TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE Juzuu 24

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE12%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: Qurani tukufu

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
  • Anza
  • Iliyopita
  • 30 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 28928 / Pakua: 5102
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE Juzuu 24

Mwandishi:
Swahili

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE

IMEANDIKWA NA: SHEIKH MUHAMMAD JAWAD MUGHNIYYA

IMETAFSIRIWA NA: SHEIKH HASAN MWALUPA

IMEHARIRIWA NA: USTADH ABDALLAH MOHAMED

IMEPANGWA KATIKA KOMPYUTA NA: UKHT PILI RAJABU

UTANGULIZI WA MCHAPISHAJI

Kitabu hiki kilichoko mikononi mwako hivi sasa ni juhudi ya miaka mingi sana ya watu waliojitolea kuona kazi hii imefanikiwa bila ya kumsahau Marhum Abu Muhammad wa London.

Kama lilivyo jina la Tafsiri ndivyo ilivyo Tafsiri yenyewe ambayo mwanachuoni huyu mahiri kabisa aliyeifafanua ni mtu aliyebobea katika fani zote ambazo mfasiri (Mfafanuzi) anatakiwa awe nazo.

Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya ameonesha cheche zake katika vitabu vingi alivyoviandika katika maudhui mbali mbalimbali na hivyo kujipatia wasomaji wengi sana.

Msomi huyu, mwenye fikra huru na anayetetea kile anachokiamini, ni mtu mwenye mawazo mapana na kuyaangalia mambo kwa undani sana, kipaumbele chake ni katika maslahi ya umma huu na amejaribu sana kwenda na wakati.

Sifa kubwa pekee ya mwanachuoni huyu ni kuwa yeye hakujihusisha sana na kung'ang'ania madhehebu fulani tu, labda hii yatokana na wadhifa wake wa ukadhi aliokuwa nao katika nchi ya Lebanon ambayo ina madhehebu mengi, ambapo sula la madhehebu ni nyeti nchini humo, hata hivyo yeye aliweza kuamua matatizo ya watu kwenye ofisi yake kulingana na madhehebu yao pale walipomwendea. Hiyo ilimsaidia sana hata kuweza kutoa kitabu kitwacho Al-Fiqh a'laa madhaahabil-khamsah (Fikhi ya madhehebu matano) yaani ya Hanafi, Maaliki, Shafi, Hambali na Shia (ambacho twataraji kitatoka kwa lugha ya kiswahili hivi karibuni Inshaallah).

Jambo lililotupa msukumo wa kukifasiri kitabu hiki kwa lugha ya Kiswahili ni zile faida nyingi atakazozipata msomaji na kujua mambo mengi na ya ajabu yaliyo mapya kwake ambayo si rahisi kuyapata kwa wafasiri wengine.

Msomaji atapata faida katika fani za Sayansi, Siasa, Historia, Mashairi, visa vizuri, na Saikolojia miongoni mwa mengine; ndiyo maana msomaji atashangaa kidogo anapoisoma Tafsiri hii atakapoona mwandishi amewataja na kuwanukuu watu kama kina Mfalme Edward, wanasayansi kama kina Enstein, wasanii kama Charlie Champlin (Mchekeshaji maarufu), na wengineo, hali inayoifanya tafsiri hii kuwa ni ya kipekee kabisa.

Mtindo alioutumia mwandishi ni sahali uliokusudiwa watu wa tabaka mbalimbali, wanavyuoni na watu wa kawaida.

Nia yetu ni kukigawanya kitabu hiki bure lakini tumelazimika kukiuza kwa bei nafuu ili kurudisha gharama za uchapishaji.

Mwisho: Shukrani kubwa iwaendee bila ya kuwataja watu waliojitolea usiku na mchana, jopo la wafasiri, wahariri, wachapaji, waliotupa moyo na kutoa maoni yao na walioisimamia ili kuhakikisha kwamba kitabu kimemfikia msomaji.

MAKOSA YA CHAPA

Sikumbuki kama nimewahi kusoma kitabu kilichotoka kupigwa chapa, cha zamani au cha sasa, bila ya kukuta makosa ya chapa, Nafikiri sitasoma kitabu kisichokuwa hivyo. Nimejaribu sana kuliepuka hilo katika tungo zangu, lakini sikufanikiwa.

Nilikuwa sifikirii kama ninaweza kuona makosa haya katika maandishi ya msahafu mtukufu, kama yale yaliyo katika baadhi ya chapa; kwa mfano neno yabswutu kwa swad, badala ya yabsutu kwa sin, na katika chapa ya Tafsir Arrazi ya Misr ya mwaka 1935, Sura ya (2:146), Imeandikwa La Ya'alamuun, (hawajui) badala ya Ya'alamuun (wanajua). Mfano wa makosa haya hausameheki.

Katika Tafsir Al-Manar, chapa ya Pili, sura (5:212), imeandikwa Fawqahum ila yawmil qiyama badala ya Fawqahum yawamal qiyama. Hatuwezi kusema kosa hili ni kubwa zaidi kuliko lile.

Lakini mkosaji atatuletea udhuru kwa msemo mashuhuri huko kwetu Jabal amil 'Makosa ya chapa.'

Katika Tafsiri Majmau chapa ya Urfan, Sura (46:15), imeandikwa: Hatta idha balagha arbai' na sanah badala ya: Hattaidha balagha ashuddahu arbai ' na sanah"

Kusema hivi sio kama ninajitetea kutokana na makosa ya chapa atakayoyakuta msomaji katika kitabu hiki, ijapokuwa naomba msamaha kama litatokea hili, lakini makusudio yangu hasa ni kumwambia yule atakayefungua macho yake kwenye makosa ya matamko na kuufungia macho uzuri wa maana.

Vilevile ninamwambia yule ambaye siku moja aliniambia: "Vitabu vyako vimejaa makosa ya chapa.” Kama kwamba hakuna kitu chochote katika vitabu hivyo isipokuwa makosa ya chapa tu. Wote hao ninawaambia: Mungu awasamehe na aniongoze mimi na nyinyi.

Vyovyote iwavyo, mimi ninaomba msamaha kutokana na makosa ya kifikra na ya chapa. Anasema Amirul Muminiin(a.s) :"Watu wote ni wapungufu wenye kuchanganyikiwa, isipokuwa yule aliyehifadhiwa na Mwenyezi Mungu." Na Mwenyezi Mungu (s.w.t) ndiye mwenye jukumu la kunikubalia yale niliyoyapatia na kunisamehe niliyakosea, kwa jaha ya Mtume na kizazi chake, ziwashukie rehema na amani (Amin).

MUHAMMAD JAWAD MUGHNIYYAH

1

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE

Sura Ya Hamsini Na Nane: Al–Mujadala. Imeshuka Madina. Imesemekana kinyume na hivyo, Ina Aya 22.

بِسْمِ اللَّهِ الرَّحْمَٰنِ الرَّحِيمِ

Kwa jina la Mwenyezi Mungu Mwingi wa rehema, Mwenye kurehemu.

قَدْ سَمِعَ اللَّـهُ قَوْلَ الَّتِي تُجَادِلُكَ فِي زَوْجِهَا وَتَشْتَكِي إِلَى اللَّـهِ وَاللَّـهُ يَسْمَعُ تَحَاوُرَكُمَا إِنَّ اللَّـهَ سَمِيعٌ بَصِيرٌ ﴿١﴾

1. Mwenyezi Mungu amekwisha­sikia usemi wa mwanamke anayejadiliana nawe juu ya mumewe, na anamshitakia Mwenyezi Mungu. Na Mwenyezi Mungu anayasikia majibizano yenu. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusikia, Mwenye kuona.

الَّذِينَ يُظَاهِرُونَ مِنكُم مِّن نِّسَائِهِم مَّا هُنَّ أُمَّهَاتِهِمْ إِنْ أُمَّهَاتُهُمْ إِلَّا اللَّائِي وَلَدْنَهُمْ وَإِنَّهُمْ لَيَقُولُونَ مُنكَرًا مِّنَ الْقَوْلِ وَزُورًا وَإِنَّ اللَّـهَ لَعَفُوٌّ غَفُورٌ ﴿٢﴾

2. Wale miongoni mwenu wanaowafanyia dh h. wake zao, hao si mama zao. Hawakuwa mama zao ila wale waliowazaa. Na hakika hao wanasema neno linalochusha na la uwongo. Na hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusamehe, Mwenye kughufi­ria.

وَالَّذِينَ يُظَاهِرُونَ مِن نِّسَائِهِمْ ثُمَّ يَعُودُونَ لِمَا قَالُوا فَتَحْرِيرُ رَقَبَةٍ مِّن قَبْلِ أَن يَتَمَاسَّا ذَٰلِكُمْ تُوعَظُونَ بِهِ وَاللَّـهُ بِمَا تَعْمَلُونَ خَبِيرٌ ﴿٣﴾

3. Na wale wanaowafanyia dhiha­ wake zao kisha wakarudi kuachana na yale walioyase­ma, basi ni kumwacha huru mtumwa kabla hawajagusana. Mnapewa mawaidha kwa hayo. Na Mwenyezi Mungu anayajua mnayoyatenda.

فَمَن لَّمْ يَجِدْ فَصِيَامُ شَهْرَيْنِ مُتَتَابِعَيْنِ مِن قَبْلِ أَن يَتَمَاسَّا فَمَن لَّمْ يَسْتَطِعْ فَإِطْعَامُ سِتِّينَ مِسْكِينًا ذَٰلِكَ لِتُؤْمِنُوا بِاللَّـهِ وَرَسُولِهِ وَتِلْكَ حُدُودُ اللَّـهِ وَلِلْكَافِرِينَ عَذَابٌ أَلِيمٌ ﴿٤﴾

4. Na asiyepata, basi afunge miezi miwili ya kufuatana kabla hawajagusana. Na asiyeweza basi awalishe masikini sitini. Hayo ni hivyo ili mumwamini Mwenyezi Mungu na Mtume wake. Na hiyo ndiyo mipaka ya Mwenyezi Mungu Na kwa makafiri iko adhabu chungu.

DHIHAR

Aya 1 – 4

LUGHA

Dhihar ni mume kumwambia mkewe: ‘Wewe kwangu ni kama mgongo wa mama yangu;’ akimaanisha kuwa ni haramu kwake kama alivyo mama yake. Akishasema hivyo basi mke anakuwa haramu kwake mpaka atoe kafara; kama yatakavyokuja maelezo.

KISA KWA UFUPI

Wameafikiana wafasiri kuwa Aya hizi zilishuka kwa tukio maalum. Kwa ufupi, tukio lenyewe ni kama ifutavyo:-

Mtu mmoja alimkasirikia mkewe akamwambia: wewe kwangu ni kama mgongo wa mama yangu, na hiyo ilikuwa ni talaka wakati wa Jahilia. Basi mwanamke akahuzunika, na mwanamume akajuta kwa haraka yake alioifanya, akamwambia mkewe nenda kwa Mtume umpe habari ya yaliyotokea, mimi ninaona haya kumuuliza.

Mke akaenda na kumsimulia Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w. w ) na akamsisitiza, huku akisema: Ninamshtakia Mwenyezi Mungu haja yangu. Mwenyezi Mungu akaitikia dua yake na akateremsha Aya hizi. Kisa hiki kinaafikiana na dhahiri ya Aya.

Vyovyote iwavyo ni kuwa: Dhihar ni mlango katika milango ya fiqhi ya waislamu.

MAANA

Mwenyezi Mungu amekwishasikia usemi wa mwanamke anayejadiliana nawe juu ya mumewe, na anamshitakia Mwenyezi Mungu. Na Mwenyezi Mungu anayasikia majibizano yenu.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) anamwambia Mtume wake mtukufu kuwa Mwenyezi Mungu amekwishajua hali ya mwanamke na anavyokuelezea kuhusu mumewe. Vile vile amekwishajua mashtaka yake na maombi yake; na amekwishaitikia maombi yake.Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusikia, Mwenye kuona; hakifichiki kwake chochote cha kujificha.

Kisha Mwenyezi Mungu (s.w.t) akabainisha hukumu ya tukio hili na mfano wake kwa kusema:

Wale miongoni mwenu wanaowafanyia dh h. wake zao, hao si mama zao. Hawakuwa mama zao ila wale waliowazaa. Na hakika hao wanasema neno linalochusha na la uwongo.

Dhihari imeharamishwa katika dini ya Mwenyezi Mungu, kwa sababu ni uwongo unaohalifu uhalisia. Vipi mke awe ni mama!

Na hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusamehe, Mwenye kughufiria, yule mwenye kutubia na akarejea nyuma. Baadhi ya mafakihi wame­sema kuwa dhihari ni haramu hilo halina shaka yoyote, kwa sababu Mwenyezi Mungu ameisifu kuwa ni ya kuchukiza na ni uwongo, lakini haina dhambi kwa anayeifanya, kwa sababu ameikutanisha na msamaha.

Lakini kauli ya kutokuwa na dhambi ameirudi Shahidi wa pili kwa kuse­ma kuwa msamaha katika Aya ni wakiujumla na hauhusiki na dhihari.

Na wale wanaowafanyia Dhihar wake zao kisha wakarudi kuachana na yale waliyoyasema, basi ni kumwacha huru mtumwa kabla hawajagusana.

Kurudi na kuyaacha yale waliyoyasema ni wale wanaofanya dhihari kisha wakajuta na kuiacha kauli yao.

Ibn Hisham, katika Mughni anasema: herufi lam inakuja kwa maana ya herufi a’yn (kuachana na) kama ilivyo katika Juz. 12 (11:31). Pia huwa inakuja kwa maana ya herufi fi (katika); kama ilivyo katika Juz. 17 (21:47). Wametofautiana kuhusu kugusana.

