TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI Juzuu 20

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI0%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: Qurani tukufu

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI

Mwandishi: Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya
: HASANI MWALUPA
Kundi:

Matembeleo: 14318
Pakua: 2503


Maelezo zaidi:

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 25 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 14318 / Pakua: 2503
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI Juzuu 20

Mwandishi:
Swahili

5

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI

فَلَمَّا قَضَىٰ مُوسَى الْأَجَلَ وَسَارَ بِأَهْلِهِ آنَسَ مِن جَانِبِ الطُّورِ نَارًا قَالَ لِأَهْلِهِ امْكُثُوا إِنِّي آنَسْتُ نَارًا لَّعَلِّي آتِيكُم مِّنْهَا بِخَبَرٍ أَوْ جَذْوَةٍ مِّنَ النَّارِ لَعَلَّكُمْ تَصْطَلُونَ ﴿٢٩﴾

29. Basi Musa alipomaliza muda wake na akasafiri na ahli zake, aliona moto upande wa mlima; akawaambia ahli zake: Ngojeni, mimi nimeona moto, pengine nitawaletea kutoka huko habari au kijinga cha moto mpate kuota.

فَلَمَّا أَتَاهَا نُودِيَ مِن شَاطِئِ الْوَادِ الْأَيْمَنِ فِي الْبُقْعَةِ الْمُبَارَكَةِ مِنَ الشَّجَرَةِ أَن يَا مُوسَىٰ إِنِّي أَنَا اللَّـهُ رَبُّ الْعَالَمِينَ ﴿٣٠﴾

30. Basi alipoufikia aliitwa kutoka upande wa kulia wa bonde, katika eneo lilobarikiwa, kutoka mtini, kwamba ewe Musa! Hakika mimi ndiye Mwenyezi Mungu Mola wa viumbe.

وَأَنْ أَلْقِ عَصَاكَ فَلَمَّا رَآهَا تَهْتَزُّ كَأَنَّهَا جَانٌّ وَلَّىٰ مُدْبِرًا وَلَمْ يُعَقِّبْ يَا مُوسَىٰ أَقْبِلْ وَلَا تَخَفْ إِنَّكَ مِنَ الْآمِنِينَ ﴿٣١﴾

31. Na kwamba, itupe fimbo yako! Alipoiona inatingishika, kama kwamba ni nyoka aligeuka kurudi nyuma wala hakungoja. Ewe Musa! Njoo mbele wala usihofu! Hakika wewe ni miongoni mwa waliosalimika.

اسْلُكْ يَدَكَ فِي جَيْبِكَ تَخْرُجْ بَيْضَاءَ مِنْ غَيْرِ سُوءٍ وَاضْمُمْ إِلَيْكَ جَنَاحَكَ مِنَ الرَّهْبِ فَذَانِكَ بُرْهَانَانِ مِن رَّبِّكَ إِلَىٰ فِرْعَوْنَ وَمَلَئِهِ إِنَّهُمْ كَانُوا قَوْمًا فَاسِقِينَ ﴿٣٢﴾

32. Na ingiza mkono wako katika mfuko wako utatoka mweupe pasipo ubaya na vutia mkono wako kwako kutuliza hofu. Basi hizo ni dalili mbili kutoka kwa Mola wako kwa ajili ya Firauni na wakuu wake. Hakika wao ni watu mafasiki.

MUSA ANAMALIZA MUDA

Aya 29 – 32

MAANA

Baada ya kutimia muda walioafikana Musa na baba mkwe, alifungasha virago vyake na akelekea Misri pamoja na ahli zake. Katika Kamusi ya Kitabu kitakatifu, imeandikwa: “Musa alikwenda Misri pamoja na mkewe na wanawe wawili.”

Basi alipofika jangwani alipotea njia kwenye giza la usiku wenye baridi; kama inavyofahamisha kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: “Mpate kuota.” Wakati akiwa hajui la kufanya, mara akaona moto unawaka, ndipo akawaaambia watu wake, ningojeni niende kwenye ule moto niwaletee habari za njia au angalau niwaletee moto wa kuota. Umetangulia mfano wake katika Juz. 16 (20:10) na Juz. 19 (27:7).

Basi alipoufikia aliitwa kutoka upande wa kulia wa bonde. Yaani upande wa kulia wa Musa.Katika eneo lilobarikiwa, kutokana na Mitume wengi kutokea huko na heri zake nyingi,kutoka mtini, kwamba ewe Musa! Hakika mimi ndiye Mwenyezi Mungu Mola wa viumbe.

Kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: “kutoka mtini,” inafahamisha kwamba Mwenyezi Mungu aliumba maneno kwenye mti.

Wale wanaosema kuwa maneno ya Mwenyezi Mungu ni ya kuzuka na wala siyo ya tangu zamani, wametoa dalili kwa Aya hii. Umetangulia mfano wake katika Juz. 16 (19: 52) na (20: 12).

Na kwamba, itupe fimbo yako! Alipoiona inatingishika, kama kwamba ni nyoka aligeuka kurudi nyuma wala hakungoja. Ewe Musa! Njoo mbele wala usihofu! Hakika wewe ni miongoni mwa waliosalimika.

Umetangulia mfano wake katika Juz. Juz. 19 (27:10).

Na ingiza mkono wako katika mfuko wako utatoka mweupe pasipo ubaya na vutia mkono wako kwako kutuliza hofu. Basi hizo ni dalili mbili kutoka kwa Mola wako kwa ajili ya Firauni na wakuu wake. Hakika wao ni watu mafasiki.

