TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA TATU Juzuu 23

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA TATU0%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA TATU Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: Qurani tukufu

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA TATU

Mwandishi: Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya
: HASANI MWALUPA
Kundi:

Matembeleo: 26254
Pakua: 2524


Maelezo zaidi:

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 30 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 26254 / Pakua: 2524
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA TATU

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA TATU Juzuu 23

Mwandishi:
Swahili

14

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA TATU

Sura Ya Hamsini na Moja: Surat Adh-Dhariyat. Imeshuka Makka. Ina Aya 60.

بِسْمِ اللَّهِ الرَّحْمَٰنِ الرَّحِيمِ

Kwa jina la Mwenyezi Mungu Mwingi wa rehema Mwenye kurehemu

وَالذَّارِيَاتِ ذَرْوًا ﴿١﴾

1. Naapa kwa zinazotawanya sana.

فَالْحَامِلَاتِ وِقْرًا ﴿٢﴾

2. Na zinazobeba mizigo.

فَالْجَارِيَاتِ يُسْرًا ﴿٣﴾

3. Na zinazokwenda kwa wepesi.

فَالْمُقَسِّمَاتِ أَمْرًا ﴿٤﴾

4. Na zinazogawanya amri.

إِنَّمَا تُوعَدُونَ لَصَادِقٌ ﴿٥﴾

5. Hakika mnayoahidiwa bila ya shaka ni kweli.

وَإِنَّ الدِّينَ لَوَاقِعٌ ﴿٦﴾

6. Na kwa hakika dini bila ya shaka itatokea.

وَالسَّمَاءِ ذَاتِ الْحُبُكِ ﴿٧﴾

7. Naapa kwa mbingu zenye umbile zuri.

إِنَّكُمْ لَفِي قَوْلٍ مُّخْتَلِفٍ ﴿٨﴾

8. Hakika nyinyi bila ya shaka mko katika kauli inayokhitalifiana.

يُؤْفَكُ عَنْهُ مَنْ أُفِكَ ﴿٩﴾

9. Anageuzwa nayo mwenye kugeuzwa.

قُتِلَ الْخَرَّاصُونَ ﴿١٠﴾

10. Wazushi wameangamizwa.

الَّذِينَ هُمْ فِي غَمْرَةٍ سَاهُونَ ﴿١١﴾

11. Ambao wameghafilika katika ujinga.

يَسْأَلُونَ أَيَّانَ يَوْمُ الدِّينِ ﴿١٢﴾

12. Wanauliza: Ni lini hiyo siku ya malipo?

يَوْمَ هُمْ عَلَى النَّارِ يُفْتَنُونَ ﴿١٣﴾

13. Ni siku watakayojaribiwa Motoni.

ذُوقُوا فِتْنَتَكُمْ هَـٰذَا الَّذِي كُنتُم بِهِ تَسْتَعْجِلُونَ ﴿١٤﴾

14. Onjeni fitna yenu! Haya ndiyo mliyo kuwa mkiyahimiza.

NAAPA KWA ZINAZOTAWANYA

Aya 1 – 14

MAANA

Naapa kwa zinazotawanya sana, na zinazobeba mizigo, na zinazokwenda kwa wepesi, na zinazogawanya amri.

Katika kufasiri sifa hizi nne kuna rai kadhaa: Kuna waliosema kuwa Makusudio ya zinazotawanya ni pepo, zinazobeba ni mawingu zinazokwenda kwa wepesi ni jahazi na zinazogawanya ni malaika.

Kauli yenye nguvu ni kuwa zote hizi ni sifa za pepo. Ndizo zinazotawanya kwa vile zinatawanya mchanga nk. Akitumia neno hilo, Mwenyezi Mungu Mtufu anasema:

هَشِيمًا تَذْرُوهُ الرِّيَاحُ ...﴿٤٥﴾

“Majani makavu yaliyokatikakatika yanayopeperushwa na upepo.” Juz. 15 (18:45).

Mwenyezi Mungu (s.w.t) ameapa kwa upepo kuashiria manufaa yake, pia kuwa Mwenyezi Mungu anaweza kuapa na kila anachokitaka katika viumbe vyake. Tazama Juz. 23 (37:1-10)

Sifa ya pili ni ‘Na zinazobeba mizigo,’ Makusudio yake hapa ni kuwa pepo zinabeba mzigo wa mawingu. Anasema Mwenyezi Mungu Mtufu:

سُقْنَاهُ لِبَلَدٍ مَّيِّتٍ ﴿٥٧﴾

“Tunayasukuma kwa ajili ya mji uliokufa.” Juz. 8 (7:57).

Sifa ya tatu: ‘Na zinazokwenda kwa wepesi,’ ni kuwa pepo zinakwenda kwa wepesi zikiwa zinabeba mawingu. Sifa ya nne: ‘Na zinazogawanya amri.’ Pepo zinatawanya mvua katika ardhi; kama ilivyoelezwa kwenye Juz. 8 (7:57).

Hakika mnayoahidiwa bila ya shaka ni kweli, Na kwa hakika dini bila ya shaka itatokea.

Hili n jawabu la kiapo. Makusudio ya mnayoahidiwa ni uhai baada ya mauti. Na dini ni hisabu na malipo.Maana ni kuwa Mwenyezi Mungu atawafufua tu walio makaburini, hilo halina shaka. Na kwamba Yeye atamlipa mtu kwa matendo yake. Yakiwa heri basi ni heri na yakiwa shari basi ni shari.

Naapa kwa mbingu zenye umbile zuri.

‘Umbile zuri’ tumelifasiri kutokana na neno la kiarabu ‘Hubuk’ ambalo wafasiri wamelitolea kauli nyingi. Lakini iliyo na nguvu ni hii tuliyoifasiri; kwa maana ya kuwa katika maumbile ya mbingu kuna mpangilio, nidhamu, uzuri na kupendeza.

Hakika nyinyi bila ya shaka mko katika kauli inayokhitalifiana.

