TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE Juzuu 24

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE0%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: Qurani tukufu

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE

Mwandishi: Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya
: HASANI MWALUPA
Kundi:

Matembeleo: 26044
Pakua: 3253


Maelezo zaidi:

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 30 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 26044 / Pakua: 3253
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE Juzuu 24

Mwandishi:
Swahili

3

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE

Sura Ya Hamsini Na Tisa: Surat Al-Hashr. Imeshuka Madina. Ina Aya 24.

بِسْمِ اللَّهِ الرَّحْمَٰنِ الرَّحِيمِ

Kwa jina la Mwenyezi Mungu Mwingi wa rehema, Mwenye kurehemu.

سَبَّحَ لِلَّـهِ مَا فِي السَّمَاوَاتِ وَمَا فِي الْأَرْضِ وَهُوَ الْعَزِيزُ الْحَكِيمُ ﴿١﴾

1. Vinamsabihi Mwenyezi Mungu vilivyo katika mbingu na vilivyo katika ardhi. Na Yeye ndiye Mwenye nguvu, Mwenye hikima.

هُوَ الَّذِي أَخْرَجَ الَّذِينَ كَفَرُوا مِنْ أَهْلِ الْكِتَابِ مِن دِيَارِهِمْ لِأَوَّلِ الْحَشْرِ مَا ظَنَنتُمْ أَن يَخْرُجُوا وَظَنُّوا أَنَّهُم مَّانِعَتُهُمْ حُصُونُهُم مِّنَ اللَّـهِ فَأَتَاهُمُ اللَّـهُ مِنْ حَيْثُ لَمْ يَحْتَسِبُوا وَقَذَفَ فِي قُلُوبِهِمُ الرُّعْبَ يُخْرِبُونَ بُيُوتَهُم بِأَيْدِيهِمْ وَأَيْدِي الْمُؤْمِنِينَ فَاعْتَبِرُوا يَا أُولِي الْأَبْصَارِ ﴿٢﴾

2. Yeye ndiye Aliewatoa walioku­furu miongoni mwa Watu wa Kitabu katika nyumba zao wakati wa mkusanyiko wa kwanza. Hamkudhani kuwa watatoka, nao walidhani kuwa ngome zao zitawalinda na Mwenyezi Mungu. Lakini Mwenyezi Mungu aliwafikia kwa mahali wasipopatazamia, na akatia woga katika nyoyo zao. Wakawa wanazibomoa nyumba zao kwa mikono yao na mikono ya Waumini. Basi zingatieni enyi wenye busara!

وَلَوْلَا أَن كَتَبَ اللَّـهُ عَلَيْهِمُ الْجَلَاءَ لَعَذَّبَهُمْ فِي الدُّنْيَا وَلَهُمْ فِي الْآخِرَةِ عَذَابُ النَّارِ ﴿٣﴾

3. Na lau kuwa Mwenyezi Mungu asingeliwaandikia uhamisho, angeliwaadhibu katika dunia. Na katika Akhera watapata adhabu ya Moto.

ذَٰلِكَ بِأَنَّهُمْ شَاقُّوا اللَّـهَ وَرَسُولَهُ وَمَن يُشَاقِّ اللَّـهَ فَإِنَّ اللَّـهَ شَدِيدُ الْعِقَابِ ﴿٤﴾

4. Hayo ni kwa sababu walimpin­ga Mwenyezi Mungu na Mtume wake. Na mwenye kumpinga Mwenyezi Mungu, basi hakika Mwenyezi Mungu ni Mkali wa kuadhibu.

مَا قَطَعْتُم مِّن لِّينَةٍ أَوْ تَرَكْتُمُوهَا قَائِمَةً عَلَىٰ أُصُولِهَا فَبِإِذْنِ اللَّـهِ وَلِيُخْزِيَ الْفَاسِقِينَ ﴿٥﴾

5. Mtende wowote mlioukata au mliouacha umesimama vile vile juu ya mashina yake, basi ni kwa idhini ya Mwenyezi Mungu, na kwa kuwahizi mafasiki.

VINAMSABIHI MWENEYEZI MUNGU

Aya 1 – 5

KISA CHA BANI NADHIR KWA UFUPI

Aya hizi zinahusiana na ushindi wa Mtume(s.a.w.w) dhidi ya mayahudi wa Bani Nadhir. Hawa walikuwa wakiishi viungani mwa Madina. Mtume(s.a.w.w) alipohamia huko, aliwekeana nao mkataba wa amani. Waislamu walipowashinda Makuraishi vita vya Badr, Bani Nadhir walifurahi sana, lakini waliposhindwa kwenye vita vya Uhud walivunja makataba na waka­panga njama za kummaliza Mtume na kiongozi wao, Kaa’b bin Ashraf akaungana na Abu Sufyan dhidi ya Nabii(s.a.w.w) .

Inasemekana kuwa Kaa’b alimshambulia Mtume kwa mashairi, Mtume akamwamuru mmoja wa maswahaba zake kumuua. Kisha Mtume(s.a.w.w) akawaendea Bani Nadhir na akawaamuru kutoka Madina, lakini wanafiki wakiongozwa na Abdallah bin Ubayya, waliwatumia ujumbe kuwa msikubali, sisi tuko pamoja nanyi. Basi wakawa na matumaini na wakashikilia kupigana. Hapo Mtume akawahusuru kwa muda wa siku 21, kama yanavyosema baadhi ya mapokezi.

Mtume(s.a.w.w) aliamuru kukatwa baadhi ya mitende yao. Hakuna yeyote katika wanafiki aliyejaribu kuwasaidia. Basi wakalazimika kusalimu amri, na Mtume akasuluhishana nao kuwa watoke Madina; kila watu watatu wachukue ngamia mmoja atakayewabebea wanachotaka. Basi wakakubali na wakatoka Madina kabisa.

Sura hii imewashukia wao. Ibn Abas alikuwa akiita Sura hii Sura ya Bani Nadhir.

MAANA

Vinamsabihi Mwenyezi Mungu vilivyo katika mbingu na vilivyo kati­ka ardhi. Na Yeye ndiye Mwenye nguvu, Mwenye hikima.

Vitu vyote vilivyoko vinamsabihi (vinamtakasa) na kutukuza uweza wake Mwenyezi Mungu na hekima yake, kwa lugha ya maneno na lugha ya hali. Umetangulia mfano wake katika Juz. 27 (57:1).

Yeye ndiye Aliyewatoa waliokufuru miongoni mwa Watu wa Kitabu katika nyumba zao wakati wa mkusanyiko wa kwanza.

