TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TISA Juzuu 19

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TISA33%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TISA Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: Qurani tukufu

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
  • Anza
  • Iliyopita
  • 14 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 8933 / Pakua: 3824
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TISA

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TISA Juzuu 19

Mwandishi:
Swahili

1

9

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TISA

Sura Ya Ishirini Na Saba: Surat An-Naml. Imeshuka Makka ina Aya 93

بِسْمِ اللَّهِ الرَّحْمَٰنِ الرَّحِيمِ

Kwa jina la Mwenyezi Mungu Mwingi wa rehema, Mwenye kurehemu.

طس تِلْكَ آيَاتُ الْقُرْآنِ وَكِتَابٍ مُّبِينٍ ﴿١﴾

1. Twa siin. Hiyo ni Aya za Qur’an na Kitabu kinachobainisha.

هُدًى وَبُشْرَىٰ لِلْمُؤْمِنِينَ ﴿٢﴾

2. Mwongozo na bishara kwa waumini.

الَّذِينَ يُقِيمُونَ الصَّلَاةَ وَيُؤْتُونَ الزَّكَاةَ وَهُم بِالْآخِرَةِ هُمْ يُوقِنُونَ ﴿٣﴾

3. Wale ambao wanasimamisha Swala na wakatoa Zaka na wana yakini na Akhera.

إِنَّ الَّذِينَ لَا يُؤْمِنُونَ بِالْآخِرَةِ زَيَّنَّا لَهُمْ أَعْمَالَهُمْ فَهُمْ يَعْمَهُونَ ﴿٤﴾

4. Hakika ambao hawaiamini Akhera, tumewapambia vitendo vyao, basi wao wanamanga-manga.

أُولَـٰئِكَ الَّذِينَ لَهُمْ سُوءُ الْعَذَابِ وَهُمْ فِي الْآخِرَةِ هُمُ الْأَخْسَرُونَ ﴿٥﴾

5. Hao ndio watakaopata adhabu mbaya, na wao katika Akhera ni wenye kupata hasara.

MWONGOZO NA BISHARA KWA WAUMINI

Aya 1-5

MAANA

Twa siin.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 1 (2:1)

Hiyo ni Aya za Qur’an na Kitabu kinachobainisha.

Hiyo ni ishara ya Sura hii. Qur’an na Kitabu ina maana moja. Tofauti ni wasifu tu, sio kwa dhati yake. Ni Qur’an kwa vile inasomwa, kutokana na neno na qiraa lenye maana ya kusoma. Na kitabu kwa vile imeandikwa, kutokana na neno kitaba lenye maana ya kuandika.

Ni chenye kubainisha kwa vile kiko wazi. Pia vilevile ni mwongozo na bishara kwa waumini.

Kinamuongoza mwenye kutafuta uongofu na kumpa habari njema ya Pepo ikiwa ataamini na kutenda mema.

Wale ambao wanasimamisha Swala na wakatoa Zaka na wana yakini na Akhera.

Imani peke yake si kitu mbele ya Mwenyezi Mungu ila zikidhihiri athari zake; miongoni mwa zile zilizo muhimu zaidi ni swala na zaka. Kwa ufupi ni kuwa kuamini haki sio fikra ya kichwani wala maneno ya mdomoni; isipokuwa ni matendo na tabia.

Unaweza kuuliza : Wenye kusimamisha Swala na kutoa Zaka tayari wana yakini na Akhera, sasa kuna wajihi gani wa kusema na wana yakini na akhera?

Jibu : Makusudio ni kuwa wanaiamini Akhera kwa imani isiyo na shaka; kama vile wameiona.

Hakika ambao hawaiamin Akhera, tumewapambia vitendo vyao, basi wao wanamangamanga.

Nyoyo zimepofuka, hazioni matendo yao. Kwa hiyo wanafanya bila ya kuhofia hisabu wala adhabu.

Unaweza kuuliza : Hapa Mwenyezi Mungu (s.w.t) ametegemeza kupambia kwake yeye mwenyewe na katika Aya nyingine amekutegemeza kwa shetani: “Lakini shetani aliwapambia vitendo vyao.” Juz. 14 (16:63). Sasa je, kuna wajihi gani wa kuunganisha Aya mbili hizi?

Jibu : Kule kumetegemezwa kupamba kwa shetani kwa kuangalia kuwa yeye ni mhalifu na mtia wasiwasi. Hapa kumetegemzwa kwa Mwenyezi Mungu kwa kuangalia kuwa desturi ya Mwenyezi Mungu na matakwa yake yamepitisha kupofuka na uovu wa matendo yake yule asiyeamini Siku ya Mwisho; sawa kama yalivyopitisha matakwa yake Mwenyezi Mungu kufa kwa yule anayefuata njia inayopelekea kifo.

Kwa maneno mengine ni kuwa yule asiyeamini Akhera anafanya haramu huku akiona ni halali, kwa sababu Mwenyezi Mungu amejaalia kukosa imani ni sababu ya kutojua haramu.

Kama mtu atasema, hilo si ni jambo la kawaida? Tutajibu: Vitu vyote vya kawaida ya maumbile na sababu vinakomea kwake Mwenyezi Mungu Mtukufu, kwa sababu yeye ndiye aliyeleta hayo maumbile ya kawaida na ulimwengu kwa ujumla.

Hao ndio watakaopata adhabu mbaya, na wao katika Akhera ni wenye kupata hasara.

Wamepata hasara duniani kwa sababu wameiacha na wamepata hasara Akhera ya thawabu na kupata adhabu. Hiyo ndiyo hasara ya dhahiri.

وَإِنَّكَ لَتُلَقَّى الْقُرْآنَ مِن لَّدُنْ حَكِيمٍ عَلِيمٍ ﴿٦﴾

6. Na kwa hakika wewe unapewa Qur’an kutoka kwake Mwenye hekima, Mwenye ujuzi.

إِذْ قَالَ مُوسَىٰ لِأَهْلِهِ إِنِّي آنَسْتُ نَارًا سَآتِيكُم مِّنْهَا بِخَبَرٍ أَوْ آتِيكُم بِشِهَابٍ قَبَسٍ لَّعَلَّكُمْ تَصْطَلُونَ ﴿٧﴾

7. Musa alipowaambia ahli zake: Hakika nimeona moto, nitakwenda kuwaletea habari au kuwaletea kijinga kinachowaka ili mpate kuota.

فَلَمَّا جَاءَهَا نُودِيَ أَن بُورِكَ مَن فِي النَّارِ وَمَنْ حَوْلَهَا وَسُبْحَانَ اللَّـهِ رَبِّ الْعَالَمِينَ ﴿٨﴾

8. Basi alipoufikia, pakanadiwa kwamba umebarikiwa uliomo katika moto huu na aliyeko pembezoni mwake na ametakasika Mwenyezi Mungu Mola wa walimwengu wote.

يَا مُوسَىٰ إِنَّهُ أَنَا اللَّـهُ الْعَزِيزُ الْحَكِيمُ ﴿٩﴾

9. Ewe Musa! Hakika mimi ndiye Mwenyezi Mungu Mwenye nguvu, Mwenye hekima.

وَأَلْقِ عَصَاكَ فَلَمَّا رَآهَا تَهْتَزُّ كَأَنَّهَا جَانٌّ وَلَّىٰ مُدْبِرًا وَلَمْ يُعَقِّبْ يَا مُوسَىٰ لَا تَخَفْ إِنِّي لَا يَخَافُ لَدَيَّ الْمُرْسَلُونَ ﴿١٠﴾

10. Na itupe fimbo yako! Alipoiona inatingishika, kama kwamba ni nyoka, aligeuka kurudi nyuma wala hakungoja. Ewe Musa! Usihofu! Hakika mimi hawagopi mbele yangu mitume.

إِلَّا مَن ظَلَمَ ثُمَّ بَدَّلَ حُسْنًا بَعْدَ سُوءٍ فَإِنِّي غَفُورٌ رَّحِيمٌ ﴿١١﴾

11. Ila aliyedhulumu kisha akabadilisha wema baada ya ubaya, basi hakika mimi ni Mwingi wa maghufira, Mwenye kurehemu.

وَأَدْخِلْ يَدَكَ فِي جَيْبِكَ تَخْرُجْ بَيْضَاءَ مِنْ غَيْرِ سُوءٍ فِي تِسْعِ آيَاتٍ إِلَىٰ فِرْعَوْنَ وَقَوْمِهِ إِنَّهُمْ كَانُوا قَوْمًا فَاسِقِينَ ﴿١٢﴾

12. Na ingiza mkono wako katika mfuko wako utatoka mweupe pasipo ubaya. Ni katika ishara tisa kwa Firauni na watu wake. Hakika wao ni watu mafasiki.

فَلَمَّا جَاءَتْهُمْ آيَاتُنَا مُبْصِرَةً قَالُوا هَـٰذَا سِحْرٌ مُّبِينٌ ﴿١٣﴾

13. Zilipowafikia ishara zetu zionyeshazo, walisema: Huu ni uchawi dhahiri.

وَجَحَدُوا بِهَا وَاسْتَيْقَنَتْهَا أَنفُسُهُمْ ظُلْمًا وَعُلُوًّا فَانظُرْ كَيْفَ كَانَ عَاقِبَةُ الْمُفْسِدِينَ ﴿١٤﴾

14. Na wakazikataa kwa dhulma na kujivuna, na hali ya kuwa nafsi zao zina yakini nazo. Basi angalia ulikuwaje mwisho wa wafisadi.

MUSA

Aya 6 – 14

MAANA

Na kwa hakika wewe unapewa Qur’an kutoka kwake Mwenye hekima, Mwenye ujuzi.

Maneno yanaelekezwa kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) . Maana ni kuwa Mwenyezi Mungu ndiye aliyekupa Qur’an na wala haitoki kwako, kama wanavyodai wapinzani.

Musa alipowaambia ahli zake: Hakika nimeona moto, nitakwenda kuwaletea habari au kuwaletea kijinga kinachowaka ili mpate kuota.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 16 (20:10).

Basi alipoufikia, pakanadiwa kwamba umebarikiwa uliomokatika moto huu na aliyeko pembezoni mwake na ametakasika Mwenyezi Mungu Mola wa walimwengu wote.

Makusudio ya moto hapa ni nuru, uliomo ndani yake ni uweza wa Mwenyezi Mungu na aliyeko pembeni ni Musa.

Maana ni kuwa, ewe Musa! Kile ulichokiona ukadhania ni moto ni nuru iliyobarikiwa iliyoletwa na Mwenyezi Mungu kwa uweza wake na wewe uliyesimama pembeni mwa nuru hii pia umebarikiwa vilevile. Kwa sababu mimi nimekuchagua kwa risala yangu, upeleke bishara, kuonya na kueneza baraka ardhini. Hivi ndivyo tulivyoifahamu Aya baada ya kufuatilia na kutaamali. Ikiwa ndio makusudio ni sawa; ikiwa sivyo, lakini maelezo yenyewe ni sahihi.

Ewe Musa! Hakika mimi ndiye Mwenyezi Mungu Mwenye nguvu, Mwenye hekima.

Alimfichulia Mwenyezi Mungu (s.w.t) kuwa anayemuita na kumwambia maneno ni Mola Mwenyezi, ili asikie na kutii.

Na itupe fimbo yako! Alipoiona inatingishika, kama kwamba ni nyoka, aligeuka kurudi nyuma wala hakungoja. Ewe Musa! Usihofu! Hakika mimi hawagopi mbele yangu mitume.

Neno nyoka hapa limefasiriwa kutokana na neno la kiarabu Jann lenye maana ya Jinn. Limefasiriwa kutokana na Aya nyingine zinazotaja nyoka moja kwa moja:

فَأَلْقَاهَا فَإِذَا هِيَ حَيَّةٌ تَسْعَىٰ ﴿٢٠﴾

“Akaitupa mara ikawa nyoka anayekwenda mbio.” Juz. 16 (20:20),

فَأَلْقَىٰ عَصَاهُ فَإِذَا هِيَ ثُعْبَانٌ مُّبِينٌ ﴿١٠٧﴾

“Akaitupa fimbo yake mara ikawa nyoka dhahiri.” Juz. 9 (7:107).

Musa ni mtu, na kawaida ya mtu ni lazima ahofie. Ni nani asiyeogopa atakapoiona kanzu yake iliyo mwilini imegeuka kuwa mnyama anayeshambulia, pete iliyomo kidoleni mwake imekuwa nge au fimbo iliyo mkononi mwake imegeuka nyoka?

Musa alihofia, kwa vile yeye ni mtu, anakula chakula, anatembea sokoni n.k. Lakini Mwenyezi Mungu alimpa amani na akamwambia kuwa wewe ni mjumbe wangu na wajumbe wangu wote wako katika amani na salama.

Ila aliyedhulumu kisha akabadilisha wema baada ya ubaya, basi haki- ka mimi ni Mwingi wa maghufira, Mwenye kurehemu.

Mitume hawahofii, kwa sababu wao hawazidhulumu nafsi zao wala kuwadhulumu wengine; isipokuwa anayetakiwa kuwa na hofu ni yule aliyemdhulumu Mwenyezi Mungu kwa ushirikina na kufuru, kujidhulumu yeye mwenyewe kwa maasi au kuwadhulumu wengine kwa kuingilia haki zao.

Lakini aliyetubia baada ya dhulma yake basi Mwenyezi Mungu atam- takabalia toba na kumpa msamaha na rehema yake.

