TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI Juzuu 20

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI0%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: Qurani tukufu

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI

Mwandishi: Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya
: HASANI MWALUPA
Kundi:

Matembeleo: 14325
Pakua: 2503


Maelezo zaidi:

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 25 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 14325 / Pakua: 2503
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI Juzuu 20

Mwandishi:
Swahili

15

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI

وَلَهُ مَن فِي السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ كُلٌّ لَّهُ قَانِتُونَ ﴿٢٦﴾

26. Ni vyake vilivyo katika mbingu na ardhi. Vyote vinamtii.

وَهُوَ الَّذِي يَبْدَأُ الْخَلْقَ ثُمَّ يُعِيدُهُ وَهُوَ أَهْوَنُ عَلَيْهِ وَلَهُ الْمَثَلُ الْأَعْلَىٰ فِي السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ وَهُوَ الْعَزِيزُ الْحَكِيمُ ﴿٢٧﴾

27. Naye ndiye ambaye anaanzisha uumbaji kisha ataurudisha, na jambo hili ni jepesi zaidi kwake. Naye ndiye mwenye mfano bora katika mbingu na ardhi. Na yeye ndiye Mwenye uwezo, Mwenye hekima.

ضَرَبَ لَكُم مَّثَلًا مِّنْ أَنفُسِكُمْ هَل لَّكُم مِّن مَّا مَلَكَتْ أَيْمَانُكُم مِّن شُرَكَاءَ فِي مَا رَزَقْنَاكُمْ فَأَنتُمْ فِيهِ سَوَاءٌ تَخَافُونَهُمْ كَخِيفَتِكُمْ أَنفُسَكُمْ كَذَٰلِكَ نُفَصِّلُ الْآيَاتِ لِقَوْمٍ يَعْقِلُونَ ﴿٢٨﴾

28. Amewapigia mfano kutokana na nafsi zenu. Je, katika hao iliyowamiliki mikono yenu ya kuume mnao washirika katika hivyo tulivyowaruzuku, mkawa nyinyi katika hivyo ni sawasawa, mkawahofia kama mnavyohofiana? Namna hiyo tunazipambanua Aya zetu kwa watu wenye akili.

بَلِ اتَّبَعَ الَّذِينَ ظَلَمُوا أَهْوَاءَهُم بِغَيْرِ عِلْمٍ فَمَن يَهْدِي مَنْ أَضَلَّ اللَّـهُ وَمَا لَهُم مِّن نَّاصِرِينَ ﴿٢٩﴾

29. Bali waliodhulumu wamefuata hawa zao pasi na kujua. Basi ni nani atamwongoa ambaye Mwenyezi Mungu amempoteza?

VYOTE VINAMTII YEYE

Aya 26 – 29

MAANA

Ni vyake vilivyo katika mbingu na ardhi. Vyote vinamtii.

Ulimwengu na vilivyomo ndani yake ni miliki ya Mwenyezi Mungu na vinakwenda kulingana na utashi wake; hata wale wanaomuasi pia anawafanya atakavyo, bila ya mpinzani.

Naye ndiye ambaye anaanzisha uumbaji kisha ataurudisha, na jambo hili ni jepesi zaidi kwake.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) ameumba ulimwengu, kisha atauondoa, tena ataurudisha mara nyingine.

Makusudio ya wepesi zaidi hapa ni wepesi tu; sio kuwa kuna mengine ni mepesi kidogo na mengine zaidi; kama vile kusema Mwenyezi Mungu ni Mkubwa zaidi, haimaanishi kuwa kuna mwingine aliye mkubwa na yeye ni mkubwa zaidi. Kwa sababu ambaye hana mfano wa kitu chochote, mambo yote kwake ni sawa. Haifai kusema ni mkubwa zaidi ya mwingine wala hili ni jepesi zaidi ya mengine.

Naye ndiye mwenye mfano bora katika mbingu na ardhi. Na yeye ndiye Mwenye uwezo, Mwenye hekima.

Makusudio ya mfano bora hapa ni sifa bora ambazo hashirikianai na yeyote katika sifa hizo. Nazo ni kuwa: Hakuna Mola isipokuwa yeye na Yeye ndiye Mwenye nguvu ambaye hashindwi na mwenye hekima asiyefanya mchezo.

Amewapigia mfano kutokana na nafsi zenu. Je, katika hao iliyowamiliki mikono yenu ya kuume mnao washirika katika hivyo tulivyowaruzuku, mkawa nyinyi katika hivyo ni sawasawa, mkawahofia kama mnavyohofiana?

Mfano huu, Mwenyezi Mungu (s.w.t), anaupiga kwa mataghuti wapenda anasa ambao wanamiliki watumwa na mali na wanadai kuwa Mwenyezi Mungu ana washirika katika kuumba kwake. Ufafanuzi wake ni kuwa: Angalieni enyi washirikina wapenda anasa.

Nyinyi mna watumwa na mali, lakini hamuwashirikishi kwenye mali zenu, wala hamkubali wazitumie ila kwa idhini yenu; wala hamuwahofii, wakati mnapowatumia, kama mnavyowahofia washirika wenu wasiokuwa watumwa na hali ya kuwa wale ambao mmewafanya watumwa sio milki yenu hasa.

Sasa vipi wale ambao ni milki ya Mwenyezi Mungu hasa mmewafanya ni washirika wake katika miliki yake na kuumba kwake. Vipi mnamnasibishia Mwenyezi Mungu yale ambayo nyinyi hamyaridhii. Nyinyi mnachukia kuwa na ushirika na wale mnaodai ni watumwa wenu, lakini Mwenyezi Mungu asichukie kuwa na ushirika na viumbe wake. Ole wenu! Mnahukumu vipi?

Hii ni sawa na kusema kwao kuwa Mwenyezi Mungu ana watoto wasichana na sisi tuna wavulana:

“Na wamemfanyia Mwenyezi Mungu mabinti. Ametakata na hayo! Na hali wao hupata wanavyovitamani. Na mmoja wao akibashiriwa msichana uso wake unasawijika naye amejaa chuki.” Juz. 14 (16: 57 – 58).

Namna hiyo tunazipambanua Aya zetu kwa watu wenye akili.

Mfano huu ni wazi kabisa kuwa Mwenyezi Mungu hana mshirika, wala hawapofuki na mfano huu ispokuwa watu wa masilahi na matamanio.

Bali waliodhulumu wamefuata hawa zao pasi na kujua.

Ambapo haki iko katika hawa zao na uadilifu uko katika wanayoyatamani. Huu ndio ujinga wa mwisho na upotevu ulio wazi.

Basi ni nani atamwongoa ambaye Mwenyezi Mungu amempoteza?

