TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MOJA Juzuu 21

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MOJA0%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MOJA Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: Qurani tukufu

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MOJA

Mwandishi: Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya
: HASANI MWALUPA
Kundi:

Matembeleo: 25363
Pakua: 3087


Maelezo zaidi:

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 32 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 25363 / Pakua: 3087
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MOJA

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MOJA Juzuu 21

Mwandishi:
Swahili

22

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MOJA

Sura Ya Thelathini Na Nane: Surat Saad. Imeshuka Makka, Ina aya 88

بِسْمِ اللَّهِ الرَّحْمَٰنِ الرَّحِيمِ

Kwa jina la Mwenyezi Mungu Mwingi wa rehema Mwenye kurehemu.

ص وَالْقُرْآنِ ذِي الذِّكْرِ ﴿١﴾

1. Swaad. Naapa kwa Qur’an yenye ukumbusho.

بَلِ الَّذِينَ كَفَرُوا فِي عِزَّةٍ وَشِقَاقٍ ﴿٢﴾

2. Lakini waliokufuru wamo katika majivuno na upinzani.

كَمْ أَهْلَكْنَا مِن قَبْلِهِم مِّن قَرْنٍ فَنَادَوا وَّلَاتَ حِينَ مَنَاصٍ ﴿٣﴾

3. Vizazi vingapi tumeviangamiza kabla yao, na wakapiga kelele, lakini wakati wa kuokoka ulikwishapita.

وَعَجِبُوا أَن جَاءَهُم مُّنذِرٌ مِّنْهُمْ وَقَالَ الْكَافِرُونَ هَـٰذَا سَاحِرٌ كَذَّابٌ ﴿٤﴾

4. Na walistaajabu kuwajia mwonyaji anayetokana na wao. Na makafiri wakasema: Huyu ni mchawi, mwongo.

أَجَعَلَ الْآلِهَةَ إِلَـٰهًا وَاحِدًا إِنَّ هَـٰذَا لَشَيْءٌ عُجَابٌ ﴿٥﴾

5. Amewafanya miungu wote kuwa ni Mungu Mmoja tu? Hakika hili kweli ni jambo la ajabu.

وَانطَلَقَ الْمَلَأُ مِنْهُمْ أَنِ امْشُوا وَاصْبِرُوا عَلَىٰ آلِهَتِكُمْ إِنَّ هَـٰذَا لَشَيْءٌ يُرَادُ ﴿٦﴾

6. Na wakaondoka wakubwa wao wakiwaambia: Nendeni zenu na dumuni na miungu yenu, kwani hili ni jambo lililopangwa.

مَا سَمِعْنَا بِهَـٰذَا فِي الْمِلَّةِ الْآخِرَةِ إِنْ هَـٰذَا إِلَّا اخْتِلَاقٌ ﴿٧﴾

7. Sisi hatukusikia haya katika mila hii ya mwisho. Haya si chochote ila ni uzushi tu.

أَأُنزِلَ عَلَيْهِ الذِّكْرُ مِن بَيْنِنَا بَلْ هُمْ فِي شَكٍّ مِّن ذِكْرِي بَل لَّمَّا يَذُوقُوا عَذَابِ ﴿٨﴾

8. Ati yeye ndiye aliyeteremshiwa mawaidha kati yetu?” Bali wao wana shaka na mawaidha yangu; bali hawajaionja adhabu yangu.

أَمْ عِندَهُمْ خَزَائِنُ رَحْمَةِ رَبِّكَ الْعَزِيزِ الْوَهَّابِ ﴿٩﴾

9. Au wanazo wao hazina za rehema za Mola wako, Mwenye nguvu, Mpaji?

أَمْ لَهُم مُّلْكُ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ وَمَا بَيْنَهُمَا فَلْيَرْتَقُوا فِي الْأَسْبَابِ ﴿١٠﴾

10. Au wao wana ufalme wa mbingu na ardhi na vilivyomo kati yake? Basi na wazipande sababu zote.

جُندٌ مَّا هُنَالِكَ مَهْزُومٌ مِّنَ الْأَحْزَابِ ﴿١١﴾

11. Ni jeshi litakaloshindwa miongoni mwa makundi yatayoshindwa.

NAAPA KWA QUR’AN YENYE MAWAIDHA

Aya 1 – 11

MAANA

Swaad.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 1 (2:1).

Naapa kwa Qur’an yenye ukumbusho, Lakini waliokufuru wamo katika majivuno na upinzani.

Jawabu la kiapo linakadiriwa kuwa ni ‘Hakika hiyo ni haki.’ Makuraishi walikadhibisha Qur’an ambayo ina kheri yao na enzi yao. Ndio Mwenyezi Mungu (s.w.t) akaapa kwa Qur’an yenyewe kwamba hiyo ni haki kutoka kwa Mwenyezi Mungu na kwamba hakuna sababu ya kukadhibisha huku isipokuwa kiburi cha wakadhibishaji, kuikimbia kwao haki na uadui wao kwa Muhammad(s.a.w. w ) .

