MASIMULIZI (HADITHI) KATIKA QUR'AN

MASIMULIZI (HADITHI) KATIKA QUR'AN0%

MASIMULIZI (HADITHI) KATIKA QUR'AN Mwandishi:
Kundi: Qurani tukufu

MASIMULIZI (HADITHI) KATIKA QUR'AN

Mwandishi: AMIRALY M.H.DATOO
Kundi:

Matembeleo: 5726
Pakua: 1871

Maelezo zaidi:

MASIMULIZI (HADITHI) KATIKA QUR'AN
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 13 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 5726 / Pakua: 1871
Kiwango Kiwango Kiwango
MASIMULIZI (HADITHI) KATIKA QUR'AN

MASIMULIZI (HADITHI) KATIKA QUR'AN

Mwandishi:
Swahili

MASIMULIZI (HADITHI) KATIKA QUR’ANI

MTUNZI: AMIRALY M. DATO0

MALAIKA: HARUT NA MARUT

Imepokelewa riwaya kutoka kwa Imam Muhammad al-Baquir (a.s) kuwa:

Baada ya kifo cha Mtume Sulayman bin Daud (a.s), Ibilisi alitengeneza uchawi na kuuviringa na nyuma yake aliandika kuwa mzigo huu umetengenezwa na Asif bin Barkhiyyah kwa ajili ya ufalme wa Mtume Suleyman, na kwamba imetolewa kutoka hazina ya ilimu. Na kwa nguvu zake kila jambo linawezekana. Na baada ya hapo aliifukia chini ya kiti cha Mtume Sulayman (a.s) Na baadaye aliifukua chini ya kiti hicho na kuidhihirisha mbele ya watu wa zama hizo. Kwa kuyaona hayo, wale waliokuwa Makafiri walianza kusema kuwa Mtume Suleyman (a.s) aliweza kuwatawala kwa uchawi lakini wale waliokuwa Mumin walikuwa wakisema kuwa Mtume Sulayman (a.s) alikuwa ni Mtume wa Allah (s.w.t) na mwenye taqwa. Allah (s.w.t) anatuambia kuwa ni Sheitani ndiye asemaye kuwa Mtume Suleyman (a.s) alikuwa ni mchawi. Na jambo hilo ndilo walilolifuata na kuliamini Mayahudi. Lakini Mtume Suleyman (a.s) kamwe hakufanya tendo lolote la kukufuru au la ushirikina hivyo kamwe hawezi kuwa mchawi. Wale wanaohalalisha uchawi ni makafiri kwa sababu Masheitani walikuwa wakifanya uchawi na kuwafundisha watu uchawi na ushirikina.

Baada ya kupita zama za Mtune Nuh (a.s), kulikuja zama moja ambamo wakazi wake walikuwa wakijishughulisha mno na mambo ya uchawi na ushirikina, kwa sababu ya kufuata imani hizo zilizopotofu, kulikuwa kukitendeka matendo maovu kabisa. Hivyo wakazi walikuwa wameupuuzia Uislamu, na kwa hayo Allah (s.w.t) aliwatuma malaika wawili waliokuwa wakiitwa Harut na Marut, ambao walitumwa katika mji uitwao Babul, katika maumbile ya mwanadamu ili waweze kuwazuia wanadamu wasiendelee na uchawi na ushirikina uliokuwa umepindukia kiasi.

Malaika hao walitii amri ya Allah (s.w.t) na walimwelezea Mtume wa zama hizo kuwa uwafundishe mambo fulani fulani wakazi wako ili waweze kujiepusha na uchawi na ushirikina huo uliokuwa umewapotosha kabisa. Basi Mtume huyo aliwaambia watu wake kuwa wajifunze mafunzo hayo makhsusi ili waweze kujiepushe na uchawi na kamwe wasiwatendee chochote wenzao. Allah (s.w.t) anatuambia kuwa katika mji huo wa Babul kulikuwapo na Mayahudi ambao wao kwa hakika walikuwa wakitenda kinyume na kile walichokuwa wakiambiwa na Mtume huyo, yaani wao badala ya kuutokomeza uchawi, wao ndio wakawa waabudu wa uchawi na wakawa wakifanya uchawi. Malaika wakawaambia sisi tunawafundisheni haya kwa ajili ya kutaka kuwajaribu na kuwajua wale waliona imani ya kurudi kwa Allah (s.w.t) na hivyo kujiepusha na uchawi. Na kutaka kuwatambua wale walioasi na kutumia ilimu hii kwa ajili ya kuwadhuru wengine.

Hapo ndipo watu walikuwa wakijifunza uchawi za aina zote mbili yaani watu hao walikuwa wakijifunza uchawi uliokuwa umezuliwa na Shaytani kwa jina la Asif bin Barkhiyyah na ilimu waliofundishwa na Mtume Suleyman (a.s) kwa ajili ya kujikinga na uchawi wa aina yoyote. Wao walikuwa wakijifunza uchawi hata wa kuwatenganisha mume na mke wake na walikuwa wakiwapatia hasara kubwa sana watu. Kwa hakika sote tunaelewa kuwa Allah (s.w.t) kamwe hapendezewi na matendo kama haya na hivyo huwaadhibu wale wote wanaojishughulisha na matendo maovu kama haya ya Sihri. Katika Ayah hapa panazungumziwa neno idhn ingawaje kunamaanisha bila ya ruhusa ya Allah (s.w.t), lakini wanazuoni wanasema kuwa kuna maana nyingi na kwa neno idhn hapa kunamaanishwa ilimu yaani kujua, hivyo Allah (s.w.t) anayajua yote yanayotendeka. Iwapo sisi tutachukulia maana ya idhn kuwa ni idhini basi kumwua Mtume na kumdhulumu haki zake ni kwa idhini yake Allah (s.w.t). Na kwa hakika Allah (s.w.t) si dhalimu na hivyo hawezi kamwe kuwafanyisha watu mambo yoyote yaliyo batili.

Na hapo anasema kuwa wao wanajifunza mambo ambayo yatawaletea hasara siku ya Qiyama na wala hawapati faida ndani mwake katika Dini na duniya. Kwa uhakika hao Mayahudi wana fahamu kuwa mtu yeyote aiachayo Dini ya Allah (s.w.t) kwa badili ya kuchukulia uchawi, kwake hana faida ya aina yoyote huko Akhera na kamwe hawatapata uokovu kutokea adhabu za Jahannamu. Hivyo wao kwa makusudi wamejichukulia adhabu za Jahannam na kwa hayo wao kwa hakika wameziuza nafsi zao. Ni mambo maovu kabisa. Iwapo wao walitambua ubaya wa mambo hayo basi wao kamwe hawakufuata kiasi chochote walichokuwa wameelewa na hivyo watambue kuwa ni sawa na kutojua chochote.

Habari nyingine isemayo…

Wengi wanasema kuwa Harut na Marut ni Malaika waliokuwa wametumwa na Allah (s.w.t). Wao walikusanyika katika nyumba ya mwanamke mmoja na humo walikunywa pombe, wakaua na kuabudu miungu na kwa hayo wameadhibiwa adhabu ya kuning’inizwa katika kisima kimoja kilichokuwa kikijulikana kwa jina la Babul.

Kwa hakika masimulizi kama haya hayana uhakika wowote kwa masimulizi kama haya yanapotosha na ni yenye kuzuliwa kwani ni kinyume na akili zetu. Kwa sababu Malaika ni viumbe wasio na wala hawatendi madhambi ya aina yoyote ile.

