TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TISA Juzuu 19

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TISA0%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TISA Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: Qurani tukufu

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TISA

Mwandishi: Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya
: HASANI MWALUPA
Kundi:

Matembeleo: 7516
Pakua: 2028


Maelezo zaidi:

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 14 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 7516 / Pakua: 2028
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TISA

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TISA Juzuu 19

Mwandishi:
Swahili

5

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TISA

فَجُمِعَ السَّحَرَةُ لِمِيقَاتِ يَوْمٍ مَّعْلُومٍ ﴿٣٨﴾

38. Basi wakakusanywa wachawi wakati wa siku maalum.

وَقِيلَ لِلنَّاسِ هَلْ أَنتُم مُّجْتَمِعُونَ ﴿٣٩﴾

39. Na watu wakaambiwa: Je, mtakusanyika?

لَعَلَّنَا نَتَّبِعُ السَّحَرَةَ إِن كَانُوا هُمُ الْغَالِبِينَ ﴿٤٠﴾

40. Huenda tutawafuata wachawi wakiwa wao ndio watakaoshinda.

فَلَمَّا جَاءَ السَّحَرَةُ قَالُوا لِفِرْعَوْنَ أَئِنَّ لَنَا لَأَجْرًا إِن كُنَّا نَحْنُ الْغَالِبِينَ ﴿٤١﴾

41. Basi walipokuja wachawi wakamwambia Firauni: Je, tutapata ujira ikiwa tutashinda?

قَالَ نَعَمْ وَإِنَّكُمْ إِذًا لَّمِنَ الْمُقَرَّبِينَ ﴿٤٢﴾

42. Akasema: Ndio, hapo nanyi hakika mtakuwa miongoni mwa wanaokurubishwa.

قَالَ لَهُم مُّوسَىٰ أَلْقُوا مَا أَنتُم مُّلْقُونَ ﴿٤٣﴾

43. Musa akawaambia: Tupeni mnavyotaka kutupa.

فَأَلْقَوْا حِبَالَهُمْ وَعِصِيَّهُمْ وَقَالُوا بِعِزَّةِ فِرْعَوْنَ إِنَّا لَنَحْنُ الْغَالِبُونَ ﴿٤٤﴾

44. Wakatupa kamba zao na fimbo zao na wakasema: Kwa nguvu za Firauni hakika sisi bila shaka ni wenye kushinda.

فَأَلْقَىٰ مُوسَىٰ عَصَاهُ فَإِذَا هِيَ تَلْقَفُ مَا يَأْفِكُونَ ﴿٤٥﴾

45. Musa akatupa fimbo yake, mara ikavimeza walivyovibuni.

فَأُلْقِيَ السَّحَرَةُ سَاجِدِينَ ﴿٤٦﴾

46. Wachawi wakapomoka kusujudu.

قَالُوا آمَنَّا بِرَبِّ الْعَالَمِينَ ﴿٤٧﴾

47. Wakasema: Tumemwamini Mola wa Walimwengu.

رَبِّ مُوسَىٰ وَهَارُونَ ﴿٤٨﴾

48. Mola wa Musa na Harun.

قَالَ آمَنتُمْ لَهُ قَبْلَ أَنْ آذَنَ لَكُمْ إِنَّهُ لَكَبِيرُكُمُ الَّذِي عَلَّمَكُمُ السِّحْرَ فَلَسَوْفَ تَعْلَمُونَ لَأُقَطِّعَنَّ أَيْدِيَكُمْ وَأَرْجُلَكُم مِّنْ خِلَافٍ وَلَأُصَلِّبَنَّكُمْ أَجْمَعِينَ ﴿٤٩﴾

49. Akasema Firauni: Je, mmemwamini kabla sijawaruhusu. Hakika yeye ndiye mkubwa wenu aliyewafundisha uchawi, lakini punde mtajua. Nitawakata mikono yenu na miguu yenu kwa kubadilisha, kisha nitawasulubu nyote.

قَالُوا لَا ضَيْرَ إِنَّا إِلَىٰ رَبِّنَا مُنقَلِبُونَ ﴿٥٠﴾

50. Wakasema: Haidhuru, hakika sisi ni wenye kurejea kwa Mola wetu.

إِنَّا نَطْمَعُ أَن يَغْفِرَ لَنَا رَبُّنَا خَطَايَانَا أَن كُنَّا أَوَّلَ الْمُؤْمِنِينَ ﴿٥١﴾

51. Hakika sisi tunatumai Mola wetu atughufirie makosa yetu kwa kuwa ndio wa kwanza kuamini.

WALIFIKA WACHAWI

Aya 38 – 51

MAANA

Basi wakakusanywa wachawi wakati wa siku maalum.

Siku yenyewe ni sikukuu; kama alivyosema Mwenyezi Mungu:

قَالَ مَوْعِدُكُمْ يَوْمُ الزِّينَةِ وَأَن يُحْشَرَ النَّاسُ ضُحًى ﴿٥٩﴾

“Akasema: Miadi yenu ni siku ya sikukuu na watu wakusanywe kabla ya adhuhuri.” Juz. 16 (20:59).

Na watu wakaambiwa: Je, mtakusanyika ili mshuhudie mapambano haya? Watu hawahitaji kuhimizwa kwenye mambo haya; hao wenyewe watashindana kufika. Na hili ndilo alilolitaka Musa, ili haki idhihirike na batili ibatilike machoni mwa watu.

Huenda tutawafuata wachawi wakiwa wao ndio watakaoshinda.

Waliosema haya kwa watu ni Firauni na wakuu wake. Dhahiri ya kauli yao hii inaashiria kuwa wana shaka na dini ya wachawi na kwamba wao wanitafuta haki ili waifuate, lakini haya sio makusudio yao. Kwa sababu wao na wachawi wako kwenye dini moja. Makusudio yao ni kuwa huenda tutabaki kwenye uthabiti wa dini yetu wala hatutamfuta Musa.

Basi walipokuja wachawi wakamwambia Firauni: Je, tutapata ujira ikiwa tutashinda? Akasema: Ndio, hapo nanyi hakika mtakuwa miongoni mwa wanaokurubishwa. Musa akawaambia: Tupeni mnavyotaka kutupa. Wakatupa kamba zao na fimbo zao na wakasema:

“Kwa nguvu za Firauni hakika sisi bila shaka ni wenye kushinda. Musa akatupa fimbo yake, mara ikavimeza walivyovibuni. Wachawi wakapomoka kusujudu.Wakasema: Tumemwamini Mola wa Walimwengu. Mola wa Musa na Harun.