Mwenyezi Mungu amewapoteza kwa vile wameamua kufuata njia ya upotevu. Kila mwenye kufuata njia atafika; iwe njia ya kheri au ya shari; ya kuokoka au ya kuangamia.

Nao hawatakuwa na wasaidizi.

Vipi wawe na usaidizi na hali wao wameamua kufuata njia ya maangamizi kutokana na uchaguzi wao mbaya, wala hawakuonyeka au kukoma na makemeo yoyote.

فَأَقِمْ وَجْهَكَ لِلدِّينِ حَنِيفًا فِطْرَتَ اللَّـهِ الَّتِي فَطَرَ النَّاسَ عَلَيْهَا لَا تَبْدِيلَ لِخَلْقِ اللَّـهِ ذَٰلِكَ الدِّينُ الْقَيِّمُ وَلَـٰكِنَّ أَكْثَرَ النَّاسِ لَا يَعْلَمُونَ ﴿٣٠﴾

30. Basi uelekeze uso wako sawa-sawa kwenye dini–ndilo umbile la Mwenyezi Mungu alilowaumbia watu. Hapana mabadiliko katika uumbaji wa Mwenyezi Mungu. Hiyo ndiyo dini ya sawasawa, lakini watu wengi hawajui.

مُنِيبِينَ إِلَيْهِ وَاتَّقُوهُ وَأَقِيمُوا الصَّلَاةَ وَلَا تَكُونُوا مِنَ الْمُشْرِكِينَ ﴿٣١﴾

31. Muwe wenye kurejea kwake na mcheni. Na simamisheni Swala wala msiwe katika washirikina.

مِنَ الَّذِينَ فَرَّقُوا دِينَهُمْ وَكَانُوا شِيَعًا كُلُّ حِزْبٍ بِمَا لَدَيْهِمْ فَرِحُونَ ﴿٣٢﴾

32. Katika wale walioigawa dini yao na wakawa makundi makundi. Kila kundi hufurahia waliyo nayo.

DINI YA SAWASAWA

Aya 30 – 32

MAANA

Dini Ya Mwenyezi Mungu Na Maumbile

Basi uelekeze uso wako sawasawa kwenye dini–ndilo umbile la Mwenyezi Mungu alilowaumbia watu. Hapana mabadiliko katika uumbaji wa Mwenyezi Mungu. Hiyo ndiyo dini ya sawasawa, lakini watu wengi hawajui.

Aya hii, mara nyingi, inakuwa vinywani mwa mahatibu na kwenye kalamu za waandishi. Kuna wale wanaotosheka na kuitolea dalili tu. Wengine wanaipamba wakisema: Hii ndio dini iliyo sahihi iliyo kubwa n.k.

Bila shaka Aya hii inathibisha msingi unaotiliwa mkazo na itikadi ya Kiislamu na sharia yake. Na inafahamisha wazi kwamba mafunzo ya dini kuanzia alifu mpaka ye (a mpaka z) yanaongoza kwenye uongofu na utekelezaji wa matakwa ya maisha, ukuaji na maendeleo yake.

Kwanza tutanza kufasiri misamiati iliyo katika Aya hii, kisha tutaja maana kijumla.

Neno umbile kwa ujumla linamanisha tabia iliyo ndani ya mtu, inayoikubali kheri inapoijua kuwa ni kheri na kulazimiana nayo kwa vile tu kheri inakubalika. Na tabia hiyo inaikataa shari inapoijua kuwa ni shari, si kwa jingine ila ni kwamba shari inakataliwa na kuepukwa.

Hii ni itakapokuwa umbile la mtu ni safi, halina takataka za desturi na uuigizaji wala halikuchafuliwa na hawaa. Mwanchuoni mkuu Hilli (Allama Hilli) ameipigia mfano tabia hii kwa kusema: “Lau mwenye akili atahiyarishwa kusema ukweli na apewe pesa au aseme uwongo pia apewe pesa, basi atachagua ukweli.”

Tabia hii inayochagua ukweli kuliko uongo ndio ile aliyoizungumzia Mwenyezi Mungu pale aliposema: “Je, mimi si Mola wenu? Wakasema: Kwa nini!” Juz. 9 (7:152). Pia ndiyo iliyokusudiwa na Hadith mashuhuri iliyopokewa kutoka kwa Mtume(s.a.w.w) : “Kila anayezaliwa anazaliwa na umbile mpaka wazazi wake wamfanye Yahudi au Mnaswara.”

Ama neno ‘kwenye dini’ hapa linamanisha msimamo wa umbile ambalo Mwenyezi Mungu amewaumbia watu la kuwa mbali na hawaa za nafsi.

Makusudio ya kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: “Hapana mabadiliko katika uumbaji wa Mwenyezi Mungu,” ni kuwa dini mbele ya Mwenyezi Mungu ni yenye kuthibiti kwa msingi wa kimaumbile, hauepukani nayo.

Neno ‘Hiyo’ ni ishara ya yale aliyoyawajibisha Mwenyezi Mungu kwa waja kulazimiana nayo kwa kauli na vitendo. Kwa sababu ndiyo dini ya kisawasawa isiyokuwa na kombokombo.

Ama kwa ujumla wake inafahamisha kuwa dini inafungamana na maumbile ya mtu, lakini hii haimaanishi kuwa umbile ndilo muamrishaji na mkatazaji na dini ielezee hukumu zake, hapana! Mwenyezi Mungu ambaye ameumba dini na maumbile ndiye muweka sharia wa kwanza. Ni Yeye pekee mwenye kuamrisha na kukataza.

Hakika makusudio ya Aya ni kuelezea kipimo tunachopimia dini ya Mwenyezi Mungu na kwamba itikidi, sharia na maadili yake yanenda sambamba na umbile la watu na masilahi yao; na Mwenyezi Mungu (s.w.t.) hakuweka hukumu kwa waja wake kupingana na manufaa ya mtu binafsi au jamii.

Huu ndio udhibiti na tofauti iliyoko baina ya hukumu ya Mwenyezi Mungu na hukumu nyinginezo, tofauti baina ya sharia ya haki na sharia ya batili. Ama kauli za maulama wa fiqih, tafsir na falsafa sio msingi wa Uislamu, wala haifai kuwategemea kama dalili ya sharia. Kwa sabau kauli zao hizo zinaakisi tu juhudi na fahamu zao katika dini ya Mwenyezi Mungu na hukumu zake, wala haziakisi uhakika na uhalisi wa dini.

Kwa ufupi ni kuwa Uislamu haukatai yote yaliyo katika dini na madhehbu mengineyo; bali unaangalia kwa mtazamo wa undani na usanifu. Unakubaliana yale yanayoafikiana na umbile la Mwenyezi Mungu na kukataa yasiyokuwa hayo.

Muwe wenye kurejea kwake na mcheni . Rudini kwenye dini hii na mtii hukumu zake zote.