Kuvutia mkono ni kuuweka kifuani;yaani hilo linatuliza hofu. Umetangulia mfano wake katika Juz. 9 (7:108), Juz. 16 (20:22) na Juz. 19 (26:33) na (16:12).

قَالَ رَبِّ إِنِّي قَتَلْتُ مِنْهُمْ نَفْسًا فَأَخَافُ أَن يَقْتُلُونِ ﴿٣٣﴾

33. Akasema: Mola wangu! Hakika mimi nilimuua mtu katika wao, kwa hiyo nahofia wataniua.

وَأَخِي هَارُونُ هُوَ أَفْصَحُ مِنِّي لِسَانًا فَأَرْسِلْهُ مَعِيَ رِدْءًا يُصَدِّقُنِي إِنِّي أَخَافُ أَن يُكَذِّبُونِ ﴿٣٤﴾

34. Na ndugu yangu Harun ni fasaha zaidi kwa ulimi kuliko mimi, basi mtume pamoja nami awe msaidizi. Hakika mimi nahofia watanikadhibisha.

قَالَ سَنَشُدُّ عَضُدَكَ بِأَخِيكَ وَنَجْعَلُ لَكُمَا سُلْطَانًا فَلَا يَصِلُونَ إِلَيْكُمَا بِآيَاتِنَا أَنتُمَا وَمَنِ اتَّبَعَكُمَا الْغَالِبُونَ ﴿٣٥﴾

35. Akasema: Tutautia nguvu mkono wako kwa ndugu yako. Na tutawapa madaraka hawatawafikia. Kwa sababu ya ishara zetu, nyinyi na watakaowafuata mtashinda.

فَلَمَّا جَاءَهُم مُّوسَىٰ بِآيَاتِنَا بَيِّنَاتٍ قَالُوا مَا هَـٰذَا إِلَّا سِحْرٌ مُّفْتَرًى وَمَا سَمِعْنَا بِهَـٰذَا فِي آبَائِنَا الْأَوَّلِينَ ﴿٣٦﴾

36. Basi alipowafikia Musa na ishara zetu zilizo wazi wazi, walisema: Haya si chochote ila ni uchawi uliotungwa. Na hatukuyasikia haya kwa baba zetu wa zamani.

وَقَالَ مُوسَىٰ رَبِّي أَعْلَمُ بِمَن جَاءَ بِالْهُدَىٰ مِنْ عِندِهِ وَمَن تَكُونُ لَهُ عَاقِبَةُ الدَّارِ إِنَّهُ لَا يُفْلِحُ الظَّالِمُونَ ﴿٣٧﴾

37. Na akasema Musa: Mola wangu ndiye anayemjua kabisa nani anayekuja na uwongofu kutoka kwake na ni nani atakayekuwa na mwisho mwema wa makazi. Hakika wenye kudhulumu hawatafanikiwa.

NAHOFIA WASIJE WAKANIUA

Aya 33 – 37

MAANA

Akasema: “Mola wangu! Hakika mimi nilimuua mtu katika wao, kwa hiyo nahofia wataniua.”

Umetangulia mfano wake katika Juz. 19 (26:14).

Na ndugu yangu Harun ni fasaha zaidi kwa ulimi kuliko mimi, basi mtume pamoja nami awe msaidizi. Hakika mimi nahofia watanikadhibisha.

Hii inaashiria kuwa mwito wowote hauna budi uwe na wasaidizi. Na kwamba ilimu peke yake haitoshi kuitetea haki ikiwa haikwenda pamoja na ufasaha wa ulimi na ubainifu.

Vile vile Aya inafahamisha kuwa Qur’an inaunga mkono nyenzo za uenezaji habari; kama vile idhaa, magazeti n.k., lakini kwa sharti ya kuwa na mwelekeo wa kuithibitisha haki na kuwatetea watu wake na kuibatilisha batili na kuwatangaza wasaidizi wake; sawa na alivyoitumia Harun elimu yake na ufasaha wake dhidi ya utaghuti wa Firaun.

Imesemekana kuwa Harun ni mkubwa wa Musa kwa miaka mitatu. Sijui aliokoka vipi na kuchinjwa. Sio mbali kuwa Harun alizaliwa kabla ya Firauni kuamuru achinjwe kila mwana wa Israili atakayezaliwa. Katika Tawrat, kitabu cha Kutoka 32 imeelezwa kuwa Harun ndiye aliyewatengenezea wana wa israil ndama na kuwajengea dhabihu na wala sio Msamaria, kama ilivyoelezwa katika Qur’an Juz. 16 (20:95).

Akasema: Tutautia nguvu mkono wako kwa ndugu yako.

Mwenyezi Mungu alimwitikia Musa maombi yake, kama alivyotaka. Kauli ya Musa ya kuhofia kuuawa ameijibu Mwenyezi Mungu Mtukufu kwa kusema:

Na tutawapa madaraka hawatawafikia. Kwa sababu ya ishara zetu, nyinyi na watakaowafuata mtashinda.

Katika Juz. 16, amesema: “Msiogope! Hakika mimi niko pamoja nanyi. Nasikia na ninaona,” na hapa akasema kuwa nitawapa silaha itakayomtisha Firauni na jeshi lake na mtaneemeka kwayo nyinyi na wale watakaowaamini. Silaha hii au madaraka hayo ni ishara na miujiza; kama vile fimbo kugeuka nyoka, mkono kuwa mweupe, nzige, chawa, vyura n.k.

