TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE Juzuu 24

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE18%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: Qurani tukufu

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
  • Anza
  • Iliyopita
  • 30 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 29568 / Pakua: 5450
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE Juzuu 24

Mwandishi:
Swahili

3

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE

Sura Ya Hamsini Na Tisa: Surat Al-Hashr. Imeshuka Madina. Ina Aya 24.

بِسْمِ اللَّهِ الرَّحْمَٰنِ الرَّحِيمِ

Kwa jina la Mwenyezi Mungu Mwingi wa rehema, Mwenye kurehemu.

سَبَّحَ لِلَّـهِ مَا فِي السَّمَاوَاتِ وَمَا فِي الْأَرْضِ وَهُوَ الْعَزِيزُ الْحَكِيمُ ﴿١﴾

1. Vinamsabihi Mwenyezi Mungu vilivyo katika mbingu na vilivyo katika ardhi. Na Yeye ndiye Mwenye nguvu, Mwenye hikima.

هُوَ الَّذِي أَخْرَجَ الَّذِينَ كَفَرُوا مِنْ أَهْلِ الْكِتَابِ مِن دِيَارِهِمْ لِأَوَّلِ الْحَشْرِ مَا ظَنَنتُمْ أَن يَخْرُجُوا وَظَنُّوا أَنَّهُم مَّانِعَتُهُمْ حُصُونُهُم مِّنَ اللَّـهِ فَأَتَاهُمُ اللَّـهُ مِنْ حَيْثُ لَمْ يَحْتَسِبُوا وَقَذَفَ فِي قُلُوبِهِمُ الرُّعْبَ يُخْرِبُونَ بُيُوتَهُم بِأَيْدِيهِمْ وَأَيْدِي الْمُؤْمِنِينَ فَاعْتَبِرُوا يَا أُولِي الْأَبْصَارِ ﴿٢﴾

2. Yeye ndiye Aliewatoa walioku­furu miongoni mwa Watu wa Kitabu katika nyumba zao wakati wa mkusanyiko wa kwanza. Hamkudhani kuwa watatoka, nao walidhani kuwa ngome zao zitawalinda na Mwenyezi Mungu. Lakini Mwenyezi Mungu aliwafikia kwa mahali wasipopatazamia, na akatia woga katika nyoyo zao. Wakawa wanazibomoa nyumba zao kwa mikono yao na mikono ya Waumini. Basi zingatieni enyi wenye busara!

وَلَوْلَا أَن كَتَبَ اللَّـهُ عَلَيْهِمُ الْجَلَاءَ لَعَذَّبَهُمْ فِي الدُّنْيَا وَلَهُمْ فِي الْآخِرَةِ عَذَابُ النَّارِ ﴿٣﴾

3. Na lau kuwa Mwenyezi Mungu asingeliwaandikia uhamisho, angeliwaadhibu katika dunia. Na katika Akhera watapata adhabu ya Moto.

ذَٰلِكَ بِأَنَّهُمْ شَاقُّوا اللَّـهَ وَرَسُولَهُ وَمَن يُشَاقِّ اللَّـهَ فَإِنَّ اللَّـهَ شَدِيدُ الْعِقَابِ ﴿٤﴾

4. Hayo ni kwa sababu walimpin­ga Mwenyezi Mungu na Mtume wake. Na mwenye kumpinga Mwenyezi Mungu, basi hakika Mwenyezi Mungu ni Mkali wa kuadhibu.

مَا قَطَعْتُم مِّن لِّينَةٍ أَوْ تَرَكْتُمُوهَا قَائِمَةً عَلَىٰ أُصُولِهَا فَبِإِذْنِ اللَّـهِ وَلِيُخْزِيَ الْفَاسِقِينَ ﴿٥﴾

5. Mtende wowote mlioukata au mliouacha umesimama vile vile juu ya mashina yake, basi ni kwa idhini ya Mwenyezi Mungu, na kwa kuwahizi mafasiki.

VINAMSABIHI MWENEYEZI MUNGU

Aya 1 – 5

KISA CHA BANI NADHIR KWA UFUPI

Aya hizi zinahusiana na ushindi wa Mtume(s.a.w.w) dhidi ya mayahudi wa Bani Nadhir. Hawa walikuwa wakiishi viungani mwa Madina. Mtume(s.a.w.w) alipohamia huko, aliwekeana nao mkataba wa amani. Waislamu walipowashinda Makuraishi vita vya Badr, Bani Nadhir walifurahi sana, lakini waliposhindwa kwenye vita vya Uhud walivunja makataba na waka­panga njama za kummaliza Mtume na kiongozi wao, Kaa’b bin Ashraf akaungana na Abu Sufyan dhidi ya Nabii(s.a.w.w) .

Inasemekana kuwa Kaa’b alimshambulia Mtume kwa mashairi, Mtume akamwamuru mmoja wa maswahaba zake kumuua. Kisha Mtume(s.a.w.w) akawaendea Bani Nadhir na akawaamuru kutoka Madina, lakini wanafiki wakiongozwa na Abdallah bin Ubayya, waliwatumia ujumbe kuwa msikubali, sisi tuko pamoja nanyi. Basi wakawa na matumaini na wakashikilia kupigana. Hapo Mtume akawahusuru kwa muda wa siku 21, kama yanavyosema baadhi ya mapokezi.

Mtume(s.a.w.w) aliamuru kukatwa baadhi ya mitende yao. Hakuna yeyote katika wanafiki aliyejaribu kuwasaidia. Basi wakalazimika kusalimu amri, na Mtume akasuluhishana nao kuwa watoke Madina; kila watu watatu wachukue ngamia mmoja atakayewabebea wanachotaka. Basi wakakubali na wakatoka Madina kabisa.

Sura hii imewashukia wao. Ibn Abas alikuwa akiita Sura hii Sura ya Bani Nadhir.

MAANA

Vinamsabihi Mwenyezi Mungu vilivyo katika mbingu na vilivyo kati­ka ardhi. Na Yeye ndiye Mwenye nguvu, Mwenye hikima.

Vitu vyote vilivyoko vinamsabihi (vinamtakasa) na kutukuza uweza wake Mwenyezi Mungu na hekima yake, kwa lugha ya maneno na lugha ya hali. Umetangulia mfano wake katika Juz. 27 (57:1).

Yeye ndiye Aliyewatoa waliokufuru miongoni mwa Watu wa Kitabu katika nyumba zao wakati wa mkusanyiko wa kwanza.

Makusudio ya waliokufuru hapa ni Bani Nadhir. Wametofautiana wafasiri kuhusu mkusanyiko wa kwanza. Razi anasema: “Ibn Abbas na wafasiri wengi wamesema kuwa maana ya mkusanyiko wa kwanza ni kuwa hiyo ilikuwa ni mara ya kwanza kwa watu wa Kitab kutolewa Bara Arabu. Kabla yake walikuwa na nguvu… Hili haliko mbali kwa sababu kutolewa kwa pili kulitokea kwa khalifa wa pili.

Maana ni kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) aliwatoa Bani Nadhir kupitia mikononi mwa waislamu. Na hii ilikuwa ni mara ya kwanza kutolewa watu wa Kitabu huko. Na sababu ya kutolewa kwao ni hiyana yao na kuvunja kwao mapatano ya amani waliyowekeana na Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) wao wenyewe.

Unaweza kuuliza : Kwanini Mwenyezi Mungu aliwaadhibu kwa kuwatoa na kuchukua mali yao na kuna aina nyingine za kuwaadhibu?

Jibu : Aliwachukulia kwa sharia ya dini yao. Tawrat yao inasema: “Utakaposongea karibu ya mji kwenda kupigana juu yake, ndipo utakapowapigia ukelele wa amani.

Itakuwa utakapokujibu kwa amani, na kukufungulia, ndipo watu wote watakaoonekana humo, watafanya kazi ya shoka, na kukutumikia. Na kama hautaki kufanya amani nawe, lakini utafanya vita juu yako, ndipo uhusuru; na Bwana, Mungu wako, autiapo mkononi mwako, mpige kila mume aliyemo kwa makali ya upanga; lakini wanawake na watoto na wanyama wa mji, na vilivyo mjini vyote, navyo ni nyara zake zote, uvitwae viwe mateka; nawe utakula nyara za adui zako alizokupa Bwana, Mungu wako” (Kumbukumbu 20:10 -14).

Hakuna mwenye shaka kwamba mwenye kufuata dini au misingi hana budi kufuata hukumu zake zote na kuzitekeleza yeye mwenyewe kabla ya kutekelezea mwenginewe. Tena Nabii(s.a.w.w) aliwahurumia Bani Nadhir, kwa sababu hakuwaua wanaume wao wala kuwateka wanawake na watoto; kama ilivyo nukuu ya Tawrat yao.

Hayo tumeyazungumzia kwa ufafanuzi zaidi katika Juz. 21 (33: 16-20), kifungu cha ‘Je, Muhammad aliwadhulumu Bani Quraydha?’

Hamkudhani kuwa watatoka, nao walidhani kuwa ngome zao zitawalinda na Mwenyezi Mungu.

Yaani waislamu hawakutegemea kabisa kuwa Bani Nadhir watatoka majumbani mwao na kuwaachia maadui zao waislamu, kutokana na inadi yao na nguvu walizokuwa nazo kwa uwezo na idadi yao.

Vile vile Bani Nadhir walikuwa wakijiamini kuwa wana nguvu na uwezo kuwa ni ngome isiyoingiliwa na mkono wowote. Lakini ulikuwa ni uwezo na ngome ya khiyana, haiwezi kumlinda mwenye kuikimbilia.

PROPAGANDA ZA UPOTOFU NA WAKATI MNASABA

Lakini Mwenyezi Mungu aliwafikia kwa mahali wasipopatazamia, na akatia woga katika nyoyo zao.

Walidhani kuwa ngome zao zitawalinda, lakini Mwenyezi Mungu akatia hofu kwenye nyoyo zao baada ya kumjaza haiba Mtume(s.a.w.w) na jeshi lake. Basi ngome zao zikayayuka, kwa sababu nyoyo ndio msingi wa nguvu zote.

Ndio maana waovu na wafanyibiashara wa silaha wanafanya bidii sana kwenye vita vya nafsi na kutafuta nyenzo na pesa, lakini wame­sahau au wamejitia kusahau kuwa hakuna njia ya kuufikia moyo isipokuwa haki, kheri na hisani. Ikiwa propaganda za upotevu zitapata waungaji mkono basi ni kwa muda, kisha zinafichuka; hata kama muda utakuwa mrefu.

Aliulizwa Charles Mwigizaji maarufu wa tamthilia kuhusu mambo ya maisha: Mtu anahitaji nini ili aweze kutengeneza njia yake ya maisha? Akasema: “Jambo muhimu ni kujua wakati mnasaba.” Nasi tunamwambia Charles: “Ndio hakuna budi ya wakati, lakini ni lazima uwe unanasibiana na masilahi ya kheri sio ya shari, na ya haki sio ya batili. Kwa sababu shari inaondoka pamoja na watu wake, hata kama ni kuchelewa kwa kiasi gani.

Wakawa wanazibomoa nyumba zao kwa mikono yao na mikono ya Waumini.

Badhi ya wafasiri wamesema kuwa makusudio ya kubomoa nyumba ni kuziacha na kwa mikono yao ni kuwa wao ndio sababu ya kuondoka kwao; pale walipovunja maelewano na Mtume. Mikono ya waumini ni ishara ya kuwa waislamu ndio waliowatoa Bani Nadhir majumbani mwao.

Wafasiri wengine wakasema kuwa Bani Nadhir waliziharibu hasa nyumba zao ili zisibakie salama mikononi mwa waislamu, na kwamba waislamu walizipondaponda ngome za mayahudi ili wapate kuwafikia. Tafsiri hii iko karibu na maana na inatiwa nguvu na dhahiri ya Aya; wala haipingani na ile ya kwanza, bali ni natija ya kuondoka mji.

Basi zingatieni enyi wenye busara!

Kuzingatia kitu ni kukirudisha kwenye mtazamo na kukihukumu kwa mfano wake. Mwenyezi Mungu aliwatoa Bani Nadhir majumbani mwao yakiwa ni malipo ya hiyana yao. Basi mwenye akili anatakikana kupata somo na ajiepushe na hiyana na njama, ili yasimfike yaliyowafika.

Na lau kuwa Mwenyezi Mungu asingeliwaandikia uhamisho, angeli­waadhibu katika dunia. Na katika Akhera watapata adhabu ya Moto.

Mwenyezi Mungu amewaadhibu duniani kwa kuwahamisha kutoka majumbani mwao na lau si hivyo angeliwaadhibu kwa kuwaua; kama walivyofanywa Bani Quraydha. Na hawataepuka adhabu ya Moto.

Hayo ni kwa sababu walimpinga Mwenyezi Mungu na Mtume wake.

Walistahili adhabu ya dunia na Akhera, kwa sababu wao walimhalifu Mwenyezi Mungu, wakipituka mipaka yake, na kumwekea uadui Mtume wake.

Na mwenye kumpinga Mwenyezi Mungu, basi hakika Mwenyezi Mungu ni Mkali wa kuadhibu.

Hili ni onyo na kiaga kwa kila jabari mwenye kiburi.

Mtende wowote mlioukata au mliouacha umesimama vile vile juu ya mashina yake, basi ni kwa idhini ya Mwenyezi Mungu, na kwa kuwahizi mafasiki.

Mtume(s.a.w.w) alikuwa ameamrisha kukatwa baadhi ya mitende ya Bani Nadhir ili kuwakasirisha kwa hilo. Baadhi wakadhani kuwa hiyo ni aina ya uharibifu. Ndio Mwenyezi Mungu akabainisha kwamba kila liliotukia kati­ka kukatwa mitende au kuachwa ni kwa amri ya Mwenyezi Mungu na wala haitoki kwa Mtume(s.a.w.w) , na lengo ni kuwakasirisha makafiri kwa kuikata na pia kuwakasirisha kwa ile ilioachwa kwa vile watanufaika nayo wale wanaowaona ni maadui zao.

Ieleweke kuwa kukata miti na mengineyo wakati wa vita haifai kuchukuli­wa ni msingi maalum; inaweza kuwa ni wajibu na inaweza kuwa ni hara-mu, kulingana na masilahi ya kumpiga adui; sawa na yanavyovunjwa majumba kwa ajili ya kupitisha barabara, siku ambazo si za vita.

وَمَا أَفَاءَ اللَّـهُ عَلَىٰ رَسُولِهِ مِنْهُمْ فَمَا أَوْجَفْتُمْ عَلَيْهِ مِنْ خَيْلٍ وَلَا رِكَابٍ وَلَـٰكِنَّ اللَّـهَ يُسَلِّطُ رُسُلَهُ عَلَىٰ مَن يَشَاءُ وَاللَّـهُ عَلَىٰ كُلِّ شَيْءٍ قَدِيرٌ ﴿٦﴾

6. Na Aliyoleta Mwenyezi Mungu kwa Mtume wake kutoka kwao hamkuyaendea kwa farasi wala ngamia. Lakini Mwenyezi Mungu huwapa mamlaka Mitume wake juu ya wowote awatakao. Na Mwenyezi Mungu ni Muweza juu ya kila kitu.

مَّا أَفَاءَ اللَّـهُ عَلَىٰ رَسُولِهِ مِنْ أَهْلِ الْقُرَىٰ فَلِلَّـهِ وَلِلرَّسُولِ وَلِذِي الْقُرْبَىٰ وَالْيَتَامَىٰ وَالْمَسَاكِينِ وَابْنِ السَّبِيلِ كَيْ لَا يَكُونَ دُولَةً بَيْنَ الْأَغْنِيَاءِ مِنكُمْ وَمَا آتَاكُمُ الرَّسُولُ فَخُذُوهُ وَمَا نَهَاكُمْ عَنْهُ فَانتَهُوا وَاتَّقُوا اللَّـهَ إِنَّ اللَّـهَ شَدِيدُ الْعِقَابِ ﴿٧﴾

7. Aliyoleta Mwenyezi Mungu kwa Mtume wake kutoka kwa watu vijijini ni kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, na kwa ajili ya Mtume, na jamaa, na maya­tima, na masikini, na mwananjia, Ili yasiwe yakizunguka baina ya matajiri miongoni mwenu. Na anachowapa Mtume kichukueni, na ana­chowakataza jiepusheni nacho. Na mcheni Mwenyezi Mungu. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mkali wa kuadhibu.

لِلْفُقَرَاءِ الْمُهَاجِرِينَ الَّذِينَ أُخْرِجُوا مِن دِيَارِهِمْ وَأَمْوَالِهِمْ يَبْتَغُونَ فَضْلًا مِّنَ اللَّـهِ وَرِضْوَانًا وَيَنصُرُونَ اللَّـهَ وَرَسُولَهُ أُولَـٰئِكَ هُمُ الصَّادِقُونَ ﴿٨﴾

8. Wapewe mafukara wahajiri waliotolewa majumbani mwao na mali yao kwa ajili ya kutafuta fadhila kutoka kwa Mwenyezi Mungu na radhi zake, na wanamsaidia Mwenyezi Mungu na Mtume wake. Hao ndio wa kweli.

MALI ISIZUNGUKE KWA MATAJIRI

Aya 6–8

MAANA

Na Aliyoleta Mwenyezi Mungu kwa Mtume wake kutoka kwao hamkuyaendea kwa farasi wala ngamia.

Neno ‘Aliyoleta’ tumelifasiri kutokana na neno la kiarabu Fay’i ambalo ki lugha ya kiarabu lina maana ya kurejesha. Fay’i katika sharia ya kiislamu ni mali waliyoipata waislamu kutoka kwa makafiri bila ya vita. Na ghani­ma (ngawira) ni mali iliyopatikana kwa vita.

Vyovyote iwavyo ni kuwa Aya tuliyo nayo inahusika na mali ya Bani Nadhir. Kwa hiyo maana yanakuwa, mali ya Bani Nadhir ameijaalia ni nyara kwa Mtume wake kuifanyia anavyotaka, waislamu hawana chao hapo kwa vile hawakuitolea jasho lolote.

Lakini Mwenyezi Mungu huwapa mamlaka Mitume wake juu ya wowote awatakao.

Miongoni mwa mamlaka hayo ni kuwa Mwenyezi Mungu Mtukufu alitia hofu kwenye nyoyo za Bani Nadhir kutoka kwa Mtume(s.a.w.w) ili wasalimu amri yake wakiwa dhalili, bila ya vita.

Na Mwenyezi Mungu ni Muweza juu ya kila kitu.

Miongoni mwa hayo ni kudhalilika watu wenye nguvu, ngome na idadi, mbele ya mtumwa miongoni mwa watumwa wa Mwenyezi Mungu.

Aliyoleta Mwenyezi Mungu kwa Mtume wake kutoka kwa watu vijijini kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, na kwa ajili ya Mtume, na jamaa, na mayatima, na masikini, na mwananjia.

Makusudio ya watu wa vijiji hapa ni makafiri wengine wasiokuwa Bani Nadhir. Maana ni kuwa mali ya fay’i isiyokuwa ya Bani Nadhir ni ya Mwenyezi Mungu na Mtume. Mwananjia ni msafiri aliyekatikiwa njiani na kushindwa kurudi kwa watu wake.

Kimsingi ni kuwa mali ya Mwenyezi Mungu ni ya Mtume(s.a.w.w) . Wameafikiana kwa kauli moja, isipokuwa kidogo, kwamba makusudio ya jamaa ni jamaa wa Mtume(s.a.w.w) katika Bani Hashim. Ama kuhusu may­atima, masikini na mwananjia, Shia Imamiya wamesema kuwa wanahusi­ka wa Bani Hashim tu. Wengine wamesema ni yeyote awe Hashim au mwinginewe [1] .

Tumeyazungumzia hayo kwa ufafanuzi zaidi katika Juz. 10 (8:41).

Ili yasiwe yakizunguka baina ya matajiri miongoni mwenu.

Uislamu ni dini ya Mwenyezi Mungu kwa ajili ya watu, inachunga masi­lahi ya wote bila ya kuwabagua. Hautatui tatizo la mtu kwa gharama ya mwingine, wala haumkandamizi mtu ili kumnufaisha mwingine. Wote mbele ya uislamu ni sawasawa.

Haya yanajitokeza kwenye hukumu zake na misingi yake. Miongoni mwa misingi hiyo ni kuwa mali isizunguke kwa matajiri tu. Hiyo ni pamoja na kukataza riba, ghushi na unyonyaji.

Ieleweke kwamba hii haifahamishi kwa karibu wala umbali kuwa uislamu unakubaliana na siasa ya ujamaa au haukubali nayo. Ieleweke tu kuwa uis­lamu katika hukumu zake zote kunajengeka fikra ya uadilifu na usawa na unakubaliana na kila lenye heri ya watu na manufaa yao. Hili ni jambo jingine na kutaifisha mali za watu kuwa mali za uma ni jambo jingine.

Tazama Juz. 4 (3:180-182), kifungu cha: ‘Matajairi ni mawakala sio wenyewe.’

Na anachowapa Mtume kichukueni, na anachowakataza jiepusheni nacho. Na mcheni Mwenyezi Mungu. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mkali wa kuadhibu.

Aya hii imeunganisha baina ya kauli ya Mwenyezi Mungu na Mtume wake na ikawajibisha kuzisikiliza kauli zote mbili, kwa sababu kauli ya Mtume inatokana na wahyi kutoka kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu:

وَمَا يَنطِقُ عَنِ الْهَوَىٰ ﴿٣﴾ إِنْ هُوَ إِلَّا وَحْيٌ يُوحَىٰ ﴿٤﴾

“Wala hatamki kwa matamanio. Hayakuwa haya ila ni wahyi uliotolewa.” Juz. 27 (53:3-4).

Mwenyezi Mungu amesema katika Aya kadhaa: “Mtiini Mwenyezi Mungu na Mtume.”

