TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI Juzuu 20

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI23%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: Qurani tukufu

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
  • Anza
  • Iliyopita
  • 25 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 16602 / Pakua: 3729
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI Juzuu 20

Mwandishi:
Swahili

1

2

3

4

19

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI

Sura Ya Thelathini Na Mbili: Surat As-Sajda. Ina Aya 30. Mwenye Majmaul-bayan anasema: Imeshuka Makka isipokuwa Aya tatu zimeshuka Madina; kuanzia 18 – 20.

بِسْمِ اللَّهِ الرَّحْمَٰنِ الرَّحِيمِ

Kwa jina la Mwenyezi Mungu Mwingi wa rehema, Mwenye kurehemu.

الم ﴿١﴾

1. Alif Laam Miim.

تَنزِيلُ الْكِتَابِ لَا رَيْبَ فِيهِ مِن رَّبِّ الْعَالَمِينَ ﴿٢﴾

2. Ni uteremsho wa Kitabu kisicho na shaka ndani yake, kinachotoka kwa Mola wa walimwengu wote.

أَمْ يَقُولُونَ افْتَرَاهُ بَلْ هُوَ الْحَقُّ مِن رَّبِّكَ لِتُنذِرَ قَوْمًا مَّا أَتَاهُم مِّن نَّذِيرٍ مِّن قَبْلِكَ لَعَلَّهُمْ يَهْتَدُونَ ﴿٣﴾

3. Au wanasema amekizua? Bali hicho ni haki itokayo kwa Mola wako, ili uwaonye watu wasiofikiwa na mwonyaji kabla yako, huenda wakaongoka.

اللَّـهُ الَّذِي خَلَقَ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضَ وَمَا بَيْنَهُمَا فِي سِتَّةِ أَيَّامٍ ثُمَّ اسْتَوَىٰ عَلَى الْعَرْشِ مَا لَكُم مِّن دُونِهِ مِن وَلِيٍّ وَلَا شَفِيعٍ أَفَلَا تَتَذَكَّرُونَ ﴿٤﴾

4. Mwenyezi Mungu ndiye aliyeziumba mbingu na ardhi na vilivyomo kati yake katika siku sita. Kisha akatawala kwenye Arshi. Hamna walii wala mwombezi isipokuwa Yeye. Basi je hamkumbuki?

يُدَبِّرُ الْأَمْرَ مِنَ السَّمَاءِ إِلَى الْأَرْضِ ثُمَّ يَعْرُجُ إِلَيْهِ فِي يَوْمٍ كَانَ مِقْدَارُهُ أَلْفَ سَنَةٍ مِّمَّا تَعُدُّونَ ﴿٥﴾

5. Hulipanga jambo kutoka mbinguni hadi ardhini, kisha linapanda kwake katika siku ambayo kipimo chake ni miaka elfu kwa mnavyohisabu.

ذَٰلِكَ عَالِمُ الْغَيْبِ وَالشَّهَادَةِ الْعَزِيزُ الرَّحِيمُ ﴿٦﴾

6. Huyo ndiye Mjuzi wa mambo ya ghaibu na ya dhahiri, Mwenye uwezo, Mwenye kurehemu.

الَّذِي أَحْسَنَ كُلَّ شَيْءٍ خَلَقَهُ وَبَدَأَ خَلْقَ الْإِنسَانِ مِن طِينٍ ﴿٧﴾

7. Ambaye ametengenza vizuri umbo la kila kitu. Na akaanzisha umbo la mtu kwa udongo.

ثُمَّ جَعَلَ نَسْلَهُ مِن سُلَالَةٍ مِّن مَّاءٍ مَّهِينٍ ﴿٨﴾

8. Kisha akajaalia uzao wake utokane na kizazi cha maji hafifu.

ثُمَّ سَوَّاهُ وَنَفَخَ فِيهِ مِن رُّوحِهِ وَجَعَلَ لَكُمُ السَّمْعَ وَالْأَبْصَارَ وَالْأَفْئِدَةَ قَلِيلًا مَّا تَشْكُرُونَ ﴿٩﴾

9. Kisha akamlinganisha sawa na akampulizia roho yake. Na amewajaalia kusikia na kuona na nyoyo. Ni uchache mnavyoshukuru.

AMETENGENEZA VIZURI UMBO LA KILA KITU

Aya 1 – 9

MAANA

Alif Laam Miim.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 1 (2:1).

Ni uteremsho wa Kitabu kisicho na shaka ndani yake, kinachotoka kwa Mola wa walimwengu wote.

Ushahidi wa hilo tumeuleza kwenye Aya kadhaa; kama vile Juz. 1 ( 2:23 – 25), Juz. 5 (4:80 – 82) na Juz. 18 (24:55 – 57).

Au wanasema amekizua? Bali hicho ni haki itokayo kwa Mola wako, ili uwaonye watu wasiofikiwa na mwonyaji kabla yako, huenda wakaongoka.

Wapenda anasa wanaojitia kwenye upotevu, katika vigogo wa kikuraishi, walisema: “Qur’an ni utungo wa Muhammad.” Mwenyezi Mungu (s.w.t.) akasema, kuwarudi, kuwa hapana bali ni wahyi wa Mwenyezi Mungu na Muhammad amewajia na yale ambayo hajawaletea yeyote kabla yake wala hatawaletea yeyote baada yake.

Amewajia na kheri ya dunia na akhera akawakataza dhulma na ufisadi mlio nao, ili mpate mawaidha na muache kabla hayajawafikia majanga. Ilitakiwa mumshukuru Muhammad kwa fadhila hii badala ya kumpangia njama za kiuadui na kumfanya ni mwongo mzushi.

Mwenyezi Mungu ndiye aliyeziumba mbingu na ardhi na vilivyomo kati yake katika siku sita. Kisha akatawala kwenye arshi. Hamna walii wala mwombezi isipokuwa Yeye. Basi je hamkumbuki?

Siku sita ni kinaya cha mikupuo au mara. Makusdio ya Arshi ni utawala. Umetangulia mfano wake katika Juz. 8 (7:54), Juz. 11 (10:3) na Juz. 19 (25:59). Katika Juz. 8 (54:56) tumeeleza kauli zilizosemwa kuhusu siku sita na rai yetu.

Hulipanga jambo kutoka mbinguni hadi ardhini, kisha linapanda kwake katika siku ambayo kipimo chake ni miaka elfu kwa mnavyohisabu.

Makusudio ya kupanga jambo ni kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) ameumba ulimwengu, kila kiumbe akakipa sifa kwa namna inavyotaka hekima yake. Akamwajibishia kiumbe ambaye amempa uweza na utambuzi kulazimiana na njia aliyomwongoza.

Makusudio ya ‘kupanda kwake katika siku’ ni kuwa matendo ya viumbe yatakwenda kwake Siku ya Kiyama. Miaka elfu ni kinaya cha kurefuka zama.

Maana ni kuwa viumbe wote wamezungukwa na mipangilio ya Mungu na ulinzi wake. Yeye ndiye aliyewaleta na akawapangilia vizuri: “ambaye amekipa kila kitu umbo lake kisha akakiongoza” Juz. 16 (20:50). Ni Yeye atakayekimaliza na kukirudisha, na matendo yatapelekwa kwake siku ambayo itakuwa ndefu na nzito kwa waasi na wakosefu.

Huyo ndiye Mjuzi wa mambo ya ghaibu na ya dhahiri, Mwenye uwezo Mwenye kurehemu.

Muumba wa kila kitu na msimamizi wa kila kitu. Ni Mjuzi wa ya lililokuwa na litakalokuwa, liwe dogo au kubwa, la dhahiri au la kujificha. Ni Mwenye nguvu kwa uweza wake na ufalme wake na Mwenye huruma kwa viumbe wake na waja wake.

Ambaye ametengenza vizuri umbo la kila kitu.

Kila kiumbe kilichopatikana kwa nidhamu kamili basi ni kizuri na kimepangika, kikifahamisha uwezo wa mtengenezaji na utukufu wake. Hakuna kitu chochote kilichopo ila utaona nidhamu na uwiano unaofahamisha kuweko mjuzi mwenye hekima:

مَّا تَرَىٰ فِي خَلْقِ الرَّحْمَـٰنِ مِن تَفَاوُتٍ فَارْجِعِ الْبَصَرَ هَلْ تَرَىٰ مِن فُطُورٍ ﴿٣﴾

“Hutaona tofauti yoyote katika uumbaji wa Mwingi wa rehema. Hebu rudisha jicho, je unaona kosa lolote” (67:3).

Na akaanzisha umbo la mtu kwa udongo.

Makusudio ya mtu hapa ni baba wa watu, Adam.

Kisha akajaalia uzao wake utokane na kizazi cha maji hafifu ambayo ni manii. Kisha akamlimganisha sawa katika umbile zuri na akampulizia roho yake.

Hiki ni kinaya cha uhai. Umetangulia mfano wake katika Juz. 7 (6:2) na Juz. 18 (23:12 – 14).

Amewajaalia kusikia na kuona na nyoyo. Ni uchache mnavyoshukuru.

Neema ya ubainifu inatokana na neema ya usikizi uoni na utambuzi. Ama matamanio ya chakula ni kwa ajili ya kuishi na matamanio ya jinsia ni kwa ajli ya kubakia. Hakuna matamanio yoyote kwa mtu isipokuwa yana faida na hekima.

وَقَالُوا أَإِذَا ضَلَلْنَا فِي الْأَرْضِ أَإِنَّا لَفِي خَلْقٍ جَدِيدٍ بَلْ هُم بِلِقَاءِ رَبِّهِمْ كَافِرُونَ ﴿١٠﴾

10. Na husema: Ati tutakapopotea ardhini, kweli tutakuwa kwenye umbo jipya? Bali wao wanakanusha kukutana na Mola wao.

قُلْ يَتَوَفَّاكُم مَّلَكُ الْمَوْتِ الَّذِي وُكِّلَ بِكُمْ ثُمَّ إِلَىٰ رَبِّكُمْ تُرْجَعُونَ ﴿١١﴾

11. Sema, atawafisha malaika wa mauti aliyewakilishwa kwenu; kisha mtarejeshwa kwa Mola wenu.

وَلَوْ تَرَىٰ إِذِ الْمُجْرِمُونَ نَاكِسُو رُءُوسِهِمْ عِندَ رَبِّهِمْ رَبَّنَا أَبْصَرْنَا وَسَمِعْنَا فَارْجِعْنَا نَعْمَلْ صَالِحًا إِنَّا مُوقِنُونَ ﴿١٢﴾

12. Na ungeliwaona wakosefu wanavyoinamisha vichwa vyao mbele ya Mola wao. Mola wetu! Tumeona na tumesikia, turejeshe tutatenda mema, kwani hakika sisi tuna yakini.

وَلَوْ شِئْنَا لَآتَيْنَا كُلَّ نَفْسٍ هُدَاهَا وَلَـٰكِنْ حَقَّ الْقَوْلُ مِنِّي لَأَمْلَأَنَّ جَهَنَّمَ مِنَ الْجِنَّةِ وَالنَّاسِ أَجْمَعِينَ ﴿١٣﴾

13. Na lau tungelitaka tungeipa kila nafsi muongozo wake. Lakini imehakikika kauli kutoka kwangu: Kwa hakika nitaijaza Jahannam kwa wote majini na watu.

فَذُوقُوا بِمَا نَسِيتُمْ لِقَاءَ يَوْمِكُمْ هَـٰذَا إِنَّا نَسِينَاكُمْ وَذُوقُوا عَذَابَ الْخُلْدِ بِمَا كُنتُمْ تَعْمَلُونَ ﴿١٤﴾

14. Basi onjeni kwa sababu ya kusahau mkutano wa siku yenu hii, hakika sisi tumewasahau. Na onjeni adhabu yenye kudumu kwa yale mliyokuwa mkiyatenda.

WAKOSEFU WANAINAMISHA VICHWA VYAO.

Aya 10-14

MAANA

Na husema: Ati tutakapopotea ardhini, kweli tutakuwa kwenye umbo jipya?”

Hii ni sawa na kauli yao:

أَإِذَا كُنَّا تُرَابًا أَإِنَّا لَفِي خَلْقٍ جَدِيدٍ أُولَـٰئِكَ الَّذِينَ كَفَرُوا بِرَبِّهِمْ ﴿٥﴾

“Ati tutakapokuwa mchanga, kweli tutakuwa katika umbo jipya?” Juz.13(13:5)

Bali wao wanakanusha kukutana na Mola wao.

Unaweza kuuliza : Washirikina walitangaza waziwazi kufuru yao ya kukutana na Mwenyezi Mungu waziwazi. Sasa kuna haja gani ya kusema wanakanusha kukutana na Mola wao? Si ni sawa na kumwambia aliyetangaza ukafiri kuwa wewe ni kafiri?

Jibu : makusudio ni kuwa wao hawakuipinga akhera kwa ujuzi, bali ni kwa ujinga na kuiga; sawa na kumwambia aliyetangaza ukafiri: wewe ni mjinga.

Sema, atawafisha malaika wa mauti aliyewakilishwa kwenu; kisha mtarejeshwa kwa Mola wenu.

Yaani, ewe Muhammad! Waambie waliokufuru kuwa nyinyi mtakufa tu, hilo halina shaka. Baada ya mauti hakika itawafunukia na mtajua kuwa bila shaka saa ya Kiyama itakuja na kwamba Mwenyezi Mungu atawafufua walio katika makaburi.

Na ungeliwaona wakosefu wanavyoinamisha vichwa vyao mbele ya Mola wao.

Walipinga ufufuo na wakawafanyia maskhara waliouamini, waliowapa mwito wake na kuwahadhari na mwisho mbaya. Watapofufuliwa na kusimama mbele ya Mola wao kwa ajili ya hisabu watainamisha vichwa vyao kwa kuona haya na majuto na kusema:

Mola wetu! Tumeona na tumesikia, turejeshe tutatenda mema, kwani hakika sisi tuna yakini.

Umetangulia mfano wake katika Juz.7 (6:27) na Juz. 18 (23:99 – 100).

Na lau tungelitaka tungeipa kila nafsi muongozo wake.

Razi anasema: “ Hii ni wazi kuwa madhehebu yetu yako sahihi pale tunaposema: Mwenyezi Mungu hakutaka imani kutoka kwa kafiri na hakutaka kwake isipokuwa kufuru.”

Nasi tunamwambia Razi: Ikiwa Mwenyezi Mungu ndiye aliyetaka kufuru kwa kafiri, na hakuna anayerudisha matakwa yake, basi kwa nini atamwadhibu. Vipi na Yeye ndiye aliyesema: “Wala hatukuwadhulumu, bali wao ndio waliokuwa madhalimu” (43:76).

Usahihi ni kuwa makusudio ya matakwa ya Mwenyezi Mungu hapa ni matakwa ya kiuumbaji ambayo ni kusema ‘kuwa.’

Yaani lau Mwenyezi Mungu angelitaka kuwalazimisha uongofu wangeliongoka. Na kama angelifanya hivyo, basi kusingekuwa na thawabu wala adhabu. Hayo tumeyaeleza mara kadhaa. Tazama Juz. 6 (5:49 – 50).

Lakini imehakikika kauli kutoka kwangu: Kwa hakika nitaijaza Jahannam kwa wote majini na watu.

Imehakikika kauli kutoka kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu kwamba ataijaza Jahannam kwa wafisadi na wale walioasi kwa hiyari na matakwa yao wenyewe. Ama wale ambao walimwitikia Mola wao wana maghufira na malipo makubwa. Kuna Hadith Qudsi inayosema: “Nimeiumba Pepo kwa anayenitii hata kama ni mtumwa Muhabeshi; na moto kwa anayeniasi hata kama ni bwana wa kikuraishi.”

Basi onjeni kwa sababu ya kusahau mkutano wa siku yenu hii, hakika sisi tumewasahau. Na onjeni adhabu yenye kudumu kwa yale mliyokuwa mkiyatenda.

Hakuna yoyote aliyefuata matamanio yake na hawa yake ila atamsahau Mwenyezi Mungu na hisabu na ataikufuru haki na dhamiri. Na kesho malaika wa adhabu watamwambia mkosaji huyu: umelewa utamu wa dunia basi leo onja uchungu wa akhera. Umetangulia mfano wake katika Juz. 8 (7:51) na Juz. 10 (9:67).

إِنَّمَا يُؤْمِنُ بِآيَاتِنَا الَّذِينَ إِذَا ذُكِّرُوا بِهَا خَرُّوا سُجَّدًا وَسَبَّحُوا بِحَمْدِ رَبِّهِمْ وَهُمْ لَا يَسْتَكْبِرُونَ ﴿١٥﴾

15. Hakika wanaoziamni Aya zetu ni wale tu ambao wanapokumbushwa hizo huanguka kusujudu na humsabihi kwa kumsifu Mola wao, nao hawatakabari.

تَتَجَافَىٰ جُنُوبُهُمْ عَنِ الْمَضَاجِعِ يَدْعُونَ رَبَّهُمْ خَوْفًا وَطَمَعًا وَمِمَّا رَزَقْنَاهُمْ يُنفِقُونَ ﴿١٦﴾

16. Mbavu zao zinaachana na vitanda kumwomba Mola wao kwa hofu na tumaini, na hutoa katika yale tuliyowaruzuku.

فَلَا تَعْلَمُ نَفْسٌ مَّا أُخْفِيَ لَهُم مِّن قُرَّةِ أَعْيُنٍ جَزَاءً بِمَا كَانُوا يَعْمَلُونَ ﴿١٧﴾

17. Nafsi yoyote haijui waliyofichiwa katika yanayofurahisha maisha. Ni malipo ya yale waliyokuwa wakiyatenda.

أَفَمَن كَانَ مُؤْمِنًا كَمَن كَانَ فَاسِقًا لَّا يَسْتَوُونَ ﴿١٨﴾

18. Je, aliye mumin ni sawa na aliye fasiki? Hawawi sawa.

أَمَّا الَّذِينَ آمَنُوا وَعَمِلُوا الصَّالِحَاتِ فَلَهُمْ جَنَّاتُ الْمَأْوَىٰ نُزُلًا بِمَا كَانُوا يَعْمَلُونَ ﴿١٩﴾

19. Ama wale ambao wameamini na wakatenda mema watakuwa na bustani za makao. Ndipo pa kufikia kwa waliyokuwa wakiyatenda.

وَأَمَّا الَّذِينَ فَسَقُوا فَمَأْوَاهُمُ النَّارُ كُلَّمَا أَرَادُوا أَن يَخْرُجُوا مِنْهَا أُعِيدُوا فِيهَا وَقِيلَ لَهُمْ ذُوقُوا عَذَابَ النَّارِ الَّذِي كُنتُم بِهِ تُكَذِّبُونَ ﴿٢٠﴾

20. Na ama wale ambao wamefanya ufuska, basi makazi yao ni motoni; kila wakitaka kutoka humo watarudishwa humo humo. Na wataambiwa: Onjeni adhabu ya moto ambayo mlikuwa mkiikadhibisha.

وَلَنُذِيقَنَّهُم مِّنَ الْعَذَابِ الْأَدْنَىٰ دُونَ الْعَذَابِ الْأَكْبَرِ لَعَلَّهُمْ يَرْجِعُونَ ﴿٢١﴾

21. Na kwa hakika tutawaonjesha adhabu hafifu kabla ya adhabu kubwa, labda watarejea.

وَمَنْ أَظْلَمُ مِمَّن ذُكِّرَ بِآيَاتِ رَبِّهِ ثُمَّ أَعْرَضَ عَنْهَا إِنَّا مِنَ الْمُجْرِمِينَ مُنتَقِمُونَ ﴿٢٢﴾

22. Ni nani dhalimu mkubwa kuliko yule anayekumbushwa kwa ishara za Mola wake kisha akazikataa. Hakika sisi ni wenye kuwachukulia kisasi wakosefu.

MUUMIN ANAWEZA KUWA SAWA NA FASIKI?

