TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MOJA Juzuu 21

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MOJA15%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MOJA Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: Qurani tukufu

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
  • Anza
  • Iliyopita
  • 32 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 28394 / Pakua: 5243
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MOJA

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MOJA Juzuu 21

Mwandishi:
Swahili

1

2

17

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MOJA

وَأَقْبَلَ بَعْضُهُمْ عَلَىٰ بَعْضٍ يَتَسَاءَلُونَ ﴿٢٧﴾

27. Watakabiliana wao kwa wao kuulizana.

قَالُوا إِنَّكُمْ كُنتُمْ تَأْتُونَنَا عَنِ الْيَمِينِ ﴿٢٨﴾

28. Watasema: Kwa hakika nyinyi mlikuwa mkitujia upande wa kuume.

قَالُوا بَل لَّمْ تَكُونُوا مُؤْمِنِينَ ﴿٢٩﴾

29. Watasema: Bali nyinyi wenyewe hamkuwa waumini.

وَمَا كَانَ لَنَا عَلَيْكُم مِّن سُلْطَانٍ بَلْ كُنتُمْ قَوْمًا طَاغِينَ ﴿٣٠﴾

30. Na hatukuwa na mamlaka juu yenu, bali nyinyi mlikuwa waasi.

فَحَقَّ عَلَيْنَا قَوْلُ رَبِّنَا إِنَّا لَذَائِقُونَ ﴿٣١﴾

31. Basi kauli ya Mola wetu imekwishatuthibitika. Hakika bila ya shaka tutaonja.

فَأَغْوَيْنَاكُمْ إِنَّا كُنَّا غَاوِينَ ﴿٣٢﴾

32. Tuliwapoteza kwa sababu sisi wenyewe tulikuwa wapotovu.

فَإِنَّهُمْ يَوْمَئِذٍ فِي الْعَذَابِ مُشْتَرِكُونَ ﴿٣٣﴾

33. Basi hakika wao siku hiyo watashirikiana katika adhabu.

إِنَّا كَذَٰلِكَ نَفْعَلُ بِالْمُجْرِمِينَ ﴿٣٤﴾

34. Hivyo ndivyo tutakavyowafanyia wakosefu.

إِنَّهُمْ كَانُوا إِذَا قِيلَ لَهُمْ لَا إِلَـٰهَ إِلَّا اللَّـهُ يَسْتَكْبِرُونَ ﴿٣٥﴾

35. Wao walipokuwa wakiambiwa: Hapana Mola ila Mwenyezi Mungu (La ilaha illa Llahu) tu, wakijivuna.

وَيَقُولُونَ أَئِنَّا لَتَارِكُو آلِهَتِنَا لِشَاعِرٍ مَّجْنُونٍ ﴿٣٦﴾

36. Na wakisema: Hivi tuiache miungu yetu kwa ajili ya huyu mshairi mwendawazimu?

بَلْ جَاءَ بِالْحَقِّ وَصَدَّقَ الْمُرْسَلِينَ ﴿٣٧﴾

37. Bali ameleta haki, na amewasadikisha Mitume.

WATAKABILANA WAO KWA WAO

Aya 27 – 37

MAANA

Watakabiliana wao kwa wao kuulizana. Watasema: Kwa hakika nyinyi mlikuwa mkitujia upande wa kuume.

Neno yamin, tulilolifasiri kwa maana ya kuume, huwa lina maana nyingi; miongoni mwazo ni: mkono, upande usiokuwa wa kushoto na baraka na nguvu. Makusudo hapa ni kupoteza.

Wahalifu wataulizana na kulaumiana wakati watakapoiona adhabu. Wanyonge watawatupia lawama viongozi kuwa kama si nyinyi tunge- likuwa waumini. Hadaa hii wameiletea ibara ya kuume. Kwa sababu waarabu wanakiona kitu kinachokuja kwa upande wa kuume kuwa ni kizuri. Kwa hiyo kusema kwao mkitujia kwa upande wa kuume ni sawa na anayesema umenilenga hasa au umeniwahi kweli. Umetangulia mfano wake katika Juz. 8 (7:38).

Watasema: Bali nyinyi wenyewe hamkuwa waumini. Na hatukuwa na mamlaka juu yenu, bali nyinyi mlikuwa waasi. Basi kauli ya Mola wetu imekwishatuthibitikia. Hakika bila ya shaka tutaonja. Tuliwapoteza kwa sababu sisi wenyewe tulikuwa wapotovu.

Hii ni kauli ya viongozi wakiwajibu wale wanyonge, kwamba sisi kazi yetu ilikuwa ni kutoa mwito na kuupamba, nanyi mkauitikia. Nasi tuliwaita kwenye kufuru mkaitikia na mtume akawaita kwenye imani mkamkimbia, kwa sababu ya uhabithi na upotevu wenu. Vinginevyo sisi tuna uwezo gani juu yenu lau mngeliamua kumwamini Mwenyezi Mungu; kama walivyoamini wengine?

Kwa hiyo basi natija ya ukafiri wetu na upotevu wenu na kutuitikia ni kustahiki kauli ya adhabu kwetu na kwenu; kama muonavyo.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 20 (29:25) na Juz. 22 (33:67).

Basi hakika wao siku hiyo watashirikiana katika adhabu.

Haya ni maneno ya Mwenyezi Mungu (s.w.t). Maana yake ni kuwa adhabu itawaangukia wote siku hiyo watakayolaumiana.

Hivyo ndivyo tutakavyowafanyia wakosefu.

Adhabu ya daima bila ya kutofautisha mfuasi na mwenye kufuatwa.

Wao walipokuwa wakiambiwa:Hapana Mola ila Mwenyezi Mungu (La ilaha illa Llahu) tu, wakijivuna.

Walijivuna na wajifanya wakubwa kuliko haki, ndio yakawapata yaliyowapata wajivuni waliokuwa kabla yao.

Na wakisema: Hivi tuiache miungu yetu kwa ajili ya huyu mshairi mwendawazimu?

Wafasiri wamesema kuwa washirikina walijichanganya kwenye maneno yao; pale walipomsifu Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w. w ) kuwa ni mshairi na mwenda wazimu, ambapo mshairi huwa anatumia akili kupangilia maneno yake kwa usanifu wa hali ya juu. Sasa mwendawazimu anaweza kweli kazi hii.

Bali ameleta haki, na amewasadikisha Mitume.

Hapana! Huyo si mshairi wala mwendawazimu isipokuwa ni Mtume mtukufu, ameleta haki kutoka kwa Mwenyezi Mungu, na amewasadikisha Mitume waliomtangulia na vitabu vyao.

Baada ya hayo. Kwa hakika mwendawazimu ni bora kuliko yule aliyemsifu Muhammad,(s.a.w. w ) aliyeteulia na Mwenyezi Mungu na kumchagua kwa ujumbe wake na kumjaalia ni bwana na mwisho wa Mitume, kuwa ni mwendawazimu. Tazama tafsri ya (36:69) katika Juzuu hii tuliyo nayo.

إِنَّكُمْ لَذَائِقُو الْعَذَابِ الْأَلِيمِ ﴿٣٨﴾

38. Hakika nyinyi bila ya shaka mtaionja adhabu chungu.

وَمَا تُجْزَوْنَ إِلَّا مَا كُنتُمْ تَعْمَلُونَ ﴿٣٩﴾

39. Wala hamtalipwa ila mliyokuwa mkiyafanya.

إِلَّا عِبَادَ اللَّـهِ الْمُخْلَصِينَ ﴿٤٠﴾

40. Isipokuwa waja wa Mwenyezi Mungu waliotakaswa.

أُولَـٰئِكَ لَهُمْ رِزْقٌ مَّعْلُومٌ ﴿٤١﴾

41. Hao ndio watakaopata riziki maalum.

فَوَاكِهُ وَهُم مُّكْرَمُونَ ﴿٤٢﴾

42. Matunda, nao watahishimiwa.

فِي جَنَّاتِ النَّعِيمِ ﴿٤٣﴾

43. Katika Bustani za neema.

عَلَىٰ سُرُرٍ مُّتَقَابِلِينَ ﴿٤٤﴾

44. Wako juu ya viti wameelekeana.

يُطَافُ عَلَيْهِم بِكَأْسٍ مِّن مَّعِينٍ ﴿٤٥﴾

45. Wakizungushiwa kikombe cha chemchem.

بَيْضَاءَ لَذَّةٍ لِّلشَّارِبِينَ ﴿٤٦﴾

46. Cheupe kitamu kwa wanywao.

لَا فِيهَا غَوْلٌ وَلَا هُمْ عَنْهَا يُنزَفُونَ ﴿٤٧﴾

47. Hakina madhara, wala hakimaliziki.

وَعِندَهُمْ قَاصِرَاتُ الطَّرْفِ عِينٌ ﴿٤٨﴾

48. Na watakuwa nao wanawake wenye macho makunjufu.

كَأَنَّهُنَّ بَيْضٌ مَّكْنُونٌ ﴿٤٩﴾

49. Kama kwamba wao ni mayai yaliyohifadhika.

JUU YA VITANDA WAMEELEKEANA

Aya 38 – 49

MAANA

Hakika nyinyi bila ya shaka mtaionja adhabu chungu.Wala hamtalipwa ila mliyo kuwa mkiyafanya.

Baada ya Mwenyezi Mungu kusema kuwa wakosefu watashirikiana katika adhabu, sasa anawaambia kuwa adhabu yao ni malipo ya yaliyochumwa na mikonoi yao, wala hawatadhulumia hata chembe.

Isipokuwa waja wa Mwenyezi Mungu waliotakaswa. Hao ndio watakaopata riziki maalumu.

Hii ni desturi ya Qur’an, kuwataja wakosefu na adhabu yao kisha kufuatia kuwataja wema na malipo yao. Malipo yenyewe kwa ujumla ni riziki maalum ya Mwenyezi Mungu kwa ajili yao.

Ama ufafanuzi wa riziki hiyo ni kama ifuatavyo:

Matunda, wanayoyatamani,nao watahishimiwa. Kwa sababu matunda na kudharauliwa ni sumu na huzuni. Kuna mithali isemayo: “Niheshimu wala usinilishe”

Katika Bustani za neema, zinazopitiwa na mito.Wako juu ya viti wamekabiliana, wakiangaliana kwa raha na furaha

Wakizungushiwa kikombe cha chemchem. Vijana watawapatia kinywajicheupe kitamu kwa wanywao, chenye rangi na ladha nzuri.Hakina madhara, Hakiumizi kichwawala kuleta maumivu wala hakimaliziki.

Neno nazaf likitumika kwenye kinywaji lina maaana ya kumalizika na likitumika kwa mtu lina maana ya kuisha akili yake; ndio maana baadhi ya wafasiri wakasema “Hakiwaleweshi;” yaani kinywaji hakimalizi akili yao.

Na watakuwa nao wanawake wenye macho makunjufu

Matunda, heshima, furaha, watumishi na zaidi ya hayo ni wanawake safi warembo wenye macho makunjufu na mazuri,kama kwamba wao ni mayai yaliyohifadhika. Kuwa kama mayai ni kinaya cha usafi wao na kuwa hawajaguswa na mikono wala kutazamwa na mcho.

WANAWAKE NA WATUMISHI

Hivi karibuni nilipata barua kutoka kwa mwananfunzi mmoja wa kike wa Kuwait, ikisema kuwa alikuwa na mazungumzo na rika lake. Yeye akasema kuwa Uislamu haumtofautishi mwanamume na mwanamke.

Wenzake wakampinga na kumwambia kuwa Qur’an imeelezea wazi kuwa Mwenyezi Mungu kesho atawalipa wanaume wema mahurulaini na hakusema vile atakavyowalipa wanawake wema. Kama haki ingelikuwa sawa, basi malipo yangelikuwa ya aina moja. Msichana anasema alishindwa kujibu na akataka nimwandikie ili awakinaishe wenzake.

Majibishano haya mazuri yanatufahamisha kuwa mwanamke ni sawa na mwanamume katika mataminio yake ya kimwili na mapendeleo yake. Na kwamba kupata mume ndio malipo bora zaidi, kama ilivyo kwa mwana- mume kupata mke. Vile vile inatufahamisha kuwa wivu wa mwanamke kwa mwanamume ni kama wa mwanamume.

