MAOBOLEZO YA KIFO CHA IMAM HUSEIN (A.S)

MAOBOLEZO YA KIFO CHA IMAM HUSEIN (A.S)0%

MAOBOLEZO YA KIFO CHA IMAM HUSEIN (A.S) Mwandishi:
: SHEIKH MUSABBAH SHA'ABANI
Kundi: Imam Husein (A.S)

  • Anza
  • Iliyopita
  • 7 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 8295 / Pakua: 1947
Kiwango Kiwango Kiwango
MAOBOLEZO YA KIFO CHA IMAM HUSEIN (A.S)

MAOBOLEZO YA KIFO CHA IMAM HUSEIN (A.S)

Mwandishi:
Swahili

1

MAOBOLEZO YA KIFO CHA IMAM HUSEIN(A.S)

SAFARI YA IMAM HUSEIN(A.S) TOKA MADINA HADI MAKKA

Baada ya Imam Hasan(a.s) kufariki. Mashia waliokuwa Iraq walimuandikia Imam Husein kumjulisha kwamba wao waniempa baia na wako tayari kumnusuru.

Imam(a.s) aliwajibu kwa kusema: "Baina yetu ma Muawiya upo mkataba kuhusu jambo hili, hivyo haifai kuuvunja mkataba huo ".

Katikati ya mwezi wa Rajab mwaka wa Sitini Hijiriyah Muawiyyah Bin Abi Sufian alikufa na Yazid mwanawe Muawiyyah akachukua mahali pa baba yake, na ile ahadi na makubaliano aliyoyafanya Imam Hasan na Muawiyyah yakavunjwa, kwani usia wa Muawiyyah ulitaka Yazid ndiyo awe Khalifa kinyume na makubaliano kwamba atakapokufa Muawiyyah ukhalifa urudishwe katika nyumba ya Mtume(s.a.w.w) .

Basi ilikuwaje alipochukua Ukhalifa Yazid yule mlevi asiyejali utu wake, mcheza na mbwa, hana akijuacho katika dini kama alivyokiri yeye mwenyewe ndani ya ibara ziftuatazo baada ya kukalia Ukhalifa akasema: "...na kwa hakika nimetawazwa baada yake (Muawiyyah) na wala sitowi udhuru (wa kuacha jambo hili) kutokana na ujinga (nilionao) na wala sijisumbui kutafuta elimu ".[12]

Kitabu hiki kinatolewa na Wizara ya Elimu ya Saud Arabia kwa ajili ya shule za kati kwa wasichana ndani ya sahi ya tatu."[13]

Jambo aliloona kwamba ndiyo maslahi kwake yeye Yazid, ni kuandika barua kumpelekea lbn Ami yake Walid bin Utba ambaye alikuwa ndiyo Gavana wa Madina siku hizo, akamuamuru achukue baia kutoka kwa watu wote na kutoka kwa Imam Husein(a.s) kwa niaba yake yeye Yazid, akasema katika barua hiyo "Iwapo Husein(a.s) atakataa kutoa baia basi muuwe na uniletee kichwa chake".

Walid bin Utba alipoipata barua hiyo alimtaka ushauri Marwan.

Marwan akamwambia Walid "Hakika Husein(a.s) hawezi kumbai Yazid, lakini Iau mimi ningekuwa na cheo kama chako ningemuua."

Baadaye Walid alimwita Imam Husein(a.s) , naye akaja kwa Walid akiwa na watu thelathini miongoni mwao wakiwa ni watu wa nyumba yake na wafuasi wake.

Imam Husein(a.s) alipofika mbele ya Walid, yeye Walid akamjulisha Imam(a.s) juu ya kifo cha Muawiyyah na pia akawa anamlazimisha ampe baia Yazid.

Imam Husein(a.s) akamwambia "Hakika kiapo cha utii (baia) siyo jambo la siri, basi kesho waite watu nasi pia tuite (tutafanya hiyo baia).

Marwan akasema kumwambia Walid "Ewe Amir usikubali udhuru wake, kama ni baia atowe sasa hivi au sivyo muuwe."

Imam Husein(a.s) akakasirishwa na maneno ya Marwan akamwambia "Ewe mwana wa Zarqaa unaniuwa wewe au yeye? Hakika wewe ni muongo tena umefanya jambo Ia uovu (Kutamka hivyo)". Kisha Imam akamgeukia Walid akasema: "Kwa yakini sisi ndiyo watu wa Nyumba ya Mtume(s.a.w.w) , na kwetu ndiyo kwenye kituo cha Ujumbe (wa Mwenyezi Mungu) na Mwenyezi Mungu alileta nusra kupitia kwetu sisi na akaukamilisha Ujumbe wake kwa Ulimwengu kwetu sisi, na huyu Yazid ni mtu mlevi, muuwaji wa nafsi bila sababu, anafanya maovu wazi wazi, kwa hiyo basi watu kama mimi hawawezi kumpa baia mtu kama yeye". Kisha Imam Husein(a.s) alitoka mahala hapo akaenda zake.

Marwan akamwambia Walid: "Unaona ulipinga ushauri wangu". (Sasa Husein amekukatalia wazi wazi) Walid akamkemea Marwan akasema: "Kefule!!! Ulilokuwa umenishauri ni jambo la kuniharibia Dunia yangu na Akhera yangu, Wallahi sipendi kuona Dunia yote inakuwa yangu wakati nitakuwa nimemuuwa Husein eti kwa sababu amesema hatombai Yazid, walasidhani kama ye yote atakayemuuwa Husein kwamba atakutana na Mwenyezi Mungu akasalimika, bali mtu huyo atajikuta siku ya Qiyama mizani yake ni nyepesi (hana chochote) na Mwenyezi Mungu hatomtazama mtu huyo wala hatamtakasa na atapata adhabu kali". (kwa kumuuwa Husein).

Basi Imam Husein alikaa Nyumbani kwake usiku huo ambao ulikuwa ni usiku wa kuamkia Jumamosi tarehe 27 Rajab mwaka wa Sitini.

Kulipokucha akatoka ili apate kujua habari zilizoko mjini, mara akakutana na Marwan, kisha Marwan akasema: "Ewe Abu Abdillah (Imam Husein) mimi ninayo nasaha kwa ajili yako tafadhali nitii kwa nitakayokuambia utafanikiwa".

Imam Husein(a.s) akasema: "Ni nasaha gani hiyo sema niisikie"?

Marwan akasema: "Hakika mimi nakuamuru umtii Yazid kwani jambo halo ni bora kwako na ni bora katika Dini yako na Dunia yako".

Imam Husein(a.s) akasema: "Hakika sisi ni milki ya Mwenyezi Mungu na hakika sisi kwake tutarejea, Eti mimi kumtii Yazid ndiyo itakuwa ni amani kwa Uislamu? Hakika Ummah umepata mtihani mkubwa kwa kuwa na kiongozi mfano wa Yazid".

