TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI Juzuu 22

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI0%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: Qurani tukufu

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI

Mwandishi: Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya
: HASANI MWALUPA
Kundi:

Matembeleo: 19905
Pakua: 2195


Maelezo zaidi:

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 29 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 19905 / Pakua: 2195
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI Juzuu 22

Mwandishi:
Swahili

5

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI

وَأَنذِرْهُمْ يَوْمَ الْآزِفَةِ إِذِ الْقُلُوبُ لَدَى الْحَنَاجِرِ كَاظِمِينَ مَا لِلظَّالِمِينَ مِنْ حَمِيمٍ وَلَا شَفِيعٍ يُطَاعُ ﴿١٨﴾

18. Na waonye siku inayokaribia, wakati nyoyo zitakapofika kooni, nao wamejaa huzuni. Madhalimu hawatakuwa na rafiki, wala mwombezi wa kuitikiwa.

يَعْلَمُ خَائِنَةَ الْأَعْيُنِ وَمَا تُخْفِي الصُّدُورُ ﴿١٩﴾

19. Anajua hiyana ya macho na yanayoficha vifua.

وَاللَّـهُ يَقْضِي بِالْحَقِّ وَالَّذِينَ يَدْعُونَ مِن دُونِهِ لَا يَقْضُونَ بِشَيْءٍ إِنَّ اللَّـهَ هُوَ السَّمِيعُ الْبَصِيرُ ﴿٢٠﴾

20. Na Mwenyezi Mungu huhukumu kwa haki. Na wale ambao wanaomba kinyume chake hawahukumu chochote. Hakika Mwenyezi Mungu ndiye Mwenye Kusikia, Mwenye kuona.

أَوَلَمْ يَسِيرُوا فِي الْأَرْضِ فَيَنظُرُوا كَيْفَ كَانَ عَاقِبَةُ الَّذِينَ كَانُوا مِن قَبْلِهِمْ كَانُوا هُمْ أَشَدَّ مِنْهُمْ قُوَّةً وَآثَارًا فِي الْأَرْضِ فَأَخَذَهُمُ اللَّـهُ بِذُنُوبِهِمْ وَمَا كَانَ لَهُم مِّنَ اللَّـهِ مِن وَاقٍ ﴿٢١﴾

21. Je, hawatembei katika ardhi wakaona vipi ulikuwa mwisho wa waliokuwa kabla yao? Nao walikuwa na nguvu zaidi kuliko wao na athari katika nchi. Na Mwenyezi Mungu aliwakamata kwa sababu ya madhambi yao. Na wala hapakuwa wa kuwalinda na Mwenyezi Mungu.

ذَٰلِكَ بِأَنَّهُمْ كَانَت تَّأْتِيهِمْ رُسُلُهُم بِالْبَيِّنَاتِ فَكَفَرُوا فَأَخَذَهُمُ اللَّـهُ إِنَّهُ قَوِيٌّ شَدِيدُ الْعِقَابِ ﴿٢٢﴾

22. Hayo ni kwa sababu walikuwa wanawajia Mitume wao kwa hoja zilizo wazi, lakini wakawakataa, ndipo Mwenyezi Mungu akawakamata. Bila ya shaka Yeye ni Mwenye nguvu, Mkali wa kuadhibu.

WAONYE SIKU INAYOKURUBIA

Aya 18 – 22

MAANA

Na waonye siku inayokaribia, wakati nyoyo zitakapofika kooni, nao wamejaa huzuni. Madhalimu hawatakuwa na rafiki, wala mwombezi wa kuitikiwa.

Maneno yanaelekezwa kwa Mtume(s.a.w. w ) na wanaotakiwa kuonywa ni washirikina wa kiarabu. Maana ni kuwa kazi yako ewe Muhammad ni kuwaonya washirikina na adhabu ya siku ambayo nyoyo zitayeyuka kwa fazaa; ambapo hakutakuwa na rafiki wala mwombezi. Na siku hii iko karibu tu bila shaka itafika.

Mwenyezi Mungu anajua hiyana ya macho na yanayoficha vifua. Na Mwenyezi Mungu huhukumu kwa haki.

Hakuna jambo alilolidhamiria mtu au kuliangalia kwa jicho la hiyana, ila Mwenyezi Mungu atakuwa analijua na atalitolea hukumu kesho kwa ilimu yake na uadilifu, kwa kila mhaini mwenye hatia. Hukumu yake itakuwa ya mwisho haina rufaa.

Na wale ambao wanaomba kinyume chake Mwenyezi Mungu hawahukumu chochote.

Makusudio ya kinyume chake ni kila kisichokuwa Mwenyezi Mungu wanchokiabudu watu; iwe ni sanamu, mali, cheo au mengineyo.

Hakika Mwenyezi Mungu ndiye Mwenye Kusikia, Mwenye kuona.

Hii ni ibara nyingine baada ya ile isemayo:

وَأَنَّ اللَّـهَ قَدْ أَحَاطَ بِكُلِّ شَيْءٍ عِلْمًا ﴿١٢﴾

“Na kwamba Mwenyezi Mungu amekizunguka kila kitu kwa elimu.” (65:12).

Je, hawatembei katika ardhi wakaona vipi ulikuwa mwisho wa waliokuwa kabla yao? Nao walikuwa na nguvu zaidi kuliko wao na athari katika nchi. Na Mwenyezi Mungu aliwakamata kwa sababu ya madhambi yao. Na wala hapakuwa wa kuwalinda na Mwenyezi Mungu.

