TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE Juzuu 24

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE12%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: Qurani tukufu

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
  • Anza
  • Iliyopita
  • 30 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 28948 / Pakua: 5121
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE Juzuu 24

Mwandishi:
Swahili

1

7

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE

Sura Ya Sitini Na Mmoja: Surat As – Saff. Imeshuka Madina. Ina ya 14.

بِسْمِ اللَّهِ الرَّحْمَٰنِ الرَّحِيمِ

Kwa jina la Mwenyezi Mungu Mwingi wa rehema Mwenye kure­hemu.

سَبَّحَ لِلَّـهِ مَا فِي السَّمَاوَاتِ وَمَا فِي الْأَرْضِ وَهُوَ الْعَزِيزُ الْحَكِيمُ ﴿١﴾

1. Vinamsabihi Mwenyezi Mungu vilivyo katika mbingu na vilivyo katika ardhi. Na Yeye ni Mwenye nguvu, Mwenye hikima

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا لِمَ تَقُولُونَ مَا لَا تَفْعَلُونَ ﴿٢﴾

2. Enyi mlioamini! Kwa nini mnasema msiyoyatenda?

كَبُرَ مَقْتًا عِندَ اللَّـهِ أَن تَقُولُوا مَا لَا تَفْعَلُونَ ﴿٣﴾

3. Ni chukizo kubwa kwa Mwenyezi Mungu kusema msiyoyatenda.

إِنَّ اللَّـهَ يُحِبُّ الَّذِينَ يُقَاتِلُونَ فِي سَبِيلِهِ صَفًّا كَأَنَّهُم بُنْيَانٌ مَّرْصُوصٌ ﴿٤﴾

4. Kwa hakika Mwenyezi Mungu anawapenda wanaopigana katika Njia yake kwa safu kama kwamba wao ni jengo lililojengwa kwa risasi.

وَإِذْ قَالَ مُوسَىٰ لِقَوْمِهِ يَا قَوْمِ لِمَ تُؤْذُونَنِي وَقَد تَّعْلَمُونَ أَنِّي رَسُولُ اللَّـهِ إِلَيْكُمْ فَلَمَّا زَاغُوا أَزَاغَ اللَّـهُ قُلُوبَهُمْ وَاللَّـهُ لَا يَهْدِي الْقَوْمَ الْفَاسِقِينَ ﴿٥﴾

5. Na Musa alipowaambia watu wake: Enyi watu wangu! Kwa nini mnaniudhi, nanyi mnajua kuwa hakika mimi ni Mtume wa Mwenyezi Mungu niliyetumwa kwenu? Walipopotoka, Mwenyezi Mungu alizipotoa nyoyo zao. Na Mwenyezi Mungu hawaon­goi watu mafasiki

وَإِذْ قَالَ عِيسَى ابْنُ مَرْيَمَ يَا بَنِي إِسْرَائِيلَ إِنِّي رَسُولُ اللَّـهِ إِلَيْكُم مُّصَدِّقًا لِّمَا بَيْنَ يَدَيَّ مِنَ التَّوْرَاةِ وَمُبَشِّرًا بِرَسُولٍ يَأْتِي مِن بَعْدِي اسْمُهُ أَحْمَدُ فَلَمَّا جَاءَهُم بِالْبَيِّنَاتِ قَالُوا هَـٰذَا سِحْرٌ مُّبِينٌ ﴿٦﴾

6. Na Isa bin Maryam aliposema: Enyi Wana wa Israili! Hakika mimi ni Mtume wa Mwenyezi Mungu kwenu, ninayethibitisha yaliyokuwa kabla yangu katika Tawrat, na mwenye kubashiria Mtume atakayekuja baada yangu; jina lake ni Ahmad. Lakini alipowaletea hoja zilizo wazi, walisema: Huu ni uchawi ulio dhahiri!

KAMA KWAMBA WAO NI JENGO

Aya 1 – 6

MAANA

Vinamsabihi Mwenyezi Mungu vilivyo katika mbingu na vilivyo kati­ka ardhi. Na Yeye ni Mwenye nguvu, Mwenye hikima.

Kila kilichoko kinashuhudia uwezo wake Mwenyezi Mungu (s.w.t) na hikima yake, kwa lugha ya maneno au ya hali. Imetangulia kwa herufi zake. Katika Juz. 27 (57:1) na katika Juzuu hii tuliyo nayo mwanzo wa sura 59. na tumelizungumzia hilo kwa ufafanuzi katika Juz. 15 (17:44).

Enyi mlioamini! Kwa nini mnasema msiyoyatenda?

Watu wengi wanakusudia uwongo; wanafanya kwa kujificha yale ambayo hawezi kuyadhihirisha. Hakuna mwenye shaka kwamba hawa ni wanafiki kwa kila maana ya neno unafiki.

Basi haifai kuitwa enyi waumini! Hata kama watadhihirisha imani.

Kuna watu wengine wanasema na wanajiandaa kwa nia ya ukweli na kutekeleza, lakini wanapata matatizo yasiyoweza kuzuilika na kushindwa kutekeleza pamoja na juhudi walizofanya. Hawa wanasamehewa, hilo halina shaka.

Na kuna wengine wanasema na wanakuwa na nia ya kutekeleza, lakini uki­fika wakati wananaza kuwa wavivu, waoga au mabakhili. Hawa ni wau­mini lakini ni wapuuzaji, wadhaifu kwenye utashi wao na mbele ya nafsi zao zinazoamrisha sana uovu. Aina hii ya watu ndio wanaokusudiwa kwenye Aya hii.

Ni chukizo kubwa kwa Mwenyezi Mungu kusema msiyoyatenda.

Na mwenye kuchukiwa na Mwenyezi Mungu ameanguka kwenye adhabu ya moto. Wafasiri wengi wamesema kuwa jamaa katika maswahaba walikuwa waki­tamani kupigana kabla ya vita havijaanza, lakini vikija vita na kuwajibishiwa kupigana, basi wanakuwa wazito. Ndio ikashuka aya hii.

Kwa hakika Mwenyezi Mungu anawapenda wanaopigana katika Njia yake kwa safu kama kwamba wao ni jengo lililojengwa kwa risasi.

Yaani lililojengwa kwa mpangilio na lililothabiti. Imenukuliwa kutoka kwa wanaaikolgia, kuwa wao wamegundua majengo ya zamani yaliyojengwa kwa madini ya risasi. Mwenyezi Mungu amesema akimsimulia Dhulqarnain:

آتُونِي أُفْرِغْ عَلَيْهِ قِطْرًا ﴿٩٦﴾

“Nileteeni shaba iliyoyeyuka nimwagie juu yake.” Juz. 16 (18:96).

Ziyada ya maneno ni kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) anapenda mshika­mano wa watu katika kila lililo na heri na masilahi.

Na Musa alipowaambia watu wake: Enyi watu wangu! Kwa nini mna­niudhi, nanyi mnajua kuwa hakika mimi ni Mtume wa Mwenyezi Mungu niliye tumwa kwenu?

Swali hili liko pamoja na jawabu lake. Kwa sababu Waisrail ndio wauaji wa manabii kwa nukuu ya kitabu chao kitakatifu; kama ilivyo katika Nehemia (9:26), inasema: “Walakini hawakukutii, wakakuasi, wakaitupa sheria yako nyuma yao, wakawaua manabii wako walioshuhudu juu yao wapate kuwarejeza kwako; wakatenda machukizo makuu.”

Qur’an imesajili Aya kadhaa kuhusiana na kuuwa kwao manabii.

Kama muulizajai atauliza: hakuna chochote kinachojulisha kuwa Waisrail walimuudhi Nabii Musa, hasa kwakuwa alikuwa mwokozi na mhisani wao, nasi tutamjibu hivi: Maudhi ya Waisrail kwa Nabii Musa ni mengi; miongoni mwayo ni kumwambia: Tuonyeshe Mwenyezi Mungu waziwazi, tufanyie Mungu kama wao walivyo na Mungu, hatuwezi kuvumilia chakula kimoja na mengineyo.

Walipopotoka, Mwenyezi Mungu alizipotoa nyoyo zao.

Aya hii inaeleza waziwazi kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) hampotoi mtu mpaka apotoke yeye mwenyewe kwa uchaguzi wake mbaya, wala hamtwezi mtu na kumwangamiza ila akijiangamiza yeye mwenyewe na kujidharau. Aya hii haina tofauti na kauli ya anayesema: “ mwenye kuwa na tamaa ya haramu Mwenyezi Mungu humdhalilisha na kumfedhehsha, na mwenye kukinai na halali, Mwenyezi Mungu humtukuza na kumta­jirisha.

Vile vile Aya hii ni tafsiri ya Aya zinazoonyesha kwa dhahiri kuwa Mwenyezi Mungu ndiye ampotezaye mtu; kama ile isemayo: “Humpoteza Mwenyezi Mungu amtakaye na humwongoza amtakaye.” Yaani Mwenyezi Mungu Mtukufu ametaka kumpoteza anayefuata njia ya upotevu na humwangamiza mwenye kujitia kwenye maangamizi yeye mwenyewe.

Na Mwenyezi Mungu hawaongoi watu mafasiki maadamu wanang’ang’ania ufuska.

Na Isa bin Maryam aliposema: Enyi Wana wa Israili! Hakika mimi ni Mtume wa Mwenyezi Mungu kwenu, ninayethibitisha yaliyokuwa kabla yangu katika Tawrat, na mwenye kubashiria Mtume atakayeku­ja baada yangu; jina lake ni Ahmad.

Aya ya pili katika maudhui haya inasema:

الَّذِينَ يَتَّبِعُونَ الرَّسُولَ النَّبِيَّ الْأُمِّيَّ الَّذِي يَجِدُونَهُ مَكْتُوبًا عِندَهُمْ فِي التَّوْرَاةِ وَالْإِنجِيلِ ﴿١٥٧﴾

“Ambao wanamfuata Nabii asiyesoma wala kuandika ambaye wanamkuta ameandikwa kwao katika Tawrat na Injili.” Juz. 9 (7:157)

Ya tatu inasema:

الَّذِينَ آتَيْنَاهُمُ الْكِتَابَ يَعْرِفُونَهُ كَمَا يَعْرِفُونَ أَبْنَاءَهُمْ وَإِنَّ فَرِيقًا مِّنْهُمْ لَيَكْتُمُونَ الْحَقَّ وَهُمْ يَعْلَمُونَ ﴿١٤٦﴾

“Wale tuliowapa Kitabu wanamjua yeye kama wanavyowajua watoto wao. Na hakika kundi katika wao wanaificha haki na hali wanaijua. Juz. 2 (2:146)

Qur’an imeeleza waziwazi kuwa Tawrat ilyoteremshiwa Musa na Injili ili­yoteremshiwa Isa, zimetoa bishara ya unabii wa Muhammad(s.a.w.w) . Na imewakabili kwa hakika hii, ulama wa kiyahudi na kinaswara, na ikashindana nao, kupinga hilo. Lakini Historia haijataja yeyote katika hawa, aliyekana; bali wamethibitisha wale wachunga haki katika wao, wakakiri na wakasilimu; kama vile Abadallh bin Salaam na wengineo; ingawaje walikuwa ni maadui wa Mtume wa Mwenyezi Mungu.

KUPOTOLEWA TAWRAT

Unaweza kuuliza : Mwislamu atamjibu nini Yahudi au Mkristo akisema: Qur’an yenu imesema kuwa Tawrat na Injil imetoa bishara ya Muhammad na hakuna athari yoyote ya bishara hii kwenye nakala ya Tawrat na Injil tuliyo nayo?

Jibu : Atakayeuliza hivi, basi Mwislamu anatakiwa amjibu: Swali hili wamelijibu ulama wa kiyahudi na kinaswara wao wenyewe, pale walipo­kiri waziwazi kuwa Tawrat ya asili iliyoteremshwa kwa Musa imepotea na baada ya kupita miaka akaja mmoja akadai kuwa ameihifadhi moyoni na akaandika madai yake haya; kisha akasema: na iwe ni Tawrat ya Musa, basi ikawa. Hivyo hivyo ikatokea kwa Injil.