Makusudio ya waliokufuru hapa ni Bani Nadhir. Wametofautiana wafasiri kuhusu mkusanyiko wa kwanza. Razi anasema: “Ibn Abbas na wafasiri wengi wamesema kuwa maana ya mkusanyiko wa kwanza ni kuwa hiyo ilikuwa ni mara ya kwanza kwa watu wa Kitab kutolewa Bara Arabu. Kabla yake walikuwa na nguvu… Hili haliko mbali kwa sababu kutolewa kwa pili kulitokea kwa khalifa wa pili.

Maana ni kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) aliwatoa Bani Nadhir kupitia mikononi mwa waislamu. Na hii ilikuwa ni mara ya kwanza kutolewa watu wa Kitabu huko. Na sababu ya kutolewa kwao ni hiyana yao na kuvunja kwao mapatano ya amani waliyowekeana na Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) wao wenyewe.

Unaweza kuuliza : Kwanini Mwenyezi Mungu aliwaadhibu kwa kuwatoa na kuchukua mali yao na kuna aina nyingine za kuwaadhibu?

Jibu : Aliwachukulia kwa sharia ya dini yao. Tawrat yao inasema: “Utakaposongea karibu ya mji kwenda kupigana juu yake, ndipo utakapowapigia ukelele wa amani.

Itakuwa utakapokujibu kwa amani, na kukufungulia, ndipo watu wote watakaoonekana humo, watafanya kazi ya shoka, na kukutumikia. Na kama hautaki kufanya amani nawe, lakini utafanya vita juu yako, ndipo uhusuru; na Bwana, Mungu wako, autiapo mkononi mwako, mpige kila mume aliyemo kwa makali ya upanga; lakini wanawake na watoto na wanyama wa mji, na vilivyo mjini vyote, navyo ni nyara zake zote, uvitwae viwe mateka; nawe utakula nyara za adui zako alizokupa Bwana, Mungu wako” (Kumbukumbu 20:10 -14).

Hakuna mwenye shaka kwamba mwenye kufuata dini au misingi hana budi kufuata hukumu zake zote na kuzitekeleza yeye mwenyewe kabla ya kutekelezea mwenginewe. Tena Nabii(s.a.w.w) aliwahurumia Bani Nadhir, kwa sababu hakuwaua wanaume wao wala kuwateka wanawake na watoto; kama ilivyo nukuu ya Tawrat yao.

Hayo tumeyazungumzia kwa ufafanuzi zaidi katika Juz. 21 (33: 16-20), kifungu cha ‘Je, Muhammad aliwadhulumu Bani Quraydha?’

Hamkudhani kuwa watatoka, nao walidhani kuwa ngome zao zitawalinda na Mwenyezi Mungu.

Yaani waislamu hawakutegemea kabisa kuwa Bani Nadhir watatoka majumbani mwao na kuwaachia maadui zao waislamu, kutokana na inadi yao na nguvu walizokuwa nazo kwa uwezo na idadi yao.

Vile vile Bani Nadhir walikuwa wakijiamini kuwa wana nguvu na uwezo kuwa ni ngome isiyoingiliwa na mkono wowote. Lakini ulikuwa ni uwezo na ngome ya khiyana, haiwezi kumlinda mwenye kuikimbilia.

PROPAGANDA ZA UPOTOFU NA WAKATI MNASABA

Lakini Mwenyezi Mungu aliwafikia kwa mahali wasipopatazamia, na akatia woga katika nyoyo zao.

Walidhani kuwa ngome zao zitawalinda, lakini Mwenyezi Mungu akatia hofu kwenye nyoyo zao baada ya kumjaza haiba Mtume(s.a.w.w) na jeshi lake. Basi ngome zao zikayayuka, kwa sababu nyoyo ndio msingi wa nguvu zote.

Ndio maana waovu na wafanyibiashara wa silaha wanafanya bidii sana kwenye vita vya nafsi na kutafuta nyenzo na pesa, lakini wame­sahau au wamejitia kusahau kuwa hakuna njia ya kuufikia moyo isipokuwa haki, kheri na hisani. Ikiwa propaganda za upotevu zitapata waungaji mkono basi ni kwa muda, kisha zinafichuka; hata kama muda utakuwa mrefu.

Aliulizwa Charles Mwigizaji maarufu wa tamthilia kuhusu mambo ya maisha: Mtu anahitaji nini ili aweze kutengeneza njia yake ya maisha? Akasema: “Jambo muhimu ni kujua wakati mnasaba.” Nasi tunamwambia Charles: “Ndio hakuna budi ya wakati, lakini ni lazima uwe unanasibiana na masilahi ya kheri sio ya shari, na ya haki sio ya batili. Kwa sababu shari inaondoka pamoja na watu wake, hata kama ni kuchelewa kwa kiasi gani.

Wakawa wanazibomoa nyumba zao kwa mikono yao na mikono ya Waumini.

Badhi ya wafasiri wamesema kuwa makusudio ya kubomoa nyumba ni kuziacha na kwa mikono yao ni kuwa wao ndio sababu ya kuondoka kwao; pale walipovunja maelewano na Mtume. Mikono ya waumini ni ishara ya kuwa waislamu ndio waliowatoa Bani Nadhir majumbani mwao.

Wafasiri wengine wakasema kuwa Bani Nadhir waliziharibu hasa nyumba zao ili zisibakie salama mikononi mwa waislamu, na kwamba waislamu walizipondaponda ngome za mayahudi ili wapate kuwafikia. Tafsiri hii iko karibu na maana na inatiwa nguvu na dhahiri ya Aya; wala haipingani na ile ya kwanza, bali ni natija ya kuondoka mji.

Basi zingatieni enyi wenye busara!

Kuzingatia kitu ni kukirudisha kwenye mtazamo na kukihukumu kwa mfano wake. Mwenyezi Mungu aliwatoa Bani Nadhir majumbani mwao yakiwa ni malipo ya hiyana yao. Basi mwenye akili anatakikana kupata somo na ajiepushe na hiyana na njama, ili yasimfike yaliyowafika.

Na lau kuwa Mwenyezi Mungu asingeliwaandikia uhamisho, angeli­waadhibu katika dunia. Na katika Akhera watapata adhabu ya Moto.

Mwenyezi Mungu amewaadhibu duniani kwa kuwahamisha kutoka majumbani mwao na lau si hivyo angeliwaadhibu kwa kuwaua; kama walivyofanywa Bani Quraydha. Na hawataepuka adhabu ya Moto.

Hayo ni kwa sababu walimpinga Mwenyezi Mungu na Mtume wake.

