TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI Juzuu 22

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI0%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: Qurani tukufu

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI

Mwandishi: Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya
: HASANI MWALUPA
Kundi:

Matembeleo: 19882
Pakua: 2185


Maelezo zaidi:

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 29 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 19882 / Pakua: 2185
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI Juzuu 22

Mwandishi:
Swahili

21

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI

Sura Ya Arubaini Na Nne: Surat Ad-Dukhan. Imeshuka Makka. Ina Aya 59.

بِسْمِ اللَّهِ الرَّحْمَٰنِ الرَّحِيمِ

Kwa jina la Mwenyezi Mungu Mwingi wa rehema Mwenye kurehemu.

حم ﴿١﴾

1. Haa Mim.

وَالْكِتَابِ الْمُبِينِ ﴿٢﴾

2. Naapa kwa Kitabu kinachobainisha.

إِنَّا أَنزَلْنَاهُ فِي لَيْلَةٍ مُّبَارَكَةٍ إِنَّا كُنَّا مُنذِرِينَ ﴿٣﴾

3. Hakika tumekiteremsha katika usiku uliobarikiwa. Hakika Sisi ni waonyaji.

فِيهَا يُفْرَقُ كُلُّ أَمْرٍ حَكِيمٍ ﴿٤﴾

4. Katika huo hubainishwa kila jambo la hikima.

أَمْرًا مِّنْ عِندِنَا إِنَّا كُنَّا مُرْسِلِينَ ﴿٥﴾

5. Ni amri itokayo kwetu. Hakika Sisi ndio wenye kutuma.

رَحْمَةً مِّن رَّبِّكَ إِنَّهُ هُوَ السَّمِيعُ الْعَلِيمُ ﴿٦﴾

6. Ni rehema itokayo kwa Mola wako. Hakika Yeye ni Mwenye kusikia, Mwenye kujua.

رَبِّ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ وَمَا بَيْنَهُمَا إِن كُنتُم مُّوقِنِينَ ﴿٧﴾

7. Mola wa mbingu na ardhi na vilivyomo kati yake, ikiwa nyinyi mna yakini.

لَا إِلَـٰهَ إِلَّا هُوَ يُحْيِي وَيُمِيتُ رَبُّكُمْ وَرَبُّ آبَائِكُمُ الْأَوَّلِينَ ﴿٨﴾

8. Yeye Hakuna mungu ila Yeye; anahuisha na anafisha - Mola wenu na Mola wa baba zenu wa mwanzo.

بَلْ هُمْ فِي شَكٍّ يَلْعَبُونَ ﴿٩﴾

9. Lakini wao wamo katika shaka wakicheza.

TUMEITEREMSHA USIKU ULIOBARIKIWA

Aya 1 – 9

MAANA

Haa Mim.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 1 (2:1)

Naapa kwa Kitabu kinachobainisha. Hakika tumekiteremsha katika usiku uliobarikiwa.

Umebarikiwa kwa kuteremkiwa na Qur’an. Tukiunganisha Aya hii na ile isemayo:

إِنَّا أَنزَلْنَاهُ فِي لَيْلَةِ الْقَدْرِ ﴿١﴾

“Hakika tumeiteremsha katika usiku wa heshima (Laylatul-qadr.) (97:1)

Na pia ile isemayo:

شَهْرُ رَمَضَانَ الَّذِي أُنزِلَ فِيهِ الْقُرْآنُ ﴿١٨٥﴾

“Ni mwezi wa Ramadhani ambao imeteremshwa ndani yake Qur’an.” Juz.2 (2:185),

Tukiunganisha Aya hizi tatu, tunapata maana kuwa usiku uliobarikiwa ni Laylatul-qadr, na kwamba uko ndani ya mwezi wa Ramadhani uliobarikiwa.

Katika Juz. 2 (2: 183-185), Tumesema kwamba mwanzo wa kushuka Qur’an ulikuwa kwenye Layaltul-qadr, sio kuwa ilishuka Qur’an yote usiku huo. Kwa maelezo zaidi rudia huko.

Hakika Sisi ni Waonyaji wa adhabu kali kwa atakayeasi na kufanya ufisadi katika ardhi. Onyo hili limekuja katika Qur’an iliyoteremshwa kwenye moyo wa Muhammad(s.a.w. w ) .

Katika usiku huu hubainishwa kila jambo la hikima. Ni amri itokayo kwetu.

Wafasiri wametofautiana kuhusu ‘jambo la hikima.’ wengi wameonelea ni kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) anagawanyia waja wake riziki na muda wa kifo katika usiku huu. Pia anasamehe makosa mengi kwa anayemtaka.

Wengine wakasema kuwa Makusudio ya jambo la hikima ni ubainifu wa kila jambo la dini uliokuja katika Qur’an. Lakini ikumbukwe Mwenyezi Mungu amesema katika huu, na hakusema katika hii. Ubainifu zaidi utaku- ja katika Juz. 30 (97).

Hakika Sisi ndio wenye kutuma. Ni rehema itokayo kwa Mola wako.

Yaani Mwenyezi Mungu alimtuma Muhammad kuwa ni rehema kwa viumbe vyote; kama ilivyoelezwa katika Juz. 17 (21:107).

Hakika Yeye ni Mwenye kusikia Mwenye kujua.

Anasikia kauli na anajua yaliyo kwenye nia.

Mola wa mbingu na ardhi na vilivyomo kati yake, ikiwa nyinyi mna yakini.

Mwenye akili akiuangalia ulimwengu kwa mtazamo safi na kutilia maanani, atashuhudia kwa ikhlasi na yakini kwamba Mwenyezi Mungu ndiye mmiliki wa ulimwengu na vilivyomo ndani yake na kwambaYeye Hakuna mungu ila Yeye; anahuisha na anafisha.

Hakuna yeyote anayeleta uhai isipokuwa Yeye. Na muda ukifika hakuna kinachoweza kuusogeza mbali wala karibu.

Mola wenu na Mola wa baba zenu wa mwanzo . Vipi basi mnaabudu mizimu na kumtii shetani badala ya Mwenyezi Mungu?

Lakini wao wamo katika shaka wakicheza.

Wametia shaka ya kutumwa Muhammad(s.a.w. w ) pamoja na dalili na ubainifu na wanafanya mchezo na mwisho wao na yale wanayotakiwa kuyafanya.