Akasema tena:

وَمَن يَعْصِ اللَّـهَ وَرَسُولَهُ فَقَدْ ضَلَّ ضَلَالًا مُّبِينًا ﴿٣٦﴾

“Na yeyote mwenye kumwasi Mwenyezi Mungu na Mtume wake, basi amepotea upotevu ulio wazi.” Juz. 22 (33:36).

Zimekuja Hadith mutawatir kwamba Mtume hakuona ndoto yoyote ila ina­jitokeza kama asubuhi. Waislamu wameafikiana kwa kauli moja kuwa hakuna wahyi wala sharia au Ijtihadi baada ya Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) ila ikiwa kauli ya mujtahidi inatokana na sharia ya Mwenyezi Mungu na Mtume wake.

Tazama Juz. 22 (33: 36-40) kifungu cha: ‘kwani utume uliishia kwa Muhammad?’ na Juz. 27 (56: 75-96), kifungu cha ‘Uislamu na wanafikra wakuu wa Ulaya.’

Wapewe mafukara wahajiri waliotolewa majumbani mwao na mali yao kwa ajili ya kutafuta fadhila kutoka kwa Mwenyezi Mungu na radhi zake, na wanamsaidia Mwenyezi Mungu na Mtume wake.

Makusudio ya wahajiri hapa ni wale waliohama na Mtume kutoka Makka kwenda Madina kwa kutaka radhi za Mwenyezi Mungu na thawabu zake na katika kuusaidia Uislamu na kupigana jihadi katika njia yake. Hawa ndio waliofaa zaidi kupewa zaka kwa kutangulia kwao na juhudi yao na pia kuwa na haja nayo.

Anasema Tabari akinukuu kutoka kwa Qatada: “Wahajiri hawa waliacha majumba yao, mali na familia kwa kumpenda Mwenyezi Mungu na Mtume wake.

Wakachagua Uislamu pamoja na shida zake. Hali ilifikia mtu anafunga jiwe tumboni ili kuuzuia mgongo wake na njaa na kuchim­ba shimo wakati wa kipupwe kuwa ndio blanketi ya kujifunika.

Sijaona wasifu wa maswahaba uliokuwa fasaha zaidi kuliko aliousema Imam Zaynul-abidin(a.s) akiwa anawaombea Mwenyezi Mungu (s.w.t) awatakabalie matendo yao; kwa kusema:

“Ewe Mola! Hasa maswahaba wa Muhammad ambao walikuwa na usuhuba mzuri, wakawa na majaribu mema katika kumsaidia kwake. Wakamwitikia alipowaeleza hoja ya ujumbe wake. Wakapigana na mababa zao na watoto wao ili kuuthibisha unabii wake na wakashinda kupitia kwake. Waliozingirwa na mapenzi wakitarajia biashara isiyo na hasara kwa ajili ya kumpenda kwake.

Wakatengwa na jamaa zao waliposhikamana na kamba yake. Udugu ulikwisha walipotulia chini ya kivuli cha udugu wake. Basi ewe Mola usiwasahu kwa yale waliyoyaacha kwa ajili yako. Na uwa­ ridhie kwa radhi zako.”

Hao ndio wa kweli katika imani na jihadi yao, kwa kauli na vitendo.

4

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE

وَالَّذِينَ تَبَوَّءُوا الدَّارَ وَالْإِيمَانَ مِن قَبْلِهِمْ يُحِبُّونَ مَنْ هَاجَرَ إِلَيْهِمْ وَلَا يَجِدُونَ فِي صُدُورِهِمْ حَاجَةً مِّمَّا أُوتُوا وَيُؤْثِرُونَ عَلَىٰ أَنفُسِهِمْ وَلَوْ كَانَ بِهِمْ خَصَاصَةٌ وَمَن يُوقَ شُحَّ نَفْسِهِ فَأُولَـٰئِكَ هُمُ الْمُفْلِحُونَ ﴿٩﴾

9. Na waliofanya maskani na imani yao kabla yao, wanawapenda waliohamia kwao wala hawapati dhiki kati­ka vifua vyao kwa walivyope­wa, na wanawapendelea kuliko nafsi zao, ingawa wao wenyewe ni wahitaji. Na mwenye kue­pushwa na uchoyo wa nafsi yake, basi hao ndio wenye kufaulu.

وَالَّذِينَ جَاءُوا مِن بَعْدِهِمْ يَقُولُونَ رَبَّنَا اغْفِرْ لَنَا وَلِإِخْوَانِنَا الَّذِينَ سَبَقُونَا بِالْإِيمَانِ وَلَا تَجْعَلْ فِي قُلُوبِنَا غِلًّا لِّلَّذِينَ آمَنُوا رَبَّنَا إِنَّكَ رَءُوفٌ رَّحِيمٌ ﴿١٠﴾

10. Na waliokuja baada yao wanasema: Mola wetu! Tughufirie sisi na ndugu zetu waliotutangulia kwa Imani, wala usijaalie ndani ya nyoyo zetu undani kwa walioamini. Mola wetu! Hakika Wewe ni Mpole Mwingi wa rehema.

أَلَمْ تَرَ إِلَى الَّذِينَ نَافَقُوا يَقُولُونَ لِإِخْوَانِهِمُ الَّذِينَ كَفَرُوا مِنْ أَهْلِ الْكِتَابِ لَئِنْ أُخْرِجْتُمْ لَنَخْرُجَنَّ مَعَكُمْ وَلَا نُطِيعُ فِيكُمْ أَحَدًا أَبَدًا وَإِن قُوتِلْتُمْ لَنَنصُرَنَّكُمْ وَاللَّـهُ يَشْهَدُ إِنَّهُمْ لَكَاذِبُونَ ﴿١١﴾

11. Je, Huwaoni wanaofanya unafiki wanawaambia ndugu zao waliokufuru katika Watu wa Kitabu: Mkitolewa na sisi lazima tutatoka pamoja nanyi, wala hatutamtii yeyote kabisa dhidi yenu.

Na mkipig­wa vita lazima tutawasaidia. Na Mwenyezi Mungu ana­shuhudia kuwa hao hakika bila ya shaka ni waongo.

لَئِنْ أُخْرِجُوا لَا يَخْرُجُونَ مَعَهُمْ وَلَئِن قُوتِلُوا لَا يَنصُرُونَهُمْ وَلَئِن نَّصَرُوهُمْ لَيُوَلُّنَّ الْأَدْبَارَ ثُمَّ لَا يُنصَرُونَ ﴿١٢﴾

12. Wakitolewa hawatatoka pamoja nao na wakipigwa vita hawatawasaidia. Na kama wakiwasaidia basi watageuza migongo; Kisha hawatanusuriwa.

لَأَنتُمْ أَشَدُّ رَهْبَةً فِي صُدُورِهِم مِّنَ اللَّـهِ ذَٰلِكَ بِأَنَّهُمْ قَوْمٌ لَّا يَفْقَهُونَ ﴿١٣﴾

13. Hakika nyinyi ni tishio zaidi katika vifua vyao kuliko Mwenyezi Mungu. Hayo ni kwa kuwa hao ni watu wasio­fahamu.

لَا يُقَاتِلُونَكُمْ جَمِيعًا إِلَّا فِي قُرًى مُّحَصَّنَةٍ أَوْ مِن وَرَاءِ جُدُرٍ بَأْسُهُم بَيْنَهُمْ شَدِيدٌ تَحْسَبُهُمْ جَمِيعًا وَقُلُوبُهُمْ شَتَّىٰ ذَٰلِكَ بِأَنَّهُمْ قَوْمٌ لَّا يَعْقِلُونَ ﴿١٤﴾

14. Hawatapigana nanyi kwa mkusanyiko isipokuwa katika vijiji vilivyozatitiwa kwa ngome au nyuma ya kuta. Wao kwa wao vita vyao ni vikali. Utawadhania kuwa wako pamoja, kumbe nyoyo zao ni mbali mbali. Hayo ni kwa kuwa wao ni watu wasio na akili.

كَمَثَلِ الَّذِينَ مِن قَبْلِهِمْ قَرِيبًا ذَاقُوا وَبَالَ أَمْرِهِمْ وَلَهُمْ عَذَابٌ أَلِيمٌ ﴿١٥﴾

15. Ni kama mfano wa waliokuwa kabla yao hivi karibuni. Walionja ubaya wa mambo yao. Nao watapata adhabu iliyo chungu.

WANAWAPENDELEA KULIKO NAFSI ZAO

Aya 9 – 15

MAANA

Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kubainisha daraja ya wahajiri katika Aya iliyotangulia, sasa anabainisha daraja ya Answar, kwa kusema, kama ifuatavyo:-

Na waliofanya maskani na Imani yao kabla yao, wanawapenda waliohamia kwao.

Makusudio ya maskani hapa ni Madina. Maana ni kuwa Answar, wenyeji wa Madina, walimsaidia Mtume pamoja na wale waliohama naye. Wakajitolea kwa nafsi zao na mali zao; bali waliwapendela wao kuliko nafsi zao; kama itakavyoashiria Aya.

Miongoni mwa Aya zilizoshuka kwa ajili ya Answar ni:

وَالَّذِينَ آمَنُوا وَهَاجَرُوا وَجَاهَدُوا فِي سَبِيلِ اللَّـهِ وَالَّذِينَ آوَوا وَّنَصَرُوا أُولَـٰئِكَ هُمُ الْمُؤْمِنُونَ حَقًّا لَّهُم مَّغْفِرَةٌ وَرِزْقٌ كَرِيمٌ ﴿٧٤﴾

“Na wale waliokaribisha na kusaidia, hao ndio waumini kweli, wana wao maghufira na riziki njema.” Juz. 10 (8:74).

Wala hawapati dhiki katika vifua vyao kwa walivyopewa Wahajiri.

Mwanzoni Wahajiri walikuwa ni mafukara zaidi katika Madina wakipata tabu. Lau si Answar wangelikufa na njaa. Mtume(s.a.w.w) alikuwa akiwapa sadaka mafukara na hawapi matajiri na walio na uwezo wa kuchuma.

Kwa hiyo alikuwa akiwapa kipaumbele Wahajiri; mara nyingine akiwapa ngawira wao tu. Answar walikuwa wakiliridhia hilo bila ya kuona choyo wala dhiki nyoyoni, na wakiona ni haki kabisa. Ndio akasajili Mwenyezi Mungu (s.w.t) sifa zao hizi kwenye Kitabu chake.

Na wanawapendelea kuliko nafsi zao, ingawa wao wenyewe ni wahitaji.

Kumpendela mwingine kuliko nafsi yake mtu, akiwa na mahitaji, hakuwezi kulinganihswa na jambo lolote isipokuwa kujitolea mhanga. Imeelezwa katika vitabu vya Tafsir na Historia kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) aliwaambia Answar: “Mkipenda ngawira hii iwe baina yenu na Wahajiri, lakini mshirikiane nao katika mali yenu, au muwaachie ngawira na nyinyi mbaki na mali yenu. Answar wakasema: bali tutawaachia ngawira na tutashirikiana nao katika mali yetu ewe Mjumbe wa Mwenyezi Mungu. Hapo Mtume akawaombea dua na kusema: “Ewe Mwenyezi Mungu! Warehemu Answar na watoto wa Answar.”

Na mwenye kuepushwa na uchoyo wa nafsi yake, basi hao ndio wenye kufaulu.

Uchoyo ni mama wa maovu. Mwenye kuuitikia utamzuia na kila heri, na mwenye kuushinda kwenye nafsi yake basi atakuwa ameikinga na kila uovu na hatari.

Na waliokuja baada yao wanasema: Mola wetu! Tughufirie sisi na ndugu zetu waliotutangulia kwa Imani.

Yaani waliokuja baada ya Answar na Wahajiri. Makusudio ya waliokuja baada yao ni kila mwenye kufuata sera mpaka siku ya Kiyama, wala haku­na njia ya kuwahusisha Tabiina (waliowafuatia maswahaba). Kwa sababu linalozingatiwa ni matendo sio mahali fulani wala wakati. Maswahaba hawakufikia walipokuwa ila ni kwakuwa walisikilza kauli wakafuata mazuri yake.

Wala usijaalie ndani ya nyoyo zetu undani kwa walioamini.

Ni muhali kabisa kuwa pamoja imani na undani. Inawezekana mtu kujiwekea undani?

Mola wetu! Hakika Wewe ni Mpole Mwingi wa rehema kwa waja wako walioitakasa dini yao na nyoyo zao kutokana undani na unafiki.

Je, Huwaoni wanaofanya unafiki wanawaambia ndugu zao walioku­furu katika Watu wa Kitabu: Mkitolewa na sisi lazima tutatoka pamo­ja nanyi, wala hatutamtii yeyote kabisa dhidi yenu. Na mkipigwa vita lazima tutawasaidia.

Makusudio ya watu wa Kitab hapa ni Bani Nadhir, ndugu wa wanafiki katika ukafiri na uadui kwa Mtume. Aya inaashiria tukio maalum. Pale Mtume(s.a.w.w) alipotangaza vita dhidi ya Bani Nadhir, wanafiki wakion­gozwa na Abadallah bin Ubayya waliwaambia: piganeni na Muhammad na sisi tuko na nyinyi, akiwapiga nasi tutampiga na wakiwatoa Madina tuta­toka nanyi; hatutamsikiliza Muhammad wala mwenginewe.

Na Mwenyezi Mungu anashuhudia kuwa hao hakika bila ya shaka ni waongo kwenye kauli yao na ahadi yao.

Wakitolewa Bani Nadhirhawatatoka pamoja nao wanafiki,na wakipigwa vita hawatawasaidia. Na kama wakiwasaidia basi watageuza migongo;

Hii ndio hali ya mnafiki, ulimi wake unahalifiwa na moyo wake na dhahiri yake inahalifiwa na siri yake.

Kisha hawatanusuriwa wala kunufaika na kwa vitimbi na unafiki wao.

Hakika nyinyi ni tishio zaidi katika vifua vyao kuliko Mwenyezi Mungu. Hayo ni kwa kuwa hao ni watu wasiofahamu.

Wanafiki wanawaogopa waumini kwa ukali wao wa vita, kwa sababu wao wanatazamia shari ya haraka wala hawatazimii adhabu inayokuja Akhera.

Hawatapigana nanyi kwa mkusanyiko isipokuwa katika vijiji vilivyo zatitiwa kwa ngome, au nyuma ya kuta.

Mayahudi hawakabiliani na waumini uso kwa uso katika uwanja wa vita, bali wanajificha kwenye mitaa yao nyuma ya ngome na kuta na kuwarushia waumini mishale na mawe; kama ilivyo hali ya mwoga.

Wao kwa wao vita vyao ni vikali. Utawadhania kuwa wako pamoja, kumbe nyoyo zao ni mbali mbali.

Wao wana nguvu kwa maandalizi yao na idadi yao, lakini masilahi na hawa za nafsi zimewatawanyisha. Wao wamechangukana, hata kama wanajionyesha kuwa na umoja na mapenzi.

Lau wangelikuwa na umoja na kupendana wangeliwatokea kupambana nanyi, lakini hawakupigana nanyi. Hili liko kwa wayahudi na wasiokuwa wayahudi, kwani umoja ni nguvu hata kama idadi na nyenzo ni ndogo, na utengano ni udhaifu hata kama kuna nyenzo na wingi wa watu.

Tumeshuhudia ushindi wa watu wasio na haki wachache juu ya walio na haki wengi na wenye nyenzo. Siri ni utengano wa hawa kwenye haki yao na umoja wa wale kwenye batili yao.

Hayo ni kwa kuwa wao ni watu wasio na akili ya kufahamu kuwa umoja ni nguvu na utengano ni udhaifu. Ni kama mfano wa waliokuwa kabla yao hivi karibuni. Walionja ubaya wa mambo yao. Nao watapata adhabu iliyo chungu.

Mayahudi walijenga uadui na Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w ) ; ni sawa na hali ya makafiri wa kikuraishi na wengineo waliompiga vita Mtume; pale walipoishia kwenye fedheha ya duniani na Akhera ni adhabu ya kuungua.

كَمَثَلِ الشَّيْطَانِ إِذْ قَالَ لِلْإِنسَانِ اكْفُرْ فَلَمَّا كَفَرَ قَالَ إِنِّي بَرِيءٌ مِّنكَ إِنِّي أَخَافُ اللَّـهَ رَبَّ الْعَالَمِينَ ﴿١٦﴾

16. Ni kama mfano wa Shetani anapomwambia mtu: kufuru. Na akikufuru humwambia: Mimi si pamoja nawe. Hakika mimi namwogopa Mwenyezi Mungu, Mola wa walimwengu wote.

فَكَانَ عَاقِبَتَهُمَا أَنَّهُمَا فِي النَّارِ خَالِدَيْنِ فِيهَا وَذَٰلِكَ جَزَاءُ الظَّالِمِينَ ﴿١٧﴾

17. Basi ikawa mwisho wa wote wawili hao ni kuingia Motoni, wadumu humo daima; na hayo ndiyo malipo ya madhal­imu.

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا اتَّقُوا اللَّـهَ وَلْتَنظُرْ نَفْسٌ مَّا قَدَّمَتْ لِغَدٍ وَاتَّقُوا اللَّـهَ إِنَّ اللَّـهَ خَبِيرٌ بِمَا تَعْمَلُونَ ﴿١٨﴾

18. Enyi mlioamini! Mcheni Mwenyezi Mungu, na kila nafsi iangalie inayoyatan­guliza kwa ajili ya Kesho. Na mcheni Mwenyezi Mungu. Hakika Mwenyezi Mungu ana habari za mnayoyatenda.

وَلَا تَكُونُوا كَالَّذِينَ نَسُوا اللَّـهَ فَأَنسَاهُمْ أَنفُسَهُمْ أُولَـٰئِكَ هُمُ الْفَاسِقُونَ ﴿١٩﴾

19. Wala msiwe kama wale waliomsahau Mwenyezi Mungu, na Yeye akawasa­haulisha nafsi zao. Hao ndio mafasiki.

لَا يَسْتَوِي أَصْحَابُ النَّارِ وَأَصْحَابُ الْجَنَّةِ أَصْحَابُ الْجَنَّةِ هُمُ الْفَائِزُونَ ﴿٢٠﴾

20. Hawawi sawa watu wa Motoni na watu wa Peponi. Watu wa Peponi ndio wenye kufuzu.

AKIKUFURU HUMWAMBIA MIMI NIKO MBALI NAWE

Aya 16 – 20

MAANA

Ni kama mfano wa Shetani anapomwambia mtu: kufuru. Na akikufu­ru humwambia: Mimi si pamoja nawe. Hakika mimi namwogopa Mwenyezi Mungu, Mola wa walimwengu wote.

Wanafiki waliwaambia Bani Nadhir: “Piganeni na Muhammad na sisi tuko pamoja nanyi katika vita,” lakini yalipowafika yaliowafika, walijificha kwenye viota vyao na hawakuonekana hata athari yao.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) ameifananisha hali ya wanafiki na Bani Nadhir na hali ya shetani na mtu mwenye kutenda dhambi. Huwa anamhadaa kwa ufisadi na upotevu na kumpa tamaa ya amani. Mambo yakichacha humwacha na adhabu na maangamizi na kujitenga naye na kudhihirisha hofu kutoka kwa Mwenyezi Mungu.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 10 (8:48) na Juz. 13 (14:22).

Basi ikawa mwisho wa wote wawili hao ni kuingia Motoni, wadumu humo daima; na hayo ndiyo malipo ya madhalimu.

Wawili ni shetani na mtu aliyeingia kwenye mtego wake. Maana yako wazi. Kwa ufupi ni kuwa kila mmoja, mwenye kuhadaa na mwenye kuhadaiwa, atakuwa katika Jahannam ambayo ni marejeo mabaya.

Enyi mlioamini! Mcheni Mwenyezi Mungu, ambaye nyinyi mko mikononi mwake, na mwenye kumcha Mwenyezi Mungu humfanyia wepesi mambo yake; kama anavyosema Mwenyezi Mungu katika Qur’an (65:4).

Na kila nafsi iangalie inayoyatanguliza kwa ajili ya Kesho.

Kila analolifanya mtu katika maisha haya huwa amelifanya kwa ajili ya Akhera. Mwenye busara anaangalia kwenye dunia yake kwa mtazamo wa mwenye kuicha kwa wema sio mwenye kuchukua anasa zake.

Na mcheni Mwenyezi Mungu. Hakika Mwenyezi Mungu ana habari za mnayoyatenda.

Mwenyezi Mungu anamjua mwenye kuamini kwa kauli na vitendo na mwenye kumwamini kwa fikra tu anayoisema na kuisahau kwenye viten­do. Mwenyezi Mungu (s.w.t) amelikariri jambo la takua kwa ukomo wa kuhimiza na kupendekeza.

Wala msiwe kama wale waliomsahau Mwenyezi Mungu, na Yeye akawasahaulisha nafsi zao.

Walisahau kufanya kwa amri ya Mwenyezi Mungu na Mwenyezi Mungu akawasahaulisha kufanya kwa masilahi ya nafsi zao. na aliyedanganyika zaidi katika watu ni yule aliyejisahau na asifanye kwa ajili ya usalama wake kujiepusha na maangamizi.

Hao ndio mafasiki. Kwa sababu hawakunufaika na ubainifu wa Mwenyezi Mungu na kupata funzo kwa mawaidha yake.

Hawawi sawa watu wa Motoni na watu wa Peponi. Watu wa Peponi ndio wenye kufuzu.

Vipi atakuwa sawa mwema na mwovu? Umetangulia mfano wake katika Aya kadhaa miongoni mwazo ni Juz. 21 (32:18).

لَوْ أَنزَلْنَا هَـٰذَا الْقُرْآنَ عَلَىٰ جَبَلٍ لَّرَأَيْتَهُ خَاشِعًا مُّتَصَدِّعًا مِّنْ خَشْيَةِ اللَّـهِ وَتِلْكَ الْأَمْثَالُ نَضْرِبُهَا لِلنَّاسِ لَعَلَّهُمْ يَتَفَكَّرُونَ ﴿٢١﴾

21. Lau tungelieiteremsha hii Qur’an juu ya mlima, basi bila ya shaka ungeliuona ukinyenyekea, ukipasuka kwa hofu ya Mwenyezi Mungu. Na hiyo ni mifano tunawapigia watu ili wafikiri.