Kuna waliosema kuwa ni kugusana kwa maana yake ya kilugha yalivyo. Wengine wakasema ni kuingiliana. Kauli hii haiko mbali na lugha ya Qur’an; kama alivyosema Mwenyezi Mungu: “Na kama mkiwapa talaka kabla ya kuwagusa…” Juz. 2 (2:237), kwa maana ya kabla ya kuwaingilia; kama walivyoafikina mafakihi

Mnapewa mawaidha kwa hayo. Na Mwenyezi Mungu anayajua mnayoyatenda.

‘Hayo,’ ni hayo ya wajibu wa kafara la dhihari. Makusudio ya mawaidha hapa ni maonyo. Maana ni kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) amewajibisha kafara la dhihari ili liwe ni onyo na kukemea isifanyike, kwa sababu ni jambo la kuchukiza na ni uwongo. Na Mwenyezi Mungu anamjua muasi na mtiifu na kumfanyia kila mmoja stahiki yake.

Na asiyepata mtumwa wa kumkomboa,basi afunge miezi miwili ya kufuatana kabla hawajagusana. Na asiyeweza basi awalishe maskini sitini.

Wameafikiana kwamba mwenye kumwambia mkewe: Wewe kwangu ni kama mgongo wa mama yangu,’ haiwi halali kwake kumwingilia mke huyo, mpaka atoe kafara, kwa kumwacha huru mtumwa, akishindwa kupa­ta mtumwa, afunge miezi miwili ya kufuatana na akishindwa kufunga basi awalishe masikini sitini. Vile vile wameafikiana kuwa akimwingilia kabla ya kutoa kafara atakuwa ameasi, lakini Shia Imamiya wamewajibisha kafara mbili kwa hilo.

Shia Imamiya pia wameweka sharti la kuweko waadilifu wawili watakaosikia kauli ya mume na kuwa mke awe katika twahara (asiwe hedhini) ambayo hakuingiliwa na mumewe; sawa na yalivyo masharti ya talaka; kama ambavyo wahakiki miongoni mwao wameweka pia sharti la kuwa awe amekwishawahi kuingiliwa na mumewe; vinginevyo itakuwa hakuna dhihari. Ufafanuzi uko kwenye vitabu vya Fiqh.

Hayo ni hivyo ili mumwamini Mwenyezi Mungu na Mtume wake.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) ameisahilisha sharia kwa waja wake ili waiami­ni na ili iwe ni hoja wazi kwa yule anayeipinga sharia.

Na hiyo ndiyo mipaka ya Mwenyezi Mungu, basi msiikeuke.

Na kwa makafiri iko adhabu chungu kwa kupinga kwao sharia ya Mwenyezi Mungu na hukumu yake. Ndani yake kuna ishara kuwa mwenye kuhalifu sharia ya Mwenyezi Mungu basi anahukumiwa kuwa ni kafiri.

إِنَّ الَّذِينَ يُحَادُّونَ اللَّـهَ وَرَسُولَهُ كُبِتُوا كَمَا كُبِتَ الَّذِينَ مِن قَبْلِهِمْ وَقَدْ أَنزَلْنَا آيَاتٍ بَيِّنَاتٍ وَلِلْكَافِرِينَ عَذَابٌ مُّهِينٌ ﴿٥﴾

5. Hakika wanaopingana na Mwenyezi Mungu na Mtume wake, watadhalilishwa kama walivyodhalilishwa wale waliokuwa kabla yao. Na tulik­wishateremsha Ishara zilizo wazi. Na makafiri watapata adhabu ifedheheshayo.

يَوْمَ يَبْعَثُهُمُ اللَّـهُ جَمِيعًا فَيُنَبِّئُهُم بِمَا عَمِلُوا أَحْصَاهُ اللَّـهُ وَنَسُوهُ وَاللَّـهُ عَلَىٰ كُلِّ شَيْءٍ شَهِيدٌ ﴿٦﴾

6. Siku atapowafufua Mwenyezi Mungu, na awaambie yale waliyoyatenda. Mwenyezi Mungu ameyadhibiti, na wao wameyasahau! Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kushuhu­dia kila kitu.

أَلَمْ تَرَ أَنَّ اللَّـهَ يَعْلَمُ مَا فِي السَّمَاوَاتِ وَمَا فِي الْأَرْضِ مَا يَكُونُ مِن نَّجْوَىٰ ثَلَاثَةٍ إِلَّا هُوَ رَابِعُهُمْ وَلَا خَمْسَةٍ إِلَّا هُوَ سَادِسُهُمْ وَلَا أَدْنَىٰ مِن ذَٰلِكَ وَلَا أَكْثَرَ إِلَّا هُوَ مَعَهُمْ أَيْنَ مَا كَانُوا ثُمَّ يُنَبِّئُهُم بِمَا عَمِلُوا يَوْمَ الْقِيَامَةِ إِنَّ اللَّـهَ بِكُلِّ شَيْءٍ عَلِيمٌ ﴿٧﴾

7. Kwani huoni kwamba Mwenyezi Mungu anajua vilivyo katika mbingu na vilivyo katika ardhi? Hauwi mnong’ono wa watu watatu ila Yeye huwa ni wanne wao, wala wa watano ila Yeye huwa ni wa sita wao. Wala wa wachache kuliko hao, wala walio wengi zaidi, ila Yeye yuko pamoja nao popote pale walipo. Kisha Siku ya Kiyama atawaambia waliyoyatenda. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mjuzi wa kila kitu.

أَلَمْ تَرَ إِلَى الَّذِينَ نُهُوا عَنِ النَّجْوَىٰ ثُمَّ يَعُودُونَ لِمَا نُهُوا عَنْهُ وَيَتَنَاجَوْنَ بِالْإِثْمِ وَالْعُدْوَانِ وَمَعْصِيَتِ الرَّسُولِ وَإِذَا جَاءُوكَ حَيَّوْكَ بِمَا لَمْ يُحَيِّكَ بِهِ اللَّـهُ وَيَقُولُونَ فِي أَنفُسِهِمْ لَوْلَا يُعَذِّبُنَا اللَّـهُ بِمَا نَقُولُ حَسْبُهُمْ جَهَنَّمُ يَصْلَوْنَهَا فَبِئْسَ الْمَصِيرُ ﴿٨﴾

8. Kwani huwaoni wale waliokatazwa kunong’ona, kisha wakayarudia yale uadui, na ya kumwasi Mtume? Na wakikujia hukuamkia sivyo anavyokuamkia Mwenyezi Mungu. Na husema katika nafsi zao: Mbona Mwenyezi Mungu hatuadhibu kwa haya tuyasemayo? Jahannamu itawatosha; wataingia humo! Ni marejeo mabaya sana.

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا إِذَا تَنَاجَيْتُمْ فَلَا تَتَنَاجَوْا بِالْإِثْمِ وَالْعُدْوَانِ وَمَعْصِيَتِ الرَّسُولِ وَتَنَاجَوْا بِالْبِرِّ وَالتَّقْوَىٰ وَاتَّقُوا اللَّـهَ الَّذِي إِلَيْهِ تُحْشَرُونَ ﴿٩﴾

9. Enyi mlioamini! Mnapo nong’onezana. Msinong’onezane kwa sababu ya mambo ya madhambi, na uadui, na kumuasi Mtume. Bali nong’onezaneni kwa kutenda mema na takua. Na mcheni Mwenyezi Mungu ambaye kwake mtakusanywa.

إِنَّمَا النَّجْوَىٰ مِنَ الشَّيْطَانِ لِيَحْزُنَ الَّذِينَ آمَنُوا وَلَيْسَ بِضَارِّهِمْ شَيْئًا إِلَّا بِإِذْنِ اللَّـهِ وَعَلَى اللَّـهِ فَلْيَتَوَكَّلِ الْمُؤْمِنُونَ ﴿١٠﴾

10. Kwa hakika minong’ono hiyo inatokana na Shetani ili awahuzunishe walioamini, na wala hatawadhuru chochote ila kwa idhini ya Mwenyezi Mungu. Basi waumini wamtegemea Mwenyezi Mungu. Basi waumini wamtegemee Mwenyezi Mungu.

KUNONG’ONEZANA

Aya 5 – 10

MAANA

Hakika wanaopingana na Mwenyezi Mungu na Mtume wake, watad­halilishwa kama walivyodhalilishwa wale waliokuwa kabla yao.

Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kutaja mipaka yake, sasa anampa onyo yule atakayeipetuka mipaka na akampa sifa ya adui wa Mwenyezi Mungu na Mtume wake na kwamba adhabu yao ni kushindwa na hizaya; kama ilivyokuwa adhabu ya umma zilizotangulia.

Na tulikwishateremsha Ishara zilizo wazi. Na makafiri watapata adhabu ifedheheshayo.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) amesimamisha hoja waziwazi za kuweko Yeye na unabii wa mjumbe wake(s.a.w. w ) na akabainisha halali na haramu. Dalili hizi zinafahamisha kuwa kumtii Mwenyezi Mungu na Mtume ni wajibu na

kwamba mwenye kuhalifu anastahili adhabu itakayomfedhehesha,siku atapowafufua Mwenyezi Mungu, na awaambie yale waliyoyatenda. Mwenyezi Mungu ameyadhibiti, na wao wameyasahau! Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kushuhudia kila kitu.

Kesho Mwenyezi Mungu atawakusanya kwa ajili ya hisabu na malipo kwa yale walioyafanya. Mkosefu akisahau madhambi Alioyafanya yote au baadhi yake, Mwenyezi Mungu anakuwa ameyajua yote na atamfedhehe­sha nayo na kumwonjesha adhabu kwa haki na uadilifu wala hatadhulumiwa.

Kwani huoni kwamba Mwenyezi Mungu anajua vilivyo katika mbin­gu na vilivyo katika ardhi?

Hujui ewe Muhammad kwamba kwa Mwenyezi Mungu hakifichiki chochote mbinguni na ardhini. Vile vile anajua kuwaHauwi mnong’ono wa watu watatu ila Yeye huwa ni wa nne wao, wala wa watano ila Yeye huwa ni wa sita wao. Wala wa wachache kuliko hao, wala walio wengi zaidi, ila Yeye yuko pamoja nao popote pale walipo. Kisha Siku ya Kiyama atawaambia waliyoyatenda.

Kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: ‘wala wachache kuliko hao,’ ni ishara ya chini ya watatu, na ‘wala walio wengi zaidi,’ ni zaidi ya watano. Kundi la wafasiri wamesema kuwa watu katika mayahudi na wanafiki walikuwa wakikutana kupanga njama dhidi ya Mtume na maswahaba wake, ndio ikawashukia Aya hii.

Hili haliko mbali, kwa sababu dhahiri ya Aya inalitilia nguvu, pia mazowea ya hali. Kwani kusengenya na siri ni mazowea ya wanafiki kila wakati na kila mahali.

Vyovyote iwavyo, maana ni kuwa, usihofu ewe Muhammad njama zao kwako na kwa maswahaba wako! Utahofia nini nawe una yakini kwamba Mwenyezi Mungu anajua siri na dhahiri na minong’ono ya wenye kujificha wawe wachache au wengi? Vile vile unajua kuwa atawakusanya siku ya Kiyama na kuwaadhibu kwa yale waliyokuwa wakiyafanya?

Makusudio ya kutaja tatu na tano ni kiasi cha kutoa mfano tu.Hakika Mwenyezi Mungu ni Mjuzi wa kila kitu, hata kutingishika mdomo na kurudia maneno.

Kwani huwaoni wale waliokatazwa kunong’ona, kisha wakayarudia yale waliyokatazwa, na wakanong’onezana juu ya mambo ya dhambi, na ya uadui, na ya kumwasi Mtume?

Hii inaashiria kwamba Mtume(s.a.w. w ) alikuwa amewanasihi wale wenye kujifichaficha na minong’ono kuwa wakome wala wasirudie, lakini hawakukubali, bali walirudia kwa jeuri na inadi. Basi Mwenyezi Mungu akawakaripia kwa tamko la kushangaa alilomwelekezea Mtume wake mtukufu; kama unavyomwambia mwenzako: Unamuona huyu asivyokuwa na adabu?

Na wakikujia hukuamkia sivyo anavyokuamkia Mwenyezi Mungu.

Kuna riwaya kuwa watu katika mayahudi waliingia kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w. w ) wakamwamkia: “Assaamu alayka ya Abalqasim” wakimaanisha mauti yakufikie ewe babake Kasim. Mtume naye akawajibu: “Waalykum!” na juu yenu pia. Ndio ikashuka Aya hii.

Sisi hatuna shaka na usahihi wa riwaya hii, kwa sababu inasadikisha zaidi ukosefu wa adabu wa mayahudi na chuki yao kwa haki na watu wake.

Na husema katika nafsi zao: Mbona Mwenyezi hatuadhibu kwa haya tuyasemayo?

Walifanya hivi kisha wakasema: Lau Muhammad angelikwa Nabii basi Mwenyezi Mungu angelituteremshia adhabu kwa jeuri tuliyomfanyia Nabii wake.

Jahannamu itawatosha; wataingia humo! Ni marejeo mabaya sana.

Msiwe na haraka na hali itakayokuwa, kwani Mwenyezi Mungu (s.w.t) amewaandalia Jahannam ambayo ni marejeo mabaya kabisa na kwamba kesho kuanzia leo ni karibu.

Enyi mlioamini! Mnaponong’onezana msinong’onezane kwa sababu ya mambo ya madhambi, na uadui, na kumuasi Mtume. Bali nong’onezaneni kwa kutenda mema na takua. Na mcheni Mwenyezi Mungu ambaye kwake mtakusanywa.