Akasema Firauni: Je, mmemwamini kabla sijawaruhusu. Hakika yeye ndiye mkubwa wenu aliyewafundisha uchawi, lakini punde mtajua. Nitawakata mikono yenu na miguu yenu kwa kubadilisha, kisha nitawasulubu nyote. Wakasema: Haidhuru, hakika sisi ni wenye kurejea kwa Mola wetu. Hakika sisi tunatumai Mola wetu atughufirie makosa yetu kwa kuwa ndio wa kwanza kuamini.

Aya hizi zote zimetajwa katika Juz. 9 (7: 113 – 126); wala hakuna tofauti baina ya hapa na huko, isipokuwa katika baadhi ya ibara tu; kwa mfano kule imesemwa: ‘wakaja wachawi’ na hapa ikasemwa; ‘walipokuja wachawi,’ n.k.

وَأَوْحَيْنَا إِلَىٰ مُوسَىٰ أَنْ أَسْرِ بِعِبَادِي إِنَّكُم مُّتَّبَعُونَ ﴿٥٢﴾

52. Na tulimpelekea wahyi Musa kwamba nenda na waja wangu wakati wa usiku, kwa hakika mtafuatwa.

فَأَرْسَلَ فِرْعَوْنُ فِي الْمَدَائِنِ حَاشِرِينَ ﴿٥٣﴾

53. Basi Firauni akawatuma mjini wakusanyao.

إِنَّ هَـٰؤُلَاءِ لَشِرْذِمَةٌ قَلِيلُونَ ﴿٥٤﴾

54. Hakika hawa ni kikundi kidogo.

وَإِنَّهُمْ لَنَا لَغَائِظُونَ ﴿٥٥﴾

55. Nao wanatuudhi.

وَإِنَّا لَجَمِيعٌ حَاذِرُونَ ﴿٥٦﴾

56. Na sisi ni wengi wenye kuchukua hadhari.

فَأَخْرَجْنَاهُم مِّن جَنَّاتٍ وَعُيُونٍ ﴿٥٧﴾

58. Basi tukawatoa katika mabustani na chemchem.

وَكُنُوزٍ وَمَقَامٍ كَرِيمٍ ﴿٥٨﴾

58. Na mahazina na vyeo vya heshima.

كَذَٰلِكَ وَأَوْرَثْنَاهَا بَنِي إِسْرَائِيلَ ﴿٥٩﴾

59. Hivyo ndivyo! Na tukawarithisha wana wa Israil.

فَأَتْبَعُوهُم مُّشْرِقِينَ ﴿٦٠﴾

60. Kisha wakawafuata walipotokewa na jua.

فَلَمَّا تَرَاءَى الْجَمْعَانِ قَالَ أَصْحَابُ مُوسَىٰ إِنَّا لَمُدْرَكُونَ ﴿٦١﴾

61. Yalipoonana makundi mawili, watu wa Musa wakasema: Hakika tumepatikana.

قَالَ كَلَّا إِنَّ مَعِيَ رَبِّي سَيَهْدِينِ ﴿٦٢﴾

62. Akasema: Hapana! Hakika Mola wangu yuko pamoja nami, ataniongoza.

فَأَوْحَيْنَا إِلَىٰ مُوسَىٰ أَنِ اضْرِب بِّعَصَاكَ الْبَحْرَ فَانفَلَقَ فَكَانَ كُلُّ فِرْقٍ كَالطَّوْدِ الْعَظِيمِ ﴿٦٣﴾

63. Tulimpelekea wahyi Musa tukamwambia: Piga bahari kwa fimbo yako. Basi ikatengana na kila sehemu ikawa kama milima mkubwa.

وَأَزْلَفْنَا ثَمَّ الْآخَرِينَ ﴿٦٤﴾

64. Na tukawajongeza hapo wale wengine.

وَأَنجَيْنَا مُوسَىٰ وَمَن مَّعَهُ أَجْمَعِينَ ﴿٦٥﴾

65. Na tukamwokoa Musa na waliokuwa pamoja naye wote.

ثُمَّ أَغْرَقْنَا الْآخَرِينَ ﴿٦٦﴾

66. Kisha tukawazamisha hao wengine.

إِنَّ فِي ذَٰلِكَ لَآيَةً وَمَا كَانَ أَكْثَرُهُم مُّؤْمِنِينَ ﴿٦٧﴾

67. Hakika bila shaka katika hayo ipo ishara lakini wengi wao si wenye kuamini.

وَإِنَّ رَبَّكَ لَهُوَ الْعَزِيزُ الرَّحِيمُ ﴿٦٨﴾

68. Na hakika Mola wako ndiye Mwenye nguvu, Mwenye kurehemu.

KUGHARIKI FAIRAUNI NA WATU WAKE

Aya 52 – 68

MAANA

Na tulimpelekea wahyi Musa kwamba nenda na waja wangu wakati wa usiku, kwa hakika mtafuatwa.

Mwenyezi Mungu alimwamrisha Musa atoke na wana wa Israil kutoka ardhi ya Misri usiku na akampa habari kwamba Firauni atawafuata ili awarudishe.

Basi Firauni akawatuma mjini wakusanyao.

Firauni alipojua kuwa Musa na watu wake wametoka aliwakusanyia watu ili awarudishe kwenye utawala wake na awape adhabu ya utoro.

Akasema: Hakika hawa ni kikundi kidogo nao wanatuudhi na sisi ni wengi wenye kuchukua hadhari.

Ni nani huyo Musa na watu wake. Wao si chochote kwetu; wanajaribu kutukasirisha na kutufanyia jeuri, na sisi tunawachunga. Basi watapata adhabu ya matendo yao. Lakini juu ya mipango ya Firauni kuna mipango ya Mwenyezi Mungu. Imam(a.s) anasema:Mambo yanakuwa kwa makadirio ili maangamizi yawe kwa mpangilio.

Basi tukawatoa katika mabustani na chemchem na mahazina na vyeo vya heshima.

Firauni na jeshi lake alitoka ili amwadhibu Musa na watu wake, lakini Mungu akawaadhibu wao na akawatoa katika yale waliyokuwa wakiyamilikii na kustarehe nayo; yakiwemo makasri ya ghorofa, mito inayotiririka, miti iliyojaa matunda kochokocho, mahazina yaliyojificha, mabembea, mabwawa ya kuogelea na sehemu za kupunga upepo. Yote haya na mengineyo waliyaacha bila ya kurudi.

