TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TISA Juzuu 19

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TISA0%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TISA Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: Qurani tukufu

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TISA

Mwandishi: Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya
: HASANI MWALUPA
Kundi:

Matembeleo: 7430
Pakua: 1928


Maelezo zaidi:

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 14 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 7430 / Pakua: 1928
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TISA

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TISA Juzuu 19

Mwandishi:
Swahili

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TISA

IMEANDIKWA NA: SHEIKH MUHAMMAD JAWAD MUGHNIYYA

IMETAFSIRIWA NA: SHEIKH HASAN MWALUPA

IMEHARIRIWA NA: USTADH ABDALLAH MOHAMED

IMEPANGWA KATIKA KOMPYUTA NA: UKHT PILI RAJABU

UTANGULIZI WA MCHAPISHAJI

Kitabu hiki kilichoko mikononi mwako hivi sasa ni juhudi ya miaka mingi sana ya watu waliojitolea kuona kazi hii imefanikiwa bila ya kumsahau Marhum Abu Muhammad wa London.

Kama lilivyo jina la Tafsiri ndivyo ilivyo Tafsiri yenyewe ambayo mwanachuoni huyu mahiri kabisa aliyeifafanua ni mtu aliyebobea katika fani zote ambazo mfasiri (Mfafanuzi) anatakiwa awe nazo.

Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya ameonesha cheche zake katika vitabu vingi alivyoviandika katika maudhui mbali mbalimbali na hivyo kujipatia wasomaji wengi sana.

Msomi huyu, mwenye fikra huru na anayetetea kile anachokiamini, ni mtu mwenye mawazo mapana na kuyaangalia mambo kwa undani sana, kipaumbele chake ni katika maslahi ya umma huu na amejaribu sana kwenda na wakati.

Sifa kubwa pekee ya mwanachuoni huyu ni kuwa yeye hakujihusisha sana na kung'ang'ania madhehebu fulani tu, labda hii yatokana na wadhifa wake wa ukadhi aliokuwa nao katika nchi ya Lebanon ambayo ina madhehebu mengi, ambapo sula la madhehebu ni nyeti nchini humo, hata hivyo yeye aliweza kuamua matatizo ya watu kwenye ofisi yake kulingana na madhehebu yao pale walipomwendea. Hiyo ilimsaidia sana hata kuweza kutoa kitabu kitwacho Al-Fiqh a'laa madhaahabil-khamsah (Fikhi ya madhehebu matano) yaani ya Hanafi, Maaliki, Shafi, Hambali na Shia (ambacho twataraji kitatoka kwa lugha ya kiswahili hivi karibuni Inshaallah).

Jambo lililotupa msukumo wa kukifasiri kitabu hiki kwa lugha ya Kiswahili ni zile faida nyingi atakazozipata msomaji na kujua mambo mengi na ya ajabu yaliyo mapya kwake ambayo si rahisi kuyapata kwa wafasiri wengine.

Msomaji atapata faida katika fani za Sayansi, Siasa, Historia, Mashairi, visa vizuri, na Saikolojia miongoni mwa mengine; ndiyo maana msomaji atashangaa kidogo anapoisoma Tafsiri hii atakapoona mwandishi amewataja na kuwanukuu watu kama kina Mfalme Edward, wanasayansi kama kina Enstein, wasanii kama Charlie Champlin (Mchekeshaji maarufu), na wengineo, hali inayoifanya tafsiri hii kuwa ni ya kipekee kabisa.

Mtindo alioutumia mwandishi ni sahali uliokusudiwa watu wa tabaka mbalimbali, wanavyuoni na watu wa kawaida.

Nia yetu ni kukigawanya kitabu hiki bure lakini tumelazimika kukiuza kwa bei nafuu ili kurudisha gharama za uchapishaji.

Mwisho: Shukrani kubwa iwaendee bila ya kuwataja watu waliojitolea usiku na mchana, jopo la wafasiri, wahariri, wachapaji, waliotupa moyo na kutoa maoni yao na walioisimamia ili kuhakikisha kwamba kitabu kimemfikia msomaji.

MAKOSA YA CHAPA

Sikumbuki kama nimewahi kusoma kitabu kilichotoka kupigwa chapa, cha zamani au cha sasa, bila ya kukuta makosa ya chapa, Nafikiri sitasoma kitabu kisichokuwa hivyo. Nimejaribu sana kuliepuka hilo katika tungo zangu, lakini sikufanikiwa.

Nilikuwa sifikirii kama ninaweza kuona makosa haya katika maandishi ya msahafu mtukufu, kama yale yaliyo katika baadhi ya chapa; kwa mfano neno yabswutu kwa swad, badala ya yabsutu kwa sin, na katika chapa ya Tafsir Arrazi ya Misr ya mwaka 1935, Sura ya (2:146), Imeandikwa La Ya'alamuun, (hawajui) badala ya Ya'alamuun (wanajua). Mfano wa makosa haya hausameheki.

Katika Tafsir Al-Manar, chapa ya Pili, sura (5:212), imeandikwa Fawqahum ila yawmil qiyama badala ya Fawqahum yawamal qiyama. Hatuwezi kusema kosa hili ni kubwa zaidi kuliko lile.

Lakini mkosaji atatuletea udhuru kwa msemo mashuhuri huko kwetu Jabal amil 'Makosa ya chapa.'

Katika Tafsiri Majmau chapa ya Urfan, Sura (46:15), imeandikwa: Hatta idha balagha arbai' na sanah badala ya: Hattaidha balagha ashuddahu arbai ' na sanah"

Kusema hivi sio kama ninajitetea kutokana na makosa ya chapa atakayoyakuta msomaji katika kitabu hiki, ijapokuwa naomba msamaha kama litatokea hili, lakini makusudio yangu hasa ni kumwambia yule atakayefungua macho yake kwenye makosa ya matamko na kuufungia macho uzuri wa maana.

Vilevile ninamwambia yule ambaye siku moja aliniambia: "Vitabu vyako vimejaa makosa ya chapa.” Kama kwamba hakuna kitu chochote katika vitabu hivyo isipokuwa makosa ya chapa tu. Wote hao ninawaambia: Mungu awasamehe na aniongoze mimi na nyinyi.

Vyovyote iwavyo, mimi ninaomba msamaha kutokana na makosa ya kifikra na ya chapa. Anasema Amirul Muminiin(a.s) :"Watu wote ni wapungufu wenye kuchanganyikiwa, isipokuwa yule aliyehifadhiwa na Mwenyezi Mungu." Na Mwenyezi Mungu (s.w.t) ndiye mwenye jukumu la kunikubalia yale niliyoyapatia na kunisamehe niliyakosea, kwa jaha ya Mtume na kizazi chake, ziwashukie rehema na amani (Amin).

MUHAMMAD JAWAD MUGHNIYYAH

1

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TISA

Mwendelezo Wa Sura Ya Ishirini Na Tano: Surat Al-Furqan.