Huku ni kutahadharishwa kunakotoka kwa Mwenyezi Mungu kwa wakosefu, kwamba mwisho wao utakuwa kama mwisho wa waliokuwa kabla yao. Walikuwa wengi na wenye mali nyingi, lakini ilipokuja adhabu hawakupata wa kuwasaidia wala wa kuwalinda. Umetangulia mfano wake katika Juz. 13 (12:109), Juz. 17 (22:46), Juz. 21 (30:9) na Juz. 22 (35:44).

Hayo ni kwa sababu walikuwa wanawajia Mitume wao kwa hoja zilizo wazi, lakini wakawakataa, ndipo Mwenyezi Mungu akawakamata. Bila ya shaka Yeye ni Mwenye nguvu, Mkali wa kuadhibu.

Yametangulia maelezo mara nyingi, kwamba mwisho wa waliokadhibisha mitume ni kuvunjika na kubomoka. Kesho hakutakuwa na tofauti baina ya waliowakataa mitume na wale waliowamini lakini wakahalifu mafunzo yao na wakazima desturi zao; hata kama duniani watachukuliwa kuwa ni waislamu.

وَلَقَدْ أَرْسَلْنَا مُوسَىٰ بِآيَاتِنَا وَسُلْطَانٍ مُّبِينٍ ﴿٢٣﴾

23. Na kwa hakika tulimtuma Musa pamoja na Ishara zetu na hoja zilizo wazi.

إِلَىٰ فِرْعَوْنَ وَهَامَانَ وَقَارُونَ فَقَالُوا سَاحِرٌ كَذَّابٌ ﴿٢٤﴾

24. Kwa Firauni na Hamana na Qaruni. Wakasema: “Ni mchawi, mwongo mkubwa.

فَلَمَّا جَاءَهُم بِالْحَقِّ مِنْ عِندِنَا قَالُوا اقْتُلُوا أَبْنَاءَ الَّذِينَ آمَنُوا مَعَهُ وَاسْتَحْيُوا نِسَاءَهُمْ وَمَا كَيْدُ الْكَافِرِينَ إِلَّا فِي ضَلَالٍ ﴿٢٥﴾

25. Basi alipowaletea Haki inayotoka kwetu, walisema: ‘Waueni watoto wanaume wa wale waliomuamini na wawacheni hai wanawake wao.’ Na haviwi vitimbi vya makafiri ila katika upotovu.

وَقَالَ فِرْعَوْنُ ذَرُونِي أَقْتُلْ مُوسَىٰ وَلْيَدْعُ رَبَّهُ إِنِّي أَخَافُ أَن يُبَدِّلَ دِينَكُمْ أَوْ أَن يُظْهِرَ فِي الْأَرْضِ الْفَسَادَ ﴿٢٦﴾

26. Na Firauni akasema: Niachieni nimuuwe Musa, naye amwite Mola wake! Hakika Mimi nachelea asije kubadilisha dini yenu, au akadhihirisha uharibifu katika nchi.

وَقَالَ مُوسَىٰ إِنِّي عُذْتُ بِرَبِّي وَرَبِّكُم مِّن كُلِّ مُتَكَبِّرٍ لَّا يُؤْمِنُ بِيَوْمِ الْحِسَابِ ﴿٢٧﴾

27. Na Musa akasema: Hakika Mimi najikinga kwa Mola wangu na Mola wenu anilinde na kila mwenye kiburi asiyeiamini Siku ya Hisabu.

وَقَالَ رَجُلٌ مُّؤْمِنٌ مِّنْ آلِ فِرْعَوْنَ يَكْتُمُ إِيمَانَهُ أَتَقْتُلُونَ رَجُلًا أَن يَقُولَ رَبِّيَ اللَّـهُ وَقَدْ جَاءَكُم بِالْبَيِّنَاتِ مِن رَّبِّكُمْ وَإِن يَكُ كَاذِبًا فَعَلَيْهِ كَذِبُهُ وَإِن يَكُ صَادِقًا يُصِبْكُم بَعْضُ الَّذِي يَعِدُكُمْ إِنَّ اللَّـهَ لَا يَهْدِي مَنْ هُوَ مُسْرِفٌ كَذَّابٌ ﴿٢٨﴾

28. Na akasema mtu mmoja Muumini, katika watu wa Firauni, anayeficha Imani yake: Mtamuuwa mtu kwa sababu anasema Mola wangu ni Mwenyezi Mungu? Na hali amewajia na hoja zilizo wazi? Na akiwa ni mwongo basi uwongo wake ni juu yake mwenyewe, na akiwa ni mkweli yatawafika baadhi ya hayo anayowaahidi; Hakika Mwenyezi Mungu hamwongoi apindukiaye mipaka, mwongo mkubwa.

يَا قَوْمِ لَكُمُ الْمُلْكُ الْيَوْمَ ظَاهِرِينَ فِي الْأَرْضِ فَمَن يَنصُرُنَا مِن بَأْسِ اللَّـهِ إِن جَاءَنَا قَالَ فِرْعَوْنُ مَا أُرِيكُمْ إِلَّا مَا أَرَىٰ وَمَا أَهْدِيكُمْ إِلَّا سَبِيلَ الرَّشَادِ ﴿٢٩﴾

29. Enyi watu wangu! Leo mna ufalme, mmeshinda katika nchi; basi ni nani atakayetusaidia kutuokoa na adhabu ya Mwenyezi Mungu kama ikitufikia? Firauni akasema: Siwapi rai ila ile niliyoiona, wala siwaongozi ila kwenye njia ya uwongofu.

