JOHARI ZA HEKIMA KWA VIJANA

JOHARI ZA HEKIMA KWA VIJANA0%

JOHARI ZA HEKIMA KWA VIJANA Mwandishi:
: HEMEDI LUBUMBA SELEMANI
Kundi: Vitabu mbali mbali

JOHARI ZA HEKIMA KWA VIJANA

Mwandishi: Muhammad Reyshahri
: HEMEDI LUBUMBA SELEMANI
Kundi:

Matembeleo: 14487
Pakua: 2340

Maelezo zaidi:

JOHARI ZA HEKIMA KWA VIJANA
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 11 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 14487 / Pakua: 2340
Kiwango Kiwango Kiwango
JOHARI ZA HEKIMA KWA VIJANA

JOHARI ZA HEKIMA KWA VIJANA

Mwandishi:
Swahili

2

JOHARI ZA HEKIMA KWA VIJANA

3 - UHUSIANO NA MWENYEZI MUNGU

THAMANI YA IBADA KATIKA KIPINDI CHA UJANA

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Ubora wa kijana ambaye anajishughulisha na ibada ujanani juu ya mzee ambaye ana- jishughulisha na ibada baada ya miaka yake kukua ni sawa na ubora wa Mitume juu ya watu wengine ." [127]

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Mwenyezi Mungu asema: 'Kijana mwenye kuamini kadari Yangu, mwenye kuridhia Kitabu Changu, mwenye kutosheka na riziki Yangu na mwenye kuachana na mata- manio yake kwa ajili Yangu, yeye Kwangu ni sawa na baadhi ya malaika Wangu ." [128]

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Hakika Mwenyezi Mungu humpenda kijana ambaye anaumaliza ujana wake katika kumtii Mwenyezi Mungu ." [129]

Imam Al-Baqir(a.s) amesema: "Ibrahim aliamka akaona mvi moja kwenye ndevu zake, akasema: 'Kila sifa njema ni ya Mwenyezi Mungu, Ambaye amenifikisha kiwango hiki huku nikiwa sijamwasi Mwenyezi Mungu hata kidogo ."[130]

Mwenyezi Mungu hujifakharisha kupitia ibada ya kijana: Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Hakika Mwenyezi Mungu hujifakharisha kwa malaika kupitia kijana mfanya ibada, huwaam- bia: Mtazameni mja Wangu! Ameacha matamanio yake kwa ajili Yangu ." [131]

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Hakuna kijana yeyote anayeacha ladha ya dunia na matamanio yake, na kuelekea kumtii Mwenyezi Mungu kwa ujana wake ila ni lazima Mwenyezi Mungu atam- pa ujira wa wasema kweli sabini na mbili ."

Kisha akasema:'Mwenyezi Mungu husema: Ewe kijana mwenye kuacha matamanio yake kwa ajili Yangu, mwenye kuutumia ujana wake kwa ajili Yangu, wewe kwangu ni sawa na baadhi ya malaika wangu ."[132]

Imam As-Swadiq(a.s) amesema: "Kiumbe apendwaye sana na Mwenyezi Mungu ni kijana chipukizi wa miaka aliye katika sura nzuri, ambaye ameuweka ujana wake na uzuri wake katika kumtii Mwenyezi Mungu. Huyo ndiye ambaye Mwenyezi Mungu hujifakharisha mbele ya malaika kupitia yeye kwa kuwaambia: Huyu ndiye mja Wangu kweli ."[133]

BARAKA ZA IBADA YA UJANANI

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Atakaemwabudu Mwenyezi Mungu kwa ufanisi ujanani mwake, Mwenyezi Mungu atampa hekima ujanani . Mwenyezi Mungu asema: " Na alipofikia baleghe yake na akastawi, tulimpa hukumu na elimu na hivyo ndivyo tunavyowalipa wenye kufanya mema ." (Surat Al-Qasas: 14).

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Watu wa aina saba Mwenyezi Mungu atawafunika kwa kivuli chake siku ambayo hakuna kivuli ila kivuli Chake tu: Imam mwadilifu na kijana aliyekulia katika ibada ya Mwenyezi Mungu.. "[134]

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Chipukizi yeyote atakayekulia katika elimu na ibada mpaka akawa mtu mzima, Mwenyezi Mungu atampa siku ya Kiyama thawabu za wasema kweli sabini ."[135]

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Ewe Abu Dhari! Hakuna kijana yeyoye anayeiacha dunia na matamanio yake kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, na kuumaliza ujana wake katika kumtii Mwenyezi Mungu ila ni lazima Mwenyezi Mungu atampa ujira wa wasema kweli sabini na mbili ." [136]

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Mbora katika umma wangu ni yule mwenye kuuponda ujana wake katika kumtii Mwenyezi Mungu, na kuitenga nafsi yake na ladha za dunia na kuifunganisha na akhera, hakika malipo yake juu ya Mwenyezi Mungu ni daraja ya juu kabisa ya Pepo ." [137]

Imam As-Sadiq(a.s) amesema: "Watu wa aina tatu Mwenyezi Mungu atawaingiza peponi bila hesabu..Imam mwadilifu, mfanyabiashara mkweli na mzee aliemaliza umri wake katika kumtii Mwenyezi Mungu ."[138]

MAANA YA IBADA

Imepokewa ndani ya kitabu Muhjjatul-Baydhai kuwa: "Siku moja Mtume wa Mwenyezi Mungun (s.a.w.w) alikuwa ameketi na sahaba zake, akam- tazama kijana shupavu mwenye nguvu ametangulia akitembea kwa juhudi, wakasema: 'Tazama huyu, kwa nini asiutumie ujana wake na ushupavu wake katika njia ya Mwenyezi Mungu?' Mtume wa Mwenyezi Mungu akasema: 'Msiseme hivyo, kwani ikiwa yeye anafanya juhudi kwa ajili ya nafsi yake ili aizuie isiombeombe na isiwahitajie watu, basi yeye yupo katika njia ya Mwenyezi Mungu. Na ikiwa anafanya juhudi kwa ajili ya wazazi wake wawili madhaifu au kizazi chake dhaifu ili awatosheleze na kuwatimizia mahitaji yao, basi yeye yuko katika njia ya Mwenyezi Mungu. Na ikiwa anafanya juhudi ili ajifakharishe na kujigamba kwa wingi wa mali, basi yeye yupo katika njia ya shetani ."[139]

WASTANI KATIKA IBADA

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Dini hii ni nzito, basi iingieni kwa wepesi, wala msilazimishe ibada za Mwenyezi Mungu kwa waja wa Mwenyezi Mungu, mkaja kuwa kama mpandaji aliyepanda ambaye hana safari aliyoisafiri wala mgongo alioubakisha ." [140]

Imam As-Sadiq(a.s) amesema: "Nilifanya juhudi katika ibada nami nikiwa bado kijana, ndipo baba yangu akaniambia: 'Ewe Mwanangu mpendwa! Punguza ninachokuona ukifanya, kwani hakika Mwenyezi Mungu ampendapo mja humridhia kwa kichache ."[141]

4 - RAFIKI MWEMA

NAFASI YA RAFIKI MAISHANI

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Mtu huwa katika dini ya rafiki yake, basi mmoja wenu achunguze ni yupi anayemfanya kuwa rafiki yake ." [142]

Imam Ali(a.s) amesema: "Aliye madhubuti ni yule mwenye kupata kheri kwa urafiki wake, kwani hakika mtu hupimwa kupitia rafiki yake ."[143]

Imam Ali(a.s) amesema: "Urafiki una majuto ila kwa walio wachamungu ."[144]

Imam Ali(a.s) amesema: "Rafiki wa mtu ni dalili ya akili yake ."[145]

Imepokewa kuwa Sulayman(a.s) alisema: "Msimhukumu mtu kwa chochote mpaka mchunguze husuhubiana na nani, kwani hakika mtu hujulikana kupitia wenzi wake na marafiki wake, na hunasibishwa kwa sahiba zake na wapambe wake ."[146]

KUMJARIBU RAFIKI

Imam Ali(a.s) amesema: "Kumwamini kila mtu kabla ya kumjaribu ni dalili ya kushindwa ."[147]

Imam Ali(a.s) amesema: "Tangulizeni majaribio na fanyeni juhudi katika uchunguzi wakati wa kuchagua ndugu, la sivyo utalazimika kufanya urafi- ki na waovu. "[148]

Imam Ali(a.s) amesema: "Akili za watu hujaribiwa kwa mambo sita: Urafiki, muamala, utawala, kuvuliwa madaraka, utajiri na ufakiri ."[149]