وَقَالَ الَّذِينَ لَا يَرْجُونَ لِقَاءَنَا لَوْلَا أُنزِلَ عَلَيْنَا الْمَلَائِكَةُ أَوْ نَرَىٰ رَبَّنَا لَقَدِ اسْتَكْبَرُوا فِي أَنفُسِهِمْ وَعَتَوْا عُتُوًّا كَبِيرًا ﴿٢١﴾

21. Na walisema wale wasiotarajia kukutana nasi: Mbona sisi hatuteremshiwi Malaika au hatumwoni Mola wetu. Hakika wametakabari katika nafsi zao na wameasi uasi mkubwa.

يَوْمَ يَرَوْنَ الْمَلَائِكَةَ لَا بُشْرَىٰ يَوْمَئِذٍ لِّلْمُجْرِمِينَ وَيَقُولُونَ حِجْرًا مَّحْجُورًا ﴿٢٢﴾

22. Siku watakayowaona Malaika, haitakuwa furaha siku hiyo kwa wakosefu, na watasema: Kuwe na kizuizi kizuiacho.

وَقَدِمْنَا إِلَىٰ مَا عَمِلُوا مِنْ عَمَلٍ فَجَعَلْنَاهُ هَبَاءً مَّنثُورًا ﴿٢٣﴾

23. Na tutayaendea yale waliyoyatenda katika matendo, kisha tutayafanya mavumbi yaliyotawanyika.

أَصْحَابُ الْجَنَّةِ يَوْمَئِذٍ خَيْرٌ مُّسْتَقَرًّا وَأَحْسَنُ مَقِيلًا ﴿٢٤﴾

24. Watu wa Peponi siku hiyo watakuwa katika makazi bora na mapumziko mazuri zaidi.

وَيَوْمَ تَشَقَّقُ السَّمَاءُ بِالْغَمَامِ وَنُزِّلَ الْمَلَائِكَةُ تَنزِيلًا ﴿٢٥﴾

25. Siku itakapopasuka mbingu kwa mawingu na watateremshwa malaika kwa wingi.

الْمُلْكُ يَوْمَئِذٍ الْحَقُّ لِلرَّحْمَـٰنِ وَكَانَ يَوْمًا عَلَى الْكَافِرِينَ عَسِيرًا ﴿٢٦﴾

26. Ufalme wa haki siku hiyo utakuwa wa Mwingi wa rehema. Na itakuwa siku ngumu kwa makafiri.

وَيَوْمَ يَعَضُّ الظَّالِمُ عَلَىٰ يَدَيْهِ يَقُولُ يَا لَيْتَنِي اتَّخَذْتُ مَعَ الرَّسُولِ سَبِيلًا ﴿٢٧﴾

27. Na siku dhalimu atajiuma mikono yake akisema: Laiti ningelishika njia pamoja na Mtume!

يَا وَيْلَتَىٰ لَيْتَنِي لَمْ أَتَّخِذْ فُلَانًا خَلِيلًا ﴿٢٨﴾

28. Ee ole wangu! Laiti nisingelimfanya fulani kuwa rafiki.

لَّقَدْ أَضَلَّنِي عَنِ الذِّكْرِ بَعْدَ إِذْ جَاءَنِي وَكَانَ الشَّيْطَانُ لِلْإِنسَانِ خَذُولًا ﴿٢٩﴾

29. Kwa hakika amenipoteza nikaacha dhikri baada ya kunijia, na shetani ndiye anayemtupa mtu.

HAKUNA FURAHA KWA WAKOSEFU

Aya 21 – 29

MAANA

Na walisema wale wasiotarajia kukutana nasi: Mbona sisi hatuteremshiwi Malaika au hatumwoni Mola wetu.

Bado maneno yanaendelea kuwahusu washirikina, wasiotarajia kukutana na Mola wao, wala kuhofia adhabu yake.

Mwenyezi Mungu (s.w.t), katika Aya hii, amewazungumzia kwamba wao wamependekeza washuke Malaika ili wawape habari kuwa Muhammad ni Nabii au aje Yeye mwenyewe Mwenyezi Mungu atoe habari hiyo. Umetangulia mfano wake katika Juz. 15 (17:92)

Hakika wametakabari katika nafsi zao na wameasi uasi mkubwa.

Kuna kiburi gani kikubwa zaidi kuliko jeuri yao hii ya kutaka kumuona Mungu na kuzungumza naye ana kwa ana? Hawa hawana tofauti na wale waliosema kuwa hatumwamini Mungu mpaka tumuone, wakati huo wanaamini vitu ambavyo haviingii katika hisia yoyote.

Watu wa kimaada wanadai kuwa hakuna kitu chochote isipokuwa asili pofu ambayo ilijileta yenyewe au ilipatikana kwa sadfa, na ndiyo iliyoupangilia ulimwengu huu wa ajabu na iliyoumba usikizi na uoni. Katika mantiki yao ni kwamba asili ndiyo iliyo na uwezo wa kila kitu, lakini hiyo yenyewe haitambui kitu.

Wao wanajipinga wenyewe, kwa sababu kukubali kwao kupatikana nidhamu, ni kukiri kuweko nguvu yenye uwezo na ujuzi; na kusema kwao kuwa hakuna chochote isipokuwa asili pofu ni kuikana nguvu hiyo. Maana yake ni kuwa asili ina utambuzi na haina utambuzi, inajua na haijui.

Siku watakayowaona Malaika, haitakuwa furaha siku hiyo kwa wakosefu.

Washirikina walipendekeza washukiwe na malaika, ndipo Mwenyezi Mungu (s.w.t) akawajibu kuwa kutakuwa na siku ambayo watawaona malaika, Siku ya Kiyama, lakini hakutakuwa na jambo la kuwafurahisha , bali ni majanga juu ya majanga yatakayowapata:

يَوْمَ يَغْشَاهُمُ الْعَذَابُ مِن فَوْقِهِمْ وَمِن تَحْتِ أَرْجُلِهِمْ وَيَقُولُ ذُوقُوا مَا كُنتُمْ تَعْمَلُونَ ﴿٥٥﴾

“Siku itakapowafunika adhabu kutoka juu yao na chini ya miguu yao, na atasema: Onjeni hayo mliyokuwa mkiyatenda” (29:55).

Na watasema: Kuwe na kizuizi kizuiacho.

Watakaosema ni malaika. Maana ni kuwa malaika watawaambia wakosefu, leo ni haramu mtazuiwa kuona mnayoyataka.

Imesemekana kuwa watakaosema ni wakosefu kuwaambia malaika kuwa haifai nyinyi leo kutuudhi na kutuadhibu.

Tafsiri zote mbili zinafaa na zinarejea kwenye maana moja ambayo ni kuhofia wakosefu shari ya siku ya Kiyama na vituko vyake.

Na tutayaendea yale waliyoyatenda katika matendo, waliyodhani kuwa yatawafaa leo,kisha tutayafanya mavumbi yaliyotawanyika.