Jambo la kushangaza ni kuwa Injil ya Bwana Masih(a.s) , baada ya kupo­tea, yamezaliwa makumi ya Injil zaidi ya hamsini. Mnamo mwaka 325 walikongamana viongozi wa kikiristo na wakakubali injil nne, na hali Isa alikuwa na Injil moja tu, kama wanavyokubaliana manaswara wote. Ni nani basi aliyefanya moja kuwa nne? Lau wangelikubali tatu tungelisema kila mmoja katika watatu (baba mwana na roho mtakatifu) ana yake.

Kinachofahamisha zaidi kuwa Injil hii inatokana na watu wa kanisa, na sio na Masih, ni kuwa ilizuka baada ya kusulubiwa kwake, kuzikwa kwake na kupaa kwake mbinguni. Je alishukiwa na wahyi baada ya kusulubiwa na kuzikwa?

Ikiwa hilo linawezekana, je inawezekana katika hukumu ya kiakili na uhalisia kushukiwa na wahyi ulioandikwa kwenye Injil baada ya yeye kupaa mbinguni?

Swali la pili : Je, kukiri huku kunapatikana wapi kwa ulama wa kiyahudi na kinaswara?

Jibu : Kwenye vitabu vyao kadhaa vya kiarabu na vya lugha nyinginezo. Katika vya kiarabu ni Qamusul kitabulmuqaddas (Kamusi ya Kitabu kitakatifu), ambayo walishiriki wataalamu 27 kuitengeneza. Katika mada ya Yoshua, inasema: “Ni jambo lisilo na shaka kwamba sehemu kubwa ya kitabu kitakatifu iliharibiwa au ilikosekana wakati wa kumritadi Mwenyezi Mungu na vikwazo.” Katika mada ya Vitabu inasema: “Kuna rai inayosema kuwa walioongeza sifa ya kanuni ya agano la kale ni waandishi wenyewe wa kitabu, na rai nyingine inasema ni waandishi wanaosaidiwa na roho mtakatifu, wakiwe­mo viongozi wa kidini wa kiyahudi na wa kimasihi ambao walikubali kita­bu hiki kwa kuongozwa na roho mtakatifu vile vile.”

Huku ni kukiri kusiko na shaka kwamba vitabu vya asili vimepotea na kwamba jamaa waliandika vitabu na kuongeza sifa ya utakatifu wao wenyewe. Na kauli nyingine ni kwa kuongozwa na roho mtakatifu. Tukichukua kauli ya kwanza au ya pili yote ni sawa, natija ni moja tu, kwamba wanakubali kuwa vitabu vilivyoko hivi sasa sio vitabu vya asili vya Musa na Isa; isipokuwa ni vitabu vipya vilivyoandikwa na wale wanaodai ni watakatifu au wanaodaiwa ni watakatifu kwa kupewa nguvu na roho mtakatifu.

Roho mtakatifu, kwao, ni roho wa Mungu katika wale watatu. Mwenyezi Mungu amemwita roho, kwa vile analeta uhai, na mtakatifu kwa vile anaz­itakasa roho za waumini.

Maulama wa Kiislamu wametunga makumi ya vitabu vinavyofahamisha kupotolewa Tawrat na Injil; miongoni mwavyo ni Idh-harulhaqq cha Sheikh Rahmatullah Al-Hindiy.

Ndani yake mna ushahidi 100 wa kuthibitisha upotofu wa Tawrat na Injil, kimatamshi na kimaana. Mwenye Tafsir Al-manar amemwashiria mwandishi huyu alipofasiri sura Annisa aya 46.

Vitabu vingine ni: Arrihlatulmadrasiya cha Sheikh Jawad Albalaghi, Muhammad rasulullah fi bisharatil-anbiya cha Muhammad Abdulghaffar, Muhammad hakadha basharat al-anajil cha Bushra Zachary Michael Kitabu cha mwisho kukisoma katika maudhui haya ni Bisharat wal­muqaranat cha Sheikh Muhammad Assadiq Tehraniy, kilichotoka hivi karibuni. Kimejaa ushahidi mkataa kutoka kwenye vitabu vya kiyahudi na kinaswara, kuhusu kupotolewa Tawrat na Injil zilizoko hivi sasa.

Lakini alipowaletea hoja zilizo wazi, walisema: Huu ni uchawi ulio dhahiri!

Mayahudi hawakutosheka kumwambia Bwana Masih(a.s) kuwa ni mchawi, bali walithubutu kusema kuwa ni mtoto wa seremala; kama ilivyosemwa kwenya Injil ya Mathayo (13:55) na Injil Marko (6:3). ikinukuu kuwa Mayahudi walimtusi Bibi bikira kuwa alizini.

Lakini pamoja na yote hayo tunawaona wakirsto wengi wanaungana na uzayuni, ulio adui wa dini na utu, hasa kwa Bwana Masihi. Wanaungana dhidi ya Uislamu uliosema:

مَّا الْمَسِيحُ ابْنُ مَرْيَمَ إِلَّا رَسُولٌ قَدْ خَلَتْ مِن قَبْلِهِ الرُّسُلُ وَأُمُّهُ صِدِّيقَةٌ ﴿٧٥﴾

“Masih mwana wa Maryam hakuwa ila ni Mtume. Wamepita kabla yake Mitume, na mama yake ni mkweli.” Juz. 6 (5:75).

Hii inafahamisha tu kuwa umasihi, kwa wale wanaowasaidia waisrail, ni kiasi cha nembo tu ya makusudio mengine na kwamba dini yao na dhamiri zao ni kutawala na kuchokoza; sawa na uzayuni ulivyo.

وَمَنْ أَظْلَمُ مِمَّنِ افْتَرَىٰ عَلَى اللَّـهِ الْكَذِبَ وَهُوَ يُدْعَىٰ إِلَى الْإِسْلَامِ وَاللَّـهُ لَا يَهْدِي الْقَوْمَ الظَّالِمِينَ ﴿٧﴾

7. Na ni nani mwenye kudhulu­mu zaidi kuliko yule anayem­zulia Mwenyezi Mungu uwon­go, naye anaitwa kwenye Uislamu? Na Mwenyezi Mungu hawaongoi watu mad­haalimu.

يُرِيدُونَ لِيُطْفِئُوا نُورَ اللَّـهِ بِأَفْوَاهِهِمْ وَاللَّـهُ مُتِمُّ نُورِهِ وَلَوْ كَرِهَ الْكَافِرُونَ ﴿٨﴾

8. Wanataka kuizima nuru ya Mwenyezi Mungu kwa vinywa vyao. Na Mwenyezi Mungu atakamilisha nuru yake ijapo­kuwa makafiri watachukia.

هُوَ الَّذِي أَرْسَلَ رَسُولَهُ بِالْهُدَىٰ وَدِينِ الْحَقِّ لِيُظْهِرَهُ عَلَى الدِّينِ كُلِّهِ وَلَوْ كَرِهَ الْمُشْرِكُونَ ﴿٩﴾

9. Yeye ndiye Aliyemtuma Mtume wake kwa uongofu na dini ya haki ili ipate kushinda dini zote, ijapokwa washiriki­na watachukia.

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا هَلْ أَدُلُّكُمْ عَلَىٰ تِجَارَةٍ تُنجِيكُم مِّنْ عَذَابٍ أَلِيمٍ ﴿١٠﴾

10. Enyi mlioamini! Je, niwajulis­he biashara itakayowaokoa na adhabu iliyo chungu?

تُؤْمِنُونَ بِاللَّـهِ وَرَسُولِهِ وَتُجَاهِدُونَ فِي سَبِيلِ اللَّـهِ بِأَمْوَالِكُمْ وَأَنفُسِكُمْ ذَٰلِكُمْ خَيْرٌ لَّكُمْ إِن كُنتُمْ تَعْلَمُونَ ﴿١١﴾

11. Mwaminini Mwenyezi Mungu na Mtume wake, na piganeni Jihadi katika Njia ya Mwenyezi Mungu kwa mali yenu na nafsi zenu. Haya ni bora kwenu, ikiwa nyinyi mnajua.

يَغْفِرْ لَكُمْ ذُنُوبَكُمْ وَيُدْخِلْكُمْ جَنَّاتٍ تَجْرِي مِن تَحْتِهَا الْأَنْهَارُ وَمَسَاكِنَ طَيِّبَةً فِي جَنَّاتِ عَدْنٍ ذَٰلِكَ الْفَوْزُ الْعَظِيمُ ﴿١٢﴾

12. Atawasamehe dhambi zenu, na atawatia katika Mabustani yapitiwayo na mito kati yake, na maskani nzuri katika Bustani za milele. Huko ndio kufuzu kukubwa.

وَأُخْرَىٰ تُحِبُّونَهَا نَصْرٌ مِّنَ اللَّـهِ وَفَتْحٌ قَرِيبٌ وَبَشِّرِ الْمُؤْمِنِينَ ﴿١٣﴾

13. Na kinginecho mkipendacho ­nusura itokayo kwa Mwenyezi Mungu na ushindi uliokaribu. Na wabashirieni Waumini!

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا كُونُوا أَنصَارَ اللَّـهِ كَمَا قَالَ عِيسَى ابْنُ مَرْيَمَ لِلْحَوَارِيِّينَ مَنْ أَنصَارِي إِلَى اللَّـهِ قَالَ الْحَوَارِيُّونَ نَحْنُ أَنصَارُ اللَّـهِ فَآمَنَت طَّائِفَةٌ مِّن بَنِي إِسْرَائِيلَ وَكَفَرَت طَّائِفَةٌ فَأَيَّدْنَا الَّذِينَ آمَنُوا عَلَىٰ عَدُوِّهِمْ فَأَصْبَحُوا ظَاهِرِينَ ﴿١٤﴾

14. Enyi mlioamini! Kuweni wasaidizi wa Mwenyezi Mungu, kama alivyosema Isa bin Maryam kuwaambia wanafunzi wake: Nani wasai­dizi wangu kwa Mwenyezi Mungu? Wakasema wanafun­zi: Sisi ni wasaidizi wa Mwenyezi Mungu! Basi taifa moja la Wana wa Israili lilia­mini, na taifa jingine lilikufuru. Ndipo tukawaunga mkono walioamini dhidi ya maadui zao, wakawa wenye kushinda.

MWENYEZI MUNGU ANAKAMILISHA NURU YAKE

Aya 7 – 14

MAANA

Na ni nani mwenye kudhulumu zaidi kuliko yule anayemzulia Mwenyezi Mungu uwongo, naye anaitwa kwenye Uislamu?

Mtume(s.a.w.w) aliwalingania watu wake watupilie mbali ushirikina na kumwamini Mwenyezi Mungu peke yake. Wakaona dhiki, wakampangia njama, wakatengenezea shaka juu yake na wakamzushia. Hivi ndivyo alivyo mbatilifu mwenye inadi, huwa anatengeneza uwongo na kuzua ubatil­fiu kila anapolinganiwa kwenye haki; ni sawa mlinganiaji awe Nabii au la.Na Mwenyezi Mungu hawaongoi watu madhaalimu, wale wanaomzus­hia Mwenyezi Mungu uwongo. Mfano wake ni kauli yake Mwenyezi Mungu:

لَا تَفْتَرُوا عَلَى اللَّـهِ كَذِبًا فَيُسْحِتَكُم بِعَذَابٍ وَقَدْ خَابَ مَنِ افْتَرَىٰ ﴿٦١﴾

“Msimzulie Mwenyezi Mungu uwongo, asije akawafutilia mbali kwa adhabu, hakika ameshindwa mwenye kuzua.” Juz. 16 (20:61).

Wanataka kuizima nuru ya Mwenyezi Mungu kwa vinywa vyao. Na Mwenyezi Mungu atakamilisha nuru yake ijapokuwa makafiri watachukia

Walijaribu kuumaliza Uislamu kwa uwongo na kusingizia, wakawa ni sawa na anayepingana na Mwenyezi Mungu katika ufalme wake. Mwenyezi Mungu hashindwi na jambo lake, lakini watu wengi hawajui.

