JOHARI ZA HEKIMA KWA VIJANA

JOHARI ZA HEKIMA KWA VIJANA0%

JOHARI ZA HEKIMA KWA VIJANA Mwandishi:
: HEMEDI LUBUMBA SELEMANI
Kundi: Vitabu mbali mbali

JOHARI ZA HEKIMA KWA VIJANA

Mwandishi: Muhammad Reyshahri
: HEMEDI LUBUMBA SELEMANI
Kundi:

Matembeleo: 14458
Pakua: 2305

Maelezo zaidi:

JOHARI ZA HEKIMA KWA VIJANA
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 11 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 14458 / Pakua: 2305
Kiwango Kiwango Kiwango
JOHARI ZA HEKIMA KWA VIJANA

JOHARI ZA HEKIMA KWA VIJANA

Mwandishi:
Swahili

JOHARI ZA HEKIMA KWA VIJANA

UDONDOZI KUTOKA KITABU: JAWAAHIRU AL-HIKMAH LI 'SH-SHABAAB

KIMEANDIKWA NA: MUHAMMAD REYSHAHRI

KIMETARJUMIWA: HEMEDI LUBUMBA SELEMANI

KIMEPANGWA KATIKA KOMPYUTA NA: HAJAT PILI RAJAB

NENO LA MCHAPISHAJI

Kitabu kilichoko mikononi mwako ni tarjuma ya kitabu cha Kiarabu kiitwacho, Jawaahiru 'Al-Hikmah li 'sh-Shabaab, ambacho tumekifupisha na kukiita: (JOHARI ZA HEKIMA KWA VIJANA).

Kwa hakika kitabu hiki kinazungumzia maadili ya vijana kwa mtazamo wa Kiislamu. Kama tujuavyo, Uislamu ni dini na mfumo kamili wa maisha, kwa hiyo, haukuacha chochote kinachomhusu mwanadamu katika maisha yake ya hapa duniani na ya kesho Akhera.

Mwandishi wa kitabu hiki amejaribu kwa uwezo wake kuwakumbusha vijana juu ya wajibu wao katika jamii na kuwarejesha katika maadili mema. Na katika kuikamilisha kazi yake hii amerejea sana kwenye mafunzo ya Uislamu ambayo chimbuko lake ni Qur'ani na Sunna. Hivyo basi, huu ni mwongozo halisi kwa vijana unaolenga kuwaokoa katika harakati zao za maisha na hatimaye wawe ni wenye kufuzu kesho Akhera.

Sisi tumekiona kitabu hiki ni chenye manufaa sana, hususan wakati huu ambapo vijana wengi wamejitumbukiza katika mambo yenye kuangamiza maisha yao kwa kuacha utamaduni wao bora wa Kiislamu na kuiga tamaduni potofu, fasiki na fisadi za watu wa Magharibi (wazungu). Watu wenye busara huiga mambo mazuri na huwaachia wenyewe yale machafu, lakini kwa vijana wetu sivyo, wamepupia sana katika kuiga kama kima kila jambo karihifu la watu wa Magharibi. Hivyo kitabu hiki kitakuwa ni mwongozo mzuri kwa vijana wetu wa Kiislamu na hata wasio Waislamu.

Kutokana na ukweli huo, Taasisi yetu ya Al-Itrah Foundation imeamua kukichapisha kitabu hiki kwa lugha ya Kiswahili kwa madhumuni yake yaleyale ya kuwahudumia Waislamu, hususan wazungumzaji wa Kiswahili.

Tunamshukuru ndugu yetu, Hemedi Lubumba Selemani kwa kukubali jukumu hili la kukitarjumi kitabu hiki. Vilevile tunawashukuru wale wote walioshiriki kwa njia moja au nyingine hadi kufanikisha kuchapishwa kwake. Ni matumaini yetu kwamba kitabu hiki kitakuwa ni mwanga kwa wasomaji wetu na kuzidisha upeo wao wa elimu ya dini ni ya jamii.

