• Anza
  • Iliyopita
  • 21 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 20665 / Pakua: 3967
Kiwango Kiwango Kiwango
MAISHA YA ABU DHARR

MAISHA YA ABU DHARR

Mwandishi:
Swahili

MAISHA YA ABU DHARR

KIMEANDIKWA NA: KIKUNDI CHA WANACHUONI ISLAMIC SEMINARY PUBLICATIONS

KIMETARJUMIWA NA: AL-AKH SALMAN SHOU

KIMEHARIRIWA NA: USTADH ABDALLAH MOHAMED

NENO LA MCHAPISHAJI

Kitabu kilichoko mikononi mwako, ni tarjuma ya kitabu cha Kiingereza, kwa jina la: "Abu Dharr"

Kitabu hiki kinahusu maisha ya Sahaba mkubwa na mashuhuri; Abu Dharr (Jundab bin Junadah). Abu Dharr alikuwa mtu wa tano kuingia kwenye Uislamu na upanga wake ulikuwa unafaa sana katika kuendeleza Uislamu. Aliona mikengeuko mingi katika Uislamu tangu kuanza kwake, na baada ya kifo cha Mtukufu Mtume mambo hayakuwa mazuri. Alishuhudia mitafaruku mingi wakati wa makhalifa watatu wa mwanzo kiasi kwamba hakuweza kuvumilia, na alianza kukemea maovu yanayofanywa na makhalifa wazi wazi na kwa ujasiri mkubwa sana mpaka ikafikia Khalifa wa tatu kuchukua hatua za kumhamisha na kumpeleka jangwani ambako aliishi maisha ya dhiki mpaka kifo kikamkuta huko.

Kwa bahati mbaya sana wanahistoria wengi wa Kiislamu na wasio wa Kiislamu hawakuzungumza habari zake kwa kina na kama inavyostahiki kuwa. Kwa hakika Abu Dharr pamoja na Masahaba wengine kama vile Amar bin Yasir, Mikidadi, Salman Farsy, halikadhalika na ami yake Mtukufu Mtume, mzee Abu Twalib na mke wa Mtume Bibi Khadija, alikuwa ni madhulumu wa historia.

Tumekiona kitabu hiki ni chenye manufaa sana, hususan wakati huu wa maendeleo makubwa ya elimu katika nyanja zote, ambapo uwongo, ngano za kale na upotoshaji wa historia ni mambo ambayo hayana nafasi tena katika akili za watu. Kutokana na ukweli huo,

Taasisi yetu ya 'Al-Itrah Foundation' imeona ikitoe kitabu hiki kwa luhga ya Kiswahili, kwa madhumuni yake yale yale ya kuwahudumia Waislamu, hususan wazungumzaji wa Kiswahili.

Tunamshukuru ndugu yetu, Salman Shou kwa kukubali jukumu hili la kukifanyia tarjuma kitabu hiki. Vile vile tunawashukuru wale wote walioshiriki kwa njia moja au nyingine hadi kufanikisha kuchapishwa kwa kitabu hiki.

Ni matumaini yetu kwamba kitabu hiki kitakuwa ni mwanga kwa wasomaji wetu na kuzidisha upeo wao wa elimu katika dini.

KUHUSU WACHAPISHAJI

Leo hii akili yenye hadhari inaona kiakili mabadiliko ya maisha ya mwanadamu. Sayansi na teknolojia na mafanikio yao ya kushangaza yanaonekana yamefika kwenye kilele chao. Mahitaji ya kidunia hisia kali za matamanio ya mamlaka na ukubwa, ni mambo ambayo yamemwelekeza mwanadamu kwenye muflisi wa maadili mema. Katika hali hii ya kukatisha tamaa, mtu analazimika kutulia na kukadiria upya hatari zinazoweza kuwa tishio kwa mwanadamu kwa ujumla. Mwanadamu kwa mara nyingine tena ameelekeza macho yake kwa Mwenyezi Mungu, Mwingi wa rehema, Mwenye kurehemu kwani sasa ametambua kwamba ufumbuzi wa matatizo yake na hatima ya ukombozi wake ni mambo yaliyomo katika kufuata na kutekeleza.

Kuhama huku kutoka kwenye fikra ya mambo ya kidunia na kwenda kwenye mambo ya kiroho ni hali inayoafikiana kikamilifu na malengo na madhumuni ya seminari ya Kiislamu. Miongozo ya kidini, iliyo sambamba na maendeleo ya wakati uliopo, yanatoa kimbilio linalohi-tajiwa sana na akili inayosumbuliwa na yenye wasi wasi. ni matokeo ya ongezeko la utambuzi, kwamba imeeleweka kwamba siri ya kuishi maisha ya uadilifu hapa duniani kuelekeza kwenye furaha kamili ya milele ya maisha ya Peponi. Huu ni ujumbe wa Uislamu kwa ulimwengu wote.

Jumuiya yetu ya Kiislamu inataka kunyanyua juu mwenge wa mwongozo wa kiroho na kusaidia kwa moyo wote kutangaza urithi wa kiroho wa mwanadamu. Inaonyesha njia ya maisha kwa mujibu wa Quran katika utukufu wake ulio safi kabisa. Inaonyesha hayo tu yenye mamlaka na yaliyothabiti. Uenezi wake umebuniwa kwa jinsi inayoweza kukidhi mahitaji ya kiroho katika wakati uliopo.

Itahudumia kama chemchem ya kudumu kwa wale wenye kiu ya ujuzi. Seminari ya Kiislamu ni taasisi ya kimataifa ambayo inajaribu kuleta udugu wa Kislamu. Inapata mchango mzuri sana kutoka kwa wanachuo, kama nyongeza ya kuwa na msaada wa kimataifa kwa ajili ya kutimiza lengo lake kubwa. Inayo vituo; Asia, Afrika, Ulaya, Amerika, Canada na Mashariki ya mbali.

MPENDWA MSOMAJI

Kitabu hiki kimechapishwa na Seminari ya Kiislamu. Uenezi wake umebuniwa kwa ajili ya kuhudumia mahitaji ya kiroho katika kipindi hiki ukiwa na msisitizo mahsusi kusafisha akili na fikra ya Muislamu. Juhudi kubwa sana zimefanywa na Seminari kuweka katika machapisho yake yale ambayo yanaaminika na thabiti kweli katika Uislamu.

Unaombwa kwa ukarimu kukisoma kitabu hiki kwa moyo ambao umekusudiwa. Pia unaombwa uwe huru kuwasilisha kwetu maoni yako ambayo yatathaminiwa sana kuhusu uenezi wetu.

Kutangaza ujumbe wa Uislamu ni kazi inayotaka ushirikiano wa watu wote. Seminari inakukaribisha katika kazi hii ikikubaliana kwa furaha na Aya ya Quran Tukufu.

"Sema; Mimi ninakunasihini kwa jambo moja tu ya kwamba msimame kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, wawili wawili na mmoja mmoja. " (34:46).

Mwenyezi Mungu na akurehemu. Wako katika Uislamu.

UTANGULIZI

Baada ya miaka kumi na tatu ya mfululizo wa mateso na mapambano, Mtume wa Uislamu aliondoka Makkah na kwenda Madina. Alihisi kwamba kipindi cha uvunjaji sheria na kutangazwa kwa siri kwa Uislamu kilikwisha na kwa msaada wa masahaba wake waaminifu na jasiri angeweza kujenga jumba kubwa la dola ya Kiislamu na kuweka msingi wa serikali ya kisiyasa kama anavyotaka Mwenyezi Mungu.

Mara tu baada ya kufika Madina, Mtukufu Mtume alijenga msikiti hapo. Alijenga nyumba yake iliyotazamana na msikiti, na alifanya mlango wake wa kuingia moja kwa moja msikitini. Hapakuwepo na mabadiliko ya maisha yake tangu mwanzo hadi mwisho. Tabia, mwenendo na maadili mema yalikuwa hivyo hata baada ya kuanzisha serikali ya Kiislamu katika Arabia yote.

Mfumo wa utawala mpya na dola mpya vilitokeza na kuanza kuwepo katikati ya dola mbili za wakati huo. Kwenye Serikali hii ya Kiislamu hapakuwepo na mtawala na mtawaliwa, hapakuwepo afisa na wa chini yake, na hapakuwepo na bwana na mtumwa. Wote walikuwa sawa mbele ya Mwenyezi Mungu.

Mwasisi wa mfumo huu mpaya wa utawala alitawafu na baada ya kunyang'anywa Ali urithi na kuundwa kwa vikundi vya kisiasa, mkengeuko wa kwanza ambao ulitikisa msingi wa Kiislamu ulitokeza kwenye jambo la Ukhalifa.

Mmojawapo wa masahaba waaminifu sana na jasiri sana wa Mtukufu Mtume alikuwa Abu Dharr. Alikuwa mtu wa tano kuingia kwenye Uislamu na upanga wake ulikuwa unafaa sana katika kuendeleza Uislamu. Aliona mikengeuko yote hii. Ali ambaye alikuwa mfano halisi wa wema na ukweli, alilazimika kuishi maisha ya upweke na

maadui wa Uislamu walipe na kwenye mfumo wa Ukhalifa na walikuwa wanauharibu Uislamu kwama mchwa.

Abu Dharr alisumbuliwa sana na kushtuka na aliona kwamba hali ya Uislamu ya siku za usoni ilikuwa ya wasi wasi na kuogopesha. Hata hivyo pia aliona kwamba kwa hali yoyote ile msafara wa Uislamu ulikuwa unaendelea kwenye njia yake, ingawa haki kuu ilikuwa, mpangilio wa Kiislamu hakuvunjika kabisa. Kwa hivyo, ingawa alihuzunika na kufadhaika, alinyamaza kimya!

Mfumo wa utawala wa Uthman ulipopata uwezo kamili wa serikali ya Kiislamu, haki za wafanya kazi na Waislamu wasio jiweza zilikiuka na wala riba, wanao shughulika na watumwa, matajiri na makabaila, ambao walifika kwenye baraza la Uthman na Muawiyah. Tofauti za matabaka na kuhodhi utajiri ni tabia zilizoanzishwa tena na Uislamu uliotishiwa na hatari kubwa. Njia na tabia za Mtukufu Mtume ziliachwa. Maelfu ya dinari zilitumika kujenga Ikulu ya Muawiyah iliyoitwa (Green Palace) ya mtawala wa Kiislamu na utaratibu wa mabaraza ya Kifalme ulianzishwa. Umari aliendesha maisha yake kama mtu wa kawaida na Abu Bakr naye aliishi hivyo hivyo, ili kuendesha maisha yake, alikuwa anafanya kazi ya kukamua mbuzi wa Myahudi ambapo kidani cha mke wa Uthman, Khalifa wa tatu kiligharimu thuluthi moja (1/3) ya pato la lililoletwa kutoka Afrika.

Akichukua nafuu isiyostahili ya kazi anayofanya baba yake, mtoto wa kiume wa mmojawapo wa maofisa wa ngazi ya juu sana katika utawala wa Umari alichukua farasi wa mtu kwa lazima. Kwa upande mwingine Uthman alimteua Marwan bin Hakam kama mshauri wake mtu ambaye alipewa adhabu ya uhamisho na Mtukufu Mtume na akampa zawadi ya kiunga cha Kheybar pamoja na malipo kutoka Afrika!

Abu Dharr alipochunguza shughuli hizi za kuaibisha hakuweza kuvumilia yote haya, aliamua kufanya upinzani dhidi ya mfumo huo wa kidikteta. Yalikuwa maasi ya kijasiri na ukakamavu ambayo yalisababisha nchi zote za Kiislamu kufanya uasi dhidi ya Uthman; mawimbi yake yanayo rindima bado yanaweza kuonekana kwenye jamii nyingi za binadamu.

1

MAISHA YA ABU DHARR

Abu Dharr alikuwa na shauku ya kuanzisha mfumo wa maadili ya Kiislamu, ambapo utawala wa Uthman ulikuwa unakiuka kwa kuhuisha utawala wa kitabaka. Abu Dharr aliona Uislamu kuwa ndio kimbilio la wasiojiweza, na mafakiri waliokuwa wanakandamizwa, na Uthman aliufanya utawala wake kuwa njia ya kuwafadhili jamii ya watu wakuu na wala riba.

Ugomvi huu baina ya Abu Dharr na Uthman uliendelea, hatimaye Abu Dharr alipoteza maisha yake kwa sababu hii.

Abu Dharr alimtambua Mwenyezi Mungu Mweza wa yote; kwa hiyo kamwe hakutetereka katika njia Yake hata kwa nukta moja. Aligeuka kuwa mtu bora katika kundi la Uislamu na ndio jambo ambalo linatosha kuonyesha umashuhuri wake.