Imam Ali(a.s) amesema: "Watu hawajulikani ila kwa majaribio, basi mjaribu mkeo na wanao katika ghaibu yako, rafiki yako katika msiba wako, mwenye ukaribu na wewe katika ukata wako na mwenye mapenzi na wewe wakati wa kutengana naye, ili ujue ni ipi nafasi yako kwao ."[150]

Imam As-Sadiq(a.s) amesema: "Msimuone mtu kuwa ni rafiki mpaka mumjaribu kwa mambo matatu: "Mghadhibishe uone ghadhabu zake je zitamtoa kwenye haki hadi kwenye batili, na wakati wa dinari na dirhamu (Dola na shilingi), na mpaka usafiri naye ."[151]

AINA ZA MARAFIKI

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Zama za mwisho kutakuwa na watu, wao ni marafiki kwa nje na maadui kwa ndani." Akaambiwa: 'Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, hiyo inakuwaje?' Akasema: 'Hiyo ni kwa kupendana wao kwa wao na kuogopana wao kwa wao. " [152]

Imam Ali(a.s) amesema: "Marafiki zako ni wa aina tatu na maadui zako ni wa aina tatu: Marafiki zako ni rafiki yako, rafiki wa rafiki yako na adui wa adui yako. Na maadui zako ni adui yako, adui wa rafiki yako na rafiki wa adui yako ."[153]

Imam Al-Baqir(a.s) amesema: "Mtu mmoja huko Basra alisimama kwa kiongozi wa waumini na kumwambia: 'Ewe kiongozi wa waumini tupe habari kuhusu ndugu.' Akasema: 'Ndugu wana namna mbili: Ndugu wa kweli na ndugu wa uongo. Ama ndugu wa kweli wao ndio uwezo, rafiki, ndugu na mali. Ukiwa na imani na ndugu yako basi jitolee kwake mali yako na mwili wako, msafie nia aliyemsafia nia na mfanyie uadui aliyemfanyia uadui, mfichie siri yake na aibu yake na mdhihirishie wema. Na jua ewe muulizaji hakika wao ni wachache kuliko madini ya kibiriti chekundu. Ama ndugu wa uongo, hakika wewe utapata ladha yako (manufaa) kutoka kwao, hivyo usilikatishe hilo kutoka kwao, na wala usitafute yaliyo nyuma ya hayo kutoka katika dhamiri zao, na wape ucheshi wa uso na utamu wa ulimi kama walivyokupa ."[154]

Imam As-Sadiq(a.s) amesema: "Ndugu wana namna tatu: Mmoja ni kama chakula ambaye anahitajika kila wakati, naye ni yule mwenye akili. Wa pili ni sawa na ugonjwa naye ni yule mpumbavu. Na wa tatu ni sawa na dawa naye ni yule mwerevu ."[155]

MARAFIKI BORA

Amesema Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) : "Ndugu bora ni yule mwenye kukusaidia katika amali za Akhera ." [156]

Amesema Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) : "Aliye bora kati ya ndugu zako ni yule anayekusaidia katika kumtii Mwenyezi Mungu, anayekuzuia kumwasi Mwenyezi Mungu na anayekuamuru kumridhisha ." [157]

Amesema Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) : "Mbora kati ya ndugu zenu ni yule mwenye kuwazawadieni (kukujulisheni) aibu zenu ." [158]

Alipoulizwa: Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu ni yupi aliye mbora kukaa naye? Akasema: "Ni yule ambaye kumtazama kwake kunawakumbusha Mwenyezi Mungu, kuongea kwake kunawaongezea elimu na matendo yake yanawakumbusha Akhera ."[159]

Amesema Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) : "Wanafunzi wa Isa walimuuliza: 'Ewe roho wa Mwenyezi Mungu, tukae na nani?' Akasema: 'Yule ambaye kumtazama kwake kunawakumbusha Mwenyezi Mungu, kuongea kwake kunawaongezea elimu, na matendo yake yanawaraghibisha Akhera ." [160]

Imam Ali(a.s) amesema: "Ndugu bora ni yule aliye mchache wa hadaa katika nasaha ."[161]

Imam Ali(a.s) amesema: "Ndugu bora ni yule ambaye mapenzi yake ni kwa ajili ya Mwenyezi Mungu ."[162]

Imam Ali(a.s) amesema: "Ubora wa kila kitu ni upya wake, na ndugu bora ni wa zamani ."[163]

Imam Al-Baqir(a.s) amesema: "Mfuate anaekuuliza ilihali akikunasihi, wala usimfuate anayekuchekesha ilihali akikuhadaa ."[164]

Imam As-Sadiq(a.s) amesema: "Shikamana na rafiki wa zamani kwani kila mpya hana ahadi na uaminifu, wala dhima na mkataba. Na chukua tahadhari sana dhidi ya yule uliye na imani naye sana, kwani watu ni maadui wa neema ."[165]

Imam Al-Askar(a.s) amesema: "Ndugu aliye bora kwako ni yule aliyesa- hau makosa yako na akakumbuka ihsani yako kwake ."[166]

Imam Hasan(a.s) amesema: "Mtume(s.a.w.w) aliulizwa: 'Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu ni yupi rafiki bora?' Akajibu: 'Rafiki ambaye unapomkumbuka Mwenyezi Mungu anakusaidia na unapomsahau anakukumbusha.' Wakamwambia: 'Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, tuonyeshe aliye mbora kwetu ili tumfanye rafiki na mtu wa kukaa naye.' Akasema: 'Ndio, yule ambaye akitazamwa Mwenyezi Mungu hukumbukwa."[167]

HAKI YA MWENZI WAKO

Imam Zaynul-Abidina(a.s) amesema: "Ama haki ya mwenzi wako uliyekaa naye ni uwe mpole kwake na kumfanyia insafu katika utamshi wa lafudhi. Usisimame toka ulipokaa ila kwa idhini yake, na aliyekaa kwako anaruhusiwa kusimama toka kwako bila idhini yako. Sahau makosa yake na hifadhi kheri zake na wala usimsikilizishe ila kheri ."[168]

5 - MAHITAJI YA HALALI NA NGUVU ZA MWILI

NGUVU ZA MWILI ZASIFIWA

Mwenyezi Mungu amesema: "Na Nabii wao akawaambia: Hakika Mwenyezi Mungu amewawekea Taalut kuwa ni mfalme juu yenu. Wakasema: 'Atakuwaje yeye na ufalme juu yetu na sisi tuna haki zaidi ya ufalme kuliko yeye wala hakupewa wasaa wa mali?' Akasema: Hakika Mwenyezi Mungu amemchagua juu yenu na amemzidishia wasaa wa elimu na kiwiliwili. Na Mwenyezi Mungu huumpa ufalme wake amtakaye na Mwenyezi Mungu ni Mwenye wasaa Mwenye kujua ." (Al-Baqarah: 247).

Mwenyezi Mungu amesema tena: "Ewe Yahya! Shika Kitabu kwa nguvu, na tukampa hekima angali mtoto ." (Surat Maryam: 12).

Imepokewa kutoka kwa Is'haqa bin Ammar amesema: "Nilimuuliza Abu Abdullah kuhusu kauli ya Mwenyezi Mungu: "Chukueni tulichowapa kwa nguvu ." Je ni nguvu za mwili au nguvu za roho? Akasema:'Ni zote mbili ."[169]

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Ni uzuri kwa aliyesil- imu maisha yake yawe yamtosheleza na nguvu yake iwe imara ." [170]

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Muumini mwenye nguvu ni bora kuliko muumini dhaifu, na katika kila kheri ." [171]

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Ndani ya sahifa ya Ibrahim mlikuwa na: 'Na mwenye akili anapokuwa hajashindwa kiakili awe na saa: Saa humo anamnong'oneza Mola wake Mlezi. Saa anaitath- mini nafsi yake. Saa humo anatafakari kuhusu ihsani aliyofanyiwa na Mwenyezi Mungu na saa anakaa faragha na kuiepusha nafsi yake na halali, kwani saa hii ni msaada wa saa zile na ni kuuimarisha moyo na kuupumzisha ." [172]

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Inapasa kwa mwenye akili ikiwa kweli ana akili awe na saa nne mchana: Saa humo anamnong'oneza Mola wake Mlezi. Saa anaitathmini nafsi yake. Saa anawaen- dea wenye elimu na wanamfumbua macho katika dini yake na kumnasihi na saa anakaa faragha na kuiepusha nafsi yake na ladha miongoni mwa mambo ya dunia, yaliyo halali na jamali ." [173]