هُوَ اللَّـهُ الَّذِي لَا إِلَـٰهَ إِلَّا هُوَ عَالِمُ الْغَيْبِ وَالشَّهَادَةِ هُوَ الرَّحْمَـٰنُ الرَّحِيمُ ﴿٢٢﴾

22. Yeye ndiye Mwenyezi Mungu, ambaye hapana mungu isipo kuwa Yeye tu, Mwenye kuya­jua yaliyofichikana na yanay­oonekana. Yeye ndiye Mwingi wa rehema, Mwenye kurehemu.

هُوَ اللَّـهُ الَّذِي لَا إِلَـٰهَ إِلَّا هُوَ الْمَلِكُ الْقُدُّوسُ السَّلَامُ الْمُؤْمِنُ الْمُهَيْمِنُ الْعَزِيزُ الْجَبَّارُ الْمُتَكَبِّرُ سُبْحَانَ اللَّـهِ عَمَّا يُشْرِكُونَ ﴿٢٣﴾

23. Yeye ndiye Mwenyezi Mungu ambaye hapana mungu isipo kuwa Yeye tu. Mtakatifu, Mwenye salama, Mtoaji wa amani, Mwangaliaji, Mwenye nguvu, Jabari, Mkubwa; Ametakasika Mwenyezi Mungu na hayo wanay­omshirikisha nayo.

هُوَ اللَّـهُ الْخَالِقُ الْبَارِئُ الْمُصَوِّرُ لَهُ الْأَسْمَاءُ الْحُسْنَىٰ يُسَبِّحُ لَهُ مَا فِي السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ وَهُوَ الْعَزِيزُ الْحَكِيمُ ﴿٢٤﴾

24. Yeye ndiye Mwenyezi Mungu, Muumbaji, Mtengenezaji, Mtia sura, Mwenye majina mazuri kabisa. Kinamsabihi kilicho katika mbingu na ardhi, naye ni Mwenye nguvu, Mwenye hikima.

LAU TUNGELIITERMSHA HII QUR’ANI JUU MLIMA

Aya 21 – 24

MAANA

Lau tungelieiteremsha hii Qur’an juu ya mlima, basi bila ya shaka ungeliuona ukinyenyekea, ukipasuka kwa hofu ya Mwenyezi Mungu.

Hii ni kiasi cha kukadiria tu, kunakofahamika kutokana na neno ‘Lau.’ Lengo ni kubainisha ukuu wa Qur’an, kwamba ina nguvu na athari; kiasi ambacho lau itateremshwa kwenye jabali basi lingenyenyeka na kulainika pamoja na ugumu wake. Pia lingelipasuka na kuanguka kwa kumwogopa Mwenyezi Mungu. Basi vipi mtu ambaye anaumizwa na chawa na kufa kwa kusongwa koo na jasho humfanya anuke; kama alivyosema Amirul Muminin, Ali(a.s) ?

Ana nini mtu huyu mnyonge, “anayesikia Aya za Mwenyezi Mungu akisomewa, kisha anang’ng’ania huku akijivuna, kama kwamba hakuzisikia. ” Juz. 25 (45:8).

Je, ni kwa kuwa moyo wake ni mgumu kama jabali ambalo limekazana sana, au ni ujinga, inadi na kung’ang’ania upotevu?

Na hiyo ni mifano tunawapigia watu ili wafikiri, katika hikima ya Qur’an, mawaidha yake, dalili yake, na ubainifu wake, na waongoke, kwa nuru yake, kwenye njia ya usawa, lakini:

إِنَّ فِي ذَٰلِكَ لَذِكْرَىٰ لِمَن كَانَ لَهُ قَلْبٌ أَوْ أَلْقَى السَّمْعَ وَهُوَ شَهِيدٌ ﴿٣٧﴾

“Hakika katika hayo kuna ukumbusho kwa mwenye moyo au akatega sikio naye ni shahidi.”

Juz. 26 (50:37).

Baada ya hayo yote, hakika ukuu wa Qur’an ni ukuu wa Mwenyezi Mungu (s.w.t). Walisema wakale: maneno ni sifa ya mwenye kusema; hasa yale yanayorudia ilimu yake.

Ndio maana Mwenyezi Mungu akaisifia Qur’an kwa sifa zake; kama vile nguvu, hekima, utukufu, ukuu, nuru, haki, rehe­ma, ukweli n.k.

Kisha Mwenyezi Mungu (s.w.t) akajisifu kwa sifa zake tukufu akasema:Yeye ndiye Mwenyezi Mungu, ambaye hapana mungu isipo kuwa Yeye tu, apasaye kuabudiwa kwa haki, anayesifika kwa sifa zote nzuri za ukamilifu; zikiwemo hizi zifuatazo:-

Mwenye kuyajua yaliofichikana na yanayoonekana . Anayajua yaliyoghaibu kwa watu na yaliyo dhahiri.

Yeye ndiye Mwingi wa rehema, Mwenye kurehemu . Sifa mbili hizi zimetokana na rehema kwa maana ya hisani. Inawezekana kuwa kuchanganywa matamko mawili ni kuashiria kuwa rehema yake imeenea kila kitu, hata katika hali ya kughadhibika kwake; na kwamba kuikatia tamaa ni kufuru na upotevu.

Yeye ndiye Mwenyezi Mungu ambaye hapana mungu isipo kuwa Yeye tu. Huu ni msisitizo wa tawhid. Yeye niMfalme; ni wake ufalme wa mbingu na ardhi, Ndiye anayetoa uhai na kufisha.

Mtakatifu; yaani ametakasika na yasiyolaikiana na utukufu wake.Mwenye salama ; kwa sababu inatokana na Yeye mtukufu utulivu na amaniMtoaji wa amani ; Anawapa thawabu waumini na anawapa amani ya adhabu ya moto.Mwangaliaji ; Mwenye kuchunga na kuhifadhi.

Mwenye nguvu ; asiyeshindwa wala kuzidiwa nguvu.Jabari ; Aliye juu bila ya kufikiwa.Mkubwa; Ana ukubwa na utukufu.Ametakasika Mwenyezi Mungu na hayo wanayomshirikisha nayo , ya kuwa na mshirika, mke na mtoto.Yeye ndiye Mwenyezi Mungu, Muumbaji, Mtengenezaji .

Hizi ni sifa mbili tofauti. Neno mtengenezaji tumelifasiri kutokana na neno Bariu ambalo imesemekana kuwa hapa lina maana ya kuwa mbali na upun­gufu.Mtia sura ; Mwenye kuumba sura na umbo.Mwenye majina mazuri kabisa.

Kila jina lake Mwenyezi Mungu Mtukufu ni zuri na ni kuu. Tazama Juz. 9 (7:180) Kifungu cha: ‘Je, majina ya Mwenyezi Mungu ni hayo hayo?’

Kinamsabihi kilicho katika mbingu na ardhi, naye ni Mwenye nguvu, Mwenye hikima.

Tasbihi inakuwa kwa lugha ya maneno na lugha ya hali. Tazama Juz. 15 (15:44) kifungu cha ‘Kila kitu kinamsabihi.

MWISHO WA SURA YA HAMSINI NA TISA: SURAT AL-HASHR

6

DALILI ZA KIAMA

KUANGAMIA KWA MIJI MIKUU:

Vita na majanga Miongoni mwa mambo aliyoyasema Mtume kuhusiana na zama za mwisho ni hili:

Miji mikuu itaangamia na itakuwa kana kwamba haikupata kuwepo hapo kabla (Al-Muttaq Al-Hindi Al Burhan fi Alamat Al Mahadi Akhir al Zaman)

Kuangamia kwa miji mikuu iliyozungumzwa katika hadithi hii kunatukumbusha maangamizi ambayo yanatokea hivi leo kutokana na vita na majanga mbali mbali ya asili. Silaha za kisasa za Nyuklia, Madege ya Kivita, Mabomu, Makombora na Zana nyingine za kisasa zimesababisha maangamizi yasiyosemeka.

Zana hizi za hatari zimeleta kiwango kikubwa cha maangamizi ambacho dunia haijapa kukiona hapo kabla. Kwahakika miji mikuu ndio imekuwa malengo makuu ya mashambulizi na imekuwa ikiathirika zaidi kutokana na maangamizi haya. Maangamizi yasiyo na mfano ya vita ya pili ya dunia ni kielezeo cha haya. Kwa kutumika bomu la Atomic katika vita kuu ya dunia, miji ya Hiroshima na Nagasaka iliangamizwa kabisa.

Kutokana na Mabomu mazito, miji mikuu ya Ulaya na miji mingine mikubwa imepata kiwango kikubwa cha hasara. Buku la marejeleo (Encylopedia Britannica) linaelezea hasara iliyosababishwa na vita kuu ya pili ya dunia katika miji ya Ulaya: Maangamizi yaliyotokea yameigeuza sehemu kubwa ya Ulaya kuwa kama taka taka na ilimalizwa na mabomu ya moto, bara bara zilijaa mashimo matupu, sura ya nchi ilikuwa giza tupu njia za reli zikaharibiwa na kutofanya kazi, madaraja yalibomolewa na bandari zilijaa Meli. Berin, anasema Jenerali Lusias D. Clay, Naibu Gavana wa Jeshi katika ukanda wa Post war German, lilikuwa kama jiji la wafu.

Kwa kifupi maangamizi ambayo yalisababishwa na vita ya pili ya dunia yanashabihiana kabisa na hadithi ya Mtume (s.a.w.w) Sababu nyingine ya maangamizi ya miji mikuu ni majanga ya asili. Ni ukweli wa kitakwimu kuwa zama tunazoishi hivi leo zimeshuhudia kuongezeka kwa idadi na madhara ya majanga ya asili. Katika miaka kumi iliyopita, majanga ya asili yaliyosababishwa na mabadiliko ya hali ya hewa yalikuwa ni mambo ambayo hayakuwahi kutokea.

Maangamizi, Umasikini, mauaji, machafu kuongezeka Sababu nyingine ya maangamizi katika miji ni majanga ya asili. Kulingana na takwimu, zama zetu zimeshuhudia ongezeko la idadi na ukubwa wa majanga ya asili. Katika kipindi cha miaka kumi iliyopita kulikuwa na majanga yaliyosababishwa na mabadiliko ya hali ya hewa. Haya yalikuwa ni majanga ya aina yake.

Hatari kubwa ya uchafuzi wa hali ya hewa unaosababishwa na viwanda ni tishio kwa dunia nzima. Viwanda vinavuruga urari wa angahewa ya dunia na kuongeza mabadiliko ya hali ya hewa. Mwaka 1998 ulikuwa ni mwaka wa joto kali sana duniani tangu rekodi za hali ya hewa zianze kuwekwa. Kwa mujibu wa maelezo ya kituo cha taarifa za hali ya hewa cha Marekani, idadi kubwa ya majanga yaliyotokana na hali ya hewa ilikuwa mwaka huo wa 1998.

Kwa mfano, Kimbunga kimeelezewa na wachunguzi wengi kuwa ndio janga baya mno la kimaumbile lililoikumba Amerika ya kati. Katika miaka michahe iliyopita vimbunga, dhoruba, tufani na majanga mengine yameleta maangamizi katika bara la Amerika na katika sehemu nyingine kadha wa kadha za dunia. Mbali na hayo mafuriko nayo yameleta maangamizi katika maeneo kadhaa ya watu. Aidha mitetemeko ya ardhi, Volkeno nayo pia yamesababisha maangamizi makubwa. Hivyo basi maangamizi yote haya yaliyotokea katika miji ni ishara muhimu.

Mitetemeko ya ardhi Hapana shaka kuwa katika historia, hakuna majanga ya asili ambayo yamewaathiri watu kwa kiasi kikubwa kama mitetemeko ya ardhi. Mitetemeko ya ardhi hutokea mahali popote na wakati wowote. Kwa karne zote mitetemeko ya ardhi imesababisha maafa na hasara kubwa ya mali. Kwa sababu hii tetemeko la ardhi ni janga linalohofiwa mno. Hata teknolojia ya karne ya Ishirini na Ishirini na moja imeweza kwa kiasi kidogo sana kuzuia uharibifu wa tetemeko la ardhi.

Tetemeko la ardhi la mwaka 1995 kule Kobe laweza kuwa somo kwa wale wanaodhani kuwa teknolojia itaweza kudhibiti maumbile. Itakumbukwa kuwa tetemeko hili la ardhi lilitokea bila kutarajiwa kwenye eneo kubwa la viwanda na usafirishaji. Licha ya ukweli kwamba lilidumu kwa sekunde ishirini tu, kama lilivyoripoti gazeti la Time, bado lilisababisha hasara ya dola bilioni 100. Kadhalika tetemeko la ardhi ndani ya bahari lililofahamika kama Tsunami fukweni mwa nchi za Indonesia, Thailand na ukanda mzima wa Pwani ya Asia, lilikuwa la aina yake kupata kutokea katika historia ya mwanaadamu.

Katika miaka michache iliyopita mitetemeko mikubwa ya ardhi imetokea mara kwa mara na ndio matishio makubwa ya maisha ya watu duniani kote. Tukiangalia takwimu zilizokusanywa na kituo cha taarifa za matetemeko ya ardhi cha Amerika mwaka 1999 tunaona kuwa mitetemeko ipatayo 20, 832 ilitokea sehemu mbali mbali duniani. Matokeo yake watu wanaokadiriwa kufikia 500,000 walikufa. Matukio yote haya yanakumbushia maneno ambayo Mtume (s.a.w) aliyasema miaka 1400 iliyopita: Kiama hakitasimama mpaka pale mitetemeko ya ardhi itakapotokea mara kwa mara. (Bukhari).

Katika Qur'an kuna aya kadhaa zinazobainisha uhusiano kati ya mitetemeko ya ardhi na zama za mwisho. Sura ya 99 inaitwa suratil Zil Zaala ambayo maana yake ni mtikisiko au tetemeko la ardhi. Sura hii yenye aya nane inaelezea mtetemeko mkubwa wa ardhi na inasema kuwa kufuatia mtetemeko huo siku ya hukumu itakuwa imefika. Watu watafufuliwa makaburini na kutoa hesabu ya amali zao kwa Mwenyezi Mungu na kupata malipo yao hata kwa jambo dogo sana walilolifanya:

Itakapotetemeshwa ardhi kwa mtetemesho wake mkubwa. Na itakapotoa ardhi mizigo yake, na binadamu akasema (wakati huo) (oh!) ina nini leo ardhi? Siku hiyo itatoa habari zake zote kwa kuwa Mola wake ameifunulia (ameiamrisha kufanya hayo). Siku hiyowatu watatoka (makaburini) vikundi vikundi ili waonyeshwe vitendo vyao. Basi anayefanya wema hata kwa kiasi cha uzito wa mdudu chungu ataona jazaa yake na anayefanya uovu hata kwa kiasi cha uzito wa mdudu chungu ataona jazaa yake. (99:1-8).

7

DALILI ZA KIAMA

UMASIKINI

Inafahamika kuwa umasikini ni ukosefu wa chakula, makazi, mavazi, huduma za afya na mahitaji mengine ya msingi kwa sababu ya kipato duni. Licha ya fursa zinazopatikana kutokana na maendeleo ya teknolojia, umasikini hivi leo ni moja kati ya matatizo makubwa kabisa yanayoukabili ulimwengu. Katika mabara ya Afrika, Asia, Amerika Kusini na Ulaya Mashariki watu wengi wanahangaika na njaa kila siku. Kwa sababu ya mgao mbaya wa rasilimali za ulimwengu umasikini umesababisha uwepo mgawanyiko kati ya nchi za kaskazini ya jangwa la sahara ambazo ni za ulimwengu wa kwanza na nchi za kusini maskini ambazo ni za ulimwengu wa tatu.

Ubeberu na Ubepari usio na mipaka unazuia mgawanyo wa kipato ulimwenguni kote na unakwaza maendeleo ya nchi changa na nchi zinazoendelea. Wakati ambapo kuna watu wachache wanaofurahia kipato kinachozidi mahitaji yao, kuna idadi kubwa ya watu wanaohangaika na matatizo ya umasikini na ufukara. Katika Ulimwengu wa leo umasikini umefikia hatua mbaya au kiwango kibaya sana.

Ripoti ya mwisho ya UNICEF ilieleza kuwa mmoja kati ya kila watu wanne duniani anaishi katika tabu na shida isiyoelezeka. Watu bilioni 1.3 duniani wanaishi kwa wastani wa chini ya dola moja kwa siku. Watu bilioni 3 duniani wanaishi kwa dola mbili kwa siku. Takribani watu bilioni 1.3 hawapati maji safi. Watu bilioni 2.6 hawapati maji salama.

Kwa mujibu wa ripoti ya shirika la chakula duniani, (FAO) , Mwaka 2000, watu milioni 826 duniani kote hawapati chakula cha kutosha. Kwa maneno mengine mmoja katika kila watu sita ana njaa. Katika miaka kumi iliyopita dhulma katika mgawanyo wa kipato imeongezeka kwa kiwango kisichosemeka.

Ripoti za umoja wa Mataifa zinaonesha kuwa, katika mwaka 1960 asilimia 20 (20%) ya watu wanaoishi katika nchi tajiri kabisa duniani walikuwa na pato lilozidi mara thelathini pato la nchi 20 masikini kabisa. Hadi kufikia mwaka 1995 iliongezeka mara 82. Kikiwa ni kielezeo cha kutoweka kwa haki ulimwenguni, mali za matajiri 225 wakubwa kabisa ulimwenguni ni sawa na pato la mwaka la asilimia 47 (47%) ya nchi masikini ulimwenguni.

Takwimu za sasa zinaonyesha yale ambayo Mtume (s.a.w.w) aliyasema juu ya kuongezeka kwa umasikini. Katika hadithi inabainishwa kuwa umasikini na njaa ni miongoni mwa dalili za kipindi cha kwanza cha zama za mwisho:

Masikini wataongezeka (Amal Al Diin Al Qazwin, Mufid Al Ulum wa Mubid Al humum) Kipato kitagawanywa kwa matajiri tu, hakuna mafao kwa masikini. (Tirmidhi). Ni dhahiri kuwa kipindi hicho kilichobashiriwa na Mtume (s.a.w.w) kinawiana na hali ya wakati wetu wa leo. Tukiangalia karne zilizopita tunaona kuwa shida na tabu zilizoletwa na ukame, vita na majanga mengine zilikuwa za muda mfupi na ziliishia katika eneo moja moja. Lakini umasikini na shida za leo ni za kudumu na sugu. Kwa hakika Mola wetu ni Mwingi wa Rehma, yeye hadhulumu watu lakini kwa sababu ya ukosefu wa shukurani wa wanadamu na maovu wanayoyafanya, umasikini na tabu vimeongezeka. Kwa hakika hali ya mambo ya kusikitisha inaonesha wazi kuwa dunia imetanzwa na uchoyo na ubinafsi.

Kuporomoka kwa maadili, kushamiri kwa ushoga na ukahaba Katika zama zetu za leo kuna janga kubwa linalohatarisha uhai wa jamii ulimwenguni. Mithili ya virusi vinavyoua mwili, janga hili linasababisha msiba mkubwa wa kijamii. Janga hilo ni mmomonyoko wa maadili ambayo husaidia kustawisha jamii. Ushoga, Ukahaba, uhusiano haramu wa kijinsia kabla ya ndoa na nje ya ndoa, Filamu za ngono, Picha za ngono, unyanyasaji wa kijinsia na ongezeko la maradhi ya zinaa, mashindano ya kukaa uchi maarufu ulimbwende, uuzaji na utumiaji wa vileo na dawa za kulevya miongoni mwa vijana ni miongoni mwa ishara kubwa za kuporomoka kwa maadili.

Mambo haya ndiyo yamekuwa yakizishughulisha jamii. Idadi kubwa ya watu haijali hatari hii inayozidi kuwa kubwa na wanaiona kama jambo la kawaida tu. Lakini takwimu zinaonesha kuwa kila siku ipitayo kiwango cha hatari kinazidi kuongezeka. Ongezeko la maradhi ya zinaa ni kigezo kikuu cha kusaidia kuonesha ukubwa wa matatizo yanayomkabili mwanadamu. Kwa mujibu wa rekodi za Shirika la Afya ulimwenguni magonjwa yanayotokana na zinaa yanachukuwa sehemu kubwa ya maradhi. Ripoti zinaonesha kuwa kati ya kesi mpya za magonjwa ya zinaa zinazokadiriwa kufikia milioni 333 kila mwaka ulimwenguni kote, Ukimwi ndio tatizo kubwa zaidi.

Takwimu za Shirika la Afya ulimwenguni (WHO) zinaonesha kuwa idadi ya vifo vinavyotokana na ugonjwa wa Ukimwi tokea pale ulipoanza imefikia watu milioni 18.8. Ripoti za shirika hilo kwa mwaka 2000 zinaielezea hivi hali ya mambo: "Ukimwi una nafasi ya kipekee katika kuleta athari mbaya za kijamii, kiuchumi na katika mipango ya sensa ya maendeleo".

Miongoni mwa mambo mabaya kabisa yanayozidi kushamiri ni ushoga. Katika baadhi ya nchi jambo hili limehalalishwa kama ndoa, linapewa heshima zote za ndoa na limeundiwa vyama na jumuiya. Duniani kote uovu huu unapingwa. Kushamiri kwa ushoga hivi leo kunatukumbusha hatima ya watu wa Lut waliokithiri katika uovu huu. Kama isemavyo Qur'an walipoukataa wito wa Lut kuiendea njia sahihi, Mwenyezi Mungu aliuangamiza mji na watu wake kwa maangamizi makubwa.