Abu Dharr ni mmojawapo wa wale viongozi na wakombozi wa uhuru ambapo mwanadamu anautaka leo hii. Hususan kwa vile utaratibu wa muda umefanyiza hali ya wasiwasi mkubwa katika ulimwengu wa uchumi na matatizo ya kiuchumi yanashughulikiwa kuwa ndio matatizo ya msingi zaidi ya maisha, maoni yake yamepata umuhimu mkubwa. Hali hiyo hiyo iliyoanzisha huko Syria na Madina kwa kuwakusanya mafakiri na wasiojiweza na kuwashawishi waasi dhidi ya wala riba na wanaohodhi utajiri, pia leo hii imejitokeza. Waislamu hapa duniani wanakumbuka maneno yake ya kuvutia, maoni sahihi na ho tuba kali. Inawezekana kwamba wanaweza kuona kwenye sehemu za mbali sana historia kwamba amewakusanya wanaokandamizwa na

wasiojiweza kwenye msikiti na ana chokonowa hisia zao dhidi ya wale waishio kwenye ikulu (majumba ya maraisi wa mataifa mbali mbali duniani) na utaratibu mchafu wa Uthman na kutangaza hadharani: "Watu hao wanao hodhi dhahabu na fedha na hawatumii katika njia ya Mwenyezi Mungu, wanapaswa kujua kwamba adhabu yao itakuwa mateso makali ." (Quran 9:34).

"Ewe Muawiyah! Endapo unajenga Ikulu hii kwa fedha yako mwenyewe ni ubadhilifu, na kama unajenga kwa kutumia hazina ya taifa, huko ni kuitwalia ."

"Ewe Uthman! Masikini wamekuwa masikini zaidi na matajiri wamekuwa matajiri zaidi. Yote haya yanasababishwa na wewe."

SURA YA KWANZA

Abu Dharr alikuwa mmojawapo wa hao masahaba wa Mtume wa Uislamu, Muhammad(s.a.w.w) ambao walikuwa wachaji Mungu na wapenda uhuru na walikuwa na tabia bora kwa mujibu wa maneno ya Mtukufu Mtume: Pepo na wakazi wa huko wanawataka haraka sana. Alifaidika kuwa na Mtume katima uhalisi wake.

Abu Dharr mwenyewe anasema: "Jina langu halisi ni Jundab bin Junadah, lakini baada ya kuingia kwenye Uislamu, Mtume alinipatia jina la 'Abdullah' na hili ndilo jina ninalolipenda hasa ."

Abu Dharr ilikuwa Kuniyah yake (kutokana na mtoto wake wa kwanza aliyeitwa Dhar).

Wanavyuoni wanakubaliana kwamba Abu Dharr alikuwa mtoto wa kiume wa Junadah bin Qays bin Saghir bin Hazam bin Ghafir na mama yake alikuwa Ramlah binti Wafiah Ghifariah. Alikuwa wa jamii ya Kiarabu na alikuwa wa kabila la Ghifar. Ndio sababu ya neno 'Ghifar; limeandikwa na jina lake.

Abdullah al-Subaiti ameandika: "Tunapoangalia wasifu wa Abu Dharr inaonekana kama vile ni nuru iliyopewa umbo la Binadamu. Alikuwa mfano halisi wa sifa za mtu mashuhuri. Alikuwa na sifa pekee ya akili, uelewa, busara na werevu." Kwa maneno ya Imamu Jafar Sadiq: "Wakati wote alikuwa katika tafakuri na Swala zake ziliegemezwa kwenye mawazo kuhusu Mungu ." (Sahih Muslim).

Mwandishi maarufu wa Misri Abdul Hamid Jaudatus Sahar, kwenye kitabu 'Al-Ishtiraki az-Zahid, ameandika: Wakati fulani ilitokea njaa kali. Watemi wa kabila la Ghifar walikusanyika kwa ajili ya kushauriana ili wapate ufumbuzi wa tatizo hilo kwa sababu ya ukame wa muda mrefu. Kwa hiyo hicho kilikuwa kipindi cha mateso makubwa. Wanyama walikonda na akiba kwenye maghala ilikwisha. Waliambizana wao kwa wao, 'Hatujui kwa nini Mungu wetu (Sanamu Manat) amekasirishwa na nini kutoka kwetu, ingawa tumeomba mvua, tumetoa sadaka ya ngamia na tumefanya kila linalowezekana ili atupendelee.

Msimu wa mvua sasa umekwisha. Hakuna hata dalili ya wingu angani. Hapajatokea mngurumo na rasha rasha ya mvua kipindi hiki, hakuna hata tone la mvua au manyunyu. Unafikiria nini? Tumekuwa wapotevu hivyo kwamba ghadhabu ya mungu wetu imetuangukia? Kwa nini ahisi amekosewa na sisi ambapo tumetoa sadaka nyingi kwa ajili ya kumfurahisha yeye?"

Watu walianza kutafakari juu ya jambo hili na kubadilishana mawazo. 'Binadamu hawezi kuingilia mipango ya Mbinguni. Hakuna

mtu yeyote anayeweza kuleta mawingu ya mvua kutoka angani. Anayeweza kufanya hivyo ni 'Manat' tu. Kwa hiyo hatuna njia nyingine isipokuwa sisi, wanaume na wanawake, twende Hija huku tunalia kwa huzuni na kusali na kumwombea kwa huzuni na kusali na kumwomba Manat atusamehe. Labda inawezekana akatusamehe na mvua ikaanza kunyesha na kuifanya ardhi kuwa kijani kibichi baada ya ukame, ili umasikini wetu ubadilike kuwa mafanikio, uchungu kuwa furaha na matatizo kuwa raha na starehe."

Kwa hiyo, kabila lote lilianza matayarisho ya safari ya kwenda kumuona Manat. Wale waliokuwa wamelala waliamka na kuweza kuweka mito ya kukalia juu ya migongo ya ngamia wao. Unais (ndugu yake Abu Dharr) naye pia alipanda ngamia wake na kumwendesha, ili aungane na msafara, karibu na Pwani ya bahari, Mushalsal na Qadid sehemu zilizomo kati ya Makkah na Madina, ambapo ndipo Manat alipo.

Unais alitazama huku na kule lakini hakumuona kaka yake. Alimbembeleza ngamia akakaa chini. alikimbia kuelekea nyumbani. Aliingia ndani huku akiita 'Jundab!

Mara tu Unais aliposikia hivyo, alikimbia kwenda huko. Alipofika hapo, alimuona mtu anasema, "Sifa zote zinastahiki kwake Mwenyezi Mungu. Ninamsifu Yeye na ninahitaji msaada Wake. Ninamwamini Yeye, ninamtegemea Yeye na ninashahidilia kwamba hapana mungu ila Mwenyezi Mungu na Hana mshirika."

Katika nukuu ya Subaiti, Unais alimsikia mtu huyo akitangaza, "Enyi watu! Nimekuleteeni neema ya dunia hii na baada ya maisha haya. Semeni kwamba hapana mungu isipokuwa Allah ili muweze kupata ukombozi. Mimi ni Mjumbe wa Mwenyezi Mungu na nimekuja kwenu. Ninawaonya kuhusu adhabu ya siku ya Hukumu. Kumbukeni kwamba hakuna mtu atakayepata kuokolewa isipokuwa yule anayekuja mbele ya Mwenyezi Mungu kwa moyo wa unyenyekevu. Wala utajiri hautakuwa na manufaa kwake, ama watoto hawatawasaidieni. Mwogopeni Mwenyezi Mungu, Mwenyezi Mungu atakuwa mwema kwenu. Enyi watu! Nisikilizeni! Ninasema wazi kabisa kwamba mababu zetu walifanya upotovu kwa kuacha njia iliyonyooka na kuanza kuabudu masanamu haya na nyinyi mnafuata nyayo zao. Kumbukeni kwamba masanamu wala hayawezi kuwaumizeni ama kuwanufaisheni. Wala hayawezi kuwazuieni ama kuwaongozeni."

Unais aliposikia hotuba hii yenye ushawishi mkubwa alishangaa. Lakini katika kustajabu kwake aliona kwamba watu walikuwa wanasema mambo tofauti dhidi yake.

Aliposikia Mtume alisema, "Mitume hawasemi uongo. Ninaapa kwa jina la Mwenyezi Mungu ambaye hapana mungu mbali na Yeye, kwamba nimetumwa kwenu kama mjumbe. Kwa jina la Mwenyezi Mungu mtakufa kama mnavyolala na mtafufuka kama mnavyoamka. mtaitwa kuhesabiwa matendo yenu. Halafu mtapewa Pepo au Jahanamu ya milele!"

Aliposema hivi watu walimuuliza Mtume, watafufukaje baada ya kuwa vumbi?

Wakati huu huu Mwenyezi Mungu aliteremsha Aya zifuatazo: "Sema: Kuweni hata mawe, na chuma. au umbo lolote mnaloliona kubwa katika vifua. Watasema: Nani atakayeturudisha tena? Sema: Yule aliye kuumbeni mara ya kwanza! Watakutikisia vichwa vyao, na watasema: Lini hayo? Sema: Asaa yakawa karibu! " (17:50-51).

Mara tu Mtume alipomaliza hotuba yake watu walinyanyuka. Wakati walipokuwa wanasambaa, mmoja wao alisema: "Huyu ni mtabiri?" Mwingine akasema, "Huyu ni mchawi."

Unais alimsikiliza Mtume na watu. Aliinamisha kichwa chake kwa muda fulani na akanong'ona: "Kwa jina la Mwenyezi Mungu maneno yake ni matamu. Hayo aliyoyasema ni kweli na watu wanaompinga ni wapumbavu."

Halafu akapanda ngamia wake akaanza safari ya kuelekea kwao. Aliendelea kufikiria kuhusu Muhammad, Mtume wa Mwenyezi Mungu wakati wote wa safari yake, na alikuwa anashangaa kuhusu mazungumzo yake, hadi alipoonana na Abu Dharr.

Abu Dharr alipomuona Unais, alimuuliza kwa shauku kubwa, "Kuna taarifa gani? Uliona nini Makkah?"

Unais: "Wanasema kwamba mtu huyu ni mshairi, mchawi na mtabiri. Lakini nilipochunguza mazungumzo yake kulingana na wale wanaosema kuwa ni mshairi, niliona kwamba maneno yake si mashairi wala si utabiri kwani nimewahi kukutana na watabiri wengi, na mazungumzo yake si sawa na yale ya watabiri.

Abu Dharr: "Hufanya nini na husema nini?"

Unais: "Husema mambo ya ajabu."

Abu Dharr: "Huwezi kukumbuka chochote katika yale aliyosema."

Unais: "Kwa jina la Mwenyezi Mungu! Hotuba yake ilikuwa tamu sana lakini sikumbuki chochote zaidi ya yale ambayo nimekwisha kwambia, lakini nimemuona anasali karibu na Al-Ka'abah, na pia nimemuona kijana moja mwenye sura ya kupendeza ambaye haja-balekhe, akisali pamoja naye. Watu wanasema kwamba huyo ni binamu yake Ali. Pia niliona mwanamke anasali nyuma ya mtu huyu. Watu waliniambia huyo ni mke wake, Khadijah.

SURA YA PILI

Baada ya kumsikiliza kaka yake, Abu Dharr alisema, "Sijaridhishwa na ripoti yako. Nitakwenda huko mimi mwenyewe, nimuone na nimsikilize mimi binafsi."

Abu Dharr alifika Makkah, aliingia kwenye eneo la Ka'abah na akaanza kumtafuta Mtume, lakini wala hakumuona pale, ama kusikia akitajwa. Alikaa hapo hadi machweo ya jua. Ali aliwasili hapo na akapita karibu na pale alipoketi Abu Dharr. Alimuuliza, "Unaonekana kuwa msafiri. Ni kweli?"

Abu Dharr: "Ndio." Ali: "Njoo nifuate."

Ali alimchukua nyumbani kwake. Wote wawili walikuwa kimya wakati wanakwenda nyumbani kwa Ali. Abu Dharr hakumuuliza Ali kitu chochote hadi walipofika nyumbani. Ali alitayarisha mahali pa kulala na Abu Dharr akalala. Kesho yake asubuhi alikwenda tena Ka'abah kumtafuta Mtume. Wala hakumuuliza mtu yeyote ama mtu

yeyote kumwambia chochote. Abu Dharr aliendelea kungoja kwa hamu kubwa hadi mwisho wa siku. Ali alikwenda tena kwenye Al-Ka'abah kama kawaida yake na alipita mbele ya Abu Dharr: mara alipomuona Abu Dharr, alimuuliza: "Kwa nini hujaenda nyumbani hadi sasa?"

Abu Dharr: "Hapana."

Ali: "Vema! Sasa twende nifuate Mimi."

Wote walili walikuwa wanakwenda kimya Ali alipouliza, "kwa nini!

Umekuja hapa kwa sababu gani?"

Abu Dharr: "Ninaweza kukuambia sababu endapo hutamwambia mtu

mwingine."

Ali: "Sema wazi chochote unachotaka kusema. Sitamwambia mtu yeyote."

Abu Dharr: Nimekuja kumuona mtu baada ya kupata taarifa kwamba mtu huyu anajiita yeye Mtume. Nilimtuma kaka yangu azungumze naye. Aliporudi hakunipa taarifa ya kuridhisha. Sasa, nimeamua kumuona mtu huyu mimi mwenyewe."

