TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI Juzuu 22

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI0%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: Qurani tukufu

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI

Mwandishi: Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya
: HASANI MWALUPA
Kundi:

Matembeleo: 19902
Pakua: 2195


Maelezo zaidi:

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 29 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 19902 / Pakua: 2195
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI Juzuu 22

Mwandishi:
Swahili

3

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI

وَيَوْمَ الْقِيَامَةِ تَرَى الَّذِينَ كَذَبُوا عَلَى اللَّـهِ وُجُوهُهُم مُّسْوَدَّةٌ أَلَيْسَ فِي جَهَنَّمَ مَثْوًى لِّلْمُتَكَبِّرِينَ ﴿٦٠﴾

60. Na Siku ya Kiyama utawaona wale ambao wamemsingizia uwongo Mwenyezi Mungu nyuso zao zimesawijika. Je! Si katika Jahannamu makazi ya wanaotakabari?

وَيُنَجِّي اللَّـهُ الَّذِينَ اتَّقَوْا بِمَفَازَتِهِمْ لَا يَمَسُّهُمُ السُّوءُ وَلَا هُمْ يَحْزَنُونَ ﴿٦١﴾

61. Na Mwenyezi Mungu atawaokoa walio na takua kwa ajili ya kufuzu kwao. Hapana uovu utao wagusa, wala hawatahuzunika.

اللَّـهُ خَالِقُ كُلِّ شَيْءٍ وَهُوَ عَلَىٰ كُلِّ شَيْءٍ وَكِيلٌ ﴿٦٢﴾

62. Mwenyezi Mungu Mungu ndiye Muumba wa kila kitu; na Yeye ndiye Mlinzi juu ya kila kitu.

لَّهُ مَقَالِيدُ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ وَالَّذِينَ كَفَرُوا بِآيَاتِ اللَّـهِ أُولَـٰئِكَ هُمُ الْخَاسِرُونَ ﴿٦٣﴾

63. Anazo funguo za mbingu na ardhi. Na wale ambao wamezikataa Ishara za Mwenyezi Mungu, hao ndio wenye hasara.

قُلْ أَفَغَيْرَ اللَّـهِ تَأْمُرُونِّي أَعْبُدُ أَيُّهَا الْجَاهِلُونَ ﴿٦٤﴾

64. Sema: Je! Mnaniamrisha nimwabudu asiyekuwa Mwenyezi Mungu, enyi majahili?

وَلَقَدْ أُوحِيَ إِلَيْكَ وَإِلَى الَّذِينَ مِن قَبْلِكَ لَئِنْ أَشْرَكْتَ لَيَحْبَطَنَّ عَمَلُكَ وَلَتَكُونَنَّ مِنَ الْخَاسِرِينَ ﴿٦٥﴾

65. Na kwa hakika umepewa wahyi na waliokuwa kabla yako: Bila ya shaka ukishirikisha amali zako zitapomoka, na lazima utakuwa miongoni mwa wenye kuhasirika.

بَلِ اللَّـهَ فَاعْبُدْ وَكُن مِّنَ الشَّاكِرِينَ ﴿٦٦﴾

66. Bali muabudu Mwenyezi Mungu tu, na uwe miongoni mwa wenye kushukuru.

وَمَا قَدَرُوا اللَّـهَ حَقَّ قَدْرِهِ وَالْأَرْضُ جَمِيعًا قَبْضَتُهُ يَوْمَ الْقِيَامَةِ وَالسَّمَاوَاتُ مَطْوِيَّاتٌ بِيَمِينِهِ سُبْحَانَهُ وَتَعَالَىٰ عَمَّا يُشْرِكُونَ ﴿٦٧﴾

67. Na hawakumkadiria Mwenyezi Mungu haki ya kadiri yake. Na Siku ya Kiyama ardhi yote itakuwa mkononi mwake, na mbingu zitakunjwa katika mkono wake wa kuume. Ametakasika na Ametukuka na wanayomshirikisha nayo.

WALIOMSINGIZIA UWONGO MWENYEZI MUNGU

Aya 60 – 67

MAANA

Na Siku ya Kiyama utawaona wale ambao wamemsingizia uwongo Mwenyezi Mungu nyuso zao zimesawijika. Je! Si katika Jahannamu makazi ya wanaotakabari?

Kila anayemnasibishia Mwenyezi Mungu yale asiyokuwa na ujuzi nayo basi atakuwa amemsingizia Mwenyezi Mungu; iwe amemnasibishia kuwa na washirika, mke na mtoto, au kazi za Mwenyezi Mungu; kama kuingilia utume ukhalifa, hukumu au kutoa fatwa kwa jina la dini.

Aliulizwa Imam Ja’far As-sadiq(a.s) kuhusiana na maana ya Aya hii, akasema:“Mwenye kudai uimamu usiotokana na Mwenyezi Mungu, atakuwa amemsingizia uongo Mwenyezi Mungu” Muulizaji akasema: Hata kama ni Alawi. Imam akasema: hata kama ni Alawi. Muulizaji akaendelea kuuliza: Hata kama ni Fatimi, Imam akasema:Hata kam ni Fatimi.”

Malipo ya mwenye kumzulia Mwenyezi Mungu na Mtume wake, ni kufufuliwa akiwa na uso uliosawijika, katika kundi lililoandaliwa Jahannam na Mwenyezi Mungu, makazi mabaya kabisa.

Kauli yake Mwenyezi Mungu ‘wanotakabari’ baada ya kauli yake ‘wale ambao wamemsingizia Mwenyezi Mungu,’ inaashiria kuwa kumsingizia Mwenyezi Mungu ni kiburi.

Na Mwenyezi Mungu atawaokoa waliona takua kwa ajili ya kufuzu kwao. Hapana uovu utaowagusa, wala hawatahuzunika.

Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kuwahadharisha wasingiziaji na moto wa Jahannam, sasa anawabashiria wakweli na wenye takua, kuokoka na moto na kila ubaya. Zaidi ya hayo hawatakuwa na huzuni wala majuto kwa yale waliyoyakosa duniani.

Mwenyezi Mungu ndiye Muumba wa kila kitu.

Kila kilichoko akiwemo mtu, mnyama mimea na mawe, kinafahamisha kuweko kwa Mwenyezi Mungu kwa sura ya ufundi wa mjengaji kutokana na jengo lenyewe na aliyekitengeneza na kila jingo

Na Yeye ndiye Mlinzi juu ya kila kitu.

Yaani ni mwenye kusimamia, kwa sababu kila kitu kimepatikana kwa uweza wa Mwenyezi Mungu na kitabaki chini ya uangalizi wake mpaka atakapotaka, vinginevyo itakua hakina maana.

Anazo funguo za mbingu na ardhi.

Funguo ni kinaya cha kuwa Mwenyezi Mungu ni mzingatiaji wa ulimwen- gu na ni mjuzi wa yote yanayopita humo kuanzia chembe ndogo hadi sayari kubwa: “Na ziko kwake funguo za ghaibu” Juz. 7 (6:59).