Na ingiza mkono wako katika mfuko wako utatoka mweupe pasipo ubaya.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 9 (7: 108), Juz. 16 (20:22) na Juzuu hii tuliyo nayo (26:33).

Ni katika ishara tisa kwa Firauni na watu wake. Hakika wao ni watu mafasiki.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 15 (17:101).

Zilipowafikia ishara zetu zionyeshazo, walisema: Huu ni uchawi dhahiri.

Yaani zionyeshazo watu haki watakapoona hiyo miujiza tisa aliyokuja nayo Musa. Firauni na watu wake waliiona haki walipoona miujiza hii tisa, lakini walifanya kiburi na inadi, wakamkadhibisha Mwenyezi Mungu na wao wenyewe kwa kusema kuwa ni uchawi dhahiri. Ndio maana Mwenyezi Mungu Mtukufu akasema:

Na wakazikataa kwa dhulma na kujivuna, na hali yakuwa nafsi zao zina yakini nazo.

Nyoyo zao na akili zao zilikuwa na yakini na ukweli wa Musa na miujiza yake, lakini walimpinga kwa ndimi zao kuhofia manufaa yao na vyeo. Haya ndio makusudio ya kauli yake Mwenyezi Mungu: ‘Kwa dhulma na kujivuna.

Basi angalia ulikuwaje mwisho wa wafisadi katika ardhi kwa kufuru, dhulma na ufisadi?

وَلَقَدْ آتَيْنَا دَاوُودَ وَسُلَيْمَانَ عِلْمًا وَقَالَا الْحَمْدُ لِلَّـهِ الَّذِي فَضَّلَنَا عَلَىٰ كَثِيرٍ مِّنْ عِبَادِهِ الْمُؤْمِنِينَ ﴿١٥﴾

15. Na hakika tulimpa Daud na Suleiman elimu na wakasema: Sifa njema zote (alham-du-lillah) ni za Mwenyezi Mungu ambaye ametufadhilisha kuliko wengi katika waja wake waumini.

وَوَرِثَ سُلَيْمَانُ دَاوُودَ وَقَالَ يَا أَيُّهَا النَّاسُ عُلِّمْنَا مَنطِقَ الطَّيْرِ وَأُوتِينَا مِن كُلِّ شَيْءٍ إِنَّ هَـٰذَا لَهُوَ الْفَضْلُ الْمُبِينُ ﴿١٦﴾

16. Na Suleiman alimrithi Daud. Na akasema: “Enyi watu! Tumefunzwa usemi wa ndege. Na tumepewa kila kitu. Hakika hii ni fadhila iliyo dhahiri.

وَحُشِرَ لِسُلَيْمَانَ جُنُودُهُ مِنَ الْجِنِّ وَالْإِنسِ وَالطَّيْرِ فَهُمْ يُوزَعُونَ ﴿١٧﴾

17. Na alikusanyiwa Suleiman majeshi yake kutokana na majini na watu na ndege nayo yakapangwa kwa nidhamu.

حَتَّىٰ إِذَا أَتَوْا عَلَىٰ وَادِ النَّمْلِ قَالَتْ نَمْلَةٌ يَا أَيُّهَا النَّمْلُ ادْخُلُوا مَسَاكِنَكُمْ لَا يَحْطِمَنَّكُمْ سُلَيْمَانُ وَجُنُودُهُ وَهُمْ لَا يَشْعُرُونَ ﴿١٨﴾

18. Hata walipofikia kwenye bonde la chungu, alisema chungu mmoja: Enyi chungu, ingieni maskani zenu, asije akawaponda Suleiman na jeshi lake na hali wao hawatambui.

فَتَبَسَّمَ ضَاحِكًا مِّن قَوْلِهَا وَقَالَ رَبِّ أَوْزِعْنِي أَنْ أَشْكُرَ نِعْمَتَكَ الَّتِي أَنْعَمْتَ عَلَيَّ وَعَلَىٰ وَالِدَيَّ وَأَنْ أَعْمَلَ صَالِحًا تَرْضَاهُ وَأَدْخِلْنِي بِرَحْمَتِكَ فِي عِبَادِكَ الصَّالِحِينَ ﴿١٩﴾

19. Basi akatabasamu akicheka kwa kauli yake, akasema: Ewe Mola wangu! Nizindue niishukuru neema yako uliyonineemesha na wazazi wangu na nipate kutenda mema unayoyaridhia na uni- ingize kwa rehema yako katika waja wako wema.

SULEIMAN

Aya 15 – 19

MAANA

Na hakika tulimpa Daud na Suleiman elimu, iliyowaongoza kwenye utiifu wa Mwenyezi Mungu na manufaa ya watu. Wala hawakujivuna nayo kwa waja wa Mungu au kuvumbua nayo silaha za maangamizi ili kuwakandamiza wanyonge wawanyonye nyenzo zao.

Bali hawa wawili walimtii Mwenyezi Mungu katika maamrisho yake na makatazo yake na wakamshukuru kwa neema ya elimu ambayo hailinganishwi na chochotena wakasema: Sifa njema zote (alhamdu lillah) ni za Mwenyezi Mungu ambaye ametufadhilisha kuliko wengi katika waja wake waumini.

Makusudio ya kufadhilishwa (kufanywa bora) hapa, ni kufadhilishwa kwa elimu yenye manufaa. Maana ya kuiliko wengi katika waumini ni wale wasiofikia cheo chao cha elimu.

Hapo kuna ishara kuwa katika waumini wako waliofadhilishwa zaidi yao. Na hivyo ndivyo ilivyo.

Kwa vyovyote iwavyo ni kuwa ubora mbele ya Mwenyezi Mungu haupimwi kwa elimu wala kwa kuupeleka upepo au kulainisha chuma; isipokuwa ni kwa manufaa ya watu na masilahi yao.

Na Suleiman alimrithi Daud.

Daud(a.s ) ni katika kizazi cha Ya’qub bin Is-haq bin Ibrahim. Mwenyezi Mungu alimtukuza kwa utume, akamteremshia Zabur, akamfanya ni khalifa katika ardhi, akamuhusisha kuwa na sauti nzuri zaidi na akamlainishia chuma. Yeye ni mfalme wa pili wa dola ya kiyahudi.

Alipewa jina la Mfalme Daud. Mfalme wa kwanza alikuwa ni Talut, kama alivyosema Mwenyezi Mungu:

إِنَّ اللَّـهَ قَدْ بَعَثَ لَكُمْ طَالُوتَ مَلِكًا ﴿٢٤٧﴾

Hakika Mwenyezi Mungu amewachagulia Talut kuwa mfalme. Juz.2 (2:247).

Mwanawe Suleiman(a.s ) alikuwa ni mtume vile vile. Naye Mwenyezi Mungu alimpa neema nyingi, zikiwemo kurithi ufalme wa baba yake. Historia inasema kuwa ufalme wao uliendelea kwa miaka sabini.

Baada ya kufa Suleiman, mayahudi waligawanyika dola mbili zinazopigana: Dola ya Israil na dola ya Yahudha. Alipokuja Nebuchadnezzar aliwafyeka na hakukua na dola tena ya kiyahudi, mpaka pale ukoloni wa Anglo America ulipoanzisha kambi ya kijeshi kulinda masilahi yake mashariki ya kati, ukaipa jina la dola Israil kwenye ardhi ya Palestina mnamo mwaka 1948.

Mayahudi wanamzungumza vibaya mfalme wao Daud, kwamba alikuwa akiwapora wanawake na kuwaua waume zao na mwanawe Suleman alikuwa ni jabari mkandamizaji na mwenye israfu.

Baadhi ya wafasiri wanasema kuwa makusudio ya kauli yake Mwenyezi Mungu: “Na Suleiman alimrithi Daud” ni kuwa alirithi elimu tu kutoka kwa baba yake. Lakini ilivyo hasa ni kuwa Aya inafahamisha urithi wa ufalme; kama ilivyotokea hasa. Ama elimu haiwi kwa kurithi, bali ni kwa juhudi au kwa wahyi kutoka kwa Mwenyezi Mungu.

Kuna tofauti katika Hadith ya “Sisi Mitume haturithiwi,” baina ya Waislamu. Kuna walioithibitisha na walioikanusha.

Na akasema: Enyi watu! Tumefunzwa usemi wa ndege.

Uislamu umethibitisha fikra ya muujiza mikononi mwa mitume. Mwenye kuikana si Mwislamu, kwa sababu ukanusho huo ni sawa na kumkadhibisha Mwenyezi Mungu na Mtume wake. Ni kwa muujiza pekee yake ndio tunaweza kufasiri kauli ya Nabii Suleiman: ‘Na tumefunzwa usemi wa ndege.”

Na tumepewa kila kitu. Hakika hii ni fadhila iliyo dhahiri.

Makusudio ya neno ‘kila’ hapa ni wingi sio kuenea kwenye kila kitu; ni sawa na kusema fulani ana kila kitu, kwa kuelezea kuwa ana vitu vingi.

Aya inafahamisha kuwa ndege wana utambuzi na lugha inayofahamika. Hilo linasisitizwa na kauli yake Mwenyezi Mungu:

وَمَا مِن دَابَّةٍ فِي الْأَرْضِ وَلَا طَائِرٍ يَطِيرُ بِجَنَاحَيْهِ إِلَّا أُمَمٌ أَمْثَالُكُم ﴿٣٨﴾

Na hakuna mnyama katika ardhi wala ndege arukaye kwa mbawa zake, ila ni umma kama nyinyi. Juz. 7 (6:38).

Na alikusanyiwa Suleiman majeshi yake kutokana na majini na watu na ndege, nayo yakapangwa kwa nidhamu.

Neno ‘kutokana’ ni baadhi; yaani baadhi ya majini, watu na ndege. Tumesema mara nyingi kwamba sisi tunaamini kuweko majini, kwa sababu Qur’an inathibitisha hilo na akili haikatai.

Suleiman alikuwa na jeshi la majini, watu na ndege. Kila moja ya makundi haya matatu lilikuwa na kamanda wake anayechunga nidhamu ya kutembea n.k. Hii ndio maana ya kupangwa kwa nidhamu.

SOMO NA MAZINGATIO KATIKA CHUNGU WA SULEIMAN

Hata walipofikia kwenye bonde la chungu, alisema chungu mmoja: Enyi chungu, ingieni maskani zenu, asije akawaponda Suleiman na jeshi lake na hali wao hawatambui.

Wafasiri wametofautiana kuhusu bonde hili. Kuna waliosema ni Taif na wengine wakasema ni Sham. Vyovyote iwavyo ni kuwa Aya inafahamisha kuwa wadudu chungu wana utambuzi, lugha na nidhamu. Haya yamethibitishwa na elimu. Ama Suleiman kujua lugha ya chungu, hilo halina tafsiri isipokuwa ni muujiza.

Unaweza kuliza : Vipi Suleiman aliweza kusikia maneno ya chungu na yaye alikuwa mbali nao kiasi ambacho anayejua ni Mungu tu; kama tunavyojua kuwa lau mmoja wetu ataingiwa na chungu sikioni hawezi kusikia?

Jibu : Baadhi ya riwaya zinasema kuwa upepo ulichukua maneno ya chungu kwa Suleiman. Haya yanatiliwa nguvu na kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu:

فَسَخَّرْنَا لَهُ الرِّيحَ تَجْرِي بِأَمْرِهِ ﴿٣٦﴾

“Basi tukamtiishia upepo ukienda kwa amri yake.” (38:36).

Basi akatabasamu akicheka kwa kauli yake, akasema: Ewe Mola wangu! Nizindue niishukuru neema yako uliyonineemesha na wazazi wangu na nipate kutenda mema unayoyaridhia na uniingize kwa rehe- ma yako katika waja wako wema.

Suleiman alipoomba ufalme ambao hataupata yeyote baada yake, alikusudia kuwatumia majini, upepo, ndege n.k. Kwa sababu ni wengi waliomakinika katika ardhi.

Suleiman alipofika kwenye bonde la chungu na upepo kuchukua maneno ya chungu hadi masikioni mwake na kufahamu maana yake, alitambua kuwa haya ni katika ambayo hatakuwa nayo yeyote baada yake.

Basi aliihisi raha kwa neema hii na akatekeleza haki yake ya kumshukuru Mwenyezi Mungu. Kutambua tu, kwamba neema hii inatoka kwa Mwenyezi Mungu ni aina ya shukrani. Na shukrani kubwa zaidi ni kufanya kheri kwa ajili ya Mwenyezi Mungu.

Kama ambavyo Aya inafahamisha kuwa Suleiman ana dola na jeshi lake na kwamba Mwenyezi Mungu (s.w.t) amempa elimu ya kujua lugha ya chungu; vile vile Aya inafahamisha kuwa chungu naye ana dola yake na raia zake na kwamba Mwenyezi Mungu naye amempa elimu ya kuwajua baadhi ya binadamu na majina yao. Kama si hivyo alijuaje kuwa huyu anayekuja na msafara wa jeshi ni Suleiman bin Daud?

Hakika mdudu huyo aliyewaambia wenzake, alikuwa mkubwa katika ulimwengu wake, kama alivyokuwa Suleiman katika ulimwengu wake. Na kwamba alikuwa akiwafanyia uadilifu raia wake, akiwahurumia, kujali masilahi yao na kutekelza haki kamili ya uongozi, kama anavyofanya Suleiman na viongozi wengineo waadilifu na wa haki.