Msemo unaelekezwa kwa wale wanaomkadhibisha Mtume(s.a.w.w) na kauli zao zote ni za mgongano, mkorogano, uwongo na njozi; kama vile kusema kuwa Mtume ni mshairi, mara mwendawazimu na mara nyingine ni mchawi. Na kuhusu Qur’an wakasema ni vigano vya watu wa kale au imetungwa na Muhammad(s.a.w.w) n.k.

Anageuzwa nayo mwenye kugeuzwa.

Yaani anageuzwa na dini na haki yule anayeigeuka kwa hawa na ujinga; mfano wake ni sawa na kauli: “Hapofuki na hilo ila kipofu.”

Wazushi wameangamizwa.

Hao ni wale aliowabainisha Mwenyezi Mungu (s.w.t) kwa kusema:

Ambao wameghafilika katika ujinga.

Ujinga na upotevu umewavaa kuanzia kichwani hadi unyayoni, wakazipeleka dhana zao ovyoovyo na bila ya msingi wowote, kwenye ardhi na mbinguni na kwenye ufufuo na malipo. Wakasema kuwa Mwenyezi Mungu ana washirika katika mawe na ana mabinti katika Malaika na wengine aliozaa na majini. Ama ufufuo na hisabu kwao ni upotevu.

Wanauliza: Ni lini hiyo siku ya malipo?

Wenye dharau wanauliza, huo ufufuo utakuwa lini? Mwenyezi Mungu (s.w.t) naye anawajibu:

Ni siku watakayojaribiwa Motoni.

Ufufuo utakuwa siku watakayoonyeshwa moto na kuunguzwa humo. Husemwa kuwa kitu kimejaribiwa, ili kutoa kilichoghushiwa, kikiunguzwa motoni. Malaika wa Motoni watawaambia:

Onjeni fitna yenu! Haya ndiyo mliyokuwa mkiyahimiza.

Hii ndio adhabu mliyokuwa mkihimiza na kuifanyia dharau jana. Je, mmeionaje ladha yake?

إِنَّ الْمُتَّقِينَ فِي جَنَّاتٍ وَعُيُونٍ ﴿١٥﴾

15. Hakika wenye takua watakuwa katika mabustani na chemchem.

آخِذِينَ مَا آتَاهُمْ رَبُّهُمْ إِنَّهُمْ كَانُوا قَبْلَ ذَٰلِكَ مُحْسِنِينَ ﴿١٦﴾

16. Wakipokea aliyowapa Mola wao. Kwa hakika hao walikuwa kabla ya haya wakifanya mema.

كَانُوا قَلِيلًا مِّنَ اللَّيْلِ مَا يَهْجَعُونَ ﴿١٧﴾

17. Walikuwa wakilala kidogo tu usiku,

وَبِالْأَسْحَارِ هُمْ يَسْتَغْفِرُونَ ﴿١٨﴾

18. Na kabla ya alfajiri wakiomba maghufira.

وَفِي أَمْوَالِهِمْ حَقٌّ لِّلسَّائِلِ وَالْمَحْرُومِ ﴿١٩﴾

19. Na katika mali zao ipo haki ya mwenye kuomba na anayejizuia.

وَفِي الْأَرْضِ آيَاتٌ لِّلْمُوقِنِينَ ﴿٢٠﴾

20. Na katika ardhi zipo Ishara kwa wenye yakini

وَفِي أَنفُسِكُمْ أَفَلَا تُبْصِرُونَ ﴿٢١﴾

21. Na katika nafsi zenu, Je, hamwoni?

وَفِي السَّمَاءِ رِزْقُكُمْ وَمَا تُوعَدُونَ ﴿٢٢﴾

22. Na katika mbingu ziko riziki zenu na mliyoahidiwa.

فَوَرَبِّ السَّمَاءِ وَالْأَرْضِ إِنَّهُ لَحَقٌّ مِّثْلَ مَا أَنَّكُمْ تَنطِقُونَ ﴿٢٣﴾

23. Basi naapa kwa Mola wa mbingu na ardhi, hakika haya ni kweli kama ilivyo, kuwa nyinyi mnasema.

هَلْ أَتَاكَ حَدِيثُ ضَيْفِ إِبْرَاهِيمَ الْمُكْرَمِينَ ﴿٢٤﴾

24. Je, imekufikia hadithi ya wageni wa Ibrahim wanaohishimiwa?

إِذْ دَخَلُوا عَلَيْهِ فَقَالُوا سَلَامًا قَالَ سَلَامٌ قَوْمٌ مُّنكَرُونَ ﴿٢٥﴾

25. Walipoingia kwake wakasema: Salam! Na yeye akasema: Salam! watu nisiowajua.

فَرَاغَ إِلَىٰ أَهْلِهِ فَجَاءَ بِعِجْلٍ سَمِينٍ ﴿٢٦﴾

26. Akaenda kwa ahali yake na akaja na ndama aliyenona.

فَقَرَّبَهُ إِلَيْهِمْ قَالَ أَلَا تَأْكُلُونَ ﴿٢٧﴾

27. Akawakaribisha, akasema: Mbona hamli?

فَأَوْجَسَ مِنْهُمْ خِيفَةً قَالُوا لَا تَخَفْ وَبَشَّرُوهُ بِغُلَامٍ عَلِيمٍ ﴿٢٨﴾

28. Akahisi kuwaogopa. Wakasema: Usiwe na khofu, na wakambashiria kupata kijana

mwenye ilimu.

فَأَقْبَلَتِ امْرَأَتُهُ فِي صَرَّةٍ فَصَكَّتْ وَجْهَهَا وَقَالَتْ عَجُوزٌ عَقِيمٌ ﴿٢٩﴾

29. Ndipo mkewe akawaelekea, na ukelele na akapiga uso wake, na kusema: kongwe tasa!

قَالُوا كَذَٰلِكِ قَالَ رَبُّكِ إِنَّهُ هُوَ الْحَكِيمُ الْعَلِيمُ ﴿٣٠﴾

30. Wakasema: Ndivyo vivyo hivyo alivyosema Mola wako. Hakika Yeye ni Mwenye hikima Mjuzi.

HAKI YA MWENYE KUOMBA NA ASIYEOMBA

Aya 15 – 30

MAANA

Hakika wenye takua watakuwa katika Mabustani na chemchem. Wakipokea aliyowapa Mola wao. Kwa hakika hao walikuwa kabla ya haya wakifanya mema.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) anapokea kutoka kwa wema matendo yao; kama alivyosema:

وَيَأْخُذُ الصَّدَقَاتِ ﴿١٠٤﴾

“Na huzipokea sadaka.” Juz. 11 (9:104).