Walistahili adhabu ya dunia na Akhera, kwa sababu wao walimhalifu Mwenyezi Mungu, wakipituka mipaka yake, na kumwekea uadui Mtume wake.

Na mwenye kumpinga Mwenyezi Mungu, basi hakika Mwenyezi Mungu ni Mkali wa kuadhibu.

Hili ni onyo na kiaga kwa kila jabari mwenye kiburi.

Mtende wowote mlioukata au mliouacha umesimama vile vile juu ya mashina yake, basi ni kwa idhini ya Mwenyezi Mungu, na kwa kuwahizi mafasiki.

Mtume(s.a.w.w) alikuwa ameamrisha kukatwa baadhi ya mitende ya Bani Nadhir ili kuwakasirisha kwa hilo. Baadhi wakadhani kuwa hiyo ni aina ya uharibifu. Ndio Mwenyezi Mungu akabainisha kwamba kila liliotukia kati­ka kukatwa mitende au kuachwa ni kwa amri ya Mwenyezi Mungu na wala haitoki kwa Mtume(s.a.w.w) , na lengo ni kuwakasirisha makafiri kwa kuikata na pia kuwakasirisha kwa ile ilioachwa kwa vile watanufaika nayo wale wanaowaona ni maadui zao.

Ieleweke kuwa kukata miti na mengineyo wakati wa vita haifai kuchukuli­wa ni msingi maalum; inaweza kuwa ni wajibu na inaweza kuwa ni hara-mu, kulingana na masilahi ya kumpiga adui; sawa na yanavyovunjwa majumba kwa ajili ya kupitisha barabara, siku ambazo si za vita.

وَمَا أَفَاءَ اللَّـهُ عَلَىٰ رَسُولِهِ مِنْهُمْ فَمَا أَوْجَفْتُمْ عَلَيْهِ مِنْ خَيْلٍ وَلَا رِكَابٍ وَلَـٰكِنَّ اللَّـهَ يُسَلِّطُ رُسُلَهُ عَلَىٰ مَن يَشَاءُ وَاللَّـهُ عَلَىٰ كُلِّ شَيْءٍ قَدِيرٌ ﴿٦﴾

6. Na Aliyoleta Mwenyezi Mungu kwa Mtume wake kutoka kwao hamkuyaendea kwa farasi wala ngamia. Lakini Mwenyezi Mungu huwapa mamlaka Mitume wake juu ya wowote awatakao. Na Mwenyezi Mungu ni Muweza juu ya kila kitu.

مَّا أَفَاءَ اللَّـهُ عَلَىٰ رَسُولِهِ مِنْ أَهْلِ الْقُرَىٰ فَلِلَّـهِ وَلِلرَّسُولِ وَلِذِي الْقُرْبَىٰ وَالْيَتَامَىٰ وَالْمَسَاكِينِ وَابْنِ السَّبِيلِ كَيْ لَا يَكُونَ دُولَةً بَيْنَ الْأَغْنِيَاءِ مِنكُمْ وَمَا آتَاكُمُ الرَّسُولُ فَخُذُوهُ وَمَا نَهَاكُمْ عَنْهُ فَانتَهُوا وَاتَّقُوا اللَّـهَ إِنَّ اللَّـهَ شَدِيدُ الْعِقَابِ ﴿٧﴾

7. Aliyoleta Mwenyezi Mungu kwa Mtume wake kutoka kwa watu vijijini ni kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, na kwa ajili ya Mtume, na jamaa, na maya­tima, na masikini, na mwananjia, Ili yasiwe yakizunguka baina ya matajiri miongoni mwenu. Na anachowapa Mtume kichukueni, na ana­chowakataza jiepusheni nacho. Na mcheni Mwenyezi Mungu. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mkali wa kuadhibu.

لِلْفُقَرَاءِ الْمُهَاجِرِينَ الَّذِينَ أُخْرِجُوا مِن دِيَارِهِمْ وَأَمْوَالِهِمْ يَبْتَغُونَ فَضْلًا مِّنَ اللَّـهِ وَرِضْوَانًا وَيَنصُرُونَ اللَّـهَ وَرَسُولَهُ أُولَـٰئِكَ هُمُ الصَّادِقُونَ ﴿٨﴾

8. Wapewe mafukara wahajiri waliotolewa majumbani mwao na mali yao kwa ajili ya kutafuta fadhila kutoka kwa Mwenyezi Mungu na radhi zake, na wanamsaidia Mwenyezi Mungu na Mtume wake. Hao ndio wa kweli.

MALI ISIZUNGUKE KWA MATAJIRI

Aya 6–8

MAANA

Na Aliyoleta Mwenyezi Mungu kwa Mtume wake kutoka kwao hamkuyaendea kwa farasi wala ngamia.

Neno ‘Aliyoleta’ tumelifasiri kutokana na neno la kiarabu Fay’i ambalo ki lugha ya kiarabu lina maana ya kurejesha. Fay’i katika sharia ya kiislamu ni mali waliyoipata waislamu kutoka kwa makafiri bila ya vita. Na ghani­ma (ngawira) ni mali iliyopatikana kwa vita.

Vyovyote iwavyo ni kuwa Aya tuliyo nayo inahusika na mali ya Bani Nadhir. Kwa hiyo maana yanakuwa, mali ya Bani Nadhir ameijaalia ni nyara kwa Mtume wake kuifanyia anavyotaka, waislamu hawana chao hapo kwa vile hawakuitolea jasho lolote.

Lakini Mwenyezi Mungu huwapa mamlaka Mitume wake juu ya wowote awatakao.

Miongoni mwa mamlaka hayo ni kuwa Mwenyezi Mungu Mtukufu alitia hofu kwenye nyoyo za Bani Nadhir kutoka kwa Mtume(s.a.w.w) ili wasalimu amri yake wakiwa dhalili, bila ya vita.

Na Mwenyezi Mungu ni Muweza juu ya kila kitu.

Miongoni mwa hayo ni kudhalilika watu wenye nguvu, ngome na idadi, mbele ya mtumwa miongoni mwa watumwa wa Mwenyezi Mungu.

Aliyoleta Mwenyezi Mungu kwa Mtume wake kutoka kwa watu vijijini kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, na kwa ajili ya Mtume, na jamaa, na mayatima, na masikini, na mwananjia.

Makusudio ya watu wa vijiji hapa ni makafiri wengine wasiokuwa Bani Nadhir. Maana ni kuwa mali ya fay’i isiyokuwa ya Bani Nadhir ni ya Mwenyezi Mungu na Mtume. Mwananjia ni msafiri aliyekatikiwa njiani na kushindwa kurudi kwa watu wake.