Katika ‘Uyunul Akhbar al-Ridha ni mashuhuri kuwa mtu mmoja alimwuliza Imam al-Ridha (a.s) kuwa nimesikia kwamba dunia ilipojaa madhambi na maovu, basi Allah (s.w.t) aliwatuma Malaika Harut na Marut kama makhalifa na kuwatuma duniani. Vile vile inasemekana kuwa wao walifanya mapenzi pamoja na mwanamke mmoja aliyejulikana kwa jina la Zehra, na pia walikunywa pombe, wakaabudu miungu, wakaua na kuzini, walizini. Ewe Mjukuu wa Mtume (s.a.w.w), unasemaje kuhusu habari hizi?

Malaika hawakufuru…

Kwa kuyasikia hayo, Imam (a.s) alijibu Madhallah! Si hivyo kwani Malaika ni viumbe visivyo na makosa na wapo mbali na kufuru na maovu. Imam (a.s) aliwathibitishia hao kuwa Malaika ni viumbe visivyo na kasoro zozote kwa Ayah za Qur’an na kuwaambia kuwa nyinyi ni lazima muamini kuwa Allah (s.w.t) aliwatuma hao Malaika katika maumbile ya mwanadamu ili waweze kuwaonya na kuwaonyesha wanaadamu kuhusu uchawi uliokuwa ukiendelea katika zama zao. Kwa kifupi Malaika hawatendi makosa ya aina yoyote.

Kwa hayo watu waliuliza:

“Ewe Imam wetu ! Iwapo Malaika hawatendi makosa, sasa je Ibilisi Sheitani hakuwa Malaika?”

Basi Imam (a.s) aliwajibu kuwa:

Yeye alikuwa ni Jinn na hayo yamesemwa katika Qur’an Tukufu ”.

Nasiha

Inatubidi sisi tuisome Qur’an tukufu na kuielewa maana ya Ayah zilizomo na kujaribu kujifunza kutokana na kusoma kwetu ili tuweze kuishi vile Allah (s.w.t) atutakavyo na tujiepushe pamoja na maovu ambayo ndiyo sababu kuu za maangamizo na mateketezo yetu. Vile vile tuwe na tahadhari ya masimulizi na maelezo ya mufassirina wengine ambao wanaweza kutupotosha kwani maelezo yao yanapingana pamoja na Ayah za Qur’an Tukufu pamoja na masimulizi tuliyoyapata kutoka kwa Mtume (s.a.w.w) pamoja na Aimma Toharifu (a.s).

MASIMULIZI (HADITHI) KATIKA QUR’ANI

MTUNZI: AMIRALY M. DATO0

YAJUJ NA MAJUJ

Allah (s.w.t) anasema katika Quran, Sura Al-Kahf, 18, Ayah 92 - 99.

“Kisha akaifuata njia.

Hata alipofika katikati ya milima miwili,alikuta nyuma yake watu ambao waliweza kwa shida kufahamu neno (wanaloambiwa).

Wakasema:“Ewe Dhulqarnain! Hakika Yajuj na Majuj wanafanya uharibifu katika ardhi.Basi je,tukupe ujira ili utie baina yetu na baina yao kizuizi?”

Akasema:“Yale ambayo Allah (s.w.t) wangu amenimakinishia ni bora (kuliko ujira wenu.Nitakufanyieni bure);Lakini nisaidieni kwa nguvu zenu. Nitaweka baina yenu na baina yao kizuizi chenye imara.”

Nileteeni vipande vya chuma.” Hata alipoijaza nafasi iliyo katikati ya milima miwili,alisema:“Pulizeni”mpaka alipokifanya (kile chuma) kuwa moto,alisema “Nileteeni shaba iliyoyayuka niimwage juu yake.”

Hivyo (Yajuj na Majuj) hawakuweza kuukwea wala hawakuweza kuutoboa.

Akasema:“Hili ni rehema itokayo kwa Allah (s.w.t) wangu.Na itakapofika ahadi ya Allah (s.w.t) wangu ya kufika Qayama), atauvunjavunja. Na ahadi ya Allah (s.w.t) wangu ni kweli tu.”

Yajuj na Majuj walikuwa ni viumbe vyenye miguu minne na wakifanana na wanaadamu kisura na wao walikuwa ni wafupi mno mbele ya watu wa zama hizo. Na watoto wao walikuwa wakizaliwa kama watoto wa wanaadamu na walikuwa hawakui zaidi ya shubiri tano na sura zao zilikuwa aina moja na walikuwa wazururaji.Kwa kuwa ngozi zao zilikuwa ngumu kama zile za ngamia, hivyo hawakuathirika kwa baridi wala joto. Walikuwa na makucha makubwa na meno makali na masikio yao yalikuwa marefu kiasi kwamba walikuwa wakitandika moja na kujifunika kwa la pili. Walikuwa wakiingiliana kama wanyama na chakula chao kikubwa kilikuwa ni samaki kwa sababu kulikuwa kukinyesha mvua za samaki, na kama kulikuwa na kasoro ya samaki basi walikuwa wakishambulia miji na kuchafua na kuvuruga kila kitu kiasi kwamba watu walipokuwa wakizisikia sauti zao,walikuwa wakikimbia na kuacha makazi yao kwa sababu ilikuwa ni vigumu mno kuwakabili kwani walipokuwa wakiingia mijini basi miji yote ilikuwa ikijaa wao tu. Idadi yao ilikuwa kubwa mno kiasi kwamba hakuna mtu mwingine ajuaye isipokuwa Allah (s.w.t) Wao walikuwa hawafi hadi wamezaa watoto zaidi ya elfu moja.

Katika vitabu tunapata habari zaidi kuwa Yajuj na Majuj ni makabila mawili yaliyokuwa makubwa kutokana na kizazi cha Yafus, mwana wa Mtume Nuh (a.s). Na katika Agano la Kale, Majuj anaelezwa kuwa ni Chifu wa Mashech na Tunal. Kwa sasa Moscow ndio mto unaosimama mji huo,uitwao Moscow, mji mkuu wa Urusi; Tabul ni mto huko Urusi ambapo kuna mji Tobolsk.

Katika eneo la Ulaya ya Kusini na Urusi ya Kiasia,baina ya Wacarpathiani na Don, kulikaliwa katika enzi za zamani na kabila katili kabisa ambao waliiteka Asia ya Magharibi kuanzia karne ya 7 Kabla ya Kristo hadi mwanzoni mwa kipindi cha Kikristo, wakati mashambulizi yao yalipokwisha kwa sababu ya Bwana Dhulqarnain alipoujenga huo ukuta.

Vile vile inasemekana kuwa neno Mongol ni mvurugano wa neno la Kichina Mongog au Manchog Iwapo utafiti huu utakuwa wa kweli,hivyo. Hivyo itamaanisha kuwa eneo la Yajuj na Majuj inaanzia Mto wa Moscow hadi Turkistan ya Kichina na Mangolia.

Maelezo ya ‘kuta’ katika Quran Tukufu yanaonyesha kuwa lazima iwe imejengwa pale penye njia ili kuzuia makabila hayo ya wachochezi na wakatili kuwashambulia majirani wao waliokuwa mafundi stadi katika kazi za kufua vyuma na walikuwa matajiri.

Sheikh Abul-Kalam Azad,katika moja ya makala yake (katika Jannatul-Ma’arif) anaelezea kuwa kuta hizo zimeendelea hadi Uturuki.

Ayatullah Agha Haji Mirza Mahdi Puya Yazdi (katika hashia ya Tafsiri ya Quran iliyofanywa na S.V. Mir Ahmad Ali) anawanakili wengine wakisema kuwa kuta hizo zipo baina ya milima ya Armenia na Azerbaijan.

Hata hivyo kuna tofauti ya maoni kuhusu utambulisho wa Dhulqarnain. Bwana ‘Abdullah Yusuf Ali anadhani kuwa jina hilo linaelezea kuwa ni Alexandar Mkuu wa Misri.