Kwa sababu yalikuwa kwenye misingi isiyokuwa ya imani wala ikhalsi: “Mfano wa wale ambao wamemkufuru Mola wao vitendo vyao ni kama majivu yanayopeperushwa kwa nguvu za upepo katika siku ya kimbunga. Hawana uwezo wa chochote juu ya walichokichuma. Huko ndiko kupotelea mbali.” Juz. 13 (14:18).

Watu wa Peponi siku hiyo watakuwa katika makazi bora na mapumziko mazuri zaidi.

Makusudio ya bora na zaidi sio uzaidi wa mengine, isipokuwa makusudio ni kuwa makazi na mapumziko hayo yenyewe ni bora na mazuri; ni kama kusema Mwenyezi Mungu ni mkubwa zaidi, kwa maana ya kuwa ni mkubwa zaidi katika dhati yake na sifa zake.

Siku itakapopasuka mbingu kwa mawingu.

Makusudio ya siku hapa ni Siku ya Kiyama; na mawingu ni sayari ambazo zitakuwa chembechembe zisizoweza kuonekana hata kwa macho, zitaijaza anga, kama vile mawingu. Mwenyezi Mungu (s.w.t) ameashiria kuharibika kwa Siku hiyo, kwenye Aya nyingi; kama vile:

إِذَا الشَّمْسُ كُوِّرَتْ ﴿١﴾

“Jua litakapokunjwa.” (81:1),

وَإِذَا الْكَوَاكِبُ انتَثَرَتْ ﴿٢﴾

“Na nyota zitakapotawanyika.” (82:2).

Yaani jua litakapozimika na nyota zitakapoanguka.”

Na watateremshwa malaika kwa wingi, wakiwa na ya kuwafurahisha wema na kuwachukiza wakosefu.

Ufalme wa haki siku hiyo utakuwa wa Mwingi wa rehema Yeye tu peke yake, hakuna atakayekuwa na lolote.

Na itakuwa siku ngumu kwa makafiri.

Hakuna siku ngumu zaidi kwa mkosefu kuliko siku ya kuhukumiwa kwake, kuhisabiwa makosa yake na kutolewa hukumu ya haki na uadilifu? Lau angelihukumiwa kunyongwa ingelikuwa mambo yamekwisha, lakini ni hukumu ya kudumu:

كُلَّمَا نَضِجَتْ جُلُودُهُم بَدَّلْنَاهُمْ جُلُودًا غَيْرَهَا لِيَذُوقُوا الْعَذَابَ ﴿٥٦﴾

“Kila zitakapoiva ngozi zao, tutawabadilishia ngozi nyingine ili waonje adhabu.” Juz.5 (4:56).

Na siku dhalimu atajiuma mikono yake akisema: Laiti ningelishika njia pamoja na Mtume!

Hiki ni kinaya cha majuto na masikitiko. Hapo ndio ukomo wa kila mwenye kughurika, mzushi na muongo. Miongoni mwa dua zilipokewa kutoka kwa Nabii(s.a.w.w) ni:“Ewe Mola wangu! Najilinda kwako na madhambi yanayoleta majuto.”

Ee ole wangu! Laiti nisingelimfanya fulani kuwa rafiki.

Makusudio ya fulani hapa ni kila mwenye kufuatwa aliyempoteza mfuasi wake na kumwongoza kwenye maangamizi. Kuna Hadith isemayo:“Mtu atafufuliwa kwenye dini ya rafiki yake.”

Jamaa katika wafasiri wamesema kuwa Aya hii ilimshukiwa Uqba bin Mu’it na Ubayya bin Khalaf. Kwamba dhalimu atakayeuma mikono yake ni huyo wa kwanza na fulani ni huyo wa pili. Hata kama tukikadiria usahihi wa riwaya, ni kuwa sababu ya kushuka Aya haizuwii kuenea kwa wengine.

Hakika amenipoteza nikaacha dhikri baada ya kunijia, na shetani ndiye anayemtupa mtu.

Makusudio ya dhikri hapa ni Qur’an, kwa sababu Mwenyezi Mungu (s.w.t) amelitumia neno hili kwa kukusudia Qur’an katika Aya kadhaa; kama vile:

ص وَالْقُرْآنِ ذِي الذِّكْرِ ﴿١﴾

“Naapa kwa Qur’an yenye dhikri.” (38:1).

Aya inafahamisha kuwa wale walioisikiza Qur’an walikinai kwenye nafsi zao, lakini mashetani-watu waliwadanganya na wakawaepusha na haki, ikawa mwisho wao ni kufedheka. Na huu ndio mwisho wa kila mwenye kufanya kwa maelekezo ya watu wa hawa, si kwa maelekezo ya imani yake na dhamiri yake.

وَقَالَ الرَّسُولُ يَا رَبِّ إِنَّ قَوْمِي اتَّخَذُوا هَـٰذَا الْقُرْآنَ مَهْجُورًا ﴿٣٠﴾

30. Na Mtume alisema: Ewe Mola wangu! Hakika watu wangu wameifanya hii Qur’an ni mahame.

وَكَذَٰلِكَ جَعَلْنَا لِكُلِّ نَبِيٍّ عَدُوًّا مِّنَ الْمُجْرِمِينَ وَكَفَىٰ بِرَبِّكَ هَادِيًا وَنَصِيرًا ﴿٣١﴾

31. Na hivi hivi tumemfanyia kila Nabii adui miongoni mwa wakosefu. Na Mola wako anatosha kuwa mwenye kuongoza na mwenye kunusuru.

وَقَالَ الَّذِينَ كَفَرُوا لَوْلَا نُزِّلَ عَلَيْهِ الْقُرْآنُ جُمْلَةً وَاحِدَةً كَذَٰلِكَ لِنُثَبِّتَ بِهِ فُؤَادَكَ وَرَتَّلْنَاهُ تَرْتِيلًا ﴿٣٢﴾

32. Na walisema wale ambao wamekufuru: Mbona haikuteremshwa kwake Qur’an yote mara moja? Ndivyo hivyo, ili tuuimarishe kwayo moyo wako, na ndio tumeisoma kwa mafungu.