Hivyo ndivyo! Na tukawarithisha wana wa Israil.

Tabari anasema: “Mwenyezi Mungu (s.w.t) aliwarithisha wana wa Israil majumba ya Firauni na watu wake.” Abu Hayyani Al-Andalusi naye amesema katika kitabu Al-bahrul-Muhit: “Haya ndio maana ya dhahiri, kwa sababu Aya ya kurithishwa wana wa Israil, imekuja moja kwa moja baada ya Aya ya kuwatoa.”

Wengine wamesema kuwa Mwenyezi Mungu aliwarithisha wana wa Israil mfano wa alivyokuwa Firauni na watu wake. Kwa sababu Waisrail hawakurudi Misri baada ya kuitoka.

Vyovyote iwavyo Aya inaeleza kuwa Mwenyezi Mungu hawaachi madhal- imu na dhulma yao na kwamba yeye anawaadhibu mikononi mwa wenye ikhlasi au kwa sababu yoyote. Haya ndiyo tunayoyaamini na kuyakubali. Ama uchunguzi wa historia na mfano wake tunawaachia wataalamu wake, ila ikiwa tuna yakini nayo.

Kisha wakawafuata walipotokewa na jua.

Firauni alitoka na jeshi lake la wapanda farasi na wendao kwa miguu kumtafuta Musa na watu wake wakawapata lilipochomoza jua.

Yalipoonana makundi mawili, kundi la Musa na la Firauni, watu wa Musa wakasema : Hakika tumepatikana.

Walisema hivyo kwa hofu na fazaa, kuwa adui amekwishatufikia hatuna la kufanya.

Akasema: Hapana! Hakika Mola wangu yuko pamoja nami, ataniongoza. Tulimpelekea wahyi Musa tukamwambia: Piga bahari kwa fimbo yako. Basi ikatengana na kila sehemu ikawa kama milima mkubwa.

Musa aliwaambia watu wake kuwa msimuogope Firauni na nguvu zake. Hakika Mwenyezi Mungu ana nguvu zaidi na yuko pamoja nami, nanyi mtaona.

Hakumaliza maneno yake, mara Mwenyezi Mungu akamwamrisha kupiga bahari kwa fimbo yake. Alipoipiga ikapasuka njia kumi na mbili kulingana na koo za waisrail. Maji yakainuka baina ya njia moja na nyingine kama mlima. Musa na watu wake wakavuka hadi ng’ambo ya pili.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 16 (20:77).

Na tukawajongeza hapo wale wengine. Na tukamwokoa Musa na waliokuwa pamoja naye wote. Kisha tukawazamisha hao wengine.

Makusudio ya wengine ni kundi la Firauni. Maana ni kuwa baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kuwavusha wana wa Israil upande wa pili na wakawa wameokoka, kundi la Firauni nalo liliwasili. Wakaona muuujiza mkubwa – maji ya bahari yamesimama kama jabali na kutengeneza njia. Firauni akawaambia watu wake: Tazameni bahari ilivyoitikia matakwa yangu na kunifungulia njia ya kuwafuata walionitoroka.

Kisha wakajitoma na wakaenda kwa amani na utulivu. Hawakufika katikati, bahari ikawafunika wote, baada ya kuhadharishwa na kupewa muda mrefu, lakini walizama kwenye upotevu wao.

Hakika bila shaka katika hayo ipo ishara ya muujiza, mazingatio na mawaidha, lakini wengi wao si wenye kuamini. Na hakika Mola wako ndiye Mwenye nguvu, Mwenye kurehemu.

Wengi wao hapa wanakusudiwa wana wa Israil waliookolewa na Mwenyezi Mungu mikononi mwa Firauni, kwa kuchukilia dhahiri ya mfumo wa maneno ulivyo.

Na wala sio walioangamia, kama wasemavyo baadhi ya wafasiri. Dalili ya kuwa makusudio ni wana wa Israil ni kuwa wafuasi wa Firauni wote wlikuwa makafiri, bila ya kubaki; hasa wale aliokuwa nao. Na wana wa Israili, walipookolewa na Mungu kutoka kwa Firauni, walimwambia Musa: Tunataka sanamu tuliabudu badala ya Mwenyezi Mungu:

وَجَاوَزْنَا بِبَنِي إِسْرَائِيلَ الْبَحْرَ فَأَتَوْا عَلَىٰ قَوْمٍ يَعْكُفُونَ عَلَىٰ أَصْنَامٍ لَّهُمْ قَالُوا يَا مُوسَى اجْعَل لَّنَا إِلَـٰهًا كَمَا لَهُمْ آلِهَةٌ ﴿١٣٨﴾

“Na tukawavusha bahari wana wa Israil na wakawafikia waliokuwa wakiyaabudu masanamu yao; wakasema: Ewe Musa! Hebu nasi tufanyie waungu kama hawa walivyo na waungu.” Juz. 9 (7:138).

Kwa hiyo maana yanakuwa kwamba Waisraili walishuhudia muujiza wa kupasuka bahari na miujiza mingineyo, lakini bado waliendelea kung’ang’ania ukafiri wao na jeuri yao.

وَاتْلُ عَلَيْهِمْ نَبَأَ إِبْرَاهِيمَ ﴿٦٩﴾

69. Na wasomee habari za Ibrahim.

إِذْ قَالَ لِأَبِيهِ وَقَوْمِهِ مَا تَعْبُدُونَ ﴿٧٠﴾

70. Alipomwambia baba yake na kaumu yake: Mnaabudu nini?

قَالُوا نَعْبُدُ أَصْنَامًا فَنَظَلُّ لَهَا عَاكِفِينَ ﴿٧١﴾

71. Wakasema: Tunaabudu masanamu nasi tutaendelea kuyanyenyekea.

قَالَ هَلْ يَسْمَعُونَكُمْ إِذْ تَدْعُونَ ﴿٧٢﴾

72. Akasema: Je yanawasikia mnapoyaita?

أَوْ يَنفَعُونَكُمْ أَوْ يَضُرُّونَ ﴿٧٣﴾

73. Au yanawafaa au yanawadhuru?

قَالُوا بَلْ وَجَدْنَا آبَاءَنَا كَذَٰلِكَ يَفْعَلُونَ ﴿٧٤﴾

Wakasema: Bali tumewakuta mababa zetu wakifanya hivyo hivyo.