فَارْتَقِبْ يَوْمَ تَأْتِي السَّمَاءُ بِدُخَانٍ مُّبِينٍ ﴿١٠﴾

10. Basi ingoje siku ambayo mbingu italeta moshi ulio dhahiri.

يَغْشَى النَّاسَ هَـٰذَا عَذَابٌ أَلِيمٌ ﴿١١﴾

11. Utakaowafunika watu. Hii ni adhabu chungu!

رَّبَّنَا اكْشِفْ عَنَّا الْعَذَابَ إِنَّا مُؤْمِنُونَ ﴿١٢﴾

12. Mola wetu! Tuondolee adhabu hii. Hakika tutaamini.

أَنَّىٰ لَهُمُ الذِّكْرَىٰ وَقَدْ جَاءَهُمْ رَسُولٌ مُّبِينٌ ﴿١٣﴾

13. Kutafaa nini kukumbuka kwao? Na alikwishawafikia Mtume mwenye kubainisha.

ثُمَّ تَوَلَّوْا عَنْهُ وَقَالُوا مُعَلَّمٌ مَّجْنُونٌ ﴿١٤﴾

14. Kisha wakamgeuzia uso, na wakasema: Amefunzwa, mwenda wazimu.

إِنَّا كَاشِفُو الْعَذَابِ قَلِيلًا إِنَّكُمْ عَائِدُونَ ﴿١٥﴾

15. Hakika tutaiondoa adhabu kidogo, (lakini) nyinyi kwa yakini mtarudia.

يَوْمَ نَبْطِشُ الْبَطْشَةَ الْكُبْرَىٰ إِنَّا مُنتَقِمُونَ ﴿١٦﴾

16. Siku tutakayowashika kwa mashiko makubwa, hakika sisi ni wenye kutesa.

وَلَقَدْ فَتَنَّا قَبْلَهُمْ قَوْمَ فِرْعَوْنَ وَجَاءَهُمْ رَسُولٌ كَرِيمٌ ﴿١٧﴾

17. Na hakika kabla yao tuliwajaribu watu wa Firauni, na aliwafikia Mtume Mtukufu.

أَنْ أَدُّوا إِلَيَّ عِبَادَ اللَّـهِ إِنِّي لَكُمْ رَسُولٌ أَمِينٌ ﴿١٨﴾

18. Nipeni waja wa Mwenyezi Mungu; kwa hakika mimi kwenu ni Mtume mwaminifu.

وَأَن لَّا تَعْلُوا عَلَى اللَّـهِ إِنِّي آتِيكُم بِسُلْطَانٍ مُّبِينٍ ﴿١٩﴾

19. Na msijitukuze mbele ya Mwenyezi Mungu; hakika mimi nitawaletea uthibitisho ulio wazi.

وَإِنِّي عُذْتُ بِرَبِّي وَرَبِّكُمْ أَن تَرْجُمُونِ ﴿٢٠﴾

20. Nami najikinga kwa Mola wangu na Mola wenu, ili msinirujumu.

وَإِن لَّمْ تُؤْمِنُوا لِي فَاعْتَزِلُونِ ﴿٢١﴾

21. Na ikiwa hamniamini, basi jitengeni nami.

SIKU AMBAYO MBINGU ITALETA MOSHI

Aya 10 – 21

MAANA

Basi ingoje siku ambayo mbingu italeta moshi ulio dhahiri, utakaowafunika watu.

Maneno yanatoka kwa Mwenyezi Mungu kwenda kwa Nabii wake mtukufu Muhammad(s.a.w. w ) akimwahidi kumkubalia dua yake. Hiyo ni baada ya Makuraishi kuzidi sana kumuudhi Mtume(s.a.w. w ) . Akawaombea dua mbaya, akasema:“Ewe Mola wangu wafanyie miaka kama ya Yusuf.” Basi mvua ikakatika na ardhi ikawa kame, makuraishi wakapatwa na njaa mpaka wakawa wanakula mifupa na mizoga. Kutokana na njaa mtu alikuwa akiona kama moshi mbinguni.

Wakasema: Hii ni adhabu chungu! Mola wetu! Tuondolee adhabu hii. Hakika tutaamini.

Walimjia Mtume(s.a.w. w ) na kumwambia: Muombe Mwenyezi Mungu (s.w.t) atuondolee adhabu hii na sisi tutaamini risala yako.

Kutafaa nini kukumbuka kwao? Na alikwishawafikia Mtume mwenye kubainisha. Kisha wakamgeuzia uso, na wakasema: Amefunzwa, mwendawazimu.

Walitoa ahadi ya kuwaidhika na kukumbuka kama Mwenyezi Mungu atawaondolea adhabu, lakini wao hawatubii wala hawatekelezi ahadi. Kwani hawakushuhudia dalili za Tawhid, lakini pamoja na hayo wakamshirikisha Mwenyezi Mungu? Je, hakuwajia Mtume na hoja zilizo wazi wakamkadhibisha? Wakasema ni mwendawazimu, anafundishwa baadhi ya matamshi na jinni au mtu, kisha anakuja kutusomea?

Hakika tutaiondoa adhabu kidogo, (lakini)nyinyi kwa yakini mtarudia.

Makusudio ya adhabu hapa ni adhabu ya kahati na njaa. Kurudia, ni kuvunja ahadi kwa kurudia makosa. Maana ni kuwa tutawaondolea shida waliyo nayo, katika baadhi ya wakati, lakini sisi tunajua wazi kuwa watavunja ahadi. Lakini hiyo ni katika upande wa kutimiza na kuondoa visababu.

Siku tutakayowashika kwa mashiko makubwa, hakika sisi ni wenye kutesa.

Hili ni tishio kuwa Mwenyezi Mungu siku ya kiyama atawashika kwa adhabu ya kufedhehesha kutokana na uasi na jeuri yao.

Kwa ufupi ni kuwa makuraishi walimuudhi Nabii(s.a.w. w ) , naye akawombea dua mbaya. Ilipowapata shida walimkimbilia Mtume na kumwahidi kutubia, lakini walivunja ahadi baada ya kupata faraja, ndio Mwenyezi Mungu (s.w.t) akawatishia kwa Jahannam na makazi mabaya.

Na hakika kabla yao tuliwajaribu watu wa Firauni, na aliwafikia Mtume Mtukufu.

Yaani kabla ya makuraishi. Maana ni kuwa Mwenyezi Mungu aliwapa mtihani watu wa Firauni kwa neema na kumakinishwa katika ardhi; kama walivyopewa mtihani makuraishi kwa kuondolewa adhabu. Mwenyezi Mungu alimtuma Musa kwa watu wa Firauni; kama alivyomtuma Muhammad kwa makuraishi. Wote wakaasi amri ya Mwenyezi Mungu.

Na Musa akamwambia Firauni na watu wake:Nipeni waja wa Mwenyezi Mungu; kwa hakika mimi kwenu ni Mtume mwaminifu.

Firauni alikuwa akiwakandamiza wana wa Israil kwa kuwachinja watoto wa kiume na kuwabakisha wa kike kwa ajili ya utumishi. Kwa hiyo Musa akamtaka Firauni amwachie ili aende nao anapotaka. Mfano wake ni kauli yake Mwenyezi Mungu:

فَأَرْسِلْ مَعَنَا بَنِي إِسْرَائِيلَ وَلَا تُعَذِّبْهُمْ ﴿٤٧﴾

“Basi tuwachie wana wa Israil wala usiwaadhibu.” Juz. 16 (20:47).