Basi nikamjibu hivi: “Qur’an imeelezea waziwazi usawa baina ya mwanamume na mwanamke kama msingi wa ujumla. Kwenye hilo inasema:

أَنِّي لَا أُضِيعُ عَمَلَ عَامِلٍ مِّنكُم مِّن ذَكَرٍ أَوْ أُنثَىٰ ﴿١٩٥﴾

“ …kwamba mimi sitapoteza amali ya mfanya amali miongoni mwenu, akiwa mwanamume au mwanamke” Juz. 4 (3:195).

“Mwenye kufanya mema - mwanamume au mwanamke - hali ya kuwa ni mwenye kuamini, basi hao wataingia Peponi wala hawatadhulumiwa hata kitobwe cha kokwa ya tende.” Juz. 5 (4:124).

Hakuna mwenye shaka kwamba atakayeingia Peponi atapata kila kinachotamaniwa na nafsi na kuburudisha macho awe mwanamume au mwanamke, kama ilivyoelezwa kwenye (43:71).

Vile vile Qur’an imewataja watumishi kama ilivyowataja Hurulaini. Ilipowasifu Hurulaini kuwa ni kama mayai yaliyohifadhika, pia imewataja watumishi kuwa ni lulu iliyotawanywa, kama iliyosemwa kwenye. (76:19)

Sio mbali kuwa kunyamazia kutaja kuwa mwanamke atalipwa kwa kijana mzuri kumefuata ada na desturi iliyozoeleka kwa watu ya kumzungumzia kijana kuoa na kumuuliza, kwa nini huoi? Lakini hawamuulizi msichana, kwa nini huolewi; kwa vile wanakuwa na haya sana. Wakale walisema: “Ana haya kama msichana.”

Vile vile imesemekana kuwa ladha za Peponi zote ni za kiroho si za kimaada au jinsia, na kwamba kutaja hurilaini, matunda na vikombe ni kama ishara na alama ya ladha ya kimwili kwenye ladha ya kiroho na kwamba viti na vitanda ni kinaya cha cheo na daraja.

فَأَقْبَلَ بَعْضُهُمْ عَلَىٰ بَعْضٍ يَتَسَاءَلُونَ ﴿٥٠﴾

50. Tena watakabiliana wao kwa wao wakiulizana.

قَالَ قَائِلٌ مِّنْهُمْ إِنِّي كَانَ لِي قَرِينٌ ﴿٥١﴾

51. Aseme msemaji miongoni mwao: Hakika mimi nilikuwa na rafiki.

يَقُولُ أَإِنَّكَ لَمِنَ الْمُصَدِّقِينَ ﴿٥٢﴾

52. Aliyekuwa akiniambia: Hivyo wewe ni katika wanaosadiki.

أَإِذَا مِتْنَا وَكُنَّا تُرَابًا وَعِظَامًا أَإِنَّا لَمَدِينُونَ ﴿٥٣﴾

53. Ati tukishakufa tukawa udongo na mifupa, ndio tutahisabiwa?

قَالَ هَلْ أَنتُم مُّطَّلِعُونَ ﴿٥٤﴾

54. Atasema: Je! Nyie mtachungulia?

فَاطَّلَعَ فَرَآهُ فِي سَوَاءِ الْجَحِيمِ ﴿٥٥﴾

55. Basi atachungulia amwone katikati ya Jahannamu.

قَالَ تَاللَّـهِ إِن كِدتَّ لَتُرْدِينِ ﴿٥٦﴾

56. Aseme Wallahi! Ulikaribia kuniangamiza.

وَلَوْلَا نِعْمَةُ رَبِّي لَكُنتُ مِنَ الْمُحْضَرِينَ ﴿٥٧﴾

57. Na lau si neema ya Mola wangu bila ya shaka ningelikuwa miongoni mwa waliohudhurishwa.

أَفَمَا نَحْنُ بِمَيِّتِينَ ﴿٥٨﴾

58. Je! Sisi hatutakufa?

إِلَّا مَوْتَتَنَا الْأُولَىٰ وَمَا نَحْنُ بِمُعَذَّبِينَ ﴿٥٩﴾

59. Isipokuwa kifo chetu cha kwanza; wala sisi hatutaadhibiwa.

إِنَّ هَـٰذَا لَهُوَ الْفَوْزُ الْعَظِيمُ ﴿٦٠﴾

60. Hakika huku, bila ya shaka, ndiko kufuzu kukubwa.

لِمِثْلِ هَـٰذَا فَلْيَعْمَلِ الْعَامِلُونَ ﴿٦١﴾

61. Kwa mfano wa haya nawafanye wafanyao.

أَذَٰلِكَ خَيْرٌ نُّزُلًا أَمْ شَجَرَةُ الزَّقُّومِ ﴿٦٢﴾

62. Je! Kukaribishwa hivi ni bora, au mti wa Zaqum?

إِنَّا جَعَلْنَاهَا فِتْنَةً لِّلظَّالِمِينَ ﴿٦٣﴾

63. Hakika Sisi tumeufanya huo kuwa ni fitna kwa waliodhulumu.

إِنَّهَا شَجَرَةٌ تَخْرُجُ فِي أَصْلِ الْجَحِيمِ ﴿٦٤﴾

64. Hakika huo ni mti unaotoka katikati ya Moto.

طَلْعُهَا كَأَنَّهُ رُءُوسُ الشَّيَاطِينِ ﴿٦٥﴾

65. Mashada yake ni kama vichwa vya mashetani.

فَإِنَّهُمْ لَآكِلُونَ مِنْهَا فَمَالِئُونَ مِنْهَا الْبُطُونَ ﴿٦٦﴾

66. Basi hakika hao bila ya shaka watakula katika huo, na wajaze matumbo kwa huo.

ثُمَّ إِنَّ لَهُمْ عَلَيْهَا لَشَوْبًا مِّنْ حَمِيمٍ ﴿٦٧﴾

67. Kisha juu yake wapewe mchanganyiko wa maji ya moto.

ثُمَّ إِنَّ مَرْجِعَهُمْ لَإِلَى الْجَحِيمِ ﴿٦٨﴾

68. Kisha hakika marejeo yao bila ya shaka yatakuwa kwenye Jahannamu.

KWA MFANO WA HAYA NAWAFANYE WAFANYAO

Aya 50 – 68

MAANA

Tena watakabilaiana wao kwa wao wakiulizana.

Bado maneno yanaendelea kuhusu watu wa Peponi. Katika Aya iliyotangulia, Mwenyezi Mungu (s.w.t) amesema kuwa watu wa Peponi watakuwa na aina mbali mbali za starehe.

Katika Aya hii anasema kuwa watazungumziana wao kwa wao, huku wakiwa na furaha, kuhusiana na maisha yao ya duniani. Miongoni mwayo ni:

Aseme msemaji miongoni mwao: Hakika mimi nilikuwa na rafiki aliyekuwa akiniambia: Hivyo wewe ni katika wanaosadiki ati tukishakufa tukawa udongo na mifupa, ndio tutahisabiwa?

Mumin huyu atawazungumzia wenzake na jirani zake kuhusiana na vile waumini wa malipo ya kiyama walivyokuwa wakifanyiwa masikhara wakisema wasioamini, ati mamake fulani, kweli tukishakufa na kuisha kabisa tutafufuliwa tuwe hai?

Hivi ndivyo alivyo kila mlahidi. Na hiyo hasa inatokana na kuwa kuamini ufufuo ni sehemu ya kuamini wahyi wa Mwenyezi Mungu kwa yule aliyemteua katika waja wake. Ikiwa mlahidi haamini wahyi huu, ataweza kweli kuamini ufufuo baada ya mauti? Kwa maneno mengine ni kuwa ufufuo ni katika mambo ya ghaibu ambayo kwa mlahidi ni vigano tu.

Atasema: Je! Nyie mtachungulia?

Mumin ataendelea kuwaambia wenzake akiwaomba waangalie Jahnnam ili waone mwisho wa aliyekuwa na dharau.

Basi atachungulia amwone katikati ya Jahannamu.

Akishawaambia wenzake atachungulia kwenye Jahannam amwone jamaa yuko katikati ya Jahannam.Aseme - kwa kumtahayariza-Wallahi! Ulikaribia kuniangamiza. Yaani kunitia kwenye shaka kwa wasiwasi wako na shaka zako.Na lau si neema ya Mola wangu bila ya shaka ningelikuwa miongoni mwa waliohudhurishwa pamoja nawe katika moto.

Kisha mumin atawageukia wenzake awaambie:

Je! Sisi hatutakufa, isipokuwa kifo chetu cha kwanza? Wala sisi hatutaadhibiwa. Hakika huku, bila ya shaka, ndiko kufuzu kukubwa.

Atazungumza haya kwa furaha kutokana na aliyoyapata huku akisema alhamudulillah, tumepita mtihani vizuri, hakuna mauti tena wala tabu. Hakuna isipokuwa radhi za Mwenyezi Mungu na neema zake. Katika maana haya ni kauli yake Mwenyezi Mungu: “Hawataonja humo isipokuwa mauti ya kwanza na atawakinga na adhabu ya moto” (44:57).

Kwa mfano wa haya nawafanye wafanyao na washindane wanaoshindana.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) amewaachia waja matendo na amali, akawajibishia kufanya yale yaliyo na kheri nao na masilahi kwao; na akawakataza yale yaliyo na shari yao na ufisadi. Kisha akwaachia hiyari ya kufanya na kuacha. Mwenye kutii akamwahidi Pepo na mwenye kuasi akamwahidi adhabu ya kuunguza.

Hakuna mwenye shaka kuwa mwenye akili atajihurumia na kuchagua lililo na masilahi zaidi. Imeelezwa kwenye Nahjul-balagha: “Hakuna thamani ya nafsi zenu ispokuwa Pepo. Basi msiziuze ila kwayo.”

Je! Kukaribishwa hivi ni bora, au mti wa Zaqum? Hakika Sisi tumeufanya huo kuwa ni fitna kwa waliodhulumu.

Kukaribishwa hivi ni kukaribishwa kwenye neema. Makusudio ya fitna hapa ni adhabu. Ama mti wa Zaqum ameubanisha Mwenyezi Mungu kwa kusema:

Hakika huo ni mti unaotoka katikati ya Moto. Mashada yake ni kama vichwa vya mashetani. Basi hakika hao bila ya shaka wataku- la katika huo, na wajaze matumbo kwa huo.

Zaqqum ni kauli ya waarabu kwa chakula kinachochukiza kukila. Kwenye Tafsir Tabari kuna maelezo Haya: “Iliposhuka Aya hii Abu Jahl alisema kwa madharau: “Mimi nitawaletea Zaqqum.” Akaleta siagi na tende kisha akasema: Haya! Nyinyi kuleni Zaqqum. Basi hii ndio Zaqqum anayowatisha nayo Muhammad.

Vichwa vya mashetani, ni kinaya cha ubaya na mandhari ya kutisha ya huo mti. Yule anayesema kuwa Zaqqum ni nembo ya ubaya wa adhabu, hatuwezi kumpinga.

Kisha juu yake wapewe mchanganyiko wa maji ya moto.

Yaani watakula zaqqum na wanywe maji ya usaha; kama anavyosema Mwenyezi Mungu: “Nyuma yake iko Jahannam na atanyeshwa maji ya usaha uliochanganyika na damu” Juz.13 (14: 16).

Kisha hakika marejeo yao bila ya shaka yatakuwa kwenye Jahannamu.

Makusudio ya marejeo ni makazi ya mwisho na makao yao ya kudumu. Maana ni kuwa chakula chao ni Zaqqum na kinywaji chao ni maji moto. Ama kivazi chao, Mwenyezi Mungu amekiashiria kwa kusema:

سَرَابِيلُهُم مِّن قَطِرَانٍ ﴿٥٠﴾

“Nguo zao zitakuwa za lami” Juz. 13 (14:50).

