TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA TATU Juzuu 23

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA TATU0%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA TATU Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: Qurani tukufu

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA TATU

Mwandishi: Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya
: HASANI MWALUPA
Kundi:

Matembeleo: 26474
Pakua: 2629


Maelezo zaidi:

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 30 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 26474 / Pakua: 2629
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA TATU

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA TATU Juzuu 23

Mwandishi:
Swahili

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA TATU

IMEANDIKWA NA: SHEIKH MUHAMMAD JAWAD MUGHNIYYA

IMETAFSIRIWA NA: SHEIKH HASAN MWALUPA

IMEHARIRIWA NA: USTADH ABDALLAH MOHAMED

IMEPANGWA KATIKA KOMPYUTA NA: UKHT PILI RAJABU

UTANGULIZI WA MCHAPISHAJI

Kitabu hiki kilichoko mikononi mwako hivi sasa ni juhudi ya miaka mingi sana ya watu waliojitolea kuona kazi hii imefanikiwa bila ya kumsahau Marhum Abu Muhammad wa London.

Kama lilivyo jina la Tafsiri ndivyo ilivyo Tafsiri yenyewe ambayo mwanachuoni huyu mahiri kabisa aliyeifafanua ni mtu aliyebobea katika fani zote ambazo mfasiri (Mfafanuzi) anatakiwa awe nazo.

Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya ameonesha cheche zake katika vitabu vingi alivyoviandika katika maudhui mbali mbalimbali na hivyo kujipatia wasomaji wengi sana.

Msomi huyu, mwenye fikra huru na anayetetea kile anachokiamini, ni mtu mwenye mawazo mapana na kuyaangalia mambo kwa undani sana, kipaumbele chake ni katika maslahi ya umma huu na amejaribu sana kwenda na wakati.

Sifa kubwa pekee ya mwanachuoni huyu ni kuwa yeye hakujihusisha sana na kung'ang'ania madhehebu fulani tu, labda hii yatokana na wadhifa wake wa ukadhi aliokuwa nao katika nchi ya Lebanon ambayo ina madhehebu mengi, ambapo sula la madhehebu ni nyeti nchini humo, hata hivyo yeye aliweza kuamua matatizo ya watu kwenye ofisi yake kulingana na madhehebu yao pale walipomwendea. Hiyo ilimsaidia sana hata kuweza kutoa kitabu kitwacho Al-Fiqh a'laa madhaahabil-khamsah (Fikhi ya madhehebu matano) yaani ya Hanafi, Maaliki, Shafi, Hambali na Shia (ambacho twataraji kitatoka kwa lugha ya kiswahili hivi karibuni Inshaallah).

Jambo lililotupa msukumo wa kukifasiri kitabu hiki kwa lugha ya Kiswahili ni zile faida nyingi atakazozipata msomaji na kujua mambo mengi na ya ajabu yaliyo mapya kwake ambayo si rahisi kuyapata kwa wafasiri wengine.

Msomaji atapata faida katika fani za Sayansi, Siasa, Historia, Mashairi, visa vizuri, na Saikolojia miongoni mwa mengine; ndiyo maana msomaji atashangaa kidogo anapoisoma Tafsiri hii atakapoona mwandishi amewataja na kuwanukuu watu kama kina Mfalme Edward, wanasayansi kama kina Enstein, wasanii kama Charlie Champlin (Mchekeshaji maarufu), na wengineo, hali inayoifanya tafsiri hii kuwa ni ya kipekee kabisa.

Mtindo alioutumia mwandishi ni sahali uliokusudiwa watu wa tabaka mbalimbali, wanavyuoni na watu wa kawaida.

Nia yetu ni kukigawanya kitabu hiki bure lakini tumelazimika kukiuza kwa bei nafuu ili kurudisha gharama za uchapishaji.

Mwisho: Shukrani kubwa iwaendee bila ya kuwataja watu waliojitolea usiku na mchana, jopo la wafasiri, wahariri, wachapaji, waliotupa moyo na kutoa maoni yao na walioisimamia ili kuhakikisha kwamba kitabu kimemfikia msomaji.

MAKOSA YA CHAPA

Sikumbuki kama nimewahi kusoma kitabu kilichotoka kupigwa chapa, cha zamani au cha sasa, bila ya kukuta makosa ya chapa, Nafikiri sitasoma kitabu kisichokuwa hivyo. Nimejaribu sana kuliepuka hilo katika tungo zangu, lakini sikufanikiwa.

Nilikuwa sifikirii kama ninaweza kuona makosa haya katika maandishi ya msahafu mtukufu, kama yale yaliyo katika baadhi ya chapa; kwa mfano neno yabswutu kwa swad, badala ya yabsutu kwa sin, na katika chapa ya Tafsir Arrazi ya Misr ya mwaka 1935, Sura ya (2:146), Imeandikwa La Ya'alamuun, (hawajui) badala ya Ya'alamuun (wanajua). Mfano wa makosa haya hausameheki.

Katika Tafsir Al-Manar, chapa ya Pili, sura (5:212), imeandikwa Fawqahum ila yawmil qiyama badala ya Fawqahum yawamal qiyama. Hatuwezi kusema kosa hili ni kubwa zaidi kuliko lile.

Lakini mkosaji atatuletea udhuru kwa msemo mashuhuri huko kwetu Jabal amil 'Makosa ya chapa.'

Katika Tafsiri Majmau chapa ya Urfan, Sura (46:15), imeandikwa: Hatta idha balagha arbai' na sanah badala ya: Hattaidha balagha ashuddahu arbai ' na sanah"

Kusema hivi sio kama ninajitetea kutokana na makosa ya chapa atakayoyakuta msomaji katika kitabu hiki, ijapokuwa naomba msamaha kama litatokea hili, lakini makusudio yangu hasa ni kumwambia yule atakayefungua macho yake kwenye makosa ya matamko na kuufungia macho uzuri wa maana.