Basi alipowafikia Musa na ishara zetu zilizo wazi wazi, walisema: Haya si chochote ila ni uchawi uliotungwa. Na hatukuyasikia haya kwa baba zetu wa zamani.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 9 (7:109) na Juz. 16 (20:63).

Na akasema Musa: Mola wangu ndiye anayemjua kabisa nani anayekuja na uwongofu kutoka kwake na ni nani atakayekuwa na mwisho mwema wa makazi. Hakika wenye kudhulumu hawatafanikiwa.

Walimkadhibisha Musa wakamwambia ni mchawi, akawajibu kwa jawabu la asiyejali kukadhibisha kwao na inadi yao, kwa kumtegemea Mwenyezi Mungu na ahadi yake.

Kwa ufupi, jawabu ni kuwa Mwenyezi Mungu anajua kuwa mimi niko katika haki na uongofu na kwamba nyinyi mko kwenye batili na upotevu. Vile vile anajua kwamba mwisho mwema ni wangu na wanonifuata, nanyi mtapata mwisho wa maangamizi duniani na adhabu ya moto huko akhera.

وَقَالَ فِرْعَوْنُ يَا أَيُّهَا الْمَلَأُ مَا عَلِمْتُ لَكُم مِّنْ إِلَـٰهٍ غَيْرِي فَأَوْقِدْ لِي يَا هَامَانُ عَلَى الطِّينِ فَاجْعَل لِّي صَرْحًا لَّعَلِّي أَطَّلِعُ إِلَىٰ إِلَـٰهِ مُوسَىٰ وَإِنِّي لَأَظُنُّهُ مِنَ الْكَاذِبِينَ ﴿٣٨﴾

38. Na akasema Firauni: Enyi waheshimiwa! Sijui kama mnaye Mungu asiyekuwa mimi. Ewe Haman! Niwashie moto unichomee udongo, unijengee mnara nipate kumchungulia Mungu wa Musa na hakika mimi namuona yeye ni katika waongo.

وَاسْتَكْبَرَ هُوَ وَجُنُودُهُ فِي الْأَرْضِ بِغَيْرِ الْحَقِّ وَظَنُّوا أَنَّهُمْ إِلَيْنَا لَا يُرْجَعُونَ ﴿٣٩﴾

39. Na akawa na kiburi yeye na majeshi yake katika nchi bila ya haki. Na wakadhani kuwa hawatarudishwa kwetu.

فَأَخَذْنَاهُ وَجُنُودَهُ فَنَبَذْنَاهُمْ فِي الْيَمِّ فَانظُرْ كَيْفَ كَانَ عَاقِبَةُ الظَّالِمِينَ ﴿٤٠﴾

40. Basi tukamshika yeye na majeshi yake na tukawatupa baharini. Basi hebu angalia ulikuwaje mwisho wa wenye kudhulumu.

وَجَعَلْنَاهُمْ أَئِمَّةً يَدْعُونَ إِلَى النَّارِ وَيَوْمَ الْقِيَامَةِ لَا يُنصَرُونَ ﴿٤١﴾

41. Na tukawafanya ni maimamu waitao kwenye moto. Na siku ya Kiyama hawatanusuriwa.

وَأَتْبَعْنَاهُمْ فِي هَـٰذِهِ الدُّنْيَا لَعْنَةً وَيَوْمَ الْقِيَامَةِ هُم مِّنَ الْمَقْبُوحِينَ ﴿٤٢﴾

42. Na tukawafuatishia laana katika dunia hii. Na siku ya Kiyama watakuwa miongoni mwa wanaokebehiwa.

وَلَقَدْ آتَيْنَا مُوسَى الْكِتَابَ مِن بَعْدِ مَا أَهْلَكْنَا الْقُرُونَ الْأُولَىٰ بَصَائِرَ لِلنَّاسِ وَهُدًى وَرَحْمَةً لَّعَلَّهُمْ يَتَذَكَّرُونَ ﴿٤٣﴾

43. Na hakika tulimpa Musa Kitabu, baada ya kuziangamiza karne za kwanza, ili kiwafumbue macho watu na kiwe uongofu na rehema ili wapate kukumbuka.

SIJUI KAMA MNA MUNGU MWINGINE

Aya 38 – 43

MAANA

Na akasema Firauni: Enyi waheshimiwa! Sijui kama mnaye Mungu asiyekuwa mimi.

Alisema hivi kwa vile alipata wa kumsadiki. Nilihifadhi mithali tangu utotoni bado naikumbuka: “Firauni aliulizwa, ni nani Firauni wako? Akasema: Sijapata wa kunipinga”

Watu wengi wangelikuwa mafirauni lau kusingelikuweko upinzani. yatakuja maelezo katika Juz.30 (79:24).

Katika Kamusi ya Kitabu kitakatifu, imeelezwa kuwa neno Firauni ni la kimisri lenye maana ya nyumba kubwa nalo ni msimbo wa wafalme wa Misri.

Ewe Haman! Niwashie moto unichomee udongo, unijengee mnara nipate kumchungulia Mungu wa Musa na hakika mimi namuona yeye ni katika waongo.