Na simamisheni Swala kwani inawakumbusha Mwenyezi Mungu; wala msiwe katika washirikina.

Mfanyieni ikhlasi Mwenyezi Mungu peke yake kwenye kauli zenu na vitendo vyenu.

Katika wale walioigawa dini yao na wakawa makundi makundi. Kila kundi hufurahia waliyo nayo.

Umepita mfano wake katika Juz. 8 (6:158) na Juz. 18 (23:53).

وَإِذَا مَسَّ النَّاسَ ضُرٌّ دَعَوْا رَبَّهُم مُّنِيبِينَ إِلَيْهِ ثُمَّ إِذَا أَذَاقَهُم مِّنْهُ رَحْمَةً إِذَا فَرِيقٌ مِّنْهُم بِرَبِّهِمْ يُشْرِكُونَ ﴿٣٣﴾

33. Watu yakiwagusa madhara humwomba Mola wao wakiwa wanarejea kwake. Kisha akiwaonjesha rehema kutoka kwake, mara kikundi miongoni mwao humshirikisha Mola wao.

لِيَكْفُرُوا بِمَا آتَيْنَاهُمْ فَتَمَتَّعُوا فَسَوْفَ تَعْلَمُونَ ﴿٣٤﴾

34. Ili wapate kuyakana tuliyowapa. Basi stareheni. Mtakuja jua.

أَمْ أَنزَلْنَا عَلَيْهِمْ سُلْطَانًا فَهُوَ يَتَكَلَّمُ بِمَا كَانُوا بِهِ يُشْرِكُونَ ﴿٣٥﴾

35. Au tumewateremshia hoja inayowaambia juu ya yale wamshirikishayo nayo?

وَإِذَا أَذَقْنَا النَّاسَ رَحْمَةً فَرِحُوا بِهَا وَإِن تُصِبْهُمْ سَيِّئَةٌ بِمَا قَدَّمَتْ أَيْدِيهِمْ إِذَا هُمْ يَقْنَطُونَ ﴿٣٦﴾

36. Na watu tunapowaonjesha rehema huifurahia. Na ukiwasibu uovu kwa iliyoyatanguliza mikono yao wenyewe, mara wanakata tamaa.

أَوَلَمْ يَرَوْا أَنَّ اللَّـهَ يَبْسُطُ الرِّزْقَ لِمَن يَشَاءُ وَيَقْدِرُ إِنَّ فِي ذَٰلِكَ لَآيَاتٍ لِّقَوْمٍ يُؤْمِنُونَ ﴿٣٧﴾

37. Je, hawaoni kwamba Mwenyezi Mungu humkunjulia riziki amtakaye na humkunjia. Hakika katika hayo kuna ishara kwa watu wanaoamini.

فَآتِ ذَا الْقُرْبَىٰ حَقَّهُ وَالْمِسْكِينَ وَابْنَ السَّبِيلِ ذَٰلِكَ خَيْرٌ لِّلَّذِينَ يُرِيدُونَ وَجْهَ اللَّـهِ وَأُولَـٰئِكَ هُمُ الْمُفْلِحُونَ ﴿٣٨﴾

37. Basi mpe jamaa haki yake na masikini na mwananjia. Hayo ni kheri kwa wale watakao radhi ya Mwenyezi Mungu na hao ndio wenye kufanikiwa.

وَمَا آتَيْتُم مِّن رِّبًا لِّيَرْبُوَ فِي أَمْوَالِ النَّاسِ فَلَا يَرْبُو عِندَ اللَّـهِ وَمَا آتَيْتُم مِّن زَكَاةٍ تُرِيدُونَ وَجْهَ اللَّـهِ فَأُولَـٰئِكَ هُمُ الْمُضْعِفُونَ ﴿٣٩﴾

39. Na mnachokitoa katika riba ili kiongezeke katika mali ya watu, basi hakiongezeki mbele ya Mwenyezi Mungu. Lakini mlichokitoa Zaka kwa kutaka radhi ya Mwenyezi Mungu, basi hao ndio watakaozidishiwa.

اللَّـهُ الَّذِي خَلَقَكُمْ ثُمَّ رَزَقَكُمْ ثُمَّ يُمِيتُكُمْ ثُمَّ يُحْيِيكُمْ هَلْ مِن شُرَكَائِكُم مَّن يَفْعَلُ مِن ذَٰلِكُم مِّن شَيْءٍ سُبْحَانَهُ وَتَعَالَىٰ عَمَّا يُشْرِكُونَ ﴿٤٠﴾

40. Mwenyezi Mungu ndiye aliyewaumba, kisha akawaruzuku, kisha atawafisha na kisha atawafufua. Je katika mnaowashirikisha yuko awezaye kufanya lolote katika hayo? Ametakasika na ametukuka na hayo wanayomshirikisha nayo.

DHARA INAPOGUSA WATU

Aya 33 – 40

MAANA

Watu yakiwagusa madhara humwomba Mola wao wakiwa wanarejea kwake. Kisha akiwaonjesha rehema kutoka kwake, mara kikundi miongoni mwao humshirikisha Mola wao.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 11 (10:12) na Juz. 15 (17:67).

Ili wapate kuyakana tuliyowapa. Basi stareheni. Mtakuja jua.

Umetangulia mfano wake katika Juzuu hii (29:66).

Au tumewateremshia hoja inayowaambia juu ya yale wamshirikishayo nayo?

Au hapa ni kwa maana ya mbali. Maana ni kuwa Je, kuna wahyi au akili yoyote inayoshuhudia kuwa ushirikina mlio nao ni sawa na haki? Makusudio ya swali hili ni kupinga na kukemea.

Na watu tunapowaonjesha rehema huifurahia. Na ukiwasibu uovu kwa iliyoyatanguliza mikono yao wenyewe, mara wanakata tamaa.

Huyu ndiye binadamu. Akipata heri anafurahi na kujifaharisha na akipat- wa na shari anakata tamaa. Umetangulia mfano wake katika Juz. 12 (11:9).

Je, hawaoni kwamba Mwenyezi Mungu humkunjulia riziki amtakaye na humkunjia. Hakika katika hayo kuna ishara kwa watu wanaoamini.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 13 (13:26) na Juz. 15 (17:30).

Basi mpe jamaa haki yake na masikini na mwananjia.

Jamaa aliye fukara ana haki kwa jamaa yake aliye tajiri ya kumpa cha kusitiri haja. Shafii na Shia Imamiya wamesema kuwa ni wajibu kumtunza jamaa akiwa ni baba na kuendelea juu na mtoto na kuendelea chini.

Malik akasema: “Hakuna wajibu isipokuwa kwa wazazi na watoto wa karibu tu, sio baba wa baba au mtoto wa mtoto.”