Imam Ali(a.s) amesema: "Ewe Mola Mlezi! Ewe Mola Mlezi! Vipe viun- go vyangu nguvu katika kukutumikia, na imarisha azima yangu ."[174]

Imam Ali(a.s) amesema: "Muumini ana saa tatu: Saa humo anamnong'oneza Mola wake Mlezi. Saa anatafuta maisha yake na saa anaie- pusha nafsi yake na ladha zilizo halali na jamali ."[175]

Imam As-Sadiq(a.s) amesema: "Na miongoni mwa hekima za jamaa wa Daud ilikuwa ni: Ni lazima kwa mwislamu mwenye akili awe na saa anayoimalizia kati yake na Mwenyezi Mungu kwa amali. Saa anakutana na ndugu zake anaowazunguka na wanaomzunguka katika jambo la Akhera yake. Na saa anaiepusha nafsi yake na ladha katika mambo yasiyo ya hara- mu, kwani yenyewe ndio msaada kwa saa hizo nyingine ."[176]

Imam Al-Kadhim(a.s) : "Jitahidini katika zama zenu muwe na saa nne: Saa kwa ajili ya kumnong'oneza Mwenyezi Mungu. Saa kwa ajili ya mambo ya maisha. Saa ya kushirikiana na jamaa na waaminifu ambao wanawaonyesha aibu zenu na wanawasafia nia. Na saa ya kujiepusha na ladha zenu katika mambo yasiyokuwa ya haramu ."[177]

SABABU ZA MVUTO

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Kwa mambo matatu mwili hustawi na kuvutia: Manukato, mavazi mepesi na kuramba asali ." [178]

Imam Ali(a.s) amesema: "Manukato hufurahisha, asali hufurahisha, kutazama uoto kunafurahisha na kupanda kipando hufurahisha ."[179]

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Manukato hufurahisha, asali hufurahisha, kutazama uoto kunafurahisha na kupanda kipando hufurahisha ." [180]

Imam As-Sadiq(a.s) amesema: "Furaha hupatikana katika mambo kumi: Kutembea, kupanda, kupiga mbizi majini, kutazama uoto, kula na kunywa, kumtazama mwanamke mrembo, kujamiiana, kupiga mswaki, kuosha kichwa kwa mti wa khatami huko hamamu na kuongea na wanaume ."[181]

BURUDANI

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Burudikeni na chezeni kwani mimi nachukia kuona ususuavu ndani ya dini yenu ." [182]

Imepokewa kutoka kwa Abu Rafiu amesema: "Nilikuwa namchezesha Hasan bin Ali(a.s) kwa mchezo wa kumchenga akiwa angali mtoto, basi ninapomshika, namwambia nibebe, naye ananiambia: 'Ole wako je unau- panda mgongo ambao ameubeba Mtume wa Mwenyezi Mungu?' basi hapo namwacha. Na anaponishika namwambia sikubebi kama ambavyo hukunibeba. Basi ananiambia: 'Hivi huridhii kuubeba mwili ambao kaubeba Mtume wa Mwenyezi Mungu?' Basi hapo nambeba."[183]

MATEMBEZI

Imepokewa kutoka kwa Amru bin Hurayth amesema: "Niliingia kwa Abu Abdillah (a.s) naye akiwa nyumbani kwa ndugu yake Abdullah bin Muhammad, nikamwambia: 'Mimi ni fidia kwako, kitu gani kilichokuleta kwenye nyumba hii?' Akasema: 'Nimekuja kutembea ."[184]

Imepokewa kutoka kwa Ibrahim bin Abu Mahmud amesema: "Ridhaa(a.s) alituambia: 'Ni chachandu ipi inafaa kwa chakula?' Wenzi wetu wakesema: 'Nyama.' Wengine wakasema: 'Siagi.' Na wengine wakadai: 'Maziwa.' Yeye akasema:'Hapana! Bali ni chumvi. Tulitoka kwenda matembezini basi kijana wetu akasahau chumvi, basi huko wakatuchinjia kondoo mnono mno lakini hatukunufaika naye kwa chochote mpaka tukaondoka ."[185]

MIZAHA

Mtume wa Mwenyezi Mungu alikuwa anafanya mizaha lakini hasemi ila ukweli. Anas bin Malik alisema: "Amekufa Nughayru kwa Abu Umayru, naye ni mwana wa mama Sulaym." Basi Mtume(s.a.w.w) akawa anasema: "Ewe Abu Umayru Tughayru amefanya nini ." [186]

Mmoja kati ya wakeze(s.a.w.w) alikuwa na mfanyakazi anayeitwa Anjashatah (yaani mashine ya kusagia), basi Mtume(s.a.w.w) akawa anamwambia: "Ewe Anjashatah fanya urafiki na vigae ." [187]

Kuna mtu alimwambia Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) : "Nibebe ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu." Akamjibu: 'Nitakubeba juu ya mtoto wa ngamia.' Akasema: 'Nitamfanyia nini mtoto wa ngamia?' Akamjibu: 'Ngamia hazai ila mtoto wa ngamia ." [188]

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) alimwambia mwanamke aliyekuwa kamtaja mume wake: "Je ni yule mwenye weupe jichoni?" akasema: 'Hana weupe.' Basi alipokuja kumwambia mumewe, mume akamwambia: 'Hivi huoni kuwa weupe wa jichoni mwangu ni mkubwa kuliko weusi ." [189]

Ajuza mmoja kati ya Maanswari alisema kumwambia Mtukufu Mtume(s.a.w.w) : "Niombee Pepo." Mtume(s.a.w.w) akamwambia: "Peponi haingii ajuza ." Basi mwanamke yule akalia, ndipo Mtume akacheka na kumwambia: "Hivi hujasikia kauli ya Mwenyezi Mungu : " Hakika tumewaumba (wanawake ) kwa umbo (bora). Na tukawafanya ndio kwanza wanaolewa ." (Surat Al-Waqia: 35 - 36)."[190]

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) alimwambia ajuza wa Ashjaiyya: "Ewe Ashjaiyyah ajuza haingii peponi ." Ndipo Bilal akamuona akilia akaenda kumwambia Mtume(s.a.w.w) , Mtume akasema: "Na mweusi pia ." Basi wote wawili wakakaa wakilia. Ndipo Abbas akawaona na akaenda kumwambia Mtume(s.a.w.w) , Mtume akasema: "Na mzee pia ." Kisha akawaita wote na kuwaambia: Mwenyezi Mungu atawaumba kwa uzuri kama walivyokuwa."Na akawaambia kuwa wao wataingia Peponi wakiwa vijana wenye kung'aa kwa nuru na kuwa watu wa peponi ni weupe wenye kupakwa wanja ." [191]

Suwaybitu Al-Muhajiriyyu alimwambia Nuuman Al-Badriyyu: "Nilishe." Na alikuwa na chakula huku wakiwa safarini. Basi akamjibu: "Subiri mpaka waje jamaa." Basi wakawakuta jamaa, ndipo Suwaybitu akawaam- bia: "Mtamnunua mtumwa wangu kutoka kwangu?" wakasema: "Ndio." Akawaambia: "Yeye ni mtumwa mwenye maneno mengi, hivyo atawaam- bieni: Mimi ni muungwana, mkimsikiliza mtakuwa mmeniharibia mtumwa wangu dhidi yangu. Mnunueni kwa ngamia kumi." Basi wakaja na kutupia kamba shingoni mwake. Nuuman akasema: "Huyu anawafanyia mzaha, hakika mimi ni muungwana." Wakamwambia: "Tumeshasikia habari yako." Basi wakamchukua na kuondoka naye mpaka watu wengine walipowafuata na kumwokoa. Tangu kipindi hicho Mtume(s.a.w.w) akawa anacheka akumbukapo."[192]

Nuuman alimwona bedui akiwa na chupa ya asali akainunua na kuja nayo nyumbani kwa Aisha siku hiyohiyo, akamwambia ichukue, basi Mtume(s.a.w.w) akadhani amempa zawadi. Ghafla Nuuman na bedui wakapita mlangoni, basi bedui alipoona muda unazidi kwenda akamwambia Nuuman: "Nirudishie chupa yangu kama hujapata thamani yake." Ndipo Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) akawa amegundua kisa chote. Mtume akamwambia Nuuman: "Kitu gani kilichokupelekea kufanya hivi ulivyofanya?" Akajibu: "Niliona Mtume wa Mwenyezi Mungu anapenda asali na nikaona bedui ana chupa ya asali." Basi Mtume wa Mwenyezi Mungu akacheka na wala hakudhihirisha kuchukizwa. [193]

