TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE Juzuu 24

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE0%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: Qurani tukufu

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE

Mwandishi: Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya
: HASANI MWALUPA
Kundi:

Matembeleo: 26017
Pakua: 3245


Maelezo zaidi:

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 30 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 26017 / Pakua: 3245
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE Juzuu 24

Mwandishi:
Swahili

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE

IMEANDIKWA NA: SHEIKH MUHAMMAD JAWAD MUGHNIYYA

IMETAFSIRIWA NA: SHEIKH HASAN MWALUPA

IMEHARIRIWA NA: USTADH ABDALLAH MOHAMED

IMEPANGWA KATIKA KOMPYUTA NA: UKHT PILI RAJABU

UTANGULIZI WA MCHAPISHAJI

Kitabu hiki kilichoko mikononi mwako hivi sasa ni juhudi ya miaka mingi sana ya watu waliojitolea kuona kazi hii imefanikiwa bila ya kumsahau Marhum Abu Muhammad wa London.

Kama lilivyo jina la Tafsiri ndivyo ilivyo Tafsiri yenyewe ambayo mwanachuoni huyu mahiri kabisa aliyeifafanua ni mtu aliyebobea katika fani zote ambazo mfasiri (Mfafanuzi) anatakiwa awe nazo.

Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya ameonesha cheche zake katika vitabu vingi alivyoviandika katika maudhui mbali mbalimbali na hivyo kujipatia wasomaji wengi sana.

Msomi huyu, mwenye fikra huru na anayetetea kile anachokiamini, ni mtu mwenye mawazo mapana na kuyaangalia mambo kwa undani sana, kipaumbele chake ni katika maslahi ya umma huu na amejaribu sana kwenda na wakati.

Sifa kubwa pekee ya mwanachuoni huyu ni kuwa yeye hakujihusisha sana na kung'ang'ania madhehebu fulani tu, labda hii yatokana na wadhifa wake wa ukadhi aliokuwa nao katika nchi ya Lebanon ambayo ina madhehebu mengi, ambapo sula la madhehebu ni nyeti nchini humo, hata hivyo yeye aliweza kuamua matatizo ya watu kwenye ofisi yake kulingana na madhehebu yao pale walipomwendea. Hiyo ilimsaidia sana hata kuweza kutoa kitabu kitwacho Al-Fiqh a'laa madhaahabil-khamsah (Fikhi ya madhehebu matano) yaani ya Hanafi, Maaliki, Shafi, Hambali na Shia (ambacho twataraji kitatoka kwa lugha ya kiswahili hivi karibuni Inshaallah).

Jambo lililotupa msukumo wa kukifasiri kitabu hiki kwa lugha ya Kiswahili ni zile faida nyingi atakazozipata msomaji na kujua mambo mengi na ya ajabu yaliyo mapya kwake ambayo si rahisi kuyapata kwa wafasiri wengine.

Msomaji atapata faida katika fani za Sayansi, Siasa, Historia, Mashairi, visa vizuri, na Saikolojia miongoni mwa mengine; ndiyo maana msomaji atashangaa kidogo anapoisoma Tafsiri hii atakapoona mwandishi amewataja na kuwanukuu watu kama kina Mfalme Edward, wanasayansi kama kina Enstein, wasanii kama Charlie Champlin (Mchekeshaji maarufu), na wengineo, hali inayoifanya tafsiri hii kuwa ni ya kipekee kabisa.

Mtindo alioutumia mwandishi ni sahali uliokusudiwa watu wa tabaka mbalimbali, wanavyuoni na watu wa kawaida.

Nia yetu ni kukigawanya kitabu hiki bure lakini tumelazimika kukiuza kwa bei nafuu ili kurudisha gharama za uchapishaji.

Mwisho: Shukrani kubwa iwaendee bila ya kuwataja watu waliojitolea usiku na mchana, jopo la wafasiri, wahariri, wachapaji, waliotupa moyo na kutoa maoni yao na walioisimamia ili kuhakikisha kwamba kitabu kimemfikia msomaji.

MAKOSA YA CHAPA

Sikumbuki kama nimewahi kusoma kitabu kilichotoka kupigwa chapa, cha zamani au cha sasa, bila ya kukuta makosa ya chapa, Nafikiri sitasoma kitabu kisichokuwa hivyo. Nimejaribu sana kuliepuka hilo katika tungo zangu, lakini sikufanikiwa.

Nilikuwa sifikirii kama ninaweza kuona makosa haya katika maandishi ya msahafu mtukufu, kama yale yaliyo katika baadhi ya chapa; kwa mfano neno yabswutu kwa swad, badala ya yabsutu kwa sin, na katika chapa ya Tafsir Arrazi ya Misr ya mwaka 1935, Sura ya (2:146), Imeandikwa La Ya'alamuun, (hawajui) badala ya Ya'alamuun (wanajua). Mfano wa makosa haya hausameheki.

Katika Tafsir Al-Manar, chapa ya Pili, sura (5:212), imeandikwa Fawqahum ila yawmil qiyama badala ya Fawqahum yawamal qiyama. Hatuwezi kusema kosa hili ni kubwa zaidi kuliko lile.

Lakini mkosaji atatuletea udhuru kwa msemo mashuhuri huko kwetu Jabal amil 'Makosa ya chapa.'

Katika Tafsiri Majmau chapa ya Urfan, Sura (46:15), imeandikwa: Hatta idha balagha arbai' na sanah badala ya: Hattaidha balagha ashuddahu arbai ' na sanah"

Kusema hivi sio kama ninajitetea kutokana na makosa ya chapa atakayoyakuta msomaji katika kitabu hiki, ijapokuwa naomba msamaha kama litatokea hili, lakini makusudio yangu hasa ni kumwambia yule atakayefungua macho yake kwenye makosa ya matamko na kuufungia macho uzuri wa maana.

Vilevile ninamwambia yule ambaye siku moja aliniambia: "Vitabu vyako vimejaa makosa ya chapa.” Kama kwamba hakuna kitu chochote katika vitabu hivyo isipokuwa makosa ya chapa tu. Wote hao ninawaambia: Mungu awasamehe na aniongoze mimi na nyinyi.

Vyovyote iwavyo, mimi ninaomba msamaha kutokana na makosa ya kifikra na ya chapa. Anasema Amirul Muminiin(a.s) :"Watu wote ni wapungufu wenye kuchanganyikiwa, isipokuwa yule aliyehifadhiwa na Mwenyezi Mungu." Na Mwenyezi Mungu (s.w.t) ndiye mwenye jukumu la kunikubalia yale niliyoyapatia na kunisamehe niliyakosea, kwa jaha ya Mtume na kizazi chake, ziwashukie rehema na amani (Amin).

MUHAMMAD JAWAD MUGHNIYYAH

1

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE

Sura Ya Hamsini Na Nane: Al–Mujadala. Imeshuka Madina. Imesemekana kinyume na hivyo, Ina Aya 22.

بِسْمِ اللَّهِ الرَّحْمَٰنِ الرَّحِيمِ

Kwa jina la Mwenyezi Mungu Mwingi wa rehema, Mwenye kurehemu.

