TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI Juzuu 22

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI0%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: Qurani tukufu

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI

Mwandishi: Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya
: HASANI MWALUPA
Kundi:

Matembeleo: 19751
Pakua: 2115


Maelezo zaidi:

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 29 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 19751 / Pakua: 2115
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI Juzuu 22

Mwandishi:
Swahili

11

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI

إِنَّ الَّذِينَ قَالُوا رَبُّنَا اللَّـهُ ثُمَّ اسْتَقَامُوا تَتَنَزَّلُ عَلَيْهِمُ الْمَلَائِكَةُ أَلَّا تَخَافُوا وَلَا تَحْزَنُوا وَأَبْشِرُوا بِالْجَنَّةِ الَّتِي كُنتُمْ تُوعَدُونَ ﴿٣٠﴾

30. Hakika wale ambao wamesema: Mola wetu ni Mwenyezi Mungu! Kisha wakawa na msimamo. Huwateremkia Malaika: Msiwe na hofu, wala msihuzunike; nanyi furahini kwa Pepo mliyokuwa mkiahidiwa.

نَحْنُ أَوْلِيَاؤُكُمْ فِي الْحَيَاةِ الدُّنْيَا وَفِي الْآخِرَةِ وَلَكُمْ فِيهَا مَا تَشْتَهِي أَنفُسُكُمْ وَلَكُمْ فِيهَا مَا تَدَّعُونَ ﴿٣١﴾

31. Sisi ni mawalii wenu katika maisha ya dunia na katika Akhera, na humo mtapata kinachotamaniwa na nafsi zenu, na humo mtapata mtakavyovitaka.

نُزُلًا مِّنْ غَفُورٍ رَّحِيمٍ ﴿٣٢﴾

32. Ni takrima itokayo kwa mwingi wa Maghufira, Mwenye kurehemu.

وَمَنْ أَحْسَنُ قَوْلًا مِّمَّن دَعَا إِلَى اللَّـهِ وَعَمِلَ صَالِحًا وَقَالَ إِنَّنِي مِنَ الْمُسْلِمِينَ ﴿٣٣﴾

33. Na ni nani mbora wa kusema kuliko aitaye kwa Mwenyezi Mungu na akatenda mema, na akasema: Hakika mimi ni katika Waislamu?

وَلَا تَسْتَوِي الْحَسَنَةُ وَلَا السَّيِّئَةُ ادْفَعْ بِالَّتِي هِيَ أَحْسَنُ فَإِذَا الَّذِي بَيْنَكَ وَبَيْنَهُ عَدَاوَةٌ كَأَنَّهُ وَلِيٌّ حَمِيمٌ ﴿٣٤﴾

34. Mema na maovu hayawi sawa. Zuia uovu kwa lilio jema zaidi. Mara yule ambaye baina yako naye pana uadui atakuwa kama rafiki mkubwa.

وَمَا يُلَقَّاهَا إِلَّا الَّذِينَ صَبَرُوا وَمَا يُلَقَّاهَا إِلَّا ذُو حَظٍّ عَظِيمٍ ﴿٣٥﴾

35. Lakini hawapewi hayo ila wanaosubiri, wala hawapewi ila wenye bahati kubwa.

وَإِمَّا يَنزَغَنَّكَ مِنَ الشَّيْطَانِ نَزْغٌ فَاسْتَعِذْ بِاللَّـهِ إِنَّهُ هُوَ السَّمِيعُ الْعَلِيمُ ﴿٣٦﴾

36. Na kama Shetani akikuchochea kwa uchochezi basi jikinge kwa Mwenyezi Mungu. Hakika Yeye ni Mwenye kusikia, Mwenye kujua.

WALISEMA MOLA WETU NI MWENYEZI MUNGU KISHA WAKAWA NA MSIMAMO

Aya 30 – 36

MWENYEZI MUNGU NA MTU NA MATENDO

Mwenye kufuatilia Aya za Qur’ani yenye hekima, atakuta kwamba mantiki yake yote na ufahamu wake unajulisha kuwa matendo na imani ndio kila kitu kwa mtu. Hebu angalia dalili zifuatazo:

1. Aya zinazofahamisha kuwa lengo la kwanza na hekima kubwa ya kuweko mtu ni kutenda mambo mema; miongoni mwa Aya hizo ni:

الَّذِي خَلَقَ الْمَوْتَ وَالْحَيَاةَ لِيَبْلُوَكُمْ أَيُّكُمْ أَحْسَنُ عَمَلًا وَهُوَ الْعَزِيزُ الْغَفُورُ ﴿٢﴾

“Ambaye ameumba mauti na uhai ili kuwajaribu ni nani miongoni mwenu mwenye vitendo vizuri zaidi” (67:2).

Tazama Juz. 21 (31:33) kifungu ’Kwa nini Mungu akamuumba mtu?’

2. Aya zinazofahamisha kuwa matendo ndio mizani ya kumpima mtu kwenye msingi wake; mfano kauli hizi za Mwenyezi Mungu mtukufu:

كُلُّ امْرِئٍ بِمَا كَسَبَ رَهِينٌ ﴿٢١﴾

“Kila mtu atalipwa alichokichuma” (52:21)

وَمَا تُجْزَوْنَ إِلَّا مَا كُنتُمْ تَعْمَلُونَ ﴿٣٩﴾

“Na hamtalipwa ila mliyokuwa mkiyafanya” Juz. 23 (37:39)

وَلِكُلٍّ دَرَجَاتٌ مِّمَّا عَمِلُوا وَمَا رَبُّكَ بِغَافِلٍ عَمَّا يَعْمَلُونَ ﴿١٣٢﴾

“Na wote wana daraja mbalimbali kutokana na yale waliyoyatenda” (Juz. 8 (6:132) na nyinginezo.

3. Ama kauli yake Mwenyezi mungu Mtukufu:Hakika wale ambao wamesema: Mola wetu ni Mwenyezi Mungu! Kisha wakawa na msimamo, ni dalili wazi na mkataa kwamba vitendo ndio dhahiri ya pekee inayoakisi imani ya kweli ya Mwenyezi Mungu iliyo halisi na kwamba yeyote mwenye kusema kuwa mimi ni mumin bila ya kuitafsiri imani yake kwa vitendo katika mfungamano wake na wa muumba wake na nafsi yake na jamii yake, basi huyo atakuwa ni muongo mzushi.

Kuongezea zaidi ni kuwa makusudio ya Qur’ani kuhusu matendo ni matendo ya kujenga yenye kuzaa matunda. Tumezungumzia kwa ufafanuzi zaidi kuhusu msimamo katika Juz. 12 (11: 110 – 115) kifungu cha ’Msimamo.’