Ali: Umefika. Sasa ninakwenda pale alipo. Nifuate. Ingia popote nitakapoingia. Endapo nitaona hatari yoyote nitaanza kukiweka sawa kiatu changu, nikiwa nimesimama karibu na ukuta, na nikianza kufanya hivyo, wewe rudi."

2

MAISHA YA ABU DHARR

Abu Dharr anasema, "Ali alinipeleka hadi ndani ya nyumba. Niliona nuru katika umbo la mtu inaonekana hapo. Mara tu nilipo muona, nilivutiwa kwake na nikahisi ninataka kubusu miguu yake. Kwa hiyo, nilimsalimia Assalamu Alaykum." (Alikuwa mtu wa kwanza kumsalimia Mtume wa Uislamu kwa desturi ya Kiislamu, kabla ya kusilimu).

Alijibu salamu, akasema, "Waa Aliakum as Salam, wa rahmatullah

wa Barakatuh. Ndio Unataka nini?"

Nilijibu; "Nimekuja kuwako kwa moyo na imani."

Alinielekeza mambo fulani muhimu na akanitaka nikariri Kalimah

(Shahada) yaani (La ilaha illalah Muhammadun Rasulul lah) nilisoma

hivyo, na kwa hiyo nikaingia kwenye Uislamu.

Baada ya hapo, aliondoka kwenda Ka'abah. Alipofika hapo alipoona kundi kubwa la makafiri wa kabila la Quraishi, alisema kwa sauti kubwa, "Sikilizeni enyi Waquraishi nina shahidilia kwamba Mwenyezi Mungu ni Mmoja na Muhammad ni Mtume Wake."

Sauti hii iliwaogofya Quraishi na kuvunja sanamu lao la Lat na Uzza. Hisia za Quraishi kwamba heshima ya masanamu yao imeshushwa iliwatia wasiwasi sana.

Hatimaye watu walimzunguka Abu Dharr wakaanza kumpiga sana hadi akazirai. Ilibakia kidogo afe lakini Abbas bin Abd al-Mutalib alifika hapo ghafla. Alipoona kwamba mfuasi wa Muhammad alikaribia kufa, alilazimika kumlalia Abu Dharr.

Akasema: "Enyi watu! Nini kimewatokea ninyi? Munataka kumuua mtu mkubwa wa kabila la Bani Ghifar. Mmesahau kwamba nyinyi hufanya biashara na Bani Ghifar na huwa mnatembelea huko mara kwa mara. Hamliogopi kabila lake kabisa!"

Baada ya kusikia hayo, watu hao waliondoka hapo na Abu Dharr ambaye alikuwa anatoka damu, alinyanyuka na kwenda kwenye kisima cha zam zam.

Alihisi kiu sana kwa sababu ya majeraha makubwa na kutoka damu nyingi. kwa hiyo, kwanza alikunywa maji halafu akasafisha mwili

wake. Baada ya hapo alikwenda kwa Mtukufu Mtume huku akigumia. Mara tu Mtume alipomuona katika hali ile, alisikitika sana na akasema, "Abu Dharr! Umekula au kunywa chochote?"

Abu Dharr: "Bwana wangu! Nimeona nafuu kidogo baada ya kunywa

maji ya Zam zam."

Mtume: "Bila shaka maji hayo hutoa nafuu."

Baada ya hapo alimliwaza Abu Dharr na akampa chakula. Ingawa

Abu Dharr aliumia sana kwa sababu ya hotuba yake, bado hamasa ya

dini haikumruhusu aondoke kwenda kwao kimya kimya. Imani yake

ilimtaka awafanye Maquraishii waamini kwamba akili ya

mwanadamu hudharau ushirikina wa uchaji masanamu.

Aliondoka hapo akaenda kwenye eneo la Al-Ka'abah tena. Alisimama sehemu iliyoinuka na akaita kwa sauti ya ushupavu imara. "Enyi watu wa Quraishii! Nisikilizeni! Ninashahidilia kwamba hapana mungu ila Mwenyezi Mungu na ninashahidilia kwamba Muhammad ni Mjumbe wa Mwenyezi Mungu."

Waliposikia hivyo wale wapotovu ambao waliona misingi ya miungu yao inatikiswa na ambao walikasirishwa sana na hotuba yake ya mwanzo, kwa mara nyingine waligutushwa na wakawa katika hali ya wasiwasi na wakageuka kuelekea upande inakotoka sauti na haraka sana walikusanyika na kumzunguka yeye. Walikuwa wanapiga kelele "Muueni huyu Ghifari haraka iwezekanavyo kwani yeye nia yake ni kuwatukana miungu wetu."

Mkusanyiko wote ulisema kwa sauti moja, Mueni Abu Dharr." Kwa hiyo walimpiga Abu Dharr hadi akazirai.

Abbas bin Abdul Muttalib alipoona hivi alijitokeza mbele na kumlalia Abu Dharr kama ilivyofanya jana yake, na akasema; "Enyi Quraishi!

Nini kimewatokeeni kwamba mnamuua mtu wa kabila la Ghifari ingawa mnao uhusiano mzuri na kabila lake na biashara yenu inaendelea vizuri kwa msaada wa kabila lake. Msiendelee kumpiga."

Baada ya kusikia haya, watu wote waliondoka na kumwacha Abu Dharr akiwa amepoteza fahamu. Alipopata fahamu, alikwenda kwenye kisima cha Zam zam! na baada ya kunywa maji alisafisha mwili wake uliokuwa umetapakaa damu.

Abdullah Subaiti ameandika kwamba ingawa Abu Dharr aliteseka sana kwa majeraha lakini hata hivyo aliwalazimisha Quraishi kuwa na maoni kwa mujibu wa ho tuba zake kwamba Uislamu ulikwisha enea kwa watu na uliwavutia sana.

Kwa ufupi Abu Dharr alinyanyuka kutoka kwenye kisima cha Zamzam na kwenda kwa Mtukufu Mtume. Mtume alipomuona Abu Dharr katika hali hiyo alisema, "Ewe Abu Dharr! Ulikwenda wapi na kwa nini umekuwa katika hali hii?" Abu Dharr alijibu, "Nilekwenda kwenye Ka'abah tena. Nilitoa ho tuba tena na nikatapakaa damu kwa kipigo. Sasa nimekuja kwako baada ya kuoga maji ya Zam zam." Mtume akasema; "Ewe Abu Dharr! Sasa ninakuamuru urudi nchini kwako mara moja. Nisikilize! Utakapofika nyumbani kwako, mjomba wako tayari atakuwa amekufa. Kwani hana mrithi mwingine isipokuwa wewe, wewe utakuwa mrithi wake na kuwa mmiliki wa rasilimali yake. Nenda ukatumie mali hiyo kwa kutangaza Uislamu. Baada ya muda mfupi nitakwenda na kuhamia Madina mji wa mitende. Wewe endelea kufanya kazi huko hadi nitakapohamia huko." Abu Dharr alisema, "Ndio! Bwana wangu vyema sana. Nitaondoka hivi karibuni na kuendelea kutangaza Uislamu." Sahih Bukhari, Sura ya Uislamu na Abu Dharr, chapa ya Misri, 1312 Hijiriya.

SURA YA TATU

Baada ya kuingia kwenye Uislamu, Abu Dharr aliondoka Makkah kwenda nchini kwake. Abdullah Subaiti ameandika kwamba Abu Dharr alipoondoka, alikuwa anabubujika imani, kamili, na alikuwa na furaha sana. Alifurahia sana kwamba Mwenyezi Mungu, alimwongoza kwenye imani ambayo imekubaliwa na waliotakasika na dhamira imeridhika nayo na akili inakaribisha kwa ukamilifu.

Aliendelea na safari hadi nchini kwake. Mtu wa kwanza kumsalimia alikuwa kaka yake Unais na pia alikuwa mtu wa kwanza kupata mwamko wa imani yake. Unais alikwenda kubusu miguu ya kaka yake na kusema, "Ewe ndugu yangu! Umepitisha siku nyingi sana Makkah sasa niambie ulichopata huko."

Abu Dharr alisema, "Unais! Nimefanya uamuzi wenye busara. Niliamua baada ya kutafakari sana kwamba lazima nikubali imani ya Muhammad! Ewe Unais! siwezi kukuambia kwamba nilipokutana na Muhammad na kumtazama uso wake, nilihisi kama vile kifua changu kilikuwa kinaongezeka. Moyo wangu ulijaa furaha na akili yangu ililewa imani. Mara nikakariri kalimah-shahada na kukubali Utume wake nilimwomba alifundishe vipengele vya imani. Kwa hiyo alinieleza kanuni za Uislamu. Ewe Unais ninakuomba kwa kweli na kwa moyo safi na nia njema uinamishe kichwa chako kwa unyenyekevu mbele ya Mwenyezi Mungu na uache kuabudu miungu hii iliyotengenezwa na mikono ya watu yenye asili ya mawe."

Aliposikia hivi, Unais alikaa chini huku akiwa ameinamisha kichwa chake na kuanza kufikiri. Alipatwa na hali kama vile umelewa. Unais alikumbuka mambo hayo yote aliyo yaona huko Makkah. Baada ya muda fulani alisema, "Ewe Ndugu! Akili yangu imethibitisha ukweli

wako na mantiki yangu inanieleza nikutii wewe. kwa hiyo sikiliza! Ninashahidilia kwamba hapana mungu ila Mwenyezi Mungu na ninakiri kwamba Muhammad ni Mtume wa Mwenyezi Mungu."

Abu Dharr alifurahi sana kuona Unais anaikubali imani. Alimwambia: "Sasa twende kwa mama yetu." Wote wawili walikwenda kwa mama yao. Baada ya kumuamkia mama yao, Abu Dharr akasema, "Mama yangu mpendwa! Nakuomba unisamehe! Nimekuwa mbali na wewe kwa kipindi kirefu sana. Lakini, nimepata kitu cha nadra ambacho hakuna mtu aliye nacho hapa."

Mama Akamuuliza, "Kitu hicho ni kipi ambacho kinakubainisha wewe?" Abu Dharr alisema, "Hii ni tunu ya imani mama. Nilikutana na mtu huko Makkah ambaye uso wake uling'aa nuru ya uadilifu, hana wa kumlinganisha kwa uzuri wa tabia yake na ukarimu wake. "Yeye husema kweli tupu. Yeye husema kilicho sahihi. Hutenda haki. Maneno yake yanayo busara. Mama! Maadui zake pia humwita mkweli na mwaminifu. Huwaita watu wamwelekee Mwenyezi Mungu ambaye ni muumba wa mbinguni na ardhi na mpangiliaji wa kuweza kudumu kwa ulimwengu huu.

"Nimekubali kumuamini mtu huyu kwa kuvutiwa na mwelekeo wake, maneno yake na semi zake, na Unais pia amekuwa Muislamu. Tumekubali Upweke wa Mwenyezi Mungu na Utume wa Muhammad."

Mama yake Abu Dharr akasema: "Mwanangu, endapo ndio hivyo, mimi pia nina shahidilia kwamba hapana mungu ila Mwenyezi Mungu, na kukiri kwamba Muhammad ni Mtume wa Mwenyezi Mungu."

Abu Dharr alitiwa moyo baada ya kaka yake na mama yake kuingia kwenye Uislamu na sasa alianza kutafakari jinsi ya kuwashawishi

watu wa kabila lake na kuwavuta waelekee kwenye njia iliyonyooka. Baada ya kufikiri sana Abu Dharr alitoka nje ya nyumba yake. Mama na kaka yake pia walikuwa naye. Baada ya kusafiri mwendo mfupi walipiga hema lao karibu na mahema ya watu wa kabila lao.

Usiku uliingia. Wasafiri hawa waliochoka walikuwa wamelala kwenye mahema yao walipohisi kwamba watu wengi wa kabila hilo waliokuwa pale walikuwa wanasimuliana hadithi wao kwa wao na kuelezea matukio mbali mbali. Walikuwa katika mazungumzo mfululizo.

Abu Dharr alipojaribu kusikiliza kwa siri walikuwa wanasema nini, alisikia kwamba walikuwa wanamsema yeye. Baada ya hapo watu waliondoka kutoka kwenye mahema yao na kwenda kwenye hema la Abu Dharr, akamwambia kaka yake, Unais, "Watu wa kabila letu wamekuja karibu na hema letu. Nenda nje ukawaone."

Unais alitoka nje mara moja. Aliwaona vijana wa kabila hilo walikuwa karibu na hema. Walikwenda karibu na hema ili wajue endapo Unais na Abu Dharr walikuwa hapo. Walimsalimia. Baada ya Unais kujibu salamu yao, aliwauliza sababu ya wao kutembelea hapo. Wakasema, "Tumekuja tu kukuona wewe na Abu Dharr."

Unais alirudi ndani na akamwambia Abu Dharr, "Vijana wa kabila letu wamekuja kutaka kujua hali ya safari."

Abu Dharr alisema, "Waambie waingie ndani. Nitazungumza nao. Inawezekana labda nikawasilimisha waanze kumuabudu Mwenyezi Mungu, Aliye Pekee."