وَلَا يَأْتُونَكَ بِمَثَلٍ إِلَّا جِئْنَاكَ بِالْحَقِّ وَأَحْسَنَ تَفْسِيرًا ﴿٣٣﴾

33. Wala hawatakuletea mfano wowote ila nasi tutakuletea haki na tafsiri iliyonzuri.

الَّذِينَ يُحْشَرُونَ عَلَىٰ وُجُوهِهِمْ إِلَىٰ جَهَنَّمَ أُولَـٰئِكَ شَرٌّ مَّكَانًا وَأَضَلُّ سَبِيلًا ﴿٣٤﴾

34. Wale watakaokusanywa kifudifudi kwenye Jahannam, hao watakuwa mahali pabaya na ndio wenye kupotea njia sana.

وَلَقَدْ آتَيْنَا مُوسَى الْكِتَابَ وَجَعَلْنَا مَعَهُ أَخَاهُ هَارُونَ وَزِيرًا ﴿٣٥﴾

35. Na hakika tulimpa Musa Kitabu na tukamuweka pamoja naye nduguye, Harun, kuwa waziri.

فَقُلْنَا اذْهَبَا إِلَى الْقَوْمِ الَّذِينَ كَذَّبُوا بِآيَاتِنَا فَدَمَّرْنَاهُمْ تَدْمِيرًا ﴿٣٦﴾

36. Tukawaambia nendeni kwa watu waliozikadhibisha Ishara zetu, basi tukawaangamiza kabisa.

وَقَوْمَ نُوحٍ لَّمَّا كَذَّبُوا الرُّسُلَ أَغْرَقْنَاهُمْ وَجَعَلْنَاهُمْ لِلنَّاسِ آيَةً ۖ وَأَعْتَدْنَا لِلظَّالِمِينَ عَذَابًا أَلِيمًا ﴿٣٧﴾

37. Na watu wa Nuh walipowakadhibisha mitume, tuliwagharikisha na tukawafanya ni ishara kwa watu. Na tumewaandalia madhalimu adhabu chungu.

وَعَادًا وَثَمُودَ وَأَصْحَابَ الرَّسِّ وَقُرُونًا بَيْنَ ذَٰلِكَ كَثِيرًا ﴿٣٨﴾

38. Na kina Ad na Thamud na watu Rass na vizazi vingi vilivyokuwa baina yao.

وَكُلًّا ضَرَبْنَا لَهُ الْأَمْثَالَ وَكُلًّا تَبَّرْنَا تَتْبِيرًا ﴿٣٩﴾

39. Na wote tuliwapigia mifano na wote tuliwaangamiza kabisa kabisa.

وَلَقَدْ أَتَوْا عَلَى الْقَرْيَةِ الَّتِي أُمْطِرَتْ مَطَرَ السَّوْءِ أَفَلَمْ يَكُونُوا يَرَوْنَهَا بَلْ كَانُوا لَا يَرْجُونَ نُشُورًا ﴿٤٠﴾

40. Na kwa hakika wao walifika kwenye mji ulionyeshewa mvua mbaya, basi je hawakua wakiuona? Bali walikuwa hawatarajii kufufuliwa.

WAMEIFANYA QUR’AN NI MAHAME

Aya 30 – 40

MAANA

Na Mtume alisema: Ewe Mola wangu! Hakika watu wangu wameifanya hii Qur’an ni mahame.

Yaani wameachana nayo na wakakataa kuiamini au kuipa mtazamo wa kutafuta haki ili kuwa na yakini nayo. Vigogo wa kikuraishi waliukadhibisha unabii wa Muhammad(s.a.w.w) na yaliyosemwa na Qur’an kwa kuhofia uchumi wao na kupupia vyeo vyao.

Ndipo Mtume akapeleka mashtaka yake kwa Mola wake ambaye mambo yote yako mikononi mwake. Hivi ndivyo afanyavyo mwenye akili, hashtakii haja yake isipokuwa kwa yule ambaye hukumu ya mashtaka hayo iko mikononi mwake.

Ndio, inawezekana mtu kumshtakia rafiki yake atakayemliwaza na kumpa moyo. Imam Jafar Sadiq(a.s) amesema:“Mwenye kumshtakia ndugu yake amemshitakia Mwenyezi Mungu, na mwenye kumshtakia mwingine atakuwa amemshtaki Mungu.” Anakusudia ndugu wa kiimani, na kwamba muuminii akimshtakia muuminii kama yeye humwombea Mungu ampe faraja na kumwamrisha awe na subira, kumtegemea Mwenyezi Mungu na kutokata tamaa na rehema yake Mwenyezi Mungu Mtukufu, lakini akimshitakia asiyekuwa muumini humshakizia au kumshauri kuepukana na Mungu.

Na hivi hivi tumemfanyia kila Nabii adui miongoni mwa wakosefu.

Mkombozi anaweza akamwambia taghuti, ewe mkosefu, na kumlaumu kwa ufisadi, upotevu na kuvunja haki za binadamu na mengineyo, lakini taghuti ametulia tu, wala hajali. Umetangulia mfano wake katika Juz. 8 (6:112).

Huko tumejibu swali la: Ikiwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) ndiye aliyewajaalia Manabii wawe na maadui, kama inavyoonyesha Aya, kwa nini basi awaadhibu kwa kuwafanyia uadui Mitume?

Na Mola wako anatosha kuwa mwenye kuongoza na mwenye kunusuru.

Maneno yanaelekezwa kwa Mtume(s.a.w.w) yakiwa na ahadi kutoka kwake Mwenyezi Mungu Mtukufu kumsaidia Mtume wake kutokana na maadui zake; kama alivyomsadia kumuongoza kwenye haki na kuidhihirisha dini yake kuliko dini zote, wajapochukia washirikina.

Na walisema wale ambao wamekufuru: Mbona haikuteremshwa kwake Qur’an yote mara moja?

Qur’an ilishuka kwa vipindi kulingana na haja ya watu. Mwanzo wa kushuka kwake ulikuwa pale Mtume(s.a.w.w) alipokuwa na miaka arubaini ya umri wake mtukufu. Ukaendelea wahyi kushuka polepole mpaka pale Mtume alipohama kwenda mahali pa hali ya juu akiwa na miaka 63.

Washirikina walijaribu kila mbinu kuwaepusha watu na Qur’an. Wakasema ni vigano vya watu wa kale, lakini hawakuendelea na mbinu hii, kwa sababu ilikuwa ikijipinga yenyewe. Wakatafuta propaganda nyingine, wakasema mbona Qur’an isiteremshwe mara moja, kwani Mungu anahitaji kufikiria, kama wafanyavyo watunzi?

Hata kama ingeliteremka mara moja wasingelikosa la kusema, kama kawaida ya wapinzani, kuwa mbona isingeliteremka kidogo kidogo ili tuweze kuifahamu, kuathirika nayo na kuizowea. Lakini ukweli hujitokeza, hata wakiupinga.

Ndivyo hivyo, ili tuuimarishe kwayo moyo wako, na ndio tumeisoma kwa mafungu.

Yaani tumeiteremsha Qur’an kwa mpangilio wa moja baada ya nyingine, ili moyo wake uwe na nguvu ya kuuhifadhi, kufahamu maana yake na kudhibiti hukumu zake.

Wala hawatakuletea mfano wowote ila nasi tutakuletea haki na tafsiri iliyo nzuri, wale watakaokusanywa kifudifudi kwenye Jahannam, hao watakuwa mahali pabaya na ndio wenye kupotea njia sana.

Maneno yanaelekezwa kwa Mtume(s.a.w.w) . Watakaoleta mfano na kufufuliwa kifudifudi ni washirikina. Makusudio ya mfano wowote ni kila wanalomtaaradhi nalo Mtume mtukufu.

