TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MOJA Juzuu 21

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MOJA0%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MOJA Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: Qurani tukufu

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MOJA

Mwandishi: Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya
: HASANI MWALUPA
Kundi:

Matembeleo: 25581
Pakua: 3259


Maelezo zaidi:

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 32 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 25581 / Pakua: 3259
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MOJA

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MOJA Juzuu 21

Mwandishi:
Swahili

7

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MOJA

وَقَالَ الَّذِينَ كَفَرُوا لَن نُّؤْمِنَ بِهَـٰذَا الْقُرْآنِ وَلَا بِالَّذِي بَيْنَ يَدَيْهِ وَلَوْ تَرَىٰ إِذِ الظَّالِمُونَ مَوْقُوفُونَ عِندَ رَبِّهِمْ يَرْجِعُ بَعْضُهُمْ إِلَىٰ بَعْضٍ الْقَوْلَ يَقُولُ الَّذِينَ اسْتُضْعِفُوا لِلَّذِينَ اسْتَكْبَرُوا لَوْلَا أَنتُمْ لَكُنَّا مُؤْمِنِينَ ﴿٣١﴾

31. Na walisema waliokufuru: Hatutaiamini Qur’an hii, wala yaliyokuwa kabla yake. Na ungeliwaona madhalimu watakaposimamishwa mbele ya Mola wao wakirudishiana maneno! wale wanyonge wakiwaambia wale waliojifanya wakubwa: Lau si nyinyi bila shaka tungelikuwa waumini.

قَالَ الَّذِينَ اسْتَكْبَرُوا لِلَّذِينَ اسْتُضْعِفُوا أَنَحْنُ صَدَدْنَاكُمْ عَنِ الْهُدَىٰ بَعْدَ إِذْ جَاءَكُم بَلْ كُنتُم مُّجْرِمِينَ ﴿٣٢﴾

32. Wale waliojiona wakubwa watawaambia wale wanyonge: Kwani sisi ndio tuliowazuia na uongofu baada ya kuwafikia? Bali nyinyi wenyewe mlikuwa waovu. Kwani wanalipwa ila kwa waliokuwa wakiyatenda?

وَقَالَ الَّذِينَ اسْتُضْعِفُوا لِلَّذِينَ اسْتَكْبَرُوا بَلْ مَكْرُ اللَّيْلِ وَالنَّهَارِ إِذْ تَأْمُرُونَنَا أَن نَّكْفُرَ بِاللَّـهِ وَنَجْعَلَ لَهُ أَندَادًا وَأَسَرُّوا النَّدَامَةَ لَمَّا رَأَوُا الْعَذَابَ وَجَعَلْنَا الْأَغْلَالَ فِي أَعْنَاقِ الَّذِينَ كَفَرُوا هَلْ يُجْزَوْنَ إِلَّا مَا كَانُوا يَعْمَلُونَ ﴿٣٣﴾

33. Na wale wanyonge watawaambia wale waliojifanya wakubwa: Bali ni vitimbi vyenu vya usiku na mchana, mlipokuwa mkituamrisha tumkufuru Mwenyezi Mungu na tumfanyie washirika, nao wataficha majuto watakapoiona adhabu. Na tutaweka minyororo shingoni mwa wale waliokufuru kwani wanalipwa ila kwa waliokuwa wakiyatenda?.

HAWATAAMINI QUR’AN

Aya 31-33

MAANA

Na walisema waliokufuru: Hatutaiamini Qur’an hii, wala yaliyokuwa kabla yake, kama vile Tawrat na Injil. Walioyasema haya ni washirikina, kwa dalili ya kauli yake Mwenyezi Mungu:

وَقَالَ الرَّسُولُ يَا رَبِّ إِنَّ قَوْمِي اتَّخَذُوا هَٰذَا الْقُرْآنَ مَهْجُورًا {30 }

Na Mtume alisema: Ewe Mola wangu! Hakika watu wangu wameifanya hii Qur’an ni mahame.” Juz. 19 (25:30).

Wameihama na kuikana kwa sababu inamfanya sawa mweusi na mweupe na ikawaambia:

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا لَا يَسْخَرْ قَوْمٌ مِّن قَوْمٍ عَسَىٰ أَن يَكُونُوا خَيْرًا مِّنْهُمْ وَلَا نِسَاءٌ مِّن نِّسَاءٍ عَسَىٰ أَن يَكُنَّ خَيْرًا مِّنْهُنَّ وَلَا تَلْمِزُوا أَنفُسَكُمْ وَلَا تَنَابَزُوا بِالْأَلْقَابِ بِئْسَ الِاسْمُ الْفُسُوقُ بَعْدَ الْإِيمَانِ وَمَن لَّمْ يَتُبْ فَأُولَـٰئِكَ هُمُ الظَّالِمُونَ ﴿١١﴾

“Enyi ambao mmeamini! Wanaume wasiwadharau wanaume wengine, huenda wakawa bora kuliko wao; wala wanawake kwa wanawake wengine, huenda wakawa bora kuliko wao. Wala msitiane kasoro, wala msiitane majina ya kejeli. Ni uovu kutumia jina baya baada ya imani.” (49:11).

Vile vile waliukana utume wa Muhammad(s.a.w. w ) kwa sababu alitaka kuwatoa kwenye ujinga na kurudi nyuma, waende kwenye elimu na maendeleo.

Mtaalamu mmoja wa Ulaya, Jack Rezler, aliyeandika kitabu kuhusu mwamko wa kiislamu na kingine kinachozungumzia maendeleo ya waarabu ambavyo vilichapishwa ufaransa mnamo 1962, alisema: “Hatua ya kwanza ya maendeleo ya waarabu ilianza kwa kujitokeza dini ya kiislamu.

Kuna sababu kadhaa zilizofanya maendeleo haya na kuenea kwake; sababu kubwa zaidi ni kuweko na roho ya kimaana kwa Waislamu kupitia dini hii mpya; jambo ambalo limeleta ushujaa, kiasi cha kufikia kuyadharau mauti kwa ajili ya Mwenyezi Mungu.”

Na ungeliwaona madhalimu watakaposimamishwa mbele ya Mola wao wakirudishiana maneno!

Baada ya Mtume(s.a.w. w ) kukata tamaa kuwa washirikina wataamini, Mola Mtukufu alimtuliza na kumwambia kuwa kesho utaona hawa waongo watakavyokuwa dhalili na kuhizika pale watakaposimama mbele ya Mwenyezi Mungu kwa hisabu, jinsi mfuasi atakavyomlaumu aliyemfuata kila mmoja atamtia makosani mwinginewale wanyonge wakiwaambia wale waliojifanya wakubwa: Lau si nyinyi bila shaka tungelikuwa waumini.

Wanyonge ni wale wafuasi; na waliojifanya wakubwa ni viongozi.