Yaani anazikubali sadaka na kuzilipa. Vilevile watu wema watapokea thawabu walizopewa kwa shangwe na furaha. Kwa maneno mengine ni:

رَّضِيَ اللَّـهُ عَنْهُمْ وَرَضُوا عَنْهُ ذَٰلِكَ الْفَوْزُ الْعَظِيمُ ﴿١١٩﴾

“Mwenyezi Mungu amewawia radhi na wao wamemwia radhi. Huko ndiko kufuzu kukubwa.”

Juz. 7 (5:119).

Walikuwa wakilala kidogo tu usiku, na kabla ya alfajiri wakiomba maghufira.

Walikuwa wakilala usiku, lakini kidogo, na mara nyingi tahajudi yao inaungana na alfajiri, wakifanya tasbihi na istighifari.

Imam Ali(as) anasema katika wasifu wao:“Ama wakati wa usiku wanatandika miguu yao wakisoma Qur’an kwa mpangilio… wakipitia Aya yenye shauku wanakuwa na tamaa nayo …. Na wakipitia yenye hofu wanaitegea masikio ya nyoyo zao wakidhani kuwa Jahannam inachachati- ka na kuunguruma ndani ya masikio yao; basi wao wanainama kwa migongo yao wakitandika chini mapaji ya nyuso zao, na viganja vyao na ncha za nyao zao (yaani wanasujudu ) wakimtaka Mwenyezi Mungu azi fungue shingo zao”

Na katika mali zao ipo haki ya mwenye kuomba na anayejizuia.

Mwenye kuomba ni yule anayeomba watu sadaka, na anayejizuia ni fukara ambaye anajizuia kuomba watu. Huyu amesadikishwa na kauli yake Mwenyezi Mungu Mtufu:

يَحْسَبُهُمُ الْجَاهِلُ أَغْنِيَاءَ مِنَ التَّعَفُّفِ تَعْرِفُهُم بِسِيمَاهُمْ لَا يَسْأَلُونَ النَّاسَ إِلْحَافًا ﴿٢٧٣﴾

“Asiyewajua anawadhania kuwa ni matajiri kwa kujizuia. Utawafahamu kwa alama zao; hawaombi watu wakan’gan’gania.” Juz. 3 (2:273).

Neno ‘haki’ linafahamisha kuwa fukara ni mshirika wa tajiri katika mali yake. Hilo tumelizungumzia kwa ufafanuzi zaidi katika kifungu cha Zaka kwenye Juz. 3 2: (272-274) na katika Juz. 4 (3: 180-182) kwenye kifungu: ‘Matajiri ni mawakala sio wenyewe.’

MWENYEZI MUNGU NA MAARIFA YA HISIA

Na katika ardhi zipo Ishara kwa wenye yakini na katika nafsi zenu, Je, hamwoni?

Mwenye kupeleleza kwenye viumbe vyote vilivyoko na akachunguza kwa makini, hana budi kujiuliza: ni nani aliyepangilia kwa mpangilio wa uten- genezaji huu? Hatapata jawabu la kukinaisha na tafsiri sahihi isipokuwa kuweko nguvu ya hali ya juu inayoongoza. Ikiwa hatakinai na jibu hili, basi hatapata mbele yake isipokuwa sadfa na umbile pofu. Hakuna mwenye shaka kuwa hii inazidisha ujinga na upofu. Wamaada wanasema kuwa hakuna njia ya maarifa isipokuwa hisia na majaribio.

Na Mwenyezi Mungu haingii kwenye hisia wala majaribio. Kwa hiyo kumwamini hakutegemei dalili, bali ni ujinga na upotevu.

Tunajibu :Kwanza : hatukubaliani kuwa sababu za maarifa zinakuwa tu kwenye hisia na majaribio; bali kuna maarifa ya kiakili yanayofikiwa kwa nguvu ya dhahania. Na mwenye kuiangusha akili na mazingatio na akakana hoja inayohusiana nayo, atakuwa ameukana utu kabisa. Kwa sababu hakuna utu bila ya akili inayokata.

Zaidi ya hayo ni kuwa mwenye kukana maaarifa ya akili atakuwa ameipinga nafsi yake yeye mwenyewe; kwa kuwa atakuwa ameyakana maarifa ya akili kwa akili, na akatoa dalili ya kutokuweko kitu kwa kuweko kwake.

Pili : Hata kama tungekubali kuwa hakuna njia ya maarifa isipokuwa hisia na majaribio, bado tunamthibitisha Mwenyezi Mungu kwa njia hiyo hiyo hasa. Kwamba yuko katika kila mashuhudio ya maumbile.

Ushuhuda huu umefikia ukomo wa uwazi na ufafanuzi na kutufikisha kwenye ilimu ya mwanzilishi, kwa kiasi cha kuangalia tu na kuchunguza bila ya kuhitajia mitambo wala ala zozote.

Lau kungekua kumjua Mwenyezi Mungu kunahitajia mitambo, basi kumwamini Mungu kungelikuwa kwa wataalamu peke yao, na isingelifaa kwa Mwenyezi Mungu kuwambia watu wote:“Enyi watu! Mcheni Mola wenu.”

Inajulikana wazi kuwa yeye, ambaye imetukuka hekima yake, amewajibisha imani kwa waja wake wote, lakini baada ya kuwawekea dalili mkataa ya kuondoa udhuru wote wa kutokuweko kwake. Mwenyezi Mungu (s.w.t) amezisimamisha dalili hizi kutokana na maumbile ya kiakili na kwenye hisia vilevile kwa kutumia msingi wa kiakili unaosema: “Ushahidi ni wa mwenye kudai.”