Vilevile ninamwambia yule ambaye siku moja aliniambia: "Vitabu vyako vimejaa makosa ya chapa.” Kama kwamba hakuna kitu chochote katika vitabu hivyo isipokuwa makosa ya chapa tu. Wote hao ninawaambia: Mungu awasamehe na aniongoze mimi na nyinyi.

Vyovyote iwavyo, mimi ninaomba msamaha kutokana na makosa ya kifikra na ya chapa. Anasema Amirul Muminiin(a.s) :"Watu wote ni wapungufu wenye kuchanganyikiwa, isipokuwa yule aliyehifadhiwa na Mwenyezi Mungu." Na Mwenyezi Mungu (s.w.t) ndiye mwenye jukumu la kunikubalia yale niliyoyapatia na kunisamehe niliyakosea, kwa jaha ya Mtume na kizazi chake, ziwashukie rehema na amani (Amin).

MUHAMMAD JAWAD MUGHNIYYAH

1

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA TATU

Sura Ya Arubaini Na Sita: Surat Al-Ahqaf. Imeshuka Makka. Ina Aya 35.

بِسْمِ اللَّهِ الرَّحْمَٰنِ الرَّحِيمِ

Kwa jina la Mwenyezi Mungu Mwingi wa rehema Mwenye kurehemu.

حم ﴿١﴾

1. Haa miim.

تَنزِيلُ الْكِتَابِ مِنَ اللَّـهِ الْعَزِيزِ الْحَكِيمِ ﴿٢﴾

2. Uteremsho wa Kitabu umetoka kwa Mwenyezi Mungu, Mwenye nguvu, Mwenye hikima.

مَا خَلَقْنَا السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضَ وَمَا بَيْنَهُمَا إِلَّا بِالْحَقِّ وَأَجَلٍ مُّسَمًّى وَالَّذِينَ كَفَرُوا عَمَّا أُنذِرُوا مُعْرِضُونَ ﴿٣﴾

3. Hatukuziumba mbingu na ardhi na vilivyomo baina yake ila kwa haki na kwa muda uliowekwa. Na wale waliokufuru wanayapuuza yale wanayoonywa.

قُلْ أَرَأَيْتُم مَّا تَدْعُونَ مِن دُونِ اللَّـهِ أَرُونِي مَاذَا خَلَقُوا مِنَ الْأَرْضِ أَمْ لَهُمْ شِرْكٌ فِي السَّمَاوَاتِ ائْتُونِي بِكِتَابٍ مِّن قَبْلِ هَـٰذَا أَوْ أَثَارَةٍ مِّنْ عِلْمٍ إِن كُنتُمْ صَادِقِينَ ﴿٤﴾

4. Sema: Je, mnawaona wale mnaowaomba badala ya Mwenyezi Mungu? Nionyesheni wameumba nini katika ardhi; au wana shirika katika mbingu? Nileteeni Kitabu kilicho kuwa kabla ya hiki, au athari yoyote ya ilimu, ikiwa mnasema kweli.

وَمَنْ أَضَلُّ مِمَّن يَدْعُو مِن دُونِ اللَّـهِ مَن لَّا يَسْتَجِيبُ لَهُ إِلَىٰ يَوْمِ الْقِيَامَةِ وَهُمْ عَن دُعَائِهِمْ غَافِلُونَ ﴿٥﴾

5. Na ni nani mpotofu mkubwa kuliko yule anayeomba asiyekuwa Mwenyezi Mungu, ambaye hatamjibu mpaka Siku ya Kiyama, Na wala hawatambui maombi yao.

وَإِذَا حُشِرَ النَّاسُ كَانُوا لَهُمْ أَعْدَاءً وَكَانُوا بِعِبَادَتِهِمْ كَافِرِينَ ﴿٦﴾

6. Na watakapokusanywa watu watakuwa maadui zao, na wataikataa ibada yao.

IKO WAPI DALILI IKIWA NYINYI NI WA KWELI?

Aya 1-6

MAANA

Haamiim. Uteremsho wa Kitabu umetoka kwa Mwenyezi Mungu, Mwenye nguvu, Mwenye hikima.

Imetangulia kwa herufi zake katika Juz. 25 (45:1) na Juz. 23 (39:1).

Hatukuziumba mbingu na ardhi na vilivyomo baina yake ila kwa haki na kwa muda uliowekwa.

Mwenyezi Mungu ni mwenye hekima, haumbi kitu ila kwa hikima, na ni muhali kuumba kwa mchezo. Ameuumba ulimwengu na yaliyomo ndani yake kwa hikima na malengo sahihi. Akauwekea muda maalum wa kwisha kwake; baada yake ni hisabu na malipo katika nyumba ya pili.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 21 (30:8).

Na wale waliokufuru wanayapuuza yale wanayoonywa.

Mwenyezi Mungu anawahofisha wakosefu na siku ya Kiyama na vituko vyake, na akawawekea dalili wazi, lakini wakakataa isipokuwa inadi na jeuri.

Je, mnawaona wale mnaowaomba badala ya Mwenyezi Mungu? Nionyesheni wameumba nini katika ardhi; au wana shirika katika mbingu?

Maana ni kuwa nipeni habari enyi waabudu masanamu, ni jambo gani liliowafanya muyafanye masanamu ni miungu na kuyaabudu. Je, ni kwa kuwa yameumba kitu katika ardhi na mbinguni au yalishirikiana na Mwenyezi Mungu katika kuumba mbingu au sehemu yake?

Nileteeni Kitabu kilicho kuwa kabla ya hiki cha Qur’an; kama vile Tawrat, Injil n.k., kinachosema kuwa masanamu ni washirika wa Mwenyezi Mungu katika kuumba kwake au kuwa yanaweza kuwaombea kwa Mungu au kuwa na utajo wowote.

Au athari yoyote ya ilimu, ikiwa mnasema kweli.

Ikiwa hamna dalili ya nukuu yoyote, je mnayo dalili ya kiakili kusadikisha myasemayo na kuyafanya sahihi mnayoyaabudu?