Kuapa kwake Mwenyezi Mungu kwa Qur’an kunaashiria kwamba hiyo Qur’an kushinda kwake kunafahamishwa na ufasaha wake na ukweli wake unafahamishwa na mafunzo yake. Kisha Mwenyezi Mungu (s.w.t) akawahadharisha makuraishi na kuwakumbusha maangamizi ya waliotangulia pale walipowakadhibisha mitume, kwa kusema:

Vizazi vingapi tumeviangamiza kabla yao, na wakapiga kelele, lakini wakati wa kuokoka ulikwishapita.

Wa mwanzo walijizuia na haki na kuwafanya watu wa haki ni mahasimu wao; sawa na mlivyofanya nyinyi. Walipojiwa na adhabu wakaanza kurudi nyuma na kunyenyekea, lakini muda ulikwishapita tena. Kwa hiyo bora muamini sasa kabla ya kupita muda mkajuta ambapo majuto hayatafaa kitu tena.

KUMWIGA MWENYE KUMPWEKESHA MUNGU NA KUMWIGA MSHIRIKINA

Na walistaajabu kuwajia mwonyaji anayetokana na wao.

Muhammad(s.a.w. w ) ni Mkuraishi, hilo halina shaka, lakini si katika vigogo wala mataghuti wao, vipi awe ni miongoni mwao? Lau angelikuwa mion- goni mwao angewafanya watu watumwa wake na akawa na hazina au nyumba ya dhahabu. Tazama Juz. 15 (17: 90) kifungu cha ‘Kupenda mali’ na Juz. 18 (25:7) kifungu cha ‘Mantiki ya watu wa pesa ni benki na ardhi.’

Na makafiri wakasema: Huyu ni mchawi, mwongo.

Kwa nini ni muongo?

Jibu ni:

Amewafanya miungu wote kuwa ni Mungu Mmoja tu? Hakika hili kweli ni jambo la ajabu.

Ajabu kwa hawa sio kuwa Muhammad(s.a.w. w ) anapinga shirki na kuweko waungu wengi, ingawaje hilo wanaliwaza, lakini ajabu hasa ni Muhammad(s.a.w. w ) kutoka kwenye maigizo yao na mazowea yao waliyoyarithi tangu jadi na jadi. Wao hasa wanatetea kuiga kwa mababa na mababu zao kuwa ndio dini na msingi; sio kuwa wanatetea masanamu kwa kuwa ni masanamu. Wanatetea masanamu kwa vile ni turathi na urithi kutoka kwa wakale wao:

إِنَّا وَجَدْنَا آبَاءَنَا عَلَىٰ أُمَّةٍ وَإِنَّا عَلَىٰ آثَارِهِم مُّقْتَدُونَ ﴿٢٣﴾

“Kwa hakika tuliwakuta baba zetu juu ya mila na hakika sisi tunafuata nyayo zao.” (43:23).

Imani ya wajinga hawa ni sawa na imani ya washirikina, kwa sababu chimbuko la imani mbili ni moja nalo ni kuiga. Tofuati ni kuwa kumuiga mwenye kumpwekesha Mungu ni sahihi na kwenye kukubalika kwa sababu kuna msingi wa hali halisi; kama, kwa mfano, nikikuambia:

“Mwenye nadharia ya mvutano ni Newton na mwenye nadhariya ya uwiyano ni Einstein” Lakini kuiga kwa washirikina ni upotevu.

Na mwenye kuiga hivyo atabeba majukumu na atawajibishwa ila akiwa hana ajualo; kama mnyama. Kwa sababu kumshirikisha Mwenyezi Mungu hakuna msingi wowote kwake.

Kwa maneno mengine ni kuwa fikra itakuwa ni ya kweli ikiwa inatokana na uhalisi wa hali; iwe imetokana na elimu au kuiga. Tazama Juz.2 (2:168-170). Kifungu: ‘Kufuata na msingi wa itikadi.’

Na wakaondoka wakubwa wao wakiwaambia: Nendeni zenu na dumuni na miungu yenu, kwani hili ni jambo lililopangwa. Sisi hatukusikia haya katika mila hii ya mwisho. Haya si chochote ila ni uzushi tu.

Makusudio ya wakubwa wao ni vigogo wa kikuraishi. Kudumu kwenye miungu ni kudumu kuiabudu. Jambo lililopangwa ni kudumu kwenye ibada ya masanamu. Mila ya mwisho ni itikadi ya utatu ya kimasihi (kikiristo). Washirikina waliita ya mwisho kwa vile ndiyo dini ya mwisho kujitokeza wakati wao.

Kwenye Tafsir Tabariy na nyinginezo imeelezwa kuwa wazee wa kikuraishi walimwendea Abu Twalib na kumwambia: “Mwana wa nduguyo na aachane na miungu yetu nasi tutamwacha na Mungu wake anayemwabudu. Abu Twalib alipomwambia hilo Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w. w ) alisema:

“Ninawataka neno moja tu waliseme, basi waarabu na waajemi watawafuata.” Wakasema tutakukubalia hilo na mengine kumi, ni lipi hilo? Akasema: “Hapana mola isipokuwa Mwenyezi Mungu. (Lailaha illa llah)” wakaondoka zao huku wakisema: “Hivi miungu yote ameifanya kuwa mmoja!”

Riwaya hii inaafikiana na dhahiri ya Aya na inasaidiwa na hali halisi ya washirikina na nafasi ya mzee aliyelemewa.

Ati yeye ndiye aliyeteremshiwa mawaidha kati yetu?