Yeye ndiye Aliyemtuma Mtume wake kwa uongofu na dini ya haki ili ipate kushinda dini zote, ijapokwa washirikina wamechukia.

Makusudio ya Mtume hapa ni Muhammad(s.a.w.w) . Uwongofu ni Qur’an na dini ya haki ni Uislamu. Aya hii na ile iliyo kabla yake zimepita kwa herufi zake katika Juz. 10 (32-33).

Enyi mlioamini! Je, niwajulishe biashara itakayowaokoa na adhabu iliyo chungu?

Dunia ni biashara ya kila mtu. Hakuna yeyote katika maisha haya ila anakusudia masilahi na faida katika matendo yake na matumizi yake. Lakini kuna masilahi mabaya; kama yule anayefanya kwa ajili ya umashuhuri na kurundika mali kwa njia yoyote ile. Masilahi mengine ni mazuri na ya heri; kama yule anayefanya kwa ajili ya haja yake na haja ya wengine.

Kwa kuwa faida ndio msukumo wa kwanza wa kufanya amali, ndio Mwenyezi Mungu (s.w.t) akawaonyesha waja wake biashara itakayowaokoa na ghadhabu na adhabu yake na kufuzu kwa kupata radhi na thawabu zake. Hakuna faida kama amani na kupata Pepo. Mwenyezi Mungu ameweka masharti ya kupata faida hii, kwa kauli yake:

Mwaminini Mwenyezi Mungu na Mtume wake, na piganeni Jihadi katika Njia ya Mwenyezi Mungu kwa mali yenu na nafsi zenu.

Hii ndio thamani ‧ imani isiyokuwa na shaka, kujitolea mhanga na kujitolea mali. Likishahakika hilo itatimia kandarasi na Mwenyezi Mungu. Na ninani mwenye kutekeleza ahadi zaidi kuliko Mwenyezi Mungu? Imesemwa katika Nahjulbalagha:“Hakuna thamani ya nafsi zenu isipokuwa Pepo, basi msiiuze ila kwenye hiyo.”

Haya ni bora kwenu, ikiwa nyinyi mnajua.

Kuokoka na adhabu ya Mwenyezi Mungu na kufuzu kupata thawabu zake ni bora kuliko nafsi, mali na watoto.

Atawasamehe dhambi zenu, na atawatia katika Mabustani yapitiwayo na mito kati yake, na maskani nzuri katika Bustani za milele.

Huu ni ubainifu na ufafanuzi wa faida inayopatikana kutokana na biashara hii. Faida ya kwanza ni kughufiriwa dhambi. Hakuna uhuru zaidi mbele ya Mwenyezi Mungu kuliko kuwa huru na dhambi zake. Faida ya pili, ni makazi ya kudumu na neema ya milele.

Huko ndio kufuzu kukubwa ambako hakuna kufuzu kwingine zaidi yake.Na kinginecho mkipendacho nusura itokayo kwa Mwenyezi Mungu na ushindi uliokaribu. Na wabashirieni Waumini!

Makusudio ya nusura hapa ni ushindi wa kuiteka Makka; kama inavyoku­ja haraka akilini. Maswahaba walikuwa wakitamani sana ushindi huu kutokana na adha waliyokuwa wakiipata kutoka kwa washirikina wa Makka. Ndio Mwenyezi Mungu (s.w.t) akamwambia Mtume wake awabashirie ushindi huu na kuwa uko karibu, baada ya kuwabashiria maghufira na Pepo.

Enyi mlioamini! Kuweni wasaidizi wa Mwenyezi Mungu, kama alivyosema Isa bin Mariamu kuwaambia wanafunzi wake: Nani wasaidizi wangu kwa Mwenyezi Mungu? Wakasema wanafunzi: Sisi ni wasaidizi wa Mwenyezi Mungu!

Maneno yanaelekezwa kwa mswahaba, Mwenyezi Mungu akiwaamuru, wawe na Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) , kama vile walivyokuwa wanafunzi wa Isa kwa kauli na vitendo. Umetangulia mfano wake katika Juz. 3 (3:52). Katika kamusi ya Kitabu kitakatifu imeandikwa: “Yesu anaitwa Mnazareti (mnaswara)… jina hilo linarudia mji wa Nazareti (Naswiriy).

Ama masia (masih) ni msimbo wake. Ameitwa hivyo kwa kujitolea kwake. Waumini wake wameitwa wamasia mwaka 42 au 43. Mwanzoni jina hili lilikuwa ni tusi. Baina ya Isa na Musa kuna miaka si chini ya 1200 na si zaidi ya 1491. kwa sababu wanahistoria wana kauli nyingi juu ya hilo.

Basi taifa moja la Wana wa Israili liliamini, na taifa jingine lilikufuru. Ndipo tukawaunga mkono walioamini dhidi ya maadui zao, wakawa wenye kushinda.

Makusudio ya kushinda hapa ni kushinda kwa hoja na dalili. Maana ni kuwa wana wa Israil walitofautiana kuhusiana na Isa akiwa anatokana na wao. Kuna waliosema ni mja wa Mwenyezi Mungu na Mtume wake, wengine wakasema ni Mungu na mayahudi wakasema ni mchawi na mtoto wa zina. Mwenyezi Mungu (s.w.t) akawapa nguvu waliosema ni Mtume wa Mwenyezi Mungu dhidi ya wale waliosema ni Mungu.

Katika Waraka wa Yohana imeelezwa kuwa, aliye dhidi ya Masih ni yule anayekana kuwa na mwili na kuungana umungu wa masih na ubinadamu wake. Ama Qur’an inasema kuwa maadui wa Masih ni wale waliozama sana kuhusu yeye na waliosema dhidi yake.

MWISHO WA SURA YA SITINI NA MOJA: SURAT AS – SAFF

8

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE

Sura Ya Sitini Na Mbili: Surat Al-Jum’a. Imeshuka Madina Ina Aya 11.

بِسْمِ اللَّهِ الرَّحْمَٰنِ الرَّحِيمِ

Kwa jina la Mwenyezi Mungu Mwingi wa rehema Mwenye kurehemu.

يُسَبِّحُ لِلَّـهِ مَا فِي السَّمَاوَاتِ وَمَا فِي الْأَرْضِ الْمَلِكِ الْقُدُّوسِ الْعَزِيزِ الْحَكِيمِ ﴿١﴾

1. Vinamsabihi vilivyo katika mbingu na vilivyo katika ardhi, Mfalme, Mtakatifu, Mwenye nguvu, Mwenye hiki­ma

هُوَ الَّذِي بَعَثَ فِي الْأُمِّيِّينَ رَسُولًا مِّنْهُمْ يَتْلُو عَلَيْهِمْ آيَاتِهِ وَيُزَكِّيهِمْ وَيُعَلِّمُهُمُ الْكِتَابَ وَالْحِكْمَةَ وَإِن كَانُوا مِن قَبْلُ لَفِي ضَلَالٍ مُّبِينٍ ﴿٢﴾

2. Yeye ndiye Aliyempeleka Mtume kwenye watu wasiojua kusoma, aliyetokana na wao, awasomee Aya zake, na awatakase, Na awafunze Kitabu na hikima, Japokuwa hapo kabla walikuwa katika upotofu uliodhahiri.

وَآخَرِينَ مِنْهُمْ لَمَّا يَلْحَقُوا بِهِمْ وَهُوَ الْعَزِيزُ الْحَكِيمُ ﴿٣﴾

3. Na kwa wengine ambao bado hawajaungana nao. Na Yeye ndiye Mwenye nguvu, Mwenye hikima.

ذَٰلِكَ فَضْلُ اللَّـهِ يُؤْتِيهِ مَن يَشَاءُ وَاللَّـهُ ذُو الْفَضْلِ الْعَظِيمِ ﴿٤﴾

4. Hayo ni fadhila ya Mwenyezi Mungu anayompa amtakaye. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye fadhila kubwa.

NDIYE ALIEWAPELEKEA MTUME

Aya 1-4

MAANA

Vinamsabihi vilivyo katika mbingu na vilivyo katika ardhi, Mfalme, Mtakatifu, Mwenye nguvu, Mwenye hikima.

Kila kilicho katika ulimwengu kinafahamisha umoja wa Mwenyezi Mungu na uweza wake. Hii ni tasbihi na kutukuza, ni ufalme unaotawala, utakati­fu wa kuepuka na vile visivyolaikina naye, ni nguvu isiyoshindwa na hiki­ma katika matumizi yake. Umetangulia mfano wake katika Juz. 27 (57:1), na katika Juzuu hii tuliyo nayo mwanzo wa sura 59 na 61.

Yeye ndiye Aliyempeleka Mtume kwenye watu wasiojua kusoma, aliyetokana na wao.

Makusudio ya wasiojua kusoma hapa ni waarabu. Mwenyezi Mungu (s.w.t) amewasifu kuwa hawajui kusoma kwa vile siku hizo wengi wao walikuwa hawasomi wala hawaandiki.

Neno wasiojua ‘kusoma,’ tumelifasiri kutokana na neno la kiarabu ummiy, ambalo baadhi wamesema kuwa makusudio ya Ummiy hapa ni watu wa Makka, kwa sababu Makka pia inaitwa Ummulqura, hivyo ummiy liwe limetokana na ummu.

Lakini kauli hii tunaipinga kwa sababu zifuatazo:­

1. Neno la kutojua kusoma ndilo linalokuja kwanza kwenye ufa­hamu.

2. Kauli yake Mwenyezi Mungu kwa kutumia neno hilo hilo ummiy:

وَمِنْهُمْ أُمِّيُّونَ لَا يَعْلَمُونَ الْكِتَابَ إِلَّا أَمَانِيَّ وَإِنْ هُمْ إِلَّا يَظُنُّونَ ﴿٧٨﴾

“Na wako miongoni mwao wasiojua kusoma; hawajui kitabu isipokuwa matamanio tu.”

Juz. 1 (2:78).

Na Qur’an inajifasiri yenyewe.

3. Kauli yake Mtume(s.a.w. w ) : Sisi ni umma usiosoma, hatuandiki wala hatuhisabu.”

Baaadhi ya watu wa Kitab wamesema kuwa kauli yake Mwenyezi Mungu: “Yeye ndiye Aliempeleka Mtume kwenye watu wasiojua kusoma, aliyeto­kana na wao, “ inajulisha kuwa Muhammad ni Mtume wa waarabu tu.

Hilo tumelijibu kwa ufafanuzi zaidi katika Juz. 7 (6:91-92) na katika Juz. 22 (33:36 - 40) kifungu cha: “Kwanini utume uliishia kwa Muhammad?

Kisha Mwenyezi Mungu (s.w.t) akabainisha ufahamu wa risala ya Nabii wake Mtukufu, kama ifuatavyo:- Awasomee Aya zake. Awafikishie risala ya Mola wake ambayo watak­wenda nayo kwenye njia ya maisha na uokovu.

Na awatakase . Azisafishe nafsi zao na shirki, akili zao na ujinga na amali zao na uovu na madhambi.

Na awafunze Kitabu . Awagurishe kutoka kwenye giza la upofu na ujinga kwenda kwenye nuru ya ilimu na uongofu, kwa mafundisho yake ambayo yanaitukuza ilimu na kutupilia mbali upotofu; na yanayojikita kwenye akili na maumbile ya kibinadamu.

Na hikima . kila linaloongoza kwenye heri katika itikadi na maadili basi hilo ni hikima. Ibn Al-arabi anasema: Hikima ni sifa ya kuhukumia wala haihukumiwi; yaani inakua juu wala haikaliwi juu.

Kwa ufupi ni kuwa risala ya Muhammad(s.a.w. w ) ni risala ya ubinadamu kwa ujumla, ikizungumza na watu kwa mazungumzo ya kiakili.

Sifa muhimu ya uislamu inayoutofautisha na dini nyingine, ni kuwa inakaribisha somo lolote la kimaudhui lenye insafu.