Katika Aya ya 5, ya Sura hii kwenye Juzuu iliyopita, wanapinga kwa kusema kuwa ni ngano za watu wa kale, katika Aya ya 7, wanasema kwa nini anakula na kutembea sokoni, katika Aya 8, wanasema amerogwa, katika Aya ya 21, iliyo kwenye Juzuu hii, wanasema kwa nini hakuteremshiwa malaika au tumuone Mungu na katika Aya 32 wanasema kwa nini isiteremshwe mara moja.

Baada ya kuyabatilisha madai yao haya ndio Mwenyezi Mungu (s.w.t) hapa anamwambia Mtume wake:‘Wala hawatakuletea mfano wowote ila nasi tutakuletea haki na tafsiri iliyo bora’

Yaani washirikina watakujadili kwa batili na sisi tutakuunga mkono kwa haki iliyo wazi na hoja ambayo itavunja kauli zao na kufedhesha batili zao. Hiyo ni hapa duniani. Ama malipo yao huko akhera, ni kuwa mazabania watawavuta kwenye nyuso zao.

Ambaye atakuwa katika hali hii huyo ndiye muovu wa viumbe vya Mungu na mwenye makazi mabaya zaidi.

Na hakika tulimpa Musa Kitabu na tukamuweka pamoja naye nduguye, Harun, kuwa waziri. Tukawaambia nendeni kwa watu waliozikadhibisha Ishara zetu, basi tukawaangamiza kabisa.

Kisa cha Musa na Firauni kimekwishatangulia kwenye Aya kadhaa; miongoni mwazo ni: Juz.9 (7:103 – 145). Katika Juz. 16 (20:9), tumezungumzia sababu za kukaririka kisa cha Musa(a.s) .

Na watu wa Nuh walipowakadhibisha mitume, tuliwagharikisha na tukawafanya ni Ishara kwa watu. Na tumewaandalia madhalimu adhabu chungu.

Pia kisa cha Nuh kimekwishapita mara kadhaa. Tazama Juz.12 (11:25 – 49).

Na kina Ad na Thamud na watu a Rass.

Rass ni jina la kisima na watu wake ni kaumu ya Shu’ayb. Imetangulia mifano katika Juz. 12 (11:50 – 61 na 84 – 95).

Na vizazi vingi vilivyokuwa baina yao.

Yaani, vile vile tuliangamiza kaumu nyingi zilizokuwa baina ya kina Ad na watu wa Rass, kwa sababu wao waliwakadhibisha manabii na mitume.

Na wote tuliwapigia mifano na wote tuliwaangamiza kabisa kabisa.

Tuliwaangamiza baada ya ubainifu, onyo, mawaidha ya visa na kupiga mifano, lakini wao waling’ang’ania ukafiri na upotevu. Ikawa malipo yao ni kuangamizwa.

Na kwa hakika wao walifika kwenye mji ulionyeshewa mvua mbaya, basi je hawakua wakiuona? Bali walikuwa hawatarajii kufufuliwa.

Makusudio ya mji hapa ni mji wa kaumu ya Lut kutokana na kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu:

وَلُوطًا آتَيْنَاهُ حُكْمًا وَعِلْمًا وَنَجَّيْنَاهُ مِنَ الْقَرْيَةِ الَّتِي كَانَت تَّعْمَلُ الْخَبَائِثَ ﴿٧٤﴾

“Na Lut tukampa hukumu na elimu na tukamwokoa na ule mji uliokuwa ukifanya maovu.” Juz. 17 (21:74).

na pia kauli yake:

فَلَمَّا جَاءَ أَمْرُنَا جَعَلْنَا عَالِيَهَا سَافِلَهَا وَأَمْطَرْنَا عَلَيْهَا حِجَارَةً مِّن سِجِّيلٍ مَّنضُودٍ ﴿٨٢﴾

“Basi ilipofika amri yetu tuliigeuza juu chini. Na tukawateremshia mvua ya mawe ya udongo mkavu yaliyopandana.” Juz. 12 (11:82).

Maana ni kuwa washirikina walipokuwa kwenye misafara yao wakipitia mji wa Lut na kuona athari ya maangamizi na kubomoka, walitakiwa wapate funzo na waamini utume wa Muhammad, lakini wakapinga na kuwa na inadi, kwa sababu hawana yakini na ufufuo, hisabu na malipo.

2

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TISA

وَإِذَا رَأَوْكَ إِن يَتَّخِذُونَكَ إِلَّا هُزُوًا أَهَـٰذَا الَّذِي بَعَثَ اللَّـهُ رَسُولًا ﴿٤١﴾

41. Na wanapokuona hawakufanyii ila kejeli tu, ati huyu ndiye Mwenyezi Mungu aliyemtuma kuwa mtume?

إِن كَادَ لَيُضِلُّنَا عَنْ آلِهَتِنَا لَوْلَا أَن صَبَرْنَا عَلَيْهَا وَسَوْفَ يَعْلَمُونَ حِينَ يَرَوْنَ الْعَذَابَ مَنْ أَضَلُّ سَبِيلًا ﴿٤٢﴾

42. Kwa hakika alikuwa karibu kutupoteza kwa miungu yetu, kama tusingelikazana juu yao. Na karibu watajua watakapoiona adhabu, ni nani aliyepotea njia.

أَرَأَيْتَ مَنِ اتَّخَذَ إِلَـٰهَهُ هَوَاهُ أَفَأَنتَ تَكُونُ عَلَيْهِ وَكِيلًا ﴿٤٣﴾

43. Je, umemuona aliyeyafanya matamanio yake kuwa ndio Mungu wake? Basi je, wewe utakuwa ni wakili wake?

أَمْ تَحْسَبُ أَنَّ أَكْثَرَهُمْ يَسْمَعُونَ أَوْ يَعْقِلُونَ إِنْ هُمْ إِلَّا كَالْأَنْعَامِ بَلْ هُمْ أَضَلُّ سَبِيلًا ﴿٤٤﴾

44. Au unadhani kwamba wengi wao wanasikia na wanafahamu? Hao hawakuwa ila ni kama wanyama howa; bali wao wamepotea zaidi njia.

ATI HUYU NDIYE MTUME?

Aya 41 – 44

MAANA

BAINA YA ISA NA MUHAMMAD

Na wanapokuona hawakufanyii ila kejeli tu, ati huyu ndiye Mwenyezi Mungu aliyemtuma kuwa Mtume?

Kwa muda wa miaka 13, Mtume(s.a.w.w) alikuwa akiwalingania watu wake kwenye imani ya Mungu mmoja, akiamrisha uadilifu na kukataza dhulma. Mbele yake mweusi na mweupe walikuwa sawa. Vile vile tajiri na fukara. Hakuna kuzidiana isipokuwa kwa takua.

Si ajabu kuwa hili liliwafanya vigogo wa kikuraishi kumpa dhiki Muhammad(s.a.w.w) na kumkejeli kutokana na mwito wake huo. Mada ya usawa ndiyo waliyoitumia sana kumkejelia: Bilal, mtumwa fukara anawezaje kuwa sawa na Abu Jahl, mungwana na mwenye mali; tena ati awe bora zaidi yake kwa Mungu kwa vile ni mwenye takua! Ilikuwa ni ajabu hilo kwao.