18

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MOJA

إِنَّهُمْ أَلْفَوْا آبَاءَهُمْ ضَالِّينَ ﴿٦٩﴾

69. Hakika waliwakuta baba zao wamepotea.

فَهُمْ عَلَىٰ آثَارِهِمْ يُهْرَعُونَ ﴿٧٠﴾

70. Na wao wakafanya haraka kufuata nyayo zao.

وَلَقَدْ ضَلَّ قَبْلَهُمْ أَكْثَرُ الْأَوَّلِينَ ﴿٧١﴾

71. Na hakika walikwishapotea kabla yao wengi wa watu wa zamani.

وَلَقَدْ أَرْسَلْنَا فِيهِم مُّنذِرِينَ ﴿٧٢﴾

72. Na hakika tuliwapelekea waonyaji.

فَانظُرْ كَيْفَ كَانَ عَاقِبَةُ الْمُنذَرِينَ ﴿٧٣﴾

73. Basi tazama jinsi ulivyokuwa mwisho wa wale walioonywa.

إِلَّا عِبَادَ اللَّـهِ الْمُخْلَصِينَ ﴿٧٤﴾

74. Isipokuwa waja wa Mwenyezi Mungu waliosafishwa.

وَلَقَدْ نَادَانَا نُوحٌ فَلَنِعْمَ الْمُجِيبُونَ ﴿٧٥﴾

75. Na hakika Nuh alituita, na Sisi ni bora wa waitikiaji.

وَنَجَّيْنَاهُ وَأَهْلَهُ مِنَ الْكَرْبِ الْعَظِيمِ ﴿٧٦﴾

76. Na tulimwokoa yeye na ahali zake kutokana na msiba mkubwa.

وَجَعَلْنَا ذُرِّيَّتَهُ هُمُ الْبَاقِينَ ﴿٧٧﴾

77. Na tuliwajaalia dhuriya zake ndio wenye kubakia.

وَتَرَكْنَا عَلَيْهِ فِي الْآخِرِينَ ﴿٧٨﴾

78. Na tukamwachia kwa walio baadaye.

سَلَامٌ عَلَىٰ نُوحٍ فِي الْعَالَمِينَ ﴿٧٩﴾

79. Amani kwa Nuh ulimwenguni kote!

إِنَّا كَذَٰلِكَ نَجْزِي الْمُحْسِنِينَ ﴿٨٠﴾

80. Kwa hakika hivyo ndivyo tunavyowalipa watendao mema.

إِنَّهُ مِنْ عِبَادِنَا الْمُؤْمِنِينَ ﴿٨١﴾

81. Hakika yeye ni katika waja wetu walio waumini.

ثُمَّ أَغْرَقْنَا الْآخَرِينَ ﴿٨٢﴾

82. Kisha tukawagharikisha wale wengine.

WALIPOTEA KABLA YAO WATU WENGI WA ZAMANI

Aya 69 – 82

MAANA

Hakika waliwakuta baba zao wamepotea. Na wao wakafanya haraka kufuata nyayo zao.

Wanazungumziwa washirikina wa kiarabu waliofuata nyayo za mababu zao bila ya kufanya utafiti wowote au mazingatio. Aya inaashiria kwamba mpotevu na mpotezaji wako sawa katika maasi na kustahili adhabu. Ama yule anayefuata uongofu na utengenevu anakuwa katika amani na adhabu ya Mwenyezi Mungu.

Hilo linafahamishwa na kauli yake Mwenyezi Mungu: “Husema: Bali tuta- fuata yale tuliyowakuta nayo baba zetu. Je, hata kama baba zao walikuwa hawafahamu chochote wala hawakuongoka?” Juz. 2 (2:170). Maana yake ni kuwa, lau baba zao wangelikuwa kwenye uongofu, ingelifaa kuwafuata. Kwa maelezo zaidi tazama Juz.2 (2:168 – 170) kifungu cha ‘Kufuata na misingi ya itikadi.’

Na hakika walikwishapotea kabla yao wengi wa watu wa zamani. Na hakika tuliwapelekea waonyaji.

Ikiwa watakukadhibisha ewe Muhammad na kupotea na haki, basi walikwishapotea kabla yao wengi katika umma, ingawaje Mwenyezi Mungu aliwapeleka mitume na wabashiri; wakawatimizia hoja na kuwabainishia mapenzi yake na machukivu yake, wakaacha hayo wakafuata yale. Basi likastahili kwao neno la adhabu.Basi tazama jinsi ulivyokuwa mwisho wa wale walioonywa walivyohizika na kubomolewa;isipokuwa waja wa Mwenyezi Mungu waliosafishwa, amewaokoa Mwenyezi Mungu (s.w.t) na adhabu yake na akawalipa ujira wake na thawabu zake.

Na hakika Nuh alituita, na Sisi ni bora wa waitikiaji.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) anaashiria yale yaliyoelezwa kwenye Aya nyingine: “Na akasema Nuh: Mola wangu! Usiache Katika ardhi mkazi yeyote katika makafiri” (71:26).

Na tulimwokoa yeye na ahali zake kutokana na msiba mkubwa.

Mwenyezi Mungu alimnusuru Nuh na watu wake kutokana na mataghuti. Akawangamiza wote bila ya kubakia, kwa kuitikia maombi ya Nabii wake Nuh. Kwa hiyo akamuokoa yeye na walikouwa pamoja naye na udhia wa ukafiri muovu na kumuhifadhi na msiba na majanga.

SAM, YAFITH NA HAM

Na tuliwajaalia dhuriya zake ndio wenye kubakia, peke yao baada ya tufani.

Katika Tafsir Tabariy imesemwa: “Dhuria wa Nuh ndio waliobakia katika ardhi baada ya kuangamia kaumu yake. Na watu wote baada yake, mpaka leo, ni wa kizazi cha Nuh.

Waajemi na waarabu wanatokana na watoto wa Sam bin Nuh,Waturuki na Waslovenia ni watoto wa Yafith na weusi ni watoto wa Ham. Ulama na mapokezi yameeleza hivyo.”

Tabari alifariki mwaka 310 (A.H.), yaani zaidi ya miaka elfu moja iliyopita. Waliomtangulia na waliokuja baada yake walimbandika jina la sheikh wa wafasiri.

Katika Kamusi ya Kitabu kitakatifu imeandikwa: “Sam ni jina la kiebrania likiwa na maana ya isimu (jina). Yeye ndiye mtoto mkubwa wa Nuh. Kizazi chake ni waarabu, Waarmenia, waashwar na wayahudi. Ndio maana lugha zao wote hao zinatiwa Saamiya, kwa kunasibishwa naye; mfano: lugha ya kiarabu na kiebrania…Yafith huenda maana yake ni uzuri… kizazi chake ni wakazi wa kuanzia magharibi mwa Najad, kusini mwa Bahari ya Kazwin (Caspian sea) na Bahari nyeusi (Black sea) hadi fukwe na visiwa vya Bahri ya kati (Mediterranean Sea) katika asili ya wahindi wa Ulaya–katika hawa wanaingia waturuki na waslovania aliowaashiria Tabariy-Na ham ni jina la kiebrania yaani mwenye kuchemka naye ni mdogo wa watoto wa Nuh”

Na tukamwachia kwa walio baadaye.

Yaani tukamwachia utajo wa sifa katika uhai wake

Amani kwa Nuh ulimwenguni kote!

Yeye yuko kwenye amani ya Mungu kwa kutotajwa na mabaya. Mitume walikuwa wakimwomba Mwenyezi Mungu (s.w.t) kuwa na utajo mzuri kwa watu wakiondoka. Ibrahim(a.s ) alisema:

وَاجْعَل لِّي لِسَانَ صِدْقٍ فِي الْآخِرِينَ ﴿٨٤﴾

“Na unijaalie kutajwa kwa wema na wengine” Juz. 19 (26:84).

Kwa hakika hivyo ndivyo tunavyowalipa watendao mema.

Yaani atawafanyia wema Mwenyezi Mungu kwa vile hapotezi amali ya yeyote mwenye kutenda, awe mume au mke.

Hakika yeye ni katika waja wetu walio waumini.

Kwa sababu alifanya wema katika matendo yake, akapigana katika njia ya Mwenyezi Mungu kwa jihadi yake ya haki. Hii ndio nembo na dalili ya mumin.

Kisha tukawagharikisha wale wengine duniani na akhera watakuwa na adhabu chungu kwa yale waliyokuwa wakiyafanya.

وَإِنَّ مِن شِيعَتِهِ لَإِبْرَاهِيمَ ﴿٨٣﴾

83. Na hakika Ibrahim alikuwa katika kundi lake.

إِذْ جَاءَ رَبَّهُ بِقَلْبٍ سَلِيمٍ ﴿٨٤﴾

84. Alipomjia Mola wake kwa moyo ulio salama.

إِذْ قَالَ لِأَبِيهِ وَقَوْمِهِ مَاذَا تَعْبُدُونَ ﴿٨٥﴾

85. Alipomwambia baba yake na watu wake: Mnaabudu nini?

أَئِفْكًا آلِهَةً دُونَ اللَّـهِ تُرِيدُونَ ﴿٨٦﴾

86. Je, kwa kuzua tu mnataka miungu mingine badala ya Mwenyezi Mungu?

فَمَا ظَنُّكُم بِرَبِّ الْعَالَمِينَ ﴿٨٧﴾

87. Mnamdhania nini Mola wa walimwengu wote?

فَنَظَرَ نَظْرَةً فِي النُّجُومِ ﴿٨٨﴾

88. Kisha akapiga jicho kutazama nyota.

فَقَالَ إِنِّي سَقِيمٌ ﴿٨٩﴾

89. Akasema: Hakika mimi ni mgonjwa!

فَتَوَلَّوْا عَنْهُ مُدْبِرِينَ ﴿٩٠﴾

90. Nao wakamuacha, wakampa kisogo.

فَرَاغَ إِلَىٰ آلِهَتِهِمْ فَقَالَ أَلَا تَأْكُلُونَ ﴿٩١﴾

91. Basi akaiendea miungu yao kwa siri.

مَا لَكُمْ لَا تَنطِقُونَ ﴿٩٢﴾

92. Akaiambia: Mbona hamli? Mna nini hata hamsemi?

فَرَاغَ عَلَيْهِمْ ضَرْبًا بِالْيَمِينِ ﴿٩٣﴾

93. Kisha akaigeukia kuipiga kwa mkono wa kuume.

فَأَقْبَلُوا إِلَيْهِ يَزِفُّونَ ﴿٩٤﴾

94. Basi wakamjia upesi upesi.

قَالَ أَتَعْبُدُونَ مَا تَنْحِتُونَ ﴿٩٥﴾

95. Akasema: Je, mnaviabudu vitu mnavyovichonga?

وَاللَّـهُ خَلَقَكُمْ وَمَا تَعْمَلُونَ ﴿٩٦﴾

96. Na hali Mwenyezi Mungu ndiye aliyewaumba nyinyi na mnavyovifanya!

قَالُوا ابْنُوا لَهُ بُنْيَانًا فَأَلْقُوهُ فِي الْجَحِيمِ ﴿٩٧﴾

97. Wakasema: Mjengeeni jengo, kisha mtupeni motoni.

فَأَرَادُوا بِهِ كَيْدًا فَجَعَلْنَاهُمُ الْأَسْفَلِينَ ﴿٩٨﴾

98. Basi walitaka kumfanyia vitimbi, lakini tukawafanya wao ndio wa chini.

وَقَالَ إِنِّي ذَاهِبٌ إِلَىٰ رَبِّي سَيَهْدِينِ ﴿٩٩﴾

99. Na akasema: Hakika mimi nakwenda kwa Mola wangu atakayeniongoza.

IBRAHIM ALIKUWA KATIKA KUNDI LAKE

Aya 83 – 99

LUGHA

Neno kundi limefasiriwa kutokana na neno la kiarabu shia’ lenye maana ya mfuasi anayefuta dini na njia ya yule anayemfuata. Kisha neno hili shia likazoeleka kuwa na maana ya mfuasi wa Imam Ali (a.s.) na yule aliyechukua nafasi yake katika watoto wake.

MAANA

Na hakika Ibrahim alikuwa katika kundi lake.

Kundi lake, yaani kundi la Nuh. Maana ni kuwa Ibrahim alifuata njia ya Nuh kiitikadi na kimatendo. Mfasiri mmoja wa kale anasema kuwa baina ya Nuh na Ibrahim kulikuwa na miaka 2640. mwenye kauli hii hakutege- meza kwenye rejea za kutegemewa.

Alipomjia Mola wake kwa moyo ulio salama.

Mwenye moyo huu ni yule aliyemfanyia ikhlasi Mwenyezi Mungu peke yake katika kauli zake na vitendo vyake vyote. Kuna Hadith isemyo: “Imani ya mja haisimami sawa mpaka usimame sawa moyo wake.” Kwenye Nahjul-balgha kuna maneno haya: “Heri zote ni za moyo ulio salama uliomtii anayeuongoza na kujiepusha na anayeudekeza.”

