TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE Juzuu 24

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE0%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: Qurani tukufu

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE

Mwandishi: Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya
: HASANI MWALUPA
Kundi:

Matembeleo: 26031
Pakua: 3249


Maelezo zaidi:

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 30 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 26031 / Pakua: 3249
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE Juzuu 24

Mwandishi:
Swahili

11

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE

Sura Ya Sitini Na Tano: Suarat At-Talaq. Imeshuka Madina. Ina Aya 12.

بِسْمِ اللَّهِ الرَّحْمَٰنِ الرَّحِيمِ

Kwa jina la Mwenyezi Mungu Mwingi wa Rehema Mwenye kurehemu.

يَا أَيُّهَا النَّبِيُّ إِذَا طَلَّقْتُمُ النِّسَاءَ فَطَلِّقُوهُنَّ لِعِدَّتِهِنَّ وَأَحْصُوا الْعِدَّةَ وَاتَّقُوا اللَّـهَ رَبَّكُمْ لَا تُخْرِجُوهُنَّ مِن بُيُوتِهِنَّ وَلَا يَخْرُجْنَ إِلَّا أَن يَأْتِينَ بِفَاحِشَةٍ مُّبَيِّنَةٍ وَتِلْكَ حُدُودُ اللَّـهِ وَمَن يَتَعَدَّ حُدُودَ اللَّـهِ فَقَدْ ظَلَمَ نَفْسَهُ لَا تَدْرِي لَعَلَّ اللَّـهَ يُحْدِثُ بَعْدَ ذَٰلِكَ أَمْرًا ﴿١﴾

1. Ewe Nabii! Mtakapowapa talaka wanawake, basi wapeni talaka katika wakati wa eda zao, na fanyeni hisabu ya eda, na mcheni Mwenyezi Mungu, Mola wenu. Msiwatoe katika nyumba zao, wala wasitoke wenyewe, ila wakifanya uchafu ulio wazi. Hiyo ndiyo mipaka ya Mwenyezi Mungu msiikiuke; na mwenye kuikiuka mipaka ya Mwenyezi Mungu, basi amejidhulumu nafsi yake Hujui; pengine Mwenyezi Mungu ataleta jambo jengine baada ya haya.

فَإِذَا بَلَغْنَ أَجَلَهُنَّ فَأَمْسِكُوهُنَّ بِمَعْرُوفٍ أَوْ فَارِقُوهُنَّ بِمَعْرُوفٍ وَأَشْهِدُوا ذَوَيْ عَدْلٍ مِّنكُمْ وَأَقِيمُوا الشَّهَادَةَ لِلَّـهِ ذَٰلِكُمْ يُوعَظُ بِهِ مَن كَانَ يُؤْمِنُ بِاللَّـهِ وَالْيَوْمِ الْآخِرِ وَمَن يَتَّقِ اللَّـهَ يَجْعَل لَّهُ مَخْرَجًا ﴿٢﴾

2. Basi wanapofikia muda wao, muwashike kwa wema, au farakianeni nao kwa wema. Na mshuhudishe mashahidi waw­ili waadilifu miongoni mwenu. Na simamisheni ushahidi kwa ajili ya Mwenyezi Mungu. Hivyo ndivyo anavyoagizwa anayemuamini Mwenyezi Mungu na Siku ya Mwisho. Na anayemcha Mwenyezi Mungu humtengezea njia ya kutokea.

وَيَرْزُقْهُ مِنْ حَيْثُ لَا يَحْتَسِبُ وَمَن يَتَوَكَّلْ عَلَى اللَّـهِ فَهُوَ حَسْبُهُ إِنَّ اللَّـهَ بَالِغُ أَمْرِهِ قَدْ جَعَلَ اللَّـهُ لِكُلِّ شَيْءٍ قَدْرًا ﴿٣﴾

3. Na humruzuku kwa upande asiotazamia. Na anayemtege­mea Mwenyezi Mungu Yeye humtosha. Hakika Mwenyezi Mungu anatimiza amri yake. Mwenyezi Mungu amejaalia kila kitu na kipimo chake.

وَاللَّائِي يَئِسْنَ مِنَ الْمَحِيضِ مِن نِّسَائِكُمْ إِنِ ارْتَبْتُمْ فَعِدَّتُهُنَّ ثَلَاثَةُ أَشْهُرٍ وَاللَّائِي لَمْ يَحِضْنَ وَأُولَاتُ الْأَحْمَالِ أَجَلُهُنَّ أَن يَضَعْنَ حَمْلَهُنَّ وَمَن يَتَّقِ اللَّـهَ يَجْعَل لَّهُ مِنْ أَمْرِهِ يُسْرًا ﴿٤﴾

4. Na wale waliokoma hedhi miongoni mwa wanawake wenu, ikiwa mnayoshaka, basi eda yao ni miezi mitatu, pamo­ja na ambao hawakupata hedhi. Na wenye mimba eda yao ni mpaka watakapozaa. Na anayemcha Mwenyezi Mungu, Mwenyezi Mungu humfanyia mambo yake

kuwa mepesi.

ذَٰلِكَ أَمْرُ اللَّـهِ أَنزَلَهُ إِلَيْكُمْ وَمَن يَتَّقِ اللَّـهَ يُكَفِّرْ عَنْهُ سَيِّئَاتِهِ وَيُعْظِمْ لَهُ أَجْرًا ﴿٥﴾

5. Hiyo ni amri ya Mwenyezi Mungu amewateremshia. Na anayemcha Mwenyezi Mungu atamfutia maovu yake, na atampa ujira mkubwa.