Na msijitukuze mbele ya Mwenyezi Mungu; hakika mimi nitawaletea uthibitisho ulio wazi.

Haya ni maneno ya Musa kwa watu wa Firauni. Maana ni kuwa msijiweke juu ya twaa ya Mwenyezi Mungu, kwani mimi nina hoja za kutosha za kuthibitisha haki.

Nami najikinga kwa Mola wangu na Mola wenu, ili msinirujumu.

Najilinda na ninakimbilia kwake ikiwa mtanikusudia ubaya.

Na ikiwa hamniamini, basi jitengeni nami. Achaneni na mimi, kama hamtaki kunisadiki na kuitikia mwito wangu.

فَدَعَا رَبَّهُ أَنَّ هَـٰؤُلَاءِ قَوْمٌ مُّجْرِمُونَ ﴿٢٢﴾

22. Ndipo akamwomba Mola wake kuwa watu hawa ni wakosefu.

فَأَسْرِ بِعِبَادِي لَيْلًا إِنَّكُم مُّتَّبَعُونَ ﴿٢٣﴾

23. Basi nenda na waja wangu usiku. Hakika mtafuatwa.

وَاتْرُكِ الْبَحْرَ رَهْوًا إِنَّهُمْ جُندٌ مُّغْرَقُونَ ﴿٢٤﴾

24. Na iache bahari imetulia, hakika wao ni jeshi litakalozamishwa.

كَمْ تَرَكُوا مِن جَنَّاتٍ وَعُيُونٍ ﴿٢٥﴾

25. Mabustani mangapi, na chemchem ngapi waliziacha!

وَزُرُوعٍ وَمَقَامٍ كَرِيمٍ ﴿٢٦﴾

26. Na mimea na mahala pa fahari!

وَنَعْمَةٍ كَانُوا فِيهَا فَاكِهِينَ ﴿٢٧﴾

27. Na neema walizokuwa wakijistareheshea!

كَذَٰلِكَ وَأَوْرَثْنَاهَا قَوْمًا آخَرِينَ ﴿٢٨﴾

28. Ndivyo hivyo! na tukawarithisha haya watu wengine.

فَمَا بَكَتْ عَلَيْهِمُ السَّمَاءُ وَالْأَرْضُ وَمَا كَانُوا مُنظَرِينَ ﴿٢٩﴾

29. Mbingu na ardhi hazikuwalilia; wala hawakupewa muda.

وَلَقَدْ نَجَّيْنَا بَنِي إِسْرَائِيلَ مِنَ الْعَذَابِ الْمُهِينِ ﴿٣٠﴾

30. Na hakika tuliwaokoa wana wa Israili katika adhabu ya kuwadhalilisha.

مِن فِرْعَوْنَ إِنَّهُ كَانَ عَالِيًا مِّنَ الْمُسْرِفِينَ ﴿٣١﴾

31. Ya Firauni. Hakika yeye alikuwa jeuri katika wenye kupituka mipaka.

وَلَقَدِ اخْتَرْنَاهُمْ عَلَىٰ عِلْمٍ عَلَى الْعَالَمِينَ ﴿٣٢﴾

32. Na hakika tuliwachagua kwa ujuzi kuliko walimwengu wengine.

وَآتَيْنَاهُم مِّنَ الْآيَاتِ مَا فِيهِ بَلَاءٌ مُّبِينٌ ﴿٣٣﴾

33. Na tukawapa katika ishara zenye majaribio yaliyo wazi.

WATU HAWA NI WAKOSEFU

Aya 22 – 33

MAANA

Ndipo akamwomba Mola wake kuwa watu hawa ni wakosefu.

Musa alikata tamaa na Firauni na watu wake, ndipo akawaombea mabaya na akasema: “Ewe Mwenyezi Mungu waharakishie maangamizi duniani kwa sababu ya kufuru yao.” Mwenyezi Mungu akamwitikia dua yake na kumwambia:Basi nenda na waja wangu usiku. Hakika mtafuatwa.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) alimwamrisha atoke Misri yeye na wana wa Israil usiku na akamjulisha kuwa Firauni na watu wake watawafuata.

Na iache bahari imetulia, hakika wao ni jeshi litakalozamishwa.

Fuata njia ya baharini, ukishavuka upande wa pili, wewe iwache kama ilivyo, kwa sababu jeshi la adui litaingia na wataangamia wote.

Mabustani mangapi, na chemchem ngapi waliziacha! Na mimea na mahala pa fahari! Na neema walizokuwa wakijistareheshea! Ndivyo hivyo! na tukawarithisha haya watu wengine.

Watu wa Firauni walikuwa katika starehe za vyakula na vinywaji, wana utawala, makasri, mito na matunda. Mwenyezi Mungu akawatumia Musa kuwalingania kwenye uadilifu na kuacha ufisadi katika nchi, lakini hawakumwitikia mlinganiaji wa Mwenyezi Mungu. Basi akawaangamiza na akawarithisha watu ambao hawakuwa na uhusiano wowote na wao.

Sheikh Al-Maraghi anasema akifasiri Aya hii: “Wakati fulani wasyria walichukua Misr na wakati mwingine ikachukuliwa na wababilon na pia wahabeshi. Kisha wafursi, wayunani (wagiriki), waroma, na waarabu. Vile vile utawala wa Altoulenion, Alikhchidip, Fatimid, Ayyubids, Mamluk, Uturuki, Ufaransa na Uingereza. Na sisi hivi sasa tunapigana ili kuwatoa katika nchi yetu ili tuweze kumakinika na uhuru wa chi yetu.”

Sheikh huyu alikuwa katika zama za mfalme Faruk Bin Fuad. Nasi tunaunganisha maneno yake kwa kusema: Hivi sasa Uzayuni umepora Sinai na ukanda wa mashariki katika mfereji wa Suez, kwa msaada U.S.A. kambi mpya ya ukoloni.

Na wamisri wanajitahidi na kupigana kuwatoa wavamizi kwenye ardhi yao. Haya ndio maisha ya jihadi na mapigano. Mtu kufa na bunduki mkononi akipigania nchi yake na heshima yake ni bora zaidi kuliko kuishi maisha ya udhalili na utwevu.

Mbingu na ardhi hazikuwalilia.

Hiki ni kinaya cha kutowapa umuhimu watu wa Firauni pale Mwenyezi Mungu alipowagharikisha baharini,wala hawakupewa muda; bali Mwenyezi Mungu aliharakisha maangamizi yao duniani.