قَدْ سَمِعَ اللَّـهُ قَوْلَ الَّتِي تُجَادِلُكَ فِي زَوْجِهَا وَتَشْتَكِي إِلَى اللَّـهِ وَاللَّـهُ يَسْمَعُ تَحَاوُرَكُمَا إِنَّ اللَّـهَ سَمِيعٌ بَصِيرٌ ﴿١﴾

1. Mwenyezi Mungu amekwisha­sikia usemi wa mwanamke anayejadiliana nawe juu ya mumewe, na anamshitakia Mwenyezi Mungu. Na Mwenyezi Mungu anayasikia majibizano yenu. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusikia, Mwenye kuona.

الَّذِينَ يُظَاهِرُونَ مِنكُم مِّن نِّسَائِهِم مَّا هُنَّ أُمَّهَاتِهِمْ إِنْ أُمَّهَاتُهُمْ إِلَّا اللَّائِي وَلَدْنَهُمْ وَإِنَّهُمْ لَيَقُولُونَ مُنكَرًا مِّنَ الْقَوْلِ وَزُورًا وَإِنَّ اللَّـهَ لَعَفُوٌّ غَفُورٌ ﴿٢﴾

2. Wale miongoni mwenu wanaowafanyia dh h. wake zao, hao si mama zao. Hawakuwa mama zao ila wale waliowazaa. Na hakika hao wanasema neno linalochusha na la uwongo. Na hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusamehe, Mwenye kughufi­ria.

وَالَّذِينَ يُظَاهِرُونَ مِن نِّسَائِهِمْ ثُمَّ يَعُودُونَ لِمَا قَالُوا فَتَحْرِيرُ رَقَبَةٍ مِّن قَبْلِ أَن يَتَمَاسَّا ذَٰلِكُمْ تُوعَظُونَ بِهِ وَاللَّـهُ بِمَا تَعْمَلُونَ خَبِيرٌ ﴿٣﴾

3. Na wale wanaowafanyia dhiha­ wake zao kisha wakarudi kuachana na yale walioyase­ma, basi ni kumwacha huru mtumwa kabla hawajagusana. Mnapewa mawaidha kwa hayo. Na Mwenyezi Mungu anayajua mnayoyatenda.

فَمَن لَّمْ يَجِدْ فَصِيَامُ شَهْرَيْنِ مُتَتَابِعَيْنِ مِن قَبْلِ أَن يَتَمَاسَّا فَمَن لَّمْ يَسْتَطِعْ فَإِطْعَامُ سِتِّينَ مِسْكِينًا ذَٰلِكَ لِتُؤْمِنُوا بِاللَّـهِ وَرَسُولِهِ وَتِلْكَ حُدُودُ اللَّـهِ وَلِلْكَافِرِينَ عَذَابٌ أَلِيمٌ ﴿٤﴾

4. Na asiyepata, basi afunge miezi miwili ya kufuatana kabla hawajagusana. Na asiyeweza basi awalishe masikini sitini. Hayo ni hivyo ili mumwamini Mwenyezi Mungu na Mtume wake. Na hiyo ndiyo mipaka ya Mwenyezi Mungu Na kwa makafiri iko adhabu chungu.

DHIHAR

Aya 1 – 4

LUGHA

Dhihar ni mume kumwambia mkewe: ‘Wewe kwangu ni kama mgongo wa mama yangu;’ akimaanisha kuwa ni haramu kwake kama alivyo mama yake. Akishasema hivyo basi mke anakuwa haramu kwake mpaka atoe kafara; kama yatakavyokuja maelezo.

KISA KWA UFUPI

Wameafikiana wafasiri kuwa Aya hizi zilishuka kwa tukio maalum. Kwa ufupi, tukio lenyewe ni kama ifutavyo:-

Mtu mmoja alimkasirikia mkewe akamwambia: wewe kwangu ni kama mgongo wa mama yangu, na hiyo ilikuwa ni talaka wakati wa Jahilia. Basi mwanamke akahuzunika, na mwanamume akajuta kwa haraka yake alioifanya, akamwambia mkewe nenda kwa Mtume umpe habari ya yaliyotokea, mimi ninaona haya kumuuliza.

Mke akaenda na kumsimulia Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w. w ) na akamsisitiza, huku akisema: Ninamshtakia Mwenyezi Mungu haja yangu. Mwenyezi Mungu akaitikia dua yake na akateremsha Aya hizi. Kisa hiki kinaafikiana na dhahiri ya Aya.

Vyovyote iwavyo ni kuwa: Dhihar ni mlango katika milango ya fiqhi ya waislamu.

MAANA

Mwenyezi Mungu amekwishasikia usemi wa mwanamke anayejadiliana nawe juu ya mumewe, na anamshitakia Mwenyezi Mungu. Na Mwenyezi Mungu anayasikia majibizano yenu.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) anamwambia Mtume wake mtukufu kuwa Mwenyezi Mungu amekwishajua hali ya mwanamke na anavyokuelezea kuhusu mumewe. Vile vile amekwishajua mashtaka yake na maombi yake; na amekwishaitikia maombi yake.Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusikia, Mwenye kuona; hakifichiki kwake chochote cha kujificha.

Kisha Mwenyezi Mungu (s.w.t) akabainisha hukumu ya tukio hili na mfano wake kwa kusema:

Wale miongoni mwenu wanaowafanyia dh h. wake zao, hao si mama zao. Hawakuwa mama zao ila wale waliowazaa. Na hakika hao wanasema neno linalochusha na la uwongo.

Dhihari imeharamishwa katika dini ya Mwenyezi Mungu, kwa sababu ni uwongo unaohalifu uhalisia. Vipi mke awe ni mama!

Na hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusamehe, Mwenye kughufiria, yule mwenye kutubia na akarejea nyuma. Baadhi ya mafakihi wame­sema kuwa dhihari ni haramu hilo halina shaka yoyote, kwa sababu Mwenyezi Mungu ameisifu kuwa ni ya kuchukiza na ni uwongo, lakini haina dhambi kwa anayeifanya, kwa sababu ameikutanisha na msamaha.

Lakini kauli ya kutokuwa na dhambi ameirudi Shahidi wa pili kwa kuse­ma kuwa msamaha katika Aya ni wakiujumla na hauhusiki na dhihari.

Na wale wanaowafanyia Dhihar wake zao kisha wakarudi kuachana na yale waliyoyasema, basi ni kumwacha huru mtumwa kabla hawajagusana.

Kurudi na kuyaacha yale waliyoyasema ni wale wanaofanya dhihari kisha wakajuta na kuiacha kauli yao.

Ibn Hisham, katika Mughni anasema: herufi lam inakuja kwa maana ya herufi a’yn (kuachana na) kama ilivyo katika Juz. 12 (11:31). Pia huwa inakuja kwa maana ya herufi fi (katika); kama ilivyo katika Juz. 17 (21:47). Wametofautiana kuhusu kugusana.

Kuna waliosema kuwa ni kugusana kwa maana yake ya kilugha yalivyo. Wengine wakasema ni kuingiliana. Kauli hii haiko mbali na lugha ya Qur’an; kama alivyosema Mwenyezi Mungu: “Na kama mkiwapa talaka kabla ya kuwagusa…” Juz. 2 (2:237), kwa maana ya kabla ya kuwaingilia; kama walivyoafikina mafakihi

Mnapewa mawaidha kwa hayo. Na Mwenyezi Mungu anayajua mnayoyatenda.