Wale waliojiona wakubwa watawaambia wale wanyonge: Kwani sisi ndio tuliowazuia na uongofu baada ya kuwafikia? Bali nyinyi wenyewe mlikuwa waovu, sawa na kauli yake Mwenyezi Mungu:

كَمَثَلِ الشَّيْطَانِ إِذْ قَالَ لِلْإِنسَانِ اكْفُرْ فَلَمَّا كَفَرَ قَالَ إِنِّي بَرِيءٌ مِّنكَ إِنِّي أَخَافُ اللَّـهَ رَبَّ الْعَالَمِينَ ﴿١٦﴾

“Kama mfano wa shetani anapomwambia mtu: Kufuru. Na akikufuru humwambia: Mimi si pamoja nawe. Hakika mimi namwogopa Mwenyezi Mungu, Mola wa walimwengu. (59:16).

Sio mbali kuwa shetani katika Aya hii ni kinaya cha viongozi wapotevu wanaopoteza.

Na wale wanyonge watawaambia wale waliojifanya wakubwa: Bali ni vitimbi vyenu vya usiku na mchana, mlipokuwa mkituamrisha tumkufuru Mwenyezi Mungu na tumfanyie washirika.

Wafuasi na viongozi watakapokata tamaa ya kuokoka watatupiana lawama na kutuhumiana, kila kundi likijaribu kuwatupia makosa wengine; sawa na wezi wanapoafikiana kufanya uhalifu, lakini wanaposhikwa wanalaniana wao kwa wao.

Mwisho ushindi utakuwa ni wa wafuasi, kwa kuwakabili waliojifanya wakubwa kwa njama walizozifanya usiku na mchana na kuwadanga na ukafiri na ushirikina kwa njia mbalimbali.

Hata hivyo hilo halitawaondolea adhabu wala kuwapunguzia, maadamu walikuwa na akili na kulifanya hilo kwa hiyari yao: “Wa mwisho wao watawasema wa mwanzo wao: Mola wetu! Hawa ndio waliotupoteza basi uwape adhabu ya moto maradufu. Atasema: Itakuwa maradufu kwenu nyote, lakini hamjui.” Juz. 8 (7:38).

Nao wataficha majuto watakapoiona adhabu. Yaani wafuasi na waliofuatwa. Kila mwenye kuzembea na kupituka mipaka mwisho wake ni adhabu na majuto.

Na tutaweka minyororo shingoni mwa wale waliokufuru, viongozi na wafuasi wao.Kwani wanalipwa ila kwa waliyokuwa wakiyatenda? Kabisa! Mtu atalipwa kwa aliyoyafanya tu na Mola wako si mwenye kuwadhulumua waja.

وَمَا أَرْسَلْنَا فِي قَرْيَةٍ مِّن نَّذِيرٍ إِلَّا قَالَ مُتْرَفُوهَا إِنَّا بِمَا أُرْسِلْتُم بِهِ كَافِرُونَ ﴿٣٤﴾

34. Na hatukumtuma mwonyaji yeyote kwenye mji ila walisema wapenda anasa wake: Hakika sisi tunayakataa hayo mliyotumwa nayo.

وَقَالُوا نَحْنُ أَكْثَرُ أَمْوَالًا وَأَوْلَادًا وَمَا نَحْنُ بِمُعَذَّبِينَ ﴿٣٥﴾

35. Na wakasema: Sisi tuna mali nyingi zaidi na watoto, wala sisi hatutaadhibiwa.

قُلْ إِنَّ رَبِّي يَبْسُطُ الرِّزْقَ لِمَن يَشَاءُ وَيَقْدِرُ وَلَـٰكِنَّ أَكْثَرَ النَّاسِ لَا يَعْلَمُونَ ﴿٣٦﴾

36. Sema: Hakika Mola wangu humkunjulia riziki amtakaye na huikunja, lakini watu wengi hawajui.

وَمَا أَمْوَالُكُمْ وَلَا أَوْلَادُكُم بِالَّتِي تُقَرِّبُكُمْ عِندَنَا زُلْفَىٰ إِلَّا مَنْ آمَنَ وَعَمِلَ صَالِحًا فَأُولَـٰئِكَ لَهُمْ جَزَاءُ الضِّعْفِ بِمَا عَمِلُوا وَهُمْ فِي الْغُرُفَاتِ آمِنُونَ ﴿٣٧﴾

37. Na si mali yenu wala watoto wenu watakaowajongeza kwetu muwe karibu, isipokuwa aliyeamini na akatenda mema. Hao basi watapata malipo maradufu, kwa waliyoyafanya nao watakuwa salama katika maghorofa.

وَالَّذِينَ يَسْعَوْنَ فِي آيَاتِنَا مُعَاجِزِينَ أُولَـٰئِكَ فِي الْعَذَابِ مُحْضَرُونَ ﴿٣٨﴾

38. Na wale ambao wanajitahidi kuzipinga ishara zetu, wakaona watashinda, hao watahudhurishwa kwenye adhabu.

قُلْ إِنَّ رَبِّي يَبْسُطُ الرِّزْقَ لِمَن يَشَاءُ مِنْ عِبَادِهِ وَيَقْدِرُ لَهُ وَمَا أَنفَقْتُم مِّن شَيْءٍ فَهُوَ يُخْلِفُهُ وَهُوَ خَيْرُ الرَّازِقِينَ ﴿٣٩﴾

39. Sema: Hakika Mola wangu humkunjulia riziki amtakaye katika waja wake na humkunjia. Na chochote mtakachotoa Yeye atakilipa. Naye ni Mbora wa wanaoruzuku.

وَيَوْمَ يَحْشُرُهُمْ جَمِيعًا ثُمَّ يَقُولُ لِلْمَلَائِكَةِ أَهَـٰؤُلَاءِ إِيَّاكُمْ كَانُوا يَعْبُدُونَ ﴿٤٠﴾

40. Na siku atakayowakusanya wote, kisha atawaambia Malaika: Je, hawa walikuwa wakiwaabudu?

قَالُوا سُبْحَانَكَ أَنتَ وَلِيُّنَا مِن دُونِهِم بَلْ كَانُوا يَعْبُدُونَ الْجِنَّ أَكْثَرُهُم بِهِم مُّؤْمِنُونَ ﴿٤١﴾

41. Watasema: Umetakasika! Wewe ndiye walii wetu sio hao. Bali walikuwa wakiwaabudu majini; wengi wao wakiwaamini hao.

فَالْيَوْمَ لَا يَمْلِكُ بَعْضُكُمْ لِبَعْضٍ نَّفْعًا وَلَا ضَرًّا وَنَقُولُ لِلَّذِينَ ظَلَمُوا ذُوقُوا عَذَابَ النَّارِ الَّتِي كُنتُم بِهَا تُكَذِّبُونَ ﴿٤٢﴾

42. Na leo hii hawataweza baadhi yenu kuwaletea nafuu wengine wala kuwadhuru. Na tutawaambia wale ambao wamedhulumu: Onjeni adhabu ya Moto mliokuwa mkiukadhibisha.

WAPENDA ANASA

Aya 34 – 42

MAANA

Na hatukumtuma mwonyaji yeyote kwenye mji ila walisema wapenda anasa wake: Hakika sisi tunayakataa hayo mliyotumwa nayo. Na wakasema: Sisi tuna mali nyingi zaidi na watoto, wala sisi hatutaadhibiwa.

Hii ndio fikra ya wapenda anasa na hii ndio lugha yao. Mali ndio ya kwanza na ya mwisho; ndiyo bwana na wao ni watumwa.

