TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI Juzuu 20

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI0%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: Qurani tukufu

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI

Mwandishi: Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya
: HASANI MWALUPA
Kundi:

Matembeleo: 14257
Pakua: 2445


Maelezo zaidi:

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 25 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 14257 / Pakua: 2445
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI Juzuu 20

Mwandishi:
Swahili

7

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI

إِنَّكَ لَا تَهْدِي مَنْ أَحْبَبْتَ وَلَـٰكِنَّ اللَّـهَ يَهْدِي مَن يَشَاءُ وَهُوَ أَعْلَمُ بِالْمُهْتَدِينَ ﴿٥٦﴾

56. Kwa hakika wewe humuongoi umtakaye, lakini Mwenyezi Mungu humuongoa amtakaye naye ndiye anayewajua zaidi waongokao.

وَقَالُوا إِن نَّتَّبِعِ الْهُدَىٰ مَعَكَ نُتَخَطَّفْ مِنْ أَرْضِنَا أَوَلَمْ نُمَكِّن لَّهُمْ حَرَمًا آمِنًا يُجْبَىٰ إِلَيْهِ ثَمَرَاتُ كُلِّ شَيْءٍ رِّزْقًا مِّن لَّدُنَّا وَلَـٰكِنَّ أَكْثَرَهُمْ لَا يَعْلَمُونَ ﴿٥٧﴾

57. Na wakasema: Tukifuata muongozo huu pamoja nawe, tutanyakuliwa kutoka nchi yetu. Je, kwani hatukuwaweka imara mahali patakatifu pa amani, panapoletwa matunda ya kila aina kuwa ni riziki itokayo kwetu? Lakini wengi wao hawajui.

وَكَمْ أَهْلَكْنَا مِن قَرْيَةٍ بَطِرَتْ مَعِيشَتَهَا فَتِلْكَ مَسَاكِنُهُمْ لَمْ تُسْكَن مِّن بَعْدِهِمْ إِلَّا قَلِيلًا وَكُنَّا نَحْنُ الْوَارِثِينَ ﴿٥٨﴾

58. Na ni miji mingapi iliyojifaharisha maisha yake tumeiangamiza! Na hayo maskani yao hayakukaliwa tena baada yao ila kwa uchache tu. Na sisi ndio tumekuwa warithi.

وَمَا كَانَ رَبُّكَ مُهْلِكَ الْقُرَىٰ حَتَّىٰ يَبْعَثَ فِي أُمِّهَا رَسُولًا يَتْلُو عَلَيْهِمْ آيَاتِنَا وَمَا كُنَّا مُهْلِكِي الْقُرَىٰ إِلَّا وَأَهْلُهَا ظَالِمُونَ ﴿٥٩﴾

59. Na Mola wako haangamizi miji mpaka ampeleke Mtume katika mji wao mkuu awasomee Aya zetu. Wala hatuiangamizi miji mpaka watu wake wawe madhalimu.

وَمَا أُوتِيتُم مِّن شَيْءٍ فَمَتَاعُ الْحَيَاةِ الدُّنْيَا وَزِينَتُهَا وَمَا عِندَ اللَّـهِ خَيْرٌ وَأَبْقَىٰ أَفَلَا تَعْقِلُونَ ﴿٦٠﴾

60. Na chochote mlichopewa ni matumizi ya maisha ya dunia na pambo lake. Na yaliyoko kwa Mwenyezi Mungu ndio bora na yatakayobaki zaidi. Basi je, hamfahamu?

أَفَمَن وَعَدْنَاهُ وَعْدًا حَسَنًا فَهُوَ لَاقِيهِ كَمَن مَّتَّعْنَاهُ مَتَاعَ الْحَيَاةِ الدُّنْيَا ثُمَّ هُوَ يَوْمَ الْقِيَامَةِ مِنَ الْمُحْضَرِينَ ﴿٦١﴾

61. Je yule tuliyemuahidi ahadi nzuri tena naye akaipata, ni kama tuliyemstarehesha kwa starehe za maisha ya duniani na kisha siku ya Kiyama akawa miongoni mwa wanaohudhurishwa?

HUWEZI KUMUONGOA UMTAKAYE

Aya 56 - 61

MAANA

ABU TWALIB NA UISLAMU

Kwa hakika wewe humuongoi umtakaye, lakini Mwenyezi Mungu humuongoa amtakaye, naye ndiye anayewajua zaidi waongokao.

Wametofautiana katika sababu ya kushuka Aya hii. Wakasema wafisri wengi katika Sunni kuwa ilishuka kwa ajili ya ami wa Mtume, Abu Twalib. Shia wakasema Aya haikumuhusu yeye wala mwinginewe. Mtume(s.a.w.w) anapenda kila mmoja aongoke, awe ni wa karibu naye au wa mbali naye. Herufi man, katika Aya ni ya kuenea.

Kuitumia Aya kwa kumhusu Abu Twalib peke yake, hiyo itakuwa ni kuyatumia maneno ya Mwenyezi Mungu bila ya dalili. Ama riyawa inayosema kuwa Aya imeshuka kwa Abu Twalib peke yake, hiyo haikuthibiti kwetu.

Kwa hiyo basi Aya hii itakuwa inarudufu Aya nyingine isemayo: “Je, wewe unaweza kuwaongoza vipofu ingawa hawaoni? Juz. 13 (10:43).

Mwenye Tafsiri Fii dhilal amerefusha maneno, kisha akaishia kwenye madhehebu ya mababa na mababu, akategemea dalili za wakale ingawaje zinapingana na maumbile ya kiakili.

Naye amekariri mara kadhaa kuwa Qur’an inazungumza na umbile la akili kwa undani. Nasi tutayahukumu maneno yake kwa mahakama ya maumbile ya kiakili na ya kimaudhui, sio ya kimadhehebu wala ya kiupendeleo. Tunamtarajia msomaji aangalie kauli yetu kwa mtazamo wa kielimu usiokuwa na upendeleo.

Anasema mwenye Fii dhilal, ninamnukuu: “Huyu ami wa Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) , mlezi wake muhami wake na mgombezi wake, Mwenyezi Mungu hamwandikii imani, ingawaje anampenda sana Mtume wa Mwenyezi Mungu na Mtume wa Mwenyezi Mungu naye anampenda sana, Mwenyezi Mungu hamwandikii kuamini.

Maana ya kauli hii ni kuwa Mwenyezi Mungu alichukia Abu Twalib kusema: Lailaha illa llah, Muhammadu rrasulullah (Hapana mola isipokuwa Mwenyezi Mungu na Muhammad ni Mtume wa Mwenyezi Mungu), lakini Mtume wa Mwenyezi Mungu alipenda na kung’ang’ani aseme kauli hii.

