio ya nuru ya Mwenyezi Mungu ni ukuu wake katika uweza wake, ujuzi wake na hekima yake. Ukuu huu unajitokeza katika kuumba ulimwengu. Kila kitu katika ardhi yake mbingu yake na kinafahamisha kwa mfahamisho ulio wazi juu ya kuweko kwake Mwenyezi Mungu na ukuu wake.

Hapa inatubainikia kuwa hakuna tofauti baina ya kusema: Mbingu na ardhi ni nuru ya Mwenyezi Mungu na kusema kuwa Mwenyezi Mungu ni nuru ya mbingu na ardhi.

Kwa sababu maana ya jumla ya kwanza ni kuwa ukuu wa ulimwengu unafahamisha ukuu wa Mwenyezi Mungu na maana ya jumla ya pili ni kuwa ukuu wa Mwenyezi Mungu unajitokeza kwenye ukuu wa ulimwengu. Ni sawa na kusema; Mpangilio mzuri wa jengo hili unafahamisha umahiri wa mjengaji au umahiri wa mjengaji unajitokeza katika mpangilio mzuri wa jengo hili.

Mfano wa nuru yake ni kama shubaka ndani yake mna taa, taa hiyo imo katika tungi, tungi hilo ni kama nyota inayomeremeta, inayowashwa kwa mafuta yanayotokana na mti uliobarikiwa, mzaituni. Si wa mashariki wala magharibi. Yanakurubia mafuta yake kun'gaa ingawa hayajaguswa na moto.

Huu ni mfano alioutoa Mwenyezi Mungu (s.w.t) kuweka wazi dalili za kuweko kwake Mwenyezi Mungu; kwamba dalili hizo ziko kwenye kila sehemu ya ulimwengu.

Muhtasari wa mfano huu ni taa iliyowekwa kwenye ukuta wa nyumba ikiwa na mwanga wala haifikiwi na upepo kwa vile iko kwenye kandili ya kioo ambacho ni safi kikimeremeta kama nyota inayoangaza.

Mafuta yenyewe yametokana na mzaituni ambao sio kuwa unapata jua linapochomoza tu au linapotua bali unapata jua wakati wote kwa sababu unaelekea jua, wala haupatwi na kivuli cha mti wala mlima. Ndio maana mafuta yake ni safi yanayotoa mwanga yenyewe kabla ya kuunguzwa, na yanapochomwa ndio yanatoa mwanga zaidi.

Nuru juu ya nuru. Nuru ya mafuta safi na nuru ya taa. Yaani Taa ime- ongeza mwangaza kutokana na usafi wa mafuta, usafi wa kioo, uthibiti wa shubaka ukutani na kutopata mvumo wa upepo.

Mwenyezi Mungu humuongoza kwenye nuru yake amtakaye.

Ikiwa watafuata njia aliyoiweka kwa ajili ya uongofu, kwa sababu Mwenyezi Mungu (s.w.t) ni mwenye hekima, hafanyi mambo hovyo hovyo. Wale ambao anawaongoza na kuwathibitisha ni wale ambao wanaona dalili zake Mwenyezi Mungu na kuzifanyia kazi.

Mwenyezi Mungu amewaashiria katika Aya zinazofuatia kwa kusema: 'Watu ambao biashara wala kuuza hakuwashughulishi na kumdhukuru Mwenyezi Mungu.'

Na Mwenyezi Mungu huwapigia watu mifano ikiwemo hiyo iliyotajwa, "Ili aangamie wa kuangami kwa dalili dhahiri na awe hai wa kuwa hai kwa dalili dhahiri" Juz. 10 (8:42).

Na Mwenyezi Mungu ni mwenye kujua kila kitu.

Anajua wenye kukana na kuzifanyia inadi dalili zake zenye kuenea na awalipe Jahannam ambayo ni makazi mabaya.

Katika nyumba ambazo Mwenyezi Mungu ameruhusu ziinuliwe na kutajwa humo jina lake.

Makusudio ya nyumba hapa ni misikiti, na kuinuliwa ni kujengwa. Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kutaja kwamba Yeye humuongoza kwenye nuru yake amtakaye, sasa anataja misikiti na kwamba yeye ameruhusu ijengwe kwa sababu waumini wanaswali humo.