قَالَ أَفَرَأَيْتُم مَّا كُنتُمْ تَعْبُدُونَ ﴿٧٥﴾

75. Akasema: Je, mmewaona mnaowaabudu?

أَنتُمْ وَآبَاؤُكُمُ الْأَقْدَمُونَ ﴿٧٦﴾

76. Nyinyi na baba zenu wa zamani?

فَإِنَّهُمْ عَدُوٌّ لِّي إِلَّا رَبَّ الْعَالَمِينَ ﴿٧٧﴾

77. Hakika hao ni maadui zangu isipokuwa Mola wa walimwengu wote.

الَّذِي خَلَقَنِي فَهُوَ يَهْدِينِ ﴿٧٨﴾

78. Ambaye ameniumba naye ananiongoza.

وَالَّذِي هُوَ يُطْعِمُنِي وَيَسْقِينِ ﴿٧٩﴾

79. Na ambaye ananilisha na kuninywesha.

وَإِذَا مَرِضْتُ فَهُوَ يَشْفِينِ ﴿٨٠﴾

80. Na ninapougua basi yeye ananiponya.

وَالَّذِي يُمِيتُنِي ثُمَّ يُحْيِينِ ﴿٨١﴾

81. Na ambaye atanifisha kisha atanihuisha.

وَالَّذِي أَطْمَعُ أَن يَغْفِرَ لِي خَطِيئَتِي يَوْمَ الدِّينِ ﴿٨٢﴾

82. Na ambaye ndiye ninayemtumai kunighufuria makosa yangu siku ya malipo.

رَبِّ هَبْ لِي حُكْمًا وَأَلْحِقْنِي بِالصَّالِحِينَ ﴿٨٣﴾

83. Mola wangu! Nitunukie hukumu na uniunganishe na wema.

وَاجْعَل لِّي لِسَانَ صِدْقٍ فِي الْآخِرِينَ ﴿٨٤﴾

84. Na unijaalie kutajwa kwa wema na wengine.

وَاجْعَلْنِي مِن وَرَثَةِ جَنَّةِ النَّعِيمِ ﴿٨٥﴾

85. Na unijaalie katika warithi wa Bustani za neema.

وَاغْفِرْ لِأَبِي إِنَّهُ كَانَ مِنَ الضَّالِّينَ ﴿٨٦﴾

86. Na umghufirie baba yangu, kwani alikuwa miongoni mwa wapotevu.

وَلَا تُخْزِنِي يَوْمَ يُبْعَثُونَ ﴿٨٧﴾

87. Wala usinihizi siku watakapofufuliwa.

يَوْمَ لَا يَنفَعُ مَالٌ وَلَا بَنُونَ ﴿٨٨﴾

88. Siku ambayo haitafaa mali wala wana.

إِلَّا مَنْ أَتَى اللَّـهَ بِقَلْبٍ سَلِيمٍ ﴿٨٩﴾

89. Isipokuwa mwenye kuja kwa Mwenyezi Mungu na moyo uliosalimika.

IBRAHIM

Aya 69 – 89

MAANA

Mwenyezi Mungu (s.w.t) amekitaja kisa cha Ibrahim kwa kukigawa kulingana na mnasaba ulivyo.

Katika Aya hizi Mwenyezi Mungu (s.w.t) amerudia majibizano baina ya Ibrahim na watu wake, kwa mfumo mwingine unaotofautiana na ule ulio katika Juz. 17 (21:51).

Na wasomee habari za Ibrahim.

Maneno yanaelekezwa kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) kuwa awasomee makuraishi ambao wanadai kuwa ni kizazi cha Ibrahim na wako kwenye dini yake.

Alipomwambia baba yake na kaumu yake: Mnaabudu nini?

Katika Juz.7 (6:74) tumetaja tofauti za wafasiri kuhusu baba aliyeambiwa maneno haya na Ibrahim, kuwa je, ni baba yake hasa au ni baba wa kimajazi au ni ami yake?

Wakasema: Tunaabudu masanamu nasi tutaendelea kuyanyenyekea.

Tutadumu kuyaabudu na kuyatukuza. Kukubali kwao kuabudu masanamu kunajulisha kuwa neno sanamu halikuwa linamaanisha shutuma katika ufahamu wao, kama tunavyofahamu sisi; bali neno hilo lilikuwa likimaanisha utukufu na ukuu.

Akasema: Je yanawasikia mnapoyaita? Au yanawafaa au yanawadhuru?

Ni kawaida anayeabudiwa asikie, aone, adhuru na kunufaisha. Je, haya mnayoyaabudu yana sifa hizi? Swali hapa ni la kupinga.

Wakasema: Bali tumewakuta mababa zetu wakifanya hivyo hivyo.

Hii ni kukubali kuwa wao ni waigaji. Wala hilo si ajabu. Katika karne ya ishirini, zama za kutembea angani, tumeona wafuasi wakiwaiga viongozi wao na wakitoa dalili kwa kauli zao na kuzichukulia kuwa ni msingi, bila ya kuhakisha na kuchunguza.

Akasema: Je, mmewaona mnaowaabudu nyinyi na baba zenu wa zamani? Hakika hao ni maadui zangu isipokuwa Mola wa walimwengu wote.

Ikiwa nyinyi mnawaiga baba zenu, basi mimi simwigi yeyote na ninatangaza kujitenga kwangu na uadui wangu kwa hao waungu wenu; wala siabudu isipokuwa Mola wa walimwengu wote. Yeye ndiye walii wangu duniani na akhera. Yakiwa masanamu ni miungu, kama mnavyodai, basi na waniteremshie hasira zao, mimi napingana nao.

Ambaye ameniumba naye ananiongoza.

Mwenyezi Mungu amenipa akili nami naitumia kuniongoza kwenye haki. Ninaifuata na ninaitumia vizuri; wala simuigi yoyote; kama mnavyodai.

Na ambaye ananilisha na kuninywesha.

Kwa kuzifanya nyepesi sababu kwangu mimi na kwa viumbe vyake vyote.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) ameiumba ardhi hii na akaweka kila wanayoyahitajia na akasema: Yeye ndiye aliyeidhalisha ardhi kwa ajili yenu, basi tembeeni katika pande zake na kuleni katika riziki zake. Na kwake yeye ndio kufufuliwa.

Na ninapougua basi yeye ananiponya kutokana na madawa aliyoyaumba.