4. Zaidi ya yote ni kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) amefahamisha kuweko kwake na utukufu wake kwa matendo. Anasema:

سَنُرِيهِمْ آيَاتِنَا فِي الْآفَاقِ وَفِي أَنفُسِهِمْ حَتَّىٰ يَتَبَيَّنَ لَهُمْ أَنَّهُ الْحَقُّ ﴿٥٣﴾

“Tutawaonyesha Ishara zetu katika upeo wa mbali na katika nafsi zao mpaka iwabainikie kwamba haya ni kweli.” (41:53)

Kisha akataja Mwenyezi Mungu (s.w.t) Aya kadhaa zinazohusiana na haya, tutatosheka na hizi tu:

خَلَقَ الْإِنسَانَ ﴿٣﴾ عَلَّمَهُ الْبَيَانَ ﴿٤﴾ الشَّمْسُ وَالْقَمَرُ بِحُسْبَانٍ ﴿٥﴾

“Amemuumba mtu, akamfundisha kubaini. Jua na mwezi (huenda) kwa hisabu” (55:3-5).

Huwateremkia Malaika wakawaambia: Msiwe na hofu, wala msihuzunike; nanyi furahini kwa Pepo mliyokuwa mkiahidiwa.

Kila jambo lina muda maalum. Utakapokuja muda wa wale waliokuwa na msimamo katika njia ya Mwenyezi Mungu, Malaika watawateremkia na rehema kwa utulivu na habari njema kwamba Mwenyezi Mungu ameyaona matendo yao na kuridhia mahangaiko yao. Kwa hiyo amewaandalia makazi ya heshima aliyowaahidi kupitia kwa manabi na mitume wake.

Sisi ni mawalii wenu katika maisha ya dunia na katika Akhera, na humo mtapata kinachotamaniwa na nafsi zenu, na humo mtapata mtakavyovitaka.

Ni takrima itokayo kwa Mwingi wa maghufira, Mwenye kurehemu.

Bado yanaendelea mazungumzo baina ya Malaika wa rehema na wale waliokuwa na msimamo. Yaani watiifu na wenye msimamo watakuwa kwa Mola wao Mwenye kurehemu na watapata kila wakitakacho kutokana na riziki ya ukarimu.

Ibn Al-arabi katika Futahitil-Makkiya anasema kuhusu Aya hii, kwamba Malaika watawaambia wenye ikhlasi kabla ya kutoka kwenye makazi ya kuisha kwenda kwenye makazi ya kudumu: Sisi tumekuwa mawalii wenu duniani kwa sababu shetani aliwajaribu kuwahadaa muache njia iliyonyooka na sisi tukiwakataza na mlikuwa mkitusikiliza. Vile vile sisi ni mawalii wenu Akhera kwa sababu tunawatolea ushahidi wa imani na msimamo mbele ya Mwenyezi Mungu.

Na ni nani mbora wa kusema kuliko aitaye kwa Mwenyezi Mungu na akatenda mema, na akasema: Hakika mimi ni katika Waislamu?

Tukiunganisha Aya hii na ile isemayo “Hakika wale ambao wamesema: Mola wetu ni Mwenyezi Mungu kisha wakawa na msimamo,” tutapata maana kuwa imani ya kweli iko sehemu tatu: Kwanza, kutangaza kumwamini Mwenyezi Mungu. Pili, kutenda kwa mujibu wa sharia ya Mwenyezi Mungu. Na matendo yaliyo muhimu na adhimu zaidi ni kuwahudumia watu. Tatu, ni kutoa mwito wa Mwenyezi Mungu.

I. Ya kwanza inafahamishwa na kauli: “Wale ambao wamesema Mola wetu ni Mwenyezi Mungu;” yaani wamelitangaza hilo mbele ya watu.

II. Ya pili inafahamishwa na kauli: “Kisha wakawa na msimamo.”

III. Na ya tatu: “Aitaye kwa Mwenyezi Mungu.” Mwenye kukusanya sifa tatu hizi anayo haki ya kusema “Hakika mimi ni katika Waislamu.” Lakini atakayesema hivyo bila ya kumwamini Mwenyezi Mungu au amemuamini Mwenyezi Mungu bila ya kuwahudumia watu na bila ya kulingania kwa Mwenyezi Mungu, basi huyo si Mwislamu kitu; ingawaje duniani anachukuliwa kama Mwislamu.

Mema na maovu hayawi sawa. Zuia uovu kwa lilio jema zaidi. Mara yule ambaye baina yako naye pana uadui atakuwa kama rafiki mkubwa.

Makusudio ya mema hapa ni mema ya mjumbe anayelingania kwa Mwenyezi Mungu ambayo ni jihadi yake na uvumilivu wake wa maudhi kwenye njia hii. Na makusudio ya uovu ni uovu wa safihi aliye mjinga wa dini.

Maana ni kuwa tofauti ni kubwa baina yako wewe Muhammad, ukiwa unalingania kwa Mwenyezi Mungu na unavumilia maudhi kwa kutaka radhi ya Mwenyezi Mungu, na yule ambaye ameitika mwito wako kwa upinzani, maudhi na kukuzulia. Matendo yako ni baraka na wema na matendo yao ni uovu na laana. Lakini pamoja na yote hayo ni juu yako kuwachukulia kwa upole na kuwasamehe, ukivumilia usafihi wao, kwani miongoni mwao wako ambao lau utawakabili kwa namna hii basi wanaweza kurudi kwa Mola wao na uadui ukageuka kuwa mahaba na chuki ikawa mapenzi.

Mtu yeyote anaweza kupata marafiki watakaomsaidia kwa maneno mazuri na anaweza kujitengenezea maadui kwa maneno machafu. Maneno ya watu wema yameweza kuwaongoza waovu wengi na kutatua matatizo mengi. Lau si hayo basi mito ingelijaa damu.

Lakini hawapewi hayo ila wanaosubiri, wala hawapewi ila wenye bahati kubwa.

Hayo ni hayo ya kuzuia uovu kwa wema. Mwenye bahati kubwa ni yule anayeridhiwa mbele ya Mwenyezi Mungu. Maana ni kuwa kuzuia uovu kwa wema ni daraja kubwa ambayo haipati isipokuwa mwenye kuwa mvumilivu wa shida na akawa ana mwelekeo wa Mwenyezi Mungu.

Kwenye Nahjul-balagha imesemwa:“Subira katika imani ni kama kichwa katika mwili. Hakuna kheri katika mwili usiokuwa na kichwa wala katika imani isiyokuwa na subira.” Imesemwa tena:“Iondoe shari iliyoko kifuani kwa mwenzako kwa kuing’oa kifuani mwako.”

Na kama Shetani akikuchochea kwa uchochezi basi jikinge kwa Mwenyezi Mungu. Hakika Yeye ni Mwenye kusikia, Mwenye kujua.

Maneno yanaelekezwa kwa Muhammad(s.a.w. w ) . Tukiibia Aya ufahamu wake ni kuwa inapaswa mtu achukue hadhari wala asijione ni msafi hata akiwa na dini, elimu au akili kiasi gani. Imetangulia kwa herufi zake katika Juz. 9 (7:200).