Firauni alishindwa kuikabili hoja kwa hoja, akamuhofia Musa na fimbo yake. Akajaribu kuificha hofu yake hii na kushindwa kwake kwa kuwavun- ga watu wake kuhusu Musa, ndipo akadhihirisha shaka ya kuweko Mungu asiyekuwa yeye na kwamba yeye atamchunguza na kumtafuta. Akimpata atapambana naye; vinginevyo basi Musa atakuwa ni muongo.

Ili kusisitiza uvungaji huu machoni mwa wale walio bendera kufuata upepo, alimwambia Haman amwashie moto na atengeneze mnara mrefu utakaomwezesha kupanda mbinguni ili amtafute Mungu wa Musa.

Haman hakujenga mnara, kama tunavyodhani, kwa sababu ana yakini na vitimbi vya Firauni. Ni nani mwenye akili anayeweza kujaribu kujenga jengo lisilo na mwisho na kuwa na njozi za kuwa udongo na miti inaweza kufika kwenye mbingu za juu na kumjua aliyeko huko?

Na akawa na kiburi yeye na majeshi yake katika nchi bila ya haki. Na wakadhani kuwa hawatarudishwa kwetu.

Walijikweza juu ya watu, wakajivuna na wakaeneza ufisadi na shari. Sababu ya kwanza na ya mwisho ni kwamba wao hawamwamini Mwenyezi Mungu na siku ya mwisho, wala misingi na dhamiri. Hawaamini kitu chochote isipokuwa nafsi zao na manufaa yao. Kwa sababu hiyo Mwenyezi Mungu akawanyakua mnyakuo wa mwenye nguvu na uweza.

Basi tukamshika yeye na majeshi yake na tukawatupa baharini. Basi hebu angalia ulikuwaje mwisho wa wenye kudhulumu?

Mama yake Musa alimtupa mwanawe kwa kumhofia Firauni, lakini adui huyu wa Mungu na wa Musa akamuokota ili anufaike naye. Musa alipokuwa mkubwa alijaribu kwa juhudi zake kumnufaisha Firauni kwa kumuokoa na maangamizi na adhabu, lakini akakataa na kuwa na kiburi, ukawa mwisho wake ni kuangamia kwenye bahari ile ile aliyomuokota Musa. Katika hayo kuna mazingatio kwa wenye busara, lakini wako wapi?

Na tukawafanya ni maimamu waitao kwenye moto. Na siku ya Kiyama hawatanusuriwa.

Hao ni Firauni na majeshi yake. Maana ni kuwa wao, duniani wamepotea na kuwapoteza wengine na akhera ni wenye hasara.

Maana ya tumewajaalia ni kuwa Mwenyezi Mungu amepitisha kadari kuwa mwenye kufuata njia ya maangamizi basi ataangamia. Hilo tumelibainisha mara nyingi huko nyuma.

Imepokewa riwaya kutoka kwa Imam Jafar Assadiq(a.s) kwamba maimamu katika Kitabu cha Mwenyezi Mungu ni aina mbili: Maimamu wa uongofu ambao amewaashiria Mwenyezi Mungu (s.w.t) kwa kauli yake:

وَجَعَلْنَاهُمْ أَئِمَّةً يَهْدُونَ بِأَمْرِنَا ﴿٧٣﴾

“Na tukawafanya maimamu wakiongoza kwa amri yetu. ” Juz. 17 (21:73).

Hao wanatanguliza amri ya Mwenyezi Mungu kabla ya amri yao na hukumu yake kabla ya hukumu yao. Aina ya pili ni maimamu waitao kwenye moto, wakitanguliza amri yao kabla ya amri ya Mwenyezi Mungu na hukumu yao kabla ya hukumu ya Mwenyezi Mungu.

Vile vile wanachukua hawa zao kinyume na ilivyo katika Kitabu cha Mwenyezi Mungu.

Na tukawafuatishia laana katika dunia hii. Na siku ya Kiyama watakuwa miongoni mwa wanaokebehiwa.

Duniani wana laana ya dunia, ya Mwenyezi Mungu na ya wenye kulaani na Akhera watapata adhabu ya moto.

Na hakika tulimpa Musa Kitabu, baada ya kuziangamiza karne za kwanza, ili kiwafumbue macho watu na kiwe uongofu na rehema ili wapate kukumbuka.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) alimtermshia Musa Tawrat baada ya kuangamizwa kaumu ya Nuh, A’d na Thamud.

Lengo la kuteremshwa kwake ni kuwapa mawaidha watu na kutumia hukumu yake. Kwa sababu Tawrat, kabla ya kupotoshwa ilikuwa ni nuru, mwongozo na rehema.

Lakini Tawrat ya leo inawambia Waisraili: “ Uweni wanaume, watoto na wanawake, isipokuwa bikra, wabakisheni kwa ajili ya kustarehe nao Na mpore wanyama na milki zote... Mchome miji makazi na makambi.” kama ilivyoelezwa Kitabu cha Hisabu 32.

Je, baada ya haya kuna haja ya kuuliza kwa nini Israil imeuchoma Msikiti wa Aqsa? Itikadi ya kiyahudi ni ya shari na uadui kwa dini zote, sharia na misimamo ya kiubinadamu.