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) anasema, “Hakika kila ugonjwa una dawa, dawa ikifika kwenye ugonjwa hupona kwa idhini ya Mwenyezi Mungu.” Kuna Hadithi nyingine isemayo: Hakika Mwenyezi Mungu ameteremsha ugonjwa na dawa, basi fanyeni dawa wala msifanye dawa kwa haramu.

Na ambaye atanifisha kisha atanihuisha na ambaye ndiye ninayemtumai kunighufuria makosa yangu siku ya malipo.

Uhai, mauti na maghufira yako mikononi mwa Mwenyezi Mungu, hilo halina shaka. Na Ibrahim(a.s) ni mwenye kuhifadhiwa na makosa na hatia (maasumu). Katika isma ya kila maasumu ni kuikuza hofu yake kwa Mwenyezi Mungu.

Mola wangu! Nitunukie hukumu.

Makusudio ya hukumu hapa, sio utawala bali ni hekima na kukata hukumu:

وَآتَيْنَاهُ الْحِكْمَةَ وَفَصْلَ الْخِطَابِ ﴿٢٠﴾

“Na tukampa hekima na kukata hukumu.” (38:20).

Na uniunganishe na wema.

Unipe tawfiki ya kufuata nyao zao na kutenda matendo yao.

Na unijaalie kutajwa kwa wema na wengine.

Makusudio ya wengine ni umma utakaokuja baadaye. Maana ni nijaalie kutajwa kwa wema baina ya watu baada yangu. Mwenyezi Mungu aliitikia dua yake; ambapo dini zote za mbinguni zimeafikiana kumtukuza na kumwadhimisha Nabii Ibrahim(a.s) .

Na unijaalie katika warithi wa Bustani za neema.

Ni nani anayestahiki hizo zaidi kuliko Ibrahim.

Na umghufirie baba yangu, kwani alikuwa miongoni mwa wapotevu.

Angalia tafsiri ya “Na haikuwa Ibrahim kumtakia msamaha baba yake ila ni kwa sababu ya ahadi aliyofanya naye, lakini ilipopambanukia kuwa yeye ni adui wa Mwenyezi Mungu, alijiepusha naye.” Juz. 11 (9:114).

Wala usinihizi siku watakapofufuliwa.

Dua hii ni katika aina ya dua za mitume na viongozi wema.Siku ambayo haitafaa mali wala wana. Isipokuwa mwenye kuja kwa Mwenyezi Mungu na moyo uliosalimika.

Kutokana na maafa ya ukafiri, unafiki, mifundo, ria na maafa mengineyo na maradhi.

Moyo ukiwa salama na uchafu, basi viungo vyote huwa salama: ulimi utasalimika na uwongo, kusengenya, kusikiliza upuzi na ubatilifu. Vile vile mkono unasalimika na kufanya haramu na tupu kutokana na zina na uovu.

6

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TISA

وَأُزْلِفَتِ الْجَنَّةُ لِلْمُتَّقِينَ ﴿٩٠﴾

90. Na Bustani (Pepo) itasogezwa kwa wenye takua.

وَبُرِّزَتِ الْجَحِيمُ لِلْغَاوِينَ ﴿٩١﴾

91. Na Jahannam itadhihirishwa kwa wapotofu.

وَقِيلَ لَهُمْ أَيْنَ مَا كُنتُمْ تَعْبُدُونَ ﴿٩٢﴾

92. Na wataambiwa, wako wapi mliokuwa mkiwaabudu.

مِن دُونِ اللَّـهِ هَلْ يَنصُرُونَكُمْ أَوْ يَنتَصِرُونَ ﴿٩٣﴾

93. Badala ya Mwenyezi Mungu? Je, watawasaidia au kujisaidia wenyewe?

فَكُبْكِبُوا فِيهَا هُمْ وَالْغَاوُونَ ﴿٩٤﴾

94. Basi watavurumizwa humo wao na wapotofu.

وَجُنُودُ إِبْلِيسَ أَجْمَعُونَ ﴿٩٥﴾

95. Na majeshi ya Ibilisi yote.

قَالُوا وَهُمْ فِيهَا يَخْتَصِمُونَ ﴿٩٦﴾

96. Watasema na hali ya kuwa wanazozana humo:

تَاللَّـهِ إِن كُنَّا لَفِي ضَلَالٍ مُّبِينٍ ﴿٩٧﴾

97. Wallah! Hakika tulikuwa katika upotevu ulio wazi.

إِذْ نُسَوِّيكُم بِرَبِّ الْعَالَمِينَ ﴿٩٨﴾

98. Tulipowafanya sawa na Mola wa walimwengu wote.

وَمَا أَضَلَّنَا إِلَّا الْمُجْرِمُونَ ﴿٩٩﴾

99. Na hawakutupoteza ila wakosefu.

فَمَا لَنَا مِن شَافِعِينَ ﴿١٠٠﴾

100. Basi hatuna waombezi.

وَلَا صَدِيقٍ حَمِيمٍ ﴿١٠١﴾

101. Wala rafiki wa dhati.

فَلَوْ أَنَّ لَنَا كَرَّةً فَنَكُونَ مِنَ الْمُؤْمِنِينَ ﴿١٠٢﴾

102. Laiti tungepata kurejea tena tungelikuwa katika waumi- ni.

إِنَّ فِي ذَٰلِكَ لَآيَةً وَمَا كَانَ أَكْثَرُهُم مُّؤْمِنِينَ ﴿١٠٣﴾

103. Hakika bila shaka katika hayo ipo ishara, lakini wengi wao si wenye kuamini.

وَإِنَّ رَبَّكَ لَهُوَ الْعَزِيزُ الرَّحِيمُ ﴿١٠٤﴾

104. Na hakika Mola wako ndiye mwenye nguvu mwenye kurehemu.

PEPO KWA WENYE TAKUA NA MOTO KWA WAPOTEVU

Aya 90 – 104

MAANA

Na Bustani (Pepo) itasogezwa kwa wenye takua

Bila shaka iko karibu na mwenye kuongoka na akamcha Mungu na iko mbali na mwenye kupotea.

Na Jahannam itadhihirishwa kwa wapotofu.

Ataidhihirisha Mwenyezi Mungu kwa wale walioikana na kuikadhibisha.

Na wataambiwa wako wapi mliokuwa mkiwaabudu badala ya Mwenyezi Mungu? Na mkiwatarajia kwa siku hii, huku mkisema kuwa mliwabudu ili wawakurubishe kwa Mwenyezi Mungu?