Na wale ambao wamezikataa Ishara za Mwenyezi Mungu, hao ndio wenye hasara.

Makusudio ya ishara za Mwenyezi Mungu ni ulimwengu na nidhamu yake ya ajabu ambayo lau itakoseka kwa kiasi cha unywele tu, basi utaharabika.

Maana ya kuzikataa ishara za Mwenyezi Mungu ni kutozikubali dalili za nidhamu hii kuwa kuna aliyezipanga na uhandisi na mhandisi wake.

Wakadhibishaji wamezitia hasara akili zao na dalili hizi, kwa sababu zimepofuka na hisia. Vile vile wamezitia hasara nafasi zao na akhera, kwa vile wamezichagulia ukafiri na inadi; na Jahannam yatakuwa ndio makazi ya kila kafiri mwenye inadi.

Sema: Je! Mnaniamrisha nimwabudu asiyekuwa Mwenyezi Mungu, enyi majahili?

Kuna mapokezi yanayosema kuwa washirikina walimjia Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w. w ) na kusema: Tutakupa mali itakayokufanya uwe tajiri zaidi ya wote katika Makka na tutakuoza msichana unayemtaka, kwa sharti ya kuwa uache mwito wako. Ndio ikashuka Aya hii.

Iwe riwaya hii ni sahihi au la lakini inafafanua zaidi na Aya hii. Ni vizuri tudokoe maneno yafuatayo kutoka katika makala ya marehemu Mustafa Sadiq Ar-rafii, yenye kichwa cha maneno ‘Dirhamu na dinari’: “Nimewaona baadhi ya mafakihi wakitoa mawaidha na kuwaambia watu halali na haramu, lakini hakika wanawafanyia maskhara vile anavyomfanyia maskhara mwizi anayempa mawaidha mwizi mwingine na kumwambia usiibe.”

Hali hii pia iko kwa waandishi wanasiasa na wengineo wanaobeba nembo za uzalendo na ubinadamu. Ar-rafii anaendelea kusema: “Mwenye kutukuza dirhamu na dinari (pesa) huwa anautukuza unafiki, tamaa na uwongo… Hakika haiba ya Uislamu ni kujitolea maisha sio kupupia maisha, na kuwasaidia waumini sio kuwafanyia uadui. Na utajiri unapimwa kwa inavyofanya kazi mali sio kukusanya mali.”

Na kwa hakika umepewa wahyi na waliokuwa kabla yako: Bila ya shaka ukishirikisha amali zako zitapomoka, na lazima utakuwa miongoni mwa wenye kuhasirika.

Makusudio ya kupomoka (kuanguka) amali ni kukosa thawabu. Kushirikisha ni muhali kwa mitume, lakini kukadiria muhali sio muhali. Zaidi ya hayo ni kuwa kutahadharishwa kitu hakufahamishi kuwa aliyehadharishwa anadhaniwa kuwa atafanya alilohadharishwa.

Maana ni kuwa Mwenyezi Mungu hakubali ibada ya yeyote ila ikiwa imetakata na kuwa safi kwa ajili ya Mwenyezi Mungu tu. Mwenye kumwabudu Mwenyezi Mungu pamoja na mwingine, basi hastahiki thawabu; hata akiwa ni kama mtume. Tumefafanua kuanguka amali katika Juz. 2 (2:216 – 218), kifungu cha ‘Kupomoka.’

Bali muabudu Mwenyezi Mungu tu, na uwe miongoni mwa wenye kushukuru.

Kwa dhahiri hii ni amri, lakini kwa hakika ni kuelezea kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w. w ) haabudu isipokuwa Mwenyezi Mungu tu wala hamshukuru yeyote asiyekuwa yeye. Imekuja kwa tamko la amri kutanabahisha waja kuwa ibada na shukrani ni lazima iwe kwa ajili ya Mwenyezi Mungu mmoja tu.

Zaidi ya hayo Mwenyezi Mungu (s.w.t) mara nyinyi huwaambia wote kwa kumtuma Mtume wake mtukufu: “Na kwamba elekeza uso wako kwenye dini safi, wala usiwe miongoni mwa washirikina.” Juz. 11 (10:105), “Basi simama sawa sawa kama ulivyoamrishwa wewe...” Juz. 12 (11:112) na “Na simamisha Swala katika ncha mbili za mchana...” Juz. 12 (11:114).

Na hawakumkadiria Mwenyezi Mungu haki ya kadiri yake kwa sababu wao wamemkataa na kuamini masanamu na pesa.

Na Siku ya Kiyama ardhi yote itakuwa mkononi mwake, na mbingu zitakunjwa katika mkono wake wa kuume.

Hiki ni kinaya cha ukuu wa Mwenyezi Mungu na uweza wake; na kwamba mbingu na ardhi na vyote viliomo baina yake vinanyenyekea amri yake.

Ametakasika na Ametukuka na wanayomshirikisha nayo.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) ametakasika na kila shirki na wanayoyasema kuwa ana mkono wa kuume. Na pia ametakasika na ufananisho wanaomsifu nao majahili.

وَنُفِخَ فِي الصُّورِ فَصَعِقَ مَن فِي السَّمَاوَاتِ وَمَن فِي الْأَرْضِ إِلَّا مَن شَاءَ اللَّـهُ ثُمَّ نُفِخَ فِيهِ أُخْرَىٰ فَإِذَا هُمْ قِيَامٌ يَنظُرُونَ ﴿٦٨﴾

68. Na itapulizwa parapanda, wazimie waliomo mbinguni na waliomo ardhini, ila ambaye Mwenyezi Mungu amemtaka. Kisha itapulizwa mara nyengine. Hapo watainuka wawe wanangojea.

وَأَشْرَقَتِ الْأَرْضُ بِنُورِ رَبِّهَا وَوُضِعَ الْكِتَابُ وَجِيءَ بِالنَّبِيِّينَ وَالشُّهَدَاءِ وَقُضِيَ بَيْنَهُم بِالْحَقِّ وَهُمْ لَا يُظْلَمُونَ ﴿٦٩﴾

69. Na ardhi itang’ara kwa Nuru ya Mola wake, na Kitabu kitawekwa, Na wataletwa Manabii na mashahidi, na patahukumiwa baina yao kwa haki, wala hawatadhulumiwa.