Ijapokuwa hapo kabla walikuwa katika upotofu uliodhahiri, wa ushirikina, ujinga, dhulma, chuki na mengineyo mabaya na machafu.

Na kwa wengine ambao bado hawajaungana nao.

Makusudio ya wengine ni kila mwenye kuingia uislamu baada ya Muhammad(s.a.w. w ) mpaka siku ya Kiyama, awe mwarabu au sio mwarabu. Maana ni kuwa Muhammad(s.a.w. w ) ni Nabii wa rehema kwa vizazi vyote na mwito wake ni wa watu wote. Wameuamini waarabu na wasiokuwa waarabu katika wakati wake na wanaendelea kuaamini wanofuatia mpaka siku ya ufufuo.

Na Yeye ndiye Mwenye nguvu, Mwenye hikima . Na kwa nguvu yake ameupa nguvu uislamu, akaueneza mashariki mwa ardhi na magharibi yake na kwa hikima yake amemchagua Muhammad(s.a.w. w ) kwa risala yake yenye kuenea.

Hayo ni fadhila ya Mwenyezi Mungu anayompa amtakaye. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye fadhila kubwa.

Hayo ni hayo ya kumtuma Muhammad(s.a.w. w ) . Ni fadhila kutoka kwa Mwenyezi Mungu na rehema kwa binadamu wote. Mfano ni kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu:

وَمَا أَرْسَلْنَاكَ إِلَّا رَحْمَةً لِّلْعَالَمِينَ ﴿١٠٧﴾

“Na hatukukutuma ila uwe ni rehema kwa walimwengu.” Juz. 17 (21:107)

مَثَلُ الَّذِينَ حُمِّلُوا التَّوْرَاةَ ثُمَّ لَمْ يَحْمِلُوهَا كَمَثَلِ الْحِمَارِ يَحْمِلُ أَسْفَارًا بِئْسَ مَثَلُ الْقَوْمِ الَّذِينَ كَذَّبُوا بِآيَاتِ اللَّـهِ وَاللَّـهُ لَا يَهْدِي الْقَوْمَ الظَّالِمِينَ ﴿٥﴾

5. Mfano wa waliobebeshwa Tawrati kisha wasiibebe, ni mfano wa punda anayebeba vitabu vikubwa. Mfano muovu mno wa watu waliokadhibisha Ishara za Mwenyezi Mungu, na Mwenyezi Mungu hawaongoi watu madhalimu.

قُلْ يَا أَيُّهَا الَّذِينَ هَادُوا إِن زَعَمْتُمْ أَنَّكُمْ أَوْلِيَاءُ لِلَّـهِ مِن دُونِ النَّاسِ فَتَمَنَّوُا الْمَوْتَ إِن كُنتُمْ صَادِقِينَ ﴿٦﴾

6. Sema: Enyi mlio Mayahudi! Ikiwa nyinyi mnadai kuwa ni vipenzi vya Mwenyezi Mungu pasipo kuwa watu wengine, basi yatamanini mauti, ikiwa mnasema kweli.

وَلَا يَتَمَنَّوْنَهُ أَبَدًا بِمَا قَدَّمَتْ أَيْدِيهِمْ وَاللَّـهُ عَلِيمٌ بِالظَّالِمِينَ ﴿٧﴾

7. Wala hawatayatamani kabisa, kwa sababu ya iliyokwisha yatanguliza mikono yao. Na Mwenyezi Mungu anawajua madhalimu.

قُلْ إِنَّ الْمَوْتَ الَّذِي تَفِرُّونَ مِنْهُ فَإِنَّهُ مُلَاقِيكُمْ ثُمَّ تُرَدُّونَ إِلَىٰ عَالِمِ الْغَيْبِ وَالشَّهَادَةِ فَيُنَبِّئُكُم بِمَا كُنتُمْ تَعْمَلُونَ ﴿٨﴾

8. Sema: Hakika mauti mnayoy­akimbia, bila ya shaka yatawakuta. Kisha mtarudishwa kwa Mwenye kuyajua ya ghaibu yanayoonekana. Hapo atawaambia mliyokuwa mkiyatenda.

KAMA MFANO WA PUNDA WAALIOBEBA VITABU

Aya 5 – 8

MAANA

Mfano wa waliobebeshwa Tawrati kisha wasiibebe, ni mfano wa punda anayebeba vitabu vikubwa.

Mayahudi wanasema sisi ni watu wa Tawrat na ndio kitabu chetu kitakati­fu, lakini pamoja na hayo wanamkana Muhammad aliyenukuliwa kwenye Tawrat. Kwa hiyo hali yao ni kama punda aliyebebeshwa mzigo wa vitabu vya ilimu kwenye mgongo wake, lakini hana akili ya kilichomo ndani yake wala kunufaika nacho.

Mayahudi wameipotoa Tawrat ya Musa na vitabu vingine vitakatifu kwao, hilo halina shaka. Tazama Aya 6 ya sura iliyopita. Kisha baada ya kuipotoa wakayafanyia kazi yale waliyoyapotoa. Tunataja mfano wa hayo katika kitabu walichokinasibisha kwa Ezekieli, ninanukuu:

“Na hao wengine aliwambia, nami nalisikia, Piteni kati ya miji nyuma yake; mkapige jicho lenu lisiachilie, wala msione huruma; waueni kabisa, mzee, na kijana, na msichana, na watoto wachanga, na wanawake…” Ezekili 9: (5-6).

Hii ndio Israil inayofuata misingi hii kila inapopata fursa, kuwaua wazee, vijana, watoto na wanawake, si kwa chochote ila kwa maangamizi na kumaliza.

Unaweza kuuliza : waislamu wengi hawaitumii Qur’an, je mfano wao ni kama mfano wa punda anayechukua mizigo?

Jibu : Waislamu hawakuipotoa Qur’an na kuondoa Aya zinazomkubali Musa, Isa, Tawrat na Injil za asili zilizo sahihi, kama walivyopotoa maya­hudi Tawrat na wanaswara Injil: “Semeni: Tumemwamini Mwenyezi Mungu na yale tuliyoteremshiwa na yale yaliyoteremshwa kwa Ibrahim na Ismail na Is’hak na Yaqub na wajukuu na aliyopewa Musa na Isa na pia yale waliyopewa Manabii (wengine) kutoka kwa Mola wao; hatutafautishi baina ya yeyote katika hao na sisi tumesilimu (tumenyenyekea) kwake.”Juz. 1 (2:136)

Kwa hiyo basi hakuna njia yoyote ya kufananisha wala kulaumu.

Mfano muovu mno wa watu waliokadhibisha Ishara za Mwenyezi Mungu.

Kila mwenye kukadhibisha haki anakuwa ametoa mfano kutoka kwenye nafsi yake juu ya ukafiri na ufisadi wake. Inafaa kila mtu kumwambia: Ni aibu kwako na huzuni.

Na Mwenyezi Mungu hawaongoi watu madhalimu.

Wataongoka vipi na hali upotevu umemea kwenye nyoyo zao.

Sema: Enyi mlio Mayahudi! Ikiwa nyinyi mnadai kuwa ni vipenzi vya Mwenyezi Mungu pasipo kuwa watu wengine, basi yatamanini mauti, ikiwa mnasema kweli. Wala hawatayatamani kabisa, kwa sababu ya iliyokwisha yatanguliza mikono yao. Na Mwenyezi Mungu anawajua madhalimu.

Mayahudi walidai kuwa wao ni taifa teule la Mwenyezi Mungu na kwam­ba ni vipenzi wa Mwenyezi Mungu na Pepo ni yao tu. Ndio akawarudi Mwenyezi Mungu kwamba wao ni waongo katika madai yao. Kama wangelikuwa wakweli katika madai yao wangelitamani kukutana na Mwenyezi Mungu. Kwa sababu yaliyoko kwake ni yenye kubaki na bora zaidi kuliko fedheha waliyo nayo.

Wapi! Wao wanachukia mauti na wanayahofia, kwa wingi wa madhambi yao. La kushangaza ni kuwa wao bado wanaendelea na kung’ang’ania yale wanayohofia mauti kwayo. Umetangulia mfano wake katika Juz. 1 (2:94).

Sema: Hakika mauti mnayoyakimbia, bila ya shaka yatawakuta. Kisha mtarudishwa kwa Mwenye kuyajua ya ghaibu yanayoonekana.

Hapo atawaambia mliyokuwa mkiyatenda duniani, yakupotoa Kitabu na mengineyo ya ufisadi na makosa na atawalipa adhabu kali ya Jahannam.

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا إِذَا نُودِيَ لِلصَّلَاةِ مِن يَوْمِ الْجُمُعَةِ فَاسْعَوْا إِلَىٰ ذِكْرِ اللَّـهِ وَذَرُوا الْبَيْعَ ذَٰلِكُمْ خَيْرٌ لَّكُمْ إِن كُنتُمْ تَعْلَمُونَ ﴿٩﴾

9. Enyi mlioamini! Ikinadiwa Swala siku ya Ijumaa, nendeni upesi kwenye dhikri ya Mwenyezi Mungu, na wacheni biashara. Hayo ni bora kwenu, kama mnajua.

فَإِذَا قُضِيَتِ الصَّلَاةُ فَانتَشِرُوا فِي الْأَرْضِ وَابْتَغُوا مِن فَضْلِ اللَّـهِ وَاذْكُرُوا اللَّـهَ كَثِيرًا لَّعَلَّكُمْ تُفْلِحُونَ ﴿١٠﴾

10. Na itakapokwisha Swala, tawanyikeni katika ardhi mtafute fadhila za Mwenyezi Mungu, na mkumbukeni Mwenyezi Mungu kwa wingi ili mpate kufaulu.

وَإِذَا رَأَوْا تِجَارَةً أَوْ لَهْوًا انفَضُّوا إِلَيْهَا وَتَرَكُوكَ قَائِمًا قُلْ مَا عِندَ اللَّـهِ خَيْرٌ مِّنَ اللَّـهْوِ وَمِنَ التِّجَارَةِ وَاللَّـهُ خَيْرُ الرَّازِقِينَ ﴿١١﴾

11. Na wanapoiona biashara au pumbao wanayakimbilia hayo na wakakuacha umesi­mama. Sema: Yaliyoko kwa Mwenyezi Mungu ni bora kuliko pumbao na biashara. Na Mwenyezi Mungu ni Mbora wa watoa riziki.

SWALA YA IJUMA

Aya 9 – 11

MAANA

Enyi mlioamini! Ikinadiwa Swala siku ya Ijumaa, nendeni upesi kwenye dhikri ya Mwenyezi Mungu.

Kunadi swala ni kuadhini.

Swala ya Ijumaa ni wajibu kwa Kitabu, Sunna na Ijmai. Ina rakaa mbili kwa kutanguliwa na khutba mbili. Inaitosheleza swala ya Adhuhuri. Inahusika na wanaume. Hakuna tofauti baina ya waislamu katika hayo. Isipokuwa tofauti inakuwa ni: Je, ni wajibu bila ya masharti au ni lazima aweko kiongozi au naibu wake?

Hanafi na Shia Imamia wamesema, kuweko kiongozi (wa dini) au naibu wake ni sharti, lakini Imamia wameongeza sharti la uadilifu wa huyo kion­gozi; vinginevyo itakuwa kupatikana kwake na kukosekana kwake itakuwa ni sawa. Hanafi wametosheka na kuweko tu huyo kiongozi hata kama si mwadilifu.

Shafii, Malik na Hambali wamesema ni wajibu kwa hali yoyote ile. Imamia wamesema kama hakupatikana kiongozi na akawako fakihi mwadilifu kutakuwa na hiyari baina ya Ijumaa na Adhuhuri. Ufafanuzi uko kwenye Kitabu chetu Fiqh Imam Ja’afar As-swadiq Juz. 1.

Na wacheni biashara.