KUOGELEA NA KUTUPA MSHALE

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Burudani bora kwa muumini ni kuogelea ." [194]

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Wafunzeni wanenu kuogelea na kutupa mshale ." [195]

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Kati ya haki za mtoto kwa baba yake ni amfunze kuandika, kuogelea na kutupa mshale ." [196]

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Burudani ipendwayo sana kwa Mwenyezi Mungu ni kuwashindanisha ngamia na kutupa mshale ." [197]

Imepokewa kutoka kwa Sulayman At-Tamiymiy amesema: "Mtume wa Mwenyezi Mungu (s.a.w.w) alikuwa anafurahishwa na mtu kuwa mwoge- leaji mwenye kujua kutupa mshale ."[198]

MIELEKA

Hakika Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) alitoka siku moja kwenda Abtah, akamwona bedui akichunga kondoo na alikuwa akisifika kwa nguvu, basi bedui yule akamwambia Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) : "Je uko tayari tushindane mieleka?" Mtume(s.a.w.w) akamwambia: "Utanipa nini?" Akasema: "Mbuzi." Basi wakaanza miele- ka na ndipo Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) akambwaga chini. Bedui akasema: "Je uko tayari turudie tena?" Akamuuliza: "Utanipa nini?" Akajibu: "Mbuzi." Basi wakaanza mieleka na Mtume akambwaga tena chini. Bedui akasema: "Nifunze Uislamu, kwani hakuna yeyote aliyewahi kunibwaga zaidi yako." Basi akamsilimisha na akamrudishia mbuzi wake. [199]

Hakika Rukana bin Abdi bin Zayd bin Hashim alikuwa na nguvu sana miongoni mwa makurayshi, ndipo siku moja wakiwa kwenye bonde lisilokuwa na kitu Mtume akamwambia: "Ewe Rukanata hivi humwogopi Mwenyezi Mungu na kukubali ninayokulingania?" Akasema: "Lau mimi ningejua kuwa ni haki basi ningekufuata."

Mtume(s.a.w.w) akamwambia: "Hivi unaona ikiwa nikikubwaga utajua fika kuwa nisemayo ni haki?" Akasema: "Ndio." Basi akamwambia simama tushindane kwa mieleka. Basi Rukana akasimama na kushindana naye na hatimaye Mtume wa Mwenyezi Mungu akamshinda na kumbwaga chini. Basi wakarudia tena na Mtume akambwaga tena . [200]

Kiongozi wa waumini alishindana mieleka na mtu mmoja na hatimaye akambwaga chini. Basi mtu yule akamwambia Ali: "Ewe kiongozi wa waumini Mwenyezi Mungu akuimarishe." Ali akamwambia:"(Akiimarishe) Kifua chako ."[201]

MASHINDANO

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Malaika hawashududii chochote kati ya burudani zenu ila mashindano ya ngamia na utupaji wa mishale ." [202]

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Mashindano ya ngamia hufurahisha ." [203]

Imam Ali(a.s) amesema: "Isma'il na Is'haq walipofikia ujana walishin- dana na hatimaye Ismail akashinda, basi Ibrahim akamchukua na kumuweka mapajani mwake na akamkalisha Is'haqa pembeni mwake ."[204]

Imam Ali(a.s) amesema: "Mtume wa Mwenyezi Mungu aliruhusu kushindanisha ngamia na yeye alishindanisha, na katika hilo akaweka zawadi ya wakia za madini ya fedha ."[205]

Imam Muhammadi Al-Baqir amesema: "Mtume wa Mwenyezi Mungu alimshindanisha ngamia ambaye alipunguzwa uzito toka Al-Hayfau hadi msikiti wa Bani Zurayqi, na alimshindanisha kwa makole matatu ya tende, basi akampa mshindi kole, na akampa mwenye kusali kole na wa tatu kole ."[206]

Ibnu Umar amesema: "Mtume wa Mwenyezi Mungu alishindanisha kati ya ngamia, basi yule aliyekuwa amepunguzwa uzito alimshindanisha toka huko Al-Hayfau mpaka Thaniyatul-Wadai, na yule aliyekuwa hajapunguzwa uzito akamshindanisha toka Thaniyatul-Wadai mpaka msikiti wa Bani Zurayqi. Abdullah anasema:'Siku hiyo nilikwa nikimkimbiza farasi basi nikawashinda watu na ndipo farasi wa msikiti wa Bani Zurayqi akawa sawa na mimi ."[207]

Imepokewa kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) alipita na kuwakuta vijana wa kianswari wakishindana kutupa mishale, basi Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) akasema: "Mimi niko kwenye kundi ambalo yumo mtoto wa Adrai." Basi kundi la pili likaacha kutupa na likasema: "Halitoshindwa kundi ambalo yumo Mtume wa Mwenyezi Mungu." Mtume akasema: "Tupeni bila shaka mimi nitatupa pamoja nanyi." Basi akatupa kwa kushiriki kwenye kila kundi dhidi ya jingine, basi hatimaye hakuna aliyeshinda. Wakaendelea kushindana wao, watoto wao hadi wajukuu zao lakini hakuna walioshinda." [208]

Abu Lubayd amesema: "Ibnu Malik aliulizwa: 'Je mlikuwa mnashindana kwa kuweka zawadi zama za Mtume wa Mwenyezi Mungu?' Akasema:'Ndio Mtume wa Mwenyezi Mungu alismshindanisha farasi wake kwa kuweka zawadi, basi akashinda na akafurahishwa kwa hilo ."[209]

6 - THAMANI YA TABIA NJEMA NA MATENDO MEMA

KUACHA MAASI

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Atakaetoka kwenye udhalili wa kumuasi Mwenyezi Mungu hadi kwenye heshima ya kumtii Mwenyezi Mungu basi Mwenyezi Mungu atamliwaza bila kuwepo mlewezeshaji na atampa auni bila mali ." [210]

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Mtu hawi ni mwenye uwezo wa kutenda haramu kisha akaacha kwa ajili ya kumwogopa Mwenyezi Mungu ila ni lazima Mwenyezi Mungu atampa badala hapa duniani kabla ya Akhera kwa kumpa kilicho bora kuliko hicho ." [211]

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Itakapofika Siku ya Kiyama baadhi ya watu toka katika umma wangu Mwenyezi Mungu atawaoteshea mbawa, na hapo wataruka toka makaburini mwao mpaka Peponi, watatembea humo na kustarehe watakavyo. Basi Malaika watawaambia: Je mmeona heasabu? Watasema: Hatujaona hesabu. Watawaambia: Je mmevuka Sirat? Watasema: Hatujaiona Sirat. Watawaambia: Je mmeona Jahannam? Watasema: Hatujaona chochote. Malaika watawauliza: Ninyi ni kutoka umma wa nani? Watasema: Ni kutoka umma wa Muhammad. Watawaambia: Tunawaapisha kwa Mwenyezi Mungu, hebu tusimulieni ni amali gani mlikuwa mkiifanya duniani? Watasema: Tulikuwa na sifa mbili basi Mwenyezi Mungu kwa rehema Zake akatufikisha katika hadhi hii. Watawaambia: Ni zipi hizo? Watasema: Tulikuwa tuwapo faragha huona haya kumwasi Mwenyezi Mungu, na tunaridhia kwa kidogo tulichopewa. Basi Malaika watawaambia: Hadhi hii ni haki yenu."[212]

TOBA

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Toba ni nzuri lakini kwa vijana ni nzuri zaidi ." [213]

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Hakuna kitu kipendwacho zaidi na Mwenyezi Mungu kama kijana mwenye kutubu. Na hakuna kitu kimchukizacho mno Mwenyezi Mungu kama mzee mwenye kuendelea ndani ya maasi ." [214]

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Hakika Mwenyezi Mungu Mtukufu humpenda sana kijana mwenye kutubu ." [215]

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Mwenyezi Mungu hufurahishwa sana na toba ya mja wake kuliko mgumba aliyezaa na mpotevu aliyepata na mwenye kiu aliyekata kiu ." [216]

Imam Ali(a.s) amesema: "Ukifanya kosa fanya haraka kulifuta kwa kutubia ."[217]