Mazungumzo baina yao yalikuwa mengi kiasi ambacho Marwan aliondoka il-hali kachukia.

Jioni ya Jumamosi Walid alituma watu waende kwa Imam Husein(a.s) ili aje afanye baia.

Imam Husein akawaambia: "Ngojeni kutapokucha kesho kisha mtaona ni lipi la kufanya, nasi pia tutaona la kuamua". Wakanyamaza wala hawakuendelea kumlazimisha afanye baia.

Basi Imam Husein alitoka usiku wa kuamkia Jumapili tarehe 28 Rajab kuelekea Makkah, pamoja na wanawe na ndugu zake na kikundi cha watu wa nyumba yake, akaondoka Madina hali anasoma Aya ya Qur'an isemayo: "Akatoka katika mji huo hali anakhofu, anangoja (lipi litamfika) akasema: "Mola wangu niokowe kutokana na watu madhalimu ". Sura Al-Qasas: 21.

Alipita njia kuu iliyo mashuhuri, akaombwa abadili njia kukwepa kufuatwa na adui kama alivyofanya Ibnuz-Zubair, akakataa kufanya hivyo na akasema: "Sitaiacha njia hii mpaka Mwenyezi Mungu aamuwe chochote atakachoniamulia".

Imam Husein(a.s) alifika Makkah usiku wa kuamkia Ijumaa tarehe tatu Shaaban, na aliingia Makkah huku akisoma Aya ifuatayo:

"Na alipoelekea upande wa Madiyan alisema: Huenda Mola wangu ataniongoza njia iliyo sawa ". Sura Al-Qasas Aya 22.

Alikaa hapo Makka kuanzia Mwezi huo wa Shaaban mpaka mfungo pili na siku nane za Mwezi wa mfungo tatu, kisha aliona usalama wake pale Makka in mdogo.

Kwa hiyo Imam Husein hakuwa na utulivu tena wa kumuwezesha kukamilisha Ibada yake ya Hija kwa kuhofia kukamatwa na majasusi ambao wangemkamata hapo Makka na kumpeleka kwa Yazid Bin Muawiyyah.

Hivyo basi akafungua Ihram yake na akaifanya kuwa ni Umra.

Imam Husein(a.s) akautoka Mji wa Makka ambao in Mji wa Mwenyezi Mungu uliotukuka, katika Mji huo ndege na wanyama wanapewa amani waingiapo, basi vipi kwa mjukuu wa Mtume(s.a.w.w) kutishiwa amani yake?

Alitoka Makka kama alivyo uacha mji Mtukufu wa Madina mji wa babu yake ambaye in Mtume wa Mwenyezi Mungu, hali anakhofu mwenye kungojea lipi litamtokea.

MAJLISI YA SITA

YALIYOTOKEA MAKKA BAADA YA IMAM HUSEIN(A.S) KUFIKA HAPO

Ilipofahamika kwa wakazi wa Makkah kwamba, Imam Husein(a.s) yupo Mjini hapo, wakazi wa Mji huo walianza kumtembelea kwa wingi.

Miongoni mwa watu waliofika kwake ni pamoja na wageni kutoka sehemu mbalimbali waliokuja Makka kufanya Umra.

Ikawa watu wanapishana, hawa wanatoka na wengine wanaingia. Pia Abdallah Bin Abbas na Talha Bin Zubair nao walifika kumuona Imam Husein(a.s) .

Wawili hawa walimtaka Imam Husein(a.s) akae hapo Makkah na anyamaze. (Asijihusishe na mambo ya Ukhaiifa).

Imam aliwajibu akasema, "Hakika Mtume wa Mwenyezi Mungu aliniamuru jambo ambalo mimi nitalitekeleza ".

Vile vile Abdallah bin Omar bin Khatab alifika kwa Imam Husein(a.s) na kumtaka afanye mapatano na Yazid bin Muawiya bin Abi Sufiyan.

Imam(a.s) alijibu akasema, "Ewe Baba Abdur-Rahman, unafahamu kwamba Dunia hii kwa uovu uliyomo ni pamoja na kuvinyanyasa viumbe vitukufu vya Mwenyezi Mungu, na elewa pia kwamba kichwa cha Mtume Yahya bin Zakariya kilitolewa na kuwa kama zawadi kwa mtu muovu miongoni mwa watu waovu wa Kiban-Israil?" Akaendelea Imam(a.s) kusema, "Je unafahamu kwamba, wana wa Israil walikuwa wakiwauwa manabii sabini katika kipindi cha kuchomoza Al-fajiri na kutoka jua, kisha baada ya kufanya tendo hili, huenda wakakaa sokoni na kufanya biashara zao za kununua na kuuza kama kwamba hawakutenda chochote cha uovu? Lakini Mwenyezi Mungu hakufanya haraka kuwaadhibu kutokana na maovu yao bali baadaye aliwaadhibu adhabu kali, basi muogope Mwenyezi Mungu ewe baba Abdur-Rahman na wala usiache kunisaidia".

Katika mji wa Al-Kufah, habari za kifo cha Muawiyya zilipowafikia watu wa Mji huo pia kutawazwa kwa Yazid kuwa ndiyo Khalifa wao hawakupendezwa.

Na waIipofahamu kuwa Imam Husein amekataa kumpa baia Yazid na kwamba yuko Makkah, Mashia walikusanyika katika nyumba ya bwana Suleiman bin Surd AI-Khuzai.

Walipokamilika Bwana Sulaiman alisimama akasema, "Kwa hakika Muawiyya amekufa na Husein amekataa kuwatii waliotwaa madaraka na ameondoka Madina sasa yuko Makkah, nanyi ndiyo wafuasi wa baba yake basi ikiwa mnajua kwamba mnaowajibu wa kumsaidia na kumpiga adui yake na kuziangamiza nafsi zetu kwa ajili yake muandikieni barua aje, na kama mtaogopa kushindwa basi musimuite mtu huyu".

Wakajibu kwa kusema; "Sisi tuko tayari kutoa nafsi zetu kwa ajili yake na tutampiga adui yake".

Sulaiman akasema, "Basi muandikieni". Wakamuandikia Imam Husein(a.s) .

BISMILLAAH RAHMAN RAHIM

Barua kwa Husein bin Ali(a.s) kutoka kwa Sulaiman bin Surd na Musayib bin Najiya na Rifaat Shadad na Habib bin Mudhhir na Mashia wake Waumini Waislam katika watu wa Al-Kufah.

Amani iwe juu yake, hakika tunamtukuza Mwenyezi Mungu ambaye hapana Mola ila yeye.