Mwenyezi Mungu atamchagua vipi Muhammad na hali hana jaha wala mali?

Bali wao wana shaka na mawaidha yangu,

Wao ni washirikina. Kwa sababu miongoni mwao kuna waliompinga Muhammad(s.a.w. w ) kwa hasadi na wengine wakampinga kwa kulinda masilahi yao.

Bali hawajaionja adhabu yangu.

Wakishaionja shaka itawaondokea na “wataficha majuto” Juz. 11 (10:54).

Au wanazo wao hazina za rehema za Mola wako, Mwenye nguvu, Mpaji?

Makusudio ya hazina za rehema hapa ni utume tu, au utume na neema nyinginezo za Mwenyezi Mungu na hisani yake. Maana ni kuwa kwa nini washirikina wanalalamikia na kupinga rehema ya Mwenyezi Mungu ya kumchagua kwake kuwa mjumbe kwa walimwengu? Je ni kwa kuwa wao wanamiliki hiyari hii badala ya Mwenyezi Mungu?

Au wao wana ufalme wa mbingu na ardhi na vilivyomo kati yake?

Mmliki wa ulimwengu ni yule anayemiliki utume, kuutoa na kumuenzi nao amtakye. Na washirikina hawamiliki chochote kwa Mwenyezi Mungu kuweza kumpa utume mtu mkubwa kati ya miji miwili.

Kuna jambo moja ambalo wanaweza kwalo kumiliki mbingu na ardhi nalo ni Basi nawazipande sababu zote.

Makusudio ya sababu ni njia na nyenzo. Maana ni kuwa utume anauhukumu ambaye anamiliki ulimwengu na viliomo ndani yake. Basi vigogo wa kikuraishi wakitaka kumchagua kwa utume yule wanayemtaka, kabla ya chochote nawamiliki nyenzo za kufikia kwenye umiliki huu ikiwa wanaweza. Changamoto hii ni ubainifu wa kutosha kabisa.

Ni jeshi litakaloshindwa miongoni mwa makundi yatayoshindwa.

Wale waliokupiga vita, ewe Muhammad, si chochote, watashindwa mbele ya mwito pamoja na wingi wa majeshi na vikosi vyao.

كَذَّبَتْ قَبْلَهُمْ قَوْمُ نُوحٍ وَعَادٌ وَفِرْعَوْنُ ذُو الْأَوْتَادِ ﴿١٢﴾

12. Walikadhibisha kabla yao kaumu ya Nuh, na kina A’adi na Firauni mwenye vigingi.

وَثَمُودُ وَقَوْمُ لُوطٍ وَأَصْحَابُ الْأَيْكَةِ أُولَـٰئِكَ الْأَحْزَابُ ﴿١٣﴾

13. Na Thamud na kaumu ya Lut na watu wa mwituni. Hayo ndiyo makundi.

إِن كُلٌّ إِلَّا كَذَّبَ الرُّسُلَ فَحَقَّ عِقَابِ ﴿١٤﴾

14. Wote waliwakadhibisha Mitume; basi wakastahili adhabu yangu.

وَمَا يَنظُرُ هَـٰؤُلَاءِ إِلَّا صَيْحَةً وَاحِدَةً مَّا لَهَا مِن فَوَاقٍ ﴿١٥﴾

15. Na hawa hawangojei ila ukelele mmoja tu usio na muda.

وَقَالُوا رَبَّنَا عَجِّل لَّنَا قِطَّنَا قَبْلَ يَوْمِ الْحِسَابِ ﴿١٦﴾

16. Na wao husema: Mola wetu Tuletee upesi sehemu yetu kabla ya Siku ya Hisabu.

اصْبِرْ عَلَىٰ مَا يَقُولُونَ وَاذْكُرْ عَبْدَنَا دَاوُودَ ذَا الْأَيْدِ إِنَّهُ أَوَّابٌ ﴿١٧﴾

17. Subiri kwa wayasemayo, Na umkumbuke mja wetu Daud. Mwenye nguvu. Hakika yeye alikuwa mwingi wa kutubia.

إِنَّا سَخَّرْنَا الْجِبَالَ مَعَهُ يُسَبِّحْنَ بِالْعَشِيِّ وَالْإِشْرَاقِ ﴿١٨﴾

18. Hakika tuliidhalilisha milima pamoja naye ikisabihi jioni na asubuhi

وَالطَّيْرَ مَحْشُورَةً كُلٌّ لَّهُ أَوَّابٌ ﴿١٩﴾

19. Na pia ndege waliokusanywa makundi; wote walikuwa wanyenyekevu kwake.

وَشَدَدْنَا مُلْكَهُ وَآتَيْنَاهُ الْحِكْمَةَ وَفَصْلَ الْخِطَابِ ﴿٢٠﴾

20. Na tukautia nguvu ufalme wake. Na tukampa hikima na kukata hukumu.

SUBIRI JUU YA HAYO WANAYOSEMA

Aya 12 – 20

MAANA

Walikadhibisha kabla yao kaumu ya Nuh, na kina A’adi na Firauni mwenye vigingi Na Thamud na kaumu ya Lut na watu wa mwituni.

Wote hawa waliwakanusha mitume; baadhi yao wakaangamizwa kwa tufani; kama vile watu wa Nuh, wengine kwa kuzama baharini, kama Firauni.