Abu Basir amesema: "Nilikuwa nina jirani alikuwa ni mpambe wa mtawala basi akawa amepata mali, akaandaa mabinti wanenguaji na alikuwa anawakusanya kwake anakunywa pombe na kuniudhi, basi nikam- lalamikia hilo zaidi ya mara moja lakini hakujali. Basi nilipomsisitizia hilo akaniambia: 'Ewe ndugu mimi ni mtu mwenye maradhi na wewe ni mtu mwenye afya njema, natamani lau kama ungepeleka tatizo langu kwa rafi- ki yako, nataraji Mwenyezi Mungu ataniokoa kupitia kwako.' Basi hilo likakaa moyoni mwangu na nilipokwenda kwa Abu Abdillah nilimuelezea hali yake, naye akaniambia: 'Utakaporejea huko Kufa atakujia basi mwambie: "Jafar bin Muhammad anasema: 'Acha uliyonayo nakudhamini Pepo toka kwa Mwenyezi Mungu.' Basi niliporejea Kufa alinijia akiwa miongoni mwa walionijia, nikamzuia mpaka nyumba yangu ilipobaki faragha, ndipo nikamwambia: 'Ewe ndugu yangu mimi nimekutaja mbele ya Abu Abdullah Jafar bin Muhammad As- Sadiq(a.s) akaniambia: "Utakaporejea Kufa atakujia basi mwambie: 'Jafar bin Muhammad anakwambia: 'Acha uliyonayo ninakudhamini pepo toka kwa Mwenyezi Mungu.' Amesema: Basi akalia kisha akaniambia: 'Wallahi ni kweli Abu Abdullah kakwambia haya?' Nikamwapia kuwa hakika ameniambia niliyokuwambia. Akasema: 'Inatosha na imekwisha." Baada ya siku alini- tumia mtu akiniita ghafla nikamkuta nyuma ya nyumba yake akiwa uchi, akaniambia: 'Ewe Abu Basir, wallahi sijabakiwa na chochote nyumbani mwangu ila nimekitoa na nimebaki kama unionavyo. Akasema: 'Ndipo nikaenda kwa baadhi ya ndugu zetu nikakusanya kiasi kilichoweza kumvisha, kisha hazikupita siku nyingi akawa amenitumia mtu kuwa mimi ni mgonjwa njoo kunitazama. Nikawa nakwenda kwake mara kwa mara kumtibu, na hata alipofikwa na mauti nilikuwa nimekaa kwake akiwa anahangaika na nafsi yake na ndipo akazimia na kisha akazinduka na kuniambia: 'Ewe Abu Basira rafiki yako amenitekelezea ahadi aliyoahidi.' Nilipohiji nilikwenda kwa Abu Abdullah(a.s) nikamwomba ruhusa na nilipoingia yeye alianza kuniambia toka ndani ya nyum- ba huku mguu wangu mmoja ukiwa kizingitini na mwingine ukiwa nje: 'Ewe Abu Basira tumeshamtekelezea rafiki yako."[218]

Abu Nasri Bishru bin Al-Harith bin Abdu-Rahman mwenye asili ya Al- Marawaziyu aliyekuwa akiishi huko Baghdad, mwanairfani na mtawa ambaye ni mmoja wa nguzo za mfumo wa utawa. Inasemekana kuwa alikuwa mmoja wa watoto wa Marais na maafisa wa serikali, naye alikuwa kati ya watu wa anasa na miziki.

Inasemekana kuwa sababu kubwa ya kutubu kwake ni kwamba Maulana Imam Musa bin Jafar(a.s) alipita nyumbani kwake huko Baghadad akasikia miziki na sauti za nyimbo huku fujo ikitoka ndani ya nyumba hiyo, ghafla akatoka mtumwa wa kike huku mkononi akiwa na uchafu akautupa jalalani na ndipo Imam(a.s) akamwambia: "Ewe binti! Je mwenye nyumba hii ni muungwana au mtwana?" Akajibu: "Hapana ni muungwana." Imam akasema: "Umesema kweli kwani angekuwa ni mtwana basi angemuogopa bwana wake." Basi aliporejea ndani bwana wake akamwambia akiwa yuko kwenye meza ya vileo: "Kitu gani kilichokuchelewesha?" Akajibu: "Mtu mmoja ameni- ambia kadha wa kadha." Ndipo akatoka akiwa peku mpaka akamkuta maulana Al-Kadhim(a.s) akatubu mikononi mwake na kuomba msamaha na akalia mbele yake kwa kuona haya kutokana na amali zake."[219]

Imam Jafar As-Sadiq(a.s) amesema: "Kulikwa na mchamungu mmoja zama za Bani Israil alikuwa hajajichumia chochote kati ya mambo ya dunia, basi Ibilisi akapuliza mluzi na kuwakusanya askari wake kwake, akawaambia: Nani atamrubuni fulani? Mmoja akasema: Mimi nitamrubuni. Akamuuliza: Utamwendea kwa kitu gani? Akasema: Nitatumia wanawake. Akamwambia: Humuwezi, hajawahi kuwagusa wanawake. Mwingine akasema: Mimi hapa nitamrubuni. Akamuuliza: Utamwendea kwa kitu gani? Akasema: Nitatumia vileo na starehe. Akamwambia: Humuwezi, huyu harubuniwi kwa hivi. Mwingine akasema: Mimi hapa nitamrubuni. Akamuuliza: Utamwendea kwa kitu gani? Akasema: Nitatumia mema yake. Akamwambia: Nenda wewe ndiye utakayemuweza.

Basi akaenda mpaka alipokuwepo mtu yule, akasimama usawa wake huku akisali basi mtu yule alikuwa analala lakini shetani halali, anapumzika na shetani hapumziki, ndipo mtu yule alipomgeukia (shetani) huku akiwa anaona amali yake ni ndogo na nafsi yake imeshindwa, akamwambia: "Ewe mja wa Mwenyezi Mungu ni kupitia kitu gani umepata nguvu za kuswali swala hii?" Lakini shetani hakumjibu kitu. Akarudia tena na ndipo akamjibu kwa kusema: "Hakika mimi nilitenda dhambi nami hapa ninatubia, hivyo ninapoikumbuka dhambi hiyo napata nguvu za kuswali." Yule mtu akamwambia: "Niambie hiyo dhambi yako ili niitende na nitubie, kwani nikiifanya nitakuwa napata nguvu za kuswali." Akamwambia: Nenda mjini na muulizie malaya fulani, mpe dirhamu mbili na ujamiiane naye." Akasema: "Nitazipata wapi hizo dirhamu mbili na wala sijui ni nini dirhamu mbili?" Ndipo shetani akazitwaa toka chini ya unyayo wake na kumpa. Basi mtu yule akaingia mjini akiwa na joho lake huku akiuliza nyumba ya malaya fulani, basi watu wakamwelekeza ilipo wakidhani kuwa amekuja ili kumpa mawaidha, basi walipomwelekeza akamwendea na kumtupia ndowano ya dirhamu mbili, akamwambia simama, akasimama na kuingia nyumbani mwake. Mwanamke akamwambia: "Ingia lakini wewe umekuja katika namna ambayo huwa siijiwi kwa namna hiyo, nipe habari zako." Basi akampa habari na ndipo malaya yule akamwambia: "Ewe mja wa Mwenyezi Mungu! Kuacha dhambi ni rahisi kuliko kutafuta toba na wala si kila atafutaye toba huipata. Na ni lazima huyo alikuwa ni shetani aliye- jimithili kwako, ondoka hakika wewe hutoona kitu." Basi akaondoka na usiku uleule mwanamnke yule akafariki, basi walipoamka asubuhi watu wakakuta juu ya mlango wake kumeandikwa: "Hudhurieni msiba wa fulani kwani hakika yeye ni miongoni mwa watu wa peponi." Watu wakaingiwa na shaka wakakaa siku tatu bila kumzika wakiwa na shaka kuhusu jambo lake. Ndipo Mwenyezi Mungu akafunua ufunuo kwa Nabii miongoni mwa Manabii ambaye simjui ila Musa bin Imran akimwambia: "Nenda kwa fulani ukamsalie na waamuru watu wamsalie, kwani hakika Mimi nimeshamsamehe, na nimewajibisha apate pepo kwa kitendo cha kuzuia mja wangu fulani dhidi ya kuniasi."[220]

Inasemekana Mwenyezi Mungu alimfunulia Daudi wahyi kwamba: "Ewe Daudi lau kama wanaonipa kisogo wangejua jinsi gani ninavyowangojea, ninavyowahurumia na jinsi nilivyo na shauku ya kuona wao wanaacha maasi yao, basi wangekufa kwa ajili ya shauku ya kutaka kuja kwangu, na viungo vyao vingekatikakatika kutokana na mapenzi yao Kwangu ."[221]

NIDHAMU

Imam Ali(a.s) amesema alipokuwa akiwausia Hasan na Husein(a.s) baada ya kupigwa dhoruba ya upanga na Ibnu Muljim mlaanifu: "Ninawausieni ninyi, wanangu wote, ahali zangu na yeyote atakayefikiwa na ujumbe wangu, nawausieni kumcha Mwenyezi Mungu na kunadhimu mambo yenu ."[222]

KUHESHIMU HAKI ZA WAZAZI WAWILI

Mwenyezi Mungu amesema: "Na Mola wako Mlezi ameamuru kuwa msimwabudu (yeyote) ila Yeye tu, na wazazi wawili muwatendee wema ." (S urat Bani Israail: 23).