Wanamtakasa humo asubuhi na jioni. Watu ambao biashara wala kuuza hakuwashughulishi na kumdhukuru Mwenyezi Mungu, na kuisimamisha Swala na kutoa Zaka.

Makusudio ya biashara hapa ni kinaya cha kazi yoyote ambayo ni kwa ajili ya dunia. Imetajwa biashara kwa sababu ndio yenye faida sana na yenye matumizi mengi.

Maana ni kuwa waumini wanafanya kazi kwenye masoko, mashambani, viwandani n.k., na wakati huo wakifanya kwa ajili ya akhera.

Wanaswali, wanafunga wanatoa Zaka na kuhiji. Kwa hiyo sio dunia inayowashughulisha kuicha akhera wala akhera, haiwafanyi waiache dunia. Kutokana na kauli yake Mwenyezi Mungu:

وَابْتَغِ فِيمَا آتَاكَ اللَّـهُ الدَّارَ الْآخِرَةَ وَلَا تَنسَ نَصِيبَكَ مِنَ الدُّنْيَا ﴿٧٧﴾

" Na utafute kwa aliyokupa Mwenyezi Mungu makazi ya akhera wala usisahu fungu lako katika dunia." (28:77).

Wanaihofu siku ambayo nyoyo na macho yatageuka.

Hiki ni kinaya cha fazaa watakayoipata wakosefu. Ama wale wema watakuwa katika amani ili Mwenyezi Mungu awalipe mazuri ya yale waliyoyatenda, katika matendo mema. Imam Ali(a.s ) anasema:"Hatafuzu kwa kheri ila aliyeifanya na wala hatalipwa malipo ya shari ila aliyeifanya."

Na awazidishie katika fadhila zake zaidi na zaidi.

Na Mwenyezi Mungu humruzuku amtakaye bila ya hisabu; yaani bila ya kustahiki, bali kwa fadhila zake na ukarimu. Amesema mwenye kitabu Al- asfar:

"Ambaye kitabu chake hakina maovu, ataingia Peponi bila ya hisabu. Na yule ambaye kitabu chake hakina mema ataingia motoni bila ya hisabu. Watakaohisabiwa ni wale ambao wamechanganya mema na maovu."

10

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA NANE

وَالَّذِينَ كَفَرُوا أَعْمَالُهُمْ كَسَرَابٍ بِقِيعَةٍ يَحْسَبُهُ الظَّمْآنُ مَاءً حَتَّىٰ إِذَا جَاءَهُ لَمْ يَجِدْهُ شَيْئًا وَوَجَدَ اللَّـهَ عِندَهُ فَوَفَّاهُ حِسَابَهُ وَاللَّـهُ سَرِيعُ الْحِسَابِ ﴿٣٩﴾

39. Na wale ambao wamekufuru vitendo vyao ni kama sarabi jangwani, mwenye kiu huyadhania ni maji, hata akiyaendea hapati chochote. Na atamkuta Mwenyezi Mungu hapo naye amlipe hisabu yake sawasawa. Na Mwenyezi Mungu ni mwepesi wa kuhisabu.

أَوْ كَظُلُمَاتٍ فِي بَحْرٍ لُّجِّيٍّ يَغْشَاهُ مَوْجٌ مِّن فَوْقِهِ مَوْجٌ مِّن فَوْقِهِ سَحَابٌ ظُلُمَاتٌ بَعْضُهَا فَوْقَ بَعْضٍ إِذَا أَخْرَجَ يَدَهُ لَمْ يَكَدْ يَرَاهَا وَمَن لَّمْ يَجْعَلِ اللَّـهُ لَهُ نُورًا فَمَا لَهُ مِن نُّورٍ ﴿٤٠﴾

40. Au ni kama giza katika bahari kuu, iliyofunikwa na mawimbi juu ya mawimbi na juu yake yapo mawingu-Giza juu ya giza. Akiutoa mkono wake anakurubia asiuone. Na ambaye Mwenyezi Mungu hakumjaalia kuwa na nuru, basi hawi na nuru.