Kuwa na vigingi ni kinaya cha kujikita ufalme wake kama linavyokitwa hema na vigingi kwenye ardhi.

“Basi Thamud waliangamizwa kwa balaa kubwa (la ukelele wa adhabu). Ama A’d waliangamizwa kwa upepo mkali usiozuilika” (69:5-6).

Kaumu ya Lut majumba yao yalipinduliwa juu chini. Tazama Juz. 12 (11:82). Watu wa mwituni Mwenyezi Mungu aliwaadhibu adhabu chungu. Tazama Juz.14 (15:78) na Juz. 19 (26:176).

Hayo ndiyo makundi. Wote waliwakadhibisha Mitume; basi wakastahili adhabu yangu.

Mwenyezi Mungu aliviadhibu vikosi vya shetani kwa sababu ya madhambi yao; ikiwa ni malipo ya yale waliyoyafanya. Je, wanaomkadhibisha Muhammad(s.a.w.w) hawahofii kuwafika yaliyowafika hao.

Na hawa hawangojei ila ukelele mmoja tu usio na muda.

Hawa ni waliomkadhibisha Muhammad(s.a.w.w) . Maana ni; wanangoja nini kwa Mungu baada ya kukukadhibisha ewe Muhammad na hali Mwenyezi Mungu, kwa neno moja tu anaweza kuwapelekea adhabu itayowafyeka katika muda ambao hawataweza kuusia wala kurudi kwa watu wao.

Na wao husema: Mola wetu! Tuletee upesi sehemu yetu kabla ya Siku ya Hisabu.

Yaani sehemu yetu ya adhabu. Mwenyezi Mungu (s.w.t) aliwatishia na adhabu ya Jahannam kupitia kwa Mtume wake mtukufu, lakini wao wakasema kwa madharau kuwa ikiwa ni kweli basi anangoja nini mpaka siku ya Kiyama? Basi na iwe duniani sio akhera.

Subiri kwa wayasemayo, kuwa wewe ni mwongo na mengineyo ya uzushi. Kwani mwisho wa mambo yao ni hasara na kusalimu amri.

Mtume(s.a.w.w) alisubiri na kuvumilia adha ya washirikina kwa muda wa mika 13 na vitimbi vya wanafiki kwa miaka kadhaa huko Madina. Alivumilia muda huu mrefu akiwa na mategemeo ya mustkabali hata kama utachelewa. Hazikupita siku Muhammad(s.a.w.w) akashinda kwa msaada wa Mwenyezi Mungu, na akaudhihirisha uislamu kuliko dini zote, wajapochukia washirikina.

Na umkumbuke mja wetu Daud.

Hili ni jina la kiebrania lenye maana ya mpendwa (mahboob). Yeye alikuwa mfalme wa pili wa Kiyahudi, wa kwanza alikuwa Talut:

إِنَّ اللَّـهَ قَدْ بَعَثَ لَكُمْ طَالُوتَ مَلِكًا ﴿٢٤٧﴾

“Hakika Mwenyezi Mungu amewachagulia Talut kuwa mfalme.” Juz. 2 (2:247).

Tawrat imemwita Talut huyu kwa jina la Shaul (Saulo). Imeelezwa kwenye Kamusi ya Kitabu kitakatifu’ kwamba Shaul ndiye mfalme wa kwanza wa waisrail na kwamba Daud alipigana katika jeshi lake. Razi anasema kuwa Mwenyezi Mungu amemsifu Daud kwa sifa nyingi. Kisha akazifafanua kwenye kurasa nne. Tutazifupiliza kwenye mistari ifuatayo: Mwenyezi Mungu alimwambia Muhammad(s.a.w.w) :

Subiri kwa wayasemayo, na umkumbuke mja wetu Daud.

Hii ni karama kwa Daud.

Mwenye nguvu; yaani mwenye nguvu ya kumtii Mwenyezi Mungu.

Hakika yeye alikuwa mwingi wa kutubia; yaani akiyarudisha mambo yote kwa Mwenyezi Mungu.

Hakika tuliidhalilisha milima pamoja naye ikisabihi jioni na asubuhi pamoja naye. Na pia ndege waliokusanywa makundi; wote walikuwa wanyenyekevu kwake.

Mfano wake ni kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu:

يَا جِبَالُ أَوِّبِي مَعَهُ وَالطَّيْرَ ﴿١٠﴾

“Enyi milima sabihini pamoja naye na ndege” Juz. 22 (34:10).

وَسَخَّرْنَا مَعَ دَاوُودَ الْجِبَالَ يُسَبِّحْنَ وَالطَّيْرَ ﴿٧٩﴾

“Na tuliidhalilisha milima na ndege pamoja na Daud ikisabihi.” Juz. 17: (21:79).

Kwa maelezo zaid kuhusu Daud rejea huko.

Na tukautia nguvu ufalme wake.

Na tukampa hikima.

Ambayo ni kukiweka kitu mahali pake. Kwa ibara ya Razi ni elimu na kuitumia. Imeitwa hivyo kwa sababu hekima ni kupanga mambo na kuyaweka sawa.

Na kukata hukumu.