Wanabeba bendera ya shari na uchokozi kwa watu kwa ajili ya mali, wanatawala masoko na vyakula, wanaanzisha vita moto na vita baridi, wanatafuta kila namna ya kutawala maisha na kila kitu wanakifungamanisha na chumo lao na faidia yao.

Kwao elimu sio chochote ila ikiwa inazidisha utajiri wao, dini ni ugaidi ila ikiwa inalinda masilahi yao, na amani ni wao wapore na wanayang’anye bila ya ya kuulizwa au kukemewa. Tazama Juz. 15: (17:16,90).

Sema: Hakika Mola wangu humkunjulia riziki amtakaye na huikunja, lakini watu wengi hawajui.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 13 (13:26) kifungu cha ‘riziki na mtu.

Na si mali yenu wala watoto wenu watakaowajongeza kwetu muwe karibu, isipokuwa aliyeamini na akatenda mema. Hao basi watapata malipo maradufu, kwa waliyoyafanya nao watakuwa salama katika maghorofa.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) hapimi kheri na fadhila kwa mali na watoto, wala kwa vyeo na nasaba; bali ni kwa imani na matendo mema. Ni kwa mawili haya ndio mja anakuwa ni mwenye kuridhiwa mbele ya Mwenyezi Mungu kwa thawabu zake na fadhila zake.

Imam Ali(a.s) anasema:“Heri sio kuwa nyingi mali yako na watoto, lakini heri ni kuwa nyingi elimu yako na kuwa na ustahamilivu mkubwa, na ushindane na watu kwa kumwabudu Mola wako. Ukifanya vizuri msifu Mwenyezi Mungu na ukifanya uovu muombe msamaha Mwenyezi Mungu; wala hakuna heri isipokuwa kwa watu wawili: Mtu aliyefanya dhambi akaiunganisha na toba, na mtu anayeharakisha kheri.”

Na wale ambao wanajitahidi kuzipinga ishara zetu, wakaona watashinda, hao watahudhurishwa kwenye adhabu.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 17 (22:51).

Sema: Hakika Mola wangu humkunjulia riziki amtakaye katika waja wake na humkunjia.

Unaweza kuuliza : Kwa nini Mwenyezi Mungu (s.w.t) amekariri Aya hii, pamoja na kujua kuwa kuna mtengano wa Aya mbili tu?

Wafasiri wamejibu kwamba Aya ya kwanza inahusika na makafiri na ya pili ni ya waumini. Razi anasema: “Dalili ya hilo ni kuwa Mwenyezi Mungu Mtukufu katika Aya ya pili amesema katika ‘waja wake’ na ya kwanza amesema ‘waja’ tu, na mja anayetegemezwa kwake Mwenyezi Mungu anakusudiwa muumini.”

Sio mbali kuwa makusudio ya kukaririka ni mawaidha na kuhimiza kutoa ambako Mwenyezi Mungu amekuashiria kwa kusema:

Na chochote mtakachotoa Yeye atakilipa. Naye ni Mbora wa wanaoruzuku.

Kuna Hadith ya Mtume mtukufu(s.a.w. w ) , amesema:“Kila usiku kuna mnadi anayenadi kwa kusema: “Ewe Mola wangu! Mlipe kila mtoaji. Na mnadi mwingine ananadi: Ewe Mola angu! Mlipe kila mzuiaji kuangamia.” kwenye Nahjul-Balagha imeelezwa:“Iteremsheni riziki kwa sadaka.”

Na siku atakayowakusanya wote, kisha atawaambia Malaika: Je, hawa walikuwa wakiwaabudu?

Makusudio ya kuelekeza swali hili kwa Malaika ni kuwatahayariza washirikina. Aya inafahamisha kuwa baadhi ya waarabu walikuwa wakiwaabudu malaika. Hayo yanaashiriwa na kauli yake Mwenyezi Mungu: “Je, Mola wenu amewachagulia watoto wa kiume na yeye akajichukulia watoto wa kike katika Malaika?” Juz. 15 (17:40).

Mwenye kumnasibishia Mwenyezi Mungu mwana basi amemfanya Mungu kuwa na mfano na mshirika katika uungu wake.

Watasema: Umetakasika! Wewe ndiye walii wetu sio hao.

Wewe ndiye bwana wetu na wao ni maadui zetu nasi tunajitenga nao.

Bali walikuwa wakiwaabudu majini; wengi wao wakiwaamini hao.

Kundi la wafasiri wamesema kuwa makusudio ya jini hapa ni mashetani na kwamba wao wanawapambia washirikina wawaabudu malaika na wengineo badala ya Mwenyezi Mungu.

Wengine wakasema kuwa ibada ya majini ilikuwa maarufu kwa waarabu; kwa hiyo maana ya Aya yatabaki kwenye dhahiri yake, wala hakuna haja ya kufanya taawili.

Iwe ni majini ndio waliokuwa wakiabudiwa au wengineo kwa kudanganywa na shetani, bado makusudio ya kwanza ya Aya ni kukanusha kumshirikisha Mwenyezi Mungu na kwamba hakuna uombezi kwake ila kwa idhini yake. Vile vile hakuna kimbilio isipokuwa kwake yeye tu.

Ndio maana Mwenyezi Mungu Mtukufu akafuatishia na kauli yake:

Na leo hii hawataweza baadhi yenu kuwaletea nafuu wengine wala kuwadhuru.

Si malaika, watu wala majini wanaoweza wao wenyewe kujikinga, sikwambii tena kuwasaidia wengine. Yeye peke yake ndiye mwenye ufalme na sifa njema, naye ni muweza wa kila kitu.

Na tutawaambia wale ambao wamedhulumu: Onjeni adhabu ya Moto mliokuwa mkiukadhibisha.

Walisema kuwa hakuna Pepo wala Moto, wala hatutauamini mpaka tutakapouona waziwazi. Basi ndio Mwenyezi Mungu akawachoma kuitikia matakwa yao.

Aya hii imenikumbusha wanaosema kuwa hakuna elimu wala maarifa ila kwa njia ya kushuhudia au majaribio; hata katika visivyoonekana na kuhisiwa.

8

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MOJA

وَإِذَا تُتْلَىٰ عَلَيْهِمْ آيَاتُنَا بَيِّنَاتٍ قَالُوا مَا هَـٰذَا إِلَّا رَجُلٌ يُرِيدُ أَن يَصُدَّكُمْ عَمَّا كَانَ يَعْبُدُ آبَاؤُكُمْ وَقَالُوا مَا هَـٰذَا إِلَّا إِفْكٌ مُّفْتَرًى وَقَالَ الَّذِينَ كَفَرُوا لِلْحَقِّ لَمَّا جَاءَهُمْ إِنْ هَـٰذَا إِلَّا سِحْرٌ مُّبِينٌ ﴿٤٣﴾

43. Na wanaposomewa Aya zetu zilizo wazi wanasema: Huyu si chochote ila ni mtu anayetaka kuwazuia na waliyokuwa wakiyaabudu baba zenu. Na wakasema: Haya si chochote ila ni uongo uliozuliwa.” Na wale waliokufuru waliiambia haki pale ilipowajia: “Haya si chochote ila ni uchawi ulio dhahiri.