أَلَمْ تَرَ أَنَّ اللَّـهَ يُسَبِّحُ لَهُ مَن فِي السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ وَالطَّيْرُ صَافَّاتٍ كُلٌّ قَدْ عَلِمَ صَلَاتَهُ وَتَسْبِيحَهُ وَاللَّـهُ عَلِيمٌ بِمَا يَفْعَلُونَ ﴿٤١﴾

41. Je, huoni kwamba Mwenyezi Mungu vinamtaksa vilivyomo mbinguni na ardhini na ndege wakikunjua mbawa zao? Kila mmoja amekwishajua Swala yake na tasbihi yake. Na Mwenyezi Mungu ni Mjuzi wa wayatendayo.

وَلِلَّـهِ مُلْكُ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ وَإِلَى اللَّـهِ الْمَصِيرُ ﴿٤٢﴾

42. Na ni wa Mwenyezi Mungu ufalme wa mbingu na ardhi, na kwa Mwenyezi Mungu ndio marejeo.

VITENDO VYAO NI KAMA SARABI (MANGATI)

Aya 39 – 42

MAANA

Na wale ambao wamekufuru vitendo vyao ni kama sarabi jangwani, mwenye kiu huyadhania ni maji, hata akiyaendea hapati chochote.

Makusudio ya makafiri hapa ni wale wanaokana utume wa Muhammad, kwa sababu ya inadi, ubaguzi, kupuuza au uzembe; yaani hakuutafuta uhakika akiwa ana uwezo wa kufanya utafiti na kuchunguza.

Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kuwataja wale ambao mambo ya dunia hayawafanyi wakaacha akhera na kwamba yeye atawalipa kwa yale mema waliyoyafanya, sasa anawataja hawa wapinzani wakanushaji, kwamba wao wametegemea batili na wakaitakidi kuwa ni haki itakayowafaa mbele ya Mwenyezi Mungu; sawa na mwenye kiu anavyotegemea mazigazi. Akitaka kuyafikia basi anakuta ni jua kali linalomzidishia kiu.

Wala hakuhusika na wasifa huu yule anayemkufuru Mwenyezi Mungu au utume wa Muhammad(s.a.w. w ) tu. Isipokuwa wanahusika wengi katika umma wa Muhammad(s.a.w. w ) ambao wanajidhania kuwa ni watu wa heri na takua, huku wakiwafanyia chuki na hasadi waja wa Mwenyezi Mungu na wakiipupia dunia na majanga yake.

Na atamkuta Mwenyezi Mungu hapo naye amlipe hisabu yake sawa-sawa. Na Mwenyezi Mungu ni mwepesi wa kuhisabu.

Kumkuta Mwenyezi Mungu ni kukuta hisabu yake na malipo yake. Maana ni kuwa kafiri anaitakidi akiwa duniani kwamba yeye ataokoka na adhabu ya Mwenyezi Mungu kutokana na amali njema aliyoifanya, lakini atakaposimama mbele ya Mwenyezi Mungu ili aangalie hisabu, hatapata kitu katika vile alivyoviwazia; bali atakuta dhambi, hisabu na adhabu. Matumaini yote yatayeyuka, kama yalivyoyeyuka ya yule aliyetegemea mangati.

Au ni kama giza katika bahari kuu, iliyofunikwa na mawimbi juu ya mawimbi na juu yake yapo mawingu. Giza juu ya giza. Akiutoa mkono wake anakurubia asiuone.

Bahari kuu ni bahari yenye maji mengi, mawimbi yamepandana na juu yake kuna mawingu mazito. Huu ni mfano fasaha zaidi wa watu wenye matamanio ambao wamezama katika bahari ya maovu na machafu: uongo, riya, mifundo, majisifu, kiburi, tamaa, pupa na mengineyo yasiyokuwa na kikomo. Mwenye kuishi katika giza hili ambalo haoni kitu, ataona vipi hakika na kuielewa.

Na ambaye Mwenyezi Mungu hakumjaalia kuwa na nuru, basi huyo hana nuru.

Tabrasi amesema: "Makusudio ni ambaye Mwenyezi Mungu hakumjaalia wokovu katika akhera, basi hana uokovu." Tuonavyo sisi ni kuwa wale ambao hawaongoki kwenye njia ya haki aliyowapa muongozo Mwenyezi Mungu, basi wao wataishi katika kuzubaa, ujinga na upotevu.