Sisi sio tuliojitungia maneno haya wala kukosa adabu; isipokuwa Yeye, ambaye imetukuka hikima yake, ndiye aliyesema:

سَنُرِيهِمْ آيَاتِنَا فِي الْآفَاقِ وَفِي أَنفُسِهِمْ حَتَّىٰ يَتَبَيَّنَ لَهُمْ أَنَّهُ الْحَقُّ ﴿٥٣﴾

“Tutawaonyesha Ishara zetu katika upeo wa mbali na katika nafsi zao mpaka iwabainikie kwamba haya ni kweli.” Juz. 24 (41:53)

Mtu mwenyewe na vilivyo katika upeo ni katika vinavyoshudiwa na vinavyohisiwa vinavyofahamisha kuweko Mwenyezi Mungu. Na kwavyo inadhihiri haki isiyokuwa na shaka.

Mwenye kufuatilia Aya za Qur’an yenye hikima atajikuta yuko mbele ya idadi ya ishara hizi za kilimwengu zinazotoa mwito wa kumwamini Mwenyezi Mungu kwa njia ya maarifa ambayo ni matunda ya hisia na akili; miongoni mwayo ni kauli yake Mwenyezi Mungu Mtufu: “Je, hawatazami ufalme wa mbingu na ardhi na alivyoviumba Mwenyezi Mungu” Juz. 9 (7:185). Yaani vitu vinavyohisiwa na kuguswa.

Kumwamini Mwenyezi Mungu ni imani isiyoonwa na jicho wala kuguswa na mkono, lakini imani hii inalazimishwa na kuwekwa na vinavyoonwa na vinavyoguswa; sawa na anavyoamini daktari mjuzi kuwa kwenye mwili wa binadamu kuna ugonjwa fulani.

Na anaweza kugundua hivyo, kwa kiasi cha kumshika tu mgonjwa, bila ya kutumia darubini au kipimo chochote. Hakuna yeyote awe mumin au mlahidi ila atakuwa anaamini, kwa imani ya mkato, vitu vingi visivyoingia kwenye hisia.

Na katika mbingu ziko riziki zenu na mliyoahidiwa.

Yaani kuna sababu za riziki zenu; kama vile mvua n.k. Wakale walisema: “Lau si mbingu, watu wasingelibakia.”

Wametofautiana katika tafsiri ya “mliyoahidiwa.” Kuna aliyesema ni Pepo na Moto, mwingine akaseama ni heri na shari na wa tatu akasema ni riziki inayogawanywa.

Rai yetu ni kuwa Makusudio ya ya mliyoahidiwa ni sababu hasa za riziki, kwa dalili ya kuwa, Mwenyezi Mungu Mtufu, ameashiria kwenye Aya kwamba katika ardhi na katika nafsi zetu kuna ishara za kuhisiwa zinazoguswa, zinazomfahaisha Mwenyezi Mungu Mtufu na ukuu wake. Na kimsingi ni kuwa ishara za kuhisiwa katika mbingu zitakuwa ni mvua na sayari na wala sio Pepo, Moto nk.

Basi naapa kwa Mola wa mbingu na ardhi, hakika haya ni kweli kama ilivyo, kuwa nyinyi mnasema.

Razi amesema dhamiri inarudia kwenye Qur’an, kwa hiyo isemwe: ‘Hakika hiyo ni kweli;’ kama kwamba Mwenyezi Mungu amesema: Hakika Qur’an ni haki wameitamka malaika kama mnavyotamka nyinyi.

Hakuna mwenye shaka kuwa Qur’an ni haki isiyo na shaka na kwamba Jibril ameitamka pia, lakini kuanzia mwanzo wa sura hii hadi hapa tulipo bado haijatajwa Qur’an wala Malaika. Iiyotajwa ni siku ya malipo na hisabu katika Aya 12, kisha Mwenyezi Mungu akataja yaliyo katika ardhi na mbinguni kuwa ni dalili ya kuweko aliyeyaanzisha. Basi bora ni kuirudisha dhamiri kwenye yote haya.

Kwa hiyo basi Maana ni kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) ameapa kwa utukufu wake kwamba Mwenyezi Mungu ni haki na ufufuo ni haki, wala haitakikani kutia shaka katika hayo, baada ya kusimama dalili; sawa na inavyotakikana kwa mtu kutoyatilia shaka aliyoyatamka.

Kuna riwaya inayosema kuwa bedui mmoja aliposikia Aya hii, alisema: “Nani huyo aliyemkasirisha Mwenyezi Mungu Mtufu mpaka akalazimika kuapa?” Haya si mageni kwa ambaye amekulia katika umbile alilozaliwa nalo.

Kwa manasaba wa hayo ni kua watu wa lugha wanasema: matamshi ni aina mbili: ya nje ambayo ni kutamka na ya ndani ambayo ni kufikiria na kutambua. Watu wa mantiki wakasema katika kumwelezea mtu kuwa ni mnyama anayetamka; yaani anayefikiria. Decarte naye anasema: “Mimi ninafikiria, kwa hiyo nipo.”

Misingi hii inakanusha shaka ya kuweko mwenye kufikiria, kwa sababu imetoka kwake hasa. Kwa hiyo tunaweza kufasiri kama ilivyokuwa nyinyi mnasema au kama ilivyokuwa nyinyi mnafikiria. Kwa sababu yote mawili, kutamka na kufikiria, yanakanusha shaka ya kuweko mwenye kutamka au kufikiria.

Je, imekufikia hadithi ya wageni wa Ibrahim wanaohishimiwa?

Neno wageni tumelifasiri kutokana na neno la kiarabu dhayf ambalo lina- tumika kwa mgeni mwanamume au mwanamke, mmoja au wengi.

Makusudio ya wageni wa Ibrahim ni malaika waliokuja kumpa bishara ya kumzaa Is-haq na kuangamizwa kaumu ya Lut. Mwenyezi Mungu (s.w.t) amewapa sifa ya waheshimiwa kwa kuwa ni waheshimiwa kwake na kwa waja wake waumini.

Walipoingia kwake wakasema: Salam! Na yeye akasema: Salam! watu nisiowajua.

Walimwamkia naye akawarudishia, akasema watu hawa hatuwajui.

Akenda kwa ahali yake na akaja na ndama aliyenona.