Hambali anasema: “Ni wajibu kumtunza ndugu kwa sharti ya kuwa mtunzaji awe ni mrithi wa anayemtunza.” Ama Hanafi wanaona kuwa sharti la msingi ni kuwa ndugu aliye maharimu kuoana naye. Ufafanuzi uko katika Kitabu chetu Alfiqh ala madhahibil-khamsa (Fiqh ya madhehebu matano).

Ama masikini na mwananjia yametangulia maelezo yao katika Juz. 10 (9:60).

Hayo ni kheri kwa wale watakao radhi ya Mwenyezi Mungu na hao ndio wenye kufanikiwa.

‘Hayo’ ni ishara ya kutoa - kwamba ni wajibu kuwe ni kwa kutaka radhi ya Mwenyezi Mungu, kama ilivyo kwa watu wema na wa kufaulu.

Na mnachokitoa katika riba ili kiongezeke katika mali ya watu, basi hakiongezeki mbele ya Mwenyezi Mungu.

Kuna kundi la wafasiri waliosema kuwa makusudio ya riba hapa ni ile riba ya haramu. Wengine wakasema makusudioa yake ni riba ya halali; kama vile mtu kumpa zawadi tajiri ili arudishe zawadi kubwa zaidi.

Vizuri ni kuichukulia Aya kwa yote mawili – kwamba zote mbili hazina thawabu mbele ya Mwenyezi Mungu; isipokuwa ya kwanza ina adhabu na ya pili haina thawabu wala adhabu.

Lakini mlichokitoa Zaka kwa kutaka radhi ya Mwenyezi Mungu, basi hao ndio watakaozidishiwa.

Yaani watazidishiwa thawabu na malipo. Maana ya kiujumla ni kuwa mwenye kutoa kwa kutaka radhi ya Mwenyezi Mungu Mtukufu, Mwenyezi Mungu humzidishia mali yake duniani na thawabu zake akhera. Imam Ali(a.s) anasema:“Mkifilisika basi fanyeni biashara na Mwenyezi Mungu.” Kauli hii imechukuliwa kutokana na kauli yake Mwenyezi Mungu:“Ni nani atakayemkopesha Mwenyezi Mungu mkopo mzuri, ili amzidishie ziada nyingi?” Juz. 2 (2:245).

Mwenyezi Mungu ndiye aliyewaumba, kisha akawaruzuku, kisha atawafisha na kisha atawafufua. Je katika mnaowashirikisha yuko awezaye kufanya lolote katika hayo?

Mnavifanyia ubakhili alivyowapa Mwenyezi Mungu na mnataka riziki kwa wengine; na hali Yeye Mwenyezi Mungu ndiye aliyewafanya muweko baada ya kuwa hamko, akawamiminia baraka zake nyingi. Yeye ndiye anayewafisha na kuwapa uhai kisha awakusanye kwa ajili ya hisabu na malipo? Je, katika hao mnaowatarajia fadhila zao na kutarajia kuwanufaisha kuna anayeweza kutoa uhai na kufisha? Tukikadiria kuwa wanaweza kufanya baadhi ya mambo katika maisha haya, je kesho wataweza kunufaisha na kudhuru?

Ametakasika na ametukuka na hayo wanayomshirikisha naye.

Kuna hadith isemayo: “Shirki imejificha zaidi kuliko kutambaa kwa chungu.” Hapa kuna ishara kwamba shirki ziko aina nyingi, ikiwemo ile ya kumtegemea muumbwa badala ya Muumba.

16

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI

ظَهَرَ الْفَسَادُ فِي الْبَرِّ وَالْبَحْرِ بِمَا كَسَبَتْ أَيْدِي النَّاسِ لِيُذِيقَهُم بَعْضَ الَّذِي عَمِلُوا لَعَلَّهُمْ يَرْجِعُونَ ﴿٤١﴾

41. Ufisadi umedhihiri bara na baharini kwa sababu ya iliyoyafanya mikono ya watu. Ili Mwenyezi Mungu awaonjeshe baadhi ya waliyoyatenda. Huenda wakarejea.

قُلْ سِيرُوا فِي الْأَرْضِ فَانظُرُوا كَيْفَ كَانَ عَاقِبَةُ الَّذِينَ مِن قَبْلُ كَانَ أَكْثَرُهُم مُّشْرِكِينَ ﴿٤٢﴾

42. Sema: Nendeni katika ardhi na tazameni ulikuwaje mwisho wa wale waliotangulia, wengi wao walikuwa washirikina.

فَأَقِمْ وَجْهَكَ لِلدِّينِ الْقَيِّمِ مِن قَبْلِ أَن يَأْتِيَ يَوْمٌ لَّا مَرَدَّ لَهُ مِنَ اللَّـهِ يَوْمَئِذٍ يَصَّدَّعُونَ ﴿٤٣﴾

43. Basi uelekeze uso wako kwenye dini ya sawasawa, kabla ya kufika siku isiyozuilika, inayotoka kwa Mwenyezi Mungu. Siku hiyo watatengana.

مَن كَفَرَ فَعَلَيْهِ كُفْرُهُ وَمَنْ عَمِلَ صَالِحًا فَلِأَنفُسِهِمْ يَمْهَدُونَ ﴿٤٤﴾

44. Anayekufuru basi ukafiri wake utakuwa juu yake, na anayetenda mema basi wanazitengenezea nafsi zao.

لِيَجْزِيَ الَّذِينَ آمَنُوا وَعَمِلُوا الصَّالِحَاتِ مِن فَضْلِهِ إِنَّهُ لَا يُحِبُّ الْكَافِرِينَ ﴿٤٥﴾

45. Ili awalipe walioamini na wakatenda mema kutokana na fadhila yake. Hakika Yeye hapendi makafiri.

UFISADI UMEDHIHIRI BARA NA BAHARINI

Aya 41 – 45

MAANA

Ufisadi umedhihiri bara na baharini kwa kwa sababu ya iliyoyafanya mikono ya watu.

Kundi la wafasiri limesema makusudio ya baharini hapa ni miji ya pwani na bara ni miji iliyo mbali na pwani. Wengine wamesema makusudio ya bahari ni mji kutokana na wingi wa wakazi wake na bara ni kijiji kutokana na uchache wa wakazi wake.

Tunavyofahamu sisi ni kuwa bara na baharini ni kinaya cha wingi wa ufisadi na kuenea kwake.

Kila aliloliharamisha Mwenyezi Mungu na kulikataza kulifanya ni kosa na ufisadi katika ardhi; kama vile vita dhulma, israfu, uasherati, pombe, kamari, kuzipuuza faradhi za Mwenyezi Mungu na waja wake n.k.

Ikiwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) amesifia zama za ujahili kwa kudhihiri ufisadi bara na baharini; ambapo hakukuwa na silaha za kemikali wala mabomu ya atomiki au mashirika ya ulanguzi na unyonyaji wala makasino na mabaa. Je, itakuwaje kwa hivi sasa ambapo nusu ya ulimwengu inahofiwa kuangamizwa wakati wowote, sio kwa kitendo cha Mwenyezi Mungu wala majanga ya asili, bali ni kwa kitendo cha binadamu wenyewe wanaomiliki silaha za maangamizi?

Hakuna njia ya kusalimika watu na shari hii isipokuwa kuangamizwa sila- ha zote. Ama umoja wa mataifa na shirika linalosimamia nguvu za nyuklia halijamhakikishia binadamu usalama wake wala si ya kutegemewa.

Ili Mwenyezi Mungu awaonjeshe baadhi ya waliyoyatenda. Huenda wakarejea.

Ufisadi katika ardhi ni natija ya kuachana na Mwenyezi Mungu na kutojilazimisha na maamrisho yake na makatazo yake. Neno ‘baadhi’ hapa linaashiria adhabu ya dunia na adhabu ya akhera ni mbaya zaidi na ya kufedhehesha. Katika dua zilizopokewa, kuna dua hii: “Ewe Mola wangu! Hakika mimi ninajilinda kwako kutokana na dhambi inayobadilisha neema na kuteremsha balaa.” Bwana wa Mitume anasema:“Ogopeni dhambi kwani zinafuta kheri.” Inatosha kuwa ni ushahidi wa hilo kauli yake Mwenyezi Mungu:

وَتِلْكَ الْقُرَىٰ أَهْلَكْنَاهُمْ لَمَّا ظَلَمُوا وَجَعَلْنَا لِمَهْلِكِهِم مَّوْعِدًا ﴿٥٩﴾

“Na miji hiyo tuliwaangamiza walipodhulumu na tukawawekea miadi ya maangamizo yao.”

Juz. 15 (18:59).

Sema: Nendeni katika ardhi na tazameni ulikuwaje mwisho wa wale waliotangulia, wengi wao walikuwa washirikina.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 4 (3:137), Juz.7 (6:11) na Juz. 20 (27:69).

Basi uelekeze uso wako kwenye dini ya sawasawa, kabla ya kufika siku isiyozuilika, inayotoka kwa Mwenyezi Mungu ambayo ni siku ya hisabu na malipo isiyokimbilika. Mwema ni yule ambaye amemfanyia ikhlasi Mwenyezi Mungu katika matendo yake na makusudio yake na akaihisabu nafsi yake kabla ya kuhisabiwa.

Siku hiyo watatengana. Watatawayika makundi mawili: kundi moja Peponi na jingine Motoni. Umetangulia mfano wake katika Juzuu na Sura hii Aya 14.

Anayekufuru basi ukafiri wake utakuwa juu yake, na anayetenda mema basi wanazitengenezea nafsi zao.

Neno kutengeneza, limefasiriwa kutokana na neno Yamhadun lenye maana ya kutandika kitanda. Watu wenye matendo mema wanajitandikia makaburi yao na kufanya maandalizi ya mahitaji ya amani na raha kabla ya kuingia huko; sawa na inavyoandaliwa nyumba ya kuishi duniani. Imepokewa Hadith kutoka kwa Imam Ja’far Sadiq(a.s) :“Hakika matendo mema yanamtangulia mtendaji ili kumwandalia, sawa na mtumishi amwandaliavyo bwana wake.”

Umetangulia mfano wake katika Juz. Juz. 3(2:286).

Ili awalipe walioamini na wakatenda mema kutokana na fadhila yake. Hakika Yeye hapendi makafiri.

Maneno hapa yanafungamana na ‘siku hiyo watatengana.’ Maana ni kuwa Mwenyezi Mungu Siku ya Kiyama atawafanya watu makundi mawili ili awalipe Pepo waumini kutokana na matendo yao, kwa sababu anawapenda na anapenda matendo yao mema. Mwenyezi Mungu anawachukia makafiri na atalipa wanavyostahili.

Katika Nahjul-balagha imesemwa:“Hakika Mwenyezi Mungu anampemda mja na kuchukia matendo yake na anapenda matendo na kumchukia mtendaji wake.” yaani anampenda mumin kwa imani yake na anachukia matendo yake mabaya na anamchukia kafiri kwa kufuru yake na anapenda matendo yake mazuri.

وَمِنْ آيَاتِهِ أَن يُرْسِلَ الرِّيَاحَ مُبَشِّرَاتٍ وَلِيُذِيقَكُم مِّن رَّحْمَتِهِ وَلِتَجْرِيَ الْفُلْكُ بِأَمْرِهِ وَلِتَبْتَغُوا مِن فَضْلِهِ وَلَعَلَّكُمْ تَشْكُرُونَ ﴿٤٦﴾

46. Na katika ishara zake ni kuzituma pepo ziletazo bishara na ili kuwaonjesha rehema yake na ili majahazi yatembee kwa amri yake; na mtafute kutokana na fadhila yake, na ili mumshukuru.

وَلَقَدْ أَرْسَلْنَا مِن قَبْلِكَ رُسُلًا إِلَىٰ قَوْمِهِمْ فَجَاءُوهُم بِالْبَيِّنَاتِ فَانتَقَمْنَا مِنَ الَّذِينَ أَجْرَمُوا وَكَانَ حَقًّا عَلَيْنَا نَصْرُ الْمُؤْمِنِينَ ﴿٤٧﴾

47. Na hakika tulikwishawatuma mitume kwa kaumu zao na wakawajia na hoja zilizo waziwazi. Tukawaadhibu wale waliofanya makosa na ilikuwa ni haki juu yetu kuwanusuru waumini.

اللَّـهُ الَّذِي يُرْسِلُ الرِّيَاحَ فَتُثِيرُ سَحَابًا فَيَبْسُطُهُ فِي السَّمَاءِ كَيْفَ يَشَاءُ وَيَجْعَلُهُ كِسَفًا فَتَرَى الْوَدْقَ يَخْرُجُ مِنْ خِلَالِهِ فَإِذَا أَصَابَ بِهِ مَن يَشَاءُ مِنْ عِبَادِهِ إِذَا هُمْ يَسْتَبْشِرُونَ ﴿٤٨﴾

48. Mwenyezi Mungu ndiye anayezituma pepo zikayatimua mawingu, kisha akayatandaza mbinguni kama apendavyo. Na akayafanya mapande mapande, basi ukaiona mvua inatoka ndani yake. Anapowafikishia awatakao katika waja wake, mara wanakuwa na furaha.