Akasema tena: "Basi akatabasamu akiichekea kauli yake na akasema: Ewe Mola wangu! Nipe nguvu nishukuru neema yako uliyonineemesha mimi na wazazi wangu na nipate kufanya vitendo vizuri uvipendavyo, na uniingize kwa rehema zako katika waja wako wema ." (Surat Namlu: 19).

Akasema tena: "Na tumemuusia mwanadamu afanye wema kwa wazazi wake, mama yake amechukua mimba yake kwa taabu na amemzaa kwa taabu, na kumbeba na kumwachisha ziwa (kunyonya) ni miezi thelathini, hata anapofikia baleghe yake na akawa mwenye umri wa miaka arobaini, akasema: Ee Mola wangu Mlezi! Niwezeshe nishukuru neema zako ulizonineemesha mimi na wazazi wangu, na ili nifanye vitendo vizuri unavyovipenda, na unitengenezee watoto wangu, kwa hakika ninatubu kwako na hakika mimi ni miongoni mwa walionyenyekea ." (Surat Ahqaf: 15).

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Dua ya mzazi kwa mwanae ni kama kuchukua kwa mkono ." [223]

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Watu watatu walitoka wakizunguka ardhini basi walipokuwa wakimwabudu Mwenyezi Mungu pangoni chini ya jabali ndipo jiwe kubwa lilipotoka juu ya mlima na kuziba mlango wa pango. Wakaanza kuambizana: Enyi waja wa Mwenyezi Mungu, wallahi hatowaokoeni mpaka mumsadikishe Mwenyezi Mungu vilivyo, leteni yale mliyotenda kwa moyo mmoja kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, kwani mmepata mtihani huu kutokana na dhambi. Mmoja wao akasema: 'Ewe Mwenyezi Mungu ikiwa unajua kuwa mimi nilimtafuta mwanamke kwa ajili ya uzuri wake na urembo wake, nikampa mali nyingi, nilipompata na kumkalia mkao wa mwanaume kwa mwanamke nilikumbuka moto, ikiwa ni kwa kukuogapa wewe basi ewe Mwenyezi Mungu tuondolee jiwe hili.' Basi likajipasua hadi mwanya ukaonekana. Mwingine akasema: 'Ewe Mwenyezi Mungu ikiwa unajua kuwa mimi niliwaajiri watu wanilimie, kila mtu kati yao kwa nusu dirhamu, na walipo- maliza niliwapa malipo yao. Mmoja wao akasema: 'Nimefanya kazi za watu wawili, wallahi sichukui ila dirham maja.' Akawa ameacha mali yake kwangu, nami nikaitumia hiyo nusu dirhamu kwenye ardhi, basi Mwenyezi Mungu akatoa riziki kutokana na nusu hiyo. Alipokuja mwenyewe na kuitaka nusu dirhamu yake nilimpa dirhamu kumi na nane elfu. Ikiwa unajua kuwa nilifanya hivyo kwa ajili ya kukuogopa basi tuondolee jiwe hili.' Basi likaacha uwazi mpaka wakawa wanaweza kuonana. Akasema wa tatu wao: 'Ewe Mwenyezi Mungu ikiwa unajua kuwa baba yangu na mama yangu walikuwa wamelala nikawaletea bakuli la maziwa na nikahofia kuwa nikiyaweka chini wadudu watayaramba, na nikahofia kuwa nikiwaamsha nitakuwa nimewaudhi, basi nikaendelea kuwa katika hali hiyo mpaka wakaamka na wakayanywa. Ewe Mwenyezi Mungu ikiwa unajua kuwa mimi nilifanya hivyo ili kutafuta radhi Zako basi tuondolee jiwe hili.' Ndipo jiwe likapasuka kabisa mpaka njia ikawa nyepesi kwao."Kisha Mtume(s.a.w.w) akasema:'Atakayemsadikisha Mwenyezi Mungu atafaulu ." [224]

Insafu katika muamala na watu: Imam Ali(a.s) amesema: "Ni lipi neno lililokusanya yote? Ni uwapen- delee watu lile unalopenda kwa ajili ya nafsi yako, na uchukie kuwatendea lile unalochukia kwa ajili ya nafsi yako ."[225]

Imam Ali(a.s) amesema: "Inatosha kuwa ni ujinga kwa mtu kukataza watu wasitendewe yale yale anayowatendea yeye ."[226]

Imam Ali(a.s) amesema: "Mtu mbaya zaidi kati ya watu ni yule anayefu- atilia aibu za watu huku akifumbia macho aibu zake ."[227]

Imam Ali(a.s) amesema katika barua yake kwa Imam Hasan: "Ewe mwanangu mpendwa! Ifanye nafsi yako kuwa ndio mizani ya yale yaliyopo kati yako na mwenzio, hivyo mpendelee mwenzako yale unayoyapenda kwa ajili ya nafsi yako, na chukia kumtendea yale unayochukia kwa ajili yako ."[228]

KAZI

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Kutafuta halali ni faradhi kwa kila mwislamu wa kiume na wa kike ." [229]

Imam Ali(a.s) amesema: "Afanyaye kazi huongeza nguvu, na anayepu- uzia kazi huzidi kulegea ."[230]

Imam As-Sadiq(a.s) amesema: "Jemedari wa waumini alikuwa akitoka huku akiwa na mizigo ya kokwa za tende kabeba. Anapoambiwa: 'Ewe Abul Hasan ni nini hiki ulichobeba?' Husema: 'Ni mitende atakapotaka Mwenyezi Mungu.' Basi anazipanda na hakuna hata moja inayomtoka ."[231]

Abu Amru As-Shaybaniy amesema: "Nilimwona Abu Abdullah (a.s) na mikononi akiwa na koleo na kajifunika joho zito akifanya kazi bustanini kwake huku jasho likimtoka mgongoni. Nikamwambia: Mimi ni fidia kwako nipe nikufanyie. Akaniambia: 'Mimi napenda mtu apate adha ya ukali wa joto la jua akiwa anatafuta maisha ."[232]

Abdul-Aala mtumwa wa Ali Saam amesema: "Nilimkuta Abu Abdillah kwenye baadhi ya njia za Madina, siku yenye joto kali la kiangazi, nikamwambia: 'Mimi ni fidia kwako! Hali yako kwa Mwenyezi Mungu na ukuruba wako kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu bado unafanya juhudi mwenyewe katika siku kama hii?'Akasema:'Ewe Abdul-Aala nimetoka ili kutafuta riziki ili nisiwahitajie watu mfano wako ."[233]

Imam As-Sadiq(a.s) amesema: "Ambaye haoni haya katika kutafuta maisha yake basi matumizi yake yatapungua na akili yake kupumzika na familia yake kuneemeka ."[234]

Ali bin Abu Hamza amesema: "Nilimwona Abul Hasan(a.s) akifanya kazi kwenye ardhi yake huku nyayo zake zikiwa zimelowa jasho, nikamwambia: 'Mimi ni fidia kwako, wako wapi watumishi?' Akasema: 'Ewe Ali, amefanya kazi kwa mkono wake katika ardhi yake yule aliyekuwa bora kuliko mimi na baba yangu.' Nikamwambia ni nani huyo? Akasema: 'Rasuli wa Mwenyezi Mungu, jemedari wa waumini na mababa zangu, wote walikuwa wakifanya kazi kwa mikono yao, nacho ni miongo- ni mwa vitendo vya Manabii na Mitume, Mawasii na watu wema."[235]

Ufanisi wa kazi: Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Mwenyezi Mungu Mtukufu anapenda mmoja wenu anapofanya kazi yoyote aifanye kwa ufanisi ." [236]

Imam Ali(a.s) amesema: "Unapenda uwe miongoni mwa kundi la Mwenyezi Mungu lililoshinda? Mche Mwenyezi Mungu na fanya vizuri kwenye kila jambo lako, kwani hakika Mwenyezi Mungu yuko pamoja na wenye kumcha na wale ambao hufanya vizuri ."[237]