Watu wengi huwa wanamwamini Mwenyezi Mungu, wakafunga kwa ajili yake na wakaswali kiukweli na haki si kwa uongo wala ria, lakini mara nyingi wanasahau imani hii na wakanong’ona kwa mambo ya dhambi, sawa na wanavyofanya wanafiki na makafiri.

Maneno katika Aya hii yanaelekezwa kwa hawa walioghafilika na imani yao; na Mwenyezi Mungu (s.w.t) akawaamuru wanong’one kwa mambo ya heri, kwani hilo ndio laiki ya waumini; hawanong’onezani kwa shari kama makafiri na wanafiki.

Kama kwamba Aya hii imezishukia baadhi ya dola zinazojionyesha kuwa ni za kiislamu huku zikiwasaidia waisrail na kuwasheheneza aina kwa aina za silaha ili wawaue wanawake na watoto wadogo; wavunje majumba na kuwafukuza wakazi wake kutoka kwenye miji yao. Ni unafiki gani mkub­wa zaidi ya mtu kudai kuwa yeye ni mwislamu anayemwamini Mwenyezi Mungu na siku ya mwisho na huku anasaidiana na maadui wa Mwenyezi Mungu na wa utu; tena anapongeza dhulma na unyanyasaji?

Mwenyezi Mungu (s.w.t) amewakataza waumini kusaidiana na madhalimu hata kama ni kwa neno la siri, na akawaamuru kupambana nao kwa kauli na vitendo kwa siri na kwa jahara.

Kwa hakika minong’ono hiyo inatokana na Shetani ili awahuzunishe walioamini, na wala hatawadhuru chochote ila kwa idhini ya Mwenyezi Mungu.

Makusudio ya minong’ono hapa ni minong’ono ya shari na ya dhambi. Maana ni kuwa shetani anawahadaa wafuasi wake kwa minon’ono miovu kwa kukusudia kuwaudhi waumini na kuwahuzunisha, lakini waumini wako katika ngao madhubuti hayawapati madhara yoyote isipokuwa kwa idhini ya Mwenyezi Mungu.

Basi waumini wamtegemee Mwenyezi Mungu tu katika mambo yao yote wala wasiogope madhara kutoka kwa yoyote au kungojea manufaa isipokuwa kutoka kwake Mwenyezi Mungu Mtukufu tu. Na mwenye kumtegemea shetani atamwongoza kwenye maangamizi.

2

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا إِذَا قِيلَ لَكُمْ تَفَسَّحُوا فِي الْمَجَالِسِ فَافْسَحُوا يَفْسَحِ اللَّـهُ لَكُمْ وَإِذَا قِيلَ انشُزُوا فَانشُزُوا يَرْفَعِ اللَّـهُ الَّذِينَ آمَنُوا مِنكُمْ وَالَّذِينَ أُوتُوا الْعِلْمَ دَرَجَاتٍ وَاللَّـهُ بِمَا تَعْمَلُونَ خَبِيرٌ ﴿١١﴾

11. Enyi mlioamini! Mkiambiwa: fanyeni nafasi katika vikao, basi fanyeni nafasi. Na Mwenyezi Mungu atawafanyia nafasi. Na mki­ambiwa: ondokeni, basi ondokeni. Mwenyezi Mungu atawainua daraja walioamini miongoni mwenu, na waliope­wa ilimu. Na Mwenyezi Mungu kwa mnayoyatenda anazo habari.

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا إِذَا نَاجَيْتُمُ الرَّسُولَ فَقَدِّمُوا بَيْنَ يَدَيْ نَجْوَاكُمْ صَدَقَةً ذَٰلِكَ خَيْرٌ لَّكُمْ وَأَطْهَرُ فَإِن لَّمْ تَجِدُوا فَإِنَّ اللَّـهَ غَفُورٌ رَّحِيمٌ ﴿١٢﴾

12. Enyi mlioamini! Mnapo­nong’onezana na Mtume, basi tangulizeni sadaka kabla ya kunong’ona kwenu. Hiyo ni kheri kwenu na usafi zaidi. Na ikiwa hamkupata cha kutoa, basi Mwenyezi Mungu ni Mwingi wa maghufira, Mwenye kurehemu.

أَأَشْفَقْتُمْ أَن تُقَدِّمُوا بَيْنَ يَدَيْ نَجْوَاكُمْ صَدَقَاتٍ فَإِذْ لَمْ تَفْعَلُوا وَتَابَ اللَّـهُ عَلَيْكُمْ فَأَقِيمُوا الصَّلَاةَ وَآتُوا الزَّكَاةَ وَأَطِيعُوا اللَّـهَ وَرَسُولَهُ وَاللَّـهُ خَبِيرٌ بِمَا تَعْمَلُونَ ﴿١٣﴾

13. Mnachelea kutanguliza hiyo sadaka kabla ya kunong’ona kwenu? Ikiwa hamkufanya hayo, na Mwenyezi Mungu akapokea toba yenu, basi simamisheni Swala, na toeni Zaka, na mtiiini Mwenyezi Mungu na Mtume wake. Na Mwenyezi Mungu ana habari kwa mnayoyatenda.

FANYENI NAFASI MWENYEZI MUNGU ATAWAFANYIA NAFASI

Aya 11 – 13

MAANA

Enyi mlioamini! Mkiambiwa: fanyeni nafasi katika vikao, basi fanyeni nafasi. Na Mwenyezi Mungu atawafanyia nafasi.

Maswahaba walikuwa wakiwahi kwenye vikao vya Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w. w ) na wakipupia kuwa karibu naye. Mara nyingi vikao vilikuwa na msongamano wa watu. Aliyewahi hakuwa akimpa nafasi anayekuja, basi analazimika kurudi au kukalia nyayo zake. Ndio Mwenyezi Mungu (s.w.t) akawafundisha adabu ya kiislamu; Akawaamuru kuwapa nafasi wengine kwenye vikao na akawaahidi kuwapa nafasi Peponi.

Na mkiambiwa: ondokeni, basi ondokeni.

Kwanza Mwenyezi Mungu (s.w.t) aliwaamuru waliokaa wawatengenezee nafasi wengine; kisha akawaamuru kumsikiliza Mtume(s.a.w. w ) akiwataka kuachia nafasi wengine ikiwa nafasi haitoshi.

Kuna riwaya inayosema kuwa Mtume(s.a.w. w ) alikuwa akiwasimamisha baadhi ili wakae wale waliotangulia kwenye mambo mema, na ikawa wengine wanaonyesha kuchukia kwenye nyuso zao. Lakini baada ya kushuka Aya hii walifanya heshima na kuwapisha ndugu zao kwa moyo safi kabla ya kuamuriwa na Mtume(s.a.w. w ) .

Kuna tafsiri nyingine zinazosema kuwa maana ni: mkiambiwa ondokeni kwenda kwenye mambo ya heri basi itikieni. Hili haliko mbali, kwa sababu amri inaenea kwenye maana yote; iwe ni kutoa nafasi, kufanya jihadi au mengineyo.

Ndio! Katika adabu za Qur’an ni mtu kumfanyia nafasi ndugu yake au kumpisha pale alipokaa yeye, lakini sio adabu wala maadili mema kwa yule aliyekuja kumwondoa mahali pake yule aliyekaa.

Mtume(s.a.w. w ) alikuwa akikaa mwisho walipokaa watu, ila ikiwa mwenye kikao atamtaka mtu ampishe ndio anamwitikia, lakini vile vile haitakikani kwa mwenye kikao kumwondoa mtu isipokuwa kwa sababu ya maana; kama vile aliyekaa kukikosea adabu kikao au ikiwa aliyekuja ana shani na daraja mbele ya Mwenyezi Mungu. Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema:

Mwenyezi Mungu atawainua daraja walioamini miongoni mwenu, na waliopewa ilimu. Na Mwenyezi Mungu kwa mnayoyatenda ana habari.

Mwenyezi Mungu anawajua watu bora na anajua daraja za ubora naye anampa kila mwenye fadhila haki yake. Bora zaidi katika watu ni yule aliye zaidi kujichunga na aliyoyaharimisha Mwenyezi Mungu. Ikiwa pamoja na kujichunga hivi ana mwamko na ilimu basi atakuwa juu ya walio juu.

Hakuna mwenye shaka kwamba kumwadhimisha aliyeadhimishwa na Mwenyezi Mungu ni faradhi ya lazima. Kuna Hadith inayosema kuwa Mtume alikuwa akiwatukuza watu wa Badr na kuwatanguliza juu ya wengine. Siku moja waliingia baadhi yao kwenye majilisi yake wakakuta watu wamesongamana kwake wala hakuna yeyote aliyewapisha.

Mtume(s.a.w. w ) akawaambia wale waliokaribu yake: ni nani ambaye si katika watu wa Badr. Simama ewe fulani na wewe ewe fulani, na akawakalisha watu wa Badr.

Riwaya hii inaafikiana na kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: “Mwenyezi Mungu atawainua daraja walioamini miongoni mwenu…”

KUKAA MBELE KWENYE KIKAO

Mimi ninaposoma makala ya gazeti inayofungamana na maudhui ya Aya yoyote katika Qur’an Tukufu huwa ninaiweka kwenye faili maalum, mpaka nikifikia kuifasiri basi ninairudia ile makala na kuitolea ushahidi.

Pia huwa ninaashiria jina la gazeti na tarehe yake, kwa sababu kizazi kipya wanakinaika na magazeti zaidi kuliko rejea nyingine; kwa mfano kama kwenye Juz. 13 (13:5-7) kifungu cha ‘wanaoamini maada na maisha baada ya mauti.’ Juz. 15 (17: 82-85), kfungu cha: ‘Mwenyezi Mungu na ilimu ya chembe hai,’ Juz. 23 (38: 65-88), kifungu cha: Uislamu na msichana wa kiingereza,’ na Juz. 24 (41:37-46) kifungu cha ‘safari ya mwezini.’

Basi siku moja nilisoma mojawapo ya majarida ya wanasiasa wakubwa kuhusu meza ya maelewano kuwa ni nani atakayekaa mbele, ni nani atakayekuwa nyuma na ni ujumbe upi utatangulia kwenye chumba cha mkutano kabla ya mwingine.

Katika mfano alioutoa mwandishi ni ule wa mwaka 1945 baada ya vita ya pili ya dunia: Waliafikiana Churchill, Stalin na Roosevelt kukutana kwa majadiliano ya mapatano mjini Budabest, lakini wakatofautiana kuwa ni nani atakayeingia kwanza kwenye ukumbi wa mkutano. Ubishi huu uliendelea kwa muda kisha suluhisho likawa wakutane kwenye ukumbi wenye milango mitatu ili wote waingie kwa wakati mmoja.

Nimeikumbuka makala hiyo na kuileta hapa ili aone msomaji kuwa Uislamu unaipa kipaumbele ilimu na ikhlasi. Haya ndio maendeleo ya haki na uadilifu kwa maana yake sahihi, lakini kuwatukuza wanaotengeneza mauti, wanaomiliki makombora ya Menotman na CC, na silaha nyingine­zo za maangamizi, hakuna uzito wowote isipokuwa katika sharia ya shetani na maendeleo ya vita na uchokozi.

Enyi mlioamini! Mnaponong’onezana na Mtume, basi tangulizeni sadaka kabla ya kunong’ona kwenu. Hiyo ni kheri kwenu na usafi zaidi. Na ikiwa hamkupata cha kutoa, basi Mwenyezi Mungu ni Mwingi wa maghufira, Mwenye kurehemu.

Sioni tafsiri nzuri zaidi ya Aya hii kuliko ile ya Muqatil bin Hayan, ali­posema: “Matajiri waliwazidi mafukara kwenye vikao vya Mtume(s.a.w. w ) - hii ndio hali yao kila mahali na kila wakati - wakazidisha kum­nong’oneza Mtume mpaka akachukia kukaa kwao sana, ndio Mwenyezi Mungu akaamuru sadaka.

Basi matajiri wakajizuia kutoa na mafukara wakakosa cha kutoa, wakamlilia hali Mtume na kutamani kutoa lau wan­gelikua nacho na kukifikisha kwenye vikao vya Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w. w ) . Hapo daraja ya mafukara ikazidi, mbele ya Mwenyezi

Mungu na daraja ya matajiri ikaanguka.” Katika tafsiri kadhaa ikiwemo Tafsiru ttabari na Tafsiru rrazi imeelezwa kuwa hakuifanyia kazi Aya hii isipokuwa Ali bin Abu Twalib(a.s ) . Alikuwa na dinar moja akaivunja zikawa dirham 10, akawa kila anapotaka kusemezana na Mtume hutoa sadaka dirhamu moja. Kisha hukumu hiyo ikaondolewa kabla ya kuitekeleze mwingine asiyekuwa Ali.

Mwenye Tafsir Ruhulbayan anasema: “Imepokewa kutoka kwa Imran kuwa Yeye amesema: Imepokewa kutoka kwa Abdallah bin Imran kuwa amesema: Ali alikuwa na mambo matatu, lau ningelikuwa na mojawapo kati ya hayo ingelikuwa bora kwangu kuliko wanyama wekundu: Kumuoa Fatima, kupewa bendera siku ya Khaybar na Aya ya mnong’ono.”

Mnachelea ufukara kuwa hamtaweza kutanguliza hiyo sadaka kabla ya kunong’ona kwenu? Ikiwa hamkufanya hayo, na Mwenyezi Mungu akapokea toba yenu, basi simamisheni Swala, na toeni Zaka, na mtiii­ni Mwenyezi Mungu na Mtume wake.