Ibrahim alifanya haraka kwenda kwa familia yake, akawaamuru wawaandalie wageni ndama aliyenona. Basi ikawa kama alivyotaka, nyama ikaiva,akawakaribisha, akasema: “Mbona hamli? “ Lakini waliendela kutokula, kwa vile wao si watu, hawali chakula.

Akahisi kuwaogopa. Wakasema: Usiwe na khofu, nao wakambashiria kupata kijana mwenye ilimu.

Walimjulisha jambo walilokuja nalo la kumpa habari njema ya kumzaa Is-haq.Ndipo mkewe Sara aliposikia bishara ya Is-haqakawaelekea, na ukelele wa mshangaona akapiga uso wake, kwa furaha na mshangaona kusema : Mimi nikikongwe tasa! Nitazaa kweli?

Wakasema: Ndivyo vivyo hivyo alivyosema Mola wako. Hakika Yeye ni Mwenye hikima Mjuzi.

Mwenyezi Mungu anajua kuwa wewe ni kikongwe tena tasa, lakini hikima yake inataka kukutunuku mtoto pamoja na uzee wako. Mwenyezi Mungu akilitaka jambo ni kuliambia ‘Kuwa na linakuwa.’

Tumefupisha tafsiri ya Aya hizi kwa vile ziko wazi na pia zimekwishatangulia katika Juz. 12 (11: 69-73) na katika Juz. 14 (15:51-56).

15

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA TATU

قَالَ فَمَا خَطْبُكُمْ أَيُّهَا الْمُرْسَلُونَ ﴿٣١﴾

31. Akasema: "Basi makusudio yenu ni nini, enyi mliotumwa?

قَالُوا إِنَّا أُرْسِلْنَا إِلَىٰ قَوْمٍ مُّجْرِمِينَ ﴿٣٢﴾

32. Wakasema: Hakika sisi tume tumwa kwa watu wakosefu.

لِنُرْسِلَ عَلَيْهِمْ حِجَارَةً مِّن طِينٍ ﴿٣٣﴾

33. Tuwatupie mawe ya udongo,

مُّسَوَّمَةً عِندَ رَبِّكَ لِلْمُسْرِفِينَ ﴿٣٤﴾

34. Yaliyotiwa alama kutoka kwa Mola wako kwa ajili ya wanaopituka mipaka.

فَأَخْرَجْنَا مَن كَانَ فِيهَا مِنَ الْمُؤْمِنِينَ ﴿٣٥﴾

35. Kwa hivyo tutawatoa katika hao wale walioamini.

فَمَا وَجَدْنَا فِيهَا غَيْرَ بَيْتٍ مِّنَ الْمُسْلِمِينَ ﴿٣٦﴾

36. Lakini hatukupata humo ila nyumba moja tu yenye Waislamu!

وَتَرَكْنَا فِيهَا آيَةً لِّلَّذِينَ يَخَافُونَ الْعَذَابَ الْأَلِيمَ ﴿٣٧﴾

37. Na tukaacha humo Ishara kwa ajili ya wanaoiogopa adhabu chungu.

وَفِي مُوسَىٰ إِذْ أَرْسَلْنَاهُ إِلَىٰ فِرْعَوْنَ بِسُلْطَانٍ مُّبِينٍ ﴿٣٨﴾

38. Na katika Musa, tulipomtuma kwa Firauni na hoja wazi.

فَتَوَلَّىٰ بِرُكْنِهِ وَقَالَ سَاحِرٌ أَوْ مَجْنُونٌ ﴿٣٩﴾

39. Lakini alipuuza kwa sababu ya nguvu zake na akasema: Huyu ni mchawi au mwendawazimu!

فَأَخَذْنَاهُ وَجُنُودَهُ فَنَبَذْنَاهُمْ فِي الْيَمِّ وَهُوَ مُلِيمٌ ﴿٤٠﴾

40. Basi tukamkamata yeye na majeshi yake na tukawatupa baharini, na yeye ndiye wa kulaumiwa.

وَفِي عَادٍ إِذْ أَرْسَلْنَا عَلَيْهِمُ الرِّيحَ الْعَقِيمَ ﴿٤١﴾

41. Na katika A’di tulipowapelekea upepo wa kukata uzazi.

مَا تَذَرُ مِن شَيْءٍ أَتَتْ عَلَيْهِ إِلَّا جَعَلَتْهُ كَالرَّمِيمِ ﴿٤٢﴾

42. Haukuacha chochote ulichokifikia ila ulikifanya kama unga.

وَفِي ثَمُودَ إِذْ قِيلَ لَهُمْ تَمَتَّعُوا حَتَّىٰ حِينٍ ﴿٤٣﴾

43. Na katika Thamudi walipoambiwa: Stareheni kwa muda mdogo tu.

فَعَتَوْا عَنْ أَمْرِ رَبِّهِمْ فَأَخَذَتْهُمُ الصَّاعِقَةُ وَهُمْ يَنظُرُونَ ﴿٤٤﴾

44. Basi wakaasi amri ya Mola wao, mara kimondo kikawanyakua nao wanaona.

فَمَا اسْتَطَاعُوا مِن قِيَامٍ وَمَا كَانُوا مُنتَصِرِينَ ﴿٤٥﴾

45. Basi hawakuweza kusimama wala hawakuwa wenye kujitetea.

وَقَوْمَ نُوحٍ مِّن قَبْلُ إِنَّهُمْ كَانُوا قَوْمًا فَاسِقِينَ ﴿٤٦﴾

46. Na kaumu ya Nuh hapo mbele. Hakika hao walikuwa watu mafasiki.

BASI MAKUSUDIO YENU NI NINI ENYI MLIOTUMWA?

Aya 31 – 46

MAANA

Akasema: Basi makusudio yenu ni nini, enyi mliotumwa?

Ibrahim(a.s) anawauliza wageni wake baada ya kuwajua ni akina nani, kuwa je, wanakwenda wapi na wanataka nini?

Wakasema: Hakika sisi tumetumwa kwa watu wakosefu; yaani kaumu ya Lut. Walikuwa ni wakosefu waliopituka mipaka, kwani walikuwa wakiwaendea wanaume kwa matamanio badala ya wanawake.