Wengineo,kama Agha Puya, wanafikiri kuwa huyo anatambulishwa kama ni Mfalme wa Kiajemi aliyekuwa akiitwa Darius.

Kwetu sisi hatumaanishi kuingia katika mazungumzo mengi kuhusu mjadala huu lakini inatubidi liwe jambo lililowazi mbele yetu kuwa kwa mujibu wa Quran Tukufu, Dhulqarnain alikuwa ni mcha Mungu hivyo kamwe haiwezekani kumtambulisha Dhulqarnain kama kafiri au mpagani.

Kwa mujibu wa Quran Tukufu,Itakapokaribia Siku ya Qayama, kabila hizi zitafanikiwa kuvunja kuta, yaani zitaenea zaidi kuliko mipaka yao ya awali.Upanuzi huo unaweza kuwa kimantiki;ambapo inaweza kumaanisha kuwa itikadi zao (ukomunisti na ukafiri) zinaweza kuenezwa nje ya mipaka ya nchi zao. Au itakuwa aina ya kikoloni yaani kukalia maeneo ya mashariki ya Ulaya,Asia ya Kusini na maeneo mengineyo. Au inaweza kumaanisha yote.

Imeandikwa katika Tafsir Majma’-ul-Bayan kuwa baada ya kuteka maeneo ya ardhi watajararibu kuiteka mbingu.“Hivyo watatupa mishale yao kuelekea angani,na itawarejea zikiwa na alama kama za damu. Hivyo watasema:‘Sisi tumekwishawateka wakazi wa dunia na tumewateka wakazi wa angani.”

Ni dhahiri kuwa mishale inamaanisha maroketi na vyombo vya angani. Maneno itawarejea zikiwa na alama kama za damu inamaanisha kuwa vyombo vya angani vitafikia malengo yao na kurejea duniani.

Kwa mujibu wa Tafsiri hiyo,“wakati watakapokuwa na takabari kubwa kwa sababu ya kushinda anga za juu, Allah (s.w.t) atawaumba funza au minyoo ambayo itawaingia masikio yao, na kuwaua wote.Inamaanisha kuwa hatima yao itakuwa kwa kuangamizwa kwa maafa makhsusi, au kwa magonjwa ya kuambukizwa yatakayotokana na vijidudu.

MASIMULIZI (HADITHI) KATIKA QUR’ANI

MTUNZI: AMIRALY M. DATO0

PEPO ( JANNAT ) YA SHADDAD

Je Shaddad ni nani …

Mtume Muhammad Mustafa (s.a.w.w) alipokwenda katika Mi’raj alikutana na Malakul Mauti. Mtume Muhammad Mustafa (s.a.w.w) alimwuliza :

“Je ni wakatigani ambapo wewe kwa hakika ulisikitika katika kutoa roho ya wanaadamu ?”

Kwa hayo Malakul Maut akajibu :

“Ewe Mtume wa Allah (s.w.t) !

Zipo nyakati mbili tu ambapo mimi kwa hakika nilisikitika mno wakati wa kutoa Roho nazo ni, kwanza kulikuwa na jahazi moja iliyokuwa baharini ikiwa na wasafiri walikuwamo humo, na Allah (s.w.t) aliniamrisha kuipindua jahazi hiyo na kuzitoa roho zote za wasafiri waliokuwamo isipokuwa mwanamke mmoja aliyekuwa ana mimba. Nami nikafanya hivyo hivyo nilivyoamrishwa.

Mwanamke huyo aliweza kuelea kwa msaada wa ubao alioupata wakati wa kuzama. Wakati mwanamke huyo anaelea, alimzaa mtoto, ndiye aliyeitwa Shaddad. Alipomzaa mtoto huyo, mama huyo akafa( hapa niliposikitika wakati wa kuitoa roho ya mama huyu) na mtoto akabakia peke yake majini juu ya ubao, ambapo kwa amri za Allah (s.w.t) aliweza kufika salama u salimini hadi nchi kavu (kisiwa kilichokuwapo karibu).Hapo Allah (s.w.t) alimwamrisha Swala mmoja kumnyonyehsa maziwa mtoto huyo kwa muda usipungua miaka miwili.

Ulifika wakati ambapo kulitokezea wasafiri kisiwani hapo na walipomwona mtoto huyo na alivyokuwa mzuri, walishauriana kumpelekea mfalme kwani alikuwa hana mtoto. Na walifanya hivyo, na Mfalme alimpenda mtoto huyo na kumchukua kama mtoto wake …..

Mtume Adam (a.s) tangu aje duniani humu ilipofika miaka 2647 ndipo Mtume Hud (a.s) alipozaliwa na kulipofika miaka 2700 ndipo Shaddad bin ‘Aad alipokuwa Mfalme na ni Mfalme huyu ambaye ametengeneza mfano wa Jannat (Peponi) yenye bustani za kupendeza humu duniani. Humu yeye alijenga majumba ya kuvutia na kupendeza, na aliweka wajakazi warembo:wasichana kwa wavulana kutoka sehemu mbalimbali humu duniani ambao kwa hakika waliifanya pepo yake ipendeze na kuvutia.

Je kuna mtu aliyebahatika kuiona Pepo hiyo?

Katika zama za Mtume Muhammad Mustafa (s.a.w.w) kuna mtu mmoja aitwaye ‘Bwana ‘Abdullah bin Kalaba ndiye aliyebahatika kuiona. Na hapa tunaelezea vile inavyopatikana katika vitabu vya historia.

Wasemavyo wanahistoria

“Katika Bara la Uarabuni kulikuwa na Shakhsiyyah moja aliyekuwa akiitwa ‘Bwana ‘Abdullah bin Kalaba ambaye alikuwa na Ngamia wake aliyekuwa ametoroka na kupotelea katika majangwa ya ‘Aden na katika kumtafuta huyo ngamia wake alifika katika majangwa ambapo aliuona mji mmoja ukivutia. Mji huo ulikuwa umezungukwa na ngome. Ndani ya mji huo kulikuwa na majumba ya kupendeza na yenye kuvutia sana. Na juu ya kila jengo kulikuwa na bendera zilizokuwa zikipepea. Yeye anasema kuwa alifanikiwa kuingia ndani ya mji huo.

‘Bwana ‘Abdullah anaelezea alivyiona pepo ya Sahaddad

“Mimi niliteremka chini kutokea ngamia wangu na nikamfunga katika nguzo mojawapo. Nikauchukua upanga wangu nikawa ndani ya ngome hiyo. Milango yake ilikuwa ni madhubuti na ya kupendeza sana kiasi kwamba kamwe nilikuwa sijawahi kuona kabla ya hapo. Milango ilikuwa imetengenezwa kwa ubao mzuri sana na manukato mazuri sana na ufundi uliotumika ulikuwa ni wa utalaamu wa hali ya juu sana na juu ya mbao zake kulikuwa kumepachikwa Yaqut za rangi mbalimbali. Ukiangalia chumba kimoja utakisahau chumba cha pili katika ngome hiyo. Madirisha yake yalikuwa yametengenezwa kwa dhahabu na shaba, ukiona milango , kuta na sakafu yake ilivyokuwa iking’ara na kwa hakika kila kitu humo utakachokiona utastaajabika mno.”

‘Bwana ‘Abdullah alipoyaangalia majengo hayo yaliyokuwa mazuri na yenye kuvutia alishangazwa kuona kuwa hapakuwapo na mtu yeyote, na alijaribu kusonga mbele akaona miti ambayo imejaa maua ikiwa inapeperushwa na upepo mzuri sana. Na chini mwake kulikuwa na mito iliyokuwa ikitiririsha maji.