MUSA

Aya 23 – 29

MAANA

Maelezo kuhusiana na Musa yamepita mara kadhaa, tukiwa tunaashiria jina la sura na Aya iliyopita kila inapokuja Aya nyingine. Hivi sasa kimerudi kisa cha Musa na kitaendelea kurudi kwenye Aya za mbele.

Katika Juz. 16 (20:9 – 16) kifungu cha ‘kukaririka kisa’ tumebainisha sababu za kukaririka huku. Na hivi sasa tunaunganisha tuliyoyabainisha huko na hapa; kwamba sio mbali kuwa kila Aya, hata kama ikikaririka, huwa inatoa mwanga mpya uliofichika kwetu, kwa kuwa sisi hatukufikia utafiti wake au hatukuwa na uwezo wa kuutambua. Vyovyote iwavyo, jipya katika Aya hizi tulizo nazo sasa, ni kuwa zinamzungumzia mumin wa watu wa Firauni.

Na kwa hakika tulimtuma Musa pamoja na Ishara zetu na hoja zilizo wazi, kwa Firauni na Hamana na Qaruni,

Hamana ni waziri wa Firauni na Qaruni alikuwa tajiri mkubwa kuliko wote wakati wa Firauni. Inasemekana alikuwa waziri wa fedha wa utawala wa Firauni. Mwenyezi Mungu (s.w.t) alimtuma Musa kwa watu wote wa zama zake. Wamehusishwa kutajwa hawa watatu, kwa sababu wao ndio msingi wa ufisadi na chimbuko la upotevu. Kama wangeliamini hawa, basi wangeliamini wote.

Wakasema: Ni mchawi, mwongo mkubwa; sawa na walivyosema waliokuwa kabla yao na baada yao, kumwambia kila anyayewajia na ubainifu na hoja.

Basi alipowaletea Haki inayotoka kwetu, walisema: Waueni watoto wanaume wa wale waliomuamini na wawacheni hai wanawake wao.

Aliamrisha kuuliwa watoto wa kiume kwa kuwahofia na kuwabakisha wa kike kwa ajili ya kuwahudumia. Unaweza kuuliza: Firauni alitoa amri hii kabla ya kuzaliwa Musa. Je kuna makusudio gani ya kukaririka tena?

Baadhi ya wafasiri wamejibu kuwa Firauni alizuia kuuliwa watoto baada ya kuzaliwa Musa, lakini Musa alipotumwa na Mwenyezi Mungu, Firauni alirudia kuua. Kauli hii inahitaji kuthibitishwa. Sio mbali kuwa amri ya pili ya kuua ni kuendeleza ile amri ya kwanza; kwamba kuua kuendelee tu wala kusisimamishwe kwa hali yoyote.

Na haviwi vitimbi vya makafiri ila katika upotovu.

Yaani: “Na vitimbi viovu havimpati ila mwenyewe. Basi hawangoji ila desturi ya wa zamani.” Juz. 22 (35:43).

Na Firauni akasema: Niachieni nimuuwe Musa, naye amwite Mola wake!

Hii inaashiria kuwa badhi ya watu wa Firauni walimshauri asimuue Musa kwa kuhofia Mola wake atalipiza kisasi.

Firauni aliendelea kusema:Hakika Mimi nachelea asije kubadilisha dini yenu, au akadhihirisha uharibifu katika nchi.

Firauni ni mzuri kwa vile yeye anasema, mimi ndiye mola wenu mkuu na mimi simjui Mungu mwingine kwenu zaidi yangu. Na Musa ni mharibifu kwa vile yeye ana mwito wa kuwakomboa watu kwenye utumwa wa watu wengine! Haya siyo mageni. Ndio mantiki ya viongozi wa mabavu kila wakati na kila mahali.

Na Musa akasema: Hakika Mimi najikinga kwa Mola wangu na Mola wenu anilinde na kila mwenye kiburi asiyeiamini Siku ya Hisabu.

Musa anajilinda kwa Mwenyezi Mungu asiwe na kiburi na kutomwogopa Mwenyezi Mungu na hisabu yake na adhabu yake. Kwa sababu mtu duni zaidi ni yule aliye na mambo haya mawili.

Na akasema mtu mmoja Muumini, katika watu wa Firauni, anayeficha Imani yake: Mtamuuwa mtu kwa sababu anasema Mola wangu ni Mwenyezi Mungu? Na hali amewajia na hoja zilizo wazi?

Haki huwa haikosi mtetezi, ijapokuwa ni kwaneno la ikhlasi linaloelekezwa kwa watu wa batili na upotevu. Huyu hapa mtu katika watu wa Firauni, aliyemwamini Mwenyezi Mungu kwa ukweli na yakini, lakini alificha imani yake, kwa kuhofia kuuliwa.

Firauni alipotaka kumfanyia shari Musa, imani halisi iliugusa moyo wake, kiasi cha kulipinga hilo na kulihadharisha, lakini kwa mfumo wa kiakili na kihekima, akasema: Amekosa nini mtu huyu mpaka akastahiki kuuliwa? Ni kwa vile tu amesema: Mola wangu ni Mwenyezi Mungu, akiwa na hoja mkataa zilizowaziba mdomo na kuwashinda; kama vile mkono mweupe na fimbo iliyomeza mliyokuwa mkiyazua?