Umetangulia mfano wake katika Juz. 22 (35:40).

KUABUDU MASANAMU WAKATI MAENDELEO YA KUFIKA ANGANI

Unaweza kuuliza : Kwa nini Mwenyezi Mungu (s.w.t) ametilia umuhimu sana kuwarudi wenye kuabudu masanamu na mizimu kwenye Aya hii na nyinginezo, na hali hili sio jambo zito sana na liko wazi kabisa? Kuupinga uungu wa masanamu si ni jambo liliowazi; sawa na kuukanusha upofu na uoni na giza na nuru?

Jibu : Kuyatukuza masanamu na kuyaabudu, kumekua ni sehemu ya maisha ya mtu kuanzia zama na Nuh(a.s ) mpaka zama za Muhammad(s.a.w. w ) , ambapo baina ya wawili hao kuna maelefu ya miaka; bali mpaka hivi sasa kwenye maendeleo ya kufika angani, bado masanamu yameenea mashariki mwa ardhi na magharibi yake.

Masanamu yaliyoko kwenye nyumba za ibada, siku hizi, kwenye njia panda na kwenye vilele vya milima. Pia mapicha kwenye kuta yaliyoenea huku na huko na kwenye vitabu vya kumbukumbu si ni aina ya kuabudu masanamu?

Umetukuka ukuu wa Muhammad(s.a.w. w ) katika kumtukuza mtu kwa kumsafisha na ibada ya masanamu yaliyotengenezwa na mikono yake. Mshairi anasema:

Namshangaa insani mchonga jiwe ambaye

Hulifanya rahamani Mungu aabudiwaye

Huku adhani moyoni hudhuru na kumfaaye

Si aabudu mikono ilochonga hilo jiwe

Hayo si ndio maono lau ataka ajuwe

Basi na iwe mikono ya kuabudu si jiwe

Ndiyo imechonga jiwe kama anavyoelewa

Na nani mpotofu mkubwa kuliko hao wanaowaomba, badala ya Mwenyezi Mungu, ambao hawatawaitikia mpaka Siku ya Kiyama.

Makusudio ya kusema ‘mpaka siku ya Kiyama,’ ni milele na kutowezekana kujibu kabisa. Maana ni kuwa hakuna mjinga aliyepotea zaidi kuliko yule anayeabudu kisichosikia anayeita wala kumjibu anayeomba.

Na wala hawatambui maombi yao.

Washirikina wanaabudu masanamu, lakini masanamu hayana habari nao, wala hayana hisia yoyote.

Na watakapokusanywa watu watakuwa maadui zao, na wataikataa ibada yao.

Vile vile siku ya Kiyama wakati watu watakapofufuliwa kwa hisabu na malipo, miungu ya washirikina itajitenga nao na kuwakataa. Tazama Juz.11 (10:28).

وَإِذَا تُتْلَىٰ عَلَيْهِمْ آيَاتُنَا بَيِّنَاتٍ قَالَ الَّذِينَ كَفَرُوا لِلْحَقِّ لَمَّا جَاءَهُمْ هَـٰذَا سِحْرٌ مُّبِينٌ ﴿٧﴾

7. Na wanaposomewa Aya zetu zilizo wazi, wale waliokufuru husema juu ya haki inapowajia: Huu ni uchawi ulio wazi.

أَمْ يَقُولُونَ افْتَرَاهُ قُلْ إِنِ افْتَرَيْتُهُ فَلَا تَمْلِكُونَ لِي مِنَ اللَّـهِ شَيْئًا هُوَ أَعْلَمُ بِمَا تُفِيضُونَ فِيهِ كَفَىٰ بِهِ شَهِيدًا بَيْنِي وَبَيْنَكُمْ وَهُوَ الْغَفُورُ الرَّحِيمُ ﴿٨﴾

8. Au wanasema: Ameizua! Sema: Ikiwa nimeizua mimi, basi nyinyi hamwezi kunifaa chochote mbele ya Mwenyezi Mungu. Yeye anajua zaidi hayo mnayoropokwa; anatosha kuwa shahidi baina yangu na nyinyi. Na Yeye ni Mwingi wa Maghufira, Mwenye kurehemu.

قُلْ مَا كُنتُ بِدْعًا مِّنَ الرُّسُلِ وَمَا أَدْرِي مَا يُفْعَلُ بِي وَلَا بِكُمْ إِنْ أَتَّبِعُ إِلَّا مَا يُوحَىٰ إِلَيَّ وَمَا أَنَا إِلَّا نَذِيرٌ مُّبِينٌ ﴿٩﴾

9. Sema, mimi si kioja miongoni mwa Mitume. Wala sijui nitakavyofanywa mimi wala nyinyi. Mimi nafuata niliyopewa Wahyi tu, wala mimi si chochote ila ni mwonyaji, mwenye kubainisha.

قُلْ أَرَأَيْتُمْ إِن كَانَ مِنْ عِندِ اللَّـهِ وَكَفَرْتُم بِهِ وَشَهِدَ شَاهِدٌ مِّن بَنِي إِسْرَائِيلَ عَلَىٰ مِثْلِهِ فَآمَنَ وَاسْتَكْبَرْتُمْ إِنَّ اللَّـهَ لَا يَهْدِي الْقَوْمَ الظَّالِمِينَ ﴿١٠﴾

10. Sema: Mwaonaje yakiwa haya ni kweli yametoka kwa Mwenyezi Mungu, nanyi mmeyakataa, na alishuhudia shahidi miongoni mwa Wana wa Israili juu ya mfano wa haya, na akaamini, na nyinyi mnafanya kiburi? Hakika Mwenyezi Mungu hawaongozi watu madhalimu.