وَوُفِّيَتْ كُلُّ نَفْسٍ مَّا عَمِلَتْ وَهُوَ أَعْلَمُ بِمَا يَفْعَلُونَ ﴿٧٠﴾

70. Na kila nafsi italipwa kwa yale iliyoyafanya, na Yeye anayajua sana wanayoyatenda.

وَسِيقَ الَّذِينَ كَفَرُوا إِلَىٰ جَهَنَّمَ زُمَرًا حَتَّىٰ إِذَا جَاءُوهَا فُتِحَتْ أَبْوَابُهَا وَقَالَ لَهُمْ خَزَنَتُهَا أَلَمْ يَأْتِكُمْ رُسُلٌ مِّنكُمْ يَتْلُونَ عَلَيْكُمْ آيَاتِ رَبِّكُمْ وَيُنذِرُونَكُمْ لِقَاءَ يَوْمِكُمْ هَـٰذَا قَالُوا بَلَىٰ وَلَـٰكِنْ حَقَّتْ كَلِمَةُ الْعَذَابِ عَلَى الْكَافِرِينَ ﴿٧١﴾

71. Na wale ambao wamekufuru watasukumwa kwenye Jahannamu kwa makundi. Mpaka watakapoifikia itafunguliwa milango yake, na walinzi wake watawaambia: Kwani hawakuwajia Mitume miongoni mwenu wakiwasomea Aya za Mola wenu na kuwaonya kukutana na siku yenu hii? Watasema: Ndio! Lakini limekwisha thibiti neno la adhabu juu ya makafiri.

قِيلَ ادْخُلُوا أَبْوَابَ جَهَنَّمَ خَالِدِينَ فِيهَا فَبِئْسَ مَثْوَى الْمُتَكَبِّرِينَ ﴿٧٢﴾

72. Itasemwa: Ingieni milango ya Jahannamu mdumu humo. Basi ni ubaya ulioje wa makazi ya wanaotakabari.

WALIOKUFURU WATASUKUMWA

Aya 68 – 72

MAANA

Na itapulizwa parapanda, wazimie waliomo mbinguni na waliomo ardhini, ila ambaye Mwenyezi Mungu amemtaka.

Kupuziwa parapanda ni kinaya cha ukelele. Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema:

يَوْمَ يَسْمَعُونَ الصَّيْحَةَ بِالْحَقِّ ذَٰلِكَ يَوْمُ الْخُرُوجِ ﴿٤٢﴾

“Siku watakaposikia ukelele kwa haki, hiyo ndiyo siku ya kutoka.” (50:42).

Katika baadhi ya tafsiri imeelezwa kuwa ukelele au mpulizo huu utakaririka mara tatu: Wa kwanza ni ule ilioelezwa katika Aya isemayo:

وَيَوْمَ يُنفَخُ فِي الصُّورِ فَفَزِعَ مَن فِي السَّمَاوَاتِ وَمَن فِي الْأَرْضِ إِلَّا مَن شَاءَ اللَّـهُ وَكُلٌّ أَتَوْهُ دَاخِرِينَ ﴿٨٧﴾

“Na siku itakapopuziwa parapanda, watafazaika waliomo mbinguni na waliomo ardhini, ila amtakaye Mwenyezi Mungu.” Juz. 20 (27:87).

Ambaye Mwenyezi Mungu amemtaka ni yule mwenye takua ambaye umemtangulia wema.

Mpulizo wa pili ni wa mauti ulioashiriwa kwenye Aya hii tuliyo nayo. Na makusudio ya ila ambaye Mwenyezi Mungu amemtaka ni kuwa watu wa ardhini watakufa wote na wa mbinguni hawatabaki isipokuwa ambaye Mwenyezi Mungu atamtaka.

Wafasiri wametofautiana kuhusiana na huyo ambaye Mwenyezi Mungu atamtaka katika wa mbinguni. Ikasemekana kuwa ni Jibril na Israfil. Wengine wakasema ni mashahidi. Mwingine hata akathubutu kusema ni Mwenyezi Mungu – Tunamuomba msamaha Mwenyezi Mungu na tunatubu kwake.

Sio mbali kuwa kusema ila ambaye Mwenyezi Mungu amemtaka, sio hakika bali ni majazi ya kuwa amri siku hiyo ni ya Mwenyezi Mungu peke yake na kwamba:

كُلُّ مَنْ عَلَيْهَا فَانٍ ﴿٢٦﴾ وَيَبْقَىٰ وَجْهُ رَبِّكَ ذُو الْجَلَالِ وَالْإِكْرَامِ ﴿٢٧﴾

“Kila kilichoko juu yake kitatoweka na itabaki dhati ya Mola wako mwenye utukufu na heshima” (55:26-27).

Mpulizo wa tatu ni wa ufufuo amabao amaeuashiria Mwenyezi Mungu Mtukufu kwa kusema:Kisha itapulizwa mara nyengine. Hapo watainuka wawe wanangojea hukumu ya Mwenyezi Mungu kwao.

Kwenye Nahajul-balagha imeelezwa: “Na itapulizwa parapanda, kila chenye uhai kitakufa na kila sauti itakuwa bubu, milima na majabali yataporomoka na mawe yageuke mchanga na iwe tamabarare. Hakutakuwa na muombezi wa kuombea wala ndugu wa kutetea wala udhuru utakaonufaisha.[1]

Na ardhi itang’ara kwa Nuru ya Mola wake.

Makusudio ya ardhi hapa ni ardhi ya ufufuo na mkusanyiko. Nayo itang’arishwa na nuru ya Mwenyezi Mungu Mtukufu, kwa sababu yenyewe ni twahara isyokuwa na aina yoyote ya upotevu na ufisadi; haku- na isipokuwa haki na uadilifu.

Na Kitabu kitawekwa, yaani mandishi ya matendo yote:

وَنُخْرِجُ لَهُ يَوْمَ الْقِيَامَةِ كِتَابًا يَلْقَاهُ مَنشُورًا ﴿١٣﴾

“Na Siku ya Kiyama tutamtolea kitabu atakachokikuta kimekunjuliwa.” Juz. 15 (17:13).

Mulla Sadra anasema katika Al-asfar: “Mwenye kutenda kitendo au kusema kauli, athari yake inajitokeza kwenye nafsi yake na moyo wake.

Athari hii inayopatikana kwenye moyo na roho iko kama nakshi na maandishi katika vitabu na mbao. Nyoyo na roho hizo, ambazo zina athari ya vitendo na kauli, kwa lugha ya sharia zinaitwa kurasa za matendo.”

Na wataletwa Manabii na mashahidi, na patahukumiwa baina yao kwa haki, wala hawatadhulumiwa. Na kila nafsi italipwa kwa yale iliyoyafanya, na Yeye anayajua sana wanayoyatenda.

Makusudio ya mashahidi hapa ni manaibu wa mitume katika kufikisha ujumbe wao na desturi zao kwa watu. Maana ni kuwa Mwenyezi Mungu kesho atawafufua watu kwa ajili ya hisabu. Atawaleta manabii wawe mashahidi kwa manaibu wao kuwa wao walichukua ujumbe kwa manabii ili waufikishe kwa watu.