Ni dhahiri kuwa zile hadithi zinazoelezea zama za mwisho na mporomoko wa maadili zinathibitika hivi leo. Hadithi moja inasema kuwa kutoweka kwa aibu katika dhambi ya ukahaba ni dalili ya kiama:

Kutashitadi maingiliano haramu ya kijinsia wazi wazi (Bukhari). Saa hiyo itafika wakati uzinzi utakapokuwa umeenea sana (Al-Haythami, kitab al fitan) Kufifia kwa maadili na hisia ya aibu kunaelezwa kwa maneno haya:

Saa ya mwisho haitasimama hadi pale watu watakapofanya uzinzi njiani (njia wanazopita watu) ( Ibn Iban na Bazzar). Yafaa kukumbuka kuwa hivi sasa matukio ya ukahaba yanayochukuliwa na kamera za siri yamekuwa yakioneshwa katika Internate, vituo vya Televisheni na katika magazeti yanayoitwa ya ngono na udaku. Makahaba wanaingiliana na wateja wao wazi wazi katikati ya mitaa. Hali kadhalika kuna Filamu na picha nyingi zinazosambazwa ulimwenguni kote ambazo zinaonesha uzinzi unavyofanyika wazi wazi. Takriban katika miji mingi duniani makahaba wamekuwa wakisimama na wateja wao na kufanya mambo ya ajabu barabarani hasa nyakati za usiku.

Hii ni dalili nyingine ya kiama iliyobainishwa katika hadithi. Mamilioni ya watu wanaishuhudia wenyewe dalili hii duniani kote. Hadithi zifuatazo zinaonyesha kuwa kuibuka kwa ushoga kuwa jambo la kawaida la maisha ni ishara kuu ya zama zinazokaribia siku ya mwisho:

Wanaume watawaiga wanawake na Wanawake watawaiga wanaume. (Allama Jalaluddin Swiyuti, Durre- Mansuri). Watu watazama katika ushoga na usagaji (Al Mutaqi al Hindi, Muntakhab, Kanzul Ummaal).

Vitendo vya wanaume kuwaiga wanawake na wanawake kuwaiga Wanaume vimekuwa vingi hivi leo. Tunashuhudia Wanaume wanaosuka nywele zao na pia tunashuhudia Wanaume wanaowasuka nywele wanawake kwenye Masaluni na majumbani. Imekuwa ni aina ya ajira kwa wanaume hawa hasa Wamasai kupita mitaani kusuka nywele akina Mama.

Pia tunashuhudia Wanaume wakivaa hereni masikioni na vidani shingoni. Tunashuhudia teknolojia ikitumika vibaya kubadilisha maumbile ambako kumeleta kiroja cha mwanaume kubeba uzazi na kujifungua! Kwa upande mwingine tunashuhudia Wanawake wakivaa mavazi ya Wanaume, wakijaribu kuiga usemaji wa kiume. Wakioa wanawake wenziwao na wakifanya kazi za mitulinga. Tunashuhudia wanawake wakivaa mavazi yenye kuonesha vivazi vyao vya ndani na maungo mateke ili kushawishi uzinzi.

8

DALILI ZA KIAMA

KUKANUSHA DINI SAHIHI NA MAADILI YA QUR'AN

Hadithi zinazozungumzia dalili za siku ya mwisho zinatupa maelezo ya kina juu ya wakati ambao dalili hizi zitadhihirika. Twaweza kufahamikiwa kutokana na hadithi za Mtume (s.a.w.w) kuwa awamu ya kwanza ya zama za mwisho ni kipindi ambacho kitaonekana kuwa cha kidinidini, lakini kumbe ni kipindi ambacho kitaikataa kabisa dini ya Allah na maadili ya Qur'an.

Ni kipindi ambacho yale mambo yaliyobainishwa katika aya za Qur'an yatafumbiwa macho, dini itatumbukia katika mifarakano, migogoro, hamasa na ushabiki. Ibada zitafanywa kwa ria na dini itatumika kama biashara ya kujipatia faida na maslahi ya kidunia. Ni katika kipindi hiki ambapo Imani haitategemea elimu na utafiti bali itakuwa mwigo wa kufuata mkumbo tu na hamasa ya mtu. Katika kipindi hiki watu wanaoitwa Waislamu watakuwa wengi mno wakati ambapo wanazuoni wa kweli na Waislamu wenye Ikhlasi watakuwa wachache mno.

Zifuatazo ni dalili zilizotajwa na Mtume (s.a.w.w) Karne 14 zilizopita, dalili ambazo zinathibitika wazi wazi katika wakati tulionao: Kwa mujibu wa Qur'an, Mtume (s.a.w.w) anasema kuwa watu wake wameitelekeza Qur'an:

Na Mtume alikuwa akisema, Ewe Mola wangu! Hakika watu wangu wameifanya Qur'an hii kuwa kitu kilichoachwa. (25:30). Inabainishwa katika hadithi kuwa katika zama za mwisho muongozo wa Qur'an utatupiliwa mbali na watu watajitenga nao:

Karibia ya kusimama kwa saa kutakuwa na zama ambazo elimu ya (Qur'an) itatoweka na giza totoro litagubika (Bukhari).

Utakuja wakati wa uma wangu ambapo hakutabaki chochote kilichobaki katika Qur'an isipokuwa sura yake ya nje tu na hakutabaki chochote cha Uislamu isipokuwa jina lake tu na wao watajiita kwa jina hili ingawaje ni watu w aliombali kabisa na Uislamu. (Ibn Babuya, Thawab ul-A'amal). Mfano umetolewa katika suratil Jumaa aya 5:

Mfano wa wale waliopewa Taurat, kisha hawakuichukua kwa ktuitumia ni kama Punda anayebeba vitabu vikubwa vikubwa.

Hapana shaka kuwa aya hii inatoa onyo kwa Waislamu, ikiwakumbusha kuwa wajihadhari wasije wakatumbukia katika dhambi ileile nzito. Qur'an imeshushwa kama kitabu cha muongozo ambao watu waufuate.

Mtume (s.a.w.w) kasema kuwa licha ya ukweli kuwa Qur'an itasomwa lakini elimu na hekima iliyomo ndani yake hatazingatiwa. Hii ni dalili nyingine ya ule wakati wa zama za mwisho:

Utakuja wakati juu ya umma ambapo watu watasoma Qur'an lakini haitakwenda kokote isipokuwa itaishia kwenye makoo yao (haitaingia nyoyoni.) (Bukhari).

Mtume wa Allah alisema jambo fulani kisha akasema utatokea wakati ambapo elimu haitakuwepo tena. Aliuliza Ziyadi: Ewe Mtume wa Allah itatowekaje elimu licha ya ukweli kuwa tutakuwa tukiisoma Qur'an na kuwafundisha watoto wetu kuisoma na watoto wetu nao watawafundisha watoto wao kuisoma hadi siku ya kufufuliwa? Hapo Mtume akasema je Mayahudi na Wakristo hawasomi Taurati na Biblia na kutotenda kwa mujibu wa yale yaliyomo humo? (Ahmad, ibn Majah, Tirmidhi).

Watu kuitumia dini kwa malengo ya kidunia na kujivika ngozi ya kondoo waonekane wema. Kufuata maadili ya Wayahudi na Wakristo Ni dalili moja wapo ya kiama kuwa baadhi ya Waislamu watafuata nyendo za Wayahudi na Wakristo tena watawaiga kimasonge. Mtume (s.a.w.w) kasema:

"Kwa hakika mtafuata nyendo za watu waliokuwepo kabla yenu shubiri kwa shubiri na dhiraa kwa dhiraa (Inchi hadi Inchi) kiasi ambacho hata wakitumbukia kwenye shimo la Kenge nanyi pia mtawafuata humo" tukauliza, ewe Mtume wa Allaha, una maana kuwa ni Wayahudi na Wakristo? Akajibu, kama si wao ni nani tena? (Bukhari) kutokana na hadithi hiyo tunaona kuwa kabla ya zama za mwisho kutakuwa na mielekeo mibovu ya kifikra na kimaadili na kwamba tawala zitakazokuwepo zitajitenga mbali na ukweli na haki jambo litakalosababisha mfarakano mkubwa na kuwatoa watu katika mafundisho ya Mwenyezi Mungu.

Jambo la kuzingatia hapa ni kuwa maadili ya Wayahudi na Wakristo ndio maadili ya magharibi au ya Wazungu, na mifumo ya maisha iliyojitenga na Qur'an ndio mifumo ya Magharibi inayotawala dunia hivi leo.

Muumini na Kafiri Mtume wa Mwenyezi Mungu kasema:

Kabla ya saa ya mwisho kutakuwa na vurugu vurugu tupu ambapo mtu atakuwa Muumini asubuhi na Kafiri jioni yake au atakuwa Muumini jioni na Kafiri asubuhi yake. (Abuu Daudi) Kuna vielezeo vingi vinavyoonesha hali hiyo hivi leo. Mtu anaweza kuswali swala tano lakini akawa muasherati, anaweza kushinda kutwa nzima anaswali lakini usiku anazini, anaweza kushinda na swaumu kutwa nzima lakini usiku yuko na hawara au kimada, mwingine anaweza kuwa sala tano lakini muongo, mwizi, tapeli, mla rushwa, mla riba na kadhalika. Mseto huu wa Uumini na Ukafiri unaonekana kwa watu wengi hivi leo japo kwa sura tofauti.

Kutozingatia halali na haramu Dalili nyingine ya kiama ni kuwa watu hawatazingatia yaliyoharamishwa na Mwenyezi Mungu katika Qur'an. Mtume (s.a.w.w) kasema: Utafika wakati ambapo mtu hatojali kama vitu avipatavyo ni vya halali au ni vya haramu (Bukhari).

Wanazuoni wenye nyuso mbili Mtume (s.a.w.w) kasema:

Katika zama za mwisho baadhi ya watu wanaokubalika kama wanazuoni watakuwa wanafiki kweli kweli wenye nyuso mbili; Mbwa Mwitu watasoma katika zama za mwisho. Wale watakaoziona zama hizo waombe nusra kwa Mwenyezi Mungu kutokana na uovu wa wanazuoni hao. Kutakuwa na mafisadi kweli kweli. Unafiki ndio utakaoshitadi. (Tirmidhi, Nawadil al Usul.)

Kutatokea watu katika zama za mwisho ambao watajinufaisha kwa kutumia dini (Tirmidhi) Kutumia dini kwa malengo ya kidunia Mtume wa Allah kasema;

Katika zama za mwisho watu wataitumia dini kitapeli kwa malengo yao ya kidunia na kujivika ngozi za kondoo hadharani kuonesha unyenyekevu. Ndimi zao zitakuwa tamu kama sukari lakini nyoyo zao zitakuwa nyoyo za Mbwa mwitu. (Tirmidh).

Watu hawatoheshimu mipaka ya sheria za Kiislamu. Hawatochelea kuutumia Uislamu kwa ajili ya kujipatia maslahi yao. Watu watajali zaidi kuonekana wanatenda mambo kwa ajili ya Mwenyezi Mungu wakiwa hawana chembe ya wema, huruma na usaidizi kwa wanaowahubiria. Watakuwa wakiwakamua wafuasi wao kutoa kwa kutumia aya na mahubiri ya kukhofisha na kutumainisha hali yakuwa wao wenyewe hawana ukweli katika nafsi zao.

Katika zama za mwisho za umma wa walioamini, watu watapamba Misikiti lakini wataziacha nafsi zao katika maangamizi, watu ambao watashindwa kuitunza dini ya Mwenyezi Mungu kama wanavyozitunza nguo zao, watatelekeza majukumu ya dini yao kwa sababu ya shughuli zao, watu hawa watakuwa wengi.

9

DALILI ZA KIAMA

KUTOTEKELEZA AMRI YA KUTENDA MEMA NA KUEPUKA MABAYA

Miongoni mwa dalili za kukaribia kiama ni kuwa watu wanaojua kuwa Mwenyezi Mungu amewaamrisha kutenda mema na kuepuka uovu hawatatekeleza jambo hilo: Siku ya mwisho haitasimama mpaka watakapobakia watu ambao hawatajali mema na kamwe hawatozuia maovu (Ahmad).

Karibu na kusimama kwa kiama mambo mema yatapungua (Bukhari) Katika hadithi nyingine inabainishwa dalili ya kiama kuwa Waislamu walioamini watadhoofishwa kwa msukumo wa watenda dhambi:

Saa itafika pale sauti zitakapopazwa misikitini (Tirmidh) Saa itafika pale viongozi watakapokuwa madhalimu (Al Haithami, Kitab al Fitan)

Mtume (s.a.w.w) kasema:

katika zama za mwisho, kutakuwa na watu wachache sana wanaoweza kuitwa waumini: Utafika wakati kwa watu wangu ambapo misikiti itajaa watu lakini watakuwa hawana muongozo sahihi (Ibn Babuya, Thawab ul A'mal Hadith moja inasema kuwa waislamu wa kweli watalazimika kuficha imani zao na kufanya ibada kwa siri:

Wakati utafika ambapo wanafiki wataishi kwa siri miongoni mwenu na wenye imani watajaribu kuhuisha dini yao kwa watu wengine Katika Hadith ifuatayo inabainishwa ishara ya zama za mwisho kuwa Misikiti itafanywa sehemu za mikusanyiko ya kijamii tu. Utafika wakati ambapo watu watatumia misikiti kama vijiwe tu vya kukutania. Katika zama mwisho, watatokea watu watakaosoma Qur'an kwa ajili tu ya kujinufaisha badala ya kupata radhi za Allah:

Na aombe thawabu kwa Allah yule asomaye Qur'an. Kwa sababu katika zama za mwisho kutakuwa na watu wengi watakaosoma Qur'an na kutafuta malipo kwa watu wengine (Tirmidhi). Dalili nyingine ni kuwa Qur'an itasomwa kwa ajili ya kujifurahisha (kujiburudisha) tu kama vile wimbo:

Wakati Qur'an itakaposomwa mithili ya uimbaji wa nyimbo na wakati mtu atakapoheshimika (atakaposifika) kwa kuimba namna hiyo hata kama hana ilimu ( Al-Tabarani, Al-Kabir) Baadhi ya watu watakaotambuliwa kama Waislamu watakuwa na uelewa potofu juu ya kadari, wakati ambapo wengine wataamini nyota kuwa zinaweza kuwapatia ujuzi wa kujua maisha yao ya baadae. Hii ni dalili ya zama za mwisho:

Saa itafika wakati watu watakapoamini nyota na kukanusha Qadari (Al-Haythami, Kitab al Fitan) Licha ya ukweli kwamba Mwenyezi Mungu ameharamisha riba hivi leo riba ndio mtindo wa maisha. Katika Hadith ifuatayo hii inaelezewa kama dalili mojawapo ya ya kiama:

Bila shaka kitakuja kipindi ambacho hakuna hata mtu mmoja atakayesalimika na riba. Endapo mtu ataepuka riba kwa njia ya moja kwa moja basi hatoweza kuukwepa moshi (athari) utakaotokana nayo. Kwa kiasi fulani athari zake zitamfika tu (Imesimuliwa na Abu Huraira)

Hapa labda tutoe ufafanuzi kidogo. Katika ulimwengu wetu wa leo riba imejikita katika mifumo ya fedha na uchumi wa kitaifa na kimataifa. Aidha sekta za kiserikali na binafsi zinashiriki katika uchumi wa riba. Mabenki na makampuni binafsi ya kitaifa na kimataifa hasa yale yanayoendesha shughuli za ukopeshaji wa fedha au bidhaa yanatoza riba kwa viwango mbalimbali. Karibu Asasi zote za utoaji wa mikopo ya fedha zinatoza riba.

Kwa hali hiyo hakuna mtu ambaye anaweza kudai kuwa yeye amesalimika na riba. Maadam mfumo wa uchumi wa Taifa haukusalimika na riba basi sote tunahusika na jambo hili. Hivyo hadithi ya Mtume (s.a.w.w) inawafikiana kabisa na mazingira yetu.

Dalili nyingine ya zama za mwisho ni kuwa Hija itafanywa kwa ajili ya kusafiri tu, kufanya biashara, kujionesha tu na kuombaomba. Wakati huo utafika pale matajiri watakapokwenda Hija kwa malengo ya kusafiri kwa minajili ya kujifurahisha, biashara, kujifaharisha na kujionesha, na masikini kwenda kuomba. Imesimuliwa na Anas (r.a )

Tatizo kubwa ambalo Wanaadamu wanakabiliana nalo hivi leo ni kusambaratika kwa jamii. Kuporomoka huku kwaonekana katika vipengele mbali mbali vya maisha. Kuvunjika kwa familia, ongezeko la talaka na uzazi haramu ndio mambo ambayo yanapelekea kusambaratika kwa taasisi ya familia. Maisha hivi leo yamekuwa ya misukosuko, mashaka, huzuni, wasiwasi na vurugu tupu. Watu waliokosa maadili ya kiroho wanaona kuwa ili kuondokana na adha ya dunia basi bora wajitumbukize katika ulevi wa pombe na dawa za kulevya. Wengine wanaona kuwa hakuna ufumbuzi wa hali ngumu inayowakabili basi njia wanayoona itawatowa matatizoni ni kujinyonga. Moja ya Ishara kubwa za kuanguka kwa jamii ni kule kuongezeka kwa mambo ya haramu.

Kiwango cha uhalifu kimeongezeka kwa kiasi kinachowashangaza mabingwa wa maswala ya jamii. Ripoti ya uhalifu na haki ulimwenguni, "Universal Crime and Justice," Iliyotayarishwa na kituo cha udhibiti wa jinai cha umoja wa mataifa, United Nations' International Crime' imetoa tathmini ya jumla ya uhalifu ulimwenguni. Ripoti hiyo inasema:

Kimsingi, kama ilivyokuwa katika miaka ya themanini, kiwango cha uhalifu pia kiliendelea kuongezeka katika miaka ya tisini. Kila mahali ulimwenguni, katika kila kipindi cha miaka mitano, theluthi moja ya watu wanaoishi mijini wamekumbwa na mikasa ya uhalifu. Kote ulimwenguni vitendo vya wizi, ujambazi, utapeli, uasherati vimekuwa vikiongezeka siku hadi siku. Matukio haya, pamoja na sababu nyinginezo, yamekuwa yakihusishwa na athari mbaya za kiuchumi.

Kiwango cha utumiaji wa dawa mbali mbali za kulevya nacho kimeongezeka katika miaka ya karibuni. Watu hasa vijana wamekuwa wakibwia unga na kujidunga sindano zenye dawa za kulevya. Kwa kweli tatizo hili limeleta madhara ya kiafya, athari mbaya za kifamilia na kijamii.

Kwa hakika sababu za matatizo yote haya zimeelezwa katika Qur'an pale inaporejea historia ya jamii zilizopita. Kuporomoka kwa jamii na matatizo mbali mbali ni matokeo ya wanadamu kumsahau Mwenyezi Mungu na lengo halisi la maisha na hivyo kuyatupa maadili ya kiroho.

Matukio yote ya kuporomoka kwa jamii tunayoyashudia hivi leo tayari yalikwishabashiriwa na Mtume (s.a.w.w) karne 14 zilizopita. Mtume (s.a.w.w) amesema kuwa miongoni mwa dalili za zama za mwisho ni pale watu watakapokabiliana na vita na mabadiliko ya kijamii (Ahmad Diya"al diin al Kamush Khanawi, Ramuzi al ahadith). Zifuatazo ni hadith zinazohusiana na awamu ya kwanza ya zama za mwisho:

Kutakuwa na miaka ya udanganyifu ambapo mtu mkweli hatoaminiwa na muongo ataaminiwa (Ibn Kathir). Kutakuwa na miaka ya vurugu. Watu watamuamini muongo na kutomuamini yule anayesema ukweli. Watu hawatamuamini mtu mkweli na watamuamini yule ambaye ni fisiki. (Ahmad). Siku ya kiama haitakuja mpaka watu duni kabisa wawe watu wenye furaha kabisa (Tirmidh).

Kama inavyosomeka katika hadithi hizo kutakuwa na ongezeko la watu waovu ambapo wale wanaoonekana wakweli kumbe ni waongo na wale wanaoonekana waongo kumbe ndio wakweli. Hizi ni dalili za zama za mwisho. Hadithi moja inabainisha kuwa kutakuwa na watu wachache sana wakweli na kiasi kidogo sana cha pesa kitakachopatikana kwa kuzingatia kanuni na sheria za dini yetu:

Katika zama za mwisho watu watakuwa wakifanya biashara lakini hakutakuwa na mtu yeyote mkweli (Bukhari na Muslim). Ushahidi wa kweli utatupiliwa mbali na ushahidi wa uongo na kusingiziana ndivyo vitakavyoshamiri. Hii ni dalili nyingine ya zama za mwisho. Kwa hakika katika saa ya mwisho kutakuwa na ushahidi wa uongo na ufichaji wa ushahidi (Ahmed na Hakim). Kutakuwa na shutuma za uongo za mambo machafu na masingiziano. (Tirmidh)

Kigezo pekee ambacho kwacho watu watapimwa ubora wao ni mali, hashima itategemea mtu ni tajiri kiasi gani:

Kabla ya saa ya mwisho kufika, kutakuwa na salamu maalumu kwa watu wa tabaka fulani. (Ahamad) Hakutakuwa na hukumu mpaka pale salamu zitakapotolewa sio kwa watu bali kwa watu mahususi. (Mukhtasari Tazkira Khutub). Inasemwa katika hadithi kuwa dalili nyingine ni kuvurugika kwa uhusiano wa kijamii baina ya watu:

Ni wale watu ambao mtu anawajuwa tu ndio watakaopewa salamu (Ahmad Diyal al diya'al Din al Kamushi Khanawi, Ramuzi al ahadithi) Katika hadithi ifuatayo inaelezwa kuwa nafasi za kazi zitatolewa kwa watu wasio na sifa: Pale madaraka na mamlaka yatakapokwenda mikononi mwa watu wasio na sifa, basi hapo muisubiri ile saa (kiama). (Bukhari). Dalili nyingine ya zama hizo itakuwa ni kuvunjika kwa uhusiano wa wanafamilia, marafiki, majirani na kuvurugika kwa jamii na maadili:

Mtu kutokuwa na mapenzi na Mama yake na kumfurusha Baba yake (Tirmidh). Kwanza kutakuwa na sokomoko kwa mtu kuhusiana na familia yake, mali yake, nafsi yake, watoto wake, jirani zake (Bukhari na Muslimu).