DIBAJI

Bismilahi Rahman Rahim. Rehema na amani zimwendee Mtukufu wa Daraja Mtume Muhammad(s.a.w.w) , yeye na kizazi chake watoharifu maasumina(a.s) . Bila shaka kipindi cha ujana ndio fursa muhimu inayompa mwanadamu uwezo wa kutimiza vipaji na uwezo binafsi, kama ambavyo vijana ni haz- ina kubwa yenye thamani ndani ya jamii mbalimbali za wanadamu. Kuanzia hapa ndipo maendeleo yote ya nchi yoyote ile yakategemea jinsi vipaji vya vijana vitakavyotunzwa, na jinsi watakavyoelimishwa na vipaji vyao kukuzwa. Kwa ajili hiyo daima wanaharakati, viongozi wa kidini na wa kisiasa wametilia sana umuhimu wa harakati za vijana ndani ya zama zote za historia ya mwanadamu. Katika zama zetu hizi za maendelelo ya sayansi na teknolojia, upande mmoja tunakuta kitendo cha vijana kukusanya maalumati na maarifa mbal- imbali kimesaidia sana katika kuleta maendeleo ya kielimu na kiteknolo- jia. Upande mwingine ni kuwa watu wa manufaa na wafanyabiashara wenye masilahi binafsi ya kisiasa na kiuchumi katika ulimwengu huu, wamejiandaa kutumia fursa hii kwa lengo la kutumia vibaya vipaji vya vijana kuliko zamani, hivyo ndio maana suala la vijana limekuwa na umuhimu sana leo kuliko hapo kabla. Bila shaka kipindi hiki cha ujana ndio ardhi munasibu yenye rutuba safi na mbolea bora ya kuweza kuhifadhi mbegu bora na hatimaye kuotesha mazao endelevu kwa ajili ya leo na kesho, kwani ndio kipindi ambacho Mwenyezi Mungu amekipa sifa ya nguvu na uwezo wa kila kitu, kiasi kwamba ubora na ufanisi upatikanao ndani ya kipindi hiki hauwezi kupatikana nje ya kipindi hiki. Mwenyezi Mungu asema:

Mwenyezi Mungu ndiye aliyekuumbeni katika udhaifu, na baada ya udhaifu akafanya nguvu, kisha baada ya nguvu akaufanya udhaifu na uzee, huumba apendavyo, naye ni Mjuzi Mwenye uwezo ." (Surat Rum: 54).

Kisha akasema tena: "Yeye ndiye aliyekuumbeni kwa udongo, kisha kwa manii, kisha kwa pande la damu, halafu akakutoeni katika hali ya mtoto mchanga, kisha ili mpate nguvu zenu kamili, kisha (akakuacheni) muwe wazee, na wengine wenu hufishwa kabla (ya uzee) na ili mfikie muda uliowek- wa, na ili mpate kufahamu. " (Surat Muumin / Ghafir: 67). Ni dhahiri Aya zilizotangulia zimeonyesha thamani ya ujana na matarajio endelevu kutoka ndani ya kipindi hicho ambacho Imam Jafar As-Sadiq(a.s) amekiwekea kikomo kwa kusema: "Mtu akizidi miaka thelathini basi ameshakuwa mzee, na akizidi arubaini basi tayari keshakuwa kikongwe ."[1]

Japokuwa katika zama zetu hizi kila taifa au kundi hujiwekea mwanzo na kikomo cha ujana, lakini hakuna anayeepuka umri huo uliotajwa na Imam Jafar(a.s) , na hivyo naweza kusema kuwa lengo si umri, bali lengo ni jinsi gani mwanadamu ndani ya maisha yake anaweza kutumia vizuri kipindi chake chote cha uwezo na nguvu zenye ufanisi na ubora, kipindi ambacho bila shaka ndio kipindi cha ujana. Sijaona msiba mkubwa katika nchi zetu za kiafrika na hasa Tanzania kama msiba huu wa vijana kutokujali kabisa kipindi chao hiki, lakini linaloshangaza zaidi ni kuona wazee ambao ni waathirika wa mafunzo ya ujana jinsi gani wameshindwa kabisa kuwaandaa watoto wao kwa ajili ya kipindi hiki chenye thamani. Kutokana na uzembe huo wa wazee vijana wengi wameshindwa kujua thamani ya ujana wao, na hivyo kusababisha baadhi ya hasara za kijamii za kujitakia ikiwemo, ujinga, viongozi mbum- bumbu, ufisadi, utumiaji wa madawa ya kulevya, ulevi, ushoga, ukahaba, ubakaji, ujambazi, ufukara, umaskini, maradhi na mengine mengi yanay- ochangiwa sana na kitendo cha vijana wa zamani kutowaandalia mazingi- ra vijana wa sasa. Uisilamu unatambua thamani ya ujana na athari zake za kiroho na kimwili hadi kimaada, ndipo Imam Ali(a.s) akasema: "Hakika moyo wa kijana ni sawa na ardhi tupu, chochote kitakachotupwa hapo hukikubali ." Hapo Imam akataka vijana wapandikizwe maadili mema na mtazamo sahihi ili maadui wa ubinadamu wasiweze kutumia fursa hiyo kupanda mbegu zenye sumu kwa jamii. Mtume(s.a.w.w) alijali sana kuwasomesha na kuwalea vijana, hivyo jiwe lake la kwanza alilolitaka katika msingi wa Uislamu lilikuwa ni vijana, na hivyo ndivyo ilivyokuwa, na kijana wa kwanza akiwa ni Ali (a.s) ambaye kwa ujana wake aliusimamisha Uislamu, ndipo Mtume(s.a.w.w) akawausia sahaba zake:

"Nawausia kheri kwa vijana, kwani hakika wao ni wenye vifua vyepesi, Mwenyezi Mungu alinituma niwe mbashiri na muonyaji, vijana wakaniunga mkono, na wazee wakanipinga ."