Aya 15 – 22

MAANA

Hakika wanaoziamni Aya zetu ni wale tu ambao wanapokumbushwa hizo huanguka kusujudu na humsabihi kwa kumsifu Mola wao.

Makusudio ya waumini hapa ni wale wanaoijua haki na kuitumia na kujitolea muhanga kwa ajaili yake; wanamwabudu Mwenyezi Mungu usiku na mchana kwa kumtegemea Yeye na kumfanyia ikhlasi peke yake, asiyekuwa na mshirika. Ama tasbihi, rukui na sujudi kwa msukumo wa chumo na kibiashara kwa dini, yote hayo ni unafiki sio ibada na ni uzandiki sio imani.

Nao hawatakabari; yaani waumini wanaikaribisha haki na kuacha masilahi yao binafsi kwa ajili ya haki; kwa sabu hiyo ndiyo dini yao na masilahi yao.

Ni wajibu kusujudi kwa mwenye kuisoma Aya hii au kuisikiliza na imesemekana hata mwenye kuisikia pia bila ya kukusudia.

Mbavu zao zinaachana na vitanda kumwomba Mola wao kwa hofu na tumaini.

Vitanda ni kinaya cha usingizi. Tukiunganisha Aya hii na kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: “Watu ambao biashara wala kuuza hakuwashughulishi na kumdhukuru Mwenyezi Mungu.” Juz. 18 (24:37), maana yatakuwa: Hakika waumini haiwashughulishi biashara wala usingizi kuacha ibada ya Mwenyezi Mungu, jambo ambalo linaelezea kuhofia kwao adhabu yake na kutumai kwao thawabu zake.

Ibada hiyo ndiyo aliyoikusudia Mwenyezi Mungu aliposema: “Na usi- mamishe Swala, hakika Swala inakataza machafu na maovu.” Kuna Hadith isemayo: Kisimamo cha mja kinamkurubisha kwa Mwenyezi Mungu, kinamkataza dhambi, kinafuta maovu na kufukuza ugonjwa mwilini.” Ama Swala ya kibiashara huwa inaamrisha uovu na ubaya. Kwa sababu ubaya unaelekeza kwenye mfano wake na vile vile wema.

Na hutoa katika yale tuliyowaruzuku.

Wamemwabudu Mwenyezi Mungu kwa nyoyo, miili na mali.

Nafsi yoyote haijui waliyofichiwa katika yanayofurahisha maisha. Ni malipo ya yale waliyokuwa wakiyatenda.

Makusudio ya nafsi ni nafsi yoyote, iliyokuwa na itakayokuwa katika ardhi au mbingu. Maana ni kuwa hakuna yeyote anayejua uhakika wa thawabu za kufurahisha ambazo Mwenyezi Mungu amewaandalia waumini, wenye kufanya matendo. Mtume anasema katika Hadith: “Mwenyezi Mungu anasema: “Nimewaandalia waja wangu wema ambayo hakuna jicho liliyaona wala sikio lililoyoyasikia, wala moyo uliyoyawazia.”

Je, aliye mumin ni sawa na aliye fasiki? Hawawi sawa.

Tafsri nyingi; ikiwemo Jamiu ya Tabariy, Bahrul-muhit ya Andalusi, Ruhul-bayan ya Haqi, zimesema kuwa Aya hii ilishuka Madina kuhusiana na Ali bin Abi Twalib na Walid bin U’qba bin Abi Mu’it. Tutanukuu yale ya Tabariy: “Kulipita maneno baina ya Walid na Ali. Walid akasema: “Mimi nina ulimi mpana kuliko wewe, nina meno makali kuliko wewe na ninafaa zaidi kwenye jeshi kuliko wewe.” Ali akamwambia, nyamaza wewe ni fasiki, ndipo ikashuka: ‘Je, aliye mumin ni sawa na aliye fasiki? Hawawi sawa.

Hapana wallah hawawi sawa duniani wala kwenye mauti na akhera pia.

Ama wale ambao wameamini na wakatenda mema watakuwa na bustani za makao. Ndipo pa kufikia kwa waliyokuwa wakiyatenda.

Hii ni kutofautisha baina ya mumin mwenye takua na kafiri muovu; ni sawa na kutofautisha wema na uovu, heri na shari na Pepo iliyoandaliwa wenye takua na moto ulioandaliwa wakosefu.

Na ama wale ambao wamefanya ufuska, basi makazi yao ni motoni; kila wakitaka kutoka humo watarudishwa humo humo. Na wataambiwa: Onjeni adhabu ya moto ambayo mlikuwa mkiikadhibisha.

Waumini watapata Pepo zenye neema na mafasiki watapata moto unaowaka. Umetangulia mfano wake katika Juz. 17 (22:22).

Na kwa hakika tutawaonjesha adhabu hafifu kabla ya adhabu kubwa, labda watarejea.

Makusudio ya adhabu hafifu ni adhabu ya duniani; kama vile kahati, balaa n.k. Anawaonya kwayo na kwa nguvu za hoja, wale walioghafilika na wanaojishughulisha na mambo ya batili na kuiacha haki, ili waonyeke na wapate mawaidha.

Vinginevyo watafikiwa na adhabu kubwa: “Moto wa Jahanam hali ya kudumu humo. Ni tosha yao. Na Mwenyezi Mungu amewalaani. Na wana wao adhabu ya kudumu.” Juz. 10 (9:68).

Kwa hakika ilivyo ni kuwa viongozi na watawala ndio chimbuko la kwanza la ufisadi na uovu. Kuna Hadith zinayosema: “Watawala wakiwa waongo huzuiliwa mvua, na mtawala akiwa jeuri dola inakuwa dhalili.”

Ni nani dhalimu mkubwa kuliko yule anayekumbushwa kwa ishara za Mola wake kisha akazikataa. Hakika sisi ni wenye kuwachukulia kisasi wakosefu.

Mwenye kupata mawaidha kisha asiwaidhike nayo basi huyo ni katika wakosefu wakubwa. Mwenyezi Mungu (s.w.t) amewaonya kwa ulimi wa mitume wake na kwa madhara na shida, lakini nyoyo zao zikasusuwaa na wakaendelea na dhulma na ufisadi. Ndio Mwenyezi Mungu akawalipiza kisasi na Yeye ni mwenye nguvu Mwenye kulipiza kisasi.

وَلَقَدْ آتَيْنَا مُوسَى الْكِتَابَ فَلَا تَكُن فِي مِرْيَةٍ مِّن لِّقَائِهِ وَجَعَلْنَاهُ هُدًى لِّبَنِي إِسْرَائِيلَ ﴿٢٣﴾

23. Hakika tulimpa Musa Kitabu basi usiwe na shaka ya kukipokea kwake, na tukakifanya ni mwongozo kwa wana wa Israil.

وَجَعَلْنَا مِنْهُمْ أَئِمَّةً يَهْدُونَ بِأَمْرِنَا لَمَّا صَبَرُوا وَكَانُوا بِآيَاتِنَا يُوقِنُونَ ﴿٢٤﴾

24. Na tukawafanya miongoni mwao maimamu wanaoongoza kwa amri yetu waliposubiri, na wakawa na yakini na ishara zetu.

إِنَّ رَبَّكَ هُوَ يَفْصِلُ بَيْنَهُمْ يَوْمَ الْقِيَامَةِ فِيمَا كَانُوا فِيهِ يَخْتَلِفُونَ ﴿٢٥﴾

25. Hakika Mola wako ndiye atakayefafanua baina yao Siku ya Kiyama katika lile walilohitalifiana.

أَوَلَمْ يَهْدِ لَهُمْ كَمْ أَهْلَكْنَا مِن قَبْلِهِم مِّنَ الْقُرُونِ يَمْشُونَ فِي مَسَاكِنِهِمْ إِنَّ فِي ذَٰلِكَ لَآيَاتٍ أَفَلَا يَسْمَعُونَ ﴿٢٦﴾

26. Je, haikuwabainikia, ni vizazi vingapi tuliviangamiza kabla yao nao wanatembea katika maskani zao. Hakika katika hayo kuna ishara, basi je, hawasikii.

أَوَلَمْ يَرَوْا أَنَّا نَسُوقُ الْمَاءَ إِلَى الْأَرْضِ الْجُرُزِ فَنُخْرِجُ بِهِ زَرْعًا تَأْكُلُ مِنْهُ أَنْعَامُهُمْ وَأَنفُسُهُمْ أَفَلَا يُبْصِرُونَ ﴿٢٧﴾

27. Je, hawaoni kwamba tunayapeleka maji kwenye ardhi kame, kisha kwayo tunaitoa mimea wanayokula wanyama wao. Je, hawapati busara.

وَيَقُولُونَ مَتَىٰ هَـٰذَا الْفَتْحُ إِن كُنتُمْ صَادِقِينَ ﴿٢٨﴾

28. Na wanasema: Ushindi huu utatokea lini, ikiwa nyinyi mnasema kweli?

قُلْ يَوْمَ الْفَتْحِ لَا يَنفَعُ الَّذِينَ كَفَرُوا إِيمَانُهُمْ وَلَا هُمْ يُنظَرُونَ ﴿٢٩﴾

29. Sema: Siku ya ushindi wale ambao wamekufuru haitafaa imani yao, wala hawatapewa muda.

فَأَعْرِضْ عَنْهُمْ وَانتَظِرْ إِنَّهُم مُّنتَظِرُونَ ﴿٣٠﴾

30. Basi achana nao na ungoje; hakika wao wanangoja.

USIWE NA SHAKA YA KUIPOKEA KWAKE

Aya 23 – 30

MAANA

Hakika tulimpa Musa Kitabu basi usiwe na shaka ya kukipokea kwake, na tukakifanya ni mwongozo kwa wana wa Israil.

Wafasiri wengi wamesema kuwa ‘Kwake’ inarudi kwa Musa; kwa maana ya kuwa Muhammad atakutana na Musa usiku wa Miraji. Ilivyo hasa ni kuwa dhamiri hiyo inarudia kwenye Qur’an; kwa maana ya kuwa, ewe Muhammad! Tumekutermshia Qur’an kama tulivyomteremshia Musa Tawrat. Wala haitakikani kutia shaka katika hilo wewe wala mwingine.

Kuhusu kukatazwa Mtume kutia shaka tumekuelezea mara nyingi. Tazama Juz. 3 (3:59-63).

Na tukawafanya miongoni mwao maimamu wanaoongoza kwa amri yetu waliposubiri, na wakawa na yakini na ishara zetu.

Makusudio ya maimamu hapa ni mitume wa Kiisrail; kama vile Musa, na Isa ambaye nasaba ya upande wa mama yake inafikia kwa Daud. Kila Mtume wa kiisraili alipata aina kwa aina ya adhabu na mateso; bali waisrail waliwaua manabii wao kadhaa:

وَيَقْتُلُونَ النَّبِيِّينَ بِغَيْرِ الْحَقِّ ذَٰلِكَ بِمَا عَصَوا وَّكَانُوا يَعْتَدُونَ ﴿٦١﴾

“Na wakiwaua Manabii pasipo haki. Basi haya ni kwa sababu ya kuasi kwao na kupituka mipaka.” Juz. 1 (2:61).

Pamoja na yote hayo, waliweza kuvumilia wakawa na subira na wakaendelea kutekeleza risala yao. Kwa hiyo nawe Muhammad vumilia maudhui ya watu wako na uendelee na risala yako.

Hakika Mola wako ndiye atakayefafanua baina yao Siku ya Kiyama katika lile walilohitalifiana.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 1 (2:113), Juz. 11(10:93) na Juz. 14 (16:124).

Je, haikuwabainikia, ni vizazi vingapi tuliviangamiza kabla yao nao wanatembea katika maskani zao. Hakika katika hayo kuna Ishara, basi je, hawasikii.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 16 (20).

Je, hawaoni kwamba tunayapeleka maji kwenye ardhi kame, kisha kwayo tunaitoa mimea wanayokula wanyama wao.

Je, hawapati busara kwa jinsi Mwenyezi Mungu alivyoipa uhai ardhi baada ya kufa kwake na akaotesha humo kila aina za mimea wanayokula watu na wanyama? Kama hivyo atawafufua wafu baada ya kuwa ni mchanga na mifupa

Umetangulia mfano wake katika Aya kadhaa; kama Juz. 17: (22:5).

Na wanasema: ushindi huu utatokea lini, ikiwa nyinyi mnasema kweli?

Aya hii ni mfano wa ile isemayo: “Na wanasema: Ahadi hii itatokea lini, ikiwa nyinyi mnasema kweli?” Juz. 17 (21:38). Kwa sababu makusudio ya ushindi hapa ni siku itakayohukumiwa kwa haki. Hilo linatiliwa nguvu na kauli inayofuatia:

Sema: Siku ya ushindi wale ambao wamekufuru, na wakaifanyia inadi haki katika maisha ya dunia,haitafaa imani yao huko akhera wakati watakapoiona adhabu. Kwa sababu imani hiyo itakuwa ni kuukimbia moto sio imani ya kweli na yakini.

Wala hawatapewa muda.

Mwenyezi Mungu hawezi kuwapa muda siku ya Kiyama, kwa sababu ali- wapa muda mrefu duniani, lakini hawakuitumia fursa hiyo.

Basi achana nao na ungoje; hakika wao wanangoja.

Wao wanangoja ufikwe na majanga, basi achana nao na ungoje kidogo tu, utaona hukumu ya Mwenyezi Mungu kwako na kwao. Yeye atakunusuru na atawafedhehsha wao:

هُوَ الَّذِي أَرْسَلَ رَسُولَهُ بِالْهُدَىٰ وَدِينِ الْحَقِّ لِيُظْهِرَهُ عَلَى الدِّينِ كُلِّهِ وَلَوْ كَرِهَ الْمُشْرِكُونَ ﴿٣٣﴾

“Yeye ndiye aliyemtuma Mtume wake kwa uongofu na dini ya haki ili ipate kushinda dini zote, ijapokwa washirikina wamechukia.” Juz. 10 (9:33).

20

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI

Sura Ya Thelathini Na Tatu: Surat Ahzab. Imeshuka Madina, Ina Aya 73.

بِسْمِ اللَّهِ الرَّحْمَٰنِ الرَّحِيمِ

Kwa jina la Mwenyezi Mungu, Mwingi wa rehema, Mwenye kurehemu.

يَا أَيُّهَا النَّبِيُّ اتَّقِ اللَّـهَ وَلَا تُطِعِ الْكَافِرِينَ وَالْمُنَافِقِينَ إِنَّ اللَّـهَ كَانَ عَلِيمًا حَكِيمًا ﴿١﴾

1. Ewe Nabii! Mche Mwenyezi Mungu wala usiwatii makafiri na wanafiki. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mjuzi, Mwenye hekima.

وَاتَّبِعْ مَا يُوحَىٰ إِلَيْكَ مِن رَّبِّكَ إِنَّ اللَّـهَ كَانَ بِمَا تَعْمَلُونَ خَبِيرًا ﴿٢﴾

2. Na fuata uliyoletewa wahyi kutoka kwa Mola wako. Hakika Mwenyezi Mungu ana habari za mnayoyatenda.

وَتَوَكَّلْ عَلَى اللَّـهِ وَكَفَىٰ بِاللَّـهِ وَكِيلًا ﴿٣﴾

3. Na mtegemee Mwenyezi Mungu. Na Mwenyezi Mungu anatosha kuwa ni wa kutegemewa.

EWE NABII, MCHE MWENYEZI MUNGU

Aya 1-3

MAANA

Ewe Nabii! Mche Mwenyezi Mungu wala usiwatii makafiri na wanafiki. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mjuzi Mwenye hekima. Na fuata uliyoletewa wahyi kutoka kwa Mola wako. Hakika Mwenyezi Mungu ana habari za mnayoyatenda. Na mtegemee Mwenyezi Mungu. Na Mwenyezi Mungu anatosha kuwa ni wa kutegemewa.

Katika Aya hizi Mwenyezi Mungu (s.w.t) amemwamrisha Nabii wake mtukufu, kuwa na takua, kumtegemea Yeye, kuutumia wahyi wake na kutowatii makafiri na wanafiki.

Wafasiri wamejiuliza kuwa Nabii ni maasumu, sasa kuna haja gani ya amri zote hizi na kukatazwa uasi?

Kuna waliojibu kuwa hii ni kusisitiza utiifu na unyenyekevu alio nao Nabii(s.a.w.w) . Wengine wakasema kuwa Abu Sufyan alimtaka Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) kutoyatukana masanamu wanayoyaubudu makauraishi. Abu Sufyani wakati huo alikuwa pamoja na kundi la makafiri na wanafiki.

Sisi huko nyuma tumesema mara kwa mara kuwa aliye juu ana uwezo wa kumwamrisha aliye chini na kumkataza maasi hata kama ni maasumu. Hivi sasa tunayaunganisha hayo na haya yafutayo:

Hakuna kitu kizito kwa yule asiyemuogopa Mwenyezi Mungu kuliko tamko la ‘mche Mungu;’ wala hakuna adui mkubwa kuliko atakayelisema tamko hilo kwake. Imenukuliwa kutoka kutoka kwa Abdul-Malik bin Marwani kwamba yeye alipotawala alisema katika hotuba: “Kuanzia leo, atakayeniambia: mche Mungu, nitamkata shingo yake.”

Ama yule mwenye kuhofia kukutana na Mola wake na akaikanya nafsi na matamanio, basi kwake yeye hilo ni tamko la mapenzi na huruma na hutamani lau angelisikia mara kwa mara; hata kama ni maasumu wa makosa na madhambi; bali huko kulipenda na kulisikilza kumetokana na umaasumu na utiifu wake. Mtu adhimu huwa anajituhumu kwa upunguvu kadiri atakavyoweza kujitahidi.

Kwa hiyo basi hakuna haja ya kuleta taawili na tafsiri nyingine. Kuongezea kuwa amri ya takuwa kwa bwana wa watu na majini ni hekima na somo kubwa kwa wenye vyeo na watawala, kwamba kwa vyovyote watakavyokuwa wakubwa, lakini hawako zaidi ya kuamrishwa uadilifu na takua.

Kwenye Nahjul balagha imeelezwa: “Ambaye itakuwa uzito kwake kuambiwa neno la haki au kuelezwa uadilifu basi itakuwa kuyafanya mawili hayo ni uzito zaidi.”

مَّا جَعَلَ اللَّـهُ لِرَجُلٍ مِّن قَلْبَيْنِ فِي جَوْفِهِ وَمَا جَعَلَ أَزْوَاجَكُمُ اللَّائِي تُظَاهِرُونَ مِنْهُنَّ أُمَّهَاتِكُمْ وَمَا جَعَلَ أَدْعِيَاءَكُمْ أَبْنَاءَكُمْ ذَٰلِكُمْ قَوْلُكُم بِأَفْوَاهِكُمْ وَاللَّـهُ يَقُولُ الْحَقَّ وَهُوَ يَهْدِي السَّبِيلَ ﴿٤﴾

4. Mwenyezi Mungu hakumwekea mwanamume nyoyo mbili ndani yake. Wala hakuwafanya wake zenu – mnaowalinganisha migongo yao na migongo ya mama zenu – kuwa ni mama zenu. Wala hakuwafanya watoto wenu wa kupanga kuwa ni wana wenu. Hiyo ni kauli yenu kwa vinywa vyenu tu. Na Mwenyezi Mungu anasema haki, naye huongoza njia.

ادْعُوهُمْ لِآبَائِهِمْ هُوَ أَقْسَطُ عِندَ اللَّـهِ فَإِن لَّمْ تَعْلَمُوا آبَاءَهُمْ فَإِخْوَانُكُمْ فِي الدِّينِ وَمَوَالِيكُمْ وَلَيْسَ عَلَيْكُمْ جُنَاحٌ فِيمَا أَخْطَأْتُم بِهِ وَلَـٰكِن مَّا تَعَمَّدَتْ قُلُوبُكُمْ وَكَانَ اللَّـهُ غَفُورًا رَّحِيمًا ﴿٥﴾

5. Waiteni kwa baba zao. Hilo ndio uadilifu zaidi mbele ya Mwenyezi Mungu. Kama hamuwajui mababa zao basi ni ndugu zenu katika dini na rafiki zenu. Si vibaya kwenu kwa mlivyokosea, lakini kwa yale ziliyoyakusudia nyoyo zenu. Na Mwenyezi Mungu ni Mwingi wa maghufira, Mwenye kurehemu.