Tuwatupie mawe ya udongo, yaliyotiwa alama kutoka kwa Mola wako kwa ajili ya wanaopituka mipaka.

Tutawaangamiza kwa mawe yaliyotiwa alama yanayotokana na udongo mkavu aliyoyaandaa Mwenyezi Mungu kwa wanaopituka mipaka katika ukafiri dhulma na ufisadi.

Kwa hivyo tutawatoa katika hao wale walioamini ili yasiwasibu yale yatakayowasibu waliopituka mipaka.

Lakini hatukupata humo ila nyumba moja tu yenye Waislamu! Hiyo ni nyumba ya Lut, ukimtoa mkewe aliyekuwa katika walioangamia.

Na tukaacha humo Ishara kwa ajili ya wanaoiogopa adhabu chungu.

Yaani humo mjini mwa watu wa Lut. Makusudio ya ishara ni athari zinazojulisha kuangamia kwao na adhabua yao, ili iwe ni funzo kwa mwenye kutaamali.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 8 (7: 80-84) na Juz. 12 (11: 77-83).

Na katika habari zaMusa, tulipomtuma kwa Firauni na hoja wazi.

Mwenyezi Mungu alimtuma Musa kwa Firauni akiwa na miujiza ya kutosheleza kumkemea Firauni na upotevu wake,Lakini alipuuza kwa sababu ya nguvu zake.

Alipuuza kwa kughurika na jeshi lake na utawala wake.

Na akasema: Huyu ni mchawi au mwendawazimu!

Kwa nini Musa ni mchawi au mwendawazimu katika mantiki ya Musa? Ni kwa vile alimwambia wewe si Mungu wa kuabudiwa na akamhadharisha na dhulma na kupituka mipaka.

Basi tukamkamata yeye na majeshi yake na tukawatupa baharini, na yeye ndiye wa kulaumiwa.

Alipituka mipaka na akasema: Mimi ndiye Mola wenu mkubwa, ikawa mwisho wake ni kuangamia na kulaumiwa.

Katika ziada ya maneno ni kuwa huko nyuma tuliashiria sababu za kukaririka. Katika Juz. 16 (20:9-16), tulitaja sababu za kukaririka kisa cha Musa. Ama hapa tunasema: “Mwenyezi Mungu ndiye mjuzi zaidi.”

Na katika habari zaA’di tulipowapelekea upepo wa kukata uzazi.

Mwenyezi Mungu aliwaangamiza A’di na kaumu ya Hud kwa upepo unaovuma, unaobomoa kila kitu.Haukuacha chochote ulichokifikia ila ulikifanya kama unga. Kila unachokipitia unakivunja na kukipondaponda.

Kisa cha Hud na watu wake kimetangulia katika Juz. 8 (7:73-79) na Juz. 12 (11:50-60).

Na katika habari zaThamudi walipoambiwa: Stareheni kwa muda mdogo tu.

Thamud ni watu wa Swaleh. Aya hii inaashiria yaliyoelezwa katika Juz. 12 (11:65): “Basi (Swaleh) akasema: Stareheni katika mji wenu kwa siku tatu. Hiyo ni ahadi isiyokadhibishwa.”

Basi wakaasi amri ya Mola wao, mara kimondo kikawanyakua nao wanaona.

Walimwasi Mwenyezi Mungu na Mtume, ndio Mwenyezi Mungu (s.w.t.) akawateremshia adhabu kutoka mbinguni.

Walipoona zikipomoka nguvu zao,basi hawakuweza kusimama wala hawakuwa wenye kujitetea.

وَإِذَا أَرَادَ اللَّـهُ بِقَوْمٍ سُوءًا فَلَا مَرَدَّ لَهُ وَمَا لَهُم مِّن دُونِهِ مِن وَالٍ ﴿١١﴾

“Mwenyezi Mungu akiwatakia watu uovu hakuna cha kuwazuia wala hawana mlinzi yeyote badala yake.” Juz. 13 (13:11).

Kisa cha Swaleh kimetangulia katika Juz. 8 (7: 73 – 79) na katika Juz. 12 (11: 61-68).

Na kaumu ya Nuh hapo mbele Mwenyezi Mungu aliwaangamiza kwa dhambi zao.

Hakika hao walikuwa watu mafasiki wakifanya mambo ya kuangamiza na kuvunja miko ya haramu. Kimetangulia kisa cha Nuh, Juz. 8 (7: 59 – 64) Juz. 12 (11: 25-49).

وَالسَّمَاءَ بَنَيْنَاهَا بِأَيْدٍ وَإِنَّا لَمُوسِعُونَ ﴿٤٧﴾

47. Na mbingu tumezifanya kwa nguvu na uwezo na hakika Sisi bila ya shaka ndio wenye kutanua.

وَالْأَرْضَ فَرَشْنَاهَا فَنِعْمَ الْمَاهِدُونَ ﴿٤٨﴾

48. Na ardhi tumeitandaza; basi bora ya watandazaji ni sisi.

وَمِن كُلِّ شَيْءٍ خَلَقْنَا زَوْجَيْنِ لَعَلَّكُمْ تَذَكَّرُونَ ﴿٤٩﴾

49. Na katika kila kitu tumeumba dume na jike ili mzingatie.

فَفِرُّوا إِلَى اللَّـهِ إِنِّي لَكُم مِّنْهُ نَذِيرٌ مُّبِينٌ ﴿٥٠﴾

50. Basi kimbilieni kwa Mwenyezi Mungu, hakika mimi ni mwonyaji kwenu wa kubainisha nitokae kwake.

وَلَا تَجْعَلُوا مَعَ اللَّـهِ إِلَـٰهًا آخَرَ إِنِّي لَكُم مِّنْهُ نَذِيرٌ مُّبِينٌ ﴿٥١﴾

51. Wala msifanye kuwa kuna mungu mwengine pamoja na Mwenyezi Mungu. Hakika mimi ni mwonyaji kwenu wa kubainisha nitokaye kwake.