Mtume(s.a.w.w) alivumilia maudhi yao, akaendelea na mwito wake. Kwa sababu yale anayoyapigania yanamfanya asijali lolote. Hivi ndivyo anavyokuwa imara mtu adhimu kwa wapumbavu na washari walio wapotevu; anategemea kuwa Mwenyezi Mungu yuko pamoja naye na kwamba kesho ni yake, kwa sababu batili itaisha tu hata kama muda utarefuka.

Mustafa Sadiq Rafi, analinganisha baina ya Isa(a.s) alipokejeliwa na wana wa Israil na Muhammad(s.a.w.w) alipokejeliwa na makuraish. Miongoni mwa aliyoyasema ni: “Walimkejeli Bwana Masih hapo zamani, akawaambia: Hakuna Mtume asiyetukuzwa isipokuwa mjini na nyumbani kwake. Hivi ndivyo alivyowajibu wale waliomdharau.

Lakini Mtume(s.a.w.w) hakuwajibu waliomkejeli hata pale alipokuwa na nguvu za uarabuni kote. Alikuwa hasemi isipokuwa lile analolifanyia kazi. Kunyamaza kwake kulikuwa na maneno mengi katika falsafa ya utashi, uhuru na maendeleo. Na kwamba hapana budi kuweko na mageuzi ya watu.

Na mti uchipue na utoe majani mapya yatakayoendeleza maisha. Yeye hakuchukia wala hakusema kitu. Alikuwa kama mtengenezaji ambaye hachukii wala kukata tamaa kwa kosa la kifaa, bali hupeleka mkono wake kurekebisha.

Ni juu yetu sisi waislamu katika somo hili kupata funzo la uthabiti, ukakamavu na kujitolea muhanga kwenye haki. Tusikate tamaa ya haki kuishinda batili hata kama watu wake ni wengi.

Kwa sababu miongoni mwao wamo waliodanganyika na uongo ambao utafichuka na kuyeyuka siku zikipita; kuna wale walioghafilika dhamiri zao na Mola wao, kisha watarejea na kutubia dhambi zao.

Vile vile haitakikani tumwamini kila anayedai ni mtetezi wa haki, kwa sababu wadanganyifu na wafanya biashara ya dini ni wengi.

Kwa hakika alikuwa karibu kutupoteza kwa miungu yetu, kama tusingelikazana juu yao.

Haya ni maneno ya makuraishi ambao walimdharau Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) . Wanasema haya kwa kujipinga wenyewe bila ya kujitambua. Wanakubali kuwa Muhammad alikurubia kuwatia shaka kwenye masanamu yao kutokana na dalili, hoja na miujiza iliyodhihiri mikononi mwake.

Vilevile walikubali kuwa akili zao walizisimamisha kwa hawa na matamaanio yao. “Kwa hakika alikuwa karibu kutupoteza kwa miungu yetu, kama tusingelikazana juu yao,” hiyo ni fedheha na kupingana na kejeli zao kwa Muhammad. Walimkejeli na wakati huo huo wanakubali kuwa ana nguvu ya hoja. Hivi ndivyo alivyo kila mbatilifu; maneno yake yanagongana bila ya kujitambua. Siri katika hilo ni kuwa haki inaelea haizami.

Na karibu watajua watakapoiona adhabu, ni nani aliyepotea njia.

Walisema kuwa Muhammad anakurubia kuwapoteza, ndipo Mwenyezi Mungu (s.w.t) akawajibu kuwa kesho mtakapokabiliana na vituko vikubwa ndio mtajua kuwa nyinyi ndio mliopotea na mlio na hasara, sio Muhammad na waliomwamini.

Je, umemuona aliyeyafanya matamanio yake kuwa ndio Mungu wake?

Kila ambaye matamanio yake yanashinda dini yake, atakuwa ameyafanya ndio mungu wake, atake asitake. Anayekuwa hivyo, hakuna matumaini ya kuongoka kwake. Kwa sababu kila hoja kwake ni upuzi, kwa vile inapingana na matamanio na matakwa yake.

Basi je, wewe utakuwa ni wakili wake?

Utakayemtetea na ufisadi na upotevu wake? Achana naye hana kheri yoyote. Umekwisha muonya. Basi ni juu yetu hisabu yake.

WAMEPOTEA ZAIDI KULIKO WANYAMA

Au unadhani kwamba wengi wao wanasikia na wanafahamu? Hao hawakuwa ila ni kama wanyama howa; bali wao wamepotea zaidi njia.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) amesema wengi wao, kwa sababu baadhi yao walipinga mwanzoni, kisha wakarejea, wakaelekea kwenye uongofu na wakaifuata. Mwenyezi Mungu akaondoa usikizi na akili kwa wale waliong’ang’ania upinzani, kwa sababu hawakunufaikia na usikizi wao wala akili zao. Kila ambalo halitumainiwi kupatikana ni sawa na kuwa haliko.

Mwenyezi Mungu, imetukuka hekima yake, amewafananisha na wanyama, kwa sababu wao hawakuzingatia dalili wala kuwaidhika na hekima na mazingatio; bali ni afadhali wanyama kuliko wao. Kwa sababu wanyama howa (wakufugwa) wanatekelza wajibu wao kulingana na maumbile yao; wanafuata amri na makatazo ya wachungaji wao; wanajua yanayowadhuru na kuayaacha na yanayowanufaisha wakayafanya.

Lakini wao wafisadi hawamfuati Muumba wao, hawaogopi adhabu yake wala hawatarajii thawabu zake. Zaidi ya hayo, wanyama hawamdhuru yoyote aliye jinsi yake na asiyekuwa jinsi yake; bali watu wananufaika nao kwa kuwapanda, maziwa na sufu zao. Ama wafisadi na wapotevu, wao ni balaa kwa jamii yao na ndio sababu ya majanga na chimbuko la kutoendelea.

Kwa hakika wasifu huu hauhusiki na yule anayemkufuru Mwenyezi Mungu au kumshirikisha tu. Kila anayeipinga haki pamoja na kuweko dalili na hoja, huyo atakuwa amepotea zaidi kuliko mnyama; ni sawa awe amepinga kwa kiburi na inadi au kwa uzembe na kupuuza dalili za haki na rejea zake.

أَلَمْ تَرَ إِلَىٰ رَبِّكَ كَيْفَ مَدَّ الظِّلَّ وَلَوْ شَاءَ لَجَعَلَهُ سَاكِنًا ثُمَّ جَعَلْنَا الشَّمْسَ عَلَيْهِ دَلِيلًا ﴿٤٥﴾

45. Je, umeona jinsi Mola wako alivyokitandaza kivuli? Na angelitaka angelikifanya kitulie. Kisha tukalifanya jua ni dalili yake.