Makusudio ya biashara hapa ni matumizi yoyote yatakayozuia swala ya Ijumaa, iwe biashara au la. Mwenyezi Mungu (s.w.t) ametaja biashara, kwa vile mara nyingi huwa inategemea wakati au kwa vile watu wanapen­dela sana biashara kuliko viwanda na kilimo. Mafakihi wametofautiana kuhusiana na biashara inayofanywa wakati wa kunadiwa Ijumaa, je itaswihi au itaharibika na kutokuwa na athari yoyote, lakini ina dhambi kwa muuzaji na mnunuzi?

Biashra hii - kwetu - ni sahihi. Kwa sababu kukatazwa muamala hakufahamishi kuharibika, lakini hilo amelipinga mwenye Majamaul-bayan.

Hayo ni bora kwenu, kama mnajua mambo ya kheri na shari na yanayowadhuru na kuwanufaisha.

Na itakapokwisha Swala, tawanyikeni katika ardhi mtafute fadhila za Mwenyezi Mungu, na mkumbukeni Mwenyezi Mungu kwa wingi ili mpate kufaulu.

Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kuamuru swala ameamrisha kuhangaika kutafuta riziki na maisha kwa biashara na mengineyo, pamoja na kumtegemea Mwenyezi Mungu, katika hali zote. Kwa kipimo hiki ndio kutahakikika kufaulu duniani na Akhera; mfano wake ni kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu:

وَابْتَغِ فِيمَا آتَاكَ اللَّـهُ الدَّارَ الْآخِرَةَ وَلَا تَنسَ نَصِيبَكَ مِنَ الدُّنْيَا ﴿٧٧﴾

“Na utafute kwa aliyokupa Mwenyezi Mungu makazi ya akhera; wala usisahau fungu lako la dunia.” Juz. 20 (28:77).

Kwa maneno mengine ni kuwa hakuna tofauti mbele ya Mwenyezi Mungu baina ya anayeacha kuifanyia kazi Akhera yake na anayeacha kuifanyia kazi dunia yake.

Na wanapoiona biashara au pumbao wanayakimbilia hayo na wakakuacha umesimama.

Katika vitabu vya tafsir na Hadith kuna maelezo kuwa siku moja Mtume(s.a.w. w ) alipokuwa amesima akihutubia swala ya Ijumaa, uliingia msafara wa ngamia uliobeba chakula, basi maswahaba wakautokea, na hawakubakia na Mtume isipokuwa watu 12, ndio ikashuka Aya hii.

Riwaya hii imepokewa kwa njia mbalimbali na kuandikwa kwenye vitaba vya sahih, kwa sababu mmojawapo wa wapokezi wake ni Jabir bin Abdillah Al-answari, ambaye ni katika watu wakweli na mwadilifu. Kwa hiyo riwaya inakuwa ni tafsiri na ubainifu wa Aya.

Kwa mnasaba huu tunaashiria kwamba masilahi ya kimada yana athari kubwa katika maisha ya watu. Kwa sababu uchumi ni mhimili wa maisha. Hilo halina shaka. Ndio maana Mwenyezi Mungu (s.w.t) akasema mkimaliza swala tawanyikeni katika ardhi mtafute.

Hata hivyo si sahihi kuse­ma kuwa uchumi ndio msukumo pekee wa kila harakati na msimamo wa mtu. Hapana! Kuna upande mwingine unamsukuma mtu kwenye harakati na kufanya kazi. Maswahaba wengi walimwacha Mtume akiwa amesima­ma na kwenda kwenye biashara, kama ilivyonukuu Aya, lakini wako waliobakia na Mtume, kama ilivyonukuu riwaya.

Sema: Yaliyoko kwa Mwenyezi Mungu ni bora kuliko pumbao na biashara. Na Mwenyezi Mungu ni Mbora wa watoa riziki.

Kwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) kuna riziki ya dunia na ya Akhera, na baina yake hakuna kizuizi. Si amali ya Akhera inayopunguza riziki ya dunia wala sio amali ya dunia inayopunguza riziki ya Akhera; bali kila amali inay­otekeleza haja ya maisha basi hiyo ni amali ya Akhera vile vile.

Sitakua nimekwenda mbali kama nikisema kuwa kila amali aliyoyahalal­isha Mwenyezi Mungu, katika maisha haya, basi ni ngazi ya Akhera. Na aliyoyahalalisha Mwenyezi Mungu kwa waja wake ni mengi mno. Imam Ali(a.s ) anasema:“aliyowahalalishia Mwenyezi Mungu ni mengi zaidi ya aliyowaharamishia. Basi acheni yaliyo machache mchukue mengi, na muwache yaliyofinyu mchukue yaliyo na nafasi.”

MWISHO WA SURA YA SITINI NA MBILI: SURAT AL-JUM’A

6

ILI NIWE PAMOJA NA WAKWELI

UCHAMBUZI WA MADA

Madda muhimu katika uchambuzi: Imebakia madda moja muhimu ndani ya uchambuzi wote huu, madda ambayo inataka kuangaliwa kwa makini na kusomwa, na huenda hiyo pekee ndiyo kikwazo ambacho huwachemua wapinzani pale wanaposhinikizwa kwa hoja nzito. Utawaona wanashangaa na kutokuamini ya kuwa Masahaba wapatao laki moja walihudhuria kutawazwa kwa Imam Ali (kuwa Khalifa wa Mtume) na hatimaye hao hao Masahaba wakaafikiana wote kumkhalifu Imam Ali na kumpuuza na miongoni mwao wamo Masahaba wakubwa.

Hali hii (ya kushangazwa kwa wapinzani) imepata kunitokea mimi mwenyewe wakati nilipoingia kikamilifu ndani ya utafiti, sikuamini na haiwezekani kwa mtu yeyote kuamini pindi tukio hili linapoaridhiwa kama lilivyo, lakini wakati tunapolisoma tukio hili kwa pande zote basi kule kushangaa kunaondoka kwani hali halisi haiko kama tunavyoitazamia sisi au kama wanavyoiaridhi Masunni (ya kuwa) haiwezekani Masahaba laki moja wakaenda kinyume na amri ya Mtume, hivyo basi ilikuwaje mambo yakatokea kama yalivyotokea?

Kwanza Siyo kila aliyehuduria Baia ya Ghadir alikuwa akiishi Madina, bali ilikuwa kama ambavyo hali halisi ilivyokuwa kwamba kwa kiasi kikubwa itakuwa ni watu elfu tatu au Nne tu miongoni mwa Masahaba hao ndiyo waliokuwa wakiishi Madina.Na tutakapofahamu ya kwamba wengi wa hawa walikuwa ni watumwa na walioachwa huru na wanyonge ambao walimfikia Mtume (s.a.w.) kutoka sehemu mbali mbali na hapo Madina hawakuwa na uwenyeji wala jamaa (kwa mfano watu wa As-Safah) basi haitabakia isipokuwa nusu yao yaani watu elfu mbili tu, na hata hawa nao ni watiifu kwa viongozi wa makabila na muongozo wa kidugu ambao ndiyo wanaohusika nao na Mtume aliwakubalia (kuwa watiifu kwa viongozi wao) kwani ulipokuwa ukimfikia ujumbe wa kabila fulani, Mtume (s.a.w.) humtawalisha juu yao kiongozi wao, na kwa ajili hiyo ndiyo tumekuta katika Uislamu Istilahi ya kuitwa kwao kuwa ni Ahlul-Hilli wal-Iqdi, watu wanaotumainiwa kutowa maamuzi katika jamii au nchi.

Kadhalika tunapoutazama mkutano wa Saqifah ambao ulikutana mara tu baada ya kufariki Mtume (s.a.w.), tunawakuta waliohudhuria ambao waliuthibitisha uchaguzi wa Abubakar kuwa ni khalifa, idadi yao haizidi watu mia moja kwa makadirio ya juu, kwani katika Ansari ambao ndiyo wenyeji wa Madina hawakuhudhuria isipokuwa viongozi wao kama ambavyo Muhajirina ambao ni wenyeji wa Maka waliohama pamoja na Mtume (s.a.w.) hawakuhudhuria isipokuwa watu watatu au wanne wakiwakilisha Maquraishi. Hali hii itoshe basi kuwa ni dalili ya kupima ukubwa wa hiyo Saqifah ikoje, Saqifah ambayo ilikuwa haina nafasi ya kutosha, kwani haikuwa inakosa kuwa karibu katika kila nyurnba.

Kwa hiyo haikuwa uwanja wa maadhimisho wala siyo jumba la mikutano, na tunaposema kuwa watu mia moja walihudhuria hapo Saqifah bani Saida basi idadi hiyo sisi ndiyo tunaoizidisha ili tu, mwenye kutafiti aweze kufahamu kwamba wale Masahaba laki moja hawakuwepo wala hata hawakusikia mazungumzo yalivyofanyika ndani ya Saqifah isipokuwa baada ya muda mrefu kupita, .kwani hapo zamani hapakuwa na mawasiliano ya anga wala simu au Satellite.

Na baada ya mabwana wakubwa hawa kuafikiana juu ya Abubakar pamoja na upinzani wa bwana wa Kiansari Saad bin Ubbadah ambaye ni kiongozi wa kabila la Khazraj na mwanawe Qais, lakini wengi mno miongoni mwao (kama isemwavyo hii leo) walipitisha makubaliano hayo na kumpa Abubakar mkono wa Baia, wakati ambapo Waislamu wengi hawakuwepo hapo Saqifah, na baadhi yao walikuwa wameshughulika kumuandaa Mtume (s.a.w.) kwa mazishi au walihamanika kutokana na khabari za kifo chake, ambapo Umar bin Al-Khatab naye alikuwa amewatisha na kuwatia khofu iwapo watasema kuwa Mtume amefariki. Taz: Sahih BukhariJuz. 4 -195.

Zaidi ya hayo wengi wa Masahaba wa Mtume walikuwa amewateua wawemo ndani ya Jeshi la Usamaha na wengi wao walikuwa wameweka kambi mahala paitwapo Jorfi wakiwa tayari kwenda vitani na jeshi la Usamah hawakuwepo Mtume alipofariki wala hawakuhudhuria mkutano wa Saqifah. Basi je, inaingia akilini baada ya haya yaliyotokea kwamba mtu fulani katika kabila au ukoo kumpinga kiongozi wake kwa lile alilolipitisha na hasa inapokuwa hilo alilolipitisha lina ubora na utukufu mkubwa ambao kila kabila linaukimbilia? Ni nani ajuwaye ya kwamba huenda siku moja naye atawatawalia Waislamu wote, maadamu mwenye haki hiyo kisheria amekwisha tupwa mbali na mambo sasa yanakwenda kwa kushauriana wanabadilishana kwa kuachiana, basi ni kwa nini wasilifurahie hilo, na ni kwa nini wasiliunge mkono?

Pili Ikiwa wenye uwezo wa kuamua ni wakaazi wa Madina na wamepitisha jambo fulani, basi watu walio mbali katika sehemu mbali mbali za bara Arabu hawawezi kupinga na hali ya kuwa hawajui yanayopita wakati hawapo kwani vifaa vya mawasiliano kwa zama hizo vilikuwa ni vile vya kizamani kisha wao walikuwa wakifahamu kwamba wakazi wa Madina ndiyo waliokuwa wakiishi na Mtume wa Mwenyezi Mungu hivyo basi hao ndiyo wajuao mno mambo mapya miongoni mwa hukmu, kwani huenda ukashuka Wahyi wakati wowote au siku yoyote. Kisha kama kuna kiongozi wa kabila lolote lililo mbali na makao makuu basi jambo la Ukhalifa kwake si muhimu sana sana iwapo Abubakr atakuwa Khalifa au Ali au mtu mwingine yeyote, kwani watu wa Maka ndiyo wajuao zaidi utaifa wao, na cha muhimu kwao ni kubakia kwenye uongozi wa ukoo wake ambapo hakuna anayemkera katika uongozi huo.