Ama Baad:

Sifa njema ni zake Mwenyezi Mungu ambaye amemuangamiza adui yako aliyekuwa jeuri na mpinzani wa haki huku anaijua.

Adui huyo aliukandamiza Umma huu kwa nguvu, akapora mali za Umma, akautawala Umma hali yakuwa hautaki kutawaliwa naye, kisha akawa anauwa watu wema katika Umma huu na kubakisha watu waovu mali ya Mwenyezi Mungu akaifanya ni ya kutumiwa na matajiri na wakatili, basi na alaaniwe kama walivyolaaniwa watu wa Thamud.

Kwa hakika sisi hatuna kiongozi wa kutuongoza, basi njoo ili Mwenyezi Mungu apate kutuunganisha katika haki kwako wewe.

Na huyu Nuuman (Gavana wa Muawiyya hapo al-Kufah) sisi hatushirikiani naye kwenye Ibaada ya Ijumaa wala hatutoki pamoja naye kwenye sala ya Idi.

Iwapo tutafahamu tu kwamba tayari umeshafika mjini hapa, basi tutamtoa tumrudishe Shamu Insha-Aallah.

Amani iwe juu yako ewe mwana wa Mtume wa Mwenyezi Mungu na pia amani imshukie Baba yako, wala hapana hila wala nguvu isipokuwa vitoke kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu."

Kisha barua hiyo wakapewa Mabwana Abdallah bin Masmaa Al-Hamadani na Abdallah bin Wail waipeleke Makkah na wakawaamuru kwenda mwendo wa haraka.

Baada ya siku mbili kupita tangu walipotuma barua yao, watu wa Mji wa Al-Kufah waliwatuma Mabwana wafuatao.

1. Qais bin Mas-har As-Saidawi

2. Abdalla na Abdur-Rahman watoto wa Shadad Al-ar-habi.

3. Ammarah bin Abdallah Al-Saluli

Waliwapatia barua zisizopungua mia tano kila mtu.

Baada ya siku mbili tena wakawatuma Mabwana Hani bin Haniy As-Subai na Said bin Abdallah Al-Hanafi waende kwa Imam Husein(a.s) kumpelekea barua iliyokuwa na maneno yafuatayo.

BISMILLAHI RAHMAN RAHIM

Kwa Husein bin Ali(a.s) barua kutoka kwa wafuasi wake miongoni mwa Waumini na Waislamu.

Ama baada salaam:

Njoo haraka, kwa hakika watu wanakusubiri, hawana rai nyingine ila kukusubiri wewe.

Basi fanya haraka tena haraka sana"

Barua kwenda kwa Imam Husein(a.s) zilifuatana mfululizo kiasi cha kufikia barua kumi na mbili alfu.

Pamoja na wingi wa barua na kuhimizwa kote alikohimizwa ndani ya barua hizo, Imam Husein(a.s) alikuwa mzito kuwajibu watu hao.

Siku moja ilitokea zikamfikia barua mia sita wajumbe waliotumwa wote wakakutana kwa Imam Husein katika kipindi hicho hicho.

Imam Husein(a.s) akawauliza kuhusu hali ya watu ilivyo huko watokako, kisha akawaambia mabwana Hani na Said bin Abdallah al-Hanafi, "Hebu niambieni ni kina nani hasa waliojumuika kuniandikia barua hii?

Mabwana hawa wakamfahamisha Imam Husein hali halisi ya watu wa Al-Kufah ilivyo na wakamtajia pia watu wenye msimamo na rai ya kumwita yeye Imam(a.s) .

Basi baada ya kutoshelezwa na maelezo ya mabwana hawa, Imam(a.s) alisimama akaswali rakaa mbili halafu akaandika barua ifuatayo.

BISMILLAAH RAHMAN RAHIM

Barua toka kwa Husein Bin Ali, kwenda kwa Watukufu Waumini na Waislamu.

Ama baad, hakika Hani na Said wamenifikia wakiwa na barua zenu, nao ni watu waliofika mwisho miongoni mwa wajumbe wenu niliowatuma.

Kwa kweli niineyafahamu yote mliyoyaeleza, na jambo muhimu mlilozungumza ni kwamba, "Hakika sisi hatuna kiongozi, basi njoo huenda Mwenyezi Mungu akatuimarisha kwenye haki na uongofu kupitia kwako".

Mimi ninanituma ndugu yangu na ibn ammi yangu naye ni miongoni mwa watu wa nyumba yangu (Muslim bin Aqiil) aje huko. Basi iwapo ataniandikia kuniarifu kuwa rai za viongozi wenu na watu bora miongoni mwenu zimeafikiana kama ambavyo wajumbe wenu walivyonijulisha, na nilivyosoma barua zenu, basi mimi nitakuja huko haraka apendapo Mwenyezi Mungu Mtukufu.

Kwa Yaqin naapa, "Hawi mtu ni Imam (kiongozi wa haki) ila yule anayehukumu kwa mujibu wa Qur'an, mwenye kusimamia haki, anayeishi kwa mujibu wa mafundisho ya dini ya haki (Uislamu) mwenye kuifunga nafsi yake katika dhati ya Mwenyezi Mungu.

Wasalaam.

Baada ya kuandika barua hiyo, Imam Husein(a.s) alimwita nduguye Bwana Muslim bin Aqiil na akamtuma aende Al-Kufah, afuatane na mabwana Qais bin Mas-har As-Saidawi, Ammaarah bin Abdallah na Abdallah na Abdur-Rahman watoto wa Shadad Al-Arhabi.

Imam(a.s) akamuusia nduguye kumcha Mwenyezi Mungu na awe mpole pia asizungumze sababu za yeye kwenda huko.

Mwisho alimtaka afanye haraka kwenda, kwani yaonesha watu wameshikamana pamoja juu ya kumtaka Imam Husein(a.s) kwenda huko.

Muslim bin Aqiil aliondoka kuelekea AI-Kufah kupitia Madina, mahala ambapo alipofika, aliingia katika Msikiti wa Mtume(s.a.w.w) akaswali kisha aliwaaga watu wa nyombani kwake na wangine aliopenda kuwaaga. Baada ya hapo aliondoka mpaka Al-Kufah na akafikia katika nyumba ya bwana Mukhtar bin Ubaid At-Thaqafi. Mashia wa Al-Kufah walipopata habari za kuwasili kwa Muslim bin Aqiil, wakawa wanapishana katika nyumba ya Mukhtar ili waonane naye, na kila wakikusanyika kikundi huwasomea barua ya Imam Husein, kitu ambacho kilikuwa kikiwafanya walie.

Wakampa baia Muslim bin Aqiil watu wapatao elfu kumi na nane.

Muslim bin Aqiil alipoiona hali hiyo kutoka kwa watu wa Al-Kufah, alimuandikia Imam Husein(a.s) kumjulisha na kumtaka aende huko.