Kwa hakika hii ndiyo ile Jannat ambayo Allah (s.w.t) ametupa habari zake. Basi mimi kwa hayo nilimshukuru Allah (s.w.t) kwa kunijaalia bahati hiyo. Mimi niliokota vipande vidogo vidogo vyenye harufu nzuri mno ya Mishk na Ambar. Na hapo nikawaza kuwa sasa itabidi nitoke zangu nje kwa haraka. Nilipofika katika mji wa Yemen huko niliwasimulia watu kuhusu Jannat hii. Kwa hakika nilishangazwa kuona kuwa habari zangu hizi zilienea kila mahali kama upepo.

Mu’awiya alimtuma mjumbe kwenda kwa Hakim San’aan ili kumwita ‘Bwana ‘Abdullah na kutaka kujua kwa undani zaidi kuhusu swala hili. Huyo ‘Bwana ‘Abdullah alielezea yote yale kwa uhakika vile alivyokua ameyaona. Na hapo Mu’awiya alimwita Ka’bul Ahbar na kumuuliza

“Je yanayozungumzwa na ‘Bwana ‘Abdullah yanapatikana katika vitabu vya historia vyovyote vile unavyovijua wewe ? Je kuna mji wowote humu duniani ambao umetengenezwa na kurembeshwa kwa fedha Ambamo kuna aina mbalimbali za miti na mimea zinazoota ? Na ardhi ambayo inanukia kwa manukato mazuri sana, na badala ya mchanga kumetandazwa vito mbalimbali vya thamani ?”

Ka’bul akamjibu kuwa mji huu kama ulivyo wa Jannat umetengenezwa na mtoto wa ‘Aad aliyekuwa akiitwa Shaddad kama vile ambavyo Allah (s.w.t) anaizungumzia ka tika Qur'an Tukufu.: Sura Al-Fajr, 89, ayah 6-8.

Kwani hakuona jinsi Allah (s.w.t) Mlezi alivyo wafanya kina A’adi ?

Wa Iram, wenye majumba marefu ?

Kwa kuyasikia hayo yote Mu’awiya alimwambia Ka’bul kuwa

“Mimi ninataka habari kamili za kihistoria kuhusu watu wa Makabila hayo ya ‘Aad.

Ka’bul alimwambia

“Kabla ya ‘Aad kulikuwapo na ‘Aad mmoja katika Kabila la Mtume Hud (a.s) Naye alikuwa ana watoto wawili. Mmoja alikuwa akiitwa Shadiid na mwingine akiitwa Shaddad na baada ya ‘Aad kufa basi watoto wote wawili wakawa Wafalme ambao walikuwa wanatawala dunia nzima na hivyo watu wa mashariki hadi magharibi kwa kila upande walikuwa wakiwafuata kama ndio watawala wao. Na Shadiid pia baada ya muda si mwingi alikufa, na hivyo akabakia Shaddad ambaye akawa ndiye mfalme pekee wa dunia nzima.

Shaddad alikuwa na tabia ya kusoma sana na alikuwa amesoma mambo mengi sana na katika kusoma kwake huku mara nyingi alikuwa akisoma kuhusu habari na sifa na mandhari za Jannat ambayo Allah (s.w.t) ameitengeneza kwa ajili ya muumin na waja wake wema.

Shaddad naye pia akasema kuwa yeye angeweza kutengeneza Jannat kama vile alivyoitengeneza Allah (s.w.t) Na azma yake hiyo alitaka kuitekeleza haraka iwezekanavyo.

Mtume aliyekuwapo wakati wa zama zake alipokuwa akifanya kazi ya Tabligh, Shaddad alikuwa akimwuliza ‘je kwa kuwa mja mwema Allah (s.w.t) atakulipa nini ?’ Basi Mtume wa zama zake hizo alimjibu kuwa, ‘Allah (s.w.t) atakulipa Jannat.’

Na kwa hayo Shaddad aliuliza ‘Je Jannat ni nini na humo kuna nini.’ Huyo Mtume aliyekuwepo katika zama za Shaddad alimjibu na kumwelezea ‘mazuri yote yalivyokuwa katika Jannat ya Allah (s.w.t) .’

Shaddad kwa kuyasikia hayo alimwambia Mtume huyo kuwa yeye pia alikuwa na uwezo kamili wa kuweza kutengeneza Jannat kama hiyo na hapo ndipo alipojitangaza kuwa yeye ni mungu. Hivyo watu wote wamwabudu yeye. Ili kutaka kutimiza azma yake hiyo yeye aliwakusanya wataalamu mia moja wa fani mbalimbali na kila mmoja wao aliwapa watu elfu moja wafanye kazi nao haraka iwezekanavyo kwa kutafuta kwanza kabisa mahali yeye anapotaka kujenga mji mmoja wa kiajabu kabisa ambao haujawahi kutokea. Mji ambao utakuwa na majumba ya kushangaza na kuvutia mno ambayo yatakuwa yamejengwa kwa dhahabu na fedha na watandaze Yaqut na lulu na almasi chini na kuwe na manukato ya kila aina yaliyo bora kabisa kiasi kwamba hata hewa inapovuma inavuma iwe ya manukato. Mtengeneze mito inayotiririka maji humo vizuri.

Kwa kuyasikia hayo hao walistushwa kwa maagizo hayo na wakamwuliza Shaddad : ‘Ewe Mfalme wetu! Je kiasi chote hiki cha dhahabu, fedha, almasi na lulu tutatoa wapi ?’

Kwa kuyasikia hayo Mfalme mwenye kiburi alianza kupiga makelele kama inavyo unguruma radi na akasema:

‘Je dunia nzima haipo mikononi mwangu ? Machimbo yote ya ulimwenguni ya fedha na dhahabu na vito vingine vya thamani vyote vichukuliwe mikononi mwetu na si hayo tu bali raia wote wanyang’anywe fedha na dhahabu na vito vya thamani walivyonavyo na ujenzi wa mji huu wa ajabu kabisa uanze mara moja bila ya uchelewesho wa aina yoyote ile. Muwaandikieni barua magavana mia nne kuwa wao nao washiriki nami katika kutekeleza swala hili.”

Kwa kutokana na amri hii au mwito huu uliotolewa na Shaddad Magavana wote walimwitikia na kushirikiana naye katika kulitimiza azma aliyokuwa anayo yeye.

Kwa hivyo wafanya kazi wote walikuwa wakifanya kazi ngumu sana kwa usiku na mchana na hatimaye baada ya miaka mia tatu kupita (wengine wanasema miaka mia moja) mji huu wa ajabu na wa aina yake ulikuwa tayari. Shaddad aliwatafuta wasichana na wavulana warembo kabisa kutoka sehemu mbalimbali za duniani kuja kubakia katika Jannat hiyo ambayo yeye aliipa jina la babu yake Iram na humo aliwaleta matajiri kabisa waje kuishi humo.

Shaddad alitoa amri kuwa raia wote wajiandae kwa ajili ya sherehe kubwa ambayo ataitangaza kuhusiana na kuwa tayari kwa Jannat yake hiyo. Inasemekana kuwa kulichukua muda wa miaka kumi kufanya matayarisho ya kwenda katika Jannat yake hiyo. Shaddad pamoja na jeshi lake na watu wengi mno kupita kiasi waliandamana kwenda katika Jannat hiyo.

Wakati anaendelea na safari yake ya kwenda katika Jannat yake hiyo, kulipobakia safari ya kama masaa ishirini na manne alisikia sauti moja ambayo ilimtia hofu mno na alipoinua macho yake akaona uso wenye kuchukiza na kutisha mno. Na hakusita kuuliza,

“Je ni nani wewe ?”