TALAKA KWA WAKATI WA EDA

Aya 1 – 5

MAANA

Hiyo ni amri ya Mwenyezi Mungu amewateremshia. Na anayemcha Mwenyezi Mungu atamfutia maovu yake, na atampa ujira mkubwa.

Katika Aya hizi Mwenyezi Mungu (s.w.t) ametaja hukumu za talaka, kama ifuatavyo:

1.Ewe Nabii! Mtakapowapa talaka wanawake, basi wapeni talaka katika wakati wa eda zao.

Maneno yanaelekezwa kwa Mtume(s.a.w. w ) , lakini wanakusdiwa wenye kukalifiwa na sharia wote. Kwa sababu sharia inawahusu wote.

Maana ni kuwa mwislamu akitaka kumpa talaka mkewe, anatakikana angoje wakati mnasaba wa kuingia kwenye eda; kiasi amabacho wakati wa talaka utakuwa ni sehemu ya eda. Madhehebu yote ya kiislamu yamekongamana kwenye hilo.

Lakini Sunni wanasema uharamu huu hauharibu talaka kwa kukosekana sharti hilo; bali talaka itakuwa sahihi na mtaliki atapata dhambi.

Shia Imamiya wamesema talaka itakuwa ni upuzi tu, kwa sababu lil­iokatazwa ni tendo; sawa na kukatazwa kuuza pombe, lengo lake ni kukataza tendo lenyewe sio kukataza tamko lake.

Miongoni mwa waliyoyatolea dalili Shia ni yaliyoelezwa kwenye Sahih Bukhar na Sahii Muslim kwamba Ibn Umar alimpa talaka mkewe akiwa katika hedhi, basi Umar akamuuliza Mtume(s.a.w. w ) kuhusu hilo, akasema Mtume: Mwamrishe amrejee, kisha amwache mpaka atwaharike kisha aingie hedhini tena atwaharike. Hapo sasa akipenda ataamzuia na akipen­da atampa talaka kabla ya kumgusa. Hiyo ndio eda alioyoiamuru Mwenyezi Mungu Mtukufu apewe talaka kwayo.

Kauli yake Mtume(s.a.w. w ) “Akitaka amzuie na akitaka amwache kabla ya kumgusa,” ni ubainifu na tafsiri ya kauli yake: “Amrejee.” Kwamba yaani bado ni mkewe, kwa hiyo amzuie kwa hali yoyote ile wala hakuna hiyari isipokuwa akimpa talaka kwa masharti yake.

Haya ndio maana ya amrejee. Si sahihi kuwa hiyo ni amri ya kumrejea kitalaka; kama walivyosema wanafiqh wa madhehebu mengine. Kwa sababu kumrejea kwa talaka ni kumzuia mke ambako ni natija ya kauli yake ‘Na amrejee!’ na kimsigi jambo haliwezi kuwa hilo lenyewe ndio natija.

Zaidi ya hayo kurejea kwa talaka hakuondoi dhambi iliyotangulia ili kuam­ruwe na Mtume(s.a.w. w ) . Madhehbu yote yameafikiana kwa kauli moja kuwa mke ambaye hajaingiliwa na mumewe anaweza kuachika hata akiwa kwenye hedhi, kwa sababu Mwenyezi Mungu Mtukufu amesema: Kwa eda yao, na asiyeingili­wa hana eda kutokana na kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: “Enyi ambao mmeamini! Mkiwaoa wanawake waumini kisha mkawaacha kabla ya kuwagusa, basi hamna eda juu yao mtakayoihisabu.” Juz. 22 (33:49).

2.Na fanyeni hisabu ya eda.

Mjue mwanzo wa eda na mwisho wake, kwa sababu ina hukumu zinazo­husiana nayo; kama posho ya aliye kwenye eda, haki ya kurejelewa ikiwa ni talaka rejea, haki yake ya kurudia alichokitoa, ikiwa ni talaka ya kujivua (Khul’u), uharamu wa kuolewa mpaka amalize eda na mengineyo waliyoyataja wana fiqh katika vitabu vyao…

Na mcheni Mwenyezi Mungu, Mola wenu katika yale aliyowawajibishia katika hukumu za eda.

3.Msiwatoe katika nyumba zao, wala wasitoke wenyewe.

Makusudio ya nyumba zao ni nyumba wanazokaa, sio nyumba za kumiliki; sawa na kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: “Na kaeni majumbani mwenu…Na kumbukeni yanayosomwa majumbani mwenu” Juz. 22 (33:33-34).

Wameafikiana mafaqihi kuwa mwenye kuachwa talaka rejea anastahki posho, pamoja na makazi muda ule atakaokaa eda. Wametofautiana katika posho ya aliyeachwa talaka baini.[2]

Hanafi wamesema anastahiki posho, awe ana mimba au la. Malik akasema akiwa hana mimba anastahiki makazi tu na akiwa na mimba basi anastahiki posho kamili. Shafii, Shia Imamiya na Hambali wamesema hana posho akiwa hana mimba, lakini akiwa nayo basi anastahiki posho.

Ikiwa wajibu posho basi ni wajibu kwa mtalikiwa kubakia kwenye nyumba aliyotalikiwa mpaka uishe muda wa eda na ni haramu kutoka au kum­toa; kama alivyosema Mwenyezi Mungu: ‘Wasitoke …. Wala msiwatoe.’Ila wakifanya uchafu ulio wazi ; yaani utakaothibitika kisharia.