Mashia waliendelea kumtembelea Muslim bin Aqiil, mpaka Nuuman bin Bashir aliyekuwa Gavana wa Al-Kufah wakati wa Muawiyya na baadaye katika kipindi cha Yazid, akautambua mkusanyiko huo. Pamoja na kutambua hali hiyo, Nuuman bin Bashiri hakumfanyia lolote Ia ubaya Muslim bin Aqiil.

Lakini baada ya muda kupita, Abdallah bin Muslim bin Rabia Al-Hadhrami ambaye alikuwa mfuasi mkubwa wa bani Ummaya, akamuendea Nuuman bin Bashir akamwambia, "Hakika yote uyaonayo yanatendeka hapa hayana mafanikio kwako ila utapoteza madaraka, na msimamo unaouonyesha baina yako na adui yako ni msimamo wa watu wanyonge".

Kisha huyu Abdallah alimuandikia barua Yazid na akamuambia "Hakika Muslim bin Aqiil amefika hapa Al-Kufah, na watu wamempa baia kwa niyaba ya Husein, basi iwapo wewe unaitaka nchi hii ibaki mikononi mwako, mlete mtu imara atakayesimamia maslahi yako, na atafanya vile ambavyo wewe unamfanyia adni yako, kwani Nuuman ni mtu dhaifu au pengine anajifanya dhaifu."

Nao kina Ammarah bin Uqba na Omar bin Saad, kila mmoja alimuandikia Yazid barua mfano wa ile aliyoandika Abdallah.

Barua hizi zilipomfikia Yazid, mara moja akamuandikia Ubaidullah bin Ziyad aliyekuwa Gavana wa Basra akamjulisha kwamba, kuanzia sasa yeye ni Gavana wa al-Kufah na amemkabidhi nchi hiyo.

Kisha Yazid alimjulisha lbn Ziyad Khabari za Muslim bin Aqiil na akamsisitiza kumkamata na hatimaye amuuwe.

Ubaidullahi bin Ziyad aliyelaaniwa, aliondoka haraka kutoka Basra kuelekea Al-Kufah na akamkabidhi madaraka ya hapo Basra nduguye aliyekuwa akiitwa Athuman.

Ubaidullahi aliingia Al-Kufah usiku, na watu wakadhani kuwa ni Imam(a.s) , wakafurahia na kumsogelea. Walipotambua kwamba kumbe ni lbn Ziyad walitawanyika na kumuacha, naye akaenda hadi kwenye jumba la utawala wa bani Umayya akalala mpaka asubuhi.

Kulipokucha alitoka akaanza kutishia na kuonya kwa ukali wale wanaomuunga mkono Muslim bin Aqiil. Muslim bin Aqiil aliposikia habari za vitisho vya Ibn Ziyad akachelea usalama wake na akaenda nyumbani kwa Bwana Hani bin Urwa mahali ambapo alipewa hifadhi.

Baada ya vitisho na maonyo ya ibn Ziyad hali iligeuka ikawa mbaya sana, kiasi cha kuwafanya watu waliokuwa wamempa baia Muslim bin Aqiil wahitilafiane na wakavunja baia yao, wala hawakuthubutu tena kujitokeza kumtetea Muslim bin Aqiil na ahadi yao ya kumsaidia wakashindwa kuitimiza.

Kwa hakika kilikuwa kipindi kigumu kwa Muslim bin Aqiil, kipindi chenye mateso na tishio la kuuawa. Ni wakati mgumu kwa kuwa waliokuwa wamemuahidi kumsaidia na kumhifadhi walimtelekeza. Kutelekezwa alikotelekezwa Muslim bin Aqiil kulitoa nafasi kwa adui yake kuzidisha uovu wake dhidi yake na ikafikia Muslim bin Aqiil kuwa anasakwa kila mahali na kuzinngirwa barabara katika kila upande hali ya kuwa mpweke hana wakumsaidia.

Muslim bin Aqiil alipata mtihani unaowafika watu wema na alivumilia kungoja matokeo kutokana na vitisho vya panga za maadui zake.

MAJLISI YA SABA

YALIYOTOKEA AL-KUFAH BAADA YA IBN ZIYAD KUFIKA HAPO

Ibn Ziyad alipokwisha wasili katika mji wa AI-Kufah, alijiimarisha kwa kutawanya majasusi kufuatilia nyendo za Muslim bin Aqiil. Matokeo ya ujasusi huo yalimfanya yeye lbn Ziyad afahamu kuwa Muslim bin Aqiil yuko katika nyumba ya Bwana Hani.

Kwa hiyo lbn Ziyad aliwaita mabwana Muhammad bin Al Ashath na Hasan bin Asma bin Kharijah na Amru bin Al-Hajaaj akawaambia, "Ni kitu gani kinamfanya Hani asije kwetu (kutusalimia)?"

Wao wakamjibu, "Hatujui lakini inasemekana ni mgonjwa". lbn Ziyad akasema "Habari hizo nazifahamu, lakini pia nafahamu kwamba kesha pona na kwamba yeye mara kwa mara anaonekana mlangoni kwake amekaa, na lau ningefahamu kuwa bado anaumwa bila shaka ningelimtembelea kumjua hali".

Ibn Ziyad aliendelea kuwaambia, "Nendeni mkamwambie asiache kufanya wajibu wake juu ya haki yetu, (kutoa baia) hakika mimi sipendi kuuona ufisadi mbele yangu unaotokana na mtu mtukufu miongoni mwa Waarabu mfano wake yeye Hani".

Ilipokuwa jioni, mabwana hawa wakaenda nyumbani kwa Bwana Hani na wakasimama mbele ya mlango wa nyumba yake wakamwambia, "Ni kitu gani kinachokuzuia usikutane na Amiri (lbn Ziyad) kwani yeye amekutaja na amesema lau ningefahamu kwamba (Hani) anaumwa ningelimtembelea kumjua hali".

Hani akasema, "Ni maradhi ndiyo yanayonizuia nisiende kukutana naye".

Wale mabwana wakasema kumwambia Hani, "Hakika zimeshamfikia habari kwamba wewe kila jioni unakaa mlangoni nyunbani kwako, naye anakuvumilia kwa hilo, na fahamu kuwa mtawala hawezi kuendelea kuwavumilia watu mfano wako, kwani wewe ni kiongozi wa watu wako, nasi tunakuapia ukweli ulivyo twende pamoja mpaka kwa Ibn Ziyad".

Waliendelea kujadiliana naye mpaka wakamshinda, kisha aliagiza mavazi yake akavaa na hatimaye akaomba aletewe nyumbu wake akapanda na wakaondoka. Walipolisogelea jumba Ia Ibn Ziyad Hani alihisi kutatokea mambo ambayo si mazuri kwake kama ambavyo tangu mwanzo alikuwa akihisi hivyo. Hani akamwambia Hasan bin Asma bin Kharijah, "Ewe mtoto wa ndugu yangu, kwa kweli mimi ninayohofu kubwa juu ya mtu huyu wewe unaonaje"?