Mwenye kuchunguza na kutaamali tukio la chungu na Suleiman atafikia kwenye somo na mazingatio yafuatayo:-

1. Nidhamu na mpangilio uko kwenye viumbe vyote; kuanzia kidogo, kama chunguchungu, hadi kikubwa, kama sayari. Hakuna tafisiri ya nid- hamu hii ya hali ya juu na mpangilio huu wa ajabu isipokuwa kuweko Muweza aliye Mjuzi: “Na ameumba kila kitu na akikadiria kipimo.” Juz. 18 (25:2).

2. Ushirikiano na kutambua majukumu, hakuhusuki na watu tu, bali hata kwa wanyama, ndege, wadudu n.k. Kijichembe hiki ambacho mara nyingine hata hakionekani kwa macho, kilipohisi hatari kwa jamaa zake, kilisimama kuwahadharisha kikisema: ‘ingieni maskani yenu, asije akawaponda Suleiman na jeshi lake.’ Wataalamu wameleta ushahidi mwingi wa hakika hii ya maisha ya wanyama.

3. Mtu ni lazima ashukuru anaponeemeshwa na Mwenyezi Mungu (s.w.t) kwa elimu, utawala au mengine. Amshukuru Mwenyezi Mungu na awanyenyekee watu; sio kujivuna na kujiona kwa wengine kwa sababu ya neema ya Mwenyezi Mungu.

Pia, mtu akineemeka, inatakikana ajue kwamba Mwenyezi Mungu amekwishaitoa neema kama hiyo au kushinda hiyo kwa kiumbe kilicho dhaifu zaidi; na binadamu sio peke yake anayeneemeshwa na Mwenyezi Mungu.

Uvumbuzi wa elimu umegundua kuwa kuna maumbile makubwa zaidi ya haya tuyaonayo; hakuna hata mmoja anayeweza kujua hakika yake isipokuwa Muumba. Binadamu si chochote katika maumbile hayo. Hayo yanaashiriwa na kauli yake Mwenyezi Mungu:

لَخَلْقُ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ أَكْبَرُ مِنْ خَلْقِ النَّاسِ ﴿٥٧﴾

“Bila shaka kuumba mbingu na ardhi ni kukubwa zaidi kuliko kuwaumba watu.” (40:57).

Kwa hiyo basi, Aya:

وَاللَّـهُ يَخْتَصُّ بِرَحْمَتِهِ مَن يَشَاءُ ﴿١٠٥﴾

“Na Mwenyezi Mungu humhusisha kwa rehema zake amtakaye.” Juz. 1 (2:105),

تُؤْتِي الْمُلْكَ مَن تَشَاءُ ﴿٢٦﴾

“Humpa ufalme umtakaye.” Juz. 3 (3:26)

وَإِن مِّنْ أُمَّةٍ إِلَّا خَلَا فِيهَا نَذِيرٌ ﴿٢٤﴾

“Na hapana umma wowote ila ulipata muonyaji.” (35:24)

Zote hizi, na mfano wake, zinaenea kwa binadamu na wasiokuwa binadamu.

Ikumbukwe kwamba Mwenyezi Mungu amelitumia neno umma kwa wasiokuwa binadamu; kama kauli yake: Na hakuna mnyama katika ardhi wala ndege arukaye kwa mbawa zake, ila ni umma kama nyinyi.” Juz. 7 (6:38).

10

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TISA

وَتَفَقَّدَ الطَّيْرَ فَقَالَ مَا لِيَ لَا أَرَى الْهُدْهُدَ أَمْ كَانَ مِنَ الْغَائِبِينَ ﴿٢٠﴾

20. Na akawakagua ndege na akasema: Mbona simwoni Hud-hud au amekuwa miongoni mwa walio ghaibu.

لَأُعَذِّبَنَّهُ عَذَابًا شَدِيدًا أَوْ لَأَذْبَحَنَّهُ أَوْ لَيَأْتِيَنِّي بِسُلْطَانٍ مُّبِينٍ ﴿٢١﴾

21. Kwa yakini nitamwadhibu kwa adhabu kali au nitamchinja, au aniletee hoja iliyo wazi.

فَمَكَثَ غَيْرَ بَعِيدٍ فَقَالَ أَحَطتُ بِمَا لَمْ تُحِطْ بِهِ وَجِئْتُكَ مِن سَبَإٍ بِنَبَإٍ يَقِينٍ ﴿٢٢﴾

22. Basi hakukaa sana mara akasema: Nimegundua usiloligundua na nimekujia na habari za yakini kutoka Sabai.

إِنِّي وَجَدتُّ امْرَأَةً تَمْلِكُهُمْ وَأُوتِيَتْ مِن كُلِّ شَيْءٍ وَلَهَا عَرْشٌ عَظِيمٌ ﴿٢٣﴾

23. Hakika nimemkuta mwanamke anayewatawala na amepewa kila kitu na anacho kiti cha enzi kikubwa.

وَجَدتُّهَا وَقَوْمَهَا يَسْجُدُونَ لِلشَّمْسِ مِن دُونِ اللَّـهِ وَزَيَّنَ لَهُمُ الشَّيْطَانُ أَعْمَالَهُمْ فَصَدَّهُمْ عَنِ السَّبِيلِ فَهُمْ لَا يَهْتَدُونَ ﴿٢٤﴾

24. Nimemkuta yeye na watu wake wanalisujudia jua badala ya Mwenyezi Mungu; na shetani amewapambia vitendo vyao na akawazuilia njia. Kwa hivyo hawakuongoka.

أَلَّا يَسْجُدُوا لِلَّـهِ الَّذِي يُخْرِجُ الْخَبْءَ فِي السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ وَيَعْلَمُ مَا تُخْفُونَ وَمَا تُعْلِنُونَ ﴿٢٥﴾

25. Kwamba hawamsujudii Mwenyezi Mungu ambaye huyatoa yaliyofichikana katika mbingu na ardhi na huyajua mnayoyaficha na mnayoyadhihirisha.

اللَّـهُ لَا إِلَـٰهَ إِلَّا هُوَ رَبُّ الْعَرْشِ الْعَظِيمِ ﴿٢٦﴾

26. Mwenyezi Mungu hapana Mola ila Yeye Mola wa arshi tukufu.

MBONA SIMWONI HUD-HUD

Aya 20 – 26

MAANA

Na akawakagua ndege na akasema: Mbona simwoni Hud-hud au amekuwa miongoni mwa walio ghaibu. Kwa yakini nitamwadhibu kwa adhabu kali au nitamchinja, au aniletee hoja iliyo wazi.

Suleiman alikuwa na aina ya ndege wanaofuata amri yake, wakiwa wako huru sio ndani ya tundu. Siku moja alipokuwa anawakaguakagua, kama anavyokagua kamanda jeshi lake, akamkosa Hud-hud, na hakuwa amemruhusu kundoka. Akatishia – mbele ya ndege wengine - kumwadhibu; kama kumtia jela n.k. Au kumuua, ikiwa hatakuwa na hoja wazi ya udhuru wa kutoweka kwake.

Basi hakukaa sana mara akasema: Nimegundua usiloligundua.

Haukupita muda wa kutishia Suleiman ila alikuja Hud-hud na akasema: Nimegundua kitu muhimu usichokijua pamoja na upana wa elimu yakona nimekujia na habari za yakini kutoka Sabai.

Hakika nimemkuta mwanamke anayewatawala na amepewa kila kitu na anacho kiti cha enzi kikubwa.

Makusudio ya Sabai (Sheba) ni watu wanaonasibika na Sabai bin Yashjab bin Ya’rub bin Qahtan. Mwanamke (Malkia wa Sheba) alikuwa ni Bilqis bint Sharahil, aliyekuwa mfalme na kurithiwa na binti yake huyo, aliyekuwa akimiliki utajiri na starehe zote.

Alikuwa akikaa kwenye kiti cha hali ya juu na cha thamani, kikiwa kimepambwa na nyoyo za maskini na kupakwa jasho lao na damu zao. Ajabu ni kauli ya baadhi ya wafasiri waliosema kuwa kilikuwa kimeezekwa na kwamba upana wake ulikuwa ni futi 80 za mraba na kimo chake pia ni futi 80.

Nimemkuta yeye na watu wake wanalisujudia jua badala ya Mwenyezi Mungu; na shetani amewapambia vitendo vyao na akawazuilia njia. Kwa hivyo hawakuongoka.

Unaweza kuuliza : Ndege, wanyama na wadudu kwa maumbile yao wanajua chakula chao, kinywaji chao, kinachowadhuru na kinachowanufaisha. Wanajua hivyo na vinginevyo kwa sababu ndio nyenzo za kuishi kwao, kuhifadhi maisha yao na kuendela kuwepo.

Lakini kumtambua mume na mke katika binadamu, kujua kuwa kabila hili ni la wasabai na lile ni la Thamud, kujua hawa wanamuamini Mwenyezi Mungu na wale ni makafiri, haya yote hayalingani na maisha yao kwa umbali wala karibu.

Basi Hud-hud aliwezaje kujua jina la kabila, mwanamke anayewatawala na kwamba wao wanaabudu jua? Sisi wanadamu tu, hatuwezi kutambua baina ya mume na mke katika aina nyingi za ndege, wadudu na wanyama?

Jibu : Aya imethibitisha sifa hizi kwa Hud-hud wa Suleiman tu, jambo ambalo halilazimishi kuthibiti katika ndege wote au kwa Hud-hud wote; kama ambavyo kujua kiingereza kwa mtu fulani hakulazimishi kujua kiingereza kwa watu wote. Ama maarifa ya Hud-hud wa Suleiman kwa aliyoyatolea habari, sisi hatuna tafsiri yake isipokuwa matakwa ya Mwenyezi Mungu.

Kwamba hawamsujudii Mwenyezi Mungu ambaye huyatoa yaliyofichikana katika mbingu na ardhi na huyajua mnayoyaficha na mnayoyadhihirisha.

Makusudio ya yaliyofichikana hapa ni kheri za ulimwengu. Mwenyezi Mungu (s.w.t) huzitoa kwa waja wake kwa sababu zake za kimaumbile; kama mimea inayotoka ardhini kwa sababu ya mvua, kuzaana kwa sababu ya kupandishwa au kwa nyenzo nyingine za kielimu anazozitoa Mwenyezi Mungu kupitia mikononi mwa wataalamu na vifaa vyao.

Sababu na nyenzo zote hizi, Mwenyezi Mungu (s.w.t) ameziletea ibara ya mkono wa Mungu pale aliposema:

أَوَلَمْ يَرَوْا أَنَّا خَلَقْنَا لَهُم مِّمَّا عَمِلَتْ أَيْدِينَا أَنْعَامًا فَهُمْ لَهَا مَالِكُونَ ﴿٧١﴾

“Je, hawaoni kwamba tumewaumbia kutokana na iliyofanya mikono yetu wanyama wa mifugo, na wao wakawa wenye kuwamiliki?” (36:71).

Mwenyezi Mungu hapana Mola ila Yeye Mola wa arshi tukufu, ambaye haufananishwi ufalme wake wala ukuu wake na wa yeyote.

قَالَ سَنَنظُرُ أَصَدَقْتَ أَمْ كُنتَ مِنَ الْكَاذِبِينَ ﴿٢٧﴾

27.Akasema: Tutatazama, umesema kweli au uko katika waongo.

اذْهَب بِّكِتَابِي هَـٰذَا فَأَلْقِهْ إِلَيْهِمْ ثُمَّ تَوَلَّ عَنْهُمْ فَانظُرْ مَاذَا يَرْجِعُونَ ﴿٢٨﴾

28. Nenda na barua yangu hii na uwafikishie, kisha waache na utazame watarejesha nini.”

قَالَتْ يَا أَيُّهَا الْمَلَأُ إِنِّي أُلْقِيَ إِلَيَّ كِتَابٌ كَرِيمٌ ﴿٢٩﴾

29. Akasema: Enyi waheshimiwa! Hakika imeletwa kwangu barua tukufu.

إِنَّهُ مِن سُلَيْمَانَ وَإِنَّهُ بِسْمِ اللَّـهِ الرَّحْمَـٰنِ الرَّحِيمِ ﴿٣٠﴾

Imetoka kwa Suleiman, nayo ni: Kwa jina la Mwenyezi Mungu, Mwingi wa rehema, Mwenye kurehemu.

أَلَّا تَعْلُوا عَلَيَّ وَأْتُونِي مُسْلِمِينَ ﴿٣١﴾

31. Kwamba msinifanyie jeuri na fikeni kwangu mkiwa waislamu.

قَالَتْ يَا أَيُّهَا الْمَلَأُ أَفْتُونِي فِي أَمْرِي مَا كُنتُ قَاطِعَةً أَمْرًا حَتَّىٰ تَشْهَدُونِ ﴿٣٢﴾

Akasema: Enyi waheshimiwa! Nipeni ushauri katika jambo langu hili, kwani mimi sikati shauri lolote mpaka muhudhurie.