12

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI

وَمِنْ آيَاتِهِ اللَّيْلُ وَالنَّهَارُ وَالشَّمْسُ وَالْقَمَرُ لَا تَسْجُدُوا لِلشَّمْسِ وَلَا لِلْقَمَرِ وَاسْجُدُوا لِلَّـهِ الَّذِي خَلَقَهُنَّ إِن كُنتُمْ إِيَّاهُ تَعْبُدُونَ ﴿٣٧﴾

37. Na katika Ishara zake ni usiku na mchana, na jua na mwezi. Msilisujudie jua wala mwezi, bali msujudieni Mwenyezi Mungu aliyeviumba, ikiwa nyinyi mnamuabudu Yeye tu.

فَإِنِ اسْتَكْبَرُوا فَالَّذِينَ عِندَ رَبِّكَ يُسَبِّحُونَ لَهُ بِاللَّيْلِ وَالنَّهَارِ وَهُمْ لَا يَسْأَمُونَ ﴿٣٨﴾

38. Na ikiwa watafanya kiburi, basi hao walioko kwa Mola wako wanamtakasa Yeye usiku na mchana, na wao hawachoki.

وَمِنْ آيَاتِهِ أَنَّكَ تَرَى الْأَرْضَ خَاشِعَةً فَإِذَا أَنزَلْنَا عَلَيْهَا الْمَاءَ اهْتَزَّتْ وَرَبَتْ إِنَّ الَّذِي أَحْيَاهَا لَمُحْيِي الْمَوْتَىٰ إِنَّهُ عَلَىٰ كُلِّ شَيْءٍ قَدِيرٌ ﴿٣٩﴾

39. Na katika Ishara zake ni kwamba unaiona ardhi imetulia, lakini tunapoiteremshia maji mara unaiona inashtuka na kututumka. Bila ya shaka aliyeihuisha ardhi ndiye atakayehuisha wafu. Hakika Yeye ni Muweza juu ya kila kitu.

إِنَّ الَّذِينَ يُلْحِدُونَ فِي آيَاتِنَا لَا يَخْفَوْنَ عَلَيْنَا أَفَمَن يُلْقَىٰ فِي النَّارِ خَيْرٌ أَم مَّن يَأْتِي آمِنًا يَوْمَ الْقِيَامَةِ اعْمَلُوا مَا شِئْتُمْ إِنَّهُ بِمَا تَعْمَلُونَ بَصِيرٌ ﴿٤٠﴾

40. Hakika wale ambao wanaupotoa ukweli uliomo katika Ishara zetu hawatufichikii Sisi. Je, Atakayetupwa Motoni ni bora au atakayekuja kwa amani Siku ya Kiyama? Tendeni mpendavyo, kwa hakika Yeye anayaona mnayoyatenda.

إِنَّ الَّذِينَ كَفَرُوا بِالذِّكْرِ لَمَّا جَاءَهُمْ وَإِنَّهُ لَكِتَابٌ عَزِيزٌ ﴿٤١﴾

41. Hakika wale ambao wanakataa dhikiri inapowajia. Na hayo bila ya shaka ni Kitabu chenye nguvu.

لَّا يَأْتِيهِ الْبَاطِلُ مِن بَيْنِ يَدَيْهِ وَلَا مِنْ خَلْفِهِ تَنزِيلٌ مِّنْ حَكِيمٍ حَمِيدٍ ﴿٤٢﴾

42. Hautakifikia upotovu mbele yake wala nyuma yake. Kimeteremshwa na Mwenye hikima, Msifiwa.

مَّا يُقَالُ لَكَ إِلَّا مَا قَدْ قِيلَ لِلرُّسُلِ مِن قَبْلِكَ إِنَّ رَبَّكَ لَذُو مَغْفِرَةٍ وَذُو عِقَابٍ أَلِيمٍ ﴿٤٣﴾

43. Haambiwi ila yale yale waliyoambiwa Mitume wa kabla yako. Hakika Mola wako bila ya shaka ni Mwenye maghufira, na ni Mwenye adhabu chungu.

وَلَوْ جَعَلْنَاهُ قُرْآنًا أَعْجَمِيًّا لَّقَالُوا لَوْلَا فُصِّلَتْ آيَاتُهُ أَأَعْجَمِيٌّ وَعَرَبِيٌّ قُلْ هُوَ لِلَّذِينَ آمَنُوا هُدًى وَشِفَاءٌ وَالَّذِينَ لَا يُؤْمِنُونَ فِي آذَانِهِمْ وَقْرٌ وَهُوَ عَلَيْهِمْ عَمًى أُولَـٰئِكَ يُنَادَوْنَ مِن مَّكَانٍ بَعِيدٍ ﴿٤٤﴾

44. Na lau tungeliifanya Qur’ani kwa lugha ya kigeni wangelisema: Kwa nini Aya zake hazikupambanuliwa? Yawaje lugha ya kigeni na mwarabu? Sema: Hii Qur’ani ni uwongofu na ponyo kwa wenye kuamini. Na wasioamini umo uziwi katika masikio yao, nayo kwao imezibwa hawaioni. Hao wanaitwa nao wako mahali mbali.

وَلَقَدْ آتَيْنَا مُوسَى الْكِتَابَ فَاخْتُلِفَ فِيهِ وَلَوْلَا كَلِمَةٌ سَبَقَتْ مِن رَّبِّكَ لَقُضِيَ بَيْنَهُمْ وَإِنَّهُمْ لَفِي شَكٍّ مِّنْهُ مُرِيبٍ ﴿٤٥﴾

45. Na hakika tulimpa Musa Kitabu, lakini pakatokea hitilafu kati yake. Na lau kuwa halikwishatangulia neno la Mola wangelihukumiwa. Na hakika wao wamo katika shaka nayo yenye kuwatia wasiwasi.

مَّنْ عَمِلَ صَالِحًا فَلِنَفْسِهِ وَمَنْ أَسَاءَ فَعَلَيْهَا وَمَا رَبُّكَ بِظَلَّامٍ لِّلْعَبِيدِ ﴿٤٦﴾

46. Anayetenda mema basi anajitendea mwenyewe, na anayetenda uovu basi ni juu ya yake; na Mola wako si mwenye kuwadhulumu waja.

HAUTAKIFIKIA UPOTOVU MBELE YAKE WALA NYUMA YAKE

Aya 37 – 46

SAFARI YA MWEZINI

Na katika Ishara zake ni usiku na mchana, na jua na mwezi.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) ametaja, katika Kitabu chake Kitukufu, Aya kadhaa za kilimwengu na zinavyomfahamisha Muumba na sifa Zake. Miongoni mwa Aya hizo ni zile za kutofautiana usiku na mchana, kuumbwa jua na mwezi n.k. Tazama Juz. 3 (3:27) Juz. 23 (36:37 – 40) na (39:5). Humo mumetajwa usiku, mchana, jua na mwezi.