Sheikh Maraghi, katika tafsiri yake, anasema, ninamnukuu: “Mtu mmoja mumin ni binamu yake Firauni, mrithi wake na mkuu wa polisi. Huyu aliokoka pamoja na Musa. Na ndiye aliyekusudiwa katika kauli yake Mwenyezi Mungu:

وَجَاءَ مِنْ أَقْصَى الْمَدِينَةِ رَجُلٌ يَسْعَىٰ قَالَ يَا قَوْمِ اتَّبِعُوا الْمُرْسَلِينَ ﴿٢٠﴾

“Na akaja mtu mbio kutoka upande wa mbali wa mjini” Juz. 22 (36:20).

Ikumbukwe kwamba Sheikh Maraghi alipokuwa akifasiri sura Yasin alisema kuwa mtu huyu aliyekuja mbio kutoka mjini alikuwa katika zama za Isa; kama walivyosema hivyo wafasiri wengineo. Sasa ni nani aliyemfufua wakati wa Musa, ambapo kati yake na Isa kuna zaidi ya miaka 1200; kama walivyosema wanahistoria? Lakini wasiokosea ni wale maasum (waliohifadhiwa na makosa).

Na akiwa ni mwongo basi uwongo wake ni juu yake mwenyewe, mwacheni na uwongo wakena akiwa ni mkweli yatawafika baadhi ya hayo anayowaahidi; iwe mtamuua au mtamuacha. Alisema baadhi ya anayowaahidi na wala hakusema yote anayowaahidi, kwa sababu baadhi yanatosha kuangamiza.

Hakika Mwenyezi Mungu hamwongoi apindukiaye mipaka, mwongo mkubwa.

Mmedai kuwa yeye ni mwongo, basi mwacheni apate malipo ya uwongo. Hapa kuna ishara kuwa wasifu huu ni wa Firauni na kwamba yeye atapambana na malipo ya uwongo wake na kupaetuka kwake mipaka tu.

Enyi watu wangu! Leo mna ufalme, mmeshinda katika nchi; basi ni nani atakaye tusaidia kutuokoa na adhabu ya Mwenyezi Mungu kama ikitufikia?

Bado maneno yanatoka kwa mumin kuwaambia watu wake, watu wa Firauni. Maana yake ni kuwa, nyinyi hivi sasa mko katika amani na mnao ufalme ulioshinda. Basi neema hii aliyowaneemesha Mwenyezi Mungu, msiiondoe kwa kumuua anayesema Mwenyezi Mungu ndiye Mola wangu. Basi ni nani atakayetuokoa na uovu wake akitujia usiku au mchana?

Kwa ufupi ni kuwa mumin alimkinga Musa kwa njia nzuri na akawajadili maadui wa Mungu kwa hekima na mawaidha mazuri; kwanza alimwepusha Musa na makosa. Pili akawatishia maadui zake kwa hatari na madhara. Tatu akawakumbusha neema ya Mwenyezi Mungu kwao na akawahadhrisha wasiibadilishe na kufuru.

Kwa mfumo huu aliweza kubadilisha azma ya taghuti na kushikilia kwake kumuua Musa, mpaka Firauni akasema:

Siwapi rai ila ile niliyoiona, wala siwaongozi ila kwenye njia ya uwongofu.

Kauli hii ya Firauni inafanana na kuomba msamaha kutokana na yale aliyoyaazimia, kumuua Musa. Na hiyo ni kutokana na nasaha za mumin. Maana ni kuwa mimi sikutoa shauri ya kumuua Musa ila baada ya kufikiria vizuri; na sikutaka haya ila kwa masilahi yenu.

6

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI

وَقَالَ الَّذِي آمَنَ يَا قَوْمِ إِنِّي أَخَافُ عَلَيْكُم مِّثْلَ يَوْمِ الْأَحْزَابِ ﴿٣٠﴾

30. Na akasema yule aliyeamini: Enyi watu wangu! Hakika mimi nawahofia mfano wa siku za makundi.

مِثْلَ دَأْبِ قَوْمِ نُوحٍ وَعَادٍ وَثَمُودَ وَالَّذِينَ مِن بَعْدِهِمْ وَمَا اللَّـهُ يُرِيدُ ظُلْمًا لِّلْعِبَادِ ﴿٣١﴾

31. Mfano wa hali ya watu wa Nuh na A’di na Thamudi na wale wa baada yao. Na Mwenyezi Mungu hataki kuwadhulumu waja.

وَيَا قَوْمِ إِنِّي أَخَافُ عَلَيْكُمْ يَوْمَ التَّنَادِ ﴿٣٢﴾

32. Na enyi watu wangu! Hakika mimi nawahofia Siku ya kunadi.

يَوْمَ تُوَلُّونَ مُدْبِرِينَ مَا لَكُم مِّنَ اللَّـهِ مِنْ عَاصِمٍ وَمَن يُضْلِلِ اللَّـهُ فَمَا لَهُ مِنْ هَادٍ ﴿٣٣﴾

33. Siku mtakapogeuka kurudi nyuma, hamtakuwa na wa kuwalinda kwa Mwenyezi Mungu. Na ambaye Mwenyezi Mungu amempoteza, basi huyo hana wa kumwongoa.