MWENYEZI MUNGU HAKUMWEKA MTU MMOJA NYOYO MBILI

Aya 4 – 5

MAANA

Mwenyezi Mungu hakumwekea mwanamume nyoyo mbili ndani yake.

Hata mwanamke pia ni kama mwanamume. Mwenyezi Mungu (s.w.t) amemuhusu mwanmume hapa kwa sababu amemwamrisha Mtume(s.a.w.w) wake mtukufu kuwa na takua, kwa hiyo ikanasibiana kufuatishia amri hii kuwa mwanamume hawezi kuwa na moyo mmoja wa kumcha Mwenyezi Mungu na mwingine wa kucha watu.

Lengo ni Mwenyezi Mungu (s.w.t) anabainisha kuwa mtu hawezi kuamini mambo mawili yanayopingana kwa wakati mmoja; kwa mfano aamini dini inayokataza dhulma na uchokozi, Uislamu na Ukiristo, na wakati huo huo ahalalishe dhulma na uchokozi.

Ila ikiwa ana nyoyo mbili na nyuso mbili; kama waamerika ambao wameleta kununi mpya, kwamba mmarekani anaweza kuwa ni mwisrail na kupigana na mwarabu kwa jina la Israil na wakati huo bado ni raia wa Marekani.

Au itabidi tuseme kuwa Israil ni kambi ya jeshi la uchokozi la marekani na kwamba urai wa Israil ni jina tu; hata watawala pia; kwa vile ni kikosi tu cha kulinda masilahi ya ukoloni na unyonyaji.

Mtu mmoja alimwambia Imam Ali(a.s ) : “Mimi nakupenda wewe na ninampenda Muawiya.” Imam akamwambia:“Wewe ni chongo, sasa chagua ama uwe kipofu au upone chongo.”

Unaweza kuuliza : Utasemaje kuhusiana na anayesema; mimi ni mwislamu au mkristo kiitikadi, lakini kisiasa ninafuata siasa za mashariki au magharibi. Je inawezekana kuchanganya mawili haya?

Jibu : Mtu yoyote anayeamini haki kwa ukweli na usafi wa nia, inafaa, bali ni wajibu kumuunga mkono kila kwenye msimamo wa kuinusuru haki na uadilifu; awe ni wa mashariki au magharibi. Wala haijuzu kumuunga mkono tu, hivi hivi, bila ya msingi wowote. Kwa maana hiyo basi haiwezekeni kuchanganya baina ya itikadi ya kiislamu na kuunga mkono tu hivi hivi kwa hali yoyote.

Hii ni katika yanayohusiana na Uislamu. Ama yanayohusiana na itikadi ya kikiristo tunawaachia makasisi walio huru waliotangaza hasira zao kwa baba mtakatifu aliyekataa kukutana nao, lakini wakati huo huo akakutana na viongozi wa kimarekani.

Wakasema katika mateta yao: “Mkutano huu wa Baba mtakatifu na viongozi hawa unaonyesha wazi uhusiano wa nguvu ulioko baina ya kanisa kama tasisi ya dini na siasa za kiuchumi zinazosimamia ukandamizaji na dhulma dhidi ya watu wengi.” Makasisi hawa walitangaza kuwa wangejaribu kuuangamiza uhusiano huu[6] .

Wala hakuwafanya wake zenu – mnaowalinganisha migongo yao na migongo ya mama zenu – kuwa ni mama zenu.

Wakati wa ujahiliya mtu alikuwa akimwacha mkewe kwa kumwambia: Wewe kwangu ni kama mgongo wa mama yangu (Dhihar). Uislamu ukalikataza hilo, kwa sabau mke hawezi kuwa mama kwa kauli hii, na ukawajibisha kafara kwa atakayesema kauli hiyo, yakipatikana masharti yake, ambayo yatabainishwa mwanzoni mwa Juzuu ya 28. (inshaallah).

Wala hakuwafanya watoto wenu wa kupanga kuwa ni wana wenu.

Wakati wa ujahiliya mtu alikuwa akimchukua mtoto wa mwingine kumfanya mwanawe hasa na kumwingiza kwenye ukoo wake, anakuwa na hukumu ya mtoto wake halisi katika kila kitu na watu wakimwita kwa jina la baba aliyemchukua badala ya baba yake. Ndipo Uislamu ukakataza mtindo huu[7] .

Hiyo ni kauli yenu kwa vinwywa vyenu tu.

Na kauli haibadilishi uhalisi wa mambo.

Na Mwenyezi Mungu anasema haki naye huongoza njia.

Kauli ya haki na njia ya sawa ni kuwa mtoto wa kupanga sio mtoto wa kiuhakika; wala mke hawi ni mama kwa dhihari.

Waiteni kwa baba zao waliowazaa sio waliowapanga.Hilo ndio uadilifu zaidi mbele ya Mwenyezi Mungu. yaani hilo la kuwaita kwa ubini wa baba zao.

Kama hamuwajui mababa zao basi ni ndugu zenu katika dini na rafiki zenu.

Neno rafiki limefasiriwa kutokana na neno mawla, pia lina maana ya huria; mtumwa aliyeachwa huru. Mtu alikuwa anaweza kuitwa huria wa fulani.

Wafsiri na watu wa sera wanasema kuwa Zayd Bin Haritha alitekwa nyara akiwa mdogo. Hakim bin Huzam akamnunua kwa ajili ya kumpatia shangazi yake Khadija Bint Khuwalid. Mtume(s.a.w.w) alipomuoa akapewa zawadi na mkewe. Baada ya kushuka wahyi kwa Nabii, akamlingania kwenye Uisalamu na akasilimu. Akamfanya ndugu na ami yake Hamza bin Abu Twalib.

Haritha, Baba yake Zayd, akaja siku moja kwa Mtume(s.a.w.w) na kumwambia, ama uniuzie mwanangu, au mwache huru. Mtume akamwacha huru na kumwambia nenda upendako. Basi akakataa kuachana na Mtume. Ndipo watu wakawa wanamwita Zayd bin Muhammad mpaka iliposhuka Qur’an kubatilisha hilo.

Si vibaya kwenu kwa mlivyokosea, lakini kwa yale ziliyoyakusudia nyoyo zenu. Na Mwenyezi Mungu ni Mwingi wa maghufira, Mwenye kurehemu.

Anayemwita mtu asiyekuwa baba yake kwa kufikiria kuwa ni baba yake, hana lawama; isipokuwa mwenye dhambi ni yule aliyejua na akakusudia: Mtume(s.a.w.w) anasema: “Umma wangu umeondolewa kukosea na kusahau na yale waliyolazimishwa na wasiyoyajua na wasiyoyaweza na wanayokuwa na dharura nayo,” kwa sharti la kutotokea hayo kwa uzembe na kupuuza.

النَّبِيُّ أَوْلَىٰ بِالْمُؤْمِنِينَ مِنْ أَنفُسِهِمْ وَأَزْوَاجُهُ أُمَّهَاتُهُمْ وَأُولُو الْأَرْحَامِ بَعْضُهُمْ أَوْلَىٰ بِبَعْضٍ فِي كِتَابِ اللَّـهِ مِنَ الْمُؤْمِنِينَ وَالْمُهَاجِرِينَ إِلَّا أَن تَفْعَلُوا إِلَىٰ أَوْلِيَائِكُم مَّعْرُوفًا كَانَ ذَٰلِكَ فِي الْكِتَابِ مَسْطُورًا ﴿٦﴾

6. Nabii ni aula kwa waumini kuliko nafsi zao. Na wake zao ni mama zao. Na ndugu wa tumbo ni aula wenyewe kwa wenyewe, katika Kitabu cha Mwenyezi Mungu, kuliko waumini wengine na wahajiri. Ila muwe mnafanya wema kwa marafiki zenu. Hayo yamekwishaandikwa kitabuni.

وَإِذْ أَخَذْنَا مِنَ النَّبِيِّينَ مِيثَاقَهُمْ وَمِنكَ وَمِن نُّوحٍ وَإِبْرَاهِيمَ وَمُوسَىٰ وَعِيسَى ابْنِ مَرْيَمَ وَأَخَذْنَا مِنْهُم مِّيثَاقًا غَلِيظًا ﴿٧﴾

7. Na tulipochukua kwa manabii agano lao na kwako wewe na Nuh na Ibrahim na Isa mwana wa Maryam, na tulichukua kwao agano madhubuti.

لِّيَسْأَلَ الصَّادِقِينَ عَن صِدْقِهِمْ وَأَعَدَّ لِلْكَافِرِينَ عَذَابًا أَلِيمًا ﴿٨﴾

8. Ili awaulize wakweli juu ya ukweli wao. Na amewandaalia makafiri adhabu chungu.

NABII NI AULA KWA WAUMINI KULIKO NAFSI ZAO

Aya 6 – 8

MAANA

Je, Nabii Ni Hakimu Kwa Amri Yake? Nabii Ni Aula Kwa Waumini Kuliko Nafsi Zao.

Neno aula tumelifasiri kutokana na neno la kiarabu linalotamkwa hivyo hivyo awla lililonyumbuliwa kutokana na neno wilaya na walii, ambalo maana yake yanatofautiana kulingana na yule anayezungumziwa. Akizungumziwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) basi maana yake ni utawala na nguvu zisizoshindwa na yeyote. Akizungumziwa Nabii(s.a.w.w) inakuwa maana ni utiifu usiopingwa. Haya ndiyo maana yaliyokusudiwa hapa.

Sasa unaweza kuuliza: Si itakuwa maana yake ni kuwa Nabii ni hakimu na mtoa amri tu, mwengine hana uhuru. Tutalinganisha vipi hili na lile la msingi wa uhuru ambao ni haki ya kiasili ya kila mtu?

Jibu : Tutalinganisha uhuru wa mtu na utiifu wa Mwenyezi Mungu. Nabii(s.a.w. w ) anamsemea na kumbainishia Mwenyezi Mungu:

وَمَا يَنطِقُ عَنِ الْهَوَىٰ ﴿٣﴾ إِنْ هُوَ إِلَّا وَحْيٌ يُوحَىٰ ﴿٤﴾

“Hatamki kwa matamanio. Hayakuwa haya ila ni wahyi uliofunuliwa” 53 (3 – 4).

Kuna Hadith sahihi kutoka kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema:“Haamini mmoja wenu mpaka matamanio yake yafuate yale niliyokuja nayo.” Kwa hiyo kufuata na kutii ni aliyokuja nayo kutoka kwa Mwenyezi Mungu sio kutoka kwake.

Zaidi ya hayo uhuru ni kushikamana na njia ya usawa, kutumia haki na kubeba majukumu kwa utashi wake, huku akiipigania haki kwa nguvu zake zote. Lakini mwenye kuwa na msukumo wa mapendeleo bila ya kujali hisabu wala mchungaji, huyo ni mtumwa wa matamanio. Mwana falsafa mmoja mashuhuri alisema: “Uhuru sio kujifadhilisha kiundani kunakoruhusu tujifadhilishe sisi kuliko majukumu; isipokuwa ni uwezo wa kujenga mustakabali.”

Na wake zao ni mama zao.

Wake za mitume wana heshima na uharamu wa kuolewa baada yake sawa na mama, lakini kwenye mambo mengine ni watu kando kama wengine.

Na ndugu wa tumbo ni aula wenyewe kwa wenyewe, katika Kitabu cha Mwenyezi Mungu, kuliko waumini wengine na wahajiri.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 10 (9:75).

Ila muwe mnafanya wema kwa marafiki zenu

Makusudio ya wema hapa ni wasia, na marafiki wanakuwa ni pamoja na walioachwa huru au ndugu wasiorithi. Maana ni kuwa mirathi ni ya ndugu wa karibu wa maiti, lakini wasia ni wa aliyeusiwa awe wa mbali au wa karibu.

Hayo yamekwishaandikwa kitabuni.

Yaani hukumu imekwishathibiti Kitabuni mbele ya Mwenyezi Mungu na mwenye kuiasi atakuwa miongoni mwa walioangamia.

Na tulipochukua kwa manabii agano lao na kwako wewe na Nuh na Ibrahim na Isa mwana wa Maryam, na tulichukua kwao ahadi ngumu.

‘Kwako wewe,’ anaambiwa Muhammad(s.a.w. w ) . Makusudio ya agano ni kufikisha (Tabligh) risala ya Mwenyezi Mungu kwa ukamilifu wake na kuwa na subira na yatakayowapata katika njia yake. Amehusisha kutaja Nuh, Ibrahim, Musa, Isa na Muhammad, baada ya kuwataja manabii kwa ujumla kwa vile wao ni bora ya manabii wote, na ametangulizwa Muhammad kwa vile yeye ni mbora wao hao watano.

Katika Juz. 26 (46:35) wameashiriwa mitume Ulul-azmi (wenye ustahamilivu). Sababu ya kuitwa hivyo, kama zilivyopokewa baadhi ya riwaya, ni kuwa kila Nabii baada ya Nuh alikwa akifuata sharia ya Nuh, kisha sharia yake ikafutwa na sharia ya Ibrahim nayo ikafutwa na sharia ya Musa, nayo ikafutwa na Isa, kisha ikafutwa na ya Muhammad (s.a.w.) ambayo haitafutwa hadi Kiyama, kwa vile hakuna Nabii mwingine baada yake.

Na tulichukua kwao agano madhubuti.

Hili ndilo agano la kwanza, na amerudia kulitaja ili alisifu kuwa ni imara na lenye nguvu. Mwenyezi Mungu ameyapa sifa ya maagano madhibuti katika sehemu tatu katika Kitabu chake kitukufu:

Kwanza, ni agano la ndoa aliposema: “Na hali wao wamechukua kwenu agano madhubuti?” Juz. 4 (4:21). Pili ni agano alilochukua na wana wa Israil aliposema: “Na tukachukua kwao agano madhubuti.” Juz. 6 (4:154). Agano la tatu ni hili la Manbii tunalolizungumzia.

Sheikh Mahmud Shaltut, alighafilika kidogo pale aliposema: “Wasifu wa agano madhubuti haukuja katika sehemu yoyote ile katika sehemu zake – yaani Qur’an - isipokuwa katika kufunga ndoa.” Kutokosea ni kwa Mungu.

Ili awaulize wakweli juu ya ukweli wao.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) amewatuma Manabii na akachukua kwao agano la kufikisha ujumbe ili wakawaulize wakweli, walikusudia nini kwenye ukweli wao. Je, walikusudia radhi ya Mwenyezi Mungu au ni kwa ajili ya kuwaambia watu kuwa wao ni wakweli na mengineyo ya kibinafsi.

Imam Ja’far Sadiq(a.s) anasema: “Mwenyezi Mungu akimuuliza mtu kuhusu ukweli wake ni kwa njia gani aliusema, basi atamlipa kulingana nao, je vipi hali ya muongo?”

Na amewandalia makafiri adhabu chungu.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) alipowataja mitume sasa anawataja makafiri kwa mkabala wa kuwataja wema.

6

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA PILI

﴿الشَّهْرُ الْحَرَامُ بِالشَّهْرِ الْحَرَامِ وَالْحُرُمَاتُ قِصَاصٌ فَمَنِ اعْتَدَىٰ عَلَيْكُمْ فَاعْتَدُوا عَلَيْهِ بِمِثْلِ مَا اعْتَدَىٰ عَلَيْكُمْ وَاتَّقُوا اللَّـهَ وَاعْلَمُوا أَنَّ اللَّـهَ مَعَ الْمُتَّقِينَ ﴾

194.Mwezi mtakatifu kwa mwezi mtakatifu; na vitu vitakatifu vina kisasi. Basi wanaowachokoza, pia nanyi wachokozeni kwa kadiri walivyowachokoza. Na mcheni Mwenyezi Mungu na jueni kwamba Mwenyezi Mungu yuko pamoja na wanaomcha.

﴿وَأَنفِقُوا فِي سَبِيلِ اللَّـهِ وَلَا تُلْقُوا بِأَيْدِيكُمْ إِلَى التَّهْلُكَةِ وَأَحْسِنُوا إِنَّ اللَّـهَ يُحِبُّ الْمُحْسِنِينَ﴾

195.Na toeni katika njia ya Mwenyezi Mungu wala msijitie kwa mikono yenu katika maangamivu, na fanyeni wema. Hakika Mwenyezi Mungu huwapenda wafanyao wema.

MIEZI MITAKATIFU

Aya 194 - 195

MAANA

Mwezi mtakatifu kwa mwezi mtakatifu.

Miezi mitakatifu ni minne; mitatu inafuatana, nayo ni Dhul-Qaada, Dhul Hijja na Muharram (mfunguo pili, mfunguo tatu na mfunguo nne). Na mwezi mmoja uko pekee na ni (Rajab). Miezi hii imeitwa mitakatifu kwa sababu ya kuharamishwa kuuana ndani ya miezi hiyo. Katika wakati wa ujahiliya na wa Uislamu, ilikuwa mtu anaweza kukutana na mtu aliyemuua baba yake katika miezi hiyo na asimfanye chochote. Yameshatangulia maelezo kwamba Mtume na sahaba zake walitaka kufanya umra katika mwezi wa dhul-Qaada (mfunguo pili) mwaka wa sita (6 Hijriya), wakazuiwa na washirikina na wakatupiwa mishale na mawe; kisha waka-fanyiana suluhu kuwa Waislamu warudi mwaka utakaofutia. Lakini Waislamu wakaogopa washirikina wasije wakaanza kupigana katika mwezi mtakatifu; ndipo Mwenyezi Mungu akawapa idhini ya kupigana na washirikina na akabainisha kuwa lenye kukatazwa ni kuanza uadui wa kupigana na sio kujikinga. Kwa hivyo maana ya mwezi mtakatifu kwa mwezi mtakatifu ni kwamba mwenye kuihalalisha damu yenu enyi Waislamu katika mwezi huu, basi nanyi ihalalisheni damu yake katika mwezi huo huo.

Na vitu vitakatifu vina kisasi. Yaani mwenye kuvunja heshima ya Mwenyezi Mungu atalipizwa kisasi na atafanywa kama alivyofanya. Hiyo ndiyo asili kwa ujumla inayoondoa kila udhuru wa mwenye kuvunja heshima. Mwenye kuhalalilisha damu za watu, mali zao na heshima zao, naye atahalalishwa kwa kiasi kile alichowafanyia. Heshima kwa mtu mwingine inatokana na heshima ya Mwenyezi Mungu isipokuwa kama akivunja heshima ya mwingine. Hapo itakuja haki ambayo daima inakuwa juu na wala haikaliwi. Hapa ndipo tunapata tafsiri ya:

Anayechokoza pia nanyi mchokozeni kwa kadiri alivyo wachokoza. Sharti la kulipiza ni kuwa sawa na kosa la aliyeanza bila ya kuzidisha au kupunguza. Hicho ndio kisasi hasa kilivyo. Unaweza kuuliza: Mwenye kuchokoza , yeye ni mchokozi bila ya wasiwasi wowote, lakini mwenye kulipiza kisasi bila shaka siye mchokozi. Kwa hiyo kuna wajihi gani kwa Mwenyezi Mungu kusema:Mchokozeni

Jibu : Makusudio ya kuwafanyia uchokozi, sio uchokozi hasa kwa maana yake, isipokuwa makusudio ni malipo ya uchokozi uliofanywa kwa kipimo chake bila ya kudhulumu. Hayo ni mfano wa kauli yake Mwenyezi Mungu(s.w.t.):

"Na malipo ya ubaya ni ubaya ulio sawa na (ubaya) huo..." (42:40)

KUTOA KATIKA NJIA YA MWENYEZI MUNGU

Na toeni katika njia ya Mwenyezi Mungu. Kutoa katika njia yake Mwenyezi Mungu kunakuwa ni kwa masilahi ya umma; kama vile shule, hospitali na nyumba za kulea mayatima. Vile vile jihadi, sadaka kwa mafukara na masikini na kuwalisha watu wa nyumbani. Bora zaidi ya kutoa ni kule kunakohusika na kutia nguvu na kuieneza dini, kuthibitisha haki na kuibatilisha batili.