Razi anasema ni uwezo wa kudhibiti maana na kuyatolea tafsiri ya upeo wa juu. Hivi ni zaidi ya tunavyofahamu kuwa kukata hukumu ni elimu ya kuhukumu, kwa uadilifu, mambo ya wanaoteta.

Hivi ndivyo Qur’an ilivyomsifu Daud kwa sifa bora za ukamilifu, lakini Tawrat imemsifu kwa sifa mbaya mbaya; kama dhulma, ufuska, hadaa na kunyanyag’anya wanawake; kiasi amabacho waliochangia kuweka kamusi ya Kitabu Kitakatifu wakasema katika ukurasa 365, chapa ya mwezi Machi 1967, ninanukuu: “Mara nyingine Daud aliweza kufanya mambo ya kufedhehesha na ya aibu.”

23

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MOJA

وَهَلْ أَتَاكَ نَبَأُ الْخَصْمِ إِذْ تَسَوَّرُوا الْمِحْرَابَ ﴿٢١﴾

21. Na je, imekufikia habari ya wagombanao walipopindukia ukuta kuingia mihrabu.

إِذْ دَخَلُوا عَلَىٰ دَاوُودَ فَفَزِعَ مِنْهُمْ قَالُوا لَا تَخَفْ خَصْمَانِ بَغَىٰ بَعْضُنَا عَلَىٰ بَعْضٍ فَاحْكُم بَيْنَنَا بِالْحَقِّ وَلَا تُشْطِطْ وَاهْدِنَا إِلَىٰ سَوَاءِ الصِّرَاطِ ﴿٢٢﴾

22. Walipomuingilia Daudi, naye akawaogopa. Wakasema: Usiogope! Ni mahasimu wawili, mmoja wetu amemdhulumu mwenziwe. Basi tuhukumu kwa haki, wala usipendelee. Na utuongoze kwenye njia iliyo sawa.

إِنَّ هَـٰذَا أَخِي لَهُ تِسْعٌ وَتِسْعُونَ نَعْجَةً وَلِيَ نَعْجَةٌ وَاحِدَةٌ فَقَالَ أَكْفِلْنِيهَا وَعَزَّنِي فِي الْخِطَابِ ﴿٢٣﴾

23. Hakika huyu ndugu yangu ana kondoo wa kike tisini na tisa; na mimi nina kondoo mke mmoja. Akasema: Nipe huyo! Na amenishinda kwa maneno.

قَالَ لَقَدْ ظَلَمَكَ بِسُؤَالِ نَعْجَتِكَ إِلَىٰ نِعَاجِهِ وَإِنَّ كَثِيرًا مِّنَ الْخُلَطَاءِ لَيَبْغِي بَعْضُهُمْ عَلَىٰ بَعْضٍ إِلَّا الَّذِينَ آمَنُوا وَعَمِلُوا الصَّالِحَاتِ وَقَلِيلٌ مَّا هُمْ وَظَنَّ دَاوُودُ أَنَّمَا فَتَنَّاهُ فَاسْتَغْفَرَ رَبَّهُ وَخَرَّ رَاكِعًا وَأَنَابَ ﴿٢٤﴾

24. Akasema: Kweli amekudhulumu kwa kumtaka kondoo wako mmoja kuongezea kwenye kondoo wake. Na hakika washirika wengi hudhulumiana wao kwa wao. Isipokuwa walioamini na wakatenda mema. Na hao ni wachache. Na Daud akaona kuwa tumemfanyia mtihani. Basi akamwomba maghufira Mola wake na akaanguka kunyenyekea na kutubia.

فَغَفَرْنَا لَهُ ذَٰلِكَ وَإِنَّ لَهُ عِندَنَا لَزُلْفَىٰ وَحُسْنَ مَآبٍ ﴿٢٥﴾

25. Basi tukamghufiria kwa hayo. Naye kwa hakika anao ukuruba na marejeo mazuri kwetu.

KONDOO 99 KWA KONDOO 1

Aya 21 – 25

TAFSIRI NA HADITH ZA KIISRAIL

Baadhi ya wafasiri, wakifafanua Aya hii, wamemnasibishia Nabii Daud mambo ambayo si laiki hata ya mtu wa kawaida mwenye murua na haya; sikwambii tena mtume aliye maasumu. Wakataja kisa kirefu kutoka katika Biblia kitabu cha 2 Samweli: 11 na 12, kutoka agano la kale ambalo mahala pake pamechukuliwa na hukumu ya Qur’an. Nukuu za agano lenyewe kuhusiana na hilo haziingiliki akili.

Muhtasari wa kisa chenyewe ni kuwa Daud alimtamani mke wa mmoja wa watumishi wake aliye pia mwanajeshi wake. Basi akamfanyia hila ya kumuua ili amchukue mkewe. Biblia inasema kuwa Mwenyezi Mungu alikasirika sana na kumkemea kwa kitendo kibaya alichokifanya; miongoni mwa aliyoyasema ni “…Umempiga Uria, Mhiti, kwa upanga, nawe ukamtwaa mkewe awe wako… Basi sasa upanga hautaondoka nyumbani mwako, kwa sababu umenidharau…Nitakuondokeshea uovu katika nyumba yako, nami nitawatwaa wake zako mbele ya macho yako na kumpa jirani yako, naye atalala na wake zako mbele ya jua hili. Maana wewe ulifanya jambo hili kwa siri; bali mimi nitalifanya jambo hili mbele ya Israil wote na mbele ya jua” (2 Samweli 12:9-12.).