Je, watawasaidia au kujisaidia wenyewe?

Hakika wao hawawezi kuwasaidia wala kujisaidia wenyewe.

Basi watavurumizwa humo wao na wapotofu na majeshi ya Ibilisi yote.

Wao ni hao waungu wao na wapotofu ni wale walioabudu. Mwanajeshi wa Ibilisi ni kila mpotofu na mpotoshaji. Mwenyezi Mungu atawachanganya wote kisha awatupe kwenye shimo la Jahannam.

Watasema na hali ya kuwa wanazozana humo: Wallah! Hakika tulikuwa katika upotevu ulio wazi, tulipowafanya sawa na Mola wa walimwengu wote. Na hawakutupoteza ila wakosefu.

Wapotofu kesho watasema, baada ya kupitwa na wakati, kuwaambia waungu wao na mashetani wao, kwamba nyinyi ndio mliokuwa viongozi wetu wa upofu na upotevu, wakati tulipowaabudu na kuwafanya mko sawa na Mwenyezi Mungu. Na wakosefu ndio waliokuwa kikwazo, ambao ni viongozi wa manufaa na masilahi, asili ya ufisadi na balaa.

Basi hatuna waombezi wala rafiki wa dhati.

Kesho hakuna uombezi wala ugombezi. Hakuna kitakachomfaa mtu isipokuwa moyo ulio salama na amali njema. Na muovu ni yule asiyekuwa na mawili hayo.

Laiti tungepata kurejea tena tungelikuwa katika waumini.

Baada ya kukata tamaaa na kila kitu ndio wanatamani kurudi duniani ili waamiini na kutenda. Mwenyezi Mungu anasema:

وَلَوْ رُدُّوا لَعَادُوا لِمَا نُهُوا عَنْهُ وَإِنَّهُمْ لَكَاذِبُونَ ﴿٢٨﴾

“Na kama wangelirudishwa, bila shaka wangeyarudia yale waliyokatazwa na hakika wao ni waongo.” Juz. 7 (6:28)

Hakika bila shaka katika hayo ipo ishara, lakini wengi wao si wenye kuamini. Na hakika Mola wako ndiye Mwenye nguvu, Mwenye kurehemu.

Imetangulia kwa herufi zake, katika Aya 67 na 68 ya sura hii.

كَذَّبَتْ قَوْمُ نُوحٍ الْمُرْسَلِينَ ﴿١٠٥﴾

105. Kaumu ya Nuh waliwakadhibisha mitume.

قَالَ لَهُمْ أَخُوهُمْ نُوحٌ أَلَا تَتَّقُونَ ﴿١٠٦﴾

106. Alipowaambia ndugu yao Nuh: Je, hamna takua?

إِنِّي لَكُمْ رَسُولٌ أَمِينٌ ﴿١٠٧﴾

107. Hakika mimi kwenu ni Mtume mwaminifu.

فَاتَّقُوا اللَّـهَ وَأَطِيعُونِ ﴿١٠٨﴾

108. Basi mcheni Mwenyezi Mungu na mnitii.

وَمَا أَسْأَلُكُمْ عَلَيْهِ مِنْ أَجْرٍ إِنْ أَجْرِيَ إِلَّا عَلَىٰ رَبِّ الْعَالَمِينَ ﴿١٠٩﴾

109. Na siwataki ujira juu yake, kwani ujira wangu hauko ila kwa Mola wa walimwengu wote.

فَاتَّقُوا اللَّـهَ وَأَطِيعُونِ ﴿١١٠﴾

110. Basi mcheni Mwenyezi Mungu na mnitii.

قَالُوا أَنُؤْمِنُ لَكَ وَاتَّبَعَكَ الْأَرْذَلُونَ ﴿١١١﴾

111. Wakasema: Je, tukuamini na hali wanaokufuata ni walio duni?

قَالَ وَمَا عِلْمِي بِمَا كَانُوا يَعْمَلُونَ ﴿١١٢﴾

112. Akasema: Nayajuaje waliyokuwa wakiyafanya?

إِنْ حِسَابُهُمْ إِلَّا عَلَىٰ رَبِّي لَوْ تَشْعُرُونَ ﴿١١٣﴾

113. Hisabu yao haiko ila kwa Mola wangu. Lau mngelitambua.

وَمَا أَنَا بِطَارِدِ الْمُؤْمِنِينَ ﴿١١٤﴾

114. Wala mimi si mwenye kuwafukuza waumini.

إِنْ أَنَا إِلَّا نَذِيرٌ مُّبِينٌ ﴿١١٥﴾

115. Sikuwa mimi ila ni muonyaji aliye dhahiri.

قَالُوا لَئِن لَّمْ تَنتَهِ يَا نُوحُ لَتَكُونَنَّ مِنَ الْمَرْجُومِينَ ﴿١١٦﴾

116. Wakasema: Kama hutakoma ewe Nuh bila shaka utapigwa mawe.

قَالَ رَبِّ إِنَّ قَوْمِي كَذَّبُونِ ﴿١١٧﴾

117. Akasema: Mola wangu! Hakika kaumu yangu wamenikadhibisha.

فَافْتَحْ بَيْنِي وَبَيْنَهُمْ فَتْحًا وَنَجِّنِي وَمَن مَّعِيَ مِنَ الْمُؤْمِنِينَ ﴿١١٨﴾

118. Basi amua baina yagu mimi na wao uamuzi. Na uniokoe na walio pamoja nami katika waumini.

فَأَنجَيْنَاهُ وَمَن مَّعَهُ فِي الْفُلْكِ الْمَشْحُونِ ﴿١١٩﴾

119. Basi tukamuokoa na walio pamoja naye katika jahazi iliyosheheni.

ثُمَّ أَغْرَقْنَا بَعْدُ الْبَاقِينَ ﴿١٢٠﴾

120. Kisha tukawagharikisha baadaye waliobaki.

إِنَّ فِي ذَٰلِكَ لَآيَةً وَمَا كَانَ أَكْثَرُهُم مُّؤْمِنِينَ ﴿١٢١﴾

121. Hakika bila shaka katika hayo ipo ishara, lakini wengi wao si wenye kuamini.

وَإِنَّ رَبَّكَ لَهُوَ الْعَزِيزُ الرَّحِيمُ ﴿١٢٢﴾

122. Na hakika Mola wako ndiye Mwenye nguvu, Mwenye kurehemu.

NUH

Aya 105 – 122

MAANA

Kaumu ya Nuh waliwakadhibisha mitume.