Kisha manaibu nao watatoa ushahidi kuwa wao waliwafundisha watu na waliufikisha ujumbe kwa ukamilifu. Baada ya kupatikana ushahidi wa manabii kwa manaibu na wa manibu kwa watu, hapo Mwenyezi Mungu atawahukumu wote kwa uadilifu bila ya kumpunguzia thawabu mtiifu wala kumzidishia adhabu Muasi.

Yeye anawajua zaidi wote, wakiwemo manabii na mashahidi, kuliko nafsi zao. Amewaita hapa kwa ushahidi kukamilisha hoja na kuondoa visababu vyote.

Tazama Juz. 2 (2:143).

Na wale ambao wamekufuru watasukumwa kwenye Jahannamu kwa makundi. Mpaka watakapoifikia itafunguliwa milango yake.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) ametaja, katika Kitabu aina kwa aina ya dhabu ya wakosefu; kama vile: udhalili na utwevu, upofu na kusawijika uso, minyororo na nguo za moto, chakula cha Zaqqum na kinywaji cha usaha na kusukumwa na malaika kupelekwa kwenye Jahannam ili wawe kuni zake. Hao malaika wana miadi nao ya kuwangoja, ndio maana watakuta milango tayari iko wazi.

Na walinzi wake watawaambia: Kwani hawakuwajia Mitume miongoni mwenu wakiwasomea Aya za Mola wenu na kuwaonya kukutana na siku yenu hii?

Makusudio ya swali hili ni kutahayariza na kwamba wao ndio waliojichagulia mwisho huu mbaya.

Watasema: Ndio! Lakini limekwishathibiti neno la adhabu juu ya makafiri.

Mfano wake ni kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu:

وَقَالُوا لَوْ كُنَّا نَسْمَعُ أَوْ نَعْقِلُ مَا كُنَّا فِي أَصْحَابِ السَّعِيرِ ﴿١٠﴾ فَاعْتَرَفُوا بِذَنبِهِمْ فَسُحْقًا لِّأَصْحَابِ السَّعِيرِ ﴿١١﴾

“Na watasema: lau tungelikuwa tunasikia au kutia akilini, tusingelikuwa katika watu wa Motoni! Wakakiri dhambi zao. Basi kuangamia ni kwa watu wa motoni!” (67:10-11).

Itasemwa: Ingieni milango ya Jahannamu mdumu humo.

Basi ni ubaya ulioje wa makazi ya wanaotakabari kwenye haki na kutoka kwenye uadilifu.

Lau kusingelikuwa na dalili nyingine ya kuandaliwa Jahannam isipokuwa kwa wenye kiburi, mataghuti, wafisadi na wapotevu tu, ingelitosha. Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema:

إِنَّ الْمُنَافِقِينَ فِي الدَّرْكِ الْأَسْفَلِ مِنَ النَّارِ ﴿١٤٥﴾

“Hakika wanafiki watakuwa katika tabaka ya chini motoni. Juz. 5 (4:145)

Akasema tena:

إِنَّ جَهَنَّمَ كَانَتْ مِرْصَادًا ﴿٢١﴾ لِّلطَّاغِينَ مَآبًا ﴿٢٢﴾

“Hakika Jahannam inangojea. Ni marejeo kwa wenye kupetuka mipaka” (78:21-22).

Huko nyuma tumewahi kusema kuwa lau kusingeliku na mahakama, huko akhera, ya kisasi cha aliyedhulimiwa kwa dhalimu, basi ingelikuwa aliyeuliwa kidhulma ana hali mbaya zaidi ya aliyemuua.

Tazama Juz. 11 (10:3-4) kifungu cha: ‘malipo ni lazima.’

وَسِيقَ الَّذِينَ اتَّقَوْا رَبَّهُمْ إِلَى الْجَنَّةِ زُمَرًا حَتَّىٰ إِذَا جَاءُوهَا وَفُتِحَتْ أَبْوَابُهَا وَقَالَ لَهُمْ خَزَنَتُهَا سَلَامٌ عَلَيْكُمْ طِبْتُمْ فَادْخُلُوهَا خَالِدِينَ ﴿٧٣﴾

73. Na waliomcha Mola wao watapelekwa Peponi kwa makundi, mpaka watakapoifikia, nayo milango yake imekwishafunguliwa, walinzi wake watawaambia: Salaamun Alaikum, (Amani iwe juu yenu!) Mmekua wema. Basi ingieni humu mkae milele.

وَقَالُوا الْحَمْدُ لِلَّـهِ الَّذِي صَدَقَنَا وَعْدَهُ وَأَوْرَثَنَا الْأَرْضَ نَتَبَوَّأُ مِنَ الْجَنَّةِ حَيْثُ نَشَاءُ فَنِعْمَ أَجْرُ الْعَامِلِينَ ﴿٧٤﴾

74. Na watasema: Alhamdulillah, (Sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu) aliyetutimizia ahadi yake, na akaturithisha ardhi, tunakaa katika Bustani popote tupendapo. Basi ni malipo mazuri yaliyoje ya watendao!

وَتَرَى الْمَلَائِكَةَ حَافِّينَ مِنْ حَوْلِ الْعَرْشِ يُسَبِّحُونَ بِحَمْدِ رَبِّهِمْ وَقُضِيَ بَيْنَهُم بِالْحَقِّ وَقِيلَ الْحَمْدُ لِلَّـهِ رَبِّ الْعَالَمِينَ ﴿٧٥﴾

75. Na utawaona Malaika wak- izunguka pembeni mwa Arshi ya Mwenyezi Mungu, wakimsabihi na kumsifu Mola wao. Na patahukumiwa baina yao kwa haki na patasemwa: Sifa zote njema ni za Mwenyezi Mungu, Mola wa viumbe vyote!

WALIOMCHA MOLA WAO WATAPELEKWA PEPONI

Aya 73 – 75

MAANA

Na waliomcha Mola wao watapelekwa Peponi kwa makundi, mpaka watakapoifikia, nayo milango yake imekwishafunguliwa, walinzi wake watawaambia: Salaamun Alaikum, (Amani iwe juu yenu!) Mmekua wema. Basi ingieni humu mkae milele.

Wakosefu watapelekwa kwenye Jahannam huku Malaika wa adhabu wakiwasukuma kwa nguvu na kwa udhalili. Wenye takua wanaingia Peponi wakiwa wamezungukwa na Malaika kwa taadhima na takrima na watasema:

Alhamdulillah, (Sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu) aliyetutimizia ahadi yake, na akaturithisha ardhi, tunakaa katika Bustani popote tupendapo. Basi ni malipo mazuri yaliyoje ya watendao!

Wanaosema hayo ni waumini. Makusudio ya ardhi hapa ni ardhi ya Peponi. Wataitumia kama vile anavyotumia mrithi, mali aliyoachiwa. Kule duniani waliifanyia kazi Pepo wakitegemea na kuamini aliyoahidi Mwenyezi Mungu kwa wenye takua na subira. Watapoiona watafurahia na kumsifu Mwenyezi Mungu wakijua kuwa ahadi yake ni ya kweli na haki.