Kimsingi ni kuwa mali ya Mwenyezi Mungu ni ya Mtume(s.a.w.w) . Wameafikiana kwa kauli moja, isipokuwa kidogo, kwamba makusudio ya jamaa ni jamaa wa Mtume(s.a.w.w) katika Bani Hashim. Ama kuhusu may­atima, masikini na mwananjia, Shia Imamiya wamesema kuwa wanahusi­ka wa Bani Hashim tu. Wengine wamesema ni yeyote awe Hashim au mwinginewe [1] .

Tumeyazungumzia hayo kwa ufafanuzi zaidi katika Juz. 10 (8:41).

Ili yasiwe yakizunguka baina ya matajiri miongoni mwenu.

Uislamu ni dini ya Mwenyezi Mungu kwa ajili ya watu, inachunga masi­lahi ya wote bila ya kuwabagua. Hautatui tatizo la mtu kwa gharama ya mwingine, wala haumkandamizi mtu ili kumnufaisha mwingine. Wote mbele ya uislamu ni sawasawa.

Haya yanajitokeza kwenye hukumu zake na misingi yake. Miongoni mwa misingi hiyo ni kuwa mali isizunguke kwa matajiri tu. Hiyo ni pamoja na kukataza riba, ghushi na unyonyaji.

Ieleweke kwamba hii haifahamishi kwa karibu wala umbali kuwa uislamu unakubaliana na siasa ya ujamaa au haukubali nayo. Ieleweke tu kuwa uis­lamu katika hukumu zake zote kunajengeka fikra ya uadilifu na usawa na unakubaliana na kila lenye heri ya watu na manufaa yao. Hili ni jambo jingine na kutaifisha mali za watu kuwa mali za uma ni jambo jingine.

Tazama Juz. 4 (3:180-182), kifungu cha: ‘Matajairi ni mawakala sio wenyewe.’

Na anachowapa Mtume kichukueni, na anachowakataza jiepusheni nacho. Na mcheni Mwenyezi Mungu. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mkali wa kuadhibu.

Aya hii imeunganisha baina ya kauli ya Mwenyezi Mungu na Mtume wake na ikawajibisha kuzisikiliza kauli zote mbili, kwa sababu kauli ya Mtume inatokana na wahyi kutoka kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu:

وَمَا يَنطِقُ عَنِ الْهَوَىٰ ﴿٣﴾ إِنْ هُوَ إِلَّا وَحْيٌ يُوحَىٰ ﴿٤﴾

“Wala hatamki kwa matamanio. Hayakuwa haya ila ni wahyi uliotolewa.” Juz. 27 (53:3-4).

Mwenyezi Mungu amesema katika Aya kadhaa: “Mtiini Mwenyezi Mungu na Mtume.”

Akasema tena:

وَمَن يَعْصِ اللَّـهَ وَرَسُولَهُ فَقَدْ ضَلَّ ضَلَالًا مُّبِينًا ﴿٣٦﴾

“Na yeyote mwenye kumwasi Mwenyezi Mungu na Mtume wake, basi amepotea upotevu ulio wazi.” Juz. 22 (33:36).

Zimekuja Hadith mutawatir kwamba Mtume hakuona ndoto yoyote ila ina­jitokeza kama asubuhi. Waislamu wameafikiana kwa kauli moja kuwa hakuna wahyi wala sharia au Ijtihadi baada ya Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) ila ikiwa kauli ya mujtahidi inatokana na sharia ya Mwenyezi Mungu na Mtume wake.

Tazama Juz. 22 (33: 36-40) kifungu cha: ‘kwani utume uliishia kwa Muhammad?’ na Juz. 27 (56: 75-96), kifungu cha ‘Uislamu na wanafikra wakuu wa Ulaya.’

Wapewe mafukara wahajiri waliotolewa majumbani mwao na mali yao kwa ajili ya kutafuta fadhila kutoka kwa Mwenyezi Mungu na radhi zake, na wanamsaidia Mwenyezi Mungu na Mtume wake.

Makusudio ya wahajiri hapa ni wale waliohama na Mtume kutoka Makka kwenda Madina kwa kutaka radhi za Mwenyezi Mungu na thawabu zake na katika kuusaidia Uislamu na kupigana jihadi katika njia yake. Hawa ndio waliofaa zaidi kupewa zaka kwa kutangulia kwao na juhudi yao na pia kuwa na haja nayo.

Anasema Tabari akinukuu kutoka kwa Qatada: “Wahajiri hawa waliacha majumba yao, mali na familia kwa kumpenda Mwenyezi Mungu na Mtume wake.

Wakachagua Uislamu pamoja na shida zake. Hali ilifikia mtu anafunga jiwe tumboni ili kuuzuia mgongo wake na njaa na kuchim­ba shimo wakati wa kipupwe kuwa ndio blanketi ya kujifunika.

Sijaona wasifu wa maswahaba uliokuwa fasaha zaidi kuliko aliousema Imam Zaynul-abidin(a.s) akiwa anawaombea Mwenyezi Mungu (s.w.t) awatakabalie matendo yao; kwa kusema:

“Ewe Mola! Hasa maswahaba wa Muhammad ambao walikuwa na usuhuba mzuri, wakawa na majaribu mema katika kumsaidia kwake. Wakamwitikia alipowaeleza hoja ya ujumbe wake. Wakapigana na mababa zao na watoto wao ili kuuthibisha unabii wake na wakashinda kupitia kwake. Waliozingirwa na mapenzi wakitarajia biashara isiyo na hasara kwa ajili ya kumpenda kwake.

Wakatengwa na jamaa zao waliposhikamana na kamba yake. Udugu ulikwisha walipotulia chini ya kivuli cha udugu wake. Basi ewe Mola usiwasahu kwa yale waliyoyaacha kwa ajili yako. Na uwa­ ridhie kwa radhi zako.”

Hao ndio wa kweli katika imani na jihadi yao, kwa kauli na vitendo.

4

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE

وَالَّذِينَ تَبَوَّءُوا الدَّارَ وَالْإِيمَانَ مِن قَبْلِهِمْ يُحِبُّونَ مَنْ هَاجَرَ إِلَيْهِمْ وَلَا يَجِدُونَ فِي صُدُورِهِمْ حَاجَةً مِّمَّا أُوتُوا وَيُؤْثِرُونَ عَلَىٰ أَنفُسِهِمْ وَلَوْ كَانَ بِهِمْ خَصَاصَةٌ وَمَن يُوقَ شُحَّ نَفْسِهِ فَأُولَـٰئِكَ هُمُ الْمُفْلِحُونَ ﴿٩﴾

9. Na waliofanya maskani na imani yao kabla yao, wanawapenda waliohamia kwao wala hawapati dhiki kati­ka vifua vyao kwa walivyope­wa, na wanawapendelea kuliko nafsi zao, ingawa wao wenyewe ni wahitaji. Na mwenye kue­pushwa na uchoyo wa nafsi yake, basi hao ndio wenye kufaulu.