Alipomwambia baba yake na watu wake: Mnaabudu nini? Je, kwa kuzua tu mnataka miungu mingine badala ya Mwenyezi Mungu?

Ibrahim alipinga ibada ya masanamu kwa watu wake akawakabili na kauli ya haki kwa kusema kuwa mnataka uzushi na batili kwa kumrejea asiyekuwa Mwenyezi Mungu na kujikurubisha kwa ibada kwa asiyekuwa Yeye? Umetangulia mfano wake katika Juz.7 (6:74).

Mnamdhania nini Mola wa walimwengu wote?

Je, mnamdhania kuwa ni jiwe au nyota naye ameumba ulimwengu? Je, akili yenu haiamki hata kidogo au kuzinduka kutokana na ujinga huu?

Katika Juz. 13 (13:16), kifungu cha ‘akili za watu haziwatoshelezi,’ tumebinisha kwa nini washirikina waliabudu mawe yanayokojolewa na mambwa na vicheche?

Kisha akapiga jicho kutazama nyota, akiwapa dhana watu wake kuwa anatafuta muumba wa ulimwengu, kwa vile wao walikuwa wakiabudu miungu mingi; hasa Nanar, mungu wa mwezi na mkewe Nanjal; kama ilivyoelezwa katika Kamusi ya Kitabu kitakatifu.

Maana ya Aya hii yamekuja katika Juz. 7 (6:74-79).

Akasema: Hakika mimi ni mgonjwa!

Wafasiri wana kauli nyingi kuhusu makusudio ya ugonjwa. Yenye nguvu zaidi ni ile inayosema kuwa makusudio ya ugonjwa hapa ni shaka. Na maana yanakuwa kwamba Ibrahim aliwaambia watu wake, mimi hivi sasa nimedangana natafuta ukweli na uhakika ili niweze kuongoka kuweza kumjua muumbaji.

Nimeangalia masanamu nikapata uhakika kuwa hayawezi kuwa miungu; kisha nikaangalia nyota na sikupata mwongozo wowote; nimebaki kwenye shaka na kudangana.

Mfumo wa Aya unasaidia maana haya au angalau unayapa nguvu, kwa sababu yanaunganisha baina ya kuangalia kwenye nyota na kuwa mgonjwa.

Wala kauli yake hii ya kusema ana shaka hatuwezi kusema kuwa ni uwongo, kwa sababu ni katika hali ya kwenda na mbishani ili kumchukua kwenye hoja na kumkatia nyudhuru zote.

Nao wakamwacha, wakampa kisogo.

Walimwacha na wakajiendea zao.

Basi akaiendea miungu yao kwa siri.

Alichukua fursa ya kuondoka kwao na kwenda haraka kwenye masanamu. Walikuwa wameyawekea chakula ili yakibariki, akaiambia:

Mbona hamli? Mna nini hata hamsemi?

Alisema hivi kwa kuibeza na kutoa hoja kwa anayeiabudu na kutabaruku nayo.

Kisha akaigeukia kuipiga kwa mkono wa kuume.

Aliavunja masanamu vipande vipande kwa mkono wake wa kuume na kabakisha kubwa lao, angalau waweze kurejea.

Basi wakamjia upesi upesi.

Watu walikuja haraka kwa Ibrahim na kuanza kumuuliza: wewe ndiwe uliyeifanyia hivi miungu yetu?

Akasema: Je, mnaviabudu vitu mnavyo vichonga?

Yaani ole wenu! Msimzulie Mwenyezi Mungu uwongo. Hakika Mola ni Muumba sio muumbwa na Mwenye kuruzuku sio mwenye kuruzukiwa. Nyinyi mmeyatengeneza masanamu haya kwa mikono yenu na mnayalinda, vipi yatakuwa miungu?

Na hali Mwenyezi Mungu ndiye aliyewaumba nyinyi na mnavyovifanya!

Yeye ndiye Muumba wa kila kitu na marejeo ni kwake.

Wakasema: Mjengeeni jengo, kisha mtupeni motoni.

Walishindwa kuikabili hoja kwa hoja, wakakimbila maguvu; kama ilivyo hali ya mataghuti, huwasha moto na kuwatupa humo wapigania haki na kheri; kama ilivyokuwa zamani. Na elimu ya uvunjaji ilipoondelea sasa wanautupa moto kwa wananchi wanyonge pamoja na wanawake na watoto wao.

Basi walitaka kumfanyia vitimbi, lakini tukawafanya wao ndio wa chini, pale alipoufanya moto ni baridi na salama kwa Ibrahim.

Na akasema: Hakika mimi nakwenda kwa Mola wangu ndiye atakayeniongoza.

Baada ya Mwenyezi Mungu kumwokoa Ibrahim na vitimbi vya watu wake, alihama kutoka mji wake wa Urulkaldaniyya (Chaldeans) – Babilon – kwenda Sham.

Katika Kamusi ya Kitabu kitakatifu imeandikwa: “Yaligunduliwa mabaki na michoro ya mika elfu mbili kabla ya miladi (B.C.).

Lilikutwa jina la Ibrahim kwa mfumo wa Abramu au Abrama. Ugunduzi wa historia wa sasa umedhihirisha hali ya mji wa Uru, aliouhama Ibrahim, kama ulivyokuwa wakati huo.”

Umetangulia mfano wake kwa ufafunizi kidogo kwenye Juz. 17 (21:51-60).

7

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MOJA

وَقَالَ الَّذِينَ كَفَرُوا لَن نُّؤْمِنَ بِهَـٰذَا الْقُرْآنِ وَلَا بِالَّذِي بَيْنَ يَدَيْهِ وَلَوْ تَرَىٰ إِذِ الظَّالِمُونَ مَوْقُوفُونَ عِندَ رَبِّهِمْ يَرْجِعُ بَعْضُهُمْ إِلَىٰ بَعْضٍ الْقَوْلَ يَقُولُ الَّذِينَ اسْتُضْعِفُوا لِلَّذِينَ اسْتَكْبَرُوا لَوْلَا أَنتُمْ لَكُنَّا مُؤْمِنِينَ ﴿٣١﴾

31. Na walisema waliokufuru: Hatutaiamini Qur’an hii, wala yaliyokuwa kabla yake. Na ungeliwaona madhalimu watakaposimamishwa mbele ya Mola wao wakirudishiana maneno! wale wanyonge wakiwaambia wale waliojifanya wakubwa: Lau si nyinyi bila shaka tungelikuwa waumini.

قَالَ الَّذِينَ اسْتَكْبَرُوا لِلَّذِينَ اسْتُضْعِفُوا أَنَحْنُ صَدَدْنَاكُمْ عَنِ الْهُدَىٰ بَعْدَ إِذْ جَاءَكُم بَلْ كُنتُم مُّجْرِمِينَ ﴿٣٢﴾

32. Wale waliojiona wakubwa watawaambia wale wanyonge: Kwani sisi ndio tuliowazuia na uongofu baada ya kuwafikia? Bali nyinyi wenyewe mlikuwa waovu. Kwani wanalipwa ila kwa waliokuwa wakiyatenda?

وَقَالَ الَّذِينَ اسْتُضْعِفُوا لِلَّذِينَ اسْتَكْبَرُوا بَلْ مَكْرُ اللَّيْلِ وَالنَّهَارِ إِذْ تَأْمُرُونَنَا أَن نَّكْفُرَ بِاللَّـهِ وَنَجْعَلَ لَهُ أَندَادًا وَأَسَرُّوا النَّدَامَةَ لَمَّا رَأَوُا الْعَذَابَ وَجَعَلْنَا الْأَغْلَالَ فِي أَعْنَاقِ الَّذِينَ كَفَرُوا هَلْ يُجْزَوْنَ إِلَّا مَا كَانُوا يَعْمَلُونَ ﴿٣٣﴾

33. Na wale wanyonge watawaambia wale waliojifanya wakubwa: Bali ni vitimbi vyenu vya usiku na mchana, mlipokuwa mkituamrisha tumkufuru Mwenyezi Mungu na tumfanyie washirika, nao wataficha majuto watakapoiona adhabu. Na tutaweka minyororo shingoni mwa wale waliokufuru kwani wanalipwa ila kwa waliokuwa wakiyatenda?.

HAWATAAMINI QUR’AN

Aya 31-33

MAANA

Na walisema waliokufuru: Hatutaiamini Qur’an hii, wala yaliyokuwa kabla yake, kama vile Tawrat na Injil. Walioyasema haya ni washirikina, kwa dalili ya kauli yake Mwenyezi Mungu:

وَقَالَ الرَّسُولُ يَا رَبِّ إِنَّ قَوْمِي اتَّخَذُوا هَٰذَا الْقُرْآنَ مَهْجُورًا {30 }

Na Mtume alisema: Ewe Mola wangu! Hakika watu wangu wameifanya hii Qur’an ni mahame.” Juz. 19 (25:30).

Wameihama na kuikana kwa sababu inamfanya sawa mweusi na mweupe na ikawaambia:

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا لَا يَسْخَرْ قَوْمٌ مِّن قَوْمٍ عَسَىٰ أَن يَكُونُوا خَيْرًا مِّنْهُمْ وَلَا نِسَاءٌ مِّن نِّسَاءٍ عَسَىٰ أَن يَكُنَّ خَيْرًا مِّنْهُنَّ وَلَا تَلْمِزُوا أَنفُسَكُمْ وَلَا تَنَابَزُوا بِالْأَلْقَابِ بِئْسَ الِاسْمُ الْفُسُوقُ بَعْدَ الْإِيمَانِ وَمَن لَّمْ يَتُبْ فَأُولَـٰئِكَ هُمُ الظَّالِمُونَ ﴿١١﴾

“Enyi ambao mmeamini! Wanaume wasiwadharau wanaume wengine, huenda wakawa bora kuliko wao; wala wanawake kwa wanawake wengine, huenda wakawa bora kuliko wao. Wala msitiane kasoro, wala msiitane majina ya kejeli. Ni uovu kutumia jina baya baada ya imani.” (49:11).

Vile vile waliukana utume wa Muhammad(s.a.w. w ) kwa sababu alitaka kuwatoa kwenye ujinga na kurudi nyuma, waende kwenye elimu na maendeleo.

Mtaalamu mmoja wa Ulaya, Jack Rezler, aliyeandika kitabu kuhusu mwamko wa kiislamu na kingine kinachozungumzia maendeleo ya waarabu ambavyo vilichapishwa ufaransa mnamo 1962, alisema: “Hatua ya kwanza ya maendeleo ya waarabu ilianza kwa kujitokeza dini ya kiislamu.

Kuna sababu kadhaa zilizofanya maendeleo haya na kuenea kwake; sababu kubwa zaidi ni kuweko na roho ya kimaana kwa Waislamu kupitia dini hii mpya; jambo ambalo limeleta ushujaa, kiasi cha kufikia kuyadharau mauti kwa ajili ya Mwenyezi Mungu.”

Na ungeliwaona madhalimu watakaposimamishwa mbele ya Mola wao wakirudishiana maneno!

Baada ya Mtume(s.a.w. w ) kukata tamaa kuwa washirikina wataamini, Mola Mtukufu alimtuliza na kumwambia kuwa kesho utaona hawa waongo watakavyokuwa dhalili na kuhizika pale watakaposimama mbele ya Mwenyezi Mungu kwa hisabu, jinsi mfuasi atakavyomlaumu aliyemfuata kila mmoja atamtia makosani mwinginewale wanyonge wakiwaambia wale waliojifanya wakubwa: Lau si nyinyi bila shaka tungelikuwa waumini.

Wanyonge ni wale wafuasi; na waliojifanya wakubwa ni viongozi.

Wale waliojiona wakubwa watawaambia wale wanyonge: Kwani sisi ndio tuliowazuia na uongofu baada ya kuwafikia? Bali nyinyi wenyewe mlikuwa waovu, sawa na kauli yake Mwenyezi Mungu:

كَمَثَلِ الشَّيْطَانِ إِذْ قَالَ لِلْإِنسَانِ اكْفُرْ فَلَمَّا كَفَرَ قَالَ إِنِّي بَرِيءٌ مِّنكَ إِنِّي أَخَافُ اللَّـهَ رَبَّ الْعَالَمِينَ ﴿١٦﴾

“Kama mfano wa shetani anapomwambia mtu: Kufuru. Na akikufuru humwambia: Mimi si pamoja nawe. Hakika mimi namwogopa Mwenyezi Mungu, Mola wa walimwengu. (59:16).