Je, huoni kwamba Mwenyezi Mungu vinamtaksa vilivyomo mbinguni na ardhini na ndege wakikunjua mbawa zao? Kila mmoja amekwishajua Swala yake na tasbihi yake. Na Mwenyezi Mungu ni Mjuzi wa wayatendayo.

Umepita mfano wake katika Juz. 15 (17:44).

Na ni wa Mwenyezi Mungu ufalme wa mbingu na ardhi, kwa sababu ndiye aliyeziumba na muumba ni mfalme wa kweli.

Na kwa Mwenyezi Mungu ndio marejeo ya hisabu na malipo.

أَلَمْ تَرَ أَنَّ اللَّـهَ يُزْجِي سَحَابًا ثُمَّ يُؤَلِّفُ بَيْنَهُ ثُمَّ يَجْعَلُهُ رُكَامًا فَتَرَى الْوَدْقَ يَخْرُجُ مِنْ خِلَالِهِ وَيُنَزِّلُ مِنَ السَّمَاءِ مِن جِبَالٍ فِيهَا مِن بَرَدٍ فَيُصِيبُ بِهِ مَن يَشَاءُ وَيَصْرِفُهُ عَن مَّن يَشَاءُ يَكَادُ سَنَا بَرْقِهِ يَذْهَبُ بِالْأَبْصَارِ ﴿٤٣﴾

43. Je, huoni kwamba Mwenyezi Mungu huyasukuma mawingu, kisha huyaambatanisha pamoja, kisha huyafanya mrundo? Basi utaona mvua ikitokea kati yake. Na huteremsha kutoka mbinguni, kwenye milima ya mawingu, mvua ya mawe, akamsibu nayo amtakaye na akamuepusha nayo amtakaye. Hukurubia mmemetuko wa umeme wake kupofua macho.

يُقَلِّبُ اللَّـهُ اللَّيْلَ وَالنَّهَارَ إِنَّ فِي ذَٰلِكَ لَعِبْرَةً لِّأُولِي الْأَبْصَارِ ﴿٤٤﴾

44. Mwenyezi Mungu hubadilisha usiku na mchana. Hakika katika hilo kuna mazingatio kwa wenye busara.

وَاللَّـهُ خَلَقَ كُلَّ دَابَّةٍ مِّن مَّاءٍ فَمِنْهُم مَّن يَمْشِي عَلَىٰ بَطْنِهِ وَمِنْهُم مَّن يَمْشِي عَلَىٰ رِجْلَيْنِ وَمِنْهُم مَّن يَمْشِي عَلَىٰ أَرْبَعٍ يَخْلُقُ اللَّـهُ مَا يَشَاءُ إِنَّ اللَّـهَ عَلَىٰ كُلِّ شَيْءٍ قَدِيرٌ ﴿٤٥﴾

45. Na Mwenyezi Mungu amemuumba kila mnyama kutokana na maji. Wengine katika wao huenda kwa matumbo, na wengine huenda kwa miguu miwili na wengine huenda kwa minne. Mwenyezi Mungu huumba ayatakayo. Hakika Mwenyezi Mungu ni Muweza wa kila kitu.

لَّقَدْ أَنزَلْنَا آيَاتٍ مُّبَيِّنَاتٍ وَاللَّـهُ يَهْدِي مَن يَشَاءُ إِلَىٰ صِرَاطٍ مُّسْتَقِيمٍ ﴿٤٦﴾

46. Hakika tumeteremsha Ishara zinazobainisha. Na Mwenyezi Mungu humuongoza atakaye kwenye njia iliyonyooka.

MAJI

Aya 43 – 46

MAANA

Je, huoni kwamba Mwenyezi Mungu huyasukuma mawingu, kisha huyaambatanisha pamoja, kisha huyafanya mrundo. Basi utaona mvua ikitokea kati yake. Na huteremsha kutoka mbinguni, kwenye milima ya mawingu, mvua ya mawe.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) hupeleka upepo unoasukuma mawingu kutoka mji mmoja hadi mwingine, kisha huyakusanya pamoja yakiwa mrundo kwa umbo la mlima. Kwenye mawingu haya kunakuwa na maji yanayomiminika na yanayoganda katika vipande vya theluji ambavyo ndivo vinavyoitwa mvua ya mawe.