قَالُوا نَحْنُ أُولُو قُوَّةٍ وَأُولُو بَأْسٍ شَدِيدٍ وَالْأَمْرُ إِلَيْكِ فَانظُرِي مَاذَا تَأْمُرِينَ ﴿٣٣﴾

33. Wakasema: Sisi ni wenye nguvu na wakali wa vita, na amri iko kwako, basi tazama nini unaamrisha.

قَالَتْ إِنَّ الْمُلُوكَ إِذَا دَخَلُوا قَرْيَةً أَفْسَدُوهَا وَجَعَلُوا أَعِزَّةَ أَهْلِهَا أَذِلَّةً وَكَذَٰلِكَ يَفْعَلُونَ ﴿٣٤﴾

34. Akasema: Hakika wafalme wanapouingia mji wanauharibu na wanawafanya wale watukufu wake kuwa wanyonge, na hivyo ndivyo watendavyo.

وَإِنِّي مُرْسِلَةٌ إِلَيْهِم بِهَدِيَّةٍ فَنَاظِرَةٌ بِمَ يَرْجِعُ الْمُرْسَلُونَ ﴿٣٥﴾

35. Na mimi ninawapelekea zawadi ningoje watakayorudi nayo wajumbe.

NENDA NA BARUA YANGU HII

Aya 27 – 35

MAANA

Akasema: Tutatazama, umesema kweli au uko katika waongo.

Hud-hud alimpa habari Suleiman kuhusu watu wa Sabai, akamwambia tutachunguza maneno yako tuone kama yana ukweli.

Nenda na barua yangu hii na uwafikishie, kisha waache na utazame watarejesha nini.

Suleiman aliwaandikia barua watu wa Sabai akiwaita kwenye twaa yake na akampatia Hud-hud akamwamabia ifikishe hii kwa njia yoyote, kisha ujitenge nao sehmu ambayo utaweza kujua au kusikia wanasema nini na wanaafikiana nini, kisha urudi uniletee habari.

Akasema: Enyi waheshimiwa! Hakika imeletwa kwangu barua tukufu, imetoka kwa Suleiman, nayo ni: Kwa jina la Mwenyezi Mungu, Mwingi wa rehema, Mwenye kurehemu, kwamba msinifanyie jeuri na fikeni kwangu mkiwa waislamu.

Hud-hud alichukua barua na akaitupa mahali kwenye kasri ya malkia kwa namna ambayo inaweza kuonekana bila ya kujulikana aliyeileta, kama linavyojulisha neno ’imeletwa.’ Kisha Hud-hud akajiweka kando kuchunguza harakati za watu na mazungumzo yao; sawa na mwandishi wa habari.

Malkia alipoiona na akajua kilichoandikwa, aliwakusanya mawaziri na washauri, akawaonyesha na akaisifu kwa utukufu, kwa sababu mwenye barua hiyo ni mwenye cheo kikubwa cha heshima.

Bismillah ilikuwa ni sehemu ya barua hiyo ambayo aliifupisha kwa kutoa mwito wa utiifu bila ya utangulizi wala kuzidisha maneno. Hii ndio desturi ya mitume katika barua zao kwenda kwa wafalme. Mtume(s.a.w.w) alikuwa akifupiliza barua zake kwa wafalme kwa kusema: “Silimu utasalimika” baada ya bismillah na Alhamdu.

Akasema: Enyi waheshimiwa! Nipeni ushauri katika jambo langu hili, kwani mimi sikati shauri lolote mpaka muhudhurie.

Nipeni ushauri, maana mimi sipitishi jambo mpaka nipate rai yenu. Hii inaashiria kuwa demokrasia ya serikali ina mizizi yake katika historia ya mbali; kisha ikakua hadi ilivyo hivi sasa.

Wakasema: Sisi ni wenye nguvu na wakali wa vita, na amri iko kwako, basi tazama nini unaamrisha.

Walisema hivi kwa njia ya kujishasha, kutangaza nguvu zao na kumwachia majukumu yote malkia hata kama uamuzi wake utakuwa na mwisho mbaya.

Akasema: Hakika wafalme wanapouingia mji wanauharibu na wanawafanya wale watukufu wake kuwa wanyonge, na hivyo ndivyo watendavyo.

Mfasiri mmoja wa kisasa akifafanua Aya hii anasema: “Inajulikana kuwa ni tabia ya kimaumbile ya wafalme wanapoingia mji wanaeneza ufisadi na wanawaangusha viongozi na kuwafanya ni watu wa chini. Haya ndio mazowea yao wanayoyafanya.”

Ukweli ni kuwa ufisadi unaenea ardhini kwa kiasi cha nguvu za mfisadi, na unazidi kadiri nguvu zao zinavyozidi, wawe wafalme au si wafalme. Aya imewahusu kuwataja wafalme kwa sababu wao wanakuwa na nguvu zaidi kuliko wengine.

Uhakika wa mhalifu unajificha kwenye unyonge wake, na unajitokeza anapokuwa na guvu. Kwa hiyo ni makosa kuuweka uhakika wa mtu anapokuwa mnyonge.

Kuna badhi ya watu tunaowajua ambao walikuwa ni mashuhuri kwa takua wakati walipokuwa hohehahe, lakini mara tu walipopata madaraka wakaandamwa na tuhuma ambazo hazifutiki hata siku zikipita. Tunamuomba Mwenyezi Mungu atupe hidaya sisi na wao.

Kwa hiyo inatubainikia kuwa sifa ya ufisadi haihusiki kwa wafalme tu wala si tabia yao ya kimaumbile, vinginevyo ingelikuwa ni muhali kupatikana uadilifu na utengeneo kwao. Isipokuwa hiyo ni tabia ya wahalifu wenye nguvu; ni sawa iwe nguvu ya mali, cheo, akili au utawala na, kidini au kidunia. Wala hakuna wa kumzuia mkosefu mwenye nguvu isipokuwa dini tu.

Imam Ali(a.s) anasema: Mwenye uzowefu wa maisha na uelewa wa mambo anaweza akaona ujanja wa kukwepa amri ya Mwenyeezi Mungu akaachana nao; lakini asiyejilinda (na dini) anaitumia fursa hiyo (Nahjul balagha khutba 41).

Na mimi ninawapelekea zawadi ningoje watakayorudi nayo wajumbe.

Mawaziri na washauri walimwachia malkia amri ya vita au usalama. Kabla ya kuamua chochote aliona kwanza ampelekee Suleiman zawadi ya thamani kubwa, kisha aangalie, je, ataikubali au ataikataa. Akiikubali basi atakuwa anatafuta dunia sio dini. Kwa hiyo ataweza kumtengeneza kwa mali na kama ataikataa na kung’ang’ania kuwa tumwendee tukiwa wanyenyekevu, basi atakua ni katika wenye misingi ya risala na misimamo ya itikadi yao wakijitolea muhanga kwa kila hali. Watu wa namna hiyo haifai kuwapiga vita.

فَلَمَّا جَاءَ سُلَيْمَانَ قَالَ أَتُمِدُّونَنِ بِمَالٍ فَمَا آتَانِيَ اللَّـهُ خَيْرٌ مِّمَّا آتَاكُم بَلْ أَنتُم بِهَدِيَّتِكُمْ تَفْرَحُونَ ﴿٣٦﴾

36. Alipokuja kwa Suleiman, alisema: Hivi nyinyi mnanisaidia kwa mali? Aliyonipa Mwenyezi Mungu ni bora zaidi kuliko aliyowapa nyinyi, lakini nyinyi mnaifurahia zawadi yenu.

ارْجِعْ إِلَيْهِمْ فَلَنَأْتِيَنَّهُم بِجُنُودٍ لَّا قِبَلَ لَهُم بِهَا وَلَنُخْرِجَنَّهُم مِّنْهَا أَذِلَّةً وَهُمْ صَاغِرُونَ ﴿٣٧﴾

37. Rejea kwao! Kwa yakini tutawajia na majeshi wasiyoweza kuyakabili na hakika tutawatoa humo na hali wao wamekuwa madhalili na wanyonge.

قَالَ يَا أَيُّهَا الْمَلَأُ أَيُّكُمْ يَأْتِينِي بِعَرْشِهَا قَبْلَ أَن يَأْتُونِي مُسْلِمِينَ ﴿٣٨﴾

38. Akasema: Enyi wakuu wa baraza! Ni nani kati yenu atakayeniletea kiti chake cha enzi kabla hawajanijia nao wamekwisha salimu amri.

قَالَ عِفْرِيتٌ مِّنَ الْجِنِّ أَنَا آتِيكَ بِهِ قَبْلَ أَن تَقُومَ مِن مَّقَامِكَ وَإِنِّي عَلَيْهِ لَقَوِيٌّ أَمِينٌ ﴿٣٩﴾

39. Akasema afriti katika majini: Mimi nitakuletea kabla hujainuka mahala pako. Na mimi hakika nina nguvu, mwaminifu.

قَالَ الَّذِي عِندَهُ عِلْمٌ مِّنَ الْكِتَابِ أَنَا آتِيكَ بِهِ قَبْلَ أَن يَرْتَدَّ إِلَيْكَ طَرْفُكَ فَلَمَّا رَآهُ مُسْتَقِرًّا عِندَهُ قَالَ هَـٰذَا مِن فَضْلِ رَبِّي لِيَبْلُوَنِي أَأَشْكُرُ أَمْ أَكْفُرُ وَمَن شَكَرَ فَإِنَّمَا يَشْكُرُ لِنَفْسِهِ وَمَن كَفَرَ فَإِنَّ رَبِّي غَنِيٌّ كَرِيمٌ ﴿٤٠﴾

40. Akasema mwenye elimu ya Kitabu: Mimi nitakuletea kabla ya kupepesa jicho lako. Basi alipokiona kimewekwa mbele yake, alisema: Haya ni katika fadhila za Mola wangu, ili anijaribu, nitashukuru au nitakufuru. Na mwenye kushukuru kwa hakika anashukuru kwa manufaa ya nafsi yake na mwenye kukufuru kwa hakika Mola wangu ni Mkwasi, Mkarimu.

KITI CHA ENZI CHA BILQIS

Aya 36 – 40

MAANA

Alipokuja mjumbe kwa Suleiman, alisema: Hivi nyinyi mnanisaidia kwa mali? Aliyonipa Mwenyezi Mungu ni bora zaidi kuliko aliyowapa nyinyi, lakini nyinyi mnaifurahia zawadi yenu.

Ujumbe wa malkia ulifika kwa Suleiman ukiwa na zawadi ya thamani kubwa. Alipoiona alimwambia yule aliyekuja nayo kuwa mimi ninawaita kwa Mwenyezi Mungu na nyinyi mnanipa mali nami nina mali nyingi kama uonavyo; bali Mwenyezi Mungu amenineemesha kwa makubwa zaidi kuliko mali, ambayo ni: utume, elimu na kuutumia upepo majini na ndege. Hivi mnanikisia kuwa ni katika waabudu mali?

Kisa hiki kinatukumbusha makuraishi, wakati walipomtaka mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) aachane na jambo lake hili, wakamwambia:“Ukiwa, kwa jambo hili, unataka mali basi sisi tutakukusanyia mali mpaka uwe ni tajiri zaidi kuliko sisi, na kama unataka ufalme tutakupa.

Waliposhindwa naye wakakimbilia kwa ami yake Abu Talib ili amkinaishe mwana wa nduguye akubali mali, vinginevyo atapigwa vita. Mtume(s.a.w. w ) akasema maneno yake mashuhuru:“Wallah! Ewe Ami yangu! Lau wataliweka jua kuumeni kwangu na mwezi kushotoni kwangu kwamba niliache jambo hili sitaliacha mpaka alidhihirishe Mwenyezi Mungu au niangamie.”

Rejea kwao! Kwa yakini tutawajia na majeshi wasiyoweza kuyakabili na hakika tutawatoa humo na hali wao wamekuwa madhalili na wanyonge.

Maneno haya anaambiwa kiongozi wa msafara uliokuja na zawadi. Maana yake ni rejea wewe na wenzako na hiyo mliyokuja nayo. Wambie watu wako kuwa mimi nitakuja na jeshi langu la watu majini na ndege ambalo hamtaliweza si nyinyi wala wengene.

Hud-hud alikuwa amemwambia walivyosema: ‘Hakika wafalme wanapouingia mji wanauharibu na wanawafanya wale watukufu wake kuwa wanyonge.’ Kwa hiyo Suleiman akasisitiza kauli ya malkia kwa kusema: ‘Tutawatoa humo na hali wao wamekuwa madhalili na wanyonge.’

Akasema: Enyi wakuu wa baraza! Ni nani kati yenu atakayeniletea kiti chake cha enzi kabla hawajanijia nao wamekwishasalimu amri.

Msafara uliporeja kutoka kwa Suleiman na wakampa habari Malkia kwa waliyoyaona na kuyasikia, aliona hapana budi isipokuwa kusikiliza na kutii. Akaelekea kwa Suleiman pamoja na wapambe wake. Akakiacha kiti cha enzi kikilindwa na askari.

Suleiman alipojua kufika Bilqis alipendelea kumuonyesha miujiza ya kufahamisha utume wake na ukuu wake; na kwamba muujiza huo uwe ni kukichukua kiti chake ambacho ndicho kinachoonyesha enzi yake na umalkia wake. Ndipo akauliza wale waliokuwapo mbele yake, ni nani atakayeniletea?

Akasema afriti katika majini: Mimi nitakuletea kabla hujainuka mahala pako. Na mimi hakika nina nguvu, mwaminifu.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) alimtiishia Suleiman upepo ukienda kwa amri yake. Bila shaka huu ni mujiza. Akamtiisha ndege wakifuata amri yake.