Kutokana na kutajwa mwezi tutaashiria tukio muhimu lilitokea ulimwenguni la safari ya anga za mbali ya waamerika wawili Neil Amstrong na Edwin kwenda mwezini, katika majira ya kiangazi ya mwaka 1969. Watu walilizungumzia sana tukio hili na wengi wakaniuliza kuhusu maoni ya dini kuhusiana na safari hii. Nikajibu kwa makala iliyosambazwa magazetini, kisha nikaiunganisha na Tafsir Al-kashif kulingana na Aya zinazotaja mwezi. Basi kabla ya kuchapishwa tafsiri, mfanyakazi mmoja wa kiwanda cha uchapishaji akanishauri niiondoe makala hiyo, nami nikakubali bila ya kujua sababu.

Baada ya kupita muda mchache tangu kuchapishwa Tafsir Al-kashif , ikanibainikia kuwa ilikuwa vizuri sikuweka makala hiyo kwenye Tafsiri. Hiyo ilitokana na kuwa nilisoma kwenye gazeti la Al-akhabar la Misr la 6-2-1970, makala, iliyofasiriwa kutoka kwenye gazeti la Pravda la Urusi, ya wanasayansi wawili wa kirusi, Mikhail Vassin na Alexander Cherbakov.

Wataalamu hawa wawili walichunguza matokeo waliyoyatangaza wamarekani katika uchunguzi wao wa mchanga wa mwezini na madini yaliyopatikana kwenye ardhi ya mwezi, wakasema: “Somo hili linakataa nadharia zote zilizoenea kuhusiana na asili ya mwezi, wala halikubali isipokuwa tafsiri moja tu; kwamba mwezi umetengenezwa kwa usanii wa hali ya juu wenye mpangilio. Na iliyoutengeneza ni nguvu ya ajabu yenye uwezo usioweza kufikiwa na chochote.”

Hii inamaanisha kwamba wanavyoamini wamaada kuhusu ulimwengu ni njozi tu. Makala hii inaendelea kusema: “Uchunguzi wa kielimu wa kisasa unakataa nadharia zote na makisio yote kuhusu chanzo cha mwezi na kuan- za fikra mpya ya kutatua kitandawili hiki inayosema: Usanii wa mwezi umetokana na kitu kilichoendelea sana kielimu na kifani, kisha kikaunda harakati ya mwezi kwa vifaa vilivyoendela sana. Ndani ya mwezi kuna mamabo ya ajabu yasiyowezakana kupatikana kwa sadfa.”

Gamba la nje la mwezi liko na tabaka mbili za kimsingi: ya kwanza ni tabaka ya kutenganisha joto lenye unene wa 4 km. La pili lina unene wa 300 km. Juu yake kuna aina mbalimbali ya vifaa vilivyoundwa kuzuia mtingishiko. Kwa hiyo mwezi unaweza kuhimili safari bila ya kuondoka sehemu yake kwa mamilioni ya mamilioni ya miaka.”

Lakini kuna swali linataka majibu: Ikiwa mwezi umetengenezwa na kitu chenye akili iliyoendela, basi kitu hiki kimetoka wapi? Kwa nini kikafanya bidii ya kutengenza sayari hii? Ni kwa ajili ya kuzunguka kwenye sayari tu basi?

Nadharia ya kisasa haiwezi kujibu swali hili. Lakini inaamini kuwa makisio ya karibu zaidi kuliko jambo lolote ni kuwa mwezi umetengenezwa na kwamba mtenegenzaji wake amekuwa na mpangilio wa kiajabu.”

Wakomonisti wawili wanasema: “Akili inakataa makadirio na tafsiri yoyote isipokuwa moja tu, kwamba mwezi umetengenezwa na ilioutengeneza ni nguvu ya ajabu.”

Ndio! Ni kweli umetengenezwa, na mtengenezaji wake hana mshirika wala wa kufanana naye. Uhandisi wake ndio uliotuongoza kujua hilo.

Ama kauli ya wataalamu wawili kuwa umetengenezwa na kitu kilichoendelea sana na mfumo wake ni wa ajabu sana, kauli hii ni kukiri waziwazi kwamba kwenye mwezi kuna mpangilio ambao hauwezi kutokea kwa yeyote isipokuwa kwa aliye Muweza, Mwenye hekima ambaye hana mfano na chochote naye ni Muumba aliye Mjuzi.

Tuna uhakika kwamba hivi karibuni tutasoma kukiri wazi zaidi ya hivi, kutakakovunja kauli za wamaada na nadharia za walahidi. Na itathibitika kwa hisia na majaribio kwamba nyuma ya ulimwengu huu kuna nguvu inayoshinda nguvu zote inayokiamabia kitu kuwa na kikawa.

Hili haliwezi kuepukwa na maendeleo ya elimu na akili huru. Hapa ndio inakuwa siri ya kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu:

أَوَلَمْ يَنظُرُوا فِي مَلَكُوتِ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ وَمَا خَلَقَ اللَّـهُ مِن شَيْءٍ ﴿١٨٥﴾

“Je, hawatazami ufalme wa mbingu na ardhi na alivyoviumba Mwenyezi Mungu?”

Juz. 9 (7:185).

إِنَّ فِي ذَٰلِكَ لَآيَاتٍ لِّقَوْمٍ يَعْقِلُونَ ﴿٤﴾

“Hakika katika hayo kuna ishara kwa watu wanotia akilini (mambo).” Juz. 13 (13:4)

هَـٰذَا خَلْقُ اللَّـهِ فَأَرُونِي مَاذَا خَلَقَ الَّذِينَ مِن دُونِهِ بَلِ الظَّالِمُونَ فِي ضَلَالٍ مُّبِينٍ ﴿١١﴾

“Huu ni uumbaji wa Mwenyezi Mungu. Basi nionyesheni wameumba nini hao wasiokuwa Yeye?” Juz. 21 (31:11)

Msilisujudie jua wala mwezi, bali msujudieni Mwenyezi Mungu aliye- viumba, ikiwa nyinyi mnamuabudu Yeye tu.

Aliyeviumba, ni aliyeumba usiku, mchana, jua na mwezi au aliyeumba sayari na nyota zote. Mwenyezi Mungu (s.w.t) ameleta ibara ya jua na mwezi, kwa sababu ndivyo vilivyojitokeza zaidi kwa watu.

Mafakihi wameafikiana kwa kauli moja kwamba ni wajibu kusujudu kwa mwenye kuisoma au kuisikia Aya hii. Wengine wakasema, bali hata aliyesikia bila ya kukusudia pia atasujudu.

Aya inawaambia wasabai, walioabudu nyota, kutokana na manufaa yake, kuwa Mwenyezi Mungu ndiye ambaye ameumba sayari na akazifanya ziwe na manufaa kwa waja, nazo ni viumbe tu kama sisi, zinamwelekea Mwenyezi Mungu Mtukufu kwa kumsujuduia na kukubali utumishi.