Akamsibu nayo amtakaye na akamuepusha nayo amtakaye.

Mwenyezi Mungu kutumia mvua ya mawe kwa mujibu wa hekima. Ikiwa hekima imepitisha kuangamia mimea au kitu chochote, basi huipelekea mvua; vinginevyo huiepusha.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 13 (13: 12 -13). Huko na sehemu nyingine zinazonasibiana nazo tumeeleza kuwa dhahiri ya ulimwengu inategemea sababu zake za kimaumbile moja kwa moja na zinakomea kwake Mwenyezi Mungu Mtukufu kwa kuwa ndiye muumba wa ulimwengu na vilivyomo ndani yake.

Hukurubia mmemetuko wa umeme wake kupofua macho.

Umeme wake ni wa hayo mawingu. Mahali pengine Mwenyezi Mungu anasema: "Unakurubia umeme kunyakua macho yao." Juz. 1 (2:20).

Mwenyezi Mungu hubadilisha usiku na mchana, kwa urefu na ufupi.

Hakika katika hilo la kubadilishakuna mazingatio kwa wenye busara, ambao hawagandi tu kwenye sababu za maumbile, bali wanamtafuta aliyezifanya na kuzitengeneza na kumtambua.

Na Mwenyezi Mungu amemuumba kila mnyama kutokana na maji. Wengine katika wo huenda kwa matumbo, na wengine huenda kwa miguu miwili na wengine huenda kwa minne.

Hakika uweza wa Mwenyezi Mungu na umoja una ushahidi mwingi usiokuwa na idadi. Miongoni mwao ni ule unajitokeza katika kuumba vitu vilivyoganda, tunayoyashuhudia katika uumbaji mimea, wanyama na wanaotembea ardhini.

Hayo ndiyo yaliyoashiriwa katika Aya hii. Tukiangalia mfungamano wa maji katika kutengenezwa mnyama ni kuwa hakika ya maji ni moja, lakini wanyama walioumbwa kutokana na maji hayo wanatofautiana, wengine wanatembea kwa tumbo, kama wale wanaotambaa, wengine wanatembea kwa miguu miwili, kama binadamu na wengine kwa miguu mine, kama ngamia nyumbu wanyama mwitu na wengineo ambao Mwenyezi Mungu amewaashiria kwa kauli yake:

Mwenyezi Mungu huumba ayatakayo. Hakika Mwenyezi Mungu ni Muweza wa kila kitu.

Wanyama wote, kuanzia aina ndogo hadi kubwa, wako kwenye nidhamu kamili, ambapo kila mmoja anafanya kuliangana na inavyoafikiana na maslahi yake. Hii ni dalili mkataa kwamba nyuma ya yote hayo kuna mpangaji aliye hodari na mwenye hekima.

Hakika tumeteremsha Ishara zinazobainisha.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) ameleta dalili za kuweko kwake, ukuu wake na umoja wake; kama hizi za kuumba aina mbalimbali za wanyama. Hakuacha udhuru wowote kwa mwenye kutafuta sababu. Imam Ali(a.s) anasema:"Amewabunia umbile la ajabu katika vyenye uhai na visivyokuwa na uhai na vilivyotulia na vyenye harakati, akaweka ushahidi na ubainifu katika utovu wa utengenezaji wake na ukuu wa cheo chake, kiasi cha akili kuweza kumfuata na kumkubali na kusalimu amri kwake."

Na Mwenyezi Mungu humuongoza atakaye kwenye njia iliyonyooka.

Hakuna shaka kwamba mwenye kufuata njia iliyonyooka ambayo Mwenyezi Mungu ameiamrisha basi huyo ameongoka mbele ya Mwenyezi Mungu. Lakini mwenye kuasi amri yake Mwenyezi Mungu Mtukufu, huyo amepotea kwa Mungu na kwa watu wote, hilo halina shaka.