Nao pia ni muujiza. Vile vile Mwenyezi Mungu alimuhusisha na baadhi ya askari binadamu na majini, wakifanya maajabu kulingana na wakati wo. Walikuwa wakiandamana na jeshi la Suleiman, wakisaidiana kumshinda adui; kama wafanyavyo wataalamu wa kiufundi hivi sasa.

Hilo linaashiriwa na matakwa ya Suleiman kwao kuwaletea kiti cha enzi cha Bilqis katika muda mchache na hali anajua kuwa kiko masafa ya mbali sana. Mmoja wa majini akamwambia nitakuletea kikiwa salama, kama kilivyo ukiwa wewe umekaa hapa.

Lakini akasema mwenye elimu ya Kitabu: Mimi nitakuletea kabla ya kupepesa jicho lako.

Ikawa ushindi ni wa huyu ambapo, kwa uweza wa elimu alio nao, aliweza kukileta kiti wakati uliotakiwa.

Haya ndiyo yaliyofahamishwa na dhahiri ya Aya. Ama maswali ya kuwa ni nani huyo aliyekuwa na elimu ya kitabu? Je, alikuwa ni Malaika, Khidhr au mja mwema katika binadamu aliyeitwa Asif bin Barkhiya Na kwamba je yeye alikuwa akijua jina kuu la Mwenyezi Mungu au ni elimu gani hiyo aliyoitumia?

Maswali yote haya na mengineyo mengi, jibu lake liko kwa Mola wangu. Kwa sababu Aya haikuweka wazi hilo, wala hakuna Hadith sahih iliyothibiti.

Uwezekano wa karibu, tunaoweza kusema ni kuwa yeye hakuwa katika majini, kwa sababu alimzidi jini Afrit, kama ilivyoweka wazi Aya, kwamba yeye alikileta kiti kabla ya kupepesa jicho. Miujiza inayodhihiri kwa mitume, pia inadhihiri kwa wale ambao wamechaguliwa na mitume kwa idhini ya Mwenyezi Mungu.

La muhimu kujua, katika tukio hili, ni kwamba Bilqis aliyekuwa na madaraka makubwa na neema, alimnyenyekea Suleiman.

Basi alipokiona kimewekwa mbele yake, alisema: Haya ni katika fadhila za Mola wangu, ili anijaribu, nitashukuru au nitakufuru.

Makusudio ya kukufuru hapa ni kukufuru neema, sio kumkufuru Mwenyezi Mungu. Suleiman hawezi kuzikufuru neema za Mola wake, kwa sababu yeye ni maasum. Alisema haya kama utangulizi wa kusema:

Na mwenye kushukuru kwa hakika anashukuru kwa manufaa ya nafsi yake na mwenye kukufuru kwa hakika Mola wangu ni Mkwasi, Mkarimu.

Katika maana ya Aya hii ni ile isemayo:

إِنْ أَحْسَنتُمْ أَحْسَنتُمْ لِأَنفُسِكُمْ وَإِنْ أَسَأْتُمْ فَلَهَا ﴿٧﴾

“Mkifanya uzuri mnajifanyia wenyewe na mkifanya ubaya mnajifanyia wenyewe.” Juz. 15 (17:7).

5

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TISA

فَجُمِعَ السَّحَرَةُ لِمِيقَاتِ يَوْمٍ مَّعْلُومٍ ﴿٣٨﴾

38. Basi wakakusanywa wachawi wakati wa siku maalum.

وَقِيلَ لِلنَّاسِ هَلْ أَنتُم مُّجْتَمِعُونَ ﴿٣٩﴾

39. Na watu wakaambiwa: Je, mtakusanyika?

لَعَلَّنَا نَتَّبِعُ السَّحَرَةَ إِن كَانُوا هُمُ الْغَالِبِينَ ﴿٤٠﴾

40. Huenda tutawafuata wachawi wakiwa wao ndio watakaoshinda.

فَلَمَّا جَاءَ السَّحَرَةُ قَالُوا لِفِرْعَوْنَ أَئِنَّ لَنَا لَأَجْرًا إِن كُنَّا نَحْنُ الْغَالِبِينَ ﴿٤١﴾

41. Basi walipokuja wachawi wakamwambia Firauni: Je, tutapata ujira ikiwa tutashinda?

قَالَ نَعَمْ وَإِنَّكُمْ إِذًا لَّمِنَ الْمُقَرَّبِينَ ﴿٤٢﴾

42. Akasema: Ndio, hapo nanyi hakika mtakuwa miongoni mwa wanaokurubishwa.

قَالَ لَهُم مُّوسَىٰ أَلْقُوا مَا أَنتُم مُّلْقُونَ ﴿٤٣﴾

43. Musa akawaambia: Tupeni mnavyotaka kutupa.

فَأَلْقَوْا حِبَالَهُمْ وَعِصِيَّهُمْ وَقَالُوا بِعِزَّةِ فِرْعَوْنَ إِنَّا لَنَحْنُ الْغَالِبُونَ ﴿٤٤﴾

44. Wakatupa kamba zao na fimbo zao na wakasema: Kwa nguvu za Firauni hakika sisi bila shaka ni wenye kushinda.

فَأَلْقَىٰ مُوسَىٰ عَصَاهُ فَإِذَا هِيَ تَلْقَفُ مَا يَأْفِكُونَ ﴿٤٥﴾

45. Musa akatupa fimbo yake, mara ikavimeza walivyovibuni.

فَأُلْقِيَ السَّحَرَةُ سَاجِدِينَ ﴿٤٦﴾

46. Wachawi wakapomoka kusujudu.

قَالُوا آمَنَّا بِرَبِّ الْعَالَمِينَ ﴿٤٧﴾

47. Wakasema: Tumemwamini Mola wa Walimwengu.

رَبِّ مُوسَىٰ وَهَارُونَ ﴿٤٨﴾

48. Mola wa Musa na Harun.

قَالَ آمَنتُمْ لَهُ قَبْلَ أَنْ آذَنَ لَكُمْ إِنَّهُ لَكَبِيرُكُمُ الَّذِي عَلَّمَكُمُ السِّحْرَ فَلَسَوْفَ تَعْلَمُونَ لَأُقَطِّعَنَّ أَيْدِيَكُمْ وَأَرْجُلَكُم مِّنْ خِلَافٍ وَلَأُصَلِّبَنَّكُمْ أَجْمَعِينَ ﴿٤٩﴾

49. Akasema Firauni: Je, mmemwamini kabla sijawaruhusu. Hakika yeye ndiye mkubwa wenu aliyewafundisha uchawi, lakini punde mtajua. Nitawakata mikono yenu na miguu yenu kwa kubadilisha, kisha nitawasulubu nyote.

قَالُوا لَا ضَيْرَ إِنَّا إِلَىٰ رَبِّنَا مُنقَلِبُونَ ﴿٥٠﴾

50. Wakasema: Haidhuru, hakika sisi ni wenye kurejea kwa Mola wetu.

إِنَّا نَطْمَعُ أَن يَغْفِرَ لَنَا رَبُّنَا خَطَايَانَا أَن كُنَّا أَوَّلَ الْمُؤْمِنِينَ ﴿٥١﴾

51. Hakika sisi tunatumai Mola wetu atughufirie makosa yetu kwa kuwa ndio wa kwanza kuamini.

WALIFIKA WACHAWI

Aya 38 – 51

MAANA

Basi wakakusanywa wachawi wakati wa siku maalum.

Siku yenyewe ni sikukuu; kama alivyosema Mwenyezi Mungu:

قَالَ مَوْعِدُكُمْ يَوْمُ الزِّينَةِ وَأَن يُحْشَرَ النَّاسُ ضُحًى ﴿٥٩﴾

“Akasema: Miadi yenu ni siku ya sikukuu na watu wakusanywe kabla ya adhuhuri.” Juz. 16 (20:59).

Na watu wakaambiwa: Je, mtakusanyika ili mshuhudie mapambano haya? Watu hawahitaji kuhimizwa kwenye mambo haya; hao wenyewe watashindana kufika. Na hili ndilo alilolitaka Musa, ili haki idhihirike na batili ibatilike machoni mwa watu.

Huenda tutawafuata wachawi wakiwa wao ndio watakaoshinda.

Waliosema haya kwa watu ni Firauni na wakuu wake. Dhahiri ya kauli yao hii inaashiria kuwa wana shaka na dini ya wachawi na kwamba wao wanitafuta haki ili waifuate, lakini haya sio makusudio yao. Kwa sababu wao na wachawi wako kwenye dini moja. Makusudio yao ni kuwa huenda tutabaki kwenye uthabiti wa dini yetu wala hatutamfuta Musa.

Basi walipokuja wachawi wakamwambia Firauni: Je, tutapata ujira ikiwa tutashinda? Akasema: Ndio, hapo nanyi hakika mtakuwa miongoni mwa wanaokurubishwa. Musa akawaambia: Tupeni mnavyotaka kutupa. Wakatupa kamba zao na fimbo zao na wakasema:

“Kwa nguvu za Firauni hakika sisi bila shaka ni wenye kushinda. Musa akatupa fimbo yake, mara ikavimeza walivyovibuni. Wachawi wakapomoka kusujudu.Wakasema: Tumemwamini Mola wa Walimwengu. Mola wa Musa na Harun.

Akasema Firauni: Je, mmemwamini kabla sijawaruhusu. Hakika yeye ndiye mkubwa wenu aliyewafundisha uchawi, lakini punde mtajua. Nitawakata mikono yenu na miguu yenu kwa kubadilisha, kisha nitawasulubu nyote. Wakasema: Haidhuru, hakika sisi ni wenye kurejea kwa Mola wetu. Hakika sisi tunatumai Mola wetu atughufirie makosa yetu kwa kuwa ndio wa kwanza kuamini.

Aya hizi zote zimetajwa katika Juz. 9 (7: 113 – 126); wala hakuna tofauti baina ya hapa na huko, isipokuwa katika baadhi ya ibara tu; kwa mfano kule imesemwa: ‘wakaja wachawi’ na hapa ikasemwa; ‘walipokuja wachawi,’ n.k.

وَأَوْحَيْنَا إِلَىٰ مُوسَىٰ أَنْ أَسْرِ بِعِبَادِي إِنَّكُم مُّتَّبَعُونَ ﴿٥٢﴾

52. Na tulimpelekea wahyi Musa kwamba nenda na waja wangu wakati wa usiku, kwa hakika mtafuatwa.

فَأَرْسَلَ فِرْعَوْنُ فِي الْمَدَائِنِ حَاشِرِينَ ﴿٥٣﴾

53. Basi Firauni akawatuma mjini wakusanyao.

إِنَّ هَـٰؤُلَاءِ لَشِرْذِمَةٌ قَلِيلُونَ ﴿٥٤﴾

54. Hakika hawa ni kikundi kidogo.

وَإِنَّهُمْ لَنَا لَغَائِظُونَ ﴿٥٥﴾

55. Nao wanatuudhi.

وَإِنَّا لَجَمِيعٌ حَاذِرُونَ ﴿٥٦﴾

56. Na sisi ni wengi wenye kuchukua hadhari.

فَأَخْرَجْنَاهُم مِّن جَنَّاتٍ وَعُيُونٍ ﴿٥٧﴾

58. Basi tukawatoa katika mabustani na chemchem.

وَكُنُوزٍ وَمَقَامٍ كَرِيمٍ ﴿٥٨﴾

58. Na mahazina na vyeo vya heshima.

كَذَٰلِكَ وَأَوْرَثْنَاهَا بَنِي إِسْرَائِيلَ ﴿٥٩﴾

59. Hivyo ndivyo! Na tukawarithisha wana wa Israil.

فَأَتْبَعُوهُم مُّشْرِقِينَ ﴿٦٠﴾

60. Kisha wakawafuata walipotokewa na jua.

فَلَمَّا تَرَاءَى الْجَمْعَانِ قَالَ أَصْحَابُ مُوسَىٰ إِنَّا لَمُدْرَكُونَ ﴿٦١﴾

61. Yalipoonana makundi mawili, watu wa Musa wakasema: Hakika tumepatikana.

قَالَ كَلَّا إِنَّ مَعِيَ رَبِّي سَيَهْدِينِ ﴿٦٢﴾

62. Akasema: Hapana! Hakika Mola wangu yuko pamoja nami, ataniongoza.

فَأَوْحَيْنَا إِلَىٰ مُوسَىٰ أَنِ اضْرِب بِّعَصَاكَ الْبَحْرَ فَانفَلَقَ فَكَانَ كُلُّ فِرْقٍ كَالطَّوْدِ الْعَظِيمِ ﴿٦٣﴾

63. Tulimpelekea wahyi Musa tukamwambia: Piga bahari kwa fimbo yako. Basi ikatengana na kila sehemu ikawa kama milima mkubwa.