Sio mbali kuwa shetani katika Aya hii ni kinaya cha viongozi wapotevu wanaopoteza.

Na wale wanyonge watawaambia wale waliojifanya wakubwa: Bali ni vitimbi vyenu vya usiku na mchana, mlipokuwa mkituamrisha tumkufuru Mwenyezi Mungu na tumfanyie washirika.

Wafuasi na viongozi watakapokata tamaa ya kuokoka watatupiana lawama na kutuhumiana, kila kundi likijaribu kuwatupia makosa wengine; sawa na wezi wanapoafikiana kufanya uhalifu, lakini wanaposhikwa wanalaniana wao kwa wao.

Mwisho ushindi utakuwa ni wa wafuasi, kwa kuwakabili waliojifanya wakubwa kwa njama walizozifanya usiku na mchana na kuwadanga na ukafiri na ushirikina kwa njia mbalimbali.

Hata hivyo hilo halitawaondolea adhabu wala kuwapunguzia, maadamu walikuwa na akili na kulifanya hilo kwa hiyari yao: “Wa mwisho wao watawasema wa mwanzo wao: Mola wetu! Hawa ndio waliotupoteza basi uwape adhabu ya moto maradufu. Atasema: Itakuwa maradufu kwenu nyote, lakini hamjui.” Juz. 8 (7:38).

Nao wataficha majuto watakapoiona adhabu. Yaani wafuasi na waliofuatwa. Kila mwenye kuzembea na kupituka mipaka mwisho wake ni adhabu na majuto.

Na tutaweka minyororo shingoni mwa wale waliokufuru, viongozi na wafuasi wao.Kwani wanalipwa ila kwa waliyokuwa wakiyatenda? Kabisa! Mtu atalipwa kwa aliyoyafanya tu na Mola wako si mwenye kuwadhulumua waja.

وَمَا أَرْسَلْنَا فِي قَرْيَةٍ مِّن نَّذِيرٍ إِلَّا قَالَ مُتْرَفُوهَا إِنَّا بِمَا أُرْسِلْتُم بِهِ كَافِرُونَ ﴿٣٤﴾

34. Na hatukumtuma mwonyaji yeyote kwenye mji ila walisema wapenda anasa wake: Hakika sisi tunayakataa hayo mliyotumwa nayo.

وَقَالُوا نَحْنُ أَكْثَرُ أَمْوَالًا وَأَوْلَادًا وَمَا نَحْنُ بِمُعَذَّبِينَ ﴿٣٥﴾

35. Na wakasema: Sisi tuna mali nyingi zaidi na watoto, wala sisi hatutaadhibiwa.

قُلْ إِنَّ رَبِّي يَبْسُطُ الرِّزْقَ لِمَن يَشَاءُ وَيَقْدِرُ وَلَـٰكِنَّ أَكْثَرَ النَّاسِ لَا يَعْلَمُونَ ﴿٣٦﴾

36. Sema: Hakika Mola wangu humkunjulia riziki amtakaye na huikunja, lakini watu wengi hawajui.

وَمَا أَمْوَالُكُمْ وَلَا أَوْلَادُكُم بِالَّتِي تُقَرِّبُكُمْ عِندَنَا زُلْفَىٰ إِلَّا مَنْ آمَنَ وَعَمِلَ صَالِحًا فَأُولَـٰئِكَ لَهُمْ جَزَاءُ الضِّعْفِ بِمَا عَمِلُوا وَهُمْ فِي الْغُرُفَاتِ آمِنُونَ ﴿٣٧﴾

37. Na si mali yenu wala watoto wenu watakaowajongeza kwetu muwe karibu, isipokuwa aliyeamini na akatenda mema. Hao basi watapata malipo maradufu, kwa waliyoyafanya nao watakuwa salama katika maghorofa.

وَالَّذِينَ يَسْعَوْنَ فِي آيَاتِنَا مُعَاجِزِينَ أُولَـٰئِكَ فِي الْعَذَابِ مُحْضَرُونَ ﴿٣٨﴾

38. Na wale ambao wanajitahidi kuzipinga ishara zetu, wakaona watashinda, hao watahudhurishwa kwenye adhabu.

قُلْ إِنَّ رَبِّي يَبْسُطُ الرِّزْقَ لِمَن يَشَاءُ مِنْ عِبَادِهِ وَيَقْدِرُ لَهُ وَمَا أَنفَقْتُم مِّن شَيْءٍ فَهُوَ يُخْلِفُهُ وَهُوَ خَيْرُ الرَّازِقِينَ ﴿٣٩﴾

39. Sema: Hakika Mola wangu humkunjulia riziki amtakaye katika waja wake na humkunjia. Na chochote mtakachotoa Yeye atakilipa. Naye ni Mbora wa wanaoruzuku.

وَيَوْمَ يَحْشُرُهُمْ جَمِيعًا ثُمَّ يَقُولُ لِلْمَلَائِكَةِ أَهَـٰؤُلَاءِ إِيَّاكُمْ كَانُوا يَعْبُدُونَ ﴿٤٠﴾

40. Na siku atakayowakusanya wote, kisha atawaambia Malaika: Je, hawa walikuwa wakiwaabudu?

قَالُوا سُبْحَانَكَ أَنتَ وَلِيُّنَا مِن دُونِهِم بَلْ كَانُوا يَعْبُدُونَ الْجِنَّ أَكْثَرُهُم بِهِم مُّؤْمِنُونَ ﴿٤١﴾

41. Watasema: Umetakasika! Wewe ndiye walii wetu sio hao. Bali walikuwa wakiwaabudu majini; wengi wao wakiwaamini hao.

فَالْيَوْمَ لَا يَمْلِكُ بَعْضُكُمْ لِبَعْضٍ نَّفْعًا وَلَا ضَرًّا وَنَقُولُ لِلَّذِينَ ظَلَمُوا ذُوقُوا عَذَابَ النَّارِ الَّتِي كُنتُم بِهَا تُكَذِّبُونَ ﴿٤٢﴾

42. Na leo hii hawataweza baadhi yenu kuwaletea nafuu wengine wala kuwadhuru. Na tutawaambia wale ambao wamedhulumu: Onjeni adhabu ya Moto mliokuwa mkiukadhibisha.

WAPENDA ANASA

Aya 34 – 42

MAANA

Na hatukumtuma mwonyaji yeyote kwenye mji ila walisema wapenda anasa wake: Hakika sisi tunayakataa hayo mliyotumwa nayo. Na wakasema: Sisi tuna mali nyingi zaidi na watoto, wala sisi hatutaadhibiwa.

Hii ndio fikra ya wapenda anasa na hii ndio lugha yao. Mali ndio ya kwanza na ya mwisho; ndiyo bwana na wao ni watumwa.

Wanabeba bendera ya shari na uchokozi kwa watu kwa ajili ya mali, wanatawala masoko na vyakula, wanaanzisha vita moto na vita baridi, wanatafuta kila namna ya kutawala maisha na kila kitu wanakifungamanisha na chumo lao na faidia yao.

Kwao elimu sio chochote ila ikiwa inazidisha utajiri wao, dini ni ugaidi ila ikiwa inalinda masilahi yao, na amani ni wao wapore na wanayang’anye bila ya ya kuulizwa au kukemewa. Tazama Juz. 15: (17:16,90).

Sema: Hakika Mola wangu humkunjulia riziki amtakaye na huikunja, lakini watu wengi hawajui.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 13 (13:26) kifungu cha ‘riziki na mtu.

Na si mali yenu wala watoto wenu watakaowajongeza kwetu muwe karibu, isipokuwa aliyeamini na akatenda mema. Hao basi watapata malipo maradufu, kwa waliyoyafanya nao watakuwa salama katika maghorofa.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) hapimi kheri na fadhila kwa mali na watoto, wala kwa vyeo na nasaba; bali ni kwa imani na matendo mema. Ni kwa mawili haya ndio mja anakuwa ni mwenye kuridhiwa mbele ya Mwenyezi Mungu kwa thawabu zake na fadhila zake.

Imam Ali(a.s) anasema:“Heri sio kuwa nyingi mali yako na watoto, lakini heri ni kuwa nyingi elimu yako na kuwa na ustahamilivu mkubwa, na ushindane na watu kwa kumwabudu Mola wako. Ukifanya vizuri msifu Mwenyezi Mungu na ukifanya uovu muombe msamaha Mwenyezi Mungu; wala hakuna heri isipokuwa kwa watu wawili: Mtu aliyefanya dhambi akaiunganisha na toba, na mtu anayeharakisha kheri.”

Na wale ambao wanajitahidi kuzipinga ishara zetu, wakaona watashinda, hao watahudhurishwa kwenye adhabu.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 17 (22:51).

Sema: Hakika Mola wangu humkunjulia riziki amtakaye katika waja wake na humkunjia.

Unaweza kuuliza : Kwa nini Mwenyezi Mungu (s.w.t) amekariri Aya hii, pamoja na kujua kuwa kuna mtengano wa Aya mbili tu?

Wafasiri wamejibu kwamba Aya ya kwanza inahusika na makafiri na ya pili ni ya waumini. Razi anasema: “Dalili ya hilo ni kuwa Mwenyezi Mungu Mtukufu katika Aya ya pili amesema katika ‘waja wake’ na ya kwanza amesema ‘waja’ tu, na mja anayetegemezwa kwake Mwenyezi Mungu anakusudiwa muumini.”

Sio mbali kuwa makusudio ya kukaririka ni mawaidha na kuhimiza kutoa ambako Mwenyezi Mungu amekuashiria kwa kusema:

Na chochote mtakachotoa Yeye atakilipa. Naye ni Mbora wa wanaoruzuku.

Kuna Hadith ya Mtume mtukufu(s.a.w. w ) , amesema:“Kila usiku kuna mnadi anayenadi kwa kusema: “Ewe Mola wangu! Mlipe kila mtoaji. Na mnadi mwingine ananadi: Ewe Mola angu! Mlipe kila mzuiaji kuangamia.” kwenye Nahjul-Balagha imeelezwa:“Iteremsheni riziki kwa sadaka.”

Na siku atakayowakusanya wote, kisha atawaambia Malaika: Je, hawa walikuwa wakiwaabudu?

Makusudio ya kuelekeza swali hili kwa Malaika ni kuwatahayariza washirikina. Aya inafahamisha kuwa baadhi ya waarabu walikuwa wakiwaabudu malaika. Hayo yanaashiriwa na kauli yake Mwenyezi Mungu: “Je, Mola wenu amewachagulia watoto wa kiume na yeye akajichukulia watoto wa kike katika Malaika?” Juz. 15 (17:40).

Mwenye kumnasibishia Mwenyezi Mungu mwana basi amemfanya Mungu kuwa na mfano na mshirika katika uungu wake.

Watasema: Umetakasika! Wewe ndiye walii wetu sio hao.

Wewe ndiye bwana wetu na wao ni maadui zetu nasi tunajitenga nao.

Bali walikuwa wakiwaabudu majini; wengi wao wakiwaamini hao.

Kundi la wafasiri wamesema kuwa makusudio ya jini hapa ni mashetani na kwamba wao wanawapambia washirikina wawaabudu malaika na wengineo badala ya Mwenyezi Mungu.

Wengine wakasema kuwa ibada ya majini ilikuwa maarufu kwa waarabu; kwa hiyo maana ya Aya yatabaki kwenye dhahiri yake, wala hakuna haja ya kufanya taawili.

Iwe ni majini ndio waliokuwa wakiabudiwa au wengineo kwa kudanganywa na shetani, bado makusudio ya kwanza ya Aya ni kukanusha kumshirikisha Mwenyezi Mungu na kwamba hakuna uombezi kwake ila kwa idhini yake. Vile vile hakuna kimbilio isipokuwa kwake yeye tu.

Ndio maana Mwenyezi Mungu Mtukufu akafuatishia na kauli yake:

Na leo hii hawataweza baadhi yenu kuwaletea nafuu wengine wala kuwadhuru.

Si malaika, watu wala majini wanaoweza wao wenyewe kujikinga, sikwambii tena kuwasaidia wengine. Yeye peke yake ndiye mwenye ufalme na sifa njema, naye ni muweza wa kila kitu.

Na tutawaambia wale ambao wamedhulumu: Onjeni adhabu ya Moto mliokuwa mkiukadhibisha.