Dalili nyingine ya zama za mwisho ni kuwa vijana watakuwa waasi na mapenzi na heshima kati ya vijana na wazee vitapungua: Wakati wazee watakapokosa huruma kwa vijana, na wakati vijana watakapokosa heshima kwa wazee Watoto watakapokuwa na jazba Basi hapo hukumu ipo jirani.

(Imeripotiwa na Umar (r.a)). Hadithi nyingine zinaonyesha dalili nyingine ya zama za mwisho kuwa talaka na idadi ya watoto wa nje ya ndoa vitaongezeka: Talaka itakuwa ni jambo la kila siku (Allamah Safarini, Ahwal Yaum al Kiyama). Kutakuwa na wingi wa watoto wa haramu (Al Muttaqi Al Hindi, Muntakhab Kanzul Ummaal).

Kwa kutenzwa na itikadi ya Ulahidi na mtazamo wa kidunia, watu wataikumbatia dunia kupindukia na wataghafilika na maisha ya akhera. Hii ni dalili nyingine ya zama za mwisho: Uchoyo na Uroho utaongezeka. (Muslim, ibn Majah). Wakati huo, watu wataiuza dini yao kwa kiasi kidogo cha maslahi ya dunia (Ahmad). Hadithi nyingine inasema kuwa watu watalaaniana na kuapizana: Katika siku za mwisho kutakuwa na watu ambao pale wakutanapo hulaaniana na kutukanana badala ya kusabahiana (kwa salamu) (Allama) (Jalaludiin) Suyuti, Durre Mansouri). Dalili nyingine ya zama hizo ni utesi na dharau kwa watu wengine:

Kutakuwa na wingi wa wasutaji, vizabizabina, Wambea, wagombanishaji, waamsha fitina na watu wenye dharau katika jamii. (Al Mutaqi Al Hindi, Muntakhab Kanzul Ummaal) Dalili nyingine ya Kiama ni rushwa:

Udanganyifu na ulaghai yatakuwa mambo ya kawaida (Allama Safarini Ahwal Yaum al Qiyama) Rushwa itaitwa zawadi na itaonekana kama halali tu: (Ammal Al diin al Qazwini, Mufid al ulumi wa Mubid al Humum). Mtume (s.a.w.w) kasema, mauaji yataongezeka sana katika zama za mwisho: Kiama hakitasimama hadi pale mauaji yatakapozidi. (Bukhari).

10

DALILI ZA KIAMA

KUKUA KWA SAYANSI NA TEKNOLOJIA

Mtume Muhammad(saw), kama sote tujuavyo aliishi karne kumi na nane zilizopita. Kumbukumbu za Historia zinaonesha kuwa wakati Qur'an ilipofunuliwa jamii ya Waarabu haikuwa na teknolojia ya kuwawezesha kufanya tafiti za dunia au ulimwengu.

Kwa sababu hiyo kuna tofauti kubwa kati ya kiwango cha sayansi na Teknolojia cha wakati wa alioishi Mtume (s.a.w.w) na wakati huu wetu. Tofauti hii ilianza kuwa kubwa hasa zaidi mwanzoni mwa karne ya ishirini. Kielezeo cha wazi cha hilo ni mageuzi makubwa ya kiteknolojia yanayoonekana katika wakati wetu huu ambayo, hayakupata kuonekana sio tu wakati wa Mtume bali hata katika miongo michache iliyopita. Licha ya tofauti hiyo, bado katika karne ya saba Mtume(s.a.w) alizungumzia mambo mengi ya hakika juu ya maisha. Hapa tutaziangalia Hadithi zinazoelezea kiwango cha maarifa ya sayansi na Teknolojia katika zama za mwisho. Tutaona kuwa yale aliyoyabainisha Mtume (s.a.w.w) karne kumi na nne zilizopita yanadhihirika leo.

Elimu Tofauti kubwa inayobainika kati ya krne za 20 na 21 na zama zilizopita ni kuongezeka kwa mwamko wa elimu. Huko nyuma uwezo wa kusoma na kuandika ulihodhiwa na watu wachache. Lakini kuanzia mwishoni mwa karne ya ishirini UNESCO na taasisi za serikali pamoja na mashirika binafsi yamefanya kazi kubwa ya kusambaza elimu.

Kwa mujibu wa ripoti ya UNESCO, kiwango cha elimu ya kujua kusoma na kuandika kilifikia asilimia 77.4 mwaka 1997. Kiwango hiki ni kikubwa mno. Mtume (s.a.w.w) aliielezea hali hii kama ni dalili mojawapo ya zama za mwisho; "Mwamko wa elimu(literacy) utaongezeka pale hukumu inapokaribia"(Ahmad Diyaal-Din-Alkhamush Khanawi, Ramuz-al-Ahadith). i

Teknolojia ya ujenzi Dalili nyingine ambayo Mtume (s.a.w.w) ameitaja kuhusiana na zama za mwisho ni ujenzi wa maghorofa marefu:

"Hakutakuwa na hukumu hadi pale maghorofa marefu sana yatakayojengwa"(imesimuliwa na Abu Huraira) "Kiama hakitasimama mpaka watu washindane kujenga maghorofa marefu. (Bukhari)

Tukiingalia historia ya usanifu majengo na uhandisi, tunaona kuwa maghorofa mengi marefu yalianza kujengwa na mwishoni mwa karne ya kumi na tisa. Maendeleo ya Teknolojia kuongezeka kwa matumizi ya chuma cha pua na matumizi ya Kambarau(lifti za kupandia maghorofani) kumeongezeka kasi ya ujenzi wa maghorofa. Maghorofa marefu yameshamiri kweli kweli hivi leo. Alichokisema Mtume (s.a.w.w) katika Hadithi kinadhihirika wazi wazi. Watu na mataifa yanashindana kuongeza maroshani ya ghorofa.

Teknolojia ya usafiri Katika historia yote, kumekuwa na uhusiano kati ya maendeleo na mawasiliano. Jamii ambazo zimeweza kujiwekea miundo mbinu bora ikiwa ni pamoja na mifumo bora ya usafiri zimejipatia maendeleo. Akizungumzia dalili za zama za mwisho, Mtume (s.a.w.w) kayataja maendeleo ya usafiri. "Kiama hakitasimama hadi muda utakapopita upesi upesi (Bukhari) Masafa ya mbali mno yatafikiwa kwa muda mfupi. (Ahmad Musnad)

Ujumbe unaobebwa na Hadithi hiyo unadhihirika wazi wazi hivi leo. Katika zama hizi masafa ya mbali yanafikiwa kwa muda mfupi tu. Madege, magari na Treni ni vyombo vinavyoweza kusafiri masafa ya mbali kwa muda mfupi. Huko nyuma safari za masafa marefu zilichukua miezi. Qur'an pia inavielezea vyombo hivi:

"Na amewaumbia Farasi na nyumbu na punda ili muwapande na (wawe) mapambo. Na ataumba vipano) msivyovijua (6:8).

Hebu tuutafakari huu usemi wa muda utapita upesi upesi katika ile hadithi ya kwanza. Kwa kuzingatia yale tuliyoyaeleza, ni wazi kama Mtume (s.a.w.w) alivyonena kuwa katika zama za mwisho, kazi zitafanywa kwa muda mfupi kuliko zilivyokuwa zikifanywa huko nyuma.

Kwa kweli maendeleo ya sayansi yamewezesha mambo mengi kutimizwa kwa muda mfupi zaidi. Hadithi hiyo hiyo inathibitisha jambo hili: Kiama hakitakuja kabla muda kupungua. Mwaka uwe kama mwezi, mwezi uwe kama wiki na wiki iwe kama siku (Tirmidh).

Mathalani zama zilizopita, mawasiliano ya kimataifa yalichukua majuma mengi lakini sasa yanafanyika kwa sekunde tu kwa tovuti na teknolojia nyinginezo za mawasiliano. Kurahisishwa kwa mawasiliano kumewezesha chombo cha anga cha Marekani kutumwa katika sayari Mars zaidi ya maili milioni 106 ambacho hivi kinaendelea kuleta taarifa mbali mbali za kiuchunguzi duniani pamoja na picha kwa muda mfupi sana.

Katika zama za nyuma bidhaa zilifika kule zilikopelekwa baada ya safari ndefu za miezi, hivi leo zinafika mapema kabisa. Hivi sasa mamilioni ya vitabu yanaweza kuchapwa kwa muda uliotumika kuchapwa kitabu kimoja karne chache zilizopita. Katika masuala ya afya na njia za utayarishaji wa vyakula hapahitajiki tena muda mrefu wa kushughulikia kutokana na Teknolojia ya sasa.

Unaweza kutoa mifano mingi mno. Hata hivyo tumalizie hapa kwa kusema kuwa dalili zote alizozieleza Mtume (s.a.w.w) katika karne ya saba zinaonekana wazi wazi hivi sasa. Dalili nyingine aliyoitaja Mtume (s.a.w.w) ni kuongezeka kwa biashara, kama iliyoripotiwa na Ibn Mas'uud(r.a). Biashara inakwenda pamoja na maendeleo ya Teknolojia na usafirishaji wa kisasa umeiwezesha kila nchi duniani kujenga uhusiano na ushirikiano wa karibu wa kibishara na nchi nyingine.

11

DALILI ZA KIAMA

TEKNOLOJIA YA MAWASILIANO

Baadhi ya Hadithi za Mtume (s.a.w.w) zimeelezea Teknolojia ya leo ya mawasiliano;

"Saa ya mwisho haitafika kabla jumbe hajasemeshwa na fimbo yake .(Tirmidh)

Tukiiangalia hadithi kwa makini, twaweza kuona ukweli uliomo ndani yake. Katika zama zilizopita fimbo ilitumika kuendeshea wanyama wa kupanda hasa hasa ngamia na farasi. Hapa tunaona Mtume (s.a.w.w) Hapa tunaona Mtume (s.a.w.w) ametumia tamathali.

Hebu tujiulize ni kitu gani kinachosema ambacho twaweza kukilinganisha na fimbo kwa sifa za maumbile? Jibu la kwamza laweza kuwa simu. Au vyombo vingine vya mawasiliano. Vyombo vya mawasiliano visivyotumia waya kama vile simu za mkononi na simu za upepo kama sattilaiti ni vyombo vya hivi karibuni kabisa. Kwa kuvitazama vyombo tutaona wazi wazi kule kutimia kwa bishara ya Mtume (s.a.w.w) iliyotolewa miaka 1400 iliyopita. Kwa hivyo huu ni ushahidi kuwa zama zetu ziko jirani na siku ya hukumu. Katika Hadithi nyingine Mtume (s.a.w.w) anaelezea maendeleo ya Teknolojia ya mawasiliano:

"Hakutakuwa na hukumu mpaka sauti ya mtu imsemeshe yeye mwenyewe(Hadi mtu asemeshwe na sauti yake.(Mukhtasar Tazkira; Allama Qurtubi). Ujumbe wa Hadithi hii unathibitika hivi leo.Ili mtu aisikiye sauti yake kwanza hurekodiwa na kisha kusikilizishwa. Teknolojia ya kunasa na kutoa sauti ni ya karne ya ishirini. Huu ndio ulikuwa mwanzo wa maendeleo ya sayansi ambayo ndio imezaa vyombo vya mawasiliano na habari. Unasaji wa sauti sasa umefikia kiwango cha juu kutokana na matumizi ya kompyuta.

Kwa kifupi vyombo vya elektroniki vya hivi leo kuna vipaza sauti ambavyo vimewezesha mtu kujinasa na kujisikia sauti yake mbali ya kanda za rekodi na vionesho vya picha(video). Hii inadhihirisha kuwa Hadithi ya Mtume iliyonukuliwa hapo imetimia. Kwa hiyo hii ni dalili nyingine ya kiama. Si hadithi hizo tu bali kuna ishara nyingine zilizotajwa na Hadithi zifuatazo:

Mkono utanyooshwa kutoka angani na watu watautazama na kuuona.(Ibn Hajar Haythami, AlQawl al Mukhtasar fil alamat al Mahdi al Muntanzir. Dalili ya siku hiyo mkono kunyooshwa angani na watu kuacha kuangalia.(Al-Muttaqil al Hindi, AlBurhan fi Ahmad al-Mahdi Akhir al-Zaman)

Ni dhahiri kuwa neno "mkono" katika hadithi hiyo limetumika kwa tamathali. Katika zama zilizopita neno hili huenda halikueleweka zaidi. Lakini ikitazamwa teknolojia ya leo, kauli yaweza kutafsiriwa kwa namna nyingi. Kwa mfano Televisheni ambayo imekuwa sehemu muhimu ya maisha ya leo pamoja na kamera na Kompyuta zaweza kubeba tafsiri ya kauli hiyo.

Neno "mkono" yawezekana limetumika likiwa na maana ya uwezo. Yaweza kuwa na maana pia taswira zinazotoka angani kwa sura ya mawimbi ambayo ni televisheni:

"Sauti itamwita mtu kwa jina lake na hata watu wa magharibi na mashariki watasikia .(Ibn Hajar Haythami, Al Qawl al Mukhtasar fi alamat ala Mahdi al Muntazar). Sauti hii itavuma itaenea duniani kote na kila kabila litaisikia kwa lugha yao wenyewe(Al-Muttaq al Hindi, al Burhani fi alamat al Mahd Akhir al Zaman).

Sauti kutoka mbinguni ambayo kila mtu ataisikia kwa lugha yake. (Al-Muttaq al Hindi, al Burhani fi alamat al Mahd Akhir al Zaman). Hadithi hapa zinataja sauti ambayo itasikika dunia nzima na kwa lugha ya kila mtu. Ni dhahiri hii ina maana ya Radio, Televisheni, simu za mikononi na nyenzo nyingine za mawasiliano. Huu ni muujiza kwamba Mtume(s.a.w) alitaja maendeleo ambayo hayakufikirika katika kipindi cha miaka mia moja tu iliyopita. Mfasiri maarufu Badiuzzaman wakati akifasiri hadithi hizi alieleza kuwa, zimebashiri kimiujiza kuja kwa radio, televisheni na vyombo vingine vya aina hiyo.

Kuzuka kwa manabii wa uongo Inafahamika kuwa katika kipindi chote cha historia, kumekuwa na manabii wengi wa uongo. Katika hadithi inabainishwa kuwa Manabii wa uongo watazuka kabla ya siku ya hukumu. Saa ya mwisho haitafika kabla ya kuja kwa Madajali(Wadanganyifu) thelathini kila mmoja akijitambulisha kama nabii wa Allah.(Abu Dawood) Kwa kutumia fursa ya matazamio ya Waislamu na itikadi ya dini ya kikristo kuwa Nabii Isa au Yesu atarejea, idadi kubwa ya watu wadanganyifu wamejitokeza kudai unabii.

Kumbukumbu zinaonesha kuwa , Manabii wa uongo walianza kujitokeza katika miaka ya 70. Ifuatayo ni baadhi ya mikasa iliyotokana na madai ya unabii yaliyojitolewa na watu mbali mblia katika nchi mbali mbali. Maafa ya moto; David Koresh na wafuasi wake wapatao 74 katika eneo la Waco, Texas walikufa kwa kujiwasha moto.

Wiki moja kabla ya hapo maeneo mawili ya Uswisi na moja nchni Canada, walikufa jumla ya Wafuasi 53 wa Jouret, wakiwemo na watoto wao. Polisi katika nchi hizo mbili wanafanya uchunguzi kujua kama vifo hivyo ni vya kujiua, kuuawa au yote mawili kutokana na imani za ajabu.

Sun Myung Moon, mwasisi wa Kanisa la Unification anadai yeye ni Masihi aliyekuja kwa mara ya pili. Kanisa la Unification lilianzishwa rasmi na Moon mnamo mwaka 1954. Moon anadai kuwa mwaka 1936 yeye alipokuwa na umri wa miaka 16, Yesu alimtokea upande wa mlimani kaskazini magharibi mwa Korea na kumwambia kuwa Mungu amemchagua kwa kazi ya utume wa kusimamisha Ufalme wa mbinguni na ardhini.

Zaidi ya watu 1000 wahofiwa kufa baada ya kugundulika kwa makaburi mengi zaidi nchini Uganda. Hao walikuwa wafuasi wa mtu aliyedai kuwa nabii Kibwetere. Zaidi ya watu 900, wafuasi wa dhehebu moja, walikutwa wamekufa pamoja katika msitu wa Amerika kusini. Watu wote waliokufa walikuwa wafuasi wa Mchungaji Jim Jones, kiongozi wa hekalu mjini San Francisco.

Qur'an pia inaeleza kuja kwa mnabii wa uongo; Na ni nani dhalimu mkubwa kuliko yule amtungiyae uongo Mwenyezi Mungu au mwenye kusema: Nimeletewa Wahyi", na hali hakufunuliwa chochote; na yule asemaye: Nimeteremsha(ufunuo) kama ule aliouteremsha Mwenyezi Mungu. Na kama ungewaona madhalimu watakapokuwa katika mahangaiko ya mauti na malaika wamewanyooshea mikono(kuwaambia) zitoeni roho zenu! Leo mtalipwa adhabu ifedheheshayo kwa sababu ya yale mliyokuwa mkizifanyia kiburi Aya zake(ungeona namna gain wanavyopapatika) (6:93).

Kama inavyoelezwa katika aya hiyo watu hawa wazushi kwa hakika watapata malipo yao kwa uongo waliozusha. Hapana shaka kuwa utafika wakati ambapo uongo wote wa manabii wa uongo utafutiliwa mbali. Mtume(s.a.w) akasema kuwa baada ya warongo hawa kuondoka ndipo Isa (s.a) atakapokuja tena.

Kama tulivyoeleza kurasa za nyuma kuwa Qur'an inatufahamisha kurejea kwake duniani, na kwamba Waislamu na Wakristo, kwa hamu, wanasubiri ujio wake, kuna Hadithi chache za Mtume (s.a.w.w) Mwanazuoni wa kiislamu Shawkani kasema kuwa kuna Hadithi 29 zinazoelezea kurejea kwa Issa na kwamba maelezo yaliyomo katika hadithi hizi hayawezi kupotoshwa.(Ibn Majah)

Kuna jambo moja muhimu linalotujia kutokana na Haithi hizi. Kurejea kwa Isa kutatokea awamu ya pili ya zama za mwisho na ndio itakuwa ishara muhimu(dalili kuu) ya siku ya hukumu. Hadithi zinazohusiana na jambo hili ni hizi;

Saa ya mwisho haitafika mpaka muone mshuko wa Issa (a.s) mwana wa Mariamu (Muslim). Naapa kwa yule ambaye roho yangu iko mikononi mwake. Mwana wa Maryamu, muda si mrefu atashuka miongoni mwenu (Waislamu) kama mtawala mwadilifu wa haki(Bukheri).

Saa haitasimama hadi pale atakaposhuka mwana wa Maryamu miongoni mwenu kama mtawala mwadilifu(Bukhari) Mtume (s.a.w.w) anatueleza kile atakachofanya Isa pale atakaporejea; unapowadia wakati wa kifo chake Isa atakuwa ameonekana tena duniani kwa kipindi cha miaka 40.(Abu Dawuud).

Isa (a.s) mwana wa Maryamu atashuka kutawala kwa miaka arobaini kwa kitabu cha Allah na kwa Sunna yangu hadi anapokufa. (Al-Muttaqi al Hindi, Al Burhani fi Alamat al Mahdi Akhir al zaman)

12

DALILI ZA KIAMA

ZAMA BORA

Sifa za zama bora zilizoelezewa kwa kina na Mtume (s.a.w.w) ni dalili muhimu ya siku ya hukumu. Kipindi hicho kinachoitwa "Golden age" kitakuwa bora kwa sababu ya kule kulinganishwa kwake na pepo kwa maelezo ya Mwanachuoni wa kiislamu.

Imeelezwa katika Hadithi kuwa zama hizo bora zitakuwa katika awamu ya pili ya zama za mwisho. Sifa moja kuu ya kipindi hiki cha furaha itakuwa ni ule utajiri wake mkubwa wa mali. Hadithi zinasema kuwa utajiri huo hautakuwa na mfanowe katika historia:

Umma wangu utapata hali bora katika zama hiyo ambayo mfano wake haujapata kuonekana hapo kabla (ibn Majah). Umma wangu wa wema na wabaya utaneemeshwa neema ambazo haukupata kuziona kabla (Al-Muttaq al Hind Al Burhan fi Alamat al Mahd Akhira Zaman).

Hadithi nyingine inaelezea utajiri wa zama hizo: Katika kipindi hicho, ardhi itatupa nje hazina yake. (Ibn Hajar Haythami, AlQawli al Mukhtasar fii alamat al Mahdi al Muntazar) Hadithi nyingine zinaelezea kuwa miaka ya mashaka na huzuni itakwisha. Hakuna mtu atakayekuwa katika shida. Hakuna mtu atakayetakiwa kutoa zaka.

"Toeni zaka kwani utakuja wakati ambapo mtu atakwenda na zaka yake huku na kule asipate mtu wa kuipokea (Bukhari). Kwa hakika bidhaa zitakuwa nyingi na zitamwagika kama maji lakini hakuna atakayeziokota(Al Halimi). Sifa nyingine ya zama bora itakuwa ni kushitadi kwa haki na ukweli. Utakuwa wakati ambapo sheria na haki zitachukua nafasi ya hofu, mfarakano na dhuluma.