Akajibiwa kuwa

“Mimi ni Malakul Mauti yaani mimi ni yule malaika ambaye natoa roho za watu humu duniani. Na mimi nimetumwa na Allah (s.w.t) kuja kuitoa roho yako.”

Shaddad alimwambia :

“Ninaomba unipe muhula kiasi cha kwamba mimi niweze kwenda kuangalia Jannat na mabustani niliyoyatengeneza !!!”

Malaika huyo mtoa roho akamwambia kuwa

“Wewe hauna ruhusa hiyo.”

Na imepatikana katika riwaya kwamba mguu wake mmoja ulikuwa ndani ya Jannat na mguu wa pili ulikuwa nje ndipo hapo roho yake ilipotolewa na pepo hiyo na mabustani yake ikapotea katika macho ya watu. Na watu waliokuwamo humo wote wakateketea kwa pamoja.

Kwa kusema hayo Ka’bul Ahbar akasema kuwa katika zama hizi kutatokezea mtu mmoja ambaye atakuwa ametoka kwenda kumtafuta ngamia wake huko porini na atabahatika kuangalia mabustani haya. Mtu huyo uso wake na nywele zake zitakuwa za rangi nyekundu, atakuwa ni mtu mfupi, na upande wa shingo utakuwa na madoa mawili meusi.

Wakati mazungumzo haya yalipokuwa yakifanyika

Bwana ‘Abdullah Kalaba alikuwa ameketi hapo. Na wakati Ka’bul anazungumza alimwona huyo mtu na mara kwa ghafla akasema kwa sauti ya juu:

“Bwana ‘Abdullah mwenyewe aliyeiona Jannat ya Shaddad ndiye huyo aliyeketi hapo.”

MASIMULIZI (HADITHI) KATIKA QUR’ANI

MTUNZI: AMIRALY M. DATO0

WATU WA TEMBO ( AS-HAB-I-FIIL )

Allah (s.w.t) anatuambia katika Qur'an Tukufu, Sura Al Fiil, 105, Ayah ya 1-5:

Kwani hukuona jinsi Allah (s.w.t), Mlezi wako alivyo watendEa wale wenye tembo ?

Kwani hakujaalia vitimbi vyao kuharibika ?

Na akawapelekea ndege makundi kwa makundi,Wakiwatupia mawe ya udongo wa Motoni,Akawafanya kama majani yaliyoliwa!

Najjashi (Negus), alikuwa ni Mfalme wa Abisynnia ambaye alijichukulia jukumu la kueneza Ukristo na alifanya kila jitihada alizoziweza ili aweze kuirudisha vile ilivyo kuwa miongoni mwa watu wake na ikafuatwa na wingi wa raia zake.

Alipopata habari kuwa watu kutoka sehemu mbalimbali za Ulimwenguni walikuwa wakienda Makka kuhiji huko Al Ka’abah Tukufu, basi naye aliamua kuvumbua jambo ambalo litawavutia watu kutokwenda Makkah kuizuru Al Ka’abah Tukufu na badala yake waende nchini mwake.

Hivyo, basi yeye alijenga Kanisa moja kubwa katika Sana’, mji uliopo Yemen na kuipamba vizuri kwa kila kitu cha kuvutia zikiwemo mazulia, mapazia n.k. Kwa hakika lilikuwa ni jambo la kuvutia sana kwa mtu yeyote aliye angalia kwa kuona ufundi wa kistadi uliotumika katika ujenzi wake. Najjashi alifikiria kuwa baada ya kuona maajabu ya ujenzi huo wa Kanisa watu hawatakwenda tena Makkah kuzuru Al-Ka’abah Tukufu na badala yake watakwenda Sana’ kuzuru hilo Kanisa, na vile vile watu wa Makkah pia watakuja kuhiji hapo Sana’, Yemen. Pamoja na hayo yote watu wa Makkah hawakujali chochote. Vile vile sio kwamba ni watu wa Yemen na Abisynnia tu walioisahau Makkah, laa, wao kama kawaida yao waliendelea na safari zao za kwenda mji mtukufu wa Makkah na kuzuru Al Ka’abah Tukufu.

Kwa kuona haya kulimwia jambo la kusikitisha na likawa ndilo tatizo kubwa kwake. Na kwa hakika likawa ni jambo gumu kabisa kuwalazimsha watu wenye imani zao kwenda kinyume na imani na itikadi zao.

Ikatokezea kwamba kukawa na msafara wa wafanya biashara kutoka Makkah waliofika Sana’. Wao wote wakawa ni Waarabu na wakawa wamekuja huko katika safari ya kibiashara. Baadhi yao walipumzika hapo Kanisani usiku katika safari yao na usiku huo ulikuwa ni wa baridi na ili kutaka kupata ujoto kidogo wao walikoka moto ili kupunguza ubaridi uliokuwa humo chumbani na kwa bahati mbaya wakati wa kuondoka wao walisahau kuuzima huo moto, na ikatokezea kwamba Kanisa hilo likashika moto na likachomwa na kuwaka moto. Najjashi alipopata habari kuwa Kanisa hilo limechomwa moto, hakusita kufikiria kuwa Waarabu wale waliokuwapo usiku huo ndio walioichoma moto kwa makusudi. Na katika ghadhabu hii yeye aliamua kwenda kuiteketeza na kuibomoa Al Ka’abah Tukufu huko Makka.

Ili kutimiza azma yake hii, yeye alimtuma Kamanda Amir Jeshi wake Abraha kutangulia Makka pamoja na jeshi moja kubwa wenye farasi, waliopanda tembo na vikosi mbalimbali.

Abraha alielekea Makka akiwa pamoja na jeshi lenye nguvu sana na wakiwa njiani, miji yote walipopita waliiteketeza na kuiharibu na walikuwa wakishika wanyama waliokumbana nao humo njiani. Katika jangwa la Arabia yeye alikutana na mtu mmoja mwenye ngamia wasio pungua mia mbili. Ngamia hao walikuwa ni mali ya Bwana ‘Abdul Muttalib. Abraha aliwachukuwa hao ngamia wa Bwana ‘Abdul Muttalib. Yeye aliendelea kuelekea Makkah. Alipoukaribia mji wa Makka alipiga kambi katika vitongoji vya kukaribia Makka. Abraha alikuwa amekaa katika kiti chake na maaskari walikuwa wakimlinda. Punde akaja askari na kusema,

“Ewe Mheshimiwa ! Mheshimiwa wa Makka na Chifu wa kabila la Quraishi, ambaye jina lake ni Bwana ‘Abdul Muttalib, yuko nje ya kambi yetu na anataka kuonana nawe.”

Abraha alimwambia askari wake amruhusu Bwana ‘Abdul Muttalib aje mbele yake. Na punde si punde Bwana ‘Abdul Muttalib aliingia ndani ya hema lake. Heshima pamoja utukufu na nuru yalikuwa yakionyesha usoni mwa Bwana Bwana ‘Abdul Muttalib.

Abraha alipo mwona tu Bwana Bwana ‘Abdul Muttalib, aliinuka na kutoa heshima na kumwambia akae karibu naye. Na kwa kupitia Mkalimani Abraha alimwuliza sababu ya Bwana ‘Abdul Muttalib kutaka kumwona yeye.

Bwana ‘Abdul Muttalib alijibu:

“Mimi nimepata habari kuwa majeshi yako wamewachukua ngamia zangu. Na nimekuja hapa kukuomba unirudishie ngamia zangu hizo.”