Unais alitoka nje na akawaambia, "Ingieni ndani kwani kaka Abu Dharr anawaiteni."

Wote walikwenda kwa Abu Dharr. Mmojawao akasema, "Ewe Abu Dharr! Hatujakuona kwa kipindi kirefu na matokeo yake ni kwamba tunasikitika sana."

Abu Dharr akasema, "Wapendwa wangu vijana! Moyo wangu unayo mapenzi makubwa sana kwenu, na ninawahurumieni."

Mtu mmoja: "Abu Dharr! Ulikuwa wapi kwa muda mrefu hivi? Tumeshindwa kukuona kwa kipindi kirefu."

Abu Dharr: "Nilikwenda Makkah. Nilirudi siku chache zilizopita." Mtu wa pili: "Tunafurahi kwamba ulikwenda Makkah."

Abu Dharr: "Kama mambo yalivyo, nilikwenda Makkah, lakini sikutoa sadaka kwa Hubal wala sikuwasujudia Lat na Uzza. Vijana wangu! Kwa nini nifanye yote haya ambapo ninafahamu kwamba masanamu haya wala hayana uhai, ama kuweza kuumiza au kumnufaisha yeyote? Wala hayawezi kuona ama kusikia, ama kuzuia janga linaloweza kuwapata.

"Sikilizeni! Mimi nimekimbilia kwa Mwenyezi Mungu katika matendo yangu na mambo yangu yote. hakika Yeye ni Peke yake, hana mfano wala mshirika, na ninakiri kwa Mwenyezi Mungu ambaye ni Yeye peke yake anapaswa kuabudiwa, Yeye ni Muumbaji wa kila kitu na mwezeshaji wa kila kiumbe.

Ninawaomba njooni kwangu tuwe pamoja katika mpango wetu wa utekelezaji na mshahidilie Upweke wa Mwenyezi Mungu kama sisi" Waliposikia hivi, watu wote walianza kutetemeka. Mmoja wao

alisema kwa mshangao, "Ewe Abu Dharr! Unasema nini?" Abu Dharr: "Sikilizeni kwa yale ninayowaambieni ingawa siwezi kumuona Mwenyezi Mungu kwa macho yangu bado ninaweza kumuona Yeye kwa jicho langu la kiroho na sikilizeni! Inawezekanaje kitu chochote kinachotengenezwa na mikono ya mwanadamu kiwe na thamani ya kuabudiwa na binadamu? Si busara kuabudu masanamu yaliyotengenezwa kwa mawe na miti, na kuyaomba ili yatutimizie haja zetu.

"Watu wa kabila langu! mnajua kwamba masanamu haya hayana uwezo wowote. Wala hayawezi kuzuia uovu, ama kuwa na nguvu ya kupata manufaa?"

Baada ya kusikia ushawishi huu wa Abu Dharr, watu walianza kunong'onezana wao kwa wao.

Mmoja wao alisema; "Nimekwisha waambieni kwamba huko Makkah, mtu amejitokeza, anajiita yeye ni Mtume na anawaita watu kumwabudu Mwenyezi Mungu Mmoja. Abu Dharr amekutana na mtu huyu, na mahubiri ya mtu huyu yamesisimua sana hivyo kwamba fikra zozote anazozitoa Abu Dharr ni za mtu huyo."

Mtu mwingine akasema; "Hali ni mbaya sana. Sasa tupo hatarini ambayo inatujia kupitia kwa Abu Dharr na mahubiri yake. Tunadhani kwamba endapo ataendelea kuhubiri namna hii, tofauti zitajitokeza kwenye kabila letu na maisha yetu yataharibika. Ni vema twende kwa mtemi wetu Khafaf, tumwelekeze hatari zote zinazoweza kujitokeza, na tumsisitizie na alipatie jambo hili kipaumbele ili tuweze kukabiliana nalo."

Vijana wa kabila la Ghifari waliondoka nyumbani kwa Abu Dharr na walikwenda kumwona Khafaf. Wakati wapo njiani walibadilishana

mawazo wao kwa wao. Mmoja wao alisema, "Abu Dharr ameanzisha ghasia kubwa."

Mwingine akasema, "Itakuwa aibu kubwa sana kwetu kama tutaifumbia macho dhambi hii kubwa ya Abu Dharr. Anaifanyia ufisadi dini yetu waziwazi na kukebehi miungu yetu." Mtu wa tatu akasema, "Ni wajibu wetu kumfukuza kutoka kwenye kabila letu bila kuchelewa hata kidogo, kwa sababu kama tukichelewa kumtenga katika kipindi kifupi tu, atawaelemea vijana wetu, wanawake zetu, watumwa wetu na kuwatia mawazo yake maovu akilini mwao. Endapo inatokea hivyo, tutapata hasara kubwa sana."

Mtu wa nne akasema, "Maoni yako ni sahihi. Lakini, nani atamfunga paka kengele? Huyu ni mtu mashuhuri wa kabila na ni mzee wa kaya. Ninaona kwamba hata Unais anayo mawazo haya haya, na yeye pia ni mtu mwenye kuheshimiwa."

Mtu wa tano akasema, "Hakuna haja ya wasi wasi. Njooni tukamtaarifu Khafaf. Tunao uhakika kwamba Khafaf na watu wengine waungwana wa kabila ndio watakao mfukuza kutoka kwenye kabila."

Mtu wa sita akasema, "Ninatafakari kuhusu mawazo yao. Sina uhakika kama wataweza kuwabadili. Inawezekana kwamba wao ndio watakao badilika na kwenda kwenye njia iliyo nyooka tusijisumbue, lakini na tutafakari kuhusu dini yao. Nisikilizeni! Ninaona kuna ukweli kwenye imani yao. Hata hivyo karibu tutafika kwa mtemi Khafaf. Baada ya mazungumzo yetu na yeye, tunategemea kufikia uamuzi wenye msimamo."

Kwa ufupi, wakizungumza pamoja, watu hawa walifika nyumbani kwa mtemi wa kabila la Ghifar na wakamwambia, "Tumetoka kwa Abu Dharr kuja kwako."

Khafaf: "Abu Dharr amerudi kutoka safari yake ya kutoka Makkah?" Mtu mmoja akasema, "Bwana, Abu Dharr ameasi. Aliwabeza miungu wetu. Anasema kwamba yupo mtu ameteuliwa kuwa Mtume. Kazi yake ni kuwaita watu waende kumuabudu Mungu Mmoja na pia kufundisha mambo mazuri. Abu Dharr haridhiki bila kukubali utume wa mtu huyu na kuendelea na msimamo huo, lakini wakati wote anahubiri kwa watu na kuwaita wote wengine waende kwa Mtume huyo na Mungu wake.

Khafaf aliposikia, alisema, "inasikitisha kuona kwamba Abu Dharr, anawaacha miungu wote, na kutangaza kumuabudu Mungu Mmoja. Ni uovu mkubwa sana na kutia kinyaa.

Ninaona kwamba jambo hili litachochea vurugu kubwa katika kabila letu, na matokeo yake kabila litaangamia. Enyi vijana wangu! Msifanye haraka lakini nipeni, muda wa kutafakari kuhusu jambo hili la Abu Dharr."

Baada ya vijana hao kuondoka na kurudi makwao, Khafaf mtemi wa kabila, alianza kufikiri kwa nini wote walikuwa wanasema kwa kumpinga Abu Dharr. Aliendelea kutafakari usiku wote akiwa kitandani kwake. Hali ilimkanganya sana na hakuweza kufanya msimamo hasa. Lakini akili yake ilikuwa na fikra nzito kuhusu maneno yaliyosemwa na Abu Dharr. Saa nyingi zilipita bila kupata usingizi, na alikuwa anafumba macho yake.

Mtemi Khafaf pia alikumbuka hotuba ya mwanafalsafa wa Kiarabu, Qays bin Saidah, pale sokoni. Alisema kwamba Muumbaji wa ulimwengu bila shaka ni Mmoja na ni Yeye tu ndiye anaye stahiki kuabudiwa. Aliunga mkono kikamilifu maoni ya Abu Dharr kwenye hayo mahubri yake ya kusifika na pia alitamka kwamba fikra za Warqa bin Naufal, Zayd binAmr, Uthman bin Hoverath na Abdallah bin Hajash kuelekea kwenye imani ya Abu Dharr.

Alikuwa katika hali hii ya kustaajabisha ambapo akili yake ilimuongoza na akajisemea mwenyewe, 'Naam! Abu Dharr yu sahihi kwa sababu Qays bin Saida amemuunga mkono na ninao uhakika kwamba Qays hawezi akashindwa kuelewa wala kukubali itikadi yoyote ya uongo. Bila shaka, lazima atakuwepo muongozaji wa dunia hii, na lazima pawepo na nguvu yenye uwezo wa kuendesha mpangilio wote wa ulimwengu na ni dhahiri kwamba miungu wetu wa mawe na miti hawana kabisa uwezo kama huu. Ee Mungu wa Abu Dharr! Tuongoze na utukomboe kutoka kwenye uovu huu na utuweke kwenye njia ya haki."

Wakati ambapo Khafaf alikuwa anafanya uamuzi wake muhimu, siku ilipambazuka hadi jua lilionekana angani pamoja na kuenea kwa mwanga wa jua, pia habari zilizidi kuenea kwamba Abu Dharr, kaka yake na mama yake wote wamerudi kutoka Makkah na wamemuabudu Mungu Mmoja tu.

Pamoja na kuenea habari hizi hasira ilichochewa. Watu walianza kumlaani Abu Dharr na kusema, 'Amepata kichaa na hawezi kuelewa kwamba haya masanamu yetu hutuponya maradhi, yanatupatia riziki na kutulinda. Abu Dharr ni mtu wa ajabu ambaye anatuita twende kwa mungu asiyeonekana! Inaonyesha kama vile Abu Dharr anataka kuanzisha vurumai na matatizo miongoni mwa vijana wetu na kuwapotosha watoto wetu na wanawake wetu. Hakika mtu huyu ni muongo na madai yake si sahihi. Lazima afukuzwe kutoka kwenye kabila."

Mmojawao akasema, "Kwa nini! Unawezaje kuelezea wazo la kumfukuza mtu huyu? Itafanyikaje? Hapana , kamwe! Haiwezekani kutokea. Huyu ni mtu jasiri katika kabila letu."

Baada ya mazungumzo haya watu hao waliamua kutaka wasikilizwe na wazee kuhusu suala hili. Kufuatana na uamuzi wao, waliwaendea

wazee wao kushughulikia jambo hili. Wazee wao waliamua kulipeleka jambo hili la Abu Dharr kwa mtemi. Kwa hiyo, wote walikwenda kwa Khafaf.

Mtemi wa kabila alimtuma mtumwa wake haraka aende kumwita Abu Dharr. Mtumwa huyo alipofika nyumbani kwa Abu Dharr alisema, "Abu Dharr! Wewe na Unais mnaitwa na Mtemi."

Abu Dharr akajibu kwamba alikuwa tayari kwenda kwa mtemi. Mtumwa alipoondoka, Abu Dharr alichukua upanga wake na kuhifadhi kwenye mkanda na alimwambia kaka yake, Unais, "Njoo; twende kwa Khafaf!"

Unais: "Ewe kaka! Nimesikia mambo mabaya yanazungumzwa na watu kuhusu wewe. Nina hofu huu mkutano wetu unaweza usiwe na manufaa, jambo lisilotegemewa linaweza kutokea badala ya mategemeo yetu."

Abu Dharr: "Hapana, siyo. Namjua Khafaf vizuri sana. Ni mtu mwenye hekima. Mwenyezi Mungu amempa hekima. Ni mtu mwenye akili sana miongoni mwa kabila letu."

Ndugu hawa wawili waliendelea kuzungumza hadi wakafika kwa Khafaf. Hapo waliona kwamba watu maarufu wa kabila hilo walikuwa wamekaa kumzunguka Khafaf. Akawaamkia wote Abu Dharr akasema, "Salaamu Alaykum " (Amani iwe kwenu).

Waliposikia maamkizi ya Abu Dharr kwa jinsi ya Kiislamu, wazee wa kabila hilo walikasirika na walisema kwa hasira; "Salamu gani hii ambayo hatujawahi kuisikia kamwe." Halafu mmojawao akasema "Inasikitisha. Hatujui Abu Dharr anakoelekea."

Mtu mwingine akasema, "Hebu mtazame. Amekaa na upanga wake, na hana heshima kwa mtemi." Mtu wa tatu akasema, maneno yako ni sahihi. Lakini, huyu ni mpanda farasi wa kabila letu na watu jasiri wakati wote huwa tayari kwa lolote."

Abu Dharr akasema, "Silikizeni! Ninawaheshimu nyinyi kwa sababu ni watu maarufu wa kabila letu, ambao mnastahili kujivuniwa na kuwaenzi. Salaamu niliyo wapeni ni Salamu ya Kiislamu."