Na hakika tuliwaokoa wana wa Israili katika adhabu ya kuwadhalilisha ambayo ni kuuawa watoto wao wa kiume na kutumikishwa wanawake wao na mabinti zao na pia kudhalilishwa wanaume kwa kazi za sulubu

Ya Firauni. Hakika yeye alikuwa jeuri katika wenye kupituka mipakaya kila ufisadi, uasi na kiburi. Na hakika tuliwachagua kwa ujuzi kuliko walimwengu wengine.

Mwenyezi Mungu (s.w.t), katika Kitabu chake, amewasifu kwa sifa mbaya wana wa Israil, akasajili

makosa makubwa waliyoyafanya; kama vile usaliti, kuifanyia jeuri haki na kula mali kwa dhulma.

Vile vile amewasifu kwa ukafiri, dhulma na akawalaani katika Aya kadhaa na kuwatishia kwa adhabu kali.

Kwa maana hii ndio wafasiri wakakongamana kuwa makusudio ya walimwengu, katika Aya hii na mfano wake, ni walimwengu wa zama zao si kila zama.

Katika Juz. 1 (2:47-48) tulisema kuwa Mwenyezi Mungu aliwafadhilisha juu ya watu wa zama hizo kwa vile tu Mwenyezi Mungu aliwatuma mitume wengi kutokana na wao. Hivi sasa tumepata wazo kutokana na Aya tuliyo nayo kuwa makusudio ya walimengu ni Firauni na wale walioukubali uungu wake na wala sio watu wote wa wakati ule. Siri ya kufadhilishwa huko ni kuwa waisrail hawakumwabudu Firauni kama wamisri waliotangulia.

Na tukawapa katika ishara zenye majaribio yaliyo wazi.

Makusudio ya ishara hapa ni miujiza; kama kupasuka bahari, kufunikwa na kiwingu, kuteremshiwa Manna na Salwa na kububujika maji kutoka kwenye jiwe. Na Makusudio ya majaribio ni neema. Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema:

وَنَبْلُوكُم بِالشَّرِّ وَالْخَيْرِ فِتْنَةً وَإِلَيْنَا تُرْجَعُونَ ﴿٣٥﴾

“Na tutawajaribu kwa mtihani wa shari na heri na kwetu mtarejeshwa.” Juz. 17 (21:35).

22

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI

إِنَّ هَـٰؤُلَاءِ لَيَقُولُونَ ﴿٣٤﴾

34. Hakika hawa wanasema:

إِنْ هِيَ إِلَّا مَوْتَتُنَا الْأُولَىٰ وَمَا نَحْنُ بِمُنشَرِينَ ﴿٣٥﴾

35. Hapana ila kufa kwetu mara ya kwanza tu, wala sisi hatu- fufuliwi.

فَأْتُوا بِآبَائِنَا إِن كُنتُمْ صَادِقِينَ ﴿٣٦﴾

36. Basi warudisheni baba zetu, ikiwa mnasema kweli.

أَهُمْ خَيْرٌ أَمْ قَوْمُ تُبَّعٍ وَالَّذِينَ مِن قَبْلِهِمْ أَهْلَكْنَاهُمْ إِنَّهُمْ كَانُوا مُجْرِمِينَ ﴿٣٧﴾

37. Je, wao ni bora au watu wa Tubbaa’ na walio kuwa kabla yao? Tuliwaangamiza. Hakika hao walikuwa wakosefu.

وَمَا خَلَقْنَا السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضَ وَمَا بَيْنَهُمَا لَاعِبِينَ ﴿٣٨﴾

38. Na hatukuziumba mbingu na ardhi na vilivyomo kati yake kwa mchezo.

مَا خَلَقْنَاهُمَا إِلَّا بِالْحَقِّ وَلَـٰكِنَّ أَكْثَرَهُمْ لَا يَعْلَمُونَ ﴿٣٩﴾

39. Hatukuviumba ila kwa haki. Lakini wengi wao hawajui.

إِنَّ يَوْمَ الْفَصْلِ مِيقَاتُهُمْ أَجْمَعِينَ ﴿٤٠﴾

40. Hakika siku ya Upambanuzi ni wakati uliowekwa kwa wao wote.

يَوْمَ لَا يُغْنِي مَوْلًى عَن مَّوْلًى شَيْئًا وَلَا هُمْ يُنصَرُونَ ﴿٤١﴾

41. Siku ambayo rafiki hatamfaa rafiki yake kwa chochote, wala hawatanusuriwa.

إِلَّا مَن رَّحِمَ اللَّـهُ إِنَّهُ هُوَ الْعَزِيزُ الرَّحِيمُ ﴿٤٢﴾

42. Isipokuwa yule ambaye Mwenyezi Mungu atamrehemu Hakika Yeye ndiye Mwenye nguvu, Mwenye kurehemu.

JE, WAO NI BORA AU WATU WA TUBBAA’

Aya 34 – 42

MAANA

Hakika hawa wanasema: Hapana ila kufa kwetu mara ya kwanza tu, wala sisi hatufufuliwi.

‘Hawa’ ni ishara ya washirikina wa Makka, walisema hakuna uhai wala ufufuo baada ya mauti na wakatoa hoja kwa kusema:Basi warudisheni baba zetu, ikiwa mnasema kweli. Wao hawaamini kuwa Mwenyezi Mungu anaweza kuwafufua wafu ila wakiona hilo kwa macho; wakasahau umbile la kwanza, kwamba yule aliyeleta mwanadamu, aliyekuwa hayuko, ndiye huyo huyo mwenye uweza wa kufufua mifupa iliyosagika.

Je, wao ni bora au watu wa Tubbaa’ na walio kuwa kabla yao? Tuliwaangamiza. Hakika hao walikuwa wakosefu.

Watubba’ walikuwa na dola yenye nguvu katika Yemen, na walikuwa na mali na hali nzuri zaidi kuliko makuraishi. Walipoasi amri ya Mola wao, Mwenyezi Mungu aliwakamata na akawaangamiza; kama alivyowaangamiza watu wa Nuh, A’d na Thamud kutokana na kufuru na ufisadi. Lau wangelizingatia wangeliona na wakaamini, lakini wao ni watu wasiofahamu.

Na hatukuziumba mbingu na ardhi na viliomo kati yake kwa mchezo. Hatukuviumba ila kwa haki.

Mwenyezi Mungu ni mwenye hikima na mwenye hikima hawezi kufanaya mchezo. Kwa hiyo haumbi kitu ila kwa masilahi yanayorudia kuumba. Lengo la kuumbwa mtu ni kuishi maisha mema ya milele yasiyokuwa na mwisho. Kwa hiyo basi hakuna budi kuweko na ufufuo; vinginevyo itakuwa kuumbwa mtu ni kwa mchezo tu. Tazama Juz. 21 (31:33-34) kifungu cha: ‘Kwa nini Mungu akamuumba mtu?’

Lakini wengi wao hawajui kwamba Mwenyezi Mungu ameumba ulimwengu na vilivyomo ndani yake kwa hikima na malengo sahihi.