Mtume aliyetumwa kwao ni mmoja ambaye ni Nuh, lakini mwenye kumkadhibisha Mtume mmoja ni kama amewakadhibisha mitume wote, kwa vile aliyewatuma ni mmoja na ujumbe ni mmoja.

Alipowaambia ndugu yao Nuh: Je, hamna takua?

Mwenye kuishika takua atakuwa katika amani na atasalimika na ghadhabu ya Mwenyezi Mungu na adhabu yake.

Hakika mimi kwenu ni Mtume mwaminifu.

Alijisifu kwa uaminifu ambao waliujua kwake akiwa mdogo na mtu mzima; sawa na makuraishi walivyomjua Muhammad(s.a.w.w) kwa ukweli na uaminifu katika hali zake zote.

Basi mcheni Mwenyezi Mungu na mnitii. Kwa sababu ninawaita kwenye lile ambalo lina kheri yenu ya dunia na akhera.

Na siwataki ujira juu yake, kwani ujira wangu hauko ila kwa Mola wa walimwengu wote.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 7 (6:90) na Juz. 12 (11:29).

Basi mcheni Mwenyezi Mungu na mnitii.

Hakuna sababu ya kukaririka jambo la takua (kumcha Mungu) isipokuwa ni jambo muhimu na la msingi.

Wakasema: Je, tukuamini na hali wanaokufuata ni walio duni.

Walimtia ila Nuh, si kwa lolote ila ni kwa kuwa mafukara walimwamini na kwao, hawana thamani. Kwa hiyo utume wa Nuh hauna thamani. Kwa maneno mengine ni kuwa wapenda anasa hawaoni kuwa ufukara ni maisha. Vipi wataamini waliloliamini mafukara? Hivi ndivyo wafanyavyo wapenda anasa; wanakuwa vipofu wa haki na wanakuwa na kiburi.

Akasema: Nayajuaje waliyokuwa wakiyafanya? Hisabu yao haiko ila kwa Mola wangu.

Nuh aliwaambia wale waliomjadili kuhusu ufukara, kuwa thamani ya mtu ni matendo yake na malengo yake, sio kwa cheo na mali. Na mimi sijui kuwa wao walimfanyia ubaya mtu yoyote kwa kauli au vitendo. Siri iko kwa Mwenyezi Mungu. Yeye peke yake ndiye anayejua na kuhisabu.

Lau mngelitambua kwamba thamani ya mtu ni kwa matendo sio kwa mali na dhahiri ni ya watu na batini ni ya Mwenyezi Mungu.

Wala mimi si mwenye kuwafukuza waumini. Sikuwa mimi ila ni muonyaji aliye dhahiri.

Umetangulia mfano wake katika Juz. Juz. 12 (11: 29).

Wakasema: Kama hutakoma ewe Nuh bila shaka utapigwa mawe.

Wameshindwa kuijadili haki wakakimbilia vitisho na mabavu. Hii ndio tabia ya wasiofuta haki, kila mahali na kila wakati.

Akasema: Mola wangu! Hakika kaumu yangu wamenikadhibisha. Basi amua baina yagu mimi na wao uamuzi.

Walipompa vitisho vya kutumia nguvu, alimuomba msaada Mwenyezi Mungu na nguvu zake. Na kwa unyenyekevu akamuomba Mwenyezi Mungu ahukumu, baina yake na yao, hukumu itakayomnusuru mwenye haki na kumwadhibu mwenye batili.

Na uniokoe na walio pamoja nami katika waumini pale itakapowashukia adhabu makafiri.

Basi tukamuokoa na walio pamoja naye katika jahazi iliyosheheni walioamini katika watu wake na wengineo na viumbe wengine wa kiume na wa kike. Kisha tukawagharikisha baadaye waliobaki.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 8 (7:64) na Juz. 12 (11:40).

Hakika bila shaka katika hayo ipo ishara, lakini wengi wao si wenye kuamini . Na hakika Mola wako ndiye Mwenye nguvu, Mwenye kurehemu. Imetangulia kwa herufi zake, katika Aya 67 na 68 ya Sura hii.

كَذَّبَتْ عَادٌ الْمُرْسَلِينَ ﴿١٢٣﴾

123. A’d waliwakadhibisha mitume.

إِذْ قَالَ لَهُمْ أَخُوهُمْ هُودٌ أَلَا تَتَّقُونَ ﴿١٢٤﴾

124. Alipowaambia ndugu yao Hud: Je, hamna takua?

إِنِّي لَكُمْ رَسُولٌ أَمِينٌ ﴿١٢٥﴾

125. Hakika mimi kwenu ni Mtume mwaminifu.

فَاتَّقُوا اللَّـهَ وَأَطِيعُونِ ﴿١٢٦﴾

126. Basi mcheni Mwenyezi Mungu na mnitii.

وَمَا أَسْأَلُكُمْ عَلَيْهِ مِنْ أَجْرٍ إِنْ أَجْرِيَ إِلَّا عَلَىٰ رَبِّ الْعَالَمِينَ ﴿١٢٧﴾