وَقَالَ الَّذِينَ كَفَرُوا لِلَّذِينَ آمَنُوا لَوْ كَانَ خَيْرًا مَّا سَبَقُونَا إِلَيْهِ وَإِذْ لَمْ يَهْتَدُوا بِهِ فَسَيَقُولُونَ هَـٰذَا إِفْكٌ قَدِيمٌ ﴿١١﴾

11. Na wale ambao wamekufuru waliwaambia wale ambao wameamini: Lau hii ingelikuwa ni heri, wasingelitutangulia. Na walipokosa kuongoka kwayo basi wakasema: Huu ni uzushi wa zamani.

وَمِن قَبْلِهِ كِتَابُ مُوسَىٰ إِمَامًا وَرَحْمَةً وَهَـٰذَا كِتَابٌ مُّصَدِّقٌ لِّسَانًا عَرَبِيًّا لِّيُنذِرَ الَّذِينَ ظَلَمُوا وَبُشْرَىٰ لِلْمُحْسِنِينَ ﴿١٢﴾

12. Na kabla yake kilikuwapo Kitabu cha Musa, kuwa kiongozi na chenye rehema. Na hiki ni Kitabu chenye kusadikisha cha lugha ya kiarabu, ili kiwaonye wale waliodhulumu, na kiwe ni bishara kwa watendao mema.

AU WANASEMA WAMEYATUNGA?

Aya 7 – 12

MAANA

Na wanaposomewa Aya zetu zilizo wazi, wale waliokufuru husema juu ya haki inapowajia: Huu ni uchawi ulio wazi.

Makusudio ya ishara zetu na haki ni Qur’an. Maana ya zilizo wazi ni kuwa Aya za Qur’an ziko wazi hazikufunganafungana. Lakini pamoja na kuwa Qur’an iko wazi na kudhihiri dalili kuwa ni haki, bado wazushi, walio mataghuti na wapenda anasa wameipa sifa ya uchawi ulio waziwazi. Si kwa lolote ila ni kwa kuwa imewafanya wao kuwa sawa na watu wengine. Umetangulia mfano wa hayo katika Aya kadhaa huko nyuma.

Au wanasema: Ameizua! Sema: Ikiwa nimeizua mimi, basi nyinyi hamwezi kunifaa chochote mbele ya Mwenyezi Mungu.

Je, washirikina wanadai kuwa umeizua hii Qur’an ewe Muhammad(s.a.w. w ) ? Waambie: vipi nimzulie Mungu uwongo na hali mimi ndiye ninayemuhofia zaidi? Je, mtanikinga na ghadhabu ya Mwenyezi Mungu na adhabu yake ikiwa nitasema uwongo au kumzulia? Aliyasema haya Mtume kutegemea vile wanavyomjua yeye jinsi anavyochukia uwongo na tabia nyinginezo mbaya.

Yeye anajua zaidi hayo mnayoropokwa; anatosha kuwa shahidi baina yangu na nyinyi.

Hakifichiki kitu katika kauli zenu na vitendo vyenu nanyi mtahisabiwa navyo; na Mwenyezi Mungu ananijua mimi na nyinyi, kwa hiyo anashudia ukweli na uaminifu kwangu na anashuhudia uwongo na hiyana kwenu

Na Yeye ni Mwingi wa maghufira, Mwenye kurehemu.

Atawasamehe na kuwachanganya kwenye rehema yake ikiwa mtatubia na kurejea.

Sema: mimi si kioja miongoni mwa Mitume.

Mimi si wa kwanza kufikisha ujumbe wa Mungu. Wamenitangulia mitume na manabii wengi

Wala sijui nitakavyofanywa mimi wala nyinyi.

Mtume(s.a.w. w ) anajua hali yake na hali ya washirikina huko Akhera. Kwa sababu Mwenyezi Mungu alimpa habari ya hilo; kama zinavyoeleza Aya kadhaa; mbali ya kuwa ilimu hii ni katika nyenzo za utume. Zimekuja Hadith mutawatir, kwamba Mtume aliwabashiria pepo watu kadhaa.

Kwa hiyo basi Maana ya Aya ni kuwa Mtume hajui yatakayowatokea katika maisha ya duniani na atawatia mtihani gani Mwenyezi Mungu. Vile vile hajui kuwa Mwenyezi Mungu atawaadhibu hapa duniani au ataahirisha adhabu yao mpaka siku ya ufufuo.

Mimi nafuata niliyopewa Wahyi tu, wala mimi si chochote ila ni mwonyaji mwenye kubainisha.

Sio kazi ya muonyaji kujua ilimu ya ghaibu; isipokuwa yeye anafikisha anayopewa wahyi na Mwenyezi Mungu kuhusiana na yale yatakayowatokea washirikina.

Ieleweke kuwa Aya hii ilishuka kabla ya kushuka Aya inayosema kuwa mwisho ni wa dini ya Mwenyezi Mungu na Mtume wake, wajapochukia washirikina. Au pengine ni miongoni mwa mifumo ya kutoa mwito kwa hikima na mawaidha mazuri.

Sema: Mwaonaje yakiwa haya ni kweli yametoka kwa Mwenyezi Mungu, nanyi mmeyakataa, na alishuhudia shahidi miongoni mwa Wana wa Israili juu ya mfano wa haya, na akaamini, na nyinyi mnafanya kiburi? Hakika Mwenyezi Mungu hawaongoi watu madhalimu.

Sura hii tuliyo nayo imeshuka Makka isipokuwa Aya hii tuliyo nayo, ilishuka Madina kwa ajili ya Abdullah bin Salim, aliposilimu Madina. Yeye alikuwa mwanachuoni mkubwa wa Wana wa Israil. Haya ndiyo yaliyoelezwa kwenye tafsiri nyingi.

Maana ni sema ewe Muhammad kuwaambia wale wanaodai kuwa Qur’an ni uchawi uliozushwa, hebu niambieni itakuwaje hali yenu mbele ya Mwenyezi Mungu ikithibiti kuwa Qur’an ni haki na kweli na akaiamini mwana wa chuoni katika wana wa Israil; kama vile Abdullah bin Salam ambaye anatambua siri za wahyi na kushuudia kuwa mafunzo ya Qur’an ni kama mafunzo ya Tawrat iliyoteremshwa na Mwenyezi Mungu kwa Musa? Basi mtakuwaje mkibaki na upotevu wenu na inada yenu? Je mjidhulumu kwa hiyari yenu na kujianika kwenye adhabu ya Mwenyezi Mungu?