Wameafikiana kwamba zina ni uchafu unapelekea kutolewa nyumbani. Lakini wametofautina katika isiyokuwa zina. Tuonavyo sisi ni kuwa makusudio ya uchafu hapa, (Fahisha), ni zina tu, kwa sababu neno hili likinasibishwa kwa wanawake basi fahamu inayokuja haraka akilini ni zina.

Hiyo ndiyo mipaka ya Mwenyezi Mungu msiikiuke.

Yaani masharti ya talaka na hukumu za eda. Nazo ni hukumu za Mwenyezi Mungu na mipaka yake aliyoibainisha katika Kitabu chake na kupitia kwa Mtume wake.

Na mwenye kuikiuka mipaka ya Mwenyezi Mungu, basi amejidhulumu nafsi yake , kwa sababu ameipeleka kwenye ghadhabu ya Mwenyezi Mungu na adhabu yake. Aya nyingine inasema:

وَمَن يَعْصِ اللَّـهَ وَرَسُولَهُ وَيَتَعَدَّ حُدُودَهُ يُدْخِلْهُ نَارًا خَالِدًا فِيهَا وَلَهُ عَذَابٌ مُّهِينٌ ﴿١٤﴾

“Na mwenye kumwasi Mwenyezi Mungu na Mtume wake na akapetuka mipaka yake, atamtia katika moto; ni mwenye kudumu humo, na atapata adhabu idhalilishayo.” Juz. 4 (4:14).

Hujui; pengine Mwenyezi Mungu ataleta jambo jengine baada ya haya.

Hujui wewe mtaliki labda Mwenyezi Mungu anaweza kuunganisha nyoyo mbili zilizotengana na mambo yakarudi kama zamani. Hapa kuna ishara kwamba nyoyo zina wakati, na inatikakana mtu asiseme jambo kuwa nital­ifanya kesho ila kwa kusema inshallah. Ndio maana Imam Ali(a.s ) akasema:“Nimemjua Mwenyezi Mungu kwa kuvurugika maazimio.’ Yaani kuharibika maazimio ni dalili wazi kuwa kwenye mipango ya mtu kuna mipango ya juu na yenye nguvu zaidi.

4.Basi wanapofikia muda wao, muwashike kwa wema, au farakianeni nao kwa wema.

Ikiwa muda wa eda unakurubia kwisha basi, mtaliki ana hiyari, akitaka atabadilisha azma yake na kumrudisha mtalikiwa kwenye hifadhi yake na akipenda atabakia kwenye hukumu ya kufarikiana na kukatika mfunga­mano baina yao. katika hali zote mbili anatakikana asimdhuru mke, bali amtekelezee haki yake kwa ukamilifu. Haya ndio makusudio ya kumweka kwa wema au kufarikiana naye kwa wema. Umetangulia mfano wake katika Juz. 2 (2:231).

Mtalikiwa anaweza kuwa amekoma kutoka hedhi, ana mimba au hana mimba. Kuhusu wawili wa mwanzo maelezo yao yatakuja.

Ama muda wa eda ya asiyekuwa na mimba ni twahara tatu zikiwa ni pamoja na ile aliyepewa talaka. Hii ni kwa Shia Imamiya, Malik na Shafii. Ama kwa Hanafi na Hambali eda yake ni hedhi tatu. Tazama Juz. 2 (2:228).

5.Na mshuhudishe mashahidi wawili waadilifu miongoni mwenu.

Mafaqihi wa madhehebu wameafikana kuweko ushahidi wa waadilifu wawili kwa mujibu wa Aya hii, lakini wakatofautiana ushahidi uwe kwenye nini? Kwenye kurejea au kwenye talaka? Mafakihi wa kisunni wamesema, unazingatiwa kwenye kurejea, lakini wengine wakasema ni wajib; kama Shafii na wengine wakasema ni sunna; kama Hanafi.

Shia imamiya wanasema kuwa si wajibu ushahidi kwenye kurejea, isipokuwa kwenye talaka. Dkt. Muhammad Yusuf Musa, mhadhiri na raisi wa kitengo cha shariya ya Kiislamu, kitivo cha haki katika chuo Kikuu cha Azhar, anasema katika kitabu chake: Al-ahawalu shakhsiyya Uk. 271, chapa ya 1958:

Shia Imammiya wanaona kuwa miongoni mwa masharti muhimu ya talaka ni kuhudhuria mashahidi wawili waadilifu, kutokana na kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: “Na mshuhudishe mashahidi wawili waadilifu miongoni mwenu.”

Na katika hilo anasema mmoja wa ulama wao: Hii ni nyenzo nzuri zaidi ya muungano wa wanandoa, kwa sababu watu wema wana athari katika nafsi kuweza kutuliza mawimbi yawe sawa. Ikiwa nasa­ha zao hazitafaulu, lakini angalau talaka zitapungua kwa kuweko sharti la waadilifu wawili.” Dkt. anaongeza kusema: “Hili halitakikani kufumbiwa macho. Kwa kweli kuichukua rai hii kutaandaa njia ya kutengenea mambo mengi.”

Na simamisheni ushahidi kwa ajili ya Mwenyezi Mungu.

Maneno yanaelekezwa kwa mashahidi. Maana ni kuwa msigeuze kitu kati­ka ushahidi, bali utekelezeni kwa njia yake kwa kukusudia kuithibitisha haki, sio kuwaridhisha au kukomoa wanaoshudiliwa.

Umetangulia mfano wake katika Juz. 3 (2:283).

Hivyo ndivyo anavyoagizwa anayemuamini Mwenyezi Mungu na Siku ya Mwisho.