Katika 1 Wafalme 1 imeelezwa kuwa jina la mke wa Uria ni Bath-sheba naye ndiye mama yake Suleiman bin Daud.

Daud azini kwa siri na Mwenyezi Mungu, badala ya kumpa adhabu ya hadd ya zina au kumlaumu na kumtaka atubie, badala ya kumfanyia hivyo, anamtia adabu kwa kuwavunjia heshima wakeze wawe uchi na wafanye machafu hadharani kweupe mchana kadmanasi!

Haya ndio maandiko matakatifu yanavyomsifu muumba kwa sifa za unyama. Mwenyezi Mungu Mtukufu ametakata kabisa na hayo wanayomsifu nayo. Huu ni mfano mmoja kati ya mifano kadhaa. Soma kuhusu kupigana miereka Mwenyezi Mungu na Ya’qub na kushindikana kupatikana mshindi, mpaka Ya’qub akalazimika kupiga mfupa wa paja wa Mwenyezi Mungu.

Vile vile soma yaliyoandikwa kwenye biblia, Kumbukumbu la Torat, 7, kwamba Mungu amewahalalishia Mayahudi kula mataifa yote, bila ya huruma. Baadhi ya wafasiri wametegemea Hadith hizi za kiisrail, katika kufasiri Aya za Qur’an yenye mawaidha, biashara na maonyo; ikiwemo hii tuliyo nayo. Kwa hiyo ni juu ya msomaji kuzikabili kauli zao na tafsiri zao kwa jicho la hadhari sana.

MAANA

Na je, imekufikia habari ya wagombanao walipopindukia ukuta kuingia mihrabu. Walipomuingilia Daudi, naye akawaogopa.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) anamsilmulia Nabii wake mtukufu kisa cha Daud, kwamba siku moja Daud alipokuwa amemwelekea Mola wake kwenye mswala wake, ghafla watu wawili wakajitokeza mbele yake ana kwa ana. Basi kushtukiza huku kulimshtua; tena kuingia kwao kwa njia isiyokuwa ya kawaida.

Hata hivyo kuingia kwao huko, kusikokuwa kwa kawaida, hakufahamishi lolote kuwa ni malaika; kama walivyolitolea dalili baadhi ya wafasiri. Kwa sababu hata binadamu pia anaweza kuingia nyumbani kwa njia isiyokuwa ya kawaida kutokana na sababu fulani. Pia Aya haikuashiria kuwa ni malai- ka. Kwa hiyo hakuna sababu ya kuleta taawili ya kuwa ni malaika.

Wakasema: Usiogope! Ni mahasimu wawili, mmoja wetu amemdhulumu mwenziwe. Basi tuhukumu kwa haki, wala usipendelee. Na utuon- goze kwenye njia iliyo sawa.

Walipoona hofu iliyomjaa, haraka sana wakamtuliza na kusema, sisi tumekuja kwako kuhukumiwa, basi utuhukumu kwa uadilifu na utuongoze kwenye haki wala usikengeuke nayo. Kisha mmoja wao akasema:

Hakika huyu ndugu yangu ana kondoo wa kike tisini na tisa; na mimi nina kondoo mke mmoja. Akasema: Nipe huyo! Na amenishinda kwa maneno.

Hapa hakuna haja yoyote ya kuleta taawili. Dhahiri ya Aya inaonyesha kuwa tukio hili lilitokea wakati wa zama za Nabii Daud; nalo lina mfano wake katika kila zama na kila wakati; hasa wakati wetu huu wa sasa. Kwa hiyo ni wajibu kuichukulia dhahiri yake na kuitumia.

Akasema: Kweli amekudhulumu kwa kumtaka kondoo wako mmoja kuongezea kwenye kondoo wake.

Daud aliyasema haya kabla ya kusikiliza ushahidi kutoka kwa mdai na kujibu mdaiwa.

Na hakika washirika wengi hudhulumiana wao kwa wao.

Hapa itabidi kuchukulia majazi neno washirikia, kuwa na maana ya wenye mabavu. Kwa sababu hakukua na ushirika wowote kati ya wale mahasimu wawili.

Isipokuwa walioamini na wakatenda mema. Na hao ni wachache.

Nguvu inakuwa ni ya haki ikiwa kwa watu wema, lakini ikiwa kwa waovu basi, bila shaka yoyote, itakuwa dhidi ya haki. Na watu wema ni wachache kwa idadi, lakini wana nguvu katika maadili yao na sifa zao.

Na Daud akaona kuwa tumemfanyia mtihani. Basi akamwomba maghufira Mola wake na akaanguka kunyenyekea na kutubia

Baada ya Daud kutoa hukumu, alitanabahi kuwa amehukumu kabla ya kutaka dalili upande wa pili. Kwa hiyo akajuta na akamuomba msamaha Mwenyezi Mungu.

Basi tukamghufiria kwa hayo. Naye kwa hakika anao ukuruba na marejeo mazuri kwetu.

Mwenyezi Mungu alimsamehe Daud kwa vile alikuwa ni miongoni mwa waliotangulia kumtii Mwenyezi Mungu na kutaka radhi yake.