‘Hayo,’ ni hayo ya wajibu wa kafara la dhihari. Makusudio ya mawaidha hapa ni maonyo. Maana ni kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) amewajibisha kafara la dhihari ili liwe ni onyo na kukemea isifanyike, kwa sababu ni jambo la kuchukiza na ni uwongo. Na Mwenyezi Mungu anamjua muasi na mtiifu na kumfanyia kila mmoja stahiki yake.

Na asiyepata mtumwa wa kumkomboa,basi afunge miezi miwili ya kufuatana kabla hawajagusana. Na asiyeweza basi awalishe maskini sitini.

Wameafikiana kwamba mwenye kumwambia mkewe: Wewe kwangu ni kama mgongo wa mama yangu,’ haiwi halali kwake kumwingilia mke huyo, mpaka atoe kafara, kwa kumwacha huru mtumwa, akishindwa kupa­ta mtumwa, afunge miezi miwili ya kufuatana na akishindwa kufunga basi awalishe masikini sitini. Vile vile wameafikiana kuwa akimwingilia kabla ya kutoa kafara atakuwa ameasi, lakini Shia Imamiya wamewajibisha kafara mbili kwa hilo.

Shia Imamiya pia wameweka sharti la kuweko waadilifu wawili watakaosikia kauli ya mume na kuwa mke awe katika twahara (asiwe hedhini) ambayo hakuingiliwa na mumewe; sawa na yalivyo masharti ya talaka; kama ambavyo wahakiki miongoni mwao wameweka pia sharti la kuwa awe amekwishawahi kuingiliwa na mumewe; vinginevyo itakuwa hakuna dhihari. Ufafanuzi uko kwenye vitabu vya Fiqh.

Hayo ni hivyo ili mumwamini Mwenyezi Mungu na Mtume wake.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) ameisahilisha sharia kwa waja wake ili waiami­ni na ili iwe ni hoja wazi kwa yule anayeipinga sharia.

Na hiyo ndiyo mipaka ya Mwenyezi Mungu, basi msiikeuke.

Na kwa makafiri iko adhabu chungu kwa kupinga kwao sharia ya Mwenyezi Mungu na hukumu yake. Ndani yake kuna ishara kuwa mwenye kuhalifu sharia ya Mwenyezi Mungu basi anahukumiwa kuwa ni kafiri.

إِنَّ الَّذِينَ يُحَادُّونَ اللَّـهَ وَرَسُولَهُ كُبِتُوا كَمَا كُبِتَ الَّذِينَ مِن قَبْلِهِمْ وَقَدْ أَنزَلْنَا آيَاتٍ بَيِّنَاتٍ وَلِلْكَافِرِينَ عَذَابٌ مُّهِينٌ ﴿٥﴾

5. Hakika wanaopingana na Mwenyezi Mungu na Mtume wake, watadhalilishwa kama walivyodhalilishwa wale waliokuwa kabla yao. Na tulik­wishateremsha Ishara zilizo wazi. Na makafiri watapata adhabu ifedheheshayo.

يَوْمَ يَبْعَثُهُمُ اللَّـهُ جَمِيعًا فَيُنَبِّئُهُم بِمَا عَمِلُوا أَحْصَاهُ اللَّـهُ وَنَسُوهُ وَاللَّـهُ عَلَىٰ كُلِّ شَيْءٍ شَهِيدٌ ﴿٦﴾

6. Siku atapowafufua Mwenyezi Mungu, na awaambie yale waliyoyatenda. Mwenyezi Mungu ameyadhibiti, na wao wameyasahau! Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kushuhu­dia kila kitu.

أَلَمْ تَرَ أَنَّ اللَّـهَ يَعْلَمُ مَا فِي السَّمَاوَاتِ وَمَا فِي الْأَرْضِ مَا يَكُونُ مِن نَّجْوَىٰ ثَلَاثَةٍ إِلَّا هُوَ رَابِعُهُمْ وَلَا خَمْسَةٍ إِلَّا هُوَ سَادِسُهُمْ وَلَا أَدْنَىٰ مِن ذَٰلِكَ وَلَا أَكْثَرَ إِلَّا هُوَ مَعَهُمْ أَيْنَ مَا كَانُوا ثُمَّ يُنَبِّئُهُم بِمَا عَمِلُوا يَوْمَ الْقِيَامَةِ إِنَّ اللَّـهَ بِكُلِّ شَيْءٍ عَلِيمٌ ﴿٧﴾

7. Kwani huoni kwamba Mwenyezi Mungu anajua vilivyo katika mbingu na vilivyo katika ardhi? Hauwi mnong’ono wa watu watatu ila Yeye huwa ni wanne wao, wala wa watano ila Yeye huwa ni wa sita wao. Wala wa wachache kuliko hao, wala walio wengi zaidi, ila Yeye yuko pamoja nao popote pale walipo. Kisha Siku ya Kiyama atawaambia waliyoyatenda. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mjuzi wa kila kitu.

أَلَمْ تَرَ إِلَى الَّذِينَ نُهُوا عَنِ النَّجْوَىٰ ثُمَّ يَعُودُونَ لِمَا نُهُوا عَنْهُ وَيَتَنَاجَوْنَ بِالْإِثْمِ وَالْعُدْوَانِ وَمَعْصِيَتِ الرَّسُولِ وَإِذَا جَاءُوكَ حَيَّوْكَ بِمَا لَمْ يُحَيِّكَ بِهِ اللَّـهُ وَيَقُولُونَ فِي أَنفُسِهِمْ لَوْلَا يُعَذِّبُنَا اللَّـهُ بِمَا نَقُولُ حَسْبُهُمْ جَهَنَّمُ يَصْلَوْنَهَا فَبِئْسَ الْمَصِيرُ ﴿٨﴾

8. Kwani huwaoni wale waliokatazwa kunong’ona, kisha wakayarudia yale uadui, na ya kumwasi Mtume? Na wakikujia hukuamkia sivyo anavyokuamkia Mwenyezi Mungu. Na husema katika nafsi zao: Mbona Mwenyezi Mungu hatuadhibu kwa haya tuyasemayo? Jahannamu itawatosha; wataingia humo! Ni marejeo mabaya sana.

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا إِذَا تَنَاجَيْتُمْ فَلَا تَتَنَاجَوْا بِالْإِثْمِ وَالْعُدْوَانِ وَمَعْصِيَتِ الرَّسُولِ وَتَنَاجَوْا بِالْبِرِّ وَالتَّقْوَىٰ وَاتَّقُوا اللَّـهَ الَّذِي إِلَيْهِ تُحْشَرُونَ ﴿٩﴾

9. Enyi mlioamini! Mnapo nong’onezana. Msinong’onezane kwa sababu ya mambo ya madhambi, na uadui, na kumuasi Mtume. Bali nong’onezaneni kwa kutenda mema na takua. Na mcheni Mwenyezi Mungu ambaye kwake mtakusanywa.

إِنَّمَا النَّجْوَىٰ مِنَ الشَّيْطَانِ لِيَحْزُنَ الَّذِينَ آمَنُوا وَلَيْسَ بِضَارِّهِمْ شَيْئًا إِلَّا بِإِذْنِ اللَّـهِ وَعَلَى اللَّـهِ فَلْيَتَوَكَّلِ الْمُؤْمِنُونَ ﴿١٠﴾

10. Kwa hakika minong’ono hiyo inatokana na Shetani ili awahuzunishe walioamini, na wala hatawadhuru chochote ila kwa idhini ya Mwenyezi Mungu. Basi waumini wamtegemea Mwenyezi Mungu. Basi waumini wamtegemee Mwenyezi Mungu.