Ukweli ni kuwa wanaonufaika na ubainifu wa Mwenyezi Mungu na kutumia hukumu zake ni wale wanaomcha Mungu. Lakini wale wasioamini isipokuwa nafsi zao na masilahi yao, hao ni kama wanyama, hamu yao ni matumbo yao na moto ndio makazi yao.

Na anayemcha Mwenyezi Mungu humtengezea njia ya kutokea.

kwenye haramu yake kwenda kwenye halali yake na kwenye maasi yake kwenda kwenye twaa yake na humtoshea na kuhitajia wengine,na hum ruzuku kwa upande asiotazamia.

Tunavyofahamu kutokana na Aya hii ni kuwa riziki haina udhibiti maalumu wala kiasi. Inaweza ikaja bila ya kutazamia na inaweza kuondoka bila ya kutazamia. Kuna matukio mangapi mazuri yanamtokea mtu bila ya kutarajia na kuyapanga na ni matukio mangapi mabaya ya kuumiza, yasiyotazamiwa kutokea, yanatokea? Hakuna shaka kuwa baadhi yanatokea kwa kupuuza na mengine ni kwa mipangilio ya mpangiliaji wa viumbe.

Na anayemtegemea Mwenyezi Mungu Yeye humtosha.

Kumtegemea Mwenyezi Mungu ni kuchukua desturi yake ya kufanyakazi na kuhangaika kwa kufuata nyenzo: “Basi tembeeni katika pande zake na kuleni katika riziki zake.” (67:15).

Na Hadith inasema:“Tia akili na utawakali.”

Hakika Mwenyezi Mungu anatimiza amri yake . Analolitaka linakuwa na asilolitaka haliwi.

Mwenyezi Mungu amejaalia kila kitu na kipimo chake , hakuna mchezo, wala vurugu au sadfa. Katika Aya nyingine anasema: “Na ameum­ba kila kitu na akikadiria kipimo.” Juz. 18 (25:2). Pia amesema: “Na kila kitu kwake ni kwa kipimo.” Juz. 13 (13:8).

6.Na wale waliokoma hedhi miongoni mwa wanawake wenu, ikiwa mnayoshaka, basi eda yao ni miezi mitatu, pamoja na ambao hawakupata hedhi.

Mafaqihi wa kisunni wametofautiana sana kuhusiana na umri wa kukoma hedhi; kiasi cha kufikia mgongano na kutatizika. Kuna aliyesema ni miaka 50, mwingine akasema ni 55, watatu akasema ni 60, wanne akasema ni 62,watano akatofautisha baina ya wanawake waarabu na wasiokuwa waarabu akasema kuwa waarabu wana nguvu kimaumbile na wa sita akasema, kila mwanamke ataangalia desturi ya ukoo wake. Na wengi katika wao wamenyamaza hawakuweka kiwango cha mwaka wa kukoma hedhi.

Vile vile wametofautiana katika neno ‘ikiwa mnayo shaka.’ Mmoja akasema ni kutia shaka katika hukumu ya eda si katika hali ya mwanamke na kufikia kwake mwaka wa kukoma hedhi. Wengine wakaseam makusudio ni kutia shaka katika hali ya mwanamke na kukoma kwake.

Ama Shia wamesema: Mwaka wa kukoma hedhi kwa mkuraishi ni miaka 60 na kwa asiyekuwa mkuraishi ni miaka 50, wakitegemea riwaya za Ahlulbayt.

Vile vile wamesema kiwango cha chini kuweza kutoka hedhi ni miaka 9. Hii inaafikiana na yaliyoelezwa kwenye kitabu Almughni cha Ibn Quddama, katika sunni: “Uchache wa umri wa kupata hedhi ni miaka 9, kwa sababu marejeo katika hilo ni kupatikana, na amepatikana aliyetoka hedhi katika umri wa miaka 9. Na imepokewa kutoka kwa Shafii kwamba yeye alimuona mwanamke mwenye wajukuu akiwa na miaka 21.”

Nimesoma katika gazeti kuwa kuna msichana aliyepata hedhi kabla ya miaka9.

Wametofautiana Sunni na Shia katika kufasiri Aya hii. Mafaqihi wa kisunni wakasema kuwa makusudio ya waliokoma kupata hedhi ni waliokatikiwa na hedhi kwa sababu ya umri wao mkubwa, na ambao hawakupata hedhi ni wale ambao hawajapata hedhi kwa sababu ya umri wao mdogo. Wote hawa eda yao ni miezi mitatu, wakiwa wameingiliwa na waume zao.

Hii inaafikiana na baadhi ya mafaqihi wakubwa katika Shia imamiya; kama vile Sayyid Almurtadha, Ibn Zuhra, Ibn Samaa na Ibn Shahr Shub. Hata hivyo wengi katika Shia imamiya, wamesema kuwa makusudio ya waliokoma kupata hedhi ni wanaotiliwa shaka kuwa hedhi yao imekatika kwa umri au kwa jambo jingine.

Na wakafasiri kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: “Ikiwa mnayo shaka,” kuwa ni kutia shaka katika hali yao. Ama makusudio ya ambao hawakupata hedhi ni wale walio katika umri wa hedhi, lakini hawapati hedhi kwa sababu nyingine isiyokuwa ya umri mdogo au mkubwa. Wote hawa eda yao ni miezi mitatu. Wametegemea riwaya za Ahlu bayt katika hilo. Kwa hiyo basi Aya haikuelezea eda ya aliyekoma kutoka hedhi kwa umri mkubwa; si kwa kichanya wala kihasi

Na wenye mimba eda yao ni mpaka watakapozaa.