Imeelezwa kwenye Nahajul-balagha: “Malaika watawazunguka watu Peponi, watawashukia kwa upole, na watawafungulia milango ya mbingu. Watawaandalia sehemu za heshima alizowafahamisha Mwenyezi Mungu, akaridhia mahangaiko na kusifia makazi yao”[2] .

Na utawaona Malaika wakizunguka pembeni mwa Arshi ya Mwenyezi Mungu, wakimsabihi na kumsifu Mola wao.

Katika Juz. 8 (7:53), tumebainisha, kwa ushahidi wa Qur’ani, kuwa Makusudio ya Arshi ni kuwa amri yote ni ya Mwenyezi Mungu. Kwa hiyo maana yake hapa ni kuwa Malaika hawafanyi lolote ila kwa amri ya Mwenyezi Mungu; kama ulivyokuja wasifu wao katika kauli yake Mwenyezi Mungu:

بَلْ عِبَادٌ مُّكْرَمُونَ ﴿٢٦﴾ لَا يَسْبِقُونَهُ بِالْقَوْلِ وَهُم بِأَمْرِهِ يَعْمَلُونَ ﴿٢٧﴾

“Bali hao ni waja waliotukuzwa. Hawamtangulii kwa neno nao wanafanya kwa amri yake.”

Juz. 17 (21:26-27)

Na patahukumiwa baina yao kwa haki na patasemwa Sifa zote njema ni za Mwenyezi Mungu, Mola wa viumbe vyote!

Yaani muasi hatazidishiwa adhabu, wala mtiifu hatapunguziwa thawabu. Kuna tafsiri nyingine zinazasema kuwa Mwenyezi Mungu alipoanza kuumba alisema: Sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu, Mola wa viumbe vyote.

Baada ya kufa viumbe na kuwafufua na kutulia watu wa peponi atasema: Sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu, Mola wa viumbe vyote, ili awafundishe waja wake adabu yake ya kuanza kila jambo kwa sifa njema na kumalizia kwa sifa njema.

MWISHO WA SURA YA THELATHINI NA TISA: SURAT AZ-ZUMAR

4

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI

Sura Ya Arubaini : Surat Al-Ghaafir.

Ina Aya 85. Imeshuka Makka. Imesemekana Aya mbili hazikushuka Makka. Pia inaitwa Sura Mumin

بِسْمِ اللَّهِ الرَّحْمَٰنِ الرَّحِيمِ

Kwa jina la Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema Mwenye kurehemu.

حم ﴿١﴾

1. Hamim.

تَنزِيلُ الْكِتَابِ مِنَ اللَّـهِ الْعَزِيزِ الْعَلِيمِ ﴿٢﴾

2. Uteremsho wa Kitabu umetoka kwa Mwenyezi Mungu Mwenye nguvu, Mwenye kujua.

غَافِرِ الذَّنبِ وَقَابِلِ التَّوْبِ شَدِيدِ الْعِقَابِ ذِي الطَّوْلِ لَا إِلَـٰهَ إِلَّا هُوَ إِلَيْهِ الْمَصِيرُ ﴿٣﴾

3. Mwenye kughufiria dhambi na anayekubali toba, Mkali wa kuadhibu, Mwenye fadhila. Hakuna mungu ila Yeye. Marejeo ni Kwake.

مَا يُجَادِلُ فِي آيَاتِ اللَّـهِ إِلَّا الَّذِينَ كَفَرُوا فَلَا يَغْرُرْكَ تَقَلُّبُهُمْ فِي الْبِلَادِ ﴿٤﴾

4. Hawabishani katika Ishara za Mwenyezi Mungu ila wale ambao wamekufuru. Basi kusikughuri kutangatanga kwao katika nchi.

كَذَّبَتْ قَبْلَهُمْ قَوْمُ نُوحٍ وَالْأَحْزَابُ مِن بَعْدِهِمْ وَهَمَّتْ كُلُّ أُمَّةٍ بِرَسُولِهِمْ لِيَأْخُذُوهُ وَجَادَلُوا بِالْبَاطِلِ لِيُدْحِضُوا بِهِ الْحَقَّ فَأَخَذْتُهُمْ فَكَيْفَ كَانَ عِقَابِ ﴿٥﴾

5. Kabla yao walikadhibisha kaumu ya Nuh na makundi baada yao. Na kila uma ulikuwa na hamu juu ya Mtume wao wamkamate. Na walibishana kwa upotovu ili kuipindua haki. Kwa hivyo niliwakamata. Basi ilikuwaje adhabu yangu!

وَكَذَٰلِكَ حَقَّتْ كَلِمَتُ رَبِّكَ عَلَى الَّذِينَ كَفَرُوا أَنَّهُمْ أَصْحَابُ النَّارِ ﴿٦﴾

6. Namna hivi limewathibitikia makafiri neno la Mola wako kwamba wao ni watu wa Motoni.

MWENYE KUSAMEHE DHAMBI NA KUKUBALI TOBA

Aya 1 – 6

MAANA

Hamim.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 1(2:1).

Uteremsho wa Kitabu umetoka kwa Mwenyezi Mungu.

Kwa sababu ni mizani ya haki na ya uadilifu na ni nuru inayoongoza kutokana na giza la upotevu na ujinga.

Mwenye nguvu, Mwenye kujua, Mwenye kughufiria dhambi na anayekubali toba, Mkali wa kuadhibu, Mwenye fadhila.

Kila sifa katika wasifu huu ina mfungamano na athari katika ulimwengu na binadamu na mwenendo wake: Mwenye kuumba ulimwengu ni lazima aujue na awe na uweza. Ndio ikaja sifa ya mwenye nguvu mwenye kujua. Kuwa na nguvu ni kuwa na uwezo.

Dhambi na toba ni vitendo vya mtu, lakini kukubali toba na kusamehewa ni kwa Mwenyezi Mungu. Yeye Mwenyezi Mungu (s.w.t) husamehe kwa toba au kwa utiifu, kwa sababu mema yanafuta maovu. Vile vile Yeye ni mkali kwa anayeng’ang’ania uasi, wakati huohuo yeye ni mwenye fadhila kwa sababu anampa anayemuomba na asiyemuomba na anamuongezea mengi mtenda mema

Hakuna mungu ila Yeye.

Amepwekeka na sifa ya Tawhid, elimu ya ghaibu na uwezo juu ya kila kitu. Wenye madhambi wote wanahitajia msamaha wake na huruma yake.

Marejeo ni kwake.

Hakuna pa kukimbia kuepuka kukutana naye na hisabu yake na malipo yake. Heri zote ni za yule asiyeona yeyote mwenye kustahiki sifa hizi isipokuwa Mwenyezi Mungu, na wala asiogope yeyote asiyekuwa Yeye.