Abraha akasema:

“Jambo gani hili la kushangaza ? Mimi nimekuja hapa kuiteketeza na kuiharibu kabisa Al Ka’abah na kuuondoa kabisa utukufu wake. Lakini mtu huyu naona hayajali hayo na badala yake naona anawajali ngamia zake. Lau kama Bwana ‘Abdul Muttalib angekuja kuniomba mimi nisiivunje na kubomoa Al Ka'abah Tukufu, basi kwa hakika kwa heshima zote nisingebomoa na badala yake ningerudi bila kutenda vurugu yoyote.”

Kwa kumjibu Abraha, Bwana ‘Abdul Muttalib alijibu:

“Mimi ni mmiliki wa ngamia zangu na hiyo Nyumba Tukufu (Al Ka'abah Tukufu) inayo mmiliki wake, vile vile. Mimi inanibidi nijali mali yangu na mwenye Nyumba hiyo Tukufu atajua mwenyewe namna ya kuiokoa na kuinusuru.”

Abraha kwa kusikia hayo alishangazwa mno na alitoa amri kuwa ngamia wa Bwana ‘Abdul Muttalib zirejeshwe kwake. Na baadae aliendelea na safari yake ya azma yake ya kuibomoa na kuiteketeza Al Ka'abah Tukufu.

Jeshi zima kuteketezwa

Alikuwa bado hajafika mbali katika kuukaribia Makka mara akakuta kundi kubwa la ndege wadogo wadogo waliokuwa wameitwa Ababil walionekana katika anga za Makkah na wakakuta wote wapo wanaruka juu ya vichwa vya majeshi ya Abraha. Kwa hakika ndege hawa walikuwa ni kama ndege za kivita kwani wao walikuwa wanavyo vijiwe vidogo vidogo mdomoni mwao na walikuwa wakiyadondosha juu ya vichwa vya wanajeshi hao wa Abraha. Na kila jiwe lililodondoshwa juu ya kichwa cha mwanajeshi kiligonga kichwa na kukipasua na wakawa wanajeshi hao wanaanguka juu ya ardhi na kufa papo hapo.

Mmoja aponea chupuchupu

Katika muda mchache kabisa wanajeshi wote wa Abraha waliuawa na ndege hao isipokuwa mmoja tu ambaye alinusurika na akakimbia hadi Abisynnia kwenda kuripoti hali hii ya maajabu yaliyotokea, kwa mfalme Najjashi. Baada ya kufika hapo alielezea habari zote za jeshi kubwa la Abraha lilivyoangamizwa na kuteketezwa na viumbe vidogo kabisa visivyo na nguvu ya aina yoyote. Najjashi alimwomba huyo mtu ampe habari zaidi kuhusu aina ya ndege aliokuwa amewaona yeye. Na ikatokezea kwamba ndege mmoja kama hao waliokuwa huko Makka alitokezea mbele yao na mtu huyo alimwelezea Najjashi kwa kumnyooshea ndege huyo kidole akisema :

“Ewe Mtukufu ! Huyu ndege ni hatari kabisa kwani hawa ndio wameweza kuliteketeza jeshi lote zima la maaskari.”

Punde alipomaliza tu kuyazungumza hayo na kutoa taarifa kamili ndege huyo alimpiga na kijiwe kidogo kutoka mdomo wake, jiwe ambalo likaenda kumpiga kichwani na hatima yake akafa papo hapo mbele ya Najjashi.

Tukio hili limetokea katika mwaka huo huo ambao Mtume Muhammad Mustafa (s.a.w.w) aliokuwa amezaliwa Makka.

WATU WA PANGONI (KAHF)

Allah (s.w.t) anatuambia katika Qur'an Tukufu, Sura Al Kahf, 18, ayah 9-14:

Bali unadhani ya kwamba wale watu wa Pangoni na Maandishi walikuwa ni ajabu miongoni mwa ishara zetu ?

Vijana hao walipo kimbilia kwenye pango walisema: Allah (s.w.t) wetu Mlezi! Tupe rehema itokayo kwako, na tutengenezee uwongofu katika jambo letu.

Tukayaziba masikio yao kuwalaza humo pangoni kwa muda wa miaka kadhaa wa kadhaa.

Kisha tukawazindua ili tujue ni lipi katika makundi mawili lilio hisabu sawa muda walio kaa.

Sisi tunakusimulia khabari zao kwa kweli. Hakika wao walikuwa ni vijana walio mwamini Allah (s.w.t) wao Mlezi. Na Sisi tukawazidisha uwongofu.

Na tukazitia nguvu nyoyo zao walipo simama na wakasema: Allah (s.w.t) wetu Mlezi ni Allah (s.w.t) Mlezi wa mbingu na ardhi. Hatutamwita mwenginewe kabisa badala yake kuwa ni mungu. Hivyo itakuwa tumesema jambo la kuvuka mpaka.

Daquis kujitangaza kuwa u mungu…

Katika ardhi ya Roma kulitawala Mfalme aliyekuwa mwadilifu kwa watu wake na ambaye alikuwa mkarimu pia. Yeye alitawala kwa kipindi kirefu cha kutosha na raia wake waliishi katika amani na hali nzuri.

Wakati Mfalme huyu alipokufa kulizuka tofauti miongoni mwa raia wake na ndicho kilichokuwa sababu ya kuleta maangamizo yao wenyewe. Mfalme wa nchi ya jirani, aliyekuwa akiitwa Daquis aliivamia nchi yao na kuimega katika ufalme wake.

Daquis alijenga ngome imara kwa ajili yake mwenyewe na aliipamba kwa kila kitu alichoweza kuipamba. Yeye aliwachagua watu sita wenye busara na waliokuwa na uwezo kutokana na watu wa ardhi zile alizoziteka na kuwafanya Mawaziri. Na baadae yeye aliwalazimisha watu kumwabudu yeye kama ndiye mungu. Majahili na wapumbavu miongoni mwa watu hao walimkubalia yeye kama ndiye mungu wao na walianza kumwabudu kwa kujitupa chini na kumwangukia sujuda.

Sherehe na habari za kuvamiwa

Kulipita muda na kuliwadia siku ya kusherehekea sherehe yao ya maadhimisho. Katika sherehe hizi Mfalme pamoja na baraza lake na raia wote walishirikiana kwa mbwembwe na shangwe kubwa. Wakati hawa wote wanasherehekea sherehe hizi, kulikuja na mleta habari na alimpa ujumbe Mfalme. Pale aliposoma habari hizo, rangi ya uso wake ulibadilika kwa sababu ya maafa yaliyokuwa yakitaka kumpata yeye pamoja na ufalme wake. Katika ujumbe huo kulikuwa kumeandikwa kuwa majeshi ya Mfalme wa Uajemi alikuwa tayari ameishaingia katika mipaka ya Roma na walikuwa wakisonga mbele kuukaribia mji mkuu wake. Kwa kuona taabu na shida hiyo katika uso wa Mfalme, iliyotokana na kusoma habari za kuvamiwa na uvamizi kutoka nje, mmoja wa Mawaziri wake sita wa Mfalme huyo aliweza kuvumbua na kujua kutokana na sura ya Mfalme huyo na alipoangalia nyuso za wenzake watano kwa kutaka kufanya utafiti, nao pia walionyesha dalili hizo. Kwa hayo tu wao waliweza kubashiri kuwa jambo fulani kubwa la kihistoria liko litatokezea.

Baada ya sherehe kumalizika kila mmoja aliondoka kwenda nyumbani kwake na Mawaziri pia waliondoka kurudi majumbani kwao ambapo wao walizoea kuitisha vikao vyao. Wakati wote walipokuwa wamesha keti pamoja, wao walizungumzia kile walichopeana habari kwa kutazamana nyuso.