Na wale ambao wamekufuru waliwaambia wale ambao wameamini: Lau hii ingelikuwa ni heri, wasingelitutangulia.

Watu wengi walioitikia mwito wa Mtume(s.a.w. w ) , mwanzo mwanzo wa mwito wa Uislamu, walikuwa ni miongoni mwa wanyonge. Kwa hiyo mamwinyi wakaifanya hiyo ni sababu ya kuituhumu risala ya Mtume. Kwa sababu, wanavyodai, ni kuwa haki ni ile inayokubaliwa na vigogo, wala sio kuwa watu wajulikane kwa kuwa na haki. Kila wanalolilifanya matajiri ndio haki na wanalolilifanya wengine ni batili. Hayo ndiyo madai yao, lakini kila mwenye kuipinga haki itamshinda.

Ndio maana hazikupita siku mtumwa wa kihabeshi akapanda kwenye mgongo wa Al-Ka’aba akinadi Lailaha illallah Muhammadurrasulullah (Hakuna Mola isipokuwa Mwenyezi Mungu, Muhammad ni Mtume wa Mwenyezi Mungu). Na Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w. w ) akayavunja masanamu na kuyatupa chini ya nyayo zake huku akisema: “Haki imefika na batili imeondoka, hakika batili ni yenye kuondoka.”

Katika Tafsir Arrazi, imeandikwa kuwa mjakazi wa Amru alisilimu na alikuwa akimpiga mpaka anachoka. Basi makafiri wakasema: “Kama Uislamu ungelikuwa ni kheri asingetutangulia majakazi wa Amru.” Lakini Amru mwenyewe alisilimu badaye, akapigana vita vya Roma na Fursi.

Na walipokosa kuongoka kwayo basi wakasema: Huu ni uzushi wa zamani.

Wanazungumziwa makafiri wa kikuraishi. ‘Kwayo’ ni hiyo Qur’an. Mataghuti waliisifu kuwa ya zamani, kwa vile, kwa madai yao, wanasema ni ngano za watu wa kale zilizopitwa na wakati.

Walisema hivi sio kwa lolote isipokuwa wao hawaamini isipokuwa masilahi yao na chumo lao tu, na Qur’an inapinga na kupiga vita hayo.

Na kabla yake kilikuwapo Kitabu cha Musa, kuwa kiongozi na chenye rehema. Na hiki ni Kitabu chenye kusadikisha cha lugha ya kiarabu, ili kiwaonye wale waliodhulumu, na kiwe ni bishara kwa watendao mema.

Qur’an ni kama Tawrat iliyomshukia Musa. Vitabu vyote hivyo viwili vinaongoza kwenye haki na ni rehema kwa mwenye kuviamini na avitumia kwa mujibu wake. Tawrat ilitoa habari za kuja Muhammad:

الَّذِي يَجِدُونَهُ مَكْتُوبًا عِندَهُمْ فِي التَّوْرَاةِ وَالْإِنجِيلِ يَأْمُرُهُم بِالْمَعْرُوفِ وَيَنْهَاهُمْ عَنِ الْمُنكَرِ ﴿١٥٧﴾

“Ambaye wanamkuta ameandikwa kwao katika Tawrat na Injili, ambaye anawaamrisha mema na anawakatazamaovu.” Juz. 9 (7:157).

Vile vile Qur’an inaisadikisha Tawrat hii na inatamka kwa lugha yenu, enyi waarabu, ikimuonya na adhabu yule atakayefanya uovu na kumpa habari njema za thawabu yule mwenye kufanya wema. Basi vipi mara mnasema ni uchawi na mara nyingine ni ngano za watu wa kale; mbona hamyasemi hayo kwa Tawrat?

2

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA TATU

إِنَّ الَّذِينَ قَالُوا رَبُّنَا اللَّـهُ ثُمَّ اسْتَقَامُوا فَلَا خَوْفٌ عَلَيْهِمْ وَلَا هُمْ يَحْزَنُونَ ﴿١٣﴾

13. Hakika wale waliosema: Mola wetu ni Mwenyezi Mungu; kisha wakawa na msimamo, hawatakuwa na hofu, wala hawatahuzunika.

أُولَـٰئِكَ أَصْحَابُ الْجَنَّةِ خَالِدِينَ فِيهَا جَزَاءً بِمَا كَانُوا يَعْمَلُونَ ﴿١٤﴾

14. Hao ndio watu wa Peponi, watadumu humo, ni malipo kwa waliyokuwa wakiyatenda.

وَوَصَّيْنَا الْإِنسَانَ بِوَالِدَيْهِ إِحْسَانًا حَمَلَتْهُ أُمُّهُ كُرْهًا وَوَضَعَتْهُ كُرْهًا وَحَمْلُهُ وَفِصَالُهُ ثَلَاثُونَ شَهْرًا حَتَّىٰ إِذَا بَلَغَ أَشُدَّهُ وَبَلَغَ أَرْبَعِينَ سَنَةً قَالَ رَبِّ أَوْزِعْنِي أَنْ أَشْكُرَ نِعْمَتَكَ الَّتِي أَنْعَمْتَ عَلَيَّ وَعَلَىٰ وَالِدَيَّ وَأَنْ أَعْمَلَ صَالِحًا تَرْضَاهُ وَأَصْلِحْ لِي فِي ذُرِّيَّتِي إِنِّي تُبْتُ إِلَيْكَ وَإِنِّي مِنَ الْمُسْلِمِينَ ﴿١٥﴾

15. Na tumemuusia mtu awafanyie wema wazazi wake wawili. Mama yake amebeba mimba yake kwa taabu, na akamzaa kwa taabu. Na kubeba mimba kwake na kumwachisha ziwa ni miezi thalathini. Hata anapofika kukomaa kwake, na akafikilia miaka arubaini. Husema: Mola wangu! Nizindue nishukuru neema yako uliyonineemesha na wazazi wangu, na nipate kutende mema unayoyaridhia. Na unitengenezee dhuriya zangu. Hakika mimi nimetubu kwako, na hakika mimi ni miongoni mwa Waislamu.