Hawabishani katika Ishara za Mwenyezi Mungu ila wale ambao wamekufuru, wasiotaka haki na uadilifu wala kuamini chochote isipokuwa hawaa na masilahi yao tu.

Pamoja na hayo wanajitafutia visababu, wakidai kuwa wao ndio walio na haki na kuijadili Qur’ani wakisema kuwa ni ngano za watu wa kale, tawhid ni upotevu na kufufuliwa ni uzushi. Dalili yao ya kwanza na ya mwisho ni kuwa wao wanawaiga mababa zao na kufuata masilahi.

Basi kusikughuri - ewe Muhammad -kutangatanga kwao katika nchi kwa ajili ya biashara na kwenda kwao Sham katika msafara wa kusi na Yemen katika msafara wa kaskazi. Yasikughuri haya, kwa sababu mwisho wake ni maangamizi:

إِنَّمَا نُمْلِي لَهُمْ لِيَزْدَادُوا إِثْمًا وَلَهُمْ عَذَابٌ مُّهِينٌ ﴿١٧٨﴾

“Hakika tunawapa muda na wanazidi tu katika dhambi na wana adhabu idhalilishayo.”

Juz. 4 (3:178).

Kabla yao walikadhibisha kaumu ya Nuh na makundi baada yao. Na kila uma ulikuwa na hamu juu ya Mtume wao wamkamate. Na walibishana kwa upotovu ili kuipindua haki.

Makusudio ya makundi hapa ni kila watu waliounda kikosi dhidi ya haki na watu wake.

Maana ni kuwa vita vyako ewe Muhammad, pamoja na washirikina, sio vita vyako wewe binafsi; isipokuwa ni vita baina ya haki na batili na kufuru na imani. Ni desturi ya waliopita na wanokuja.

Uma zilizopita ziliwakadhibisha mitume na viongozi wema. Wakawajadili kwa ujinga na inadi. Kila uma ulijaribu kumuua Nabii wao na muonyaji wao; sawa na walivyokupangia njama makuraishi ukiwa umelela kitandani mwako.

Tazama Juz. 9 (30 – 35).

Kwa hivyo niliwakamata. Basi ilikuwaje adhabu yangu!

Ilikuwa kali ya kuvunjavunja.

Namna hivi limewathibitikia makafiri neno la Mola wako kwamba wao ni watu wa Motoni.

Haya ni maonyo na hadhari kwa makuraishi kama waking’ang’ania ukafiri na upotevu, yasije yakawapata, yaliyowapata watu wa Nuh, A’d na Thamud.

Lakini kumhofisha asiyemuogopa Mwenyezi Mungu hakuna manufaa yoyote, isipokuwa kusimamisha hoja na kukata visababu vyote.

الَّذِينَ يَحْمِلُونَ الْعَرْشَ وَمَنْ حَوْلَهُ يُسَبِّحُونَ بِحَمْدِ رَبِّهِمْ وَيُؤْمِنُونَ بِهِ وَيَسْتَغْفِرُونَ لِلَّذِينَ آمَنُوا رَبَّنَا وَسِعْتَ كُلَّ شَيْءٍ رَّحْمَةً وَعِلْمًا فَاغْفِرْ لِلَّذِينَ تَابُوا وَاتَّبَعُوا سَبِيلَكَ وَقِهِمْ عَذَابَ الْجَحِيمِ ﴿٧﴾

7. Wale wanaobeba Arshi, na wanaoizunguka, wanamsabihi kwa kumuhimidi Mola wao, na wanamuamini na wanawaombea msamaha walio amini. Mola wetu! Umekienea kila kitu kwa rehema na ujuzi. Basi wasamehe ambao wametubu na wakaifuata Njia yako, na waepushe na adhabu ya Jahannamu.

رَبَّنَا وَأَدْخِلْهُمْ جَنَّاتِ عَدْنٍ الَّتِي وَعَدتَّهُمْ وَمَن صَلَحَ مِنْ آبَائِهِمْ وَأَزْوَاجِهِمْ وَذُرِّيَّاتِهِمْ إِنَّكَ أَنتَ الْعَزِيزُ الْحَكِيمُ ﴿٨﴾

8. Mola wetu! Na waingize katika Bustani za Milele ulizowaahidi. Na pia waliofanya mema miongoni mwa wazee wao na wake zao na dhuriya zao. Hakika Wewe ni Mwenye nguvu, Mwenye hikima.

وَقِهِمُ السَّيِّئَاتِ وَمَن تَقِ السَّيِّئَاتِ يَوْمَئِذٍ فَقَدْ رَحِمْتَهُ وَذَٰلِكَ هُوَ الْفَوْزُ الْعَظِيمُ ﴿٩﴾

9. Na waepushe na maovu; kwani umwepushaye maovu siku hiyo, hakika umemrehemu; na huko ndiko kufuzu kukubwa.

إِنَّ الَّذِينَ كَفَرُوا يُنَادَوْنَ لَمَقْتُ اللَّـهِ أَكْبَرُ مِن مَّقْتِكُمْ أَنفُسَكُمْ إِذْ تُدْعَوْنَ إِلَى الْإِيمَانِ فَتَكْفُرُونَ ﴿١٠﴾

10. Kwa hakika wale waliokufuru watanadiwa: Bila ya shaka kuchukia Mwenyezi Mungu ni kukubwa kuliko kujichukia nyinyi nafsi zenu, mlipokuwa mnaitwa kwenye imani mkakataa.

WANAOBEBA ARSHI

Aya 7 – 10

MAANA

Wale wanaobeba Arshi, na wanaoizunguka, wanamsabihi na kumsifu Mola wao, na wanamuamini.

Katika Juz. 8 (7:54), tulisema kuwa makusudio ya kuwa kwenye Arshi ni kutawala. Na katika Aya ya 75 ya sura iliyopita, tukasema kuwa makusudio ya Malaika kuizunguka Arshi ni kuwa hawamtangulii Mwenyezi Mungu kwa kauli na wanafanya kwa amri yake. Nasi tuna mategemeo kuwa kauli yetu hii, kwa kulinganisha na mfumo wa maneno, inaendana na tafsiri hii.

Ama mfumo wa Aya hii tuliyo nayo na ile inayosema: “Na wanane juu ya wao watachukua Arshi ya Mola wako” (69:17) unatufanya tutafute maana nyingine ya Arshi inayochukuliwa; ingawaje kuchukua Malaika Arshi hakulazimishi kuwa Mungu amekaa juu yake.

Ikiwa hivyo basi itabidi Mwenyezi Mungu awe ana mwili na pia awe yuko mahali fulani na kwengine hayuko.

Ikiwa utauliza : Kama Mwenyezi Mungu hakukaa katika Arshi (kiti cha enzi), kwa nini basi ikanasibishwa kwake, na kusemwa ‘Arshi ya Mola wako.’