وَالَّذِينَ جَاءُوا مِن بَعْدِهِمْ يَقُولُونَ رَبَّنَا اغْفِرْ لَنَا وَلِإِخْوَانِنَا الَّذِينَ سَبَقُونَا بِالْإِيمَانِ وَلَا تَجْعَلْ فِي قُلُوبِنَا غِلًّا لِّلَّذِينَ آمَنُوا رَبَّنَا إِنَّكَ رَءُوفٌ رَّحِيمٌ ﴿١٠﴾

10. Na waliokuja baada yao wanasema: Mola wetu! Tughufirie sisi na ndugu zetu waliotutangulia kwa Imani, wala usijaalie ndani ya nyoyo zetu undani kwa walioamini. Mola wetu! Hakika Wewe ni Mpole Mwingi wa rehema.

أَلَمْ تَرَ إِلَى الَّذِينَ نَافَقُوا يَقُولُونَ لِإِخْوَانِهِمُ الَّذِينَ كَفَرُوا مِنْ أَهْلِ الْكِتَابِ لَئِنْ أُخْرِجْتُمْ لَنَخْرُجَنَّ مَعَكُمْ وَلَا نُطِيعُ فِيكُمْ أَحَدًا أَبَدًا وَإِن قُوتِلْتُمْ لَنَنصُرَنَّكُمْ وَاللَّـهُ يَشْهَدُ إِنَّهُمْ لَكَاذِبُونَ ﴿١١﴾

11. Je, Huwaoni wanaofanya unafiki wanawaambia ndugu zao waliokufuru katika Watu wa Kitabu: Mkitolewa na sisi lazima tutatoka pamoja nanyi, wala hatutamtii yeyote kabisa dhidi yenu.

Na mkipig­wa vita lazima tutawasaidia. Na Mwenyezi Mungu ana­shuhudia kuwa hao hakika bila ya shaka ni waongo.

لَئِنْ أُخْرِجُوا لَا يَخْرُجُونَ مَعَهُمْ وَلَئِن قُوتِلُوا لَا يَنصُرُونَهُمْ وَلَئِن نَّصَرُوهُمْ لَيُوَلُّنَّ الْأَدْبَارَ ثُمَّ لَا يُنصَرُونَ ﴿١٢﴾

12. Wakitolewa hawatatoka pamoja nao na wakipigwa vita hawatawasaidia. Na kama wakiwasaidia basi watageuza migongo; Kisha hawatanusuriwa.

لَأَنتُمْ أَشَدُّ رَهْبَةً فِي صُدُورِهِم مِّنَ اللَّـهِ ذَٰلِكَ بِأَنَّهُمْ قَوْمٌ لَّا يَفْقَهُونَ ﴿١٣﴾

13. Hakika nyinyi ni tishio zaidi katika vifua vyao kuliko Mwenyezi Mungu. Hayo ni kwa kuwa hao ni watu wasio­fahamu.

لَا يُقَاتِلُونَكُمْ جَمِيعًا إِلَّا فِي قُرًى مُّحَصَّنَةٍ أَوْ مِن وَرَاءِ جُدُرٍ بَأْسُهُم بَيْنَهُمْ شَدِيدٌ تَحْسَبُهُمْ جَمِيعًا وَقُلُوبُهُمْ شَتَّىٰ ذَٰلِكَ بِأَنَّهُمْ قَوْمٌ لَّا يَعْقِلُونَ ﴿١٤﴾

14. Hawatapigana nanyi kwa mkusanyiko isipokuwa katika vijiji vilivyozatitiwa kwa ngome au nyuma ya kuta. Wao kwa wao vita vyao ni vikali. Utawadhania kuwa wako pamoja, kumbe nyoyo zao ni mbali mbali. Hayo ni kwa kuwa wao ni watu wasio na akili.

كَمَثَلِ الَّذِينَ مِن قَبْلِهِمْ قَرِيبًا ذَاقُوا وَبَالَ أَمْرِهِمْ وَلَهُمْ عَذَابٌ أَلِيمٌ ﴿١٥﴾

15. Ni kama mfano wa waliokuwa kabla yao hivi karibuni. Walionja ubaya wa mambo yao. Nao watapata adhabu iliyo chungu.

WANAWAPENDELEA KULIKO NAFSI ZAO

Aya 9 – 15

MAANA

Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kubainisha daraja ya wahajiri katika Aya iliyotangulia, sasa anabainisha daraja ya Answar, kwa kusema, kama ifuatavyo:-

Na waliofanya maskani na Imani yao kabla yao, wanawapenda waliohamia kwao.

Makusudio ya maskani hapa ni Madina. Maana ni kuwa Answar, wenyeji wa Madina, walimsaidia Mtume pamoja na wale waliohama naye. Wakajitolea kwa nafsi zao na mali zao; bali waliwapendela wao kuliko nafsi zao; kama itakavyoashiria Aya.

Miongoni mwa Aya zilizoshuka kwa ajili ya Answar ni:

وَالَّذِينَ آمَنُوا وَهَاجَرُوا وَجَاهَدُوا فِي سَبِيلِ اللَّـهِ وَالَّذِينَ آوَوا وَّنَصَرُوا أُولَـٰئِكَ هُمُ الْمُؤْمِنُونَ حَقًّا لَّهُم مَّغْفِرَةٌ وَرِزْقٌ كَرِيمٌ ﴿٧٤﴾

“Na wale waliokaribisha na kusaidia, hao ndio waumini kweli, wana wao maghufira na riziki njema.” Juz. 10 (8:74).

Wala hawapati dhiki katika vifua vyao kwa walivyopewa Wahajiri.

Mwanzoni Wahajiri walikuwa ni mafukara zaidi katika Madina wakipata tabu. Lau si Answar wangelikufa na njaa. Mtume(s.a.w.w) alikuwa akiwapa sadaka mafukara na hawapi matajiri na walio na uwezo wa kuchuma.

Kwa hiyo alikuwa akiwapa kipaumbele Wahajiri; mara nyingine akiwapa ngawira wao tu. Answar walikuwa wakiliridhia hilo bila ya kuona choyo wala dhiki nyoyoni, na wakiona ni haki kabisa. Ndio akasajili Mwenyezi Mungu (s.w.t) sifa zao hizi kwenye Kitabu chake.