Ilipokuwa uzito kwa matajiri kutoa sadaka kwa kuhofia kuisha mali yao, na Mwenyezi Mungu akalijua hilo, na wakajua kuwa wakati wa Mtume sio wao peke yao tu, ni wakufikisha ujumbe na kupanga mambo ya Waislamu, ndio Mwenyezi Mungu akaruhusu kunong’ona na Mtume bila ya kutoa sadaka na akawasamehe wale wasiotoa, lakini wasizembee swala, Zaka na mengineyo.

Na Mwenyezi Mungu ana habari za mnayoyatenda.

Haufichiki kwake wema wa mwenye kufanya wema na uovu wa mwenye kufanya uovu na atamlipa kila mmoja stahiki yake.

أَلَمْ تَرَ إِلَى الَّذِينَ تَوَلَّوْا قَوْمًا غَضِبَ اللَّـهُ عَلَيْهِم مَّا هُم مِّنكُمْ وَلَا مِنْهُمْ وَيَحْلِفُونَ عَلَى الْكَذِبِ وَهُمْ يَعْلَمُونَ ﴿١٤﴾

14. Huwaoni wale waliofanya urafiki na watu ambao Mwenyezi Mungu amewa­kasirikia? Hao si katika nyinyi, wala si katika wao. Na huapa kwa uwongo, na hali ya kuwa wanajua.

أَعَدَّ اللَّـهُ لَهُمْ عَذَابًا شَدِيدًا إِنَّهُمْ سَاءَ مَا كَانُوا يَعْمَلُونَ ﴿١٥﴾

15. Mwenyezi Mungu amewaan­dalia adhabu kali. Kwa haki­ka waliyokuwa wakiyatenda ni maovu kabisa.

اتَّخَذُوا أَيْمَانَهُمْ جُنَّةً فَصَدُّوا عَن سَبِيلِ اللَّـهِ فَلَهُمْ عَذَابٌ مُّهِينٌ ﴿١٦﴾

16. Wamefanya viapo vyao ni ngao, na wakaipinga Njia ya Mwenyezi Mungu. Basi wata­pata adhabu ifedheheshayo.

لَّن تُغْنِيَ عَنْهُمْ أَمْوَالُهُمْ وَلَا أَوْلَادُهُم مِّنَ اللَّـهِ شَيْئًا أُولَـٰئِكَ أَصْحَابُ النَّارِ هُمْ فِيهَا خَالِدُونَ ﴿١٧﴾

17. Haitawafaa kitu mali yao wala watoto wao kwa Mwenyezi Mungu, na wao ndio watu wa motoni, wao watadumu humo.

يَوْمَ يَبْعَثُهُمُ اللَّـهُ جَمِيعًا فَيَحْلِفُونَ لَهُ كَمَا يَحْلِفُونَ لَكُمْ وَيَحْسَبُونَ أَنَّهُمْ عَلَىٰ شَيْءٍ أَلَا إِنَّهُمْ هُمُ الْكَاذِبُونَ ﴿١٨﴾

18. Siku atakayowafufua Mwenyezi Mungu wote, wamuapie kama wanavyo­waapia nyinyi. Na watadhani kuwa wamepata kitu! Ehe! Kwa hakika hao ndio waon­go.

اسْتَحْوَذَ عَلَيْهِمُ الشَّيْطَانُ فَأَنسَاهُمْ ذِكْرَ اللَّـهِ أُولَـٰئِكَ حِزْبُ الشَّيْطَانِ أَلَا إِنَّ حِزْبَ الشَّيْطَانِ هُمُ الْخَاسِرُونَ ﴿١٩﴾

19. Shetani amewatawala na akawasahaulisha dhikr ya Mwenyezi Mungu. Hao ndio kundi la Shetani. Ehe! hakika kundi la Shetani ndilo lenye kuhasirika.

WAMEFANYA VIAPO VYAO NI NGAO

Aya 14 – 19

MAANA

Huwaoni wale waliofanya urafiki na watu ambao Mwenyezi Mungu amewakasirikia? Hao si katika nyinyi, wala si katika wao. Na huapa kwa uwongo, na hali ya kuwa wanajua.

Maneno yanaelekezwa kwa Mtume(s.a.w.w) . Waliofanya urafikki ni wanafiki, waliokasirikiwa na Mwenyezi Mungu ni mayahudi na nyinyi, ni nyinyi waislamu. Maana ni kuwa hebu niambie ewe Muhammad kuhusu wanafiki! Wamefanya urafiki na mayahudi na wakapanga njama nao dhidi ya waislamu na uislamu; wakiwa na uhakika kuwa wao si waisalamu wala si katika mayahudi, ni vizabizabina, huku hawako wala kule hawako.

Wameapa kwa kukusudia uwongo kuwa ni waislmu na kwamba hawakuse­ma kitu wala kupanga njama na mayahudi. Kwa ajili ya unafiki wao na viapo vyao vya uwongo,Mwenyezi Mungu amewaandalia adhabu kali. Kwa hakika waliyokuwa wakiyatenda ni maovu kabisa . Kila mwenye kudhihirisha kinyume na yaliyo kwenye dhamiri yake basi ni muovu kwa kauli yake na vitndo vyake, kwa sababu amejitoa kwenye dhati yake na hakika yake.

Wamefanya viapo vyao ni ngao, na wakaipinga Njia ya Mwenyezi Mungu. Basi watapata adhabu ifedheheshayo.

Yaani wanafiki wanajaribu kufanya njama zao kwa viapo vya uwongo na kujikinga navyo; huku wakiwahadaa wale wanaotaka uongofu na kuwazuia na malengo yao, lakini Mwenyezi Mungu hafichwi na kinga yoyote wala dhamiri zozote. Basi ameipasua sitara yao duniani, na Akhera watapata adhabu ya kufedhehesha.

Haitawafaa kitu mali yao wala watoto wao kwa Mwenyezi Mungu, na wao ndio watu wa motoni, wao humo watadumu.

Walipata fursa katika maisha ya duniani, lakini wakaichezea, wala hakuna kitu kwa yule mwenye kuvuta muda na kupuuza isipokuwa adhabu. Na si mali wala watoto inayoweza kurudisha yaliyopita.

Imetangulia kwa herufi zake katika Juz. 4 (3:116).

Siku atakayowafufua Mwenyezi Mungu wote, wamuapie kama wanavyowaapia nyinyi. Na watadhani kuwa wamepata kitu! Ehe! Kwa hakika hao ndio waongo.

Siku ya Kiyama, waja watakuwa na hali mbalimbali; kuna wengine watahurusiwa kuzungumza. Basi Mwenyezi Mungu atakapowapa fursa ya kuzungumza, wakosefu, watamuapia kwa uwongo, kama walivyokuwa wakimwapia Nabii na waislamu duniani; wakiamini kuwa viapo vyao vitawakinga na adhabu. Vipi iwe hivyo na hali Mwenyezi Mungu anajua kuwa wao ni waongo katika imani zao na itikadi zao?

Umetangulia mfano wake katika Juz. 7 (6:22).

Shetani amewatawala na akawasahaulisha dhikr ya Mwenyezi Mungu.

Shetani wa matamanio aliwaita kwenye upotevu na ufisadi nao wakamwitikia, basi wakapofuka na uwongofu.

Hao ndio kundi la Shetani. Ehe! hakika kundi la Shetani ndilo lenye kuhasirika.

Kwa sababu, vyovyote vile iwavyo, mwenye kumfanya shetani ni kiongozi wake, atamwongoza kwenye kila uovu na maangamizi, iwe kesho au kesho kutwa; hata kama atajisheheni mabomu na makombora.

إِنَّ الَّذِينَ يُحَادُّونَ اللَّـهَ وَرَسُولَهُ أُولَـٰئِكَ فِي الْأَذَلِّينَ ﴿٢٠﴾

20. Hakika wanaompinga Mwenyezi Mungu na Mtume wake, hao ndio miongoni mwa madhalili wa mwisho.

كَتَبَ اللَّـهُ لَأَغْلِبَنَّ أَنَا وَرُسُلِي إِنَّ اللَّـهَ قَوِيٌّ عَزِيزٌ ﴿٢١﴾

21. Mwenyezi Mungu ameandika: Hapana shaka Mimi na Mitume wangu tutashinda. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye nguvu, Mwenye kushinda.

لَّا تَجِدُ قَوْمًا يُؤْمِنُونَ بِاللَّـهِ وَالْيَوْمِ الْآخِرِ يُوَادُّونَ مَنْ حَادَّ اللَّـهَ وَرَسُولَهُ وَلَوْ كَانُوا آبَاءَهُمْ أَوْ أَبْنَاءَهُمْ أَوْ إِخْوَانَهُمْ أَوْ عَشِيرَتَهُمْ أُولَـٰئِكَ كَتَبَ فِي قُلُوبِهِمُ الْإِيمَانَ وَأَيَّدَهُم بِرُوحٍ مِّنْهُ وَيُدْخِلُهُمْ جَنَّاتٍ تَجْرِي مِن تَحْتِهَا الْأَنْهَارُ خَالِدِينَ فِيهَا رَضِيَ اللَّـهُ عَنْهُمْ وَرَضُوا عَنْهُ أُولَـٰئِكَ حِزْبُ اللَّـهِ أَلَا إِنَّ حِزْبَ اللَّـهِ هُمُ الْمُفْلِحُونَ ﴿٢٢﴾

22. Hupati watu wanaomwamini Mwenyezi Mungu na Siku ya Mwisho kuwa wanapendana na wanaompinga Mwenyezi Mungu na Mtume wake, hata wakiwa ni baba zao, au wato­to wao, au ndugu zao, au jamaa zao. Hao ameandika katika nyoyo zao Imani, na amewapa nguvu kwa Roho itokayo kwake. Na atawaingiza katika mabustani yapiti­wayo na mito chini yake. Humo watadumu. Mwenyezi Mungu awe radhi nao, na wao wawe radhi naye. Hao ndio kundi la Mwenyezi Mungu. Ehe! Hakika kundi la Mwenyezi Mungu ndilo lenye kufanikiwa.

BILA SHAKA NITASHINDA MIMI NA MITUME WANGU

Aya 20 – 22

MAANA

Hakika wanaompinga Mwenyezi Mungu na Mtume wake, hao ndio miongoni mwa madhalili wa mwisho.

Aya hii ina mshabaha wa jibu la swali la kukisiwa, kwamba maadui wa Mwenyezi Mungu wanaishi wakiwa na nguvu ya maandalizi na idadi, wakiendelea kuwatesa watu wa Mwenyezi Mungu kwa mauaji na kuwa­torosha, vipi Mwenyezi Mungu anawapa muda na kuwapa nguvu?

Aya inajibu kuwa washari ndio viumbe dhalili zaidi kuanzia mwanzo hadi mwisho, kwa sababu mwisho wao ni hizaya na udhalili duniani na Akhera. Hapa duniani ni kuwa Mwenyezi Mungu anawaadhibu kwa mikono ya waliowema:

قَاتِلُوهُمْ يُعَذِّبْهُمُ اللَّـهُ بِأَيْدِيكُمْ وَيُخْزِهِمْ وَيَنصُرْكُمْ عَلَيْهِمْ وَيَشْفِ صُدُورَ قَوْمٍ مُّؤْمِنِينَ ﴿١٤﴾

“Piganeni nao, Mwenyezi Mungu awaadhibu kwa mikono yenu, na awa­fedheheshe, na awanusuru muwashinde na avipoze vifua vya kaumu ya waumin.” Juz. 10 (9:14).

Ama adhabu ya Akhera hiyo ni kali na ni kubwa zaidi.

Mwenyezi Mungu ameandika: Hapana shaka Mimi na Mitume wangu tutashinda. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye nguvu, Mwenye kushinda.

Ushindi utakuwa Akhera, na vile vile utakuwa duniani kwa upanga, adhabu ya kutoka mbinguni, hoja na dalili au kwa kudumu utajo.

Tazama Juz. 17 (38-41) kifungu cha: “Mwenyezi Mungu huwakinga walioamini.” Vile vile Juz. 26 (47:7).

Hupati watu wanaomwamini Mwenyezi Mungu na Siku ya Mwisho kuwa wanapendana na wanaompinga Mwenyezi Mungu na Mtume wake, hata wakiwa ni baba zao, au watoto wao, au ndugu zao, au jamaa zao.

Haiwezekani kabisa imani ichanganyike na mahaba ya makafiri. Itakuwaje hivyo na hali Mwenyezi Mungu ndiye Aliyesema:

مَّا جَعَلَ اللَّـهُ لِرَجُلٍ مِّن قَلْبَيْنِ فِي جَوْفِهِ ﴿٤﴾

“Mwenyezi Mungu hakumwekea mwanamume nyoyo mbili ndani yake.” Juz. 21 (33:4).

Kuna kauli mashuhuri kutoka kwa Imam Ali(a.s ) kuwa rafiki wa adui ni adui. Pia akasema: “Tulikuwa pamoja na Mtume(s.a.w.w) mapigano yakiendela kwa mababa, watoto, ndugu na jamaa. Kila msiba na shida haukutuzidisha isipokuwa imani na kuendelea kwenye haki na kusalimu amri.” Hayo tumeyazungumzia kwa ufafanuzi zaidi kwenye Juz.4 (3:28).

Hao ameandika katika nyoyo zao Imani, na amewapa nguvu kwa Roho itokayo kwake.