Wala msijitie, kwa mikono yenu, katika maangamivu

Mwenyezi Mungu ametumia neno mikono kwa maana ya mtu kujiingiza mwenyewe. Kama tukiangalia jumla hii peke yake tu bila ya kuangalia mfumo mzima wa maneno, ingelikuwa maana yake ni kuwa haijuzu kwa mtu kufanya lolote ambalo lina madhara na bila ya kuwako manufaa kwa ujumla. Lakini tukichunga mfumo wa maneno na kuja kauli yake Mwenyezi Mungu (s.w.t.):"wala msijitie kwa mikono yenu katika maangamivu" baada ya kusema:"Na toeni katika njia ya Mwenyezi Mungu", basi maana yanakuwa, toeni katika mali zenu sio kwa ubahili wala ubadhirifu, kwa sababu yote hayo mawili yanaleta uangamivu. Kwa hivyo Aya kwa maana haya inakuwa kama ile Aya isemayo:

﴿ وَالَّذِينَ إِذَا أَنفَقُوا لَمْ يُسْرِفُوا وَلَمْ يَقْتُرُوا وَكَانَ بَيْنَ ذَٰلِكَ قَوَامًا ﴾

"Na wale ambao wanapotoa hawafanyi ubadhirifu wala ubahili, bali wanakuwa katikati ya hayo."( 25:67)

Inasemekana pia kwamba maana yake ni: Msijitie kwa mikono yenu kwenye maangamivu kwa kuacha kupigana jihadi na maadui wa dini na kutoa mali kwa ajili ya kuwaandaa wapigania jihadi, kwa sababu hilo litawaogopesha na atawaweza adui; muangamie na mdhalilike. Haya ndiyo yaliyothibitishwa na majaribio waliyoyapitia Waislamu. Wamekosa uhuru wao na heshima yao tangu walipoacha jihadi na kutoa mali kwa ajili ya kuinusuru haki na uadilifu. Hivyo akapata tamaa kila mnyang'anyaji na mnyakuzi; hata Wazayuni, vibaraka wa ukoloni, nao waliivamia Palestina mnamo 1948. Baada ya Waarabu kunyamaza na wasifanye jihadi. Baada ya miaka ishirini wakateka Sinai na ukanda wa Gaza Magharibi mwa mto Jordan; wakazikalia sehemu hizo kwa msaada wa Amerika, Uingereza na Ujerumani Magharibi. Wakawaua wanaume na kuwafukuza wanawake na watoto. Lau Waislamu wangefanya jihadi kabla yake, wangeliokoka na maangamizo haya na udhalili huu, na wala dola ya Israel isingekuwepo kabisa.Na fanyeni wema Kwa jihadi na kujitolea mali katika njia ya Mwenyezi Mungu na katika kila njia inayomridhisha Mungu na yenye sifa nzuri.

﴿ وَأَتِمُّوا الْحَجَّ وَالْعُمْرَةَ لِلَّـهِ فَإِنْ أُحْصِرْتُمْ فَمَا اسْتَيْسَرَ مِنَ الْهَدْيِ وَلَا تَحْلِقُوا رُءُوسَكُمْ حَتَّىٰ يَبْلُغَ الْهَدْيُ مَحِلَّهُ فَمَن كَانَ مِنكُم مَّرِيضًا أَوْ بِهِ أَذًى مِّن رَّأْسِهِ فَفِدْيَةٌ مِّن صِيَامٍ أَوْ صَدَقَةٍ أَوْ نُسُكٍ فَإِذَا أَمِنتُمْ فَمَن تَمَتَّعَ بِالْعُمْرَةِ إِلَى الْحَجِّ فَمَا اسْتَيْسَرَ مِنَ الْهَدْيِ فَمَن لَّمْ يَجِدْ فَصِيَامُ ثَلَاثَةِ أَيَّامٍ فِي الْحَجِّ وَسَبْعَةٍ إِذَا رَجَعْتُمْ تِلْكَ عَشَرَةٌ كَامِلَةٌ ذَٰلِكَ لِمَن لَّمْ يَكُنْ أَهْلُهُ حَاضِرِي الْمَسْجِدِ الْحَرَامِ وَاتَّقُوا اللَّـهَ وَاعْلَمُوا أَنَّ اللَّـهَ شَدِيدُ الْعِقَابِ ﴾

196.Na timizeni Hijja na Umra kwa ajili ya Mwenyezi Mungu. Na kama mkizuiliwa, basi (chinjeni) wanyama walio wepesi kupatikana. Wala msinyoe vichwa vyenu mpaka wanyama hao wafike machinjioni mwao. Na ataka-yekuwa mgonjwa katika nyinyi au ana adha kichwani mwake, basi atoe fidia kwa kufunga au sadaka au kuchinja mnyama. Na mtakapokuwa salama, basi mwenye kujistarehesha kwa kufanya Umra, kisha akahiji, achinje mnyama aliye mwepesi kumpata. Na asiyepata, ni kufunga siku tatu katika Hijja na siku saba mtakaporudi; hizo ni siku kumi kamili. Hayo ni kwa yule ambaye watu wake hawako karibu na Msikiti Mtakatifu. Na mcheni Mungu na jueni kwamba Mwenyezi Mungu ni mkali wa kuadhibu.

﴿ الْحَجُّ أَشْهُرٌ مَّعْلُومَاتٌ فَمَن فَرَضَ فِيهِنَّ الْحَجَّ فَلَا رَفَثَ وَلَا فُسُوقَ وَلَا جِدَالَ فِي الْحَجِّ وَمَا تَفْعَلُوا مِنْ خَيْرٍ يَعْلَمْهُ اللَّـهُ وَتَزَوَّدُوا فَإِنَّ خَيْرَ الزَّادِ التَّقْوَىٰ وَاتَّقُونِ يَا أُولِي الْأَلْبَابِ﴾

197.Hijja ni miezi maalumu. Na anayejilazimisha kufanya Hijja katika miezi hiyo, basi hakuna kuchafua wala ufuska wala mabishano katika Hijja. Na heri yoyote mnayoifanya Mwenyezi Mungu anaijua. Na chukueni masurufu, na hakika masurufu bora ni takua; na nicheni Mimi, enyi wenye akili.

﴿ لَيْسَ عَلَيْكُمْ جُنَاحٌ أَن تَبْتَغُوا فَضْلًا مِّن رَّبِّكُمْ فَإِذَا أَفَضْتُم مِّنْ عَرَفَاتٍ فَاذْكُرُوا اللَّـهَ عِندَ الْمَشْعَرِ الْحَرَامِ وَاذْكُرُوهُ كَمَا هَدَاكُمْ وَإِن كُنتُم مِّن قَبْلِهِ لَمِنَ الضَّالِّينَ ﴾

198.Si vibaya kwenu kutafuta riziki ya Mola wenu. Na mtakapomiminika kutoka Arafa, mtajeni Mwenyezi Mungu katika Mash'aril- Haram: Na mkumbukeni kama alivyowaongoza, ijapokuwa zamani mlikuwa miongoni mwa waliopotea.

﴿ ثُمَّ أَفِيضُوا مِنْ حَيْثُ أَفَاضَ النَّاسُ وَاسْتَغْفِرُوا اللَّـهَ إِنَّ اللَّـهَ غَفُورٌ رَّحِيمٌ ﴾

199.Kisha miminikeni kutoka mahali wanapomiminika watu (wote), na mumwombe Mwenyezi Mungu maghufira; hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye kughufiria Mwenye kurehemu.

﴿ فَإِذَا قَضَيْتُم مَّنَاسِكَكُمْ فَاذْكُرُوا اللَّـهَ كَذِكْرِكُمْ آبَاءَكُمْ أَوْ أَشَدَّ ذِكْرًا فَمِنَ النَّاسِ مَن يَقُولُ رَبَّنَا آتِنَا فِي الدُّنْيَا وَمَا لَهُ فِي الْآخِرَةِ مِنْ خَلَاقٍ ﴾

200.Na mmalizapo kuzitimiza ibada zenu, basi mtajeni Mwenyezi Mungu kama mlivyokuwa mkiwataja baba zenu; bali mtajeni zaidi. Na kuna baadhi ya watu wasemao: Mola wetu! Tupe duniani; nao katika Akhera, hawana lolote.

﴿ وَمِنْهُم مَّن يَقُولُ رَبَّنَا آتِنَا فِي الدُّنْيَا حَسَنَةً وَفِي الْآخِرَةِ حَسَنَةً وَقِنَا عَذَابَ النَّارِ ﴾

201.Na miongoni mwao kuna asemaye; Mola wetu! Tupe mema duniani na (tupe) mema Akhera, na utulinde na adhabu ya Moto.

﴿ أُولَـٰئِكَ لَهُمْ نَصِيبٌ مِّمَّا كَسَبُوا وَاللَّـهُ سَرِيعُ الْحِسَابِ ﴾

202.Hao ndio wenye fungu katika waliyoyachuma, na Mwenyezi Mungu ni Mwepesi wa kuhisabu.

﴿ وَاذْكُرُوا اللَّـهَ فِي أَيَّامٍ مَّعْدُودَاتٍ فَمَن تَعَجَّلَ فِي يَوْمَيْنِ فَلَا إِثْمَ عَلَيْهِ وَمَن تَأَخَّرَ فَلَا إِثْمَ عَلَيْهِ لِمَنِ اتَّقَىٰ وَاتَّقُوا اللَّـهَ وَاعْلَمُوا أَنَّكُمْ إِلَيْهِ تُحْشَرُونَ﴾

203.Na mtajeni Mwenyezi Mungu katika siku zinazohisabiwa. Na mwenye kufanya haraka katika siku mbili, basi si dhambi juu yake; na mwenye kukawia pia si dhambi juu yake, kwa mwenye takua. Na mcheni Mwenyezi Mungu, na jueni kwamba nyinyi mtakusanywa Kwake.

TIMIZENI HIJJA NA UMRA

Aya 196 - 203

MAANA

Aya hizi zimeonyesha baadhi ya hukumu za Hijja, Mafaqihi wameweka vitabu maalumu vinavyohusu Hijja, nami nimetunga kitabu kwa jina Al- Hajj ala Madhahabil-Khamsa; kisha nikakiunganisha katika kitabu Al- Fiqh ala Madhahabil Khamsa wakati kiliporudiwa kuchapishwa kwa mara ya tatu. Vile vile nimeizungumza kwa urefu katika Juzuu ya pili ya kitabu Fiqh ul-Imam Jaffar Sadiq(a.s) Hijja imekuwa maarufu tangu zama za Nabii Ibrahim na Ismail(a.s) na iliendelea katika zama za ujahiliya; na Uislamu ukaithibitisha baada ya kuisafisha na mambo machafu, na kuongeza baadhi ya ibada.

Na timizeni Hijja na Umra kwa ajili ya Mwenyezi Mungu.

Maana ya Hijja kilugha, ni kukusudia, na kisharia ni ibada maalum katika mahali na wakati maalum. Umra kilugha ni ziara yoyote; na kisheria ni ziara katika Al-Kaaba kwa namna maalum, Hijja ni wajibu katika Quran, Hadith na Ijami. Bali wajibu wake umethubutu kwa dhahiri ya dini. Na mwenye kuikanusha sio Mwislamu, sawa sawa na aliyekanusha wajibu wa Saumu na Swala. Shia Imamiyya na Shafii wamesema Umra ni wajibu, Hanafi na Malik wamesema ni Sunna. Kusema kwake Mwenyezi Mungu Kwa ajili ya Mwenyezi Mungu Yaani Hijini na fanyeni Umra kwa ajili ya Mwenyezi Mungu peke yake na sio kwa makusudio ya kidunia. Kwani Waarabu walikuwa wakikusudia kuhiji kwa ajili ya kukutana, kujifaharisha, kutafuta mahitaji na kuhudhuria soko. Ndipo Mwenyezi Mungu akaamrisha Hijja iwe ni kwa makusudio yake Yeye kwa ibada safi yenye kutakasika na makusudio yoyote mengine.

Na kama mkizuiliwa, basi (chinjeni) wanyama walio wepesi kupatikana.

Yaani ikiwa mmeherimia Hijja, kisha mkazuilika kukamilisha ibada kwa njia yake ya kisheria kutokana na maradhi au adui na mengineyo, basi ni juu yenu kuchinja mnyama atakayepatikana kwa urahisi; kwa uchache awe ni mbuzi, wastani ni ng’ombe na wa juu zaidi ni ngamia.

Wala msinyoe vichwa vyenu mpaka wanyama hao wafike machinjioni mwao.

Msemo unaelekezwa kwa wale waliozuilika ambao hawakuweza kutimiza Hijja au Umra. Wao hawatakuwa wametoka katika ihram yao (miko ya Hijja) mpaka wajue kwamba mnyama amefika mahali pake pa kuchinjwa. Na mahali pa kuchinja ni Mina ikiwa ni Hijja; na kama ni Umra basi ni Makka. Hayo ni itakapokuwa kizuizi ni maradhi. Ama ikiwa kizuizi ni adui, basi mahali pa kuchinja ni pale mahali palipotokea kizuizi. Kwa sababu Mtume(s.a.w.w) alichinja mnyama katika Hudaybiya, alipozuiliwa na washirikina kuzuru nyumba ya Mwenyezi Mungu tukufu (Al Kaaba).

Na atakayekuwa mgonjwa katika nyinyi au ana adha kichwani mwake, basi atoe fidia kwa kufunga au sadaka au kuchinja mnyama.

Yaani ikiwa mwenye kuhirimia atanyoa kichwa chake kwa dharura, basi ni juu yake kutoa kafara, atakuwa na hiyari baina ya kufunga siku tatu, kuwalisha masikini sitini au kuchinja mnyama; kwa uchache awe ni mbuzi.

Na mtakapokuwa salama, basi mwenye kujistarehesha kwa kufanya Umra kisha akahiji, achinje mnyama aliyemwepesi kupatikana.

Yaani mtu asiyekuwa na kizuizi, akafanya Umra kisha akahiji baadae katika mwaka huo huo, basi ni juu yake kuchinja mnyama. Hii ndiyo aina ya Hijja inayojulikana kwa jina la Haj Tamattui (Hijja ya starehe) ambayo ni wajibu kwa wasiokuwa watu wa Makka.

Imeitwa Hijja ya starehe, kwa sababu mwenye kuhiji baada ya kumaliza amali za Umra anatoka kwenye miko ya Umra mpaka aje ahirimie Hijja.

Na asiyepata, ni kufunga siku tatu katika Hijja na siku saba mtakaporudi; hizo ni siku kumi kamili.

Imam Jaffar Sadiq(a.s) amesema;Mwenye kufanya Hajj Tamattu, asipopata mnyama atafunga siku tatu katika Hijja; siku ya saba, ya nane na ya tisa katika Dhul-Hijja (mfungu tatu) wala hakuna sharti la Iqama na siku saba atafunga atakaporudi kwa watu wake. Hizo ni siku kumi kamili za kutosheleza mnyama.

Hayo ni kwa yule ambaye watu wake hawako karibu na msikiti mtakatifu.

Mwenye Majmaul Bayan amesema kuwa hayo yaliyotangulia kutajwa katika Tamattui ya Umra kisha Hijja, sio kwa watu wa Makka na walio karibu yake. Isipokuwa ni kwa ambaye hayuko Makka, yule ambaye yuko mbali na Makka kwa zaidi ya maili kumi na mbili (12) kwa kila upande. Mafaqihi wa Kishia Imamiya wamesema Hajj Tamattui ni wajibu kwa walio mbali na Makka, wala haijuzu kwa aliyembali na Makka kuhiji Hijja Qiran na Ifrad, kwani hizo ni wajibu kwa watu wa Makka na wa kando kando yake; na wao haijuzu kwao kuhiji Hajj Tamattui. Kwa ufafanuzi zaidi angalia vitabu vya Fiqh.

Hijja ni miezi maalumu.

Nayo ni kuanzia Shawwal, Dhul-qaad na kumi la mwanzo la Dhul-Hijja. (mfunguo mosi, mfunguo pili na mfunguo tatu) Mwenye kuhirimia kabla yake Hijja yake haitaswihi na mwenye kuhirimia ndani ya miezi hiyo itaswihi na ataleta amali zilizobakia.

Na anayejilazimisha Hija katika miezi hiyo, basi hakuna kuchafua wala ufuska wala mabishano katika Hijja.

Makusudio ya uchafuzi hapa ni kujamii. Mtu akimjamii mkewe na huku amehirimia Hijja, basi Hijja yake imeharibika, sawa sawa na aliyejamii au kula huku akiwa amefunga. Kwa hiyo atakamilisha Hijja yake, kisha aje alipe mwaka ujao; kama ilivyo kwa mwenye kuiharibu Saumu. Makusudio ya ufuska, ni uongo na kutukana. Ama kuhusu kubishana riwaya za Ahlul Bait zinasema, hilo ni kusema mtu; Hapana wallahi au Kwa nini, wallahi n.k.

Si vibaya kwenu kutafuta riziki ya Mola wenu.

Kwa vile wakati wa ujahilia watu walikuwa wakifanya biashara na kuchuma siku za Hijja, kukadhaniwa kuwa ni haramu, ndipo Mwenyezi Mungu (s.w.t.), akaondoa tuhuma hii na akabainisha kwamba kuchuma hakupingani na ikhlasi katika amali za Hijja.

Na mtakapomiminika kutoka Arafa, mtajeni Mwenyezi Mungu katika Masharil Haram.

Arafa ni mahali maalum. Kumiminika kutoka Arafa ni kuondoka, Masharil-Haram ndipo pale panajulikana kama Muzdalifa na kutua hapo ni wajibu; kama ilivyo kwa Arafa.

Kisha miminikeni kutoka mahali wamiminikapo watu (wote). Inasemekana kuwa Maquraish walikuwa hawatui Arafa pamoja na watu wengine kwa kiburi tu, ndipo Mwenyezi Mungu akamwamrisha Mtume wake kutua hapo na kutoka pamoja na watu ili abatilishe waliyokuwa wakiyafanya Maquraish.

Na mmalizapo kuzitimiza ibada zenu, basi mtajeni Mwenyezi Mungu zaidi.

Imepokuwa kutoka kwa Imam Baqir baba wa Imam Sadiq(a.s) kwamba watu walikuwa wanapomaliza Hijja wanakusanyika huko na kuwataja wazazi wao kwa fahari, ndipo Mwenyezi Mungu akawaamrisha kuliacha hilo na badala yake wamtaje Mwenyezi Mungu na jinsi alivyowaneemesha. Kwa sababu Yeye ndiye mwenye kuwaneemesha wao na mababa zao.

Na baadhi ya watu kuna asemaye: Mola wetu! Tupe duniani; nao katika akhera hawana lolote. Na miongoni mwao kuna asemaye: Mola wetu! Tupe mema duniani na (tupe) mema akhera, na utulinde na adhabu ya moto. Hao ndio wenye fungu katika waliyoyachuma, na Mwenyezi Mungu ni mwepesi wa kuhisabu.

Watu katika Hijja zao wako aina mbili. Aina ya kwanza ni yule asiyetaka lolote isipokuwa starehe ya dunia na hana makusudio yoyote isipokuwa dunia tu, na anapomwabudu Mwenyezi Mungu humwabudu kwa ajili ya dunia. Hawa ndio wenye kunyimwa neema ya Akhera. Ama aina ya pili ni yule anayetaka heri ya dunia na akhera na anafanya amali kwa ajili ya dunia yake na akhera yake. Huyu ndiye mwenye radhi mbele ya Mwenyezi Mungu kesho kwa kulipwa amali yake njema. Mwenye Tafsiri Rawhul Bayan amenukuu kutoka kwa Imam Ali bin Abi Twalib(a.s) kwamba wema katika dunia ni mwanamke mwema na katika akhera ni Hurulain. Ama adhabu ya moto makusudio yake ni mwanamke muovu.