Na ikiwa watafanya kiburi, basi hao walioko kwa Mola wako wanam- takasa Yeye usiku na mchana, na wao hawachoki.

Yaani ikiwa hao waabudu nyota watang’ang’ania ushirikina, basi Mwenyezi Mungu hana haja nao wala ibada yao, kwa sababu anao waja – Malaika – hawaachi kumsabihi Mwenyezi Mungu usiku na mchana.

Na katika Ishara zake ni kwamba unaiona ardhi imetulia, lakini tunapoiteremshia maji mara unaiona inashtuka na kututumka. Bila ya shaka aliyeihuisha ardhi ndiye atakayehuisha wafu. Hakika Yeye ni Muweza juu ya kila kitu.

Maana haya yamekaririka kwenye Aya kadhaa na kwa mifumo mbali mbali; miongoni mwazo ni: Juz. 17 (22:5)

Hakika wale ambao wanaupotoa ukweli uliomo katika Ishara zetu hawatufichikii sisi.

Washirikina waliitia ila Qur’ani wakasema ni uchawi na wakasema ni ngano, lakini Mwenyezi Mungu anajua kauli zao na atawauliza nazo na kuwaadhibu.

Je, Atakayetupwa Motoni ni bora au atakayekuja kwa amani Siku ya Kiyama?

Swali hili linabeba jawabu lake. Ni nani mwenye akili anayeweza kusema moto ni bora kuliko pepo au hofu ni nzuri kuliko amani? Lakini wakosefu wameghafilika na msingi huu, na wao hasa wameathirika na moto kuliko pepo na hofu kuliko amani.

Tendeni mpendavyo, kwa hakika Yeye anayaona mnayoyatenda.

Hii ni hadhri na onyo kwamba wao watakutana na adhabu baada ya kuifu- ata kwa njia ya kufuru na upotevu.

Hakika wale ambao wanakataa dhikiri inapowajia.

Makusudio ya dhikiri hapa ni Qur’ani. Hapa kuna maneno ya kukadiriwa, kuwa wataadhibiwa.

ISRAIL NA QUR’AN

Na hayo bila ya shaka ni Kitabu chenye nguvu. Hautakifikia upotovu mbele yake wala nyuma yake. Kimeteremshwa na Mwenye hikima, Msifiwa.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) ameisifu Qur’ani kuwa ina nguvu na kwamba haifikiwi na upotofu wowote. Maana ya kuwa na nguvu ni nguvu za hoja zake na dalili zake zilizo wazi. Ama kuwa haifikiwi na upotovu, wafasiri wametaja njia tano; iliyokaribu zaidi ni ile isemayo kuwa kila itikadi, sharia habari na mengineyo yaliyomo ndani yake ni haki isiyokuwa na shaka.

Yametangulia maelezo kwa ufafanuzi zaidi katika Juz.14 (15:9). Huko tumeeleza kuwa Israili ilichapisha maelfu ya nakala za Qur’ani na kuziko-roga baadhi ya Aya zake; mfano ile isemayo: “Na mwenye kutaka dini isiyokuwa Uislamu haitakubaliwa kwake.” Juz. 3 (3:85), wakaandika: “Na mwenye kutaka dini isiyokuwa Uislamu itakubaliwa kwake.” Hili lilitokea mwaka 1968. Chuo kiku cha Al-azhar kilikusanya nakala hizi na kuzizuia zisisambae.

Israil ikarudia tena mnamo mwaka 1969 na ikakoroga Aya nyingine: “Walisema Mayahudi: Mkono wa Mwenyezi Mungu umefumba. Mikono yao ndiyo iliyofumba, na wamelaaniwa kwa waliyoyasema.” Juz. 6 (5:64), wakabadilisha neno ‘wamelaaniwa’ likawa ‘wameamini.’ Nakala hizi za Qur’ani ya kiisrail zikaenea kwenye maduka ya Lebanon na kwenye miji mingi ya Uarabuni. Pia ilisambazwa huko Malesia, Pakistan, India, Indonasia, Guinea, Ivory coast (Cote de vory) Iran n.k.

Leo hii tarehe 25-2-1970. Gazeti la An-nahar la Beirut limeandika kuwa wakili Faruq Sa’d amepeleka mshtaka kwa niaba ya Ofisi na wachapishaji wa Mash-had Alhusayniy ya Cairo ya kumtia hatiani mwenye kuivuruga Qur’ani Takufu, kuiiga, kuipotoa na kuirekebesha. Pia limeandika kwamba nakala za kupotoshwa zimechapisha Ujerumani Magharibi na wachapishaji wa Cologne – Doits.

Israil haikutosheka hapa na vita vyake dhidi ya Uislamu na waislamu, wakaitangaza Qur’ani ya kukorogwa kwenye idhaa yake. Idhaa ya Cairo ilitumia mwezi mzima kurikodi Qur’ani kutoka idhaa ya Israil.

Vile vile Israil imetengeneza radio ya mkono wanayoiuza kwa bei rahisi kabisa, ambayo haishiki idhaa yoyote isipokuwa idhaa yake inayopotosha Qur’ani tu. Israili inafanya yote haya na mengineyo kwa kuitikia msingi wa kizayui alioutangaza mmoja wa viongozi wake, aliposema: “Ni lazima tuifanye Qur’ani ni silaha ya kuwamaliza waislamu.”

Tumeyaeleza yote haya kama mfano wa vita vya Israil dhidi ya Uislam, ili pengine waweze kuzinduka baadhi ya wafalme na maraisi; bali hata baadhi ya masheikh wanaojiita waislamu, lakini wanafanyakazi kwa siri kwa manufaa ya Israil na wasaidizi wake.

Nilishangazwa na kauli ya sheikh mmoja mpotofu akisema: “Israil ina afadhali kuliko wengine kwa sababu inasoma Qur’ani kwenye idhaa yake.” Ndio ewe sheikh! Wacha kutangaza, bali inachapisha na kusambaza pia, lakini ile iliyopotoshwa na kukorogwa ili kumaliza Uislamu; sawa na baadhi ya wenye vilemba vya usheikh vya upotovu.

Huambiwi ila yale yale waliyoambiwa Mitume wa kabla yako.

Washirikina wa uma zilizotangulia waliwaambia mitume na manabii wao: “Nyoyo zetu zimo katika vifuniko kwa hayo unayotuitia…Hayakuwa haya isipokuwa ni vigano vya wakale…Hakuwa huyu isipokuwa ni mchawi mzushi.” Na hivi ndivyo walivyokuambia mataghuti wa watu wako ewe Muhammad! Kwa sababu Mola aliyekutuma wewe na aliyewatuma waliokuwa kabla yako ni mmoja na risala yake ni moja, na masilahi ya mataghuti ambayo yanasigana na wafuasi wa haki ni hayo hayo wakati wowote na mahali popote.