Katika kitabu Uyunil-akhbar, imeelezwa kuwa mtu mmoja alimuuliza Imam Ar-Ridha(a.s ) kuhusu kisa cha Daud na Uria na mkewe, Imam akapinga yanayonasibishiwa Daud. Muulizaji akauliza: Kosa lake lilikuwa nini ewe mwana wa Mtume wa Mwenyezi Mungu? Basi akajibu kwa jawabu refu, miongoni mwake ni: “Daud alifanya haraka kusema: “Kweli amekudhulumu kwa kumtaka kondoo wako mmoja kuongezea kwenye kondoo wake,” bila ya kumuuliza yule mwingine unasemaje? Basi hilo likuwa ni kosa la rasimu ya mahakama, sio kosa la wanavyosema watu.

Kwani hukusikia Mwenyezi Mungu Mtukufu alivyomwambia Daud: “Basi wahukumu watu kwa haki, wala usifuate matamanio Ewe Daudi! Hakika Sisi tumekufanya uwe Khalifa ardhini.”

Unaweza kuuliza : Vipi Daud alihukumu bila ya ushahidi, na tunajua kuwa mitume wamehifadhiwa na makosa (ni maasumu).

Jibu : kuwa maasumu hakumaanishi kuwa na maumbile mengine yasiyokuwa ya kibinadamu, hapana! Maasumu ni mtu kama watu wengine. Maana ya isma ni kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) anamlinda wakati wowote; hata wakijaribu watu kumhadaa kwa mandhari ya uzuri, basi Mwenyezi Mungu mara moja humwongoza kwenye haki na uhakika, kabla ya kuiingia mtegoni. Na hivyo ndivyo ilivyomtokea Daud. Mwenye kondoo mmoja alijaribu kumhadaa kwa namna yake ya kutaka kuhurumiwa, lakini Mwenyezi Mungu alimpa ilhamu ya uhakika kabla ya kutoa hukumu, akafahamu na akatubia.

Mtume alitokewa na yaliyo karibu na haya na akakurubia kuhadaiwa lau si Mwenyezi Mungu kumwimarisha kwa kumwambia: “Hakika tumekuteremshia Kitabu kwa haki ili upate kuhukumu baina ya watu kwa alivyokufahamisha Mwenyezi Mungu; wala usiwe mtetezi wa wenye kufanya hiyana. Na muombe maghufira Mwenyezi Mungu. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwingi wa maghufira Mwenye kurehemu. Wala usiwatetee wale ambao wamezihini nafsi zao...” Juz. 5 (4:105 – 107).

Na akasema Mwenyezi Mungu kumwambia Mtume wake Mtukukufu:

وَلَوْلَا أَن ثَبَّتْنَاكَ لَقَدْ كِدتَّ تَرْكَنُ إِلَيْهِمْ شَيْئًا قَلِيلًا ﴿٧٤﴾

“Lau sikukuweka imara ungelikurubia kuwaelekea kidogo.” Juz. 15 (17:74).

Kuna Hadith isemayo: “Mimi ni mtu kama nyinyi, isipokuwa ninapewa wahyi tu. Na nyinyi mnakuja kuamuliwa kwangu. Pengine mmoja wenu anaweza kuwa hodari wa kusema kuliko mwingine na nikahukumu kulingana na nilivyosikia.

Ikiwa mtu nitamuhukumia kumpatia kitu katika haki ya ndugu yake, basi ajue ninampatia kipande cha Moto.”

Ingawaje Hadith hii haingii moja kwa moja kwenye maudhui haya tuliyo nayo, lakini tunaweza kuiunganisha nayo. Ama toba ya manabii na kutaka kwao maghufira ya dhambi, hiyo ni aina ya ibada na unyenyekevu kwa Mwenyezi Mungu (s.w.t). Hilo tumeliashiria mara kadhaa.

يَا دَاوُودُ إِنَّا جَعَلْنَاكَ خَلِيفَةً فِي الْأَرْضِ فَاحْكُم بَيْنَ النَّاسِ بِالْحَقِّ وَلَا تَتَّبِعِ الْهَوَىٰ فَيُضِلَّكَ عَن سَبِيلِ اللَّـهِ إِنَّ الَّذِينَ يَضِلُّونَ عَن سَبِيلِ اللَّـهِ لَهُمْ عَذَابٌ شَدِيدٌ بِمَا نَسُوا يَوْمَ الْحِسَابِ ﴿٢٦﴾

26. Ewe Daudi! Hakika Sisi tumekufanya uwe Khalifa ardhini. Basi wahukumu watu kwa haki, wala usifuate matamanio, yakakupoteza Njia ya Mwenyezi Mungu. Hakika wanaopotea Njia ya Mwenyezi Mungu, watapata adhabu kali kwa sababu ya kusahau kwao Siku ya Hisabu.

وَمَا خَلَقْنَا السَّمَاءَ وَالْأَرْضَ وَمَا بَيْنَهُمَا بَاطِلًا ذَٰلِكَ ظَنُّ الَّذِينَ كَفَرُوا فَوَيْلٌ لِّلَّذِينَ كَفَرُوا مِنَ النَّارِ ﴿٢٧﴾

27. Na hatukuziumba mbingu na ardhi na vilivyomo kati yake bure. Hiyo ni dhana ya waliokufuru. Ole wao walio kufuru kwa Moto.