أُولَـٰئِكَ الَّذِينَ نَتَقَبَّلُ عَنْهُمْ أَحْسَنَ مَا عَمِلُوا وَنَتَجَاوَزُ عَن سَيِّئَاتِهِمْ فِي أَصْحَابِ الْجَنَّةِ وَعْدَ الصِّدْقِ الَّذِي كَانُوا يُوعَدُونَ ﴿١٦﴾

16. Hao ndio tunaowatakabalia bora ya vitendo walivyovitenda. Na tunayasamehe mabaya yao, watakuwa miongoni mwa watu wa Peponi. Miadi ya kweli hiyo waliyoahidiwa.

KUWAFANYIA WEMA WAZAZI WAWILI

Aya 13 – 16

MAANA

Hakika wale waliosema: Mola wetu ni Mwenyezi Mungu; kisha wakawa na msimamo, hawatakuwa na hofu, wala hawatahuzunika.

Katika Juz. 17 (21:103) Mwenyezi Mungu amesema:“Hiyo fazaa kubwa haitawahuzunisha. Na Malaika watawapokea: Hii ndiyo siku yenu mliyokuwa mkiahidiwa.”

Na katika Aya hii tuliyo nayo, anasema Mwenyezi Mungu (s.w.t) kuwa: hao ni wale walioshikamana na dini ya Mwenyezi Mungu kiitikadi, kikauli na kivitendo katika maisha ya duniani. Jumla hii imetajwa hivi ilivyo na tumeifafanua zaidi katika Juz. 21 (41:30).

Hao ndio watu wa Peponi, watadumu humo, ni malipo kwa waliyokuwa wakiyatenda.

Hao ni wale walioamini na wakawa na msimamo. Kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: ‘Kwa waliyokuwa wakiyatenda,’ ni msisitizo wa kuwa hakuna imani wala msimamo bila ya matendo.

Na tumemuusia mtu awafanyie wema wazazi wake wawili. Mama yake amebeba mimba yake kwa taabu, na akamzaa kwa taabu.

Yaani amepata matatizo mengi alipokuwa na mimba, wakati wa kumzaa na hata kwenye malezi pia. Kuna riwaya inayosema kuwa haki ya mama ni zaidi ya haki ya baba, kwa sababu alimbeba wakati ambapo hakuna yoyote wa kumbeba, akamkinga kwa masikio na macho na viungo vyote, akiwa na furaha. Akakubali awe na njaa, lakini mwanawe ashibe, awe na kiu lakini anywe, awe uchi lakini avae. Basi shukrani na wema ziwe kwa kiasi hicho.

Mwanzoni mtoto alikuwa akiona kuwa ni wajibu wake kuwasikiliza na kuwatii, wazazi wake, lakini sasa mtoto anaona kuwa ni lazima wazazi wake wamtii na kumnyenyekea mtoto na kusikiliza amri zake. Yametangulia maelezo ya kuwafanyia wema wazazi wawili katika Juz. 1(2:83), Juz. 5 (4:36), Juz. 8 (6:151) na Juz. 15 (17:23).

Na kubeba mimba kwake na kumwachisha ziwa ni miezi thalathini.

Tukiunganisha Aya hii na ile isemayo:

وَفِصَالُهُ فِي عَامَيْنِ ﴿١٤﴾

“Na kumwachisha ziwa miaka miwili.” Juz. 21 (31:14),

Inatubainikia kuwa uchache wa muda wa mimba ni miezi sita. Kwa sababu tukiondoa miaka miwili ya kunyonyesha inabakia miezi sita kwa uchache. Elimu ya utabibu ya kisasa imethibitisha nadharia hii.

Sheikh Al-Maraghi Almasri katika tafsiri yake anasema: “Wa kwanza kuvumbua hukumu hii ni Ali (K.W.).”

Na amepokea Muhammad bin Is-haq, mwenye kitabu cha As-Sira, kwamba mtu mmoja alimuoa mwanamke akamzalia mtoto wa mimba ya miezi sita kamili. Akamshitakia Uthman. Alipoletewa, akaamuru arujumiwe (apigwe kwa mawe).

Ali alipopata habari alimjia akamwambia:“Kwani husomi Qur’an? “ Uthman akasema, kwa nini nasoma. Akamwambia:“Hukusikia kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: “Na kubeba mimba kwake na kumwachisha ziwa ni miezi thalathini.” Na ile isemayo “Na kumwachisha ziwa miaka miwili.”

Kwa hiyo baada ya miaka miwili, hakuna kinachobaki ila miezi sita?” Uthman akasema: Wallah! Sikujua hivyo.

Hebu nileteeni huyo mwanamke. Basi wakamkuta amezaa. Akasema Muammar bin Abdallah: “Wallah! Hakuna kunguru kwa kunguru wala yai kwa yai lilifonana kuliko mtoto huyu alivyofanana na baba yake. “ Baba yake alipomuona, akasema: “Huyu ni mwanangu, wallah, sina shaka”

Hata anapofika kukomaa kwake na akafikilia miaka arubaini,

Anapofikia baleghe mtu kwa kutoa manii au kwa miaka [1] 1, na akawa ni mwenye akili, katika matumizi yake, basi anakuwa na yale waliyo nayo watu wazima na ni juu yake kutekeleza taklifa zote za sharia.

Hata hivyo wafasiri wamesema kuwa Aya hii inaashiria maudhui mengine ambayo ni kukomaa mtu akili na mwili, kwa dalili ya kuli yake Mwenyezi Mungu: ‘Na akafikia miaka arubaini,’ ambapo anafikia ukomo wa nguvu zake.