Hakika siku ya Upambanuzi ni wakati uliowekwa kwa wao wote.

Siku ya upambanuzi ni siku ya Kiyama ambayo Mwenyezi Mungu atawakusanya watu wote kwa ajili ya kuangalia hisabu na malipo. Kuwekewa wakati kwa wote ni ahadi ya huko kukusanywa kwa hisabu na malipo.

Siku ambayo rafiki hatamfaa rafiki yake kwa chochote, wala hawatanusuriwa.

Si cheo, mali, nasabu, urafiki wala chochote kitakachoweza kufaa siku hiyo, isipokuwa matendo mema. Hayo peke yake ndiyo yatakayoweza kusaidia mbele ya Mwenyezi Mungu.

Isipokuwa yule ambaye Mwenyezi Mungu atamrehemu, lakini Mwenyezi Mungu atamrehemu yule anayestahiki kurehemiwa; kama yule mwenye vitangulizi vya kumkurubisha kwa muumba wake.

Hakika Yeye ndiye Mwenye nguvu, Mwenye kurehemu. Hakuna mwenye kunusuru wala kurehemu kesho isipokuwa Mwenyezi Mungu. Yeye ni mwenye nguvu na rehema, viumbe wananyenyekea nguvu yake na wanahitajia rehema yake.

إِنَّ شَجَرَتَ الزَّقُّومِ ﴿٤٣﴾

43. Hakika Mti wa Zaqqum.

طَعَامُ الْأَثِيمِ ﴿٤٤﴾

44. Ni chakula cha mwenye dhambi.

كَالْمُهْلِ يَغْلِي فِي الْبُطُونِ ﴿٤٥﴾

45. Kama mafuta mazito, hutokota matumboni,

كَغَلْيِ الْحَمِيمِ ﴿٤٦﴾

46. Kama kutokota kwa maji ya moto.

خُذُوهُ فَاعْتِلُوهُ إِلَىٰ سَوَاءِ الْجَحِيمِ ﴿٤٧﴾

47. Mkamateni na mburuzeni mpaka katikati ya Jahannamu!

ثُمَّ صُبُّوا فَوْقَ رَأْسِهِ مِنْ عَذَابِ الْحَمِيمِ ﴿٤٨﴾

48. Kisha mmwagieni juu ya kichwa chake adhabu ya maji yanayochemka.

ذُقْ إِنَّكَ أَنتَ الْعَزِيزُ الْكَرِيمُ ﴿٤٩﴾

49. Onja! Hakika wewe ndiye mwenye nguvu, mtukufu!

إِنَّ هَـٰذَا مَا كُنتُم بِهِ تَمْتَرُونَ ﴿٥٠﴾

50. Hakika haya ndiyo mliyokuwa mkiyatilia shaka.

إِنَّ الْمُتَّقِينَ فِي مَقَامٍ أَمِينٍ ﴿٥١﴾

51. Hakika wenye takua watakuwa katika mahali pa amani.

فِي جَنَّاتٍ وَعُيُونٍ ﴿٥٢﴾

52. Katika mabustani na chem-chem.

يَلْبَسُونَ مِن سُندُسٍ وَإِسْتَبْرَقٍ مُّتَقَابِلِينَ ﴿٥٣﴾

Watavaa hariri nyepesi na hariri nzito wakikabiliana.

كَذَٰلِكَ وَزَوَّجْنَاهُم بِحُورٍ عِينٍ ﴿٥٤﴾

54. Ndio kama hivyo! na tutawaoza mahurilaini

يَدْعُونَ فِيهَا بِكُلِّ فَاكِهَةٍ آمِنِينَ ﴿٥٥﴾

55. Humo watataka kila aina ya matunda, na wakae kwa amani.

لَا يَذُوقُونَ فِيهَا الْمَوْتَ إِلَّا الْمَوْتَةَ الْأُولَىٰ وَوَقَاهُمْ عَذَابَ الْجَحِيمِ ﴿٥٦﴾

56. Humo hawataonja mauti ila mauti yale ya kwanza, na atawalinda na adhabu ya Jahannamu.

فَضْلًا مِّن رَّبِّكَ ذَٰلِكَ هُوَ الْفَوْزُ الْعَظِيمُ ﴿٥٧﴾

57. Ni fadhila zitokazo kwa Mola wako. Huko ndiko kufuzu kukubwa.

فَإِنَّمَا يَسَّرْنَاهُ بِلِسَانِكَ لَعَلَّهُمْ يَتَذَكَّرُونَ ﴿٥٨﴾

58. Basi tumeifanya nyepesi hii kwa ulimi wako, ili wapate kukumbuka.

فَارْتَقِبْ إِنَّهُم مُّرْتَقِبُونَ ﴿٥٩﴾

59. Basi ngoja tu, na wao wanangoja.

CHAKULA CHA MWENYE DHAMBI NA CHA MWENYE TAKUA

Aya 43 – 59

MAANA

Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kuwataja wakosefu, katika Aya iliyotangulia, na kwamba ahadi yao ni siku ya Kiyama, sasa anataja hali yao itakavyokuwa, kama ifuatavyo:

Hakika Mti wa Zaqqum, Ni chakula cha mwenye dhambi, ambaye dhambi zake na makosa yake yalikithiri duniani. Mwenyezi Mungu (s.w.t) ameyasifu matunda ya mti huu kuwa ni kama mafuta mazito, hutokota matumboni kama kutokota kwa maji ya moto.

Sio mbali kuwa hiki ni kinaya cha uchungu wa adhabu na ukali wake. Mulla Sadra anasema katika Al-asfar: Mti wa Zaqqum ni itikadi za ubatilifu na tabia mbaya zinazompeleka mtu kwenye moto. Baadhi ya mapokezi yanaeleza kuwa ubakhili ni mti miongoni mwa miti ya Motoni na ukarimu ni mti miongoni mwa miti ya Peponi.

Mkamateni na mburuzeni mpaka katikati ya Jahannamu!

Yaani wataambiwa Malaika wa motoni mburuzeni hadi katikati ya Jahannam,kisha mmwagieni juu ya kichwa chake adhabu ya maji yanayochemka.

Hii inaashiria kuwa kwenye Jahannam kuna matunda, hamamu na mavazi, lakini yote yanatokana na moto.

Onja! Hakika wewe ndiye mwenye nguvu, mtukufu! Hakika haya ndiyo mliyokuwa mkiyatilia shaka.

Malaika wa adhabu watamwambia taghuti mwenye dhambi: wewe ulipinga siku ya ufufuo na ukadai kuwa ni mkubwa na mtukufu, basi hivi sasa onja malipo ya kujitukuza kwako na kiburi chako.