Tunauliza: Inaingilika akilini kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu apende jambo ambalo Mwenyezi Mungu analichukia? Basi kwa nini Mwenyezi Mungu ameilinganisha sawa twaa yake na ya Mtume, kwenye Aya kadhaa? Ikiwa Mwenyezi Mungu amechukia Abu Twalib asilimu na wala hakumwandikia kusilimu, basi kwanini amwadhibu na amuweke kwenye moto wa ‘juu juu’ kama walivyopokea wazushi? Je, inafaa mwenye nguvu kumwadhibu mnyonge kwa jambo ambalo hakulifanya? Itakuwaje na hali yeye ndiye alisema: “Na mimi si mwenye kuwadhulumu waja?”

Kwa nini Mwenyezi Mungu apende Abu Sufyani asilimu, lakini achukie kwa Abu Twalib? Ni kwa sababu Abu Sufyan alikuwa akimchukia sana Mtume, na kumkusanyia majeshi ya kumpiga vita, akapenda awe mwislamu, lakini Abu Twalib aliyempenda sana Mtume na kumuhami ndio akachukia kuwa mwislamu? Au ni kwa sababu Abu Sufyan ni mzazi wa Muawiya na Abu Twalib ni mzazi wa Ali?

Majibu ya maswali yote haya ni ndio kwa wale wanaodai kuwa Abu Twalib ni kafiri. Kwa sababu wao wanaamini kuwa Mwenyezi Mungu hawajibikiwi na lolote na wala kwake hakuna jambo baya, na kwamba inafaa kwake kuwaadhibu wema; na wale wanaomwaga damu za watu kuwafanya ni wema.

Je, mwenye Fii dhilal alikusudia kuwa maana haya ndiyo yametokana na umbile la akili la ndani?

Zaidi ya hayo, kuandika tafsiri na isiyokuwa tafsiri kunaathirika na itikadi, mazingira, utamuduni na hali ya mwandishi. Na hili halimwachi mdogo wala mkubwa. Lakini hii haina maana kwamba itikadi na mapondokeo yote hayaafikiani na haki na hali halisi. Vinginevyo ingelikuwa muhali kauli ya haki na uadilifu. Ni wajibu kwa mtu kujitahidi kuitafuta haki kutokana na chimbuko lake, si kutokana na itikadi au mazingira. Na haya ndiyo tunayojaribu na kuyakusudia.

Misitari hii tunaiunganisha na tuliyoyaandika kuhusiana na maudhui haya katika Juz. 11 (9:113).

Na wakasema: Tukifuata muongozo huu pamoja nawe, tutanyakuliwa kutoka nchi yetu.

Kuna riwaya isemayo kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) alisema: “Naapa kwa yule ambaye nafsi yangu iko mikononi mwake! Jambo hili nitalitolea mwito kwa mweusi na mweupe, kwa aliye juu ya kilele cha mlima na aliye kwenye kilindi cha maji na nitawatolea mwito watu wa Fursi na Roma.”

Basi vigogo wa kikuraishi waliposikia maneno haya wakayakuza na kumwambia Mtume(s.a.w.w) ; “Vipi tukufuate na wewe nia yako ni hii. Kama tutakuitikia, basi kutakuwa na watu wengi wakiwemo wafursi na waroma na watachukua mali zetu na miji yetu na wataivunja Al-Kaa’ba vipande vipande.”

Iwe ni sahihi riwaya au la, lakini madhumuni yake yanendana na Aya hii. Kwani Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) alimlingani mweusi na mweupe, akaendelea na mwito wake. Vigogo wa kikuraishi wakampiga vita.

Zaidi ya hayo pia riwaya inaafikiana na kauli yake Mwenyezi Mungu inayofuatia:

Je, kwani hatukuwaweka imara mahali patakatifu pa amani, panapoletwa matunda ya kila aina kuwa ni riziki itokayo kwetu?

Vipi nyinyi watu wa Makka mnawahofia watu na hali Mwenyezi Mungu (s.w.t) ameulinda mji wenu huu na mauaji na uporaji tangu siku ya kwanza? Na akajaalia nyoyo za watu zinauelekea mji huu wakileta kila aina ya matunda na mambo mazuri?

Lakini wengi wao hawajui kwamba Mwenyezi Mungu (s.w.t) ameuhusisha mji huu na sifa hizi kuliko miji mingine.

Na ni miji mingapi iliyojifaharisha maisha yake tumeiangamiza! Na hayo maskani yao hayakukaliwa tena baada yao ila kwa uchache tu. Na sisi ndio tumekuwa warithi.

Walimwambia Mtume wa Mwenyezi Mungu kuwa tunawahofia watu kama tutakufuata wewe, akawajibu Mwenyezi Mungu, katika Aya iliyotangulia, kuwa mnahofia watu na hali Mwenyezi Mungu ameujalia mji wenu huu ni mtakatifu na wa amani?

Kisha katika Aya hii anawauliza, mnawahofia watu badala ya kumhofia Mwenyezi Mungu? Je, hampati mazingatio kwa umma zilizopita ambazo zilifanya jeuri na kuzikufuru neema za Mwenyezi Mungu, ndipo Mwenyezi Mungu akaziangamiza kwa sababu ya kuzikufuru neema zake, wakaacha miji yao ni magofu isipokuwa michache tu, lakini mingi ikawa haina warithi ila yule atakayeirithi ardhi na waliomo juu yake na kwake ndio marejeo.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 16 (20:128).

Na Mola wako haangamizi miji mpaka ampeleke Mtume katika mji wao mkuu awasomee Aya zetu. Wala hatuiangamizi miji mpaka watu wake wawe madhalimu.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) ni mwadilifu na ni hakimu hamwadhibu yoyote ila baada ya mawaidha na kuhadharishwa.

Unaweza kuuliza : Dhahiri ya Aya inaonyesha kuwa Mwenyezi Mungu hatumi Mtume katika miji midogo au kama akituma mtume basi watu wake hatawaadhibu kama hawatamsikiliza. Na hii haielekiani na misingi ya usawa katika taklifa na wajibu. Sasa itakuwaje?

Jibu : Aya imekuja kwenye mfumo wa aghlab. Kwani mitume wengi walitumwa kwenye miji mikubwa na kila Mtume alikuwa akituma muongoza- ji kwenye miji midogo. Umetangulia mfano wake katika Juz. 7 (6:6) na Juz. 12 (11:118).

Na chochote mlichopewa ni matumizi ya maisha ya dunia na pambo lake. Na yaliyoko kwa Mwenyezi Mungu ndio bora na yatakayobaki zaidi. Basi je, hamfahamu?

Matumizi mabaya ya maisha ya dunia ni yale yanayomfanya mtu kuwa jeuri na kueneza ufisadi. Vingenevyo hakuna uharamu wa mapambo ya Mwenyezi Mungu na riziki njema isipokuwa kwa asiyejua dini ya Mwenyezi Mungu. Umetangulia mfano wake katika Juz. 1 (2: 103) na Juz.5 (4:77).