Kama tunavyosema katika Hadithi, dunia itajaa haki badala ya ukandamizaji na mateso (Ahmad Diya'al Din al Kamushkanawi, Ramuz al Ahadithi) Miongoni mwa sifa bora za kipindi hicho ni kunyamaa kwa silaha(kutulia kwa milio ya silaha), kutoweka kwa uadui, migogoro na kukoma kwa misambaratiko ya kijamii. Badala yake kutashamiri urafiki na mapenzi miongoni mwa watu. Kiasi kikubwa cha pesa kilichotumika kugharimia vita na viwanda vya silaha sasa kitawekezwa kwenye chakula, afya, maendeleo, utamaduni na mambo yatakayoleta furaha kwa watu wote.

Sifa nyingine ya kipindi hiki cha neema itakuwa ni kurejea katika misingi ya dini ya Mwenyezi Mungu kama ilivyofundishwa na Mtume (s.a.w.w) Zile sheria na mila zilizobuniwa baada ya Uislamu zitaondoshwa. Tafauti za Waislamu katika kuitekeleza dini yao zitakoma.

Kwa kifupi, zama bora ni kipindi cha neema nyingi, maisha bora, amani furaha, utajiri na faraja. Utakuwa ni wakati ambao maendeleo katika sanaa, tiba, mawasiliano, uzalishaji, usafirishaji na katika maeneo mengine ya maisha yatakuwa katika sura ambayo haikuwahi kuonekana katika historia ya dunia. Na watu wataishi kwa kuzingatia mafundisho ya Qur'an.

Baada ya zama bora Tunaposoma habari za Mitume katika Qur'an tunaona kuwa kanuni ya Mwenyezi Mungu imefanyakazi katika zama zote. Jamii zinazomkadhibisha Mtume wa Mwenyezi Mungu na kumpiga vita basi huishia kuangamizwa. Lakini wale wanaomtii Mtume hupata neema nyingi za kidunia na Ustawi wa Kiroho ambao dini sahihi huwaletea. Lakini baada ya kupita mitume hawa, baadhi ya Watu huanza kukengeuka na kuikanusha dini sahihi kuanza kuishirikisha na Mwenyezi Mungu.

Mifarakano na migongano hutokea. Kwa kweli watu wa jamii hizi wamejikuta wakiangamia kwa mikono yao wenyewe. Kanuni, hapana shaka, itafanya kazi katika zama za mwisho. Mtume (s.a.w.w) amebainisha kuwa kiama kitakuja baada ya kifo cha Isa(a.s) na mwishoni mwa zama bora kama tulivyosoma.

"Baada ya yake (Nabii Isa) siku ya hukumu itakuwa jambo la muda mfupi mbele (Ahmad Diy'aal Din al Kamushkanawi, Ramuz Al Ahadith). Siku ya hukumu itakuja baada yake (Nabii Isa) ( Ahmad Diy'aal Din al Kamushkanawi, Ramuz Al Ahadith.

Hapana shaka zama mwisho na zama bora vitakuwa vipindi ambapo onyo la mwisho litatolewa kwa Wanaadamu. Hadithi nyingi zinaelezea kuwa hapatakuwa na mema baada ya kipindi hiki.

Hivyo tunaona kuwa muda mfupi baada ya kifo cha Isa (a.s) watu duniani watakuwa waovu na wataitupa dini sahihi. Ule wingi wa mali katika zama bora utawazuzua na hivyo kuharibikiwa. Hapa twaweza kusema kuwa katika mazingira haya ndipo kiama kitakapotokea lakini Allah ndiye ajuaye.

Kwa jinsi tulivyoziona dalili za kiama, yaweza kusemwa kuwa Karne hii ya ishirini na moja inaashiria mwanzo wa enzi mpya kabisa za historia ya dunia. Tunamuomba Allah atufishe na kutufufua hali ya kuwa ni Waislamu.

MWISHO

13

6

DALILI ZA KIAMA

KUANGAMIA KWA MIJI MIKUU:

Vita na majanga Miongoni mwa mambo aliyoyasema Mtume kuhusiana na zama za mwisho ni hili:

Miji mikuu itaangamia na itakuwa kana kwamba haikupata kuwepo hapo kabla (Al-Muttaq Al-Hindi Al Burhan fi Alamat Al Mahadi Akhir al Zaman)

Kuangamia kwa miji mikuu iliyozungumzwa katika hadithi hii kunatukumbusha maangamizi ambayo yanatokea hivi leo kutokana na vita na majanga mbali mbali ya asili. Silaha za kisasa za Nyuklia, Madege ya Kivita, Mabomu, Makombora na Zana nyingine za kisasa zimesababisha maangamizi yasiyosemeka.

Zana hizi za hatari zimeleta kiwango kikubwa cha maangamizi ambacho dunia haijapa kukiona hapo kabla. Kwahakika miji mikuu ndio imekuwa malengo makuu ya mashambulizi na imekuwa ikiathirika zaidi kutokana na maangamizi haya. Maangamizi yasiyo na mfano ya vita ya pili ya dunia ni kielezeo cha haya. Kwa kutumika bomu la Atomic katika vita kuu ya dunia, miji ya Hiroshima na Nagasaka iliangamizwa kabisa.

Kutokana na Mabomu mazito, miji mikuu ya Ulaya na miji mingine mikubwa imepata kiwango kikubwa cha hasara. Buku la marejeleo (Encylopedia Britannica) linaelezea hasara iliyosababishwa na vita kuu ya pili ya dunia katika miji ya Ulaya: Maangamizi yaliyotokea yameigeuza sehemu kubwa ya Ulaya kuwa kama taka taka na ilimalizwa na mabomu ya moto, bara bara zilijaa mashimo matupu, sura ya nchi ilikuwa giza tupu njia za reli zikaharibiwa na kutofanya kazi, madaraja yalibomolewa na bandari zilijaa Meli. Berin, anasema Jenerali Lusias D. Clay, Naibu Gavana wa Jeshi katika ukanda wa Post war German, lilikuwa kama jiji la wafu.

Kwa kifupi maangamizi ambayo yalisababishwa na vita ya pili ya dunia yanashabihiana kabisa na hadithi ya Mtume (s.a.w.w) Sababu nyingine ya maangamizi ya miji mikuu ni majanga ya asili. Ni ukweli wa kitakwimu kuwa zama tunazoishi hivi leo zimeshuhudia kuongezeka kwa idadi na madhara ya majanga ya asili. Katika miaka kumi iliyopita, majanga ya asili yaliyosababishwa na mabadiliko ya hali ya hewa yalikuwa ni mambo ambayo hayakuwahi kutokea.

Maangamizi, Umasikini, mauaji, machafu kuongezeka Sababu nyingine ya maangamizi katika miji ni majanga ya asili. Kulingana na takwimu, zama zetu zimeshuhudia ongezeko la idadi na ukubwa wa majanga ya asili. Katika kipindi cha miaka kumi iliyopita kulikuwa na majanga yaliyosababishwa na mabadiliko ya hali ya hewa. Haya yalikuwa ni majanga ya aina yake.

Hatari kubwa ya uchafuzi wa hali ya hewa unaosababishwa na viwanda ni tishio kwa dunia nzima. Viwanda vinavuruga urari wa angahewa ya dunia na kuongeza mabadiliko ya hali ya hewa. Mwaka 1998 ulikuwa ni mwaka wa joto kali sana duniani tangu rekodi za hali ya hewa zianze kuwekwa. Kwa mujibu wa maelezo ya kituo cha taarifa za hali ya hewa cha Marekani, idadi kubwa ya majanga yaliyotokana na hali ya hewa ilikuwa mwaka huo wa 1998.

Kwa mfano, Kimbunga kimeelezewa na wachunguzi wengi kuwa ndio janga baya mno la kimaumbile lililoikumba Amerika ya kati. Katika miaka michahe iliyopita vimbunga, dhoruba, tufani na majanga mengine yameleta maangamizi katika bara la Amerika na katika sehemu nyingine kadha wa kadha za dunia. Mbali na hayo mafuriko nayo yameleta maangamizi katika maeneo kadhaa ya watu. Aidha mitetemeko ya ardhi, Volkeno nayo pia yamesababisha maangamizi makubwa. Hivyo basi maangamizi yote haya yaliyotokea katika miji ni ishara muhimu.

Mitetemeko ya ardhi Hapana shaka kuwa katika historia, hakuna majanga ya asili ambayo yamewaathiri watu kwa kiasi kikubwa kama mitetemeko ya ardhi. Mitetemeko ya ardhi hutokea mahali popote na wakati wowote. Kwa karne zote mitetemeko ya ardhi imesababisha maafa na hasara kubwa ya mali. Kwa sababu hii tetemeko la ardhi ni janga linalohofiwa mno. Hata teknolojia ya karne ya Ishirini na Ishirini na moja imeweza kwa kiasi kidogo sana kuzuia uharibifu wa tetemeko la ardhi.

Tetemeko la ardhi la mwaka 1995 kule Kobe laweza kuwa somo kwa wale wanaodhani kuwa teknolojia itaweza kudhibiti maumbile. Itakumbukwa kuwa tetemeko hili la ardhi lilitokea bila kutarajiwa kwenye eneo kubwa la viwanda na usafirishaji. Licha ya ukweli kwamba lilidumu kwa sekunde ishirini tu, kama lilivyoripoti gazeti la Time, bado lilisababisha hasara ya dola bilioni 100. Kadhalika tetemeko la ardhi ndani ya bahari lililofahamika kama Tsunami fukweni mwa nchi za Indonesia, Thailand na ukanda mzima wa Pwani ya Asia, lilikuwa la aina yake kupata kutokea katika historia ya mwanaadamu.

Katika miaka michache iliyopita mitetemeko mikubwa ya ardhi imetokea mara kwa mara na ndio matishio makubwa ya maisha ya watu duniani kote. Tukiangalia takwimu zilizokusanywa na kituo cha taarifa za matetemeko ya ardhi cha Amerika mwaka 1999 tunaona kuwa mitetemeko ipatayo 20, 832 ilitokea sehemu mbali mbali duniani. Matokeo yake watu wanaokadiriwa kufikia 500,000 walikufa. Matukio yote haya yanakumbushia maneno ambayo Mtume (s.a.w) aliyasema miaka 1400 iliyopita: Kiama hakitasimama mpaka pale mitetemeko ya ardhi itakapotokea mara kwa mara. (Bukhari).

Katika Qur'an kuna aya kadhaa zinazobainisha uhusiano kati ya mitetemeko ya ardhi na zama za mwisho. Sura ya 99 inaitwa suratil Zil Zaala ambayo maana yake ni mtikisiko au tetemeko la ardhi. Sura hii yenye aya nane inaelezea mtetemeko mkubwa wa ardhi na inasema kuwa kufuatia mtetemeko huo siku ya hukumu itakuwa imefika. Watu watafufuliwa makaburini na kutoa hesabu ya amali zao kwa Mwenyezi Mungu na kupata malipo yao hata kwa jambo dogo sana walilolifanya:

Itakapotetemeshwa ardhi kwa mtetemesho wake mkubwa. Na itakapotoa ardhi mizigo yake, na binadamu akasema (wakati huo) (oh!) ina nini leo ardhi? Siku hiyo itatoa habari zake zote kwa kuwa Mola wake ameifunulia (ameiamrisha kufanya hayo). Siku hiyowatu watatoka (makaburini) vikundi vikundi ili waonyeshwe vitendo vyao. Basi anayefanya wema hata kwa kiasi cha uzito wa mdudu chungu ataona jazaa yake na anayefanya uovu hata kwa kiasi cha uzito wa mdudu chungu ataona jazaa yake. (99:1-8).

7

DALILI ZA KIAMA

UMASIKINI

Inafahamika kuwa umasikini ni ukosefu wa chakula, makazi, mavazi, huduma za afya na mahitaji mengine ya msingi kwa sababu ya kipato duni. Licha ya fursa zinazopatikana kutokana na maendeleo ya teknolojia, umasikini hivi leo ni moja kati ya matatizo makubwa kabisa yanayoukabili ulimwengu. Katika mabara ya Afrika, Asia, Amerika Kusini na Ulaya Mashariki watu wengi wanahangaika na njaa kila siku. Kwa sababu ya mgao mbaya wa rasilimali za ulimwengu umasikini umesababisha uwepo mgawanyiko kati ya nchi za kaskazini ya jangwa la sahara ambazo ni za ulimwengu wa kwanza na nchi za kusini maskini ambazo ni za ulimwengu wa tatu.

Ubeberu na Ubepari usio na mipaka unazuia mgawanyo wa kipato ulimwenguni kote na unakwaza maendeleo ya nchi changa na nchi zinazoendelea. Wakati ambapo kuna watu wachache wanaofurahia kipato kinachozidi mahitaji yao, kuna idadi kubwa ya watu wanaohangaika na matatizo ya umasikini na ufukara. Katika Ulimwengu wa leo umasikini umefikia hatua mbaya au kiwango kibaya sana.

Ripoti ya mwisho ya UNICEF ilieleza kuwa mmoja kati ya kila watu wanne duniani anaishi katika tabu na shida isiyoelezeka. Watu bilioni 1.3 duniani wanaishi kwa wastani wa chini ya dola moja kwa siku. Watu bilioni 3 duniani wanaishi kwa dola mbili kwa siku. Takribani watu bilioni 1.3 hawapati maji safi. Watu bilioni 2.6 hawapati maji salama.

Kwa mujibu wa ripoti ya shirika la chakula duniani, (FAO) , Mwaka 2000, watu milioni 826 duniani kote hawapati chakula cha kutosha. Kwa maneno mengine mmoja katika kila watu sita ana njaa. Katika miaka kumi iliyopita dhulma katika mgawanyo wa kipato imeongezeka kwa kiwango kisichosemeka.

Ripoti za umoja wa Mataifa zinaonesha kuwa, katika mwaka 1960 asilimia 20 (20%) ya watu wanaoishi katika nchi tajiri kabisa duniani walikuwa na pato lilozidi mara thelathini pato la nchi 20 masikini kabisa. Hadi kufikia mwaka 1995 iliongezeka mara 82. Kikiwa ni kielezeo cha kutoweka kwa haki ulimwenguni, mali za matajiri 225 wakubwa kabisa ulimwenguni ni sawa na pato la mwaka la asilimia 47 (47%) ya nchi masikini ulimwenguni.

Takwimu za sasa zinaonyesha yale ambayo Mtume (s.a.w.w) aliyasema juu ya kuongezeka kwa umasikini. Katika hadithi inabainishwa kuwa umasikini na njaa ni miongoni mwa dalili za kipindi cha kwanza cha zama za mwisho:

Masikini wataongezeka (Amal Al Diin Al Qazwin, Mufid Al Ulum wa Mubid Al humum) Kipato kitagawanywa kwa matajiri tu, hakuna mafao kwa masikini. (Tirmidhi). Ni dhahiri kuwa kipindi hicho kilichobashiriwa na Mtume (s.a.w.w) kinawiana na hali ya wakati wetu wa leo. Tukiangalia karne zilizopita tunaona kuwa shida na tabu zilizoletwa na ukame, vita na majanga mengine zilikuwa za muda mfupi na ziliishia katika eneo moja moja. Lakini umasikini na shida za leo ni za kudumu na sugu. Kwa hakika Mola wetu ni Mwingi wa Rehma, yeye hadhulumu watu lakini kwa sababu ya ukosefu wa shukurani wa wanadamu na maovu wanayoyafanya, umasikini na tabu vimeongezeka. Kwa hakika hali ya mambo ya kusikitisha inaonesha wazi kuwa dunia imetanzwa na uchoyo na ubinafsi.

Kuporomoka kwa maadili, kushamiri kwa ushoga na ukahaba Katika zama zetu za leo kuna janga kubwa linalohatarisha uhai wa jamii ulimwenguni. Mithili ya virusi vinavyoua mwili, janga hili linasababisha msiba mkubwa wa kijamii. Janga hilo ni mmomonyoko wa maadili ambayo husaidia kustawisha jamii. Ushoga, Ukahaba, uhusiano haramu wa kijinsia kabla ya ndoa na nje ya ndoa, Filamu za ngono, Picha za ngono, unyanyasaji wa kijinsia na ongezeko la maradhi ya zinaa, mashindano ya kukaa uchi maarufu ulimbwende, uuzaji na utumiaji wa vileo na dawa za kulevya miongoni mwa vijana ni miongoni mwa ishara kubwa za kuporomoka kwa maadili.

Mambo haya ndiyo yamekuwa yakizishughulisha jamii. Idadi kubwa ya watu haijali hatari hii inayozidi kuwa kubwa na wanaiona kama jambo la kawaida tu. Lakini takwimu zinaonesha kuwa kila siku ipitayo kiwango cha hatari kinazidi kuongezeka. Ongezeko la maradhi ya zinaa ni kigezo kikuu cha kusaidia kuonesha ukubwa wa matatizo yanayomkabili mwanadamu. Kwa mujibu wa rekodi za Shirika la Afya ulimwenguni magonjwa yanayotokana na zinaa yanachukuwa sehemu kubwa ya maradhi. Ripoti zinaonesha kuwa kati ya kesi mpya za magonjwa ya zinaa zinazokadiriwa kufikia milioni 333 kila mwaka ulimwenguni kote, Ukimwi ndio tatizo kubwa zaidi.

Takwimu za Shirika la Afya ulimwenguni (WHO) zinaonesha kuwa idadi ya vifo vinavyotokana na ugonjwa wa Ukimwi tokea pale ulipoanza imefikia watu milioni 18.8. Ripoti za shirika hilo kwa mwaka 2000 zinaielezea hivi hali ya mambo: "Ukimwi una nafasi ya kipekee katika kuleta athari mbaya za kijamii, kiuchumi na katika mipango ya sensa ya maendeleo".

Miongoni mwa mambo mabaya kabisa yanayozidi kushamiri ni ushoga. Katika baadhi ya nchi jambo hili limehalalishwa kama ndoa, linapewa heshima zote za ndoa na limeundiwa vyama na jumuiya. Duniani kote uovu huu unapingwa. Kushamiri kwa ushoga hivi leo kunatukumbusha hatima ya watu wa Lut waliokithiri katika uovu huu. Kama isemavyo Qur'an walipoukataa wito wa Lut kuiendea njia sahihi, Mwenyezi Mungu aliuangamiza mji na watu wake kwa maangamizi makubwa.

Ni dhahiri kuwa zile hadithi zinazoelezea zama za mwisho na mporomoko wa maadili zinathibitika hivi leo. Hadithi moja inasema kuwa kutoweka kwa aibu katika dhambi ya ukahaba ni dalili ya kiama:

Kutashitadi maingiliano haramu ya kijinsia wazi wazi (Bukhari). Saa hiyo itafika wakati uzinzi utakapokuwa umeenea sana (Al-Haythami, kitab al fitan) Kufifia kwa maadili na hisia ya aibu kunaelezwa kwa maneno haya:

Saa ya mwisho haitasimama hadi pale watu watakapofanya uzinzi njiani (njia wanazopita watu) ( Ibn Iban na Bazzar). Yafaa kukumbuka kuwa hivi sasa matukio ya ukahaba yanayochukuliwa na kamera za siri yamekuwa yakioneshwa katika Internate, vituo vya Televisheni na katika magazeti yanayoitwa ya ngono na udaku. Makahaba wanaingiliana na wateja wao wazi wazi katikati ya mitaa. Hali kadhalika kuna Filamu na picha nyingi zinazosambazwa ulimwenguni kote ambazo zinaonesha uzinzi unavyofanyika wazi wazi. Takriban katika miji mingi duniani makahaba wamekuwa wakisimama na wateja wao na kufanya mambo ya ajabu barabarani hasa nyakati za usiku.

Hii ni dalili nyingine ya kiama iliyobainishwa katika hadithi. Mamilioni ya watu wanaishuhudia wenyewe dalili hii duniani kote. Hadithi zifuatazo zinaonyesha kuwa kuibuka kwa ushoga kuwa jambo la kawaida la maisha ni ishara kuu ya zama zinazokaribia siku ya mwisho:

Wanaume watawaiga wanawake na Wanawake watawaiga wanaume. (Allama Jalaluddin Swiyuti, Durre- Mansuri). Watu watazama katika ushoga na usagaji (Al Mutaqi al Hindi, Muntakhab, Kanzul Ummaal).

Vitendo vya wanaume kuwaiga wanawake na wanawake kuwaiga Wanaume vimekuwa vingi hivi leo. Tunashuhudia Wanaume wanaosuka nywele zao na pia tunashuhudia Wanaume wanaowasuka nywele wanawake kwenye Masaluni na majumbani. Imekuwa ni aina ya ajira kwa wanaume hawa hasa Wamasai kupita mitaani kusuka nywele akina Mama.

Pia tunashuhudia Wanaume wakivaa hereni masikioni na vidani shingoni. Tunashuhudia teknolojia ikitumika vibaya kubadilisha maumbile ambako kumeleta kiroja cha mwanaume kubeba uzazi na kujifungua! Kwa upande mwingine tunashuhudia Wanawake wakivaa mavazi ya Wanaume, wakijaribu kuiga usemaji wa kiume. Wakioa wanawake wenziwao na wakifanya kazi za mitulinga. Tunashuhudia wanawake wakivaa mavazi yenye kuonesha vivazi vyao vya ndani na maungo mateke ili kushawishi uzinzi.

8

DALILI ZA KIAMA

KUKANUSHA DINI SAHIHI NA MAADILI YA QUR'AN

Hadithi zinazozungumzia dalili za siku ya mwisho zinatupa maelezo ya kina juu ya wakati ambao dalili hizi zitadhihirika. Twaweza kufahamikiwa kutokana na hadithi za Mtume (s.a.w.w) kuwa awamu ya kwanza ya zama za mwisho ni kipindi ambacho kitaonekana kuwa cha kidinidini, lakini kumbe ni kipindi ambacho kitaikataa kabisa dini ya Allah na maadili ya Qur'an.