KUNONG’ONEZANA

Aya 5 – 10

MAANA

Hakika wanaopingana na Mwenyezi Mungu na Mtume wake, watad­halilishwa kama walivyodhalilishwa wale waliokuwa kabla yao.

Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kutaja mipaka yake, sasa anampa onyo yule atakayeipetuka mipaka na akampa sifa ya adui wa Mwenyezi Mungu na Mtume wake na kwamba adhabu yao ni kushindwa na hizaya; kama ilivyokuwa adhabu ya umma zilizotangulia.

Na tulikwishateremsha Ishara zilizo wazi. Na makafiri watapata adhabu ifedheheshayo.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) amesimamisha hoja waziwazi za kuweko Yeye na unabii wa mjumbe wake(s.a.w. w ) na akabainisha halali na haramu. Dalili hizi zinafahamisha kuwa kumtii Mwenyezi Mungu na Mtume ni wajibu na

kwamba mwenye kuhalifu anastahili adhabu itakayomfedhehesha,siku atapowafufua Mwenyezi Mungu, na awaambie yale waliyoyatenda. Mwenyezi Mungu ameyadhibiti, na wao wameyasahau! Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kushuhudia kila kitu.

Kesho Mwenyezi Mungu atawakusanya kwa ajili ya hisabu na malipo kwa yale walioyafanya. Mkosefu akisahau madhambi Alioyafanya yote au baadhi yake, Mwenyezi Mungu anakuwa ameyajua yote na atamfedhehe­sha nayo na kumwonjesha adhabu kwa haki na uadilifu wala hatadhulumiwa.

Kwani huoni kwamba Mwenyezi Mungu anajua vilivyo katika mbin­gu na vilivyo katika ardhi?

Hujui ewe Muhammad kwamba kwa Mwenyezi Mungu hakifichiki chochote mbinguni na ardhini. Vile vile anajua kuwaHauwi mnong’ono wa watu watatu ila Yeye huwa ni wa nne wao, wala wa watano ila Yeye huwa ni wa sita wao. Wala wa wachache kuliko hao, wala walio wengi zaidi, ila Yeye yuko pamoja nao popote pale walipo. Kisha Siku ya Kiyama atawaambia waliyoyatenda.

Kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: ‘wala wachache kuliko hao,’ ni ishara ya chini ya watatu, na ‘wala walio wengi zaidi,’ ni zaidi ya watano. Kundi la wafasiri wamesema kuwa watu katika mayahudi na wanafiki walikuwa wakikutana kupanga njama dhidi ya Mtume na maswahaba wake, ndio ikawashukia Aya hii.

Hili haliko mbali, kwa sababu dhahiri ya Aya inalitilia nguvu, pia mazowea ya hali. Kwani kusengenya na siri ni mazowea ya wanafiki kila wakati na kila mahali.

Vyovyote iwavyo, maana ni kuwa, usihofu ewe Muhammad njama zao kwako na kwa maswahaba wako! Utahofia nini nawe una yakini kwamba Mwenyezi Mungu anajua siri na dhahiri na minong’ono ya wenye kujificha wawe wachache au wengi? Vile vile unajua kuwa atawakusanya siku ya Kiyama na kuwaadhibu kwa yale waliyokuwa wakiyafanya?

Makusudio ya kutaja tatu na tano ni kiasi cha kutoa mfano tu.Hakika Mwenyezi Mungu ni Mjuzi wa kila kitu, hata kutingishika mdomo na kurudia maneno.

Kwani huwaoni wale waliokatazwa kunong’ona, kisha wakayarudia yale waliyokatazwa, na wakanong’onezana juu ya mambo ya dhambi, na ya uadui, na ya kumwasi Mtume?

Hii inaashiria kwamba Mtume(s.a.w. w ) alikuwa amewanasihi wale wenye kujifichaficha na minong’ono kuwa wakome wala wasirudie, lakini hawakukubali, bali walirudia kwa jeuri na inadi. Basi Mwenyezi Mungu akawakaripia kwa tamko la kushangaa alilomwelekezea Mtume wake mtukufu; kama unavyomwambia mwenzako: Unamuona huyu asivyokuwa na adabu?

Na wakikujia hukuamkia sivyo anavyokuamkia Mwenyezi Mungu.

Kuna riwaya kuwa watu katika mayahudi waliingia kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w. w ) wakamwamkia: “Assaamu alayka ya Abalqasim” wakimaanisha mauti yakufikie ewe babake Kasim. Mtume naye akawajibu: “Waalykum!” na juu yenu pia. Ndio ikashuka Aya hii.

Sisi hatuna shaka na usahihi wa riwaya hii, kwa sababu inasadikisha zaidi ukosefu wa adabu wa mayahudi na chuki yao kwa haki na watu wake.

Na husema katika nafsi zao: Mbona Mwenyezi hatuadhibu kwa haya tuyasemayo?

Walifanya hivi kisha wakasema: Lau Muhammad angelikwa Nabii basi Mwenyezi Mungu angelituteremshia adhabu kwa jeuri tuliyomfanyia Nabii wake.

Jahannamu itawatosha; wataingia humo! Ni marejeo mabaya sana.

Msiwe na haraka na hali itakayokuwa, kwani Mwenyezi Mungu (s.w.t) amewaandalia Jahannam ambayo ni marejeo mabaya kabisa na kwamba kesho kuanzia leo ni karibu.

Enyi mlioamini! Mnaponong’onezana msinong’onezane kwa sababu ya mambo ya madhambi, na uadui, na kumuasi Mtume. Bali nong’onezaneni kwa kutenda mema na takua. Na mcheni Mwenyezi Mungu ambaye kwake mtakusanywa.

Watu wengi huwa wanamwamini Mwenyezi Mungu, wakafunga kwa ajili yake na wakaswali kiukweli na haki si kwa uongo wala ria, lakini mara nyingi wanasahau imani hii na wakanong’ona kwa mambo ya dhambi, sawa na wanavyofanya wanafiki na makafiri.

Maneno katika Aya hii yanaelekezwa kwa hawa walioghafilika na imani yao; na Mwenyezi Mungu (s.w.t) akawaamuru wanong’one kwa mambo ya heri, kwani hilo ndio laiki ya waumini; hawanong’onezani kwa shari kama makafiri na wanafiki.

Kama kwamba Aya hii imezishukia baadhi ya dola zinazojionyesha kuwa ni za kiislamu huku zikiwasaidia waisrail na kuwasheheneza aina kwa aina za silaha ili wawaue wanawake na watoto wadogo; wavunje majumba na kuwafukuza wakazi wake kutoka kwenye miji yao. Ni unafiki gani mkub­wa zaidi ya mtu kudai kuwa yeye ni mwislamu anayemwamini Mwenyezi Mungu na siku ya mwisho na huku anasaidiana na maadui wa Mwenyezi Mungu na wa utu; tena anapongeza dhulma na unyanyasaji?