كَذَٰلِكَ مَا أَتَى الَّذِينَ مِن قَبْلِهِم مِّن رَّسُولٍ إِلَّا قَالُوا سَاحِرٌ أَوْ مَجْنُونٌ ﴿٥٢﴾

52. Basi ndio hivyo hivyo, hakuwajia kabla yao Mtume ila walisema: Huyu ni mchawi au mwendawazimu.

أَتَوَاصَوْا بِهِ بَلْ هُمْ قَوْمٌ طَاغُونَ ﴿٥٣﴾

53. Je, wameusiana kwa haya? Bali hawa ni watu waasi.

فَتَوَلَّ عَنْهُمْ فَمَا أَنتَ بِمَلُومٍ ﴿٥٤﴾

54. Basi waachilie mbali, nawe hulaumiwi.

وَذَكِّرْ فَإِنَّ الذِّكْرَىٰ تَنفَعُ الْمُؤْمِنِينَ ﴿٥٥﴾

55. Na kumbusha, kwani ukumbusho huwafaa waumini.

وَمَا خَلَقْتُ الْجِنَّ وَالْإِنسَ إِلَّا لِيَعْبُدُونِ ﴿٥٦﴾

56. Na sikuwaumba majini na watu ila waniabudu.

مَا أُرِيدُ مِنْهُم مِّن رِّزْقٍ وَمَا أُرِيدُ أَن يُطْعِمُونِ ﴿٥٧﴾

57. Sitaki kwao riziki, wala sitaki wanilishe.

إِنَّ اللَّـهَ هُوَ الرَّزَّاقُ ذُو الْقُوَّةِ الْمَتِينُ ﴿٥٨﴾

58. Hakika Mwenyezi Mungu ndiye Mwenye kuruzuku, Mwenye nguvu, Madhubuti.

فَإِنَّ لِلَّذِينَ ظَلَمُوا ذَنُوبًا مِّثْلَ ذَنُوبِ أَصْحَابِهِمْ فَلَا يَسْتَعْجِلُونِ ﴿٥٩﴾

59. Hakika waliodhulumu wana fungu lao la adhabu kama fungu la wenzao. Basi wasiniharakishe

فَوَيْلٌ لِّلَّذِينَ كَفَرُوا مِن يَوْمِهِمُ الَّذِي يُوعَدُونَ ﴿٦٠﴾

60. Ole wao walioikanusha siku yao waliyoahidiwa.

KILA KITU TUMEUMBA DUME NA JIKE

Aya 47 – 60

MAANA

Na mbingu tumezifanya kwa nguvu na uwezo na hakika Sisi bila ya shaka ndio wenye kutanua.

Baadhi ya wafasiri wamesema kuwa Makusudio ya kutanua hapa ni kuwa Mwenyezi Mungu anaipanua riziki kwa viumbe wake kwa mvua.

Lakini maana yanayoafikiana na hali halisi na ufahamisho wa Aya, ni kuwa Makusudio ya ya mbingu ni kwa maana yake yaliyo dhahiri; kuwa ni anga pana iliyo na nyota n.k.

Na Makusudio ya kutanua ni kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) anaizidisha anga upana kila siku zinavyoendelea kupita.

Wataalamau wanasema kuwa anga inaendela kujivuta kadiri siku zinavyopita, na kwamba ukubwa wa anga ya ulimwengu hivi sasa ni mara kumi zaidi tangu ilipoanza kujivuta. Anasema Sir James Jeans:

“Umbali baina ya makundi ya nyota unafikia miaka milioni moja na nusu ya mwendo wa mwanga. Mwanga unakata masafa ya maili milioni 6 katika mwaka mmoja.”

Anasema Camus kuwa imegundulika kutokana na vipimo vikubwa kwamba baina ya nyota kuna masafa ya uwazi yanayokadiriwa kufikia miaka milioni 5 ya mwaka, na kwamba kumehisabiwa makao ya nyota yanayofikia milioni moja, na kuna uwezekano kuwa kuna mkusanyiko mwingine wa makao ya nyota katika masafa yaliyo mbali zaidi. Hayo yanapatikana katika kitabu Attakamul fil Islam, (ukamilifu katika Uislamu) cha Ahmad Amin Al-iraqi Juz. 2 Uk. 67 chapa ya kwanza.

Sisi hatuna hamasa ya Qur’an kuafikiana na sayansi kutokana na hadhari tulizozieleza katika Juz. 1 (2: 2). Lakini hata hivyo hatuwezi kuepuka kusema kuwa Aya hii tukufu ni usadikisho wa ushahidi kuwa muujiza wa Muhammad bin Abdillah(s.a.w. w ) ni wa pekee na wa milele kati ya miujiza ya manabii wote na kwamba unazidi kuwa wazi zaidi kadiri sayansi inavyopiga hatua.

Na ardhi tumeitandaza; basi bora ya watandazaji ni sisi.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) amemwandalia mtu ardhi na akamkunjulia mkono wake humo ili ajenge na afanye mambo ya heri, sio shari na kubomoa. Amemwachia huru mkono wake ili afanye kazi na akampa masharti ya kuuzuia mkono huo dhidi ya ndugu yake binadamu, sio amrushie makombora na mabomu ya sumu kwenye shule za watoto, mahospitalini, na viwandani na kwa kila mwenye kuimba nyimbo ya uhuru na kukataa utumwa isipokuwa kwa Mwenyezi Mungu tu peke yake.

Na katika kila kitu tumeumba dume na jike ili mzingatie.

Dhahiri ya Aya inafahamisha kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) ameumba kila jinsi ya kitu katika viumbe vyote mke na mume; iwe ni binadamu, mnyama, mmea au vitu vigumu, kama mawe n.k. Kwa sababu neno ‘kila kitu’ linaenea kwa vyote.

Hatujui kama wataalamu wameigundua hakika hii au bado wako njiani? Tuliyoyasoma kutoka kwa wataalamu kuhusiana na maudhui haya ni kuwa hakuna chembe yoyote ulimwenguni ila inakuwa imefaungana na kani mbili: chanya na hasi (positive na negative). Yaani nguvu mbili za mvutano. Sijui kama Aya inaafikiana na hali hiyo?

Basi kimbilieni kwa Mwenyezi Mungu, hakika mimi ni mwonyaji kwenu wa kubainisha nitokae kwake.