Ni kipindi ambacho yale mambo yaliyobainishwa katika aya za Qur'an yatafumbiwa macho, dini itatumbukia katika mifarakano, migogoro, hamasa na ushabiki. Ibada zitafanywa kwa ria na dini itatumika kama biashara ya kujipatia faida na maslahi ya kidunia. Ni katika kipindi hiki ambapo Imani haitategemea elimu na utafiti bali itakuwa mwigo wa kufuata mkumbo tu na hamasa ya mtu. Katika kipindi hiki watu wanaoitwa Waislamu watakuwa wengi mno wakati ambapo wanazuoni wa kweli na Waislamu wenye Ikhlasi watakuwa wachache mno.

Zifuatazo ni dalili zilizotajwa na Mtume (s.a.w.w) Karne 14 zilizopita, dalili ambazo zinathibitika wazi wazi katika wakati tulionao: Kwa mujibu wa Qur'an, Mtume (s.a.w.w) anasema kuwa watu wake wameitelekeza Qur'an:

Na Mtume alikuwa akisema, Ewe Mola wangu! Hakika watu wangu wameifanya Qur'an hii kuwa kitu kilichoachwa. (25:30). Inabainishwa katika hadithi kuwa katika zama za mwisho muongozo wa Qur'an utatupiliwa mbali na watu watajitenga nao:

Karibia ya kusimama kwa saa kutakuwa na zama ambazo elimu ya (Qur'an) itatoweka na giza totoro litagubika (Bukhari).

Utakuja wakati wa uma wangu ambapo hakutabaki chochote kilichobaki katika Qur'an isipokuwa sura yake ya nje tu na hakutabaki chochote cha Uislamu isipokuwa jina lake tu na wao watajiita kwa jina hili ingawaje ni watu w aliombali kabisa na Uislamu. (Ibn Babuya, Thawab ul-A'amal). Mfano umetolewa katika suratil Jumaa aya 5:

Mfano wa wale waliopewa Taurat, kisha hawakuichukua kwa ktuitumia ni kama Punda anayebeba vitabu vikubwa vikubwa.

Hapana shaka kuwa aya hii inatoa onyo kwa Waislamu, ikiwakumbusha kuwa wajihadhari wasije wakatumbukia katika dhambi ileile nzito. Qur'an imeshushwa kama kitabu cha muongozo ambao watu waufuate.

Mtume (s.a.w.w) kasema kuwa licha ya ukweli kuwa Qur'an itasomwa lakini elimu na hekima iliyomo ndani yake hatazingatiwa. Hii ni dalili nyingine ya ule wakati wa zama za mwisho:

Utakuja wakati juu ya umma ambapo watu watasoma Qur'an lakini haitakwenda kokote isipokuwa itaishia kwenye makoo yao (haitaingia nyoyoni.) (Bukhari).

Mtume wa Allah alisema jambo fulani kisha akasema utatokea wakati ambapo elimu haitakuwepo tena. Aliuliza Ziyadi: Ewe Mtume wa Allah itatowekaje elimu licha ya ukweli kuwa tutakuwa tukiisoma Qur'an na kuwafundisha watoto wetu kuisoma na watoto wetu nao watawafundisha watoto wao kuisoma hadi siku ya kufufuliwa? Hapo Mtume akasema je Mayahudi na Wakristo hawasomi Taurati na Biblia na kutotenda kwa mujibu wa yale yaliyomo humo? (Ahmad, ibn Majah, Tirmidhi).

Watu kuitumia dini kwa malengo ya kidunia na kujivika ngozi ya kondoo waonekane wema. Kufuata maadili ya Wayahudi na Wakristo Ni dalili moja wapo ya kiama kuwa baadhi ya Waislamu watafuata nyendo za Wayahudi na Wakristo tena watawaiga kimasonge. Mtume (s.a.w.w) kasema:

"Kwa hakika mtafuata nyendo za watu waliokuwepo kabla yenu shubiri kwa shubiri na dhiraa kwa dhiraa (Inchi hadi Inchi) kiasi ambacho hata wakitumbukia kwenye shimo la Kenge nanyi pia mtawafuata humo" tukauliza, ewe Mtume wa Allaha, una maana kuwa ni Wayahudi na Wakristo? Akajibu, kama si wao ni nani tena? (Bukhari) kutokana na hadithi hiyo tunaona kuwa kabla ya zama za mwisho kutakuwa na mielekeo mibovu ya kifikra na kimaadili na kwamba tawala zitakazokuwepo zitajitenga mbali na ukweli na haki jambo litakalosababisha mfarakano mkubwa na kuwatoa watu katika mafundisho ya Mwenyezi Mungu.

Jambo la kuzingatia hapa ni kuwa maadili ya Wayahudi na Wakristo ndio maadili ya magharibi au ya Wazungu, na mifumo ya maisha iliyojitenga na Qur'an ndio mifumo ya Magharibi inayotawala dunia hivi leo.

Muumini na Kafiri Mtume wa Mwenyezi Mungu kasema:

Kabla ya saa ya mwisho kutakuwa na vurugu vurugu tupu ambapo mtu atakuwa Muumini asubuhi na Kafiri jioni yake au atakuwa Muumini jioni na Kafiri asubuhi yake. (Abuu Daudi) Kuna vielezeo vingi vinavyoonesha hali hiyo hivi leo. Mtu anaweza kuswali swala tano lakini akawa muasherati, anaweza kushinda kutwa nzima anaswali lakini usiku anazini, anaweza kushinda na swaumu kutwa nzima lakini usiku yuko na hawara au kimada, mwingine anaweza kuwa sala tano lakini muongo, mwizi, tapeli, mla rushwa, mla riba na kadhalika. Mseto huu wa Uumini na Ukafiri unaonekana kwa watu wengi hivi leo japo kwa sura tofauti.

Kutozingatia halali na haramu Dalili nyingine ya kiama ni kuwa watu hawatazingatia yaliyoharamishwa na Mwenyezi Mungu katika Qur'an. Mtume (s.a.w.w) kasema: Utafika wakati ambapo mtu hatojali kama vitu avipatavyo ni vya halali au ni vya haramu (Bukhari).

Wanazuoni wenye nyuso mbili Mtume (s.a.w.w) kasema:

Katika zama za mwisho baadhi ya watu wanaokubalika kama wanazuoni watakuwa wanafiki kweli kweli wenye nyuso mbili; Mbwa Mwitu watasoma katika zama za mwisho. Wale watakaoziona zama hizo waombe nusra kwa Mwenyezi Mungu kutokana na uovu wa wanazuoni hao. Kutakuwa na mafisadi kweli kweli. Unafiki ndio utakaoshitadi. (Tirmidhi, Nawadil al Usul.)

Kutatokea watu katika zama za mwisho ambao watajinufaisha kwa kutumia dini (Tirmidhi) Kutumia dini kwa malengo ya kidunia Mtume wa Allah kasema;

Katika zama za mwisho watu wataitumia dini kitapeli kwa malengo yao ya kidunia na kujivika ngozi za kondoo hadharani kuonesha unyenyekevu. Ndimi zao zitakuwa tamu kama sukari lakini nyoyo zao zitakuwa nyoyo za Mbwa mwitu. (Tirmidh).

Watu hawatoheshimu mipaka ya sheria za Kiislamu. Hawatochelea kuutumia Uislamu kwa ajili ya kujipatia maslahi yao. Watu watajali zaidi kuonekana wanatenda mambo kwa ajili ya Mwenyezi Mungu wakiwa hawana chembe ya wema, huruma na usaidizi kwa wanaowahubiria. Watakuwa wakiwakamua wafuasi wao kutoa kwa kutumia aya na mahubiri ya kukhofisha na kutumainisha hali yakuwa wao wenyewe hawana ukweli katika nafsi zao.

Katika zama za mwisho za umma wa walioamini, watu watapamba Misikiti lakini wataziacha nafsi zao katika maangamizi, watu ambao watashindwa kuitunza dini ya Mwenyezi Mungu kama wanavyozitunza nguo zao, watatelekeza majukumu ya dini yao kwa sababu ya shughuli zao, watu hawa watakuwa wengi.

9

DALILI ZA KIAMA

KUTOTEKELEZA AMRI YA KUTENDA MEMA NA KUEPUKA MABAYA

Miongoni mwa dalili za kukaribia kiama ni kuwa watu wanaojua kuwa Mwenyezi Mungu amewaamrisha kutenda mema na kuepuka uovu hawatatekeleza jambo hilo: Siku ya mwisho haitasimama mpaka watakapobakia watu ambao hawatajali mema na kamwe hawatozuia maovu (Ahmad).

Karibu na kusimama kwa kiama mambo mema yatapungua (Bukhari) Katika hadithi nyingine inabainishwa dalili ya kiama kuwa Waislamu walioamini watadhoofishwa kwa msukumo wa watenda dhambi:

Saa itafika pale sauti zitakapopazwa misikitini (Tirmidh) Saa itafika pale viongozi watakapokuwa madhalimu (Al Haithami, Kitab al Fitan)

Mtume (s.a.w.w) kasema:

katika zama za mwisho, kutakuwa na watu wachache sana wanaoweza kuitwa waumini: Utafika wakati kwa watu wangu ambapo misikiti itajaa watu lakini watakuwa hawana muongozo sahihi (Ibn Babuya, Thawab ul A'mal Hadith moja inasema kuwa waislamu wa kweli watalazimika kuficha imani zao na kufanya ibada kwa siri:

Wakati utafika ambapo wanafiki wataishi kwa siri miongoni mwenu na wenye imani watajaribu kuhuisha dini yao kwa watu wengine Katika Hadith ifuatayo inabainishwa ishara ya zama za mwisho kuwa Misikiti itafanywa sehemu za mikusanyiko ya kijamii tu. Utafika wakati ambapo watu watatumia misikiti kama vijiwe tu vya kukutania. Katika zama mwisho, watatokea watu watakaosoma Qur'an kwa ajili tu ya kujinufaisha badala ya kupata radhi za Allah:

Na aombe thawabu kwa Allah yule asomaye Qur'an. Kwa sababu katika zama za mwisho kutakuwa na watu wengi watakaosoma Qur'an na kutafuta malipo kwa watu wengine (Tirmidhi). Dalili nyingine ni kuwa Qur'an itasomwa kwa ajili ya kujifurahisha (kujiburudisha) tu kama vile wimbo:

Wakati Qur'an itakaposomwa mithili ya uimbaji wa nyimbo na wakati mtu atakapoheshimika (atakaposifika) kwa kuimba namna hiyo hata kama hana ilimu ( Al-Tabarani, Al-Kabir) Baadhi ya watu watakaotambuliwa kama Waislamu watakuwa na uelewa potofu juu ya kadari, wakati ambapo wengine wataamini nyota kuwa zinaweza kuwapatia ujuzi wa kujua maisha yao ya baadae. Hii ni dalili ya zama za mwisho:

Saa itafika wakati watu watakapoamini nyota na kukanusha Qadari (Al-Haythami, Kitab al Fitan) Licha ya ukweli kwamba Mwenyezi Mungu ameharamisha riba hivi leo riba ndio mtindo wa maisha. Katika Hadith ifuatayo hii inaelezewa kama dalili mojawapo ya ya kiama:

Bila shaka kitakuja kipindi ambacho hakuna hata mtu mmoja atakayesalimika na riba. Endapo mtu ataepuka riba kwa njia ya moja kwa moja basi hatoweza kuukwepa moshi (athari) utakaotokana nayo. Kwa kiasi fulani athari zake zitamfika tu (Imesimuliwa na Abu Huraira)

Hapa labda tutoe ufafanuzi kidogo. Katika ulimwengu wetu wa leo riba imejikita katika mifumo ya fedha na uchumi wa kitaifa na kimataifa. Aidha sekta za kiserikali na binafsi zinashiriki katika uchumi wa riba. Mabenki na makampuni binafsi ya kitaifa na kimataifa hasa yale yanayoendesha shughuli za ukopeshaji wa fedha au bidhaa yanatoza riba kwa viwango mbalimbali. Karibu Asasi zote za utoaji wa mikopo ya fedha zinatoza riba.

Kwa hali hiyo hakuna mtu ambaye anaweza kudai kuwa yeye amesalimika na riba. Maadam mfumo wa uchumi wa Taifa haukusalimika na riba basi sote tunahusika na jambo hili. Hivyo hadithi ya Mtume (s.a.w.w) inawafikiana kabisa na mazingira yetu.

Dalili nyingine ya zama za mwisho ni kuwa Hija itafanywa kwa ajili ya kusafiri tu, kufanya biashara, kujionesha tu na kuombaomba. Wakati huo utafika pale matajiri watakapokwenda Hija kwa malengo ya kusafiri kwa minajili ya kujifurahisha, biashara, kujifaharisha na kujionesha, na masikini kwenda kuomba. Imesimuliwa na Anas (r.a )

Tatizo kubwa ambalo Wanaadamu wanakabiliana nalo hivi leo ni kusambaratika kwa jamii. Kuporomoka huku kwaonekana katika vipengele mbali mbali vya maisha. Kuvunjika kwa familia, ongezeko la talaka na uzazi haramu ndio mambo ambayo yanapelekea kusambaratika kwa taasisi ya familia. Maisha hivi leo yamekuwa ya misukosuko, mashaka, huzuni, wasiwasi na vurugu tupu. Watu waliokosa maadili ya kiroho wanaona kuwa ili kuondokana na adha ya dunia basi bora wajitumbukize katika ulevi wa pombe na dawa za kulevya. Wengine wanaona kuwa hakuna ufumbuzi wa hali ngumu inayowakabili basi njia wanayoona itawatowa matatizoni ni kujinyonga. Moja ya Ishara kubwa za kuanguka kwa jamii ni kule kuongezeka kwa mambo ya haramu.

Kiwango cha uhalifu kimeongezeka kwa kiasi kinachowashangaza mabingwa wa maswala ya jamii. Ripoti ya uhalifu na haki ulimwenguni, "Universal Crime and Justice," Iliyotayarishwa na kituo cha udhibiti wa jinai cha umoja wa mataifa, United Nations' International Crime' imetoa tathmini ya jumla ya uhalifu ulimwenguni. Ripoti hiyo inasema:

Kimsingi, kama ilivyokuwa katika miaka ya themanini, kiwango cha uhalifu pia kiliendelea kuongezeka katika miaka ya tisini. Kila mahali ulimwenguni, katika kila kipindi cha miaka mitano, theluthi moja ya watu wanaoishi mijini wamekumbwa na mikasa ya uhalifu. Kote ulimwenguni vitendo vya wizi, ujambazi, utapeli, uasherati vimekuwa vikiongezeka siku hadi siku. Matukio haya, pamoja na sababu nyinginezo, yamekuwa yakihusishwa na athari mbaya za kiuchumi.

Kiwango cha utumiaji wa dawa mbali mbali za kulevya nacho kimeongezeka katika miaka ya karibuni. Watu hasa vijana wamekuwa wakibwia unga na kujidunga sindano zenye dawa za kulevya. Kwa kweli tatizo hili limeleta madhara ya kiafya, athari mbaya za kifamilia na kijamii.

Kwa hakika sababu za matatizo yote haya zimeelezwa katika Qur'an pale inaporejea historia ya jamii zilizopita. Kuporomoka kwa jamii na matatizo mbali mbali ni matokeo ya wanadamu kumsahau Mwenyezi Mungu na lengo halisi la maisha na hivyo kuyatupa maadili ya kiroho.

Matukio yote ya kuporomoka kwa jamii tunayoyashudia hivi leo tayari yalikwishabashiriwa na Mtume (s.a.w.w) karne 14 zilizopita. Mtume (s.a.w.w) amesema kuwa miongoni mwa dalili za zama za mwisho ni pale watu watakapokabiliana na vita na mabadiliko ya kijamii (Ahmad Diya"al diin al Kamush Khanawi, Ramuzi al ahadith). Zifuatazo ni hadith zinazohusiana na awamu ya kwanza ya zama za mwisho:

Kutakuwa na miaka ya udanganyifu ambapo mtu mkweli hatoaminiwa na muongo ataaminiwa (Ibn Kathir). Kutakuwa na miaka ya vurugu. Watu watamuamini muongo na kutomuamini yule anayesema ukweli. Watu hawatamuamini mtu mkweli na watamuamini yule ambaye ni fisiki. (Ahmad). Siku ya kiama haitakuja mpaka watu duni kabisa wawe watu wenye furaha kabisa (Tirmidh).

Kama inavyosomeka katika hadithi hizo kutakuwa na ongezeko la watu waovu ambapo wale wanaoonekana wakweli kumbe ni waongo na wale wanaoonekana waongo kumbe ndio wakweli. Hizi ni dalili za zama za mwisho. Hadithi moja inabainisha kuwa kutakuwa na watu wachache sana wakweli na kiasi kidogo sana cha pesa kitakachopatikana kwa kuzingatia kanuni na sheria za dini yetu:

Katika zama za mwisho watu watakuwa wakifanya biashara lakini hakutakuwa na mtu yeyote mkweli (Bukhari na Muslim). Ushahidi wa kweli utatupiliwa mbali na ushahidi wa uongo na kusingiziana ndivyo vitakavyoshamiri. Hii ni dalili nyingine ya zama za mwisho. Kwa hakika katika saa ya mwisho kutakuwa na ushahidi wa uongo na ufichaji wa ushahidi (Ahmed na Hakim). Kutakuwa na shutuma za uongo za mambo machafu na masingiziano. (Tirmidh)

Kigezo pekee ambacho kwacho watu watapimwa ubora wao ni mali, hashima itategemea mtu ni tajiri kiasi gani:

Kabla ya saa ya mwisho kufika, kutakuwa na salamu maalumu kwa watu wa tabaka fulani. (Ahamad) Hakutakuwa na hukumu mpaka pale salamu zitakapotolewa sio kwa watu bali kwa watu mahususi. (Mukhtasari Tazkira Khutub). Inasemwa katika hadithi kuwa dalili nyingine ni kuvurugika kwa uhusiano wa kijamii baina ya watu:

Ni wale watu ambao mtu anawajuwa tu ndio watakaopewa salamu (Ahmad Diyal al diya'al Din al Kamushi Khanawi, Ramuzi al ahadithi) Katika hadithi ifuatayo inaelezwa kuwa nafasi za kazi zitatolewa kwa watu wasio na sifa: Pale madaraka na mamlaka yatakapokwenda mikononi mwa watu wasio na sifa, basi hapo muisubiri ile saa (kiama). (Bukhari). Dalili nyingine ya zama hizo itakuwa ni kuvunjika kwa uhusiano wa wanafamilia, marafiki, majirani na kuvurugika kwa jamii na maadili:

Mtu kutokuwa na mapenzi na Mama yake na kumfurusha Baba yake (Tirmidh). Kwanza kutakuwa na sokomoko kwa mtu kuhusiana na familia yake, mali yake, nafsi yake, watoto wake, jirani zake (Bukhari na Muslimu).

Dalili nyingine ya zama za mwisho ni kuwa vijana watakuwa waasi na mapenzi na heshima kati ya vijana na wazee vitapungua: Wakati wazee watakapokosa huruma kwa vijana, na wakati vijana watakapokosa heshima kwa wazee Watoto watakapokuwa na jazba Basi hapo hukumu ipo jirani.

(Imeripotiwa na Umar (r.a)). Hadithi nyingine zinaonyesha dalili nyingine ya zama za mwisho kuwa talaka na idadi ya watoto wa nje ya ndoa vitaongezeka: Talaka itakuwa ni jambo la kila siku (Allamah Safarini, Ahwal Yaum al Kiyama). Kutakuwa na wingi wa watoto wa haramu (Al Muttaqi Al Hindi, Muntakhab Kanzul Ummaal).

Kwa kutenzwa na itikadi ya Ulahidi na mtazamo wa kidunia, watu wataikumbatia dunia kupindukia na wataghafilika na maisha ya akhera. Hii ni dalili nyingine ya zama za mwisho: Uchoyo na Uroho utaongezeka. (Muslim, ibn Majah). Wakati huo, watu wataiuza dini yao kwa kiasi kidogo cha maslahi ya dunia (Ahmad). Hadithi nyingine inasema kuwa watu watalaaniana na kuapizana: Katika siku za mwisho kutakuwa na watu ambao pale wakutanapo hulaaniana na kutukanana badala ya kusabahiana (kwa salamu) (Allama) (Jalaludiin) Suyuti, Durre Mansouri). Dalili nyingine ya zama hizo ni utesi na dharau kwa watu wengine:

Kutakuwa na wingi wa wasutaji, vizabizabina, Wambea, wagombanishaji, waamsha fitina na watu wenye dharau katika jamii. (Al Mutaqi Al Hindi, Muntakhab Kanzul Ummaal) Dalili nyingine ya Kiama ni rushwa:

Udanganyifu na ulaghai yatakuwa mambo ya kawaida (Allama Safarini Ahwal Yaum al Qiyama) Rushwa itaitwa zawadi na itaonekana kama halali tu: (Ammal Al diin al Qazwini, Mufid al ulumi wa Mubid al Humum). Mtume (s.a.w.w) kasema, mauaji yataongezeka sana katika zama za mwisho: Kiama hakitasimama hadi pale mauaji yatakapozidi. (Bukhari).

10

DALILI ZA KIAMA

KUKUA KWA SAYANSI NA TEKNOLOJIA

Mtume Muhammad(saw), kama sote tujuavyo aliishi karne kumi na nane zilizopita. Kumbukumbu za Historia zinaonesha kuwa wakati Qur'an ilipofunuliwa jamii ya Waarabu haikuwa na teknolojia ya kuwawezesha kufanya tafiti za dunia au ulimwengu.

Kwa sababu hiyo kuna tofauti kubwa kati ya kiwango cha sayansi na Teknolojia cha wakati wa alioishi Mtume (s.a.w.w) na wakati huu wetu. Tofauti hii ilianza kuwa kubwa hasa zaidi mwanzoni mwa karne ya ishirini. Kielezeo cha wazi cha hilo ni mageuzi makubwa ya kiteknolojia yanayoonekana katika wakati wetu huu ambayo, hayakupata kuonekana sio tu wakati wa Mtume bali hata katika miongo michache iliyopita. Licha ya tofauti hiyo, bado katika karne ya saba Mtume(s.a.w) alizungumzia mambo mengi ya hakika juu ya maisha. Hapa tutaziangalia Hadithi zinazoelezea kiwango cha maarifa ya sayansi na Teknolojia katika zama za mwisho. Tutaona kuwa yale aliyoyabainisha Mtume (s.a.w.w) karne kumi na nne zilizopita yanadhihirika leo.