وَمَا آتَيْنَاهُم مِّن كُتُبٍ يَدْرُسُونَهَا وَمَا أَرْسَلْنَا إِلَيْهِمْ قَبْلَكَ مِن نَّذِيرٍ ﴿٤٤﴾

44. Wala hatukuwapa vitabu wavisome, wala hatukuwatumia muonyaji kabla yako.

وَكَذَّبَ الَّذِينَ مِن قَبْلِهِمْ وَمَا بَلَغُوا مِعْشَارَ مَا آتَيْنَاهُمْ فَكَذَّبُوا رُسُلِي فَكَيْفَ كَانَ نَكِيرِ ﴿٤٥﴾

45. Na walikadhibisha wale waliokuwa kabla yao. Na hawakufikilia hata sehemu ya kumi ya tulivyowapa hao. Wakawakadhibisha mitume wangu. basi je, kulikuwaje kukanya kwangu?

قُلْ إِنَّمَا أَعِظُكُم بِوَاحِدَةٍ أَن تَقُومُوا لِلَّـهِ مَثْنَىٰ وَفُرَادَىٰ ثُمَّ تَتَفَكَّرُوا مَا بِصَاحِبِكُم مِّن جِنَّةٍ إِنْ هُوَ إِلَّا نَذِيرٌ لَّكُم بَيْنَ يَدَيْ عَذَابٍ شَدِيدٍ ﴿٤٦﴾

46. Sema: Hakika ninawapa mawaidha kwa jambo moja tu, kwamba msimame kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, wawili wawili na mmoja mmoja; kisha mfikiri. Mwenzenu hana wazimu. Hakuwa yeye ila ni muonyaji kwenu kabla ya kuwafikia adhabu kali.

قُلْ مَا سَأَلْتُكُم مِّنْ أَجْرٍ فَهُوَ لَكُمْ إِنْ أَجْرِيَ إِلَّا عَلَى اللَّـهِ وَهُوَ عَلَىٰ كُلِّ شَيْءٍ شَهِيدٌ ﴿٤٧﴾

47. Sema: Ujira niliowaomba ni wenu nyinyi. Sina ujira ila kwa Mwenyezi Mungu. Naye ni shahidi juu ya kila kitu.

قُلْ إِنَّ رَبِّي يَقْذِفُ بِالْحَقِّ عَلَّامُ الْغُيُوبِ ﴿٤٨﴾

48. Sema: Hakika Mola wangu hutoa haki, Mjuzi mno wa ghaibu.

قُلْ جَاءَ الْحَقُّ وَمَا يُبْدِئُ الْبَاطِلُ وَمَا يُعِيدُ ﴿٤٩﴾

49. Sema: Haki imefika na batili haijitokezi wala hairudi.

قُلْ إِن ضَلَلْتُ فَإِنَّمَا أَضِلُّ عَلَىٰ نَفْسِي وَإِنِ اهْتَدَيْتُ فَبِمَا يُوحِي إِلَيَّ رَبِّي إِنَّهُ سَمِيعٌ قَرِيبٌ ﴿٥٠﴾

50. Sema: Ikiwa nimepotea basi nimepotea kwa kuidhuru nafsi yangu tu. Na ikiwa nimeongoka basi ni kwa sababu ya kuniletea wahyi Mola wangu. Hakika Yeye ni Mwenye kusikia aliye karibu.

NINAWAPA MAWAIDHA KWA JAMBO MOJA TU

Aya 43 – 50

MAANA

Na wanaposomewa Aya zetu zilizo wazi wanasema: Huyu si chochote ila ni mtu anayetaka kuwazuia na waliyokuwa wakiyaabudu baba zenu. Na wakasema: Haya si chochote ila ni uwongo uliozuliwa. Na wale waliokufuru waliiambia haki pale ilipowajia: Haya si chochote ila ni uchawi ulio dhahiri.

Waliosema ni washirikina wa kiarabu, mtu wanayemkusudia ni Muhammad(s.a.w. w ) . Wamempa wasifa wa uzushi na uchawi kwa sababu aliwataka waachane na mizimu na maagizo ya kijahilia. Pia aliwaambia wajizuie na mambo ya haramu, uovu, kumwaga damu na kuwakandamiza wanyonge. Vile vile aliwataka wafanye mambo kielimu na kiuadilifu.

Hilo ndilo kosa la Mtume mtukufu kwao. Kama unavyoona, ni kosa la mjuzi mwenye ikhlasi mbele ya mjinga mhaini, na la tabibu mwenye kutoa nasaha mbele ya mgonjwa anayejiona ni mzima. Amesema kweli yule aliyesema: “Mjinga anajifanyia mwenyewe ambayo hata adui hawezi kumfanyia adui yake.”

Wala hatukuwapa vitabu wavisome, wala hatukuwatumia muonyaji kabla yako.

Walishirikisha ambapo kila kitu kinafahamisha kuwa Yeye ni mmoja, wakawaiga mababa na mababu bila ya kuwa na hoja ya wahyi ulioteremshwa au Nabii aliyetumwa wala athaari yoyote ya ilimu. Tazama Juz. 17 (22: 1-7) kifungu cha: ‘Mjadala wakijinga na upotevu‘.

Na walikadhibisha wale waliokuwa kabla yao. Na hawakufikilia hata sehemu ya kumi ya tulivyowapa hao. Wakawakadhibisha mitume wangu. basi je, kulikuwaje kukanya kwangu?

Kabla yenu walishirikisha watu wa uma nyingi, waliwakadhibisha mitume; kama manvyokadhibisha nyinyi, nao walikuwa na maendeleo na nguvu zaidi kuliko nyinyi, lakini pamoja na hivyo Mwenyezi Mungu aliwaadhibu kwa dhulma yao na ujeuri wao. Je, hampati funzo na kuhofia kuwafika yaliyowafika wao?

Umetangulia mfano wake katika Juz. 10 (9:70).

Sema: Hakika ninawapa mawaidha kwa jambo moja tu, kwamba msimame kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, wawili wawli na mmoja mmoja; kisha mfikiri. Mwenzenu hana wazimu. Hakuwa yeye ila ni muonyaji kwenu kabla ya kuwafikia adhabu kali.

Kusimama kwa ajili ya Mwenyezi Mungu ni kushikamana na haki na kuwa mbali na kuiga na kufuata matamanio. Wawili wawili ni mmoja kumrudia mwingine na kuuchunguza mwito na ujumbe. Mmoja mmoja ni kila mmoja kurudia akili yake na dhamiri na kufikiria yale aliyokuja nayo.

Maana ni kuwa ewe Muhammad! Waambie wale wanaokukadhibisha kwamba mimi ninawataka jambo moja tu, uadilifu wa kuchunga haki, mfikirie mkiwa pamoja na mkiwa mbalimbali kuhusu mwito wangu; kisha muangalie, je kweli mimi ni mzushi, mchawi au mwenda wazimu; kama mnavyodai? Au ni mbashiri, muonyaji na mshauri nasaha mwenye busara? Nabii mtukufu aliwapa Watu wa Kitabu mwito kama huu, pale alipowaambia:

قُلْ يَا أَهْلَ الْكِتَابِ تَعَالَوْا إِلَىٰ كَلِمَةٍ سَوَاءٍ بَيْنَنَا وَبَيْنَكُمْ أَلَّا نَعْبُدَ إِلَّا اللَّـهَ وَلَا نُشْرِكَ بِهِ شَيْئًا ﴿٦٤﴾

“Sema: Enyi watu wa Kitabu! Njooni kwenye neno la usawa baina yetu na baina yenu. Kwamba tusimwabudu yeyote ila Mwenyezi Mungu, wala tusimshirikishe na chochote.” Juz. 3 (3:64).