Na kwa msingi huu Imam Jafar As-Sadiq(a.s) akamuusia Abu Jafar Al- Ahwal akimuomba kuwasambazia vijana elimu na maarifa ya Ahlul-Bait(a.s) ili waweze kuharakisha kuelekea kwenye kila la kheri, akasema: "Shikamana na vijana, kwani hakika wao ndio wepesi kuelekea katika kila kheri ." Na hivyo kauli hii ya Imam inaelekeza na kuwajibisha majukumu kwa walezi, wazazi, viongozi wa kidini na kisiasa, wanaharakati na vion- gozi wa jamii. Mwenyezi Mungu anawapenda sana vijana, na ndio maana wafuasi shu- pavu, makini na waaminifu walikuwa ni vijana, au kwa kauli nyingine ni kuwa Manabii na Mawasii wakiwemo Maimamu wetu(a.s) walikuwa ni sehemu ya vijana. Basi Kitabu hiki ni sehemu nyingine ya mwongozo wa Mwenyezi Mungu na upendo Wake kwa vijana wote na hasa wa kizazi hiki ambacho kimezungukwa na kila aina ya mitego ya ufisadi, uovu na uasi.

JOHARI ZA HEKIMA KWA VIJANA

SEHEMU YA KWANZA

NAFASI YA KIPINDI CHA UJANA KATIKA USTAWI

1- KIPINDI CHA USTAWI WA MAISHA

Thamani ya ujana: Mwenyezi Mungu asema: "Mwenyezi Mungu ndiye aliyekuumbeni katika udhaifu, na baada ya udhaifu akafanya nguvu, kisha baada ya nguvu akaufanya udhaifu na uzee, huumba apendavyo, naye ni Mjuzi Mwenye uwezo. " (Surat Rum: 54).

Akasema tena: "Yeye ndiye aliyekuumbeni kwa udongo, kisha kwa manii, kisha kwa pande la damu, halafu akakutoeni katika hali ya mtoto mchanga, kisha ili mpate nguvu zenu kamili, kisha (akakuacheni) muwe wazee, na wengine wenu hufishwa kabla (ya uzee) na ili mfikie muda uliowekwa, na ili mpate kufahamu. " (Surat Muumin/ Ghafir: 67).

Imam Ali(a.s) amesema:

"Vitu vinne thamani yake hakuna anayeijua ila watu wa namna nne:

(a) Hakuna anayejua thamani ya ujana ila wazee.

(b) Hakuna anayejua thamani ya afya ila mwenye maradhi.

(c) Hakuna anayejua thamani ya siha ila mgonjwa.

(d) Hakuna anayejua thamani ya uhai ila wafu."[2]

Imam Ali(a.s) amesema: "Hakuna anayejua thamani ya vitu viwili ila yule aliyevikosa: Ujana na afya. "[3]

Imam Ali(a.s) amesema: "Vitu viwili lau macho mawili yatavililia kwa machozi ya damu mpaka yadondoke, bado hayatafikia uzito wake: Kupitwa na ujana na kuwakosa vipenzi. "[4]

Imam Ali(a.s) amesema: "Ujana waniliza umenitoka, natamani ujana ungenirudia. Lau ujana ungekuwa unauzwa kwa lolote, basi hakika ningempa muuzaji atakacho. Lakini ujana unapoondoka kuupata ni kazi. "[5]

KUNUFAIKA NA FURSA YA UJANA

Mwenyezi Mungu asema: "Na utafute makazi ya Akhera yale aliyokupa Mwenyezi Mungu wala usisahau sehemu yako ya dunia. " (Surat Al-Qasas: 77).

Akasema tena: "Na humo watapiga makelele: Mola wetu Mlezi! Tutoe (Motoni) tutafanya vitendo vizuri visivyokuwa vile tulivyokuwa tukifanya! Je, hatukukupeni umri (mwingi) akumbuke mwenye kukumbuka, na alikufikieni mwonyaji, basi onjeni, na hakuna msaidizi kwa ajili ya madhalimu. " (Surat Faatir: 37).

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Ewe Ali! Vitumie vitu vinne ipasanyo kabla hujafikwa na vinne:

(a) Ujana wako kabla ya utu uzima wako.

(b) Siha yako kabla ya ugonjwa wako.

(c) Utajiri wako kabla ya ufakiri wako.