وَإِن كَانُوا مِن قَبْلِ أَن يُنَزَّلَ عَلَيْهِم مِّن قَبْلِهِ لَمُبْلِسِينَ ﴿٤٩﴾

49. Ingawaje kabla ya kuteremshiwa walikuwa wenye kukata tamaa.

فَانظُرْ إِلَىٰ آثَارِ رَحْمَتِ اللَّـهِ كَيْفَ يُحْيِي الْأَرْضَ بَعْدَ مَوْتِهَا إِنَّ ذَٰلِكَ لَمُحْيِي الْمَوْتَىٰ وَهُوَ عَلَىٰ كُلِّ شَيْءٍ قَدِيرٌ ﴿٥٠﴾

50. Angalia athari za rehema ya Mwenyezi Mungu, jinsi anavyoihuisha ardhi baada ya kufa kwake. Basi hakika huyo, bila shaka, ndiye mwenye kuhuisha wafu. Na Yeye ni Muweza wa kila kitu

وَلَئِنْ أَرْسَلْنَا رِيحًا فَرَأَوْهُ مُصْفَرًّا لَّظَلُّوا مِن بَعْدِهِ يَكْفُرُونَ ﴿٥١﴾

51. Na kama tungeutuma upepo wakauona umekuwa rangi ya njano, juu ya hayo wangeku- furu.

KATIKA ISHARA YA KILIMWENGU

Aya 46 – 51

MAANA

Na katika ishara zake ni kuzituma pepo ziletazo bishara na ili kuwaonjesha rehema yake na ili majahazi yatembee kwa amri yake; na mtafute kutokana na fadhila yake na ili mumshukuru.

Kila kitu kinachofungamana na hekima katika kupatikana kwake, ni dalili mkataa ya kukanusha sadfa na kwamba kuna makusudio na utashi katika kupatikana kwake. Dalili hii ndio makusudio ya ishara za Mwenyezi Mungu zinazofahamisha kuweko kwake.

Upepo- ukiwa ni dalili ya umoja wa Mwenyezi Mungu na uweza wakeuna faida nyingi; miongoni mwa faida hizo ni: Kuleta mawingu ya mvua yanayowashiria watu kheri, kutembea majahazi kwenye maji yakiwa yanachukua chakula kutoka mji mmoja hadi mwingine na mengineyo; kama yale aliyoyaashiria Imam Ja’far Sadiq(a.s) kwa kusema:

“Lau upepo utasimama siku tatu, basi kila kitu kitaharibika juu ya uso wa ardhi na kitavunda. Kwa sababu upepo uko kwenye daraja ya kiyoyozi kinachoondosha na kukinga uchafu kwenye kila kitu. Uko kwenye daraja ya roho ikitaka mwilini unaoza na kubadilika... Ametukuka Mwenyezi Mungu mzuri wa waumbaji.”

Na ili mshukuru.

Yaani mpate kuogopa maasi kwa siri na dhahiri. Tumeashiria huko nyuma, zaidi ya mara moja, kwamba Mwenyezi Mungu anapitisha vitu kwa sababu zake na inategemezwa kwake kwa vile yeye ndiye msababishi wa kwanza ambaye sababu zote zinakomea kwake.

Na hakika tulikwishawatuma mitume kwa kaumu zao na wakawajia na hoja zilizo waziwazi. Tukawaadhibu wale waliofanya makosa na ilikuwa ni haki juu yetu kuwanusuru waumini.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) alimtuma Muhammad(s.a.w.w) na hoja za kutosheleza; kama alivyowatuma kabla yake Ibrahim, Musa, Isa na wengineo, na hoja zilizowazi. Basi wengi wakawakadhibisha na wachache wakawaamini. Mwenyezi Mungu atawaadhibu wakadhibishaji siku hiyo kubwa na atawanusuru Mitume na walio pamoja nao.

Nusra hii ni wajibu kwa Mwenyezi Mungu aliyojiwajibishia yeye mwenyewe kama alivyojiwabishia rehema. Tazama Juz. 11 (10:3-4) kifungu cha ‘Hisabu na malipo ni lazima’

Lengo la Aya hii ni onyo kwa wale waliomkadhibisha Muhammad(s.a.w.w) kuwa yatawasibu mfano wa yaliyowasibu wale waliokadhibisha mitume yake hapo kabla.

Mwenyezi Mungu ndiye anayezituma pepo zikayatimua mawingu, kisha akayatandaza mbinguni kama apendavyo. Na akayafanya mapande mapande, basi ukaiona mvua inatoka ndani yake. Anapowafikishia awatakao katika waja wake, mara wanakuwa na furaha. Ingawaje kabla ya kuteremshiwa walikuwa wenye kukata tamaa.

Huu ni ufafanuzi wa Aya ilyotangulia: ‘Na katika ishara zake ni kuzituma pepo ziletazo bishara.’

Kwa ufupi maana ni kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) anazipeleka pepo kutimua mawingu na kuyatawanya mbinguni, kisha zinayagawa mapande mapande na kulileta kila pande kwenye mji aliooukusudia Mwenyezi Mungu.

Likifika hutoka maji mawinguni na kuanguka kwenye mji uliokusudiwa. Hapo watu wake hufurahi na kupeana habari njema. Na hapo mwanzo walikuwa wamekata tamaa.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 8 (7:57).

AKILI NA FIKRA YA UFUFUO

Angalia athari za rehema ya Mwenyezi Mungu, jinsi anavyoihuisha ardhi baada ya kufa kwake. Basi hakika huyo, bila shaka, ndiye mwenye kuhuisha wafu. Na Yeye ni Muweza wa kila kitu.

Makusudio ya rehema ya Mwenyezi Mungu hapa ni mvua na athari yake ni kuwa hai ardhi baada ya kufa. Uhai huu unaonekana kwa macho ni dalili mkataa kuwa fikra ya uhai baada ya mauti na ufufuo ni sahihi isiyokubali shaka yoyote.

Kwa sababu mwenye akili akitilia maanani na kufikiria vizuri uhai wa ardhi baada ya kufa kwake hana budi kusalimu amri na kuamini fikra ya ufufuo; vinginevyo atakuwa miongoni mwa wanaoamini kuweko kitu na kutokuweko kwa wakati mmoja, jambo ambalo haliwezekani.