Je yule tuliyemuahidi ahadi nzuri tena naye akaipata, ni kama tuliyemstarehesha kwa starehe za maisha ya duniani na kisha siku ya Kiyama akawa miongoni mwa wanaohudhurishwa?

Mwenyezi Mungu aliwaahidi wale ambao wameamini na wakatenda mema Pepo ambazo hupita mito chini yake. Mwenyezi Mungu atatekeleza ahadi yake tu. Hakuna shaka kwamba mwenye kuneemeka na pepo ya milele hawezi kufananishwa na mwenye kustarehe hapa duniani kisha apelekwe Jahannam.

وَيَوْمَ يُنَادِيهِمْ فَيَقُولُ أَيْنَ شُرَكَائِيَ الَّذِينَ كُنتُمْ تَزْعُمُونَ ﴿٦٢﴾

62. Na siku atakapowaita na akasema: Wako wapi mliokuwa mkidai kuwa ni washirika wangu.

قَالَ الَّذِينَ حَقَّ عَلَيْهِمُ الْقَوْلُ رَبَّنَا هَـٰؤُلَاءِ الَّذِينَ أَغْوَيْنَا أَغْوَيْنَاهُمْ كَمَا غَوَيْنَا تَبَرَّأْنَا إِلَيْكَ مَا كَانُوا إِيَّانَا يَعْبُدُونَ ﴿٦٣﴾

63. Watasema wale iliyothibiti juu yao kauli: Mola wetu! Hawa ndio tuliowapoteza. Tuliwapoteza kama tulivyopotea sisi. Tunajitenga nao mbele yako. Hawakuwa wakituabudu sisi.

وَقِيلَ ادْعُوا شُرَكَاءَكُمْ فَدَعَوْهُمْ فَلَمْ يَسْتَجِيبُوا لَهُمْ وَرَأَوُا الْعَذَابَ لَوْ أَنَّهُمْ كَانُوا يَهْتَدُونَ ﴿٦٤﴾

64. Na itasemwa: Waiteni waungu wenu wa kishirikina. Basi watawaita, lakini hawatawaitikia. Na wataiona adhabu; laiti wangelikuwa wameongoka.

وَيَوْمَ يُنَادِيهِمْ فَيَقُولُ مَاذَا أَجَبْتُمُ الْمُرْسَلِينَ ﴿٦٥﴾

65. Na siku atakapowaita na akasema: Mliwajibu nini Mitume.

فَعَمِيَتْ عَلَيْهِمُ الْأَنبَاءُ يَوْمَئِذٍ فَهُمْ لَا يَتَسَاءَلُونَ ﴿٦٦﴾

66. Basi zitawapotea habari siku hiyo. Nao hawataulizana.

فَأَمَّا مَن تَابَ وَآمَنَ وَعَمِلَ صَالِحًا فَعَسَىٰ أَن يَكُونَ مِنَ الْمُفْلِحِينَ ﴿٦٧﴾

67. Ama mwenye kutubu na akaamini na akatenda mema, asaa akawa miongoni mwa wenye kufanikiwa.

وَرَبُّكَ يَخْلُقُ مَا يَشَاءُ وَيَخْتَارُ مَا كَانَ لَهُمُ الْخِيَرَةُ سُبْحَانَ اللَّـهِ وَتَعَالَىٰ عَمَّا يُشْرِكُونَ ﴿٦٨﴾

68. Na Mola wako huumba na huteua atakavyo; hawana hiyari. Mwenyezi Mungu ametukuka na ametakasika na hao wanaowashirikisha naye.

وَرَبُّكَ يَعْلَمُ مَا تُكِنُّ صُدُورُهُمْ وَمَا يُعْلِنُونَ ﴿٦٩﴾

69. Na Mola wako anayajua yaliyoficha vifua vyao na wanayoyatangaza.

وَهُوَ اللَّـهُ لَا إِلَـٰهَ إِلَّا هُوَ لَهُ الْحَمْدُ فِي الْأُولَىٰ وَالْآخِرَةِ وَلَهُ الْحُكْمُ وَإِلَيْهِ تُرْجَعُونَ ﴿٧٠﴾

70. Naye ni Mwenyezi Mungu, hapana mungu isipokuwa yeye. Ni zake sifa njema, mwanzo na mwisho na hukumu ni yake na kwake yeye mtarejeshwa.

WAKO WAPI WASHIRIKA WANGU

Aya 62 – 70

MAANA

Na siku atakapowaita na akasema: Wako wapi mliokuwa mkidai kuwa ni washirika wangu.

Kesho Mwenyezi Mungu (s.w.t) atawafufua waabudu mizimu, vyeo na mali awaulize kwa kuwatahayariza, wako wapi mliokuwa mkiwatumikia na kuwasafia matendo yenu badala ya Mwenyezi Mungu?

Watasema wale iliyothibiti juu yao kauli: Mola wetu! Hawa ndio tuliowapoteza. Tuliwapoteza kama tulivyopotea sisi. Tunajitenga nao mbele yako. Hawakuwa wakituabudu sisi.

Makusudio ya waliothibitikiwa na kauli ni viongozi wa ushirikina na upotevu. Makusudio ya kauli ni tamko la adhabu lilikuja katika Aya isemayo:

قَالُوا بَلَىٰ وَلَـٰكِنْ حَقَّتْ كَلِمَةُ الْعَذَابِ عَلَى الْكَافِرِينَ ﴿٧١﴾

“Lakini limekwishathibiti neno la adhabu juu yao” (39:71).

Neno ‘Hawa’ ni ishara ya wafuasi wadhaifu.

Maana ni kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) wakati atakapowauliza washirikina, wako wapi washirika wangu, wanyonge watajibu: Ewe Mola wetu! Sisi tuliwatii wakubwa zetu wakatupoteza njia.

Wakubwa nao watasema: Hapana, hatukuwalazimisha kufuata ushirikina na upotevu, lakini tuliwaita nao wakaitikia kwa hiyari yao; sawa na sisi tuliyoyaitikia matamanio yetu na kuyatii.

Nasi tunajitenga nao na matendo yao. Hawakuwa wakituabudu sisi, isipokuwa walikuwa wakiabudu masanamu na mashetani.

Hivi ndivyo wanavyofanya watu wa masilahi, wanawadanganya wapumbavu na wajinga na kuwafanya ni njia ya kupatia mlengo yao; mpaka yakiwafika wanawaruka.