6

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI

وَمَا كُنتَ بِجَانِبِ الْغَرْبِيِّ إِذْ قَضَيْنَا إِلَىٰ مُوسَى الْأَمْرَ وَمَا كُنتَ مِنَ الشَّاهِدِينَ ﴿٤٤﴾

44. Wala wewe hukuwa upande wa magharibi tulipompa Musa amri wala hukuwa miongoni mwa walioshuhudia.

وَلَـٰكِنَّا أَنشَأْنَا قُرُونًا فَتَطَاوَلَ عَلَيْهِمُ الْعُمُرُ وَمَا كُنتَ ثَاوِيًا فِي أَهْلِ مَدْيَنَ تَتْلُو عَلَيْهِمْ آيَاتِنَا وَلَـٰكِنَّا كُنَّا مُرْسِلِينَ ﴿٤٥﴾

45. Lakini tuliziumba karne na umri ukawa mrefu juu yao. Wala hukuwa mkaazi wa watu wa Madyana ukiwasomea Aya zetu, lakini ni sisi tuliokuwa tukiwatuma Mitume.

وَمَا كُنتَ بِجَانِبِ الطُّورِ إِذْ نَادَيْنَا وَلَـٰكِن رَّحْمَةً مِّن رَّبِّكَ لِتُنذِرَ قَوْمًا مَّا أَتَاهُم مِّن نَّذِيرٍ مِّن قَبْلِكَ لَعَلَّهُمْ يَتَذَكَّرُونَ ﴿٤٦﴾

46. Wala hukuwa kando ya mlima tulipomuita. Lakini ni rehema itokayo kwa Mola wako ili uwaonye watu wasiofikiwa na muonyaji kabla yako, huenda wakakumbuka.

وَلَوْلَا أَن تُصِيبَهُم مُّصِيبَةٌ بِمَا قَدَّمَتْ أَيْدِيهِمْ فَيَقُولُوا رَبَّنَا لَوْلَا أَرْسَلْتَ إِلَيْنَا رَسُولًا فَنَتَّبِعَ آيَاتِكَ وَنَكُونَ مِنَ الْمُؤْمِنِينَ ﴿٤٧﴾

47. Na usije ukawasibu msiba kwa iliyoyatanguliza mikono yao, kisha waseme: Ewe Mola wetu! Mbona hukutuletea Mtume nasi tukafuata ishara zako na tukawa miongoni mwa waumini?

فَلَمَّا جَاءَهُمُ الْحَقُّ مِنْ عِندِنَا قَالُوا لَوْلَا أُوتِيَ مِثْلَ مَا أُوتِيَ مُوسَىٰ أَوَلَمْ يَكْفُرُوا بِمَا أُوتِيَ مُوسَىٰ مِن قَبْلُ قَالُوا سِحْرَانِ تَظَاهَرَا وَقَالُوا إِنَّا بِكُلٍّ كَافِرُونَ ﴿٤٨﴾

48. Ilipowajia haki kutoka kwetu walisema: Mbona hakupewa kama aliyopewa Musa? Je, hawakuyakataa aliyopewa Musa zamani? Walisema: ni wachawi wawili wanaosaidiana. Hakika tunawakataa wote.

قُلْ فَأْتُوا بِكِتَابٍ مِّنْ عِندِ اللَّـهِ هُوَ أَهْدَىٰ مِنْهُمَا أَتَّبِعْهُ إِن كُنتُمْ صَادِقِينَ ﴿٤٩﴾

49. Sema: Basi leteni kitabu kinachotoka kwa Mwenyezi Mungu chenye mwongozo zaidi kuliko viwili nikifuate, ikiwa nyinyi mnasema kweli.

فَإِن لَّمْ يَسْتَجِيبُوا لَكَ فَاعْلَمْ أَنَّمَا يَتَّبِعُونَ أَهْوَاءَهُمْ وَمَنْ أَضَلُّ مِمَّنِ اتَّبَعَ هَوَاهُ بِغَيْرِ هُدًى مِّنَ اللَّـهِ إِنَّ اللَّـهَ لَا يَهْدِي الْقَوْمَ الظَّالِمِينَ ﴿٥٠﴾

50. Na ikiwa hawakuitikii basi jua kuwa wamejifuatia tu hawaa zao. Na ni nani aliyepotea zaidi kuliko yule anayefuata hawaa yake bila ya mwongozo utokao kwa Mwenyezi Mungu? Hakika Mwenyezi Mungu hawongozi watu madhalimu.

وَلَقَدْ وَصَّلْنَا لَهُمُ الْقَوْلَ لَعَلَّهُمْ يَتَذَكَّرُونَ ﴿٥١﴾

51. Na kwa hakika tuliwafululizia maneno ili wapate kukumbuka.

MUHAMMAD NA HABARI ZA WALIOPITA

Aya 44 -51

MAANA

Wala wewe hukuwa upande wa magharibi tulipompa Musa amri wala hukuwa miongoni mwa walioshuhudia.

Anaambiwa Muhammad(s.a.w. w ) . Makusudio ya upande wa magharibi ni upande wa magharibi mwa mlima, kama ilivyolezwa katika Tafsir Attabari, mahali alipozungumza Mwenyezi Mungu na Musa. Ama upande wa kuume ulioashiriwa kwenye Juz. 16 (19:52), ni upande wa kuumeni wa Musa. Makusudio ya amri aliyopewa Musa ni ni kuchaguliwa kwake kwa utume na unabii.

Maana ni kuwa kutoa habari Muhammad(s.a.w.w) matukio ya Musa upande wa magharibi mwa mlima ni dalili mkataa kuwa habari hizo ni wahyi kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Kwa sababu atakuwa amepata wapi elimu ya kujua hakika hiyo ya undani na wala hajaisoma katika Kitabu, kuisikia kwa yoyote wala kushuhudia yeye mwenyewe?.