Hakika Mola wako bila ya shaka ni Mwenye maghufira, na ni Mwenye adhabu chungu.

Aya imekusanya vinyume viwili: msamaha wa mwenye dhambi ikiwa atatubia, na adhabu ikiwa ataendelea. Namna hii Mwenyezi Mungu (s.w.t.) anafanya katika Aya kadhaa, anakutanisha ahadi na kiaga, kupendekeza na kuhadharisha, ili aogope mja adhabu ya Mungu apate kumcha, na wala asikate tamaa na rehema yake atubie na arejee.

Na lau tungeliifanya Qur’ani kwa lugha ya kigeni wangelisema: Kwa nini Aya zake hazikupambanuliwa? Yawaje lugha ya kigeni na mwarabu?

Qur’ani iliwateremkia waarabu kwa lugha yao wanayoipenda na kuitukuza, lakini baadhi ya mataghuti wao waliwaambia wengine: Lau ingeliteremka kwa lugha nyingine wangelitaaradhi na kusema itakuwaje Mtume mwarabu na lugha ya kigeni? Hivi ndivyo wanavyouandalia kila mlango ufunguo na kila usiku na taa. Hakuna lengo isipokuwa kuikimbia haki tu.

Sema: Hii Qur’ani ni uwongofu na ponyo kwa wenye kuamini.

Qur’ani ni mwongozo kwa mwenye kutaka uongofu na ni haki kwa njia ya haki na ni ponyo kwa mwenye kutaka kupona maradhi ya ukafiri na unafiki. Imam Ali(a.s) anasema:“Hakika katika Qur’ani kuna ponyo la ugonjwa mkubwa zaidi ambao ni unafiki na dhulma.”

Na wasioamini umo uziwi katika masikio yao, nayo kwao imezibwa hawaioni.

Qur’ani ni uongofu na mwangaza kwa wenye ikhlasi, lakini ni upofu machoni mwa wanafiki, ni uziwi masikiano mwao na maradhi nyoyoni mwao.

Hao wanaitwa nao wako mahali mbali.

Qur’ani iliwaita duniani kwa mwito wa Mwenyezi Mungu, lakini hawakuitikia kama kwamba hakuna mwito au kwamba uko mbali hausikiki. Vile vile itawaita Siku ya Kiyama: “Ehe! Kila mpanda mbegu ana wasi-wasi na matokeo ya kazi yake; isipokuwa aliyepanda Qur’ani,” kama ilivyo katika Nahajul-balagha. Wafasiri wanasema kuwa kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: ‘nao wako mahali mbali,’ ni ishara kwamba wao hawasikii wala hawafahamu, sawa anayeitwa kwa sauti ya mbali asiyoisikia wala kuifahamu.

Lakini maana haya yanapingana na lengo la kuita, kwa sababu kutakuwa hakusikiwi. Maana yaliyo na nguvu zaidi ni kuwa kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: “Nao wako mahali mbali,’ ni ishara yakuwa mwito unatoka mbinguni, lakini unasikiwa na wote. Hilo linafahamishwa na kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu:

يَوْمَ يُنَادِ الْمُنَادِ مِن مَّكَانٍ قَرِيبٍ ﴿٤١﴾ يَوْمَ يَسْمَعُونَ الصَّيْحَةَ بِالْحَقِّ ﴿٤٢﴾

“Siku atakaponadi mwenye kunadi kutoka mahali karibu, siku watakaposikia ukele wa haki.” (50:41-42).

Na hakika tulimpa Musa Kitabu, lakini pakatokea hitilafu kati yake.

Makusudio ya Kitabu hapa ni Tawrat. Walihitalifiana kwenye hiyo iliposhuka. Kuna walioisadiki na walioikadhibisha. Kadhalika Qur’ani, iliposhuka, kuna walioisadiki na walioikadhibisha.

Na lau kuwa halikwishatangulia neno la Mola wangelihukumiwa.

Imetaka hekima yake Mtukufu kuiahirisha adhabu ya wakosefu hadi siku ya ufufuo. Vinginevyo asingebakia taghuti wala mwenye dhambi yoyote.

Na hakika wao wamo katika shaka nayo yenye kuwatia wasiwasi.

‘Wao’ ni washirikina wa kiarabu, ‘nayo’ ni hiyo Qur’ani. Makusudio ya shaka hapa ni ubishi bila ya ilimu na haki. Maana ni kuwa wao wanabishana kuhusu Qur’ani, lakini kwa ujinga na upotofu. Imetangulia kwa herufi zake katika Juz. 12 (11:110).

Anayetenda mema basi anajitendea mwenyewe, na anayetenda uovu basi ni juu ya yake; na Mola wako si mwenye kuwadhulumu waja.

Maana ya Aya hii yamekaririka kwenye Aya kadhaa; zikiwemo hizi zifuatazo:

فَالْيَوْمَ لَا تُظْلَمُ نَفْسٌ شَيْئًا وَلَا تُجْزَوْنَ إِلَّا مَا كُنتُمْ تَعْمَلُونَ ﴿٥٤﴾

“Basi leo nafsi yeyote haitadhulumiwa kitu, wala hamtalipwa ila yale mliyokuwa mkiyatenda Juz. 23 (36:54)

Na ile iliyo katika Juz. Hii tuliyo nayo:

الْيَوْمَ تُجْزَىٰ كُلُّ نَفْسٍ بِمَا كَسَبَتْ لَا ظُلْمَ الْيَوْمَ ﴿١٧﴾

“Leo kila nafsi italipwa kwa iliyochuma. Hapana dhulma leo.” (40:17)

Na nyinginezo zinasema kuwa mtu anakuwa na hiyari halazimishwi.

13

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA MBILI

إِلَيْهِ يُرَدُّ عِلْمُ السَّاعَةِ وَمَا تَخْرُجُ مِن ثَمَرَاتٍ مِّنْ أَكْمَامِهَا وَمَا تَحْمِلُ مِنْ أُنثَىٰ وَلَا تَضَعُ إِلَّا بِعِلْمِهِ وَيَوْمَ يُنَادِيهِمْ أَيْنَ شُرَكَائِي قَالُوا آذَنَّاكَ مَا مِنَّا مِن شَهِيدٍ ﴿٤٧﴾

47. Ilimu ya Saa (ya Kiyama) inarudishwa kwake (Mwenyezi Mungu). Na matunda hayatoki katika mafumba yake, wala mwanamke hachukui mimba, wala hazai, ila kwa kujua kwake. Na siku atakayowaita, akawaambia: Wako wapi washirika wangu? Hapo watasema: Hapana miongoni mwetu anayeshuhudia.