Mafaqihi wa kisuni na kishia wameafikiana kuwa eda ya mtalikiwa mwenye mimba ni mpaka azae, wakatofautiana katika eda ya aliyefiwa na mumewe akiwa na mimba. Sunni wamesema ni sawa na eda ya mtalikiwa inamalizika kwa kuzaa.

Shia wanasema ataangalia muda utakaorefuka zaidi baina ya kuzaa na miezi mine na siku kumi (yaani akizaa kabla ya miezi mine na siku kumi basi atangoja hadi muda huo uishe). Kwa kuchukulia Aya hii na ile isemayo: “Na wale wanaokufa miongoni mwenu na kuacha wake (hao wake) wangoje miezi minne na siku kumi.” Juz. 2 (2:234). Huko tumefafanua zaidi.

Na anayemcha Mwenyezi Mungu, Mwenyezi Mungu humfanyia mambo yake kuwa mepesi.

Huu ni mfano wa Aya ya 2 na 3 ya Sura hii tuliyo nayo. Hatujui lengo la kukaririka huku isipokuwa kuzidi kuhimiza takua. Kwamba kule kumeku­ja kuhimiza baada ya amri ya kusimamisha ushahidi kwa njia yake. Hapa kumekuja baada ya kubainisha eda ya aliyekoma na mwenye mimba.

Hiyo ni amri ya Mwenyezi Mungu amewateremshia. Na anayemcha Mwenyezi Mungu atamfutia maovu yake, na atampa ujira mkubwa.

Manufaa ya takua hayana idadi; mingoni mwayo ni aliyoyataja Mwenyezi Mungu (s.w.t) katika Aya hizi; kama ifuatavyo:-kutoka katika dhiki ya dunia na Akhera, riziki bila ya kutazamia, nusra na kinga kutoka kwa Mwenyezi Mungu, kuwa mepesi mambo na kufutiwa maovu. Fauka ya yote ni ziada ya malipo. Lakini

أَفَأَنتَ تُسْمِعُ الصُّمَّ أَوْ تَهْدِي الْعُمْيَ وَمَن كَانَ فِي ضَلَالٍ مُّبِينٍ ﴿٤٠﴾

“Je, unaweza kumsikilizisha kiziwi, au kumwongoza kipofu na aliyemo katika upotofu ulio wazi?” Juz. 25 (43:40).

12

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA ISHIRINI NA NNE

أَسْكِنُوهُنَّ مِنْ حَيْثُ سَكَنتُم مِّن وُجْدِكُمْ وَلَا تُضَارُّوهُنَّ لِتُضَيِّقُوا عَلَيْهِنَّ وَإِن كُنَّ أُولَاتِ حَمْلٍ فَأَنفِقُوا عَلَيْهِنَّ حَتَّىٰ يَضَعْنَ حَمْلَهُنَّ فَإِنْ أَرْضَعْنَ لَكُمْ فَآتُوهُنَّ أُجُورَهُنَّ وَأْتَمِرُوا بَيْنَكُم بِمَعْرُوفٍ وَإِن تَعَاسَرْتُمْ فَسَتُرْضِعُ لَهُ أُخْرَىٰ ﴿٦﴾

6. Wawekeni mnavyokaa nyinyi kwa kadiri ya pato lenu, wala msiwaletee madhara kwa kuwadhiki. Na wakiwa wana mimba, wagharimieni mpaka wajifungue. Na wakiwany­onyeshea, basi wapeni ujira wao, na shaurianeni kwa wema. Na mkihitilafiana, basi amnyonyeshee mwanamke mwengine.

لِيُنفِقْ ذُو سَعَةٍ مِّن سَعَتِهِ وَمَن قُدِرَ عَلَيْهِ رِزْقُهُ فَلْيُنفِقْ مِمَّا آتَاهُ اللَّـهُ لَا يُكَلِّفُ اللَّـهُ نَفْسًا إِلَّا مَا آتَاهَا سَيَجْعَلُ اللَّـهُ بَعْدَ عُسْرٍ يُسْرًا ﴿٧﴾

7. Mwenye wasaa agharimie kwa wasaa wake, na mwenye dhiki agharimie katika alichompa Mwenyezi Mungu; Mwenyezi Mungu haikalifishi nafsi yoyote ila kwa kadiri ya alivyoipa. Mwenyezi Mungu atajaalia baada ya uzito wepesi.

MWENYE WASAA AGHARIMIE

Aya 6 – 7

MAANA

Wawekeni mnavyokaa nyinyi kwa kadiri ya pato lenu.

Mwenyezi Mungu Mtukufu mwanzoni mwa Sura hii alisema: “Msiwatoe majumbani mwao.” Huko tumesema kuwa ni wajibu kwa mtaliki kumpa makazi aliye katika eda. Aya hii tuliyo nayo inaungana na huko. Kwa sababu inaweka kiwango cha nyumba anayopaswa kukaa mtalikiwa akiwa kwenye eda.

Imeweka kiwango cha uweza wa mtaliki; amuweke kama anavyokaa yeye, akiwa ana nafasi basi amuweke kwa nafasi, akiwa na dhiki basi amuweke kidhiki.

Wala msiwaletee madhara kwa kuwadhiki.

Msikusudie kuwadhuru kwa kuwadhiki katika posho na makazi ili waende zao. Kuwadhuru wengine ni katika madhambi makubwa, hasa mke na jirani.

Na wakiwa wana mimba, wagharimieni mpaka wajifungue.