(d) Uhai wako kabla ya kifo chako."[6]

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Mja ajiandalie matumizi ya akhera yake kutoka kwenye dunia yake, na ya kifo chake toka kwenye uhai wake, na ya uzee wake toka kwenye ujana wake, kwani dunia imeumbwa kwa ajili yenu na nyinyi mmeumbwa kwa ajili ya Akhera. " [7]

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Enyi watu! Hakika mna dira zitazameni dira zenu na hakika nyinyi mna kikomo tazameni kikomo chenu, kwani hakika muumini yupo baina ya vitu viwili vyenye kuogopesha: Siku iliyopita ambayo hajui Mwenyezi Mungu atamuhukumia nini humo, na siku iliyobakia hajui nini Mwenyezi Mungu atamtendea humo. Basi mja achukue toka ndani ya nafsi yake kwa ajili ya nafsi yake, na toka ndani ya dunia yake kwa ajili ya akhera yake, na toka ndani ya ujana wake kwa ajili ya uzee wake, na toka ndani ya siha yake kwa ajili ya ugonjwa wake na toka ndani ya uhai wake kwa ajili ya kifo chake. Naapa kwa Ambaye nafsi yangu imo mikononi mwake kuwa baada ya mauti hakuna mkemewaji, wala baada ya dunia hakuna nyumba ila pepo au moto ." [8]

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Mambo ni rehani ya wakati wake. " [9]

Imam Ali(a.s) amesema: "Harakisheni kutumia fursa kabla haijakuwa chungu ."[10]

Imam Ali(a.s) amesema: "Dunia iko karibu mno na uondokaji, na uzee uko karibu mno na ujana. "[11]

Imam Ali(a.s) amesema: "Hakukitendea kabisa haki kifo yule anayeian- daa kesho kwa ajili yake. "[12]

Imam Ali(a.s) amesema: "Itumieni fursa ya kheri, kwani bila shaka yenyewe hupita mpito wa mawinguni. "[13]

Imam Ali(a.s) amesema kuhusu kauli ya Mwenyezi Mungu: "Wala usisahau sehemu yako ya dunia " (Surat Al-Qasas: 77) "Usisahau siha yako, nguvu zako, faragha yako, ujana wako na fungu lako kuvitumia katika kuitafuta Akhera. "[14]

Imam As-Sadiq(a.s) amesema kuhusu kauli ya Mwenyezi Mungu: "Je, hatukukupeni umri (mwingi) akumbuke mwenye kukumbuka, na alikufikieni mwonyaji, basi onjeni, na hakuna msaidizi kwa ajili ya madhalimu " (Surat Faatir: 37) "Ni kumfokea kijana wa miaka kumi na nane."[15]

Imepokewa ndani ya kitabu Tanbihul-Khawatir kuwa: "Nabii Issa(a.s) alikuwa awakutapo vijana huwaambia: "Ni mazao mangapi hayajafikia mavuno." Na akiwakuta wazee huwaambia: "Mazao yakishafikia (mavuno) huwa hakuna linalongojewa ila kuvunwa. "[16]

HAZINA YA SIKU

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Siku ya Kiyama mja atafunguliwa hazina ishirini na nne, sawa na idadi ya saa za usiku na mchana za kila siku kwa idadi ya siku za umri wake, atakuta hazina moja imejaa nuru na furaha, basi atakapoishuhudia ataichukua kwa fura- ha ambayo lau wakigaiwa watu wa motoni basi inawashtua kwa kuwaondolea hisia za machungu ya moto. Na hiyo ndio ile saa aliyomtii ndani yake Mola wake. Kisha atafunguliwa hazina nyingine, ataiona ikiwa na giza kali lenye kutisha, basi atakapoishuhudia ataichukua kwa uoga na mdhazaiko, kiasi kwamba lau wakigaiwa watu wa peponi neema Zake zitakuwa chungu kwao. Hiyo ndio ile saa aliyomuasi ndani yake Mola wake. Kisha atafunguliwa hazina nyingine na kuona ikiwa tupu haina kinachom- furahisha wala kumchukiza, hiyo ndiyo ile saa aliyolala ndani yake au kujishughulisha na jambo la halali la kidunia, hapo ataichukua kwa hasara na majuto kwa kupitwa na saa hiyo, kwani alikuwa anaweza kuijaza mema yasiyohesabika. Na hii ndio kauli ya Mwenyezi Mungu: "Hiyo ni siku ya khasara" (Surat Taghabun: 9)[17]

JUHUDI ZA DHATI KATIKA NJIA YA MAENDELEO

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Dunia ni saa moja, hivyo ifanyeni utii. " [18]

Imam As-Sadiq(a.s) amesema: "Zitakayelingana sawia siku zake mbili basi kala hasara. Utakayekuwa mwisho wa siku zake ni mbaya basi ni mwenye kulaaniwa. Asiyejua nyongeza yoyote ndani ya nafsi yake basi yuko karibu mno na upungufu. Na atakayekuwa karibu mno na upungufu basi kifo kwake ni bora kuliko uhai ."[19] Kutathmini siku za ujana: Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Hautanyanyuka unyayo wa mja mbele ya Mola wake siku ya Kiyama mpaka aulizwe kuhusu mambo matano:

(a) Umri wake ameutumia katika kitu gani.