3

MAISHA YA ABU DHARR

Baada ya haya, Abu Dharr na Unais waliketi kwenye nafasi zao wakitazamana uso kwa uso na mtemi, Khafaf. Khafaf alisema kwa sauti ya upole lakini kali, "Ewe Abu Dharr! Ninayo Taarifa kwamba wewe umekuwa na msimamo wa kumuabudu Mwenyezi Mungu Ambaye haonekani. Watu mashuhuri wa kabila letu wamekasirika na msimamo wako huu. Wanasema kwamba Abu Dharr amewatukana miungu yao na anawaita hawana hekima yoyote.

Ewe Abu Dharr! Tunakuheshimu lakini haimaanishi kwamba tupo tayari kustahamili miungu yetu kubezwa. Ninakuomba uache hoja ya mawazo yako ya sasa na urudi kwenye imani ya wahenga wako, au vinginevyo unatakiwa uieleze imani yako kwangu ili niweze kuelewa ukweli wa imani yako. Pia, ninakuhakikishia kwamba nitafikiria kuingia kwenye imani hiyo endapo utathibitisha kwamba imani yako haina shaka zaidi kuliko ya kwetu.

Abu Dharr naye alijibu, "Ewe mtemi wa kabila! Tunakuheshimu na kustahi chochote unacho sema. Lakini, wakati huo huo tunataka kueleza kwamba Mwenyezi Mungu, wa Pekee Ambaye tumeamua kumuabudu na Ambaye tunamwamini, ni huyu huyu ambaye ameumba dunia na mbingu, Ambaye huruzuku viumbe vyote, Ambaye kudhibiti maisha ya viumbe vyote vyenye uhai na Ambaye uwezo wake hauna mipaka.

Masanamu ambayo tumekuwa tunayaabudu hadi sasa, yametengenezwa na mikono yetu kwa kutumia patasi na nyundo. Akili inaweza kuamrisha kwamba yule ambaye ametengenezwa na mikono yetu anaweza kuwa muumbaji wetu, anaweza kuruzuku na tusikiliza dua zetu?

Mwanadamu ni kiumbe bora zaidi kuliko viumbe vya muumbo wote. Inawezekana yeye na heshima yake astahili kuinamisha kichwa chake mbele ya jiwe? Mtemi wangu! Tafadhali tafakari bila upendeleo kuhusu haya ninayosema. Masanamu hayana hata uwezo wa kufukuza adui yao.

Nisikilize, ewe mtemi! Wakati fulani nilikwenda kwa Manat na nikampa sadaka ya kikombe cha maziwa. Nilikuwa bado nipo eneo hilo ambapo mbweha alifika hapo na akanywa maziwa hayo yote na akamkojolea Manat. Tukio hili liliniathiri sana na nilifikiri kwa nini mungu anashindwa kujilinda mwenyewe?

Jambo hili lilinidhihirishia kwamba sanamu haliwezi kuwa mungu. Nina uhakika na kila mtu mwenye akili ataamini kwamba Muumbaji wa mbingu ni bora zaidi kuliko mbingu na muumbaji wa dunia ni bora zaidi kuliko ardhi. Kwa mujibu wa kanuni hii yenye mantiki, masanamu hayawezi kuwa ni bora kuzidi sisi, haina maana sisi kuyaabudu.

Ewe mtemi wangu! Nimekuja kwenye kweli kwamba Mwenyezi Mungu ni Peke Yake Ambaye ni Mumbaji na mwenye kuruzuku ulimwengu, na Muhammad Mustafa ambaye alipelekwa Makkah ni Mjumbe Wake.

"Anazo sifa nzuri kama hizo hivyo kwamba hakuna afananaye Naye hapa duniani. Quraishi ambao ni maadui zake wabaya wanakubali

ukweli wake na uwezo wake. hata wanapojua kuwa Muhammad ni mpinzani mkubwa wa miungu yao na dini yao, wamempatia jina la Sadiq na Amin, kama ambavyo, nimetambua hivi karibuni tu. Sikiliza! Uso wake unang'aa nuru na hekima inatiririka kutoka kwenye maneno yake."

Mara tu Abu Dharr alipomaliza hotuba yake, kelele kubwa ilitoka sehemu zote, "Jinsi gani maneno ya Abu Dharr yalivyo matamu! Kwa hiyo, miungu yetu haisikii na haisemi! Abu Dharr ameidhalilisha imani yetu na anaitukana miungu yetu!"

Kundi moja lilisema kwa pamoja, "Rafiki zangu! Msizungumze mambo yasiyo na mantiki. Kwa uaminifu tunasema kwamba lolote alilosema Abu Dharr linaonekana kuwa sahihi na akili inataka kwamba lazima tukubali ukweli. Tunao uhakika kwamba hatuwezi kupata mwongozo mzuri zaidi kuzidi yale ambayo Abu Dharr ametuletea."

Sauti nyingine ilitokeza: "Nchi ya Arabuni inahitaji muongozaji na inaonyesha kama vile hakuna mwongoaji bora zaidi kuliko huyu ambaye amedhihirishwa na Abu Dharr."

Halafu sauti nyingine ilitokeza, "Hotuba ya Abu Dharr ni ya maana sana." na baada ya hii sauti ya juu sana ilitokeza; kama vile ingetoboa masikio, Ewe Abu Dharr! Ninashahidilia kwamba hakuna mungu ila Mwenyezi Mungu na ninakiri kuamba Muhammad ni Mtume Wake!"

Alipoona hivi, Khafaf, mtemi wa kabila, baada ya kufikiri sana alinyanyua kichwa chake na akawaambia watu wake: "Wapendwa watu wa kabila langu! Nisikilizeni kwa makini. Mmesikia yote hayo aliyoyasema Abu Dharr. Ni wajibu wetu kutafakari kuhusu hotuba

yake kwa uangalifu sana na kwa makini sana na tuweze kuona inayo kiasi gani cha ukweli.

Uamuzi wa haraka haufai. Si busara kutupilia mbali ushauri wa mtu bila kuchunguza. Rafiki zangu! Mnatambua kiasi cha machafuko yaliopo miongoni mwetu na jinsi uhalifu ulivyo zidi ambao sisi tunahusika. Matajiri wanawanyonya masikini na hakuna mipaka katika kufanya dhambi na maovu.

"Mimi nimeamua kwamba lazima nikubali na kuunga mkono yale anayoyasema Abu Dharr. Sasa ni juu yenu nyinyi kujiamulia wenyewe. Sikilizeni nyinyi nyote. Ninashahidilia kwamba hakuna mungu ila Mwenyezi Mungu na Muhammad ni Mtume wake!"

Mara tu Khafaf alipotamka Kalimah (la ila ha illalah Muhammadan Rasulillah) palitokea kelele kubwa ndani ya kabila, Khafaf amekuwa Muislamu. Khafah ameingia Uislamu!"

Haikupita muda mrefu baada ya Khafaf kuingia kwenye Uislamu, hali ya kabila ilibadilika kabisa. Watu walio wengi walisilimu na kuwa Waislamu hapo hapo, ambapo wengine walingojea kukubali kuwa Waislamu mbele ya Mtukufu Mtume baada ya kuwasili huko Madina.

Kwa ufupi, kwa juhudi kubwa ya Abu Dharr watu wengi wa kabila la Ghifar walikubali kuwa Waislamu na palitokeza ukelele wa "Mungu Mkubwa! na "Mungu ndiye Mwenye Kusifiwa!" na jina la Mtukufu Mtume likaanza kutangazwa mchana na usiku.

Baada ya kujaza moyo wa Uislamu kwenye kabila la Ghifari na kuwasilimisha watu na kuingia kwenye Uislamu, Abu Dharr alielekeza umakini wake Asfan. Alipofika huko alianza kuhubiri Uislamu miongoni mwa watu. Kwa kuwa sehemu hii ilikuwa kwenye njia kuu iliyotumiwa mara nyingi na Quraishi na alijenga hisia dhidi yao kwa sababu ya mateso aliyofanyiwa nao alifanya zoezi la nidhamu kali katika kuwafanya kuwa Waislamu. Kundi la Quraishi lilipopita hapo, aliwaeleza habari ya Uislamu na kwa hiyo idadi kubwa ya Quraishi walikubali kuwa Waislamu.

SURA YA NNE

Abdul Hamid Jaudatus Sahar wa Misri ameandika, Uislamu ulienea Madina kama moto wa mbuga ya majani makavu." Kabila la Ghifar lilifurahishwa sana na hali hiyo. Waislamu walipongezana wao kwa wao kwamba makabila mawili ya Aus na Khazraj, ambao walikuwa wasemaji sana, wapiganaji wazuri sana na waunga mkono wazuri sana walikubali kuingia kwenye Uislamu, na pia kwa kuwa Mwenyezi Mungu alikwisha ridhika kuinyanyua dini Yake na alinuia kumsaidia Mtukufu Mtume na kutimiza ahadi yake.

Unais alikwenda kwa kaka yake Abu Dharr akiwa na habari za kufurahisha na akasema "Uislamu umeenea Madina na Aus na Khazraj wamekubali Uislamu!"

Abu Dharr akasema, "Mtume wa Mwenyezi Mungu atakwenda na kuhamia huko baada ya kipindi kifupi."

Unais alimwangalia kaka yake kwa mshangao na alisema, "Umepokea habari zozote za aina hiyo?"

Abu Dharr, "Hapana, wala sina taarifa yoyote kuhusu habari hizi, ama kujua kwamba watu wa Yathrib wamekuwa waumini."

Unais, "Vipi sasa ulijua kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu atahamia Yathrib?"

Abu Dharr, "Aliniambia siku hiyo hiyo nilipokutana naye, kwamba alitarajia kwenda kwenye mji wa mitende na nadhani sehemu hiyo ya Yathrib, Mtume alisema kweli."

Unais, "Inawezekana kwamba kabila lake litamruhusu aondoke hapo akiwa na Waislamu, ili kwamba baada ya matayarisho kamili awashambulie?"

Abu Dharr, "Wanaweza wakamruhusu au wasimruhusu, lakini baada ya kipindi kifupi atahamia huko. Kama mambo yalivyo, ni Mwenyezi Mungu tu ndiye anaye jua ni vipi na lini itatokea."

Abu Dharr alisilimisha kabila lake na kuingia kwenye Uislamu baada ya yeye kuwa muumini. Halafu akaelekeza shughuli hiyo Madina. tangu aliporudi kutoka Makkah hadi kuhama kwa Mtukufu Mtume, Abu Dharr alikuwa anashughulika na kuhubiri Uislamu na aliendelea kufanya juhudi kuipeleka dini ya Mungu kwa umma Mtukufu Mtume aliendelea kufanya kazi yake ya kuhubiri Uislamu na Quraishi waliendelea kufanya kazi yao ya kumtesa Mtume. Walimpa mateso makubwa sana hivyo kwamba hakuwa na uchaguzi mwingine isipokuwa kuondoka nyumbani kwake. Kwa ufupi, kwa amri ya Mwenyezi Mungu Jibril alimwambia aondoke Makkah baada ya kumwambia Ali alale kwenye kitanda cha Mtume.

Alifanya alivyoagizwa. Alimwambia alale kitandani pake na akaondoka, hivyo kwamba Quraishi hawangejua kama hayupo kitandani pake. Baada ya kukaa siku tatu kwenye pango la Hira aliondoka kwenda Madina.

Abu Dharr alikuwa anangojea uhamiaji Madina. Watu wa kabila lake pia walikuwa wanangojea na walikuwa wanauliza mara kwa mara habari za Mtukufu Mtume kwa mtu yeyote aliyetokea sehemu hiyo.

Kuanzia Makkah na baada ya kukaa kwa muda wa siku chache pangoni, Mtume aliondoka kwenda Madina. Kabila la Ghifar lilipopata taarifa kwamba alikuwa kati ya Makkah na Madina walifurahi sana. Abu Dharr alihisi wimbi la neema lilikuwa linakuja. Aliungana na kabila kungoja.

Watu walikusanyika na kumzunguka na walimuuliza kuhusu Mtume wa Mwenyezi Mungu, mwenendo wake na umbile lake alijibu, "Mtamuona baada ya muda si mrefu.

Yeye ni bora kuliko wote na anamzidi kila mtu kwa sifa." Watu walipongojea kwa kipindi kirefu, Abu Dharr alikuwa anaangalia njia, ili awe mtu wa kwanza kuwataarifu watu atakapo wasili Mtume na kutuliza nyoyo za watu na kuondoa hofu iliyokuwa inawaelemea kwa kungojea kwa kipindi kirefu hivyo.

Muda uliendelea kupita. Watu wa kabila la Ghifar walikuwa na shauku kubwa ya kumpokea Mtume. Abu Dharr alipotupa jicho aliona ngamia anakwenda hapo. Watu wote walikuwa wanaangalia macho ya Abu Dharr. Baada ya muda mfupi, Abu Dharr akasema kwa sauti ya kushangaa, "Kwa jina la Mwenyezi Mungu, Mtume anawasili!"

Allamah Subaiti ameandika, "Uso wa Mtukufu Mtume ulikuwa unatoa nuru. Kwa ufupi watu wote walimfuata Abu Dharr, huku wakisema kwa sauti moja, "Mtume wa Mwenyezi Mungu amekuja! Mtume wa Mwenyezi Mungu amekuja!" Abu Dharr alikwenda mbele haraka na akashika hatamu ya ngamia wake.