Akimpa talaka na huku ana mimba, itakuwa ni wajibu kumpa posho ikiwa ni pamoja na makazi, mpaka iishe eda kwa kujifungua; ni sawa iwe ni talaka rejea au baini.

Lakini akiwa hana mimba, ikiwa ni talaka rejea itakuwa ni wajibu posho kamili na ikiwa ni talaka baini basi hakuna wajibu wa posho wala makazi.

Kuna kundi la mafiqihi waliosema: Mwenyezi Mungu (s.w.t) aliposema: ‘wawekeni.’ Aliliachia tamko bila ya kulifunga na mimba, lakini aliposema: ‘wagharamieni,’ amelifunga na mimba. Kwa hiyo natija ni kuwa makazi ni wajibu kwa mtalikiwa yoyote, awe na mimba au la, rejea au baini. Lakini posho inakuwa ni wajibu kwa mwenye mimba hata kama itakuwa ni talaka baini.

Nasi tunajibu: Lau tutachukulia natija hii, basi itakuwa wajibu wa posho ya aliye kwenye eda ni kwa mwenye mimba tu, lakini mwingine haitakuwa ni wajibu hata kama ni talaka rejea, na hakuna anayesema hivyo kabisa; bali yamekongamana madhehebu kuwa ni wajibu posho kwa aliye katika eda ya talaka rejea, kwa nukuu ya Hadith za Mtume, ambazo ndizo zina­zobainisha na kufasiri kitabu cha Mwenyezi Mungu; hasa katika mambo yanayohusiana na halali ya Mwenyezi Mungu na haramu yake. Na hakuna katika Hadith za Mtume zinazobainisha kuwa ni wajib kumpa posho mwenye kupewa talaka baini akiwa hana mimba.

Na wakiwanyonyeshea, basi wapeni ujira wao.

Shia Imamiya wanasema kuwa mama halazimishwi kunyonyesha mtoto wake ila ikiwa kuna ulazima wa hilo; na kama atamnyonyesha katika hali hii au nyingine, basi anayo haki ya kudai ujira wa kunyonyesha; awe kwenye ndoa au ameachika. Ikiwa mtoto ana mali basi ujira wake utatokana na mali hiyo; vinginevyo atatoa baba mwenye uwezo. Akiwa hana basi hapo itakuwa ni wajibu kwa mama kumnyonyesha bure.

Haya yako karibu sana na aliyoyanukuu Ibn Quddama katika kitabu Al-Mughni, kutoka madhehebu mane ya sunni; isipokuwa Malik aliyesema kuwa mke atalazimika kunyonyesha ikiwa walio mfano wake wanawany­onyesha watoto wao. Lakini ikiwa hali yake ni juu zaidi yao basi hatalazimika.

Na shaurianeni kwa wema.

Maneno yanaelekezwa kwa wazazi. Maana ni kuwa shaurianeni na muangalie masilahi ya mtoto kwa ikhlasi katika malipo ya kunyonyesha; msameheane na msahau, ikiwa kwenye nafsi ya mmoja wenu kuna kitu, kwa masilahi ya mtoto ambaye ni amana ya Mwenyezi Mungu juu yenu.

Na mkihitilafiana, basi amnyonyeshee mwanamke mwengine.

Ikiwa baba na mama watatofautiana katika ujira wa kunyonyesha na mama akataka zaidi ya mwingine, basi hapo baba ana haki ya kum­nyang’anya mama na kumpa mwingine amnyonyeshe. Vile vile ikiwa ata­patikana atakayemnyonysha bure na mama akataka malipo. Lakini ikiwa malipo ya mama yako sawa na ya mwingine, basi mama ndiye anayestahi­ki kumnyonyesha. Kwani yeye ndiye aliye na huruma naye zaidi ya mwingine.

Mwenye wasaa agharimu kwa wasaa wake, na mwenye dhiki atoe katika alichompa Mwenyezi Mungu.

Aya hii inajulisha wazi kuwa hali ya kiuchumi ya mume ni sharti la msingi katika posho ya mke. Atatoa kwa kiasi cha uwezo wake. Ikiwa ana nafasi atatoa kinafasi na akiwa ana dhiki atatoa kidhiki. Hukumu hii ni ya kimsingi wa akili na maumbile ambayo ni kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu:

Mwenyezi Mungu haikalifishi nafsi yoyote ila kwa kadiri ya alivyoipa.

Hukumu ya sharia ikienda sambamba na maumbile ya kiakili, kunaifanya iwe ni ya mkataa isiyokubali taawili au kuihusisha wala kuifuta hukumu yake. Yametangulia maelezo ya kunyonyeshwa mtoto na mama yake na makadirio ya posho yake katika Juz. 2 (2:133).

Mwenyezi Mungu atajaalia baada ya uzito wepesi.

Hakuna kitu kinachodumu katika hali moja isipokuwa dhati Yake Mtukufu. Mara ngapi dhiki inafuatiwa na faraja! Na shida inapoisha inakuwa ni raha. Amesema kweli Mwenyezi Mungu Mtukufu: “Basi hakika baada ya uzito pana wepesi.” (94:5), hata kama uzito utachukuliwa kwa kukabwa shingo.

وَكَأَيِّن مِّن قَرْيَةٍ عَتَتْ عَنْ أَمْرِ رَبِّهَا وَرُسُلِهِ فَحَاسَبْنَاهَا حِسَابًا شَدِيدًا وَعَذَّبْنَاهَا عَذَابًا نُّكْرًا ﴿٨﴾

8. Na miji mingapi iliyovunja amri ya Mola wake na Mitume wake, basi tuliihisabia hisabu ngumu na tukaiadhibu kwa adhabu kali.