Basi ni nani ajuwaye kwamba huenda baadhi ya watu waliulizia juu ya jambo hilo (la Ukhalifa) na walitaka kufahamu mambo yalivyokwenda lakini vyombo vya mtawala viliwanyamazisha sawa iwe kwa njia ya kuwapa tamaa ya mali au vyeo au vitisho, na huenda kisa cha Malik bin Nuwairah ambaye alikataa kutoa zaka kwa Abubakr ni utokea jambo hilo. Na yeyote mwenye kufuatilia matukio hayo yaliyotokea katika vita ya wanaokataa kutoa zaka katika zama za Abubakr atakuta kuna kupingana (kwa maelezo), wala hawezi kutosheka kwa maelezo yaliyoelezwa na baadhi .ya wanahistoria kwa lengo la kulinda heshima ya Masahaba na hasa wale watawala.

Tatu Kiini cha tatizo hili ni kule kushitukizwa ghafla kupatikana kwa Khalifa, hili ni jambo lililochangia mno kukubalika kwa kile ambacho leo kinaitwa kuwa "Hali halisi iliyopo". Kwani mkutano wa Saqifah ulifanyika ghafla kwa kuwashitukiza baadhi ya Mashaba ambao walikuwa wakimshughulikia Mtume (s.a.w.), na miongoni mwao alikuwa Imam Ali na Abbas na wengine miongoni mwa Bani Hashim, Miq-dad, Salman, Abu Dharri, Ammar, Zubair na wengineo wengi. Ama wale waliokuwa Saqifah walipotoka huko hali ya kuwa wakimshangilia Abubakr walielekea msikitini huku wakitoa mwito kwa watu wafanye baia ya jumla na watu wakaipokea baia hiyo kwa wingi watake wasitake kipindi hicho Imam Ali na wafuasi wake walikuwa hawajamaliza wajibu wao Mtukufu ambao tabia zao (mwenendo wao) mwema uliwalazimisha (wautimize) basi haikuwezekana kwao kumuacha Mtume (s.a.w.) bila ya kumkosha, kumvisha sanda, kumtayarisha na kumzika eti badala yake wakimbilie Saqifah kugombea Ukhalifa.

Walipomaliza wajibu wao huo, mambo yalikuwa yamekwisha kamilika kwa Abubakr na yeyote mwenye kwenda kinyume na baia hiyo akawa anahesabiwa kuwa ni miongoni mwa watu wenye fitna ambaye anabomoa umoja wa Waislamu, hivyo ni wajibu kwa Waislamu kumpinga au hata kumuuwa ikiwa itabidi, na ndiyo maana tunamuona Umar alimuonya Saad bin Ubbadah kuwa atauawa pale alipokataa kumbai Abubakr, Umar akasema, "Muuweni hakika yeye ni mtu wa fitna"[52] na baada ya hapo Umar aliwatishia wote waliobaki ndani ya nyumba ya Ali ya kuwa atachoma moto nyumba hiyo na wote waliomo humo. Tukishakufahamu vyema maoni ya Umar bin Al-Khatab kuhusu baia tutatambua mengi baada ya hapo miongoni mwa mambo yanayotatanisha.

Kwa hakika Umar anaona kuwa baia inatosha kusihi pale mmoja miongoni mwa Waislamu anapowahi, basi hapo inakuwa ni lazima kwa wengine kumfuata na yeyote atakayeasi miongoni mwao huyo atakuwa ametoka nje ya mshikamano ya Waislamu na ni wajibu kumuuwa. Basi hebu na tumsikilize yeye mwenyewe hasa kuhusu baia, kama alivyoeleza Bukhar ndani ya Sahih yake juzuu ya nane ukurasa wa ishirini na nane, Babu Rajmi Al-Hubla Minaz-Zinaa Idha-Ah-Sanat amesema: akisimulia yale yaliyotokea ndani ya Saqifah. "Basi fujo ikazidi na sauti zikapaa mpaka nikatishika kuwa kutatokea kuhitilafiana, nikasema, Ewe Abubakr kunjua mkono wako, Abubakar akakunjua mkono wake nikambai nao muhajirina wakambai[53] Ansari (nao wakambai) na tukamruka Saad bin Ubbadah, akasema msemaji miongoni mwao, "Mmemuuwa Saad bin Ubbadah" Mimi nikasema:

"Mwenyezi Mungu amuuwe Saad bin Ubbadah" Umar akasema: "Wallahi sisi hatujakutana na jambo gumu katika yote tuliyohudhuria kuliko kumbai Abubakar, tulichelea kuwa hawa jamaa tukiwaacha bila kupitisha baia, basi watambai mtu miongoni mwao baada yetu, hivyo imma tuwape madaraka, jambo ambalo hatulikubali, au tuwapinge itokee uharibifu, (naonya) yeyote atakayetoa baia bila ya kushauriana na Waislamu asifuatwe yeye wala yule aliyembai ili asiuawe. Basi jambo lililovyo kwa Umar siyo uchaguzi wala hiyari wala mashauriano, bali inatosha pale Mwislamu mmoja anapoiwahi baia hiyo iwe ni hoja kwa wengine na ndiyo maana alimwambia Abubakr, "Kunjua mkono wako Ewe Abubakar," na Abubakr naye akakunjua mkono wake akambai bila ya mashauriano tena haraka haraka kwa kuchelea kutanguliwa na mwingine na kwa hakika Umar amekwisha ieleza rai hii pale aliposema:

"Tulichelea lau tutawaacha watu hawa bila ya kuipitisha baia, watambai mtu miongoni mwao baia yetu (Umar aliwachelea Maansar wasimtangulie wakambai mtu miongoni mwao), na kinachomuongezea ufafanuzi zaidi ni pale anaposema: "Basi imma tuwape Baia jambo ambalo hatulikubali na au tuwapinge patokee uharibifu."[54]

Na ili tuwe waadilifu katika maamuzi na wenye kuchunguza kwa undani, inatupasa tukiri kwamba Umar bin Al-Khatab alibadilisha mtazamo wake kuhusu baia mwishoni mwa uhai wake na hilo ni pale mtu mmoja alipomjia Umar mbele ya Abdur-Rahman bin 'Auf katika Hijja yake ya mwisho aliyohiji, yule mtu akamwambia: "Ewe Amirul-Muuminina unayo habari kuwa fulani anasema, bila shaka Umar akifa hakika nitambai fulani kwani wallahi baia ya Abubakar haikuwa isipokuwa kwa kushitukiza tu na ilitimia". Umar alikasirika na kwa ajili hii alisimama akawahutubia watu alipokuwa akirudi Madina, miongoni mwa aliyoyasema katika khutba yake ni haya yafuatayo:

"Kwa hakika nimepata habari kwamba kuna asemaye miongoni mwenu kuwa, Wallahi lau Umar atakufa nitambai fulani, basi na asijidanganye mmoja wenu kusema kuwa baia ya Abubakar ilikuwa hivyo lakini Mwenyezi Mungu aliikinga shari yake.."[55] Kisha Anasema: "Yeyote mwenye kumbai mtu bila mashauriano kutoka kwa Waislamu, basi huyo asipewe baia yeye wala huyo aliyembai kuhofia asije uwawa.[56]

Basi laiti Umar angekuwa na mtazamo huu siku ya Saqifah na asiwalazimishe Waislamu kumbai Abubakr ambako kulikuwa kwa kushitukiza, na Mwenyezi Mungu aliikinga shari yake kama alivyoshuhudia yeye mwenyewe, lakini imekuwaje Umari awe na rai hii mpya katika mtazamo huu mpya, hakika atakuwa amejihukumia kifo yeye mwenyewe na rafiki yake (Abubakr) kwa kuwa kwenye mtazamo wake mpya anasema: "Yeyote mwenye kumbai mtu bila ya mashauriano toka kwa Waislamu basi asipewe Baia yeye wala huyo aliyembai ili asije uwawa."

Imebakia juu yetu kufahamu ni kwa nini Umar alibadilisha maoni yake mwishoni mwa uhai wake pamoja na kwamba yeye anafahamu mno kuliko mwingine ya kuwa mtazamo wake mpya unatengua baia ya Abubakar iliyotimia bila ya mashauriano toka kwa Waislamu na ilikuwa ni baia ya kushitukiza? Pia mtazamo wake huu mpya unatengua baia yake yeye aliyopewa, kwani aliupata ukhalifa kwa tamko la Abubakar wakati wa kufa bila ya makubaliano kutoka kwa Waislamu, kiasi baadhi ya masahaba walikwenda kwa Abubakar wakamkemea kwa kuwatawalishia mtu msusuavu tena mgumu wa tabia.[57] Na Umar alipotoka ili awasomee watu maandiko ya Abubakr kuna mtu alimuuliza: "Ewe Baba Hafs kuna nini ndani ya waraka huo?" Umar akasema, Sijuwi, lakini mimi nitakuwa wa kwanza kusikiliza na kutii." yule mtu akasema: "Lakini Wallahi mimi najua kilichomo, wewe ulimtawalisha (Abubakar) kipindi cha mwanzo naye amekutawalisha kipindi hiki".

Taz: Al-Imam Was-Siyasah cha Ibnu Qutaibah Juz. 1 uk. 25Mlango unaohusu maradhi ya Abubakri na kumtawalisha kwake Umar. Kauli hii inafanana na kauli ya Imam Ali kumwambia Umar pale alipomuona anawalazimisha watu kwa nguvu wambai Abubakr akasema "Nifanye jambo ambalo wewe utakuwa na hisa (wanitaka) leo nilikazanie jambo lake ili kesho akurudishie"? Taz: Al-Imamah Was-Siyasah cha ibnu Qutaiba Juz. 1 uk. 18. Cha muhimu ni kufahamu ni kwa nini Umar alibadilisha mtazamo wake kuhusu Baia?

Mimi ninakurubia kuamini kwamba, wakati alipowasikia baadhi ya Masahaba wanataka kumbai Ali bin Abi Talib baada ya kufa Umar jambo ambalo yeye Umar kamwe hakubaliani nalo, kwa kuwa yeye ndiye aliyezipinga maagizo ya Mtume yaliyobayana, na akapinga Mtume (s.a.w.) asiwaandikie yale maandiko[58] kwa kuwa yeye alilifahamu lengo lake kiasi kwamba akamtuhumu Mtume kuwa anaweweseka na akawatisha watu wasiseme kuwa Mtume amekufa[59] yote hayo ni kwa sababu wasije wakawahi kumbai Ali. Umar alitilia mkazo baia ya Abubakr na akawalazimisha watu kwa nguvu waikubali baia hiyo na kisha kumuonya kila atayepinga kuwa atamuua[60] ili tu kumtenga mbali Ali na ukhalifa.

Hivi itawezekana Umar aridhie aseme msemaji kwamba fulani atapewa baia lau Umar atakufa? Hasa pale msemaji huyu ambaye jina lake limebakia kuwa halijulikani na hapana shaka kuwa alikuwa miongoni mwa Masahaba wakubwa? Msemaji huyu alitumia hoja ya kitendo alichokitenda Umar mwenyewe alipombai Abubakar pale anaposema: "Wallahi Baia ya Abubakr haikuwa isipokuwa ya kushitukiza na ikatimia", yaani pamoja na kuwa ilitokea kwa kuwashitukiza Waislamu na bila kupata ushauri wao lakini ilitimia na likawa jambo lililothibitika, kwa hiyo ilifaa kwa Umar kulifanya kwa Abubakr kwa nini isifae kwake kulifanya yeye mwenyewe kwa njia ile ile kwa mwingine? Na hapa tunaona kwamba ibn Abbas na Abdur-Rahman bin Auf na Umar bin Khatab wanakwepa kulitaja jina la huyu msemaji kama ambavyo wanakwepa kulitaja jina la mtu anayetaka kupewa baia msemaji huyu. Na ilipokuwa wawili hawa wanao umuhimu mkubwa kwa Waislamu, tunamuona Umar alikasirika kwa usemi huu na haraka katika Ijumaa ya kwanza aliwahutubia watu na akaieleza maudhui ya Ukhalifa itakavyokuwa baada yake na akawaonesha maoni yake mapya kuhusiana na Ukhalifa, ili azuwie njia ya huyu anayetaka kurudisha ile ghafla iliyokwisha tokea kwani njia hiyo itamnufaisha mgomvi wake, kwani kwa kupitia uchunguzi tumefahamu kuwa usemi huo haukuwa ni maoni ya fulani tu peke yake, bali ulikuwa ndiyo mtazamo wa Masahaba wengi, na ndiyo maana Bukhari anasema: "Umar alichukia na kisha akasema bila shaka apendapo Mwenyezi Mungu mimi nitasimama usiku huu miongoni mwa watu niwaonye hawa ambao wanataka kuwapora mambo yao..." [61]

Basi kubadilisha kwa Umar mtazamo wake kuhusu Baia ilikuwa ni kuwapinga hawa ambao wanataka kuwapokonya watu mambo yao na wambai Ali, na hili ni jambo ambalo Umar hakubaliani nalo kwani yeye anaitakidi kuwa Ukhalifa ni miongoni mwa mambo ya watu na siyo haki ya Ali bin abi Talib, na itikadi hii itapokuwa ni sahihi, basi ni kwa nini yeye Umar aliruhusu kuwapokonya watu mambo yao baada ya kufariki Mtume (s.a.w.) na haraka haraka akambai Abubakar bila ya makubaliano na Waislamu. Na msimamo wa Abu Hafs (Umar) dhidi ya Abul-Hasan (Ali) unaeleweka na ni mashuhuri mno, nao ni kumtenga Ali kwenye utawala kwa kutumia njia yoyote inayowezekana.