وَأَزْلَفْنَا ثَمَّ الْآخَرِينَ ﴿٦٤﴾

64. Na tukawajongeza hapo wale wengine.

وَأَنجَيْنَا مُوسَىٰ وَمَن مَّعَهُ أَجْمَعِينَ ﴿٦٥﴾

65. Na tukamwokoa Musa na waliokuwa pamoja naye wote.

ثُمَّ أَغْرَقْنَا الْآخَرِينَ ﴿٦٦﴾

66. Kisha tukawazamisha hao wengine.

إِنَّ فِي ذَٰلِكَ لَآيَةً وَمَا كَانَ أَكْثَرُهُم مُّؤْمِنِينَ ﴿٦٧﴾

67. Hakika bila shaka katika hayo ipo ishara lakini wengi wao si wenye kuamini.

وَإِنَّ رَبَّكَ لَهُوَ الْعَزِيزُ الرَّحِيمُ ﴿٦٨﴾

68. Na hakika Mola wako ndiye Mwenye nguvu, Mwenye kurehemu.

KUGHARIKI FAIRAUNI NA WATU WAKE

Aya 52 – 68

MAANA

Na tulimpelekea wahyi Musa kwamba nenda na waja wangu wakati wa usiku, kwa hakika mtafuatwa.

Mwenyezi Mungu alimwamrisha Musa atoke na wana wa Israil kutoka ardhi ya Misri usiku na akampa habari kwamba Firauni atawafuata ili awarudishe.

Basi Firauni akawatuma mjini wakusanyao.

Firauni alipojua kuwa Musa na watu wake wametoka aliwakusanyia watu ili awarudishe kwenye utawala wake na awape adhabu ya utoro.

Akasema: Hakika hawa ni kikundi kidogo nao wanatuudhi na sisi ni wengi wenye kuchukua hadhari.

Ni nani huyo Musa na watu wake. Wao si chochote kwetu; wanajaribu kutukasirisha na kutufanyia jeuri, na sisi tunawachunga. Basi watapata adhabu ya matendo yao. Lakini juu ya mipango ya Firauni kuna mipango ya Mwenyezi Mungu. Imam(a.s) anasema:Mambo yanakuwa kwa makadirio ili maangamizi yawe kwa mpangilio.

Basi tukawatoa katika mabustani na chemchem na mahazina na vyeo vya heshima.

Firauni na jeshi lake alitoka ili amwadhibu Musa na watu wake, lakini Mungu akawaadhibu wao na akawatoa katika yale waliyokuwa wakiyamilikii na kustarehe nayo; yakiwemo makasri ya ghorofa, mito inayotiririka, miti iliyojaa matunda kochokocho, mahazina yaliyojificha, mabembea, mabwawa ya kuogelea na sehemu za kupunga upepo. Yote haya na mengineyo waliyaacha bila ya kurudi.

Hivyo ndivyo! Na tukawarithisha wana wa Israil.

Tabari anasema: “Mwenyezi Mungu (s.w.t) aliwarithisha wana wa Israil majumba ya Firauni na watu wake.” Abu Hayyani Al-Andalusi naye amesema katika kitabu Al-bahrul-Muhit: “Haya ndio maana ya dhahiri, kwa sababu Aya ya kurithishwa wana wa Israil, imekuja moja kwa moja baada ya Aya ya kuwatoa.”

Wengine wamesema kuwa Mwenyezi Mungu aliwarithisha wana wa Israil mfano wa alivyokuwa Firauni na watu wake. Kwa sababu Waisrail hawakurudi Misri baada ya kuitoka.

Vyovyote iwavyo Aya inaeleza kuwa Mwenyezi Mungu hawaachi madhal- imu na dhulma yao na kwamba yeye anawaadhibu mikononi mwa wenye ikhlasi au kwa sababu yoyote. Haya ndiyo tunayoyaamini na kuyakubali. Ama uchunguzi wa historia na mfano wake tunawaachia wataalamu wake, ila ikiwa tuna yakini nayo.

Kisha wakawafuata walipotokewa na jua.

Firauni alitoka na jeshi lake la wapanda farasi na wendao kwa miguu kumtafuta Musa na watu wake wakawapata lilipochomoza jua.

Yalipoonana makundi mawili, kundi la Musa na la Firauni, watu wa Musa wakasema : Hakika tumepatikana.

Walisema hivyo kwa hofu na fazaa, kuwa adui amekwishatufikia hatuna la kufanya.

Akasema: Hapana! Hakika Mola wangu yuko pamoja nami, ataniongoza. Tulimpelekea wahyi Musa tukamwambia: Piga bahari kwa fimbo yako. Basi ikatengana na kila sehemu ikawa kama milima mkubwa.

Musa aliwaambia watu wake kuwa msimuogope Firauni na nguvu zake. Hakika Mwenyezi Mungu ana nguvu zaidi na yuko pamoja nami, nanyi mtaona.

Hakumaliza maneno yake, mara Mwenyezi Mungu akamwamrisha kupiga bahari kwa fimbo yake. Alipoipiga ikapasuka njia kumi na mbili kulingana na koo za waisrail. Maji yakainuka baina ya njia moja na nyingine kama mlima. Musa na watu wake wakavuka hadi ng’ambo ya pili.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 16 (20:77).

Na tukawajongeza hapo wale wengine. Na tukamwokoa Musa na waliokuwa pamoja naye wote. Kisha tukawazamisha hao wengine.

Makusudio ya wengine ni kundi la Firauni. Maana ni kuwa baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kuwavusha wana wa Israil upande wa pili na wakawa wameokoka, kundi la Firauni nalo liliwasili. Wakaona muuujiza mkubwa – maji ya bahari yamesimama kama jabali na kutengeneza njia. Firauni akawaambia watu wake: Tazameni bahari ilivyoitikia matakwa yangu na kunifungulia njia ya kuwafuata walionitoroka.

Kisha wakajitoma na wakaenda kwa amani na utulivu. Hawakufika katikati, bahari ikawafunika wote, baada ya kuhadharishwa na kupewa muda mrefu, lakini walizama kwenye upotevu wao.

Hakika bila shaka katika hayo ipo ishara ya muujiza, mazingatio na mawaidha, lakini wengi wao si wenye kuamini. Na hakika Mola wako ndiye Mwenye nguvu, Mwenye kurehemu.

Wengi wao hapa wanakusudiwa wana wa Israil waliookolewa na Mwenyezi Mungu mikononi mwa Firauni, kwa kuchukilia dhahiri ya mfumo wa maneno ulivyo.

Na wala sio walioangamia, kama wasemavyo baadhi ya wafasiri. Dalili ya kuwa makusudio ni wana wa Israil ni kuwa wafuasi wa Firauni wote wlikuwa makafiri, bila ya kubaki; hasa wale aliokuwa nao. Na wana wa Israili, walipookolewa na Mungu kutoka kwa Firauni, walimwambia Musa: Tunataka sanamu tuliabudu badala ya Mwenyezi Mungu:

وَجَاوَزْنَا بِبَنِي إِسْرَائِيلَ الْبَحْرَ فَأَتَوْا عَلَىٰ قَوْمٍ يَعْكُفُونَ عَلَىٰ أَصْنَامٍ لَّهُمْ قَالُوا يَا مُوسَى اجْعَل لَّنَا إِلَـٰهًا كَمَا لَهُمْ آلِهَةٌ ﴿١٣٨﴾

“Na tukawavusha bahari wana wa Israil na wakawafikia waliokuwa wakiyaabudu masanamu yao; wakasema: Ewe Musa! Hebu nasi tufanyie waungu kama hawa walivyo na waungu.” Juz. 9 (7:138).

Kwa hiyo maana yanakuwa kwamba Waisraili walishuhudia muujiza wa kupasuka bahari na miujiza mingineyo, lakini bado waliendelea kung’ang’ania ukafiri wao na jeuri yao.

وَاتْلُ عَلَيْهِمْ نَبَأَ إِبْرَاهِيمَ ﴿٦٩﴾

69. Na wasomee habari za Ibrahim.

إِذْ قَالَ لِأَبِيهِ وَقَوْمِهِ مَا تَعْبُدُونَ ﴿٧٠﴾

70. Alipomwambia baba yake na kaumu yake: Mnaabudu nini?

قَالُوا نَعْبُدُ أَصْنَامًا فَنَظَلُّ لَهَا عَاكِفِينَ ﴿٧١﴾

71. Wakasema: Tunaabudu masanamu nasi tutaendelea kuyanyenyekea.

قَالَ هَلْ يَسْمَعُونَكُمْ إِذْ تَدْعُونَ ﴿٧٢﴾

72. Akasema: Je yanawasikia mnapoyaita?

أَوْ يَنفَعُونَكُمْ أَوْ يَضُرُّونَ ﴿٧٣﴾

73. Au yanawafaa au yanawadhuru?

قَالُوا بَلْ وَجَدْنَا آبَاءَنَا كَذَٰلِكَ يَفْعَلُونَ ﴿٧٤﴾

Wakasema: Bali tumewakuta mababa zetu wakifanya hivyo hivyo.

قَالَ أَفَرَأَيْتُم مَّا كُنتُمْ تَعْبُدُونَ ﴿٧٥﴾

75. Akasema: Je, mmewaona mnaowaabudu?

أَنتُمْ وَآبَاؤُكُمُ الْأَقْدَمُونَ ﴿٧٦﴾

76. Nyinyi na baba zenu wa zamani?

فَإِنَّهُمْ عَدُوٌّ لِّي إِلَّا رَبَّ الْعَالَمِينَ ﴿٧٧﴾

77. Hakika hao ni maadui zangu isipokuwa Mola wa walimwengu wote.

الَّذِي خَلَقَنِي فَهُوَ يَهْدِينِ ﴿٧٨﴾

78. Ambaye ameniumba naye ananiongoza.

وَالَّذِي هُوَ يُطْعِمُنِي وَيَسْقِينِ ﴿٧٩﴾

79. Na ambaye ananilisha na kuninywesha.

وَإِذَا مَرِضْتُ فَهُوَ يَشْفِينِ ﴿٨٠﴾

80. Na ninapougua basi yeye ananiponya.

وَالَّذِي يُمِيتُنِي ثُمَّ يُحْيِينِ ﴿٨١﴾

81. Na ambaye atanifisha kisha atanihuisha.

وَالَّذِي أَطْمَعُ أَن يَغْفِرَ لِي خَطِيئَتِي يَوْمَ الدِّينِ ﴿٨٢﴾

82. Na ambaye ndiye ninayemtumai kunighufuria makosa yangu siku ya malipo.

رَبِّ هَبْ لِي حُكْمًا وَأَلْحِقْنِي بِالصَّالِحِينَ ﴿٨٣﴾

83. Mola wangu! Nitunukie hukumu na uniunganishe na wema.

وَاجْعَل لِّي لِسَانَ صِدْقٍ فِي الْآخِرِينَ ﴿٨٤﴾

84. Na unijaalie kutajwa kwa wema na wengine.

وَاجْعَلْنِي مِن وَرَثَةِ جَنَّةِ النَّعِيمِ ﴿٨٥﴾

85. Na unijaalie katika warithi wa Bustani za neema.

وَاغْفِرْ لِأَبِي إِنَّهُ كَانَ مِنَ الضَّالِّينَ ﴿٨٦﴾

86. Na umghufirie baba yangu, kwani alikuwa miongoni mwa wapotevu.

وَلَا تُخْزِنِي يَوْمَ يُبْعَثُونَ ﴿٨٧﴾

87. Wala usinihizi siku watakapofufuliwa.

يَوْمَ لَا يَنفَعُ مَالٌ وَلَا بَنُونَ ﴿٨٨﴾

88. Siku ambayo haitafaa mali wala wana.

إِلَّا مَنْ أَتَى اللَّـهَ بِقَلْبٍ سَلِيمٍ ﴿٨٩﴾

89. Isipokuwa mwenye kuja kwa Mwenyezi Mungu na moyo uliosalimika.

IBRAHIM

Aya 69 – 89

MAANA

Mwenyezi Mungu (s.w.t) amekitaja kisa cha Ibrahim kwa kukigawa kulingana na mnasaba ulivyo.

Katika Aya hizi Mwenyezi Mungu (s.w.t) amerudia majibizano baina ya Ibrahim na watu wake, kwa mfumo mwingine unaotofautiana na ule ulio katika Juz. 17 (21:51).

Na wasomee habari za Ibrahim.

Maneno yanaelekezwa kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) kuwa awasomee makuraishi ambao wanadai kuwa ni kizazi cha Ibrahim na wako kwenye dini yake.

Alipomwambia baba yake na kaumu yake: Mnaabudu nini?

Katika Juz.7 (6:74) tumetaja tofauti za wafasiri kuhusu baba aliyeambiwa maneno haya na Ibrahim, kuwa je, ni baba yake hasa au ni baba wa kimajazi au ni ami yake?

Wakasema: Tunaabudu masanamu nasi tutaendelea kuyanyenyekea.

Tutadumu kuyaabudu na kuyatukuza. Kukubali kwao kuabudu masanamu kunajulisha kuwa neno sanamu halikuwa linamaanisha shutuma katika ufahamu wao, kama tunavyofahamu sisi; bali neno hilo lilikuwa likimaanisha utukufu na ukuu.

Akasema: Je yanawasikia mnapoyaita? Au yanawafaa au yanawadhuru?

Ni kawaida anayeabudiwa asikie, aone, adhuru na kunufaisha. Je, haya mnayoyaabudu yana sifa hizi? Swali hapa ni la kupinga.

Wakasema: Bali tumewakuta mababa zetu wakifanya hivyo hivyo.

Hii ni kukubali kuwa wao ni waigaji. Wala hilo si ajabu. Katika karne ya ishirini, zama za kutembea angani, tumeona wafuasi wakiwaiga viongozi wao na wakitoa dalili kwa kauli zao na kuzichukulia kuwa ni msingi, bila ya kuhakisha na kuchunguza.