Iwe ni sahih Hadith hiyo au la, lakini mimi najua kuna watu wanaohisi kwamba lau wao wangekuwa katika Jahanam kisha wakahiyarishwa kutoka katika Jahanam na warudi kwa wake zao waliokuwa nao duniani au wabaki Jahannam, basi wangelichagua kubaki katika Jahannam kuliko kuishi tena na wake zao hao.

Na mtajeni Mwenyezi Mungu katika siku zinazohisabiwa.

Makusudio yake ni siku tatu za Tashriq nazo ni; Tarehe kumi na moja, kumi na mbili na kumi na tatu katika mwezi wa Dhul-Hijja (mfungo tatu). Si wajibu kwa mwenye kuhiji kulala Mina usiku wa kumi na tatu, lakini kwa sharti ya kuwa atoke Mina siku ya kumi na mbili baada ya kupinduka jua na kabla ya Maghrib na awe hakuvunja mwiko wa kuwinda au kujamii. Kwa hali hiyo ndipo tunapopata tafsiri ya kauli yake Mwenyezi Mungu:

Na mwenye kufanya haraka katika siku mbili, basi si dhambi juu yake; na mwenye kukawia pia si dhambi juu yake kwa mwenye takua.

Yaani mwenye kuacha kuwinda na wanawake katika ihram yake. Ikiwa amevunja mwiko wa kulala na mke au kuwinda au alichelewa na jua siku ya kumi na mbili akiwa yuko Mina, basi itakuwa wajibu kwake kulala usiku wa kumi na tatu na kutupia mawe vikuta vitatu (shetani).

7

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA PILI

﴿ وَمِنَ النَّاسِ مَن يُعْجِبُكَ قَوْلُهُ فِي الْحَيَاةِ الدُّنْيَا وَيُشْهِدُ اللَّـهَ عَلَىٰ مَا فِي قَلْبِهِ وَهُوَ أَلَدُّ الْخِصَامِ ﴾

204.Na katika watu kuna ambaye kauli yake inakupendeza katika maisha ya duniani, naye humshuhudiza Mwenyezi Mungu kwa yaliyo moyoni mwake na hali ni hasimu mkubwa kabisa.

﴿ وَإِذَا تَوَلَّىٰ سَعَىٰ فِي الْأَرْضِ لِيُفْسِدَ فِيهَا وَيُهْلِكَ الْحَرْثَ وَالنَّسْلَ وَاللَّـهُ لَا يُحِبُّ الْفَسَادَ﴾

205.Na anapotawala hufanya bidii katika ardhi kufanya ufisadi, na huangamiza mimea na viumbe, na Mwenyezi Mungu hapendi ufisadi.

﴿ وَإِذَا قِيلَ لَهُ اتَّقِ اللَّـهَ أَخَذَتْهُ الْعِزَّةُ بِالْإِثْمِ فَحَسْبُهُ جَهَنَّمُ وَلَبِئْسَ الْمِهَادُ ﴾

206.Na anapoambiwa. Mche Mwenyezi Mungu, hupandwa na mori wa kufanya dhambi. Basi Jahannam inamtosha, napo ni makao mabaya mno

﴿ وَمِنَ النَّاسِ مَن يَشْرِي نَفْسَهُ ابْتِغَاءَ مَرْضَاتِ اللَّـهِ وَاللَّـهُ رَءُوفٌ بِالْعِبَادِ ﴾

207.Na katika watu yuko auzaye nafsi yake kwa kutaka radhi ya Mwenyezi Mungu, na Mwenyezi Mungu ni mpole kwa waja.

KAULI ZAO ZINAKUPENDEZA

Aya 204 – 207

MAANA

Baadhi ya wafasiri wapya wamejaza kurasa kwa maneno matamu katika kufasiri Aya hizi, lakini hawakuzidisha chochote zaidi ya kuwagawanya watu kwenye wema na uovu. Kwa dhahiri haya yanajulikana na wote, hayahitaji ubainifu wowote, sikwambii tafsiri ndefu tena. Unaweza kuuliza; Ikiwa kugawanyika watu kunajulikana na wote, basi kubainisha kunakuwa ni maelezo ambayo tayari yameshaelezwa na kufafanua lililofafanuliwa na yapasa kuyachukulia maneno ya Mwenyezi Mungu (s.w.t.) vizuri? Jibu: Inawezekana kuwa makusudio ni kuongoza na kuelekeza kwamba mwenye akili anatakikana kutohadaliwa kwa mambo ya nje wala asimwamini mwenye kutegeneza maneno matamu. Kwa sababu wafisadi ni mabingwa wa kazi hiyo na kazi ya ria. Kwa hivyo ni juu yetu kutomtegemea yeyote isipokuwa baada ya kufanya majaribio na kupatikana dalili ya ukweli wake na usafi wake.

Hiyo ndiyo asili ya ujumla inayoenea katika hukumu nyingi za dini na za kidunia; kama kuchagua Hakimu, Kadhi, Naibu, Kadhi, Mufti na kila anayesimamia masilahi ya Umma. Ajabu ya maajabu ni kutakiwa shahada ya kielimu tu kwa mwenye kujitokeza kwa kazi muhimu ya mji au nchi na inayogusa maisha ya watu. Lakini haulizwi uaminifu wake na tabia yake, pamoja na kuwa hayo ndio msingi. Wengi wenye shahada wanazitumia kuwa ni zana za kuibia.

Na katika watu kuna ambaye kauli yake inakupendeza hapa duniani, naye humshuhudia Mwenyezi Mungu kwa yaliyomo moyoni mwake, na hali ni hasimu mkubwa kabisa.

Yaani wanadhihihirisha mapenzi na heri na hali wao ndio maadui zaidi wa heri na watu wa heri.

Na anapotawala hufanya bidii katika ardhi kufanya ufisadi.

Wamehitaliafiana wafasiri kuhusu neno Tawalla. Je makusudio ni kuondoka na maana yake kuwa ni, anapoondoka kwa yule aliyemdanganya, huhangaika katika ardhi kwa ufisadi. Au kwamba makusudio ni kutawala na usultani, na maana yawe, na atakapokuwa mtawala atafanya wanayoyafanya watawala waovu ya kuangamiza mimea na viumbe? Mwenye Tafsir Al manar amenakili kutoka kwa Ustadha wake Sheikh Muhammad Abduh kwamba ameyapa nguvu maana ya utawala kwa kuunganisha na kauli yake Mwenyezi Mungu (s.w.t.):

"Na anapoambiwa mche Mwenyezi Mungu, hupandwa na mori wa kufanya dhambi."

Kwa maana ya kuwa mtawala mkaidi anakuwa na kiburi kuongozwa kwenye maslahi au kupewa tahadhari ya mambo ya ufisadi, yeye hujiona yuko juu ya haki; kama vile alivyo juu ya watu wake anaowatawala, basi itawezekanaje kwa mtu kumwambia amwogope Mwenyezi Mungu.

Na huangamiza mimea na viumbe.

Mimea ni kilimo na viumbe ni wanyama. Makusudio ni maslahi yote ya kiuchumi katika kilimo, viwanda na ufugaji, mali ghafi, na mengineyo yanayohusika na uhai wa watu na maisha yao. Mwenyezi Mungu amehusisha kutaja kilimo na ufugaji kwa vile viwanda wakati huo havikuwa na umuhimu wowote kama ilivyo sasa. Uharamu wa mambo hayo kwa mtazamo wa Uislamu ni sawa na uharamu wa kumwaga damu; na mwenye kukusudia ubaya katika vitu hivyo, ndio amekusudia ubaya wa utu hasa; hata kama vitu hivyo ni milki ya adui anayepiga vita Waislamu. Mtume(s.a.w.w) amekataza kukata miti, kuharibu mimea na majengo na kutia sumu miji ya washirikina siku za vita, n.k. Lau tunailinganisha sharia ya Kiislamu na mambo yanayofanywa leo na dola za kikoloni na vita vyao vya silaha za kemikali kwenye mimea, watu na wanyama, na kuitia sumu anga kwa mabomu ya Atomic na kuyatupa kwa wanawake na watoto, lau hayo yote tunayaunganisha na Uislamu, basi tutajua huruma, uadilifu na utu wa Uislamu na unyama wa dola za Magharibi na jinsi zilivyopetuka mipaka katika dhulma na unyang'anyi.

Na Mwenyezi Mungu (s.w.t.) hapendi ufisadi.

Hakuna uharibifu mkubwa zaidi kuliko kuzusha vita na kutumia silaha zenye kubomoa ili kuwatawala watu na kuwanyang'anya chakula na matunda ya jasho lao.

Na anapoambiwa mche Mwenyezi Mungu hupandwa na mori wa kufanya dhambi.

Mtu mwema wenye ikhlasi anakubali masahihisho na nasaha, bali huzitafuta na kuzikaribisha, kwa sababu yeye hana lengo jengine zaidi ya haki, wala hatafuti sifa; kwa sababu amali yake ni kwa ajili ya Mwenyezi Mungu (s.w.t.) sio umashuhuri.

Imam Amirul Muminin(a.s) anasema katika maneno anayowasifu wanaomcha Mwenyezi Mungu:"Hawaridhii na amali zao chache wala hawakioni kingi kilicho kingi; wao wanajituhumu na wao ni wenye kunyenyekea katika amali zao."

Katika hotuba yake siku za ukhalifa wake alisema: "Mtu hata kama ana cheo kikubwa katika haki na fadhila kubwa katika dini hawezi kuwa hahitajii kusaidiwa katika aliyobebeshwa na Mungu katika haki zake; wala si mwenye kutaka kujitukuza; wala mtu hata kama nafsi zinamfanya mdogo na kudharauliwa na macho sio kuwa hawezi kusaidia au kusaidiwa... Wala msinidhanie kuwa mimi ni mzito katika haki nitakayoambiwa, kwani mwenye kuifanya nzito haki atakayoambiwa au uadilifu atakaoonyeshwa, basi kwake kuitumia haki na uadilifu ni kuzito zaidi."

Hivyo ndivyo anavyotakikana mwanachuoni mwenye ikhlasi ya kweli. Ama mnafiki mwenye hiana, haki inakuwa nzito juu yake kwa sababu itamfedhehesha; na hununua sifa kwa thamani kubwa ili azibe upungufu wake na uovu wake.

Na katika watu yuko auzaye nafsi yake kutaka radhi ya Mwenyezi Mungu.

Yaani baadhi ya waumini wanaikabili Jihadi na wanapenda mauti kwa ajili ya Mwenyezi Mungu. sawa na wale wengine wanaopenda uhai. Hawana lengo jengine isipokuwa kutaka radhi ya Mwenyezi Mungu na thawabu Zake. Razi katika kutafsiri Aya hii anasema kuhusu sababu za kushuka kwake kuwa kuna riwaya tatu; Mojawapo ni kwamba Aya hii imeshuka kwa sababu ya Ali bin Abi Twalib(a.s) alipolala kwenye kitanda cha Mtume wakati wa Hijra, alisimama Jibril kichwani mwake, Mikail miguuni mwake na Jibril: Pongezi! Pongezi! ewe Ali akisema: Mwenyezi Mungu anajionea fahari kwako, mbele ya Malalika( [7] ).

﴿ يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا ادْخُلُوا فِي السِّلْمِ كَافَّةً وَلَا تَتَّبِعُوا خُطُوَاتِ الشَّيْطَانِ إِنَّهُ لَكُمْ عَدُوٌّ مُّبِينٌ﴾

208.Enyi mlioamini! Ingieni katika usalama nyote, wala msifuate nyayo za Shetani. Kwa hakika yeye kwenu ni adui wa wazi.

﴿ فَإِن زَلَلْتُم مِّن بَعْدِ مَا جَاءَتْكُمُ الْبَيِّنَاتُ فَاعْلَمُوا أَنَّ اللَّـهَ عَزِيزٌ حَكِيمٌ ﴾

209.Na kama mkiteleza baada ya kuwafikia ubainifu, basi jueni kwamba Mwenyezi Mungu ni Mwenye nguvu, Mwenye hekima.

﴿ هَلْ يَنظُرُونَ إِلَّا أَن يَأْتِيَهُمُ اللَّـهُ فِي ظُلَلٍ مِّنَ الْغَمَامِ وَالْمَلَائِكَةُ وَقُضِيَ الْأَمْرُ وَإِلَى اللَّـهِ تُرْجَعُ الْأُمُورُ ﴾

210.Hawangoji ila kuwafikia (adhabu ya) Mwenyezi Mungu katika vivuli vya mawingu na Malaika, na liishe jambo; na mambo yote hurudishwa kwa Mwenyezi Mungu.

INGIENI KATIKA USALAMA NYOTE

Aya 208 - 210

MAANA

Enyi Mlioamini! Ingieni katika usalama nyote.

Imesemekana kuwa makusudio ya neno Silmi hapa ni Uislamu, na kwamba msemo unawaelekea wanafiki ambao wameificha kufuru na kudhihirisha Uislamu. Na imesemekana kuwa msemo unawaelekea wenye kumwamini Mwenyezi Mungu katika Ahlul Kitab ambao hawakusilimu. Na ikasemekana kuwa unawaelekea Waislamu wote kwa hivyo maana yake yanakuwa ni kumtii Mwenyezi Mungu na kumnyenyekea katika hukumu Zake zote sio baadhi. Na pia imesemekana maana yake ni suluhu kwa maana kuwa ingieni katika suluhu nyote. Tuonavyo sisi ni kwamba Mwenyezi Mungu (s.w.t.) amemwamrisha mwenye kumwamini Mwenyezi Mungu, kwa imani sahihi kuingia katika lile ambalo lina salama yake ya dunia na akhera. Na njia ya usalama inajulikana na wote, nayo ni kusaidiana, kuungana, na kuacha vita na uhasama. Vile vile kuyashinda matamanio na kuwa na ikhlasi katika kauli na vitendo.

Makusudio ya maneno hayo yanatiliwa nguvu na kauli yake Mwenyezi Mungu:Wala msifuate nyayo za shetani. Kwa hakika yeye kwenu ni adui wa wazi, Aliyoileta mara tu, baada ya kusema.Ingieni katika usalama nyote. Hapo Mwenyezi Mungu amezingatia kuwa nyayo za shetani kinyume chake ni usalama; na amemweka mtu mbele ya mambo mawili tu, hakuna la tatu; Ama kuingia katika usalama au kufuata nyayo za shetani ambazo ndio dhati ya uovu, ugomvi, shari na ufisadi.

Na kama mkiteleza baada ya kuwafikia ubainifu, basi jueni ya kwamba Mwenyezi Mungu ni Mwenye nguvu Mwenye hekima.

Baada ya Mwenyezi Mungu kuamrisha kuingia katika usalama na kukataza kufuatwa nyayo za shetani, amemhadharisha yule atakayehalifu amri yake na makatazo yake na akatishia kwa kusema: "Basi jueni kwamba Mwenyezi Mungu ni Mwenye nguvu Mwenye hekima." Mwenye nguvu, hashindwi katika amri Yake wala hakimzuwii chochote kwa alilokusudia kulifanya. Mwenye hekima, humlipa mema mtiifu na humwadhibu mwasi. Razi anasema: "Huo ndio ukomo wa kiaga kwa sababu ni kuhofisha bila ya kutaja adhabu. Huenda mzazi akamwambia mtoto wake: "Ukiniasi basi wewe wanijua na wajua uwezo wangu kwako", basi maneno hayo yanakuwa ni makemeo ya ufasaha zaidi kuliko kutaja kipigo na mengineyo.

Hawangoji ila kuwafikia (adhabu ya) Mwenyezi Mungu katika vivuli vya mawingu na Malaika. Maana kwa ujumla ni kwamba wale wenye kukadhibisha na wakaasi watajiwa na adhabu kwa ghafla wala hawataokoka. Aya iko katika mwelekeo wa Aya inayosema:

﴿ فَهَلْ يَنظُرُونَ إِلَّا السَّاعَةَ أَن تَأْتِيَهُم بَغْتَةً ﴾

"Na hawangoji ila saa ya Kiyama kiwajie kwa ghafla...?" (47:18).

Na lishe jambo; na mambo yote hurudishwa kwa Mwenyezi Mungu. Mauti ambayo hapana budi nayo, yakija na Kiyama kikija, kila kitu kitakuwa kimekwisha na hapatabakia mbele ya wenye makosa isipokuwa hisabu na mateso.

SIRI NA MATUKIO YA GHAFLA

Hakuna yeyote ajuaye yatakayomtokea mbele na siri ya wakati, heri au shari. Hawezi kuyajua hayo vyovyote atakavyokuwa na elimu au imani:

"Na nafsi yoyote haijui itachuma nini kesho." (31:34)

Mara nyingi mtu hujiwa na heri kwa ghafla wakati yeye anatazamia kupata shari; na hujiwa ghafla na shari wakati anapotazamia heri. Hakuna kitu kinachotia uchungu kama hicho cha kupata shari wakati wa kutazamia heri; kama vile ambavyo hakuna kitu kitamu kama kupata heri wakati wa kutazamia shari. Mwenye akili hawezi kughurika na alivyo navyo, bali hufikiria mzunguko wa zama; kama vile ambavyo hakati tamaa na lolote linalompata; kwani dunia inageuka milele; ndio maana ikasemwa; "Kudumu hali ni muhali na faraja inakuja kutokana na dhiki." Imam Ali(a.s) anasema:"Baada ya dhiki ni faraja. Anaendelea kusema Imam:"Hakika Musa bin Imran alitoka kuwatafutia watu wake moto akasemeshwa na Mwenyezi Mungu na akarudi akiwa Mtume." Mwenyezi Mungu anasema:

﴿ إِنَّهُ لَا يَيْأَسُ مِن رَّوْحِ اللَّـهِ إِلَّا الْقَوْمُ الْكَافِرُونَ ﴾

"...Hawakati tamaa ya rehema ya Mwenyezi Mungu isipokuwa watu makafiri." (12:87).

Na amesema tena:

﴿ فَلَا يَأْمَنُ مَكْرَ اللَّـهِ إِلَّا الْقَوْمُ الْخَاسِرُونَ ﴾

... Hawajiaminishi na mipango ya Mwenyezi Mungu ila watu wenye hasara." (7:99).

Imeelezwa katika vitabu vya Historia na Sera kwamba Ibn Ziyat alikuwa waziri na mtu wa kutegemewa na Mu'utasim, naye alikuwa ni katika mataghuti wa hali ya juu na dhalimu mkubwa. Alitengeneza tanuri la chuma alilolijaza misumari yenye ncha pambizoni mwake. Anapomkasirikia mtu humtupa ndani, kila anavyojitingisha ndivyo misumari inavyomwingia mwilini mwake. Mutawakkil alipotawala alimshika Ibn Ziyat na akamfunga kwa chuma mikononi mwake na miguuni mwake kisha akamtupa katika tanuri hilo, na baadaye akafa. Kabla ya kufa alisikika akiimba shairi hili: Sifazake tulia, hebu nenda pole pole, Kigeugeu dunia, huenda nyuma na mbele.

﴿ سَلْ بَنِي إِسْرَائِيلَ كَمْ آتَيْنَاهُم مِّنْ آيَةٍ بَيِّنَةٍ وَمَن يُبَدِّلْ نِعْمَةَ اللَّـهِ مِن بَعْدِ مَا جَاءَتْهُ فَإِنَّ اللَّـهَ شَدِيدُ الْعِقَابِ﴾

211.Waulize wana wa Israil, ishara ngapi zilizo wazi tulizowapa? Na anayezibadilisha neema za Mwenyezi Mungu baada ya kumfikia, basi hakika Mwenyezi Mungu ni Mkali wa kuadhibu.