Walisema kuwa hakuna Pepo wala Moto, wala hatutauamini mpaka tutakapouona waziwazi. Basi ndio Mwenyezi Mungu akawachoma kuitikia matakwa yao.

Aya hii imenikumbusha wanaosema kuwa hakuna elimu wala maarifa ila kwa njia ya kushuhudia au majaribio; hata katika visivyoonekana na kuhisiwa.

8

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MOJA

وَإِذَا تُتْلَىٰ عَلَيْهِمْ آيَاتُنَا بَيِّنَاتٍ قَالُوا مَا هَـٰذَا إِلَّا رَجُلٌ يُرِيدُ أَن يَصُدَّكُمْ عَمَّا كَانَ يَعْبُدُ آبَاؤُكُمْ وَقَالُوا مَا هَـٰذَا إِلَّا إِفْكٌ مُّفْتَرًى وَقَالَ الَّذِينَ كَفَرُوا لِلْحَقِّ لَمَّا جَاءَهُمْ إِنْ هَـٰذَا إِلَّا سِحْرٌ مُّبِينٌ ﴿٤٣﴾

43. Na wanaposomewa Aya zetu zilizo wazi wanasema: Huyu si chochote ila ni mtu anayetaka kuwazuia na waliyokuwa wakiyaabudu baba zenu. Na wakasema: Haya si chochote ila ni uongo uliozuliwa.” Na wale waliokufuru waliiambia haki pale ilipowajia: “Haya si chochote ila ni uchawi ulio dhahiri.

وَمَا آتَيْنَاهُم مِّن كُتُبٍ يَدْرُسُونَهَا وَمَا أَرْسَلْنَا إِلَيْهِمْ قَبْلَكَ مِن نَّذِيرٍ ﴿٤٤﴾

44. Wala hatukuwapa vitabu wavisome, wala hatukuwatumia muonyaji kabla yako.

وَكَذَّبَ الَّذِينَ مِن قَبْلِهِمْ وَمَا بَلَغُوا مِعْشَارَ مَا آتَيْنَاهُمْ فَكَذَّبُوا رُسُلِي فَكَيْفَ كَانَ نَكِيرِ ﴿٤٥﴾

45. Na walikadhibisha wale waliokuwa kabla yao. Na hawakufikilia hata sehemu ya kumi ya tulivyowapa hao. Wakawakadhibisha mitume wangu. basi je, kulikuwaje kukanya kwangu?

قُلْ إِنَّمَا أَعِظُكُم بِوَاحِدَةٍ أَن تَقُومُوا لِلَّـهِ مَثْنَىٰ وَفُرَادَىٰ ثُمَّ تَتَفَكَّرُوا مَا بِصَاحِبِكُم مِّن جِنَّةٍ إِنْ هُوَ إِلَّا نَذِيرٌ لَّكُم بَيْنَ يَدَيْ عَذَابٍ شَدِيدٍ ﴿٤٦﴾

46. Sema: Hakika ninawapa mawaidha kwa jambo moja tu, kwamba msimame kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, wawili wawili na mmoja mmoja; kisha mfikiri. Mwenzenu hana wazimu. Hakuwa yeye ila ni muonyaji kwenu kabla ya kuwafikia adhabu kali.

قُلْ مَا سَأَلْتُكُم مِّنْ أَجْرٍ فَهُوَ لَكُمْ إِنْ أَجْرِيَ إِلَّا عَلَى اللَّـهِ وَهُوَ عَلَىٰ كُلِّ شَيْءٍ شَهِيدٌ ﴿٤٧﴾

47. Sema: Ujira niliowaomba ni wenu nyinyi. Sina ujira ila kwa Mwenyezi Mungu. Naye ni shahidi juu ya kila kitu.

قُلْ إِنَّ رَبِّي يَقْذِفُ بِالْحَقِّ عَلَّامُ الْغُيُوبِ ﴿٤٨﴾

48. Sema: Hakika Mola wangu hutoa haki, Mjuzi mno wa ghaibu.

قُلْ جَاءَ الْحَقُّ وَمَا يُبْدِئُ الْبَاطِلُ وَمَا يُعِيدُ ﴿٤٩﴾

49. Sema: Haki imefika na batili haijitokezi wala hairudi.

قُلْ إِن ضَلَلْتُ فَإِنَّمَا أَضِلُّ عَلَىٰ نَفْسِي وَإِنِ اهْتَدَيْتُ فَبِمَا يُوحِي إِلَيَّ رَبِّي إِنَّهُ سَمِيعٌ قَرِيبٌ ﴿٥٠﴾

50. Sema: Ikiwa nimepotea basi nimepotea kwa kuidhuru nafsi yangu tu. Na ikiwa nimeongoka basi ni kwa sababu ya kuniletea wahyi Mola wangu. Hakika Yeye ni Mwenye kusikia aliye karibu.

NINAWAPA MAWAIDHA KWA JAMBO MOJA TU

Aya 43 – 50

MAANA

Na wanaposomewa Aya zetu zilizo wazi wanasema: Huyu si chochote ila ni mtu anayetaka kuwazuia na waliyokuwa wakiyaabudu baba zenu. Na wakasema: Haya si chochote ila ni uwongo uliozuliwa. Na wale waliokufuru waliiambia haki pale ilipowajia: Haya si chochote ila ni uchawi ulio dhahiri.

Waliosema ni washirikina wa kiarabu, mtu wanayemkusudia ni Muhammad(s.a.w. w ) . Wamempa wasifa wa uzushi na uchawi kwa sababu aliwataka waachane na mizimu na maagizo ya kijahilia. Pia aliwaambia wajizuie na mambo ya haramu, uovu, kumwaga damu na kuwakandamiza wanyonge. Vile vile aliwataka wafanye mambo kielimu na kiuadilifu.

Hilo ndilo kosa la Mtume mtukufu kwao. Kama unavyoona, ni kosa la mjuzi mwenye ikhlasi mbele ya mjinga mhaini, na la tabibu mwenye kutoa nasaha mbele ya mgonjwa anayejiona ni mzima. Amesema kweli yule aliyesema: “Mjinga anajifanyia mwenyewe ambayo hata adui hawezi kumfanyia adui yake.”

Wala hatukuwapa vitabu wavisome, wala hatukuwatumia muonyaji kabla yako.

Walishirikisha ambapo kila kitu kinafahamisha kuwa Yeye ni mmoja, wakawaiga mababa na mababu bila ya kuwa na hoja ya wahyi ulioteremshwa au Nabii aliyetumwa wala athaari yoyote ya ilimu. Tazama Juz. 17 (22: 1-7) kifungu cha: ‘Mjadala wakijinga na upotevu‘.

Na walikadhibisha wale waliokuwa kabla yao. Na hawakufikilia hata sehemu ya kumi ya tulivyowapa hao. Wakawakadhibisha mitume wangu. basi je, kulikuwaje kukanya kwangu?

Kabla yenu walishirikisha watu wa uma nyingi, waliwakadhibisha mitume; kama manvyokadhibisha nyinyi, nao walikuwa na maendeleo na nguvu zaidi kuliko nyinyi, lakini pamoja na hivyo Mwenyezi Mungu aliwaadhibu kwa dhulma yao na ujeuri wao. Je, hampati funzo na kuhofia kuwafika yaliyowafika wao?

Umetangulia mfano wake katika Juz. 10 (9:70).

Sema: Hakika ninawapa mawaidha kwa jambo moja tu, kwamba msimame kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, wawili wawli na mmoja mmoja; kisha mfikiri. Mwenzenu hana wazimu. Hakuwa yeye ila ni muonyaji kwenu kabla ya kuwafikia adhabu kali.

Kusimama kwa ajili ya Mwenyezi Mungu ni kushikamana na haki na kuwa mbali na kuiga na kufuata matamanio. Wawili wawili ni mmoja kumrudia mwingine na kuuchunguza mwito na ujumbe. Mmoja mmoja ni kila mmoja kurudia akili yake na dhamiri na kufikiria yale aliyokuja nayo.

Maana ni kuwa ewe Muhammad! Waambie wale wanaokukadhibisha kwamba mimi ninawataka jambo moja tu, uadilifu wa kuchunga haki, mfikirie mkiwa pamoja na mkiwa mbalimbali kuhusu mwito wangu; kisha muangalie, je kweli mimi ni mzushi, mchawi au mwenda wazimu; kama mnavyodai? Au ni mbashiri, muonyaji na mshauri nasaha mwenye busara? Nabii mtukufu aliwapa Watu wa Kitabu mwito kama huu, pale alipowaambia:

قُلْ يَا أَهْلَ الْكِتَابِ تَعَالَوْا إِلَىٰ كَلِمَةٍ سَوَاءٍ بَيْنَنَا وَبَيْنَكُمْ أَلَّا نَعْبُدَ إِلَّا اللَّـهَ وَلَا نُشْرِكَ بِهِ شَيْئًا ﴿٦٤﴾

“Sema: Enyi watu wa Kitabu! Njooni kwenye neno la usawa baina yetu na baina yenu. Kwamba tusimwabudu yeyote ila Mwenyezi Mungu, wala tusimshirikishe na chochote.” Juz. 3 (3:64).

Hakuna jambo linalosadikisha zaidi dalili ya ukweli wa Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w. w ) , katika aliyokuja nayo, kuliko kuwapa mwito wa haki na uadilifu mahasimu.

Imepokewa Hadith kutoka kwa Ibn Abbas, kwamba Mtume(s.a.w. w ) siku moja alipanda Swafa na akasema: “Enyi wenzangu! Neno analolitumia anayetaka kuokoka ikiwa kuna jambo kubwa, basi makuraishi wakakusanyika. Akawaambia: “Mnaonaje kama nikiwaambia adui atawajia asubuhi au jioni, mtanisadiki?” Wakasema: “Ndio!” Akasema: “Hakika ninawaonya na adhabu kali. Abu Lahab akamjibu kwa neno la kukana... lakini hazikupita siku ila walisalimu amri wakiwa wanyonge.

Sema: Ujira niliowaomba ni wenu nyinyi. Sina ujira ila kwa Mwenyezi Mungu. Naye ni shahidi juu ya kila kitu.

Makusudio ya ‘ni wenu nyinyi’ ni kukana swali la ujira. Ni mfano wa kauli yake Mwenyezi Mungu:

فَمَا سَأَلْتُكُم مِّنْ أَجْرٍ إِنْ أَجْرِيَ إِلَّا عَلَى اللَّـهِ ﴿٧٢﴾

“...basi mimi siwaombi ujira. Ujira wangu hauko ila kwa Mwenyezi Mungu.” Juz. 11 (10:72).

Sema: Hakika Mola wangu hutoa haki, Mjuzi mno wa ghaibu.

Yaani anatoa wahyi kwa haki kuupeleka kwa mitume yake naye anajua vizuri nani wa kumpelekea ujumbe wake mkuu.

Sema: Haki imefika na batili hajitokezi wala hairudi.

Makusudio ya haki hapa ni risala ya Muhammad(s.a.w. w ) na batili ni shir- ki. Kujitokeza na kurudi ni kinaya cha kwisha kabisa batili na kutodhihiri athari yake katika Bara Arabu kabisa baada ya risala ya Muhammad(s.a.w. w ) .

Sema: Ikiwa nimepotea basi nimepotea kwa kuidhuru nafsi yangu tu, wala nyinyi madhara yangu hayawahusu.

Na ikiwa nimeongoka basi ni kwa sababu ya kuniletea wahyi Mola wangu.

Ni kwake Yeye peke yake fadhila za kuongoka kwangu; wala sijimilikii wala kummilikia mwingine isipokuwa yale aliyonimilikisha Mwenyezi Mungu.

Hakika Yeye ni Mwenye kusikia aliye karibu.

Mkisema anasikia, mkidhamiria au mkitenda atajua, kwa sababu yeye yuko karibu zaidi na nyinyi kuliko mshipa wa shingo.