أَمْ نَجْعَلُ الَّذِينَ آمَنُوا وَعَمِلُوا الصَّالِحَاتِ كَالْمُفْسِدِينَ فِي الْأَرْضِ أَمْ نَجْعَلُ الْمُتَّقِينَ كَالْفُجَّارِ ﴿٢٨﴾

28. Je! Tuwafanye walioamini na wakatenda mema kama wafisadi katika ardhi? Au tuwafanye wenye takua kama waovu?

كِتَابٌ أَنزَلْنَاهُ إِلَيْكَ مُبَارَكٌ لِّيَدَّبَّرُوا آيَاتِهِ وَلِيَتَذَكَّرَ أُولُو الْأَلْبَابِ ﴿٢٩﴾

29. Hiki ni Kitabu, tumekuteremshia wewe, kimebarikiwa, ili wazizingatie Aya zake, na wawaidhike wenye akili.

TUMEKUFANYA UWE KHALIFA ARDHINI

Aya 26 – 29

MAANA

Ewe Daudi! Hakika Sisi tumekufanya uwe Khalifa ardhini.

Kila mtu aliyeko, au atakayekuweko, ardhini basi huyo ni khalifa wa Mwenyezi Mungu ardhini; kwa maana yakuwa ana majukumu mbele ya Mwenyezi Mungu ya kufanya mambo ya heri duniani na Akhera katika maisha haya.

Hayo ndio maana ya ukhalifa ardhini kwa hali yoyote ile; isipokuwa watu wanatofautiana kulingana na majukumu yenyewe; ambapo kila mmoja anatakiwa atekeleze kulingana na uwezo na wadhifa wake.

Kwa kuwa wadhifa wa manabii ni kutoa bishara na hadhari, ili watu wasiwe na hoja mbele ya Mwenyezi Mungu, basi imekuwa ni wajibu kwao kuwahukumu watu kwa haki na wengine wawasikilize wao.

Basi wahukumu watu kwa haki, wala usifuate matamanio, kwa sababu unabii uko hivyo kimaumbile.

Kwa maneno mengine ni kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t.) anamchagulia wahyi wake yule anayeiamini haki na kuitumia na inakuwa ni muhali kwake kukosea.

Yakakupoteza Njia ya Mwenyezi Mungu. Hakika wanaopotea Njia ya Mwenyezi Mungu, watapata adhabu kali kwa sababu ya kusahau kwao Siku ya Hisabu.

Muovu zaidi katika watu ni yule mwenye kumhalifu Mola wake na akafuata matamanio yake. Kuna Hadith isemayo: “Hakika ninalolihofia zaidi kwenu ni hawaa na tamaa nyingi. Hawaa inaipinga haki na tamaa nyingi inasahauliza akhera.”

Na hatukuziumba mbingu na ardhi na viliomo kati yake bure.

Lau katika kuumbwa mbingu na ardhi kungelikua na chembe ya mchezo au hivi hivi tu, basi ulimwengu usingeendelea na nidhamu kwa mamilioni ya miaka.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 4 (3:191).

Hiyo ni dhana ya waliokufuru. Ole wao waliokufuru kwa Moto.

Hiyo inaashiria kuwa hakuna tofauti kati ya aneyepinga kuweko Mwenyezi Mungu kabisa na yule anayekubali, lakini akapinga kuweko hekima katika kuumba kwake. Kwa sababu dalili zake ni wazi na alama zake ziko kweupe.

Imam Ali(a.s ) anasema:“Amekadiria aliyoumba akapangilia makadirio yake; akapangilia akafanya kwa uangalifu mipangilio yake; akaelekeza kwa maelekezo yake, lakini hakupetuka mpaka wa cheo chake wala hakupunguza ukomo wa lengo lake.”

Je! Tuwafanye walioamini na wakatenda mema kama wafisadi katika ardhi? Au tuwafanye wenye takua kama waovu?

Tofauti baina ya mwema na mfisadi na baina ya mwenye takua na muovu ni sawa na tofauti baina ya kipofu na mwenye kuona. Umetangulia mfano wake katika Juz. 7 (5:100) na Juz. 7 (6:50).

Katika kitabu Ahkamul-qur’an cha Kadhi Abi Bakri, ambaye ni maarufu kwa jina la Ibnul-arabiy, amesema: “Aya hii iliwashukia bani Hashim; na kwamba walioamini na kuwa na takua ni Ali bin Abi Twalib, ndugu yake Ja’far, Ubayda bin Tufayl, Al-harth bin Tufayl, Ummu ayman na wengineo, na kwamba wafisadi na waovu ni Bani Abd Shams.

Hiki ni Kitabu, tumekuteremshia wewe, kimebarikiwa, ili wazizingatie Aya zake, na wawaidhike wenye akili.

Hapa anaambiwa Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w. w ) . Kitabu ni Qur’an, nayo ina baraka kwa kila mwenye kuiamini, ni dawa ya ukafiri na hulka mbaya na ni uokovu wa shirki na maangamizi. Kwenye Nahjul-Balagha imeelezwa:“Itakeni nasaha kwa nafsi zenu na mzituhumu rai zenu kwayo na mtake uokofu wa hawa zenu ndani yake.”