(b) Ujana wake ameutumia katika kitu gani.

(c) Mali yake aliipata vipi

(d) Na aliitumia vipi.

(e) Na alifanya nini kuhusu yale aliyokuwa na elimu nayo."[20]

Mtume wa Mwenyezi Mungu amesema: "Hautanyanyuka unyayo wa mja mbele ya Mola wake siku ya Kiyama mpaka aulizwe kuhusu mambo manne:

(a)Umri wake ameutumia katika kitu gani.

(b) Ujana wake ameu- tumia katika kitu gani.

(c) Mali yake aliipata vipi.

(d) Na aliitumia vipi.

(e) Na kuhusu mapenzi yetu Ahlul-Bait."[21]

Imam As-Sadiq(a.s) amesema: "Miongoni mwa mawaidha ya Luqman(a.s) kwa mwanae ni: 'Jua hakika wewe kesho utaulizwa mambo manne pindi utakaposimama mbele ya Mwenyezi Mungu:

(a) Ujana wako umeu- tumia katika kitu gani.

(b) Umri wako ameutumia katika kitu gani.

(c) Mali yako uliipata vipi.

(d) Na uliitumia vipi. Basi jiandae kwa hilo na liandalie majibu."[22]

2- USTAWI KATIKA KUJIJENGA

Utayarifu wa kijana katika kujijenga kiroho na kimwili: Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Nawausia kheri kwa vijana, kwani hakika wao ni wenye vifua vyepesi, Mwenyezi Mungu alinituma niwe mbashiri na muonyaji, vijana wakaniunga mkono, na wazee wakanipinga". Kisha akasoma kauli ya Mwenyezi Mungu: "Na muda wao ukawa mrefu, kwa hivyo nyoyo zao zikawa ngumu.. " (Surat Yunus: 83).[23]

Imesemwa ndani ya Tafsiri Al-Qummiy kuhusu kauli ya Mwenyezi Mungu: "Na walishangaa kwa kuwafikia mwonyaji anayetokana nao. "(Surat Swad: 4):

Iliteremka Makka pindi Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) alipodhihirisha Uislam, kwani makur ayshi walijikusanya kwa Abu Talib na kumwambia: "Ewe Abu Talib! Bila shaka mwana wa ndugu yako kachafua ndoto zetu, katukana miungu yetu, kawaharibu vijana wetu na kavunja umoja wetu, basi ikiwa linalomsababisha kufanya hivyo ni ukata, sisi tutamkusanyia mali na kummilikisha mpaka awe mtu tajiri kuliko sisi". Basi Abu Talib akampa habari kuhusu hilo, akasema: "Wallahi lau wakiweka jua mkono wangu wa kushoto na mwezi mkono wangu wa kulia, sin- toitaka (mali hiyo)."[24]

Imam Ali(a.s) amesema: "Akili na upumbavu huendelea kumgombania mtu mpaka afikishapo miaka kumi na nane, akiifikia ndipo lenye nguvu zaidi kati ya hayo mawili hushinda. "[25]

Imam As-Sadiq(a.s) amesema: "Ewe mwana wa ndugu yangu! Shikamana na vijana na achana na wazee. "[26]

Imepokewa ndani ya kitabu Al-Kafiy kutoka kwa Ismail bin Abdul-Khaliq amesema: "Abu Abdillah(a.s) alimwambia Abu Jafar Al-Ahwal nami nikiwa nasikia: 'Je, umekwenda Basra?' Akajibu ndio. Akasema: 'Umeonaje watu wanavyoharakisha kuingia na kulikubali jambo hili?' Akasema: 'Wallahi hakika ni wachache waliofanya hivyo, na hakika hilo ni kwa uchache.' Akasema: 'Shikamana na vijana, kwani hakika wao ni wepesi wa kuelekea kila kheri."[27]

Imepokeawa ndani ya kitabu Ilalus-Sharaiu kutoka kwa Ismail bin Al- Fadhlu Al-Hashimiy amesema: "Nilimwambia Jafar bin Muhammad(a.s) , nipe habari kuhusu Yaqub(a.s) pindi wanae walipomwambia: "Ewe baba yetu! Tuombee msamaha kwa dhambi zetu, hakika sisi tulikuwa wenye makosa. "Akasema: Nitakuombeeni msamaha kwa Mola wangu Mlezi, kwani Yeye ndiye Mwingi wa kusamehe, Mwenye kurehemu " (Surat Yusuf: 97-98). Akawa amechelewesha msamaha wao. Lakini Yusuf(a.s) walipomwambia: "Wakasema: Wallahi bila shaka Mwenyezi Mungu amekufadhilisha kuliko sisi, na hakika sisi tulikuwa wenye makosa. Akasema: Hakuna lawama juu yenu leo, Mwenyezi Mungu atakusameheni, naye ni Mwenye rehema zaidi kuliko wanaorehemu. " (Surat Yusuf: 91 - 92).