Ibn Kharijah akasema, "Ewe ami yangu mimi siogopi chochote juu yako, usianze kutoa nafasi ya mashaka kwa nafsi yako".

Kwa bahati mbaya Hasan alikuwa hakufahamu dhamira na lengo la Ibn Ziyad dhidi ya Bwana Hani. Basi Hani (Mwenyezi Mungu amrehemu) akaja pamoja na jamaa hao mpaka wote wakaingia kwa lbn Ziyad. lbn Ziyad alipomuona Hani akasema, "Muhaini kaletwa na miguu yake mwenyewe".

Hani akasema, "Unakusudia nini kusema hivyo ewe Amir".

Mjadala baina yao ulipokuwa mrefu, na Hani hakukubali madai dhidi yake, lbn Ziyad alimwita Ma-Aqal ambaye alipata kuwa mtumwa wake, akaja akasimama mbele yake.

Huyu Ma-Aqal alikuwa jasusi wa ibn Ziyad na alikuwa akipeleleza nyendo zote za kina Hani na Muslim bin Aqiil hali ya kuwa wao hawana habari kwamba yule ni jasusi, kutokana kuwa akidhihirisha upendo na nia njema kwa kizazi cha Mtume(s.a.w.w) , hivyo basi alifahamu mengi kuwahusu wao.

Hani alipomuona mtu huyo, ndipo alipotambua kwamba alikuwa nijasusi la ibn Ziyad na kuwa mambo yao yote amekwisha yafikisha hapo, na amefaulu kumtumbukiza mikononi mwa ibn Ziyad.

Hali ilivyokuwa hivyo, Hani akasema kumwambia lbn Ziyad, "Mwenyezi Mungu amfanye mwema Amir, naapa kwa jina la Mwenyezi Mwigu kwamba, Muslim bin Aqiil sikumwita mimi lakini alinifikia bali ya kuwa anaomba ulinzi wangu nikamkubalia kumlinda, na niliona haya kumkatalia, na niliingiwa na utu ambao ulimlazimisha kumkaribisha, na sasa hebu nipe nafasi ili nirudi nikamuamuru atoke nyumbani mwangu aende apendako ili nijitoe kuwa mimi ni mdhamini wake, na kisha nitarudi nije nikupe kiapo changu cha utii."

lbn Ziyad akasema, "Wallahi hutoki hapa isipokuwa uniletee huyo Muslim Bin Aqiil". Hani akasema, "Wallahi sitakuletea wataka nikuletee mgeni wangu kisha umuuwe"?

lbn Ziyad akasema, "Wallahi naapa kuwa lazima utaniletea mtu huyo."

Hani naye akajibu, "Wallahi sikuletei hata kidogo".

Majibizano baina ya wawili hawa yalipozidi, bwana mmoja aitwaye Muslim bin Amri Al-Baahili akasema, "Mwenyezi Munga na amfanye mwema Amir, (Amir) hebu niachie nafasi mimi na yeye nizungumze naye. Akasimama yeye na Hani sehemu fulani humo ndani, kiasi kwamba Ibn Ziyad anawaona na anasikia wanachokisema.

Wakati mazungumzo yao yanaendelea, mara sauti zao zikapanda juu zaidi, kisha Bwana Al-Baahili akasema, "Nakuapia Mwenyezi Mungu ewe Hani usijiuwe mwenyewe, na wala usilete balaa kwa jamaa zako, Wallahi hakika mimi nakuona ni mtu muhimu sipendi kuona unanawa, mtoe huyu (Muslim bin Aqiil) uwape watawala, kwani jambo hilo la kumtoa siyo unyonge wala aibu bali unamtoa kwa mtawala (ataamua Ia kumfanya)".

Hani akajibu, "Wallahi kumtoa Muslim bin Aqiil kwangu mimi ni dalili za unyonge na aibu, nimtoe mgeni wangu na isitoshe ni Mjumbe wa mjukuu wa Mjumbe wa Mwenyezi Mungu hali nikiwa ni mzima mwenye nguvu na ninao wasaidizi wengi, Wallahi naapa japo hata ningekuwa peke yangu sina wakunisaidia nisingemtoa (Muslim bin Aqiil) mpaka nife kwa ajili yake".

Al-Baahili akawa anamsisitiza Hani amkabidhi Muslim kwa lbn Ziyad, lakini Hani hujibu, "Wallahi simtoi kamwe".

lbn Ziyad akawa ameyasikia hayo akasema, "Msogezeni hapa karibu yangu", Hani akasogezwa kisha lbn Ziyad akasema kumwambia Hani, "Wallahi lazima uniletee huyo Muslim vinginevyo nitaikata shingo yako".

Hani akasema, "Kama utaniua fahamu wazi utakuwa umewasha moto wa fitna nyumbani kwako".

Akasema: Ooo! Ole wako nakuonea huruma, unanitishia hiyo fitna"?

Kipindi hicho Hani alikuwa akidhani kwamba nduguze na jamaa zake watamsaidia.

Baada ya lbn Ziyad kutamka maneno yale akasema, "Msogezeni kwangu" akasogezwa, kisha lbn Ziyad akatoa fimbo ambayo alianza kumpiga Hani puani na usoni mpaka pua ya Hani ikakatika na nyama za usoni mwake zikachanakanchanika, damu zikawa zinamvuja na kutiririka kwenye nguo zake, na wala hakuacha kumpiga mpaka ile fimbo ikavunjika.

Naye Hani baada ya kutendewa haya, alinyoosha mkono akikusudia kuuchukua upanga wa askari moja aliyekuwa kasimama hapo, yule Askari akauvuta upanga wake kuusalimisha.

Alipoona hivyo lbn Ziyad alipiga kelele akasema "Mshikeni mara moja". Basi Hani akakamatwa na kukokotwa hadi katika moja ya nyumba akafungiwa humo na kuwekewa mlinzi.

Hasan bin Asma bin Kharijah akasimama na kumwambia lbn Ziyad, "Hatujapata kuwa wajumbe wenye khiyana isipokuwa leo ewe Amir, umetuagiza kwa mtu huyu na ukatuamru tumlete kwako, na tulipokuwa tumekuletea umeuchanachana uso wake na umeimwaga damu yake na bado unadai kwamba utamuua".

Maneno haya yakamchukiza Ibn Ziyad, akakasirika sana akasema kumwambia Hasan, "Nawewe uko hapa (kumtetea Hani)"?