فَذَاقَتْ وَبَالَ أَمْرِهَا وَكَانَ عَاقِبَةُ أَمْرِهَا خُسْرًا ﴿٩﴾

9. Basi ikauonja ubaya wa mambo yake; na mwisho wa mambo yao ulikuwa hasara.

أَعَدَّ اللَّـهُ لَهُمْ عَذَابًا شَدِيدًا فَاتَّقُوا اللَّـهَ يَا أُولِي الْأَلْبَابِ الَّذِينَ آمَنُوا قَدْ أَنزَلَ اللَّـهُ إِلَيْكُمْ ذِكْرًا ﴿١٠﴾

10. Mwenyezi Mungu amewaandalia adhabu kali. Basi mcheni Mwenyezi Mungu, enyi wenye akili, mlioamini! Hakika Mwenyezi Mungu amewateremshia Ukumbusho.

رَّسُولًا يَتْلُو عَلَيْكُمْ آيَاتِ اللَّـهِ مُبَيِّنَاتٍ لِّيُخْرِجَ الَّذِينَ آمَنُوا وَعَمِلُوا الصَّالِحَاتِ مِنَ الظُّلُمَاتِ إِلَى النُّورِ وَمَن يُؤْمِن بِاللَّـهِ وَيَعْمَلْ صَالِحًا يُدْخِلْهُ جَنَّاتٍ تَجْرِي مِن تَحْتِهَا الْأَنْهَارُ خَالِدِينَ فِيهَا أَبَدًا قَدْ أَحْسَنَ اللَّـهُ لَهُ رِزْقًا ﴿١١﴾

11. Mtume anayewasomea Aya za Mwenyezi Mungu zinazo­bainisha, ili kuwatoa walioamini na wakatenda mema kutoka gizani kuwapeleka kwenye nuru. Na mwenye kumwamini Mwenyezi Mungu, na akatenda mema, atamwingiza katika Bustani zipitiwazo na mito chini yake, wadumu humo milele. Mwenyezi Mungu amekwishampa riziki nzuri.

اللَّـهُ الَّذِي خَلَقَ سَبْعَ سَمَاوَاتٍ وَمِنَ الْأَرْضِ مِثْلَهُنَّ يَتَنَزَّلُ الْأَمْرُ بَيْنَهُنَّ لِتَعْلَمُوا أَنَّ اللَّـهَ عَلَىٰ كُلِّ شَيْءٍ قَدِيرٌ وَأَنَّ اللَّـهَ قَدْ أَحَاطَ بِكُلِّ شَيْءٍ عِلْمًا ﴿١٢﴾

12. Mwenyezi Mungu ni yule ambaye ameziumba mbingu saba, na katika ardhi kwa mfano wa hizo. Amri zake zinashuka baina yao, ili mjue kwamba Mwenyezi Mungu ni Mwenye uweza juu ya kila kitu, na kwamba Mwenyezi Mungu amekizunguka kila kitu kukijua.

MIJI MINGAPI

Aya 8 – 12

MAANA

Madhumuni ya Aya hizi yametangulia mara nyingi, kwa hiyo tutazifasiri kwa ufupilizo:

Na miji mingapi iliyovunja amri ya Mola wake na Mitume wake.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) aliwapeleka mitume kwa umma nyingi zilizopita, kuwaamrisha mema na kuwakataza mabaya, lakini wakapinga kwa inadi na kiburi.

Basi tuliihisabia hisabu ngumu na tukaiadhibu kwa adhabu kali.

Mwenyezi Mungu aliwaadhibu kwa adhabu kali baada ya kuwaondolea udhuru kwa hoja na ubainifu ulio wazi.

Basi ikauonja ubaya wa mambo yake; na mwisho wa mambo yao ulikuwa hasara.

Ubaya na mwisho mbaya una maana moja; ndio maana ikafikiriwa kuwa jumla ya pili ina maanaya ya kwanza. Tukichunguza tutaona kuwa ni kama mfano wa kumwambia aliyepata malipo ya uovu: wewe umelipwa malipo ya uovu, kwa sababu mwenye kufanya uovu halipwi ila uovu.

Mwenyezi Mungu amewaandalia adhabu kali.

Adhabu hii inakuwa Akhera, hilo limefahamishwa na neno ‘amewaandalia,’ na hisabu hiyo na adhabu ilikuwa duniani. Hilo limefahamishwa na neno ‘tuliwaadhibu.’ Maana ya Aya mbili hizi yanafupilizwa na kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu:

لَهُمْ فِي الدُّنْيَا خِزْيٌ وَلَهُمْ فِي الْآخِرَةِ عَذَابٌ عَظِيمٌ ﴿١١٤﴾

“Wana fedheha katika dunia na katika akhera wana adhabu kubwa.” Juz. 1 (2:114).

Basi mcheni Mwenyezi Mungu, enyi wenye akili, mlioamini!

Ikiwa mnaamini kweli na kudai kuwa nyinyi ni katika watu wake basi kutanisheni kauli na vitendo na ilimu na kazi; vinginevyo nyinyi mtakuwa si waumini kitu.

Hakika Mwenyezi Mungu amewateremshia Ukumbusho. Mtume anayewasomea Aya za Mwenyezi Mungu zinazobainisha, ili kuwatoa walio amini na wakatenda mema kutoka gizani kuwapeleka kwenye nuru.