Akawaharakishia. Imam(a.s) akasema: 'Kwa sababu moyo wa kijana ni mwepesi kuliko moyo wa mzee, na jinai la watoto wa Yaqub lilikuwa ni dhidi ya Yusuf, na jinai yao dhidi ya Yaqub ni kwa kuwa walimfanyia jinai Yusuf, hivyo Yusuf akaharakisha kusamahe haki yake, na Yaqub akachelewesha msamaha, kwa sababu kusamehe kwake kulikuwa ni kusamehe haki ya mwingine, hivyo akachelewesha msamaha mpaka usiku wa Ijumaa."[28]

NAFASI YA VIJANA KATIKA KUJIELIMISHA

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Atakayejifunza ujanani inakuwa kama nakshi kwenye jiwe. Na atakayejifunza ukubwani inakuwa kama kitabu juu ya maji. " [29]

Imam Ali(a.s) amesema: "Jielimisheni mkingali wadogo itawanufaisheni ukubwani ."[30]

Imam Ali(a.s) amesema: "Asiyeibidisha nafsi yake udogoni basi hatopevuka kiakili ukubwani ."[31]

Imam Ali(a.s) amesema: "Upiteni ujana kwa midahalo na mijadala. Utu uzima kwa tafakari na uzee kwa ukimya ."[32]

Imam Al-Baqir(a.s) amesema: "Baba yangu mpendwa Zaynul-Abidiin alikuwa awaonapo vijana wanaotafuta elimu huwasogeza kwake na kuwaambia: "Karibuni! Ninyi ni hazina ya elimu, ninyi leo ni wadogo wa wengine, na mnakaribia kuwa wakubwa wa wengine ."[33]

Imam As-Sadiq(a.s) amesema: "Sipendi kumwona kijana miongoni mwenu ila akiwa amezama katika hali mbili: Ima msomi au mwenye kujielimisha, na kama hatofanya hivyo basi kavuka mipaka, na akivuka mipaka kapoteza, na akipoteza katenda dhambi, na akitenda dhambi kaishi motoni. Naapa kwa yule aliyempa unabii Muhammad (s.a.w.w) kwa haki ."[34]

MAFUNZO YA KIROHO

Imam Ali(a.s) amesema: "Hakika moyo wa kijana ni sawa na ardhi tupu, chochote kitachopandwa humo hukipokea, hivyo harakisha kujifunza adabu kabla moyo wako haujasusuka ."[35]

Imam Ali(a.s) amesema alipokuwa akimuusia mwanae Imam Hasan(a.s) : "Na nikakusanya adabu yako ili uwe nayo ungali na umri mdogo, wenye akili, ukiwa na nia salama na nafsi safi. "[36]

Imam Zaynul-Abidiin(a.s) amesema: "Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) aliwakuta watu wakiinua jiwe, akawaambia: 'Kazi gani hii?' Wakamjibu: 'Tunataka kwayo tumjue ni nani mwenye nguvu kati yetu.' Akasema(s.a.w.w) : 'Je, niwaambieni ni nani mwenye nguvu kati yenu?' Wakasema ndio ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu. Akasema(s.a.w.w) : 'Mwenye nguvu kati yenu ni yule ambaye anaporidhia ridhaa yake haimwingizi katika dhambi wala batili. Anapokasirika kukasirika kwake

hakumzuii kusema haki, na anapokuwa na uwezo hatoi kisichokuwa haki."[37]

MANABII(A.S) WALITUMWA WAKIWA VIJANA

Mwenyezi Mungu amesema: "Wakasema: Tulimsikia kijana mmoja akiwataja anaitwa Ibrahim. " (Surat Anbiyai: 60).

Akasema tena: "Na alipofika (Musa) baleghe yake na akastawi, tulimpa hukumu na elimu na hivyo ndivyo tunavyowalipa watendao mema. " (Surat Al- Qasas: 14).

Na amesema: "Na alipofika (Yusuf) baleghe yake, tulimpa hukumu na elimu na hivyo ndivyo tunavyowalipa watendao mema. " (Surat Yusuf: 22).