وَلَقَدْ جَاءَكُمْ يُوسُفُ مِن قَبْلُ بِالْبَيِّنَاتِ فَمَا زِلْتُمْ فِي شَكٍّ مِّمَّا جَاءَكُم بِهِ حَتَّىٰ إِذَا هَلَكَ قُلْتُمْ لَن يَبْعَثَ اللَّـهُ مِن بَعْدِهِ رَسُولًا كَذَٰلِكَ يُضِلُّ اللَّـهُ مَنْ هُوَ مُسْرِفٌ مُّرْتَابٌ ﴿٣٤﴾

34. Na alikwishawajia Yusuf zamani kwa dalili zilizo wazi, lakini nyinyi mliendelea katika shaka kwa yale aliyowaletea; mpaka alipokufa mkasema: Mwenyezi Mungu hataleta tena Mtume baada yake. Kama hivyo Mwenyezi Mungu humpoteza yule aliyepita kiasi mwenye shaka.

الَّذِينَ يُجَادِلُونَ فِي آيَاتِ اللَّـهِ بِغَيْرِ سُلْطَانٍ أَتَاهُمْ كَبُرَ مَقْتًا عِندَ اللَّـهِ وَعِندَ الَّذِينَ آمَنُوا كَذَٰلِكَ يَطْبَعُ اللَّـهُ عَلَىٰ كُلِّ قَلْبِ مُتَكَبِّرٍ جَبَّارٍ ﴿٣٥﴾

35. Wale ambao wanajadiliana katika Ishara za Mwenyezi Mungu bila ya dalili yoyote iliyowafikia, ni chukizo kubwa mbele ya Mwenyezi Mungu na mbele ya walioamini. Hivi ndivyo Mwenyezi Mungu apigavyo chapa juu ya kila moyo wa jeuri anayejivuna.

MWENYEZI MUNGU HADHULUMU WAJA

Aya 30 – 35

MAANA

Na akasema yule aliyeamini: Enyi watu wangu! Hakika mimi nawahofia mfano wa siku za makundi. Mfano wa hali ya watu wa Nuh na A’di na Thamudi na wale wa baada yao.

Makusudio ya makundi hapa ni watu waliounda vikundi dhidi ya mitume wao; kwa dalili ya kauli yake: “Mfano wa hali ya watu wa Nuh na A’di na Thamudi na wale wa baada yao.”

Aliposema Firauni: ‘Wala siwaongozi ila kwenye njia ya uongofu’ yule mumin naye akasema: ‘mimi vile vile si kusema niliyowaambia ila kwa kuhofia yasiwapate maangamizi kama yalivyowapata wa mwanzo, pale walipowakadhibisha manabii wao.

Na Mwenyezi Mungu hataki kuwadhulumu waja, lakini wao wenyewe wanajidhulumu kwa kuwakadhibisha mitume na kuifanyia jeuri amri ya Mwenyezi Mungu.

Baada ya yule mumin kuwahadharisha na adhabu ya dunia, aliwahadharisha na adhabu ya Akhera kwa kusema:

Na enyi watu wangu! Hakika mimi nawahofia Siku ya kunadi.

Siku ya kunadi ni Siku ya Kiyama, ambapo watu watanadiwa kwa ukulele; kama ilivyo katika kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu:

يَوْمَ يُنَادِ الْمُنَادِ مِن مَّكَانٍ قَرِيبٍ ﴿٤١﴾

“Siku atakaponadi mwenye kunadi kutoka mahali karibu” (50:41).

Siku mtakapogeuka kurudi nyuma mkijaribu kukimbia adhabu ya moto, lakini wapi! Hamtakuwa na wa kuwalinda kwa Mwenyezi Mungu.

Vipi mtaweza kumkimbia na hali yeye ndiye mwenye nguvu, kwenye jambo lake, hapingwi wala hazuiwi.

Na ambaye Mwenyezi Mungu amempoteza, basi huyo hana wa kumwongoa.

Yaani atakayefuata njia ya upotevu basi Mwenyezi Mungu atampoteza; kama vile anayekunywa sumu, Mwenyezi Mungu atamuua tu, wala hutap- ata atakayemponesha na kumpa uhai.

Na alikwishawajia Yusuf zamani kwa dalili zilizo wazi, lakini nyinyi mliendelea katika shaka kwa yale aliyowaletea.

Yaani enyi wamisr! Yusuf aliwajia mababa zenu, wakatia shaka utume wake; kama hivyo nanyi mnatia shaka utume wa Musa. Katika Kamusi ya Kitabu kitakatifu, imeelezwa kuwa Yusuf ni jina la kiibrania (Hebrew) lenye maana ya anayezidisha. Mama yake alimwita hivyo, ili apate ziada ya mtoto mwingine. Naye alikufa akiwa na miaka 110.

Mpaka alipokufa mkasema: Mwenyezi Mungu hataleta tena Mtume baada yake.

Hii inaashiria kuwa wao walifurahi kwa kufa Yusuf, kwa vile watakuwa huru na taklifa za Mwenyezi Mungu. Wakasema bila ya kujali, kwa msukumo wa matamanio kwamba Mwenyezi Mungu hatapeleka tena Mtume baada ya Yusuf mpaka Siku ya Mwisho.

Kama hivyo Mwenyezi Mungu humpoteza yule aliyepita kiasi mwenye shaka kuhusu Mwenyezi Mungu na haki. Mwenyezi Mungu anampoteza mwenye kupita kiasi, kwa sababu ametoka katika uongofu na akaingia kwenye upotevu kwa uchaguzi wake mbaya na upofu.

Wale ambao wanajadiliana katika Ishara za Mwenyezi Mungu bila ya dalili yoyote iliyowafikia.