﴿ زُيِّنَ لِلَّذِينَ كَفَرُوا الْحَيَاةُ الدُّنْيَا وَيَسْخَرُونَ مِنَ الَّذِينَ آمَنُوا وَالَّذِينَ اتَّقَوْا فَوْقَهُمْ يَوْمَ الْقِيَامَةِ وَاللَّـهُ يَرْزُقُ مَن يَشَاءُ بِغَيْرِ حِسَابٍ ﴾

212.Wamepambiwa makafiri maisha ya duniani, na wanawafanyia maskhara wale walioamini. Na wale wenye takua watakuwa juu yao Siku ya Kiyama. Na Mwenyezi Mungu humruzuku amtakaye bila hisabu

WAULIZE WANAWA ISRAIL

Aya 211 – 212

MAANA

Waulize wana wa Israil, ishara ngapi zilizo wazi tulizowapa?

Makusudio ya waulize hapa sio swali hasa la kihakika, kwa sababu Mtume(s.a.w.w) anajua hali zao, wala makusudio sio kuelezea hali waliyokuwa nayo; kama ilivyo katika Aya ya 49 na inayofuatia. Isipokuwa makusudio hasa ni kuwa Waislamu wazingatie na wapate funzo na hali ya Waisrail. Njia ya kupata funzo ni kuwa Waisrail walijiwa na Mtume Musa(a.s) kwa miujiza na hoja ambayo ni mkono kuwa mweupe, fimbo kugeuka nyoka na kupasuka bahari. Vile vile kufunikwa na wingu, kuteremshiwa Manna na Salwa na jabali kutoka maji. Pamoja na hayo yote waliasi na kukhalifu, ndipo Mwenyezi Mungu akawaadhibu kwa madhila na utwevu katika dunia na adhabu iumizayo katika Akhera. Na Waislamu nao wamejiwa na Muhammad(s.a.w.w) kwa miujiza na hoja zinazofahamisha ukweli wa Utume wake na kuswihi sharia yake; naye akawafikilizia habari kutoka kwa Mwenyezi Mungu kuwa waaingie katika Uislamu wote, kwani humo watapata heri na utengeneo wao; kama wakiasi kama walivyofanya Waisrail, basi yatawapata yaliyowapata Waisrail.

Na anayezibadilisha neema za Mwenyezi Mungu baada ya kumfikia, basi hakika Mwenyezi Mungu ni mkali wa kuadhibu.

Makusudio ya neema hapa ni dalili za haki, kwani hizo ni katika neema kubwa. Kwa sababu ndani yake mna uongofu na kuokoka na kuhiliki na upotevu. Makusudio ya kuzibadilisha ni kuziasi na kuziharibu. Kwa hiyo kauli yake Mwenyezi Mungu (s.w.t.)Na anayezibadilisha neema za Mwenyezi Mungu baada ya kumfikia ni sawa na kauli yake:

﴿ فَإِن زَلَلْتُم مِّن بَعْدِ مَا جَاءَتْكُمُ الْبَيِّنَاتُ﴾

"Na kama mkiteleza baada ya kuwafikia ubainifu..." (2:209).

Vile vile kusema kwake:

﴿فَاعْلَمُوا أَنَّ اللَّـهَ عَزِيزٌ حَكِيمٌ ﴾

"Basi hakika Mwenyezi Mungu ni mkali wa kuadhibu" (2:209) ni sawa na kusema Kwamba:Mwenyezi Mungu ni Mwenye nguvu Mwenye hekima."

Maana ni moja na lengo ni moja.

HAPANA IMANI BILA TAKUA (UCHA MUNGU)

Wamepambiwa makafiri maisha ya duniani.

Hapana tofauti kati ya mwenye kukanusha kuwapo Mwenyezi Mungu na yule mwenye kuamini kinadharia tu, lakini matendo yakawa ni tofauti. Hapana tofauti kati ya wawili hao. Kwa sababu kila mmoja ameathiriwa na dunia na vipambo vyake, ameathirika na kitu cha sasa hivi kuliko cha muda ujao; heri na manufaa ameyapima kwa kiwango cha manufaa yake, wala hakupima na mambo aliyoharamisha Mwenyezi Mungu wala na msimamo wa kibinadamu. Mimi kila ninavyozidi kuzama katika tafsiri ya Qur'an na kuangalia kwa undani Aya zake, basi huwa na yakini zaidi kwamba imani bila ya ucha Mungu haina maana yoyote; na kwamba kila anayeiangalia dunia kuwa ndio makusudio yake yote, basi atakuwa ameiweka mbali sharia ya haki na dini, atake asitake.

Imekuja Hadith Mutawatir kutoka kwa Mtume Mtukufu akisema: "Dunia na akhera zina madhara" yaani zinadhuriana kuhujumu moja yao nikuiacha nyingine( [8] ).

Imam Ali(a.s) anasema: "Hakika dunia na Akhera ni maadui wawili wanaotofautiana, na ni njia mbili tofauti. Mwenye kuipenda dunia ataichukia akhera na kuwa adui yake; zote mbili ni kama Mashariki na Magharibi, mwenye kutembea kati yao huwa mbali na nyingine kila anapokaribia moja wapo.

" Na wanawafanyia maskhara wale walioamini.

Ni kawaida wale wanaozichezea Hoja za Mwenyezi Mungu na hukumu zake wakihalalisha damu na mali ya haramu kuwadharau na kuwachezea wale wanaojilinda na maharamisho na kuvumilia tabu na mashaka kwa ajili ya kumridhisha Mungu.

Na wale wenye takua watakuwa juu yao siku ya Kiyama.

Amesema wenye takua wala hakusema wale walioamini, kwa sababu imani bila takua si lolote; kama tulivyobainisha. Maana yako wazi ni kuwa makafiri wakiwadharau waumini hivi sasa, basi mambo yatabadilika kesho. Mwenyezi Mungu anasema:

﴿قَالَ الَّذِينَ أُوتُوا الْعِلْمَ إِنَّ الْخِزْيَ الْيَوْمَ وَالسُّوءَ عَلَى الْكَافِرِينَ ﴾

"...Watasema walio pewa ilimu: Hakika hizaya na ubaya leo itawafika makafiri." (16:27).

﴿فَالْيَوْمَ الَّذِينَ آمَنُوا مِنَ الْكُفَّارِ يَضْحَكُونَ ﴾

"Basi leo wale ambao wameamini wanawacheka makafiri." (83:34)

Na Mwenyezi Mungu humruzuku amtakaye bila hisabu.

Riziki ni mbili ya dunia na riziki ya Akhera. Riziki ya dunia inajulikana na riziki ya Akhera, ni neema isiyokatika na isiyokuwa na chembe ya huzuni au hofu. hataipata yeyote isipokuwa kwa imani na amali njema: Anasema Mwenyezi Mungu:

﴿وَالَّذِينَ آمَنُوا وَعَمِلُوا الصَّالِحَاتِ أُولَـٰئِكَ أَصْحَابُ الْجَنَّةِ هُمْ فِيهَا خَالِدُونَ ﴾

"Na wale walioamini na kutenda mema, hao ndio watu wa Peponi, humo watakaa milele." (2:82).

Kila mtu anaweza kupata riziki duniani, awe ni kafiri au Mumin, mwema au mwovu, na anayehangaika au asiyehan-gaika; kama vile urithi, zawadi, wasiya, n.k. Vile vile inaweza kupatikana kwa njia ya halali, au haramu, kama vile kunyang'anya, kughushi na utapeli. Mwenye Tafsir Al-Manar amenakili kutoka kwa mwalimu wake Sheikh Muhammad Abduh kwamba, amesema wakati wa kutafsiri Aya hii, kwamba riziki bila ya kuhangaika inaweza ikapatikana kwa baadhi ya watu. Ama kwa Umma ni muhali kujitosheleza isipoku-wa kwa kuhangaika na kufanya kazi. Huo ni ukweli ulio wazi kabisa.

6

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA PILI

﴿الشَّهْرُ الْحَرَامُ بِالشَّهْرِ الْحَرَامِ وَالْحُرُمَاتُ قِصَاصٌ فَمَنِ اعْتَدَىٰ عَلَيْكُمْ فَاعْتَدُوا عَلَيْهِ بِمِثْلِ مَا اعْتَدَىٰ عَلَيْكُمْ وَاتَّقُوا اللَّـهَ وَاعْلَمُوا أَنَّ اللَّـهَ مَعَ الْمُتَّقِينَ ﴾

194.Mwezi mtakatifu kwa mwezi mtakatifu; na vitu vitakatifu vina kisasi. Basi wanaowachokoza, pia nanyi wachokozeni kwa kadiri walivyowachokoza. Na mcheni Mwenyezi Mungu na jueni kwamba Mwenyezi Mungu yuko pamoja na wanaomcha.

﴿وَأَنفِقُوا فِي سَبِيلِ اللَّـهِ وَلَا تُلْقُوا بِأَيْدِيكُمْ إِلَى التَّهْلُكَةِ وَأَحْسِنُوا إِنَّ اللَّـهَ يُحِبُّ الْمُحْسِنِينَ﴾

195.Na toeni katika njia ya Mwenyezi Mungu wala msijitie kwa mikono yenu katika maangamivu, na fanyeni wema. Hakika Mwenyezi Mungu huwapenda wafanyao wema.

MIEZI MITAKATIFU

Aya 194 - 195

MAANA

Mwezi mtakatifu kwa mwezi mtakatifu.

Miezi mitakatifu ni minne; mitatu inafuatana, nayo ni Dhul-Qaada, Dhul Hijja na Muharram (mfunguo pili, mfunguo tatu na mfunguo nne). Na mwezi mmoja uko pekee na ni (Rajab). Miezi hii imeitwa mitakatifu kwa sababu ya kuharamishwa kuuana ndani ya miezi hiyo. Katika wakati wa ujahiliya na wa Uislamu, ilikuwa mtu anaweza kukutana na mtu aliyemuua baba yake katika miezi hiyo na asimfanye chochote. Yameshatangulia maelezo kwamba Mtume na sahaba zake walitaka kufanya umra katika mwezi wa dhul-Qaada (mfunguo pili) mwaka wa sita (6 Hijriya), wakazuiwa na washirikina na wakatupiwa mishale na mawe; kisha waka-fanyiana suluhu kuwa Waislamu warudi mwaka utakaofutia. Lakini Waislamu wakaogopa washirikina wasije wakaanza kupigana katika mwezi mtakatifu; ndipo Mwenyezi Mungu akawapa idhini ya kupigana na washirikina na akabainisha kuwa lenye kukatazwa ni kuanza uadui wa kupigana na sio kujikinga. Kwa hivyo maana ya mwezi mtakatifu kwa mwezi mtakatifu ni kwamba mwenye kuihalalisha damu yenu enyi Waislamu katika mwezi huu, basi nanyi ihalalisheni damu yake katika mwezi huo huo.

Na vitu vitakatifu vina kisasi. Yaani mwenye kuvunja heshima ya Mwenyezi Mungu atalipizwa kisasi na atafanywa kama alivyofanya. Hiyo ndiyo asili kwa ujumla inayoondoa kila udhuru wa mwenye kuvunja heshima. Mwenye kuhalalilisha damu za watu, mali zao na heshima zao, naye atahalalishwa kwa kiasi kile alichowafanyia. Heshima kwa mtu mwingine inatokana na heshima ya Mwenyezi Mungu isipokuwa kama akivunja heshima ya mwingine. Hapo itakuja haki ambayo daima inakuwa juu na wala haikaliwi. Hapa ndipo tunapata tafsiri ya:

Anayechokoza pia nanyi mchokozeni kwa kadiri alivyo wachokoza. Sharti la kulipiza ni kuwa sawa na kosa la aliyeanza bila ya kuzidisha au kupunguza. Hicho ndio kisasi hasa kilivyo. Unaweza kuuliza: Mwenye kuchokoza , yeye ni mchokozi bila ya wasiwasi wowote, lakini mwenye kulipiza kisasi bila shaka siye mchokozi. Kwa hiyo kuna wajihi gani kwa Mwenyezi Mungu kusema:Mchokozeni

Jibu : Makusudio ya kuwafanyia uchokozi, sio uchokozi hasa kwa maana yake, isipokuwa makusudio ni malipo ya uchokozi uliofanywa kwa kipimo chake bila ya kudhulumu. Hayo ni mfano wa kauli yake Mwenyezi Mungu(s.w.t.):

"Na malipo ya ubaya ni ubaya ulio sawa na (ubaya) huo..." (42:40)

KUTOA KATIKA NJIA YA MWENYEZI MUNGU

Na toeni katika njia ya Mwenyezi Mungu. Kutoa katika njia yake Mwenyezi Mungu kunakuwa ni kwa masilahi ya umma; kama vile shule, hospitali na nyumba za kulea mayatima. Vile vile jihadi, sadaka kwa mafukara na masikini na kuwalisha watu wa nyumbani. Bora zaidi ya kutoa ni kule kunakohusika na kutia nguvu na kuieneza dini, kuthibitisha haki na kuibatilisha batili.

Wala msijitie, kwa mikono yenu, katika maangamivu

Mwenyezi Mungu ametumia neno mikono kwa maana ya mtu kujiingiza mwenyewe. Kama tukiangalia jumla hii peke yake tu bila ya kuangalia mfumo mzima wa maneno, ingelikuwa maana yake ni kuwa haijuzu kwa mtu kufanya lolote ambalo lina madhara na bila ya kuwako manufaa kwa ujumla. Lakini tukichunga mfumo wa maneno na kuja kauli yake Mwenyezi Mungu (s.w.t.):"wala msijitie kwa mikono yenu katika maangamivu" baada ya kusema:"Na toeni katika njia ya Mwenyezi Mungu", basi maana yanakuwa, toeni katika mali zenu sio kwa ubahili wala ubadhirifu, kwa sababu yote hayo mawili yanaleta uangamivu. Kwa hivyo Aya kwa maana haya inakuwa kama ile Aya isemayo:

﴿ وَالَّذِينَ إِذَا أَنفَقُوا لَمْ يُسْرِفُوا وَلَمْ يَقْتُرُوا وَكَانَ بَيْنَ ذَٰلِكَ قَوَامًا ﴾

"Na wale ambao wanapotoa hawafanyi ubadhirifu wala ubahili, bali wanakuwa katikati ya hayo."( 25:67)

Inasemekana pia kwamba maana yake ni: Msijitie kwa mikono yenu kwenye maangamivu kwa kuacha kupigana jihadi na maadui wa dini na kutoa mali kwa ajili ya kuwaandaa wapigania jihadi, kwa sababu hilo litawaogopesha na atawaweza adui; muangamie na mdhalilike. Haya ndiyo yaliyothibitishwa na majaribio waliyoyapitia Waislamu. Wamekosa uhuru wao na heshima yao tangu walipoacha jihadi na kutoa mali kwa ajili ya kuinusuru haki na uadilifu. Hivyo akapata tamaa kila mnyang'anyaji na mnyakuzi; hata Wazayuni, vibaraka wa ukoloni, nao waliivamia Palestina mnamo 1948. Baada ya Waarabu kunyamaza na wasifanye jihadi. Baada ya miaka ishirini wakateka Sinai na ukanda wa Gaza Magharibi mwa mto Jordan; wakazikalia sehemu hizo kwa msaada wa Amerika, Uingereza na Ujerumani Magharibi. Wakawaua wanaume na kuwafukuza wanawake na watoto. Lau Waislamu wangefanya jihadi kabla yake, wangeliokoka na maangamizo haya na udhalili huu, na wala dola ya Israel isingekuwepo kabisa.Na fanyeni wema Kwa jihadi na kujitolea mali katika njia ya Mwenyezi Mungu na katika kila njia inayomridhisha Mungu na yenye sifa nzuri.

﴿ وَأَتِمُّوا الْحَجَّ وَالْعُمْرَةَ لِلَّـهِ فَإِنْ أُحْصِرْتُمْ فَمَا اسْتَيْسَرَ مِنَ الْهَدْيِ وَلَا تَحْلِقُوا رُءُوسَكُمْ حَتَّىٰ يَبْلُغَ الْهَدْيُ مَحِلَّهُ فَمَن كَانَ مِنكُم مَّرِيضًا أَوْ بِهِ أَذًى مِّن رَّأْسِهِ فَفِدْيَةٌ مِّن صِيَامٍ أَوْ صَدَقَةٍ أَوْ نُسُكٍ فَإِذَا أَمِنتُمْ فَمَن تَمَتَّعَ بِالْعُمْرَةِ إِلَى الْحَجِّ فَمَا اسْتَيْسَرَ مِنَ الْهَدْيِ فَمَن لَّمْ يَجِدْ فَصِيَامُ ثَلَاثَةِ أَيَّامٍ فِي الْحَجِّ وَسَبْعَةٍ إِذَا رَجَعْتُمْ تِلْكَ عَشَرَةٌ كَامِلَةٌ ذَٰلِكَ لِمَن لَّمْ يَكُنْ أَهْلُهُ حَاضِرِي الْمَسْجِدِ الْحَرَامِ وَاتَّقُوا اللَّـهَ وَاعْلَمُوا أَنَّ اللَّـهَ شَدِيدُ الْعِقَابِ ﴾

196.Na timizeni Hijja na Umra kwa ajili ya Mwenyezi Mungu. Na kama mkizuiliwa, basi (chinjeni) wanyama walio wepesi kupatikana. Wala msinyoe vichwa vyenu mpaka wanyama hao wafike machinjioni mwao. Na ataka-yekuwa mgonjwa katika nyinyi au ana adha kichwani mwake, basi atoe fidia kwa kufunga au sadaka au kuchinja mnyama. Na mtakapokuwa salama, basi mwenye kujistarehesha kwa kufanya Umra, kisha akahiji, achinje mnyama aliye mwepesi kumpata. Na asiyepata, ni kufunga siku tatu katika Hijja na siku saba mtakaporudi; hizo ni siku kumi kamili. Hayo ni kwa yule ambaye watu wake hawako karibu na Msikiti Mtakatifu. Na mcheni Mungu na jueni kwamba Mwenyezi Mungu ni mkali wa kuadhibu.

﴿ الْحَجُّ أَشْهُرٌ مَّعْلُومَاتٌ فَمَن فَرَضَ فِيهِنَّ الْحَجَّ فَلَا رَفَثَ وَلَا فُسُوقَ وَلَا جِدَالَ فِي الْحَجِّ وَمَا تَفْعَلُوا مِنْ خَيْرٍ يَعْلَمْهُ اللَّـهُ وَتَزَوَّدُوا فَإِنَّ خَيْرَ الزَّادِ التَّقْوَىٰ وَاتَّقُونِ يَا أُولِي الْأَلْبَابِ﴾

197.Hijja ni miezi maalumu. Na anayejilazimisha kufanya Hijja katika miezi hiyo, basi hakuna kuchafua wala ufuska wala mabishano katika Hijja. Na heri yoyote mnayoifanya Mwenyezi Mungu anaijua. Na chukueni masurufu, na hakika masurufu bora ni takua; na nicheni Mimi, enyi wenye akili.

﴿ لَيْسَ عَلَيْكُمْ جُنَاحٌ أَن تَبْتَغُوا فَضْلًا مِّن رَّبِّكُمْ فَإِذَا أَفَضْتُم مِّنْ عَرَفَاتٍ فَاذْكُرُوا اللَّـهَ عِندَ الْمَشْعَرِ الْحَرَامِ وَاذْكُرُوهُ كَمَا هَدَاكُمْ وَإِن كُنتُم مِّن قَبْلِهِ لَمِنَ الضَّالِّينَ ﴾

198.Si vibaya kwenu kutafuta riziki ya Mola wenu. Na mtakapomiminika kutoka Arafa, mtajeni Mwenyezi Mungu katika Mash'aril- Haram: Na mkumbukeni kama alivyowaongoza, ijapokuwa zamani mlikuwa miongoni mwa waliopotea.

﴿ ثُمَّ أَفِيضُوا مِنْ حَيْثُ أَفَاضَ النَّاسُ وَاسْتَغْفِرُوا اللَّـهَ إِنَّ اللَّـهَ غَفُورٌ رَّحِيمٌ ﴾

199.Kisha miminikeni kutoka mahali wanapomiminika watu (wote), na mumwombe Mwenyezi Mungu maghufira; hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye kughufiria Mwenye kurehemu.