Na wanawapendelea kuliko nafsi zao, ingawa wao wenyewe ni wahitaji.

Kumpendela mwingine kuliko nafsi yake mtu, akiwa na mahitaji, hakuwezi kulinganihswa na jambo lolote isipokuwa kujitolea mhanga. Imeelezwa katika vitabu vya Tafsir na Historia kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) aliwaambia Answar: “Mkipenda ngawira hii iwe baina yenu na Wahajiri, lakini mshirikiane nao katika mali yenu, au muwaachie ngawira na nyinyi mbaki na mali yenu. Answar wakasema: bali tutawaachia ngawira na tutashirikiana nao katika mali yetu ewe Mjumbe wa Mwenyezi Mungu. Hapo Mtume akawaombea dua na kusema: “Ewe Mwenyezi Mungu! Warehemu Answar na watoto wa Answar.”

Na mwenye kuepushwa na uchoyo wa nafsi yake, basi hao ndio wenye kufaulu.

Uchoyo ni mama wa maovu. Mwenye kuuitikia utamzuia na kila heri, na mwenye kuushinda kwenye nafsi yake basi atakuwa ameikinga na kila uovu na hatari.

Na waliokuja baada yao wanasema: Mola wetu! Tughufirie sisi na ndugu zetu waliotutangulia kwa Imani.

Yaani waliokuja baada ya Answar na Wahajiri. Makusudio ya waliokuja baada yao ni kila mwenye kufuata sera mpaka siku ya Kiyama, wala haku­na njia ya kuwahusisha Tabiina (waliowafuatia maswahaba). Kwa sababu linalozingatiwa ni matendo sio mahali fulani wala wakati. Maswahaba hawakufikia walipokuwa ila ni kwakuwa walisikilza kauli wakafuata mazuri yake.

Wala usijaalie ndani ya nyoyo zetu undani kwa walioamini.

Ni muhali kabisa kuwa pamoja imani na undani. Inawezekana mtu kujiwekea undani?

Mola wetu! Hakika Wewe ni Mpole Mwingi wa rehema kwa waja wako walioitakasa dini yao na nyoyo zao kutokana undani na unafiki.

Je, Huwaoni wanaofanya unafiki wanawaambia ndugu zao walioku­furu katika Watu wa Kitabu: Mkitolewa na sisi lazima tutatoka pamo­ja nanyi, wala hatutamtii yeyote kabisa dhidi yenu. Na mkipigwa vita lazima tutawasaidia.

Makusudio ya watu wa Kitab hapa ni Bani Nadhir, ndugu wa wanafiki katika ukafiri na uadui kwa Mtume. Aya inaashiria tukio maalum. Pale Mtume(s.a.w.w) alipotangaza vita dhidi ya Bani Nadhir, wanafiki wakion­gozwa na Abadallah bin Ubayya waliwaambia: piganeni na Muhammad na sisi tuko na nyinyi, akiwapiga nasi tutampiga na wakiwatoa Madina tuta­toka nanyi; hatutamsikiliza Muhammad wala mwenginewe.

Na Mwenyezi Mungu anashuhudia kuwa hao hakika bila ya shaka ni waongo kwenye kauli yao na ahadi yao.

Wakitolewa Bani Nadhirhawatatoka pamoja nao wanafiki,na wakipigwa vita hawatawasaidia. Na kama wakiwasaidia basi watageuza migongo;

Hii ndio hali ya mnafiki, ulimi wake unahalifiwa na moyo wake na dhahiri yake inahalifiwa na siri yake.

Kisha hawatanusuriwa wala kunufaika na kwa vitimbi na unafiki wao.

Hakika nyinyi ni tishio zaidi katika vifua vyao kuliko Mwenyezi Mungu. Hayo ni kwa kuwa hao ni watu wasiofahamu.

Wanafiki wanawaogopa waumini kwa ukali wao wa vita, kwa sababu wao wanatazamia shari ya haraka wala hawatazimii adhabu inayokuja Akhera.

Hawatapigana nanyi kwa mkusanyiko isipokuwa katika vijiji vilivyo zatitiwa kwa ngome, au nyuma ya kuta.

Mayahudi hawakabiliani na waumini uso kwa uso katika uwanja wa vita, bali wanajificha kwenye mitaa yao nyuma ya ngome na kuta na kuwarushia waumini mishale na mawe; kama ilivyo hali ya mwoga.

Wao kwa wao vita vyao ni vikali. Utawadhania kuwa wako pamoja, kumbe nyoyo zao ni mbali mbali.

Wao wana nguvu kwa maandalizi yao na idadi yao, lakini masilahi na hawa za nafsi zimewatawanyisha. Wao wamechangukana, hata kama wanajionyesha kuwa na umoja na mapenzi.

Lau wangelikuwa na umoja na kupendana wangeliwatokea kupambana nanyi, lakini hawakupigana nanyi. Hili liko kwa wayahudi na wasiokuwa wayahudi, kwani umoja ni nguvu hata kama idadi na nyenzo ni ndogo, na utengano ni udhaifu hata kama kuna nyenzo na wingi wa watu.

Tumeshuhudia ushindi wa watu wasio na haki wachache juu ya walio na haki wengi na wenye nyenzo. Siri ni utengano wa hawa kwenye haki yao na umoja wa wale kwenye batili yao.

Hayo ni kwa kuwa wao ni watu wasio na akili ya kufahamu kuwa umoja ni nguvu na utengano ni udhaifu. Ni kama mfano wa waliokuwa kabla yao hivi karibuni. Walionja ubaya wa mambo yao. Nao watapata adhabu iliyo chungu.

Mayahudi walijenga uadui na Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w ) ; ni sawa na hali ya makafiri wa kikuraishi na wengineo waliompiga vita Mtume; pale walipoishia kwenye fedheha ya duniani na Akhera ni adhabu ya kuungua.

كَمَثَلِ الشَّيْطَانِ إِذْ قَالَ لِلْإِنسَانِ اكْفُرْ فَلَمَّا كَفَرَ قَالَ إِنِّي بَرِيءٌ مِّنكَ إِنِّي أَخَافُ اللَّـهَ رَبَّ الْعَالَمِينَ ﴿١٦﴾

16. Ni kama mfano wa Shetani anapomwambia mtu: kufuru. Na akikufuru humwambia: Mimi si pamoja nawe. Hakika mimi namwogopa Mwenyezi Mungu, Mola wa walimwengu wote.