Akasema: Je, mmewaona mnaowaabudu nyinyi na baba zenu wa zamani? Hakika hao ni maadui zangu isipokuwa Mola wa walimwengu wote.

Ikiwa nyinyi mnawaiga baba zenu, basi mimi simwigi yeyote na ninatangaza kujitenga kwangu na uadui wangu kwa hao waungu wenu; wala siabudu isipokuwa Mola wa walimwengu wote. Yeye ndiye walii wangu duniani na akhera. Yakiwa masanamu ni miungu, kama mnavyodai, basi na waniteremshie hasira zao, mimi napingana nao.

Ambaye ameniumba naye ananiongoza.

Mwenyezi Mungu amenipa akili nami naitumia kuniongoza kwenye haki. Ninaifuata na ninaitumia vizuri; wala simuigi yoyote; kama mnavyodai.

Na ambaye ananilisha na kuninywesha.

Kwa kuzifanya nyepesi sababu kwangu mimi na kwa viumbe vyake vyote.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) ameiumba ardhi hii na akaweka kila wanayoyahitajia na akasema: Yeye ndiye aliyeidhalisha ardhi kwa ajili yenu, basi tembeeni katika pande zake na kuleni katika riziki zake. Na kwake yeye ndio kufufuliwa.

Na ninapougua basi yeye ananiponya kutokana na madawa aliyoyaumba.

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) anasema, “Hakika kila ugonjwa una dawa, dawa ikifika kwenye ugonjwa hupona kwa idhini ya Mwenyezi Mungu.” Kuna Hadithi nyingine isemayo: Hakika Mwenyezi Mungu ameteremsha ugonjwa na dawa, basi fanyeni dawa wala msifanye dawa kwa haramu.

Na ambaye atanifisha kisha atanihuisha na ambaye ndiye ninayemtumai kunighufuria makosa yangu siku ya malipo.

Uhai, mauti na maghufira yako mikononi mwa Mwenyezi Mungu, hilo halina shaka. Na Ibrahim(a.s) ni mwenye kuhifadhiwa na makosa na hatia (maasumu). Katika isma ya kila maasumu ni kuikuza hofu yake kwa Mwenyezi Mungu.

Mola wangu! Nitunukie hukumu.

Makusudio ya hukumu hapa, sio utawala bali ni hekima na kukata hukumu:

وَآتَيْنَاهُ الْحِكْمَةَ وَفَصْلَ الْخِطَابِ ﴿٢٠﴾

“Na tukampa hekima na kukata hukumu.” (38:20).

Na uniunganishe na wema.

Unipe tawfiki ya kufuata nyao zao na kutenda matendo yao.

Na unijaalie kutajwa kwa wema na wengine.

Makusudio ya wengine ni umma utakaokuja baadaye. Maana ni nijaalie kutajwa kwa wema baina ya watu baada yangu. Mwenyezi Mungu aliitikia dua yake; ambapo dini zote za mbinguni zimeafikiana kumtukuza na kumwadhimisha Nabii Ibrahim(a.s) .

Na unijaalie katika warithi wa Bustani za neema.

Ni nani anayestahiki hizo zaidi kuliko Ibrahim.

Na umghufirie baba yangu, kwani alikuwa miongoni mwa wapotevu.

Angalia tafsiri ya “Na haikuwa Ibrahim kumtakia msamaha baba yake ila ni kwa sababu ya ahadi aliyofanya naye, lakini ilipopambanukia kuwa yeye ni adui wa Mwenyezi Mungu, alijiepusha naye.” Juz. 11 (9:114).

Wala usinihizi siku watakapofufuliwa.

Dua hii ni katika aina ya dua za mitume na viongozi wema.Siku ambayo haitafaa mali wala wana. Isipokuwa mwenye kuja kwa Mwenyezi Mungu na moyo uliosalimika.

Kutokana na maafa ya ukafiri, unafiki, mifundo, ria na maafa mengineyo na maradhi.

Moyo ukiwa salama na uchafu, basi viungo vyote huwa salama: ulimi utasalimika na uwongo, kusengenya, kusikiliza upuzi na ubatilifu. Vile vile mkono unasalimika na kufanya haramu na tupu kutokana na zina na uovu.

6

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA KUMI NA TISA

وَأُزْلِفَتِ الْجَنَّةُ لِلْمُتَّقِينَ ﴿٩٠﴾

90. Na Bustani (Pepo) itasogezwa kwa wenye takua.

وَبُرِّزَتِ الْجَحِيمُ لِلْغَاوِينَ ﴿٩١﴾

91. Na Jahannam itadhihirishwa kwa wapotofu.

وَقِيلَ لَهُمْ أَيْنَ مَا كُنتُمْ تَعْبُدُونَ ﴿٩٢﴾

92. Na wataambiwa, wako wapi mliokuwa mkiwaabudu.

مِن دُونِ اللَّـهِ هَلْ يَنصُرُونَكُمْ أَوْ يَنتَصِرُونَ ﴿٩٣﴾

93. Badala ya Mwenyezi Mungu? Je, watawasaidia au kujisaidia wenyewe?

فَكُبْكِبُوا فِيهَا هُمْ وَالْغَاوُونَ ﴿٩٤﴾

94. Basi watavurumizwa humo wao na wapotofu.

وَجُنُودُ إِبْلِيسَ أَجْمَعُونَ ﴿٩٥﴾

95. Na majeshi ya Ibilisi yote.

قَالُوا وَهُمْ فِيهَا يَخْتَصِمُونَ ﴿٩٦﴾

96. Watasema na hali ya kuwa wanazozana humo:

تَاللَّـهِ إِن كُنَّا لَفِي ضَلَالٍ مُّبِينٍ ﴿٩٧﴾

97. Wallah! Hakika tulikuwa katika upotevu ulio wazi.

إِذْ نُسَوِّيكُم بِرَبِّ الْعَالَمِينَ ﴿٩٨﴾

98. Tulipowafanya sawa na Mola wa walimwengu wote.

وَمَا أَضَلَّنَا إِلَّا الْمُجْرِمُونَ ﴿٩٩﴾

99. Na hawakutupoteza ila wakosefu.

فَمَا لَنَا مِن شَافِعِينَ ﴿١٠٠﴾

100. Basi hatuna waombezi.

وَلَا صَدِيقٍ حَمِيمٍ ﴿١٠١﴾

101. Wala rafiki wa dhati.

فَلَوْ أَنَّ لَنَا كَرَّةً فَنَكُونَ مِنَ الْمُؤْمِنِينَ ﴿١٠٢﴾

102. Laiti tungepata kurejea tena tungelikuwa katika waumi- ni.

إِنَّ فِي ذَٰلِكَ لَآيَةً وَمَا كَانَ أَكْثَرُهُم مُّؤْمِنِينَ ﴿١٠٣﴾

103. Hakika bila shaka katika hayo ipo ishara, lakini wengi wao si wenye kuamini.

وَإِنَّ رَبَّكَ لَهُوَ الْعَزِيزُ الرَّحِيمُ ﴿١٠٤﴾

104. Na hakika Mola wako ndiye mwenye nguvu mwenye kurehemu.

PEPO KWA WENYE TAKUA NA MOTO KWA WAPOTEVU

Aya 90 – 104

MAANA

Na Bustani (Pepo) itasogezwa kwa wenye takua

Bila shaka iko karibu na mwenye kuongoka na akamcha Mungu na iko mbali na mwenye kupotea.

Na Jahannam itadhihirishwa kwa wapotofu.

Ataidhihirisha Mwenyezi Mungu kwa wale walioikana na kuikadhibisha.

Na wataambiwa wako wapi mliokuwa mkiwaabudu badala ya Mwenyezi Mungu? Na mkiwatarajia kwa siku hii, huku mkisema kuwa mliwabudu ili wawakurubishe kwa Mwenyezi Mungu?

Je, watawasaidia au kujisaidia wenyewe?

Hakika wao hawawezi kuwasaidia wala kujisaidia wenyewe.

Basi watavurumizwa humo wao na wapotofu na majeshi ya Ibilisi yote.

Wao ni hao waungu wao na wapotofu ni wale walioabudu. Mwanajeshi wa Ibilisi ni kila mpotofu na mpotoshaji. Mwenyezi Mungu atawachanganya wote kisha awatupe kwenye shimo la Jahannam.

Watasema na hali ya kuwa wanazozana humo: Wallah! Hakika tulikuwa katika upotevu ulio wazi, tulipowafanya sawa na Mola wa walimwengu wote. Na hawakutupoteza ila wakosefu.

Wapotofu kesho watasema, baada ya kupitwa na wakati, kuwaambia waungu wao na mashetani wao, kwamba nyinyi ndio mliokuwa viongozi wetu wa upofu na upotevu, wakati tulipowaabudu na kuwafanya mko sawa na Mwenyezi Mungu. Na wakosefu ndio waliokuwa kikwazo, ambao ni viongozi wa manufaa na masilahi, asili ya ufisadi na balaa.

Basi hatuna waombezi wala rafiki wa dhati.

Kesho hakuna uombezi wala ugombezi. Hakuna kitakachomfaa mtu isipokuwa moyo ulio salama na amali njema. Na muovu ni yule asiyekuwa na mawili hayo.

Laiti tungepata kurejea tena tungelikuwa katika waumini.

Baada ya kukata tamaaa na kila kitu ndio wanatamani kurudi duniani ili waamiini na kutenda. Mwenyezi Mungu anasema:

وَلَوْ رُدُّوا لَعَادُوا لِمَا نُهُوا عَنْهُ وَإِنَّهُمْ لَكَاذِبُونَ ﴿٢٨﴾

“Na kama wangelirudishwa, bila shaka wangeyarudia yale waliyokatazwa na hakika wao ni waongo.” Juz. 7 (6:28)

Hakika bila shaka katika hayo ipo ishara, lakini wengi wao si wenye kuamini. Na hakika Mola wako ndiye Mwenye nguvu, Mwenye kurehemu.

Imetangulia kwa herufi zake, katika Aya 67 na 68 ya sura hii.

كَذَّبَتْ قَوْمُ نُوحٍ الْمُرْسَلِينَ ﴿١٠٥﴾

105. Kaumu ya Nuh waliwakadhibisha mitume.

قَالَ لَهُمْ أَخُوهُمْ نُوحٌ أَلَا تَتَّقُونَ ﴿١٠٦﴾

106. Alipowaambia ndugu yao Nuh: Je, hamna takua?

إِنِّي لَكُمْ رَسُولٌ أَمِينٌ ﴿١٠٧﴾

107. Hakika mimi kwenu ni Mtume mwaminifu.

فَاتَّقُوا اللَّـهَ وَأَطِيعُونِ ﴿١٠٨﴾

108. Basi mcheni Mwenyezi Mungu na mnitii.

وَمَا أَسْأَلُكُمْ عَلَيْهِ مِنْ أَجْرٍ إِنْ أَجْرِيَ إِلَّا عَلَىٰ رَبِّ الْعَالَمِينَ ﴿١٠٩﴾

109. Na siwataki ujira juu yake, kwani ujira wangu hauko ila kwa Mola wa walimwengu wote.

فَاتَّقُوا اللَّـهَ وَأَطِيعُونِ ﴿١١٠﴾

110. Basi mcheni Mwenyezi Mungu na mnitii.

قَالُوا أَنُؤْمِنُ لَكَ وَاتَّبَعَكَ الْأَرْذَلُونَ ﴿١١١﴾

111. Wakasema: Je, tukuamini na hali wanaokufuata ni walio duni?

قَالَ وَمَا عِلْمِي بِمَا كَانُوا يَعْمَلُونَ ﴿١١٢﴾

112. Akasema: Nayajuaje waliyokuwa wakiyafanya?

إِنْ حِسَابُهُمْ إِلَّا عَلَىٰ رَبِّي لَوْ تَشْعُرُونَ ﴿١١٣﴾

113. Hisabu yao haiko ila kwa Mola wangu. Lau mngelitambua.

وَمَا أَنَا بِطَارِدِ الْمُؤْمِنِينَ ﴿١١٤﴾

114. Wala mimi si mwenye kuwafukuza waumini.

إِنْ أَنَا إِلَّا نَذِيرٌ مُّبِينٌ ﴿١١٥﴾

115. Sikuwa mimi ila ni muonyaji aliye dhahiri.

قَالُوا لَئِن لَّمْ تَنتَهِ يَا نُوحُ لَتَكُونَنَّ مِنَ الْمَرْجُومِينَ ﴿١١٦﴾

116. Wakasema: Kama hutakoma ewe Nuh bila shaka utapigwa mawe.

قَالَ رَبِّ إِنَّ قَوْمِي كَذَّبُونِ ﴿١١٧﴾

117. Akasema: Mola wangu! Hakika kaumu yangu wamenikadhibisha.

فَافْتَحْ بَيْنِي وَبَيْنَهُمْ فَتْحًا وَنَجِّنِي وَمَن مَّعِيَ مِنَ الْمُؤْمِنِينَ ﴿١١٨﴾

118. Basi amua baina yagu mimi na wao uamuzi. Na uniokoe na walio pamoja nami katika waumini.

فَأَنجَيْنَاهُ وَمَن مَّعَهُ فِي الْفُلْكِ الْمَشْحُونِ ﴿١١٩﴾

119. Basi tukamuokoa na walio pamoja naye katika jahazi iliyosheheni.

ثُمَّ أَغْرَقْنَا بَعْدُ الْبَاقِينَ ﴿١٢٠﴾

120. Kisha tukawagharikisha baadaye waliobaki.

إِنَّ فِي ذَٰلِكَ لَآيَةً وَمَا كَانَ أَكْثَرُهُم مُّؤْمِنِينَ ﴿١٢١﴾

121. Hakika bila shaka katika hayo ipo ishara, lakini wengi wao si wenye kuamini.

وَإِنَّ رَبَّكَ لَهُوَ الْعَزِيزُ الرَّحِيمُ ﴿١٢٢﴾

122. Na hakika Mola wako ndiye Mwenye nguvu, Mwenye kurehemu.

NUH

Aya 105 – 122

MAANA

Kaumu ya Nuh waliwakadhibisha mitume.