ثُمَّ قَبَضْنَاهُ إِلَيْنَا قَبْضًا يَسِيرًا ﴿٤٦﴾

46. Kisha tukakivutia kwetu kidogo kidogo.

وَهُوَ الَّذِي جَعَلَ لَكُمُ اللَّيْلَ لِبَاسًا وَالنَّوْمَ سُبَاتًا وَجَعَلَ النَّهَارَ نُشُورًا ﴿٤٧﴾

47. Yeye ndiye aliyewafanyia usiku kuwa ni vazi na usingizi kuwa ni mapumziko na akaufanya mchana kuwa ni wa matawanyiko.

وَهُوَ الَّذِي أَرْسَلَ الرِّيَاحَ بُشْرًا بَيْنَ يَدَيْ رَحْمَتِهِ وَأَنزَلْنَا مِنَ السَّمَاءِ مَاءً طَهُورًا ﴿٤٨﴾

48. Naye ndiye anayezituma pepo kuwa bishara kabla ya rehema yake na tunayateremsha kutoka mbinguni maji twahara.

لِّنُحْيِيَ بِهِ بَلْدَةً مَّيْتًا وَنُسْقِيَهُ مِمَّا خَلَقْنَا أَنْعَامًا وَأَنَاسِيَّ كَثِيرًا ﴿٤٩﴾

49. Ili kwayo tuihuishe nchi iliyokufa na tuwanyweshe miongoni mwa wanyama tuliowaumba na watu wengi.

وَلَقَدْ صَرَّفْنَاهُ بَيْنَهُمْ لِيَذَّكَّرُوا فَأَبَىٰ أَكْثَرُ النَّاسِ إِلَّا كُفُورًا ﴿٥٠﴾

50. Na hakika tumeisarifu kati yao wapate kukumbuka, lakini watu wengi wamekataa ila kukufuru.

وَلَوْ شِئْنَا لَبَعَثْنَا فِي كُلِّ قَرْيَةٍ نَّذِيرًا ﴿٥١﴾

51. Na kama tungetaka tungepeleka katika kila mji muonyaji.

فَلَا تُطِعِ الْكَافِرِينَ وَجَاهِدْهُم بِهِ جِهَادًا كَبِيرًا ﴿٥٢﴾

52. Basi usiwatii makafiri na pambana nao kwayo kwa jihadi kubwa.

وَهُوَ الَّذِي مَرَجَ الْبَحْرَيْنِ هَـٰذَا عَذْبٌ فُرَاتٌ وَهَـٰذَا مِلْحٌ أُجَاجٌ وَجَعَلَ بَيْنَهُمَا بَرْزَخًا وَحِجْرًا مَّحْجُورًا ﴿٥٣﴾

53. Yeye ndiye aliyezichanganya bahari mbili , hii ni tamu mno na hii ni chumvi sana, na akaweka kinga kati yake na kizuizi kizuiacho.

وَهُوَ الَّذِي خَلَقَ مِنَ الْمَاءِ بَشَرًا فَجَعَلَهُ نَسَبًا وَصِهْرًا وَكَانَ رَبُّكَ قَدِيرًا ﴿٥٤﴾

54. Naye ndiye aliyemuumba mwanadamu kutokana na maji na akamjaalia kuwa na nasaba na ukwe. Na Mola wako ni mwenye uwezo.

DHAHIRI YA MAUMBILE

Aya 45 – 54

MAANA

Mwenyezi Mungu (s.w.t), katika Aya hizi, ametaja badhi ya neema alizozieneza kwa waja wake, ambazo zinafahamisha kuweko kwake na ukuu wake. Anatuzindua nazo Mungu Mtukufu ili tumwamini na tumwabudu kwa kumfanyia ikhlasi. Ufafanuzi ni kama ufuatavyo:-

Je, umeona jinsi Mola wako alivyokitandaza kivuli?

Makusudio ya kutaja kivuli, ni kukumbusha neema ya kivuli ambacho kinampatia mtu mapumziko na raha na kwamba Mwenyezi Mungu ndiye anayekiweka na kukiondoa.

Na angelitaka angelikifanya kitulie.

Yaani angeliifanya ardhi ikatulia, na kwa kutulia ardhi ndio kingetulia kivuli na kuwa katika hali moja. Kwa sababu kivuli hakina uhuru, kinamfuata mwenye kivuli hicho, akitaharaki nacho hutaharaki na akitingishika nacho hutingishika.

Kisha tukalifanya jua ni dalili yake.

Lau si kuweko jua, ardhi isingelikuwa na kivuli. Kwa hiyo kupatikana kwa jua kunajulisha kupatikana kivuli; sawa na kuweko sababu kunakofahamisha kuweko kinachosababishwa.

Kisha tukakivutia kwetu kidogo kidogo.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) anakitandaza kidogo kidogo, kisha anakiondoa kidogo kidogo kulingana na harakati za ardhi.

Mwenyezi Mungu Mtukufu amenasibisha kwake kivuli na kukitandaza na kukiondoa, pamoja na kuwa hilo linategemea ardhi moja kwa moja, kwa sababu yeye Mwenyezi Mungu ndiye muathiri wa kwanza wa kupatikana kwake na dhahiri ya maumbile ni nyenzo tu.

Yeye ndiye aliyewafanyia usiku kuwa ni vazi.

Hapa Mwenyezi Mungu (s.w.t) ameusifu usiku kuwa ni vazi na katika Juz. 7 (6:96) ameusifu kuwa ni utulivu. Maana zote mbili zinakurubiana. Kwa sababu kivazi kinazuia macho na utulivu hauna sauti itakayofikia masikio.

Na usingizi kuwa ni mapumziko.

Neno subata liliofasiriwa mapumziko, lina maana ya kustarehe na kuacha kufanya kazi.

Na akaufanya mchana kuwa ni wa matawanyiko ya harakati na kufanya kazi. Tafsiri iliyo wazi zaidi ya Aya hii ni ile Aya isemayo: “Na katika rehema zake ni kuwafanyia usiku na mchana mpate kupumzika humo na mtafute fadhila zake na ili mpate kushukuru.” (28:73).

Naye ndiye anayezituma pepo kuwa bishara kabla ya rehema yake na tunayateremsha kutoka mbinguni maji twahara.

Makusudio ya rehema zake hapa ni mvua. Maana ni kuwa upepo unaleta habari njema ya kushuka maji kutoka mbinguni, ambayo ni twahara na yanatwaharisha; kama wasemavyo mafaqihi.

Ili kwayo tuihuishe nchi iliyokufa na tuwanyweshe miongoni mwa wanyama tuliowaumba na watu wengi.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) kwenye neno lililofasiriwa nchi ametumia ‘Balda’ na kwenye Juz. 8 (7:58) ametumia neno ‘Balad’ maneno yote hayo yana maana moja.

Na hakika tumeisarifu kati yao wapate kukumbuka.

Inawezekana kuwa iliyosarifiwa ni Qur’an na maana yawe kama Juz. 15 (17:41): “Hakika tumekwishasarifu katika Qur’an hii ili wapate kukumbuka, lakini haiwazidishii isipokuwa kuwa mbali.”