﴿ فَإِذَا قَضَيْتُم مَّنَاسِكَكُمْ فَاذْكُرُوا اللَّـهَ كَذِكْرِكُمْ آبَاءَكُمْ أَوْ أَشَدَّ ذِكْرًا فَمِنَ النَّاسِ مَن يَقُولُ رَبَّنَا آتِنَا فِي الدُّنْيَا وَمَا لَهُ فِي الْآخِرَةِ مِنْ خَلَاقٍ ﴾

200.Na mmalizapo kuzitimiza ibada zenu, basi mtajeni Mwenyezi Mungu kama mlivyokuwa mkiwataja baba zenu; bali mtajeni zaidi. Na kuna baadhi ya watu wasemao: Mola wetu! Tupe duniani; nao katika Akhera, hawana lolote.

﴿ وَمِنْهُم مَّن يَقُولُ رَبَّنَا آتِنَا فِي الدُّنْيَا حَسَنَةً وَفِي الْآخِرَةِ حَسَنَةً وَقِنَا عَذَابَ النَّارِ ﴾

201.Na miongoni mwao kuna asemaye; Mola wetu! Tupe mema duniani na (tupe) mema Akhera, na utulinde na adhabu ya Moto.

﴿ أُولَـٰئِكَ لَهُمْ نَصِيبٌ مِّمَّا كَسَبُوا وَاللَّـهُ سَرِيعُ الْحِسَابِ ﴾

202.Hao ndio wenye fungu katika waliyoyachuma, na Mwenyezi Mungu ni Mwepesi wa kuhisabu.

﴿ وَاذْكُرُوا اللَّـهَ فِي أَيَّامٍ مَّعْدُودَاتٍ فَمَن تَعَجَّلَ فِي يَوْمَيْنِ فَلَا إِثْمَ عَلَيْهِ وَمَن تَأَخَّرَ فَلَا إِثْمَ عَلَيْهِ لِمَنِ اتَّقَىٰ وَاتَّقُوا اللَّـهَ وَاعْلَمُوا أَنَّكُمْ إِلَيْهِ تُحْشَرُونَ﴾

203.Na mtajeni Mwenyezi Mungu katika siku zinazohisabiwa. Na mwenye kufanya haraka katika siku mbili, basi si dhambi juu yake; na mwenye kukawia pia si dhambi juu yake, kwa mwenye takua. Na mcheni Mwenyezi Mungu, na jueni kwamba nyinyi mtakusanywa Kwake.

TIMIZENI HIJJA NA UMRA

Aya 196 - 203

MAANA

Aya hizi zimeonyesha baadhi ya hukumu za Hijja, Mafaqihi wameweka vitabu maalumu vinavyohusu Hijja, nami nimetunga kitabu kwa jina Al- Hajj ala Madhahabil-Khamsa; kisha nikakiunganisha katika kitabu Al- Fiqh ala Madhahabil Khamsa wakati kiliporudiwa kuchapishwa kwa mara ya tatu. Vile vile nimeizungumza kwa urefu katika Juzuu ya pili ya kitabu Fiqh ul-Imam Jaffar Sadiq(a.s) Hijja imekuwa maarufu tangu zama za Nabii Ibrahim na Ismail(a.s) na iliendelea katika zama za ujahiliya; na Uislamu ukaithibitisha baada ya kuisafisha na mambo machafu, na kuongeza baadhi ya ibada.

Na timizeni Hijja na Umra kwa ajili ya Mwenyezi Mungu.

Maana ya Hijja kilugha, ni kukusudia, na kisharia ni ibada maalum katika mahali na wakati maalum. Umra kilugha ni ziara yoyote; na kisheria ni ziara katika Al-Kaaba kwa namna maalum, Hijja ni wajibu katika Quran, Hadith na Ijami. Bali wajibu wake umethubutu kwa dhahiri ya dini. Na mwenye kuikanusha sio Mwislamu, sawa sawa na aliyekanusha wajibu wa Saumu na Swala. Shia Imamiyya na Shafii wamesema Umra ni wajibu, Hanafi na Malik wamesema ni Sunna. Kusema kwake Mwenyezi Mungu Kwa ajili ya Mwenyezi Mungu Yaani Hijini na fanyeni Umra kwa ajili ya Mwenyezi Mungu peke yake na sio kwa makusudio ya kidunia. Kwani Waarabu walikuwa wakikusudia kuhiji kwa ajili ya kukutana, kujifaharisha, kutafuta mahitaji na kuhudhuria soko. Ndipo Mwenyezi Mungu akaamrisha Hijja iwe ni kwa makusudio yake Yeye kwa ibada safi yenye kutakasika na makusudio yoyote mengine.

Na kama mkizuiliwa, basi (chinjeni) wanyama walio wepesi kupatikana.

Yaani ikiwa mmeherimia Hijja, kisha mkazuilika kukamilisha ibada kwa njia yake ya kisheria kutokana na maradhi au adui na mengineyo, basi ni juu yenu kuchinja mnyama atakayepatikana kwa urahisi; kwa uchache awe ni mbuzi, wastani ni ng’ombe na wa juu zaidi ni ngamia.

Wala msinyoe vichwa vyenu mpaka wanyama hao wafike machinjioni mwao.

Msemo unaelekezwa kwa wale waliozuilika ambao hawakuweza kutimiza Hijja au Umra. Wao hawatakuwa wametoka katika ihram yao (miko ya Hijja) mpaka wajue kwamba mnyama amefika mahali pake pa kuchinjwa. Na mahali pa kuchinja ni Mina ikiwa ni Hijja; na kama ni Umra basi ni Makka. Hayo ni itakapokuwa kizuizi ni maradhi. Ama ikiwa kizuizi ni adui, basi mahali pa kuchinja ni pale mahali palipotokea kizuizi. Kwa sababu Mtume(s.a.w.w) alichinja mnyama katika Hudaybiya, alipozuiliwa na washirikina kuzuru nyumba ya Mwenyezi Mungu tukufu (Al Kaaba).

Na atakayekuwa mgonjwa katika nyinyi au ana adha kichwani mwake, basi atoe fidia kwa kufunga au sadaka au kuchinja mnyama.

Yaani ikiwa mwenye kuhirimia atanyoa kichwa chake kwa dharura, basi ni juu yake kutoa kafara, atakuwa na hiyari baina ya kufunga siku tatu, kuwalisha masikini sitini au kuchinja mnyama; kwa uchache awe ni mbuzi.

Na mtakapokuwa salama, basi mwenye kujistarehesha kwa kufanya Umra kisha akahiji, achinje mnyama aliyemwepesi kupatikana.

Yaani mtu asiyekuwa na kizuizi, akafanya Umra kisha akahiji baadae katika mwaka huo huo, basi ni juu yake kuchinja mnyama. Hii ndiyo aina ya Hijja inayojulikana kwa jina la Haj Tamattui (Hijja ya starehe) ambayo ni wajibu kwa wasiokuwa watu wa Makka.

Imeitwa Hijja ya starehe, kwa sababu mwenye kuhiji baada ya kumaliza amali za Umra anatoka kwenye miko ya Umra mpaka aje ahirimie Hijja.

Na asiyepata, ni kufunga siku tatu katika Hijja na siku saba mtakaporudi; hizo ni siku kumi kamili.

Imam Jaffar Sadiq(a.s) amesema;Mwenye kufanya Hajj Tamattu, asipopata mnyama atafunga siku tatu katika Hijja; siku ya saba, ya nane na ya tisa katika Dhul-Hijja (mfungu tatu) wala hakuna sharti la Iqama na siku saba atafunga atakaporudi kwa watu wake. Hizo ni siku kumi kamili za kutosheleza mnyama.

Hayo ni kwa yule ambaye watu wake hawako karibu na msikiti mtakatifu.

Mwenye Majmaul Bayan amesema kuwa hayo yaliyotangulia kutajwa katika Tamattui ya Umra kisha Hijja, sio kwa watu wa Makka na walio karibu yake. Isipokuwa ni kwa ambaye hayuko Makka, yule ambaye yuko mbali na Makka kwa zaidi ya maili kumi na mbili (12) kwa kila upande. Mafaqihi wa Kishia Imamiya wamesema Hajj Tamattui ni wajibu kwa walio mbali na Makka, wala haijuzu kwa aliyembali na Makka kuhiji Hijja Qiran na Ifrad, kwani hizo ni wajibu kwa watu wa Makka na wa kando kando yake; na wao haijuzu kwao kuhiji Hajj Tamattui. Kwa ufafanuzi zaidi angalia vitabu vya Fiqh.

Hijja ni miezi maalumu.

Nayo ni kuanzia Shawwal, Dhul-qaad na kumi la mwanzo la Dhul-Hijja. (mfunguo mosi, mfunguo pili na mfunguo tatu) Mwenye kuhirimia kabla yake Hijja yake haitaswihi na mwenye kuhirimia ndani ya miezi hiyo itaswihi na ataleta amali zilizobakia.

Na anayejilazimisha Hija katika miezi hiyo, basi hakuna kuchafua wala ufuska wala mabishano katika Hijja.

Makusudio ya uchafuzi hapa ni kujamii. Mtu akimjamii mkewe na huku amehirimia Hijja, basi Hijja yake imeharibika, sawa sawa na aliyejamii au kula huku akiwa amefunga. Kwa hiyo atakamilisha Hijja yake, kisha aje alipe mwaka ujao; kama ilivyo kwa mwenye kuiharibu Saumu. Makusudio ya ufuska, ni uongo na kutukana. Ama kuhusu kubishana riwaya za Ahlul Bait zinasema, hilo ni kusema mtu; Hapana wallahi au Kwa nini, wallahi n.k.

Si vibaya kwenu kutafuta riziki ya Mola wenu.

Kwa vile wakati wa ujahilia watu walikuwa wakifanya biashara na kuchuma siku za Hijja, kukadhaniwa kuwa ni haramu, ndipo Mwenyezi Mungu (s.w.t.), akaondoa tuhuma hii na akabainisha kwamba kuchuma hakupingani na ikhlasi katika amali za Hijja.

Na mtakapomiminika kutoka Arafa, mtajeni Mwenyezi Mungu katika Masharil Haram.

Arafa ni mahali maalum. Kumiminika kutoka Arafa ni kuondoka, Masharil-Haram ndipo pale panajulikana kama Muzdalifa na kutua hapo ni wajibu; kama ilivyo kwa Arafa.

Kisha miminikeni kutoka mahali wamiminikapo watu (wote). Inasemekana kuwa Maquraish walikuwa hawatui Arafa pamoja na watu wengine kwa kiburi tu, ndipo Mwenyezi Mungu akamwamrisha Mtume wake kutua hapo na kutoka pamoja na watu ili abatilishe waliyokuwa wakiyafanya Maquraish.

Na mmalizapo kuzitimiza ibada zenu, basi mtajeni Mwenyezi Mungu zaidi.

Imepokuwa kutoka kwa Imam Baqir baba wa Imam Sadiq(a.s) kwamba watu walikuwa wanapomaliza Hijja wanakusanyika huko na kuwataja wazazi wao kwa fahari, ndipo Mwenyezi Mungu akawaamrisha kuliacha hilo na badala yake wamtaje Mwenyezi Mungu na jinsi alivyowaneemesha. Kwa sababu Yeye ndiye mwenye kuwaneemesha wao na mababa zao.

Na baadhi ya watu kuna asemaye: Mola wetu! Tupe duniani; nao katika akhera hawana lolote. Na miongoni mwao kuna asemaye: Mola wetu! Tupe mema duniani na (tupe) mema akhera, na utulinde na adhabu ya moto. Hao ndio wenye fungu katika waliyoyachuma, na Mwenyezi Mungu ni mwepesi wa kuhisabu.

Watu katika Hijja zao wako aina mbili. Aina ya kwanza ni yule asiyetaka lolote isipokuwa starehe ya dunia na hana makusudio yoyote isipokuwa dunia tu, na anapomwabudu Mwenyezi Mungu humwabudu kwa ajili ya dunia. Hawa ndio wenye kunyimwa neema ya Akhera. Ama aina ya pili ni yule anayetaka heri ya dunia na akhera na anafanya amali kwa ajili ya dunia yake na akhera yake. Huyu ndiye mwenye radhi mbele ya Mwenyezi Mungu kesho kwa kulipwa amali yake njema. Mwenye Tafsiri Rawhul Bayan amenukuu kutoka kwa Imam Ali bin Abi Twalib(a.s) kwamba wema katika dunia ni mwanamke mwema na katika akhera ni Hurulain. Ama adhabu ya moto makusudio yake ni mwanamke muovu.

Iwe ni sahih Hadith hiyo au la, lakini mimi najua kuna watu wanaohisi kwamba lau wao wangekuwa katika Jahanam kisha wakahiyarishwa kutoka katika Jahanam na warudi kwa wake zao waliokuwa nao duniani au wabaki Jahannam, basi wangelichagua kubaki katika Jahannam kuliko kuishi tena na wake zao hao.

Na mtajeni Mwenyezi Mungu katika siku zinazohisabiwa.

Makusudio yake ni siku tatu za Tashriq nazo ni; Tarehe kumi na moja, kumi na mbili na kumi na tatu katika mwezi wa Dhul-Hijja (mfungo tatu). Si wajibu kwa mwenye kuhiji kulala Mina usiku wa kumi na tatu, lakini kwa sharti ya kuwa atoke Mina siku ya kumi na mbili baada ya kupinduka jua na kabla ya Maghrib na awe hakuvunja mwiko wa kuwinda au kujamii. Kwa hali hiyo ndipo tunapopata tafsiri ya kauli yake Mwenyezi Mungu:

Na mwenye kufanya haraka katika siku mbili, basi si dhambi juu yake; na mwenye kukawia pia si dhambi juu yake kwa mwenye takua.

Yaani mwenye kuacha kuwinda na wanawake katika ihram yake. Ikiwa amevunja mwiko wa kulala na mke au kuwinda au alichelewa na jua siku ya kumi na mbili akiwa yuko Mina, basi itakuwa wajibu kwake kulala usiku wa kumi na tatu na kutupia mawe vikuta vitatu (shetani).

7

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA PILI

﴿ وَمِنَ النَّاسِ مَن يُعْجِبُكَ قَوْلُهُ فِي الْحَيَاةِ الدُّنْيَا وَيُشْهِدُ اللَّـهَ عَلَىٰ مَا فِي قَلْبِهِ وَهُوَ أَلَدُّ الْخِصَامِ ﴾

204.Na katika watu kuna ambaye kauli yake inakupendeza katika maisha ya duniani, naye humshuhudiza Mwenyezi Mungu kwa yaliyo moyoni mwake na hali ni hasimu mkubwa kabisa.

﴿ وَإِذَا تَوَلَّىٰ سَعَىٰ فِي الْأَرْضِ لِيُفْسِدَ فِيهَا وَيُهْلِكَ الْحَرْثَ وَالنَّسْلَ وَاللَّـهُ لَا يُحِبُّ الْفَسَادَ﴾

205.Na anapotawala hufanya bidii katika ardhi kufanya ufisadi, na huangamiza mimea na viumbe, na Mwenyezi Mungu hapendi ufisadi.

﴿ وَإِذَا قِيلَ لَهُ اتَّقِ اللَّـهَ أَخَذَتْهُ الْعِزَّةُ بِالْإِثْمِ فَحَسْبُهُ جَهَنَّمُ وَلَبِئْسَ الْمِهَادُ ﴾

206.Na anapoambiwa. Mche Mwenyezi Mungu, hupandwa na mori wa kufanya dhambi. Basi Jahannam inamtosha, napo ni makao mabaya mno

﴿ وَمِنَ النَّاسِ مَن يَشْرِي نَفْسَهُ ابْتِغَاءَ مَرْضَاتِ اللَّـهِ وَاللَّـهُ رَءُوفٌ بِالْعِبَادِ ﴾

207.Na katika watu yuko auzaye nafsi yake kwa kutaka radhi ya Mwenyezi Mungu, na Mwenyezi Mungu ni mpole kwa waja.

KAULI ZAO ZINAKUPENDEZA

Aya 204 – 207

MAANA

Baadhi ya wafasiri wapya wamejaza kurasa kwa maneno matamu katika kufasiri Aya hizi, lakini hawakuzidisha chochote zaidi ya kuwagawanya watu kwenye wema na uovu. Kwa dhahiri haya yanajulikana na wote, hayahitaji ubainifu wowote, sikwambii tafsiri ndefu tena. Unaweza kuuliza; Ikiwa kugawanyika watu kunajulikana na wote, basi kubainisha kunakuwa ni maelezo ambayo tayari yameshaelezwa na kufafanua lililofafanuliwa na yapasa kuyachukulia maneno ya Mwenyezi Mungu (s.w.t.) vizuri? Jibu: Inawezekana kuwa makusudio ni kuongoza na kuelekeza kwamba mwenye akili anatakikana kutohadaliwa kwa mambo ya nje wala asimwamini mwenye kutegeneza maneno matamu. Kwa sababu wafisadi ni mabingwa wa kazi hiyo na kazi ya ria. Kwa hivyo ni juu yetu kutomtegemea yeyote isipokuwa baada ya kufanya majaribio na kupatikana dalili ya ukweli wake na usafi wake.

Hiyo ndiyo asili ya ujumla inayoenea katika hukumu nyingi za dini na za kidunia; kama kuchagua Hakimu, Kadhi, Naibu, Kadhi, Mufti na kila anayesimamia masilahi ya Umma. Ajabu ya maajabu ni kutakiwa shahada ya kielimu tu kwa mwenye kujitokeza kwa kazi muhimu ya mji au nchi na inayogusa maisha ya watu. Lakini haulizwi uaminifu wake na tabia yake, pamoja na kuwa hayo ndio msingi. Wengi wenye shahada wanazitumia kuwa ni zana za kuibia.

Na katika watu kuna ambaye kauli yake inakupendeza hapa duniani, naye humshuhudia Mwenyezi Mungu kwa yaliyomo moyoni mwake, na hali ni hasimu mkubwa kabisa.

Yaani wanadhihihirisha mapenzi na heri na hali wao ndio maadui zaidi wa heri na watu wa heri.

Na anapotawala hufanya bidii katika ardhi kufanya ufisadi.

Wamehitaliafiana wafasiri kuhusu neno Tawalla. Je makusudio ni kuondoka na maana yake kuwa ni, anapoondoka kwa yule aliyemdanganya, huhangaika katika ardhi kwa ufisadi. Au kwamba makusudio ni kutawala na usultani, na maana yawe, na atakapokuwa mtawala atafanya wanayoyafanya watawala waovu ya kuangamiza mimea na viumbe? Mwenye Tafsir Al manar amenakili kutoka kwa Ustadha wake Sheikh Muhammad Abduh kwamba ameyapa nguvu maana ya utawala kwa kuunganisha na kauli yake Mwenyezi Mungu (s.w.t.):

"Na anapoambiwa mche Mwenyezi Mungu, hupandwa na mori wa kufanya dhambi."

Kwa maana ya kuwa mtawala mkaidi anakuwa na kiburi kuongozwa kwenye maslahi au kupewa tahadhari ya mambo ya ufisadi, yeye hujiona yuko juu ya haki; kama vile alivyo juu ya watu wake anaowatawala, basi itawezekanaje kwa mtu kumwambia amwogope Mwenyezi Mungu.

Na huangamiza mimea na viumbe.