وَلَوْ تَرَىٰ إِذْ فَزِعُوا فَلَا فَوْتَ وَأُخِذُوا مِن مَّكَانٍ قَرِيبٍ ﴿٥١﴾

51. Na lau ungeliwaona watakapofazaika, basi hapana pa kukimbilia, na watakamatwa mahala pa karibu.

وَقَالُوا آمَنَّا بِهِ وَأَنَّىٰ لَهُمُ التَّنَاوُشُ مِن مَّكَانٍ بَعِيدٍ ﴿٥٢﴾

52. Na watasema: Tumemwamini! Lakini watapata wapi kutoka huko mahali mbali?

وَقَدْ كَفَرُوا بِهِ مِن قَبْلُ وَيَقْذِفُونَ بِالْغَيْبِ مِن مَّكَانٍ بَعِيدٍ ﴿٥٣﴾

53. Na walikwishamkataa hapo zamani, wakiyatupilia mbali ya ghaibu kutoka mahali mbali.

وَحِيلَ بَيْنَهُمْ وَبَيْنَ مَا يَشْتَهُونَ كَمَا فُعِلَ بِأَشْيَاعِهِم مِّن قَبْلُ إِنَّهُمْ كَانُوا فِي شَكٍّ مُّرِيبٍ ﴿٥٤﴾

54. Na watawekewa kizuizi baina yao na hayo wanayoyatamani, kama walivyofanyiwa wenzao zamani. Hakika wao walikuwa katika shaka ya kutia wasiwasi.

WATAIPATA WAPI?

Aya 51 – 54

MAANA

Na lau ungeliwaona watakapofazaika, basi hapana pa kukimbilia, na watakamatwa mahala pa karibu.

Maneno yanaelekezwa kwa Muhammad(s.a.w. w ) , kukamatwa mahala pa karibu ni kinaya cha kuwa kwenye uweza wa Mwenyezi Mungu. Maana ni kuwa, ewe Muhammad(s.a.w. w ) lau utaona kesho hofu na adhabu, isiyokuwa na kimbilio, itakayowapata wale wanaokadhibisha utume wako, basi utastaajabu.

Hii ni kemeo kwa washirikina na tulizo kwa Bwana wa Mitume.

Na watasema tumemwamini! Lakini watapata wapi kutoka huko mahali mbali?

Wanayesema ‘tumemwamini’ ni Muhammad(s.a.w. w ) , kwa sababu amekwishatajwa kwenye Aya 46 ‘Mwenzenu hana wazimu.’

Maana ni kuwa, wale waliomkadhibisha Muhammad, watakapoiona adhabu watasema tumemwamini, lakini wataipata wapi imani hii au itawafaa nini huko mbali. Kwa sababu siku ya Kiyama ni siku ya hisabu na malipo sio siku ya imani na matendo.

Imam Ali(a.s) anasema:“Leo ni matendo si hisabu na kesho ni hisabu sio matendo... Enyi waja wa Mwenyezi Mungu! Jipimeni kabla ya kupimwa na mjihisabu kabla ya kuhisabiwa.”

Na walikwishamkataa hapo zamani. Muda wa kufaa imani umekwisha.

Wakiyatupilia mbali ya ghaibu kutoka mahali mbali.

Kutupilia mbali ni kusema bila ya ilimu, kutoka mahali mbali ni kinaya cha umbali wa kuliza na kutoamini kwao haki. Maana ni kuwa, wao walikuwa wakisema Muhammad ni mzushi, mchawi na mwendawazimu; wala hakuna Pepo au Moto. Waliyasema hayo kwa ujinga na bila ya dalili.

Na watawekewa kizuizi baina yao na hayo wanayoyatamani.

Wanatamani kuokoka na adhbau ya Jahannam, ndio wakakimbilia imani na toba, lakini baada ya kupita muda, basi watazidi majuto na machungu.

Kama walivyofanyiwa wenzao zamani.

Walikuwa na wanaofanana nao katika uma zilizopita; walimpinga Mola wao katika maisha ya dunia na kufazaika akhera. Wataambiwa:

قَالَ اخْسَئُوا فِيهَا وَلَا تُكَلِّمُونِ ﴿١٠٨﴾

“Tokomeeni humo, wala msinisemeshe.” Juz. 18: (23:108).

Hakika wao walikuwa katika shaka ya kutia wasiwasi ya ufufuo.

MWISHI WA SURA YA THELATHINI NA NNE: SURAT SABA

9

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MOJA

Sura Ya Thelathini na Tano: Surat Fatir. Imeshuka Makka. Ina Aya 45.

بِسْمِ اللَّهِ الرَّحْمَٰنِ الرَّحِيمِ

Kwa jina la Mwenyezi Mungu, Mwingi wa rehema, Mwenye kurehemu.

الْحَمْدُ لِلَّـهِ فَاطِرِ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ جَاعِلِ الْمَلَائِكَةِ رُسُلًا أُولِي أَجْنِحَةٍ مَّثْنَىٰ وَثُلَاثَ وَرُبَاعَ يَزِيدُ فِي الْخَلْقِ مَا يَشَاءُ إِنَّ اللَّـهَ عَلَىٰ كُلِّ شَيْءٍ قَدِيرٌ ﴿١﴾

1. Sifa njema ni za Mwenyezi Mungu Muumba wa mbingu na ardhi aliyewafanya Malaika kuwa wajumbe wenye mbawa mbili mbili, tatu tatu na nne nne. Huzidisha katika kuumba apendavyo. Hakika Mwenyezi Mungu ni mwenye uweza juu ya kila kitu.

مَّا يَفْتَحِ اللَّـهُ لِلنَّاسِ مِن رَّحْمَةٍ فَلَا مُمْسِكَ لَهَا وَمَا يُمْسِكْ فَلَا مُرْسِلَ لَهُ مِن بَعْدِهِ وَهُوَ الْعَزِيزُ الْحَكِيمُ ﴿٢﴾

2. Rehema ambayo Mwenyezi Mungu anawafungulia watu hakuna wa kuizuia na anayoizuia hakuna wa kuiachia isipokuwa Yeye, naye ni Mwenye nguvu, Mwenye hekima.

يَا أَيُّهَا النَّاسُ اذْكُرُوا نِعْمَتَ اللَّـهِ عَلَيْكُمْ هَلْ مِنْ خَالِقٍ غَيْرُ اللَّـهِ يَرْزُقُكُم مِّنَ السَّمَاءِ وَالْأَرْضِ لَا إِلَـٰهَ إِلَّا هُوَ فَأَنَّىٰ تُؤْفَكُونَ ﴿٣﴾

3. Enyi watu! Kumbukeni neema za Mwenyezi Mungu juu yenu. Je, yuko muumba mwingine asiyekuwa Mwenyezi Mungu anayewapa riziki kutoka mbinguni na kwenye ardhi? Hapana Mola ila Yeye basi mnageuzwa wapi?.

SIFA NJEMA NI ZA MWENYEZI MUNGU

Aya 1 – 3

MAANA

Sifa njema ni za Mwenyezi Mungu Muumba wa mbingu na ardhi aliyewafanya Malaika kuwa wajumbe wenye mbawa mbili mbili, tatu tatu na nne nne. Huzidisha katika kuumba apendavyo. Hakika Mwenyezi Mungu ni mwenye uweza juu ya kila kitu.

Mwenyezi Mungu amejisifu Yeye mwenyewe ili atufundishe jinsi ya kumsifu na kumshukuru. Aya inafahamisha kuwa katika Malaika kuna walio na mbawa mbili, wenye tatu na wenye nne na kwamba Yeye Mwenyezi Mungu Mtukufu huzidisha mbawa vile atakavyo. Haya na yanayofanana nayo yanaafikiana na uwezo wa Mwenyezi Mungu na akili haiyakatai. Yasiyokuwa hayo tunamwachia Mwenyezi Mungu (s.w.t), kwa vile sisi hatutaulizwa wala hayana uhusiano wowote na maisha yetu, wala hayana dalili na Aya au Hadith mutawatir.

Ninahofia wale wanaolazimisha kuzifanyia taawili nukuu za dini ziende sambamba na elimu ya kisasa waseme kuwa mbili mbili ni ishara ya ndege yenye injini mbili, tatu tatu ni yenye tatu, nne nne ni yenye nne na kuzidisha katika kuumba ni kuwa ndege zitakazokuja baadaye zenye injini nyingi.

Rehema ambayo Mwenyezi Mungu anawafungulia watu hakuna wa kuizuia na anayoizuia hakuna wa kuiachia isipokuwa Yeye, naye ni Mwenye nguvu, Mwenye hekima.

Makusudio ya rehema hapa sio mali tu; kama walivyosema baadhi ya wafasiri. Wala sio mali, afya na cheo; kama walivyosema wengine. Kwani mali inapelekea uasi na ukandamizaji. Tumewaona wengi wenye mali wamewageuza wengine wanyonge kuwa ni mashirika wanayoyamiliki na kuwageuza kuwa ni watumwa wao wanaowatumikia au wawe wakimbizi.

Afya nayo inampelekea mtu kwenye hatari. Ama cheo, ndio kabisa, aghlabu kinakuwa ni chombo cha dhulma na uadui. Elimu nayo mara nyingine inakuwa ni afadhali ujinga; kama vile elimu iliyotengeneza bomu la nyukilia na silaha za maangamizi.

Hapana! Makusudio ya rehema yake Mwenyezi Mungu Mtukufu, katika Aya hii, sio mali peke yake, wala afya pekee yake wala sio cheo na elimu tu. Isipokuwa makusudio ni huruma ya Mwenyezi Mungu, mwongozo wake wa heri na kinga yake ya shari.

Imam Ali(a.s) anasema:“Shida inapofika kikomo huja faraja na inapokaza sana minyororo ya dhiki hupatikana raha.”

Mara nyingi tumeshuhudia matatizo madogo yanazidi kuwa makubwa kila mwenyewe anavyojitahidi kuyatatua, na tunaona yale makubwa yanatatu- ka kwa wepesi au kwa haraka. Hakuna siri ya hilo ila matakwa ya Mwenyezi Mungu na rehema yake. Amesema kweli aliyesema: “Mtu anaweza kulala kwenye miba, pamoja na rehema ya Mwenyezi Mungu, akaamka kwenye tandiko. Na anaweza kulala kwenye hariri bila ya rehe- ma ya Mwenyezi Mungu akaamka kwenye miba.”[3] .

Enyi watu! Kumbukeni neema za Mwenyezi Mungu juu yenu. Je, yuko muumba mwingine asiyekuwa Mwenyezi Mungu anayewapa riziki kutoka mbinguni na kwenye ardhi? Hapana Mola ila Yeye basi mnageuzwa wapi?

Ukumbusho huu wa neema ya Mwenyezi Mungu na kwamba Yeye peke yake ndiye muumba na mwenye kuruzuku ni kuisisitiza Aya iliyotangulia: ‘Rehema ambayo Mwenyezi Mungu anawafungulia watu...’

Katika Nahjul-Balagha imeelezwa:“Mara ngapi Mwenyezi Mungu amewahusisha na neema yake na akwaunganisha na rehema yake. Mmekuwa uchi akawasitiri, mkafanya ya kuwaadhibu akawapa muda. Basi zikamilisheni neema za Mwenyezi Mungu kwa kuwa na subira ya kumtii na kujiweka mbali na maasi, kwani hakika kesho kuanzia leo ni karibu.”

وَإِن يُكَذِّبُوكَ فَقَدْ كُذِّبَتْ رُسُلٌ مِّن قَبْلِكَ وَإِلَى اللَّـهِ تُرْجَعُ الْأُمُورُ ﴿٤﴾

4. Na kama wakikukadhibisha, basi wamekwisha kadhibishwa Mitume kabla yako na mambo yote yatarudishwa kwa Mwenyezi Mungu.

يَا أَيُّهَا النَّاسُ إِنَّ وَعْدَ اللَّـهِ حَقٌّ فَلَا تَغُرَّنَّكُمُ الْحَيَاةُ الدُّنْيَا وَلَا يَغُرَّنَّكُم بِاللَّـهِ الْغَرُورُ ﴿٥﴾

5. Hakika ahadi ya Mwenyezi Mungu ni ya haki. Basi yasiwadanganye maisha ya dunia, wala mdanganyifu asiwadanganye juu ya Mwenyezi Mungu.