Imam As-Sadiq(a.s) amesema kuhusu kauli ya Mwenyezi Mungu:

"Na alipofika (Musa) baleghe yake na akastawi, tulimpa hukumu na elimu ": "Na alipofika (Musa) baleghe yake, yaani miaka kumi na nane.Na akastawi, yaani alipoota ndevu. "[38]

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Mwenyezi Mungu hakumtuma Nabii yeyote ila alikuwa ni kijana. " [39]

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Mwenyezi Mungu hakumtuma Nabii yeyote ila alikuwa ni kijana, na msomi hakupewa elimu ila alikuwa ni kijana ." [40]

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Enyi wana wa Abdul Muttalib! Hakika wallahi simjui kijana yeyote katika waarabu aliyewaletea watu wake kitu bora kuliko nilichowaletea, kwani hakika mimi nime- waletea kheri ya dunia na Akhera ." [41]

Imam Mahdi(a.s) atadhihiri akiwa kijana: Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Mwisho wa zama atasimama mtu kutoka ndani ya kizazi changu akiwa kijana mwenye uso mzuri na pua iliyochongoka, ataijaza ardhi uadilifu na usawa kama itakavyokuwa imejaa dhulma na ujeuri. " [42]

Imam Hasan(a.s) amesema: "Wa tisa kutoka katika kizazi cha ndugu yangu Husayn ni mwana wa bibi wa vijakazi, Mwenyezi Mungu atarefusha umri wake wakati wa ghaiba yake, kisha kwa uwezo wake atamdhihirisha akiwa katika sura ya ujana chini ya miaka arubaini, hilo ni ili Mwenyezi Mungu ajulikane kuwa ni Muweza juu ya kila kitu ."[43]

Imam As-Sadiq(a.s) amesema: "Lau angekuwa ametokeza Qaim basi watu wangemkanusha, kwa sababu atarejea kwao akiwa kijana aliyelingana ."[44]

Imepokewa ndani ya kitabu Kamalud-Din kutoka kwa Abu Swalti Al-Harawiy amesema: "Nilimwambia Ar-Ridha(a.s) : Ni zipi alama za Qaim kutoka kwenu pindi atakapodhihiri? Akasema:'Alama yake ni kiumri awe mzee lakini ni kijana kimuonekano kiasi kwamba mtazamaji atadhania kuwa ni mtu wa miaka arubaini au chini yake ."[45]

3 - NAFASI YA VIJANA KATIKA SERIKALI YA

BALOZI WA KWANZA WA MTUME (s.a.w.w) NI KIJANA

As'ad bin Zarara na Dhak'wan bin Abdu Qaysi walikuja kwa Mtume(s.a.w.w) Makka kabla ya kuhama kwake, na wao wawili walikuwa mabosi wa Madina, wakaingia kwa Mtume(s.a.w.w) wakati ambao Makka ilikuwa kipindi kigumu, wakasikiliza wito wake, kisha wakasilimu na kumwambia: "Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu! Tupe mtu atakayetufunza Qur'an na kuwalingania watu katika jambo lako." [46]

Hii ilikuwa ndio mara ya kwanza Madina ambayo ilikuwa ni mji mkubwa wenye tofauti nyingi kuomba mwakilishi wa Mtume(s.a.w.w) , kama ambavyo ilikuwa ndio mara ya kwanza Mtume(s.a.w.w) kutuma mwakilishi wake rasmi nje ya Makka, hivyo ilipasa kwa ajili ya jukumu hili zito la hatari amtume mtu mwenye sifa na uwezo unaohitajika. Ndipo Mtume(s.a.w.w) akamteua Masw'ab bin Umayri, naye alikuwa kijana mwerevu.

Mtume(s.a.w.w) akampa maelekezo Masw'ab bin Umayri akiwa bado kijana kabisa na akamwamuru aende na As'ad, na Masw'ab alikuwa tayari ameshajifunza sehemu kubwa ya Qur'an.[47]

Akaondoka kijana huyu aliyejaa roho ya imani na ujana, akatekeleza jukumu lake na kusimamia kwa namna nzuri zaidi, haukupita muda mrefu watu wa Madina wakaukubali wito wake bila kujali tofauti zao, na hasa vijana na watoto wao, wakasilimu na Masw'ab akawaswalisha Swala ya Ijumaa, nayo ndio ya kwanza ya Ijumaa iliyoswaliwa Madina. Yeye ndiye wa kwanza aliyekusanya watu kwa ajili ya Ijumaa huko Madina, na mikononi mwake wakasilimu Asidu bin Hadhir na Saad bin Muadh. Hilo linatosha kuwa fahari na athari ndani ya Uisilamu.[48]

Imepokewa ndani ya kitabu Biharul-An'war: "Masw'ab alifikia kwa As'ad bin Zurara, na alikuwa kila siku anatoka na kutembelea vikao vya mak- hazraji akiwalingania waingie kwenye Uislamu, na hapo vijana wanamkubali ."[49]