Watu walianza kusema, "Allahu Akbar." (Mwenyezi Mungu Mkubwa) huku wakimzunguka Mtume kwa hamu kubwa. Wanawake wote, vijana na vikongwe, wavulana na wasichana walikuwa wanashangilia kwa furaha kubwa. Mtume wa Mwenyezi Mungu amewasili! Mtume wa Mwenyezi Mungu amewasili!"

Baada ya hapo watu wa kabila la Aslam walisema, "Pia na sisi tumekuwa Waislamu kama walivyo fanya ndugu zetu wa kabila la Ghifar." Mtume wa Mwenyezi Mungu alifurahi sana na alinyanyua mikono yake kuelekea mbinguni aliomba, "Ee Mola wa ulimwengu! Wasamehe kabila la Ghifari na uwaweke kabila la Aslam salama."

Baada ya hapo Mtukufu Mtume aliteremka kwenye ngamia na akaanza kukariri Quran. Sauti yake iliingia kwenye nyoyo za watu. Halafu akaanza kuhubiri. Watu walikwenda mbele kwa makundi na kutoa kiapo cha utii kwake. Abu Dharr alisimama kwa maringo karibu na Mtume akiwa amefurahi kupita kiasi.

Watu wa kabila la Ghifari walijitokeza mbele na wakasema, "Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu! Abu Dharr alitufundisha yote yale uliyomwambia. Tukasilimu na kuwa Waislamu na tukakiri kwamba wewe ni Mtume wa Mwenyezi Mungu."

Baada ya hapo watu walifurahi sana na walikuwa wanaangalia uso wa Mtume mara kwa mara. Abdul Hamid Jaudatus Sahar ameandika, "Watu walianza kuangalia uso wa Mtume kwa makini, waliona kwamba alikuwa mtu mwenye uso unao ng'aa midomo inayo tabasamu na tabia njema kuhusu umbo lake, hakuwa mwembamba au aliye konda ama mnene. Alikuwa na sura nzuri ya kupendeza.

Macho yalikuwa makubwa na meusi, kope za macho zilikuwa ndefu, nyusi zake nyeusi zilizojikunja mfano wa tao, nywele nyeusi, shingo

ndefu na ndevu nyingi. Alikuwa Mtukufu wakati ametulia na alikuwa anatia moyo kwa heshima wakati anasema. Mazungumzo yake yalikuwa matamu. Wala hakuwa mkimya au msemaji. Alikuwa na sura ya kupendeza sana akiwa mbali na mzuri sana akiwa karibu.

Saizi ya umbile lake ilikuwa ya kati, wala hakuwa mrefu sana kiasi cha kutokupendeza kumwangalia, ama mfupi sana kiasi cha kufikiriwa kuwa mtu duni.

Baada ya hapo Mtukufu Mtume aliondoka kwenda Madina na Abu Dharr aliendela kuishi na kabila lake."

Kutoka hapo, Mtukufu Mtume aliondoka kuelekea Madina. Alipofika Madina, watu walimkaribisha kwa moyo mkunjufu. Mara tu baada ya kufika, alianza kuhubiri ujumbe wa Uislamu. Abu Dharr ambaye hakuweza kumsindikiza Mtukufu Mtume huko Madina aliishi mjini kwake kwa kipindi kirefu sana hivyo, vita kuu tatu za Kiislamu (Ghazawat) vita vya Badr, mwaka wa 2, Hijiriya, Uhud mwaka wa 3 Hijiriya, na Ahzab mwaka wa 5 Hijiriya zilipiganwa hadi mwisho.

Baada ya vita ya Ahzab, aya ya Quran Tukufu ilimlazimisha Abu Dharr kuondoka kwenda Madina. Siku moja alikuwa anashughulika na dua baada ya Swala ya jioni kwenye msikiti wa mjini kwake, ambapo alisikia mtu anasoma kwa sauti Aya (61:10)

"Enyi mlio amini! Nikuonyesheni biashara itakayokuokoeni na adhabu iliyo chungu ."(61:10)

Baada ya kutafakari maana ya Aya hii alipata shauku ya Jihadi na akamwambia Unais, "Nitaondoka kwenda Yathrib kesho."

Unais: "Sawa! Nenda. Mwenyezi Mungu na akufikishe huko Salama!"

Abu Dharr, "Sitarudi. Nitatumia maisha yangu yote katika kumtu-mikia Mtukufu Mtume."

Unais, "Ewe ndugu yangu! Umekuwa muumini wa kweli na imani imepenya kwenye moyo na roho yako. Kabila lako na watu wako hapa wanakutaka sana. Patakuwepo pengo kubwa sana ukiondoka hapa. Nadhani ungeacha mpango wa kwenda Madina na uishi hapa hadi mwisho wa uhai wako."

Abu Dharr; "Mtukufu Mtume ni bora zaidi kuliko watu hawa. Chochote ambacho kimetekelezwa kinatosha. Mtukufu Mtume alipigana Badr, Mimi sikuwa naye. Akapigana huko Uhud Mimi si kuwepo. Hadi lini nitaendelea kulitumikia kabila langu na nikose baraka za kufa shahidi. Yote hayo ambayo yamefanyika mpaka sasa yanatosha. Sasa sitakata tama hata kwa dakika moja kuhusu uamuzi wangu wa kwenda Yathrib."

Unais, "Pendekezo langu ni kwamba wewe uendelee kuishi hapa nyumbani kama kawaida. Mtukufu Mtume atakuita yeye mwenyewe atakapokuhitaji. Wewe angalia walikuwepo watu wengi waliokuwa katika miji ya kwao na waliondoka kwenda Madina baada ya kuitwa na Mtukufu Mtume."

Abu Dharr akasema: "muda wa kungojea umepita. Endapo Mtume hajaniita mimi pia nina wajibu. Sitaendelea kungoja, nitakwenda huko bila kuitwa."

Unais: "Vema! Lakini usifanye haraka. Chukua mahitaji ya muhimu kwa safari."

Abu Dharr; "Sihitaji chochote. Vipande vya mikate mikavu vinanitosha."

Abu Dharr aliondoka nyumbani kwake na kuelekea Madina. Alipofika huko alipata heshima ya kukutana na Mtume na akawa naye.

Alikuwa na desturi ya kulala kwenye msikiti wa Mtume usiku na wakati wa mchana alikutana na watu. Alikula chakula pamoja na Mtume na akaiga maisha yake ya kidunia kwa uchaji Mungu na uadilifu. Alifanya bidii sana kujifunza hadithi za Mtume na kuzihifadhi katika kumbu kumbu.

Baada ya kuifika Madina Abu Dharr aliugua kwa sababu ya mabadiliko ya hali ya hewa. Mtume alipata taarifa ya ugonjwa wake. Akaenda kumuona Abu Dharr na akamwambia; "Abu Dharr! Unatakiwa uishi nje ya Madina kwa muda fulani sehemu ambayo ngamia, kondoo na mbuzi wa taifa huchungwa na uzingatie kwamba usile chochote isipokuwa maziwa wakati wote utakapo kuwa kule."

Mara tu baada ya kupokea amri ya Mtume, Abu Dharr aliondoka kwenda mahali hapo alipoambiwa akiwa na mkewe.

Ugonjwa ulikuwa mkali sana kwa kipindi cha siku kadhaa lakini, ulipungua pole pole akapata afya nzuri hadi akaweza kutimiza tendo la ndoa na mke wake. Sasa, palijitokeza tatizo la upatikanaji wa maji kwa ajili ya josho kubwa la kuondoa janaba kabla ya Swala. Hadi hapo alikuwa hajajua Tayamamu. Kwa hiyo alikuwa hajui la kufanya kwa muda fulani. Hatimaye akili yake ilimwongoza na akaenda kumuona Mtume kwa mwendo wa haraka sana wa ngamia. Mara tu

Mtume alipomuona Abu Dharr alitabasamu na alisema kabla Abu Dharr hajasema, "Abu Dharr! Usiwe na wasiwasi. Maji yametayarishwa kwa ajili yako hapa na sasa hivi. kwa hiyo, msichana aliyekuwa mtumishi wa Mtume alitayarisha maji na Abu Dharr akaoga. Baadaye alikwenda kwa Mtukufu Mtume na aka fundishwa jinsi ya kutumia udongo kwa ajili ya kuchukua Wudhu (Tayamamu)- (Musnad Ahmad bin Hanbal).

Abu Dharr alikuwa anaendesha maisha yake ambapo Vita ya Tabuk ilitokea mnamo mwaka wa 9 Hijiriya. Waandishi wa historia wanasema kwamba Mtume alijua kwamba Wakristo wa Syria walifanya uamuzi thabiti wa kushambulia Madina na wapiganaji elfu arobaini kutoka kwa Harcules, Mfalme wa Roma. Kwa hiyo, Mtume aliamua kuondoka kwenda Syria kama hatua ya tahadhari akiwa na wapiganaji kati ya elfu thelathini hadi arobaini. Alimteua Ali kuwa mbadala wake Madina. Baada ya kutayarisha jeshi lake aliondoka Madina.

Baada ya kuondoka Mtume wanafiki walianza kumdhihaki Ali kwamba Mtume wa Mwenyezi Mungu alimwacha ili kupunguza mzigo wake mwenyewe. Katika kuwathibitishia kwamba wanafiki ni waongo aliamua kwenda kwa Mtume.

Kwa kufuatana na Mtume mahali paitwapo Jaraf na akamtaarifu kuhusu dhihaka ya wanafiki.

Mtume akasema, "Wanafiki ni waongo. Nimekuja hapa baada ya kukufanya wewe kuwa kaimu wangu. Ewe Ali hufurahikii cheo chako cha juu zaidi. Uhusiano wako na mimi ni sawa na uhusiano aliokuwa nao Harun na Musa ila tofauti moja tu ni kwamba hapatakuwepo na Mtume baada yangu. Maana yake ni kwamba Musa alipokwenda kwenye Mlima wa Tur alimteua Harun kuwa kaimu (wakili) wake na yeye (Mtukufu Mtume) alifanya namna hiyo hiyo."

Aliposikia hivi Ali alirudi Madina na Mtume aliendelea na safari ya kwenda Tabuk sehemu iliyokuwa kwenye mpaka wa iliyokuwa Falme ya Roma katika urefu wa vituo kumi kutoka Madina na Dameski. Alipofika Tabuk, alikaa hapo kwa muda wa siku kumi. Wakati wa kuwepo yeye hapo, alimtuma Sariys (jeshi la Uislamu linaloongozwa na mtu mwingine na si Mtume) sehemu zote, na alisisitiza kuwaita watu waingie kwenye Uislamu. Hakuna jeshi lililofika hapo kutoka Roma kwa madhumuni ya vita. Kwa hiyo, alilazimika kurudi Madina.

Wakati wa safari hiyo, siku moja usiku wanafiki walitaka kumuua wakati anapita kwenye bonde la Aqaba Zi Fata, kwa kumuogofya ngamia wake, ambaye angeweza kumwangusha chini, lakini Hudhayfah bin Yaman na Ammar bin Yasir walimwokoa. Baada ya Mtukufu Mtume kuvuka bonde, alimwambia Huzayfah bin Yaman majina ya wanafiki waliotaka kumuua kwenye giza, na akamuamuru kuwa majina hayo iwe siri yake. Masahaba maarufu walikuwemo kwenye orodha hiyo.[1] Kwa mujibu wa Tahzibut Tahzib, watu hao walijaribu kupata majina hayo kutoka kwa Hudhayfah lakini hakufichua.

Hatimaye mmoja wapo wa masahaba hao alikiri mwenyewe, "Uniambie ama usiniambie, kwa jina la Mwenyezi Mungu, mimi nilikuwa miongoni mwa wanafiki hao!" Kwa ufupi, Mtume alirudi Madina wakati wa mwezi wa Ramadhani.

Wakati wa kuondoka kutoka Madina kwa madhumuni ya Vita ya Tabuk, Abu Dharr alikuwa naye. Lakini kwa kuwa ngamia wake alikuwa dhaifu na kukonda, hakuweza kuwa katika msafara. Abu Dharr, hata hivyo, alibaki nyuma ya msafara kwa umbali wa muda wa safari ya siku tatu.

Alijitahidi sana kuwa karibu na Mtume lakini alishindwa. Alihuzunika sana alipotambua kwamba haingewezekana yeye kuwa ndani ya msafara.

Kwa mujibu wa maelezo mengine, alipobaki nyuma, watu fulani walimwambia Mtume kwamba ilikuwa vigumu sana Abu Dharr kuwa naye. Aliposikia hivi, Mtume akasema, "Mwacheni huyo hivyo alivyo. Atafika Inshallah. Kwa hiyo msafara uliendelea na Abu Dharr alizidi kubaki nyuma akiwa amefadhaika na wasi wasi.