Mtume aliyetumwa kwao ni mmoja ambaye ni Nuh, lakini mwenye kumkadhibisha Mtume mmoja ni kama amewakadhibisha mitume wote, kwa vile aliyewatuma ni mmoja na ujumbe ni mmoja.

Alipowaambia ndugu yao Nuh: Je, hamna takua?

Mwenye kuishika takua atakuwa katika amani na atasalimika na ghadhabu ya Mwenyezi Mungu na adhabu yake.

Hakika mimi kwenu ni Mtume mwaminifu.

Alijisifu kwa uaminifu ambao waliujua kwake akiwa mdogo na mtu mzima; sawa na makuraishi walivyomjua Muhammad(s.a.w.w) kwa ukweli na uaminifu katika hali zake zote.

Basi mcheni Mwenyezi Mungu na mnitii. Kwa sababu ninawaita kwenye lile ambalo lina kheri yenu ya dunia na akhera.

Na siwataki ujira juu yake, kwani ujira wangu hauko ila kwa Mola wa walimwengu wote.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 7 (6:90) na Juz. 12 (11:29).

Basi mcheni Mwenyezi Mungu na mnitii.

Hakuna sababu ya kukaririka jambo la takua (kumcha Mungu) isipokuwa ni jambo muhimu na la msingi.

Wakasema: Je, tukuamini na hali wanaokufuata ni walio duni.

Walimtia ila Nuh, si kwa lolote ila ni kwa kuwa mafukara walimwamini na kwao, hawana thamani. Kwa hiyo utume wa Nuh hauna thamani. Kwa maneno mengine ni kuwa wapenda anasa hawaoni kuwa ufukara ni maisha. Vipi wataamini waliloliamini mafukara? Hivi ndivyo wafanyavyo wapenda anasa; wanakuwa vipofu wa haki na wanakuwa na kiburi.

Akasema: Nayajuaje waliyokuwa wakiyafanya? Hisabu yao haiko ila kwa Mola wangu.

Nuh aliwaambia wale waliomjadili kuhusu ufukara, kuwa thamani ya mtu ni matendo yake na malengo yake, sio kwa cheo na mali. Na mimi sijui kuwa wao walimfanyia ubaya mtu yoyote kwa kauli au vitendo. Siri iko kwa Mwenyezi Mungu. Yeye peke yake ndiye anayejua na kuhisabu.

Lau mngelitambua kwamba thamani ya mtu ni kwa matendo sio kwa mali na dhahiri ni ya watu na batini ni ya Mwenyezi Mungu.

Wala mimi si mwenye kuwafukuza waumini. Sikuwa mimi ila ni muonyaji aliye dhahiri.

Umetangulia mfano wake katika Juz. Juz. 12 (11: 29).

Wakasema: Kama hutakoma ewe Nuh bila shaka utapigwa mawe.

Wameshindwa kuijadili haki wakakimbilia vitisho na mabavu. Hii ndio tabia ya wasiofuta haki, kila mahali na kila wakati.

Akasema: Mola wangu! Hakika kaumu yangu wamenikadhibisha. Basi amua baina yagu mimi na wao uamuzi.

Walipompa vitisho vya kutumia nguvu, alimuomba msaada Mwenyezi Mungu na nguvu zake. Na kwa unyenyekevu akamuomba Mwenyezi Mungu ahukumu, baina yake na yao, hukumu itakayomnusuru mwenye haki na kumwadhibu mwenye batili.

Na uniokoe na walio pamoja nami katika waumini pale itakapowashukia adhabu makafiri.

Basi tukamuokoa na walio pamoja naye katika jahazi iliyosheheni walioamini katika watu wake na wengineo na viumbe wengine wa kiume na wa kike. Kisha tukawagharikisha baadaye waliobaki.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 8 (7:64) na Juz. 12 (11:40).

Hakika bila shaka katika hayo ipo ishara, lakini wengi wao si wenye kuamini . Na hakika Mola wako ndiye Mwenye nguvu, Mwenye kurehemu. Imetangulia kwa herufi zake, katika Aya 67 na 68 ya Sura hii.

كَذَّبَتْ عَادٌ الْمُرْسَلِينَ ﴿١٢٣﴾

123. A’d waliwakadhibisha mitume.

إِذْ قَالَ لَهُمْ أَخُوهُمْ هُودٌ أَلَا تَتَّقُونَ ﴿١٢٤﴾

124. Alipowaambia ndugu yao Hud: Je, hamna takua?

إِنِّي لَكُمْ رَسُولٌ أَمِينٌ ﴿١٢٥﴾

125. Hakika mimi kwenu ni Mtume mwaminifu.

فَاتَّقُوا اللَّـهَ وَأَطِيعُونِ ﴿١٢٦﴾

126. Basi mcheni Mwenyezi Mungu na mnitii.

وَمَا أَسْأَلُكُمْ عَلَيْهِ مِنْ أَجْرٍ إِنْ أَجْرِيَ إِلَّا عَلَىٰ رَبِّ الْعَالَمِينَ ﴿١٢٧﴾

127. Na siwataki ujira juu yake, kwani ujira wangu hauko ila kwa Mola wa walimwengu wote.

أَتَبْنُونَ بِكُلِّ رِيعٍ آيَةً تَعْبَثُونَ ﴿١٢٨﴾

128. Je, mnajenga juu ya kila muinuko ishara ya kufanyia upuuzi?

وَتَتَّخِذُونَ مَصَانِعَ لَعَلَّكُمْ تَخْلُدُونَ ﴿١٢٩﴾

129. Na mnajenga ngome ili mkae milele.

وَإِذَا بَطَشْتُم بَطَشْتُمْ جَبَّارِينَ ﴿١٣٠﴾

130. Na mnaposhika kwa nguvu mnashika kwa nguvu kwa ujabari.

فَاتَّقُوا اللَّـهَ وَأَطِيعُونِ ﴿١٣١﴾

131. Basi mcheni Mwenyezi Mungu na mnitii.

وَاتَّقُوا الَّذِي أَمَدَّكُم بِمَا تَعْلَمُونَ ﴿١٣٢﴾

132. Na mcheni ambaye amewapa mnayoyajua.

أَمَدَّكُم بِأَنْعَامٍ وَبَنِينَ ﴿١٣٣﴾

133. Amewapa wanyama na watoto wa kiume.

وَجَنَّاتٍ وَعُيُونٍ ﴿١٣٤﴾

134. Na mabustani na chemchemi.

إِنِّي أَخَافُ عَلَيْكُمْ عَذَابَ يَوْمٍ عَظِيمٍ ﴿١٣٥﴾

135. Hakika ninawahofia adhabu ya siku kubwa.

قَالُوا سَوَاءٌ عَلَيْنَا أَوَعَظْتَ أَمْ لَمْ تَكُن مِّنَ الْوَاعِظِينَ ﴿١٣٦﴾

136. Wakasema: Ni mamoja kwetu ukitupa mawaidha au kutokuwa miongoni mwa watoao mawaidha.

إِنْ هَـٰذَا إِلَّا خُلُقُ الْأَوَّلِينَ ﴿١٣٧﴾

137. Haya si chochote ila ni hulka ya wa kale.

وَمَا نَحْنُ بِمُعَذَّبِينَ ﴿١٣٨﴾

138. Wala sisi hatutaadhibiwa.

فَكَذَّبُوهُ فَأَهْلَكْنَاهُمْ إِنَّ فِي ذَٰلِكَ لَآيَةً وَمَا كَانَ أَكْثَرُهُم مُّؤْمِنِينَ ﴿١٣٩﴾

139. Basi wakamkadhibisha na tukawahilikisha. Hakika bila shaka katika hayo ipo ishara, lakini wengi wao si wenye kuamini.

وَإِنَّ رَبَّكَ لَهُوَ الْعَزِيزُ الرَّحِيمُ ﴿١٤٠﴾

140. Na hakika Mola wako ndiye Mwenye nguvu, Mwenye kurehemu.

Hud

Aya 123 – 140

MAANA

Kisa cha Hud kimetangulia katika Juz. 8 (7:65 – 72) na Juz. 12 (11:50 – 60).

A’d waliwakadhibisha mitume. Alipowaambia ndugu yao Hud: Je, hamna takua? Hakika mimi kwenu ni Mtume mwaminifu. Basi mcheni Mwenyezi Mungu na mnitii. Na siwataki ujira juu yake, kwani ujira wangu hauko ila kwa Mola wa walimwengu wote.

Zimetangulia Aya kwa herufi zake katika sehemu iliyopita ya Sura hii Aya 105 – 110, bila ya mabadiliko yoyote isipokuwa jina tu. Kule imesemwa kaumu ya Nuh na hapa ni Hud na A’d.

Siri ya hilo ni kuwa risala ya mitume wote ni moja, ikilingania kwenye umoja wa Mwenyezi Mungu na kutii amri yake na makatazo yake.

Je, mnajenga juu ya kila muinuko ishara ya kufanyia upuuzi?

Makusudio ya ishara hapa ni jengo. Kila jengo linalotekeleza haja ya maisha hilo ni la kheri na ni katika dini. Kwa sababu dini ya Mwenyezi Mungu ni dini ya maisha. Ama jengo lisilokuwa na faida zaidi ya kujionyesha na kujifaharisha, hilo ni shari kidini na kiakili. Aina hii ndio inayokusudiwa hapa kwa dalili ya kauli yake Mwenyezi Mungu ‘ya kufanyia upuuzi’ kwa sababu upuuzi ni ule usiohitajika.

Na mnajenga ngome ili mkae milele.

Makusudio ya ngome hapa ni jengo lisilokuwa na manufaaa yoyote.

Na mnaposhika kwa nguvu mnashika kwa nguvu kwa ujabari. Basi mcheni Mwenyezi Mungu na mnitii.

Kutumia nguvu kwa ujabari ni kudhulumu kwa hali ya juu, na inakuwa kubwa dhulma kwa kumdhulumu mnyonge. Lililothibiti katika dini ya Mwenyezi Mungu ni kuwa dhulma ni miogoni mwa madhambi makubwa; bali ni sawa na kumkufuru Mungu.

Tumelithibitisha hilo huko nyuma kwa nukuu ya Qur’an.

Aya hii ilishuka wakati ambao hakukuwa na silaha za maangamizi wala hakukuwa na matajiri wanaotoa mamilioni ya pesa ili waangamizwe wanawake kwa ujumla. Ilishuka wakati ambao kutumia nguvu kulikuwa ni kwa kutumia mkono zaidi - upanga mshale na mkuki.

Ikiwa Mwenyezi Mungu amesifu kuwa ni ubaya na uovu mkubwa kutumia nguvu kwa kiganja cha mkono, basi atawalipa nini wale wanaowanyeshea wanyonge mvua ya makombora, mabomu ya sumu na silaha za nuklia? Au wale ambao wameijaza ardhi na anga kwa vikosi vya majeshi. Wameijaza maroketi ya kijeshi; si kwa lolote ila wanataka kuhukumu roho za waja na nyenzo za nchi kulingana na hawa zao na masilahi yao tu.

Na mcheni ambaye amewapa mnayoyajua. Amewapa wanyama na watoto wa kiume na mabustani na chemchemi. Hakika ninawahofia adhabu ya siku kubwa.

Hud aliwalingania kwenye twaa ya Mwenyezi Mungu na akawakumbusha neema yake juu yao na anavyowapa muda na pia akawahadharisha na mwisho mbaya wa dhulma. Lakini hilo halikuwazidisha kitu isipokuwa kiburi nawakasema: Ni mamoja kwetu ukitupa mawaidha au kutokuwa miongoni mwa watoao mawaidha sisi hatutakuamini. Mawaidha yako hayatatuzidishia isipokuwa kuachana nawe.

Haya si chochote ila ni hulka ya wa kale wala sisi hatutaadhibiwa.

Haya ni ishara ya dini yao na masanamu yao wanayoyaabudu; na kwamba wao hawatayaacha kwa sababu wameyarithi kutoka jadi na jadi. Hiyo ndiyo hoja yao; hawana zaidi ya ‘tumewakuta nayo baba zetu na sisi tunafuata nyayo zao.’

Basi wakamkadhibisha na tukawahilikisha.

Hud aliwaonya watu wake kwa dalili na hoja, lakini hawakujali, wakawa miongoni mwa walioangamia.

Hakika bila shaka katika hayo ipo ishara, lakini wengi wao si wenye kuamini. Na hakika Mola wako ndiye Mwenye nguvu, Mwenye kurehemu.

Imetangulia kwa herufi zake, katika Aya 67 na 68 ya Sura hii na pia sehemu iliyopita.


4

5

6