Makusudio ya wale wanaojadiliana ni wale wenye kupita kiasi wenye shaka. Ishara za Mwenyezi Mungu ni dalili za umoja wake, unabii wa mananbii wake na hoja wazi. Maana ni kuwa wakosefu wanajibu hoja za Mwenyezi Mungu kwa matamanio yao na kuiga mababa zao.

Ni chukizo kubwa mbele ya Mwenyezi Mungu na mbele ya walioamini kujadili wakosefu bila ya ujuzi wala mwongozo au kitabu.

Hivi ndivyo Mwenyezi Mungu apigavyo chapa juu ya kila moyo wa jeuri anayejivuna.

Kiburi na kujidai ndio sababu hasa ya kupigwa chapa moyoni. Hilo limetegemezwa kwa Mwenyezi Mungu kwa vile Yeye ndiye aliyejaalia kiburi kuwa ndio sababu ya upofu wa moyo; sawa na alivyoujaalia ujinga kuwa ndio sababu ya kudangana na kuwa mbali na haki na akajaalia kusoma na kufanya utafiti ni sababu ya elimu na mwamko.

وَقَالَ فِرْعَوْنُ يَا هَامَانُ ابْنِ لِي صَرْحًا لَّعَلِّي أَبْلُغُ الْأَسْبَابَ ﴿٣٦﴾

36. Na Firauni akasema: Ewe Hamana! Nijengee mnara ili nipate kuzifikia njia.

أَسْبَابَ السَّمَاوَاتِ فَأَطَّلِعَ إِلَىٰ إِلَـٰهِ مُوسَىٰ وَإِنِّي لَأَظُنُّهُ كَاذِبًا وَكَذَٰلِكَ زُيِّنَ لِفِرْعَوْنَ سُوءُ عَمَلِهِ وَصُدَّ عَنِ السَّبِيلِ وَمَا كَيْدُ فِرْعَوْنَ إِلَّا فِي تَبَابٍ ﴿٣٧﴾

37. Njia za mbinguni ili nikamwone Mungu wa Musa. Na kwa hakika mimi bila ya shaka namjua kuwa ni mwongo tu. Na hivi ndivyo Firauni alivyopambiwa ubaya wa vitendo vyake, na akazuiliwa Njia. Na vitimbi vya Firauni havikuwa ila katika kuangamia tu.

وَقَالَ الَّذِي آمَنَ يَا قَوْمِ اتَّبِعُونِ أَهْدِكُمْ سَبِيلَ الرَّشَادِ ﴿٣٨﴾

38. Na yule ambaye aliamini alisema: Enyi watu wangu! Nifuateni, nitawaongoza njia ya uongofu.

يَا قَوْمِ إِنَّمَا هَـٰذِهِ الْحَيَاةُ الدُّنْيَا مَتَاعٌ وَإِنَّ الْآخِرَةَ هِيَ دَارُ الْقَرَارِ ﴿٣٩﴾

39. Enyi watu wangu! Hakika maisha haya ya dunia ni starehe yenye kupita tu, na hakika Akhera ndiyo nyumba ya daima.

مَنْ عَمِلَ سَيِّئَةً فَلَا يُجْزَىٰ إِلَّا مِثْلَهَا وَمَنْ عَمِلَ صَالِحًا مِّن ذَكَرٍ أَوْ أُنثَىٰ وَهُوَ مُؤْمِنٌ فَأُولَـٰئِكَ يَدْخُلُونَ الْجَنَّةَ يُرْزَقُونَ فِيهَا بِغَيْرِ حِسَابٍ ﴿٤٠﴾

40. Mwenye kutenda uovu hatalipwa ila sawa na huo, na mwenye kutenda wema, akiwa mwanamume au mwanamke, naye ni Muumini, basi hao wataingia Peponi, waruzukiwe humo bila ya hisabu.

NIZIFIKIE NJIA

Aya 36 – 40

MAANA

Na Firauni akasema: Ewe Hamana! Nijengee mnara ili nipate kuzifikia njia. Njia za mbinguni ili nikamwone Mungu wa Musa. Na kwa hakika mimi bila ya shaka namjua kuwa ni mwongo tu.

Firauni alimtaka waziri wake Hamana amjengee mnara mrefu ili apande mbinguni kwenda kumtafuta Mungu wa Musa. Alifanya hivi akiwa anajua kabisa kwamba yeye hawezi kufanya hivyo, lakini vile vile anajua kuwa katika anaowatawala kuna wenye akili fupi wasiokwa na mwamko, watakaomsadiki atakayosema. Kwani kauli yake hii sio kubwa zaidi ya kusema: Mimi ndie Mola wenu mkuuu; na asingejasiri kusema hivyo lau sikuweko watakaomwambia: ndio, wewe ndiye Mola mkuu.

Hivi sasa tukiwa katika karne ya ishirini, karne ya maendeleo hadi mtu kufika mwezini, lakini bado Dalai Lama anapata wanaomwambia: Wewe ni Mungu, na Agha Khan naye anapata wanaomwambia; Wewe ni nusu mungu. “Kila mahali kuna Al-kaaba na imam”

Na hivi ndivyo Firauni alivyopambiwa ubaya wa vitendo vyake, na akazuiliwa njia.

Mambo mawili yanampambia mtu matendo yake mabaya: Kufuata matamanio na kuendelea na ujinga. Matamanio yalimpambia Firauni kudai ungu na ujinga ukawapambia wanaomtii.