4

MAISHA YA ABU DHARR

Wakati mwingine alifikiria kurudi Madina na halafu tena alishawishika kuendelea na safari hadi Tabuk kwa jinsi yoyote ile kwa sababu kuwa nyuma ya Mtume ni hali ambayo ilimtesa sana.

Aliendesha ngamia wake kwa msisimko mkubwa lakini hakuweza kwenda haraka kwa sababu ya udhaifu wake.

Alipogundua hivi, aliteremka kutoka kwenye ngamia na akachukua mzigo wake wote na kubeba mgongoni mwake na akaendelea na safari kwa mguu. Ulikua msimu wa joto kali. Kwa hiyo, ni jambo linalojulikana kwa wasafiri kiasi cha ukali wa kiu ambayo ingempata.

Alikuwa anatembea na mzigo mgongoni mwake wakati ambapo kiu ilikaribia kumwelemea. Tayari alikwisha choka na wakati huo kiu ilifanya hali yake kua mbaya zaidi. Abu Dharr akiwa na kiu kali, alitafuta maji huku na kule akaona maji ya mvua yaliyokuwa kwenye dimbwi. Akafika kwenye dimbwi la maji ambapo alikuwa na kiu sana, na alitaka kunywa maji yaliyojaa kwenye kiganja chake, ambapo ghafla, aliwaza kwamba maji hayo yalikuwa baridi sana na haikuwa vema yeye kunywa maji hayo kabla ya Mtukufu Mtume. kwa hiyo, baada ya fikra hii kuingia akilini mwake akayamwaga maji hayo na akajaza maji hayo kwenye gudulia.

Abu Dharr alikuwa peke yake huku akiwa na kiu kali sana na gudulia lililojaa maji hadi akafika kwenye mipaka ya Tabuk.

Mara tu alipofika kwenye mipaka ya Tabuk, Waislamu walimuona na wakamtaarifu Mtume kuhusu kuwasili kwa msafiri aliyedhikika. Mara moja alisema, huyu ni sahaba wangu, Abu Dharr. Kimbieni, enyi masahaba wangu, na mleteni kwangu. Waliposikia hivyo, masahaba walikwenda haraka kwa Abu Dharr na wakamfikisha kwa Mtume.

Baada ya Mtume kuuliza kuhusu afya yake, akasema, "Ewe Abu Dharr, unayo maji. Kwa nini basi unakiu kali namna hii?"

Abu Dharr; "Bwana wangu, kama unavyoona, maji yapo, lakini siwezi kunywa."

Mtume; "Kwa sababu gani?"

Abu Dharr; "Bwana wangu! Nilipokuwa njiani. Kuja hapa niliona maji karibu na kilima, lakini dhamiri yangu haikuniruhusu kunywa maji haya kwa ajili yako. Mimi nitayaonja baada ya wewe kunywa."

Aliposikia hivi Mtume alisema; "Ewe Abu Dharr! Mwenyezi Mungu Atakuhurumia. Utaishi peke yako na utaondoka hapa duniani peke yako. Utafufuka peke yako mnamo Siku ya Hukumu. Utaingia Peponi peke yako na kundi la watu wa Iraq watapata furaha kamili kwa sababu yako, ni kwamba watakuosha watakuvika sanda na kusalia maiti yako."

Tukio hili si tu linaonyesha mapenzi makubwa ya Abu Dharr kwa Mtume lakini kupitia kwenye tukio hili Mtukufu Mtume kwa wazi kabisa alitabiri matatizo na majanga ambayo yangemfika Abu Dharr katika maisha yake. Ni dhahiri kutoka katika maneno ya mwanachuo wa madhehebu ya Shia yangemtokea Abu Dharr. Amenukuu tukio kutoka kwa Bin Babway kutoka kwa Abbas kwamba siku moja Mtume(s.a.w.w) alikuwa ameketi ndani ya msikiti wa Quba na masahaba wake wengi walikuwa wamemzunguka.

Alisema, "Mtu ambaye atakuwa wa kwanza kuingia kwenye lango la Msikiti huu, atakuwa ametoka kwenye kundi la watu wa Peponi." Baada ya muda mfupi Abu Dharr aliingia kupitia kwenye lango hilo. Alikuwa wa kwanza ambaye alitoka nje akiwa peke yake. Mtukufu Mtume akasema hapo hapo, "Ewe Abu Dharr! Wewe unatoka kwenye watu wa Peponi." Aliendelea kusema, wewe utafukuzwa Makkah kwa sababu ya kuwapenda watu wa Nyumba yangu. Utaishi ugenini na utakufa katika hali ya upweke. Kundi la watu wa Iraq wataneemeka kwa kushughulikia maziko yako na utakuwa pamoja na mimi Peponi."

SURA YA TANO

Historia inashuhudia kwamba Abu Dharr alielimika sana baada ya kuwa Muislam hivyo kwamba hapakuwepo wa kumlinganisha naye miongoni mwa masahaba. Alipata utakaso ulio bora wa imani na unyofu wa moyo hivyo kwamba alihakikisha kwamba yeye ni nguzo ya nuru kwa watu wenye utambuzi. Alizirutubisha akili za watu kwa ushauri, baada ya kuja kwa Uislamu, aliwafundisha watu masomo ya usawa na upendo na aliwafundisha jinsi ya kumtii Mwenyezi Mungu na Mtukufu Mtume.

Maisha yake ya Kiislamu yaliheshimika sana hivyo kwamba hapakuwepo na mtu wa kulingana naye miongoni mwa waumini. Abdulah Subaiti ameandika kwamba Abu Dharr alijipatia sifa sana miongoni mwa masahaba hao ambao walifanya vizuri kuzidi wengine katika uchaji Mungu, kujihini, kumuabudu Mwenyezi Mungu, ukweli,

uimara wa imani na hakuna wa kumfananisha katika kujisalimisha kwa Radhi ya Mwenyezi Mungu. Wakati wa uhai wa Mtume(s.a.w.w) chakula chake cha kila siku kilikuwa kilo tatu za tende na aliendelea hivyo hadi mwisho wa maisha yake.

Anaendelea kuandika Abdullah Subaiti kwamba Abu Dharr alinyanyuliwa juu sana katika maadili na tabia yake hiyo kwamba Mtukufu Mtume alimjumuisha kwenye kundi la Ahlul-bait (watu wa Nyumba ya Mtume) kama alivyo mjumuisha Salman Farsi. Hafiz Abu Naim anasema kwamba Abu Dharr alikuwa msalihina, mtu mchaji Mungu, na alikuwa na moyo ulioridhika. Alikuwa mtu wa nne katika msululu wa kukubali Uislamu. Aliacha maovu yote hata kabla ya kuanza kutekeleza sharia ya Kiislamu. Hili lilikuwa lengo lake alilolihifadhi, kukataa kuwatii watawala dhalimu. Alikuwa imara katika kuvumilia maumivu na huzuni. Alijipatia sifa ya juu katika kuhifadhi hadithi na nasaha za Mtukufu Mtume.

Abu Naim ameandika kwamba Abu Dharr alitoa huduma kubwa kwa Mtukufu Mtume na alipata ujuzi wa vipengele vya imani na utekelezaji akiwa naye, na alijiepusha na maovu. Sifa yake maalum ilikuwa kuuliza maswali kwa Mtukufu Mtume. Alijifunza kuhifadhi maana na fahamu zilizotolewa na yeye (Mtume) na alikuwa na shauku sana kuhusu jambo hili. Kwa ufupi, kwa kadiri alivyoweza, hakuridhika na kuuliza maswali tu lakini pia alikusanya hazina kubwa ya ujuzi wa Kiislamu kwa ajili ya wafuasi wa Uislamu.

Kitendo kingine maarufu cha maisha yake ni kwamba alifuata nyayo za Mtukufu Mtume alizozitilia maanani na kuzithibitisha, na ambazo aliziamuru zifuatwe.

Akaambatana na Imamu Ali baada ya Mtukufu Mtume na hakumkana hata kidogo. Alimfuata na alipata manufaa kutokana na ujuzi mkubwa

wa Imamu Ali. Abu Dharr alihifadhi akilini anasa za mwili, ukarimu, maadili mema na tabia njema za Imamu Ali. Ndio sababu Mtume(s.a.w.w) alisema, "Abu Dharr ni Mtu mkweli zaidi katika taifa hili."

Mahali pengine alisema, "Abu Dharr yu kama Mtume Isa katika ibada ya kujinyima anasa za mwili." Kwa mujibu wa hadithi alisema, "Mtu anayetaka kuona mfano wa maisha na staha ya Isa amwangalie Abu Dharr."

Ni dhahiri kwamba ibada ya dini kama alivyofanya Abu Dharr, haikuwekewa mpaka kwenye Swala peke yake. Alikuwa hodari kiutendaji katika aina zote za ibada. Ni jambo lisilo na upinzani kwamba, kutafakari kuwepo kwa Mwenyezi Mungu na muumbo wake, pia ni ibada kubwa. Abu Dharr alifanikiwa katika ibada hii pia.

Waandishi wa historia na hadithi wanakubaliana kwa pamoja kwamba Abu Dharr alipata kiwango kikubwa cha ujuzi na hii ilikuwa kwa sababu alipata ujuzi kwa moyo ulio nyooka wakati anafuatana na Mtukufu Mtume. Alimuuliza maswali Mtume kila wakati na alijifunza na kuhifadhi majibu yake. Alikuwa na uzoefu mkubwa wa ujuzi wakati anafuatana na Mtume. Mwandishi wa Kitabu Darayatus Rafiah anasema kwamba Abu Dharr alihesabiwa katika safu ya wanachuo wakubwa na washikilia maadili na alikuwa na daraja la pekee la kitaalam. Alikuwa sahaba mwandamizi wa Mtume alikuwa miongoni mwa watu hao waliotimiza agano lao na Mwenyezi Mungu yaani, watu hao walitimiza ahadi ambayo waliahidiana Naye kuhusu wao kuwa wafuasi wa imani iliyokamilika, na alikuwa mmojawapo wa wale watu wanne ambao waumini wote wanawajibika kuwapenda.

Allamah Manazir Ahsan Gilani ametoa maelezo mafupi kuhusu utaalamu wa juu wa Abu Dharr, ameandika, Soma tamko la Ali,

mbora wa majaji miongoni mwa masahaba, na lango la Ujuzi na uhitimishe mwenyewe kwamba anaposema, "Abu Dharr alikuwa na shauku na hamu kubwa ya kupata ujuzi;" anasema jambo lililo sahihi.

Je! Hivi ushahidi huu wa Iman Ali, hauhalalishi madai ya Abu Dharr? Wakati mwingine Abu Dharr mwenyewe alikuwa akisema kwa shauku kubwa, "Tumetenganishwa na Mtukufu Mtume wakati ambapo hakuna hata mmoja wetu ambaye anaweza kujitegemea mwenyewe, kwa sababu bado hatujajua mambo fulani maalum."[2]

Allamah Gilani ameandika kuhusu ujuzi wa Abu Dharr, "Mtu mmoja alimuuliza Imamu Ali, alimfikiriaje Abu Dharr. Akamjibu kwamba wa'aa ilman ajaza fike, yaani 'Yeye, Abu Dharr alihifadhi ujuzi ambao ulimuemea.'

Umesoma na kuona jinsi alivyo kuwa mwepesi kukubali fikira, na wewe mwenyewe unaweza kukisia kutokana na matukio. Ndio maana kila mara alikuwa tayari kutekeleza kwa mujibu wa vile alivyosikia kutoka kwa Mtukufu Mtume. Kama vile alivyo jaribu kusikia kutoka kwa Mtukufu Mtume, kutoka kwa Mtukufu Mtume alitaka kutekeleza kwa vitendo bila kusita hata kidogo. Ilikuwa utashi wa dhati kuona kwamba tendo lake liliendana kwa ukamilifu na ujuzi.

Abu Dharr alinuia sana na alikuwa imara kuhusu kipengele hiki hivyo kwamba hakujali kamwe mamlaka yenye uwezo mkubwa kuliko zote hapa duniani kama ingekuwa kipingamizi chake. Hotuba na ushawishi hazikuweza kumtikisa kutokana na msimamo wake aliokuwa nao.

Akajivunia sifa hii wakati mwingine alisema, "Enyi watu! Mnaona siku ya Hukumu, mimi nitakuwa karibu sana na Mtume(s.a.w.w) na

kundi lake, kwa sababu nimemsikia akisema kwamba atakayekuwa karibu sana naye mnamo siku ya Hukumu atakuwa mtu ambaye ataondoka katika dunia hii katika hali ile ile ambayo alimwacha. Ninaapa kwa jina la Mwenyezi Mungu kwamba sasa hapana yeyote aliye achwa miongoni mwenu ambaye yumo katika hali ile ya wakati wa uhai wa Mtukufu Mtume isipokuwa mimi na sijanajisiwa na kitu chochote kipya. (Tabaqat bin Sad na Musnad ya Ahmad bin Hanbal).

Hili halikuwa dai la haki peke yake tu, lakini pia kiongozi wa dunia na Mtume wa mwisho alishuhudia hivyo.