Hawa watawaambia kama atakavyosema shetani kesho:

وَمَا كَانَ لِيَ عَلَيْكُم مِّن سُلْطَانٍ إِلَّا أَن دَعَوْتُكُمْ فَاسْتَجَبْتُمْ لِي فَلَا تَلُومُونِي وَلُومُوا أَنفُسَكُم ﴿٢٢﴾

“Na sikuwa na mamlaka juu yenu, isipokuwa niliwaita mkaniitikia. Basi msinilaumu mimi, bali jilaumuni wenyewe” Juz. 13 (14:22)

إِنِّي بَرِيءٌ مِّنكُمْ إِنِّي أَخَافُ اللَّـهَ وَاللَّـهُ شَدِيدُ الْعِقَابِ ﴿٤٨﴾

“Mimi si pamoja nanyi... Mimi namwogopa Mwenyezi Mungu na Mwenyezi Mungu ni mkali wa kuadhibu” Juz. 10 (8:48)

Na itasemwa: Waiteni waungu wenu wa kishirikina.

Itasemwa kesho kwa wasaidizi wa dhulma na wafuasi wao, wako wapi wale mliokuwa mkiwaabudu badala ya Mwenyezi Mungu, waiteni waje wawaokoe na adhabu.

Basi watawaita, lakini hawatawaitikia.

Amedhoofika muombaji na anayeombwa.

Na wataiona adhabu; laiti wangelikuwa wameongoka.

Watajua kuwa adhabu inakuja tu. Hapo watatamani lau wangelikuwa waumini.

Na siku atakapowaita na akasema: Mliwajibu nini Mitume.

Mara ya pili Mwenyezi Mungu (s.w.t) anawauliza kwa kukusudia kuwatahayariza kuwa niliwaletea mitume wangu wakawasomea Aya zangu na wakawaonya na kukutana kwenu na siku hii, basi mtafanya nini? Je, mliwaitikia na mkawatii au mliwapinga na kuwaasi?

Basi zitawapotea habari siku hiyo.

Watakuwa hawana la kujibu kwa jinsi watakavyopigwa na butwaa.

Nao hawataulizana.

Hawataulizana kuhusu litakalowaokoa na adhabu. Vipi wataulizana na hali wao wamekata tamaa na kila kitu.

Ama mwenye kutubu na akaamini na akatenda mema, asaa akawa miongoni mwa wenye kufanikiwa.

Hii ni desturi ya Qur’an – kuuunganisha kutaja utiifu na thawabu zake uasi na adhabu yake na kinyume chake.

Neno‘asaa’ katika maneno ya viumbe linafahamisha kutarajia kitu kinachopendwa na kuhurumia jambo linalochukiza. Ama katika maneno ya muumba linafahamisha ulazima na uhakika. Kwa hiyo basi ni uhakika kuwa mwenye kutubia aliye mwema ni katika wenye kufaulu na wenye kuridhiwa mbele ya Mwenyezi Mungu.

Na Mola wako huumba na huteua atakavyo; hawana hiyari. Mwenyezi Mungu ametukuka na ametakasika na hao wanaowashirikisha naye.

Mwenyezi Mungu ndiye muumba na ni mmliki, hakuna anayemiliki kitu kwake. Vitendo vyake vyote ni hekima, heri na usawa. Hakuna yeyote anayeweza kupinga na kutaaradhi, basi vipi wanamnasibishia washirikina?

Na Mola wako anayajua yaliyoficha vifua vyao na wanayoyatangaza.

Vile vile yeye ni mjuzi wa ghaibu na dhahiri na washirika wanaodaiwa hawajui kitu.

Naye ni Mwenyezi Mungu, hapana mungu isipokuwa yeye peke yake, mwenye kustahiki ibada. Ni zake sifa njema, mwanzo na mwisho.

Sifa njema ni za Mwenyezi Mungu duniani kutokana na fadhila zake na katika akhera kwa thawabu zake.

Na hukumu ni yake yenye kutokeza katika kila kitu. Na kwake yeye mtarejeshwa.

Wala haiwezekani kulikimbia hili. Mwema ni yule ambaye zitathibiti hoja zake na kukubaliwa udhuru wake.

8

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI

قُلْ أَرَأَيْتُمْ إِن جَعَلَ اللَّـهُ عَلَيْكُمُ اللَّيْلَ سَرْمَدًا إِلَىٰ يَوْمِ الْقِيَامَةِ مَنْ إِلَـٰهٌ غَيْرُ اللَّـهِ يَأْتِيكُم بِضِيَاءٍ أَفَلَا تَسْمَعُونَ ﴿٧١﴾

71. Sema: Mwaonaje, kama Mwenyezi Mungu angeliufanya usiku uwakalie moja kwa moja mpaka siku ya Kiyama, mungu gani asiyekuwa Mwenyezi Mungu atakayewaletea mwangaza basi je, hamsikii.

قُلْ أَرَأَيْتُمْ إِن جَعَلَ اللَّـهُ عَلَيْكُمُ النَّهَارَ سَرْمَدًا إِلَىٰ يَوْمِ الْقِيَامَةِ مَنْ إِلَـٰهٌ غَيْرُ اللَّـهِ يَأْتِيكُم بِلَيْلٍ تَسْكُنُونَ فِيهِ أَفَلَا تُبْصِرُونَ ﴿٧٢﴾

72. Sema: Mwaonaje, kama Mwenyezi Mungu angeliufanya mchana uwakalie moja kwa moja mpaka siku ya Kiyama, mungu gani asiyekuwa Mwenyezi Mungu atakayewaletea usiku mkapumzika humo? Basi je, hamwoni?

وَمِن رَّحْمَتِهِ جَعَلَ لَكُمُ اللَّيْلَ وَالنَّهَارَ لِتَسْكُنُوا فِيهِ وَلِتَبْتَغُوا مِن فَضْلِهِ وَلَعَلَّكُمْ تَشْكُرُونَ ﴿٧٣﴾

73. Na katika rehema zake amewafanyia usiku na mchana mpate kupumzika humo na mtafute fadhila zake na ili mpate kushukuru.

وَيَوْمَ يُنَادِيهِمْ فَيَقُولُ أَيْنَ شُرَكَائِيَ الَّذِينَ كُنتُمْ تَزْعُمُونَ ﴿٧٤﴾

74. Na siku atakapowaita na akasema: Wako wapi mliokuwa mkidai kuwa ni washirika wangu.

وَنَزَعْنَا مِن كُلِّ أُمَّةٍ شَهِيدًا فَقُلْنَا هَاتُوا بُرْهَانَكُمْ فَعَلِمُوا أَنَّ الْحَقَّ لِلَّـهِ وَضَلَّ عَنْهُم مَّا كَانُوا يَفْتَرُونَ ﴿٧٥﴾

75. Na tutatoa shahidi katika kila umma na tuseme: Leteni hoja zenu! Hapo watajua kwamba hakika haki ni ya Mwenyezi Mungu na yatawapotea yale waliyokuwa wakiyazua.

HEKIMA YA USIKU NA MCHANA

Aya 71 – 75

MAANA

Sema: Mwaonaje, kama Mwenyezi Mungu angeliufanya usiku uwakalie moja kwa moja mpaka siku ya Kiyama, mungu gani asiyekuwa Mwenyezi Mungu atakayewaletea mwangaza basi je, hamsikii.