‘Hao’ ni ni wale ambao imani yao haiathiriki hata kwa mababa na mama zao. Maana ni kuwa Mwenyezi Mungu amethibitishia imani katika nyoyo za wenye ikhlasi na akawapa nguvu kwa hoja: “Mwenyezi Mungu huwaimarisha wale walioamini kwa kauli thabiti katika maisha ya dunia na katika Akhera.” Juz. 13 (14:27).

Na atawaingiza katika Mabustani yapitiwayo na mito chini yake. Humo watadumu. Mwenyezi Mungu awe radhi nao, na wao wawe radhi naye.

Maana ya Mwenyezi Mungu kumridhia mja wake ni kumpa fadhila zake, na maana ya mja kumridhia Mola wake ni kuridhia aliyompa. Ibn Al-ara­biy, anasema katika Futuhat: “Mwenyezi Mungu huridhia amali chache ya mja wake na wao wanaridhia thawabu chache walizopata kutoka kwa Mola wao, kwani kadiri Mwenyezi Mungu anavyotoa ni vichache kulingana na vilivyoko kwake.”

Lakini hivi alivyoviita vichache Ibn al-arabiy, ni vichache kwa Mwenyezi Mungu Mtufu na ni vingi kwa waja. Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema: “Ili amzidishie ziada nyingi.” Juz. 2 (2:245).

Hao ndio kundi la Mwenyezi Mungu. Ehe! Hakika Kundi la Mwenyezi Mungu ndilo lenye kufanikiwa.

Aya hii ni mkabala wa Aya 19 ya Sura hii tuliyo nayo inayosema: “Hao ndio kundi la Shetani. Ehe! hakika kundi la Shetani ndilo lenye kukhasirika.”

Kwa ufupi ni kuwa mtu kadiri atakavyokuwa na uwezo, lakini hawezi kuchanganya kumridhisha Mwenyezi Mungu na kuwaridhisha maadui wa Mwenyezi Mungu Mtukufu. Akiwaridhisha atakuwa amemghadhabisha Mwenyezi Mungu na akimridhisha Mungu atakuwa amewaghadhibisha maadui. Wao hawaridhii isipokuwa yule aliye katika hali yao, kwa ushahi­di wa kauli yake Mwenyezi Mungu Mtufu:

وَلَن تَرْضَىٰ عَنكَ الْيَهُودُ وَلَا النَّصَارَىٰ حَتَّىٰ تَتَّبِعَ مِلَّتَهُمْ ﴿١٢٠﴾

“Hawatakuwa radhi nawe Mayahudi wala Manaswara mpaka ufuate mila yao.” Juz. 1 (2:120).

Katika Hadith Mtume(s.a.w.w) anasema:“Ewe Mwenyezi Mungu usini­jaalie muovu wala fasiki kwangu, kwani nimekuta katika yale uliyatolea wahyi kuwa: “Hupati watu wanaomwamini Mwenyezi Mungu na Siku ya Mwisho kuwa wanapendana na wanaompinga Mwenyezi Mungu na Mtume wake.”

MWISHO WA SURA YA HAMSINI NA NANE: AL–MUJADALA

3

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE

Sura Ya Hamsini Na Tisa: Surat Al-Hashr. Imeshuka Madina. Ina Aya 24.

بِسْمِ اللَّهِ الرَّحْمَٰنِ الرَّحِيمِ

Kwa jina la Mwenyezi Mungu Mwingi wa rehema, Mwenye kurehemu.

سَبَّحَ لِلَّـهِ مَا فِي السَّمَاوَاتِ وَمَا فِي الْأَرْضِ وَهُوَ الْعَزِيزُ الْحَكِيمُ ﴿١﴾

1. Vinamsabihi Mwenyezi Mungu vilivyo katika mbingu na vilivyo katika ardhi. Na Yeye ndiye Mwenye nguvu, Mwenye hikima.

هُوَ الَّذِي أَخْرَجَ الَّذِينَ كَفَرُوا مِنْ أَهْلِ الْكِتَابِ مِن دِيَارِهِمْ لِأَوَّلِ الْحَشْرِ مَا ظَنَنتُمْ أَن يَخْرُجُوا وَظَنُّوا أَنَّهُم مَّانِعَتُهُمْ حُصُونُهُم مِّنَ اللَّـهِ فَأَتَاهُمُ اللَّـهُ مِنْ حَيْثُ لَمْ يَحْتَسِبُوا وَقَذَفَ فِي قُلُوبِهِمُ الرُّعْبَ يُخْرِبُونَ بُيُوتَهُم بِأَيْدِيهِمْ وَأَيْدِي الْمُؤْمِنِينَ فَاعْتَبِرُوا يَا أُولِي الْأَبْصَارِ ﴿٢﴾

2. Yeye ndiye Aliewatoa walioku­furu miongoni mwa Watu wa Kitabu katika nyumba zao wakati wa mkusanyiko wa kwanza. Hamkudhani kuwa watatoka, nao walidhani kuwa ngome zao zitawalinda na Mwenyezi Mungu. Lakini Mwenyezi Mungu aliwafikia kwa mahali wasipopatazamia, na akatia woga katika nyoyo zao. Wakawa wanazibomoa nyumba zao kwa mikono yao na mikono ya Waumini. Basi zingatieni enyi wenye busara!

وَلَوْلَا أَن كَتَبَ اللَّـهُ عَلَيْهِمُ الْجَلَاءَ لَعَذَّبَهُمْ فِي الدُّنْيَا وَلَهُمْ فِي الْآخِرَةِ عَذَابُ النَّارِ ﴿٣﴾

3. Na lau kuwa Mwenyezi Mungu asingeliwaandikia uhamisho, angeliwaadhibu katika dunia. Na katika Akhera watapata adhabu ya Moto.

ذَٰلِكَ بِأَنَّهُمْ شَاقُّوا اللَّـهَ وَرَسُولَهُ وَمَن يُشَاقِّ اللَّـهَ فَإِنَّ اللَّـهَ شَدِيدُ الْعِقَابِ ﴿٤﴾

4. Hayo ni kwa sababu walimpin­ga Mwenyezi Mungu na Mtume wake. Na mwenye kumpinga Mwenyezi Mungu, basi hakika Mwenyezi Mungu ni Mkali wa kuadhibu.

مَا قَطَعْتُم مِّن لِّينَةٍ أَوْ تَرَكْتُمُوهَا قَائِمَةً عَلَىٰ أُصُولِهَا فَبِإِذْنِ اللَّـهِ وَلِيُخْزِيَ الْفَاسِقِينَ ﴿٥﴾

5. Mtende wowote mlioukata au mliouacha umesimama vile vile juu ya mashina yake, basi ni kwa idhini ya Mwenyezi Mungu, na kwa kuwahizi mafasiki.

VINAMSABIHI MWENEYEZI MUNGU

Aya 1 – 5

KISA CHA BANI NADHIR KWA UFUPI

Aya hizi zinahusiana na ushindi wa Mtume(s.a.w.w) dhidi ya mayahudi wa Bani Nadhir. Hawa walikuwa wakiishi viungani mwa Madina. Mtume(s.a.w.w) alipohamia huko, aliwekeana nao mkataba wa amani. Waislamu walipowashinda Makuraishi vita vya Badr, Bani Nadhir walifurahi sana, lakini waliposhindwa kwenye vita vya Uhud walivunja makataba na waka­panga njama za kummaliza Mtume na kiongozi wao, Kaa’b bin Ashraf akaungana na Abu Sufyan dhidi ya Nabii(s.a.w.w) .

Inasemekana kuwa Kaa’b alimshambulia Mtume kwa mashairi, Mtume akamwamuru mmoja wa maswahaba zake kumuua. Kisha Mtume(s.a.w.w) akawaendea Bani Nadhir na akawaamuru kutoka Madina, lakini wanafiki wakiongozwa na Abdallah bin Ubayya, waliwatumia ujumbe kuwa msikubali, sisi tuko pamoja nanyi. Basi wakawa na matumaini na wakashikilia kupigana. Hapo Mtume akawahusuru kwa muda wa siku 21, kama yanavyosema baadhi ya mapokezi.

Mtume(s.a.w.w) aliamuru kukatwa baadhi ya mitende yao. Hakuna yeyote katika wanafiki aliyejaribu kuwasaidia. Basi wakalazimika kusalimu amri, na Mtume akasuluhishana nao kuwa watoke Madina; kila watu watatu wachukue ngamia mmoja atakayewabebea wanachotaka. Basi wakakubali na wakatoka Madina kabisa.

Sura hii imewashukia wao. Ibn Abas alikuwa akiita Sura hii Sura ya Bani Nadhir.

MAANA

Vinamsabihi Mwenyezi Mungu vilivyo katika mbingu na vilivyo kati­ka ardhi. Na Yeye ndiye Mwenye nguvu, Mwenye hikima.

Vitu vyote vilivyoko vinamsabihi (vinamtakasa) na kutukuza uweza wake Mwenyezi Mungu na hekima yake, kwa lugha ya maneno na lugha ya hali. Umetangulia mfano wake katika Juz. 27 (57:1).

Yeye ndiye Aliyewatoa waliokufuru miongoni mwa Watu wa Kitabu katika nyumba zao wakati wa mkusanyiko wa kwanza.

Makusudio ya waliokufuru hapa ni Bani Nadhir. Wametofautiana wafasiri kuhusu mkusanyiko wa kwanza. Razi anasema: “Ibn Abbas na wafasiri wengi wamesema kuwa maana ya mkusanyiko wa kwanza ni kuwa hiyo ilikuwa ni mara ya kwanza kwa watu wa Kitab kutolewa Bara Arabu. Kabla yake walikuwa na nguvu… Hili haliko mbali kwa sababu kutolewa kwa pili kulitokea kwa khalifa wa pili.

Maana ni kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) aliwatoa Bani Nadhir kupitia mikononi mwa waislamu. Na hii ilikuwa ni mara ya kwanza kutolewa watu wa Kitabu huko. Na sababu ya kutolewa kwao ni hiyana yao na kuvunja kwao mapatano ya amani waliyowekeana na Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) wao wenyewe.

Unaweza kuuliza : Kwanini Mwenyezi Mungu aliwaadhibu kwa kuwatoa na kuchukua mali yao na kuna aina nyingine za kuwaadhibu?

Jibu : Aliwachukulia kwa sharia ya dini yao. Tawrat yao inasema: “Utakaposongea karibu ya mji kwenda kupigana juu yake, ndipo utakapowapigia ukelele wa amani.

Itakuwa utakapokujibu kwa amani, na kukufungulia, ndipo watu wote watakaoonekana humo, watafanya kazi ya shoka, na kukutumikia. Na kama hautaki kufanya amani nawe, lakini utafanya vita juu yako, ndipo uhusuru; na Bwana, Mungu wako, autiapo mkononi mwako, mpige kila mume aliyemo kwa makali ya upanga; lakini wanawake na watoto na wanyama wa mji, na vilivyo mjini vyote, navyo ni nyara zake zote, uvitwae viwe mateka; nawe utakula nyara za adui zako alizokupa Bwana, Mungu wako” (Kumbukumbu 20:10 -14).

Hakuna mwenye shaka kwamba mwenye kufuata dini au misingi hana budi kufuata hukumu zake zote na kuzitekeleza yeye mwenyewe kabla ya kutekelezea mwenginewe. Tena Nabii(s.a.w.w) aliwahurumia Bani Nadhir, kwa sababu hakuwaua wanaume wao wala kuwateka wanawake na watoto; kama ilivyo nukuu ya Tawrat yao.

Hayo tumeyazungumzia kwa ufafanuzi zaidi katika Juz. 21 (33: 16-20), kifungu cha ‘Je, Muhammad aliwadhulumu Bani Quraydha?’

Hamkudhani kuwa watatoka, nao walidhani kuwa ngome zao zitawalinda na Mwenyezi Mungu.

Yaani waislamu hawakutegemea kabisa kuwa Bani Nadhir watatoka majumbani mwao na kuwaachia maadui zao waislamu, kutokana na inadi yao na nguvu walizokuwa nazo kwa uwezo na idadi yao.

Vile vile Bani Nadhir walikuwa wakijiamini kuwa wana nguvu na uwezo kuwa ni ngome isiyoingiliwa na mkono wowote. Lakini ulikuwa ni uwezo na ngome ya khiyana, haiwezi kumlinda mwenye kuikimbilia.

PROPAGANDA ZA UPOTOFU NA WAKATI MNASABA

Lakini Mwenyezi Mungu aliwafikia kwa mahali wasipopatazamia, na akatia woga katika nyoyo zao.

Walidhani kuwa ngome zao zitawalinda, lakini Mwenyezi Mungu akatia hofu kwenye nyoyo zao baada ya kumjaza haiba Mtume(s.a.w.w) na jeshi lake. Basi ngome zao zikayayuka, kwa sababu nyoyo ndio msingi wa nguvu zote.

Ndio maana waovu na wafanyibiashara wa silaha wanafanya bidii sana kwenye vita vya nafsi na kutafuta nyenzo na pesa, lakini wame­sahau au wamejitia kusahau kuwa hakuna njia ya kuufikia moyo isipokuwa haki, kheri na hisani. Ikiwa propaganda za upotevu zitapata waungaji mkono basi ni kwa muda, kisha zinafichuka; hata kama muda utakuwa mrefu.

Aliulizwa Charles Mwigizaji maarufu wa tamthilia kuhusu mambo ya maisha: Mtu anahitaji nini ili aweze kutengeneza njia yake ya maisha? Akasema: “Jambo muhimu ni kujua wakati mnasaba.” Nasi tunamwambia Charles: “Ndio hakuna budi ya wakati, lakini ni lazima uwe unanasibiana na masilahi ya kheri sio ya shari, na ya haki sio ya batili. Kwa sababu shari inaondoka pamoja na watu wake, hata kama ni kuchelewa kwa kiasi gani.