Vuguvugu la uasi na kutoroka kwa mawaziri sita

Mmoja wao akasema:

“Je mliona uso wa kiajabu wa Mfalme ! Yeye anadai kuwa yeye mwenyewe ndiye mungu wa watu ambapo yeye anawachukulia kama ni watumwa wake. Lau kama angekuwa kweli ni mungu wa watu, basi kamwe asingekuwa ni mtu ambaye ameshtushwa kwa kupata habari zisizo mfurahisha. Hali hii ya yeye kutoweza kujisaidia imetupa sisi kiasi cha kutosha cha kufikiria, na kwa hakika imetufungua macho vya kutosha kushuku kuwa kwake mungu wa malimwengu zote.

Je ni nani muumbaji?

Enyi wenzangu ! Mimi kwa hakika ninatilia maanani sana na kuliwazia jambo muhimu sana. Je nani aliyejenga ulimwengu huu ni nani aliyezipachika hizi nyota ndani yake na kwa hukumu ya nani nyota na mwezi vinazunguka katika mizunguko yake ? Kwa nini niende mbali hadi kuzungumzia jua na mwezi ? Kwa nini nisijifikirie mimi mwenyewe ? Kwa nini nisifikirie ni nani ambaye amenileta mimi hapa nilipo akanitia katika tumbo la mama yangu, ambaye amenilea na amenipa mimi kila kitu cha kuweza kuishi na hizi nguvu nilizonazo za kimwili ?

Mimi kwa hakika sasa nimekuwa na imani kuwa mambo yote haya yanafanywa na Allah (s.w.t) ambaye ni Allah (s.w.t) wa Malimwengu yote na kamwe huyu hawezi kuwa mwenye Taqwa. Yeye ni mwerevu sana na wala hawezi kuzuzuliwa na kiumbe kidogo kama yeye.

Enyi marafiki zangu ! Maisha yetu yamekuwa ya kufedhehesha kwa kubakia kama watumwa wa Daquis na jambo hili haliwezi kuwa la kudumu milele. Lazima sisi tujitoe nje ya mambo ya dunia na starehe na raha ambazo zinatupeleka mbali zinatutoa mbali na ibada halisi ya Allah (s.w.t) na lazima tumuombe Allah (s.w.t) atusamehe kwa madhambi yetu yote.”

Athari za hotuba …

Mtu huyo mwenye hekima alizungumza mambo haya kwa hali ya kusisitiza kiasi kwamba wenzake waliathirika sana na wote sita kwa pamoja waliamua kutoroka njia ya wenye kuabudu masanamu na wakaamua kwenda kuishi porini na jangwani huko katika maisha ya kujitenga kwa ajili ya ibada tupu na kumwabudu Allah (s.w.t)

Kutoroka kwao .

Siku iliyofuatia hawa sita kwa pamoja walitoa majumbani mwao kisirisiri na wakaelekea jangwani. Walipofika maili fulani kutoka majumbani kwao, wao walimwaona mchungaji mmoja akichunga kondoo zake. Wao walimwomba maji kwa ajili ya kunywa. Na mchungaji aliwaambia,

“Mimi ninahisi kwenu nyie hewa ya utukufu na ucha Mungu. Je ni nani nyie na mnakwenda wapi ?”

Wao walijibu,

“Sisi tuko sita ni Mawaziri wa Mfalme, lakini tumekana nyadhifa zetu tulizopewa na mamlaka yake. Sisi tunajitenga na tunajitolea maisha kwa ajili ya ‘ibada ya Allah (s.w.t) , Allah (s.w.t) wa malimwengu yote kwa sababu kumwabudu Daquis ndiko kuliko tumaliza sisi kiroho na hakika nafsi zetu tunahisi vibaya mno.”

Mchungaji awa mtu wa saba…

Kwa hayo mchungaji akasema: “Nami pia nina msimamo kama nyie, na nitapenda kuungana nanyi na kuungana nanyi pamoja katika safari yenu na kuwa nanyi katika ‘ibada ya Allah (s.w.t) .”

Wao walikubaliana na ushauri na ombi alilolitoa mchungaji huyo. Mchungaji huyo aliwarudisha kondoo wote kwa mwenye mali na akarejea kuungana pamoja na hawa watu sita katika safari yao hiyo.

Mbwa kujiunga nao katika safari yao…

Mchungaji huyo alikuwa na mbwa ambaye naye pia alijiunga nao katika safari hiyo. Kwa kuwafuata fuata. Hao sita walipinga mbwa kuja nao, kwa sababu walikuwa wana hofu kuwa iwapo mbwa angebweka basi pale walipojificha patajulikana.

Nao wakasema, “Itakuwa vyema iwapo sisi tutamwondoa huyu mbwa na kumwacha hapa na tukaendelea na safari yetu.” Kwa hivyo walifanya jitihada zao zote za kumwacha mbwa nyuma, lakini mbwa hakuacha kumfuata mmiliki wake. Basi wakawa hawana chaguo lingine isipokuwa kumkubalia mbwa awafuata na kuungana nao.

Mchungaji huyo aliwachukua hawa wenzake sita katika majabali mlimani, ambapo upande wa pili wake kulikuwa na mabonde yaliyokuwa na mashamba yamestawi vizuri na kumejaa miti ya matunda. Kulikuwa na mto pia ukipita hapo. Kulikuwa na hewa nzuri iliyokuwa ikipita katika bonde hilo. Wao walikula matunda, wakanywa maji, na wakaingia katika mapango yaliyokuwa yakiitwa Kahf. Miale ya jua ilikuwa ikipita katika sehemu ambayo palikuwa wazi katika pango hilo. Wao walipumzika kwa kipindi kidogo na wakajishughulisha katika ‘ibada ya Allah (s.w.t).

Usingizi mrefu: Je ni nusu siku au siku moja au miaka 300?

Allah (s.w.t) anatwambia katika Qur'an Tukufu Sura Al Kahf, 18, ayah 19-20:

Na kwa namna hii tuliwainua usingizini wapete kuulizana wao kwa wao. Alisema msemaji katika wao: Mmekaa muda gani? Wakasema: Tumekaa siku moja au sehemu ya siku. Wakasema: Allah (s.w.t) wenu Mlezi anajua zaidi muda mliokaa. Hebu mtumeni mmoja wenu na hizi fedha zenu ende mjini, akatazame chakula chake kipi kilicho bora kabisa akuleteeni cha kukila. Naye afanye mambo hayo kwa busara, wala asikutajeni kabisa kwa yeyote.

Kwani wao wakikutambueni watakupigeni mawe, au watakurudisheni katika dini yao; na hapo hamtafanikiwa kabisa !

Baada ya hawa kufanya ‘ibada walipolala pamoja na mbwa wao katika kiingilio cha pango hilo. Upepo mzuri na wa kupendeza ulikuwa ukipita juu yao pole pole na vile vile miale ya jua pia iking’ara juu yao kwa kupitia upande uliokuwa wazi wa pango lakini wao walikuwa hawana habari yoyote na hayo kwa sababu waliingia katika usingizi mrefu. Hawa As-Hab Kahf (Watu wa Pangoni) walilala zaidi ya miaka mia tatu na katika kipindi hiki cha usingizi wao mrefu wao hawakuamka kutoka usingizini mwao. Lakini baada ya kupita kipindi hicho wao waliamshwa kwa amri ya Allah (s.w.t) na wakawa wakiangalia mahala palipo wazunguka. Wao walianza kuongelea kuhusu wao wenyewe. Baadhi yao walisema, “Sisi tumelala kwa siku moja”, wengine wakasema, “Tumelala nusu siku.” Lakini jambo ambalo liliwashtua na kuwastaajabisha ni kule kupotea kabisa kwa mimea na wao walikuwa wakihisi njaa pia. Wao walikuwa wakijaribu kujiuliza itawezekanaje kwa siku moja kupotea kwa mto na uoto kwa pamoja. Hatimaye wao waliamua kwenda kufuata chakula mjini kwani hawakuweza kustahimili njaa tena na zoezi hili lilikuwa lifanyike kwa mpango kabisa ili kwamba hakuna mtu yeyote atakayeweza kushuku au kujua mahala wao walipojificha, ama sivyo watu watawaua au kuwalazimisha kurudia katika kuabudu miungu.