Lakini tuliziumba karne na umri ukawa mrefu juu yao.

Makusudio ya karne ni umma zilizotangulia na kuisha kati ya zama za Musa na Muhammad ambapo kuna karibu mika elfu mbili. Tazama tuliyoyafafanua katika Aya ya 7 ya Juzuu na sura hii tuliyo nayo.

Maana ni kuwa hakukubakia yeyote wa kutoa habari za umma alizoziumba Mwenyezi Mungu baina ya zama za Musa na Muhammad. Na hii ni dalili wazi kuwa elimu ya Muhammad inatokana na wahyi utokao kwa Mwenyezi Mungu.

Kwa hiyo basi muda mwingi ulipita na watu wakawa kwenye ujinga wa wajinga, wakawa wanahitajia Nabii atakayewaongoza na kuwaelekeza kwenye njia ya sawa. Ndipo Mwenyezi Mungu akamtuma Muhammad kuwa mbashiri na muonyaji, akawapa habari za watu wa umma zilizotangulia na mitume yao kwa wahyi kutoka kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu, kuwa ni dalili kwamba yeye ni Mtume kwa upande mmoja na ni mawaidha kwa upande wa pili.

Wala hukuwa mkaazi wa watu wa Madyana ukiwasomea Aya zetu, lakini ni sisi tuliokuwa tukiwatuma Mitume.

Madyana ni mji wa Shua’yb. Muhammad alimtolea habari Shua’yb, watu wake na watu wa mji wa Madyan; kama kwamba yeye ni Shua’yb akiwasomea watu wake Aya za Mwenyezi Mungu. Muhammad(s.a.w.w) hakuwa Mtume wa watu wa Madyana, lakini Mwenyezi Mungu ndiye aliyempa habari hizo kwa kuwa yeye ni mjumbe wa Mwenyezi Mungu kwa waja wake na mwenye amana ya wahyi wake.

Wala hukuwa kando ya mlima tulipomuita.

Yaani hukuwako ewe Muhammad wakati Mwenyezi Mungu alipomuita Musa kando ya mlima.

Unaweza kuuliza kuwa : hakuna tofauti baina ya kauli yake Mwenyezi Mungu: ‘kando ya mlima’ na ile iliyotangulia ‘upande wa magharibi.’ Sasa je, kuna makusudio gani ya kukaririka huku?

Jibu : Mwenyezi Mungu (s.w.t) alizungmza na Musa na kumwita zaidi ya mara moja. Kwa hiyo inawezekana kuwa Aya ya kwanza ni kuashiria mwito wa kwanza na Aya ya pili kuwa ni ya mwito wa pili. Zaidi ya hayo, kukaririka ni mfumo wa Qur’an. Tazama tuliyoyeleza kwa anuani ya

‘kukaririka katika Qur’an’ kwenye Juz. 1 (2:47 – 48) na Juz.5 (4:116 -122).

Lakini ni rehema itokayo kwa Mola wako ili uwaonye watu wasiofikiwa na muonyaji kabla yako, huenda wakakumbuka.

Mwenyezi Mungu alimtuma Muhammad kuwa ni rehema kwa walimwengu akionya na kutoa bishara kwa watu, ili wafuate njia itakayowapelekea kwenye wema wa nyumba mbili (Dunia na Akhera).

Unaweza kuuliza : Utaiunganisha vipi Aya hii na ile isemayo:

وَإِن مِّنْ أُمَّةٍ إِلَّا خَلَا فِيهَا نَذِيرٌ ﴿٢٤﴾

“Hakuna umma wowote ila alipata humo muonyaji.” (35:24).

Jibu : Tumesema mara nyingi kwamba Aya za Qur’an zinafasiriana, kwa sababu chimbuko lake ni moja. Kuna Aya isemayo:“Enyi watu wa Kitabu! Hakika amewafikia Mtume wetu anayebainishia, katika wakati usio na Mitume.” Juz. 6 (5:19), Yaani ulipokatika utumwaji mitume.

Kwa hiyo basi makusudio ya kauli yake Mwenyezi Mungu: “Wasiofikiwa na muonyaji kabla yako,” sio kuwa Mwenyezi Mungu hakupeleka mitume kabla ya Muhammad kabisa; bali makusudio ni kuwa hakufika mtume kwa kipindi fulani.

Na usije ukawasibu msiba kwa iliyoyatanguliza mikono yao, kisha waseme: Ewe Mola wetu! Mbona hukutuletea Mtume nasi tukafuata Ishara zako na tukawa miongoni mwa waumini?

Makusudio ya msiba ni adhabu ya Mwenyezi Mungu duniani. Maana ni kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) alipeleka mitume ili iwe ni hoja kwa watu pale itakapowafikia adhabu kwa sababu ya kufuru yao na utaghuti wao. Umepita mfano wake katika Juz. 6 (4:165) na (5:19).

Ilipowajia haki kutoka kwetu walisema: Mbona hakupewa kama aliyopewa Musa?

Mtume alipokuwa hajawajia walisema, akija tutuamwamini. Alipowajia wanatafuta visababu vya ubatilifu. Usumbufu na uhepaji huu hauhusiki na wale waliomkadhibisha Muhammad tu, waliomwambia Muhammad(s.a.w.w) : Lau ungekuja na fimbo na mkono mweupe wa Musa, tungelikuamini. Hapana! Haya ni mazowea ya mataghuti na wapenda anasa, kila wakati na kila mahali. Ni mazoweya ya wale ambao hawamini chochote isipokuwa masilahi yao na manufaa yao. Ndio wakawa vigeugeu na kuungana na shetani dhidi ya kila wema.