Kisha akatoa amri Hasan apigwe, akapigwa na baadaye akafungwa kamba na akatupwa Gerezani. Hapo Hasan akawa anaomboleza kwa kusema "Hakika sisi ni milki ya Mwenyezi Mungu na kwake tutarudi, ewe Hani kwa nafsi yangu ninakusikitikia".

Khabari za tukio hili zikamfikia Bwana Amri bin Al-Hajaaj, na kwamba Hani amekwisha kuuawa.

Bwana Hani alikuwa ni mkwe wa huyu Al-Hajaaj kwa binti yake aliyekuwa akiitwa "Ruwaihah". Hivyo basi Amri bin al-Hajaaj akafika hapo Al-Kufah akiwa na jamaa zake, wakalizunguka jumba Ia Ibn Ziyad, kisha Amri alizungumza kwa sauti kubwa akasema, "Mimi ni Amri bin Al-Hajaaj na hawa nilionao ndiyo viongozi wa jamii ya Madh-haj, nao hawajatoka katika utii wala kupinga umoja, lakini habari zimetufikia kwamba mwenzetu (Hani) kauawa".

Basi Qadhi Shuraih akaja kutoka ndani alimokuwa yeye na Ibn Ziyad na anayaona yote yaliyomfika Hani akamwambia ya kwamba Hani yu katika amani. Basi wakaridhika na kuondoka kurejea kwao.

MAJLISI YA NANE

MAAFA YALIYOMPATA MUSLIM BIN AQIL

Muslim Bin Aqiil zilipomfikia habari za matendo aliyoyatenda Ibn Ziyad kumtendea Hani, alitoka yeye pamoja na watu waliokuwa wakimtii kwenda kumsaidia Hani na kumuokoa, pia kupigana na Ibn Ziyad.

Ibn Ziyad alipogundua jambo hilo alijificha katika jumba hilo la utawala wa Bani Umayya, ikawa wafuasi wake ndiyo wanapigana na watu wa Muslim bin Aqiil.

Wafuasi wa Ibn Ziyad waliokuwa pamoja naye wakawa wanachungulia na kuwatahadharisha wafuasi wa Muslim bin Aqil na wakawaonya kuwa litakuja Jeshi kutoka Sham kwa Yazid nalo litawashambulia.

Waliendelea kufanya hivyo mpaka usiku ukaingia, hapo ndipo wafuasi wa Muslim bin Aqiil walipoanza kutawanyika kumkimbia Muslim, na wakawa wanaambiaana, "Ni kitendo gani tukifanyacho kwa kuikimbilia fitna, inatupasa kujificha majumbani wetu tuwaache hawa jamaa mpaka hapo Mwenyezi Mungu atakapoleta upatanishi baina yao."

Waliendelea kutawanyika mpaka ilipofika jioni, Muslim bin Aqill aliswali Maghrib akiwa na watu thelathini tu ndani ya msikiti. Alipoiona hali hiyo alitoka kuelekea milango ya upande wa Kindah, na hakufika hapo ila alikuwa kabaki peke yake watu wote walikwisha kumtoroka.

Kisha Muslim alitoka kupitia mlangoni, lakini ghafla akajikuta hana mtu wa kumuongoza njia, kumbe alikuwa kabaki peke yake watu wote walikwisha kumtoroka.

Muslim bin Aqiil akaendelea mbele hali ya kuwa akipita katika vichochoro vya mji wa Al-Kufah, hajuwi la kufanya wala hafahamu aendako. Alitembea mpaka akafika kwenye mlango wa nyumba ya mama mmoja aliyekuwa akiitwa "Taua" ambaye alipata kuwa mjakazi wa Ash-Ath bin Qais, alipomuacha huru akaolewa na Usaid Al-Hadhrami akamzalia mtoto aliyeitwa "Bilal".

Huyu Bilal wakati Muslim bin Aqiil anafika kwenye nyumba ya mama yake, alikuwa katoka pamoja na watu fulani, hivyo basi mama yake alikuwa akimngojea pale mlangoni.

Muslim bin Aqiil akamtolea salamu mama yule "akaitikia", kisha akamuomba maji ya kunywa "Akapewa". Yule mama aliporejesha ndani kile chombo cha maji, alitoka na kumkuta Muslim akiwa ameketi chini akamuuliza, "Je, hujanywa maji?" akajibu, "Nimekunywa".

Mama yule akaendelea kumsemesha Muslim, lakini akawa hakujibu, mwisho yule mama akasema "Sub-hana Llah!!'. Ewa mja wa Mwenyezi Mungu simama uende kwenu, haifai wewe kuendelea kukaa mlangoni kwangu wala siwezi kukuruhusu ukae hapa".

Muslim bin Aqiil akasimama na akasema, "Ewe mtumwa wa Mwenyezi Mungu, katika mji huu sina makazi wala ndugu, je wapenda kupata ujira mwema na malipo mazuri, ili nami hapo baadaye nikulipe kwa wema wako baada ya siku hii ya leo?"

Yule mama akasema "Nini makusudio yako Ewe mtumwa wa Mwenyezi Mungu?"

Akajibu "Mimi ni Muslim bin Aqiil, watu wa Mji huu wamenidanganya na wamenihadaa, na sasa wamenifukuza."

Yule mama akasema, "Wewe ndiwe Muslim"?

Akasema "Ndiyo".

Yule mama akasema "Ingia ndani".

Muslim akaingia ndani ya nyumba miongoni mwa nyumba za mama yule isiyokuwa ile anayoishi mwenyewe, na yule mama akamtayarishia Muslim mahali pa kulala, na akamletea chakula ambacho Muslim hakukila.

Mtoto wa yule mama aliporudi na akawa amemtambua Muslim basi haraka alipeleka habari kwa Ibn Ziyad kumjulisha mahali alipo Muslim bin Aqiil.

Ibn Ziyad akamleta Muhammad bin AI-Ash-ath na akamtuma pamoja naye Ubaidullah bin Abbas As-Sulami wakiwa na watu sabini wa Kabila Ia Qais mpaka kwenye nyumba aliyoko Muslim.

Basi Muslim aliposikia sauti ya kwato za farasi na sauti za watu, akafahamu kwamba amefuatwa yeye. Akawatokea akiwa na upanga wake, nao wakamvamia ndani ya nyumba kabla hajatoka, akawashambulia kwa upanga mpaka akawatoa nje. Kisha walimrudia tena naye akawashambulia vikali, na ikatokea mashambulizi yakawa baina ya Muslim na Bakru bin Hamran Al-Ahmari, basi huyo Bakru "Mwenyezi Mungu amlaani" alimpiga Muslim dhoruba Ia Upanga akamkata mdomo wa juu, na akafanya haraka kumkata mdomo wa chini pia, meno ya chini ya Muslim yakabomoka.