Hakuna jambo linalosadikisha zaidi dalili ya ukweli wa Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w. w ) , katika aliyokuja nayo, kuliko kuwapa mwito wa haki na uadilifu mahasimu.

Imepokewa Hadith kutoka kwa Ibn Abbas, kwamba Mtume(s.a.w. w ) siku moja alipanda Swafa na akasema: “Enyi wenzangu! Neno analolitumia anayetaka kuokoka ikiwa kuna jambo kubwa, basi makuraishi wakakusanyika. Akawaambia: “Mnaonaje kama nikiwaambia adui atawajia asubuhi au jioni, mtanisadiki?” Wakasema: “Ndio!” Akasema: “Hakika ninawaonya na adhabu kali. Abu Lahab akamjibu kwa neno la kukana... lakini hazikupita siku ila walisalimu amri wakiwa wanyonge.

Sema: Ujira niliowaomba ni wenu nyinyi. Sina ujira ila kwa Mwenyezi Mungu. Naye ni shahidi juu ya kila kitu.

Makusudio ya ‘ni wenu nyinyi’ ni kukana swali la ujira. Ni mfano wa kauli yake Mwenyezi Mungu:

فَمَا سَأَلْتُكُم مِّنْ أَجْرٍ إِنْ أَجْرِيَ إِلَّا عَلَى اللَّـهِ ﴿٧٢﴾

“...basi mimi siwaombi ujira. Ujira wangu hauko ila kwa Mwenyezi Mungu.” Juz. 11 (10:72).

Sema: Hakika Mola wangu hutoa haki, Mjuzi mno wa ghaibu.

Yaani anatoa wahyi kwa haki kuupeleka kwa mitume yake naye anajua vizuri nani wa kumpelekea ujumbe wake mkuu.

Sema: Haki imefika na batili hajitokezi wala hairudi.

Makusudio ya haki hapa ni risala ya Muhammad(s.a.w. w ) na batili ni shir- ki. Kujitokeza na kurudi ni kinaya cha kwisha kabisa batili na kutodhihiri athari yake katika Bara Arabu kabisa baada ya risala ya Muhammad(s.a.w. w ) .

Sema: Ikiwa nimepotea basi nimepotea kwa kuidhuru nafsi yangu tu, wala nyinyi madhara yangu hayawahusu.

Na ikiwa nimeongoka basi ni kwa sababu ya kuniletea wahyi Mola wangu.

Ni kwake Yeye peke yake fadhila za kuongoka kwangu; wala sijimilikii wala kummilikia mwingine isipokuwa yale aliyonimilikisha Mwenyezi Mungu.

Hakika Yeye ni Mwenye kusikia aliye karibu.

Mkisema anasikia, mkidhamiria au mkitenda atajua, kwa sababu yeye yuko karibu zaidi na nyinyi kuliko mshipa wa shingo.

وَلَوْ تَرَىٰ إِذْ فَزِعُوا فَلَا فَوْتَ وَأُخِذُوا مِن مَّكَانٍ قَرِيبٍ ﴿٥١﴾

51. Na lau ungeliwaona watakapofazaika, basi hapana pa kukimbilia, na watakamatwa mahala pa karibu.

وَقَالُوا آمَنَّا بِهِ وَأَنَّىٰ لَهُمُ التَّنَاوُشُ مِن مَّكَانٍ بَعِيدٍ ﴿٥٢﴾

52. Na watasema: Tumemwamini! Lakini watapata wapi kutoka huko mahali mbali?

وَقَدْ كَفَرُوا بِهِ مِن قَبْلُ وَيَقْذِفُونَ بِالْغَيْبِ مِن مَّكَانٍ بَعِيدٍ ﴿٥٣﴾

53. Na walikwishamkataa hapo zamani, wakiyatupilia mbali ya ghaibu kutoka mahali mbali.

وَحِيلَ بَيْنَهُمْ وَبَيْنَ مَا يَشْتَهُونَ كَمَا فُعِلَ بِأَشْيَاعِهِم مِّن قَبْلُ إِنَّهُمْ كَانُوا فِي شَكٍّ مُّرِيبٍ ﴿٥٤﴾

54. Na watawekewa kizuizi baina yao na hayo wanayoyatamani, kama walivyofanyiwa wenzao zamani. Hakika wao walikuwa katika shaka ya kutia wasiwasi.

WATAIPATA WAPI?

Aya 51 – 54

MAANA

Na lau ungeliwaona watakapofazaika, basi hapana pa kukimbilia, na watakamatwa mahala pa karibu.

Maneno yanaelekezwa kwa Muhammad(s.a.w. w ) , kukamatwa mahala pa karibu ni kinaya cha kuwa kwenye uweza wa Mwenyezi Mungu. Maana ni kuwa, ewe Muhammad(s.a.w. w ) lau utaona kesho hofu na adhabu, isiyokuwa na kimbilio, itakayowapata wale wanaokadhibisha utume wako, basi utastaajabu.

Hii ni kemeo kwa washirikina na tulizo kwa Bwana wa Mitume.

Na watasema tumemwamini! Lakini watapata wapi kutoka huko mahali mbali?

Wanayesema ‘tumemwamini’ ni Muhammad(s.a.w. w ) , kwa sababu amekwishatajwa kwenye Aya 46 ‘Mwenzenu hana wazimu.’

Maana ni kuwa, wale waliomkadhibisha Muhammad, watakapoiona adhabu watasema tumemwamini, lakini wataipata wapi imani hii au itawafaa nini huko mbali. Kwa sababu siku ya Kiyama ni siku ya hisabu na malipo sio siku ya imani na matendo.

Imam Ali(a.s) anasema:“Leo ni matendo si hisabu na kesho ni hisabu sio matendo... Enyi waja wa Mwenyezi Mungu! Jipimeni kabla ya kupimwa na mjihisabu kabla ya kuhisabiwa.”

Na walikwishamkataa hapo zamani. Muda wa kufaa imani umekwisha.

Wakiyatupilia mbali ya ghaibu kutoka mahali mbali.

Kutupilia mbali ni kusema bila ya ilimu, kutoka mahali mbali ni kinaya cha umbali wa kuliza na kutoamini kwao haki. Maana ni kuwa, wao walikuwa wakisema Muhammad ni mzushi, mchawi na mwendawazimu; wala hakuna Pepo au Moto. Waliyasema hayo kwa ujinga na bila ya dalili.

Na watawekewa kizuizi baina yao na hayo wanayoyatamani.

Wanatamani kuokoka na adhbau ya Jahannam, ndio wakakimbilia imani na toba, lakini baada ya kupita muda, basi watazidi majuto na machungu.

Kama walivyofanyiwa wenzao zamani.