Binadamu hufanya kazi na kupumzika kwa usingizi. Kazi inahitajia mwangaza na usingizi kwenye giza unakuwa mzito na unaleta siha ya mwili.

Ndio Mwenyezi Mungu (s.w.t) akaumba mchana kwa ajili ya kufanya kazi na usiku kwa ajili ya kupumzika. Lau usiku ungeliendelea bila ya asubuhi au mchana ukaendelea bila ya usiku basi maisha yangelikuwa balaa.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) alipotaja usiku amesema: ‘Hamsikii?’ na mchana akasema: ‘Hamuoni?’ kwa sababu usiku unanasibiana na kusikia na mchana kwa kuona.

Huko nyuma tumesema kuwa kufuatana usiku na mchana kunategemezwa moja kwa moja kwenye sababu zake za kimaumbile na kunategemezwa kwa Mwenyezi Mungu kwa kupitia hizo sababu, kwa vile yeye ndiye muumba wa ulimwengu na vilivyomo, na ndiye aliyeupangilia vizuri kwa hekima yake.

Na katika rehema zake amewafanyia usiku na mchana mpate kupumzika humo na mtafute fadhila zake na ili mpate kushukuru.

Yaani amewafanyia usiku mpumzike na amewafanyia mchana mtafute. Umetangulia mfano wake katika Juz. 11 (10:67), Juz. 15 (17:12) na Juz. 19 (25:47).

Na siku atakapowaita na akasema: Wako wapi mliokuwa mkidai kuwa ni washirika wangu.

Imetangulia punde tu katika Sura hii tuliyo nayo Aya 62. hatujui wajihi wa kukaririka huku isipokuwa kuthibitisha na kusisitiza.

Na tutatoa shahidi katika kila umma na tuseme: Leteni hoja zenu!

Kesho Mwenyezi Mungu (s.w.t) kila umma atauletea nabii wao atoe ushahidi juu yao kuwa alifikisha ujumbe na aeleze upinzani alioupata na kukadhibishwa baada ya kuwawasilishia hoja na kukata nyudhuru zote. Hapo Mwenyezi Mungu (s.w.t) atasema Mtume amenieleza yake, haya nanyi elezeni yenu na kile kilichowafanya muwakadhibishe; sawa na hakimu anavyofanya–kwanza anamsikiliza mwenye madai kisha mshatikiwa anajibu.

Hapo wataziba mdomo wabatilifu na adhabu itawastahili. Umetangulia mfano wake katika Juz. 2 (2:143), Juz. 14 (16:89).

Hapo watajua kwamba hakika haki ni ya Mwenyezi Mungu.

Yaani watajua kuwa hoja ya Mungu itawasimamia juu yao na wao hawatakuwa na hoja kwa Mwenyezi Mungu.

Na yatawapotea yale waliyokuwa wakiyazua, kuwa Mwenyezi Mungu ana mshirika na uwongo walioueneza juu ya watu wema.

إِنَّ قَارُونَ كَانَ مِن قَوْمِ مُوسَىٰ فَبَغَىٰ عَلَيْهِمْ وَآتَيْنَاهُ مِنَ الْكُنُوزِ مَا إِنَّ مَفَاتِحَهُ لَتَنُوءُ بِالْعُصْبَةِ أُولِي الْقُوَّةِ إِذْ قَالَ لَهُ قَوْمُهُ لَا تَفْرَحْ إِنَّ اللَّـهَ لَا يُحِبُّ الْفَرِحِينَ ﴿٧٦﴾

76. Hakika Qaruni alikuwa katika kaumu ya Musa, lakini aliwafanyia dhulma. Na tulimpa hazina ambazo funguo zake ziliwaelemea kundi la watu wenye nguvu. walipomwambia watu wake: Usijigambe, hakika Mwenyezi Mungu hapendi wanaojigamba.

وَابْتَغِ فِيمَا آتَاكَ اللَّـهُ الدَّارَ الْآخِرَةَ وَلَا تَنسَ نَصِيبَكَ مِنَ الدُّنْيَا وَأَحْسِن كَمَا أَحْسَنَ اللَّـهُ إِلَيْكَ وَلَا تَبْغِ الْفَسَادَ فِي الْأَرْضِ إِنَّ اللَّـهَ لَا يُحِبُّ الْمُفْسِدِينَ ﴿٧٧﴾

77. Na utafute kwa aliyokupa Mwenyezi Mungu makazi ya akhera; wala usisahau fungu lako la dunia. Na fanya wema kama alivyokufanyia wema Mwenyezi Mungu, wala usitafute ufisadi katika ardhi; hakika Mwenyezi Mungu hapendi wafisadi.

قَالَ إِنَّمَا أُوتِيتُهُ عَلَىٰ عِلْمٍ عِندِي أَوَلَمْ يَعْلَمْ أَنَّ اللَّـهَ قَدْ أَهْلَكَ مِن قَبْلِهِ مِنَ الْقُرُونِ مَنْ هُوَ أَشَدُّ مِنْهُ قُوَّةً وَأَكْثَرُ جَمْعًا وَلَا يُسْأَلُ عَن ذُنُوبِهِمُ الْمُجْرِمُونَ ﴿٧٨﴾

78. Akasema: Kwa hakika nimepewa haya kwa sababu ya elimu niliyo nayo. Je, hakujua kwamba Mwenyezi Mungu amekwishaangamiza karne zilizokuwa kabla yake waliokuwa na nguvu zaidi kuliko yeye na wenye makundi makubwa zaidi. Na wakosefu hawataulizwa dhambi zao.

فَخَرَجَ عَلَىٰ قَوْمِهِ فِي زِينَتِهِ قَالَ الَّذِينَ يُرِيدُونَ الْحَيَاةَ الدُّنْيَا يَا لَيْتَ لَنَا مِثْلَ مَا أُوتِيَ قَارُونُ إِنَّهُ لَذُو حَظٍّ عَظِيمٍ ﴿٧٩﴾

79. Basi akawatokea watu wake katika pambo lake. Wakasema wale waliokuwa wanataka maisha ya duniani: Laiti tungelikuwa nayo kama aliyopewa Qaruni! Hakika yeye ni mwenye bahati kubwa.

وَقَالَ الَّذِينَ أُوتُوا الْعِلْمَ وَيْلَكُمْ ثَوَابُ اللَّـهِ خَيْرٌ لِّمَنْ آمَنَ وَعَمِلَ صَالِحًا وَلَا يُلَقَّاهَا إِلَّا الصَّابِرُونَ ﴿٨٠﴾

80. Na wakasema wale ambao wamepewa elimu: Ole wenu! Thawabu za Mwenyezi Mungu ni bora kwa mwenye kuamini na akatenda. Na wala hawatapewa isipokuwa wenye subira.