Jibu : suala la kunasibisha ni la kawaida na jepesi sana; kwa mfano inaweza kuitwa barabara ya fulani, wakati huyo fulani mwenyewe hata haijui barabara hiyo; sembuse muumba wa ulimwengu wote? Majumba yote ya kuabudu mashariki na magharibi, sikwambii Al-Kaaba tukufu, yanaitwa ni ya Mwenyezi Mungu. Je, hiyo inamaanisha kuwa Mwenyezi Mungu anaishi humo?

Inawezekana kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) ametengeneza Arshi na kuamrisha Malaika wake waizunguke; kama alivyomwamrisha Ibrahim kujenga nyumba kongwe na kulazimisha kuizuru na kuizunguka kila mwenye kuweza kuifika.

Vyovyote iwavyo ni kuwa Malaika wanamwamini Mwenyezi Mungu na kumtukuza kwa kumsifuna wanawaombea msamaha walio amini kwa kusema:Mola wetu! Umekienea kila kitu kwa rehema na ujuzi. Basi wasamehe ambao wametubu na wakaifuata Njia yako, na waepushe na adhabu ya Jahannamu.

Waumini wenye ikhlasi wana aina nyingi ya malipo; zikiwemo Bustani zinazopitiwa na mito chini yake, kuwa marafiki wa manabii na mashahidi na kwamba Malaika wanawatukuza kwa kuwasifu na kuwaombea Mungu wawe na daraja ya juu na kukingwa na ghadhabu yake na adhabu yake.

Mola wetu! Na waingize katika Bustani za Milele ulizowaahidi. Na pia waliofanya mema miongoni mwa wazee wao na wake zao na dhuriya zao. Hakika Wewe ni Mwenye nguvu, Mwenye hikima.

Malaika watamuomba Mwenyezi Mungu kesho awakusanye familia kwenye Pepo yake; kama walivyokuwa duniani ili wazidi kuwa na furaha. Kauli yake: ‘waliofanya mema,’ inaashiria kukatika udugu baina ya mumin na kafiri, hata kama mmoja ni baba wa mwingine;

فَإِذَا نُفِخَ فِي الصُّورِ فَلَا أَنسَابَ بَيْنَهُمْ يَوْمَئِذٍ ﴿١٠١﴾

“Basi itakapopuziwa parapanda, hapo hakutakuwa na nasaba baina yao.” Juz. 18 (23:101).

الْأَخِلَّاءُ يَوْمَئِذٍ بَعْضُهُمْ لِبَعْضٍ عَدُوٌّ إِلَّا الْمُتَّقِينَ ﴿٦٧﴾

“Siku hiyo marafiki watakuwa maadui wao kwa wao isipokuwa wenye takua” (43:67).

Na waepushe na maovu; kwani umwepushaye maovu siku hiyo, hakika umemrehemu; na huko ndiko kufuzu kukubwa.

Wakinge na kila ubaya siku ya kiyama. Hakuna mwenye shaka kwamba mwenye kupata daraja hii mbele ya Mwenyezi Mungu atakuwa amefuzu fadhila zake na rehema zake.

Kwa hakika wale waliokufuru watanadiwa: Bila ya shaka kuchukia Mwenyezi Mungu ni kukubwa kuliko kujichukia nyinyi nafsi zenu, mlipokuwa mnaitwa kwenye imani mkakataa.

Watu wa motoni watachukia wakiwa humo ndani kutokana na yaliyowaleta humo. Huko duniani walikuwa wakiyapenda na kuyaridhia. Mwito utawajia huku wakijilaani wenyewe kuwa, alivyokuwa Mwenyezi Mungu akichukia kufuru yenu duniani ni zaidi sana ya mnavyojichukia nyinyi hivi sasa. Mwenyezi Mungu (s.w.t) aliwalingani kupitia mitume wake, lakini mkakataa isipokuwa ukafiri. Basi onjeni adhabu leo, na madhalimu hawana msaidizi.

قَالُوا رَبَّنَا أَمَتَّنَا اثْنَتَيْنِ وَأَحْيَيْتَنَا اثْنَتَيْنِ فَاعْتَرَفْنَا بِذُنُوبِنَا فَهَلْ إِلَىٰ خُرُوجٍ مِّن سَبِيلٍ ﴿١١﴾

11. Watasema: Mola wetu! Umetufisha mara mbili, na umetuhuisha mara mbili! Basi tunakiri madhambi yetu. Basi je, ipo njia ya kutoka?

ذَٰلِكُم بِأَنَّهُ إِذَا دُعِيَ اللَّـهُ وَحْدَهُ كَفَرْتُمْ وَإِن يُشْرَكْ بِهِ تُؤْمِنُوا فَالْحُكْمُ لِلَّـهِ الْعَلِيِّ الْكَبِيرِ ﴿١٢﴾

12. Hayo ni kwa sababu alipoombwa Mwenyezi Mungu peke yake mlikataa. Na akishirikishwa mnaamini. Basi hukumu ni ya Mwenyezi Mungu Mtukufu Mkubwa.

هُوَ الَّذِي يُرِيكُمْ آيَاتِهِ وَيُنَزِّلُ لَكُم مِّنَ السَّمَاءِ رِزْقًا وَمَا يَتَذَكَّرُ إِلَّا مَن يُنِيبُ ﴿١٣﴾

13. Yeye ndiye ambaye anawaonyesha Ishara zake, na anawateremshia riziki kutoka mbinguni. Na hapana anayekumbuka ila anaye rejea.

فَادْعُوا اللَّـهَ مُخْلِصِينَ لَهُ الدِّينَ وَلَوْ كَرِهَ الْكَافِرُونَ ﴿١٤﴾

14. Basi mwombeni Mwenyezi Mungu mkimsafia Dini Yeye, wajapochukia makafiri.

رَفِيعُ الدَّرَجَاتِ ذُو الْعَرْشِ يُلْقِي الرُّوحَ مِنْ أَمْرِهِ عَلَىٰ مَن يَشَاءُ مِنْ عِبَادِهِ لِيُنذِرَ يَوْمَ التَّلَاقِ ﴿١٥﴾

15. Ndiye Mwenye daraja za juu. Mwenye Arshi. Hupeleka Roho, kwa amri yake, juu ya amtakaye katika waja wake, ili kuonya Siku ya kukutana.

يَوْمَ هُم بَارِزُونَ لَا يَخْفَىٰ عَلَى اللَّـهِ مِنْهُمْ شَيْءٌ لِّمَنِ الْمُلْكُ الْيَوْمَ لِلَّـهِ الْوَاحِدِ الْقَهَّارِ ﴿١٦﴾

Siku watakayodhihiri wao. Hapana kitachofichikana chochote chao kwa Mwenyezi Mungu. Ufalme ni wa nani leo? Ni wa Mwenyezi Mungu Mmoja Mtenza nguvu.