Walikuwa na wanaofanana nao katika uma zilizopita; walimpinga Mola wao katika maisha ya dunia na kufazaika akhera. Wataambiwa:

قَالَ اخْسَئُوا فِيهَا وَلَا تُكَلِّمُونِ ﴿١٠٨﴾

“Tokomeeni humo, wala msinisemeshe.” Juz. 18: (23:108).

Hakika wao walikuwa katika shaka ya kutia wasiwasi ya ufufuo.

MWISHI WA SURA YA THELATHINI NA NNE: SURAT SABA

9

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MOJA

Sura Ya Thelathini na Tano: Surat Fatir. Imeshuka Makka. Ina Aya 45.

بِسْمِ اللَّهِ الرَّحْمَٰنِ الرَّحِيمِ

Kwa jina la Mwenyezi Mungu, Mwingi wa rehema, Mwenye kurehemu.

الْحَمْدُ لِلَّـهِ فَاطِرِ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ جَاعِلِ الْمَلَائِكَةِ رُسُلًا أُولِي أَجْنِحَةٍ مَّثْنَىٰ وَثُلَاثَ وَرُبَاعَ يَزِيدُ فِي الْخَلْقِ مَا يَشَاءُ إِنَّ اللَّـهَ عَلَىٰ كُلِّ شَيْءٍ قَدِيرٌ ﴿١﴾

1. Sifa njema ni za Mwenyezi Mungu Muumba wa mbingu na ardhi aliyewafanya Malaika kuwa wajumbe wenye mbawa mbili mbili, tatu tatu na nne nne. Huzidisha katika kuumba apendavyo. Hakika Mwenyezi Mungu ni mwenye uweza juu ya kila kitu.

مَّا يَفْتَحِ اللَّـهُ لِلنَّاسِ مِن رَّحْمَةٍ فَلَا مُمْسِكَ لَهَا وَمَا يُمْسِكْ فَلَا مُرْسِلَ لَهُ مِن بَعْدِهِ وَهُوَ الْعَزِيزُ الْحَكِيمُ ﴿٢﴾

2. Rehema ambayo Mwenyezi Mungu anawafungulia watu hakuna wa kuizuia na anayoizuia hakuna wa kuiachia isipokuwa Yeye, naye ni Mwenye nguvu, Mwenye hekima.

يَا أَيُّهَا النَّاسُ اذْكُرُوا نِعْمَتَ اللَّـهِ عَلَيْكُمْ هَلْ مِنْ خَالِقٍ غَيْرُ اللَّـهِ يَرْزُقُكُم مِّنَ السَّمَاءِ وَالْأَرْضِ لَا إِلَـٰهَ إِلَّا هُوَ فَأَنَّىٰ تُؤْفَكُونَ ﴿٣﴾

3. Enyi watu! Kumbukeni neema za Mwenyezi Mungu juu yenu. Je, yuko muumba mwingine asiyekuwa Mwenyezi Mungu anayewapa riziki kutoka mbinguni na kwenye ardhi? Hapana Mola ila Yeye basi mnageuzwa wapi?.

SIFA NJEMA NI ZA MWENYEZI MUNGU

Aya 1 – 3

MAANA

Sifa njema ni za Mwenyezi Mungu Muumba wa mbingu na ardhi aliyewafanya Malaika kuwa wajumbe wenye mbawa mbili mbili, tatu tatu na nne nne. Huzidisha katika kuumba apendavyo. Hakika Mwenyezi Mungu ni mwenye uweza juu ya kila kitu.

Mwenyezi Mungu amejisifu Yeye mwenyewe ili atufundishe jinsi ya kumsifu na kumshukuru. Aya inafahamisha kuwa katika Malaika kuna walio na mbawa mbili, wenye tatu na wenye nne na kwamba Yeye Mwenyezi Mungu Mtukufu huzidisha mbawa vile atakavyo. Haya na yanayofanana nayo yanaafikiana na uwezo wa Mwenyezi Mungu na akili haiyakatai. Yasiyokuwa hayo tunamwachia Mwenyezi Mungu (s.w.t), kwa vile sisi hatutaulizwa wala hayana uhusiano wowote na maisha yetu, wala hayana dalili na Aya au Hadith mutawatir.

Ninahofia wale wanaolazimisha kuzifanyia taawili nukuu za dini ziende sambamba na elimu ya kisasa waseme kuwa mbili mbili ni ishara ya ndege yenye injini mbili, tatu tatu ni yenye tatu, nne nne ni yenye nne na kuzidisha katika kuumba ni kuwa ndege zitakazokuja baadaye zenye injini nyingi.

Rehema ambayo Mwenyezi Mungu anawafungulia watu hakuna wa kuizuia na anayoizuia hakuna wa kuiachia isipokuwa Yeye, naye ni Mwenye nguvu, Mwenye hekima.

Makusudio ya rehema hapa sio mali tu; kama walivyosema baadhi ya wafasiri. Wala sio mali, afya na cheo; kama walivyosema wengine. Kwani mali inapelekea uasi na ukandamizaji. Tumewaona wengi wenye mali wamewageuza wengine wanyonge kuwa ni mashirika wanayoyamiliki na kuwageuza kuwa ni watumwa wao wanaowatumikia au wawe wakimbizi.

Afya nayo inampelekea mtu kwenye hatari. Ama cheo, ndio kabisa, aghlabu kinakuwa ni chombo cha dhulma na uadui. Elimu nayo mara nyingine inakuwa ni afadhali ujinga; kama vile elimu iliyotengeneza bomu la nyukilia na silaha za maangamizi.

Hapana! Makusudio ya rehema yake Mwenyezi Mungu Mtukufu, katika Aya hii, sio mali peke yake, wala afya pekee yake wala sio cheo na elimu tu. Isipokuwa makusudio ni huruma ya Mwenyezi Mungu, mwongozo wake wa heri na kinga yake ya shari.

Imam Ali(a.s) anasema:“Shida inapofika kikomo huja faraja na inapokaza sana minyororo ya dhiki hupatikana raha.”

Mara nyingi tumeshuhudia matatizo madogo yanazidi kuwa makubwa kila mwenyewe anavyojitahidi kuyatatua, na tunaona yale makubwa yanatatu- ka kwa wepesi au kwa haraka. Hakuna siri ya hilo ila matakwa ya Mwenyezi Mungu na rehema yake. Amesema kweli aliyesema: “Mtu anaweza kulala kwenye miba, pamoja na rehema ya Mwenyezi Mungu, akaamka kwenye tandiko. Na anaweza kulala kwenye hariri bila ya rehe- ma ya Mwenyezi Mungu akaamka kwenye miba.”[3] .

Enyi watu! Kumbukeni neema za Mwenyezi Mungu juu yenu. Je, yuko muumba mwingine asiyekuwa Mwenyezi Mungu anayewapa riziki kutoka mbinguni na kwenye ardhi? Hapana Mola ila Yeye basi mnageuzwa wapi?

Ukumbusho huu wa neema ya Mwenyezi Mungu na kwamba Yeye peke yake ndiye muumba na mwenye kuruzuku ni kuisisitiza Aya iliyotangulia: ‘Rehema ambayo Mwenyezi Mungu anawafungulia watu...’