Je, kwani hao hawakuyakataa aliyopewa Musa zamani?

Walimtaka Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) kuwaletea mfano wa miujiza ya Musa; ndipo Mwenyezi Mungu (s.w.t) akawajibu kwamba mwenye kuitafuta haki kwa ajili ya haki anaifuata popote pale itakapom- bainikia. Lakini wale ambao hawaamini isipokuwa hawaa na matamanio yao na kuyafanya kuwa ndio mwongozo wao katika mambo yao yote, basi hawa haiwafai dalili na muujiza, uwe wa Musa au wa Muhammad au wa mitume wote.

Dalili ya hakika hii ni kuwa mataghuti waliyakataa aliyokuja nayo Musa; kama ambavyo mataghuti wa kikuraishi walikataa aliyokuja nayo Muhammad. Lau Musa na miujiza yake angelikuwa nafasi ya Muhammad, wangelisema: Lau Musa angelipewa mfano wa aliyopewa Muhammad. Hivi ndivyo walivyo wabatilifu, kila mhali na kila wakati.

Walisema: ni wachawi wawili wamesaidiana. Hakika sisi tunawakataa wote.

Makusudio ya wachawi wawili hapa ni Qur’an na Tawrat na kusaidiana ni kuwa kila moja inaisadikisha nyingine.

Maana ya kiujumla ni kuwa makuraishi walisema Tawrat ni uchawi na Musa ni mchawi. Vile vile wakasema Qur’an ni uchawi na Muhammad ni mchawi na kwamba wanazipinga zote mbili.

Sema: Basi leteni kitabu kinachotoka kwa Mwenyezi Mungu chenye mwongozo zaidi kuliko viwili nikifuate, ikiwa nyinyi mnasema kweli.

Tawrat ni uchawi na mfano wake Qur’an pia ni uchawi, basi ikiwa mnacho kitabu kilicho na kheri kwa watu kuliko Tawrat na Qur’an basi kileteni na mimi nitakifuata na kukitumia. Huu ni mfano wa kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu:

قُلْ إِن كَانَ لِلرَّحْمَـٰنِ وَلَدٌ فَأَنَا أَوَّلُ الْعَابِدِينَ ﴿٨١﴾

“Sema: Ingelikuwa mwingi wa rehema ana mtoto basi ningelikuwa wa kwanza kumwabudu.” (43:81).

Na ikiwa hawakuitikii basi jua kuwa wamejifuatia tu hawaa zao.

Qur’an, kwa ufasaha na balagha yake, imeshinda fasihi na balagha zote. Na imeshinda misingi na mafunzo yote ya binadamu. Hakika Qur’an kwa itikadi yake na sharia yake, inaongoza kwenye usawa zaidi. Na hii ndiyo iliyo mikononi mwa wahakiki na wasomi. Basi na walete kilicho na mwongozo zaidi kwa watu kuliko hiyo au kilicho mfano wake na waite wanayemtaka na wanachokitaka.

Ikiwa watashindwa na wasiamini, basi watakuwa hawana dalili isipokuwa upofu na upotevu unaowaongoza kwenye uovu. Haya ndiyo makusudio ya kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu:

Na ni nani aliyepotea zaidi kuliko yule anayefuata hawaa yake bila ya mwongozo utokao kwa Mwenyezi Mungu? Hakika Mwenyezi Mungu hawongozi watu madhalimu baada ya kujiingiza wenyewe na kufuata njia ya maangamizi na upotevu.

Na kwa hakika tuliwafululizia maneno ili wapate kukumbuka.

Makusudio ya maneno hapa ni Qur’an ambayo imekwishatoa onyo, haina lawama. Maana ni kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) amewaongoza waja kwenye yale wanayostahiki wao na yale yanayostahiki kwa wengine, ili wawe na utiifu na watende. Atakayetenda na akafanya uzuri, basi huyo yuko katika amani. Na adhabu ni ya mwenye kukadhibisha na akakataa.

الَّذِينَ آتَيْنَاهُمُ الْكِتَابَ مِن قَبْلِهِ هُم بِهِ يُؤْمِنُونَ ﴿٥٢﴾

52. Wale ambao tuliwapa Kitabu kabla yake wanaiamini.

وَإِذَا يُتْلَىٰ عَلَيْهِمْ قَالُوا آمَنَّا بِهِ إِنَّهُ الْحَقُّ مِن رَّبِّنَا إِنَّا كُنَّا مِن قَبْلِهِ مُسْلِمِينَ ﴿٥٣﴾

53. Na wanaposomewa, husema: Tunaiamini. Hakika hiyo ni haki inayotoka kwa Mola wetu. Hakika sisi kabla yake tulikuwa waislamu (wanyenyekevu).

أُولَـٰئِكَ يُؤْتَوْنَ أَجْرَهُم مَّرَّتَيْنِ بِمَا صَبَرُوا وَيَدْرَءُونَ بِالْحَسَنَةِ السَّيِّئَةَ وَمِمَّا رَزَقْنَاهُمْ يُنفِقُونَ ﴿٥٤﴾

53. Basi hao watapewa ujira wao mara mbili. Na wanaondoa ubaya kwa wema na wakatoa katika tuliyowaruzuku.

وَإِذَا سَمِعُوا اللَّغْوَ أَعْرَضُوا عَنْهُ وَقَالُوا لَنَا أَعْمَالُنَا وَلَكُمْ أَعْمَالُكُمْ سَلَامٌ عَلَيْكُمْ لَا نَبْتَغِي الْجَاهِلِينَ ﴿٥٥﴾

55. Na wanaposikia upuuzi hujitenga nao na husema: Sisi tuna vitendo vyetu na nyinyi mna vitendo vyenu: Salamun alaykum! Hatuwataki wajinga.