Mwenyezi Mungu (s.w.t) amewakataza waumini kusaidiana na madhalimu hata kama ni kwa neno la siri, na akawaamuru kupambana nao kwa kauli na vitendo kwa siri na kwa jahara.

Kwa hakika minong’ono hiyo inatokana na Shetani ili awahuzunishe walioamini, na wala hatawadhuru chochote ila kwa idhini ya Mwenyezi Mungu.

Makusudio ya minong’ono hapa ni minong’ono ya shari na ya dhambi. Maana ni kuwa shetani anawahadaa wafuasi wake kwa minon’ono miovu kwa kukusudia kuwaudhi waumini na kuwahuzunisha, lakini waumini wako katika ngao madhubuti hayawapati madhara yoyote isipokuwa kwa idhini ya Mwenyezi Mungu.

Basi waumini wamtegemee Mwenyezi Mungu tu katika mambo yao yote wala wasiogope madhara kutoka kwa yoyote au kungojea manufaa isipokuwa kutoka kwake Mwenyezi Mungu Mtukufu tu. Na mwenye kumtegemea shetani atamwongoza kwenye maangamizi.

2

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا إِذَا قِيلَ لَكُمْ تَفَسَّحُوا فِي الْمَجَالِسِ فَافْسَحُوا يَفْسَحِ اللَّـهُ لَكُمْ وَإِذَا قِيلَ انشُزُوا فَانشُزُوا يَرْفَعِ اللَّـهُ الَّذِينَ آمَنُوا مِنكُمْ وَالَّذِينَ أُوتُوا الْعِلْمَ دَرَجَاتٍ وَاللَّـهُ بِمَا تَعْمَلُونَ خَبِيرٌ ﴿١١﴾

11. Enyi mlioamini! Mkiambiwa: fanyeni nafasi katika vikao, basi fanyeni nafasi. Na Mwenyezi Mungu atawafanyia nafasi. Na mki­ambiwa: ondokeni, basi ondokeni. Mwenyezi Mungu atawainua daraja walioamini miongoni mwenu, na waliope­wa ilimu. Na Mwenyezi Mungu kwa mnayoyatenda anazo habari.

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا إِذَا نَاجَيْتُمُ الرَّسُولَ فَقَدِّمُوا بَيْنَ يَدَيْ نَجْوَاكُمْ صَدَقَةً ذَٰلِكَ خَيْرٌ لَّكُمْ وَأَطْهَرُ فَإِن لَّمْ تَجِدُوا فَإِنَّ اللَّـهَ غَفُورٌ رَّحِيمٌ ﴿١٢﴾

12. Enyi mlioamini! Mnapo­nong’onezana na Mtume, basi tangulizeni sadaka kabla ya kunong’ona kwenu. Hiyo ni kheri kwenu na usafi zaidi. Na ikiwa hamkupata cha kutoa, basi Mwenyezi Mungu ni Mwingi wa maghufira, Mwenye kurehemu.

أَأَشْفَقْتُمْ أَن تُقَدِّمُوا بَيْنَ يَدَيْ نَجْوَاكُمْ صَدَقَاتٍ فَإِذْ لَمْ تَفْعَلُوا وَتَابَ اللَّـهُ عَلَيْكُمْ فَأَقِيمُوا الصَّلَاةَ وَآتُوا الزَّكَاةَ وَأَطِيعُوا اللَّـهَ وَرَسُولَهُ وَاللَّـهُ خَبِيرٌ بِمَا تَعْمَلُونَ ﴿١٣﴾

13. Mnachelea kutanguliza hiyo sadaka kabla ya kunong’ona kwenu? Ikiwa hamkufanya hayo, na Mwenyezi Mungu akapokea toba yenu, basi simamisheni Swala, na toeni Zaka, na mtiiini Mwenyezi Mungu na Mtume wake. Na Mwenyezi Mungu ana habari kwa mnayoyatenda.

FANYENI NAFASI MWENYEZI MUNGU ATAWAFANYIA NAFASI

Aya 11 – 13

MAANA

Enyi mlioamini! Mkiambiwa: fanyeni nafasi katika vikao, basi fanyeni nafasi. Na Mwenyezi Mungu atawafanyia nafasi.

Maswahaba walikuwa wakiwahi kwenye vikao vya Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w. w ) na wakipupia kuwa karibu naye. Mara nyingi vikao vilikuwa na msongamano wa watu. Aliyewahi hakuwa akimpa nafasi anayekuja, basi analazimika kurudi au kukalia nyayo zake. Ndio Mwenyezi Mungu (s.w.t) akawafundisha adabu ya kiislamu; Akawaamuru kuwapa nafasi wengine kwenye vikao na akawaahidi kuwapa nafasi Peponi.

Na mkiambiwa: ondokeni, basi ondokeni.

Kwanza Mwenyezi Mungu (s.w.t) aliwaamuru waliokaa wawatengenezee nafasi wengine; kisha akawaamuru kumsikiliza Mtume(s.a.w. w ) akiwataka kuachia nafasi wengine ikiwa nafasi haitoshi.

Kuna riwaya inayosema kuwa Mtume(s.a.w. w ) alikuwa akiwasimamisha baadhi ili wakae wale waliotangulia kwenye mambo mema, na ikawa wengine wanaonyesha kuchukia kwenye nyuso zao. Lakini baada ya kushuka Aya hii walifanya heshima na kuwapisha ndugu zao kwa moyo safi kabla ya kuamuriwa na Mtume(s.a.w. w ) .

Kuna tafsiri nyingine zinazosema kuwa maana ni: mkiambiwa ondokeni kwenda kwenye mambo ya heri basi itikieni. Hili haliko mbali, kwa sababu amri inaenea kwenye maana yote; iwe ni kutoa nafasi, kufanya jihadi au mengineyo.

Ndio! Katika adabu za Qur’an ni mtu kumfanyia nafasi ndugu yake au kumpisha pale alipokaa yeye, lakini sio adabu wala maadili mema kwa yule aliyekuja kumwondoa mahali pake yule aliyekaa.

Mtume(s.a.w. w ) alikuwa akikaa mwisho walipokaa watu, ila ikiwa mwenye kikao atamtaka mtu ampishe ndio anamwitikia, lakini vile vile haitakikani kwa mwenye kikao kumwondoa mtu isipokuwa kwa sababu ya maana; kama vile aliyekaa kukikosea adabu kikao au ikiwa aliyekuja ana shani na daraja mbele ya Mwenyezi Mungu. Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema:

Mwenyezi Mungu atawainua daraja walioamini miongoni mwenu, na waliopewa ilimu. Na Mwenyezi Mungu kwa mnayoyatenda ana habari.

Mwenyezi Mungu anawajua watu bora na anajua daraja za ubora naye anampa kila mwenye fadhila haki yake. Bora zaidi katika watu ni yule aliye zaidi kujichunga na aliyoyaharimisha Mwenyezi Mungu. Ikiwa pamoja na kujichunga hivi ana mwamko na ilimu basi atakuwa juu ya walio juu.

Hakuna mwenye shaka kwamba kumwadhimisha aliyeadhimishwa na Mwenyezi Mungu ni faradhi ya lazima. Kuna Hadith inayosema kuwa Mtume alikuwa akiwatukuza watu wa Badr na kuwatanguliza juu ya wengine. Siku moja waliingia baadhi yao kwenye majilisi yake wakakuta watu wamesongamana kwake wala hakuna yeyote aliyewapisha.