Katika Nahjul-Balagha imeelezwa:“Mara ngapi Mwenyezi Mungu amewahusisha na neema yake na akwaunganisha na rehema yake. Mmekuwa uchi akawasitiri, mkafanya ya kuwaadhibu akawapa muda. Basi zikamilisheni neema za Mwenyezi Mungu kwa kuwa na subira ya kumtii na kujiweka mbali na maasi, kwani hakika kesho kuanzia leo ni karibu.”

وَإِن يُكَذِّبُوكَ فَقَدْ كُذِّبَتْ رُسُلٌ مِّن قَبْلِكَ وَإِلَى اللَّـهِ تُرْجَعُ الْأُمُورُ ﴿٤﴾

4. Na kama wakikukadhibisha, basi wamekwisha kadhibishwa Mitume kabla yako na mambo yote yatarudishwa kwa Mwenyezi Mungu.

يَا أَيُّهَا النَّاسُ إِنَّ وَعْدَ اللَّـهِ حَقٌّ فَلَا تَغُرَّنَّكُمُ الْحَيَاةُ الدُّنْيَا وَلَا يَغُرَّنَّكُم بِاللَّـهِ الْغَرُورُ ﴿٥﴾

5. Hakika ahadi ya Mwenyezi Mungu ni ya haki. Basi yasiwadanganye maisha ya dunia, wala mdanganyifu asiwadanganye juu ya Mwenyezi Mungu.

إِنَّ الشَّيْطَانَ لَكُمْ عَدُوٌّ فَاتَّخِذُوهُ عَدُوًّا إِنَّمَا يَدْعُو حِزْبَهُ لِيَكُونُوا مِنْ أَصْحَابِ السَّعِيرِ ﴿٦﴾

6. Hakika Shetani ni adui yenu, basi mfanyeni kuwa ni adui. Kwani yeye analiita kundi lake liwe katika watu wa motoni.

الَّذِينَ كَفَرُوا لَهُمْ عَذَابٌ شَدِيدٌ وَالَّذِينَ آمَنُوا وَعَمِلُوا الصَّالِحَاتِ لَهُم مَّغْفِرَةٌ وَأَجْرٌ كَبِيرٌ ﴿٧﴾

7. Wale ambao wamekufuru watakuwa katika adhabu kali na wale ambao wameamini watapata maghufira na malipo makubwa.

أَفَمَن زُيِّنَ لَهُ سُوءُ عَمَلِهِ فَرَآهُ حَسَنًا فَإِنَّ اللَّـهَ يُضِلُّ مَن يَشَاءُ وَيَهْدِي مَن يَشَاءُ فَلَا تَذْهَبْ نَفْسُكَ عَلَيْهِمْ حَسَرَاتٍ إِنَّ اللَّـهَ عَلِيمٌ بِمَا يَصْنَعُونَ ﴿٨﴾

8. Je, yule aliyepambiwa ubaya wa tendo lake akaliona ni jema - basi hakika Mwenyezi Mungu humpoteza amtakaye na humwongoa amtakaye. Basi roho yako isitoke kwa kuwasikitikia. Hakika Mwenyezi Mungu anayajua wanayoyafanya.

WALIKADHIBISHWA MITUME KABLA YAKO

Aya 4 – 8

MAANA

Na kama wakikukadhibisha, basi wamekwisha kadhibishwa Mitume kabla yako na mambo yote yatarudishwa kwa Mwenyezi Mungu, amlipe thawabu muumini mwenye kusubiri katika jihadi yake na amuadhibu mwenye kuikadhibisha haki kwa sababu ya kukadhibisha kwake.

Lengo la Aya hii ni kumpoza Mtume(s.a.w. w ) na kuwakaripia mahasimu na maadui wake. Umetangulia mfano wake katika Juz. 4 ( 3:183) na Juz. 17 (22:42).

Hakika ahadi ya Mwenyezi Mungu ni ya haki. Basi yasiwadanganye maisha ya dunia, wala mdanganyifu asiwadanganye juu ya Mwenyezi Mungu.

Makusudio ya ahadi hapa ni hisabu na malipo baada ya mauti. Udanganyifu wa dunia ni mali, jaha, wanawake, watoto na udanganyifu wa shetani. Umetangulia mfano wake katika Juz. 21 (31:33).

Hakika Shetani ni adui yenu, basi mfanyeni kuwa ni adui. Kwani yeye analiita kundi lake liwe katika watu wa motoni.

Shetani ametangaza waziwazi uadui wake na binadamu kwa kusema: “Kwa ulivyonipoteza, basi nitahakikisha ninawazaini hapa ardhini na nitawapoteza wote.” Juz. 14 (15:39).

Kundi lake ni wale wafuasi wake wanaosikiliza wasiwasi wake na udanganyifu wake. Mwenyezi Mungu (s.w.t) ametuhadharisha kumtii, kwa sababu mwito wake ni wa ufisadi na wa maangamizi, na Mwenyezi Mungu anatoa mwito wa kheri na rehema.

Wale ambao wamekufuru watakuwa katika adhabu kali na wale ambao wameamini watapata maghufira na malipo makubwa.

Kila mtu atakuwa na mwisho, mtamu au mchungu. Mwisho wa mwenye kukufuru na akafanya ufisadi ni Jahannam, makazi maovu; na mwisho wa mwenye kuamini na akatenda mema ni Pepo ambayo ni raha ya daima.

Je, yule aliyepambiwa ubaya wa tendo lake akaliona ni jema.

Kinahaw, hapa kuna maneno ya kukadiriwa kuwa: ‘ni kama ambaye hakupambiwa’ Hakuna mtu yoyote anayeishi bila ya falsafa na kuchukulia mfano wa juu; hata wale wanaokataa falsafa na mfano, huko kukataa kwao ndio falasafa yao na mfano wa juu. Ndio maana ikasemwa: Mwenye kukataa falsafa ndio amekuwa na falsafa.

Tofauti ni kuwa kuna yale anayeijengea falsafa yake kwenye majaribio na uchambuzi, mwengine anaijengea kwenye akili au dini na kuna yale anayeijengea kwenye dhati yake, mapendeleo yake na kupinga mengine yote.

Hafanyi utafiti wala kufikiri au kufanya uchambuzi, kwa sababu haamini akili wala dini; hakuna kitu isipokuwa kilicho kwenye rai yake na mapendeleo yake.

Mtu wa aina hii anaangalia nafsi zake kuwa ndio kipimo pekee cha haki heri na usawa, na kwamba yeye siku zote yuko sawa, hana upungufu wala hakosei.

Huyu tunaweza kumwita shahidi wa upumbavu na mwenye ghururi ya kuua. Mwenyezi Mungu (s.w.t) amemwashiria mtu huyu, katika Aya kadhaa; miongoni mwazo ni: “Sema je, tuwaambie wale wenye hasara mno ya vitendo?” Juz. 16 (18:103) Nyingine ni:

وَإِذَا قِيلَ لَهُمْ لَا تُفْسِدُوا فِي الْأَرْضِ قَالُوا إِنَّمَا نَحْنُ مُصْلِحُونَ ﴿١١﴾ أَلَا إِنَّهُمْ هُمُ الْمُفْسِدُونَ وَلَـٰكِن لَّا يَشْعُرُونَ ﴿١٢﴾

“Na wanapoambiwa msifanye ufisadi katika ardhi husema, Hakika sisi ni watengezaji tu. Ehe! Hakika wao ndio wafisadi, lakini hawatambui.” Juz. 1 (2:11-12).