Wakawa wanazibomoa nyumba zao kwa mikono yao na mikono ya Waumini.

Badhi ya wafasiri wamesema kuwa makusudio ya kubomoa nyumba ni kuziacha na kwa mikono yao ni kuwa wao ndio sababu ya kuondoka kwao; pale walipovunja maelewano na Mtume. Mikono ya waumini ni ishara ya kuwa waislamu ndio waliowatoa Bani Nadhir majumbani mwao.

Wafasiri wengine wakasema kuwa Bani Nadhir waliziharibu hasa nyumba zao ili zisibakie salama mikononi mwa waislamu, na kwamba waislamu walizipondaponda ngome za mayahudi ili wapate kuwafikia. Tafsiri hii iko karibu na maana na inatiwa nguvu na dhahiri ya Aya; wala haipingani na ile ya kwanza, bali ni natija ya kuondoka mji.

Basi zingatieni enyi wenye busara!

Kuzingatia kitu ni kukirudisha kwenye mtazamo na kukihukumu kwa mfano wake. Mwenyezi Mungu aliwatoa Bani Nadhir majumbani mwao yakiwa ni malipo ya hiyana yao. Basi mwenye akili anatakikana kupata somo na ajiepushe na hiyana na njama, ili yasimfike yaliyowafika.

Na lau kuwa Mwenyezi Mungu asingeliwaandikia uhamisho, angeli­waadhibu katika dunia. Na katika Akhera watapata adhabu ya Moto.

Mwenyezi Mungu amewaadhibu duniani kwa kuwahamisha kutoka majumbani mwao na lau si hivyo angeliwaadhibu kwa kuwaua; kama walivyofanywa Bani Quraydha. Na hawataepuka adhabu ya Moto.

Hayo ni kwa sababu walimpinga Mwenyezi Mungu na Mtume wake.

Walistahili adhabu ya dunia na Akhera, kwa sababu wao walimhalifu Mwenyezi Mungu, wakipituka mipaka yake, na kumwekea uadui Mtume wake.

Na mwenye kumpinga Mwenyezi Mungu, basi hakika Mwenyezi Mungu ni Mkali wa kuadhibu.

Hili ni onyo na kiaga kwa kila jabari mwenye kiburi.

Mtende wowote mlioukata au mliouacha umesimama vile vile juu ya mashina yake, basi ni kwa idhini ya Mwenyezi Mungu, na kwa kuwahizi mafasiki.

Mtume(s.a.w.w) alikuwa ameamrisha kukatwa baadhi ya mitende ya Bani Nadhir ili kuwakasirisha kwa hilo. Baadhi wakadhani kuwa hiyo ni aina ya uharibifu. Ndio Mwenyezi Mungu akabainisha kwamba kila liliotukia kati­ka kukatwa mitende au kuachwa ni kwa amri ya Mwenyezi Mungu na wala haitoki kwa Mtume(s.a.w.w) , na lengo ni kuwakasirisha makafiri kwa kuikata na pia kuwakasirisha kwa ile ilioachwa kwa vile watanufaika nayo wale wanaowaona ni maadui zao.

Ieleweke kuwa kukata miti na mengineyo wakati wa vita haifai kuchukuli­wa ni msingi maalum; inaweza kuwa ni wajibu na inaweza kuwa ni hara-mu, kulingana na masilahi ya kumpiga adui; sawa na yanavyovunjwa majumba kwa ajili ya kupitisha barabara, siku ambazo si za vita.

وَمَا أَفَاءَ اللَّـهُ عَلَىٰ رَسُولِهِ مِنْهُمْ فَمَا أَوْجَفْتُمْ عَلَيْهِ مِنْ خَيْلٍ وَلَا رِكَابٍ وَلَـٰكِنَّ اللَّـهَ يُسَلِّطُ رُسُلَهُ عَلَىٰ مَن يَشَاءُ وَاللَّـهُ عَلَىٰ كُلِّ شَيْءٍ قَدِيرٌ ﴿٦﴾

6. Na Aliyoleta Mwenyezi Mungu kwa Mtume wake kutoka kwao hamkuyaendea kwa farasi wala ngamia. Lakini Mwenyezi Mungu huwapa mamlaka Mitume wake juu ya wowote awatakao. Na Mwenyezi Mungu ni Muweza juu ya kila kitu.

مَّا أَفَاءَ اللَّـهُ عَلَىٰ رَسُولِهِ مِنْ أَهْلِ الْقُرَىٰ فَلِلَّـهِ وَلِلرَّسُولِ وَلِذِي الْقُرْبَىٰ وَالْيَتَامَىٰ وَالْمَسَاكِينِ وَابْنِ السَّبِيلِ كَيْ لَا يَكُونَ دُولَةً بَيْنَ الْأَغْنِيَاءِ مِنكُمْ وَمَا آتَاكُمُ الرَّسُولُ فَخُذُوهُ وَمَا نَهَاكُمْ عَنْهُ فَانتَهُوا وَاتَّقُوا اللَّـهَ إِنَّ اللَّـهَ شَدِيدُ الْعِقَابِ ﴿٧﴾

7. Aliyoleta Mwenyezi Mungu kwa Mtume wake kutoka kwa watu vijijini ni kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, na kwa ajili ya Mtume, na jamaa, na maya­tima, na masikini, na mwananjia, Ili yasiwe yakizunguka baina ya matajiri miongoni mwenu. Na anachowapa Mtume kichukueni, na ana­chowakataza jiepusheni nacho. Na mcheni Mwenyezi Mungu. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mkali wa kuadhibu.

لِلْفُقَرَاءِ الْمُهَاجِرِينَ الَّذِينَ أُخْرِجُوا مِن دِيَارِهِمْ وَأَمْوَالِهِمْ يَبْتَغُونَ فَضْلًا مِّنَ اللَّـهِ وَرِضْوَانًا وَيَنصُرُونَ اللَّـهَ وَرَسُولَهُ أُولَـٰئِكَ هُمُ الصَّادِقُونَ ﴿٨﴾

8. Wapewe mafukara wahajiri waliotolewa majumbani mwao na mali yao kwa ajili ya kutafuta fadhila kutoka kwa Mwenyezi Mungu na radhi zake, na wanamsaidia Mwenyezi Mungu na Mtume wake. Hao ndio wa kweli.

MALI ISIZUNGUKE KWA MATAJIRI

Aya 6–8

MAANA

Na Aliyoleta Mwenyezi Mungu kwa Mtume wake kutoka kwao hamkuyaendea kwa farasi wala ngamia.

Neno ‘Aliyoleta’ tumelifasiri kutokana na neno la kiarabu Fay’i ambalo ki lugha ya kiarabu lina maana ya kurejesha. Fay’i katika sharia ya kiislamu ni mali waliyoipata waislamu kutoka kwa makafiri bila ya vita. Na ghani­ma (ngawira) ni mali iliyopatikana kwa vita.

Vyovyote iwavyo ni kuwa Aya tuliyo nayo inahusika na mali ya Bani Nadhir. Kwa hiyo maana yanakuwa, mali ya Bani Nadhir ameijaalia ni nyara kwa Mtume wake kuifanyia anavyotaka, waislamu hawana chao hapo kwa vile hawakuitolea jasho lolote.

Lakini Mwenyezi Mungu huwapa mamlaka Mitume wake juu ya wowote awatakao.

Miongoni mwa mamlaka hayo ni kuwa Mwenyezi Mungu Mtukufu alitia hofu kwenye nyoyo za Bani Nadhir kutoka kwa Mtume(s.a.w.w) ili wasalimu amri yake wakiwa dhalili, bila ya vita.

Na Mwenyezi Mungu ni Muweza juu ya kila kitu.

Miongoni mwa hayo ni kudhalilika watu wenye nguvu, ngome na idadi, mbele ya mtumwa miongoni mwa watumwa wa Mwenyezi Mungu.

Aliyoleta Mwenyezi Mungu kwa Mtume wake kutoka kwa watu vijijini kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, na kwa ajili ya Mtume, na jamaa, na mayatima, na masikini, na mwananjia.

Makusudio ya watu wa vijiji hapa ni makafiri wengine wasiokuwa Bani Nadhir. Maana ni kuwa mali ya fay’i isiyokuwa ya Bani Nadhir ni ya Mwenyezi Mungu na Mtume. Mwananjia ni msafiri aliyekatikiwa njiani na kushindwa kurudi kwa watu wake.

Kimsingi ni kuwa mali ya Mwenyezi Mungu ni ya Mtume(s.a.w.w) . Wameafikiana kwa kauli moja, isipokuwa kidogo, kwamba makusudio ya jamaa ni jamaa wa Mtume(s.a.w.w) katika Bani Hashim. Ama kuhusu may­atima, masikini na mwananjia, Shia Imamiya wamesema kuwa wanahusi­ka wa Bani Hashim tu. Wengine wamesema ni yeyote awe Hashim au mwinginewe [1] .

Tumeyazungumzia hayo kwa ufafanuzi zaidi katika Juz. 10 (8:41).

Ili yasiwe yakizunguka baina ya matajiri miongoni mwenu.

Uislamu ni dini ya Mwenyezi Mungu kwa ajili ya watu, inachunga masi­lahi ya wote bila ya kuwabagua. Hautatui tatizo la mtu kwa gharama ya mwingine, wala haumkandamizi mtu ili kumnufaisha mwingine. Wote mbele ya uislamu ni sawasawa.

Haya yanajitokeza kwenye hukumu zake na misingi yake. Miongoni mwa misingi hiyo ni kuwa mali isizunguke kwa matajiri tu. Hiyo ni pamoja na kukataza riba, ghushi na unyonyaji.

Ieleweke kwamba hii haifahamishi kwa karibu wala umbali kuwa uislamu unakubaliana na siasa ya ujamaa au haukubali nayo. Ieleweke tu kuwa uis­lamu katika hukumu zake zote kunajengeka fikra ya uadilifu na usawa na unakubaliana na kila lenye heri ya watu na manufaa yao. Hili ni jambo jingine na kutaifisha mali za watu kuwa mali za uma ni jambo jingine.

Tazama Juz. 4 (3:180-182), kifungu cha: ‘Matajairi ni mawakala sio wenyewe.’

Na anachowapa Mtume kichukueni, na anachowakataza jiepusheni nacho. Na mcheni Mwenyezi Mungu. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mkali wa kuadhibu.

Aya hii imeunganisha baina ya kauli ya Mwenyezi Mungu na Mtume wake na ikawajibisha kuzisikiliza kauli zote mbili, kwa sababu kauli ya Mtume inatokana na wahyi kutoka kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu:

وَمَا يَنطِقُ عَنِ الْهَوَىٰ ﴿٣﴾ إِنْ هُوَ إِلَّا وَحْيٌ يُوحَىٰ ﴿٤﴾

“Wala hatamki kwa matamanio. Hayakuwa haya ila ni wahyi uliotolewa.” Juz. 27 (53:3-4).

Mwenyezi Mungu amesema katika Aya kadhaa: “Mtiini Mwenyezi Mungu na Mtume.”

Akasema tena:

وَمَن يَعْصِ اللَّـهَ وَرَسُولَهُ فَقَدْ ضَلَّ ضَلَالًا مُّبِينًا ﴿٣٦﴾

“Na yeyote mwenye kumwasi Mwenyezi Mungu na Mtume wake, basi amepotea upotevu ulio wazi.” Juz. 22 (33:36).

Zimekuja Hadith mutawatir kwamba Mtume hakuona ndoto yoyote ila ina­jitokeza kama asubuhi. Waislamu wameafikiana kwa kauli moja kuwa hakuna wahyi wala sharia au Ijtihadi baada ya Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) ila ikiwa kauli ya mujtahidi inatokana na sharia ya Mwenyezi Mungu na Mtume wake.

Tazama Juz. 22 (33: 36-40) kifungu cha: ‘kwani utume uliishia kwa Muhammad?’ na Juz. 27 (56: 75-96), kifungu cha ‘Uislamu na wanafikra wakuu wa Ulaya.’

Wapewe mafukara wahajiri waliotolewa majumbani mwao na mali yao kwa ajili ya kutafuta fadhila kutoka kwa Mwenyezi Mungu na radhi zake, na wanamsaidia Mwenyezi Mungu na Mtume wake.

Makusudio ya wahajiri hapa ni wale waliohama na Mtume kutoka Makka kwenda Madina kwa kutaka radhi za Mwenyezi Mungu na thawabu zake na katika kuusaidia Uislamu na kupigana jihadi katika njia yake. Hawa ndio waliofaa zaidi kupewa zaka kwa kutangulia kwao na juhudi yao na pia kuwa na haja nayo.

Anasema Tabari akinukuu kutoka kwa Qatada: “Wahajiri hawa waliacha majumba yao, mali na familia kwa kumpenda Mwenyezi Mungu na Mtume wake.

Wakachagua Uislamu pamoja na shida zake. Hali ilifikia mtu anafunga jiwe tumboni ili kuuzuia mgongo wake na njaa na kuchim­ba shimo wakati wa kipupwe kuwa ndio blanketi ya kujifunika.

Sijaona wasifu wa maswahaba uliokuwa fasaha zaidi kuliko aliousema Imam Zaynul-abidin(a.s) akiwa anawaombea Mwenyezi Mungu (s.w.t) awatakabalie matendo yao; kwa kusema:

“Ewe Mola! Hasa maswahaba wa Muhammad ambao walikuwa na usuhuba mzuri, wakawa na majaribu mema katika kumsaidia kwake. Wakamwitikia alipowaeleza hoja ya ujumbe wake. Wakapigana na mababa zao na watoto wao ili kuuthibisha unabii wake na wakashinda kupitia kwake. Waliozingirwa na mapenzi wakitarajia biashara isiyo na hasara kwa ajili ya kumpenda kwake.