Mtume(s.a.w. w ) akawaambia wale waliokaribu yake: ni nani ambaye si katika watu wa Badr. Simama ewe fulani na wewe ewe fulani, na akawakalisha watu wa Badr.

Riwaya hii inaafikiana na kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: “Mwenyezi Mungu atawainua daraja walioamini miongoni mwenu…”

KUKAA MBELE KWENYE KIKAO

Mimi ninaposoma makala ya gazeti inayofungamana na maudhui ya Aya yoyote katika Qur’an Tukufu huwa ninaiweka kwenye faili maalum, mpaka nikifikia kuifasiri basi ninairudia ile makala na kuitolea ushahidi.

Pia huwa ninaashiria jina la gazeti na tarehe yake, kwa sababu kizazi kipya wanakinaika na magazeti zaidi kuliko rejea nyingine; kwa mfano kama kwenye Juz. 13 (13:5-7) kifungu cha ‘wanaoamini maada na maisha baada ya mauti.’ Juz. 15 (17: 82-85), kfungu cha: ‘Mwenyezi Mungu na ilimu ya chembe hai,’ Juz. 23 (38: 65-88), kifungu cha: Uislamu na msichana wa kiingereza,’ na Juz. 24 (41:37-46) kifungu cha ‘safari ya mwezini.’

Basi siku moja nilisoma mojawapo ya majarida ya wanasiasa wakubwa kuhusu meza ya maelewano kuwa ni nani atakayekaa mbele, ni nani atakayekuwa nyuma na ni ujumbe upi utatangulia kwenye chumba cha mkutano kabla ya mwingine.

Katika mfano alioutoa mwandishi ni ule wa mwaka 1945 baada ya vita ya pili ya dunia: Waliafikiana Churchill, Stalin na Roosevelt kukutana kwa majadiliano ya mapatano mjini Budabest, lakini wakatofautiana kuwa ni nani atakayeingia kwanza kwenye ukumbi wa mkutano. Ubishi huu uliendelea kwa muda kisha suluhisho likawa wakutane kwenye ukumbi wenye milango mitatu ili wote waingie kwa wakati mmoja.

Nimeikumbuka makala hiyo na kuileta hapa ili aone msomaji kuwa Uislamu unaipa kipaumbele ilimu na ikhlasi. Haya ndio maendeleo ya haki na uadilifu kwa maana yake sahihi, lakini kuwatukuza wanaotengeneza mauti, wanaomiliki makombora ya Menotman na CC, na silaha nyingine­zo za maangamizi, hakuna uzito wowote isipokuwa katika sharia ya shetani na maendeleo ya vita na uchokozi.

Enyi mlioamini! Mnaponong’onezana na Mtume, basi tangulizeni sadaka kabla ya kunong’ona kwenu. Hiyo ni kheri kwenu na usafi zaidi. Na ikiwa hamkupata cha kutoa, basi Mwenyezi Mungu ni Mwingi wa maghufira, Mwenye kurehemu.

Sioni tafsiri nzuri zaidi ya Aya hii kuliko ile ya Muqatil bin Hayan, ali­posema: “Matajiri waliwazidi mafukara kwenye vikao vya Mtume(s.a.w. w ) - hii ndio hali yao kila mahali na kila wakati - wakazidisha kum­nong’oneza Mtume mpaka akachukia kukaa kwao sana, ndio Mwenyezi Mungu akaamuru sadaka.

Basi matajiri wakajizuia kutoa na mafukara wakakosa cha kutoa, wakamlilia hali Mtume na kutamani kutoa lau wan­gelikua nacho na kukifikisha kwenye vikao vya Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w. w ) . Hapo daraja ya mafukara ikazidi, mbele ya Mwenyezi

Mungu na daraja ya matajiri ikaanguka.” Katika tafsiri kadhaa ikiwemo Tafsiru ttabari na Tafsiru rrazi imeelezwa kuwa hakuifanyia kazi Aya hii isipokuwa Ali bin Abu Twalib(a.s ) . Alikuwa na dinar moja akaivunja zikawa dirham 10, akawa kila anapotaka kusemezana na Mtume hutoa sadaka dirhamu moja. Kisha hukumu hiyo ikaondolewa kabla ya kuitekeleze mwingine asiyekuwa Ali.

Mwenye Tafsir Ruhulbayan anasema: “Imepokewa kutoka kwa Imran kuwa Yeye amesema: Imepokewa kutoka kwa Abdallah bin Imran kuwa amesema: Ali alikuwa na mambo matatu, lau ningelikuwa na mojawapo kati ya hayo ingelikuwa bora kwangu kuliko wanyama wekundu: Kumuoa Fatima, kupewa bendera siku ya Khaybar na Aya ya mnong’ono.”

Mnachelea ufukara kuwa hamtaweza kutanguliza hiyo sadaka kabla ya kunong’ona kwenu? Ikiwa hamkufanya hayo, na Mwenyezi Mungu akapokea toba yenu, basi simamisheni Swala, na toeni Zaka, na mtiii­ni Mwenyezi Mungu na Mtume wake.

Ilipokuwa uzito kwa matajiri kutoa sadaka kwa kuhofia kuisha mali yao, na Mwenyezi Mungu akalijua hilo, na wakajua kuwa wakati wa Mtume sio wao peke yao tu, ni wakufikisha ujumbe na kupanga mambo ya Waislamu, ndio Mwenyezi Mungu akaruhusu kunong’ona na Mtume bila ya kutoa sadaka na akawasamehe wale wasiotoa, lakini wasizembee swala, Zaka na mengineyo.

Na Mwenyezi Mungu ana habari za mnayoyatenda.

Haufichiki kwake wema wa mwenye kufanya wema na uovu wa mwenye kufanya uovu na atamlipa kila mmoja stahiki yake.

أَلَمْ تَرَ إِلَى الَّذِينَ تَوَلَّوْا قَوْمًا غَضِبَ اللَّـهُ عَلَيْهِم مَّا هُم مِّنكُمْ وَلَا مِنْهُمْ وَيَحْلِفُونَ عَلَى الْكَذِبِ وَهُمْ يَعْلَمُونَ ﴿١٤﴾

14. Huwaoni wale waliofanya urafiki na watu ambao Mwenyezi Mungu amewa­kasirikia? Hao si katika nyinyi, wala si katika wao. Na huapa kwa uwongo, na hali ya kuwa wanajua.