Basi Hakika Mwenyezi Mungu humpoteza amtakaye na humwongoa amtakaye.

Hii ni sababu ya kauli yake Mwenyezi Mungu iliyotangulia ‘Je, yule aliyepambiwa ubaya wa tendo lake akaliona ni jema.’ Yaani kwamba Mwenyezi Mungu amemuweka kwenye upotevu na mwisho mbaya kwa sababu amefuata njia inayopelekea hilo; sawa na alivyomuweka kwenye kifo mwenye kunywa sumu na kufa maji aliyejitia baharini akiwa hajui kuogelea.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 13 (13:27) na Juz. 14 (16:93).

Basi roho yako isitoke kwa kuwasikitikia. Hakika Mwenyezi Mungu anayajua wanayoyafanya.

Usisikitike wala usihuzunike, ewe Muhammad, kwa wale ambao hawakuitikia mwito wako madamu wamefuata wenyewe njia ya uovu na ya maangamizi. Mwenyezi Mungu ameyadhibiti mambo yao, madogo na makubwa. Umetangulia mfano wake katika Juz. 15 (18:2).

وَاللَّـهُ الَّذِي أَرْسَلَ الرِّيَاحَ فَتُثِيرُ سَحَابًا فَسُقْنَاهُ إِلَىٰ بَلَدٍ مَّيِّتٍ فَأَحْيَيْنَا بِهِ الْأَرْضَ بَعْدَ مَوْتِهَا كَذَٰلِكَ النُّشُورُ ﴿٩﴾

9. Na Mwenyezi Mungu ndiye anayezituma pepo ziyatimue mawingu, nasi tukayafikisha kwenye nchi iliyokufa, tukaifufua ardhi baada ya kufa kwake. Ndio kama hivyo kufufuliwa.

مَن كَانَ يُرِيدُ الْعِزَّةَ فَلِلَّـهِ الْعِزَّةُ جَمِيعًا إِلَيْهِ يَصْعَدُ الْكَلِمُ الطَّيِّبُ وَالْعَمَلُ الصَّالِحُ يَرْفَعُهُ وَالَّذِينَ يَمْكُرُونَ السَّيِّئَاتِ لَهُمْ عَذَابٌ شَدِيدٌ وَمَكْرُ أُولَـٰئِكَ هُوَ يَبُورُ ﴿١٠﴾

10. Mwenye kutaka enzi basi enzi yote ni ya Mwenyezi Mungu. Kwake hupanda neno zuri na amali njema huuinua. Na wanaopanga njama za maovu watapata adhabu kali, na njama za hao zitaangamia.

وَاللَّـهُ خَلَقَكُم مِّن تُرَابٍ ثُمَّ مِن نُّطْفَةٍ ثُمَّ جَعَلَكُمْ أَزْوَاجًا وَمَا تَحْمِلُ مِنْ أُنثَىٰ وَلَا تَضَعُ إِلَّا بِعِلْمِهِ وَمَا يُعَمَّرُ مِن مُّعَمَّرٍ وَلَا يُنقَصُ مِنْ عُمُرِهِ إِلَّا فِي كِتَابٍ إِنَّ ذَٰلِكَ عَلَى اللَّـهِ يَسِيرٌ ﴿١١﴾

11. Na Mwenyezi Mungu amewaumba kutokana na udongo. Kisha tone, kisha akawafanya aina kwa aina. Na mwanamke yeyote hachukui mimba wala hazai ila kwa elimu yake. Wala hapewi umri mwenye umri mrefu wala hapunguziwi umri wake, ila yamo katika Kitabu. Hakika hayo kwa Mwenyezi Mungu ni mepesi.

AMALI NJEMA HUIPANDISHA

Aya 9 – 11

MAANA

Na Mwenyezi Mungu ndiye anayezituma pepo ziyatimue mawingu, nasi tukayafikisha kwenye nchi iliyokufa, tukaifufua ardhi baada ya kufa kwake. Ndio kama hivyo kufufuliwa.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 8 (7:57).

Mwenye kutaka enzi basi enzi yote ni ya Mwenyezi Mungu.

Enzi ni ya Mwenyezi Mungu na ya dini ya Mwenyezi Mungu hasa; na kwa mawili hayo ndio binadamu anakuwa na enzi. Mwenye kujienzi kwa asiyekuwa Mwenyezi Mungu atadhalilika. Ibn Arabi katika kitabu Futuhatul-Makkiyya, anasema:

“Enzi ya haki hasa ni kuwa hakuna Mola ila Yeye, na enzi ya Mtume wake ni kwa Mwenyezi Mungu, na enzi ya waumini ni kwa Mwenyezi Mungu na Mtume wake. Basi yanathibiti kwenye tanzu yale yaliyonayothibiti kwenye asili.”

Kudhalilika kwa waislamu leo kumetokana na kuwa wao wanajienzi kwa usiokuwa Uislamu. Hapo mwanzo walikuwa ni wachache kuliko sasa, lakini walikuwa ni wengi kwa kujienzi na jamii na umoja wao dhidi ya adui wa Mwenyezi Mungu na adui wao.

Kwake hupanda neno zuri na amali njema huiinua.

Kupanda maneno na kuinuka matendo kwenda kwake Mwenyezi Mungu Mtukufu ni kinaya cha kuyakubali na kuyalipa thawabu. Maneno mazuri ni yale yanayonufaisha, na vile vile amali njema.

Aya inaashiria kwamba sababu ya kuenziwa na kutukuzwa mbele ya Mwenyezi Mungu ni kauli na vitendo vinavyowanufaisha watu.

Na wanaopanga njama za maovu watapata adhabu kali, na njama za hao zitaangamia.

Kupanga njama za maovu ni kupanga kuwaudhi waumini na viongozi wema. Lakini njama zao zitaambulia patupu. Maana ya Aya hii ni kama kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: Na vitimbi viovu havimpati ila mwenyewe.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 17 (22:5).

Kisha akawafanya aina kwa aina, mweusi na mweupe na mume na mke.Na mwanamke yeyote hachukui mimba wala hazai, ila kwa elimu yake, kwa sababu yeye amekizunguka kila kitu.

Wala hapewi umri mwenye umri mrefu wala hapunguziwi umri wake, ila yamo katika Kitabu. Hakika hayo kwa Mwenyezi Mungu ni mepesi.

Kupunguziwa umri ni kuwa na umri mfupi; na kuwa katika Kitabu cha Mwenyezi Mungu ni kuwa katika ujuzi wa Mwenyezi Mungu. Maana kwa ujumla ni kuwa umri wote uko mikononi mwa Mwenyezi Mungu Mtukufu. Katika Nahjul-Balagha imeelezwa:

“Hampati neema katika dunia ila ni kwa kuimaliza nyingine; wala hapati umri mwenye umri miongoni mwenu ila ni kwa kuumaliza mwingine.” Tazama Juz. 4 (3:144 – 148) kifungu cha ‘Ajali haina kinga’.