Na vitimbi vya Firauni havikuwa ila katika kuangamia tu; yaani katika hasara.

Kila aliyejaribu na atakayejaribu kuwahadaa watu na kuwafanyia vitimbi, atakuwa katika hasara; hata kama atakuwa na utawala wa Firauni na mali ya Qaruni.

Na yule ambaye aliamini alisema: Enyi watu wangu! Nifuateni, nitawaongoza njia ya uongofu.

Mumin aliwahadharisha watu wake mara ya kwanza na ya pili. Na hii sasa ni mara ya tatu anawahimiza wakubali nasaha zake, kwa sababu anataka kuwaokoa na wapate kheri. Lakini wengineo wanawaongoza kwenye shari na maangamizi.

Enyi watu wangu! Hakika maisha haya ya dunia ni starehe tu, na hakika Akhera ndiyo nyumba ya daima.

Starehe za dunia zitakwisha tu, hilo halina shaka, lakini maisha ya Akhera yatabakia daima. Basi ni maisha gani kati ya haya mawili yanayofaa kuyafanyia kazi? Katika Nahjul-balagha, imesemwa: “Anafanya nini na dunia aliyeumbiwa Akhera? Na anafanya nini na mali ambaye muda mchache atanyang’anywa na kubakia athari yake mbaya na hisabu yake?” Vile vile imesemwa: “Uchungu wa dunia ni tamu ya Akhera na tamu ya Akhera ni uchungu ya dunia/”

Mwenye kutenda uovu hatalipwa ila sawa na huo, na mwenye kutenda wema, akiwa mwanamume au mwanamke, naye ni Muumini, basi hao wataingia Peponi, waruzukiwe humo bila ya hisabu.

Mwenyezi Mungu ni mwadilifu mkarimu. Uadilifu wake unajitokeza kati- ka adhabu ya muovu. Hiyo mbele ya Mwenyezi Mungu inalingana sawa na malipo. Na hupunguza adhabu kwa huruma zake. Ama mwema huzidishiwa ziada nyingi bila ya hisabu, awe mwanamume au mwanamke. Pepo ni malipo tosha kabisa.

Aya inafahamisha wazi kuwa Pepo ni wakf hususi wa mwenye kumwamini Mwenyezi Mungu na siku ya mwisho, kwa imani isiyokuwa na shaka. Ama yule mwenye kufanya kheri kwa ajili ya kheri tu na huku anamkufuru Mwenyezi Mungu na siku ya mwisho, malipo yake yatakuwa sio Peponi, kwa sababu Pepo si ya makafiri. Tazama Juz. Juz. 4 (3:176 – 178), kifungu: ‘Kafiri na amali njema.’

Kuna mapokezi yanayosema kuwa Mtume(s.a.w. w ) amesema: “Hakufanya wema mwislamu au kafiri ila Mwenyezi Mungu humlipa.” Akaulizwa: Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu! Ni yapi malipo ya kafiri? Akasema: mali, watoto, afya nk. Akaulizwa: malipo yake akhera yatakuwa nini? Akasema: Ataadhibiwa adhabu ya chini”

وَيَا قَوْمِ مَا لِي أَدْعُوكُمْ إِلَى النَّجَاةِ وَتَدْعُونَنِي إِلَى النَّارِ ﴿٤١﴾

41. Na Enyi watu wangu! Kwa nini mimi ninawaita kwenye wokovu, nanyi mnaniita kwenye Moto?

تَدْعُونَنِي لِأَكْفُرَ بِاللَّـهِ وَأُشْرِكَ بِهِ مَا لَيْسَ لِي بِهِ عِلْمٌ وَأَنَا أَدْعُوكُمْ إِلَى الْعَزِيزِ الْغَفَّارِ ﴿٤٢﴾

42. Mnaniita nimkufuru Mwenyezi Mungu na nimshirikishe na yule ambaye simjui, nami ninawaita kwa Mwenye nguvu, Mwingi wa maghufira?

لَا جَرَمَ أَنَّمَا تَدْعُونَنِي إِلَيْهِ لَيْسَ لَهُ دَعْوَةٌ فِي الدُّنْيَا وَلَا فِي الْآخِرَةِ وَأَنَّ مَرَدَّنَا إِلَى اللَّـهِ وَأَنَّ الْمُسْرِفِينَ هُمْ أَصْحَابُ النَّارِ ﴿٤٣﴾

43. Bila ya shaka mnayeniitia, hastahiki wito duniani wala Akhera. Na hakika marejeo yetu ni kwa Mwenyezi Mungu. Na wanaopita kiasi basi hao ndio watu wa Motoni!

فَسَتَذْكُرُونَ مَا أَقُولُ لَكُمْ وَأُفَوِّضُ أَمْرِي إِلَى اللَّـهِ إِنَّ اللَّـهَ بَصِيرٌ بِالْعِبَادِ ﴿٤٤﴾

44. Basi mtayakumbuka ninayowaambia. Nami namkabidhi Mwenyezi Mungu mambo yangu. Hakika Mwenyezi Mungu ni mwenye kuwaona waja.