Na matokeo haya hatukuyafahamu kutokana na hotuba yake (Umar) iliyotangulia hapo kabla peke yake, lakini yeyote mwenye kufuatilia historia atafahamu kuwa Umar bin Al-Khatab alikuwa ndiye mtawala mtendaji hata katika Ukhalifa wa Abubakr na ndiyo maana tunamuona Abubakr anamuomba Usamah bin Zaid amuachie Umar bin Al-Khatab ili amsaidie kuhusu suala la Ukhalifa kama alivyoeleza hilo Ibn Saad ndani ya Tabaqat yake na pia wanahistoria wengi walioelezea jeshi la Usamah - pamoja na hayo tunamuona Ali bin Abi Talib anabakia mbali na majukumu, hawakumpa cheo chochote wala utawala wowote wala kumpa uamiri wa jeshi lolote lile na wala hawakumuamini kuwa mweka hazina na yote haya ni kwa kipindi cha Ukhalifa wa Abubakr, Umar na Uthman, nasi sote twamjua Ali bin Abi Talib ni nani.

Cha kushangaza kuliko yote haya ni kuwa, sisi tunasoma ndani ya vitabu vya historia kwamba kifo kilipomfikia Umar alisikitika kwamba lau Abu Ubaidah bin Al-Jarrah au Salim Huru wa Abu Hudhaifah wangekuwa hai angewatawalisha baada yake. Lakini hapana shaka Umar alikumbuka kuwa hapo kabla alikwisha badilisha mtazamo wake juu ya baia kama hii na akaiona kuwa ni ya kushitukiza na ni kupokonya mambo ya Waislamu, basi hapana budi kwake aweke njia mpya kuhusu baia ili kati kwa kati asije yeyote akafaulu kumbai amuonaye kuwa anafaa na kuwalazimisha watu kumfuata kama alivyofanya yeye kwa Abubakr na kama alivyofanya Abubakar kwake Umar au kama atakavyofanya fulani ambaye anangoja kufa kwa Umar ili ambai jamaa yake.Basi hili haliwezekani baada ya Umar kuwa ameuhukumia Ukhalifa kuwa ni jambo lililofanyika ghafla na kuwa linataka kuwa ni jambo la kupora, na haiwezekani pia kwake kuliacha jambo hili liwe la makubaliano baina ya Waislamu. Na ule mkutano wa Saqifah uliofuatia kufariki kwa Mtume (s.a.w.) yeye Umar alihudhuria na akajionea mwenyewe hitilafu iliyotokea ambayo karibu zitoke roho za watu na damu imwagike.

Basi baadaye alitoa fikra ya watu wa mashauriano au (tuseme) watu sita ambao peke yao ndiyo wenye haki ya kumchagua Khalifa na Muislamu mwingine yeyote hana haki ya kushirikiana nao katika jambo hilo, na Umar alikuwa akitambua kwamba tofauti baina ya watu hawa sita haiwezi kuepukwa, ndiyo maana aliusia ikiwa watatofautiana basi wawe kwenye upande alioko Abdur-Rahman bin Auf hata kama itapelekea kuwauwa watu watatu ambao watamkhalifu Abdur-Rahman bin Auf wakati watakapogawika watu hawa sita makundi mawili, na hilo ni muhali kwani Umar anafahamu kwamba Saad bin Abi Waqas ambaye ni ibn Ammi ya Abdur-Rahman bin Auf na wawili hawa ni ukoo wa Bani Zuhrah, na alifahamu pia kwamba Saad hampendi Ali na moyoni mwake kulikuwa na chuki kwani Ali ndiye aliyewauwa wajomba zake wa ukoo wa Abdis-Shams, kama ambavyo Umar alikuwa akifahamu kwamba Abdur-Rahman bin Auf ni shemeji wa Uthman kwani mkewe aliyekuwa akiitwa Ummu Kul-thum ni dada wa Uthman. Si hivyo tu kadhalika alifahamu kuwa Tal-hah akimpenda Uthman kutokana na mahusiano yaliyokuwepo baina yao kufuatana na maelezo ya baadhi ya wapokezi wa khabari, na hakika ilitosha kwa Tal-hah kumpenda Uthman kutokana na kumpinga kwake Ali kwani yeye Tal-hah ni katika ukoo wa Bani Taym, na kulikuwa na chuki fulani baina ya Bani Hashim na Bani Taym kutokana na Ukhalifa wa Abubakar.

Taz: Shark Najul-Balaghah ya Muhammad Abdoh, Juz. 1 uk. 88.

Umar alikuwa akiyajuwa yote hayo na kwa ajili hii ndiyo maana akawachagua hawa peke yao. Umar aliwachagua hawa watu sita na wote wakiwa ni Maquraish na wote ni kutoka katika Muhajirina na hakuna yeyote kati yao ambaye ni kutoka miongoni mwa Ansar na wote hawa kila mmoja wao akiwakilisha na kuongoza kabila lenye umuhimu wake na athari yake.

1. Ali bin Abi Talib, kiongozi wa Bani Hashim.

2. Uthman bin Affan kiongozi wa Bani Umayyah

3. Abdur-Rahman bin Auf, kiongozi wa Bani Zuhrah

4. Saad bin Abi Waqqas, yeye ni kutoka katika Bani Zuhrah na wajomba zake ni Bani Umayyah.

5. Tal-ha bin Ubaidullah, Bwana wa Bani Taym.

6. Zubair bin Al-Awwan, yeye ni mtoto wa Safiyyah ambaye ni shangazi yake Mtume na ni mume wa As-maa binti Abubakr.

Basi hawa ndiyo wenye kutoa maamuzi, na hukmu yao ikubaliwe na Waislam wote, sawa sawa wakiwa ni wakaazi wa Madina (Makao Makuu ya Ukhalifa) au wengineo katika ulimwengu wote wa Kiislamu na ni wajibu wa Waislamu yeyote atakayetoka miongoni mwao akawa kinyume cha maamuzi yao basi damu yake imwagwe (auawe). Na hili ndilo jambo pekee tulilokuwa tunataka kulisogeza katika akili ya msomaji kuhusiana na kunyamaziwa kwa tamko la Ghadir katika maelezo yaliyotangulia.

Na ikiwa Umar anaufahamu undani, mapenzi na mtazamo wa watu hawa sita, basi bila shaka yeye alikuwa kisha mpendekeza Uthman bin Affan kuwa Khalifah au alikuwa anajua kuwa wengi miongoni mwa hawa sita hawamkubali Ali, vinginevyo ni kwa nini na ni kwa haki gani Umar anatilia nguvu upande wa Abdur-Rahman bin Auf dhidi ya Ali bin Abi Talib wakati ambapo Waislamu tangu hapo zamani na mpaka leo wamekuwa wakishindana juu ya ubora wa Ali na Abubakar na hatujamsikia yeyote akimlinganisha Ali na Abdur-Rahman bin Auf.

Na hapa hapana budi nisimame kidogo ili niwaulize Masunni ambao wanatetea msingi wa mashauriano na pia (niwaulize) watu wenye fikra iliyohuru wote kwa ujumla, nawauliza wote hawa, ni vipi mnaafiki baina ya mashauriano kwa maana yake ya Kiislamu na baina ya fikra hii ambayo kama itajulisha kitu fulani basi haitajulisha isipokuwa ni maoni ya ki-dikteta, kwani yeye Umar ndiye aliyewachagua watu hawa sita na siyo Waislamu, na iwapo kuufikia kwake Ukhalifa lilikuwa ni jambo la ghafla, basi ni kwa haki ipi anawalazimisha Waislamu wakubali mmoja wa hawa sita?

Kinachojitokeza kwetu ni kwamba Umar anauona Ukhalifa kuwa ni haki ya Muhajirina peke yao na mwingine yeyote hana haki ya kuwakorofisha kwenye jambo hili, bali zaidi ya hivi ni kuwa Umar anaitakidi kama anavyoitakidi Abubakar kwamba Ukhalifa ni milki ya Maquraish, bali wamo pia wasiokuwa Waarabu, hivyo basi haistahiki kwa Sal-man Al-Farisi wala Ammar bin Yasir wala Bilal wa Uhabeshi wala Suhayb Mrumi, wala Abu Dharri Al-Ghifari wala maelfu ya Masahaba ambao siyo Maquraish (haistahiki kwao) kujitokeza kwa ajili ya Ukhalifa. Na haya siyo madai ya hivi hivi tu sivyo kabisa, bali hiyo ndiyo itikadi yao ambayo historia na wataalamu wa hadithi wameisajili kutoka vinywani mwao (kina Abubakar na Umar) na hebu tuirudie khutba yenyewe ambayo Bukhari na Muslim wameieleza ndani ya Sahih zao:

Umar bin Al-Khatab anasema:

"Nilitaka kusema, na nilikuwa nimetunga vizuri usemi ambao ulinifurahisha nikitaka niutamke mbele ya Abubakr na nilikuwa nikimzunguka karibu. Basi nilipotaka kusema Abubakr akasema, tulia (ewe Umar), na sikupenda kumkasirisha. Abubakar akazungumza, na alikuwa mpole mno kuliko mimi na mtulivu mno, Wallahi hakuacha neno lolote katika maneno nilioyaandaa isipokuwa aliyasema vizuri zaidi mpaka aliponyamaza kisha akasema, nilichokieleza kwenu katika wema ninyi ndiyo mnaostahiki (akiwaambia Maansari) na wala jambo hili halitatambulika isipokuwa kwa upande huu wa Maquraish. Taz: Sahih Bukhar Babul-Wasiyyah.

Kwa hiyo inatubainikia wazi- kwamba Abubakr na Umar hawaamini mashauriano na hiyari, na baadhi ya wanahistoria wanasema kwamba Abubakar alitoa hoja dhidi ya Maansar kwa hadithi ya Mtume (s.a.w.) isemayo kuwa "Ukhalifa uko kwa Maquraish" Na hadithi hiyo hapana shaka ni sahihi (kama walivyoitaja Bukhar na Muslim na Sahih zote kwa Masunni na Mashia) Mtume (s.a.w.) amesema: "Makhalifa baada yangu ni kumi na wawili na wote ni kutoka kwa Maquraishi" na hadithi iliyo wazi zaidi kuliko hii ni ile kauli ya Mtume (s.a.w.) aliposema:

"Jambo hili (la Ukhalifa) halitakoma kwa Maquraish muda wote hata wakibakia watu wawili"[62] pia kauli yake isemayo "Watu ni wafuasi wa Maquraishi katika kheri na shari[63].