Imam As-Sadiq(a.s) amesema: "Mtume wa Mwenyezi Mungu alishuka kaburini mpaka akamweka Saad bin Mu'adh ndani ya mwanandani na akaweka sawa tofali juu yake, akawa anasema: 'Nipe jiwe, nipe udongo mbichi huku akiimarisha tofali. Alipomaliza na akaweka udongo juu na kusawazisha kaburi, akasema: 'Hakika mimi ninajua fika kuwa litakwishana litapatwa na mtihani, lakini Mwenyezi Mungu anapenda mja anapo- fanya amali yoyote basi aifanye kwa uimara ."[238]

Imam As-Sadiq(a.s) amesema: "Atakayejiajiri mwenyewe basi amejiletea riziki yake mwenyewe. Vipi isiwe hivyo ilihali alilolipata humo ni la Mola wake Mlezi ambaye alimwajiri?! "[239]

KUWAHUDUMIA WATU

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Atakayeamka huku akiwa hajali mambo ya waislamu basi si mwislamu ." [240]

Imam As-Sadiq(a.s) amesema kuhusu kauli ya Mwenyezi Mungu: "Na akanifanya ni mwenye kubarikiwa popote nitakapokuwa ." (Surat Maryam: 31). "Ni wenye kunufaisha ."[241]

Imam As-Sadiq(a.s) amesema: "Mtume wa Mwenyezi Mungu aliulizwa: 'Ni nani mtu apendwaye sana na Mwenyezi Mungu?' Akasema: 'Yule mtu awanufaishaye sana watu ."[242]

Jamil amesema: "Nilimsikia Imam As-Sadiq(a.s) akisema:'Waumini ni wahudumu wa wenzi wao.' Nikamwambia vipi wanakuwa wahudumu wa wenzi wao? Akasema: 'Wanafaidishana wao kwa wao ."[243]

Imam As-Sadiq(a.s) amesema: "Isa(a.s) alipita akawakuta watu wamevaa majalibibi akawaulizia, akaambiwa: Ni binti wa fulani anapelekwa nyumba ya fulani. Akasema: 'Rafiki yao wa kike atakufa usiku.' Basi

walipoamka asubuhi watu wakasema bado yuko hai. Ndipo(a.s) akaenda akifuatana na watu mpaka nyumbani kwa yule mwanamke, alipotoka mumewe akamwambia: 'Muulize mkeo ni kitu gani alichotenda jana usiku?' Mke akasema: 'Sikutenda kitu ila kuna ombaomba alikuwa akini- jia kila usiku wa siku ya Ijumaa kati ya Ijumaa zilizopita naye alikuja usiku uliyopita akaita na hakuna aliyemjibu, ndipo akasema: 'Imekuwa vigumu kwangu kwani yeye hasikii sauti yangu ilihali familia yangu wanabaki usiku huu wakiwa na njaa.' Ndipo nikaamka nikiwa nimekasirishwa nikampa kiasi ambacho nilikuwa nampa hapo awali.' Isa(a.s) akasema: 'Inuka hapo ulipoketi.' Alipoinuka ghafla akatokea nyoka mkubwa toka kwenye nguo zake (mwanamke) akiwa ameng'ata mkia wake. Isa(a.s) akasema:'Kutokana na sadaka uliyotoa umeepushiwa nyoka huyo ."[244]

UAMINIFU

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Uaminifu ni utajiri ." [245]

Imam As-Sadiq(a.s) amesema: "Tazama hadhi aliyofikia Ali(a.s) kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) , nawe shikamana nayo, kwani hakika Ali(a.s) alifikia hadhi aliyofikia kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) kwa ukweli na uaminifu."[246]

Abdur-Rahman bin Sayabah amesema: "Alipohiliki baba yangu alikuja kwangu mtu mmoja kati ya ndugu zake, akagonga nami nikatoka, akanipa pole na kuniambia: 'Je baba yako ameacha chochote?' nikamwambia hapana. Basi akanipa fuko likiwa na dirhamu elfu moja, na akaniambia: 'Lihifadhi vizuri na kula fadhila zake.' Ndipo nikaingia kwa mama yangu nami nikiwa na furaha nikampa habari. Basi usiku uilipoingia nilimwendea

rafiki wa baba yangu akaninunulia bidhaa na nikaanza kukaa dukani na Mwenyezi Mungu akaniruzuku kheri nyingi. Ulipofika msimu wa Hijja nikatamani kuhiji, nikamwendea mama yangu nikampa habari, nikamwambia: Mimi ninatamani niende Makka. Akaniambia: 'Mrudishie fulani dirhamu zake.' Nikamwendea na kumpa kana kwamba mimi nimempa zawadi. Yule mtu akaniambia: 'Huenda umeziona chache, nikuongeze nyingine?' Nikamwambia: La, lakini nimetamani kuhiji hivyo nimependa kitu chako nikikabidhi kabisa.' Kisha nikatoka na nikatekeleza ibada yangu ya Hijja, kisha nikarejea Madina nikiwa na watu hadi nikaingia kwa Abu Abdillah(a.s) , naye alikuwa anawapa idhini ya ujumla, basi nikakaa mwishoni mwa watu nami nilikuwa ni kijana mdogo, na hapo walikuwa wakimuuliza maswali naye anawajibu. Watu walipopungua kwake aliniashiria nisogee nikasogea, akaniambia: Una haja yoyote? Nikamwambia: Mimi ni fidia kwako mimi ni Abdur-Rahman mwana wa Sayabah. Akaniambia: Baba yako amefanya nini? Nikamwambia: Amehiliki. Basi akaumia na kumwombea rehema, kisha akaniambia: Je ameacha kitu? Nikamwambia: Hapana. - Akaniambia: Umehiji kutokana na nini? Nikaanza kumsimulia kisa cha mtu yule. Basi hakuniacha nimalize akawa ameniambia: Umefanya nini katika elfu hizo? Nikamwambia: Nimemrudishia mwenyewe. Akaniambia: Umefanya vizuri, je nikuusie? Nikaasema: Mimi ni fidia kwako, ndio. Akaniambia: Shikamana na ukweli na kuwa mwaminifu utashirikiana na watu katika mali zao hivi. Akawa amekusanya vidole vyake. Amesema: Nikahifadhi hilo, basi nikatoa Zaka dirhamu laki tatu."[247]

Imam Muhammad Al-Baqir(a.s) amesema: "Vitu vitatu Mwenyezi Mungu hakumwekea yeyote ruhusa ya (kuvikiuka): Kuwa mwaminifu kwa mwema na muovu, kutekeleza ahadi kwa mwema na muovu na kuwatendea wema wazazi wawili, sawa wawe wema au waovu ."[248]

KUJIPAMBA

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Hakika Mwenyezi Mungu ni Mzuri anapenda uzuri ". [249]

Mtume wa Mwenyezi Mungu (s.a.w.w) amesema: "Nywele nzuri ni zawa- di ya Mwenyezi Mungu Mtukufu basi iheshimuni ."[250]

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Atakayefuga nywele azitunze au azikate ." [251]

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema kuwaambia wanaume: "Kateni kucha zenu ." Akawaambia wanawake: "Ziacheni kwani zenyewe ni mapambo yenu ." [252]

Imam Ali(a.s) amesema: "Ni lazima mmoja wenu ajipambe kwa ajili ya ndugu yake mwislamu kama ajipambavyo kwa ajili ya mgeni ambaye anapenda amwone akiwa katika hali nzuri ."[253]

Imam As-Sadiq(a.s) amesema: "Vaa na jipambe, hakika Mwenyezi Mungu ni Jamilu anapenda jamali, lakini utokane na halali ."[254]

Imam Muhammad Al-Baqir(a.s) amesema: "Haifai kwa mwanamke kuji- acha hali ya kutojipamba bali angalau aweke mkufu shingoni mwake ."[255]

Al-Hakam bin Utaybah amesema: "Niliingia kwa Abu Jafar(a.s) naye akiwa ndani ya nyumba iliyopambwa kwa samani za ndani, naye akiwa na kanzu nyepesi na joho lenye rangi huku rangi ikiwa imeathiri shingo lake, nikawa natazama nyumba na ninamtazama. Akaniambia: 'Hakam! Unasemaje katika hili?' Nikamwambia: 'Siwezi kusema chochote hali mimi naliona juu yako, ama kwetu sisi hilo hufanywa na kijana barobaro.' Akaniambia:'Ewe Hakam! Ni nani aliyeharamisha mapambo ya Mwenyezi Mungu aliyoyatoa kwa ajili ya waja wake, na vyakula vizuri miongoni mwa riziki. Na hili ni miongoni mwa aliyoyatoa Mwenyezi Mungu kwa ajili ya waja wake. Ama nyumba hii ambayo unaiona ni nyum- ba ya mwanamke, nami ni karibu nitafanyanaye harusi. Na nyumba yangu ni ile unayoitambua ."[256]