Hivyo mmoja miongoni mwao aliyekuwa na uzoefu alivaa mavazi ya mchungaji na akaelekea mjini kwenda kutafuta chakula kwenda kutafuta mikate kwa fedha kidogo walizokuwa nazo.

Mtu huyo alipo karibia katika vitongoji vya mji, akaona imebadilika kabisa na ndani ya mji akaona mambo yote ya kustaajabisha kabisa. Mitaa, vichochoro na barabara na mistari ya milango na mistari ya majumba yalivyokuwa yamejengwa yote yalikuwa yameshabadilika kabisa. Hata mavazi ya wakazi wa mjini pia yalikuwa yamebadilika kabisa. Na hivyo alishikwa na bumbuwazi kwa kuona mabadiliko hayo kwa kiasi hicho katika mpangilio wa kila jambo katika mji huo. Na hivyo aliwaza kama yeye alikuwa katika fahamu zake sahihi au hapana au alikuwa akiota ndoto. Je ameingia katika mji mwingine kwa kupotea njia ya kwenda mji wake ? Je kwa nini ameshindwa kuwatambua watu ambao aliokuwa anawajua katika mji wake huo ?

Hatimaye alifika katika tanuru la mwoka mikate. Yeye aliagiza mikate michache kwa mategemeo ya kumlipa kwa pesa alizokuwa nazo. Mwoka mkate huyo alipoziona fedha hizo, alimwuliza: “Ewe kijana ! Je kuna mahali umevumbua hazina?”

Mtu huyu wa Mapango alijibu:

“Laa, hizi fedha mimi nimelipwa na nimezipata baada ya kuuza tende zangu juzi. Na baada ya hapo nilikuwa nimekwenda safari nje ya mji na hivi ndipo nimerudi.”

Mwoka mikate hakuridhishwa na aliyoyasema huyo mtu, na hatimaye akamfikisha mbele ya Mfalme na kusema,

“Mtu huyu amevumbua hazina. Na uthibitisho wake ni kwamba ni kutokana na fedha alizonazo mikononi mwake.”

Mfalme akamwambia mtu huyo:

“Ewe kijana ! Usiniogope mimi. Niambie ukweli. Sisi kamwe hatutakudhuru. Mtume wetu Issa (a.s) mwana wa Bi. Mariam ametuamrisha kutoza Khums (Kodi ya kidini) kutoka mtu yeyote yule anayevumbua hazina.”

Mtume huyo alimlilia Mfalme ili aweze kusikiliza kilio chake hicho. Yeye akasema,

“Mimi ni mkazi wa mji huu. Ni siku mbili tu zilizopita mimi na wenzangu tuliondoka tukaenda mapangoni kwa ajili ya kufanya ibada ya Allah (s.w.t) Wakati wetu wa kuondoka kulikuwa na Mfalme aliyekuwa akiitwa Daquis (Daqyanus), ambaye ndiye alikuwa mtawala wa mji huu na ambaye alikuwa akiwalazimisha watu wamwabudu yeye kama mungu na kujitupa mbele yake katika Sujuda. Na kwa kutokana na sisi kutokumwamini yeye kama ni mungu, ndicho sisi kilicho tusababisha kuhama mji huu na kujificha katika mapango huko jangwani. Na wenzangu wapo wanasubiri kurudi kwangu mimi kwao.”

Mfalme akasema:

“Sisi tutakwenda pamoja nawe ili tukashuhudie mambo wenyewe lau kama unasema ukweli katika habari zako hizi, kwa sababu mambo unayoyazungumza wewe ni ya kustaajabisha sana, ni mambo mapya kabisa. Ni kiasi cha miaka mia tatu iliyopita tangu Daquis alipotawala huku.”

Mfalme kwenda pangoni

Kwa hivyo Mfalme pamoja na watu wa baraza lake waliandamana naye huyo mtu hadi katika mapango na yeyote yule aliyepata habari hizi pia alishirikiana nao wakaenda mpaka kwenye mapango hayo.

Wao walipofika katika mpitio wa mlima, mtu huyo wa pangoni akamwambia Mfalme,

“Itakuwa vyema iwapo nyie mtabaki hapa. Iwapo mtatokezea ghafla mbele ya wenzangu wataogopa na kushtushwa. Na inawezekana mshtuko huu ukawagharimu ukawa hatari kwao. Naomba mimi niende peke yangu mbele yao na niwaeleze habari zote ndipo nyie mje.”

Mtu huyo alipoingia ndani ya mapango na kuwaambia wenzake:

“Enyi wenzangu ! usingizi wenu ambao mnaufikiria kuwa ni wa siku moja haukuwa hivyo, ua haukuwa usingizi wa nusu siku, bali usingizi umechukuwa baadhi ya karne. Mimi nimekwenda mjini na nimeona kule kila kitu kimebadilika kabisa. Mfalme mdhalimu Daquis amekufa zaidi ya miaka mia tatu iliyopita, na hakuna chochote kinachoonyesha yeye au ufalme wake. Na kwa amri ya Allah (s.w.t) ametumwa Mtume kwa jina la Issa (a.s) mwana wa Bi. Mariam katika ardhi hiyo, na watu wa huko ndio wafuasi wake. Kwa hakika mimi nimekumbana na matatizo makubwa sana nikiwa hapo mjini. Na sarafu niliyokuwa nayo nilipowaonyesha watu, waliona maajabu kwao. Na hivyo wakadhani kuwa mimi nimevumbua hazina fulani. Wao wakanichukua kwa Mfalme wao na hapo ndipo nikaja kutambua kuwa sisi tumelala usingizi kwa amri ya Allah (s.w.t) kwa zaidi ya miaka mia tatu. Mfalme na watu wa baraza lake wametusubiri hapo nje. Wao wamekuja kuthibitisha hayo niliyoyasema. Kama nyinyi mtanikubalia, mimi ninaweza kuwaleta hapa mbele yenu.”

Wale wenzake katika pango hawakumwamini huyo mwenzao. Wao walidhani kuwa mwenzao anataka kuwaponza na wakamatwe na Mfalme. Basi hapo wao walimlilia Allah (s.w.t) na kumwomba kuwa yeye Allah (s.w.t) awarudishe katika hali waliyokuwa nayo. Wao waliinua mikono yao juu na kuomba,

“Ewe Allah (s.w.t) ! tuokoe sisi kutokana na janga hili na uturudishe katika hali yetu tuliyokuwa nayo.”

Dua yao ilikubaliwa na Allah (s.w.t) aliwafanya wao tena wakarudia usingizi wao mrefu. Mfalme na watu wake waliwasubiri hao kwa muda mrefu bila kuona mtu akirejea. Nao waliingia katika pango hilo na kwa amri ya Allah (s.w.t) wale waliokuwa wamelala hawakuweza kuonekana machoni mwa Mfalme na watu wake.

Kwa amri ya Mfalme, hapo kulijengwa Msikiti kwa ajili ya ‘ibada ya Allah (s.w.t)

Tukio hili ni mojawapo la ‘ishara za Allah (s.w.t) yaliyoonyeshwa kwa watu ili waweze kujifunza masomo kuhusu ukuu wa Allah (s.w.t) , Allah (s.w.t) wa malimwengu zote.