وَضَلَّ عَنْهُم مَّا كَانُوا يَدْعُونَ مِن قَبْلُ وَظَنُّوا مَا لَهُم مِّن مَّحِيصٍ ﴿٤٨﴾

48. Na wakawapotea wale waliokuwa wakiwaomba hapo mwanzo, na wakaona kuwa hawana pa kukimbilia.

لَّا يَسْأَمُ الْإِنسَانُ مِن دُعَاءِ الْخَيْرِ وَإِن مَّسَّهُ الشَّرُّ فَيَئُوسٌ قَنُوطٌ ﴿٤٩﴾

49. Mwanaadamu hachoki kuomba kheri, na inapomgusa shari, mara huvunjika moyo akakata tamaa.

وَلَئِنْ أَذَقْنَاهُ رَحْمَةً مِّنَّا مِن بَعْدِ ضَرَّاءَ مَسَّتْهُ لَيَقُولَنَّ هَـٰذَا لِي وَمَا أَظُنُّ السَّاعَةَ قَائِمَةً وَلَئِن رُّجِعْتُ إِلَىٰ رَبِّي إِنَّ لِي عِندَهُ لَلْحُسْنَىٰ فَلَنُنَبِّئَنَّ الَّذِينَ كَفَرُوا بِمَا عَمِلُوا وَلَنُذِيقَنَّهُم مِّنْ عَذَابٍ غَلِيظٍ ﴿٥٠﴾

50. Na tukimwonjesha rehema itokayo kwetu baada ya kumgusa dhara, bila ya shaka husema: Hii ni yangu, wala sidhani kuwa Kiyama kitakuwa. Na hata nikirudishwa kwa Mola wangu bila ya shaka nina mema yangu kwake! Basi kwa yakini tutawaelezea wale ambao wamekufuru walioyoyatenda, na kwa yakini tutawaonjesha adhabu ngumu.

ELIMU YA SAA INARUDISHWA KWAKE

Aya 47 – 50

MAANA

Ilimu ya Saa (ya Kiyama) inarudishwa kwake (Mwenyezi Mungu.)

Hakuna yoyote anayejua Kiyama kitakuwa lini isipokuwa Mwenyezi Mungu peke yake. Katika Nahjul-balagha imesemwa: ”Nyinyi na Kiyama kimewatia kamba” Yaani mnacho. Mwenye kufa ndio kiyama chake kimeanza.

Na matunda hayatoki katika mafumba yake, wala mwanamke hachukui mimba, wala hazai, ila kwa kujua kwake .[4]

Umetangulia mfano wake katika Juz. 7 (6:59).

Na siku atakayowaita, akawaambia: Wako wapi washirika wangu? Hapo watasema: Hapana miongoni mwetu anayeshuhudia.

Kesho Mwenyezi Mungu (s.w.t) atawaambia washirikina kwa kuwatahayariza: Wako wapi wale mliokuwa mkiwaabudu badala ya Mwenyezi Mungu? Je, watawasaidia? Nao watamwambia Mwenyezi Mungu, hakuna yeyote miongoni mwetu mwenye ushahidi leo, kuwa wewe una mshirika.

Na wakawapotea wale waliokuwa wakiwaomba hapo mwanzo.

Siku ya Kiyama mtu hatapata sanamu, wala mali, mtoto, mbinu wala wasila au chochote kile isipokuwa hisabu na malipo ya matendo waliyoyatenda.

Na wakaona kuwa hawana pa kukimbilia.

Kesho vifuniko vitawafanukia wakosefu na watajua kuwa hakuna kwa kuikimbia adhabu.

Mwanaadamu hachoki kuomba kheri, na inapomgusa shari, mara huvunjika moyo akakata tamaa.

Mtu huwa anataka sana kupata mali, cheo, afya na amani; anakuwa na bidii ya kuyafikia hayo bila ya kuchoka. Lakini likimsibu jambo lolote katika dunia yake basi anavunjika nguvu na kukata tamaa na rehema ya Mwenyezi Mungu.

Na tukimwonjesha rehema itokayo kwetu baada ya kumgusa dhara, bila ya shaka husema: hii ni yangu.

Anatafuta dunia kwa bidii na anakata tamaa akikosa kitu chochote kwenye hiyo dunia. Kama Mwenyezi Mungu akimwokoa na misukosuko husema: Nimeokoka kwa nguvu zangu na uwezo wangu wala hakuna yeyote aliyenifadhili.

Hakuna mwenye kusalimika na ghururi hii isipokuwa mtu wa haki na mwenye akili salama.

Wala sidhani kuwa Kiyama kitakuwa. Na hata nikirudishwa kwa Mola wangu bila ya shaka nina mema yangu kwake!

Bado mazungumzo ya mjinga aliyeghurika yanaendelea. Maana yake ni kuwa anasema mpumbavu huyu, kuwa mimi ndiye niliyefanya katika maisha ya dunia. Ama yale wanayonihofisha nayo ya baada ya mauti hayo ni njozi tu; na hata ikiwa ni kweli basi mimi huko Akhera nitakuwa na riziki bora zaidi kwa sababu mimi ni katika watu watukufu.

Mjinga huyu hata kama hana dhambi isipokuwa ufedhuli huu tu, unamtosha kuwa ni dhambi. Umetangulia mfano wake kwa upana zaidi katika Juz. 15 (18:32 – 44).

Basi kwa yakini tutawaelezea wale ambao wamekufuru walioyoyatenda, na kwa yakini tutawaonjesha adhabu ngumu.

Hakuna ovu lolote analolitenda mtu ila atalikuta kesho kwa Mwenyezi Mungu na kuulizwa nalo, kisha aadhibiwe kwalo kwa kiasi anachostahiki. Ikiwa ni katika aina ya madhambi makubwa, kama kufuru ushirikina na dhulma, basi atapata adhabu kubwa.

Na likiwa ni chini ya hapo atapata adhabu hafifu, lakini ieleweke kuwa kila balaa lisilokuwa moto wa Akhera basi si chochote.

وَإِذَا أَنْعَمْنَا عَلَى الْإِنسَانِ أَعْرَضَ وَنَأَىٰ بِجَانِبِهِ وَإِذَا مَسَّهُ الشَّرُّ فَذُو دُعَاءٍ عَرِيضٍ ﴿٥١﴾

51. Na tukimneemesha mwanadamu hugeuka na kujitenga upande, na inapomgusa shari, huwa na madua marefu marefu.

قُلْ أَرَأَيْتُمْ إِن كَانَ مِنْ عِندِ اللَّـهِ ثُمَّ كَفَرْتُم بِهِ مَنْ أَضَلُّ مِمَّنْ هُوَ فِي شِقَاقٍ بَعِيدٍ ﴿٥٢﴾

52. Sema: Mnaonaje! Ikiwa haya yanatoka kwa Mwenyezi Mungu, kisha mkayakataa, ni nani aliyepotea zaidi kuliko aliye katika upinzani wa mbali?