أَعَدَّ اللَّـهُ لَهُمْ عَذَابًا شَدِيدًا إِنَّهُمْ سَاءَ مَا كَانُوا يَعْمَلُونَ ﴿١٥﴾

15. Mwenyezi Mungu amewaan­dalia adhabu kali. Kwa haki­ka waliyokuwa wakiyatenda ni maovu kabisa.

اتَّخَذُوا أَيْمَانَهُمْ جُنَّةً فَصَدُّوا عَن سَبِيلِ اللَّـهِ فَلَهُمْ عَذَابٌ مُّهِينٌ ﴿١٦﴾

16. Wamefanya viapo vyao ni ngao, na wakaipinga Njia ya Mwenyezi Mungu. Basi wata­pata adhabu ifedheheshayo.

لَّن تُغْنِيَ عَنْهُمْ أَمْوَالُهُمْ وَلَا أَوْلَادُهُم مِّنَ اللَّـهِ شَيْئًا أُولَـٰئِكَ أَصْحَابُ النَّارِ هُمْ فِيهَا خَالِدُونَ ﴿١٧﴾

17. Haitawafaa kitu mali yao wala watoto wao kwa Mwenyezi Mungu, na wao ndio watu wa motoni, wao watadumu humo.

يَوْمَ يَبْعَثُهُمُ اللَّـهُ جَمِيعًا فَيَحْلِفُونَ لَهُ كَمَا يَحْلِفُونَ لَكُمْ وَيَحْسَبُونَ أَنَّهُمْ عَلَىٰ شَيْءٍ أَلَا إِنَّهُمْ هُمُ الْكَاذِبُونَ ﴿١٨﴾

18. Siku atakayowafufua Mwenyezi Mungu wote, wamuapie kama wanavyo­waapia nyinyi. Na watadhani kuwa wamepata kitu! Ehe! Kwa hakika hao ndio waon­go.

اسْتَحْوَذَ عَلَيْهِمُ الشَّيْطَانُ فَأَنسَاهُمْ ذِكْرَ اللَّـهِ أُولَـٰئِكَ حِزْبُ الشَّيْطَانِ أَلَا إِنَّ حِزْبَ الشَّيْطَانِ هُمُ الْخَاسِرُونَ ﴿١٩﴾

19. Shetani amewatawala na akawasahaulisha dhikr ya Mwenyezi Mungu. Hao ndio kundi la Shetani. Ehe! hakika kundi la Shetani ndilo lenye kuhasirika.

WAMEFANYA VIAPO VYAO NI NGAO

Aya 14 – 19

MAANA

Huwaoni wale waliofanya urafiki na watu ambao Mwenyezi Mungu amewakasirikia? Hao si katika nyinyi, wala si katika wao. Na huapa kwa uwongo, na hali ya kuwa wanajua.

Maneno yanaelekezwa kwa Mtume(s.a.w.w) . Waliofanya urafikki ni wanafiki, waliokasirikiwa na Mwenyezi Mungu ni mayahudi na nyinyi, ni nyinyi waislamu. Maana ni kuwa hebu niambie ewe Muhammad kuhusu wanafiki! Wamefanya urafiki na mayahudi na wakapanga njama nao dhidi ya waislamu na uislamu; wakiwa na uhakika kuwa wao si waisalamu wala si katika mayahudi, ni vizabizabina, huku hawako wala kule hawako.

Wameapa kwa kukusudia uwongo kuwa ni waislmu na kwamba hawakuse­ma kitu wala kupanga njama na mayahudi. Kwa ajili ya unafiki wao na viapo vyao vya uwongo,Mwenyezi Mungu amewaandalia adhabu kali. Kwa hakika waliyokuwa wakiyatenda ni maovu kabisa . Kila mwenye kudhihirisha kinyume na yaliyo kwenye dhamiri yake basi ni muovu kwa kauli yake na vitndo vyake, kwa sababu amejitoa kwenye dhati yake na hakika yake.

Wamefanya viapo vyao ni ngao, na wakaipinga Njia ya Mwenyezi Mungu. Basi watapata adhabu ifedheheshayo.

Yaani wanafiki wanajaribu kufanya njama zao kwa viapo vya uwongo na kujikinga navyo; huku wakiwahadaa wale wanaotaka uongofu na kuwazuia na malengo yao, lakini Mwenyezi Mungu hafichwi na kinga yoyote wala dhamiri zozote. Basi ameipasua sitara yao duniani, na Akhera watapata adhabu ya kufedhehesha.

Haitawafaa kitu mali yao wala watoto wao kwa Mwenyezi Mungu, na wao ndio watu wa motoni, wao humo watadumu.

Walipata fursa katika maisha ya duniani, lakini wakaichezea, wala hakuna kitu kwa yule mwenye kuvuta muda na kupuuza isipokuwa adhabu. Na si mali wala watoto inayoweza kurudisha yaliyopita.

Imetangulia kwa herufi zake katika Juz. 4 (3:116).

Siku atakayowafufua Mwenyezi Mungu wote, wamuapie kama wanavyowaapia nyinyi. Na watadhani kuwa wamepata kitu! Ehe! Kwa hakika hao ndio waongo.

Siku ya Kiyama, waja watakuwa na hali mbalimbali; kuna wengine watahurusiwa kuzungumza. Basi Mwenyezi Mungu atakapowapa fursa ya kuzungumza, wakosefu, watamuapia kwa uwongo, kama walivyokuwa wakimwapia Nabii na waislamu duniani; wakiamini kuwa viapo vyao vitawakinga na adhabu. Vipi iwe hivyo na hali Mwenyezi Mungu anajua kuwa wao ni waongo katika imani zao na itikadi zao?

Umetangulia mfano wake katika Juz. 7 (6:22).

Shetani amewatawala na akawasahaulisha dhikr ya Mwenyezi Mungu.

Shetani wa matamanio aliwaita kwenye upotevu na ufisadi nao wakamwitikia, basi wakapofuka na uwongofu.

Hao ndio kundi la Shetani. Ehe! hakika kundi la Shetani ndilo lenye kuhasirika.

Kwa sababu, vyovyote vile iwavyo, mwenye kumfanya shetani ni kiongozi wake, atamwongoza kwenye kila uovu na maangamizi, iwe kesho au kesho kutwa; hata kama atajisheheni mabomu na makombora.

إِنَّ الَّذِينَ يُحَادُّونَ اللَّـهَ وَرَسُولَهُ أُولَـٰئِكَ فِي الْأَذَلِّينَ ﴿٢٠﴾

20. Hakika wanaompinga Mwenyezi Mungu na Mtume wake, hao ndio miongoni mwa madhalili wa mwisho.

كَتَبَ اللَّـهُ لَأَغْلِبَنَّ أَنَا وَرُسُلِي إِنَّ اللَّـهَ قَوِيٌّ عَزِيزٌ ﴿٢١﴾

21. Mwenyezi Mungu ameandika: Hapana shaka Mimi na Mitume wangu tutashinda. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye nguvu, Mwenye kushinda.

لَّا تَجِدُ قَوْمًا يُؤْمِنُونَ بِاللَّـهِ وَالْيَوْمِ الْآخِرِ يُوَادُّونَ مَنْ حَادَّ اللَّـهَ وَرَسُولَهُ وَلَوْ كَانُوا آبَاءَهُمْ أَوْ أَبْنَاءَهُمْ أَوْ إِخْوَانَهُمْ أَوْ عَشِيرَتَهُمْ أُولَـٰئِكَ كَتَبَ فِي قُلُوبِهِمُ الْإِيمَانَ وَأَيَّدَهُم بِرُوحٍ مِّنْهُ وَيُدْخِلُهُمْ جَنَّاتٍ تَجْرِي مِن تَحْتِهَا الْأَنْهَارُ خَالِدِينَ فِيهَا رَضِيَ اللَّـهُ عَنْهُمْ وَرَضُوا عَنْهُ أُولَـٰئِكَ حِزْبُ اللَّـهِ أَلَا إِنَّ حِزْبَ اللَّـهِ هُمُ الْمُفْلِحُونَ ﴿٢٢﴾

22. Hupati watu wanaomwamini Mwenyezi Mungu na Siku ya Mwisho kuwa wanapendana na wanaompinga Mwenyezi Mungu na Mtume wake, hata wakiwa ni baba zao, au wato­to wao, au ndugu zao, au jamaa zao. Hao ameandika katika nyoyo zao Imani, na amewapa nguvu kwa Roho itokayo kwake. Na atawaingiza katika mabustani yapiti­wayo na mito chini yake. Humo watadumu. Mwenyezi Mungu awe radhi nao, na wao wawe radhi naye. Hao ndio kundi la Mwenyezi Mungu. Ehe! Hakika kundi la Mwenyezi Mungu ndilo lenye kufanikiwa.