127. Na siwataki ujira juu yake, kwani ujira wangu hauko ila kwa Mola wa walimwengu wote.

أَتَبْنُونَ بِكُلِّ رِيعٍ آيَةً تَعْبَثُونَ ﴿١٢٨﴾

128. Je, mnajenga juu ya kila muinuko ishara ya kufanyia upuuzi?

وَتَتَّخِذُونَ مَصَانِعَ لَعَلَّكُمْ تَخْلُدُونَ ﴿١٢٩﴾

129. Na mnajenga ngome ili mkae milele.

وَإِذَا بَطَشْتُم بَطَشْتُمْ جَبَّارِينَ ﴿١٣٠﴾

130. Na mnaposhika kwa nguvu mnashika kwa nguvu kwa ujabari.

فَاتَّقُوا اللَّـهَ وَأَطِيعُونِ ﴿١٣١﴾

131. Basi mcheni Mwenyezi Mungu na mnitii.

وَاتَّقُوا الَّذِي أَمَدَّكُم بِمَا تَعْلَمُونَ ﴿١٣٢﴾

132. Na mcheni ambaye amewapa mnayoyajua.

أَمَدَّكُم بِأَنْعَامٍ وَبَنِينَ ﴿١٣٣﴾

133. Amewapa wanyama na watoto wa kiume.

وَجَنَّاتٍ وَعُيُونٍ ﴿١٣٤﴾

134. Na mabustani na chemchemi.

إِنِّي أَخَافُ عَلَيْكُمْ عَذَابَ يَوْمٍ عَظِيمٍ ﴿١٣٥﴾

135. Hakika ninawahofia adhabu ya siku kubwa.

قَالُوا سَوَاءٌ عَلَيْنَا أَوَعَظْتَ أَمْ لَمْ تَكُن مِّنَ الْوَاعِظِينَ ﴿١٣٦﴾

136. Wakasema: Ni mamoja kwetu ukitupa mawaidha au kutokuwa miongoni mwa watoao mawaidha.

إِنْ هَـٰذَا إِلَّا خُلُقُ الْأَوَّلِينَ ﴿١٣٧﴾

137. Haya si chochote ila ni hulka ya wa kale.

وَمَا نَحْنُ بِمُعَذَّبِينَ ﴿١٣٨﴾

138. Wala sisi hatutaadhibiwa.

فَكَذَّبُوهُ فَأَهْلَكْنَاهُمْ إِنَّ فِي ذَٰلِكَ لَآيَةً وَمَا كَانَ أَكْثَرُهُم مُّؤْمِنِينَ ﴿١٣٩﴾

139. Basi wakamkadhibisha na tukawahilikisha. Hakika bila shaka katika hayo ipo ishara, lakini wengi wao si wenye kuamini.

وَإِنَّ رَبَّكَ لَهُوَ الْعَزِيزُ الرَّحِيمُ ﴿١٤٠﴾

140. Na hakika Mola wako ndiye Mwenye nguvu, Mwenye kurehemu.

Hud

Aya 123 – 140

MAANA

Kisa cha Hud kimetangulia katika Juz. 8 (7:65 – 72) na Juz. 12 (11:50 – 60).

A’d waliwakadhibisha mitume. Alipowaambia ndugu yao Hud: Je, hamna takua? Hakika mimi kwenu ni Mtume mwaminifu. Basi mcheni Mwenyezi Mungu na mnitii. Na siwataki ujira juu yake, kwani ujira wangu hauko ila kwa Mola wa walimwengu wote.

Zimetangulia Aya kwa herufi zake katika sehemu iliyopita ya Sura hii Aya 105 – 110, bila ya mabadiliko yoyote isipokuwa jina tu. Kule imesemwa kaumu ya Nuh na hapa ni Hud na A’d.

Siri ya hilo ni kuwa risala ya mitume wote ni moja, ikilingania kwenye umoja wa Mwenyezi Mungu na kutii amri yake na makatazo yake.

Je, mnajenga juu ya kila muinuko ishara ya kufanyia upuuzi?

Makusudio ya ishara hapa ni jengo. Kila jengo linalotekeleza haja ya maisha hilo ni la kheri na ni katika dini. Kwa sababu dini ya Mwenyezi Mungu ni dini ya maisha. Ama jengo lisilokuwa na faida zaidi ya kujionyesha na kujifaharisha, hilo ni shari kidini na kiakili. Aina hii ndio inayokusudiwa hapa kwa dalili ya kauli yake Mwenyezi Mungu ‘ya kufanyia upuuzi’ kwa sababu upuuzi ni ule usiohitajika.

Na mnajenga ngome ili mkae milele.

Makusudio ya ngome hapa ni jengo lisilokuwa na manufaaa yoyote.

Na mnaposhika kwa nguvu mnashika kwa nguvu kwa ujabari. Basi mcheni Mwenyezi Mungu na mnitii.

Kutumia nguvu kwa ujabari ni kudhulumu kwa hali ya juu, na inakuwa kubwa dhulma kwa kumdhulumu mnyonge. Lililothibiti katika dini ya Mwenyezi Mungu ni kuwa dhulma ni miogoni mwa madhambi makubwa; bali ni sawa na kumkufuru Mungu.

Tumelithibitisha hilo huko nyuma kwa nukuu ya Qur’an.

Aya hii ilishuka wakati ambao hakukuwa na silaha za maangamizi wala hakukuwa na matajiri wanaotoa mamilioni ya pesa ili waangamizwe wanawake kwa ujumla. Ilishuka wakati ambao kutumia nguvu kulikuwa ni kwa kutumia mkono zaidi - upanga mshale na mkuki.

Ikiwa Mwenyezi Mungu amesifu kuwa ni ubaya na uovu mkubwa kutumia nguvu kwa kiganja cha mkono, basi atawalipa nini wale wanaowanyeshea wanyonge mvua ya makombora, mabomu ya sumu na silaha za nuklia? Au wale ambao wameijaza ardhi na anga kwa vikosi vya majeshi. Wameijaza maroketi ya kijeshi; si kwa lolote ila wanataka kuhukumu roho za waja na nyenzo za nchi kulingana na hawa zao na masilahi yao tu.

Na mcheni ambaye amewapa mnayoyajua. Amewapa wanyama na watoto wa kiume na mabustani na chemchemi. Hakika ninawahofia adhabu ya siku kubwa.

Hud aliwalingania kwenye twaa ya Mwenyezi Mungu na akawakumbusha neema yake juu yao na anavyowapa muda na pia akawahadharisha na mwisho mbaya wa dhulma. Lakini hilo halikuwazidisha kitu isipokuwa kiburi nawakasema: Ni mamoja kwetu ukitupa mawaidha au kutokuwa miongoni mwa watoao mawaidha sisi hatutakuamini. Mawaidha yako hayatatuzidishia isipokuwa kuachana nawe.

Haya si chochote ila ni hulka ya wa kale wala sisi hatutaadhibiwa.

Haya ni ishara ya dini yao na masanamu yao wanayoyaabudu; na kwamba wao hawatayaacha kwa sababu wameyarithi kutoka jadi na jadi. Hiyo ndiyo hoja yao; hawana zaidi ya ‘tumewakuta nayo baba zetu na sisi tunafuata nyayo zao.’

Basi wakamkadhibisha na tukawahilikisha.

Hud aliwaonya watu wake kwa dalili na hoja, lakini hawakujali, wakawa miongoni mwa walioangamia.

Hakika bila shaka katika hayo ipo ishara, lakini wengi wao si wenye kuamini. Na hakika Mola wako ndiye Mwenye nguvu, Mwenye kurehemu.

Imetangulia kwa herufi zake, katika Aya 67 na 68 ya Sura hii na pia sehemu iliyopita.