فَوَقَاهُ اللَّـهُ سَيِّئَاتِ مَا مَكَرُوا وَحَاقَ بِآلِ فِرْعَوْنَ سُوءُ الْعَذَابِ ﴿٤٥﴾

45. Basi Mwenyezi Mungu akamlinda na ubaya wa hila walizozifanya. Na adhabu mbaya itawazunguka watu wa Firauni.

النَّارُ يُعْرَضُونَ عَلَيْهَا غُدُوًّا وَعَشِيًّا وَيَوْمَ تَقُومُ السَّاعَةُ أَدْخِلُوا آلَ فِرْعَوْنَ أَشَدَّ الْعَذَابِ ﴿٤٦﴾

46. Wanaonyeshwa Moto asubuhi na jioni. Na itapofika Saa: Waingizeni watu wa Firauni katika adhabu kali kabisa!.

NINAWAITA KWENYE WOKOVU NYINYI MNANIITA KWENYE MOTO

Aya 41 – 46

MAANA

Na Enyi watu wangu! Kwa nini mimi ninawaita kwenye wokovu, nanyi mnaniita kwenye Moto? Mnaniita nimkufuru Mwenyezi Mungu na nimshirikishe na yule ambaye simjui, nami ninawaita kwa Mwenye nguvu Mwingi wa maghufira?

Maneno haya na yanayofuatia mpaka Hakika Mwenyezi Mungu ni mwenye kuwaona waja, anayasimulia Mwenyezi Mungu kuhusu mumin anayetoa nasaha.

Maana ni, niambieni enyi washirikina kuhusu hali yangu na nyinyi. Mimi nawalingania kwenye kheri itakayowaokoa na adhabu na maangamizi; ambayo ni kumwamini Mwenyezi Mungu mwenye nguvu asiyekuwa na mfano na yoyote; na mwenye kumsamehe anayetubia na kurejea Kwake; na nyinyi mananiita kwenye adhabu ya kuungua na kwenye shirki asiyoisamehe Mwenyezi Mungu wala kuingia akilini. Haifuati isipokuwa mwenye kupotea njia.

Bila ya shaka mnayeniitia, hastahiki wito duniani wala Akhera.

Bila shaka yule mnayenitaka nimwabudu, kama Firauni na mwenginewe, hana faida yoyote duniani na Akhera:

إِن تَدْعُوهُمْ لَا يَسْمَعُوا دُعَاءَكُمْ وَلَوْ سَمِعُوا مَا اسْتَجَابُوا لَكُمْ وَيَوْمَ الْقِيَامَةِ يَكْفُرُونَ بِشِرْكِكُمْ ﴿١٤﴾

“Mkiwaomba, hawasikii maombi yenu. Na wakisikia hawajibu. Na Siku ya Kiyama watakataa shirki yenu.” Juz. 22 (35:14).

Na hakika marejeo yetu ni kwa Mwenyezi Mungu.

Kila kiumbe kitarudi kwa Mwenyezi Mungu kesho, sio kwa Firauni wala kwa mwenginewe. Watasimama wote mbele ya Mwenyezi Mungu kwa ajili ya hisabuna malipo na wanaopita kiasi basi hao ndio watu wa Motoni!

Amenukuu Tabari na Razi kutoka kwa Mujahid, kwamba makusudio ya wanaopita kiasi hapa ni waliomwaga damu bila ya haki.

Basi mtayakumbuka ninayowaambia yale ya ukweli na nasaha pale mtakapoona adhabu na kuwashukia balaa Nami namkabidhi Mwenyezi Mungu mambo yangu. Hakika Mwenyezi Mungu ni mwenye kuwaona waja.

Muhyiddin Bin Arabi anasema katika Futuhatil-makkiyya kuwa neno ufawwidhu (tulilolifasiri kwa maana ya kutegemeza), limechukuliwa kutoka neno fadha lenye maana ya kumimina chombo kikiwa kimejaa na hakiwezi kuchukua ziada.

Kwa hiyo mumin akibebeshwa zaidi ya uwezo wake, huipeleka ile ziada kwa Mwenyezi Mungu, naye Mwenyezi Mungu (s.w.t) hupokea ziada hiyo na kumpunguzia mzigo mumin. Na yeye Mwenyezi Mungu Mtukufu ni mjuzi na mwenye kumuona mwenye kuamini na akamtegemea na yule anayeelekea kwingine.

Basi Mwenyezi Mungu akamlinda na ubaya wa hila walizozifanya. Na adhabu mbaya itawazunguka watu wa Firauni.

Firauni alimdhamiria ubaya Musa na mumin mwenye kutoa nasaha, Mwenyezi Mungu akawaokoa na vitimbi vyake, akaangamia Firauni na watu wake kwenye maji. Namna hii Mwenyezi Mungu (s.w.t) anawaondolea ubaya wenye ikhlasi, na majanga yanawarudia viongozi wa uhaini. Hii ni kabla ya mauti.

Ama baada ya mauti, basi wanaonyeshwa Moto asubuhi na jioni.

Kuna riwaya iliyopokewa kutoka kwa Imam Ja’far Assadiq(a.s ) akisema:Hiyo itakuwa baada ya mauti na kabla ya Kiyama. Kwa sababu siku hiyo haitakuwa na asubuhi wala jioni. Lau angeliadhibiwa mwenye hatia asubihi na jioni tu, basi ingelikuwa afadhali kwake.

Na itapofika Saa ya Kiyama patasemwa: Waingizeni watu wa Firauni katika adhabu kali kabisa!

Kila mkosefu ataambiwa Siku ya Kiyama: Ingia Jahannam na ni marejeo mabaya; ni sawa awe ni katika watu wa Firauni au wengineo. Mwenyezi Mungu (s.w.t) amehusu kutaja Firauni kwa sababu mazungumzo yanamuhusu yeye hivi sasa.