فَخَسَفْنَا بِهِ وَبِدَارِهِ الْأَرْضَ فَمَا كَانَ لَهُ مِن فِئَةٍ يَنصُرُونَهُ مِن دُونِ اللَّـهِ وَمَا كَانَ مِنَ الْمُنتَصِرِينَ ﴿٨١﴾

81. Basi tukamdidimiza yeye na nyumba yake ardhini; wala hapakuwa na kundi lolote la kumsaidia kinyume na Mwenyezi Mungu wala hakuwa miongoni mwa wanaojisaidia.

وَأَصْبَحَ الَّذِينَ تَمَنَّوْا مَكَانَهُ بِالْأَمْسِ يَقُولُونَ وَيْكَأَنَّ اللَّـهَ يَبْسُطُ الرِّزْقَ لِمَن يَشَاءُ مِنْ عِبَادِهِ وَيَقْدِرُ لَوْلَا أَن مَّنَّ اللَّـهُ عَلَيْنَا لَخَسَفَ بِنَا وَيْكَأَنَّهُ لَا يُفْلِحُ الْكَافِرُونَ ﴿٨٢﴾

82. Na wakawa wanasema wale waliotamani mahala pake jana: Kumbe Mwenyezi Mungu humkunjulia riziki amtakaye, katika waja wake, na humdhikisha amtakaye. Asingetufanyia hisani Mwenyezi Mungu angelitudidimiza. Kumbe makafiri hawafanikiwi.

QARUNI NA UKANDAMIZAJI WA KIBEPARI

Aya 76 – 82

MAANA

Hakika Qaruni alikuwa katika kaumu ya Musa, lakini aliwafanyia dhulma. Na tulimpa hazina ambazo funguo zake ziliwaelemea kundi la watu wenye nguvu.

Qaruni alikuwa katika wana wa Israil, kwa sababu yeye alikuwa katika kaumu ya Musa. Inasemekana alikuwa ni binamu yake. Yeye ndiye aliyeweka jiwe la msingi la ubepari wa ukandamizaji au alikuwa ni mwakilishi wake. Kwa sababu yeye alihodhi na akawatawala watu wake, akilitetea hilo kwa kauli yake: “Nimepewa haya kwa sababu ya elimu niliyo nayo,” kama zinazosema Aya zinazofuatia.

Haya ndio madhehebu ya kiuchumi yasemayo: Mtu binafsi kwanza, kisha ndio jamii. Vile vile yanaashiriwa na Aya hii tuliyo nayo, pale ilipokutanisha dhulma na hazina ya mali. Kuna dhulma gani zaidi kuliko kuwa chakula cha viumbe kimezuiwa na mtu au baadhi ya watu mpaka watake wao?

Watu wa Qaruni walijaribu kumkemea kwa njia nzuri, walipomwambia watu wake: Usijigambe, hakika Mwenyezi Mungu hapendi wanaojigamba.

Vipi unafurahi na mali na kuhadaika nayo na kuifanya ni nyenzo ya dhulma, uadui, anasa na israfu, na karibu yako watu wanakufa njaa? Je unajigamba kwa uweza wako wa kufanya dhambi na uovu?

Na utafute kwa aliyokupa Mwenyezi Mungu makazi ya akhera.

Jitahidi na ufanye kwa ajili ya Mwenyezi Mungu kwa kila alichokupa Mwenyezi Mungu katika mali siha na akili. Kwani mtu atakuwa na majukumu na kuulizwa mbele ya Mwenyezi Mungu kuhusiana na mwili jinsi alivyoutumia, umri wake jinsi alivyoumaliza na mali yake jinsi alivyoichuma na kuitumia.

Wala usisahau fungu lako la dunia.

Usiache mahitaji ya maisha yako na starehe zako. Kula unavyotaka katika vizuri na vya halali na uvae unavyopenda katika nguo nzuri, lakini kutokana na jasho lako sio la wengine. Kwa kufanya hivi utakuwa umepata mafungu mawili: Fungu la dunia na la akhera.

Na fanya wema kama alivyokufanyia wema Mwenyezi Mungu.

Mche Mwenyezi Mungu kwa aliyokuneemesha na umshukuru kwa wema huo kwa waja wake na watu wake; usaidiane nao kwenye yale yaliyo na kheri nawe na wao.

Wala usitafute ufisadi katika ardhi, kwa kufanya jeuri, hiyana, kiburi, ubabe na kufanya israfu na hali kando yako kuna wanaokufa njaa. Huu ndio ufisadi hasa na hakika Mwenyezi Mungu hapendi wafisadi na amewandalia adhabu chungu.

Akasema kwa hakika nimepewa haya kwa sababu ya elimu niliyo nayo.

Yaani mali aliyo nayo imetokana na elimu yake, kipawa chake na ujanja wake. Kwamba mtu anaweza kuitumia elimu yake na kipawa chake kupora, kuiba, kuua na kuwatoa watu katika miji yao.

Hii sio bid’a ya Qaruni peke yake. Serikali ya U.S.A. imeweka mpango wa kununua akili na vipawa kutoka pembe zote za ulimwengu na kuwafanya wataalamu na wajuzi wahamie huko.

Mpango huu wameuita ‘Brain drain;’ yaani kunyonya akili. Lengo la hilo ni kutumia vipawa vya binadamu kupora mali za nchi na vyakula vya waja mashiriki ya ardhi na magharibi yake.

Je, hakujua kwamba Mwenyezi Mungu amekwishaangamiza karne zilizokuwa kabla yake waliokuwa na nguvu zaidi kuliko yeye na wenye makundi makubwa zaidi.

Vipi atajua naye mali na jaha zimemfurisha kichwa, ikampofusha na mwisho wa dhulma na ikamsahaulisha na aliyoyasikia kuhusu karne zilizopita–kwamba zilikuwa na mali na watu wengi zaidi kuliko yeye, lakini walipokiuka mipaka na kufanya dhulma, Mwenyezi Mungu aliwaonjesha adhabu ya kufedheheka duniani na adhabu ya akhera ni kali na ya kufedhehesha zaidi.

Wafasiri wametolea mfano wa kaumu ya Nuh, A’d na Thamud. Kama ningelikuwa wakati wao nigekubaliana nao, nao kama wangelikuwa wakati wangu wangelitosheka na yaliyotokea Libya mwezi huu ninapoandika maneno haya, Septemba1969, ambapo kuna kundi la vijana limempindua mfalme aliyekuwa na nguvu na utajiri kuliko Qaruni, akiwa anasaidiwa na uzayuni na ukoloni. Wamemng’oa na wakachukua madaraka. Vijana hawa waliteswa na mfalme, wakafungwa na kufukuzwa.

Na wakosefu hawataulizwa dhambi zao.

Yaani Mwenyezi Mungu atawaadhibu bila ya hisabu.