Kila mwenye kuuzuia mkono wake na kuwaudhi wengine, akasadikisha kauli yake, akaifanyia ikhlasi haki na uadilifu katika vitendo vyake, atakuwa amaeikimbia batili kuiendea haki, atake asitake, lakini muongo mwenye hiyana, huyo ni katika maadui wakubwa wa Mwenyezi Mungu; ajaposoma tahalili na takbiri, akaabudu na kutoa sadaka.

Wala msifanye kuwa kuna mungu mwengine pamoja na Mwenyezi Mungu. Hakika mimi ni mwonyaji kwenu wa kubainisha nitokaye kwake.

Kuna aina nyingi za shirki; miongini mwazo: ni kuabudu masanamu, kumnasibishia Mungu mtoto, kuwa kigeugeu katika dini na kuwatumikia maadui wa Mwenyezi Mungu na wa ubinadamu kwa kutumia jina la uislamu na kuleta masilahi ya waislamu.

Basi ndio hivyo hivyo, hakuwajia kabla yao Mtume ila walisema: Huyu ni mchawi au mwendawazimu.

Wakadhibishaji walikwambia wewe, kama vile wa mwanzo walivyoaambia mitume wao.

Je, wameusiana kwa haya? Bali hawa ni watu waasi.

Ni ajabu kufanana wa mwanzo na wa mwisho katika kuwakadhibisha wenye haki na viongozi wema. Je, walikongamana na kuusiana hilo? Hapana hawakukongamana wala hawakuonana au kuungana. Lililowakusanya ni uadui wa batili dhidi ya haki na ujinga dhidi ya ilimu.

Basi waachilie mbali, nawe hulaumiwi.

Usujitoe roho na kufuru yao na uasi wao ewe Muhammad! Wewe hutaulizwa kuhusu dini yao wala kauli zao na vitendo vyao.

Na kumbusha, kwani ukumbusho huwafaa Waumini.

Umuhimu wako ewe Muhammad! Ni kufikisha Qur’an na kuwatolea mawaidha kwayo watu wote. Ikiwa hatanufaika na mawaidha mwenye kung’ang’ania ukafiri na ufisadi, basi atanufaika nayo mwenye kuitafuta haki ili aiamani na kuitumia kwa mujibu wake.

Na sikuwaumba majini na watu ila waniabudu.

Maana ya kumwabudu Mwenyezi Mungu peke yake ni kuwa huru kwa kutomwabudu mtu, mali, cheo na matamanio yote, na kutonyenyekea isipokuwa kwa haki tu na uadlifu.

Vile vile, kumwabudu Mungu, kunamaanisha kufanya juhudi ya kuinusuru haki na watu wake na kufanya mambo kwa ajili ya dunia na Akhera. Hakuna anayetia shaka kwamba mwenye kufuata njia hii itampeleka kwenye nyumba ya amani.

Kwa hiyo basi lengo la kuumbwa majini na watu ni kuishi maisha mema ya milele katika nyumba ya Mwenyezi Mungu kwa sharti ya kujikomboa na aina zote za utumwa na kufanya mambo mema. Mwenye kupuuza na akazembea, asilaumu ila nafsi yake. Na Mola wako si mwenye kudhulumu waja.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 21(31:33-34), kifungu cha: ‘Kwa nini Mungu akamuumba mtu?’

Unaweza kuuliza : Utafanya nini na Hadith Qudsi inayosema: “Nilikuwa hazina iliyojificha nikataka nijulikane, basi nikaumba viumbe wakanijua,” si inafahamisha wazi kuwa lengo la kuumbwa ni kumjua Mungu?

Jibu : Hadith hii inaafikiana kwa ukamilifu na tafsiri tuliyoitaja. Kwa sababu mwenye kumjua Mwenyezi Mungu kisawasawa, hatahitajia kuwaabudu watu, cheo au mali na atafanya kulinga na radhi ya Mwenyezi Mungu na Pepo yake.

Sitaki kwao riziki, wala sitaki wanilishe.

Ni kama Mwenyezi Mungu, aliyetukuka kabisa, anasema: Sikuwaumba viumbe ili niwatumie kwenye viwanda vyangu na mashamba yangu.

Wala si kwa kuwatuma sokoni kwenda kuniuzia bidhaa zangu; wala pia sikuwaumba kwa ajili ya kuwapiga vita wanaoshindana na mimi katika uporaji na ulanguzi.

Hapana! Mwenyezi Mungu ni mwenye kujitosha na walimwengu wote. Amewaumba ili tu wafanye amali kwa pamoja kwa ajili ya heri yao wote na wapigane jihadi na yule atayejaribu kuingilia uhuru wao, heshima yao na kupora mali zao, ardhi zao na majumba yao.

Hakika Mwenyezi Mungu ndiye Mwenye kuruzuku, Mwenye nguvu, Madhubuti.

Maana ya kuwa Mwenyezi Mungu ni mwenye kuruzuku ni kuwa yeye aliye Mtukufu, amemuumbia mtu maisha na akampa nyenzo zitakazomwezesha kuvuna matunda kwa ajili ya maisha yake; kama vile akili, nguvu, usikizi na uoni, na akamwambia: shughulika kwa ajili ya dunia yako na Akhera yako, wala usifanye uchokozi, kwani Mwenyezi Mungu hapendi wachokozi.

Ni sawa na mtoto wako kama utampa mali na kumwambia: fanya biashara kwa ajili ya maisha yako na uwe mwaminifu katika muamala wako.

Hakika waliodhulumu wana fungu lao la adhabu kama fungu la wenzao.

Makusudio ya waliodhulumu hapa ni mataghuti ambao walimkadhibisha Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w. w ) . Maana ni kuwa fungu la adhabu ya hawa ni sawa na la uma zilizotangulia, walipowakadhibisha mitume wao

Basi wasiniharakishe adhabu ambayo itawshukia tu. Na leo iko karibu sana na kesho.

Ole wao walioikanusha siku yao waliyoahidiwa wanayoiharakisha. Mara ngapi mwenye kuliharakisha jambo, likija anapendelea lisingekuwa!

MWISHO WA SURA YA HAMSINI NA MOJA: SURAT ADH-DHARIYAT