Naye Muslim pamoja na hali hiyo alimpiga Bakru dhoruba kali ya kichwani, akamfuatisha nyingine katika sehemu iliyo kati ya shingo na bega, dhoruba ambayo ilikaribia kuingia ndani kabisa ya mwili wa Bakru.

Muslim pamoja na maumivu aliyokwisha yapata, aliendelea kuwashambulia watu wa ibn Ziyad mpaka akafaulu kuwauwa kikundi miongoni mwao.

Walipoona hali ya ushujaa wa Muslim, walianza kumshambulia wakiwa juu ya nyumba kwa kumtupia mawe, na wakawasha vijinga vya moto kisha wakawa wanamrushia kutoka katika paa la nyumba.

Muslim hakukata tamaa bali aliwatokea hali ya kuwa ameutoa upanga wake tayari kwa kupambana nao.

Muhammad bin AI-Ash-ath akawa anamwambia Muslim "Jisalimishe usiiue nafsi yako".

Muslim alimjibu Muhammad AI-Ash-ath hali ya kuwa akiwashambulia akasema: "Nimeapa, siuawi ila niwe katika hali ya uhuru, japokuwa mauti nayaona kuwa ni jambo gumu, nachukia kuhadaiwa au kudanganywa, nitakupigeni wala siogopi madhara".

Ibn Al-Ash-ath akapiga ukelele aksema, "Hakika wewe hudanganywi wala kuhadaiwa".

Lakini kufikia kipindi hiki Muslim akawa ameshehenezwa kwa mawe na akashindwa kuendelea na mapambano, basi akauegemeza mgongo wake ukutani.

lbn Al-Ash-ath akamwambia tena Muslim, "Jisalimishe".

Muslim akajibu, "Mimi nimekwisha salimika".

Akasema ibn Ash-ath, "Vema".

Kisha Muslim akawaambia jamaa waliokuwa wakimshambulia, "Je ninayo amani?"

Wakasema, "Ndiyo".

Akasema "Japo msinipe amani lakini siwezi kuweka mkono wangu mikononi mwenu" (Siwezi kuwatii).

Hapo wakamletea nyumbu, wakampandisha kisha wakamzunguka na wakamnyang'anya panga lake, ikawa kama kwamba Muslim katika kipindi hicho anaihuzunikia nafsi yake, basi ghafla akaaza kujawa machozi machoni mwake akasema: "Huu ndiyo mwanzo wa kuvunja ahadi, uko wapi basi uaminifu wenu?" Hapa Muslim akawa analia.

Ubaidullah As-Sulami akasema kumwambia Muslim bin Aqiil, "Hakika yeyote mwenye kutafuta mambo kama haya uyatafutayo, pindi anapofikwa na hali kama hii ihyokufika wewe hana haja ya kulia".

Muslim akajibu, "Hakika mimi Wallahi silii kwa ajili ya nafsi yangu, wala nafsi yangu siihuzunikii kutokana na kifo, japokuwa siipendelei nafsi yangu kuangamia, lakini (fahamu kwamba) nawalilia jamaa zangu wanaokuja kunifuata mimi, namlilia Husein na watu wa Husein (a.s.)."

Kisha Muslim akamuelekea Ibn Al-Ash-ath akasema: "Hakika wewe utashindwa kunipa amani, basi je kwako kuna wema wowote (unitendee)? Unaweza ukatuma mtu kutoka kwako kwa niyaba yangu akamfahamishe Husein(a.s) , kwani mimi simuoni Husein ila atakuwa leo ametoka au atatoka leo pamoja na watu wa nyumba yake basi akamwambie kwamba "Hakika mwana wa Aqiil amenituma kwako, hali ya kuwa yeye ni mateka mikononi mwa watu (wa Al-Kufah) haoni nafasi yoyote ila jioni atakuwa kisha uawa, naye anasema rudi, wewe na watu wa nyumba yako, baba yangu na mama yangu (nawatoa) iwe fidia kwako na wala wasikudanganye watu wa Al-Kufah, hakika wao ndiyo wale wale watu (waliojidai kushirikiana na) baba yako, ni wao ambao alikuwa akitamani (Baba yako) kutengana nao ima kwa mauti (ya kawaida) au kuuawa, hakika hawa watu wa Al-Kufah wamekudanganya na mwenye kudanganywa huwa hana rai".

lbn Ash-ath akamchukua Muslim mpaka kwenye mlango wa jumba la utawala, akaingia ndani na kumpa khabari zote Ibn Ziyad.

Muslim kiu kali ikawa imemsonga, na hapo kwenye mlango wa jumba hilo kuna watu wengi wanasubiri kupewa ruhusa (kuingia). Mara ghafla likaletwa jagi la maji ya baridi, Muslim akasema "Ninywesheni maji haya".

Muslim bin Amri Al-Baahili akasema, "Wayaonaje, ubaridi ulioje wa maji haya!, Wallahi hutaonja japo tone moja kabisa, mpaka kwaza uonje joto kali liliilomo katika moto wa Jahannam."

Muslim bin Aqiil akamjibu Muslim bin Amri akasema;

"Mama yako kapata hasara (kuzaa mtoto kama wewe) unauovu kiasi gani na moyo mbaya kadiri gani (bali muovu mno) ewe mwana wa Baahilah, wewe ndiyo unastahiki mno kulipata joto hilo kali na pia kuishi milele ndani ya moto wa Jahannam".

Kisha Muslim bin Aqiil akaegemea ukutani.

Bwana Amri bin Huraith akaja na kile chombo kilichokuwa na maji, juu yake kuna kitambaa, pia alikuwa na jagi ambalo alilitia maji yale na akamwambia Muslim bin Aqiil "Kunywa maji", ikawa kila anapotaka kuyanywa maji, basi lile jagi hujaa damu yake inayobubujika kutoka mdomoni mwake.

Akajaribu mara mbili kuyanywa maji hayo bila mafanikio, na alipokusudia kwa mara ya tatu kunywa, meno yake mawili ya mbele yakabomoka na kutumbukia ndani ya jagi la maji.

Muslim bin Aqiil akasema, "Al-hamdulillah (Sifa njema ni zake Mwenyezi Mungu) lau ningekuwa nayo riziki iliyogawiwa kwangu (kwenye maji haya) ningeyanywa".

Baadaye akaingizwa ndani kwa ibn Ziyad, Muslim hakumtolea salam lbn Ziyad.

Mlinzi wa Ibn Ziyad akamwambia Muslim, "Mtolee salaam Amir (kiongozi)".

Muslim akasema, "Ole wako nyamaza, Wallahi kwangu mimi (huyu) siyo Amiri."

Ibn Ziyad akasema kumwambia Muslim, "Ewe mwana wa Aqiil uliwakuta watu (hapa AI-Kufah) wakiwa pamoja, ukawatenganisha na kuwatawanya (wasikubaliane), pia ukawafanya wagombane wao kwa wao".