Wakatengwa na jamaa zao waliposhikamana na kamba yake. Udugu ulikwisha walipotulia chini ya kivuli cha udugu wake. Basi ewe Mola usiwasahu kwa yale waliyoyaacha kwa ajili yako. Na uwa­ ridhie kwa radhi zako.”

Hao ndio wa kweli katika imani na jihadi yao, kwa kauli na vitendo.

4

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE

وَالَّذِينَ تَبَوَّءُوا الدَّارَ وَالْإِيمَانَ مِن قَبْلِهِمْ يُحِبُّونَ مَنْ هَاجَرَ إِلَيْهِمْ وَلَا يَجِدُونَ فِي صُدُورِهِمْ حَاجَةً مِّمَّا أُوتُوا وَيُؤْثِرُونَ عَلَىٰ أَنفُسِهِمْ وَلَوْ كَانَ بِهِمْ خَصَاصَةٌ وَمَن يُوقَ شُحَّ نَفْسِهِ فَأُولَـٰئِكَ هُمُ الْمُفْلِحُونَ ﴿٩﴾

9. Na waliofanya maskani na imani yao kabla yao, wanawapenda waliohamia kwao wala hawapati dhiki kati­ka vifua vyao kwa walivyope­wa, na wanawapendelea kuliko nafsi zao, ingawa wao wenyewe ni wahitaji. Na mwenye kue­pushwa na uchoyo wa nafsi yake, basi hao ndio wenye kufaulu.

وَالَّذِينَ جَاءُوا مِن بَعْدِهِمْ يَقُولُونَ رَبَّنَا اغْفِرْ لَنَا وَلِإِخْوَانِنَا الَّذِينَ سَبَقُونَا بِالْإِيمَانِ وَلَا تَجْعَلْ فِي قُلُوبِنَا غِلًّا لِّلَّذِينَ آمَنُوا رَبَّنَا إِنَّكَ رَءُوفٌ رَّحِيمٌ ﴿١٠﴾

10. Na waliokuja baada yao wanasema: Mola wetu! Tughufirie sisi na ndugu zetu waliotutangulia kwa Imani, wala usijaalie ndani ya nyoyo zetu undani kwa walioamini. Mola wetu! Hakika Wewe ni Mpole Mwingi wa rehema.

أَلَمْ تَرَ إِلَى الَّذِينَ نَافَقُوا يَقُولُونَ لِإِخْوَانِهِمُ الَّذِينَ كَفَرُوا مِنْ أَهْلِ الْكِتَابِ لَئِنْ أُخْرِجْتُمْ لَنَخْرُجَنَّ مَعَكُمْ وَلَا نُطِيعُ فِيكُمْ أَحَدًا أَبَدًا وَإِن قُوتِلْتُمْ لَنَنصُرَنَّكُمْ وَاللَّـهُ يَشْهَدُ إِنَّهُمْ لَكَاذِبُونَ ﴿١١﴾

11. Je, Huwaoni wanaofanya unafiki wanawaambia ndugu zao waliokufuru katika Watu wa Kitabu: Mkitolewa na sisi lazima tutatoka pamoja nanyi, wala hatutamtii yeyote kabisa dhidi yenu.

Na mkipig­wa vita lazima tutawasaidia. Na Mwenyezi Mungu ana­shuhudia kuwa hao hakika bila ya shaka ni waongo.

لَئِنْ أُخْرِجُوا لَا يَخْرُجُونَ مَعَهُمْ وَلَئِن قُوتِلُوا لَا يَنصُرُونَهُمْ وَلَئِن نَّصَرُوهُمْ لَيُوَلُّنَّ الْأَدْبَارَ ثُمَّ لَا يُنصَرُونَ ﴿١٢﴾

12. Wakitolewa hawatatoka pamoja nao na wakipigwa vita hawatawasaidia. Na kama wakiwasaidia basi watageuza migongo; Kisha hawatanusuriwa.

لَأَنتُمْ أَشَدُّ رَهْبَةً فِي صُدُورِهِم مِّنَ اللَّـهِ ذَٰلِكَ بِأَنَّهُمْ قَوْمٌ لَّا يَفْقَهُونَ ﴿١٣﴾

13. Hakika nyinyi ni tishio zaidi katika vifua vyao kuliko Mwenyezi Mungu. Hayo ni kwa kuwa hao ni watu wasio­fahamu.

لَا يُقَاتِلُونَكُمْ جَمِيعًا إِلَّا فِي قُرًى مُّحَصَّنَةٍ أَوْ مِن وَرَاءِ جُدُرٍ بَأْسُهُم بَيْنَهُمْ شَدِيدٌ تَحْسَبُهُمْ جَمِيعًا وَقُلُوبُهُمْ شَتَّىٰ ذَٰلِكَ بِأَنَّهُمْ قَوْمٌ لَّا يَعْقِلُونَ ﴿١٤﴾

14. Hawatapigana nanyi kwa mkusanyiko isipokuwa katika vijiji vilivyozatitiwa kwa ngome au nyuma ya kuta. Wao kwa wao vita vyao ni vikali. Utawadhania kuwa wako pamoja, kumbe nyoyo zao ni mbali mbali. Hayo ni kwa kuwa wao ni watu wasio na akili.

كَمَثَلِ الَّذِينَ مِن قَبْلِهِمْ قَرِيبًا ذَاقُوا وَبَالَ أَمْرِهِمْ وَلَهُمْ عَذَابٌ أَلِيمٌ ﴿١٥﴾

15. Ni kama mfano wa waliokuwa kabla yao hivi karibuni. Walionja ubaya wa mambo yao. Nao watapata adhabu iliyo chungu.

WANAWAPENDELEA KULIKO NAFSI ZAO

Aya 9 – 15

MAANA

Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kubainisha daraja ya wahajiri katika Aya iliyotangulia, sasa anabainisha daraja ya Answar, kwa kusema, kama ifuatavyo:-

Na waliofanya maskani na Imani yao kabla yao, wanawapenda waliohamia kwao.

Makusudio ya maskani hapa ni Madina. Maana ni kuwa Answar, wenyeji wa Madina, walimsaidia Mtume pamoja na wale waliohama naye. Wakajitolea kwa nafsi zao na mali zao; bali waliwapendela wao kuliko nafsi zao; kama itakavyoashiria Aya.

Miongoni mwa Aya zilizoshuka kwa ajili ya Answar ni:

وَالَّذِينَ آمَنُوا وَهَاجَرُوا وَجَاهَدُوا فِي سَبِيلِ اللَّـهِ وَالَّذِينَ آوَوا وَّنَصَرُوا أُولَـٰئِكَ هُمُ الْمُؤْمِنُونَ حَقًّا لَّهُم مَّغْفِرَةٌ وَرِزْقٌ كَرِيمٌ ﴿٧٤﴾

“Na wale waliokaribisha na kusaidia, hao ndio waumini kweli, wana wao maghufira na riziki njema.” Juz. 10 (8:74).

Wala hawapati dhiki katika vifua vyao kwa walivyopewa Wahajiri.

Mwanzoni Wahajiri walikuwa ni mafukara zaidi katika Madina wakipata tabu. Lau si Answar wangelikufa na njaa. Mtume(s.a.w.w) alikuwa akiwapa sadaka mafukara na hawapi matajiri na walio na uwezo wa kuchuma.

Kwa hiyo alikuwa akiwapa kipaumbele Wahajiri; mara nyingine akiwapa ngawira wao tu. Answar walikuwa wakiliridhia hilo bila ya kuona choyo wala dhiki nyoyoni, na wakiona ni haki kabisa. Ndio akasajili Mwenyezi Mungu (s.w.t) sifa zao hizi kwenye Kitabu chake.

Na wanawapendelea kuliko nafsi zao, ingawa wao wenyewe ni wahitaji.

Kumpendela mwingine kuliko nafsi yake mtu, akiwa na mahitaji, hakuwezi kulinganihswa na jambo lolote isipokuwa kujitolea mhanga. Imeelezwa katika vitabu vya Tafsir na Historia kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) aliwaambia Answar: “Mkipenda ngawira hii iwe baina yenu na Wahajiri, lakini mshirikiane nao katika mali yenu, au muwaachie ngawira na nyinyi mbaki na mali yenu. Answar wakasema: bali tutawaachia ngawira na tutashirikiana nao katika mali yetu ewe Mjumbe wa Mwenyezi Mungu. Hapo Mtume akawaombea dua na kusema: “Ewe Mwenyezi Mungu! Warehemu Answar na watoto wa Answar.”

Na mwenye kuepushwa na uchoyo wa nafsi yake, basi hao ndio wenye kufaulu.

Uchoyo ni mama wa maovu. Mwenye kuuitikia utamzuia na kila heri, na mwenye kuushinda kwenye nafsi yake basi atakuwa ameikinga na kila uovu na hatari.

Na waliokuja baada yao wanasema: Mola wetu! Tughufirie sisi na ndugu zetu waliotutangulia kwa Imani.

Yaani waliokuja baada ya Answar na Wahajiri. Makusudio ya waliokuja baada yao ni kila mwenye kufuata sera mpaka siku ya Kiyama, wala haku­na njia ya kuwahusisha Tabiina (waliowafuatia maswahaba). Kwa sababu linalozingatiwa ni matendo sio mahali fulani wala wakati. Maswahaba hawakufikia walipokuwa ila ni kwakuwa walisikilza kauli wakafuata mazuri yake.

Wala usijaalie ndani ya nyoyo zetu undani kwa walioamini.

Ni muhali kabisa kuwa pamoja imani na undani. Inawezekana mtu kujiwekea undani?

Mola wetu! Hakika Wewe ni Mpole Mwingi wa rehema kwa waja wako walioitakasa dini yao na nyoyo zao kutokana undani na unafiki.

Je, Huwaoni wanaofanya unafiki wanawaambia ndugu zao walioku­furu katika Watu wa Kitabu: Mkitolewa na sisi lazima tutatoka pamo­ja nanyi, wala hatutamtii yeyote kabisa dhidi yenu. Na mkipigwa vita lazima tutawasaidia.

Makusudio ya watu wa Kitab hapa ni Bani Nadhir, ndugu wa wanafiki katika ukafiri na uadui kwa Mtume. Aya inaashiria tukio maalum. Pale Mtume(s.a.w.w) alipotangaza vita dhidi ya Bani Nadhir, wanafiki wakion­gozwa na Abadallah bin Ubayya waliwaambia: piganeni na Muhammad na sisi tuko na nyinyi, akiwapiga nasi tutampiga na wakiwatoa Madina tuta­toka nanyi; hatutamsikiliza Muhammad wala mwenginewe.

Na Mwenyezi Mungu anashuhudia kuwa hao hakika bila ya shaka ni waongo kwenye kauli yao na ahadi yao.

Wakitolewa Bani Nadhirhawatatoka pamoja nao wanafiki,na wakipigwa vita hawatawasaidia. Na kama wakiwasaidia basi watageuza migongo;

Hii ndio hali ya mnafiki, ulimi wake unahalifiwa na moyo wake na dhahiri yake inahalifiwa na siri yake.

Kisha hawatanusuriwa wala kunufaika na kwa vitimbi na unafiki wao.

Hakika nyinyi ni tishio zaidi katika vifua vyao kuliko Mwenyezi Mungu. Hayo ni kwa kuwa hao ni watu wasiofahamu.

Wanafiki wanawaogopa waumini kwa ukali wao wa vita, kwa sababu wao wanatazamia shari ya haraka wala hawatazimii adhabu inayokuja Akhera.

Hawatapigana nanyi kwa mkusanyiko isipokuwa katika vijiji vilivyo zatitiwa kwa ngome, au nyuma ya kuta.

Mayahudi hawakabiliani na waumini uso kwa uso katika uwanja wa vita, bali wanajificha kwenye mitaa yao nyuma ya ngome na kuta na kuwarushia waumini mishale na mawe; kama ilivyo hali ya mwoga.

Wao kwa wao vita vyao ni vikali. Utawadhania kuwa wako pamoja, kumbe nyoyo zao ni mbali mbali.

Wao wana nguvu kwa maandalizi yao na idadi yao, lakini masilahi na hawa za nafsi zimewatawanyisha. Wao wamechangukana, hata kama wanajionyesha kuwa na umoja na mapenzi.

Lau wangelikuwa na umoja na kupendana wangeliwatokea kupambana nanyi, lakini hawakupigana nanyi. Hili liko kwa wayahudi na wasiokuwa wayahudi, kwani umoja ni nguvu hata kama idadi na nyenzo ni ndogo, na utengano ni udhaifu hata kama kuna nyenzo na wingi wa watu.

Tumeshuhudia ushindi wa watu wasio na haki wachache juu ya walio na haki wengi na wenye nyenzo. Siri ni utengano wa hawa kwenye haki yao na umoja wa wale kwenye batili yao.

Hayo ni kwa kuwa wao ni watu wasio na akili ya kufahamu kuwa umoja ni nguvu na utengano ni udhaifu. Ni kama mfano wa waliokuwa kabla yao hivi karibuni. Walionja ubaya wa mambo yao. Nao watapata adhabu iliyo chungu.

Mayahudi walijenga uadui na Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w ) ; ni sawa na hali ya makafiri wa kikuraishi na wengineo waliompiga vita Mtume; pale walipoishia kwenye fedheha ya duniani na Akhera ni adhabu ya kuungua.