سَنُرِيهِمْ آيَاتِنَا فِي الْآفَاقِ وَفِي أَنفُسِهِمْ حَتَّىٰ يَتَبَيَّنَ لَهُمْ أَنَّهُ الْحَقُّ أَوَلَمْ يَكْفِ بِرَبِّكَ أَنَّهُ عَلَىٰ كُلِّ شَيْءٍ شَهِيدٌ ﴿٥٣﴾

53. Tutawaonyesha Ishara zetu katika upeo wa mbali na katika nafsi zao mpaka iwabainikie kwamba haya ni kweli. Je! Haikutoshi Mola wako kuwa Yeye ni Shahidi wa kila kitu?

أَلَا إِنَّهُمْ فِي مِرْيَةٍ مِّن لِّقَاءِ رَبِّهِمْ أَلَا إِنَّهُ بِكُلِّ شَيْءٍ مُّحِيطٌ ﴿٥٤﴾

54. Ehe! Hakika wao wamo katika shaka ya kukutana na Mola wao! Ehe! Hakika Yeye amekizunguka kila kitu.

TUTAWAONYESHA ISHARA ZETU

Aya 51 – 54

MAANA

Na tukimneemesha mwanadamu hugeuka na kujitenga upande, na inapomgusa shari, huwa na madua marefu marefu.

Akiwa amejitosha anakuwa makini, lakini akiwa fukara anakata tamaa na kuwa mnyonge; kama alivyosema Imam Ali(a.s ) . Umetangulia mfano wake katika Juz. 11 (10:12), Juz. 12 (11:9) na Juz. 15 (17:83).

Sema: Mnaonaje! Ikiwa haya yanatoka kwa Mwenyezi Mungu, kisha mkayakataa, ni nani aliyepotea zaidi kuliko aliye katika upinzani wa mbali?

Wanaambiwa walioikadhibisha Qur’an. Upinzani wa mbali ni inadi. Mwenyezi Mungu (s.w.t) alimwamrisha Mtume wake mtukufu kuwaambia kuwa mnadai Qur’an ni vigano, hebu niambieni itakuwaje hali yenu ikiwa Qur’an ni haki kutoka kwa Mwenyezi Mungu na hali nyinyi mnaipinga kwa inadi na kiburi? Je, hamjihurumii na mkajitoa shakani na adhabu ya moto?

ULIMWENGU NI QUR’AN KUBWA YA MWENYEZI MUNGU

Tutawaonyesha Ishara zetu katika upeo wa mbali na katika nafsi zao mpaka iwabainikie kwamba haya ni kweli.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) analeta dalili kwa waja wake ili awakinaishe kuwa yeye yuko na dini yake ni sahihi na mitume na vitabu vyake ni vya kweli. Amewawekea dalili ya hilo kwa hisia na ushahidi kutoka kwao wenyewe na kwenye ulimwengu wa dhahiri ya macho; anazifunua dalili hizo na anazitanabahisha akili kwa muumba wa mbingu na ardhi, kutofautiana mchana na usiku, kuvuma pepo na mawingu, kuhuishwa ardhi baada ya kufa harakati za nyota na manufaa yake, kuumbwa katika uzuri wa sura na mengineyo anayoyatambua mtu ambayo hisia zake zinafahamisha kuweko Mwenyezi Mungu kwa dalili mkataa na kwamba Yeye ndiye muumba wa pekee wa kila kitu.

Ikiwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) ametegema dalili za hisia kuwakinaisha waja wake na kuwaambia:

فَاعْتَبِرُوا يَا أُولِي الْأَبْصَارِ ﴿٢﴾

“Basi zingatieni enyi wenye busara” (59:2),

“Je, hawapati busara.” (32:15).

Sasa inakuwje kusemwa kuwa dini ni ya ghaibu ndani ya ughaibu, haitegemei hisia wala majaribio?

Hapana! Dini inathibitika kwa hisia na ushahidi; sawa na tunavyothibitisha akili ya mwenye akili kutokana na kauli yake na vitendo vyake. Wataalamu wa kisayansi wanathibitisha mambo mengi yasiyohisiwa wala kuonekana.

Kwa hiyo yanatubainikia makosa ya mwanafasihi mmoja aliyesema: “Mwenyezi Mungu daima anawatakabalia wale ambao wanaamini ghaibu bila ya kuwa na haja ya dalili wala kuona” Jarida la Sabahul-khayr la 26-2-1970.

Zaidi ya hayo maulamaa wa kiislamu wamekongamana kuwa ni wajibu kuchunguza na kumjua Mwenyezi Mungu Mtukufu na kumwamini. Wametegema hukumu ya kiakili na Aya za Qur’an katika hilo. Lakini anayoyasema mwanafasihi huyo ni kinyume na yanagongana na tafsiri ya Qur’an.

Ibn Al-Arabi anasema katika Futuhatil-makkiyya: “Wewe huwezi kuyakana unayoyaona; kama ambavyo huwezi kuacha kuyajua unayoyajua. Wewe unaona na kujua kwa uhakika kuweko herufi, matamshi sura na Aya zinazotamka kuweko mwandishi wake ambaye ni Mwenyezi Mungu, hata kama humuoni.

Kwa hiyo kuweko Mwenyezi Mungu ni Qur’an ambayo haifikiwi na upotofu mbele yake wala nyuma yake. Tazama Juz. 7 (6:4-6), kifungu cha ‘Hakuna udikteta Ardhini wala mbinguni.’

Je! Haikutoshi Mola wako kuwa Yeye ni Shahidi wa kila kitu?

Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kusema kuwa yeye anasimamisha dalilili kwa waja wake katika mbingu na ardhi na katika nafsi zao kuwa Mwenyezi Mungu ni kweli, Qur’an ni kweli na utume wa Muhammad ni kweli, sasa anasema kuwa inatosha kuwa dalili zake ni ushahidi wa ukweli na uadilifu wa hilo. Sufi wanasema kuhusu maana ya Aya hii kuwa Mwenyezi Mungu ndiye anayeshuhudia na kufahamisha kupatikana kingine, lakini Yeye haihitajii shahidi mwingine wa kumjulisha kuwa yuko.

Ehe! Hakika wao wamo katika shaka ya kukutana na Mola wao!

Wao wameikadhibisha Qur’an kwa vile tu wao hawaamini ghaibu na malipo. Hii inafahamisha kwamba asiyeamini kukutana na Mwenyezi Mungu, basi hawezi kuongoka kwenye kheri.

Ehe! Hakika Yeye amekizunguka kila kitu.

Anajua dhahiri ya waja na undani wao na atamlipa kila mmoja kwa yaliyochumwa na mikono yake. Ikiwa kheri basi ni kheri na ikiwa shari basi ni shari. Kwa ajili hii ndio atawaadhibu wale ambao wamekana kukutana naye na wakakadhibisha kitabu chake, yakiwa ni malipo kwa yale waliyoyachuma.

MWISHO WA SURA YA ARUBAINI NA MMOJA: SURAT FUSSILAT