Allamah Subaiti amesema kwamba mifano ya uadilifu iliyowekwa na Abu Dharr inastahili pongezi. Msimulizi anasema, "Nilipomuona Abu Dharr amejifunika blanketi na amekaa kwenye kona ya msikiti, nilimuuliza kwa nini alikuwa amekaa peke yake hapo? Alisema kwamba alimsikia Mtukufu Mtume anasema, "Ni vizuri kukaa kwenye kona peke yako kuliko kuketi katikati ya kundi la watu wabaya na ni vema kuketi na watu wenye maadili mema kuliko kuketi peke yako. Kimya ni kizuri kuliko kusema jambo baya na kusema jambo zuri ni vema kuliko kunyamaza kimya."

Abu Dharr alisema kwamba Mtukufu Mtume amemwambia mengi kuhusu maelekezo ya maadili mema. Yapo Saba:

Fanya urafiki na watu masikini na jaribu kuwa nao karibu.

Ili uweze kuboresha hali yako waangalie watu wenye hali ya chini

kuzidi wewe na usijilinganishe na watu wenye hali nzuri kuzidi yako.

Usimwombe mtu yeyote msaada wa mambo ya kidunia na ujenge tabia ya kuridhika.

Wahurumie ndugu zako na wasaidie wanapohitaji msaada. Usisite kusema kweli hata kama dunia itakugeukia wewe.

Usijali shutuma za Kafiri kuhusu Mwenyezi Mungu.

Kila mara sema. "La hawla wa la quwwata illa billah." (Hapana mweza isipokuwa Mwenyezi Mungu). Kwa maneno mengine, 'Mwenyezi Mungu ni Uwezo Usiowezwa.

Abu Dharr anasema, baada ya kusema mambo haya, Mtume alisema huku anashika kifua changu, "Ewe Abu Dharr hakuna busara nzuri zaidi kama kupanga mambo vizuri, hakuna uchaji Mungu ulio bora zaidi kama kujizuia na hapana kitu kizuri zaidi kama maadili mema."

Allamah Gihani alikinukuu Musnad ya Ahmad bin Hanbal anataja madili mawili tu miongoni mwa maadili haya yaliyotajwa hapo juu, ambayo yanaendana na kufanya urafiki na watu maskini na kuwatazama watu wenye hali ya chini kuzidi ya kwako, na halafu ameandika: "Kwa kweli, haya ndio marekebisho mazuri kuliko yote dhidi ya maradhi ya kupenda utajiri na kupenda anasa za dunia. idhaniwe kwamba yupo mtu ambaye analo shati la Muislamu na suruali ndefu kuvaa, mkate wa ngano na nyama ya kondoo kwa ajili ya chakula, na nyumba ya udongo wa mfinyazi iliyo pangwa vizuri na safi kuishi humo. Sasa, endapo mtu huyu anajilinganisha na mtu ambaye hana kitu isipokuwa nguo iliyo duni. Mkate wa shayiri nyumba iliyoezekwa kwa mabua, atamshukuru Mwenyezi Mungu kwa hali yake nzuri zaidi na hatateseka kisaikolojia, mateso ambayo angeyapata endapo angejilinganisha na mtu tajiri mwenye nguo za gharama zadi na chakula kizuri. Njia hii ndio bora zaidi kupata kujitosheleza kidunia na manufaa mengineyo ya kidunia.

Lakini wangapi miongoni mwetu wanatekeleza hivi leo? Hata ninaweza kwamba mtu hatapata matatizo yoyote endapo anafuata kanuni hii. Hii peke yake ndio kanuni ya muhimu kwa ajili ya dunia hii na kwa ajili ya Peponi, ambayo imeelezewa katika sentenso ifuatayo" ya Sheikh Sa'd, bingwa wa mashairi wa Iran.

"Nilikuwa nalilia jozi ya viatu hadi nilipo muona mtu asiyekuwa na miguu." Baada ya kupenda utajiri sehemu nyingine ya kupenda dunia ni kupenda daraja na uwezo. Hii inayo hatari zaidi na ni sababu ya uovu wa mpangilio wa dunia. Uharibifu unaendelezwa duniani na watumwa wa utajiri ni pungufu zaid kuliko ule unaosababishwa na watu wenye uroho wa cheo na uwezo.

Sababu halisi ya maradhi haya ni kwamba mtu anapohisi ubora wake katika fani fulani, husahau uwezo wa yule ambaye amemboresha, na hujifikiria yeye ni matokeo ya hivi hivi tu. Halafu hajaribu kuwafanya watu wengine, wako karibu naye, watambue umuhimu wake ambao amejipachika mwenyewe. Akiwa na hitimisho la fikra hii, hutayarisha mipango kwa mujibu wa uwezo wa akili yake. Ni mara chache sana kuonekana kwamba mtumwa wa ulafi na uchoyo ashindwe kufanya kila awezalo kwa lengo la kutimiza kusudio lake. Hujaza akili yake unafiki na wakati wote hubakia kuwepo kwake kupitia njia za halali na mbaya sana. Ubora ambao Abu Dharr alipata au alikaribia kupata, ulikuwa ule wa uchaji Mungu. Palikuwepo hofu kwamba hali ile ingemfanya kuwa na majivuno na kupenda makuu, ambayo baadaye tamaa ya hadhi na heshima huvuruga amani ya hapa duniani na Peponi. Kwa hiyo Mtume alizuia hiyo mapema na akamwambia Abu Dharr, siku moja kwa maneno ya wazi.

Mwenyezi Mungu alisema: "Enyi waja wangu! Wote nyinyi mnazo dhambi isipokuwa hao ambao nimewapa kinga. Kwa hiyo wote lazima msali mkiomba msamaha kwa utaratibu unaokubalika. Nitawasameheni.

Nitasamehe dhambi za mtu anayeniona Mimi kuwa ninao uwezo wa kutosha kumkomboa kutoka kwenye dhambi zake na kwamba ninawaokoa, na kwa mtu aliyeomba msamaha wa dhambi zake kupitia kwenye uwezo Wangu.

Enyi waja wangu! Nyote nyinyi ni wapotovu isipokuwa hao Ninawaonyesha njia iliyonyooka. kwa hiyo lazima mniombe Mimi ili niwaongoze. Wote nyinyi ni masikini na wahitaji isipokuwa wale Ninao wafanya matajiri.

Niombeni Mimi kwa ajili ya riziki yenu na kumbukeni kwamba endapo nyinyi wote walio hai na wafu, wazee na vijana, waovu na waadilifu, muungwana na kujizuia msiombe chochote kutoka kwangu hapataongezeka chochote kwenye milki Yangu. Na endapo wote nyinyi wafu na walio hai, wazee na vijana, waovu na waadilifu mnakusanyika pamoja na kuniomba Mimi niwatimizie mahitaji yenu na kuwatosheleza mahitaji yenu, hapatatokea upinzani wowote kwenye himaya yangu usiolingana hata na wingi wa maji yaliyochukuliwa na ncha ya sindano mtu anapoitumbukiza baharini. Hii ni kwa sababu Mimi ni Mkarimu, msamehevu, Mkuu, Anayetukuzwa na Aliyeko kila mahali.

Mtu yeyote anaweza kujivunia kuwepo kwake au mafanikio yake na utulivu wake baada ya kuamini ukweli wa Utulivu wa Mungu na Ufahari ambao unauona katika hali hii? Hivi mtu yeyote anaweza kuwa na kiburi hata kwa sekunde moja baada ya hapa? Mtu yeyote anayemwamini Mwenyezi Mungu anaweza kuchochea uhaini hapa duniani kwa ajili ya kituo chake cha maisha, heshima, kujionyesha na hudumu baada ya hao? Nani mwenye wazimu anayeweza kujivunia uchaji Mungu wake ambapo kila mmoja wetu ana dhambi?

Pale ambapo utajiri wa watu matajiri upo kwenye udhabiti na mamlaka ya Mwenyezi Mungu; yeyoye huyo anayeonyesha pesa si mpumbavu huyu? Endapo ni sahihi kwamba makubwa na madogo yetu hayawezi hata kwa kuungana kuongeza hata nukta moja upana wa himaya ya Mungu, mtu ambaye ni vumbi la kujaa kiganja tu atajivunia nini? Inapokuwa hii ni hali ya uhuru wake kutokana na utashi hata katika mambo ya mwongozo na ukomavu wa akili anafikiria upendeleo na uwezo a Mwenyezi Mungu kuwa ndio wakala halisi, ni katika misingi gani mhudumu wa dini au mrekebishaji atafikia juhudi zake zitastahili kuthaminiwa?

Ambapo kila kitu ni mali yake na sisi ni masikini na wahitaji, kwa nini basi kiburi hiki na kwa nini ufidhuli huu na majigambo haya?

Hizi zilikuwa amri na hotuba ambazo ziliiingiza maadili ya Mtume Isa kwenye moyo wa Abu Dharr. Hata hivyo, hali ilikuwa hiyo na hata zaidi ya Mtume alivyokuwa na desturi ya kuchokonoa tabia ya kujinyima ya Abu Dharr.

Lakini tunatakiwa kutazamna kwa makini zaidi wa upande huo wa mafundisho yake na nasaha ambamo humo ndimo Uislamu umesimama na kutofautiana na dini zingine zote.

Lazima utajihisi unataka kujaribu kufikiria kwamba kama haya yalikuwa mafundisho ya Mtukufu Mtume, kwa nini Uislamu ulipinga maisha ya utawa na kuyafikiria kuwa ni bidaa zilizoendakezwa na watawa na wahudumu wa kanisa? Nitajaribu kuelekeza usikivu wako kwenye jibu la swali hili. kwa ujumla kujizuia na uchaji mungu maana yake ni kuondoka mijini na kwenda milimani na misituni kuabudu Mwenyezi Mungu katika hali ya upweke. Abu Dharr anaeleza ifuatavyo:

Mtukufu Mtume alimwabia kwamba pia ni jambo zuri kuondoa mawe njiani, kuwasaidia wasiojiweza pia ni hisani na hata lendo la ndoa na mkeo ni kitendo cha fadhila. (Musnad Ahmad bin Hanbal)

Nilimuuliza Mtukufu Mtume kwa mshangao, pia ni sadaka kufanya tendo la ndoa na mke wa mtu, ingawa anatosheleza tamaa yake kwa tendo hili? Endapo mwanamume anatosheleza tamaa yake, pia atapata fidia kwa tendo hilo? Mtume alisema, "Vema, niambie, haitakuwa dhambi endapo ungetosheleza tamaa kwa kufanya kitendo kisicho halali na kilicho haramishwa?" Nilijibu, "Bila shaka."

Akasema, "Nyinyi watu mnafikiria kuhusu dhambi lakini si matendo mema. Kwa kawaida watu wanaoishi maisha ya kushikilia maadili kuacha kufanya kazi ili wajipatie riziki na baadaye pale ambapo mahitaji ya kidunia yanapowabana sana wanaanza kuomba."

"Siku moja Mtume(s.a.w.w) aliniita na akasema, "Unaweza kutoa kiapo cha uaminifu kwamba baada ya hapo patakuwepo Pepo tu inakungojea wewe." Nikajibu, "Ndio" Halafu nikanyosha mkono wangu. Mtukufu Mtume akasema, Ninataka useme kwamba hutaomba kitu chochote kutoka kwa mtu yeyote?" Nikajibu "Sawa" akasema, "hata ule mjeledi unaoanguka kutoka kwenye farasi wako. unatakiwa uteremke chini na kuchukua wewe mwenyewe."

Abu Dharr anasema kwamba Mtukufu Mtume alimwambia, "Usifikirie wema wowote na upendeleo kuwa ni kitu kisichokuwa na thamani na kidogo. Endapo hunacho kitu cha kumpa ndugu yako Muisilamu, angalau ni muhimu ukutane naye huku unatabasamau."

Abu Dharr anasema, "Mpendwa wangu (yaani Mtume) ameniusia kwamba niendelee kuonyesha wema kwa ndugu zangu, hata kama siwezi kutimiza kikamilifu, (Musnad Ahmad bin Hanbal) kwa sababu

ni vigumu sana. Hata hivyo mtu anatakiwa kuwafanyia wema watu wote kadiri iwezekanavyo."

Tabia ya Abu Dharr inadhihiri ambapo tunaona kwamba kila mara yupo na watu fukara na wenye kuhitaji. Alikuwa makini sana kuhusu mafundisho ya Mtume na hakuna miongoni mwa masahaba wenye mioyo migumu ambao hawakuathiriwa na maadili ya Mtume. Alikuwa muungaji mkono madhubuti wa Imamu Ali hivyo kwamba alichota tabia ya kiwango cha juu cha desturi njema za Mtume.

Agizo la Mtume lilikuwa: "Wape watumwa wako na watumishi wako chakula unachokula wewe, na wape nguo unazovaa wewe." (Musnad ya Ahmad bin Hanbal) Na Abu Dharr alifuata utaratibu huo huo. Kila siku aliwapa watumwa wake na watumwa wasichana chakula alichokula yeye na aliwapa nguo alizovaa yeye.


3

4

5

6

7

8

9

10

11