إِنَّ الشَّيْطَانَ لَكُمْ عَدُوٌّ فَاتَّخِذُوهُ عَدُوًّا إِنَّمَا يَدْعُو حِزْبَهُ لِيَكُونُوا مِنْ أَصْحَابِ السَّعِيرِ ﴿٦﴾

6. Hakika Shetani ni adui yenu, basi mfanyeni kuwa ni adui. Kwani yeye analiita kundi lake liwe katika watu wa motoni.

الَّذِينَ كَفَرُوا لَهُمْ عَذَابٌ شَدِيدٌ وَالَّذِينَ آمَنُوا وَعَمِلُوا الصَّالِحَاتِ لَهُم مَّغْفِرَةٌ وَأَجْرٌ كَبِيرٌ ﴿٧﴾

7. Wale ambao wamekufuru watakuwa katika adhabu kali na wale ambao wameamini watapata maghufira na malipo makubwa.

أَفَمَن زُيِّنَ لَهُ سُوءُ عَمَلِهِ فَرَآهُ حَسَنًا فَإِنَّ اللَّـهَ يُضِلُّ مَن يَشَاءُ وَيَهْدِي مَن يَشَاءُ فَلَا تَذْهَبْ نَفْسُكَ عَلَيْهِمْ حَسَرَاتٍ إِنَّ اللَّـهَ عَلِيمٌ بِمَا يَصْنَعُونَ ﴿٨﴾

8. Je, yule aliyepambiwa ubaya wa tendo lake akaliona ni jema - basi hakika Mwenyezi Mungu humpoteza amtakaye na humwongoa amtakaye. Basi roho yako isitoke kwa kuwasikitikia. Hakika Mwenyezi Mungu anayajua wanayoyafanya.

WALIKADHIBISHWA MITUME KABLA YAKO

Aya 4 – 8

MAANA

Na kama wakikukadhibisha, basi wamekwisha kadhibishwa Mitume kabla yako na mambo yote yatarudishwa kwa Mwenyezi Mungu, amlipe thawabu muumini mwenye kusubiri katika jihadi yake na amuadhibu mwenye kuikadhibisha haki kwa sababu ya kukadhibisha kwake.

Lengo la Aya hii ni kumpoza Mtume(s.a.w. w ) na kuwakaripia mahasimu na maadui wake. Umetangulia mfano wake katika Juz. 4 ( 3:183) na Juz. 17 (22:42).

Hakika ahadi ya Mwenyezi Mungu ni ya haki. Basi yasiwadanganye maisha ya dunia, wala mdanganyifu asiwadanganye juu ya Mwenyezi Mungu.

Makusudio ya ahadi hapa ni hisabu na malipo baada ya mauti. Udanganyifu wa dunia ni mali, jaha, wanawake, watoto na udanganyifu wa shetani. Umetangulia mfano wake katika Juz. 21 (31:33).

Hakika Shetani ni adui yenu, basi mfanyeni kuwa ni adui. Kwani yeye analiita kundi lake liwe katika watu wa motoni.

Shetani ametangaza waziwazi uadui wake na binadamu kwa kusema: “Kwa ulivyonipoteza, basi nitahakikisha ninawazaini hapa ardhini na nitawapoteza wote.” Juz. 14 (15:39).

Kundi lake ni wale wafuasi wake wanaosikiliza wasiwasi wake na udanganyifu wake. Mwenyezi Mungu (s.w.t) ametuhadharisha kumtii, kwa sababu mwito wake ni wa ufisadi na wa maangamizi, na Mwenyezi Mungu anatoa mwito wa kheri na rehema.

Wale ambao wamekufuru watakuwa katika adhabu kali na wale ambao wameamini watapata maghufira na malipo makubwa.

Kila mtu atakuwa na mwisho, mtamu au mchungu. Mwisho wa mwenye kukufuru na akafanya ufisadi ni Jahannam, makazi maovu; na mwisho wa mwenye kuamini na akatenda mema ni Pepo ambayo ni raha ya daima.

Je, yule aliyepambiwa ubaya wa tendo lake akaliona ni jema.

Kinahaw, hapa kuna maneno ya kukadiriwa kuwa: ‘ni kama ambaye hakupambiwa’ Hakuna mtu yoyote anayeishi bila ya falsafa na kuchukulia mfano wa juu; hata wale wanaokataa falsafa na mfano, huko kukataa kwao ndio falasafa yao na mfano wa juu. Ndio maana ikasemwa: Mwenye kukataa falsafa ndio amekuwa na falsafa.

Tofauti ni kuwa kuna yale anayeijengea falsafa yake kwenye majaribio na uchambuzi, mwengine anaijengea kwenye akili au dini na kuna yale anayeijengea kwenye dhati yake, mapendeleo yake na kupinga mengine yote.

Hafanyi utafiti wala kufikiri au kufanya uchambuzi, kwa sababu haamini akili wala dini; hakuna kitu isipokuwa kilicho kwenye rai yake na mapendeleo yake.

Mtu wa aina hii anaangalia nafsi zake kuwa ndio kipimo pekee cha haki heri na usawa, na kwamba yeye siku zote yuko sawa, hana upungufu wala hakosei.

Huyu tunaweza kumwita shahidi wa upumbavu na mwenye ghururi ya kuua. Mwenyezi Mungu (s.w.t) amemwashiria mtu huyu, katika Aya kadhaa; miongoni mwazo ni: “Sema je, tuwaambie wale wenye hasara mno ya vitendo?” Juz. 16 (18:103) Nyingine ni:

وَإِذَا قِيلَ لَهُمْ لَا تُفْسِدُوا فِي الْأَرْضِ قَالُوا إِنَّمَا نَحْنُ مُصْلِحُونَ ﴿١١﴾ أَلَا إِنَّهُمْ هُمُ الْمُفْسِدُونَ وَلَـٰكِن لَّا يَشْعُرُونَ ﴿١٢﴾

“Na wanapoambiwa msifanye ufisadi katika ardhi husema, Hakika sisi ni watengezaji tu. Ehe! Hakika wao ndio wafisadi, lakini hawatambui.” Juz. 1 (2:11-12).

Basi Hakika Mwenyezi Mungu humpoteza amtakaye na humwongoa amtakaye.

Hii ni sababu ya kauli yake Mwenyezi Mungu iliyotangulia ‘Je, yule aliyepambiwa ubaya wa tendo lake akaliona ni jema.’ Yaani kwamba Mwenyezi Mungu amemuweka kwenye upotevu na mwisho mbaya kwa sababu amefuata njia inayopelekea hilo; sawa na alivyomuweka kwenye kifo mwenye kunywa sumu na kufa maji aliyejitia baharini akiwa hajui kuogelea.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 13 (13:27) na Juz. 14 (16:93).

Basi roho yako isitoke kwa kuwasikitikia. Hakika Mwenyezi Mungu anayajua wanayoyafanya.

Usisikitike wala usihuzunike, ewe Muhammad, kwa wale ambao hawakuitikia mwito wako madamu wamefuata wenyewe njia ya uovu na ya maangamizi. Mwenyezi Mungu ameyadhibiti mambo yao, madogo na makubwa. Umetangulia mfano wake katika Juz. 15 (18:2).

وَاللَّـهُ الَّذِي أَرْسَلَ الرِّيَاحَ فَتُثِيرُ سَحَابًا فَسُقْنَاهُ إِلَىٰ بَلَدٍ مَّيِّتٍ فَأَحْيَيْنَا بِهِ الْأَرْضَ بَعْدَ مَوْتِهَا كَذَٰلِكَ النُّشُورُ ﴿٩﴾

9. Na Mwenyezi Mungu ndiye anayezituma pepo ziyatimue mawingu, nasi tukayafikisha kwenye nchi iliyokufa, tukaifufua ardhi baada ya kufa kwake. Ndio kama hivyo kufufuliwa.

مَن كَانَ يُرِيدُ الْعِزَّةَ فَلِلَّـهِ الْعِزَّةُ جَمِيعًا إِلَيْهِ يَصْعَدُ الْكَلِمُ الطَّيِّبُ وَالْعَمَلُ الصَّالِحُ يَرْفَعُهُ وَالَّذِينَ يَمْكُرُونَ السَّيِّئَاتِ لَهُمْ عَذَابٌ شَدِيدٌ وَمَكْرُ أُولَـٰئِكَ هُوَ يَبُورُ ﴿١٠﴾

10. Mwenye kutaka enzi basi enzi yote ni ya Mwenyezi Mungu. Kwake hupanda neno zuri na amali njema huuinua. Na wanaopanga njama za maovu watapata adhabu kali, na njama za hao zitaangamia.

وَاللَّـهُ خَلَقَكُم مِّن تُرَابٍ ثُمَّ مِن نُّطْفَةٍ ثُمَّ جَعَلَكُمْ أَزْوَاجًا وَمَا تَحْمِلُ مِنْ أُنثَىٰ وَلَا تَضَعُ إِلَّا بِعِلْمِهِ وَمَا يُعَمَّرُ مِن مُّعَمَّرٍ وَلَا يُنقَصُ مِنْ عُمُرِهِ إِلَّا فِي كِتَابٍ إِنَّ ذَٰلِكَ عَلَى اللَّـهِ يَسِيرٌ ﴿١١﴾

11. Na Mwenyezi Mungu amewaumba kutokana na udongo. Kisha tone, kisha akawafanya aina kwa aina. Na mwanamke yeyote hachukui mimba wala hazai ila kwa elimu yake. Wala hapewi umri mwenye umri mrefu wala hapunguziwi umri wake, ila yamo katika Kitabu. Hakika hayo kwa Mwenyezi Mungu ni mepesi.

AMALI NJEMA HUIPANDISHA

Aya 9 – 11

MAANA

Na Mwenyezi Mungu ndiye anayezituma pepo ziyatimue mawingu, nasi tukayafikisha kwenye nchi iliyokufa, tukaifufua ardhi baada ya kufa kwake. Ndio kama hivyo kufufuliwa.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 8 (7:57).

Mwenye kutaka enzi basi enzi yote ni ya Mwenyezi Mungu.

Enzi ni ya Mwenyezi Mungu na ya dini ya Mwenyezi Mungu hasa; na kwa mawili hayo ndio binadamu anakuwa na enzi. Mwenye kujienzi kwa asiyekuwa Mwenyezi Mungu atadhalilika. Ibn Arabi katika kitabu Futuhatul-Makkiyya, anasema:

“Enzi ya haki hasa ni kuwa hakuna Mola ila Yeye, na enzi ya Mtume wake ni kwa Mwenyezi Mungu, na enzi ya waumini ni kwa Mwenyezi Mungu na Mtume wake. Basi yanathibiti kwenye tanzu yale yaliyonayothibiti kwenye asili.”

Kudhalilika kwa waislamu leo kumetokana na kuwa wao wanajienzi kwa usiokuwa Uislamu. Hapo mwanzo walikuwa ni wachache kuliko sasa, lakini walikuwa ni wengi kwa kujienzi na jamii na umoja wao dhidi ya adui wa Mwenyezi Mungu na adui wao.

Kwake hupanda neno zuri na amali njema huiinua.

Kupanda maneno na kuinuka matendo kwenda kwake Mwenyezi Mungu Mtukufu ni kinaya cha kuyakubali na kuyalipa thawabu. Maneno mazuri ni yale yanayonufaisha, na vile vile amali njema.

Aya inaashiria kwamba sababu ya kuenziwa na kutukuzwa mbele ya Mwenyezi Mungu ni kauli na vitendo vinavyowanufaisha watu.

Na wanaopanga njama za maovu watapata adhabu kali, na njama za hao zitaangamia.

Kupanga njama za maovu ni kupanga kuwaudhi waumini na viongozi wema. Lakini njama zao zitaambulia patupu. Maana ya Aya hii ni kama kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: Na vitimbi viovu havimpati ila mwenyewe.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 17 (22:5).

Kisha akawafanya aina kwa aina, mweusi na mweupe na mume na mke.Na mwanamke yeyote hachukui mimba wala hazai, ila kwa elimu yake, kwa sababu yeye amekizunguka kila kitu.

Wala hapewi umri mwenye umri mrefu wala hapunguziwi umri wake, ila yamo katika Kitabu. Hakika hayo kwa Mwenyezi Mungu ni mepesi.

Kupunguziwa umri ni kuwa na umri mfupi; na kuwa katika Kitabu cha Mwenyezi Mungu ni kuwa katika ujuzi wa Mwenyezi Mungu. Maana kwa ujumla ni kuwa umri wote uko mikononi mwa Mwenyezi Mungu Mtukufu. Katika Nahjul-Balagha imeelezwa:

“Hampati neema katika dunia ila ni kwa kuimaliza nyingine; wala hapati umri mwenye umri miongoni mwenu ila ni kwa kuumaliza mwingine.” Tazama Juz. 4 (3:144 – 148) kifungu cha ‘Ajali haina kinga’.


5

6

7

8

9

10

11

12

13