Hapa ndio kuna siri ya kukaririka Aya zinazotanabahisha akili juu ya ufufuo wa ardhi baada ya kufa kwake, kama dalili ya uwezekano wa ufufuo wa watu; miongoni mwa Aya hizo ni:

وَاللَّـهُ الَّذِي أَرْسَلَ الرِّيَاحَ فَتُثِيرُ سَحَابًا فَسُقْنَاهُ إِلَىٰ بَلَدٍ مَّيِّتٍ فَأَحْيَيْنَا بِهِ الْأَرْضَ بَعْدَ مَوْتِهَا كَذَٰلِكَ النُّشُورُ ﴿٩﴾

“Mwenyezi Mungu ndiye anayezituma pepo zikayatimua mawingu, nasi tukayafikisha kwenye nchi iliyokufa tukaihuisha ardhi kwayo baada ya kufa kwake. Ndio kama hivyo kutakuwa kufufuliwa” (35:9)

Nyingine ni:

وَمِنْ آيَاتِهِ أَنَّكَ تَرَى الْأَرْضَ خَاشِعَةً فَإِذَا أَنزَلْنَا عَلَيْهَا الْمَاءَ اهْتَزَّتْ وَرَبَتْ إِنَّ الَّذِي أَحْيَاهَا لَمُحْيِي الْمَوْتَىٰ ﴿٣٩﴾

“Na miongoni mwa ishara zake ni kwamba unaiona ardhi ni nyonge, lakini tunapoiteremshia maji mara unaiona inataharaki na kuumuka. Hakika bila shaka aliyeihuisha ardhi ndiye atakayehuisha wafu.” (41:39)

Na nyinginezo nyingi.

Na kama tungeutuma upepo wakauona umekuwa rangi ya njano, juu ya hayo wangekufuru.

Yaani Mwenyezi Mungu akipeleka upepo utakaogeuza mimea yao rangi ya njano baada ya kuwa kijani, watakata tamaa na rehema ya Mwenyezi Mungu na wataipinga hekima yake na kumkufuru Yeye na neema yake.

Hii haifahamishi chochote isipokuwa imani yao kwa Mwenyezi Mungu ni njozi tu. Lau ingelikuwa imejikita moyoni wangelikuwa imara nayo katika shida na raha.

Imam Ali(a.s) amesema:“Katika imani kuna ile iliyothibiti na kutulia moyoni na kuna ile inayokaa nyoyoni na vifuani kwa muda tu.”

Mumin, kama binadamu, anaumia na kuhuzunika, anapopatwa na masaibu yeye mwenyewe, mtoto wake au mali yake, lakini hilo halimtoi kwenye dini yake. Mtume(s.a.w.w) alipofiwa na mtoto wake Ibrahim alisema: “Jicho linalia na moyo unahuzunika wala hatusemi yanayomchukiza Mola.”

فَإِنَّكَ لَا تُسْمِعُ الْمَوْتَىٰ وَلَا تُسْمِعُ الصُّمَّ الدُّعَاءَ إِذَا وَلَّوْا مُدْبِرِينَ ﴿٥٢﴾

52. Kwa hakika wewe huwezi kuwasikilizisha wafu wala kuwasikilizisha viziwi wanapogeuka kurudi nyuma.

وَمَا أَنتَ بِهَادِ الْعُمْيِ عَن ضَلَالَتِهِمْ إِن تُسْمِعُ إِلَّا مَن يُؤْمِنُ بِآيَاتِنَا فَهُم مُّسْلِمُونَ ﴿٥٣﴾

53. Wala huwezi kuwaongoza vipofu na upotevu wao. Huwezi kuwasikilizisha ila wale wanaoziamini ishara zetu, basi hao ndio watiifu.

اللَّـهُ الَّذِي خَلَقَكُم مِّن ضَعْفٍ ثُمَّ جَعَلَ مِن بَعْدِ ضَعْفٍ قُوَّةً ثُمَّ جَعَلَ مِن بَعْدِ قُوَّةٍ ضَعْفًا وَشَيْبَةً يَخْلُقُ مَا يَشَاءُ وَهُوَ الْعَلِيمُ الْقَدِيرُ ﴿٥٤﴾

54. Mwenyezi Mungu ndiye ambaye amewaumba katika udhaifu, kisha akajaalia nguvu baada ya udhaifu, kisha akajaalia udhaifu baada ya nguvu na uzee. Anaumba atakavyo. Naye ndiye Mjuzi, Mwenye uweza.

وَيَوْمَ تَقُومُ السَّاعَةُ يُقْسِمُ الْمُجْرِمُونَ مَا لَبِثُوا غَيْرَ سَاعَةٍ كَذَٰلِكَ كَانُوا يُؤْفَكُونَ ﴿٥٥﴾

55. Na siku itakaposimama Saa, wakosefu wataapa kuwa hawakukaa duniani ila saa moja. Hivyo ndivyo walivyokuwa wakigeuzwa.

وَقَالَ الَّذِينَ أُوتُوا الْعِلْمَ وَالْإِيمَانَ لَقَدْ لَبِثْتُمْ فِي كِتَابِ اللَّـهِ إِلَىٰ يَوْمِ الْبَعْثِ فَهَـٰذَا يَوْمُ الْبَعْثِ وَلَـٰكِنَّكُمْ كُنتُمْ لَا تَعْلَمُونَ ﴿٥٦﴾

56. Na waliopewa ilimu watasema: Hakika nyinyi mlikwisha kaa katika hukumu ya Mwenyezi Mungu mpaka siku ya kufufuliwa. Basi hii ndio siku ya kufufuliwa. Lakini nyinyi mlikuwa hamjui.

فَيَوْمَئِذٍ لَّا يَنفَعُ الَّذِينَ ظَلَمُوا مَعْذِرَتُهُمْ وَلَا هُمْ يُسْتَعْتَبُونَ ﴿٥٧﴾

57. Basi siku hiyo hautawafaa waliodhulumu udhuru wao wala hawatapokelewa toba yao.

وَلَقَدْ ضَرَبْنَا لِلنَّاسِ فِي هَـٰذَا الْقُرْآنِ مِن كُلِّ مَثَلٍ وَلَئِن جِئْتَهُم بِآيَةٍ لَّيَقُولَنَّ الَّذِينَ كَفَرُوا إِنْ أَنتُمْ إِلَّا مُبْطِلُونَ ﴿٥٨﴾

58. Na hakika tulikwishawapigia watu kila mfano katika hii Qur’an. Na ukiwaletea ishara yoyote bila shaka watasema wale ambao wamekufuru: Nyinyi si chochote ila ni wabatilifu.

كَذَٰلِكَ يَطْبَعُ اللَّـهُ عَلَىٰ قُلُوبِ الَّذِينَ لَا يَعْلَمُونَ ﴿٥٩﴾

59. Hivyo ndivyo Mwenyezi Mungu anavyopiga muhuri kwenye nyoyo za wasiojua.

فَاصْبِرْ إِنَّ وَعْدَ اللَّـهِ حَقٌّ وَلَا يَسْتَخِفَّنَّكَ الَّذِينَ لَا يُوقِنُونَ ﴿٦٠﴾

60. Basi subiri. Hakika ahadi ya Mwenyezi Mungu ni ya haki; wala wasikuhafifishe wale wasiokuwa na yakini.

AMEWAUMBA KATIKA UDHAIFU

Aya 52 – 60

MAANA

Kwa hakika wewe huwezi kuwasikilizisha wafu wala kuwasikilizisha viziwi wanapogeuka kurudi nyuma. Wala huwezi kuwaongoza vipofu na upotevu wao. Huwezi kuwasikilizisha ila wale wanaoziamini ishara zetu, basi hao ndio watiifu.