Muslim akasema, "Sivyo kabisa, mimi sikuja hapa kwa ajili hiyo, lakini watu wa Mji huu walidai kwamba Baba yako (Muawiyya) amewauwa watu wema (miongoni mwa wenyeji wa hapa) na amemwaga damu zao, na akawatendea matendo ya (Wafalme Kisra ha Kaisar, basi sisi tukawafikia (hapa) ili tuamrishe uadilifu na tuwaite (wote) kwenye hukumu ya kitabu (Qur'an)".

Ibn Ziyad akasema, "Tangu lini nawe (Muslim) ukafaa kuwa (kiongozi) wa hayo uliyoyasema? Kisha lbn Ziyad mwenye kulaaniwa akaendelea kusema kumwambia Muslim "Ewe muovu hakika nafsi yako inakutamanisha jambo ambalo Mwenyezi Mungu kisha kumpa mwingine, na haikukuonyesha mwenye kustahiki".

Muslim akasema, "Basi nani atastahiki jambo hilo (Ia uongozi wa Umma) endapo sisi (tutaonekana) hatufai?"

Ibn Ziyad akajibu akasema, "Mwenye kustahiki jambo Ia (uongozi) ni Amirul Muuminina Yazid".

Muslim aksema, "Kwa kila hali Mwenyezi Mungu ashukuriwe, sisi tumeridhia na tunaridhia kwamba Mwenyezi Mungu ndiye atakayetoa uamuzi baina yetu na ninyi".

Ibn Ziyad akasema, "Mwenyezi Mungu anilaani iwapo sitakuuwa, tena kwa uwaji baya ambalo hajapata mtu kuuliwa katika Uislam".

Muslim akasema, "Ama ilivyo kweli na hakika wewe ni mtu uliyezusha katika Uislamu mambo ambayo hapo kabla hayakuwapo, na kwa tabia yako hutaacha kufanya mauaji ya kinyama, na hutoacha kuwa ni mfano mbaya, mwenye niya mbaya, na kijicho kwa yule mwenye kustahiki mno kwa jambo hili kuliko wewe"

lbn Ziyad akamuelekea Muslim kwa ulimi wa matusi kumtukana yeye na kamtukana Husein na Ali(a.s) pia Aqiil (baba yake Muslim) akamtukana.

Muslim akanyamaza asimsemeshe kitu Ibn Ziyad, bali aliwaangalia watu waliokuwa pamoja na lbn Ziyad, akamuona Omar bin Saad akiwa ni miongoni mwao, akasema kumwambia Omar bin Saad "Ewe Omar bila shaka baina yangu mimi na wewe kuna udugu, basi mimi ninayo haja fulani kwako, na itakupasa wewe ufanikishe haja yangu hiyo, lakini ni siri baina yangu na wewe".

Omar bin Saad (mwenye kulaaniwa) akakataa kumsikiliza Muslim, lakini Ubaidullahi bin Ziyad akamuamuru Omar asikilize ombi Ia Muslim.

Basi wakajitenga wawili hao upande fulani hali ya kuwa Ibn Ziyad anawaona, Muslim akasema, "Hakika kuna baadhi ya watu wa Al-Kufah wananidai Dir-ham miasaba, basi kauze upanga wangu na deraya yangu kisha ulipe deni hilo, na nitakapokuwa nimeuawa uchukue mwili wangu na uusitiri (uuzike) na pia mtume mtu aende kwa Husein amwambie arudi (asije hapa Al-Kufah) bila shaka mimi nilimuandikia kwamba watu wanamuunga mkono (kumbe wamegeuka) nami namuona kuwa anakuja".

Ibn Saad akasema kumwambia ibn Ziyad, "Je wafahamu anasema nini (Muslim) ewe Amiri? hakika anasema kadha kadha". (Akasema yote aliyomwambia Muslim) "Ibn Ziyad akasema kumwambia Muslim bila shaka mtu mwaminifu hawezi kukufanyia khiyana lakini wewe umemuamini mtu mwenye khiyana".

Kisha huyu Ibnu Ziyad "Mwenyezi Mungu amlaani" akaamuru Muslim apandishwejuu ya paa la jumba hilo na akatwe shingo yake huko juu, na itakapoanguka wakitupe kiwiliwili chini kuifuata shingo itakayokuwa imeporomoka chini pamoja na kichwa. lbn Ziyad akamwita Bakru bin Hamran akamwambia "Panda juu ukamkate shingo yake". Akapanda.

Wakati Muslim akipandishwa juu ili akauawe, alikuwa akisoma Takbira na kuomba msamaha kwa Mwenyezi Mungu na akimsalia Bwana Mtume(s.a.w.w) na pia akawa husema, "Ewe Mwenyezi Mungu hukumu baina yetu na wale waliotudanganya na wametutweza, basi ghafla akainamishwa chini kisha shingo yake ikakatwa ikadondoka chini na mwili wake pia ukafuatishwa mpaka chini (Muslim bin Aqiil akawa ameuawa kishahidi, ewe Mola iteremshie amani na Rehema roho yake nasi tujaalie vifo vya kishahidi katika kukutumikia - Amin).

Baada ya kuuawa Muslim bin Aqiil, pale pale Ibn Ziyad akaamuru Hani atolewe (alikuwa bado kafungwa) akasema "Mtoeni mumpeleke sokoni kisha muikate shingo yake". Hani akatolewa ilhali mikono yake imefungwa na akawa anasema "Ee!!! jamaa zangu, leo sina jamaa yeyote, wako wapi jamaa zangu"?

Alipoona kwamba hakuna ye yote wa kumsaidia aliutoa kwa nguvu mkono wake katika kifungo alichofungiwa, kisha akasema, "Je hakuna fimbo au kisu au jiwe ambalo mtu anaweza kujilinda nafsi yake"?

Askari wa Ibn Ziyad wakamrukia na wakamfunga barabara na hapo hapo wakamwambia "Nyoosha shingo yako".

Hani akasema, "Sijawa mkarimu kiasi hicho kuwanyooshea shingo yangu, na pia siwezi kuwasaidieni katika kuiua nafsi yangu."

Mturuki ambaye alipata kuwa mtumwa wa lbn Ziyad akaachia dhoruba ya upanga kumkata Hani, lakini dhoruba hiyo haikumfanya kitu Hani.

Hapo Hani aksema, "Kwa Mwenyezi Mungu ndiko kwenye marejeo, Ewe Mola narudi kwenye huruma zako na radhi zako".

Yule mturuki akarudia mara ya pili kumkata Hani akafaulu kumuuwa, hivyo Hani akafa akiwa shahidi kwa kutaraji rehema za Mola wake.