Elimu Tofauti kubwa inayobainika kati ya krne za 20 na 21 na zama zilizopita ni kuongezeka kwa mwamko wa elimu. Huko nyuma uwezo wa kusoma na kuandika ulihodhiwa na watu wachache. Lakini kuanzia mwishoni mwa karne ya ishirini UNESCO na taasisi za serikali pamoja na mashirika binafsi yamefanya kazi kubwa ya kusambaza elimu.

Kwa mujibu wa ripoti ya UNESCO, kiwango cha elimu ya kujua kusoma na kuandika kilifikia asilimia 77.4 mwaka 1997. Kiwango hiki ni kikubwa mno. Mtume (s.a.w.w) aliielezea hali hii kama ni dalili mojawapo ya zama za mwisho; "Mwamko wa elimu(literacy) utaongezeka pale hukumu inapokaribia"(Ahmad Diyaal-Din-Alkhamush Khanawi, Ramuz-al-Ahadith). i

Teknolojia ya ujenzi Dalili nyingine ambayo Mtume (s.a.w.w) ameitaja kuhusiana na zama za mwisho ni ujenzi wa maghorofa marefu:

"Hakutakuwa na hukumu hadi pale maghorofa marefu sana yatakayojengwa"(imesimuliwa na Abu Huraira) "Kiama hakitasimama mpaka watu washindane kujenga maghorofa marefu. (Bukhari)

Tukiingalia historia ya usanifu majengo na uhandisi, tunaona kuwa maghorofa mengi marefu yalianza kujengwa na mwishoni mwa karne ya kumi na tisa. Maendeleo ya Teknolojia kuongezeka kwa matumizi ya chuma cha pua na matumizi ya Kambarau(lifti za kupandia maghorofani) kumeongezeka kasi ya ujenzi wa maghorofa. Maghorofa marefu yameshamiri kweli kweli hivi leo. Alichokisema Mtume (s.a.w.w) katika Hadithi kinadhihirika wazi wazi. Watu na mataifa yanashindana kuongeza maroshani ya ghorofa.

Teknolojia ya usafiri Katika historia yote, kumekuwa na uhusiano kati ya maendeleo na mawasiliano. Jamii ambazo zimeweza kujiwekea miundo mbinu bora ikiwa ni pamoja na mifumo bora ya usafiri zimejipatia maendeleo. Akizungumzia dalili za zama za mwisho, Mtume (s.a.w.w) kayataja maendeleo ya usafiri. "Kiama hakitasimama hadi muda utakapopita upesi upesi (Bukhari) Masafa ya mbali mno yatafikiwa kwa muda mfupi. (Ahmad Musnad)

Ujumbe unaobebwa na Hadithi hiyo unadhihirika wazi wazi hivi leo. Katika zama hizi masafa ya mbali yanafikiwa kwa muda mfupi tu. Madege, magari na Treni ni vyombo vinavyoweza kusafiri masafa ya mbali kwa muda mfupi. Huko nyuma safari za masafa marefu zilichukua miezi. Qur'an pia inavielezea vyombo hivi:

"Na amewaumbia Farasi na nyumbu na punda ili muwapande na (wawe) mapambo. Na ataumba vipano) msivyovijua (6:8).

Hebu tuutafakari huu usemi wa muda utapita upesi upesi katika ile hadithi ya kwanza. Kwa kuzingatia yale tuliyoyaeleza, ni wazi kama Mtume (s.a.w.w) alivyonena kuwa katika zama za mwisho, kazi zitafanywa kwa muda mfupi kuliko zilivyokuwa zikifanywa huko nyuma.

Kwa kweli maendeleo ya sayansi yamewezesha mambo mengi kutimizwa kwa muda mfupi zaidi. Hadithi hiyo hiyo inathibitisha jambo hili: Kiama hakitakuja kabla muda kupungua. Mwaka uwe kama mwezi, mwezi uwe kama wiki na wiki iwe kama siku (Tirmidh).

Mathalani zama zilizopita, mawasiliano ya kimataifa yalichukua majuma mengi lakini sasa yanafanyika kwa sekunde tu kwa tovuti na teknolojia nyinginezo za mawasiliano. Kurahisishwa kwa mawasiliano kumewezesha chombo cha anga cha Marekani kutumwa katika sayari Mars zaidi ya maili milioni 106 ambacho hivi kinaendelea kuleta taarifa mbali mbali za kiuchunguzi duniani pamoja na picha kwa muda mfupi sana.

Katika zama za nyuma bidhaa zilifika kule zilikopelekwa baada ya safari ndefu za miezi, hivi leo zinafika mapema kabisa. Hivi sasa mamilioni ya vitabu yanaweza kuchapwa kwa muda uliotumika kuchapwa kitabu kimoja karne chache zilizopita. Katika masuala ya afya na njia za utayarishaji wa vyakula hapahitajiki tena muda mrefu wa kushughulikia kutokana na Teknolojia ya sasa.

Unaweza kutoa mifano mingi mno. Hata hivyo tumalizie hapa kwa kusema kuwa dalili zote alizozieleza Mtume (s.a.w.w) katika karne ya saba zinaonekana wazi wazi hivi sasa. Dalili nyingine aliyoitaja Mtume (s.a.w.w) ni kuongezeka kwa biashara, kama iliyoripotiwa na Ibn Mas'uud(r.a). Biashara inakwenda pamoja na maendeleo ya Teknolojia na usafirishaji wa kisasa umeiwezesha kila nchi duniani kujenga uhusiano na ushirikiano wa karibu wa kibishara na nchi nyingine.

11

DALILI ZA KIAMA

TEKNOLOJIA YA MAWASILIANO

Baadhi ya Hadithi za Mtume (s.a.w.w) zimeelezea Teknolojia ya leo ya mawasiliano;

"Saa ya mwisho haitafika kabla jumbe hajasemeshwa na fimbo yake .(Tirmidh)

Tukiiangalia hadithi kwa makini, twaweza kuona ukweli uliomo ndani yake. Katika zama zilizopita fimbo ilitumika kuendeshea wanyama wa kupanda hasa hasa ngamia na farasi. Hapa tunaona Mtume (s.a.w.w) Hapa tunaona Mtume (s.a.w.w) ametumia tamathali.

Hebu tujiulize ni kitu gani kinachosema ambacho twaweza kukilinganisha na fimbo kwa sifa za maumbile? Jibu la kwamza laweza kuwa simu. Au vyombo vingine vya mawasiliano. Vyombo vya mawasiliano visivyotumia waya kama vile simu za mkononi na simu za upepo kama sattilaiti ni vyombo vya hivi karibuni kabisa. Kwa kuvitazama vyombo tutaona wazi wazi kule kutimia kwa bishara ya Mtume (s.a.w.w) iliyotolewa miaka 1400 iliyopita. Kwa hivyo huu ni ushahidi kuwa zama zetu ziko jirani na siku ya hukumu. Katika Hadithi nyingine Mtume (s.a.w.w) anaelezea maendeleo ya Teknolojia ya mawasiliano:

"Hakutakuwa na hukumu mpaka sauti ya mtu imsemeshe yeye mwenyewe(Hadi mtu asemeshwe na sauti yake.(Mukhtasar Tazkira; Allama Qurtubi). Ujumbe wa Hadithi hii unathibitika hivi leo.Ili mtu aisikiye sauti yake kwanza hurekodiwa na kisha kusikilizishwa. Teknolojia ya kunasa na kutoa sauti ni ya karne ya ishirini. Huu ndio ulikuwa mwanzo wa maendeleo ya sayansi ambayo ndio imezaa vyombo vya mawasiliano na habari. Unasaji wa sauti sasa umefikia kiwango cha juu kutokana na matumizi ya kompyuta.

Kwa kifupi vyombo vya elektroniki vya hivi leo kuna vipaza sauti ambavyo vimewezesha mtu kujinasa na kujisikia sauti yake mbali ya kanda za rekodi na vionesho vya picha(video). Hii inadhihirisha kuwa Hadithi ya Mtume iliyonukuliwa hapo imetimia. Kwa hiyo hii ni dalili nyingine ya kiama. Si hadithi hizo tu bali kuna ishara nyingine zilizotajwa na Hadithi zifuatazo:

Mkono utanyooshwa kutoka angani na watu watautazama na kuuona.(Ibn Hajar Haythami, AlQawl al Mukhtasar fil alamat al Mahdi al Muntanzir. Dalili ya siku hiyo mkono kunyooshwa angani na watu kuacha kuangalia.(Al-Muttaqil al Hindi, AlBurhan fi Ahmad al-Mahdi Akhir al-Zaman)

Ni dhahiri kuwa neno "mkono" katika hadithi hiyo limetumika kwa tamathali. Katika zama zilizopita neno hili huenda halikueleweka zaidi. Lakini ikitazamwa teknolojia ya leo, kauli yaweza kutafsiriwa kwa namna nyingi. Kwa mfano Televisheni ambayo imekuwa sehemu muhimu ya maisha ya leo pamoja na kamera na Kompyuta zaweza kubeba tafsiri ya kauli hiyo.

Neno "mkono" yawezekana limetumika likiwa na maana ya uwezo. Yaweza kuwa na maana pia taswira zinazotoka angani kwa sura ya mawimbi ambayo ni televisheni:

"Sauti itamwita mtu kwa jina lake na hata watu wa magharibi na mashariki watasikia .(Ibn Hajar Haythami, Al Qawl al Mukhtasar fi alamat ala Mahdi al Muntazar). Sauti hii itavuma itaenea duniani kote na kila kabila litaisikia kwa lugha yao wenyewe(Al-Muttaq al Hindi, al Burhani fi alamat al Mahd Akhir al Zaman).

Sauti kutoka mbinguni ambayo kila mtu ataisikia kwa lugha yake. (Al-Muttaq al Hindi, al Burhani fi alamat al Mahd Akhir al Zaman). Hadithi hapa zinataja sauti ambayo itasikika dunia nzima na kwa lugha ya kila mtu. Ni dhahiri hii ina maana ya Radio, Televisheni, simu za mikononi na nyenzo nyingine za mawasiliano. Huu ni muujiza kwamba Mtume(s.a.w) alitaja maendeleo ambayo hayakufikirika katika kipindi cha miaka mia moja tu iliyopita. Mfasiri maarufu Badiuzzaman wakati akifasiri hadithi hizi alieleza kuwa, zimebashiri kimiujiza kuja kwa radio, televisheni na vyombo vingine vya aina hiyo.

Kuzuka kwa manabii wa uongo Inafahamika kuwa katika kipindi chote cha historia, kumekuwa na manabii wengi wa uongo. Katika hadithi inabainishwa kuwa Manabii wa uongo watazuka kabla ya siku ya hukumu. Saa ya mwisho haitafika kabla ya kuja kwa Madajali(Wadanganyifu) thelathini kila mmoja akijitambulisha kama nabii wa Allah.(Abu Dawood) Kwa kutumia fursa ya matazamio ya Waislamu na itikadi ya dini ya kikristo kuwa Nabii Isa au Yesu atarejea, idadi kubwa ya watu wadanganyifu wamejitokeza kudai unabii.

Kumbukumbu zinaonesha kuwa , Manabii wa uongo walianza kujitokeza katika miaka ya 70. Ifuatayo ni baadhi ya mikasa iliyotokana na madai ya unabii yaliyojitolewa na watu mbali mblia katika nchi mbali mbali. Maafa ya moto; David Koresh na wafuasi wake wapatao 74 katika eneo la Waco, Texas walikufa kwa kujiwasha moto.

Wiki moja kabla ya hapo maeneo mawili ya Uswisi na moja nchni Canada, walikufa jumla ya Wafuasi 53 wa Jouret, wakiwemo na watoto wao. Polisi katika nchi hizo mbili wanafanya uchunguzi kujua kama vifo hivyo ni vya kujiua, kuuawa au yote mawili kutokana na imani za ajabu.

Sun Myung Moon, mwasisi wa Kanisa la Unification anadai yeye ni Masihi aliyekuja kwa mara ya pili. Kanisa la Unification lilianzishwa rasmi na Moon mnamo mwaka 1954. Moon anadai kuwa mwaka 1936 yeye alipokuwa na umri wa miaka 16, Yesu alimtokea upande wa mlimani kaskazini magharibi mwa Korea na kumwambia kuwa Mungu amemchagua kwa kazi ya utume wa kusimamisha Ufalme wa mbinguni na ardhini.

Zaidi ya watu 1000 wahofiwa kufa baada ya kugundulika kwa makaburi mengi zaidi nchini Uganda. Hao walikuwa wafuasi wa mtu aliyedai kuwa nabii Kibwetere. Zaidi ya watu 900, wafuasi wa dhehebu moja, walikutwa wamekufa pamoja katika msitu wa Amerika kusini. Watu wote waliokufa walikuwa wafuasi wa Mchungaji Jim Jones, kiongozi wa hekalu mjini San Francisco.

Qur'an pia inaeleza kuja kwa mnabii wa uongo; Na ni nani dhalimu mkubwa kuliko yule amtungiyae uongo Mwenyezi Mungu au mwenye kusema: Nimeletewa Wahyi", na hali hakufunuliwa chochote; na yule asemaye: Nimeteremsha(ufunuo) kama ule aliouteremsha Mwenyezi Mungu. Na kama ungewaona madhalimu watakapokuwa katika mahangaiko ya mauti na malaika wamewanyooshea mikono(kuwaambia) zitoeni roho zenu! Leo mtalipwa adhabu ifedheheshayo kwa sababu ya yale mliyokuwa mkizifanyia kiburi Aya zake(ungeona namna gain wanavyopapatika) (6:93).

Kama inavyoelezwa katika aya hiyo watu hawa wazushi kwa hakika watapata malipo yao kwa uongo waliozusha. Hapana shaka kuwa utafika wakati ambapo uongo wote wa manabii wa uongo utafutiliwa mbali. Mtume(s.a.w) akasema kuwa baada ya warongo hawa kuondoka ndipo Isa (s.a) atakapokuja tena.

Kama tulivyoeleza kurasa za nyuma kuwa Qur'an inatufahamisha kurejea kwake duniani, na kwamba Waislamu na Wakristo, kwa hamu, wanasubiri ujio wake, kuna Hadithi chache za Mtume (s.a.w.w) Mwanazuoni wa kiislamu Shawkani kasema kuwa kuna Hadithi 29 zinazoelezea kurejea kwa Issa na kwamba maelezo yaliyomo katika hadithi hizi hayawezi kupotoshwa.(Ibn Majah)

Kuna jambo moja muhimu linalotujia kutokana na Haithi hizi. Kurejea kwa Isa kutatokea awamu ya pili ya zama za mwisho na ndio itakuwa ishara muhimu(dalili kuu) ya siku ya hukumu. Hadithi zinazohusiana na jambo hili ni hizi;

Saa ya mwisho haitafika mpaka muone mshuko wa Issa (a.s) mwana wa Mariamu (Muslim). Naapa kwa yule ambaye roho yangu iko mikononi mwake. Mwana wa Maryamu, muda si mrefu atashuka miongoni mwenu (Waislamu) kama mtawala mwadilifu wa haki(Bukheri).

Saa haitasimama hadi pale atakaposhuka mwana wa Maryamu miongoni mwenu kama mtawala mwadilifu(Bukhari) Mtume (s.a.w.w) anatueleza kile atakachofanya Isa pale atakaporejea; unapowadia wakati wa kifo chake Isa atakuwa ameonekana tena duniani kwa kipindi cha miaka 40.(Abu Dawuud).

Isa (a.s) mwana wa Maryamu atashuka kutawala kwa miaka arobaini kwa kitabu cha Allah na kwa Sunna yangu hadi anapokufa. (Al-Muttaqi al Hindi, Al Burhani fi Alamat al Mahdi Akhir al zaman)

12

DALILI ZA KIAMA

ZAMA BORA

Sifa za zama bora zilizoelezewa kwa kina na Mtume (s.a.w.w) ni dalili muhimu ya siku ya hukumu. Kipindi hicho kinachoitwa "Golden age" kitakuwa bora kwa sababu ya kule kulinganishwa kwake na pepo kwa maelezo ya Mwanachuoni wa kiislamu.

Imeelezwa katika Hadithi kuwa zama hizo bora zitakuwa katika awamu ya pili ya zama za mwisho. Sifa moja kuu ya kipindi hiki cha furaha itakuwa ni ule utajiri wake mkubwa wa mali. Hadithi zinasema kuwa utajiri huo hautakuwa na mfanowe katika historia:

Umma wangu utapata hali bora katika zama hiyo ambayo mfano wake haujapata kuonekana hapo kabla (ibn Majah). Umma wangu wa wema na wabaya utaneemeshwa neema ambazo haukupata kuziona kabla (Al-Muttaq al Hind Al Burhan fi Alamat al Mahd Akhira Zaman).

Hadithi nyingine inaelezea utajiri wa zama hizo: Katika kipindi hicho, ardhi itatupa nje hazina yake. (Ibn Hajar Haythami, AlQawli al Mukhtasar fii alamat al Mahdi al Muntazar) Hadithi nyingine zinaelezea kuwa miaka ya mashaka na huzuni itakwisha. Hakuna mtu atakayekuwa katika shida. Hakuna mtu atakayetakiwa kutoa zaka.

"Toeni zaka kwani utakuja wakati ambapo mtu atakwenda na zaka yake huku na kule asipate mtu wa kuipokea (Bukhari). Kwa hakika bidhaa zitakuwa nyingi na zitamwagika kama maji lakini hakuna atakayeziokota(Al Halimi). Sifa nyingine ya zama bora itakuwa ni kushitadi kwa haki na ukweli. Utakuwa wakati ambapo sheria na haki zitachukua nafasi ya hofu, mfarakano na dhuluma.

Kama tunavyosema katika Hadithi, dunia itajaa haki badala ya ukandamizaji na mateso (Ahmad Diya'al Din al Kamushkanawi, Ramuz al Ahadithi) Miongoni mwa sifa bora za kipindi hicho ni kunyamaa kwa silaha(kutulia kwa milio ya silaha), kutoweka kwa uadui, migogoro na kukoma kwa misambaratiko ya kijamii. Badala yake kutashamiri urafiki na mapenzi miongoni mwa watu. Kiasi kikubwa cha pesa kilichotumika kugharimia vita na viwanda vya silaha sasa kitawekezwa kwenye chakula, afya, maendeleo, utamaduni na mambo yatakayoleta furaha kwa watu wote.

Sifa nyingine ya kipindi hiki cha neema itakuwa ni kurejea katika misingi ya dini ya Mwenyezi Mungu kama ilivyofundishwa na Mtume (s.a.w.w) Zile sheria na mila zilizobuniwa baada ya Uislamu zitaondoshwa. Tafauti za Waislamu katika kuitekeleza dini yao zitakoma.

Kwa kifupi, zama bora ni kipindi cha neema nyingi, maisha bora, amani furaha, utajiri na faraja. Utakuwa ni wakati ambao maendeleo katika sanaa, tiba, mawasiliano, uzalishaji, usafirishaji na katika maeneo mengine ya maisha yatakuwa katika sura ambayo haikuwahi kuonekana katika historia ya dunia. Na watu wataishi kwa kuzingatia mafundisho ya Qur'an.

Baada ya zama bora Tunaposoma habari za Mitume katika Qur'an tunaona kuwa kanuni ya Mwenyezi Mungu imefanyakazi katika zama zote. Jamii zinazomkadhibisha Mtume wa Mwenyezi Mungu na kumpiga vita basi huishia kuangamizwa. Lakini wale wanaomtii Mtume hupata neema nyingi za kidunia na Ustawi wa Kiroho ambao dini sahihi huwaletea. Lakini baada ya kupita mitume hawa, baadhi ya Watu huanza kukengeuka na kuikanusha dini sahihi kuanza kuishirikisha na Mwenyezi Mungu.

Mifarakano na migongano hutokea. Kwa kweli watu wa jamii hizi wamejikuta wakiangamia kwa mikono yao wenyewe. Kanuni, hapana shaka, itafanya kazi katika zama za mwisho. Mtume (s.a.w.w) amebainisha kuwa kiama kitakuja baada ya kifo cha Isa(a.s) na mwishoni mwa zama bora kama tulivyosoma.

"Baada ya yake (Nabii Isa) siku ya hukumu itakuwa jambo la muda mfupi mbele (Ahmad Diy'aal Din al Kamushkanawi, Ramuz Al Ahadith). Siku ya hukumu itakuja baada yake (Nabii Isa) ( Ahmad Diy'aal Din al Kamushkanawi, Ramuz Al Ahadith.

Hapana shaka zama mwisho na zama bora vitakuwa vipindi ambapo onyo la mwisho litatolewa kwa Wanaadamu. Hadithi nyingi zinaelezea kuwa hapatakuwa na mema baada ya kipindi hiki.

Hivyo tunaona kuwa muda mfupi baada ya kifo cha Isa (a.s) watu duniani watakuwa waovu na wataitupa dini sahihi. Ule wingi wa mali katika zama bora utawazuzua na hivyo kuharibikiwa. Hapa twaweza kusema kuwa katika mazingira haya ndipo kiama kitakapotokea lakini Allah ndiye ajuaye.

Kwa jinsi tulivyoziona dalili za kiama, yaweza kusemwa kuwa Karne hii ya ishirini na moja inaashiria mwanzo wa enzi mpya kabisa za historia ya dunia. Tunamuomba Allah atufishe na kutufufua hali ya kuwa ni Waislamu.

MWISHO

13


4

5

6

7

8

9

10

11

12

13

14

15

16