Zimetangulia kwa herufi zake katika Juz. 20 (27: 80 – 81).

Mwenyezi Mungu ndiye ambaye amewaumba katika udhaifu, kisha akajaalia nguvu baada ya udhaifu, kisha akajaalia udhaifu baada ya nguvu na uzee. Anaumba atakavyo. Naye ndiye Mjuzi, Mwenye uweza.

Mtu hakuwako, kisha akawa na akagura daraja mbali mbali; kuanzia mchanga hadi tone la manii, kijusi hadi kuwa mtoto wa kunyonya, kuachishwa ziwa (kunyonya) hadi kuwa mtoto mdogo na kuanzia ujana hadi uzee na ukongwe.

Udhaifu wa kwanza ulioashiriwa na Aya ni ule wa mwili na utambuzi wa akili kwenye utoto. Imesemekana kuwa ni udhaifu wa kuwa tone la manii. Ama nguvu ni ujana, na udhaifu wa pili ni wa ukongwe; kama walivyoafikiana wafasiri. Ndio maana tukasema udhaifu wa kwanza ni utoto kulinganisha na uzee ambao ndio udhaifu wa pili, kwa maafikiano ya wafasiri.

Kwa vyovyote iwavyo ni kuwa makusudio ya Aya kuashiria mabadiliko ya mtu kutoka hali moja hadi nyingine ni kuwa mtu atambue kuwa yeye yuko mikononi mwa Mwenyezi Mungu akimgeuza vile atakavyo; kumpa uhai, kumfisha, kumpa udhaifu na nguvu. Kisha marejo ni kwake.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 14 (16:70).

Na siku itakaposimama Saa, wakosefu wataapa kuwa hawakukaa duniani ila saa moja.

Makusudio ya Saa ni Siku ya Kiyama. Kusema isipokuwa saa moja ni kukusudia sehemu ya wakati katika maisha ya dunia. Maana ni kuwa wakosefu wakati watakapotolewa makaburini, wataapa kwa Mwenyezi Mungu kuwa hawakukaa makaburini isipokuwa muda mchache.

Umetangulia mfano wake kwa ufafanuzi zaidi katika Juz. 16 (20:102). Huko tumechanganya Aya tatu: ya kwanza ni ile inayosema:“Watanong’onezana wao kwa wao: Hamkukaa ila siku kumi tu.” Juz. 16 (20: 103) ya pili inasema:“Wakasema: Tumekaa siku moja au sehemu ya siku.” Juz. 15 (18:19). Ya tatu ni hii tuliyo nayo. Na tumejibu huko swali la je, zinaoana vipi Aya tatu hizo?

Hivyo ndivyo walivyokuwa wakigeuzwa.

Duniani walikuwa wakigeuza ukweli kuwa uongo huku wakiapa kuwa hakuna ufufuo wala hisabu. Na Akhera vilevile wataapa kuwa hawakukaa isipokuwa saa moja.

Na waliopewa ilimu watasema: hakika nyinyi mlikwisha kaa katika hukumu ya Mwenyezi Mungu mpaka siku ya kufufuliwa. Basi hii ndio siku ya kufufuliwa.

Wakosefu watasema watakayoyasema kuhusu muda wa kukaa kwao makaburini na watu wanaomwamini Mungu na hisabu yake na thawabu zake watawaambia: Mmekaa kiasi alichotaka Mwenyezi Mungu mkae na muda mliokaa makaburi ni wenye kuthibiti katika ujuzi wake Mwenyezi Mungu Mtukufu; wala hakuna aujuae isipokuwa Yeye.

Kuna faida gani ya kuzungumza kwenu kuapa kuhusu muda wa kukaa makaburini na hali nyinyi mlikuwa mkiikana siku hii ambayo leo mnaona vituko vyake kwa macho yenu?

Lakini nyinyi mlikuwa hamjui.

Yaani nyinyi mko kwenye upofu na upotevu ulio wazi.

Basi siku hiyo hautawafaa waliodhulumu udhuru wao wala hawat- apokelewa toba yao.

Kauli nyingine inayofanana na hii ni:

وَإِن يَسْتَعْتِبُوا فَمَا هُم مِّنَ الْمُعْتَبِينَ ﴿٢٤﴾

“Na wakiomba toba hawakubaliwi.” (41:24).

Yaani siku hiyo hakutakuwa na udhuru wala kukubaliwa toba ya mkosefu, baada ya kuhadharishwa na kuonywa akakataa isipokuwa ukafiri.

Na hakika tulikwishawapigia watu kila mfano katika hii Qur’an.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 15 (18:54).

Na ukiwaletea ishara yoyote bila shaka watasema wale ambao wamekufuru: Nyinyi si chochote ila ni wabatilifu.

Wanawaambia mitume, viongozi wema na wakombozi kuwa ni wabatilifu na waongo. Na wale wahaini na vibaraka wanaolipwa, kuwa ndio wenye haki. Hili si jambo geni; kwani mataghuti walio wakosefu wanaipima haki na batili kwa manufaa yao na hawaa zao.

Ikiwa inaafikiana nao basi hiyo ni haki hata kama ni shari na ufisadi; na inayohalifiana nao basi hiyo ni batili hata kama ni heri na wema.

Hivyo ndivyo Mwenyezi Mungu anavyopiga muhuri kwenye nyoyo za wasiojua.

Mwenyezi Mungu amepiga muhuri kwenye nyoyo zao kwa sababu wao walifuata kwa hiyari yao njia inayopelekea hilo. Kuwa kipofu na haki ni natija ya ujinga; na dhulma na utaghuti ni natija ya kuwa kombo na njia ya uongofu. Ama kunasibishwa hilo kwa Mwenyezi Mungu maana yae ni kuwa sababu za natija yake zinalazimiana naye.

Basi subiri. Hakika ahadi ya Mwenyezi Mungu ni ya haki; wala wasikuhafifishe wale wasiokuwa na yakini.

Vumilia ewe Muhammad, uendelee na mwito wako na uvumilie adha katika njia yake. Hazitapita siku nyingi ila ujumbe wako utaenea mashariki ya ardhi na magharibi yake jina lako litatajwa pamoja na jina la Mwenyezi Mungu na litaombewa rehema na taadhima.

Sifa njema ni za Mwenyezi Mungu ambaye ametuneemesha kwa Muhammad(s.a.w.w) , Mtume wa rehema na kiongozi wa watu kwenye heri. Basi turuzuku shafaa yake, ewe mwenye kubadili mabaya, pamoja na wingi wake, kwa mazuri.