وَيَقُولُونَ آمَنَّا بِاللَّـهِ وَبِالرَّسُولِ وَأَطَعْنَا ثُمَّ يَتَوَلَّىٰ فَرِيقٌ مِّنْهُم مِّن بَعْدِ ذَٰلِكَ وَمَا أُولَـٰئِكَ بِالْمُؤْمِنِينَ ﴿٤٧﴾

47. Na wanasema tumeamini Mwenyezi Mungu na Mtume na tumetii. Kisha kikundi katika hao hugeuka baada ya hayo. Wala wao si wenye kuamini.

وَإِذَا دُعُوا إِلَى اللَّـهِ وَرَسُولِهِ لِيَحْكُمَ بَيْنَهُمْ إِذَا فَرِيقٌ مِّنْهُم مُّعْرِضُونَ ﴿٤٨﴾

48. Na wanapoitwa kwa Mwenyezi Mungu na Mtume wake ili awahukumu baina yao, ndipo kikundi kimoja kinakataa.

وَإِن يَكُن لَّهُمُ الْحَقُّ يَأْتُوا إِلَيْهِ مُذْعِنِينَ ﴿٤٩﴾

49. Na ikiwa haki ni yao wanamjia kwa kutii.

أَفِي قُلُوبِهِم مَّرَضٌ أَمِ ارْتَابُوا أَمْ يَخَافُونَ أَن يَحِيفَ اللَّـهُ عَلَيْهِمْ وَرَسُولُهُ بَلْ أُولَـٰئِكَ هُمُ الظَّالِمُونَ ﴿٥٠﴾

50. Je, wana maradhi katika nyoyo zao au wanaona shaka au wanahofia kuwa atawadhulumu Mwenyezi Mungu na Mtume wake? Bali wao ndio madhalimu.

إِنَّمَا كَانَ قَوْلَ الْمُؤْمِنِينَ إِذَا دُعُوا إِلَى اللَّـهِ وَرَسُولِهِ لِيَحْكُمَ بَيْنَهُمْ أَن يَقُولُوا سَمِعْنَا وَأَطَعْنَا وَأُولَـٰئِكَ هُمُ الْمُفْلِحُونَ ﴿٥١﴾

51. Haiwi kauli ya waumini wanapoitwa kwa Mwenyezi Mungu na Mtume wake, ila ni kusema: Tumesikia na tumetii. Na hao ndio wenye kufaulu.

وَمَن يُطِعِ اللَّـهَ وَرَسُولَهُ وَيَخْشَ اللَّـهَ وَيَتَّقْهِ فَأُولَـٰئِكَ هُمُ الْفَائِزُونَ ﴿٥٢﴾

52. Na wenye kumtii Mwenyezi Mungu na Mtume wake na wakamwogopa Mwenyezi Mungu na wakamcha, basi hao ndio wenye kufuzu.

وَأَقْسَمُوا بِاللَّـهِ جَهْدَ أَيْمَانِهِمْ لَئِنْ أَمَرْتَهُمْ لَيَخْرُجُنَّ قُل لَّا تُقْسِمُوا طَاعَةٌ مَّعْرُوفَةٌ إِنَّ اللَّـهَ خَبِيرٌ بِمَا تَعْمَلُونَ ﴿٥٣﴾

53. Na waliapa kwa Mwenyezi Mungu kwa ukomo wa viapo vyao ya kwamba ukiwaamrisha, hakika watatoka. Sema: msiape! Utiifu unajulikana. Hakika Mwenyezi Mungu ana habari za mnayoyatenda.

قُلْ أَطِيعُوا اللَّـهَ وَأَطِيعُوا الرَّسُولَ فَإِن تَوَلَّوْا فَإِنَّمَا عَلَيْهِ مَا حُمِّلَ وَعَلَيْكُم مَّا حُمِّلْتُمْ وَإِن تُطِيعُوهُ تَهْتَدُوا وَمَا عَلَى الرَّسُولِ إِلَّا الْبَلَاغُ الْمُبِينُ ﴿٥٤﴾

54. Sema: mtiini Mwenyezi Mungu na Mtume wake. Kama mkikengeuka basi yaliyo juu yake ni aliyobebeshwa, na yaliyo juu yenu ni mliyobebeshwa. Na mkimtii yeye mtaongoka na hapana juu ya mtume ila kufikisha (ujumbe) wazi wazi.