Vyovyote iwavyo miaka haitoshi kumfanya mtu kuwa na ukomavu wa akili ikiwa hakupitia uzoefu mwingi.

Sio mbali kuwa kutajwa miaka arubaini katika Aya ni kuashiria kuwa, aghalabu, mtu katika miaka hii anapitia majaribio yenye manufaa. Wafasiri na wanahistoria wanasema kuwa Mwenyezi Mungu hakumtuma Mtume ila baada ya kufikisha miaka arubaini, isipokuwa Isa na Yahya.

Husema: Mola wangu! Nizindue nishukuru neema yako uliyonineemesha na wazazi wangu, na nipate kutenda mema unayoyaridhia.

Mwenye akili hutaka tawfiki na msaada kutoka kwa Mwenyezi Mungu, kuweza kutekeleza shukrani kwake kwa kumtii na kumnyenyekea.

Neema kubwa zaidi ni kuongozwa kwenye haki na kuitumia inavyotakikana. Ama kule kuweko mtu sio neema kwake wala kwa mwingine akiwa si nyenzo ya kufanya matendo mema.

Imetangulia Aya hii kwa herufi zake katika Juz. 19 (27:19).

Na unitengenezee dhuriya zangu.

Watoto ni mzigo mkubwa kwa wazazi, bali malezi yao na matakwa yao ni janga hasa. Lakini, maskini, baba anasahau taabu zote hizi ikiwa Mwenyezi Mungu atamneemesha kizazi chema, vinginevyo itakuwa ni majanga na masaibu makubwa.

Hakika mimi nimetubu kwako, na hakika mimi ni miongoni mwa Waislamu.

Hapa kuna ishara kuwa Mwenyezi Mungu hakubali toba ya mwenye dhambi wala haitikii dua yake ila akitubia dhambi zake na akawa na msimamo katika vitendo vyake na kauli yake.

Hao ndio tunaowatakabalia bora ya vitendo walivyovitenda.

Makusudio ya bora ya vitendo ni visivyokuwa vitendoviovu. Kwa vile vitendo viovu anavisamehe; kama alivyovyosema:Na tunayasamehe mabaya yao, kwa sababu wametubia na kufanya ikhlasi.Watakuwa miongoni mwa watu wa Peponi; yaani watakuwa pamoja nao.

Miadi ya kweli hiyo waliyoahidiwa, kuwa matendo yao yatakubaliwa, kusamehewa makosa yao na kuingia Peponi. Ahadi ya Mwenyezi Mungu Mtukufu ni kweli na kauli yake ni haki.

وَالَّذِي قَالَ لِوَالِدَيْهِ أُفٍّ لَّكُمَا أَتَعِدَانِنِي أَنْ أُخْرَجَ وَقَدْ خَلَتِ الْقُرُونُ مِن قَبْلِي وَهُمَا يَسْتَغِيثَانِ اللَّـهَ وَيْلَكَ آمِنْ إِنَّ وَعْدَ اللَّـهِ حَقٌّ فَيَقُولُ مَا هَـٰذَا إِلَّا أَسَاطِيرُ الْأَوَّلِينَ ﴿١٧﴾

17. Na ambaye amewaambia, wazazi wake Ah! Nanyi! Je, mnanitisha kuwa nitafufuliwa, na hali vizazi vingi vimekwishapita kabla yangu! Na hao humwomba msaada Mwenyezi Mungu: Ole wako! Amini! Hakika miadi ya Mwenyezi Mungu ni kweli. Na yeye husema: Hayakuwa haya ila ni ngano za watu wa kale.

أُولَـٰئِكَ الَّذِينَ حَقَّ عَلَيْهِمُ الْقَوْلُ فِي أُمَمٍ قَدْ خَلَتْ مِن قَبْلِهِم مِّنَ الْجِنِّ وَالْإِنسِ إِنَّهُمْ كَانُوا خَاسِرِينَ ﴿١٨﴾

18. Hao ndio ambao imehakikishwa kauli juu yao; kama mataifa yaliyokwishapita kabla yao miongoni mwa majini na watu. Hakika hao wamekuwa wenye kuhasirika.

وَلِكُلٍّ دَرَجَاتٌ مِّمَّا عَمِلُوا وَلِيُوَفِّيَهُمْ أَعْمَالَهُمْ وَهُمْ لَا يُظْلَمُونَ ﴿١٩﴾

19. Na wote watakuwa na daraja zao mbali mbali kwa waliyoyatenda, na ili awalipe kwa vitendo vyao, na hawatadhulumiwa.

وَيَوْمَ يُعْرَضُ الَّذِينَ كَفَرُوا عَلَى النَّارِ أَذْهَبْتُمْ طَيِّبَاتِكُمْ فِي حَيَاتِكُمُ الدُّنْيَا وَاسْتَمْتَعْتُم بِهَا فَالْيَوْمَ تُجْزَوْنَ عَذَابَ الْهُونِ بِمَا كُنتُمْ تَسْتَكْبِرُونَ فِي الْأَرْضِ بِغَيْرِ الْحَقِّ وَبِمَا كُنتُمْ تَفْسُقُونَ ﴿٢٠﴾

20. Na siku wale waliokufuru watakapoonyeshwa Moto: Nyinyi mlitwaa vitu vyenu vizuri katika maisha yenu ya dunia, na mkastarehe navyo. Basi leo mnalipwa adhabu ya fedheha kwa mlivyokuwa mkitakabari katika ardhi bila ya haki, na kwa mlivyokuwa mkifanya ufuska.

ALIYEWAAMBIA WAZAZI WAKE AKH!

Aya 17 – 20

MAANA

Na ambaye amewaambia, wazazi wake Ah! Nanyi! na akawaambia:Je, mnanitisha kuwa nitafufuliwa, na hali vizazi vingi vimekwishapita kabla yangu!