Unaweza kuuliza : Aya hii tutaiunganisha vipi na Aya isemayo:

فَوَرَبِّكَ لَنَسْأَلَنَّهُمْ أَجْمَعِينَ ﴿٩٢﴾ عَمَّا كَانُوا يَعْمَلُونَ ﴿٩٣﴾

“Naapa kwa Mola wako, tutawauliza wote yale waliyokuwa wakiyatenda.” Juz. 14 (15:92-93).

Pamoja na Aya nyingine kadhaa zenye maana hiyo?

Jibu : Makusudio ya wakosefu hapa, kulingana na mfumo wa maneno ulivyo, ni wale waliozikosea haki za watu na uhuru, wakazusha fitna na vita kwa ajili ya masilahi yao na manufaa yao. Hawa ndio ambao wataingia motoni bila ya hisabu.

Kwa hiyo kauli yake Mwenyezi Mungu: ‘Hawataulizwa dhambi zao’ inawavua kutoka wale watakoulizwa wote. Yaani kama tutaziunganisha kauli mbili, maana yatakuwa: Tutawauliza wote isipokuwa waliozikosea haki za watu; wao wataingia motoni bila yamaswali.

Basi akawatokea watu wake katika pambo lake.

Watu wake walimpa hadhari ya mwisho mbaya, lakini shetani akampuzia kwenye pua yake, kiburi kikampanda, akawakusanya watumishi wake na wapambe wake. Akapanda kipando cha fahari, kuwaonyesha watu utajiri wake na kiburi chake, kuwaonyesha wale waliomuhadharisha na kumpa mawaidha kutokana na ulevi wa starehe na dhulma.

Wakasema wale waliokuwa wanataka maisha ya duniani: Laiti tungelikuwa nayo kama aliyopewa Qaruni! Hakika yeye ni mwenye bahati kubwa.

Wadhaifu wa akili walitazama mali na vipambo, wakasahau mwisho wa uovu na kiburi, na wakatamani kuwa na starehe kama za Qaruni ili waangamie kwenye starehe na anasa. Lau wangeliangalia kwa mtazamo wa busara wangelisema kama walivyosema wenye elimu:

Na wakasema wale ambao wamepewa elimu: Ole wenu! Thawabu za Mwenyezi Mungu ni bora kwa mwenye kuamini na akatenda. Wala hawatapewa isipokuwa wenye subira.

Yaani watu wa elimu waliwaambia wale madhaifu wa akili, hayo mnayoyatamka ni ushetani na kwamba vilivyo kwa Mwenyezi Mungu ni bora na vyenye kubaki.

Yeyote anayemtukuza asiyekuwa Mwenyezi Mungu, basi hudhalilika na kuhizika. Amesema Imam Aliy(a.s) : “Ni mara ngapi aliyepungukiwa akapata faida na aliyezidishiwa akapata hasara” Nahjul Balagha Khutba na 114.

Basi tukamdidimiza yeye na nyumba yake ardhini; wala hapakuwa na kundi lolote la kumsaidia kinyume na Mwenyezi Mungu wala hakuwa miongoni mwa wanaojisaidia.

Dhalimu hawezi kuokoka na kudidimia duniani kabla ya Akhera. Si lazima kudidimia kuwe ni kuzama ardhini, inaweza kuwa ni kwa kufedheheka na kulaaniwa na viumbe wenye kudhulumiwa na kunyimwa haki zao.

Uzoefu unatufahamisha kuwa dhalimu akipatikana na wenye kulipiza kisasi na kutaka haki zao, basi watu wote hujitenga naye; hata wale wasaidizi wake na ndugu zake na kujiona kuwa amedimimia.

Na wakawa wanasema wale waliotamani mahala pake jana: Kumbe Mwenyezi Mungu humkunjulia riziki amtakaye, katika waja wake, na humdhikisha amtakaye. Asingetufanyia hisani Mwenyezi Mungu angelitudidimiza. Kumbe makafiri hawafanikiwi.

Jana wale wadhaifu wa akili walikuwa wakisema tunatamani kuwa na aliyo nayo Qaruni, kwa vile walikuwa na mtazamo wa dunia na starehe zake; wakasahau hatima ya dhulma na kiburi. Leo wameshuhudia matokeo ya uovu yakimtokea Qaruni.

Wametambua uhakika na wakamsifu Mwenyezi Mungu ambaye hakuwapa kama walivyopewa mataghuti.

Katika Nahjul Balagha, imesemwa: “Ni upungufu mngapi umekuwa faida na ziada ngapi zimekuwa ni hasara?” Kuanzia hapa ndio ikasemwa: ‘Mambo ni mwisho wake.’

تِلْكَ الدَّارُ الْآخِرَةُ نَجْعَلُهَا لِلَّذِينَ لَا يُرِيدُونَ عُلُوًّا فِي الْأَرْضِ وَلَا فَسَادًا وَالْعَاقِبَةُ لِلْمُتَّقِينَ ﴿٨٣﴾

83. Hayo ndiyo makazi ya Akhera, tumewafanyia wale wasiotaka kujitukuza duniani wala ufisadi. Na mwisho ni wa wenye takua.

مَن جَاءَ بِالْحَسَنَةِ فَلَهُ خَيْرٌ مِّنْهَا وَمَن جَاءَ بِالسَّيِّئَةِ فَلَا يُجْزَى الَّذِينَ عَمِلُوا السَّيِّئَاتِ إِلَّا مَا كَانُوا يَعْمَلُونَ ﴿٨٤﴾

84. Atakayetenda mema atapata malipo bora kuliko hayo. Na atakayetenda uovu, hawalipwi watendao uovu ila waliyokuwa wakiyatenda.

إِنَّ الَّذِي فَرَضَ عَلَيْكَ الْقُرْآنَ لَرَادُّكَ إِلَىٰ مَعَادٍ قُل رَّبِّي أَعْلَمُ مَن جَاءَ بِالْهُدَىٰ وَمَنْ هُوَ فِي ضَلَالٍ مُّبِينٍ ﴿٨٥﴾

85. Hakika aliyekulazimisha Qur’an, bila shaka atakurudisha mahali pa marejeo. Sema: Mola wangu ndiye anayemjua zaidi mwenye kuja na uongofu na aliyemo katika upotofu ulio dhahiri.

وَمَا كُنتَ تَرْجُو أَن يُلْقَىٰ إِلَيْكَ الْكِتَابُ إِلَّا رَحْمَةً مِّن رَّبِّكَ فَلَا تَكُونَنَّ ظَهِيرًا لِّلْكَافِرِينَ ﴿٨٦﴾

86. Nawe hukuwa unatarajia kuletewa Kitabu lakini ni rehema ya Mola wako. Basi usiwe kabisa msaidizi wa makafiri

وَلَا يَصُدُّنَّكَ عَنْ آيَاتِ اللَّـهِ بَعْدَ إِذْ أُنزِلَتْ إِلَيْكَ وَادْعُ إِلَىٰ رَبِّكَ وَلَا تَكُونَنَّ مِنَ الْمُشْرِكِينَ ﴿٨٧﴾

87. Wala wasikuzuie na Aya za Mwenyezi Mungu baada ya kuteremshiwa, na lingania kwa Mola wako, wala usiwe kabisa miongoni mwa washirikina.