فَكَانَ عَاقِبَتَهُمَا أَنَّهُمَا فِي النَّارِ خَالِدَيْنِ فِيهَا وَذَٰلِكَ جَزَاءُ الظَّالِمِينَ ﴿١٧﴾

17. Basi ikawa mwisho wa wote wawili hao ni kuingia Motoni, wadumu humo daima; na hayo ndiyo malipo ya madhal­imu.

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا اتَّقُوا اللَّـهَ وَلْتَنظُرْ نَفْسٌ مَّا قَدَّمَتْ لِغَدٍ وَاتَّقُوا اللَّـهَ إِنَّ اللَّـهَ خَبِيرٌ بِمَا تَعْمَلُونَ ﴿١٨﴾

18. Enyi mlioamini! Mcheni Mwenyezi Mungu, na kila nafsi iangalie inayoyatan­guliza kwa ajili ya Kesho. Na mcheni Mwenyezi Mungu. Hakika Mwenyezi Mungu ana habari za mnayoyatenda.

وَلَا تَكُونُوا كَالَّذِينَ نَسُوا اللَّـهَ فَأَنسَاهُمْ أَنفُسَهُمْ أُولَـٰئِكَ هُمُ الْفَاسِقُونَ ﴿١٩﴾

19. Wala msiwe kama wale waliomsahau Mwenyezi Mungu, na Yeye akawasa­haulisha nafsi zao. Hao ndio mafasiki.

لَا يَسْتَوِي أَصْحَابُ النَّارِ وَأَصْحَابُ الْجَنَّةِ أَصْحَابُ الْجَنَّةِ هُمُ الْفَائِزُونَ ﴿٢٠﴾

20. Hawawi sawa watu wa Motoni na watu wa Peponi. Watu wa Peponi ndio wenye kufuzu.

AKIKUFURU HUMWAMBIA MIMI NIKO MBALI NAWE

Aya 16 – 20

MAANA

Ni kama mfano wa Shetani anapomwambia mtu: kufuru. Na akikufu­ru humwambia: Mimi si pamoja nawe. Hakika mimi namwogopa Mwenyezi Mungu, Mola wa walimwengu wote.

Wanafiki waliwaambia Bani Nadhir: “Piganeni na Muhammad na sisi tuko pamoja nanyi katika vita,” lakini yalipowafika yaliowafika, walijificha kwenye viota vyao na hawakuonekana hata athari yao.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) ameifananisha hali ya wanafiki na Bani Nadhir na hali ya shetani na mtu mwenye kutenda dhambi. Huwa anamhadaa kwa ufisadi na upotevu na kumpa tamaa ya amani. Mambo yakichacha humwacha na adhabu na maangamizi na kujitenga naye na kudhihirisha hofu kutoka kwa Mwenyezi Mungu.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 10 (8:48) na Juz. 13 (14:22).

Basi ikawa mwisho wa wote wawili hao ni kuingia Motoni, wadumu humo daima; na hayo ndiyo malipo ya madhalimu.

Wawili ni shetani na mtu aliyeingia kwenye mtego wake. Maana yako wazi. Kwa ufupi ni kuwa kila mmoja, mwenye kuhadaa na mwenye kuhadaiwa, atakuwa katika Jahannam ambayo ni marejeo mabaya.

Enyi mlioamini! Mcheni Mwenyezi Mungu, ambaye nyinyi mko mikononi mwake, na mwenye kumcha Mwenyezi Mungu humfanyia wepesi mambo yake; kama anavyosema Mwenyezi Mungu katika Qur’an (65:4).

Na kila nafsi iangalie inayoyatanguliza kwa ajili ya Kesho.

Kila analolifanya mtu katika maisha haya huwa amelifanya kwa ajili ya Akhera. Mwenye busara anaangalia kwenye dunia yake kwa mtazamo wa mwenye kuicha kwa wema sio mwenye kuchukua anasa zake.

Na mcheni Mwenyezi Mungu. Hakika Mwenyezi Mungu ana habari za mnayoyatenda.

Mwenyezi Mungu anamjua mwenye kuamini kwa kauli na vitendo na mwenye kumwamini kwa fikra tu anayoisema na kuisahau kwenye viten­do. Mwenyezi Mungu (s.w.t) amelikariri jambo la takua kwa ukomo wa kuhimiza na kupendekeza.

Wala msiwe kama wale waliomsahau Mwenyezi Mungu, na Yeye akawasahaulisha nafsi zao.

Walisahau kufanya kwa amri ya Mwenyezi Mungu na Mwenyezi Mungu akawasahaulisha kufanya kwa masilahi ya nafsi zao. na aliyedanganyika zaidi katika watu ni yule aliyejisahau na asifanye kwa ajili ya usalama wake kujiepusha na maangamizi.

Hao ndio mafasiki. Kwa sababu hawakunufaika na ubainifu wa Mwenyezi Mungu na kupata funzo kwa mawaidha yake.

Hawawi sawa watu wa Motoni na watu wa Peponi. Watu wa Peponi ndio wenye kufuzu.

Vipi atakuwa sawa mwema na mwovu? Umetangulia mfano wake katika Aya kadhaa miongoni mwazo ni Juz. 21 (32:18).

لَوْ أَنزَلْنَا هَـٰذَا الْقُرْآنَ عَلَىٰ جَبَلٍ لَّرَأَيْتَهُ خَاشِعًا مُّتَصَدِّعًا مِّنْ خَشْيَةِ اللَّـهِ وَتِلْكَ الْأَمْثَالُ نَضْرِبُهَا لِلنَّاسِ لَعَلَّهُمْ يَتَفَكَّرُونَ ﴿٢١﴾

21. Lau tungelieiteremsha hii Qur’an juu ya mlima, basi bila ya shaka ungeliuona ukinyenyekea, ukipasuka kwa hofu ya Mwenyezi Mungu. Na hiyo ni mifano tunawapigia watu ili wafikiri.

هُوَ اللَّـهُ الَّذِي لَا إِلَـٰهَ إِلَّا هُوَ عَالِمُ الْغَيْبِ وَالشَّهَادَةِ هُوَ الرَّحْمَـٰنُ الرَّحِيمُ ﴿٢٢﴾

22. Yeye ndiye Mwenyezi Mungu, ambaye hapana mungu isipo kuwa Yeye tu, Mwenye kuya­jua yaliyofichikana na yanay­oonekana. Yeye ndiye Mwingi wa rehema, Mwenye kurehemu.