Kadiri ninavyotia shaka, lakini siwezi kutia shaka yoyote kuwa wale wanaopora mali za watu na kuzitengenezea silaha za maangamizi kwa ajili ya kuwaua wasiokuwa na hatia, wakiwemo wanawake na watoto, na wala wasione haki wala uadilifu isipokuwa yale wanayoyataka na kuyatamani, sitii shaka kabisa kwamba hawa wanastahiki aina hii ya adhabu; bali wanastahiki zaidi ya adhabu hii kama ingeliokuwako. Tazama Juz. 13 (14:46-52), kifungu cha ‘Jahannam na silaha za maangamizi.’

Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kubainisha hali za wakosefu, sasa anaashiria hali za wenye takua siku ya Kiyama, kwa Aya zinazofuatia:

Hakika wenye takua watakuwa katika mahali pa amani, hawatakuwa na hofu wala kuhuzunika. Katika mabustani na chemchem, wakistarehe kadiri watakavyo.

Watavaa hariri nyepesi na hariri nzito wakikabiliana.

Nguo zao ni hariri laini na nzito na watakaa kwenye viti wakielekeana wao kwa wao, wakibarizi huku wanashukuru kwa kukumbuka neema ya Mwenyezi Mungu na radhi zake.

Ndio kama hivyo! na tutawaoza mahurulaini, ambao hajawagusa mtu kabla yao wala jinni.

Humo watataka kila aina ya matunda, na wakae kwa amani.

Watataka matunda bila ya kuhofia kuwa yataisha.

Humo hawataonja mauti ila mauti yale ya kwanza, na Mwenyezi Munguatawalinda na adhabu ya Jahannamu.

Kila mtu atakufa mauti ya kwanza na baadae ataguria Peponi au Motoni, hakuna kufa huko, lakini kufa ni bora sana kuliko uhai katikati ya Jahannam.

Ni fadhila zitokazo kwa Mola wako. Huko ndiko kufuzu kukubwa.

Kuna kufuzu gani kukubwa zaidi ya kuokoka na adhabu ya moto na ghad- habu ya Mwenyezi Mungu?

Basi tumeifanya nyepesi hii kwa ulimi wako, ili wapate kukumbuka.

Iliyofanywa nyepesi ni Qur’an. Wanaotakiwa kukumbuka ni waarabu na ulimi ni wa Mtume. Maana ni kuwa tumeiteremsha Qur’an kwa kiarabu ili waarabu wanufaike na mafunzo yake na mawaidha.

Basi ngoja tu, na wao wanangoja.

Ngoja kidogo ewe Muhammad, utaona mwisho utakuwa wako. Wao wanakuduia ufikwe na mabaya, lakini: “Ameaangamia mwenye kuduia na amerudi utupu mwenye kuzua na mwenye kuigeukia haki ameangamia,” kama anavyosema Imam Ali.(a.s) .

MWISHO WA SURA YA ARUBAINI NA NNE: SURAT AD-DUKHAN

23

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI

Sura Ya Arubaini Na Tano: Surat Al-Jaathiya, Pia inaitwa Sura ya Sharia. Imeshuka Makka. Ina Aya 37.

بِسْمِ اللَّهِ الرَّحْمَٰنِ الرَّحِيمِ

Kwa jina la Mwenyezi Mungu Mwingi wa rehema Mwenye kurehemu.

حم ﴿١﴾

1. Haa mim.

تَنزِيلُ الْكِتَابِ مِنَ اللَّـهِ الْعَزِيزِ الْحَكِيمِ ﴿٢﴾

2. Uteremsho wa Kitabu umetoka kwa Mwenyezi Mungu, Mwenye nguvu, Mwenye hikima.

إِنَّ فِي السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ لَآيَاتٍ لِّلْمُؤْمِنِينَ ﴿٣﴾

3. Hakika katika mbingu na ardhi kuna Ishara kwa Waumini.

وَفِي خَلْقِكُمْ وَمَا يَبُثُّ مِن دَابَّةٍ آيَاتٌ لِّقَوْمٍ يُوقِنُونَ ﴿٤﴾

4. Na katika umbo lenu na katika wanyama aliowatawanya zimo ishara kwa watu wenye yakini.

وَاخْتِلَافِ اللَّيْلِ وَالنَّهَارِ وَمَا أَنزَلَ اللَّـهُ مِنَ السَّمَاءِ مِن رِّزْقٍ فَأَحْيَا بِهِ الْأَرْضَ بَعْدَ مَوْتِهَا وَتَصْرِيفِ الرِّيَاحِ آيَاتٌ لِّقَوْمٍ يَعْقِلُونَ ﴿٥﴾

5. Na kupishana usiku na mchana, na riziki anayoiteremsha Mwenyezi Mungu kutoka mbinguni, na kwayo akaifufua ardhi baada ya kufa kwake. Na mabadiliko ya upepo, ni Ishara kwa watu wenye akili.

تِلْكَ آيَاتُ اللَّـهِ نَتْلُوهَا عَلَيْكَ بِالْحَقِّ فَبِأَيِّ حَدِيثٍ بَعْدَ اللَّـهِ وَآيَاتِهِ يُؤْمِنُونَ ﴿٦﴾

6. Hizo ni Ishara za Mwenyezi Mungu tunakusomea kwa haki Basi hadithi gani watakayoiamini baada ya Mwenyezi Mungu na Ishara zake?

KATIKA MBINGU NA ARDHI KUNA ISHARA KWA WAUMINI

Aya 1 – 6

MAANA

Haa miim.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 1 (2:1).

Uteremsho wa Kitabu umetoka kwa Mwenyezi Mungu, Mwenye nguvu, Mwenye hikima.

Makusudio ya kitabu ni Qur’an, na yote kuanzia mwanzo wake hadi mwisho wake ni wahyi kutoka kwa Mwenyezi Mungu si kwa mwenginewe. Mwenye Ruhul-bayan anasema: “Wasifu wa Mwenyezi Mungu kuwa Mwenye nguvu, hapa unafahamisha kuwa Qur’an ni muujiza unaomshinda nguvu kila mwenye kuipinga. Na wasifu wake kuwa ni mwenye hikima unajulisha kuwa Qur’an ina hikima ya hali ya juu yenye kunufaisha. Hakuna mwenye shaka kuwa Qur’an ni muujiza unaomshinda kila mwenye kupingana nayo na kwamba hiyo ni chimbuko la hekima na kianzio chake.”

Kisha Mwenyezi Mungu (s.w.t) akaishiria kwenye dalili ya hisia zinazotamka kuweko kwake na utukufu wake; miongoni mwazo ni:

Hakika katika mbingu na ardhi kuna Ishara kwa waumini.

Yaani kwa anayetaka kuamini haki kwa kuwa ni haki. Makusudio ya Ishara hapa ni yale yanayovumbuliwa na akili kama vile nidhamu ya ulimwengu na sera yake kwenye desturi isiyokuwa na mabadiliko wala mageuzi. Lau si uthabiti wake isingeliwezekana kuipima na kufaidika nayo; hatimae ilimu ya sayari isingelikuwa na athari yoyote.