Makusudio ya ukumbusho hapa ni Qur’an; na Mtume ni Muhammad(s.a.w.w) . Alimtuma Mtume wake Muhammad kwa Qur’an ili awasomee watu Qur’an na awaongoze kwayo wenye akili awatoe kwenye giza la ukafiri kuwapeleka kwenye mwanga wa haki na imani.

Na mwenye kumwamini Mwenyezi Mungu, na akatenda mema, atamwingiza katika Bustani zipitiwazo na mito chini yake, wadumu humo milele. Mwenyezi Mungu amekwishampa riziki nzuri.

Waumini walio wema wana ujira mkubwa kwa Mola wao na riziki njema. Maana haya yamekaririka kwenye Aya kadhaa, kwa makusudio ya kuhimiza wema na kufanya heri.

MBINGU SABA NA ARDHI

Mwenyezi Mungu ni yule ambaye ameziumba mbingu saba, na katika ardhi kwa mfano wa hizo.

Kauli zimekuwa nyingi kuhusu mbingu saba na ardhi saba. zinazoingilika akilini ni kama ifuatavyo:-

Kauli ya kwanza : Ni wajibu tuamini kiujumla kuwa kuna mbingu saba na ardhi saba tu basi, na ufafanuzi tuuachie ilimu ya Mwenyezi Mungu.

Kauli ya pili : Ulimwengu mkuu unachanganya tabaka saba za ulimengu. Na kila tabaka ina sayari zisizo na idadi; mingoni mwa hizo sayari ni ardhi. Baina ya kila tabaka moja na nyingine kuna umbali wa mamilioni ya miaka kwa kasi ya mwanga. Mwenyezi Mungu (s.w.t) amezielezea hizi tabaka saba kwa kusema : mbingu saba. Ama kauli yake: ‘Na katika ardhi mfano wake,” inaashiria kwamba kila tabaka ina ardhi yake. Hayo tumeyadokeza katika Juz. 17 (23: 17).

Kauli ya tatu: Kutajwa mbingu saba hakumaanishi kuwa kuna mbingu saba; isipokuwa wahyi umehusisha kuzitaja kwa vile walioambiwa na Qur’an, wakati huo, walikuwa wakisikia tu sayari saba na nyota zake.

Wana historia wanasema kuwa wakaledonia (Chaldeans) walikuwa maarufu kwa ilimu ya unajimu, na wakafikia kujua kuwa kuna sayari saba.

Vizazi vilivyokuja baadae vikarithi fikra hiyo hadi zama za waarabu ambao Qur’an iliteremshwa kwa lugha yao. Ndio ikawazungumzia mbingu kutokana na walivyozowea kuambiana.

Kauli hii tumeidokeza katika Juz. 1 (2:29).

Inatudhihirikia kuwa kauli hii ndiyo iliyo na nguvu zaidi. Katika kuchaku­rachakura rejea za kufasiri Aya hii tumegundua Hadith na kauli ya Ibn Abbas, zinazotilia nguvu kwamba kutajwa mbingu saba hakukusudiwi kuwa ni hizo saba tu. Hadith yenyewe ameinukuu Sheikh Al-Maraghi kutoka kwa sahaba Ibn Mas’ud: “Mbingu saba na yaliyomo ndani yake na baina yake, na ardhi saba na yaliyomo ndani yake na baina yake, si chochote ila ni kama pete iliyopotea katika ardhi iliyo tamabarare.”

Na Sayansi imethibitisha hakika hii. Tazama Juz. 27 (51:47). Sasa Muhammad(s.a.w.w) ameichukua wapi ilimu hii naye ameinukia kwenye umma usiojua kusoma wala kuandika au kuhisabu.

Je ameichukua kwa mtawa au kwa kuhani? Au Muhammad(s.a.w.w) anamzulia Mwenyezi Mungu, naye analingania Kitabu kinachosema kwa ufasaha na uwazi: Na ni nani dhalimu mkubwa kuliko yule amzuliaye uwongo Mwenyezi Mungu. Au mwenye kusema: Nimeletewa Wahyi; na hali hakuletewa wahyi wowote.” Juz. 7 (6:93). “Hakika ameshindwa mwenye kuzua.” Juz. 20 (20:61).

Katika Tafsir Attabariy kuna maelezo kwamba Ibn Abbas, mwanafunzi wa Imam Ali(a.s) , alimuuliza kuhusu kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: “Mbingu saba, na katika ardhi kwa mfano wa hizo,” Akasema:Lau mtazungumzia tafsiri yake mtakufuru kwa kuikadhibisha.” Yaani akili zao hazitavumilia, kwa hiyo watatia shaka ukweli wake.

Amri zake zinashuka baina yao.

Yaani baina ya hizo mbingu na ardhi. Amezipangilia mbingu na ardhini na vilivyomo ndani yake kwa hikima yake, akazizuia kwa uweza wake na anazijua vizuri kwa ilimu yake.

Ili mjue kwamba Mwenyezi Mungu ni Mwenye uweza juu ya kila kitu, na kwamba Mwenyezi Mungu amekizunguka kila kitu kukijua.

Miongoni mwa hikima kubwa katika kuumba mbingu na ardhi ni mjue kuwa Mwenyezi Mungu ni muweza wa kila kitu hata ufufuo baada ya mauti, na kwamba yeye ni mjuzi wa kila kitu; mpaka makusudio yenu na vitendo vyenu, basi mtiini na mhofie ghadhabu zake na adhabu yake.

MWISHO WA SURA YA SITINI NA TANO: SUARAT AT-TALAQ