كَمَثَلِ الشَّيْطَانِ إِذْ قَالَ لِلْإِنسَانِ اكْفُرْ فَلَمَّا كَفَرَ قَالَ إِنِّي بَرِيءٌ مِّنكَ إِنِّي أَخَافُ اللَّـهَ رَبَّ الْعَالَمِينَ ﴿١٦﴾

16. Ni kama mfano wa Shetani anapomwambia mtu: kufuru. Na akikufuru humwambia: Mimi si pamoja nawe. Hakika mimi namwogopa Mwenyezi Mungu, Mola wa walimwengu wote.

فَكَانَ عَاقِبَتَهُمَا أَنَّهُمَا فِي النَّارِ خَالِدَيْنِ فِيهَا وَذَٰلِكَ جَزَاءُ الظَّالِمِينَ ﴿١٧﴾

17. Basi ikawa mwisho wa wote wawili hao ni kuingia Motoni, wadumu humo daima; na hayo ndiyo malipo ya madhal­imu.

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا اتَّقُوا اللَّـهَ وَلْتَنظُرْ نَفْسٌ مَّا قَدَّمَتْ لِغَدٍ وَاتَّقُوا اللَّـهَ إِنَّ اللَّـهَ خَبِيرٌ بِمَا تَعْمَلُونَ ﴿١٨﴾

18. Enyi mlioamini! Mcheni Mwenyezi Mungu, na kila nafsi iangalie inayoyatan­guliza kwa ajili ya Kesho. Na mcheni Mwenyezi Mungu. Hakika Mwenyezi Mungu ana habari za mnayoyatenda.

وَلَا تَكُونُوا كَالَّذِينَ نَسُوا اللَّـهَ فَأَنسَاهُمْ أَنفُسَهُمْ أُولَـٰئِكَ هُمُ الْفَاسِقُونَ ﴿١٩﴾

19. Wala msiwe kama wale waliomsahau Mwenyezi Mungu, na Yeye akawasa­haulisha nafsi zao. Hao ndio mafasiki.

لَا يَسْتَوِي أَصْحَابُ النَّارِ وَأَصْحَابُ الْجَنَّةِ أَصْحَابُ الْجَنَّةِ هُمُ الْفَائِزُونَ ﴿٢٠﴾

20. Hawawi sawa watu wa Motoni na watu wa Peponi. Watu wa Peponi ndio wenye kufuzu.

AKIKUFURU HUMWAMBIA MIMI NIKO MBALI NAWE

Aya 16 – 20

MAANA

Ni kama mfano wa Shetani anapomwambia mtu: kufuru. Na akikufu­ru humwambia: Mimi si pamoja nawe. Hakika mimi namwogopa Mwenyezi Mungu, Mola wa walimwengu wote.

Wanafiki waliwaambia Bani Nadhir: “Piganeni na Muhammad na sisi tuko pamoja nanyi katika vita,” lakini yalipowafika yaliowafika, walijificha kwenye viota vyao na hawakuonekana hata athari yao.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) ameifananisha hali ya wanafiki na Bani Nadhir na hali ya shetani na mtu mwenye kutenda dhambi. Huwa anamhadaa kwa ufisadi na upotevu na kumpa tamaa ya amani. Mambo yakichacha humwacha na adhabu na maangamizi na kujitenga naye na kudhihirisha hofu kutoka kwa Mwenyezi Mungu.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 10 (8:48) na Juz. 13 (14:22).

Basi ikawa mwisho wa wote wawili hao ni kuingia Motoni, wadumu humo daima; na hayo ndiyo malipo ya madhalimu.

Wawili ni shetani na mtu aliyeingia kwenye mtego wake. Maana yako wazi. Kwa ufupi ni kuwa kila mmoja, mwenye kuhadaa na mwenye kuhadaiwa, atakuwa katika Jahannam ambayo ni marejeo mabaya.

Enyi mlioamini! Mcheni Mwenyezi Mungu, ambaye nyinyi mko mikononi mwake, na mwenye kumcha Mwenyezi Mungu humfanyia wepesi mambo yake; kama anavyosema Mwenyezi Mungu katika Qur’an (65:4).

Na kila nafsi iangalie inayoyatanguliza kwa ajili ya Kesho.

Kila analolifanya mtu katika maisha haya huwa amelifanya kwa ajili ya Akhera. Mwenye busara anaangalia kwenye dunia yake kwa mtazamo wa mwenye kuicha kwa wema sio mwenye kuchukua anasa zake.

Na mcheni Mwenyezi Mungu. Hakika Mwenyezi Mungu ana habari za mnayoyatenda.

Mwenyezi Mungu anamjua mwenye kuamini kwa kauli na vitendo na mwenye kumwamini kwa fikra tu anayoisema na kuisahau kwenye viten­do. Mwenyezi Mungu (s.w.t) amelikariri jambo la takua kwa ukomo wa kuhimiza na kupendekeza.

Wala msiwe kama wale waliomsahau Mwenyezi Mungu, na Yeye akawasahaulisha nafsi zao.

Walisahau kufanya kwa amri ya Mwenyezi Mungu na Mwenyezi Mungu akawasahaulisha kufanya kwa masilahi ya nafsi zao. na aliyedanganyika zaidi katika watu ni yule aliyejisahau na asifanye kwa ajili ya usalama wake kujiepusha na maangamizi.

Hao ndio mafasiki. Kwa sababu hawakunufaika na ubainifu wa Mwenyezi Mungu na kupata funzo kwa mawaidha yake.

Hawawi sawa watu wa Motoni na watu wa Peponi. Watu wa Peponi ndio wenye kufuzu.

Vipi atakuwa sawa mwema na mwovu? Umetangulia mfano wake katika Aya kadhaa miongoni mwazo ni Juz. 21 (32:18).

لَوْ أَنزَلْنَا هَـٰذَا الْقُرْآنَ عَلَىٰ جَبَلٍ لَّرَأَيْتَهُ خَاشِعًا مُّتَصَدِّعًا مِّنْ خَشْيَةِ اللَّـهِ وَتِلْكَ الْأَمْثَالُ نَضْرِبُهَا لِلنَّاسِ لَعَلَّهُمْ يَتَفَكَّرُونَ ﴿٢١﴾

21. Lau tungelieiteremsha hii Qur’an juu ya mlima, basi bila ya shaka ungeliuona ukinyenyekea, ukipasuka kwa hofu ya Mwenyezi Mungu. Na hiyo ni mifano tunawapigia watu ili wafikiri.

هُوَ اللَّـهُ الَّذِي لَا إِلَـٰهَ إِلَّا هُوَ عَالِمُ الْغَيْبِ وَالشَّهَادَةِ هُوَ الرَّحْمَـٰنُ الرَّحِيمُ ﴿٢٢﴾

22. Yeye ndiye Mwenyezi Mungu, ambaye hapana mungu isipo kuwa Yeye tu, Mwenye kuya­jua yaliyofichikana na yanay­oonekana. Yeye ndiye Mwingi wa rehema, Mwenye kurehemu.

هُوَ اللَّـهُ الَّذِي لَا إِلَـٰهَ إِلَّا هُوَ الْمَلِكُ الْقُدُّوسُ السَّلَامُ الْمُؤْمِنُ الْمُهَيْمِنُ الْعَزِيزُ الْجَبَّارُ الْمُتَكَبِّرُ سُبْحَانَ اللَّـهِ عَمَّا يُشْرِكُونَ ﴿٢٣﴾

23. Yeye ndiye Mwenyezi Mungu ambaye hapana mungu isipo kuwa Yeye tu. Mtakatifu, Mwenye salama, Mtoaji wa amani, Mwangaliaji, Mwenye nguvu, Jabari, Mkubwa; Ametakasika Mwenyezi Mungu na hayo wanay­omshirikisha nayo.

هُوَ اللَّـهُ الْخَالِقُ الْبَارِئُ الْمُصَوِّرُ لَهُ الْأَسْمَاءُ الْحُسْنَىٰ يُسَبِّحُ لَهُ مَا فِي السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ وَهُوَ الْعَزِيزُ الْحَكِيمُ ﴿٢٤﴾

24. Yeye ndiye Mwenyezi Mungu, Muumbaji, Mtengenezaji, Mtia sura, Mwenye majina mazuri kabisa. Kinamsabihi kilicho katika mbingu na ardhi, naye ni Mwenye nguvu, Mwenye hikima.

LAU TUNGELIITERMSHA HII QUR’ANI JUU MLIMA

Aya 21 – 24

MAANA

Lau tungelieiteremsha hii Qur’an juu ya mlima, basi bila ya shaka ungeliuona ukinyenyekea, ukipasuka kwa hofu ya Mwenyezi Mungu.

Hii ni kiasi cha kukadiria tu, kunakofahamika kutokana na neno ‘Lau.’ Lengo ni kubainisha ukuu wa Qur’an, kwamba ina nguvu na athari; kiasi ambacho lau itateremshwa kwenye jabali basi lingenyenyeka na kulainika pamoja na ugumu wake. Pia lingelipasuka na kuanguka kwa kumwogopa Mwenyezi Mungu. Basi vipi mtu ambaye anaumizwa na chawa na kufa kwa kusongwa koo na jasho humfanya anuke; kama alivyosema Amirul Muminin, Ali(a.s) ?

Ana nini mtu huyu mnyonge, “anayesikia Aya za Mwenyezi Mungu akisomewa, kisha anang’ng’ania huku akijivuna, kama kwamba hakuzisikia. ” Juz. 25 (45:8).

Je, ni kwa kuwa moyo wake ni mgumu kama jabali ambalo limekazana sana, au ni ujinga, inadi na kung’ang’ania upotevu?

Na hiyo ni mifano tunawapigia watu ili wafikiri, katika hikima ya Qur’an, mawaidha yake, dalili yake, na ubainifu wake, na waongoke, kwa nuru yake, kwenye njia ya usawa, lakini:

إِنَّ فِي ذَٰلِكَ لَذِكْرَىٰ لِمَن كَانَ لَهُ قَلْبٌ أَوْ أَلْقَى السَّمْعَ وَهُوَ شَهِيدٌ ﴿٣٧﴾

“Hakika katika hayo kuna ukumbusho kwa mwenye moyo au akatega sikio naye ni shahidi.”

Juz. 26 (50:37).

Baada ya hayo yote, hakika ukuu wa Qur’an ni ukuu wa Mwenyezi Mungu (s.w.t). Walisema wakale: maneno ni sifa ya mwenye kusema; hasa yale yanayorudia ilimu yake.

Ndio maana Mwenyezi Mungu akaisifia Qur’an kwa sifa zake; kama vile nguvu, hekima, utukufu, ukuu, nuru, haki, rehe­ma, ukweli n.k.

Kisha Mwenyezi Mungu (s.w.t) akajisifu kwa sifa zake tukufu akasema:Yeye ndiye Mwenyezi Mungu, ambaye hapana mungu isipo kuwa Yeye tu, apasaye kuabudiwa kwa haki, anayesifika kwa sifa zote nzuri za ukamilifu; zikiwemo hizi zifuatazo:-

Mwenye kuyajua yaliofichikana na yanayoonekana . Anayajua yaliyoghaibu kwa watu na yaliyo dhahiri.

Yeye ndiye Mwingi wa rehema, Mwenye kurehemu . Sifa mbili hizi zimetokana na rehema kwa maana ya hisani. Inawezekana kuwa kuchanganywa matamko mawili ni kuashiria kuwa rehema yake imeenea kila kitu, hata katika hali ya kughadhibika kwake; na kwamba kuikatia tamaa ni kufuru na upotevu.

Yeye ndiye Mwenyezi Mungu ambaye hapana mungu isipo kuwa Yeye tu. Huu ni msisitizo wa tawhid. Yeye niMfalme; ni wake ufalme wa mbingu na ardhi, Ndiye anayetoa uhai na kufisha.

Mtakatifu; yaani ametakasika na yasiyolaikiana na utukufu wake.Mwenye salama ; kwa sababu inatokana na Yeye mtukufu utulivu na amaniMtoaji wa amani ; Anawapa thawabu waumini na anawapa amani ya adhabu ya moto.Mwangaliaji ; Mwenye kuchunga na kuhifadhi.

Mwenye nguvu ; asiyeshindwa wala kuzidiwa nguvu.Jabari ; Aliye juu bila ya kufikiwa.Mkubwa; Ana ukubwa na utukufu.Ametakasika Mwenyezi Mungu na hayo wanayomshirikisha nayo , ya kuwa na mshirika, mke na mtoto.Yeye ndiye Mwenyezi Mungu, Muumbaji, Mtengenezaji .

Hizi ni sifa mbili tofauti. Neno mtengenezaji tumelifasiri kutokana na neno Bariu ambalo imesemekana kuwa hapa lina maana ya kuwa mbali na upun­gufu.Mtia sura ; Mwenye kuumba sura na umbo.Mwenye majina mazuri kabisa.

Kila jina lake Mwenyezi Mungu Mtukufu ni zuri na ni kuu. Tazama Juz. 9 (7:180) Kifungu cha: ‘Je, majina ya Mwenyezi Mungu ni hayo hayo?’

Kinamsabihi kilicho katika mbingu na ardhi, naye ni Mwenye nguvu, Mwenye hikima.

Tasbihi inakuwa kwa lugha ya maneno na lugha ya hali. Tazama Juz. 15 (15:44) kifungu cha ‘Kila kitu kinamsabihi.

MWISHO WA SURA YA HAMSINI NA TISA: SURAT AL-HASHR


3

4

5

6

7

8

9

10

11

12

13

14

15

16