Na katika umbo lenu na katika wanyama aliowatawanya zimo ishara kwa watu wenye yakini.

Mwenye kutaka kujua kwa yakini kuweko Mwenyezi Mungu, naafikirie na kujitaamali yeye mwenyewe na katika kila kilicho na uhai, je, atapata kiungo hata kimoja kisicho na kazi au silika yoyote isiyokuwa na hikima?

Hii inafahamisha kwa dalili mkataa ya kuweko utashi na azma, ikiwa hatumuoni huyo mwenye utashi na azma basi tunaona athari yake kwa macho kabisa, kwa hiyo basi imani yetu kwa mambo ya ghaibu inategemea hisia na kuona.

Na kupishana usiku na mchana.

Mara nyingi Mwenyezi Mungu (s.w.t) ameashiria kuhitalifiana usiku na mchana ili kuizindua akili kwenye siri za ajabu katika mzunguko wa ardhi, kwa vile ndio sababu ya kuja usiku baada ya mchana.

Yote yaliyosemwa kuhusu sababu za mzunguko wa ardhi hiyo yenyewe au kando ya jua na sababu nyinginezo, zote zinaishia kwenye matakwa ya muumbaji wa kwanza na uwezo wake na hekima yake. Ni jambo lisiloingilika akilini kuwa chimbuko la maajabu yote haya liwe ni mada pofu inayohukumiwa na sadfa, bila ya mpangilio, wala makusdio au lengo!

Na riziki anayoiteremsha Mwenyezi Mungu kutoka mbinguni, na kwayo akaifufua ardhi baada ya kufa kwake.

Makusudio ya riziki hapa ni kila kitu chenye athari katika uhai; kama vile maji na joto la jua nk. Ambayo ndani yake kuna ufahamisho wa kuweko muumba wa viliomo mbinguni na katika ardhi. Kwa sababu vyote hivyo vimepatikana kwa lengo na hekima iliyo sahihi.

Na mabadiliko ya upepo, kusi na kaskazi, matlai na umande na joto na baridini Ishara kwa watu wenye akili.

Yote hayo na mengineyo ni dalili mkataa ya utashi wa mwenye ujuzi na hikima

Hizo ni Ishara za Mwenyezi Mungu tunakusomea kwa haki.

Hivi ndivyo Mwenyezi Mungu anavyoweka mbele ya akili ushahidi na dalili za hisia za kumjua muumba na uweza wake.

Basi hadithi gani watakayoiamini baada ya Mwenyezi Mungu na Ishara zake?

Ambaye hakunufaika na ubainifu wa Mwenyezi Mungu na kutokinai na dalili zake basi hakuna hoja yoyote itakayomfaa. Maana ya Aya hii yamekaririka mara nyingi katika Kitabu cha Mwenyezi Mungu; miongoni mwazo ni ile iliyo katika Juz. 2 (2:164).

Katika Nahjul-balagha kuna maelezo haya: “Katika kuumba kwake, kikubwa, kidogo, kizito, chenye nguvu na hafifu, ni sawa tu. Vile vile mbingu hewa, upepo na maji. Hebu angalia jua, mwezi, mimea, miti, maji, na jiwe. Pia kupishana huu usiku na mchana, kububujika hizi bahari, kukithiri milima, urefu wa vilele hivi na kutofautiana lugha na lahaja. Ole wake mwenye kumkataa mkadiriaji na akamkana mpangiliaji. Wanajifikiria ni kama mimea isiyokuwa na mkulima wala kuwa kutofautiana sura zao kusiwe na mtengenezaji. Hawana hoja na wanayodai wala uhakiki kwa waliyoyasikia. Je, jengo linaweza kuwa bila ya fundi? Au hatia bila ya kuweko mkosaji?”

وَيْلٌ لِّكُلِّ أَفَّاكٍ أَثِيمٍ ﴿٧﴾

7. Ole wakekila mtunga uongo mwenye dhambi!

يَسْمَعُ آيَاتِ اللَّـهِ تُتْلَىٰ عَلَيْهِ ثُمَّ يُصِرُّ مُسْتَكْبِرًا كَأَن لَّمْ يَسْمَعْهَا فَبَشِّرْهُ بِعَذَابٍ أَلِيمٍ ﴿٨﴾

8. Anayesikia Aya za Mwenyezi Mungu akisomewa, kisha anang’ng’ania huku akijivuna, kama kwamba hakuzisikia. Basi mbashirie adhabu chungu!

وَإِذَا عَلِمَ مِنْ آيَاتِنَا شَيْئًا اتَّخَذَهَا هُزُوًا أُولَـٰئِكَ لَهُمْ عَذَابٌ مُّهِينٌ ﴿٩﴾

9. Na anapokijua kitu katika Aya zetu hukifanyia mzaha. Hao ndio watakaokuwa na adhabu ya kufedhehesha.

مِّن وَرَائِهِمْ جَهَنَّمُ وَلَا يُغْنِي عَنْهُم مَّا كَسَبُوا شَيْئًا وَلَا مَا اتَّخَذُوا مِن دُونِ اللَّـهِ أَوْلِيَاءَ وَلَهُمْ عَذَابٌ عَظِيمٌ ﴿١٠﴾

10. Nyuma yao ipo Jahannamu. Na waliyoyachuma hayatawafaa kitu, wala mawalii waliowashika badala ya Mwenyezi Mungu. Na watapata adhabu kubwa.

هَـٰذَا هُدًى وَالَّذِينَ كَفَرُوا بِآيَاتِ رَبِّهِمْ لَهُمْ عَذَابٌ مِّن رِّجْزٍ أَلِيمٌ ﴿١١﴾

11. Hii ni mwongozo. Na wale waliozikataa Ishara za Mola wao watapata adhabu yenye maumivu iliyo chungu.

اللَّـهُ الَّذِي سَخَّرَ لَكُمُ الْبَحْرَ لِتَجْرِيَ الْفُلْكُ فِيهِ بِأَمْرِهِ وَلِتَبْتَغُوا مِن فَضْلِهِ وَلَعَلَّكُمْ تَشْكُرُونَ ﴿١٢﴾

12. Mwenyezi Mungu ndiye aliyeifanya bahari iwatumikie, ili humo yapite majahazi kwa amri yake, na ili mtafute fadhila yake, na mpate kushukuru.

وَسَخَّرَ لَكُم مَّا فِي السَّمَاوَاتِ وَمَا فِي الْأَرْضِ جَمِيعًا مِّنْهُ إِنَّ فِي ذَٰلِكَ لَآيَاتٍ لِّقَوْمٍ يَتَفَكَّرُونَ ﴿١٣﴾

13. Na amefanya viwatumikie vilivyomo mbinguni na vilivyo katika ardhi, vyote kutoka kwake. Hakika katika hayo zimo Ishara kwa watu wanaotafakari.