MAADILI MEMA

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Hakika nimetumwa ili nitimize maadili mema ." [257]

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Hakika nimetumwa ili nitimize tabia njema ." [258]

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Mwenyezi Mungu amefanya tabia njema kuwa kiungo kati Yake na viumbe Wake. Basi mmoja wenu atosheke na kushikamana na tabia zilizoungana na Mwenyezi Mungu ." [259]

Imam Ali(a.s) amesema: "Fahamuni hakuna thawabu inayotarajiwa wala adhabu inayozuilika. Je mnazipa mgongo tabia njema?! "[260]

Imam Ali(a.s) amesema: "Tabia njema ni dalili ya jadi njema ."[261]

Imam Ali(a.s) amesema: "Katika tabia njema kuna hazina za riziki ."[262]

Imam Ali(a.s) amesema: "Mtu aridhiwaye sana ni yule ambaye tabia zake ni maridhawa ."[263]

Imam Ali(a.s) amesema: "Mwenye ukamilifu wa imani miongoni mwenu ni yule mwenye tabia njema ."[264]

Imam As-Sadiq(a.s) amesema: "Tabia njema ni dini nayo huongeza riziki ."[265]

Imam As-Sadiq(a.s) amesema: "Wasia wa Waraqah bin Nawfal kwa Khadija binti Khuwaylid (r.a) alipokuwa akiingia kwake ni: 'Fahamu kuwa ujana mzuri wenye tabia njema ni ufunguo wa kheri na kufuli la shari. Na ujana wenye tabia mbaya ni kufuli la kheri na ufunguo wa shari ."[266]

Husain bin Atiyyah amepokea kutoka kwa Imam As-Sadiq(a.s) kuwa amesema: "Tabia njema ni kumi, ukiweza kujitahidi ziwepo kwako basi na ziwepo, kwani zenyewe huwa kwa mzazi na wala haziwi kwa mtoto, na huwa kwa mtoto wala haziwi kwa baba yake na huwa kwa mtwana na wala haziwi kwa muungwana." Akaulizwa ni zipi hizo? Akasema:'Ukweli wa ushujaa, ukweli wa maneno, uaminifu, kuunga udugu wa tumbo moja, kumkirimu mgeni, kumlisha ombaomba, kulipa wema kwa wema, kushutumiwa kwa ajili ya jirani yako, kushutumiwa kwa ajili ya rafiki yako, na kiongozi wao ni kuwa na haya ."[267]

Imepokewa kutoka kwa Hasan bin Muhammad kutoka kwa babu yake kutoka kwa sahaba zake zaidi ya mmoja, wamesema: "Mtu mmoja toka kizazi cha Umar bin Al-Khattab alikuwa akimuudhi Abu Hasan Musa(a.s) huko Madina, anamtukana amuonapo na kumshutumu Ali(a.s) . Ndipo wafuasi wake wakamwambia siku moja: Tuache tumuuwe muovu huyu. Lakini akawakataza kufanya hivyo kwa kuwakemea sana. Akaulizia kuhusu mjukuu huyo wa Umar akaambiwa kuwa huwa analima huko kwenye viunga vya pembezoni mwa Madina, basi akarakibu hadi kwake akamkuta shambani kwake, ndipo akaingia shambani kwa punda wake, hapo mjukuu wa Umar akapiga kelele: 'Usikanyage mazao yetu.' Lakini akayakanyaga kwa punda wake mpaka akafika kwake, akashuka na akaketi kwake kwa furaha na cheko, na akamwambia:-Umegharamia kiasi gani kwenye shamaba lako hili? -Akasema: Dinari mia moja. - Akamwambia: Unataraji kupata kiasi gani?

Akajibu: Mimi sijui ghaibu. -Akamwambia: Nimekwambia Unataraji utajiwa na kiasi gani? -Akasema: Nataraji kujiwa na dinari mia mbili. Mpokezi anasema: Basi Abu Hasan(a.s) akamtolea fuko likiwa na dinari mia tatu na kumwambia: 'Shamba lako litabaki katika hali yake na Mwenyezi Mungu atakuruzuku unayotaraji.' Basi mjukuu wa Umar akasi- mama na kubusu kichwa chake na kumwomba amsamehe makosa yake. Imam akatabasamu na kuondoka. Alipoelekea msikitini akamkuta mjukuu wa Umar kakaa, alipomuona Imam akasema: 'Mwenyezi Mungu ajua jinsi anavyoweka risala yake.' Ndipo sahaba zake waliposhituka na kumuuliza: 'Ni ipi kadhia yako? Ulikuwa ukisema yasiyokuwa haya.' Akawaambia: Mmeshasikia niliyosema hivi sasa. Na akaanza kumwombea kheri Abul Hasan(a.s) . Ndipo Abu Hasan aliporejea nyumbani kwake akawaambia wanabaraza wake waliomuomba wamuue mjukuu wa Umar: 'Ni lipi lililo bora, mlilotaka au nililotaka? Mimi nimemsawazisha kwa kiwango hiki mlichokijua, na shari yake imezuilika."[268]

UTAWA

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Enyi kundi la vijana wa kikuraishi! Hifadhini tupu zenu. Fahamuni kuwa atakaehifadhi utupu wake basi atapata pepo ." [269]

Imam Ali(a.s) amesema: "Mwenyezi Mungu anapomtakia mja kheri huli- hifadhi tumbo lake na utupu wake ."[270]

Imam Ali(a.s) amesema: "Mwenye kupigana jihadi katika njia ya Mwenyezi Mungu si mwenye malipo makubwa kuliko aliye na uwezo wa kuzini lakini akafanya utawa. Mtawa amekaribia kuwa malaika miongoni mwa malaika ."[271]

Imam Ali(a.s) amesema: "Utawa hudhoofisha matamanio ."[272]

Imam Ali(a.s) amesema: "Zaka ya uzuri ni kuwa mtawa ."[273]

Imam Ali(a.s) amesema: "Utawa huilinda nafsi na huipamba dhidi ya mambo duni ."[274]

Imam Ali(a.s) amesema: "Utawa ni kiongozi wa kila kheri ."[275]

Imam Ali(a.s) amesema: "Kazi pamoja na utawa ni bora kuliko utajiri pamoja na ufuska ."[276]

KUANGUSHA MACHO

Mtume wa Mwenyezi Mungu(s.a.w.w) amesema: "Hakuna mwislamu yeyote anayemtazama mwanamke mzuri mara ya kwanza, kisha akainamisha macho yake ila ni lazima Mwenyezi Mungu atamuwekea ibada atakayopata raha kwayo ." [277]

Imam Ali(a.s) amesema: "Atakayehifadhi macho yake sifa zake zitakuwa nzuri ."[278]

Imam Ali(a.s) amesema: "Kuhifadhi macho ni miongoni mwa murua ."[279]

Imam Ali(a.s) amesema: "Mambo matatu ni murua: Kuangusha macho, kupunguza sauti na kutembea kwa wastani ."[280]

Imam Ali(a.s) amesema: "Atakayemuona mwanamke ampendezaye basi amwendee mke wake, kwani bila shaka naye anacho mfano wa kile ali- chokiona. Na wala asimpe shetani njia moyoni mwake, na ayaepushe macho yake kwake. Na kama hana mke basi aswali rakaa mbili na amuhimidi sana Mwenyezi Mungu, amswalie Mtukufu Mtume na Aali zake (a.s.), kisha amwombe Mwenyezi Mungu fadhila zake, basi hakika atamhalalishia kwa huruma yake lile litakalomtosheleza ."[281]

Imam Ali(a.s) alipokuwa ameketi na sahaba zake ghafla akapita mwanamke mzuri na watu wakamrushia macho yao, ndipo akasema: "Amuonapo mmoja wenu mwanamke ampendezaye basi amtomasetomase mkewe, kwani hakika yeye ni mwanamke kama mke wake ."[282]

Imam As-Sadiq(a.s) amesema: "Mtazamo ni mshale miongoni mwa mishale ya Ibilisi ulio na sumu, atakayeuwacha kwa ajili ya Mwenyezi Mungu na si kwa ajili ya kingine basi Mwenyezi Mungu atamfatilizia imani ambayo atapata ladha yake ."[283]