الْيَوْمَ تُجْزَىٰ كُلُّ نَفْسٍ بِمَا كَسَبَتْ لَا ظُلْمَ الْيَوْمَ إِنَّ اللَّـهَ سَرِيعُ الْحِسَابِ ﴿١٧﴾

17. Leo kila nafsi italipwa kwa iliyoyachuma. Hapana dhulma leo. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwepesi wa kuhisabu.

UMETUFISHA MARA MBILI NA UMETUHUISHA MARA MBILI

Aya 11 – 17

MAANA

Watasema: Mola wetu! Umetufisha mara mbili, na umetuhuisha mara mbili! Basi tunakiri madhambi yetu. Basi je, ipo njia ya kutoka?

Watakaosema hivyo ni watu wa motoni. Mauti ya kwanza ni kabla ya kuto- ka matumboni mwa mama zao na ya pili ni haya mauti yaliyozoeleka. Uhai wao wa kwanza ni uhai wa duniani na wa pili ni wa ufufuo baada ya mauti.

Maana ni kuwa watu wa Jahannam, wakiwa katikati ya moto wakiadhibi- wa, watamnyenyekea Mwenyezi Mungu huku wakisema: Ewe Mola wetu! Wewe ni muweza wa kila kitu. Ulituleta duniani, ukatutoa kwenye mauti, kisha ukatufufua baada yake.

Hivi sasa tuko mbele yako tukijuta na kukiri makosa na dhambi zetu. Je, kuna njia yoyote, kutokana na karama yako, kutuwezesha kutoka motoni, tukikuahidi utiifu na kufuata amri?

Hayo ni kwa sababu alipoombwa Mwenyezi Mungu peke yake mlikataa. Na akishirikishwa mnaamini.

Hili ni jawabu la kauli yao ‘Je, ipo njia ya kutokea?’ Ufupisho wa jawabu ni kuwa mlinganiaji haki aliwapa mwito wa haki, duniani, mkaukataa. Na mlinganiaji shetani aliwapa mwito mkaukubali. Hivi sasa mnaita hamtajibiwa.

Kauli yake Mwenyezi Mungu:Basi hukumu ni ya Mwenyezi Mungu Mtukufu Mkubwa, inaashiria kuwa kesho hukumu ni ya Mwenyezi Mungu tu peke yake, hakuna mkubwa isipokuwa Yeye tu:

وَعَنَتِ الْوُجُوهُ لِلْحَيِّ الْقَيُّومِ وَقَدْ خَابَ مَنْ حَمَلَ ظُلْمًا ﴿١١١﴾

“Zitanyenyekea nyuso kwa aliye Hai, Mwangalizi Mkuu. Na hakika ameharibikiwa mwenye kubeba dhulma.” Juz. 16 (20:111).

Yeye ndiye ambaye anawaonyesha Ishara zake, na anawateremshia riziki kutoka mbinguni. Na hapana anayekumbuka ila anayerejea.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) ametuonyesha ushahidi mwingi juu ya kuweko kwake, utukufu wake, dalili za upangiliaji wake na hekima yake katika mbingu, ardhi, watu, wanyama na hata katika mvua na mimea na mengingineyo yasiyokuwa na ukomo.

Ilivyo ni kuwa dalili hizi, pamoja na wingi wake, hazijitokezi ila kwa mwenye busara na kufikiria, lakini mpofu wa moyo hayaoni hayo. Anasema Tagore:

“Hakika Mwenyezi Mungu anadhihirisha kuweko kwake katika mfumo hai wa sura mbali mbali za maumbile. Ameudhihirisha kwenye mfumo ulioko baina ya nguvu za maumbile zinazopambana katika umoja wao kwenye kanuni iliyopangiliwa isiyoepukika, wakati huo huo zikielekea kuhakikisha malengo. Kila kitu katika maumbile kina wadhifa wake maalum na malengo maulumu yaliyopangiliwa. Mbegu inafanya kazi kwa bidii ili itoe mti, mti nao unajitihidi ili utoe mau na maua nayo yana kazi ya kutoa tunda. Haya hawezi kuyatambua isipokuwa mwenye moyo ulio salama.”

Makusudio ya mwenye moyo salama ndio yale hasa yaliyokusudiwa katika kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: ‘Na hapana anayekumbuka ila anayerejea.’

Basi mwombeni Mwenyezi Mungu mkimsafia Dini Yeye, wajapochukia makafiri.

Wanaambiwa waumini. Makusudio ya kuomba hapa ni ibada na dini ni utiifu. Maana ni kuwa mwabuduni Mwenyezi Mungu peke yake na mumtii katika amri zake na makatazo yake, wala msijali lawama. Mwenyezi Mungu (s.w.t) amewasahilishia waja wake njia ya kumtii, pale alipowaongoza akiwahadharisha, akawakalifisha kwa wepesi; na hakumwachia udhuru mwenye kutafuta visababu.

Ndiye Mwenye daraja za juu.

Hiki ni kinaya cha utukufu wake. Imesemekana kuwa Makusudio ya daraja hapa ni tofauti ya wanaomojua Mungu katika maarifa yao.

Kuanzia maarifa ya mtu wa kawaida hadi maarifa ya wanafilosofia na manabii.

Mwenye Arshi.

Ni kinaya cha umiliki na utawala.

Hupeleka Roho kwa amri yake juu ya amtakaye katika waja wake, ili kuonya Siku ya kukutana.

Makusdio ya roho hapa ni wahyi. Siku ya kukutana ni Siku ya Kiyama ambapo kila mtu atakutana na malipo ya amali yake. Na makusudio ya kuonya siku hii ni kuonya adhabu. Imekuja ibara ya kuwa Yeye Mwenyezi Mungu ndiye muonyaji, kutokana na ukali na vituko vya siku hiyo.

Maana ni kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) anamteremshia wahyi anayemtaka katika waja wake, ili awaonye watu, kwamba wao watafufuliwa baada ya mauti, katika siku ambayo itakuwa mbaya kwa wenye kuvuka mipaka na waasi na kuulizwa yale waliyokuwa wakiyafanya.

Siku watakayodhihiri wao.

Yaani itadhihiri hakika yao.

Hapana kitachofichikana chochote chao kwa Mwenyezi Mungu.

Huu ni ubainfu wa kauli ya: ‘Siku watakayodhihiri.’

Ufalme ni wa nani leo?

Wataulizwa siku ya kiyama, wakiwa wametokeza kwa ajili ya hukumu: amri na hukumu ni ya nani? Mwenyezi Mungu (s.w.t) atawajibia, kwa sababu jawabu liko wazi.

Au wao wenyewe watajibu kihali na kimaneno kuwa:Ni wa Mwenyezi Mungu Mmoja Mtenza nguvu waja.

Leo kila nafsi italipwa kwa iliyoyachuma. Hapana dhulma leo. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwepesi wa kuhisabu.

Aya hii iko wazi, na imetangulia katika Juz. 13 (14:51).