قُل لِّلَّذِينَ آمَنُوا يَغْفِرُوا لِلَّذِينَ لَا يَرْجُونَ أَيَّامَ اللَّـهِ لِيَجْزِيَ قَوْمًا بِمَا كَانُوا يَكْسِبُونَ ﴿١٤﴾

14. Waambie walioamini wawasamehe wale wasiozitaraji siku za Mwenyezi Mungu, ili awalipe kwa waliyokuwa wakiyachuma.

مَنْ عَمِلَ صَالِحًا فَلِنَفْسِهِ وَمَنْ أَسَاءَ فَعَلَيْهَا ثُمَّ إِلَىٰ رَبِّكُمْ تُرْجَعُونَ ﴿١٥﴾

15. Anayetenda mema basi anajitendea mwenyewe, na anyetenda uovu basi ni juu yake; kisha mtarudishwa kwa Mola wenu.

OLE WAKE KILA MTUNGA UONGO MWENYE DHAMBI!

Aya 7- 15

MAANA

Ole wake kila mtunga uongo mwenye dhambi! Anayesikia Aya za Mwenyezi Mungu akisomewa, kisha anang’ng’ania huku akijivuna, kama kwamba hakuzisikia. Basi mbashirie adhabu chungu! Na anapokijua kitu katika Aya zetu hukifanyia mzaha.

Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kuweka wazi dalili za kihisia zinazofahamisha, kwa mkato na kwa yakini, kuweko Mwenyezi Mungu Mtukufu kwa mwenye akili, na kusema kuwa asiyeziamini hizo basi hawezi kuamini dalili nyingine zozote, sasa anampa onyo na kumwahidi yule asiyezitilia manani dalili hizi na kunufaika nazo kwa kumwita mzushi mwenye dhambi na kumpa kiaga cha adhabu chungu.

Vile vile ammempa sifa ya mpinzani wa haki na kujitia ukubwa, na kwamba hakutosha na hayo bali ameidharau na kuifanyia mzaha haki.

Kafiri huyu mwenye kuidharau haki na watu wake hana tofauti, siku ya hisabu, na yule anayeiamini haki kwa kauli tu, bila ya kufanya, na kwa nadharia tu bila ya matendo. Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema:

وَلَا تَكُونُوا كَالَّذِينَ قَالُوا سَمِعْنَا وَهُمْ لَا يَسْمَعُونَ ﴿٢١﴾

“Wala msiwe kama wale wanaosema: tumesikia; na kumbe hawasikii;” yaani hawakubali wala hawatendi. Juz.9 (8:21).

Imam Ali(a.s ) anasema:“Mwenye busara ni yule anayesikia akatafakari, akachunguza akaona na akanufaika na mazingatio.”

Hao ndio watakaokuwa na adhabu ya kufedhehesha. Nyuma yao ipo Jahannamu. Na waliyoyachuma hayatawafaa kitu, wala mawalii waliowashika badala ya Mwenyezi Mungu. Na watapata adhabu kubwa.

‘Hao’ ni kila mtunga uwongo. Makusudio ya waliyoyachuma ni watoto wao, mali zao na vyeo vyao. Na waliyoyashika ni masanamu na mizimu yao.

Maana ni kuwa wale walioifanyia kiburi haki na wakaidharau, marejeo yao ni kuingia Jahannam; hakuna atakayewaokoa na adhabu hiyo – si masanamu wala watoto wala mali au vyeo.

Hii ni mwongozo.

‘Hii’ ni ishara ya Qur’an. Hakuna mwenye shaka kuwa Qur’an ni mwongozo kwa mwenye kuiamini na ni nguvu kwa mwenye kuitegemea.

Na wale waliozikataa Ishara za Mola wao watapata adhabu yenye maumivu iliyo chungu.

Makusudio ya Ishara hapa ni dalili za kilimwengu za kuwako Mwenyezi Mungu na ukuu wake. Neno adhabu, maumivu na uchungu, yanarudiana au yanakaribiana. Lengo la kukaririka huku ni kusisitiza adhabu atakayokutana nayo mzushi mwenye dhambi ambaye ameikalia juu haki na kuidharau.

Mwenyezi Mungu ndiye aliyeifanya bahari iwatumike, ili humo yapite majahazi kwa amri yake, na ili mtafute fadhila yake, na mpate kushukuru.

Fadhila za Mwenyezi Mungu ziko bara, baharini na angani. Miongoni mwa neema zake Mwenyezi Mungu Mtukufu baharini ni chakula, chumvi, mawe ya thamani, mawasiliano, matembezi na hata michezo nk. Umetangulia mfano wake katika Aya kadhaa, ikiwemo Juz.15 (17:66) na Juz.21 (30:46).

Na amefanya viwatumikie viliomo mbinguni na vilivyo katika ardhi, vyote kutoka kwake. Hakika katika hayo zimo Ishara kwa watu wanaotafakari.

Katika ulimwengu huu mpana kuna manufaa na nyenzo zisizokuwa na idadi. Pamoja na kuendelea kwa elimu katika zama zetu hizi, lakini nyenzo zilizofichikana ni nyingi zaidi kuliko zilizobainika, lakini Mwenyezi Mungu amempa mtu maandalizi kamili ya kugundua nguvu na nyenzo zilizomo ulimwenguni na kufaidika nazo, kama atakuwa na mweleko wa elimu ya kibinadamu sio ya kibiashara, na pia kama atafanya juhudi kubwa.

Neno ‘Vyote,’ linaashiria kwamba mtu anayo maandalizi ya kumwezesha kufika mwezini na kwengineko. Tazama Juz. 20 (29:19-27) kifungu cha ‘Qur’an na fikra.’ Pia Umetangulia mfano wake katika Juz. 21 (31:20)

Waambie walioamini wawasamehe wale wasiozitaraji siku za Mwenyezi Mungu, ili awalipe kwa waliyokuwa wakiyachuma.

Makusudio ya siku za Mwenyezi Mungu hapa ni siku za adhabu yake. Wale wasiozitarajia siku za Mwenyezi Mungu ni washirikina wa kiarabu. Mwenyezi Mungu (s.w.t) alimwamrisha Mtume wake awaombe waumini wawasamehe washirikina ubaya waliowafanyia na wawalipize wema. Mwenyezi Mungu ndiye mwenye hisabu ya muovu na malipo yake.

Anayetenda mema basi anajitendea mwenyewe, na anyetenda uovu basi ni juu yake; kisha mtarudishwa kwa Mola wenu.

Maana yako wazi. Umetangulia mfano wake katika Juz. 7 (6:104) na kwa Herufi zake katika Juz. 24 (41:46).