WANAFIKI

Aya 47 – 54

MAANA

Na wanasema tumeamini Mwenyezi Mungu na Mtume na tumetii. Kisha kikundi katika hao hugeuka baada ya hayo. Wala wao si wenye kuamini.

Ambao husema tumeamini na tumetii, wako aina tatu: Ya kwanza, ni wale wanaosema kwa ulimi yale wanayoyaamini, kuyakubali moyoni na kufanya kwa mujibu wake. Hawa sio waliokusudiwa kwenye Aya tuliyo nayo.

Aina ya pili, ni wale wanaosema na kuamini, lakini wanaasi wala hawatendi kwa mujibu wake; yaani wanamini kinadharia sio kimatendo.

Aina ya tatu, ni wale wanaosema kwa ndimi zao yale ambayo hayamo nyoyoni mwao kabisa. Hawa ndio wanafiki.

Aya tuliyo nayo inahusu aina ya pili na ya tatu; wala haihusiki na wanafiki tu; kama ilivyosemekana. Kwa sababu imani bila matendo haina faida yoyote, kwa dalili ya kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Basi mtu haitamfaa imani yake ambaye hakuamini zamani au hakuchuma kheri kwa imani yake" Ju. 8 (6:158).

Na wanapoitwa kwa Mwenyezi Mungu na Mtume wake ili awahukumu baina yao, ndipo kikundi kimoja kinakataa.

Wafasiri wengi wanasema kuwa kulitokea ugomvi wa ardhi baina ya mnafiki mmoja na Yahudi. Mnafiki akasema tukaamuliwe kwa Ka'bul-akhbar, Myahudi, kwa kujua kuwa anakubali rushwa. Myahudi akamwambia tukahukumiwe kwa Muhammad kwa kujua kuwa hakubali rushwa. Lakini mnafiki alikataa. Ndio ikashuka Aya hii. Ni sawa iwe riwaya ni sahihi au la, lakini inafafanua zaidi tafisiri ya Aya.

IJARIBU DINI YAKO NA IMANI YAKO

Na ikiwa haki ni yao wanamjia kwa kutii.

Wao hawaijui haki ila ikiafikiana na matamanio yao; kama ikihalifiana nayo basi wanaikana. Huu ndio ubinafsi ambao hauhusiki na wanafiki tu; isipokuwa uko katika maisha ya baadhi ya waumini au wale wanaojiita waumin. Wanadai kuwa wanaidhihirisha haki na wanipinga batili. Lakini ni haki gani hiyo wanayoidhihirisha na batili gani hiyo wanayoipinga?

Katika ufahamu wao na imani yao, haki ni ile inayoafikiana na masilahi yao na batili ni ile inayohalifiana na masilahi yao. Wao wamejisahau.

Wanaamini kuwa hawatendi isipokuwa haki na hawatamki isipokuwa ukweli, lakini hawapati msukumo wa hilo, isipokuwa kwa msukumo wa hawaa na masilahi yao.

Hawa wana hali mbaya zaidi kuliko wanafiki ambao wanawadanganya watu na hawajidanganyi wao wenyewe. Kwa sababu wana uhakika na uongo wao na riya yao.

Lakini hawa wanafanya uovu wenyewe wakijiona wanafanya wema. Sio siri kusema kuwa wao hawana sifa ya imani. Kwa sababu mumin wa kweli hahadaiki na hila za shetani na ubatilifu wake; bali anajituhumu ikiwa kitendo chake kitampambia sifa. Kwani kazi muhimu ya shetani ni kuwapambia watu matendo yao maovu, kuwaonyesha batili kuwa ni haki na upotevu kuwa ni unyoofu.

Inasemekana kuwa mtu mmoja alimwambia Iblisi: "Wewe huwawezi waumini mfano wangu." Ibilisi akacheka na kumwambia maneno yako haya tayari yanaonyesha umekwishaingia kwenye mtego. Ghururi yako hii ni mtekelezaji aliyeingia moyoni mwako, akauharibu na akaupofusha mpaka ukawa hauna hisia.