BILA SHAKA NITASHINDA MIMI NA MITUME WANGU

Aya 20 – 22

MAANA

Hakika wanaompinga Mwenyezi Mungu na Mtume wake, hao ndio miongoni mwa madhalili wa mwisho.

Aya hii ina mshabaha wa jibu la swali la kukisiwa, kwamba maadui wa Mwenyezi Mungu wanaishi wakiwa na nguvu ya maandalizi na idadi, wakiendelea kuwatesa watu wa Mwenyezi Mungu kwa mauaji na kuwa­torosha, vipi Mwenyezi Mungu anawapa muda na kuwapa nguvu?

Aya inajibu kuwa washari ndio viumbe dhalili zaidi kuanzia mwanzo hadi mwisho, kwa sababu mwisho wao ni hizaya na udhalili duniani na Akhera. Hapa duniani ni kuwa Mwenyezi Mungu anawaadhibu kwa mikono ya waliowema:

قَاتِلُوهُمْ يُعَذِّبْهُمُ اللَّـهُ بِأَيْدِيكُمْ وَيُخْزِهِمْ وَيَنصُرْكُمْ عَلَيْهِمْ وَيَشْفِ صُدُورَ قَوْمٍ مُّؤْمِنِينَ ﴿١٤﴾

“Piganeni nao, Mwenyezi Mungu awaadhibu kwa mikono yenu, na awa­fedheheshe, na awanusuru muwashinde na avipoze vifua vya kaumu ya waumin.” Juz. 10 (9:14).

Ama adhabu ya Akhera hiyo ni kali na ni kubwa zaidi.

Mwenyezi Mungu ameandika: Hapana shaka Mimi na Mitume wangu tutashinda. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye nguvu, Mwenye kushinda.

Ushindi utakuwa Akhera, na vile vile utakuwa duniani kwa upanga, adhabu ya kutoka mbinguni, hoja na dalili au kwa kudumu utajo.

Tazama Juz. 17 (38-41) kifungu cha: “Mwenyezi Mungu huwakinga walioamini.” Vile vile Juz. 26 (47:7).

Hupati watu wanaomwamini Mwenyezi Mungu na Siku ya Mwisho kuwa wanapendana na wanaompinga Mwenyezi Mungu na Mtume wake, hata wakiwa ni baba zao, au watoto wao, au ndugu zao, au jamaa zao.

Haiwezekani kabisa imani ichanganyike na mahaba ya makafiri. Itakuwaje hivyo na hali Mwenyezi Mungu ndiye Aliyesema:

مَّا جَعَلَ اللَّـهُ لِرَجُلٍ مِّن قَلْبَيْنِ فِي جَوْفِهِ ﴿٤﴾

“Mwenyezi Mungu hakumwekea mwanamume nyoyo mbili ndani yake.” Juz. 21 (33:4).

Kuna kauli mashuhuri kutoka kwa Imam Ali(a.s ) kuwa rafiki wa adui ni adui. Pia akasema: “Tulikuwa pamoja na Mtume(s.a.w.w) mapigano yakiendela kwa mababa, watoto, ndugu na jamaa. Kila msiba na shida haukutuzidisha isipokuwa imani na kuendelea kwenye haki na kusalimu amri.” Hayo tumeyazungumzia kwa ufafanuzi zaidi kwenye Juz.4 (3:28).

Hao ameandika katika nyoyo zao Imani, na amewapa nguvu kwa Roho itokayo kwake.

‘Hao’ ni ni wale ambao imani yao haiathiriki hata kwa mababa na mama zao. Maana ni kuwa Mwenyezi Mungu amethibitishia imani katika nyoyo za wenye ikhlasi na akawapa nguvu kwa hoja: “Mwenyezi Mungu huwaimarisha wale walioamini kwa kauli thabiti katika maisha ya dunia na katika Akhera.” Juz. 13 (14:27).

Na atawaingiza katika Mabustani yapitiwayo na mito chini yake. Humo watadumu. Mwenyezi Mungu awe radhi nao, na wao wawe radhi naye.

Maana ya Mwenyezi Mungu kumridhia mja wake ni kumpa fadhila zake, na maana ya mja kumridhia Mola wake ni kuridhia aliyompa. Ibn Al-ara­biy, anasema katika Futuhat: “Mwenyezi Mungu huridhia amali chache ya mja wake na wao wanaridhia thawabu chache walizopata kutoka kwa Mola wao, kwani kadiri Mwenyezi Mungu anavyotoa ni vichache kulingana na vilivyoko kwake.”

Lakini hivi alivyoviita vichache Ibn al-arabiy, ni vichache kwa Mwenyezi Mungu Mtufu na ni vingi kwa waja. Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema: “Ili amzidishie ziada nyingi.” Juz. 2 (2:245).

Hao ndio kundi la Mwenyezi Mungu. Ehe! Hakika Kundi la Mwenyezi Mungu ndilo lenye kufanikiwa.

Aya hii ni mkabala wa Aya 19 ya Sura hii tuliyo nayo inayosema: “Hao ndio kundi la Shetani. Ehe! hakika kundi la Shetani ndilo lenye kukhasirika.”

Kwa ufupi ni kuwa mtu kadiri atakavyokuwa na uwezo, lakini hawezi kuchanganya kumridhisha Mwenyezi Mungu na kuwaridhisha maadui wa Mwenyezi Mungu Mtukufu. Akiwaridhisha atakuwa amemghadhabisha Mwenyezi Mungu na akimridhisha Mungu atakuwa amewaghadhibisha maadui. Wao hawaridhii isipokuwa yule aliye katika hali yao, kwa ushahi­di wa kauli yake Mwenyezi Mungu Mtufu:

وَلَن تَرْضَىٰ عَنكَ الْيَهُودُ وَلَا النَّصَارَىٰ حَتَّىٰ تَتَّبِعَ مِلَّتَهُمْ ﴿١٢٠﴾

“Hawatakuwa radhi nawe Mayahudi wala Manaswara mpaka ufuate mila yao.” Juz. 1 (2:120).

Katika Hadith Mtume(s.a.w.w) anasema:“Ewe Mwenyezi Mungu usini­jaalie muovu wala fasiki kwangu, kwani nimekuta katika yale uliyatolea wahyi kuwa: “Hupati watu wanaomwamini Mwenyezi Mungu na Siku ya Mwisho kuwa wanapendana na wanaompinga Mwenyezi Mungu na Mtume wake.”

MWISHO WA SURA YA HAMSINI NA NANE: AL–MUJADALA