وَلَا تَدْعُ مَعَ اللَّـهِ إِلَـٰهًا آخَرَ لَا إِلَـٰهَ إِلَّا هُوَ كُلُّ شَيْءٍ هَالِكٌ إِلَّا وَجْهَهُ لَهُ الْحُكْمُ وَإِلَيْهِ تُرْجَعُونَ ﴿٨٨﴾

88. Wala usimwombe pamoja na Mwenyezi Mungu mungu mwingine. Hapana Mungu ila Yeye. Kila kitu kitaangamia isipokuwa dhati yake, hukumu ni yake na kwake Yeye mtarejeshwa.

ATAKURUDISHA MAHALI PA KUREJEA

Aya 83 – 88

MAANA

Hayo ndiyo makazi ya Akhera, tumewafanyia wale wasiotaka kuji- tukuza duniani wala ufisadi. Na mwisho ni wa wenye takua.

Kujitukuza katika ardhi ni kujiweka juu na kuwatawala watu bila ya haki. Ufisadi ni dhulma, uadui, ufuska na uovu.

Maana ni kuwa mwenye kujikweza na kujitukuza kwa watu au kutumia vibaya haki zao, basi Mwenyezi Mungu amemharamishia Pepo na makazi yake ni Jahannam ni makazi mabaya.

Atakayetenda mema atapata malipo bora kuliko huo. Na atakayeten- da uovu, hawalipwi watendao uovu ila waliyokuwa wakiyatenda.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 8 (6160).

Hakika aliyekulazimisha Qur’an, bila shaka atakurudisha mahali pa marejeo.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) anamwambia Mtume wake kuwa aliyekuwajibishia kuitumia Qur’an ndiye atakayekurudisha Makka walikokutoa watu wako.

Inasemekana kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) alipohama Makka kuelekea Madina, akiwa njiani aliutamani, mji wake. Ndipo ikashuka Aya hii kumbashiria kurudi.

Sema: Mola wangu ndiye anayemjua zaidi mwenye kuja na uongofu na aliyemo katika upotofu ulio dhahiri.

Yaani sema ewe Muhammad kumwambia yule usiyemtarajia kuongoka na kung’ang’ania kuwa yeye ni muongofu na wewe ni mpotevu kuwa ni Mwenyezi Mungu peke yake anayeweza kumpambanua muongofu na mpotevu na mwema na muovu. Na atamlipa kila mmoja stahiki yake.

Nawe hukuwa unatarajia kuletewa Kitabu lakini ni rehema ya Mola wako.

Hii ni kumrudi yule aliyemwambia Mtume wa Mwenyezi Mungu: Wewe si Mtume kutoka kwa Mwenyezi Mungu, bali unamzulia.

Ubainfu ni kuwa, vipi wanakwambia kuwa wewe ni mzushi na hali hukuwahi hata kuwazia hilo hata siku moja; isipokuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) ndiye aliyekuneemesha na akakuteua wewe badala ya wengine?

KUFICHUA HABARI ZA VIBARAKA NA WAHAINI

Basi usiwe msaidizi wa makafiri. Wala wasikuzuie na Aya za Mwenyezi Mungu baada ya kuteremshiwa, na lingania kwa Mola wako, wala usiwe miongoni mwa washirikina. Wala usimwombe pamoja na Mwenyezi Mungu mungu mwingine. Hapana Mungu ila Yeye.

Mwenyezi Mungu amekuteua wewe ewe Muhammad ili uwapige vita wala usiwasaidie. Vile vile amekuchagua kufikisha ujumbe wake kwa waja wake, wala usilaumiwe kwa kuufikisha ujumbe; na umfanyie ikhlasi Mwenyezi Mungu peke yake kwenye kauli zako na vitendo vyako.

Huko nyuma wakati tukifasiri aina ya Aya kama hii inayomwambia maasum kuwa asifanye dhambi tulisema kuwa aliye juu anaweza kumkataza aliye chini kwa aina yoyote ya makatazo anayotaka; kuongezea kuwa jambo linalokatazwa sio lazima anayekatazwa awe anaweza kulifanya.

Hivi sasa tukifasiri Aya hizi, tumepata maana nyingine zaidi. Nayo ni kuwa aina hii ya Aya ni kufichua habari za wenye vilemba na kofia wanaojionyesha kuwa ni watu wa dini kumbe ni askari na wasaidizi wa makafiri waovu na kuelezea hali yao leo na kabla ya leo.

Tumehusisha kutaja baadhi yao hasa, pamoja na kuwa vibaraka wanatokana na kila aina ya watu, kwa vile Aya zinazungumza na anayemlinga- nia Mwenyezi Mungu na sharia yake.

Kila kitu kitaangamia isipokuwa dhati yake, hukumu ni yake na kwake Yeye mtarejeshwa.

Haya ni makemeo na kiaga kwa kila mhaini na kibaraka anayeipangia njama dini yake na nchi yake pamoja na maadui wa Mwenyezi Mungu na wa utu. Na kwamba Yeye Mwenyezi Mungu atamhukumu mshirikina ambaye amesimamiwa na hoja, lakini akafanya inadi. Kwani hakuna tofauti kabisa baina ya anayemuomba Mungu mwingine na yule anayewasaidia madhalimu mataghuti, akiwatetea na kutoa mwito waungwe mkono.

Unaweza kuuliza : Je, hii inamaanisha kuwa ni wajibu kuwachukulia wahaini na vibaraka kama washirikina katika unajisi, kuacha kurithi, kutooana nao na kutozikwa kwenye makaburi ya waislamu?

Jibu : Ni wajibu wetu kumchukulia kila aliyesema: Ash-hadu alla ilaha illallah wa anna Muhammadarasulullah: (‘Nashudia kuwa hapana Mola isipokuwa Mwenyezi Mungu na kwamba Muhammad ni Mtume wa Mwenyezi Mungu,’ kama tunavyomchukulia mwislamu; kwa namna yoyote vitakavyokuwa vitendo vyake au kwa vyovyote moyo wake utakavyokunjika.

Hiyo ni kwa sababu shahada ina athari yake ya kimaudhui haiepukani nayo kwa hali yoyote, ambayo ni utwahara, kurithiana, kuozana na kuzikwa kwenye makaburi ya waislamu. Ama akhera hiyo ni ya Mwenyezi Mungu peke yake wala hahusiki nayo yeyote asiyekuwa Yeye.

Dhahiri za Aya nyingi zimefahamisha kuwa mshirikina na dhalimu, siku ya Kiyama, watakuwa sawa. Tazama tuliyoyasema katika Juz. 19 (55–62).