Pia inawezekana iliyosarifiwa ni mvua. Maana yawe ni kwamba Mwenyezi Mungu (s.w.t) anaipeleka mvua kutoka sehemu moja hadi nyingine, kwa vile kama ingelibakia sehemu moja tu ingeleta uharibifu, pia kama ingelikatika kabisa wangelikufa na kiu.

Kila mwenye akili inampasa afikirie vizuri hekima na neema hii, ili amshukuru,lakini watu wengi wamekataa ila kukufuru. Yaani kumkana Mungu na kukufuru neema zake.

Na kama tungetaka tungepeleka katika kila mji muonyaji.

Kabla ya kutumwa Muhammad(s.a.w.w) Mwenyezi Mungu alituma Mtume kwa kila umma. Mwenyezi Mungu anasema:

وَلِكُلِّ أُمَّةٍ رَّسُولٌ ﴿٤٧﴾

“Na kila Umma una Mtume.” Juz. 11 (10:47).

Kuanzia zama za Muhammad(s.a.w.w) mpaka siku ya mwisho, Mwenyezi Mungu amefunga kupeleka mitume kwa viumbe na akatosheka na Mtume mmoja kwa viumbe wote ambaye ni Muhammad bin Abdillah(s.a.w.w) . Dini yake ndiyo dini ya mwisho kwa watu wote.

Ndio maana Mwenyezi Mungu (s.w.t) akachukua ahadi kwa kila Mtume kumtolea habari Muhammad na sifa zake:

“Na Mwenyezi Mungu alipochukua ahadi kwa manabii. Nikiwapa kitabu na hekima; kisha akawajia mtume msadikishaji wa yale yaliyo pamoja nanyi, ni juu yenu kumwamini na kumsaidia. Akasema: Je, mmekubali na mmechukua ahadi yangu kwa hayo? Wakasema: ‘Tumekubali.’ Akasema: basi shuhudieni, na mimi ni pamoja nanyi katika mashahidi.” Juz. 3 (3:81).

Hakuna aliye juu zaidi ya cheo hiki, isipokuwa Mwenyezi Mungu peke yake. Na amemkumbusha mwenye cheo hiki kwa kumwambia: ‘Na kama tungetaka tungepeleka katika kila mji muonyaji.’ Lakini hatukufanya; tumekuwakilisha wewe uzionye umma zote kwa kukuadhimisha, kwa sababu taadhima ina kiwango chake na uzito wake.

QUR’AN NA IDHAA

Basi usiwatii makafiri na pambana nao kwayo kwa jihadi kubwa.

Maneno yanaelekezwa kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) . Inafaa kukataza jambo, hata ikiwa inajulikana mwenye kukatazwa halifanyi kabisa; hasa ikiwa mkatazaji ni Mwenyezi Mungu Mtukufu. Kwayo ni kwa hiyo Qur’an.

Maana ni kuwa ewe Muhammad! Usiwaitikie makafiri kwa jambo lolote watakalokuitia; wala usiwache fursa yoyote ya kuitangaza Qur’an; uwasomee kwenye masikio yao, wapende wasipende. Na uvumilie maudhi yatakayokupata katika njia hii. Maudhi yao yasiwe ni kikwazo cha kui- tangaza; kwani kutangaza Aya za Mwenyezi Mungu ni jihadi kubwa katika njia ya haki na ya ubinadamu.

Lengo la msisitizo huu sio kuwanyamazisha wapinzani na mataghuti tu; isipokuwa ni kuwaamsha wanaokandamizwa na wasiofahamu na kuwaongoza kwenye uhuru wao ambao wameuchukua wenye nguvu; kwamba uadilifu na usawa ni haki ya kila mtu itokayo kwa Mungu; na kwamba hakuna mwenye nguvu wala tajiri au mtukufu isipokuwa kwa takua na amali njema.

Qur’an ndiyo inayodhamini haki hii. Hakuna dini wala sharia itakayoweza kutekeleza hilo ila ikiwa itasimamia uadilifu na usawa.

Hapa ndio tunajua siri iliyo katika kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu:

وَإِذَا قُرِئَ الْقُرْآنُ فَاسْتَمِعُوا لَهُ وَأَنصِتُوا لَعَلَّكُمْ تُرْحَمُونَ ﴿٢٠٤﴾

“Na isomwapo Qur’an isikilizeni na mnyamaze ili mpate kurehemiwa.” Juz. 9 (7:204).

Mwenyezi Mungu (s.w.t) alimwamrisha Mtume wake mtukufu kufanya juhudi kubwa ya kusoma Qur’an na kuitangaza, kwa sababu kwayo sauti ya haki na uadilifu itainuka na kuenea elimu na mwamko kwa watu. Hapo kila mtu atahisi heshima yake na kuilinda. Hapa inatubainikia kuwa kuisoma Qur’an katika idhaa zote za ulimwengu, sio kubainisha ufasaha kama wanavyodhani; isipokuwa umuhimu wa kwanza ni kuleta uadilifu na usawa kwa watu wote.

Yeye ndiye aliyezichanganya bahari mbili , hii ni tamu mno na hii ni chumvi sana, na akaweka kinga kati yake na kizuizi kizuiacho.

Makusudio ya bahari mbili katika Aya sio bahari mbili hasa; isipokuwa ni aina mbili za maji: moja ni tamu na nyingine ni chumvi. Neno bahari hutumiwa pia kwa maji mengi yawe chumvi au tamu.

Maana ni kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) ameyajaalia maji ya chumvi kwenye ardhi iliyoinama (pwani) na akajaalia maji tamu kwenye ardhi iliyo juu ya maji-chumvi (bara); kwa namna ambayo maji-tamu ya bara, yanaminika kwenye maji-chumvi ya pwani na maji-tamu yanabaki na utamu wake na maji-chumvi yanabaki na chumvi yake. Kama ingelikuwa kinyume, pwani ikawa juu na bara ikawa chini na maji yachanganyike, basi maji yote yangelikuwa chumvi na watu kuwa na matatizo.

Haya yote hayakutokea kisadfa; bali ni kwa makadirio ya mwenye hekima mjuzi. Kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu:’ na akaweka kati yake kinga na kizuizi kizuiacho’ ni kuwa aina mbili hizi za maji hata zikikutana hakuna moja inayozidi nyingine, bali kila moja inabakia na athari yake. Ametukuka ambaye ameumba kila kitu na akakikadiria kipimo.

Naye ndiye aliyemuumba mwanadamu kutokana na maji na akam- jaalia kuwa na nasaba na ukwe.

Makusudio ya nasaba ni udugu wa kuzaliwa na ukwe ni udugu unaotokana na kuoana. Maana ni kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) amemumba mtu, ambaye ni kiumbe wa ajabu, kutokana na manii na akajaalia udugu na kuhurumiana baina yao. Tazama Juz. 18: (23:12-14).

Na Mola wako ni mwenye uwezo.

Miongoni mwa uweza wake ni kumfanya mke na mume kutokana na chembe moja.