هُوَ اللَّـهُ الَّذِي لَا إِلَـٰهَ إِلَّا هُوَ الْمَلِكُ الْقُدُّوسُ السَّلَامُ الْمُؤْمِنُ الْمُهَيْمِنُ الْعَزِيزُ الْجَبَّارُ الْمُتَكَبِّرُ سُبْحَانَ اللَّـهِ عَمَّا يُشْرِكُونَ ﴿٢٣﴾

23. Yeye ndiye Mwenyezi Mungu ambaye hapana mungu isipo kuwa Yeye tu. Mtakatifu, Mwenye salama, Mtoaji wa amani, Mwangaliaji, Mwenye nguvu, Jabari, Mkubwa; Ametakasika Mwenyezi Mungu na hayo wanay­omshirikisha nayo.

هُوَ اللَّـهُ الْخَالِقُ الْبَارِئُ الْمُصَوِّرُ لَهُ الْأَسْمَاءُ الْحُسْنَىٰ يُسَبِّحُ لَهُ مَا فِي السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ وَهُوَ الْعَزِيزُ الْحَكِيمُ ﴿٢٤﴾

24. Yeye ndiye Mwenyezi Mungu, Muumbaji, Mtengenezaji, Mtia sura, Mwenye majina mazuri kabisa. Kinamsabihi kilicho katika mbingu na ardhi, naye ni Mwenye nguvu, Mwenye hikima.

LAU TUNGELIITERMSHA HII QUR’ANI JUU MLIMA

Aya 21 – 24

MAANA

Lau tungelieiteremsha hii Qur’an juu ya mlima, basi bila ya shaka ungeliuona ukinyenyekea, ukipasuka kwa hofu ya Mwenyezi Mungu.

Hii ni kiasi cha kukadiria tu, kunakofahamika kutokana na neno ‘Lau.’ Lengo ni kubainisha ukuu wa Qur’an, kwamba ina nguvu na athari; kiasi ambacho lau itateremshwa kwenye jabali basi lingenyenyeka na kulainika pamoja na ugumu wake. Pia lingelipasuka na kuanguka kwa kumwogopa Mwenyezi Mungu. Basi vipi mtu ambaye anaumizwa na chawa na kufa kwa kusongwa koo na jasho humfanya anuke; kama alivyosema Amirul Muminin, Ali(a.s) ?

Ana nini mtu huyu mnyonge, “anayesikia Aya za Mwenyezi Mungu akisomewa, kisha anang’ng’ania huku akijivuna, kama kwamba hakuzisikia. ” Juz. 25 (45:8).

Je, ni kwa kuwa moyo wake ni mgumu kama jabali ambalo limekazana sana, au ni ujinga, inadi na kung’ang’ania upotevu?

Na hiyo ni mifano tunawapigia watu ili wafikiri, katika hikima ya Qur’an, mawaidha yake, dalili yake, na ubainifu wake, na waongoke, kwa nuru yake, kwenye njia ya usawa, lakini:

إِنَّ فِي ذَٰلِكَ لَذِكْرَىٰ لِمَن كَانَ لَهُ قَلْبٌ أَوْ أَلْقَى السَّمْعَ وَهُوَ شَهِيدٌ ﴿٣٧﴾

“Hakika katika hayo kuna ukumbusho kwa mwenye moyo au akatega sikio naye ni shahidi.”

Juz. 26 (50:37).

Baada ya hayo yote, hakika ukuu wa Qur’an ni ukuu wa Mwenyezi Mungu (s.w.t). Walisema wakale: maneno ni sifa ya mwenye kusema; hasa yale yanayorudia ilimu yake.

Ndio maana Mwenyezi Mungu akaisifia Qur’an kwa sifa zake; kama vile nguvu, hekima, utukufu, ukuu, nuru, haki, rehe­ma, ukweli n.k.

Kisha Mwenyezi Mungu (s.w.t) akajisifu kwa sifa zake tukufu akasema:Yeye ndiye Mwenyezi Mungu, ambaye hapana mungu isipo kuwa Yeye tu, apasaye kuabudiwa kwa haki, anayesifika kwa sifa zote nzuri za ukamilifu; zikiwemo hizi zifuatazo:-

Mwenye kuyajua yaliofichikana na yanayoonekana . Anayajua yaliyoghaibu kwa watu na yaliyo dhahiri.

Yeye ndiye Mwingi wa rehema, Mwenye kurehemu . Sifa mbili hizi zimetokana na rehema kwa maana ya hisani. Inawezekana kuwa kuchanganywa matamko mawili ni kuashiria kuwa rehema yake imeenea kila kitu, hata katika hali ya kughadhibika kwake; na kwamba kuikatia tamaa ni kufuru na upotevu.

Yeye ndiye Mwenyezi Mungu ambaye hapana mungu isipo kuwa Yeye tu. Huu ni msisitizo wa tawhid. Yeye niMfalme; ni wake ufalme wa mbingu na ardhi, Ndiye anayetoa uhai na kufisha.

Mtakatifu; yaani ametakasika na yasiyolaikiana na utukufu wake.Mwenye salama ; kwa sababu inatokana na Yeye mtukufu utulivu na amaniMtoaji wa amani ; Anawapa thawabu waumini na anawapa amani ya adhabu ya moto.Mwangaliaji ; Mwenye kuchunga na kuhifadhi.

Mwenye nguvu ; asiyeshindwa wala kuzidiwa nguvu.Jabari ; Aliye juu bila ya kufikiwa.Mkubwa; Ana ukubwa na utukufu.Ametakasika Mwenyezi Mungu na hayo wanayomshirikisha nayo , ya kuwa na mshirika, mke na mtoto.Yeye ndiye Mwenyezi Mungu, Muumbaji, Mtengenezaji .

Hizi ni sifa mbili tofauti. Neno mtengenezaji tumelifasiri kutokana na neno Bariu ambalo imesemekana kuwa hapa lina maana ya kuwa mbali na upun­gufu.Mtia sura ; Mwenye kuumba sura na umbo.Mwenye majina mazuri kabisa.

Kila jina lake Mwenyezi Mungu Mtukufu ni zuri na ni kuu. Tazama Juz. 9 (7:180) Kifungu cha: ‘Je, majina ya Mwenyezi Mungu ni hayo hayo?’

Kinamsabihi kilicho katika mbingu na ardhi, naye ni Mwenye nguvu, Mwenye hikima.

Tasbihi inakuwa kwa lugha ya maneno na lugha ya hali. Tazama Juz. 15 (15:44) kifungu cha ‘Kila kitu kinamsabihi.

MWISHO WA SURA YA HAMSINI NA TISA: SURAT AL-HASHR