GAVANA WA KWANZA WA MAKKA NI KIJANA WA MIAKA ISHIRINI NA MOJA

Baada tu ya Mtume(s.a.w.w) kulikomboa Jiji la Makka zikajitokeza alama za kuja vita vya Hunayni baada ya muda mfupi, hapo Mtume(s.a.w.w) hakuwa na jingine ila ni kuandaa jeshi lake na kulitenga nje ya Makka ili kujiandaa na mapambano. Upande mwingine alikuwa analazimika Makka ambayo punde tu ameikomboa kutoka mikononi mwa mushrikina, kuiachia gavana mwenye uwezo wa kuendesha mambo ipasavyo, na hasa ukizingatia wakati huo ilikuwa ndio kituo kikuu cha Bara la Uarabu na ndio mwelekeo wa macho ya makabila na watu wote kwa ujumla, zaidi ya hapo ni kuwa ugavana huu utazuia jaribio lolote la mushrikina la kuvunja amani na uhuru wa Makka.

Hivyo Mtume(s.a.w.w) akamteua kijana wa miaka ishirini na moja kwa ajili ya jukumu hili zito na la hatari, naye ni Uttab bin Usaydu, akamkabidhi na kumwandikia hati ya ugavana wake: "Mtume (s.a.w.w) amempa ugavana Uttab bin Usaydu akiwa na umri wa miaka ishirini na moja, amempa utawala wa Makka na amemwamuru awasalishe watu. Naye ndiye gavana wa kwanza anayeswalisha jamaa Makka baada ya ukombozi wa Makka ." [50]

Kisha(s.a.w.w) akamwelekea Uttab na kumbainishia hatari ya jukumu hili zito akasema: "Ewe Uttab! Unajua nimekupa utawala uwatawale kina nani? Nimekupa utawala uwatawale watu wa Mwenyezi Mungu, na laiti ningejua wana mtu mwenye kheri kuliko wewe basi ningempa awatawale. " [51]

Katika hali ya kawaida ni lazima hati kama hii ingezua dukuduku la watu wa Makka na viongozi wao, ndipo Mtume(s.a.w.w) akaandika hati ndefu ili kuzuia upinzani wao, mwishoni akasema: "Wala yeyote mwenye hoja miongoni mwenu asimwasi kwa hoja ya udogo wa umri, kwani mkubwa si mbora, bali mbora ndiye mkubwa. " [52]

Uttab bin Usayd alibaki kama gavana wa Makka mpaka mwisho wa uhai wa Mtume(s.a.w.w) , na alitawala na kuongoza vizuri. Kiongozi wa vita vya Rum ni kijana wa miaka kumi na nane: Mtume(s.a.w.w) mwishoni mwa uhai wake aliandaa jeshi ili kuupiga utawala wa nchi kubwa ya Rum, wakajiunga na jeshi hili la waislamu sahaba wakubwa na watu maarufu miongoni mwa muhajirina na answari.

Na ni wazi kuwa ilikuwa inapasa jeshi hili aliweke chini ya uongozi wa viongozi wenye uwezo, hivyo akaliweka chini ya uongozi wa Usama bin Zaydi, na kipindi hicho alikuwa na umri wa miaka kumi na nane.[53]

Sahaba wakapinga uamuzi huu katika mazingira tete kama hayo,[54] wakatoa yaliyomo nyoyoni mwao na kutandaza ndimi zao kwa kusema: "Hivi kijana huyu anapewa uongozi juu ya muhajirina wa mwanzo?!!"[55] Mtume(s.a.w.w) alipolisikia hilo alitoka akichechemea mpaka mimbarini akiwa na ghadhabu, baada ya kumuhimidi na kumshukuru Allah akasema: "Watu wamekosoa uteuzi wa uamiri wa Usama, na tayari walikuwa wamekosoa uteuzi wa uamiri wa baba yake kabla ya hapo, na hakika wao wawili wanafaa kabisa kwa uamiri huo, na wao wawili ni watu niwapendao sana, nawausia kheri kwa Usama ." [56]

NAFASI YA VIJANA KATIKA SERIKALI YA IMAM WA ZAMA ZETU

1. Imam Ali(a.s) amesema: "Wafuasi wa Mahdi (a.s) ni vijana, hatokuwa na wazee ila kama wanja ndani ya jicho na chumvi kwenye mahitaji ya safari, na mahitaji machache mno ni chumvi ."[57]

2. Imam As-Sadiq(a.s) amesema: "Vijana wa Kishi'a watakuwa wamelala juu ya migongo ya mikeka yao, ghafla atawafikia Imam wao ndani ya usiku mmoja bila kutangulia ahadi, kisha wataamka wakiwa Makka. "[58]