Mimea ni kilimo na viumbe ni wanyama. Makusudio ni maslahi yote ya kiuchumi katika kilimo, viwanda na ufugaji, mali ghafi, na mengineyo yanayohusika na uhai wa watu na maisha yao. Mwenyezi Mungu amehusisha kutaja kilimo na ufugaji kwa vile viwanda wakati huo havikuwa na umuhimu wowote kama ilivyo sasa. Uharamu wa mambo hayo kwa mtazamo wa Uislamu ni sawa na uharamu wa kumwaga damu; na mwenye kukusudia ubaya katika vitu hivyo, ndio amekusudia ubaya wa utu hasa; hata kama vitu hivyo ni milki ya adui anayepiga vita Waislamu. Mtume(s.a.w.w) amekataza kukata miti, kuharibu mimea na majengo na kutia sumu miji ya washirikina siku za vita, n.k. Lau tunailinganisha sharia ya Kiislamu na mambo yanayofanywa leo na dola za kikoloni na vita vyao vya silaha za kemikali kwenye mimea, watu na wanyama, na kuitia sumu anga kwa mabomu ya Atomic na kuyatupa kwa wanawake na watoto, lau hayo yote tunayaunganisha na Uislamu, basi tutajua huruma, uadilifu na utu wa Uislamu na unyama wa dola za Magharibi na jinsi zilivyopetuka mipaka katika dhulma na unyang'anyi.

Na Mwenyezi Mungu (s.w.t.) hapendi ufisadi.

Hakuna uharibifu mkubwa zaidi kuliko kuzusha vita na kutumia silaha zenye kubomoa ili kuwatawala watu na kuwanyang'anya chakula na matunda ya jasho lao.

Na anapoambiwa mche Mwenyezi Mungu hupandwa na mori wa kufanya dhambi.

Mtu mwema wenye ikhlasi anakubali masahihisho na nasaha, bali huzitafuta na kuzikaribisha, kwa sababu yeye hana lengo jengine zaidi ya haki, wala hatafuti sifa; kwa sababu amali yake ni kwa ajili ya Mwenyezi Mungu (s.w.t.) sio umashuhuri.

Imam Amirul Muminin(a.s) anasema katika maneno anayowasifu wanaomcha Mwenyezi Mungu:"Hawaridhii na amali zao chache wala hawakioni kingi kilicho kingi; wao wanajituhumu na wao ni wenye kunyenyekea katika amali zao."

Katika hotuba yake siku za ukhalifa wake alisema: "Mtu hata kama ana cheo kikubwa katika haki na fadhila kubwa katika dini hawezi kuwa hahitajii kusaidiwa katika aliyobebeshwa na Mungu katika haki zake; wala si mwenye kutaka kujitukuza; wala mtu hata kama nafsi zinamfanya mdogo na kudharauliwa na macho sio kuwa hawezi kusaidia au kusaidiwa... Wala msinidhanie kuwa mimi ni mzito katika haki nitakayoambiwa, kwani mwenye kuifanya nzito haki atakayoambiwa au uadilifu atakaoonyeshwa, basi kwake kuitumia haki na uadilifu ni kuzito zaidi."

Hivyo ndivyo anavyotakikana mwanachuoni mwenye ikhlasi ya kweli. Ama mnafiki mwenye hiana, haki inakuwa nzito juu yake kwa sababu itamfedhehesha; na hununua sifa kwa thamani kubwa ili azibe upungufu wake na uovu wake.

Na katika watu yuko auzaye nafsi yake kutaka radhi ya Mwenyezi Mungu.

Yaani baadhi ya waumini wanaikabili Jihadi na wanapenda mauti kwa ajili ya Mwenyezi Mungu. sawa na wale wengine wanaopenda uhai. Hawana lengo jengine isipokuwa kutaka radhi ya Mwenyezi Mungu na thawabu Zake. Razi katika kutafsiri Aya hii anasema kuhusu sababu za kushuka kwake kuwa kuna riwaya tatu; Mojawapo ni kwamba Aya hii imeshuka kwa sababu ya Ali bin Abi Twalib(a.s) alipolala kwenye kitanda cha Mtume wakati wa Hijra, alisimama Jibril kichwani mwake, Mikail miguuni mwake na Jibril: Pongezi! Pongezi! ewe Ali akisema: Mwenyezi Mungu anajionea fahari kwako, mbele ya Malalika( [7] ).

﴿ يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا ادْخُلُوا فِي السِّلْمِ كَافَّةً وَلَا تَتَّبِعُوا خُطُوَاتِ الشَّيْطَانِ إِنَّهُ لَكُمْ عَدُوٌّ مُّبِينٌ﴾

208.Enyi mlioamini! Ingieni katika usalama nyote, wala msifuate nyayo za Shetani. Kwa hakika yeye kwenu ni adui wa wazi.

﴿ فَإِن زَلَلْتُم مِّن بَعْدِ مَا جَاءَتْكُمُ الْبَيِّنَاتُ فَاعْلَمُوا أَنَّ اللَّـهَ عَزِيزٌ حَكِيمٌ ﴾

209.Na kama mkiteleza baada ya kuwafikia ubainifu, basi jueni kwamba Mwenyezi Mungu ni Mwenye nguvu, Mwenye hekima.

﴿ هَلْ يَنظُرُونَ إِلَّا أَن يَأْتِيَهُمُ اللَّـهُ فِي ظُلَلٍ مِّنَ الْغَمَامِ وَالْمَلَائِكَةُ وَقُضِيَ الْأَمْرُ وَإِلَى اللَّـهِ تُرْجَعُ الْأُمُورُ ﴾

210.Hawangoji ila kuwafikia (adhabu ya) Mwenyezi Mungu katika vivuli vya mawingu na Malaika, na liishe jambo; na mambo yote hurudishwa kwa Mwenyezi Mungu.

INGIENI KATIKA USALAMA NYOTE

Aya 208 - 210

MAANA

Enyi Mlioamini! Ingieni katika usalama nyote.

Imesemekana kuwa makusudio ya neno Silmi hapa ni Uislamu, na kwamba msemo unawaelekea wanafiki ambao wameificha kufuru na kudhihirisha Uislamu. Na imesemekana kuwa msemo unawaelekea wenye kumwamini Mwenyezi Mungu katika Ahlul Kitab ambao hawakusilimu. Na ikasemekana kuwa unawaelekea Waislamu wote kwa hivyo maana yake yanakuwa ni kumtii Mwenyezi Mungu na kumnyenyekea katika hukumu Zake zote sio baadhi. Na pia imesemekana maana yake ni suluhu kwa maana kuwa ingieni katika suluhu nyote. Tuonavyo sisi ni kwamba Mwenyezi Mungu (s.w.t.) amemwamrisha mwenye kumwamini Mwenyezi Mungu, kwa imani sahihi kuingia katika lile ambalo lina salama yake ya dunia na akhera. Na njia ya usalama inajulikana na wote, nayo ni kusaidiana, kuungana, na kuacha vita na uhasama. Vile vile kuyashinda matamanio na kuwa na ikhlasi katika kauli na vitendo.

Makusudio ya maneno hayo yanatiliwa nguvu na kauli yake Mwenyezi Mungu:Wala msifuate nyayo za shetani. Kwa hakika yeye kwenu ni adui wa wazi, Aliyoileta mara tu, baada ya kusema.Ingieni katika usalama nyote. Hapo Mwenyezi Mungu amezingatia kuwa nyayo za shetani kinyume chake ni usalama; na amemweka mtu mbele ya mambo mawili tu, hakuna la tatu; Ama kuingia katika usalama au kufuata nyayo za shetani ambazo ndio dhati ya uovu, ugomvi, shari na ufisadi.

Na kama mkiteleza baada ya kuwafikia ubainifu, basi jueni ya kwamba Mwenyezi Mungu ni Mwenye nguvu Mwenye hekima.

Baada ya Mwenyezi Mungu kuamrisha kuingia katika usalama na kukataza kufuatwa nyayo za shetani, amemhadharisha yule atakayehalifu amri yake na makatazo yake na akatishia kwa kusema: "Basi jueni kwamba Mwenyezi Mungu ni Mwenye nguvu Mwenye hekima." Mwenye nguvu, hashindwi katika amri Yake wala hakimzuwii chochote kwa alilokusudia kulifanya. Mwenye hekima, humlipa mema mtiifu na humwadhibu mwasi. Razi anasema: "Huo ndio ukomo wa kiaga kwa sababu ni kuhofisha bila ya kutaja adhabu. Huenda mzazi akamwambia mtoto wake: "Ukiniasi basi wewe wanijua na wajua uwezo wangu kwako", basi maneno hayo yanakuwa ni makemeo ya ufasaha zaidi kuliko kutaja kipigo na mengineyo.

Hawangoji ila kuwafikia (adhabu ya) Mwenyezi Mungu katika vivuli vya mawingu na Malaika. Maana kwa ujumla ni kwamba wale wenye kukadhibisha na wakaasi watajiwa na adhabu kwa ghafla wala hawataokoka. Aya iko katika mwelekeo wa Aya inayosema:

﴿ فَهَلْ يَنظُرُونَ إِلَّا السَّاعَةَ أَن تَأْتِيَهُم بَغْتَةً ﴾

"Na hawangoji ila saa ya Kiyama kiwajie kwa ghafla...?" (47:18).

Na lishe jambo; na mambo yote hurudishwa kwa Mwenyezi Mungu. Mauti ambayo hapana budi nayo, yakija na Kiyama kikija, kila kitu kitakuwa kimekwisha na hapatabakia mbele ya wenye makosa isipokuwa hisabu na mateso.

SIRI NA MATUKIO YA GHAFLA

Hakuna yeyote ajuaye yatakayomtokea mbele na siri ya wakati, heri au shari. Hawezi kuyajua hayo vyovyote atakavyokuwa na elimu au imani:

"Na nafsi yoyote haijui itachuma nini kesho." (31:34)

Mara nyingi mtu hujiwa na heri kwa ghafla wakati yeye anatazamia kupata shari; na hujiwa ghafla na shari wakati anapotazamia heri. Hakuna kitu kinachotia uchungu kama hicho cha kupata shari wakati wa kutazamia heri; kama vile ambavyo hakuna kitu kitamu kama kupata heri wakati wa kutazamia shari. Mwenye akili hawezi kughurika na alivyo navyo, bali hufikiria mzunguko wa zama; kama vile ambavyo hakati tamaa na lolote linalompata; kwani dunia inageuka milele; ndio maana ikasemwa; "Kudumu hali ni muhali na faraja inakuja kutokana na dhiki." Imam Ali(a.s) anasema:"Baada ya dhiki ni faraja. Anaendelea kusema Imam:"Hakika Musa bin Imran alitoka kuwatafutia watu wake moto akasemeshwa na Mwenyezi Mungu na akarudi akiwa Mtume." Mwenyezi Mungu anasema:

﴿ إِنَّهُ لَا يَيْأَسُ مِن رَّوْحِ اللَّـهِ إِلَّا الْقَوْمُ الْكَافِرُونَ ﴾

"...Hawakati tamaa ya rehema ya Mwenyezi Mungu isipokuwa watu makafiri." (12:87).

Na amesema tena:

﴿ فَلَا يَأْمَنُ مَكْرَ اللَّـهِ إِلَّا الْقَوْمُ الْخَاسِرُونَ ﴾

... Hawajiaminishi na mipango ya Mwenyezi Mungu ila watu wenye hasara." (7:99).

Imeelezwa katika vitabu vya Historia na Sera kwamba Ibn Ziyat alikuwa waziri na mtu wa kutegemewa na Mu'utasim, naye alikuwa ni katika mataghuti wa hali ya juu na dhalimu mkubwa. Alitengeneza tanuri la chuma alilolijaza misumari yenye ncha pambizoni mwake. Anapomkasirikia mtu humtupa ndani, kila anavyojitingisha ndivyo misumari inavyomwingia mwilini mwake. Mutawakkil alipotawala alimshika Ibn Ziyat na akamfunga kwa chuma mikononi mwake na miguuni mwake kisha akamtupa katika tanuri hilo, na baadaye akafa. Kabla ya kufa alisikika akiimba shairi hili: Sifazake tulia, hebu nenda pole pole, Kigeugeu dunia, huenda nyuma na mbele.

﴿ سَلْ بَنِي إِسْرَائِيلَ كَمْ آتَيْنَاهُم مِّنْ آيَةٍ بَيِّنَةٍ وَمَن يُبَدِّلْ نِعْمَةَ اللَّـهِ مِن بَعْدِ مَا جَاءَتْهُ فَإِنَّ اللَّـهَ شَدِيدُ الْعِقَابِ﴾

211.Waulize wana wa Israil, ishara ngapi zilizo wazi tulizowapa? Na anayezibadilisha neema za Mwenyezi Mungu baada ya kumfikia, basi hakika Mwenyezi Mungu ni Mkali wa kuadhibu.

﴿ زُيِّنَ لِلَّذِينَ كَفَرُوا الْحَيَاةُ الدُّنْيَا وَيَسْخَرُونَ مِنَ الَّذِينَ آمَنُوا وَالَّذِينَ اتَّقَوْا فَوْقَهُمْ يَوْمَ الْقِيَامَةِ وَاللَّـهُ يَرْزُقُ مَن يَشَاءُ بِغَيْرِ حِسَابٍ ﴾

212.Wamepambiwa makafiri maisha ya duniani, na wanawafanyia maskhara wale walioamini. Na wale wenye takua watakuwa juu yao Siku ya Kiyama. Na Mwenyezi Mungu humruzuku amtakaye bila hisabu

WAULIZE WANAWA ISRAIL

Aya 211 – 212

MAANA

Waulize wana wa Israil, ishara ngapi zilizo wazi tulizowapa?

Makusudio ya waulize hapa sio swali hasa la kihakika, kwa sababu Mtume(s.a.w.w) anajua hali zao, wala makusudio sio kuelezea hali waliyokuwa nayo; kama ilivyo katika Aya ya 49 na inayofuatia. Isipokuwa makusudio hasa ni kuwa Waislamu wazingatie na wapate funzo na hali ya Waisrail. Njia ya kupata funzo ni kuwa Waisrail walijiwa na Mtume Musa(a.s) kwa miujiza na hoja ambayo ni mkono kuwa mweupe, fimbo kugeuka nyoka na kupasuka bahari. Vile vile kufunikwa na wingu, kuteremshiwa Manna na Salwa na jabali kutoka maji. Pamoja na hayo yote waliasi na kukhalifu, ndipo Mwenyezi Mungu akawaadhibu kwa madhila na utwevu katika dunia na adhabu iumizayo katika Akhera. Na Waislamu nao wamejiwa na Muhammad(s.a.w.w) kwa miujiza na hoja zinazofahamisha ukweli wa Utume wake na kuswihi sharia yake; naye akawafikilizia habari kutoka kwa Mwenyezi Mungu kuwa waaingie katika Uislamu wote, kwani humo watapata heri na utengeneo wao; kama wakiasi kama walivyofanya Waisrail, basi yatawapata yaliyowapata Waisrail.

Na anayezibadilisha neema za Mwenyezi Mungu baada ya kumfikia, basi hakika Mwenyezi Mungu ni mkali wa kuadhibu.

Makusudio ya neema hapa ni dalili za haki, kwani hizo ni katika neema kubwa. Kwa sababu ndani yake mna uongofu na kuokoka na kuhiliki na upotevu. Makusudio ya kuzibadilisha ni kuziasi na kuziharibu. Kwa hiyo kauli yake Mwenyezi Mungu (s.w.t.)Na anayezibadilisha neema za Mwenyezi Mungu baada ya kumfikia ni sawa na kauli yake:

﴿ فَإِن زَلَلْتُم مِّن بَعْدِ مَا جَاءَتْكُمُ الْبَيِّنَاتُ﴾

"Na kama mkiteleza baada ya kuwafikia ubainifu..." (2:209).

Vile vile kusema kwake:

﴿فَاعْلَمُوا أَنَّ اللَّـهَ عَزِيزٌ حَكِيمٌ ﴾

"Basi hakika Mwenyezi Mungu ni mkali wa kuadhibu" (2:209) ni sawa na kusema Kwamba:Mwenyezi Mungu ni Mwenye nguvu Mwenye hekima."

Maana ni moja na lengo ni moja.

HAPANA IMANI BILA TAKUA (UCHA MUNGU)

Wamepambiwa makafiri maisha ya duniani.

Hapana tofauti kati ya mwenye kukanusha kuwapo Mwenyezi Mungu na yule mwenye kuamini kinadharia tu, lakini matendo yakawa ni tofauti. Hapana tofauti kati ya wawili hao. Kwa sababu kila mmoja ameathiriwa na dunia na vipambo vyake, ameathirika na kitu cha sasa hivi kuliko cha muda ujao; heri na manufaa ameyapima kwa kiwango cha manufaa yake, wala hakupima na mambo aliyoharamisha Mwenyezi Mungu wala na msimamo wa kibinadamu. Mimi kila ninavyozidi kuzama katika tafsiri ya Qur'an na kuangalia kwa undani Aya zake, basi huwa na yakini zaidi kwamba imani bila ya ucha Mungu haina maana yoyote; na kwamba kila anayeiangalia dunia kuwa ndio makusudio yake yote, basi atakuwa ameiweka mbali sharia ya haki na dini, atake asitake.

Imekuja Hadith Mutawatir kutoka kwa Mtume Mtukufu akisema: "Dunia na akhera zina madhara" yaani zinadhuriana kuhujumu moja yao nikuiacha nyingine( [8] ).

Imam Ali(a.s) anasema: "Hakika dunia na Akhera ni maadui wawili wanaotofautiana, na ni njia mbili tofauti. Mwenye kuipenda dunia ataichukia akhera na kuwa adui yake; zote mbili ni kama Mashariki na Magharibi, mwenye kutembea kati yao huwa mbali na nyingine kila anapokaribia moja wapo.

" Na wanawafanyia maskhara wale walioamini.

Ni kawaida wale wanaozichezea Hoja za Mwenyezi Mungu na hukumu zake wakihalalisha damu na mali ya haramu kuwadharau na kuwachezea wale wanaojilinda na maharamisho na kuvumilia tabu na mashaka kwa ajili ya kumridhisha Mungu.

Na wale wenye takua watakuwa juu yao siku ya Kiyama.

Amesema wenye takua wala hakusema wale walioamini, kwa sababu imani bila takua si lolote; kama tulivyobainisha. Maana yako wazi ni kuwa makafiri wakiwadharau waumini hivi sasa, basi mambo yatabadilika kesho. Mwenyezi Mungu anasema:

﴿قَالَ الَّذِينَ أُوتُوا الْعِلْمَ إِنَّ الْخِزْيَ الْيَوْمَ وَالسُّوءَ عَلَى الْكَافِرِينَ ﴾

"...Watasema walio pewa ilimu: Hakika hizaya na ubaya leo itawafika makafiri." (16:27).

﴿فَالْيَوْمَ الَّذِينَ آمَنُوا مِنَ الْكُفَّارِ يَضْحَكُونَ ﴾

"Basi leo wale ambao wameamini wanawacheka makafiri." (83:34)

Na Mwenyezi Mungu humruzuku amtakaye bila hisabu.

Riziki ni mbili ya dunia na riziki ya Akhera. Riziki ya dunia inajulikana na riziki ya Akhera, ni neema isiyokatika na isiyokuwa na chembe ya huzuni au hofu. hataipata yeyote isipokuwa kwa imani na amali njema: Anasema Mwenyezi Mungu:

﴿وَالَّذِينَ آمَنُوا وَعَمِلُوا الصَّالِحَاتِ أُولَـٰئِكَ أَصْحَابُ الْجَنَّةِ هُمْ فِيهَا خَالِدُونَ ﴾

"Na wale walioamini na kutenda mema, hao ndio watu wa Peponi, humo watakaa milele." (2:82).

Kila mtu anaweza kupata riziki duniani, awe ni kafiri au Mumin, mwema au mwovu, na anayehangaika au asiyehan-gaika; kama vile urithi, zawadi, wasiya, n.k. Vile vile inaweza kupatikana kwa njia ya halali, au haramu, kama vile kunyang'anya, kughushi na utapeli. Mwenye Tafsir Al-Manar amenakili kutoka kwa mwalimu wake Sheikh Muhammad Abduh kwamba, amesema wakati wa kutafsiri Aya hii, kwamba riziki bila ya kuhangaika inaweza ikapatikana kwa baadhi ya watu. Ama kwa Umma ni muhali kujitosheleza isipoku-wa kwa kuhangaika na kufanya kazi. Huo ni ukweli ulio wazi kabisa.


8

9

10

11

12

13