Baada ya hayo! Mwenye kutaka kuijaribu imani na dini yake, inatakikana aangalie kuwa je, anaituhumu nafsi yake au anaiona ni safi isiyokuwa na kasoro? Je, anaikubali haki hata kama ni dhidi yake? Ikiwa atajituhumu na kuikubali haki kwa namna yoyote itakayokuwa basi yeye ni katika waumini, vinginevyo atakuwa katika walioangamia.

Je, wana maradhi katika nyoyo zao au wanaona shaka au wanahofia kuwa Mwenyezi Mungu na Mtume wake watawadhulumu? Bali wao ndio madhalimu.

Walikataa kuhukumiwa kwa Mtume; wala hakuna lililopelekea hilo ila chuki yao kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu au kuutilia shaka utume wake au kuhofia kuwa atawadhulumu. Sababu yoyote itakayokuwa, lakini hakatai hukumu ya Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w. w ) isipokuwa kafiri au aliyeidhulumu nafsi yake na ya mwingine.

Haiwi kauli ya waumini wanapoitwa kwa Mwenyezi Mungu na Mtume wake, ila ni kusema: Tumesikia na tumetii. Na hao ndio wenye kufaulu.

Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kutaja wanafiki na kwamba wao wana- jizuia kuiendea mahakama ya Mtume wanapoitwa huko, sasa anataja waumini, kwamba ni wale wanaomwitikia kila atakayewapa mwito wa kwenda kwa Mwenyezi Mungu na Mtume wake na wanaitikia mwito wake kwa unyenyekevu na utiifu. Hawa ndio wanachama wa Mwenyezi Mungu"Hakika wanachama wa Mwenyezi Mungu ndio wenye kufanikiwa." (58:22)

Na wenye kumtii Mwenyezi Mungu na Mtume wake na wakamwogopa Mwenyezi Mungu na wakamcha, basi hao ndio wenye kufuzu kwa kupata radhi za Mwenyezi Mungu na pepo yake.

Kuunganisha hofu na uchaji kwenye utiifu, ni kwa upande wa kuunganisha kitafsiri. Kwa sababu mwenye kumtii Mwenyezi Mungu atakuwa amemuhofia na kumcha. Lakini wafasiri hawakukubali ila kutafoutisha baina ya matendo haya. Wakasema: kumtii Mwenyezi Mungu kunakuwa katika aliyoyaamrisha na kuyakataza, kumhofia kunakuwa katika maasi na kumcha kunakuwa katika yatakayokuja.

Na waliapa kwa Mwenyezi Mungu kwa ukomo wa viapo vyao ya kwamba ukiwaamrisha, hakika watatoka.

Walioapa ni wanafiki. Wao waliaapa kwa kiapo cha nguvu kwamba Mtume akiwaamrisha waache majumba yao na mali zao basi watamsikiliza na kumtii, ndipo Mwenyezi Mungu (s.w.t) akawakemea na imani yao hiyo ya uongo kwa kusema:

Sema: msiape! Utiifu unajulikana. Hakika Mwenyezi Mungu ana habari za mnayoyatenda.

Yaani ewe Muhammad! Waambie wanafiki, msiape kwani Mwenyezi Mungu anajua kuwa utiifu wenu huu ni wa uongo na wa kujionyesha (ria) na kwamba nyinyi ni maadui wa Mwenyezi Mungu na Mtume wake na amewaandalia adhabu chungu mnayostahiki.

Sema: Mtiini Mwenyezi Mungu na Mtume wake kwa dhahiri na batini, sio kwa unafiki na ria. Kama mkikengeuka basi yaliyo juu yake ni aliyobebeshwa, na yaliyo juu yenu ni mliyobebeshwa.

Wanaambiwa wanafiki, na yaliyo juu yake ni juu yake Mtume. Maana ni kuwa Mtume ni mwenye kukalifiwa kufikisha na nyinyi ni wenye kukalifiwa kutii. Atakayepuuza basi hisabu ya kupuuza itakuwa ni yake; ni sawa awe ni Mtume au yule aliyetumiwa Mtume.

Na mkimtii yeye mtaongoka na hapana juu ya mtume ila kufikisha (ujumbe) wazi wazi. Mwenye kutekeleza aliyokalifishwa, basi malipo yake yako kwa Mwenyezi Mungu.

Mtume amekwishafikisha na kutekeleza wajibu wake, yaliyobaki, kazi kwenu.