Basi ikiwa Waislamu wote wanaziamini hadithi hizi, ni vipi mtu aseme kuwa Mtume aliliwacha suala la Ukhalifa liwe la mashauriano baina ya Waislamu wamchague wamtakaye? Na haiwezekani kwetu sisi kukwepa kupingana huku, isipokuwa tutakapoyachukua maneno ya Maimamu wa nyumba ya Mtume na wafuasi wao na baadhi ya wanachuoni wa Kisunni ambao wanasisitiza kwamba Mtume wa Mwenyezi Mungu aliwataja Makhalifa na akawabainisha kwa idadi yao na majina yao, na hapo ndipo utakapoweza pia kuufahamu msimamo wa Umar na kuuthibiti Ukhalifa kwa Maquraish na huyu Umar ni mtu aliyefahamika kwa Ijtihadi yake dhidi ya maagizo ya Mtume hata katika uhai wake mwenyewe Mtume (s.a.w.), kwani matukio ya Sul-hu ya Hudaybiyah[64] kuwasalia wanafiki,[65] msiba wa siku ya Al-Khamis,[66] na kuzuwiya kwake kubashiria watu pepo[67] ni ushahidi mkubwa wa haya tuyasemayo.

Basi haishangazi kwa Umar kufanya Ij-tihad baada ya kufariki Mtume dhidi ya hadithi inayohusu Ukhalifa, haoni ulazima wa kukubali agizo linalomuhusu Ali bin Abi Talib ambaye ni Quraish, mdogo kwa umri. Ni yeye aliyeidhibiti haki ya kumchagua Khalifa kwa Maquraish peke yao, na ni yeye ambaye alilazimisha peke yake kuchagua watu sita miongoni mwa watukufu wa Kiquraishi kabla hajafa ili ikubaliane kati ya hadithi ya Mtume (s.a.w.) na vile aonavyo yeye juu ya haki ya Maquraishi peke yao kuhusika na Ukhalifa. Huenda kumuingiza Ali katika kundi hilo hali yakuwa akifahamu kwamba wao hawatamchagua, ni udhibiti wake kwa Umma ili amlazimishe Ali kuingia pamoja nao ndani ya mchezo wa Kisiasa kama wanavyouita leo hii na ili pasibakie kwa Ali na wafuasi wake na wapenzi wake ambao walikuwa wakidai kuwa yeye ndiye wa mwanzo (pasibakie kwao) hoja yeyote. Lakini Imam Ali aliyazungumza yote hayo katika hotuba yake mbele ya watu wote akasema kuhusu jambo hilo:

"Nilivumilia muda wote wa taabu na majaribu mpaka alivyoondoka akauweka (Ukhalifa) chini ya maamuzi ya kikundi cha watu sita akidhania kuwa mimi nafanana nao oh! hayawi sawa ya Mungu na mashauriano! Toka lini nikatiliwa mashaka na wa kwanza miongoni mwao mpaka imebidi nilinganishwe na watu kama hawa! lakini nilitua walipotua na niliruka waliporuka (yaani, niliishi nao kwa hekima).

Nne: Hakika Imam Ali (a.s.) alitoa hoja dhidi yao kwa kila namna lakini bila mafanikio, na je, Imam Ali aombe baia ya watu ambao walimgeuzia nyuso zao na nyoyo zao zikawaelekea wengine imma kwa husuda dhidi yake kutokana na yale aliyompa Mwenyezi Mungu miongoni mwa fadhila zake, na imma kwa chuki dhidi yake kwani yeye ndiye aliyewaua mabwana zao, akawabomoa mashujaa wao, akawakatisha tamaa, akawadhalilisha na kuvunja ujeuri wao kwa upanga wake na ushujaa wake mpaka wakasilimu na kujisalimisha hali ya kuwa Imam Ali akiwa ni Mtukufu akimtetea mwana wa ammi yake (Mtume s.a.w.) na alipokuwa akifanya hayo haikumzuwia kuyatenda kwa ajili ya Mwenyezi Mungu lawama ya mwenye kulaumu na wala hakurudi nyuma kwenye azma yake kutokana na tamaa ya dunia. Mtume wa Mwenyezi Mungu (s.a.w.) naye alikuwa akiyajua vema hayo na kila tukio alikuwa akitilia mkazo fadhaila za nduguye na mwana wa ammi yake ili kuwafanya wampende. Mtume alikuwa akisema "Kumpenda Ali ni (dalili ya) imani na kumchukia (ni dalili ya) unafiki"[68] Na pia husema "Ali anatokana nami, nami natokana na Ali."[69] Na alikuwa akisema: "Ali ni mtawala wa kila muumini baada yangu"[70] na husema kuwa, "Ali ni mlango wa mji wa elimu yangu na ni baba wa wanangu."[71] Pia Mtume alikuwa akisema, "Ali ni Bwana wa Waislamu na ni Imamu wa wachamungu na ni kiongozi wa waumini wenye kutowa mwanga na nuru."[72]

Lakini inasikitisha kwamba yote hayo hayakuwazidishia isipokuwa chuki na husuda na kwa ajili hiyo Mtume alimuita Ali kabla ya kufariki akamkumbatia kisha akalia na akamwambia: "Ewe Ali bila shaka mimi nafahamu kwamba ndani ya nyoyo za jamaa hawa kuna shinikizo la chuki dhidi yako, na hapo baadaye watakudhihirishia baada yangu mimi, iwapo watakupa baia kubali vinginevyo basi subiri mpaka hapo utapokutana nami hali ya kuwa mwenye kudhulumiwa". Taz: Ar-Riyadun-Naz-Rah Fi Manaqibil-Asharah cha Tabari Babu Fadail Ali ibn Abi Talib. Basi ikiwa Abul-Hasan (a.s.) ilimlazimu kuvumilia baada ya baia ya Abubakr, hilo ni kutokana na usia wa Mtume kwake yeye na ndani ya hilo muna hekima ambayo iko wazi.

Tano: Zaidi ya yote hayo yaliyotangulia ni kwamba, Muislamu ataposoma Qur'an Tukufu na kuzizingatia aya zake, atafahamu kwa kupitia masimulizi yake kuhusu mambo ambayo yaliwafika watu na mataifa yaliyopita kwamba, kwao yalitokea mengi kuliko yale yaliyotokea kwetu sisi. Basi mwangalie huyu Qabil anamuuwa nduguye Habil kwa dhulma na uadui tu, na huyu hapa Nuh ambaye ni babu wa Manabii, baada ya miaka elfu moja ya jihadi hakuna aliyemfuata katika watu wake isipokuwa wachache tu, isitoshe mkewe na mwanawe walikuwa miongoni mwa makafiri.

Mtazame Nabii Lut haikupatikana katika kitongoji chake isipokuwa nyumba moja tu ya Waumini. Nao Mafirauni ambao walikuwa wenye kiburi katika nchi wakawafanya watu kuwa watumwa, hapakuwepo miongoni mwao isipokuwa Muumini mmoja anayeficha imani yake. Hawa hapa nduguze Yusuf watoto wa Yaaqub nao ni kikundi, wanakula njama kumuuwa ndugu yao mdogo asiye na kosa lolote lakini (wanafanya hivyo) kwa kumhusudu kwa kuwa yeye ni kipenzi kwa baba yao. Watazame wana wa Israel ambao Mwenyezi Mungu aliwaokoa kupitia kwa Musa na akawapasulia bahari na kumuangamiza adui yao Firauni na askari wake bila ya kuwakalifisha taabu yoyote ya vita, basi mara walipotoka baharini na nyayo zao hata hazijakauka, wakawafikia watu wanaoabudia sanamu (wana wa Israel) wakasema:

"Ewe Musa tutengenezee Mungu kama wao walivyo na Miungu, Musa akawaambia hakika ninyi ni watu msiojua." Na alipokwenda kwenye ahadi ya Mola wake na kumuacha nduguye Harun, walifanya njama dhidi yake karibu wamuuwe, wakamkufuru Mwenyezi Mungu, na wakamuabudia ndama kisha baadaye waliwauwa Manabii wa Mwenyezi Mungu. Mwenyezi Mungu anasema: "Kila walipokufikieni Mitume kwa yale ambayo nafsi zenu haziyapendi mlijivuna, kundi moja mlilipinga na kundi jingine mkaliua".(Qur'an, 2:87)

Huyu hapa naye Bwana wetu Yahya bin Zakariya naye ni Nabii na Mtawa miongoni mwa watu wema anauwawa na kichwa chake anazawadiwa mtu muovu miongoni mwa waovu wa Kibani Israel. Mayahudi na Wakristo nao walikula njama kumuua na kumsulubu bwana wetu Isa. Nao ummati wa Muhammad wanaandaa jeshi la kiasi ya watu elfu thelathini ili kumuuwa kipenzi cha Mtume wa Mwenyezi Mungu na Bwana wa vijana wa peponi ambaye hawakuwa pamoja naye isipokuwa watu Sabini miongoni mwa wafuasi wake, wakawauwa wote ikiwa ni pamoja na mwanawe mchanga. La ajabu ni lipi baada ya yote haya? Lipi litashangaza baada ya kauli ya Mtume kuwaambia Masahaba wake yakuwa: "Mutafuata nyendo za wale waliokuwa kabla yenu shubiri baada ya shubiri na dhiraa baada ya dhiraa mpaka hata wakiingia kwenye shimo la kenge nanyi mutaingia". wakasema, "Wadhani kuwa hao ni Mayahudi na Wakristo"? Mtume akasema, "Ni kina nani basi (kama si hao)"?

Taz: Sahih BukharJuz. 4 uk. 144 na Juz. 8 uk. 151. Ni kipi cha ajabu basi, nasi twasoma ndani ya Bukhar na Muslim kauli ya Mtume (s.a.w.) isemayo: "Siku ya Kiyama Masahaba wangu watapelekwa upande wa kushoto nami nitasema wanapelekwa wapi? Patasemwa Wallahi Motoni, nitasema, Ewe Mola wangu Masahaba wangu hao, patasemwa, Hakika wewe hujuwi waliyoyazusha baada yako, nitasema atengwe mbali aliyebadilisha baada yangu, na sitamuona anaokoka miongoni mwao isipokuwa kikundi kidogo kama cha ngamia waliotelekezwa".

Tax: Sahih Bukhar Juz. 7 uk. 209 na Sahih Muslim Babul-Haudh. Basi lipi la ajabu baada ya kauli yake Mtume (s.a.w.) aliposema: "Umati wangu utagawanyika makundi sabini na tatu na yote yataingia motoni isipokuwa kundi moja". Taz: Sunan Ibn Majah Kitabul-Fitan Juz. 2 hadith Na. 3993, Ahmad Juz. 3 uk. 120, Sunan Tirmidhi Kitabul-Iman. Amesema kweli Mwenyezi Mungu Mtukufu Mola mwenye nguvu na Utukufu, mjuzi wa undani wa nyoyo pale aliposema: "Na watu wengi hawataamini japo utapupia" (Qur'an, 12:103)

"Bali amewajia na ukweli na wengi wao wanaichukia kweli" (Qur'an,23:70)

"Bila shaka tumekujieni na ukweli lakini wengi wenu hawaupendi ukweli" (Qur'an 43:78)

"Fahamuni ya kwamba ahadi ya Mwenyezi Mungu ni ya kweli lakini wengi wao hawafahamu" (Qur'an, 10:55)

"Wanakuridhisheni kwa vinywa vyao na nyoyo zao zinakataa, na wengi wao ni mafasiki (Qur'an, 9:8)

"Bila shaka Mwenyezi Mungu ni mwenye fadhila juu ya watu, lakini watu wengi hawashukuru" (Qur'an, 10:60)

"Wanaitambua Neema ya Mwenyezi Mungu kisha wanaipinga na wengi wanakataa ila kukufuru tu" (Qur'an, 25:50)

"Na wengi wao hawawezi kumuamini Mwenyezi Mungu ila hali ya kuwa wanamshirikisha" (Qur'an, 12:106)

"Bali wengi wao hawaijuwi haki basi wao wanapinga" (Qur'an, 21:24)

"Hivi mwashangazwa na mazungumzo haya na mnacheka wala hamlii hali ya kuwa ninyi mmeghafilika (mmejisahau)" (Qur'an, 53:61


4

5

6

7

8

9

10

11

12

13

14

15

16