Ni nani mtoto huyu anayezungumziwa na Qur’an na kusema kuwa ni kafiri mwenye kuwaudhi wazazi wake?

Jibu : Mwenyezi Mungu hakumtaja mtu hasa. Dhahiri ya Aya inaonyesha kwamba makusudio yake ni kila mtoto anayeikanusha siku ya mwisho, naye akiwa na wazazi wanaojitahidi kumpa nasaha, kumwongoza na kumhadharisha na ghadhabu za Mwenyezi Mungu na adhabu yake, lakini bado anaona kusumbuliwa na kuwaambia: Poteleeni mbali! Vipi mtu ataweza kutoka kaburini na hali amekuwa mchanga? Je, ameshawahi kutokewa na hivyo mwingine asiyekuwa mimi katika zama zozote?

Aya hii inawaelekea vijana wengi wa kisasa, kama vile imewashukia wao. Lau kama watauliza na kujadiliana kwa kukusudia maarifa na kuongoka kwenye uhakika, basi itakuwa ni wajibu wetu tuwakaribishe na maswali na majadiliano yao; na tufanye bidii kubwa kadiri tunavyoweza ili tuwakinaishe, kwa kuifanyia kazi kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu:

لَتُبَيِّنُنَّهُ لِلنَّاسِ وَلَا تَكْتُمُونَهُ ﴿١٨٧﴾

“Lazima mtakibainisha kwa watu wala hamtakificha.” Juz. 4 (3:187).

Na pia kuwa wao wana haja zaidi ya kuongozwa na kubainishiwa.

Na hao wazazihumwomba msaada Mwenyezi Mungu na humwambia mtoto wao:Ole wako! Amini! Hakika miadi ya Mwenyezi Mungu ni kweli.

Wanamwomba msaada Mwenyezi Mungu kutokana na kufuru ya mtoto wao na kumsisitiza kwamba ufufuo ni kweli. Mara nyingi mwito wa wazazi kwa mtoto unakuwa kama kawaida tu, lakini neno ‘humwomba msaada Mwenyezi Mungu,’ linaonyesha jinsi wanavyoona uchungu na masikitiko kwa kufuru ya mtoto wao aliyewaasi na ujeuri wake. Lakini pamoja na yote hayo anang’ng’nia upotevu na yeye husema:

Hayakuwa haya ila ni ngano za watu wa kale.

Anawajibu wazazi wake pamoja na huruma zao kwake na nasaha zao: Maneno yenu haya hayana maana yoyote ispokuwa porojo tu. Hivi ndivyo vijana wengi wa kileo wanavyowangalia baba zao na mama zao. Ajabu ni kuwa kijana lau atayasikia haya kutoka kwa kijana mwenzake asingelikuwa na msimamo huu wa dharau.

Hao ndio ambao imehakikishwa kauli juu yao kama mataifa yaliyok- wishapita kabla yao miongoni mwa majini na watu.

‘Hao,’ ni kila mwenye kuifanyia inadi haki na akapinga mwito wa wenye ikhlasi. Kuhakikishiwa kauli juu yao ni neno la adhabu. Hii ni desturi ya Mwenyezi Mungu katika uma zilizotangulia, wawe maji- ni au watu.

Hakika hao wamekuwa wenye kuhasirika, kwa vile waliuacha mwito wa haki na wakamzibia masikio mtoa nasaha aliyemwaminifu.

Na wote watakuwa na daraja zao mbali mbali kwa waliyoyatenda, na ili awalipe kwa vitendo vyao, na hawatadhulumiwa.

Daraja za watu, siku ya Kiyama, zitatofautiana kulingana na matendo yao yalivyokuwa duniani. Tafisiri wazi zaidi inayofafanua Aya hii, ni kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu:

يَوْمَ تَجِدُ كُلُّ نَفْسٍ مَّا عَمِلَتْ مِنْ خَيْرٍ مُّحْضَرًا وَمَا عَمِلَتْ مِن سُوءٍ ﴿٣٠﴾

“Siku ambayo kila nafsi itakuta heri iliyoitenda imehudhurishwa, na iliyoyatenda katika uovu.” Juz. 4 (3:30).

Na siku wale waliokufuru watakapoonyeshwa Moto; yaani watakapoadhibiwa, na Malaika wa adhabu watawaambia:

Nyinyi mlitwaa vitu vyenu vizuri katika maisha yenu ya dunia, na mkastarehe navyo.

Mlikusanya mamilioni ya pesa mlizozipora kisha mkazirundika, mkajijengea viwanda na majumba marefu kwa hisabu ya wanyonge, mkatumia yote kwenye raha na starehe, bila ya kuiwekea akiba siku hii ya leo.

Basi leo mnalipwa adhabu ya fedheha kwa mlivyokuwa mkitakabari katika ardhi bila ya haki, na kwa mlivyokuwa mkifanya ufuska.

Mlionyeshwa haki mkaifanyia kiburi, mkajitukuza na mkaijaza ardhi dhulma na ufisadi. Basi onjeni uchungu wa ubaya wenu kama mlivyoonja utamu wake jana.

Katika Tafsir ya Sheikh Al-Maraghi, kuna maelezo kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w. w ) alipokuwa akitaka kusafiri, mtu wa mwisho kumuaga katika familia alikuwa ni Fatima, na mtu wa kwanza kumjulia hali, anaporudi safirini, alikuwa ni Fatima. Siku moja aliporudi kutoka katika vita alikwenda nyumbani kwa Fatima, kama desturi yake.

Akaona pazia ya sufu nzito mlangoni na akawaona Hasan Na Husein wamevishwa vikuku vya fedha, basi akarudi bila ya kuingia. Fatima akaona kuwa hakuingia kutokana na aliyoyaona. Basi akaiondoa ile pazia na vikukuu akavipeleka kwa baba yake naye akawapa masikini na akasema: “Hawa ndio watu wa nyumba yangu – akiwashiria Fatima na waliomo nyumbani mwake – wala sipendi wale vizuri vyao katika maisha yao ya dunia.”