WATAPEWA UJIRA MARA MBILI

Aya 52 – 55

MAANA

Wale ambao tuliwapa Kitabu kabla yake wanaiamini.

Yaani waliopewa Kitabu kabla ya Qur’an wanaiamini hii Qur’an. Zimethibiti Hadith Mutawatir kwamba wanaswara (wakiristo) wengi na baadhi ya mayahudi walimwamini Muhammad(s.a.w.w) , kwa sababu Tawrat na Injili zimenukuu wasifu wake, kabla hazijapotolewa:

الَّذِي يَجِدُونَهُ مَكْتُوبًا عِندَهُمْ فِي التَّوْرَاةِ وَالْإِنجِيلِ ﴿١٥٧﴾

“Ambaye wanamkuta ameandikwa kwao katika Tawrat na Injili” Juz. 9 (7:157)

Umetangulia mfano wake katika Juz. 1 (2:121) na Juz. 4 (3:199).

Na wanaposomewa, husema: Tunaiamini. Hakika hiyo ni haki inayotoka kwa Mola wetu. Hakika sisi kabla yake tulikuwa waislamu (wanyenyekevu).

Maulama wa watu wa Kitabu walisoma sifa za Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) na Qur’an Tukufu katika Tawrat na injil. Walizisoma hizo kabla ya kutumilizwa Muhammad(s.a.w.w) . Alipotumilizwa aliwasomea Qur’an wakaitambua na wakamtambua Muhammad kwa sifa zake, kama zilivyo katika vitabu viwili; sawa na walivyowajua watoto wao:

الَّذِينَ آتَيْنَاهُمُ الْكِتَابَ يَعْرِفُونَهُ كَمَا يَعْرِفُونَ أَبْنَاءَهُمْ ﴿١٤٦﴾

“Wale tuliowapa Kitabu wanamjua kama wanavyowajua watoto wao.” Juz.1 (2:146).

Basi baadhi wakaamini na wengine wakaficha haki na hali wanajua, kwa kupupia vyeo na chumo.

Basi hao watapewa ujira wao mara mbili.

Wa kwanza ni kwa sababu ya ikhlasi yao katika dini yao ambayo imewaamrisha kumfuata Muhammad na Qur’an, na wa pili ni kwa walivyovumilia adha ya makafiri wapumbavu, kwa sababu kusilimu kwao kulikuwa ni hoja kubwa kwa yule anayeng’ang’ania ukafiri kwa inadi.

SUBIRA NI HEKIMA NA USHUJAA

Na wanaondoa ubaya kwa wema.

Waislamu wa mwanzo walipambana na maudhi na mateso, kiasi ambacho Muhammad(s.a.w.w) alikuwa akizomewa na wapumbavu barabarani: “Huyoo mwenda wazimu... Huyoo mwongo... Huyoo mchawi!”

Wakawa na subira wakavumilia bila ya kulalamika. Mwenyezi Mungu (s.w.t) ameiita subira yao wema na maudhi ya washirikina akayaita ubaya.

Katika ibara hii kuna ishara kuwa silaha pekee ya mnyonge ni subira na kwamba hasira na kusimamisha mishipa ni wenda wazimu na kupigana bila ya silaha ni kujitia kitanzi.

Kwa hiyo subira ya mnyonge ni akili na hekima na ni ushujaa na werevu; kwa sharti ya kuhangaika na kufanya juhudi ya kuondoa huo unyonge na visababishi vyake. Lakini atakayebweteka na kufanya uvivu atakuwa amejitweza mwenyewe na kuridhia udhalili na unyonge.

Kwa maneno mengine ni kuwa unyonge ni kama ugonjwa, ni lazima utafutiwe dawa ya kuuondoa, sio kuvumilia kubaki na ugonjwa isipokuwa baada ya kushindwa kabisa na kukata tamaa.

Na wakatoa katika tuliyowaruzuku.

Wanaondoa shari ya uovu kwa kuvumilia. Pia wanafanya wema kwa kutoa kile wanachoruzukiwa na Mwenyezi Mungu kwa fadhila zake. Imam Ali(a.s) anasema:Muadhibu ndugu yako kwa kumfanyia wema na urudishe uovu wake kwa kumneemesha.

Na wanaposikia upuuzi hujitenga nao.

Makafiri walianzisha matusi na shutuma kwa wale waliosilimu na kumwamini Mwenyezi Mungu na Mtume wake, wakavumilia na kujitia hamnazo,na husema: Sisi tuna vitendo vyete na nyinyi mna vitendo vyenu. Nyinyi mmeridhia batili mliyo nayo na sisi tumeridhia haki tuliyo nayo.

Salamun alaykum!

Wafasiri wamesema: Salamu hii ni ya kuwavumilia majahili sio ya maamkuzi; sawa na kumwambia unayetaka uepukane naye: “Niondokee kwa amani.

Hatuwataki wajinga.

Hatuchanganyiki nao wala hatuwi na hulka zao.